Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by hon Hassan Seleman Mtenga (17 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, nianze kutoa pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais ambaye ni Mwenyekiti wetu wa Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa ambazo anazifanya. Pili nimshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Waziri Mkuu lakini kwa pamoja niwashukuru wapiga kura wa Jimbo la Mtwara Mjini ambao wameniwezesha kufika kwenye Bunge hili kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijielekeze kwenye maeneo mawili. Kabla sijaanza kuzungumza ni vema nikatoa shukrani kubwa sana, Jimbo la Mtwara Mjini tumepata miradi mingi sana. Tuna mradi wa Hospitali ya Rufaa ambayo itagharimu zaidi ya shilingi bilioni 122, tuna barabara ya kiwango cha lami ambayo inatoka Mtwara - Masasi na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa zaidi nataka tuzungumze kuhusu Mtwara Corridor. Hii Mtwara Corridor inawezekana hatuielewi vizuri na italeta maendeleo gani. Mheshimiwa Rais amewekeza fedha kwenye bandari ya Mtwara takriban shilingi bilioni 157, lengo na madhumuni ni bandari ya Mtwara iweze kufanya kazi na ilete tija kwenye uchumi wa taifa. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais ameamua kutengeneza barabara ya kutoka Mtwara - Newala ambapo itakuwa ni kiunganisho kikubwa sana kwenye zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upembuzi yakinifu umefanyika juu ya reli ya kutoka Mtwara hadi Mbambabay. Kama upembuzi yakinifu umefanyika na tunapozungumza upembuzi yakinifu ni kwamba tayari mamilioni ya shilingi yametumika kwenye kuangalia dhana nzima ya awali. Niishauri Serikali muda sasa umefika wa kutoa maamuzi ambayo yako sahihi ya kuanza kuijenga reli hii ambayo itaweza kutuletea uchumi kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia uchumi wa nchi, yako mambo matatu tunatakiwa tuyaangalie. Tunazungumzia barabara ambayo ni kiunganisho, viwanda ambacho ndiyo kiunganisho namba moja lakini lazima tuwe na watu kama hatutakuwa na watu hatutakuwa na mashamba na hatutakuwa walimaji. Kama hakuna barabara ambazo ziko sahihi hatutaweza kupitisha mazao yetu kwenye barabara husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu niiombe tena Serikali, tuna barabara ya kutoka Mtwara - Dar es Salaam, kwa muda mrefu sasa imekuwa inafanyiwa service za mara kwa mara na kutengeneza barabara ya lami kilometa moja inatugharimu fedha nyingi sana. Barabara hii imekuwa inaharibika mara kwa mara kwa sababu malori yanayopita ni makubwa na yenye uzito mkubwa. Tuna kiwanda cha Dangote, cement yote zinasafirishwa kwa njia ya gari. Tuna zao la korosho ambapo zote zinasafirishwa kwa njia ya barabara. Tumejenga bandari na tumewekeza pale shilingi milioni 157 ni kitu gani kinashindikana bandari ya Mtwara isifanye kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa suala la elimu ni vema nikampongeza sana Mheshimiwa Rais. Tunapozungumzia elimu bure kwenye shule za msingi na sekondari suala hili limeleta chachu kubwa kwa wananchi kwa ujumla wake. Hata hivyo, ni vema nikasema kuna mgawanyiko katika fedha ambazo tunazipeleka kwenye shule za sekondari na msingi. Mwanafunzi mmoja shule ya msingi anapelekewa Sh.6,000 na mwanafunzi mmoja kwenye shule ya sekondari anapata Sh.10,000…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, kengele imeshagonga

MHE. HASSAN S. MTENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dooh, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia Mpango wa Tatu wa Miaka Mitano. Pili, nimpongeze Mheshimiwa Mwigulu, Waziri wa Fedha kwa kutuletea Mpango ambao umekaa vizuri sana. Nina mambo ambayo nitayachangia kwenye maeneo zaidi ya matatu hasa tukianza kwenye miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunahitaji tuvuke na tupambane kuondoka kwenye umaskini kuingia kwenye suala zima la kimaendeleo hasa kwenye uchumi mkubwa tunapozungumza miundombinu hasa kwenye maunganisho ya nchi yetu Kusini mwa Tanzania, kule Mtwara, naishukuru sana Serikali kwa kutujengea daraja la Mtambaswala. Nataka nitoe angalizo, daraja hili limetengenezwa kwa gharama kubwa sana, lakini kwenye utengenezaji wake na matumizi ni tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nieleze uhalisia kutoka Mtwara kuelekea Masasi kuna kilometa zaidi ya 230, lakini kutoka Masasi kuelekea kwenye daraja la Mtambaswala kuna kilometa 130 lakini kutoka Mtambaswala kwenda border kuna kilometa 75. Ukitoka border kuelekea Beira Nampura pana kilometa zaidi ya 788. Hoja ni vipi? Ukitoka Mtwara kuelekea Ruvuma pana kilometa 70, kutoka Ruvuma Mpakani unaelekea Msimbwa Naplaya mpaka Nampura unatumia kilometa 445. Kama tungejenga daraja hili kupitia pale Mto Ruvuma tungeweza kufungua mawasiliano kati ya Msumbiji na Tanzania na Afrika Kusini kupitia Msumbiji kuja Tanzania. Sasa hivi wenzetu Afrika Kusini wakitaka kwenda kuuza magari wanapitia Zambia ambapo wanatumia zaidi ya kilometa 2,800 kuja Tanzania. Kwa hiyo nataka niseme hapa hapahitaji watu wenye degree wala maprofesa, ni suala la uamuzi sasa kwa Waziri mwenye dhamana alishughulikie hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nataka nimpongeze mdogo wangu Mheshimiwa Bashe. Mimi nasema Bashe ana akili kubwa sana. Pia nataka nishauri, kule kwetu Mtwara liko eneo moja linaitwa Kitele. Toka nazaliwa napata umri mpaka leo naingia uzeeni, liko eneo linamwaga maji chemchem, maji ya kutosha sana na eneo lile wakazi wa pale wanalima mpunga. Kwa kuwa mpunga ule unalimwa tofauti na viwango, hatuna scheme za umwagiliaji mpunga ule ni mzuri sana, lakini haukidhi mahitaji ya kibiashara. Sasa naiomba Wizara yenye dhamana, twende pale wakaangalie wajiwekeze ili tuweze sasa kuleta kilimo cha kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango nimeangalia kwenye suala la elimu. Kwanza niipongeze Serikali, imeweza kuwekeza kwenye mfumo wa elimu bila malipo tukisema elimu bure, hongera sana kwa Serikali yetu. Hata hivyo, bado kuna tatizo, shule za msingi katika kila pato la kichwa cha mwanafunzi tunapeleka shilingi 6,000, lakini kwenye shule za sekondari kila kichwa cha mwanafunzi tunapeleka shilingi 10,000, lakini fedha hizo tayari Wizara zinapeleka kukiwa na mgawanyiko wa matumizi. Utawala wana asilimia 10 kwenye fedha hiyo, michezo kuna asilimia 20 inagawanyika kwenye fedha hiyo, mitihani kuna asilimia 20 kwenye fedha hiyo, ukarabati kuna asilimia 20 kwenye fedha hiyo, vifaa kuna asilimia 30 kwenye fedha hiyo. Niombe fedha hii ni ndogo mno na fedha hii inasababisha sasa hivi Walimu wetu kufanya njia mbadala ya kuwafaulisha watoto ilimradi tu wasionekane kwamba wao hawana mafunzo kwenye zile shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule nyingi zimekuwa sasa wazazi wakiwa wanachangia, lakini kwenye uchangiaji wazazi wamefika mahali wanagoma. Wanasema Serikali inaleta fedha nyingi sana kwa sababu mnyumbulisho huu wazazi hawauelewi. Kwa hiyo niiombe Wizara yenye dhamana twende tujiwekeze sasa kwenye Sekta hii ya Elimu, kama tumekubali sasa Serikali kubeba mzigo wa elimu bila malipo basi twendeni sasa tuongeze ruzuku hii ambayo inapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nataka niguse kwenye suala la viwanda. Kusini tuna Kiwanda kikubwa sana cha Saruji cha Dangote. Kiwanda hiki kina wafanyakazi zaidi ya 6,000. Kimetoa ajira ya kutosha, lakini kiwanda hiki kinashindwa ku-move kwa sababu ya kodi za TRA. hHpa karibuni mlikuwa mnasikia kwamba Kiwanda cha Dangote kinataka kufungwa, lakini Kiwanda cha Dangote wamefika mahali sasa wamechoka wanataka kuondoka. Kwa mfuko wa saruji mmoja TRA wanachukua shilingi 3,000, mfuko unaouzwa shilingi 11,000 kwa bei ya jumla. Ukienda ndani ya kiwanda kile, maintenance ya kiwanda, mkanda mmoja unavyokatika wa mashine unatumia zaidi ya milioni 180 kuagiza mkanda mmoja wa mashine. Twendeni sasa tuangalie kama tunahitaji kuboresha uchumi huu wa Tanzania lazima tufike mahali sasa viwanda vyetu tuvisaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wawekezaji, kila tunapozungumza, sasa hivi nimeshazungumza na wawekezaji zaidi ya sita kutoka nje (investors) lakini wanasema kwamba Mtenga, hili suala kwenu haliwezekani. Ukitaka kufungua kiwanda, kuwa mwekezaji, shughuli yake ni kubwa mno. Mle kuna watu wapo zaidi ya nane au tisa, ukitaka kiwanda unamkuta NEMC, ukienda hapo NEMC mambo ya NEMC Mwenyezi Mungu mwenyewe anayafahamu. Pia kuna mtu anaitwa TBS, ndani ya kiwanda hicho hicho kimoja. Yuko mtu mmoja anaitwa TRA, lakini kuna janga kubwa la Kitaifa linaitwa NIDA, leo mwekezaji ametoka nje kadi ya NIDA anaipata wapi hapa Tanzania? Hili lazima tuliangalie, lakini kuna mtu anaitwa OSHA, pia mtu mwingine anaitwa Zimamoto. Vile vile Kuna kibali cha kuishi, hili nalo ni shughuli nyingine. Vibali vya kuishi leo kama kuna wawekezaji ambao tayari wana wafanyakazi wao wako wanafanya kazi, kwenda ku-renew kibali tu cha miaka miwili au mwaka mmoja wanachukua takriban zaidi ya miezi nane au tisa. Hebu tufike mahali kama kweli tunahitaji sasa, tufike mahali tubadilike ili tuingie kwenye uchumi mkubwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nishauri hawa OSHA, NIDA na kadhalika kwenye Sekta hii ya Uwekezaji hebu wakae sehemu moja ili shughuli ile iwezekane kupatikana. Yuko hapa mtu mmoja anaitwa Mkurugenzi wa NEMC, yaani afadhali leo unaweza kumtafuta Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukampata kuliko Mkurugenzi wa NEMC. Tunakwenda wapi? Leo tunazungumza kwamba nchi yetu tunataka iwe nchi ya uchumi, lakini uchumi wetu tunazungumza viwanda, ni kitu ambacho hakiwezekani. Ukiangalia kwenye viwanda vyetu, wafanyakazi ambao wanafanya kazi kwenye viwanda hivyo, mishahara yao wanayolipwa ni midogo. Serikali kama Serikali wanasema kuna viwango vya kima cha chini vimepangwa, sasa viwango vinavyopangwa vya kima cha chini tuangalie na kodi tunazowatoza wale watu na service za viwanda vyao wanavyofanya ili tufike mamlaka ya kuwabana wale juu ya mishahara yao ambao inalipwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa. Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshamaliza? Loh, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, nami nitangulize kutoa shukrani za dhati kwako kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi sana kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu kwa kazi nyingi anazozifanya. Niwapongeze na Mawaziri ambao wamepata uteuzi hivi karibuni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie suala la Hifadhi ya Ngorongoro. Hifadhi yetu ya Ngorongoro ilianza rasmi mwaka 1954. Hifadhi hii wakati inaanzishwa kulikuwa na takriban watu kama 8,000. Watu 8,000 kwa wakati huo walikuwa ni wachache sana, lakini leo tunapozungumza hapa Bungeni kuna watu takriban 110,000. Sasa ni nini nataka nizungumze. Kama tunakwenda kuwa na hifadhi ina watu zaidi ya 110,000, hatuwezi kuiita hifadhi kwa kweli, tusidanganyane kwenye Bunge hili. Lakini hii ni rasilimali ya Taifa.

Mheshimiwa Spika,tukiangalia rekodi za mapato ya makusanyo ya fedha wenye Hifadhi yetu ya Ngorongoro; mwaka 2018 tulikusanya bilioni 143.

T A A R I F A

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Simwoni anayeomba taarifa, ni nani!

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, niko hapa.

SPIKA: Nimekuona tayari, Mheshimiwa Jafari Chege.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, sina budi na wala sina namna ya kumwondoa mchangiaji kwenye hoja yake ya msingi, naaka tu nimpe taarifa kwamba nje ya watu zaidi ya 100,000 wanaopatikana pale tunachozungumza ni pamoja na aina ya shughuli zinazofanyika kwenye ile hifadhi ya Ngorongoro. Mojawapo ikiwa ni kwamba miaka hiyo ambayo watu walikuwa ni zaidi ya 8,000 ng’ombe waliokuwa kwenye hifadhi walikadiriwa kuwa 12,000. Leo tunavyozungumza kuna ng’ombe zaidi ya laki moja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimpe taarifa ili aende akijua kwamba hayo yote yanafanyika kwenye Hifadhi ya Ngorongoro.

SPIKA: Sasa kabla sijakuuliza Mheshimiwa Mtenga uendelee na mchango wako, nilikuwa najizuia kidogo kusema kanuni zetu, maana nachukua muda wenu kidogo, nilikusudia kuwakumbusha baadaye. Kwa sababu usipomsikiliza Mbunge mwenzako kumaliza hoja yake, huenda hilo jambo, yaani unatakiwa umuingizie taarifa akiwa amemaliza kile anachokisema ili ujue kuwa kuna jambo amelisahau. kwa sababu pungufu ya hapo maana yake wewe unamuingizia taarifa yako, sasa haelewi kama mtiririko wake aendelee nao ama vipi.

Kwa hiyo tuwe wavumilivu kidogo. Leo taarifa zinaruhusiwa kabisa, wala msiwe na wasiwasi, lakini mwache yule mwenye hoja amalize ile hoja, anapokwenda kwenye hoja nyingine unagundua kwamba amesahau hii sasa ngoja nimuongeze, ndilo lengo hasa la hiyo kanuni yetu ya Taarifa.

Mheshimiwa Mtenga.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, kwanza niipokee taarifa, lakini nilikuwa nazungumzia mwaka 1820 mapato ya Ngorongoro yalikuwa bilioni 143. Tulipoingia 20…

SPIKA: Samahani, ulikusudia kusema 1820 au 2018.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ni mwaka 2018, Mheshimiwa Chege alinitoa kidogo kwenye mstari.

Mheshimiwa Spika, tulipoingia mwaka 2019 tukakuta tuna fedha ambazo tulizikusanya bilioni 124, lakini 2020 tukakusanya fedha bilioni 31.

Mheshimiwa Spika, sasa naziweka hizi record ili tuone jinsi hifadhi yetu inavyokwenda kuteketea na masuala ya mifugo pamoja na kaya ambazo zipo kwenye hifadhi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwenye hifadhi hii kuna kaya zaidi ya 22, lakini leo tunapotaka kuzungumzia watalii wanaoingia Ngorongoro imekuwa ni hali ya hatari. Watalii wanapoingia Ngorongoro kwanza lazima wakutane na ng’ombe, mbuzi pamoja na kondoo ndipo waingie huko ndani.

Mheshimiwa Spika, kibaya zaidi kuna vitu vinafichwa kwenye Ngorongoro. Leo kuna watu wanauawa na simba, wanazikwa usiku, haya hayazungumzwi. Wanafika mahali kuwazika watu hawa usiku Serikali isije ikaelewa na ikatambua kwamba wananchi wao wanauawa mbugani.

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe ushauri na ushauri wangu, pale tunapozungumza kwamba tunataka hifadhi iwepo lazima tufike mahali tukubaliane kwamba hifadhi hii iwepo. Kwa sababu kwa mujibu wa sheria, kama hawa watu walikuwa 8,000, leo wako 110,000, wametokea wapi zaidi ya 102,000? Kwa mkataba upi unaozungumzwa? Lazima vitu hivi tuviangalie.

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe angalizo moja. Kwetu kule Mtwara kulikuwa na mradi wa gesi. Mradi ule wa gesi ukazua mambo mengi sana, lakini kwenye Bunge hili ikasemwa kwamba mradi ule ni wa kitaifa na Serikali ikachukua maamuzi na gesi ile ikatoka Mtwara ikaja Kinyerezi – Dar es Salaam na sasa ndiyo imekuwa sehemu ya msaada wa umeme wa gesi ya Mtwara. Hakuna sehemu tulipozungumza kwamba sasa katika hii rasilimali tugawane mbavu, hakuna. Hata hivyo, huku tunapoelekea kwenye suala la Ngorongoro, leo kuna wafugaji wako mle ndani, twendeni kwa wale wafugaji wakaombe mifugo waliyokuwa nayo halafu wataowaona watu walio nyuma ya mifugo ile.

Mheshimiwa Spika, wale waliopo ndani ya Ngorongoro si wenye mifugo yao; na hili lipo, si kwamba ni jambo ambalo tunalizungumza tu hapa. Sasa kama kuna matajiri wako nje, wanafanya kazi wao kugeuka kuwa NGOs na NGOs sasa hivi ziko kule zinaelimisha watu jinsi ya kutohama.

Mheshimiwa Spika, kwa suala la Ngorongoro tufike mahali kama Bunge tuchukue hatua. Hali ya Ngorongoro ni mbaya. Naishauri Serikali, hizi kaya 22 twendeni tuwatafutie makazi au tuwalipe fidia, hawa watu tuwaondoe kwa utaratibu.

Mheshimiwa Spika, kuna kitu ambacho kipo ndani ya pazia; leo tunazungumza wenzetu wapo mle ndani, wanafuga; si wao tu, kuna wenzetu wa nchi Jirani wanafanya kila njia Ngorongoro ife na sisi tumejifungia humu Bungeni. Pia wako wenzetu wanatumika. Huko nje kuna matajiri, kwenye hoteli kuna matajiri kutoka Ngorongoro. Lazima tuelezane humu ndani. Wamekuja kufuata nini matajiri? Mbona hatujawaona Wamasai wamekuja na lubega wanasema mimi ndiye mwenye ng’ombe 200? Wanakuja matajiri hapa wanakaa Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inaumiza sana. Nimezungumza kwa uchungu kwa sababu Jimbo langu mimi la Mtwara Mjini ni Jimbo ambalo ni masikini, na ndiyo maana leo ninazungumza kwa ukali sana. Hata tukiangalia kwenye bajeti, mimi nimetoa gesi kuileta huku, kwenye bajeti, tuiangalie Arusha, sisi tunapata sawa na Arusha? Arusha sawa na Mtwara? Si vitu viwili tofauti? Mtwara haiwezi kuingia Arusha hata kwa mara 200 wala kwa mara 100, haiwezi kuingia Arusha, lakini tunapoingia kwenye kutafuta rasilimali ya Taifa, keki tunagawana sawasawa. Kuna haja gani sasa ya wenzetu kuzuia hiyo keki wao wanataka kuihujumu hiyo keki? Hili halikubaliki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale kuna Baraza la Wafugaji. Baraza lile la Wafugaji ndicho chanzo chote mnachoona kwenye mgogoro huu tuliokuwa nao. Ngorongoro wenyewe walikuwa wanawapa hela zaidi ya bilioni tatu kwa mwaka kuendesha shughuli zao. Zile bilioni tatu sasa ndizo zimegeuka kuwa chungu kwa Serikali. Tunapigwa na fedha zile ambazo tulikuwa tunawapa Baraza la Wafugaji.

Mheshimiwa Spika, kanuni sizijui sana, lakini kuna maneno ningesema hapa, naogopa sana unaweza ukanifukuza kutoka nje, ila nikuombe, kama walipeleka Mtwara kule vifaru, ma-bulldozer pamoja na vitu vingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HASSAN S. MTENGA: …kwamba rasilimali ile ya taifa iwe keki ya Taifa, tunaogopa nini? Au kwa sababu kuna matajiri?

Mheshimiwa Spika, ni vyema sasa, kama waling’ata jongoo Mtwara wang’ate hao jongoo na sehemu nyingine. Tukiiacha Ngorongoro kesho tutakwenda Mfinga Iringa, kesho kutwa watahamia Serengeti na mwaka ujao watakuja pale Mbeya; halafu tunakaa humu tunajifungia, tunaona ni vitu vya kawaida tu?

Mheshimiwa Spika, tufike mahali…

SPIKA: Dakika moja, malizia Mheshimiwa.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru sana. Zingekuwa mbili ningekushukuru zaidi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa namna moja au nyingine mgogoro ule hauwezi kwisha kwa mazungumzo kama wanavyodai, kwa sababu wenzetu wanatoka wanakwenda kule wanashawishi watu, leo hii wameshajipanga, wanasema njia zote tu-block, tuanze Maandamano pamoja na vitu vingine.

Sasa hawa ni wenzetu wanafanya vitu hivi. Huo mgogoro wanakwambia wewe uende ukazungumza, ukazungumze na nani? Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza, nimpongeze Waziri Mkuu kwa hotuba yake ambayo kwa kweli imesheheni vipaumbele vyote vitakavyokwenda kurekebisha uhalisia wa maendeleo ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimekuwa mtumishi wa CCM kwa muda mrefu sana na nimepitia nafasi mbambali mpaka hapa nilipofikia. Hapa niliposimama inawezekana nikazungumza nitakayoyazungumza sitoweza kusahau au sitaweza kumsahau Hayati John Pombe Magufuli. Hata hivyo, siyo tu Hayati Magufuli, tunao viongozi ambao wameondoka wako mbele za haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka wakati Sokoine anafariki takribani zaidi ya miaka ya 10 hakuna impact yoyote ambayo ilikuwa inaonyesha kwamba tumkumbuke kwa matendo yake. Tulikuwa tunasikiliza kwenye asasi mbalimbali wakiwa wanatukumbusha wanasiasa na Serikali jinsi ya kuenzi viongozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nishauri Hayati Magufuli amekuwa ni kiongozi bora Barani Afrika na ni kiongozi ambaye Marais wa Afrika walikuwa wanatamani kuiga mifano yake. Sasa ikitupendeza pale Morogoro roundabout twendeni tukaweke picha yake. Kwa legacy ambayo ameiacha Hayati Magufuli na kama Bunge hili kila Mbunge anayesimama anamzungumzia na sisi tufike mahali sasa tuwaonyeshe Watanzania kwamba tunamuunga mkono kwa vigezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze mdogo wangu Mheshimiwa Bashe. Tulipokuja Disemba kuapa nilikaa naye hapa kantini lakini nilimueleza kuhusu zao la korosho na TMX, namshukuru sana amekuwa msikivu na alituelewa watu wa Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vema Wabunge wengine wakaijua TMX. Kule kwangu Mtwara zao kubwa la biashara ni korosho. Nilikuwa nasoma kwenye ripoti yao wanasema watakuja kuwa madali lakini udalali wao korosho zetu zitanunuliwa online. Makampuni yote ya korosho ambayo yako Tanzania hususani Mtwara, yana wazawa na matajiri wengine wapo Vietnam, India na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia TMX kufika mahali wao wakala number one, kinachotokea ni nini? Ni kwamba mfanyabiashara aliyeajiriwa yuko Mtwara tayari atakuwa amepoteza ajira kwa sababu korosho zitakuwa zinanunuliwa online. Kampuni ambayo iko India na iko Tanzania na hapa kuna wafanyakazi, kama wako 20 watapunguzwa atabakia mfanyakazi mmoja. Kwa hiyo, niipongeze Serikali kwa kuwa wasikivu na kukubaliana kwamba TMX sasa ifike mahala ikae pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimshukuru Waziri wa Maji. Waziri wa Maji alinitembelea Mtwara kuja kuangalia chujio na nikamueleza shida ya Mtwara siyo chujio ni maji na Serikali ikiweza kutupatia maji ya Mto Ruvuma tatizo la maji litakuwa limekwisha. Pia nikamueleza Waziri wa Maji kwamba mabomba yanayotumika hususani kwenye Jimbo la Mtwara Mjini yalifungwa na mkoloni, ni ya chuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hata leo kama mtaweka chujio likawa linafanya kazi lakini linapita kwenye bomba ambazo zina kutu. Kwa hiyo, maji yale hayatakuwa na usalama, yataendelea kuwa na ukakasi na chuma. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Maji atusaidie kwenye mpango wake kwa sababu ameshafika mahala amesema kwamba atatutengea fedha na upembuzi yakinifu utafanyika basi hilo naomba alisimamie kwa makini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine tumekuwa tunazungumza ajira za vijana, kweli hili ni janga la kitaifa. Sisi Wabunge wa Mkoa wa Mtwara tuna maeneo mengi sana ya mapori na yanahitaji kufanyiwa kazi kwenye suala la kilimo lakini hatuwezi. Hii ni kutokana na jinsi tulivyowaandaa vijana wetu kwenye familia zetu hawawezi ku-compete na kwenda shamba kulima bila Serikali kuwekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe mfano, leo tunawatibu vijana ambao wanakula madawa ya kulevya kwa gharama kubwa sana lakini tunapeleka asilimia 10 kwa ajili ya vijana, akina mama na walemavu, twende sasa na mpango endelevu, wapo vijana wako tayari kwenda kulima shambani lakini Serikali ichukuwe hatua sasa ya kuwawezesha vijana hawa tuwapeleke mashambani wakalime kilimo cha kisasa ili sasa tuweze kutoa ajira zingine mpya tofauti na zile ambazo tunazungumza.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imeshagongwa.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Ujenzi. Kwanza nilikuwa namwangalia hapa Waziri wa Ujenzi, mara nyingi amekuwa anajishika kichwa, anajishika shavu, kwa kweli tunapaswa tumsaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwangu Mtwara tuna barabara ya Mnivata ya kilometa 160; Mnivata - Mtwara mpaka Masasi. Barabara ile kwenye bajeti humu tumetengewa shilingi bilioni tatu. Kwa hali ya kawaida ukipiga mahesabu ya kilometa moja kujenga barabara ya lami, lami standard nadhani ni zaidi ya shilingi bilioni moja na something.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hizi shilingi bilioni tatu tunakwenda kutengenezewa kilometa tatu. Barabara hii sasa ina miaka takribani 10. Katika bajeti zote za miaka 10 tumetengenezewa kilometa 50. Naomba kwamba sasa kuna kila sababu, kwa kuwa barabara hii inaunganisha baadhi ya barabara zinazokwenda kwenye wilaya nyingine, pia ni barabara ya kibiashara. Kwa hiyo, tunakosa kufanya biashara zile za kisasa hasa kwa kutumia barabara hiyo kwa sababu barabara siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna barabara ya kutoka Mtwara kuelekea Mahurunga; barabara hii hatujaona kwenye bajeti kama imetengewa fedha. Barabara hii toka imeanza kutengenezwa sasa hivi ina kiwango cha lami kilometa ambazo hazizidi sita au saba, takribani ina miaka zaidi ya 15 na iko TANROADS. Naomba barabara hii sasa itengewe fedha za kutosha ili tuweze kupata barabara ya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kule inakokwenda ndiyo kwenye mpaka baina ya Msumbiji na Tanzania, lakini kumekuwa kuna matukio mengi ambayo yanatokea, watu wetu, watu wa Idara, watu wa usalama na watu wengine wanashindwa kufika kwa wakati kwenye maeneo hayo, kwa sababu barabara ni mbaya hazipitiki. Tunaomba Serikali mtusaidie kwenye hii barabara. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie barabara ya Kibiti – Lindi – Mtwara. Barabara hii kwa sasa hivi haipitiki, ni barabara ambayo tayari imeharibika, imekufa kutokana na malori ambayo yanabeba ufuta, korosho, na mahindi yanayopelekwa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwako, tunayo Bandari ya Mtwara; bandari hii imetumia shilingi bilioni 157 na fedha zile tumeziwekeza pale ili bandari ile ifanye kazi. Nataka nitoe angalizo, leo kuna makampuni yanayoleta mafuta, Serikali imeelekeza kwenye makampuni yanayoleta mafuta kwamba kwa watu wa mikoa ya kusini, itumike bandari ya Mtwara wa kubeba mafuta. Ni kitu gani kinashindikana sasa tukaelekeza kwamba korosho zote za Mtwara zipitie Bandari ya Mtwara; ufuta wote unaolimwa Lindi na Mtwara upitie Bandari ya Mtwara; na mahindi yote yanayolimwa yapitie bandari ya Mtwara? Kuna nini hapa? Naomba kufanya maintenance kwenye barabara yetu ya lami kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam a lot of shillings tutazitumia pale. Hivyo maintenance hizi tunazozifanya za kila siku kama tungeamua sasa fedha hizi tuzielekeze kwenye ujenzi wa barabara tungekuwa hatulalamiki hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo barabara ya Mtwara – Kibiti – Lindi, kila ukipita barabara ile, kila baada ya miezi miwili unakutana na shida. Mkandarasi yuko barabarani na anatengeneza barabara ile kwa ajili ya service. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nijumuike na wenzangu kumshukuru Amiri Jeshi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu. Lakini pia nichukue fursa nayo kumshukuru Waziri wa Ulinzi, kwa kweli nina kila sababu ya kuzungumza na Waziri wa Ulinzi jinsi anavyojiweka kwetu, tunavyozungumza naye na ni Waziri ambaye yupo tayari kuzungumza na kila Mbunge mmoja wapo iwe nje au ndani, kwa kweli ninampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumze kwenye masuala ya barabara ya ulinzi. Katika mipaka yetu inawezekana tukazungumza suala la ulinzi kiujumla, lakini suala la ulinzi kama hatujalipa kipaumbele inawezekana majeshi yetu tukawapa kazi kubwa sana kwenye ulinzi. Mfano nataka nizungumzie mpaka wa Mtwara na Msumbiji tuna barabara hapa ya ulinzi ya kilometa 300; unatoka Mtwara hadi Tunduru. Barabara hii kwa hali jinsi ilivyo haiwezi kupitika kwa urahisi iwapo litatokea janga lolote la kitaifa au la uvamizi hawa wanajeshi wetu hawawezi kufika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu nadhani Waziri wa Ulinzi wafanye mazungumzo na Waziri wa Ujenzi barabara ile ya ulinzi ambayo iko madhubuti kabisa kwa ajili ya ulinzi wa mpaka wa kusini iweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamezungumza sana kuhusu migogoro ya ardhi, kuhusu makambi ya majeshi yetu; kule kwangu ni sehemu pale Mtwara ni sehemu ya waathirika wa makambi hayo. Ukienda kwenye Kata ya Ufukoni ina watu takribani zaidi ya 12,000 lakini katika kata hiyo watu 12,000 kuna watu zaidi ya 4,000 wana mgogoro na Kambi ya Jeshi, na hili ni lazima nilizungumze kwa sababu kwenye mgogoro ule utawakuta wanajeshi/makamanda wako wana viwanja na wamejenga nyumba za kisasa. Kwa hiyo, rai yangu nataka nizungumze kwamba niombe muda wa bajeti hii ikishaisha tumemaliza hili Bunge ikimpendeza Waziri twende tukatatue mgogoro ule haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima tunaozungumza vijana wetu wa JKT; wenzangu wamezungumza sana, vijana hawa wa JKT tumekuwa tunawapa mafunzo na mafunzo haya wanayopewa ni mafunzo ya kijeshi. Lakini nataka nitoe angalizo kwa Serikali, vijana hawa tunapokwenda kuwapa mafunzo ya kijeshi na baadaye tukaendelea kuwaacha idle nje, iko siku hawa watabadilika sasa kuwa watu wabaya ndani ya Serikali yao. Kwa sababu tayari tumewapa mafunzo, lakini tunashindwa sasa kuwatumia kimafunzo sahihi. Nashauri wenzangu wamezungumza sana kuhusu viwanda, lakini wenzangu wamezungumza kuhusu activity nyingi kuhusu vijana hawa. Kama ikikupendeza na Serikali ikiipendeza naomba vijana hawa sasa waandaliwe shughuli mahususi wanapotoka kwenye mafunzo ya jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la ulinzi tukirudi nyuma kwenye historia ya nchi yetu tumepigana vita kule na Uganda, lakini wakati tunapigana vita na Uganda tulifika mahala tukaathirika kama Watanzania na Jeshi letu. Baada ya daraja letu ambalo tulikuwa tuna daraja pale Kagera halikuwa na uwezo wa kuwa na daraja kama daraja. Haya nayazungumza kwenye historia hii, natoa mfano sasa tunazungumza Mtwara na Msumbiji na nimekuwa nikizungumza sana Bunge hili, lakini nimekuwa naishauri sana Serikali juu ya kujenga daraja baina ya Msumbiji na Mtwara kwa pale ambapo tunasema barabara yetu ya ulinzi ya mpaka ule ndiyo inapoanzia basi twendeni sasa tujenge daraja ili jambo lolote litakalotokea kuwepo na unafuu wa kuweza kuboresha jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niendelee kulipongeza Jeshi hili, nalipongeza Jeshi katika nchi zetu za Kiafrika ni jeshi la kwanza ambalo halijayumba na hili lazima tukubaliane kwamba tayari tuna majemedari ambao wamefika mahali wamegeuka kuwa wazalendo ndani ya nchi yao. Lakini ukiangalia kwenye nafasi zao na maudhui jinsi wanavyoishi pale kwangu Mtwara tunazo nyumba za wanajeshi nyumba zile zilijengwa takribani miaka ya 1980.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyumba zile ukienda kuziona siku ya leo na ukaangalia ukaona kwamba nyumba hizi wanakaa wanajeshi wetu, ni aibu kubwa sana. Niiombe na Serikali twendeni tukazikarabati zile nyumba kwa sababu ufanisi wa jeshi letu, ufanisi wa wafanyakazi wetu lazima wafike mahala wajue yale maudhui wanayoishi kwenye Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nazungumzia wanajeshi kukaa nje ya makambi; mimi nataka niishauri Serikali hawa wenzetu wanafanya mazoezi mazito sana na kwa bahati nzuri asilimia kama 20 ya mazoezi hayo mimi nayafahamu. Lakini wanapojumuika na wananchi ndiyo tunasema hawa ni rafiki sawa na wananchi lakini yako mambo ya msingi ambayo wanajeshi kama wanajeshi kwenye taaluma yao haitakiwi kujichanganya na wananchi. (Makofi)

Sasa hili natoa angalizo kwa Serikali leo tumeona maeneo mengi nasikia jeshi wamempiga mwananchi huko, jeshi wamempiga siyo kwamba wanakusudia kufanya vile kwasababu hawa wanajeshi huwezi kumpeleka jeshi aende akalinde benki siyo kazi yake na siku utakayomchukua mwanajeshi kwenda kulinda benki, inawezekana maudhui ya yeye na mteja yakawa ni mambo mawili tofauti. Kwa sababu siyo kitu ambacho wamesomea au wamejifundisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi niiombe Serikali twendeni sasa tuwajengee mazingira ya kuishi kwenye makambi na wale maafisa ambao tunasema maafisa wetu hawakai kwenye makambi wanakaa uraiani, tutengeneze sasa nyumba za kisasa kwa ajili ya kukaa hawa wanajeshi wetu. Suala hili la ujenzi wa nyumba halikuanza jana wala juzi, kwa kumbukumbu zangu kabla sijaingia Bunge hili, lakini mabunge yaliyopita Wabunge wengine walizungumza sana kuhusu ujenzi wa nyumba za wanajeshi. Kwa hiyo na mimi niungane na wenzangu nikuombe Naibu Spika na Serikali kwa ujumla hebu twende sasa tuwaangalie wanajeshi wetu haswa kwenye makazi salama ambayo wanaishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wanajeshi wetu wanafanyakazi kubwa sana na kama Serikali itafika mahala tukatenga bajeti leo tunazungumza kuhusu vijana hawa wanaotoka JKT, wanafanya shughuli gani tunawaacha idle, kama tumeweza kupeleka fedha tukatunga sheria, tukasema sasa tunatoa asilimia 10 kwa ajili ya wajasiriamali kwenye manispaa zetu, kwanini Serikali sasa isijiwekeze tukasema sasa tunaamua sasa tutengeneze kiwanda kimoja kikubwa ndani ya nchi yetu tutafute wabia, lakini hawa vijana wetu kwa sababu wengi wanakuwa wataalam kutoka huko jeshini waende wakafanye kazi kwenye viwanda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii rai naitoa kwasababu hawa vijana wako wengi sana na kila muda tunapowachukua kuwapeleka kule Jeshini kwenye mafunzo reaction yake inakuwa kubwa ya ukomavu wale vijana. Lakini kwenye ukomavu wao hatuwajengei sympathy ya kurudi kule kwenye maeneo wakawa wana uwezo wa kujitegemea. Tutengeneza mazingira, kama tumeelemewa basi twende na njia mbadala sasa ya kufika mahali tukasema sasa vijana wetu hawa tunawatafutia activity yoyote ile ambayo inawezekana wakaweza kuishi na kufanya shughuli zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru na niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, na mimi nichukue fursa hii kukushukuru kwa kuweza kuchangia Wizara hii ya Uvuvi na Mifugo, lakini inawezekana Wabunge tukazungumza sana humu ndani, lakini bila kuelewa au kujua kwamba tunakoelekea kwenye Wizara hii ili kuleta tija ni wapi.

Mheshimiwa Spika, tunayo bajeti ya shilingi bilioni 121 bajeti hii kama itaweza kutoka kwa wakati na ikafika kwenye maeneo husika na ikaweza kufanya kazi haya mengine ambayo ni changamoto ndani ya Wizara hii inawezekana yakapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kule kwetu Mtwara tuna bandari lakini tuna bahari kubwa mno na bahari ile takribani ndani ya miaka miwili iliyopita tumeshakamata meli zaidi ya mbili na zile meli ni meli za kigeni zinakuja kuvua kwenye eneo letu. Lakini meli ya kwanza imekamatwa ikiwa ina tani zaidi ya 150,000 za samaki, meli kubwa na samaki hawa wanavuliwa kwenye bahari za kwetu lakini kikubwa zaidi ambacho tunaweza tukapiga kelele tunao wavuvi, wavuvi hawa ni wavuvi ambao tunasema ni wajasiriamali, lakini bado Wizara haijapeleka kuwatambua hawa wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa mfano leo tunazungumza kwamba mvuvi anayekwenda kuvua ambaye hana boti ana mtumbwi tu tunamwambia aende akavue mita 50. Mita 50 unazizungumzia pale Nungwi na mita 50 ili aweze kuzama mita 50 lazima awe na mtungi wa gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwangu pale Mtwara hawa wavuvi hakuna aliyeruhusiwa kuingia baharini na mtungi wa gesi. Sasa tukienda Dar es Salaam tunakuta kuna wavuvi ambao wanatumia mitungi ya gesi, sasa sielewi hizi sheria zinafanyaje na tunaangalia wapi watu wanahaki na wapi watu hawana haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna suala la uvuvi wa usiku, leo ukienda Dar es Salaam wako matajiri wakubwa wanavua mchana na matajiri wale wana maboti makubwa na wameruhusiwa, na kazi hii yote anafanya Katibu Mkuu ndiyo mwenye maelekezo ya kuwaelekeza kwamba matajiri waende wakavue mchana, maskini waende wakavue usiku, athari za uvuvi wa usiku kwasababu unapokwenda kuvua usiku, sisi ni watu wa baharini kuna maeneo yanakuwa na miamba, unapokwenda na jahazi au na chombo mwamba huwezi kuujua usiku, lazima ufike mahala uchemke ndiyo utakapojua kwamba hapa ninapoelekea pana mwamba.

Mheshimiwa Spika, Mtwara yenyewe ukizungumza Kilambo, Mtanga Mkuu, Kianga, Mikindani hapa ninapozungumza takribani ya watu zaidi ya 100 wamepotea baharini, wamefariki. Sasa huku tunakokwenda tunakoelekea Wizara yetu bado haiwawezeshi wavuvi wadogo, kinachofanya sasa hivi Wizara bado inakwenda kuwamaliza wavuvi wadogo.

Natoa mfano hawa wanaumoja wao wana asasi zao, lakini leo Katibu Mkuu unashindwa kuwaita viongozi hawa wa wavuvi mkakaa nao mkajadiliana. Lakini ukiangalia kwenye mijadala yao yote, katika paper zao zote ni za kiingereza, wale wamesoma darasa la nne hamna aliyefika hata darasa la saba wale viongozi wote wa uvuvi, wanakwenda kuelewa kitu gani? Lakini mnapitisha mle sheria, kwamba hatuwezi kuvua hapa na ring net. (Makofi)

Mheshimiwa Hayati Magufuli wakati akiwa kwenye Wizara hii alileta hapa waraka na mkakubaliana Bunge zilizopita kwamba ring net iwe sahihi kwenda kuvua sasa leo kwanini nyavu za ring net zinapigwa marufuku na wavuvi wanakamatwa? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Hassan.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niseme nikushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia Wizara ya Habari, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukizungumza suala la michezo ndani ya nchi yetu inawezekana tukazungumza kwa mapana na marefu sana kwa muda mrefu lakini bila kuelewa changamoto tulizokuwa nazo au kupata tija juu ya michezo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka nianze kwenye masuala ya mchezo wa mpira. Hatuwezi kuzungumza kwamba tunakwenda kucheza mpira bila kujiandaa, lakini mara nyingi nimekuwa nasilikiza hotuba za viongozi wetu wanatueleza kwamba Tanzania ni kichwa cha mwendawazimu, lakini haya yote yanakuja kwa sababu hatuna maandalizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la viwanja hatuwezi kulibeza, inawezekana tukawa na academy nyingi za kutosha, lakini kama hatuna msingi wa kutengeneza viwanja vya kutosha, hizi academy zitakwenda kuchaza wapi mipira.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunavyo viwanja vya Chama cha Mapinduzi, viwanja hivi mimi nadhani nimeshiriki wakati niko Hai nilijenga kiwanja pale kikubwa cha mpira na nadhani kiwanja sasa hivi kiwanja kile kinatumika, lakini nilivyofika Iringa niliboresha kiwanja cha Iringa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanja hivi vinahitaji kugharamiwa, lakini ukiangalia mapato yanayopatikana kwenye viwanja vile CCM nadhani inapata kwenye asilimia 20 ya mapato. Lakini tunapoingia sasa kuvikarabati viwanja vile mzigo unabaki kwa Chama cha Mapinduzi. Sasa angalizo langu tuna fedha sisi ambazo zinatoka FIFA kwa ajili ya kuboresha masuala yote ya mpira katika chama chetu cha mpira, lakini tujiangaliea na tuangalie kwamba je fedha hizi zinatumikaje kwenye suala la mpira? Lakini leo tuna vilabu timu nyingi zinakwenda kwenye awamu ya kwanza zikishapanda daraja, awamu ya pili timu zile zinatelemka daraja. Lakini timu hizi zinatelemka daraja kwa sababu tayari hatujafikia malengo ya kuzilea hizi timu kwa mfano mimi ninayo kule timu ya Ndanda, toka inacheza ligi kuu inatoka Mtwara timu ya Ndanda wanasafiri kuja Dar es Salaam lazima ungo utembee, lakini kuna wafadhili ambao wanaifadhili TFF, lakini ukiangalia kwenye kasma za fedha ambazo wanapewa kila klabu kwenda kuendeleza suala zima la mpira hawawezi ku-move kwenye suala zima la mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, angalizo langu leo Azam wametoa fedha nyingi sana, fedha hizi Mheshimiwa Waziri usipokuwa nazo karibu, hizi fedha zitaishia mikono ya watu, kama kuna fedha za FIFA zinakuja kwetu kwa ajili ya kuboresha mpira na fedha ni nyingi sana inayokuja Tanzania, lakini vilevile tumeshindwa kabisa hata kui-maintain timu yetu ya Taifa tutaweza haya mabilioni ya Shilingi yanayokuja, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli nikuombe kwenye suala hili la mpira kwetu Tanzania kwanza tuangalie kwenye viongozi wa TFF, hawa wanaweza wakatuvusha? Lakini la pili kuangalia mfumo wenyewe wa mpira tunaocheza Tanzania, tunazungumza kuhusu wachezaji wa kigeni, hatuwezi kuwakwepa wachezaji wa kigeni, wachezaji wa kigeni lazima waje na lazima wacheze kwa sababu hatuja waandaa wachezaji wetu humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mchezaji wa Kitanzania akishaingia amecheza Simba, amecheza Yanga na jina lake tayari limeshakuwa kuwa kubwa siku kesho anakwenda kucheza mpira leo anatafutwa yuko baa, kwa namna moja au nyingine wachezaji wetu hili lazima tulizungumze bado hawajajitambua kama mpira ni ajira. Wachezaji wa wenzetu wa kigeni wanakuja kucheza mpira Tanzania kwa sababu wanaelewa mpira ni ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Wizara ijielekeze sasa kwenye kuangalia mazingira yote ya mpira, ukiangalia pale Brazil kuna wachezaji wa zamani, lakini wale wachezaji wote wa zamani wanapomaliza muda wao wa kustaafu wanakuwa kuna chombo mahsusi ambacho kinawaweka kwa ajili ya kuwa makocha. Lakini leo ukiangalia Tanzania timu zote kubwa ukienda Namungo, Simba, Yanga na timu zingine zote kuna makocha ambao si wa zawa ni makocha wa nje, lakini timu za Brazil mnazoziona wanacheza mpira tunaziita samba wale kule kuna wazawa wenyewe ambao kuna chuo pale kinafundisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi niombe tujielekeze na sisi sasa kufundisha makocha tunaposema sasa tunataka tusome lazima tuwe na walimu, hatuwezi kuzungumza kwamba tunataka tusome wakati hatuna darasa, walimu tunasema tunakwenda kusoma kusomea mpira, ni kitu ambacho hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi wamezungumza kuhusu academy, academy hizi zina gharama kubwa sana katika bajeti hii ya Wizara niliyoiangalia sijaona sehemu ambayo Wizara inakwenda kujikita kwenda kuendesha haya madarasa ya chini ya watoto wetu ili waweze kupanda. Leo ukiangalia inawezekana tukamzungumzia Messi amekulia kwenye academy ya Barcelona na amekaa pale na wachezaji kadhaa, amelelewa, amefundishwa mpira toka akiwa na miaka mitano leo hii anaonekana mchezaji mkubwa duniani ambaye analipwa fedha nyingi duniani. Tunashindwa nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ni mambo ambayo Mheshimiwa Waziri anatakiwa afanye sasa maamuzi kwamba sasa tunaingia, tutengeneze academy na vijana wetu waweze kucheza mpira. Mimi nina imani sana kubwa mtoto ukimfundisha akiwa mdogo ni mwepesi sana kushika kile kile unachomfundisha, lakini sasa sisi bado hatujajajiwekeza huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamezungumza kuhusu BASATA; kama kuna chombo ambacho kinawezekana baadaye kikaenda kuua mziki wa kitanzania ni BASATA. Hili inawezekana Wabunge tukazungumza hapa na hatuzungumzi kwa mapana na marefu sana, lakini chombo hiki hakipo kwa ajili ya kuwa-accomadate wanamuziki, lakini chombo hiki kipo kimaslahi zaidi na matendo yao wanayoyafanya, yako ambao wanayafanya hata wanamuziki wenyewe, wasanii wenyewe wamekata tamaa na chombo hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuwa na chombo yaani leo tunampishi anasema anampikia Mtenga ugali, lakini Mtenga anatoka anakotoka akienda kwenye sahani anasema ugali huu mimi siwezi kula, ni vitu ambavyo haziwezekani. (Makofi)

Kwa hiyo tuangalie Mheshimiwa Waziri afike mahali aiangalie hii BASATA, lakini arudi tena kwa upande wa TFF nenda pale ukaangalie viongozi wako wengine wana miaka 20 pale TFF hawa waliokuwa miaka 20 ndio leadership, wale wanapanga viongozi, wanajua mambo yakufanya, wanajua deal ziende wapi. lakini wanajua mpira wao wanataka kuuendesha kwa namna gani, hatuwezi kumove kwa viongozi wale ambao ni watendaji pale TFF hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakuwa tunajidanganya, hivyo leo kama tuna premier league tuna timu zaidi ya 12 au 14, lakini timu hizi kama tungekuwa tuna watu wenye uwezo wa kufikiri tungefika mahali tukasema bwana kila timu kwa mfano kwangu mimi kule tuna timu ya Ndanda pale tuna Dangote; TFF wangekwenda kuzungumza na kampuni ya Dangote, wakafanya makubaliano wakawa mdhamini namba moja, lakini kuna Breweries, sijui Kilimanjaro kuna kampuni gani; vilabu vyote tusifike mahala hapa tukamsifia Mheshimiwa Waziri Mkuu kesho inawezekana Waziri Mkuu inawezekana akasema jamani nguvu zimeniishia za kufanya hii kazi ya mpira nani anamsaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tutengeneza sasa impact ya kujua kwamba tunawatafuta wawekezaji na hili ni suala la kulibeba Serikali sio suala la vilabu hivyi, kwa sababu vilabu vinakotokea mpaka vinapanda madaraja haya wanakwenda hawa kwa kuchangishana fedha zao. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha ahsante sana.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti. Kwanza nianze kwa kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini niwashukuru wasaidizi wake kwa ujumla nimshukuru Waziri wa Fedha na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie dakika tano hizi kwa mambo kidogo ya msingi, tunapotaka kuzungumza uchumi wa nchi yetu lazima tujikite kwenye viwanda, lakini tunapotaka kuzungumza uchumi wa nchi yetu lazima tujikite kwenye kilimo, lazima tuwe na watu ambao wana nguvu za kutosha na watu wenye uelewa. Nini maana yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu walizungumza kuhusiana hapa na vijana ambao wapo mtaani wamachinga. Genge hili la wafanyabiashara wadogo wadogo limekuwa ni kubwa mno, lakini bado sijaona kama Serikali ikiwa inajikita kuelekeza wapi iwapeleke hawa watu. Lakini nataka nitoe mfano mmoja, vijana hawa wanapanga biashara barabarani, lakini vijana hawa tayari wanafamilia zao majumbani kwao. Imetokea siku kijana huyu ambaye yupo barabarani ameumwa, kwa hali ya kawaida hawezi kumchukua mkewe aende pale barabarani akapange zile nyanya au akapange zile nguo zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa jambo lingine kwenye wamachinga hao hao kwa hali na mazingira ambayo yapo, hatuwatengenezi hawa vijana kwenda kujitegemea. Kwa sababu, kwanza hawana insurance hawakopesheki kwenye mabenki vijana hawa. Sasa, rai yangu tunayo maeneo sisi ya kutosha, maeneo haya Serikali sasa ifike mahali itambue kwamba, inaweza ikawajengea maeneo ya kisasa. Kwanza, faida yake baada ya kuwajengea maeneo ya kisasa tutaweza kupata kodi, vilevile kwenye fursa sasa ya kuwajenga vijana wetu kutoka kwenye umachinga kwenye wafanyabiashara wakubwa. Nina imani kubwa sana hata Mheshimiwa Shigongo ametokea kwenye umachinga, lakini leo amekuwa mfanyabiashara mkubwa kwa sababu yeye aliwezeshwa. Ninaiomba Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie masuala ya bandari na uchumi. Masuala ya bandari na uchumi tunazo bandari katika nchi yetu, lakini napenda sana niizungumzie bandari ya Dar es Salaam, niizungumzie bandari ya Mtwara. Ukiangalia bandari ya Dar es Salaam kwa shughuli zinazofanyika kila siku, bandari ile inaonekana kwamba iko tight. Lakini kwa nini tusifike pahali tukapanua wigo tunayo bandari ya Mtwara tunayo bandari ya Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tukienda pale Dar es Salaam tunakuta zaidi ya meli 20 au 30 ziko hangar zinasubiri kupakua pale mzigo, lakini bado tunawapelekea kupata hasara kubwa jinsi meli inavyokaa kule hangar inasubiri iingie pale. Kuna service charge ambazo zinaingia kutokana na gharama za watu ambao wamekodi meli zile. Rai yangu, tutumie bandari sasa ambazo tayari zina uwezo wa kubeba hizo meli kubwa ili tupate fursa zingine za kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nizungumze Mheshimiwa Naibu Waziri leo hii tunaishukuru sana Serikali yetu, kwa kweli mimi kwangu pale Mtwara haya mafuriko yaliyotokea hali ilikuwa ni mbaya sana. Nilivyoambiwa ninapewa milioni 500, kwanza nilisali na nikasema eeeh Mama nakushukuru sana na Serikali yako. Haijawahi kutokea katika nchi yetu kwamba, Serikali imeamua kutoa package moja kwenye mzunguko mmoja kwa Majimbo yote. Kwamba leo mnapata milioni 500 kila Jimbo, kwa ajili ya matengenezo ya barabara zetu. Hongera sana Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazungumzia zao letu la korosho la Mtwara, tulikuwa tuna Mfuko wa Export Levy. Mfuko ule ambao Serikali iliuchukua lakini mpaka leo hii kila tunapozungumza Wabunge wa Mtwara kuzungumzia juu ya fedha zetu za export levy bado hatujapata muafaka na hatujaambiwa nini kinaendelea. Rai yangu kwako Mfuko huu ndio ulikuwa unazalisha korosho kwa asilimia kubwa. Kwa sababu, ulikuwa una uwezo wa kuwenda kununua pembejeo, kwenda kuwasaidia wakulima na wakulima walikuwa hawana shida ya pembejeo kwa sababu tayari walikuwa wana mtaji wao, niiombe Serikali, nina imani Serikali yetu ni sikivu sana na inaweza kutusaidia, mfuko huu tunaomba urejeshwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine niishukuru Serikali, niishukuru Serikali kwa mpango ambao umeletwa wa NLG tunakwenda kujenga viwanda Lindi. Viwanda hivi ambavyo vinakwenda kujengwa Lindi, mimi niiombe tena Serikali gesi inatoka Mtwara na kama gesi inatoka Mtwara, basi kwenye Wizara ya Uwekezaji muda sasa umefika wa kuiangalia Mtwara kama Mtwara, iwe nayo ni zone ya kimaendeleo. Kwa sababu haiwezekani kwamba gesi iko Mtwara, lakini Mtwara hatuwajibiki kwenye masuala mazima ya gesi. Nilikuwa naomba, nimuombe Waziri wa Uwekezaji kwamba, hili ni jukumu lake na ana mamlaka makubwa sana ya kuweza kutusaidia wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini mimi niungane na wenzangu kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na hasa anavyotusikiliza Wabunge tunavyokuwa kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano na vilio vyetu huwa anavisikia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niende nimshukuru Mheshimiwa Waziri, Ndugu yangu Innocent, kwa kweli Waziri huyu sijui niseme nini kwenye Bunge lako hili tukufu. Ni kijana msikivu, lakini ni kijana ambaye anaelewa matatizo ya kila Mbunge kwenye jimbo lake, ni kijana ambaye simu yake saa 6, saa 8 za usiku anakupokelea simu; kwa hiyo, tumpongeze sana na Mungu ambariki. Lakini vilevile wasaidizi wake wamekuwa ni marafiki sana kwa Wabunge wote wawili, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nishukuru katika jimbo langu nimepata shilingi milioni 440 za madarasa ya sekondari, naishukuru sana Serikali, namshukuru Mheshimiwa Rais. Lakini nashukuru nimepata shilingi milioni 260 kwa kituo cha afya pale Kata ya Ufukoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nianzie kwa kituo cha afya. Kituo hiki cha Afya ili kikamilike kinahitaji lazima tuwe na jiko ambalo linawezekana likawepo pale lakini tuwe na eneo la kufulia nguo, ambulance, sasa tayari kile kituo kimekamilika lakini wauguzi bado hatujawapata. Kwa hiyo, niombe tunapoelekea kwenye kutekeleza haya mambo adimu kwa wananchi, huduma za wananchi tunapozimaliza kwenye majengo twende kwenye huduma nyingine ya watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, Jimbo la Mtwara Mjini tulikuwa tuna mradi wa kufunga taa barabarani; na mradi huu ulikuwa mwaka 2017/2018. Lakini kwenye bajeti ya mkandarasi ya malipo kwenye mradi huu ilielekezwa apewe shilingi 1,065,000,000, lakini kwa sintofaham Mkurugenzi na watumishi wengine ambao wana uwezo au wana mamlaka ya kulipa fedha hizo walilipa fedha 1,653,000,000; kuna fedha karibu milioni 588 ambazo zimelipwa nje ya mkataba. Fedha hizi ni fedha za wananchi, na CAG alishaelekeza fedha hizi zirudishwe lakini mpaka leo ninapozungumza fedha hizi zipo mikononi kwa watu na hakuna hatua yoyote ambayo imechukuliwa mpaka sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niishukuru Serikali hasa kupitia TARURA, lakini nataka nitoe angalizo au nitoe ushauri majimbo yapo tofauti, Jimbo la Mtwara Mjini huwezi kulinganisha na Jimbo la Nanyamba, Jimbo la Mtwara Mjini huwezi kulilinganisha na Jimbo la Kilombero, haya majimbo yapo tofauti. Lakini tunaingia kwenye migao ya fedha tunasema kwenye package ya migao ya kila jimbo TARURA tupeleke labda shilingi 1,500,000,000 au tupeleke shilingi bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo manispaa, zinakusanya almost zaidi ya shilingi bilioni 60 kwa mwaka na zipo Halmashauri hazina uwezo wa kukusanya hata shilingi milioni 200 kwa mwaka. Kwa hili mimi nilikuwa naiomba Wizara twendani tuangalie kwenye mazingira haya kama tunataka kuziinua hizi Halmashauri na manispaa basi tuangalie ni manispaa gani, Halmashauri gani ambayo ipo chini sana ili tuweze kuzisaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya mradi ya TACTIC wenzangu wamezungumza, miradi hii inatakiwa iende na wakati. Jimbo la kwangu Mtwara Mjini, ikinyesha mvua leo hapa Bungeni mimi nakuwa na wasiwasi, nitapigiwa simu ngapi mafuriko! Mradi huu tunauomba uende kwa wakati kwa sababu toka tumesikia mradi huu zaidi ya miaka miwili, kila siku mazungumzo yanafanyika. Ni mazungumzo yapi yasiyokwisha? Kwa hiyo, nikuombe mtusaidie kwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna jambo la Madiwani, tulikaa kwenye Bunge letu hili hapa tukaelekeza kwamba tufike mahala kwamba Serikali Kuu mishahara yao ipitie kwenye Serikali Kuu. Lakini pamoja na hizi posho ambazo zinapita kupitia kwenye Serikali Kuu, hali ya Madiwani ni mbaya, ni mbaya. Hali ya Madiwani kwa kweli inapelekea Diwani anashinda kwenye Halmashauri utafikiri yeye labda ni mtumishi pale; sasa kwa namna moja ama nyingine Diwani huyu hawezi kwenda kuhoja chochote chenye maslahi ya wananchi kwenye eneo husika. Hili mimi naomba tuliangalie sana, Madiwani hawa waongezewe posho, wanafanyakazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nishukuru kwa Hospitali ya Rufaa pale Mtwara Mjini. Nataka niombe kwa ridhaa yako nilizungumzie hili, hospitali imejengwa pale, lakini leo tukihitaji huduma ya simu kwenye jengo lile huduma ya simu haipatikani. Lakini unapozungumza na wahusika wanakueleza kwamba mkitaka kupata mnara basi mamlaka zinazohusika zaidi ya miezi sita watoe kibali. Jamani tupo nchi gani? Kibali cha mnara mmoja kinachukua takribani miezi sita! Hivi leo tupo pale tunataka sasa tufungue ile hospitali yetu, kuna wagonjwa, Hospitali ya Rufaa itaunganisha na mkoa mmoja wa Mtwara, Lindi na Ruvuma; mtu yupo Ruvuma anataka kujua mgonjwa wake anaendeleaje tunampataje? Hebu sasa kwenye huduma hizi nikuombe tufike mahali sasa tujiwekeze kwenye mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumejenga shule na tunaishukuru sana Serikali na iendelee kutusaidia kwenye majimbo yetu. Shule hizi tayari zimeshajengwa, lakini walimu kwenye shule hizi hakuna, majengo yale yapo lakini walimu hawapo. Kwa hiyo, Serikali ichukue hatua za kila aina tuweze kupatiwa walimu kwenye haya madarasa mapya ambayo tumejenga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye Jimbo la Mtwara Mjini sisi tunatofauti ya walimu shule za msingi tunataka tusaidiwe walimu zaidi ya 200 katika shule zetu za msingi. Lakini shule za sekondari katika Jimbo zima tunahitaji tupate zaidi ya walimu 300. Kwa uwiano huu mnaouona je, tuna elimu kabisa ambayo inawezekana mbadala wake watu wakapata elimu sahihi? Kwa hiyo, nilikuwa ninaliomba hilo ili tusaidiwe na sisi inawezekana tukafika mahali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili ni janga ambalo nataka nilizungumze wako wakandarasi wanapewa na TARURA kwenye maeneo yetu; na sielewi kwenye hii mikataba ni sheria gani ambazo zinatumika. Mkandarasi anashinda tender, anaposhinda tender kabla hajaingia site anawezekana akapewa period yake, labda ndani ya wiki mbili kwa mujibu wa sheria au mwezi mmoja haingii site. Lakini inafika takribani mpaka miezi minne, miezi mitano mpaka miezi sita mkandarasi hajaingia site, lakini tayari TARURA wameshampatia mkandarasi asilimia fulani ya mradi ule. Matokeo yake wanatuambia bwana mkandarasi ameshindwa kutengeneza barabara, lakini katika fedha ambazo tumeshampatia nadhani ana-insurance bank yatalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo ni kweli tumefikia hapa na kama sheria zipo hivyo kwa nini tusiingie hapa tukabadilisha hizo sheria? Kwa hiyo, nataka nikuambie haya mambo yanafanyika na kwenye Jimbo langu ndio mchezo ambao unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niwashukuru sana Mameneja wa TARURA pale wa Wilaya na ninamshukuru kwa sababu amekuwa ni mtu ambaye anapambana sana na wakandarasi na shida ipo. Kwamba, leo mkandarasi anatoka anakotoka yeye…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante ya pili, hiyo mengine andika.

Mheshimiwa Chaurembo, jiandae Mheshimiwa Sanga, jiandae Mheshimiwa Kanyasu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninakushukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya hasa ukilinganisha kwenye Jimbo langu la Mtwara Mjini iko miradi ya mfano ya mabilioni ya shilingi ambayo yanaendelea sasa hivi kufanyika, ni vema nikamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Makamu wa Rais Mheshimiwa Isdory Mpango, nimshukuru Waziri Mkuu na hapa nigande kidogo niseme kwamba, Waziri Mkuu nakushukuru sana kwa mambo mengi ambayo umekuwa unanishauri, unanisaidia kwenye Jimbo langu kwa kweli nakutakia kila la kheri Mwenyezi Mungu akubaliki sana. Pia kwenye shughuli ya Mwenge Mheshimiwa Waziri Mkuu umetutendea haki Wananchi wa Mtwara, kwa hiyo tunakupa pongezi la Wanamtwara wamenipa salamu tukuambie kwamba wanakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo zaidi ya matatu ya kuzungumza. Jambo la kwanza tunazungumza uchumi ndani ya nchi yetu, tunapozungumza uchumi ndani ya nchi yetu hatuwezi kuwa na uchumi ambao ni bora kama hatutakuwa na viwanda ndani ya nchi. Nimeona nilizungumze hili tukiangalia zone ya Mtwara na Lindi ni watu ambao tunazalisha au tuna maeneo mengi ya madini lakini madini haya yana uwezo wa kutengeneza gypsum yana uwezo wa kutengeneza zana za aina nyingi za ujenzi. Ninaishauri Serikali muda sasa umefika kwa sababu material haya tusifike mahala tukawa tunayatumia vibaya, material haya kama tungefika sehemu tukawaleta wawekezaji wakaweka viwanda, nadhani tungepiga hatua kiuchumi na hata vijana wetu wangepata ajira za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo ambalo mara nyingi sana nimekuwa nazungumza kwenye Bunge hili lako Tukufu, inawezekana ninaeleweka au nisieleweke hata hivyo Wabunge wanzangu naomba kwa hili mni-support. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara tulikuwa na mpango wa Mtwara Corridor na hii Mtwara corridor package yake tunazungumza bandari, tunazungumza airport, tunazungumza na reli ya Liganga na Mchuchuma, Mbamba Bay. Nimesikiliza taarifa hapa na ripoti ya Waziri Mkuu sijasikia masuala ya Reli ya Mtwara Mbamba Bay. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tumefika eneo Serikali tumewekeza bilioni 157 kwenye Bandari ya Mtwara na ninadhani uwekezaji ule umewekezwa kwa ajili ya kufungua njia na fursa za kiuchumi, ni vyema sasa nikaishauri Serikali kwamba mpango wa kutujengea reli bado ubaki palepale na jitihada ziongezeke ili reli tupate ya Mtwara Mbamba Bay. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ujenzi wa daraja, kwanza ninaishukuru Serikali mlitujengea daraja kule Mtambaswala, tunachozungumza kuhusu daraja na Mto Ruvuma tunazungumza mileage na hasa kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara Mjini kuna kiwanda cha Dangote kiwanda hiki kinapeleka cement mpaka Katavi, lakini kiwanda hiki hakina uwezo wa kupeleka cement Pemba, Mozambique na maeneo mengine kwa sababu ya mileage. Hoja yetu Wanamtwara tunasema mtufungulie daraja pale Kilambo, kutoka Mtwara Mjini mpaka unaingia Kilambo ni kilometa 70, ukitoka Kilambo mpaka unaingia Mocimboa da Praia Wilaya ya kwanza ya Mozambique pana kilometa 56. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mmoja tu, leo Waziri wa Uchukuzi alitembelea kwenye Bandari ya Mtwara akakuta kuna bomba nyingi ambazo zinakwenda Mozambique ambazo zile bomba ni za watu ambao wanakwenda kushughulika na masuala ya gesi Mozambique, lakini bandari yao ambayo wanaona ni karibu kuitumia ni Bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bomba zile ni mwaka wa pili sasa zipo bandarini hazina uwezo wa kwenda Mozambique, kwa sababu njia ambayo ipo ambayo tungeweza kuitumia, mileage zinawakataa na gharama ni kubwa sana. Sasa naomba, leo tunaizungumzia Dangote kama Dangote, mfanyabiashara mmoja mkubwa sana. Cement mfuko mmoja TRA wanachukua zaidi ya shilingi 3,000, lakini cement ya Mozambique mfuko mmoja kwa hela ya kwetu ni shilingi 35,000 kwa hela ya Tanzania. Dangote anasema kama daraja hili litapitika, nitauza cement kwa shilingi 16,000. Tunakwenda sasa kufanya biashara kubwa na TRA ya Mtwara kiujumla itakuwa imepata mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme suala hili halihitaji kuwepo na profesa, halihitaji mtu awe na degree kwenye ufahamu wa suala hili. Tumsaidie Rais. Rais wetu sasa halali usiku na mchana anahaingaika kuona ni jinsi gani Tanzania ataifikisha pale wanapohitaji Watanzania. Tunakaa humu tunahangaika na ushuru wa PP, ushuru sijui wa mbaazi, wakati item tunazo wenyewe za kuzitengeneza tukapata fedha kwenye Serikali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuliotembea tumekwenda India juzi juzi, tumeona kule sekta binafsi wanatengeneza madaraja, nchi inafunguka, wanatengeneza reli, nchi zinafunguka, hapa tunaogopa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitu vingine kwa kweli hata kuvisema vinaleta simanzi ndani ya Bunge letu hili. Mtwara ni sehemu ya Tanzania, lakini mfano mmoja, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwezi mmoja na nusu uliopita alikuwa anakwenda Lindi, wananchi wa Mtwara wamemsubiri kuanzia saa 2:00 alivyopita pale mpaka saa 10:00 wako juani, wanamsubiri Rais wao kwa mapenzi makubwa. Sasa hili siyo kwamba ni suala la Mbunge, maana leo kuna hoja zinaongelewa, suala hili ni la Mbunge. Suala hili siyo la Mbunge, ni la kitaifa. Tunapozungumzia kufungua mipaka, tunazungumzia fursa za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili mimi nilitaka nilizungumze kwa mapana na marefu sana. Tunaomba wenye mamlaka mtusaidie. Mimi nimekwenda mbali zaidi, tumewasiliana na wenzetu wa Mozambique, sisi ndio majirani, wanasema sisi tuko tayari, ni suala la Waziri wa Fedha, Waziri wa Uchukuzi, sawa bwana, tuangalie ni mpango gani tunaweza tukaenda tukamaliza hii fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya mambo ni ya msingi sana, lakini kuna suala moja la mwisho nalotaka niliseme…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mtenga, na muda wako umeisha. (Makofi)

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru na nikuombe kwa ridhaa yako nirekebishe jina. Naitwa Hassan Seleman Mtenga.

Mheshimiwa Spika, nami nianze kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anazozifanya kwenye suala la kulihudumia Taifa, hasa Jimbo la Mtwara Mjini.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumshukuru Waziri wa Viwanda na Biashara. Dada yangu kwa kweli anastahili sifa na anafanya kazi ya kumwakilisha Rais. Pia Mheshimiwa Waziri amepata msaidizi mzuri sana, Katibu Mkuu, Dkt. Hashil, naweza nikasema ni Katibu Mkuu wa mfano; moja ya Makatibu bora ambao wanapokea simu za Wabunge any time. Huyu bwana, kwa kweli anatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Liganga na Mchuchuma, tunarudi nyuma tunasema kwamba huu mfupa ambao ulimshinda fisi. Kwa ushirikiano mkubwa wa Katibu Mkuu na Waziri wa Viwanda na Biashara, nadhani mgogoro huu umefika mwisho, na Watanzania sasa watapata stahiki zao, nikizungumza Serikali kupata mafao kupitia Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ya Viwanda na Biashara ndiyo Wizara mama ambayo inategemea uchumi mkubwa ndani ya Taifa letu. Kwa nini nazungumza hivi? Tunazungumza kwamba tuna viwanda, na tunapozungumza ajira, zipo kwenye viwanda. Sasa tukiangalia Mtwara, Lindi na Dar es Salaam, tunavyo viwanda zaidi ya 5,000 ambavyo vinazalisha chumvi. Viwanda hivi 5,000 ni viwanda vidogo vidogo ambapo huko nyuma tulipoanza ingekuwa sasa hivi, tumeshapata viwanda vikubwa zaidi ya vitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo ambalo kwa kweli linasikitisha sana. Chumvi yetu ya Tanzania imefika sehemu imeuawa na kukosa soko kwa sababu ya mwekezaji mmoja tu. Chumvi hii ambayo sasa hivi imekosa soko, na mara nyingi wataalam wa Kiwanda cha Neel wanasema chumvi hii ina madini ambayo siyo salama kwa binadamu.

Mheshimiwa Spika, unayeniona nimesimama hapa, nimeanza kula chumvi ya Mtwara mpaka umri huu unaoniona, sijapinda mgongo, sijapinda kichwa wala miguu. Sasa hawa wataalam wanaofika mahali wanaua soko na chumvi ya Watanzania eti kwa sababu ya chumvi ya nje, leo chumvi ya Mtwara, Lindi na Dar es Salaam ilikuwa inauzwa Afrika kwa ujumla toka tumeanza, sasa hivi hii chumvi haiendi huko, kwa sababu wataalamu wa Neel wanaagiza chumvi kutoka nje, lakini wana- export kutoka Tanzania kwenda Kongo na Malawi wakati chumvi ya Watanzania ipo.

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri, alitembelea Lindi Mtwara na Kilwa na akaona mwenyewe kwa macho yake chumvi ilivyokuwa nzuri, na chumvi ilivyojaa kwenye maghala, alitoa tamko, akaelezea umma ya Watanzania kwamba kuanzia sasa Neel wasipewe kibali cha kuagiza chumvi nje, wachukue chumvi yetu ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo mengine yanasikitisha sana. Wakati Mheshimiwa Waziri anatoa tamko, Wizara ya Madini imefika mahali wakasema huyu tumpe kibali. Sasa ninashauri, hawa ni Mawaziri wawili, hata kama kuna mambo ya kiutaalamu, anapotoa tamko Waziri wa Madini ambalo linamhusu Waziri kwenye sekta nyingine, basi wakae wazungumze. Siyo anatoka mtumishi mmoja, anasema aah, huyu mwana mama ni mwanasiasa. Tusizungumze siasa kwenye maslahi ya watu. Tunazungumza maisha ya watu wa Lindi, Mtwara na Dar es Salaam wanaozalisha chumvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukija Mtwara ukiwaona wananchi wa Mtwara ambao walikuwa na utajiri wa chumvi, utayemkuta ana kiatu kizuri cha shilingi 60,000, ukimkuta mwananchi mwenye shamba la chumvi ana kiatu cha kuvaa chenye thamani ya shilingi 60,000 mimi nadhani nitatafuta milioni, nikakupatia, kwa hali ilivyo mbaya na wananchi jinsi walivyoathirika na uchumi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali, hawa ni Watanzania wetu, tuna kila sababu ya kuwasaidia. Tulipofikia sasa hakuna haja ya kuagiza chumvi nje. Katika viwanda hivi nazungumza zaidi ya 5,000 wamekosa ajira watu wangapi? Yuko mzee mmoja, Mohamed Nassor pale Mtwara, alikuwa na mashamba yake ya chumvi, lakini kwenye uzalishaji alikuwa ni mzalishaji bora. Kulikuwa kuna akina mama pale zaidi ya 400 ambao wanafanya kazi na wanalipwa, wale akina mama 400 wote wamepoteza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa unaweza ukatuona tunazungumza kwa sauti kubwa sana.

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, taarifa tena ndugu yangu?

SPIKA: Mheshimiwa Mtenga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Stanslaus Nyongo.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea.

TAARIFA

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, nomba nimtaarifu mzungumzaji kuwa Tanzania ina mahitaji ya chumvi tani 250,000 kwa mwaka, na tunaingiza asilimia 70 kutoka nje, na wakati sisi tuna uwezo wa kuzalisha chumvi zaidi ya tani 300,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa hiyo mchangiaji.

SPIKA: Mheshimiwa Mtenga unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea taarifa hiyo kwa mikono yote miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumze kuhusu Wizara hii. Nimeangalia bajeti ya viwanda na biashara, nadhani inafika kwenye Shilingi bilioni 109, lakini huu ndiyo uti wa mgongo wa Taifa hili. Leo tunakwenda kuweka bajeti ya Wizara fedha hii, na kwenye uhalisia hatuwezi kuwapata wawekezaji bila Ofisi ya Katibu Mkuu, Waziri mwenye dhamana, wakazunguka nje na ndani kutafuta wawekezaji, hela hii itakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kama kuna uwezekano, safari tunayokuja, ya bajeti nyingine, Wizara hii tuiangalie kwa jicho la huruma. Fedha hii iliyotengwa ni ndogo mno. Tuna haja ya kuwa na wazawa ambao wanaweza kuwa na viwanda ndani ya nchi hii, lakini kwa mfumo uliokuwepo sasa, wa mabenki yetu, hatuwezi kuwapata wazawa kwa asilimia 70 ambao wanaweza kuwa na viwanda ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, leo wako watu walikuwa wanatafuta LCs za benki wapate dhamana ya mtaji wafungue viwanda. Wamesaga lami, wamesaga viatu zaidi ya miaka saba, nane, lakini leo anakuja mtu na briefcase hapa. Tulimsikia Mheshimiwa Rais analalamika hapa, anasema kaja mtu mmoja hapa, kaingia huku, kaingia huku, hana nyumba hana kitu gani, amechukua mabilioni ya Shilingi na ameondoka. Rais wetu analalamika.

Mheshimiwa Spika, haya inawezekana humu tukaishauri Serikali kila mkoa tuunde pale Kamati, wale wafanyabiashara waliotafuta LCs za benki na wakitaka mikopo mikubwa, vikwazo gani wamekutana navyo? Tutapata majibu humu, maana yake inawezekana...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 Mheshimiwa malizia.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, inawezekana tunakuja humu tunajifungia, tunazungumza, lakini yaliyokuwa nyuma ya pazia hatuyajui. Kama tunataka kumsaidia Rais kwa dhati kabisa, hebu ifike mahali sasa tuwe tuna maamuzi. Nimeshauri kuhusu kiwanda cha Neel, biashara ya kuleta chumvi, nadhani ifike mahali tuseme, inatosha sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kukushukuru kwa kupata nafasi hii adhimu ya kuchangia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Nami niungane na mwenzangu kumshukuru Rais wetu mpendwa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan na ni wajibu wetu kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa sababu kwenye jimbo langu ni mabilioni ya shilingi ambayo yameingia kwa kipindi kifupi na kazi zinaendelea. Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe pongezi kwa Waziri wetu Mheshimiwa Mbarawa, lakini na Naibu Mawaziri kwa kazi kubwa wanazozifanya kwenye Wizara hii. Kule kwangu siwezi kumuacha Engineer wa TANROADS, Ndugu yangu Dotto, kwa kweli anaiwakilisha Mtwara vizuri na utendaji kazi wake ni mzuri kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maeneo kama kama matatu ya kuchangia, lakini eneo la kwanza ili kupunguza urasimu wa mambo yote ambayo tunayajadili ndani ya Bunge hili. Tunazungumza mambo mengi sana ya msingi, lakini kila tutakalozungumza kwenye Bunge hili linagusa sheria kwenye eneo husika. Sasa kwa nini nimezungumza sheria. Tunaizungumzia sheria leo tunazungumza masuala ya uwekezaji ndani ya nchi yetu lakini kwenye suala la uwekezaji bado kuna sheria ambayo zinatufungwa, tunashindwa kuondoka pale tulipokuwa kuelekea kwenye eneo lingine. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri katika Wizara yake watuletee sheria hapa, hata kesho tuweze kufanya mabadiliko ili tusonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi wagonjwa wa malaria nyumba moja hawawezi wakaamshana kwenda hospitali. Sasa kwa nini nazungumza hivi? Ziko hoja ambazo tunazungumza kuhusu uwekezaji wa bandari. Uwekezaji huu wa bandari kila mtu ana mawazo yake ndani ya Bunge hili, lakini kuna wengine wanasema tuendelee kujifunza, lakini TICTS wana miaka mingi wako pale bandarini na kama ni shule kwenye Serikali wamepata kupitia TICTS. Ni vyema sasa shule ile tulioipata kutokea TICTS twende tutafute wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ambayo inazungumza kwamba bandari yetu ni ndogo, bandari ile imeingia kwenye upanuzi zaidi ya mara tatu, wakati tunaanza Bandari ya Dar es Salaam haikuwa vile. Kama tunampata mwekezaji na tunasema bandari ile itakuwa ni busy zaidi kwenye mikataba tuingize suala la yeye kupanua bandari, ni kitu ambacho kinawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bandari yetu ya Dar es Salaam inatumika na nchi zaidi ya nne na ndio maana tunaiona ipo busy sana. Sasa niishauri Serikali katika Bandari ya Dar es Salaam pamoja na uwekezaji mkubwa tunaotaka kuufanya, ziko bandari zingine ambazo inawezekana vile vile tukazisaidia. Mfano, leo tunaichukua Zambia na Malawi tukasema wafanyabiashara wote wa Zambia na Malawi watumie Bandari ya Mtwara. Tukaichukua Burundi na nchi zingine na Congo waje watumie Bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili inawezekana likatupatia kipato kikubwa sana na hili nimekuwa napiga kelele sana Bungeni. Yawezekana naeleweka au inawezekana nisieleweke, lakini kwa hali nyingine nimshukuru Rais, nilikuwa napiga kelele sana kuhusu Daraja la Mto Ruvuma kule Kilambo. Naishukuru Serikali imeridhia kujenga daraja lile. Daraja lile ukubwa wake inawezekana ukawa zaidi ya kilometa mbili na point au tatu. Katika Afrika inawezekana likawa ni daraja la kwanza kuwa na ukubwa mrefu namna ile ambalo litatumia mabilioni ya shilingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu amefanya maamuzi magumu ya kuwasaidia Wananchi wa Mtwara, lakini ujenzi wa daraja lile sio la wasaidie Wananchi wa Mtwara, daraja lile ni ujenzi wa Kitaifa kwenye rasilimali ya Kitaifa kwenye mapato ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la reli. Tulikuwa na package ya Mtwara Corridor, tunazunazungumza bandari, tunazungumza airport, tunazungumza na reli. Reli ya Mtwara Mbamba Bay imekuwa ipo kwenye makabrasha miaka yote toka mimi nazaliwa na Wabunge wote waliopita kutoka Mtwara wanaizungumzia reli hata kama ilikuwepo na ikaondolewa. Sasa leo Mchuchuma na Liganga tayari tuna madini ghafi na madini haya yanatakiwa lazima tuwe na reli ya ufanisi ili yaweze kusafiri kwa wakati na mzigo ifike ikiwa salama.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, suala la Reli ya Mtwara Mbamba Bay ipewe kipaumbele sasa…

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hassan kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

TAARIFA

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba, kwa mujibu wa feasibility study iliyofanywa mwaka 2016, jumla ya tani 500,038 za makaa ya mawe zilipita kwenye barabara na kwa feasibility study ya mwaka 2022 tani milioni 1,233,000 zimepita kwenye barabara na feasibility study ya mwaka huu tani milioni 2.3 zimepita kwenye barabara. Kwa trend hii naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba anachokizungumza kina make sense kujenga reli ya kusini ili kuokoa barabara zetu kwa maslahi ya Taifa. Natoa wito kwa Mheshimiwa Waziri feasibility study ya ujenzi wa reli hii uanze haraka kwa maslahi ya Taifa na kuwasaidia watu wa Kusini, wamelia muda mrefu, inatosha. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mtenga taarifa unaipokea?

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, microphone zimegoma.

MWENYEKITI: Hamia kwa jirani yako hapo Mheshimiwa.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niko sawa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hassan taarifa unaipokea?

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naipokea kwa mikono yote na miguu na ninampenda sana, mtoaji taarifa huyu ana akili kubwa sana,Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la International Airport Mtwara. Uwanja huu naishukuru sana Serikali namshukuru Rais, tumejenga uwanja zaidi ya shilingi bilioni 14 na something lakini uwanja huu tunazungumza leo katika fedha zote zilizopangwa kwenye bajeti tulikuwa tupate na gari ya zimamoto (fire), lakini kila ukiuliza watu wa manunuzi leo ni mwaka wa tatu tunazungumza kwenye manunuzi ya kuleta gari la zimamoto Uwanja wa Ndege Mtwara, ni mwaka wa tatu tunazungumzia manunuzi. Ni vitu vya hatari sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni Sheria ya Procurement inakuwa hivi, tunatokaje hapa tulipo? Uwanja wa ndege kulikuwa kuna package ya kujenga majengo ya kukaa abiria mpaka leo kwenye bajeti hii nimechungulia sijaona na wala sijasikia. Sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri unapokuja hapa utupe majibu mazuri kuhusu uwanja ule, gari la zimamoto, tunahitaji na jengo la abiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza utanuzi ndani ya nchi haswa wa barabara na mimi naipongeza sana Serikali yangu, imefanya kazi kubwa kwenye miundombinu. Watu ambao wanatoka Mtwara na Lindi wanakwenda zao Dodoma au wanakwenda Morogoro, iko shortcut ambayo inawezekana Wizara ikakaa ikajipanga tutengeneze barabara ambayo ni shortcut. Tunafika mpaka Kibiti, unaingia mpaka Mloka, Bwawa la Mwalimu Nyerere tunakwenda hadi Morogoro. Barabara ile inakuwa ni fupi kuliko gari za mizigo zinazunguka mpaka zinaenda Dar es Salaam, zikitoka Dar es Salaam zitafute Kibaha, zitafute Morogoro, mambo mengine ya msingi yapo kwenye uwezo wetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mtenga, muda wako umeisha.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nyingi anazozifanya za kuwahudumia Watanzania. Vile vile, niwashukuru kaka yangu Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri kwa kazi wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze kuhusu suala la kodi. Wenzangu wengi wamezungumza kuhusu ukusanyaji wa kodi, lakini yako mambo ya msingi ambayo kama Wizara wanatakiwa wayaone na wayaangalie kwa mapana na marefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza nikatoa mfano mmoja, leo kontena linatolewa bandarini na likitolewa bandarini charge zote zinafanyika mle ndani. Hata hivyo, yale makontena yakishaingia Kariakoo, wakati yanatelemshwa utakuta kuna askari zaidi ya 30 wanazunguka kwenye yale makontena. Pia wale askari kuondoka kwenye yale makontena ni lazima kuwepo na utamaduni wowote ambao wao wanaufikiria na ambao ndio unaotendeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni nini ambacho nataka kukiongelea? Kama kontena linatoka bandarini likiwa limelipiwa kodi stahiki zote na linakwenda maeneo ya Kariakoo kushushwa, hakuna tena haja ya yule mfanyabiashara kwenda kutoa rushwa wakati anateremsha lile kontena. Kwa hiyo, haya mambo ndiyo wanayoyazungumza Wabunge humu ndani, ukwepaji wa kodi ni mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia Mradi wa Maji wa Ruvuma kule kwangu. Hili nalizungumza kwa masikitiko makubwa sana. Huu mradi wa Ruvuma ambao unakwenda kuwasaidia wananchi wa Mtwara na pembezoni mpaka kufika Lindi, tayari mradi huu Benki ya ADB ilishaweka token kwenye miradi yake kwa zaidi ya dola 160, wako tayari ku–engineer huu mradi ufanye kazi, lakini iko kampuni ya China Railways International Group na wao waliweka dola milioni180. Sasa, sijui uzito uko wapi au shida iko wapi wakati Mheshimiwa Rais amefika mahali sasa ametanua wigo na amempa mamlaka Mheshimiwa Waziri wetu kwamba amsaidie Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaingia 2025 wananchi wa Mtwara hawana maji salama, lakini wako watu ambao inawezekana wakasaidia kutuleta maji. Mheshimiwa Waziri, akija hapa aje na majibu kigugumizi kiko wapi? Kwa kweli Mheshimiwa Mwigulu mimi ni mdogo wangu na msikivu sana, si vema nikazungumza hapa kwa ukali sana. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kwa hili anisaidie kaka yake. Namwomba sana Mheshimiwa Mwigulu, hajawahi ku–fail kwenye jambo lolote ambalo anali–engineer. Sasa kama mimi kaka yake ananifanyia hivi mpaka napiga kelele hapa, kwa kweli ni vitu ambavyo sio vizuri sana nianze kupiga kelele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kampuni ya Alliance inaleta magari aina ya TATA. Kampuni hii imekuwa ni kampuni ya kudhulumu Watanzania toka imefika katika nchi hii. Nazungumza humu ndani tukiwa ndani ya Bunge hili, kabla Wabunge hawajaja kuwa Wabunge humu, kuna wahanga zaidi ya 30. Unakwenda kukopa hela benki na wewe unakwenda kukopa gari, unaacha pale milioni 70, unapewa gari ya milioni 130. Unaposhindwa kulipa takribani zimebakia milioni tano au sita, zile gari unanyang’anywa na Mheshimiwa Waziri, Mwigulu Nchemba, anajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaleta kampuni tukiwa na lengo kubwa la kuwasaidia Watanzania, lakini kampuni hii haiwasaidii Watanzania. Leo tukipiga parapanda hapa tuwaite Watanzania waliodhulumiwa na ile Kampuni ni hatari sana. Sasa Serikali tunayo na niishauri Serikali waamke sasa. Hawa wenzetu tayari wamefika mahali wamewadhulumu Watanzania zaidi ya asilimia 80. Kwa kweli suala hili halikubaliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimezungumza hapa kuhusu madai ya vijana wetu na wazee wetu wa Jimbo la Mtwara Mjini ya fedha za Kampuni ya PRIDE. Deni hili ni deni la muda mrefu kaka yangu Mwigulu analifahamu sana, zaidi ya milioni 500. Leo hii wale wananchi ambao wanaidai PRIDE wengi wao ukiwaona wameshauziwa nyumba zao hawana pa kwenda, lakini Serikali kila nikiingia humu ndani Bungeni naambiwa kesho, kesho kutwa utapata majibu na majibu ni haya ya malipo kulipa fedha. Sasa mimi nataka Mheshimiwa Mwigulu atakapoingia hapa anieleze kwamba bwana wale wananchi wangu ambao wanadai fedha za PRIDE zaidi ya milioni 500 lini wanakuja kuwalipa wale Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika zangu zilikuwa ni tano na mimi nimezitumia dakika tano na nusu, naunga mkono hoja.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii ya Ujenzi. Niungane na wenzangu kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya, nimshukuru Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwangu Mtwara tuna barabara moja ya kutoka Mtwara - Mingoyo mpaka Masasi. Barabara hii ni barabara ambayo inaunganisha kiuchumi hasa ukizingatia sasa makaa yote ya mawe kutoka Liganga na Mchuchuma yanapita katika barabara ile, lakini barabara ile ni chakavu sasa. Kwa mpango uliopo tulikuwa tunaelezwa, kwamba barabara ile iko mbioni kupatikana fedha, nimwombe Mheshimiwa Waziri afanye kila njia na namna fedha ipatikane kwa haraka, tuanze ujenzi kwa sababu barabara hiyo ni barabara muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru pia Serikali kwa kutujengea Bandari ya Mtwara ambayo imepanuliwa kwa kiasi kikubwa. Nataka niishauri Serikali tunapozungumza maendeleo yoyote ndani ya nchi, hatuwezi kuiacha bandari, lakini Bandari ya Mtwara mpaka sasa hivi hakuna njia mbadala ya kuweza kuitumia wakati Serikali imewekeza pale zaidi ya bilioni 157. Sasa ombi langu na ushauri kwa Serikali, tunazo nchi jirani ambazo zinaweza zikaitumia kwa ufasaha sana Bandari ya Mtwara, wenye mamlaka niwaombe tufanye mazungumzo ya haraka sana kuinusuru bandari ile ili iweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari yetu ya Dar es salaam kwa sasa ukiangalia kwa kweli imezidiwa kwa kila namna. Bandari ile kina kona unavyotaka kuingia imeelemewa na vitu vingi hasa mizigo na vitu vingine. Tuielekeze sasa Bandari ya Mtwara, twende tupanue wigo, watu wa Malawi, Zambia waitumie Bandari ya Mtwara. Ukizungumza kutoka Zambia kuja Dar es Salaam lakini ukizungumza kutoka Zambia kuja Mtwara, Mtwara ni karibu zaidi kuliko Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, isitoshe katika mikoa yote ambayo sasa hivi ina maendeleo tukizungumza Arusha, kuna mpaka wa Namanga, lakini tukizungumza Mbeya kuna mpaka kule Mbeya. Kwanza niishukuru Serikali kwa kutujengea lile Daraja la Mtambaswala, lakini daraja lile unaweza ukakaa zaidi ya miezi miwili huwezi kukuta gari inapita pale, kwa nini?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

TAARIFA

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimweleze mtoa hoja kwamba Daraja la Mtambaswala sasa hivi ndio njia kuu ya kwenda Msumbiji na linapokea magari mengi ya IT yanayopita pale. Kwa hiyo sio kweli kwamba unaweza kukaa siku nzima bila gari, hizo habari sio sahihi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mtenga, taarifa hiyo.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hiyo siipokei na mtoa taarifa nadhani hapatikani kwenye jimbo lake ndio kisa anayazungumza hayo. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mtenga, kanuni zetu haziruhusu kumsema Mbunge mwenzio, futa neno hilo.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nafuta kauli.

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunazungumzia Daraja la Mtambaswala na ninapozungumzia kujenga Daraja la Mto Ruvuma, ukitoka Mtwara Mjini kwenye Kiwanda cha Dangote mpaka Mahurunga takribani pana kilomita 70. Ukitoka Mahurunga ukivuka kwenda Msingwe Daplaya pana kilomita zaidi ya 70, tuzungumzie kiuhalisia.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

TAARIFA

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mtenga kwamba Daraja la Mtambaswala analolizungumza tayari limeshajengwa, lipo, yeye ajielekeze kwenye kuomba Daraja la Mto Ruvuma bila kubeza Daraja la Mtambaswala.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mtenga, taarifa.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa, siipokei.

NAIBU SPIKA: Endelea na mchango wako.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ukizungumza kilomita 140, ninachotaka kukisema tuna Mradi wa NLG unakuja Lindi. Mradi huu utafungua fursa kwenye nchi Jirani, hoja yangu ya msingi ni kwamba miradi hii ambayo inakuja na fursa ambazo zipo na malighafi ambazo tutakuwa tunazitengeneza katika mpaka wa Mtwara la Lindi, ziweze kufikika kwa wakati, lakini gharama iwe ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza leo Dangote wanauza sementi, sementi ya Dangote ikipita Mtambaswala mpaka kwenda Mozambique haiwezi kuuzika, lakini kama tungekuwa tuna daraja ambalo liko shortcut, sementi ile ya Dangote ingepata soko kubwa sana na Tanzania tungepata kodi ya kutosha kupitia Kiwanda cha Dangote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna suala la reli. Tunapozungumzia bandari ni mbadala lazime tuwe na reli lakini reli hii ya Mbambabay - Mtwara imezungumzwa kwa muda mrefu sana. Niiombe Serikali mazingira yote tunayotaka kuyafanya kwenye shughuli zozote za kimaendeleo, hatuwezi kuikwepa reli ya Mtwara, kwa hiyo niiombe sana Serikali, reli hii na nadhani ipo kwenye mpango, lakini nimwombe Mheshimiwa Waziri reli hii ipatikane kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna utanuzi wa airport pale nayo niishukuru Serikali wametujengea uwanja wa kisasa na naamini sasa tutakuwa International Airport Mtwara, lakini rai yangu ni moja uwanja ule unakaribia kwisha, lakini katika package ya uwanja ule bado kuna mapori ambayo yamezunguka ule uwanja, hatujaona mazingira yeyote yanayopelekea kuwa na uzio unaoendana na ujenzi wa Airport ya kisasa. Naiomba Serikali na Waziri kwamba sasa tujielekeze…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Mtenga, kengele ya pili.

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuendelea kuchangia Wizara hii ya Mipango. Vilevile, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuandaa au kuunda Wizara hii ya Mipango na Uwekezaji. Nachukua fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Rais, katika manispaa yangu Januari mpaka Desemba nilikuwa siwezi kujenga hata kituo kimoja au kuchimba choo cha matundu manne kwa manispaa, tumeletewa Mkurugenzi, kwa kweli huyu kijana lazima nizungumze hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeletewa kijana huyu ndani ya wiki mbili amekusanya zaidi ya milioni 160, ndani ya wiki mbili. Kwa hiyo, nampa pongezi Mkurugenzi Nyange na aendelee sasa kututengenezea Jimbo letu la Mtwara na Manispaa yetu ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia mipango lazima tuzungumzie kilimo. Nataka nijikite kwenye eneo hili la kilimo hasa kwanza nimpongeze Waziri wetu Bashe, kwa kazi kubwa anayoifanya. Wenzetu China waliamua kufanya mageuzi ya makusudi hasa kwenye maeneo ya vijijini, Serikali iliamua kuandaa mpango wa kuwawezesha vijana ili kwenda kutengeneza mfumo wa kilimo na kujipatia chakula cha kutosha na chakula kingine cha kuuza nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri kwamba sisi kama watu wa Mtwara, tuna maeneo makubwa sana ambayo ni mapori na kwa kuwa Mheshimiwa Rais, amefika mahali akaamua kwenye Sekta hii ya Kilimo kutoa fedha nyingi sana. Niombe kwenye mipango hii tuelekeze sasa tuachane na vijana kwenda kucheza pool table, twende tuwapeleke sasa kwenye maeneo ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza mipango, tunazungumza na Pato la Taifa. Nimekuwa mara nyingi nikiishauri Serikali, kutoka Mtwara kwenda Mji wa jirani wa Mozambique, tunachukua takribani kilometa kama 60 na hilo nalizungumza Waziri wa Mipango, alisikilize vizuri sana nadhani inawezekana lina tija kwake zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa nane ya Mozambique wanatumia Bandari ya Beira. Kutoka kwenye mkoa wa mwisho kwenda Beira zaidi ya kilometa 2,000 au 1,800. Kutoka kwenye Mkoa wa mwisho kuja kwenye Bandari ya Mtwara wanatumia kilometa 770. Ninachotaka kukizungumza tufungue mpaka ule ili tufanye biashara sasa kati ya nchi na nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wenzetu wa Mozambique wanashughulika na masuala ya gesi lakini wanashindwa gesi yao kwenda nayo kwa wakati, hawana njia ya kutumia kwa sababu wale wawekezaji Bandari ya Beira kuja mpaka Palma kuja mpaka Mchimbo Naplaya, kwenye maeneo ya gesi wanashindwa kutokana na mileage. Kwa hiyo, niombe Wizara hii iliangalie hili kwa mapana na marefu, tunakwenda kufungua nchi na biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo ambalo linawezekana kama Tanzania tukaenda kuungana nalo la viwanda. Bila viwanda hatuwezi ku-move hata siku moja, lakini tukiangalia maeneo mengi tunazungumzia Mbeya, Pwani, Lindi na Mtwara, yako maeneo makubwa ambayo kuna rasilimali, materials na kila kitu. Tunashindwaje kuwaleta wawekezaji waje waweke viwanda na tunapozungumza viwanda ndani ya nchi tunazungumza ajira ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kila kijana anaye-graduate kwenye Chuo chochote kile mawazo yake yote anakwenda kupata ajira. Katika mfumo wetu wa elimu hatuwafundishi na hatuwajengi hawa vijana watoke kwenye Vyuo waje wajitegemee, mawazo yao yote kwamba sasa wanakwenda kutafuta elimu ni vyema tukawatengenezea vijana hawa ambao wanakwenda kumaliza elimu yao waje wafanye kazi kwenye mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalo naliomba kwamba Sekta hii ya Uwekezaji twendeni tukawalete Wawekezaji wa kutujengea viwanda. Tunazungumza tuna madini, lakini leo ukienda maeneo ya Lindi na Mtwara utakuta toka miaka ya 80 yuko Mwekezaji amechukua leseni ya madini zaidi ya heka 600 au 700 na hawaonekani. Hiyo leseni kila ukigusa unaambiwa hapo kuna mwenyewe, lakini madini hayachimbwi zaidi ya miaka 30, tunazungumza mipango bila fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalo naomba liangaliwe kwa sababu nazungumza nikiwa na ushahidi wa jambo hili. Rasilimali ni ya kwetu, mtu amekuja amechukua leseni na kwenye leseni ile sasa hivi amefika zaidi ya miaka 30 hajawahi kuchimba hata siku moja. Kama hajachimba hata siku moja faida yake ni nini na mipango ipi ambayo tunaiweka kwa sababu tunazungumza mipango kwenda kutafuta fedha ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara ya Mipango, hili nalo waliangalie kwa mapana na marefu kwamba wale wote waliopata leseni wana zaidi ya miaka 20 au 30 na hawajachimba, watumie sheria ambazo inawezekana wanaziweza wawaondoe hawa watu, wananchi wetu waende wakachukue hayo maeneo ili wachimbe madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, sasa nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli kwenye Jimbo langu natembea kifua mbele, Rais, amefanya raha kubwa sana kunisukumia fedha kwenye Jimbo langu. Mungu ambariki sana na aendelee sasa kusogeza miradi kwenye Jimbo la Mtwara Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini nami niungane na wenzangu kumshukuru Rais wetu mpendwa, kwa kazi kubwa anazozifanya za kutuletea maendeleo ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wetu kwa bajeti nzuri ambayo ina matumaini kwa wananchi. Nadhani bajeti hii ikitekelezwa vizuri, inakwenda kutatua matatizo ya wananchi. Kabla sijaanza kuchangia, mimi ni Mwenyekiti wa Maadili wa Wabunge wa CCM hapa Bungeni. Napenda kulisema hili; Mbunge mwenzetu aliyetoka kuzungumza juu ya baadhi ya Wabunge kutokumuunga mkono Rais, hiki ni kitu kimoja kibaya sana na hapa haikuwa mahali pake kukizungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna moja au nyingine, Rais huyu amemgusa Mbunge kila mmoja kwenye Jimbo lake, na kwa hali ya kawaida, sidhani kama kuna Mbunge humu ndani inawezekana akatoka huko nje akamshambulia Rais. Haya nayazungumza, kesho tutasikia magazeti mengi sana yanaandika hicho kitu. Ambacho kinakwenda kufanyika sasa, ni kuwachonganisha Wabunge na Rais wao. Sasa hili siyo jambo jema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana Wabunge, kila mwenye shida ambayo inahusiana na suala zima la kiongozi, basi mtuone. Katika Kamati yetu tumeshaita Wabunge zaidi ya 14 humu ndani, lakini kwenye mambo tofauti, siyo masuala ambayo yanamhusu Rais. Kila tulipokaa nao hao Wabunge, hali ipo shwari na tunaendelea na Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niendelee na mchango wangu. Kwanza, nataka nizungumze kuhusu mapato. Hatuwezi tukaizungumzia bajeti, kila mwaka tunapokuja tunapandisha vitu bei, kila mwaka, lakini still tunavyo vitu vyetu ambavyo viko tayari. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, katika hotuba yake amezungumza, kuna baadhi ya watumishi ambao wanahusika na ukusanyaji wa kodi, wanamwangusha. Hili Mheshimiwa Waziri tunakupongeza kwa kuliona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilizungumza, yuko mtu mmoja alipeleka korosho nje lakini kwenye ushuru aliotozwa ametozwa ushuru wa mbaazi. Sasa huu ni upotoshaji, lakini pia ni wizi mkubwa ambao unaendelea kufanyika. Kwa hiyo, twende tusimamie rasilimali zetu. Hatuna shida ya kufika mahali sasa tunasema tuhangaike na viwanda vya pipi, tupandishe bei kwenye ushuru wa pipi wakati bado tuna rasilimali ambazo tunashindwa kuzisimamia ili ziweze kuleta tija zaidi. (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna watu wanaagiza magari nje, unaagiza gari IST kwa gharama ya milioni tatu, linaposhuka bandarini ushuru wake TRA ni milioni sita. Tunakwenda wapi? Kama tungepunguza bei ya ushuru, wangapi wangeagiza hayo magari IST na yangekuja kwa wingi gani na sisi tungekusanya kodi ya aina gani? Sasa kuna vitu vingine inawezekana kwamba, tunasema kwamba, tunapandisha ushuru ili tupate kodi kubwa kumbe tunakwenda kujiangamiza wenyewe. Ushauri wangu kwa Serikali, katika vyanzo vyote vya kodi tuangalie population ya bidhaa ambayo inakuja kwetu, tukipunguza kodi bidhaa hizi zitakuja kwa wingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine la wamachinga limezungumzwa sana. Asilimia kumi ambayo tunachangia sisi kutoka kwenye halmashauri zetu, fedha hizi ni msaada mkubwa sana kwa wananchi wetu. Leo tunapoamua kutoa asilimia tano kuipeleka kwenye huduma nyingine kwa sababu, ile asilimia kumi hata Wabunge wengi wamesema haitoshi kwa jinsi ambavyo tumewapa mikopo wananchi wetu, haitoshi kabisa. Sasa naiomba Serikali asilimia kumi hii ibaki palepale ilipo, lakini kama kuna uwezekano wa kuitengenzea sheria tena, tuongeze fedha katika hii asilimia kumi, ni hela ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwangu tunaondoaondoa na leo hapa nimepigiwa simu kuna maaskari huko wanafukuza na bunduki, wanafukuza wananchi kwenye maeneo. Sisi tunalo eneo pale nyuma ya Benki Kuu, eneo lile linaota nyasi, eneo lile lina vichaka zaidi ya eka 18, liko pori mjini kwenye manispaa; nimepiga kelele hili eneo tuwajengee hawa wamachinga wakae hapa waache kazi ya kutembeatembea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapomtembeza mmachinga barabarani athari zake nini? Tunakosa kukusanya kodi. Hatukusanyi kodi kwa sababu, hakuna mmachinga anayetoa risiti, lakini mmachinga anapotembea barabarani hana insurance yoyote. Leo tunazungumza tunataka tuwape mikopo, watu wa benki ukiingia kwenye mikopo wanakwambia tunataka hati ya nyumba au ofisi yako iko wapi, mkataba wako uko wapi? Kwa hiyo, hili nalo tuliangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wafanyabiashara wanakopa kwenye benki na hawa watu wanapokopa mikopo yao wanaweza wakalipa takribani zaidi ya asilimia 80. Anaposhindwa kulipa japo ameshalipa zaidi ya asilimia 80, watu wa benki wanaingia wananyang’anya nyumba za watu, wanauza nyumba. Hili ni hatari sana kwa wananchi wetu na hii ni kwa nchi nzima, wako watu wamekaa na pesa zao, kazi yao wao ku-coordinate na watu wa benki, nyumba gani itauzwa kesho, keshokutwa. Sasa hatuwasaidii wananchi wetu, tunakwenda kuwaharibu wananchi wetu. Hili nalo naomba nalo tufike mahali tuliangalie, lakini tuwasaidie wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie pia kwenye eneo moja la ujengaji wa reli yetu. Kwanza niishukuru Serikali, kwa kweli inajenga reli, lakini nataka niseme jambo moja ambalo ni ushauri kwa Serikali. Tulikuwa tuna reli ya TAZARA, reli hii ilijengwa na Mchina. Reli ya TAZARA hatukukata kipande kipande, Mchina alijenga mwanzo mpaka mwisho, lakini tukawa na reli ya kati ilijengwa na Wajerumani. Wajerumani wale walijenga reli ile mwanzo mpaka mwisho. Ushauri wangu kwa Serikali hebu tuache kuingia kwenye kuweka wakandarasi zaidi ya watatu, wanne kwenye reli kwa usalama wa Taifa letu. Reli hii ni kitu muhimu sana hatuwezi kuweka zaidi ya watatu, wanne wanakwenda kujenga reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwenye dhana ya usalama wa nchi, hebu turudi sasa tuangalie ni mkandarasi gani bora, yeye anawezekana akaingia joint venture na kampuni nyingine yoyote ikamsaidia kwenda kujenga. Kwa hili natoa mfano, tunazo barabara zetu za lami. Mimi natoka Mtwara, kule Mtwara ukiingia pale Lindi walijenga pale Kharafi, lakini kipande alichojenga Kharafi cha lami ni mkandarasi bora, mpaka leo hakijaharibika, lakini vipande vingine hivyohivyo walivyojenga kwa muda huohuo barabara hazipitiki na kila siku ziko kwenye maintenance. Sasa ombi langu kwa Serikali hebu turudi tuangalie mkandarasi mmoja anaweza akatusaidia nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie vituo vya afya. Kwangu niishukuru Serikali tumepata kituo cha afya na kimeshaisha. Niombe katika vituo hivi ambavyo vinajengwa, kwenye suala la Madaktari na Wauguzi Serikali watoe kipaumbele tuweze sasa kupata Wauguzi na Madaktari kwa sababu, majengo ni mazuri yana kila jambo ndani mle. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.