Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jonas Van Zeeland (9 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia jioni hii ya leo, lakini kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima, afya, hatimaye nimeweza kusimama mahali hapa siku hii ya leo. Nichukue nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Ni hotuba ambayo imetuonesha tulikotoka, tulipo na tunakotaka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu Kitengo cha Maafa, tumeona wametenga bilioni mbili na milioni 600, lakini milioni 600 ni kwa ajili ya shughuli mbalimbali za ofisi na bilioni mbili ni kwa ajili ya maafa. Niombe sana kwasababu kila mwaka tunapata mabadiliko ya tabia nchi, tunapata maafa na majanga mbalimbali, niombe sana fedha hizi ziongezwe ili ziweze kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano katika Jimbo langu la Mvomero katika Kata ya Muhonda na Kata ya Sungaji vijiji zaidi ya vitatu vipo kwenye hatari. Na mwaka jana tulipoteza nyumba zaidi ya 150 ziliondoka na mto, lakini mwaka huu vijiji vile ambavyo viko pembezoni yam to vipo kwenye hatari kubwa sana ya kuondoka na mto kama mvua zitaendelea kunyesha mvua kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba sana wenzetu wa mazingira watusaidie kwenda kuona yale maeneo ili kuweza kuokoa nyumba ambazo zipo katika maeneo hatarishi. Tunaweza tukapoteza vijiji kwa pamoja zaidi ya vitatu kwa hiyo, niombe sana waweze kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tunatambua kilimo ndio uti wa mgongo wa Taifa hili, lakini tuna tatizo moja ambalo tukichangia wengi tunajisahau, Maafisa Ugani ambao kimsingi hawa ndio wataalamu wa kilimo na sisi wananchi wetu wanalima kupitia jembe la mkono. Maafisa Ugani wengi wanakaa maeneo ambayo hakuna kilimo, wanatoka katika vijiji wanakwenda kufanya mpango wa kuishi katika maeneo ambayo kwao ni rafiki, wale wakulima wetu kule walipo hawana wataalamu na tunajua kila mwaka kunakuwa na mabadiliko ya kalenda ya kilimo kwa sababu ya mabadiliko ya tabia nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Wilaya yetu ya Mvomero ina tatizo kubwa sana la tembo. Tumepata bahati ya kupakana na Hifadhi ya Mikumi, lakini bahati hii sasa imegeuka kuwa laana kwa watu wa Mvomero, tumeshapoteza zaidi ya watu 23 mpaka sasa hivi. Na jana niko hapa nimetumiwa message mwananchi mmoja amekanyagwa na tembo kichwani na nimewachangia nikiwa hapahapa ndani ya Bunge, lakini hali ni mbaya hakuna mwananchi yeyote ambaye analima katika maeneo ya Tarafa nzima ya Mlali zaidi ya kata sita hakuna mtu ambaye anashughulika na shughuli za kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana kwa Serikali waende wakatusaidie. Tusipoenda kuwasaidia kuwaondoa wale tembo ambao wako katika lile eneo la Tarafa ile ya Mlali tutashindwa kulima. Nilienda kumuona Waziri wa Maliasili, alinipa ushirikiano, alituma timu yake ilikwenda, lakini tatizo bado liko palepale, lakini mbaya zaidi sheria ambayo iliwekwa kwa ajili ya fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria inasema eka moja shilingi 150,000/= lakini mbaya zaidi mtu ambaye amelima chini ya eka moja hawezi akalipwa fidia kwa mujibu wa sheria. Sasa niombe sana tufanye mabadiliko kidogo katika eneo hili kwa sababu, tunajua wakulima wetu wengi wanalima chini ya eka moja. Lakini mtu mwenye chini ya eka moja akipata madhara ya tembo basi hawezi akapata fidia yoyote, lakini wale ambao wamefariki dunia wanatakiwa kwa mujibu wa sheria walipwe shilingi 1,000,000/=, lakini mpaka sasa hivi wananchi wengi bado wanadai hizi fedha na hawajui lini watalipwa hizi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kuna hawa watu wanaoitwa TFS. TFS ni tatizo sana nchi hii, hawa ni Wakala wa Misitu Tanzania, sisi tunapotoka kule vijijini shule zetu nyingi hasa za pembezoni hazina madawati na tunayo misitu ya asili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoenda kuomba vibali kunakuwa na urasimu mkubwa sana wako tayari kuona miti inaanguka na kuoza, lakini sio kutoa kibali kwa ajili ya kuvuna na kutengeneza madawati.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia hawa ndio wanasimamia hifadhi zetu Tanzania. Wanaacha wananchi wetu wanaingia kwenye hifadhi, wanaanza kusafisha shamba, wanapanda, wanalima, kama ni mahindi ama mpunga, wakifika kwenye hatua ya kuvuna ndio wanakuja na kuanza kuharibu mazao yao, lakini wakati wanafanya maandalizi ya kupanda wanawaangalia. Kwa hiyo, niombe sana hawa wati wa TFS kuna mambo mengi sana ambayo Serikali inatakiwa wafanye mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika…

NAIBU SPIKA: Haya, kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, imegonga ya kwanza.

NAIBU SPIKA: Zikiwa dakika tano wanagonga moja.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo. Nichukue fursa hii nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uzima, lakini pia nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri anazozifanya. Nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kazi kubwa na nzuri ambazo mnazifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mengi wenzangu wamezungumza, lakini mimi naomba nijikite kwenye eneo la migogoro ya ardhi, na kwa sababu ya umuhimu wake, nitajikita zaidi jimboni kwangu, kwa sababu tuna migogoro mingi. Moja ya wilaya ambazo bado zina migogoro ya ardhi ni Wilaya ya Mvomero. Pamoja na kazi kubwa na nzuri ambazo wanazifanya watalamu wetu, akiwepo Kamishna wetu wa Ardhi, Bwana Frank ambaye yuko Morogoro na watalamu wengine ambao wako katika wilaya yetu, lakini bado migogoro hii ni mingi, na ni kwa sababu ya eneo ambalo ni potential kwa kilimo lililopo katika wilaya yetu hii ya Mvomero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mwekezaji ambaye alipewa eneo lenye ukubwa wa ekari 100,000 mwaka 1985 kwa ajili ya shughuli za ufugaji na eneo hili alipotea. Eneo hili ni lile la Kipunguni Mheshimiwa Waziri nafikili unalijua, liko Tarafa ya Mlali. Huyu mwekezaji alipewa eneo kwa ajili ya ufugaji, lakini hajawahi kufanya shughuli zozote za ufugaji kwenye hili eneo zaidi ya watu wachache aliowaweka ambao wanafuga mbuzi zisizozidi 50. Yaani mwekezaji ana eneo la ekari 100,000, anafuga, badala ya kufuga kama eneo linavyomtaka afanye, yeye anakwenda kufuga mbuzi 50 kwenye eneo. Sasa amekuja sasa hivi, anapima lile eneo, anauza vipande vipande lakini wananchi ambao wameishi na lile eneo kwa miaka mingi amewaambia atawapa eka elfu moja moja kwenye vijiji vitatu. Kijiji cha Mkata, Kijiji cha Merela Mlandizi na Kijiji cha Msongozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulipewa ekari 100,000 umeshindwa kuliendeleza, leo unakuja kuwapiga saundi wananchi kwa kuwapa eka elfu moja moja! Hata kama kuna baadhi ya maeneo huku alishatoaga akawapa wananchi, lakini kwa ekari 1,000 bado ni ndogo, na wananchi hawana maeneo mengine ya kwenda kufanya shughuli zao za kilimo na ufugaji isipokuwa ni hili eneo la Kipunguni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pia tuna wafugaji na Mheshimiwa Waziri unajua Mvomero ni eneo pia linalofanya shughuli za ufugaji. Tunao wafugaji. Sasa tunaomba katika eneo la huyu bwana wa Kipunguni ambaye alipewa mwaka 1985, eneo hili pia lipimwe wapewe wafugaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba, kuna eneo ambalo tulipewa na watu wa NARCO pale Dakawa, hili eneo tumepewa ekari 10,000. Ekari 5,000zilikwenda Luhindo kwenye Kijiji cha Luhindo, 5,000 zilikwenda kuinzisha Halmashauri. Tulipima kwenye eneo la ekari 5,000 ambalo limeanzisha halmashauri, tumepima eneo la ekari 3,000 tu, eneo la ekari 2,000 liko wazi na linaendelea kuvamiwa siku hadi siku. Sasa sielewi tatizo ni nini? Tatizo ni fedha za upimaji hakuna ili tuweze kulipanga hili eneo ni kimpango mji, ama ni uvivu tu wa wataalam wetu, wanakaa pembeni wakisubiri migogoro pengine inawezekana itakuja kuwanufaisha baadaye? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna eneo la ekari 5,000 ambazo zilikwenda pale Luhindo. Mheshimiwa Waziri hili eneo tunaomba lipimwe ili watu wamilikishwe kishera. Eneo hili tunataka kulitumia kwenye skimu ya umwagiliaji. Eneo hili sasa hivi limeshaanza kuvamiwa na mbaya zaidi wanawavamia watu ambao wanatoka nje ya Dakawa, wanatoka nje ya Kijiji cha Luhindo, mnatengeneza migogoro ninyi wenyewe halafu baadaye mnashindwa kuitatua hii migogoro. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, kama watu wako hawana fedha ya kutatua hii migogoro, wape fedha za kutosha migogoro iishe. Sehemu yenye migogoro hakuna maendeleo Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Rais; Mheshimiwa Hayati pamoja na Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia wamefuta mashamba pori tisa. Haya mashamba pori waliyoyafuta yana ukubwa wa ekari 13,000, lakini toka yamefutwa hayo mashamba Mheshimiwa Waziri pamoja na maelekezo ambayo yametolewa kwamba wapewe wakulima wadogo wadogo, wapewe wafugaji na litengwe eneo kwa ajili ya uwekezaji, mpaka leo tunavyozungumzwa hapa, hakuna kilichofanyika. Hakuna upimaji wowote. Sasa leo tunalia migogoro ya wakulima na wafugaji kwa kukosa maeneo, halafu kuna ekari 13,000 zimekaa, Rais ameshazifuta, kwenda kupima na kuwapa wananchi mnashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, Mvomero ni miongoni mwa wilaya ambazo watu walikuwa mpaka wanauana kwa sababu ya migogoro ya wakulima na wafugaji. Leo tuna ekari 13,000 mnashindwa kuwapa hao wananchi? Au mnataka waingie wenyewe wajimilikishe mle halafu baadaye mje kutumia tena nguvu za kuwatoa? Mtengeneze migogoro ambayo leo hapa tunazungumza kuitatua wakati migogoro mingine mnaitengeneza inaanza upya ambapo badaye mtashindwa tena kuja kuitatua. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kama utatenga kwenye bajeti zako, naomba uweke hili jambo ili mweze kwenda kuimaliza migogoro pale Mvomero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna eneo la Wamembiki. Hili ni eneo ambalo lina mgogoro wa muda mrefu sana. Hii mipaka inahamishwa hamishwa mara kwa mara. Wakija hawa wanasema hapa, wakija hawa wanapeleka hapa, mara tatu mipaka imehamishwa. Kuna mgogoro mkubwa sana pale kati ya hifadhi na wananchi. Naomba pia wapeni fedha watu wa Morogoro na Mvomero wakapime yale maeneo ili wananchi waweze kujua hatima ya huo mgogoro ni mgogoro wa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni Kijiji cha Mkata. Kijiji hiki kilianzishwa mwaka 1965. Mwaka 1979 Serikali ilitoa tangazo la GN Na. 75 kuongeza mipaka ya hifadhi, lakini baadaye wananchi wakaambiwa, walikuwa wanalima kwenye bonde ambalo linaitwa Ngongoro. Wakaambiwa hili bonde liende kwenye Hifadhi ya Mikumi, wao watapewa bonde linaloitwa Kidaga ambalo lipo mpakani kabisa na Kilosa kule Mkata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu, ilikuwa ni hekta 814 na wananchi wakakubaliana kila mwananchi kwa kipindi kile apewe ekari mbili mbili kwa ajili ya kulima, lakini leo Mheshimiwa Waziri ninavyozungumza hapa, kuna wasanii wawili sijui wamepataje haya maeneo? Wamechukua haya maeneo na sasa wanawakodishia wananchi. Ni mgogoro ambao unawaumiza watu. Eneo walipewa miaka ya nyuma na walimilikishwa kisheria, lakini leo wamekuja watu wawili kwa ujanja ujanja wanaoujua wao, wamekwenda wamepewa haya maeneo na sasa hivi wanafanya biashara ya kukodisha, hawalimi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, timu yako ijue kuna mgogoro huo na tunaomba muende mkautatue. Ni mgogoro wa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna mgogoro ambao uko pale kwenye mizani, ambapo ukishatoka Dumila kuna mizani, pale ndiyo mpaka wa Kilosa na Mikumi. Mwaka 2014 kulitokea mafuriko Wilaya ya Kilosa, kipindi hicho Rais alikuwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akatoa maelekezo kwamba wale wananchi ambao hawana maeneo ya kuishi baada ya mafuriko, waende pale kwenye lile eneo ambako sasa wamejenga mizani. Wale wananchi wameanza shughuli zao pale na wanazikana pale, lakini leo kuna watu wa Magereza wanataka kuwaondoa wale wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba jambo hili pia Wizara ilichukue kwa uzito wa kipekee. Nchi hii ni yetu sote. Mbona kuna maeneo mengine watu wanajifanya wao ni wakubwa sana? Hivi wewe Askari Magereza, watu wamepewa na Mheshimiwa Rais wakae, wewe unakuja kuleta kitambi chako, unasema hawa waondoke, kweli! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri hawa wananchi wabaki. Walipewa haya maeneo na Mheshimiwa Rais, kipindi hicho alikuwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, lazima hawa watu kama mnataka kuwatoa, mwafidie, lakini hawawezi kuondoka bila fidia yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tuna eneo ambalo pia lina mgogoro na eneo hili linashughulikiwa na watu wa halmashauri. Kama mgogoro huu ukishindikana kule wilayani, mimi nitakuja kwako. Eneo la mwekezaji mwenye Kiwanda cha Sukari Mtibwa na kuna eneo linaitwa Newland, hili ni eneo la muda mrefu sana lenye mgogoro wa zaidi ya miaka 30. Mimi pamoja na watalamu na watu wa Mtibwa na ninashukuru sana na kumpongeza huyu mwekezaji, ametoa ushirikiano katika kutaka kuutatua huu mgogoro na nina imani mgogoro utakwisha na kama hautakwisha kwa namna yoyote ile, Mheshimiwa Waziri nitakuja ofisini kwako ili uutatue huu mgogoro ni wa miaka 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nimalize, Mvomero hatutaki wawekezaji feki. Mheshimiwa Waziri kuna watu, na wengine wako humu ndani wana maeneo kule Mvomero, jamani, Mvomero mkichukua maeneo mlime, ama mfuge. Hatutaki mje mwekeze kule majoka. Migogoro hii haitaisha na tunawakosesha watu fursa. Kama tukitoa ardhi na mkaitumia kwenye kilimo, ama kwenye ufugaji, kwanza mtatengeneza na ajira kwenye eneo letu, lakini maeneo ambayo yanatolewa Mvomero, watu wakishapewa, akishapewa hati, anasema hili ni eneo urithi wa watoto wangu. Sasa urithi wa watoto wako si waanze kulima sasa hivi. Hao watoto wenyewe, utakuta mtu ana mtoto wa miaka mitano, anategemea aje amrithishe hilo shamba. Kwa hiyo, likae pori miaka yote hiyo kwa sababu ya mtoto wake akue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, nami nakuamini sana uchapakaji kazi wako tunaujua, Naibu wako tunamfahamu ni mchapaji kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja na nina imani migogoro itaenda kwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima afya na hatimaye nimeweza kusimama kuchangia Wizara hii muhimu, Wizara ya Maji. Pia nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Aweso pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya katika nchi hii, hasa katika kuhakikisha tatizo hili la maji linaelekea kwisha, hasa katika maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kuchangia katika hizi Jumuiya za Watumia Maji. Mheshimiwa Aweso bahati nzuri alikuja katika Wilaya yetu ya Mvomero, kama sitakosea mwaka 2016/2017 akiwa Naibu Waziri wa Maji. Tulikwenda Kibati, mimi nikiwa Mwenyekiti wa Halmashauri pale Mvomero, tulikuta mradi wa maji, Jumuiya ile ya Watumia Maji hawana hata senti moja na wameendelea kukusanya kila mwezi fedha kwa wananchi wale ambao wanatumia maji, lakini alikuta hawana hata shilingi 100. Bahati nzuri alichukua hatua akatoa maelekezo wakakamatwa, lakini hawajarejesha zile fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Aweso sasa hivi amekuwa Waziri kamili, tatizo bado liko palepale. Hizi Jumuiya za Watumia Maji zinahitaji mafunzo. Hawa ni wananchi wetu ambao wako vijijini, hawajui namna ya kusimamia hii miradi ya maji. Hii miradi inajengwa kwa gharama kubwa sana, lakini Wizara inashindwa kutenga hata siku tatu ama nne kwa ajili ya mafunzo ili hizi Jumuiya za Watumia Maji waelewe namna ya kusimamia hii miradi ya maji. Sasa hivi naongea na Mheshimiwa Waziri ule mradi ambao alikuja Mvomero pale Salawe, Kibati, hizi mvua zilizonyesha juzi miundombinu ya maji imeondoka na maji ya Mto wa Salawe, yaani yameondoka na mabomba ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo jumuiya ile hawana maji, lakini hawana senti moja kwa ajili ya kurekebisha ile miundombinu na walikuwa kila mwezi wanakusanya zaidi ya shilingi milioni moja. Sasa Mheshimiwa Aweso atapata shida sana kila atakapoenda atakamata watu, lakini hawa watu hawana uelewa, lazima wapewe mafunzo ili wajue wanachokifanya ni nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimwambie Waziri, sisi Mvomero tuna vyanzo za uhakika vya maji, lakini ni wilaya ambayo ina shida kubwa sana ya maji. Miradi mingi ambayo iko pale kwetu bado inasuasua; tuna mradi ambao uko pale Doma, tulipata fedha za World Bank, huu mradi ulianza kujengwa 2008 mpaka 2010, una vituo vya kutoa maji 15, lakini mpaka leo nazungumza vituo vinavyotoa maji ni vitatu. Vituo vingine hivi havitoi maji mpaka wasikie kuna ziara ya kiongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2013 ulipokuja mwenge pale Doma vituo vyote vilitoa maji. Mwenge ulipoondoka vituo havikutoa tena maji. Akija kiongozi mwingine yeyote yule vituo vinatoa maji. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Aweso atuangalie sana sisi Mvomero, tuna miradi mingi kama nilivyosema huu wa Doma ambayo haitoi maji, miradi hii inatoa maji pale wanapokuja viongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine, unit moja pale Doma, wana-charge kwa sh.3,000 kisingizio wanasema kuna wakati wanatumia generator ambayo inatumia mafuta. Sasa tunashindwa kuelewa maeneo mengine sh.800 na kitu, sehemu nyingine 1,000 sehemu nyingine ndio kama hivi 3,000. Bora kuwe na bei elekezi ambayo Wizara itaitoa ili wananchi wetu wajue wanatakiwa kulipa shilingi ngapi? sh.3,000 kwa mwananchi wa kawaida na pale Doma tunajua kuna tatizo kubwa sana la tembo hakuna pale mkulima yeyote sasa hivi ambaye analima. Hali ni mbaya ya kimaisha, lakini mtu analipa unit moja sh.3,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri walitupa fedha kwa ajili Miradi ya Dihinda, Masimba, Vianzi, Lubungo na Kihondo. Miradi hii imekamilika japo sio kwa asilimia 100, lakini bahati nzuri inaanza kutoa maji, inasuasua kwa sababu ya hizi jumuiya. Kuna Mradi mmoja upo Dihinda kama wiki tatu zilizopita nimetoka kufanya mkutano pale, tatizo ni kwamba jumuiya ile hata kukabidhiwa mradi hawajakabidhiwa, hawajui wasimamiaje ule mradi. Naomba sana Waziri atusaidie, lakini na miradi mingine hii kama nilivyosema bado ina changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa 2021/ 2022, nimeona katika Vijiji vya Rusungi, Mwalazi, Chenzema, Kibuko, Luwale, wametenga fedha kwa ajili ya miradi ya maji, lakini pia tutakuwa na mradi mmoja mkubwa wa kutoka Tandali kwenda Homboza ambao utakwenda mpaka Mlali. Nimpongeze sana Waziri. Pia tuna Mradi ambao nimeona Kibogoji, Pandambili na Ndole Matale; Mheshimiwa Waziri naomba sana hizi fedha zisije zikaondolewa, tupate miradi hii katika hivi vijiji ambavyo nimevisema.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine, nimwombe Mheshimiwa Aweso, tulikuwa na ma-engineer wawili wameshahamishwa wote. Mwingine amehamishwa kama wiki mbili zilizopita, pale tuna ma-technician watatu tu. Sasa tatizo na changamoto kama nilivyosema hapa za maji hazitaweza kwisha kama hatuna engineer. Nimwombe sana Mheshimiwa Aweso atupatie engineer pale, lakini pia atupatie na gari la uhakika kwa sababu jiografia yetu sisi ni kubwa sana, lazima awe na gari la uhakika la kuweza kufika maeneo yote kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ile miji 28 na sisi Mvomero katika Kata ya Dakawa, Wami Dakawa Sokoine, tumepata mradi. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri niombe tu pale Dakawa pana shida kubwa sana ya maji, tunategemea huu mradi utakwenda kumaliza tatizo lote la pale Dakawa.

Mheshimiwa Naibu spika kuna Kijiji kimoja cha Sokoine siku moja tuliona kwenye vyombo vya habari ng’ombe na wananchi wanatumia bwawa moja ambalo ni la wafugaji, wananchi na wenyewe wanakwenda kuchota maji pale. Kwa kweli, hali ni mbaya, hali inatisha, tunaomba sana watusaidie, japokuwa tumepata fedha za dharura kwa ajili ya kutoa maji Wami Dakawa kuyapeleka pale Sokoine, lakini bado tatizo lile litakuwepo kwa sababu, mradi ule ni mdogo, hautoshelezi Kijiji kizima cha Sokoine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo lingine kubwa sana la maji katika Kata ya Msongozi. Kata ya Msongozi hawana chanzo chochote cha maji, wanatumia maji ya kwenye mabwawa, wanatumia maji ya kwenye mito, ndio maji yao ambayo wanapikia, ndio maji yao ambayo wanayatumia kwa ajili ya kunywa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri atuangalie sana wananchi katika Kata hii ya Msongozi, kuna shida kubwa sana ya maji. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kama itakupendeza…

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Van Zeeland kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana Mbunge wa Mbeya Mjini. Nataka tu nimpe Taarifa mchangiaji anayechangia sasa anavyoitaja Kata ya Msongozi ndiyo kata ambayo jina hili ninalolitumia ndio nyumbani kwa mume wangu mimi. Kwa hiyo, hakikisha maji hayo yanakwenda kwenye Kata hiyo ya Msongozi, Morogoro. Ahsante sana. (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Van Zeeland, malizia mchango wako.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea Taarifa kwa mikono miwili. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge nitapambana na Mheshimiwa Aweso hadi kuhakikisha pale maji yanatoka, maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimalizie mchango wangu kwa kusema, nimkaribishe sana Mheshimiwa Aweso. Baada ya Bunge hili la Bajeti kwisha Wilaya ya Mvomero iko barabarani, ni lami tupu, twende pale tukazungumze na wananchi. Matatizo ni mengi siwezi kuyaongea yote hapa matatizo ya maji, lakini kikubwa nimkaribishe Waziri Mvomero, karibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na afya, hatimaye na mimi nimeweza kusimama mahali hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii kama kuna watu wanaichonganisha Serikali na wananchi wake basi ni watu wa TFS. Mheshimiwa Waziri kama kuna watu ambao wanaichonganisha Serikali na wananchi ni watu wa TFS. Sisi Mvomero tuna Hifadhi ya Wame Mbiki. Hifadhi hii ilianzishwa miaka ya nyuma, ni hifadhi ambayo imepakana na vijiji vingi; ni hifadhi ambayo imepakana na Kata zaidi ya nne lakini shida iliyopo katika hii hifadhi ni suala la mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishamtafuta Mheshimiwa Waziri nikamweleza habari ya mipaka. Kuna wananchi wanalima, wengine kwa kujua mipaka na wengine kwa kutokujua, lakini mbaya zaidi hawa wenzetu wa TFS wanapowakamata hawa wananchi ambao wapo ndani ya yale maeneo, wanawapiga, wanawatesa na wanawapiga mpaka risasi. Tunaye mwananchi mmoja amepigwa risasi hivi karibuni anaitwa Juma Shabani Bakari; amepigwa risasi zaidi ya mbili kisa amekutwa ndani ya hifadhi. Sasa hata kama ameingia ndani ya hifadhi, sheria zipo, kwa nini hapelekwi kwenye vyombo vya sheria, wanaamua kuchukua sheria mkononi na kumpiga risasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaye mwananchi mwingine anaitwa Said Mwanamvua; huyu alipigwa fimbo, alinyanyaswa na walitaka kumchoma moto. Walikusanya miti wakamuingiza katikati wakataka kuwasha moto ile miti ili aweze kuungua. Sasa hao wananchi wapo Tanzania, kwenye nchi ambayo ipo huru, lakini leo wanataka kuuwawa katika nchi ambayo ni huru. Naomba commitment ya Mheshimiwa Waziri katika jambo hili kwenye suala la mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi nilishawasiliana na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya nikamweleza tatizo ambalo lipo pale. Wananchi ambao wanalima yale maeneo wakati wa kulima wanaruhusiwa, wanalima vizuri, lakini wakati wa kuvuna, sasa hivi wanataka kuvunwa wanakatazwa. Wakikamatwa ndani wananyanyaswa kama nilivyosema, lakini wakati wa kulima wanaruhusiwa walime. Nimezungumza na Mkuu wa Wilaya akaniambia mimi hayanihusu hayo mambo, waache wananchi huko wafuate taratibu ambazo zimepangwa na TFS. TFS kwenye wilaya ipo chini ya Mkuu wa Wilaya, nilishamweleza Mheshimiwa Waziri habari ya TFS na hawa watu wa Wame Mbiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana leo Mheshimiwa Waziri wakati ana-wind up atupe majibu, atueleze lini watakuja kurekebisha mipaka katika vijiji ambavyo vinapakana na Wame Mbiki. Yale maeneo ambayo tayari wananchi wanayatumia kama itaonekana wako ndani ya hifadhi, basi wanaweza wakayapima wakayatoa. Wame Mbiki hii zamani ilikuwa ina jumuiya ambayo inajiendesha yenyewe, ile jumuiya imekufa, sasa hivi wanasimamia watu wa TAWA na watu wa TFS. Hawa wananchi zamani ndio walitoa hayo maeneo yao, sasa hivi kwa sababu wananchi wameongezeka wanayahitaji haya maeneo. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri busara imwongoze aweze kutupatia haya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la tembo. Wilaya ya Mvomero sisi tumepakana na Hifadhi ya Mikumi, tembo sasa hivi kwenye Tarafa ya Mlali wapo kama mbuzi, yaani wametoka kule kwenye hifadhi nafikiri kule wameisha wote, wapo kwa wananchi, lakini tukiwauliza wanakwambia huu ni ushoroba/njia ya tembo; sasa njia ya tembo, tembo ndo anakaa hapohapo mpaka wanazaliana, kama njia si apite aende kwenye safari zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tembo wamekaa eneo moja, wanazaliana na sasa hivi wanaingia kwenye nyumba za wananchi. Wakisikia harufu ya mahindi ndani wanafumua paa wanaingiza ule mkonga wao wanakula mahindi ndani. Wananchi hawalali hata ndani kwenye nyumba zao, ni mateso makubwa wanayapata, lakini tukiambiwa ushorobo, kila sehemu tembo anapoonekana ushorobo sasa ushorobo utakuwa nchi nzima. Hapa siku moja tuliambiwa, Chuo Kikuu hapa (UDOM) kwamba tembo wameonekana, tukaambiwa nako ushorobo, sasa mwisho watakuja kuingia hata kwenye Bunge hapa utaambiwa nako ushorobo, barabara hii ya tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri lazima wawe na mikakati madhubuti ya kuwarudisha tembo wanapotakiwa kuishi. Kule wekeni hata mipaka itaonyesha wazi kabisa kwamba haya ni maeneo tembo wanapita wananchi msilime lakini ikiwezekana kule kwenye hifadhi wekeni fensi ya kutosha tembo asivuke. Kwa sababu sisi ni maeneo ambayo yanatuathiri sana mfano Kata za Doma, Msongozi, Mangai, Melela na Lubungo wananchi hawalimi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi ambao wanadai fidia pamoja na fidia yenyewe ni ndogo, wapo 2,050 hawajalipwa fidia. Pia wapo wananchi ambao wameshakufa na tembo wamefika mpaka sasa hivi 26 hawajalipwa fidia na fidia yenyewe ni ndogo, hivi kweli mtu anauawa na tembo analipwa shilingi milioni moja, shamba linavamiwa na tembo analipwa shilingi laki moja. Naomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie katika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nimalizie kwenye suala la mkaa. TFS watusaidie kwenye suala la mikaa, hivi gunia moja shilingi 12,000 unatakiwa kulipa, wananchi wetu wa vijijini hawana nishati mbadala zaidi ya mkaa na kuni, lakini leo wakikamatwa anatakiwa kulipa 12,000 TFS na 2,000 halmashauri, hivi kule vijijini watatumia nini?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kengele imegonga.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nianze kwanza kwa kumshukuuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na afya hatimaye nimeweza kusimama katika Bunge lako Tukufu kutoa mchango wangu. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kaka yangu Mwigulu Nchemba na Naibu wake kwa kazi nzuri ambazo wamezifanya katika Wizara hii ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa kwa kazi nzuri ambazo amezifanya toka amechukua madaraka ya kuongoza nchi yetu kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia nimpongeze kwa namna ambavyo tumeona ana nia ya dhati kabisa ya kuhakikisha miradi ya kimkakati ambayo walianzisha pamoja na Mheshimiwa Hayati, ana nia ya kuimaliza lakini pia na kuanzisha miradi mipya ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze na suala la Madiwani. Naomba pia ku-declare interest, mimi nilikuwa Diwani kwa miaka 10 na nilikuwa Mwenyekiti wa Halmashauri kwa miaka 10. Moja ya changamoto ambayo Madiwani walikuwa wanapata ni suala la posho hizi za mwezi. Serikali kwa kuamua sasa kuwalipa moja kwa moja Waheshimiwa Madiwani, kwa kweli watakuwa wamewasaidia sana. Wakurugenzi walikuwa wana-take advantage ya kuwalipa Waheshimiwa Madiwani kwa namna wanavyotaka wao na kama kuna mambo ambayo yanataka kujadiliwa kwenye vikao, Madiwani hawana sababu ya kupinga maamuzi ya Mkurugenzi kwa sababu wanajua mwisho wa siku Mkurugenzi hatatulipa posho zetu. Sasa kwa kuwalipa moja kwa moja, wataenda kutenda haki kwenye vikao bila kumwogopa mtu yeyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia jambo kubwa hapa ni kuongezewa posho. Madiwani wanalipwa shilingi 350,000. Kazi kubwa ambazo wanazifanya Waheshimiwa Madiwani kwenye Kata kule ni kuhakikisha wanasimamia miradi ya fedha nyingi ambazo ndizo tunazipitisha hapa Bungeni, wao ndio wanakwenda kuzisimamia, lakini kwa mwezi Diwani analipwa shilingi 350,000. Hata mtendaji wake wa Kijiji anapata fedha nyingi kuliko Mheshimiwa Diwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri hebu endeleeni kuwaangalia Waheshimiwa Madiwani, angalau na wenyewe hata wakiongezwa shilingi 100,000 au shilingi 200,000 posho za kujikimu, ikafika kwenye shilingi 400,000 na kitu au shilingi 500,000, tutakuwa tumewasaidia sana. Mwisho wa siku na wenyewe wapande hadhi sasa walipwe mishahara. Wanafanya kazi kubwa, nasi Wabunge tunawategemea sana Waheshimiwa Madiwani watusaidie tukiwa huku Dodoma. Wao ndio wanafanya kazi kule usiku na mchana kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine sasa, Wakurugenzi waache visingizio vya kukosa pesa za vikao. Wameshapunguziwa mzigo mkubwa sana kwenye hii shilingi 350,000/=, wafanye vikao kwa wakati. Kamati ya Fedha inatakiwa kukaa kabla ya tarehe 15 kila mwezi, lakini baadhi ya Halmashauri wanakaa miezi mitatu halafu wanapitisha miezi miwili yote kwa pamoja kwa siku moja. Au miezi mitatu wanapitisha kikao cha siku moja, lakini kisingizio ni nini? Mkurugenzi anasema hana pesa. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri hili nalo mliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nawashukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wako kwa kututengea shilingi milioni 600 kwa kila Jimbo kwa ajili ya sekondari ya kata. Nina ushauri kidogo hapa Mheshimiwa Waziri. Mfano kwangu tuna upungufu katika Kata ya Kweuma, Mkindo, Lubungo, Kikeo, Msongozi na Homboza. Nina upungufu wa kata sita hazina sekondari ya kata. Kwa hii shilingi milioni 600 kila mwaka itabidi nikae miaka sita ndiyo jimbo langu zima liwe limepata sekondari za kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, hii shilingi milioni 600 kama inawezekana, kama mtaona mnaweza mkaigawanya na Halmashauri wenyewe kwa kushirikiana na Mbunge na Waheshimiwa Madiwani wakaweza kuhamasisha wananchi wakachangia fursa, hii shilingi milioni 300 ikanunua vitu vya madukani; mabati, nondo, cement na kulipa fundi, tunaweza tukajenga sekondari mbili kwa shilingi milioni 600. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna sekondari ambazo tumezijenga wenyewe, Serikali imekuja kumalizia kwa fedha ndogo sana. Sasa shilingi milioni 600 ni fedha ambazo tunaishukuru sana Serikali kutupatia, lakini kwa sekondari ambazo ni nyingi kama kwangu mimi; sekondari sita, hatutaweza kumaliza kwa muda mfupi, itahitaji miaka sita ili tuweza kuzimaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishukuru Serikali, kwa kipindi chote, bajeti ya TARURA katika Wilaya ya Mvomero haizidi shilingi milioni 600. Sasa hivi kwa mwaka huu wa fedha mmetenga shilingi milioni 815. Nina imani tutakwenda kutengeneza barabara hizi za TARURA vizuri zaidi na hasa barabara za pembezoni mfano Kata ya Maskat, Kata ya Kinda, Kibati Pemba, Kikeo, Nyandila na maeneo mengine, hizi barabara za TARURA ziweze kupitika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, tulilalamika hapa wakati tunachangia bajeti ya TAMISEMI kuhusu suala zima la TARURA na mmesikia kilio chetu, mmeweza kutuongezea shilingi milioni 500 nje ya bajeti. Hizi zitakwenda kufanya kazi kubwa na nzuri katika Jimbo letu. Nami nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri kama kila mwaka tutaendelea kupata hizi shilingi milioni 500 basi miji ile yote ambayo iko ndani ya Wilaya yetu ya Mvomero tunakwenda kuipa vipande vidogo vidogo vya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni hii faini ya boda boda. Faini ya Boda boda ilikuwa ni shilingi 30,000/=. Mama yetu amesikia kilio, mmepunguza mpaka shilingi 10,000/=. Tatizo kwenye hizi faini sasa, Askari wanapokamata pikipiki, badala ya kulipa lile kosa moja shilingi 10,000/= sasa watalipa makosa nane, tisa mpaka 10. Ile shilingi 30,000/= itarudi na zaidi ya ile 30,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi na bahati nzuri Waziri wa Mambo ya Ndani uko hapa, hawa Askari wakikamata hizi pikipiki, anaweza akawa amekamata kwa kosa moja pengine la kutokuvaa helmet, yule dereva wa bodaboda hana ile hela, anachukua pikipiki wanaipeleka kwenye Kituo cha Polisi. Wakati pikipiki iko pale, anapoenda kuitafuta shilingi 10,000 au ile shilingi 30,000 ya zamani ili aende akagomboe ila pikipiki, akirudi pale anaambiwa hii pikipiki ilifanya mauaji, ilibeba mtu ambaye amekwenda kushiriki mauaji. Yule dereva wa bodaboda anakimbia anaitelekeza pikipiki na yule mwenye pikipiki hakanyagi kwa sababu anajua dereva wake alishakwenda kufanya mauaji na ile pikipiki. Mwisho wake ile pikipiki inakwenda kuuzwa kwa Askari wenyewe, wanauziana ile pikipiki. Baadhi ya vituo wamefanya hivyo, hata Mheshimiwa Waziri ukitaka ushahidi nitakupa. Wamekusanya pikipiki, wameshindwa kuzigomboa, wamewapa kesi za kutisha za mauaji, wamezitelekeza, wameuziana wenyewe maaskari hizi pikipiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii shilingi 10,000/= hii ambayo mama ametaka kuwalenga hawa vijana, kama hamtakuwa makini, watakwenda kutengenezewa kesi na pikipiki watazisahau kule kwenye vituo vya polisi. Kama ni faini, hatalipa shilingi 10,000/=, atalipa kuanzia makosa Matano, sita na kuendelea kama ambavyo walikuwa wanafanya. Kwa hiyo, Mheshimwa Waziri naomba hili nalo mliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni mpango wa bima nchi nzima. Hili ni jambo jema sana, lakini hizi zahanati zetu hazina madawa na wala hazina vifaatiba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu jioni ya leo. Nianze kwanza kumshukuru Mwenyekiti Mungu kwa kunijalia, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na na Manaibu Mawaziri, Katibu Mkuu na Manaibu wake kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya katika Wizara hii ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi kifupi, sisi Mvomero, tumepokea fedha nyingi sana za miradi na kipekee naomba nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, mwaka jana nilisema, niliomba fedha mbalimbali kwa ajili ya miradi na tumepata fedha nyingi na sasa hivi ninavyozungumza hapa miradi mingine inaendelea na utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Bashungwa hivi karibuni alifanya ziara Mvomero na alijionea mwenyewe miradi inavyoendelea. Pia alipata nafasi ya kwenda kuangalia sekondari ya kumbukumbu ya Sokoine, ambayo Serikali imetupatia fedha nyingi sana na hivi juzi juzi wametupa milioni 700 kwa ajili ya kuiendeleza ile sekondari ya Sokoine. Kwa bahati mbaya kulikuwa kuna shida kidogo kwenye milioni 700 na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri alifika akatoa maelekezo, kuna ubadhirifu wa zaidi ya milioni 200 na kitu, akatoa maelekezo watumishi zaidi ya tisa wachukuliwe hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze tena kwa mara nyingine Mheshimiwa Waziri, lakini mpaka sasa hivi ninavyozungumza hapa Bungeni, hakuna mtumishi hata mmoja aliyechukuliwa hatua Mheshimiwa Waziri. Kama watumishi hawa wataendelea kubaki pale bila kuchukuliwa hatua zozote hata za kinidhamu, Mheshimiwa Waziri ataendelea kutupa fedha lakini kuna watu wamejiandaa kuendelea kuzitafuna hizi fedha. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri maelekezo yake yazingatiwe na wale watumishi wachukuliwe hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sisi tumepokea fedha bilioni 2.2 kwa ajili ya madarasa 107 yale ya COVID, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Hapa nimpongeze pia Mkuu wangu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Halmashauri na Madiwani kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya ya kutekeleza kujenga vyumba hivi 107 katika kipindi cha miezi miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Mvomero tuna maboma mengi sana ya madarasa, tunaomba sana safari hii watutengee fedha katika bajeti kwa ajili ya kumalizia haya maboma, hii ni miradi viporo vya muda mrefu sana. Tunawakatisha tamaa wananchi, wanaanzisha wao wenyewe, lakini mwisho wa siku Serikali inachukua muda mrefu sana kuleta fedha za umaliziaji.

Sisi moja kazi ya mwanasiasa ni kuhamasisha, nikiwa jimboni kule nahamasisha tuanzishe ujenzi wa zahanati, ujenzi wa vyumba vya madarasa, ujenzi wa nyumba za Walimu, lakini tunapofika kwenye hatua ya lenter, Serikali inachukua muda mrefu sana kuleta fedha za umaliziaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao ujenzi wa zahanati iko pale Dakawa, ina zaidi ya miaka kumi ile haijamaliziwa na tumeomba sana, kila bajeti tunaomba fedha kwa ajili ya kuimalizia. Tuna imani sasa hivi watatuletea fedha ili tuweze kumaliza. Pia nimpongeze Waziri, wametupa milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Mziha na ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niende moja kwa moja kwenye suala la Madiwani. Mwaka jana nilisimama nikasema suala la Madiwani na wenzangu walizungumza sana masuala ya Madiwani lakini hata bajeti unaona kila Mbunge karibuni anachangia suala la Madiwani. Nimwombe sana Waziri, mwaka jana wamewapa nafuu halmashauri kwa maana Serikali moja kwa moja inakwenda kulipa zile posho za mwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa Waziri kumlipa moja kwa moja Mkurugenzi ili awalipe Madiwani wamewasaidia watu wa Benki, kwa sababu zile 350,000 asilimia zaidi ya 90 Madiwani wamekopa. Kwa hiyo, zile fedha zikienda kwenye halmashauri zinakwenda benki, Diwani kama Diwani pengine anabakia na 50,000. Kwa hiyo, nimwombe pamoja na jambo nzuri walilolifanya, safari hii Mheshimiwa Waziri aangalie namna ya kuongeza bajeti katika suala zima la Madiwani, angalau hata wakipata kwa kuanza shilingi 500,000, sasa hivi wanalipwa shilingi 350,000 ongeza shilingi 150,000, mpaka 2025 huko angalau watafikia hata kwenye shilingi 700,000 au shilingi 800,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimwombe Mheshimiwa Waziri na hawa wenzetu wapewe kibali cha msamaha wa kodi wawe na exemption upande wa magari. Waheshimiwa Madiwani, wanafanya kazi kubwa sana, wana uwezo wa kununua magari sio wote lakini wakipata msamaha wa kodi watakuwa na uwezo wa kununua magari na wenyewe watafanya kazi kwa urahisi, wataweza kuzunguka kwenye kata zao. Niombe sana suala hili linawezekana. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri angalau wapate msamaha wa kodi ili na wenyewe waweze kununua vyombo vya moto, waweze kufanya kazi usiku na mchana, za kusimamia fedha ambazo unazipeleka kwenye majimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa TBA, kama kuna bomu lingine lipo nchi hii ni hawa watu wa TBA, miradi yote ambayo inasimamiwa na TBA, miradi hii ina mambo matatu, moja lazima kutakuwa na ongezeko la mradi, thamani ya mradi ongezeko ni kubwa sana, kama mradi wa bilioni moja, hawa TBA wakisimamia watakwenda mpaka bilioni mbili na kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, muda, miradi hii haitaisha kwa wakati, kama TBA wanasimamia. La tatu, value for money katika miradi hii hakuna. Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri, miradi mingi siyo yote ambayo inasimamiwa na TBA kuna shida afuatilie, atupie jicho la tatu huo upande wa TBA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya, lakini la pili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri ambazo anazifanya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda mbele sana kwenye mchango wangu, naomba nitoe ushauri kwa dada yangu, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Tunapokaa hapa ndani Bungeni tunapokea hizi taarifa za utekelezaji wa bajeti kwenye maeneo yetu na taarifa za mgawo wa fedha. Naomba nishauri kwanza kabla sijaenda mbele kwenye mchango wangu; taarifa hizi ni nzuri tukizipata kabla ya fedha hizi hazijaenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nimepokea taarifa miradi kule yote imeshatekelezeka na imeshaisha, leo napokea taarifa, lakini ni vizuri tukiipata mapema inatusaidia na sisi kwenda kusimamia kwenye utekelezaji. Ni ushauri tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Waziri kwa kazi nzuri na namna ambavyo wanamsaidia Mheshimiwa Rais kutekeleza ilani yetu ya uchaguzi 2025, lakini pia sisi mpaka sasa Mvomero tumeshapokea bilioni 3 na milioni 700 ya kujenga vyumba vya sekondari 187. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake. Lakini nina ombi hapa, haya madarasa tuliyoyajenga shule nyingi hasa za pembezoni hazina walimu. Tumejenga madarasa mazuri, lakini walimu ni wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, tuna uhaba mkubwa wa madarasa kwenye shule zetu za msingi. Pamoja na fedha tulizozipokea, lakini tuna uhaba mkubwa wa madarasa, lakini pia tuna uhaba mkubwa wa madawati, tuna uhaba mkubwa wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe sana, tunayo maboma ambayo tuliyajenga kwa nguvu zetu na ni maboma mengi sana. Tunaomba maboma haya Mheshimiwa Waziri utuangalie kwa macho mawili utuwekee kwenye bajeti yako mwaka huu kwa sababu, haya maboma mengine yameanza kuanguka. Yako maboma ambayo yamejengwa toka 2017 mpaka leo maboma yale yapo hayajamaliziwa, lakini tunawakatisha tamaa wananchi. Wananchi wanajitolea kwa kujenga wenyewe maboma, lakini Serikali inachukua muda mrefu kuyamalizia haya maboma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niishukuru Serikali, Mheshimiwa Waziri. Mmetupa fedha za kumalizia maboma ya zahanati pale Dihinda, mmetupa milioni 50 na boma lile tumemaliza na zahanati inafanya kazi, pale Ndole mmetupa milioni 50 tumemaliza boma na zahanati inafanya kazi. Chenzema mmetupa milioni 50, lakini mmetupa juzijuzi hapa shilingi milioni 50 pale Kidudwe na zahanati inaendelea na ujenzi. Mmetupa milioni 50 pale Manyinga ujenzi unaendelea. Lakini mmetupa milioni 500 kwa ajili ya kujenga kituo cha afya pale Mziha na tumepokea milioni 600 kwa ajili ya kujenga pia, kituo cha afya pale Mlali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, bado tuna maboma mengi ya zahanati. Fedha tulizozipokea tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini tunaomba mwaka huu muendelee kututengea fedha kwa ajili ya kumalizia maboma ambayo tunayo katika Wilaya yetu. Pia tunazo nyumba za watumishi nyingi ambazo zimeanzishwa na wananchi, tunaomba pia mtusaidie ili tuweze kuyamaliza haya maboma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye TARURA, wenzangu wamezungumza hapa na wamempongeza Engineer wa TARURA na mimi nimpongeze. Tumepokea bilioni mbili na milioni 600 tumetengeneza barabara zetu, hasa zile za pembezoni, kule ambako ndiko wanatoka wakulima wetu, ndiko ambako tuna mazao ya kimkakati. Hizi barabara tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, tumezitengeneza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu na ombi langu kwenu, hizi barabara nyingine tumeshindwa kwa sababu ya bajeti kufika mwisho. Mfano, barabara ya kutoka pale Magunga kwenda Maskat, ile barabara ina urefu wa kilometa 15, lakini kwa awamu hii tumetengeneza kilometa nane. Bado tuna upungufu pale wa fedha ya kumalizia ile barabara kilometa saba. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti yako safari hii usituache, endelea kutupa fedha tumalizie hii barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, tuna barabara ya kutoka Muhonda kwenda Kweuma. Hii barabara na yenyewe haijafika mwisho kuna kipande kama cha kilometa tatu-nne, tunaomba Mheshimiwa Waziri na hii barabara utuangalie, utupe fedha tuweze kuimalizia hii barabara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Serikali, mmetupa fedha tumeweza kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami pale Dakawa. Tumetengeneza barabara kutoka Manyinga kwenda Madizini kwa awamu ya kwanza yumeishia pale stendi kwa kiwango cha lami. Tunategemea tutaendelea kupata fedha kwa ajili ya kumalizia hizi barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuna barabara ambayo tumeitengeneza ya kutoka Sangasanga kwenda Lubungo, tunataka barabara hii iende ikatokee Kilosa. Hii ni barabara ambayo ikiisha itakuwa ni barabara kubwa ya short cut kwa wakulima wetu ambao wanazunguka umbali mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, kwa sababu ya muda, Dakawa ni eneo kubwa sana la biashara, nilikuwa ninaomba Mheshimiwa Waziri safari hii mtupe fedha tuanze ujenzi wa soko la kimkakati, Dakawa. Na pale kuna wakulima wengi, kuna wafanyabiashara wengi, tukipata fedha tukajenga soko pale la kimkakati tutawasaidia sana wananchi wetu wa Mvomero, hasa wananchi wa Dakawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jingine nimalizie, fedha zote ambazo tunazipokea sisi Mvomero, hizi za miradi, hasa hii miradi ya sekondari, vyumba vya madarasa na hii miradi ya zahanati, hawa watumishi wetu kwa maana ya watendaji, fedha nyingi zinazokuja, hasa kwenye vituo hivi vya afya mfano pale Mziha tulipopokea milioni 500 fedha ile haijatosha. Sasa hivi wanasema tuwaongezee bajeti kwa ajili ya kumalizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hizi zahanati zetu ambazo tumepokea milioni Hamsini-hamsini wanasema tuwaongezee fedha za kumalizia baadhi ya maeneo, fedha hazijatosha. Mheshimiwa Waziri nikuombe, kama unataka kweli kumsaidia Mheshimiwa Rais, Imarisha kitengo cha ukaguzi wa ndani. Kama kuna eneo ambalo tunapigwa na kama kuna mchwa ambao wapo kwenye halmashauri zetu, basi ni hawa wataalam wa haya majengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila jengo ambalo limejengwa kwenye Halmashauri lazima utaambiwa fedha ziliongezwa. Mwanzo wanafanya tathmini jengo litaisha kwa milioni 50….

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JONAS V. ZEELAND: zikija milioni 50 wanasema tupe 30 tumalizie.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa maliza.

MHE. JONAS V. ZEELAND Naomba Mheshimiwa Waziri imarisheni kitengo cha ukaguzi wa ndani, mtamsaidia sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uzima. Pili, nimshukuru sana ndugu yangu Mheshimiwa Aweso pamoja na Naibu wake, kwa kazi nzuri wanazozifanya kwenye Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, sisi Mvomero, tuna miradi ambayo inaendelea ya zaidi ya shilingi bilioni 12. Nichukue nafasi hii pia kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mvomero, kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais, kwa kutupa fedha nyingi za Miradi ya Maji. Haijawahi kutokea kupata miradi mingi ya maji kwa pamoja kama ambavyo tumepata sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, yako mambo machache ambayo tutaomba utusaidie kwenye hii miradi ambayo wakandarasi wapo site wanaendelea na kazi. Mfano kule Kibogoji na Pandambili, mlitupatia milioni 530 na mradi ule umekamilika. Lakini kuna tatizo baadhi ya vituo havitoi maji na mradi huu hauna hata miezi mitatu, minne.

Mheshimiwa Spika, tuna Kijiji kimoja pale Dibuluma kipo katika Kata ya Kibati hakina maji kabisa. Tunaomba mtusaidie ili ili tuweze kuunganisha vijiji vyote vya kata ya Kibati viweze kupata maji. Tuna vijiji vya Ndole kule Kinda, Matale pale Mvomero mmetupatia milioni 978, tatizo pale bado kitongoji kimoja ambacho kipo kwenye mkataba wa mkandarasi, kitongoji kile hakijapata maji na mkandarasi hataki kuweka maji kwenye kile kitongoji. Nimekwisha zungumza sana na engineer wetu wa Mkoa na engineer wa wilaya lakini bado tatizo hili halijaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa mara ya kwanza Tarafa ya Mgeta ambayo ina vyanzo vyenye uhakika vya maji, haikuwahi kupata miradi mingi kama ambavyo umetupatia safari hii. Mwaka 2021 nilismama hapa nikakuomba miradi mingi sana nashukuru sana mmetupa ile miradi. Tuna miradi kule Chenzema, Luale, Kibuko, Londo, Masalawe na Kibagala, mkandarasi anaendelea kazi ya shilingi bilioni 2.2 mkandarasi yuko kwa asilimia 60. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto hapa Mheshimiwa Waziri, mkandarasi huyu anapo rise certificate kwenu mnachelewa sana kumlipa. Kazi hii itachukua muda mrefu kama atacheleweshewa malipo yake. Naomba anapoleta certificate alipwe kwa wakati ili kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna mradi kule Lusungi – Mwalazi wa shilingi bilioni 2.3 mradi huu unakwenda kwenye vitongoji vya Nyabeni A na Nyabeni. Niliomba mwaka 2021 tunashukuru mmetupatia hizi fedha mkandarasi yuko kwa asilimia 25 na yeye anasuasua, ukimuuliza nini anasema malipo hajapata.

Mheshimiwa Spika, tuna mradi mkubwa na Mheshimiwa Waziri ulikuja Mvomero, wananchi wamefurahi sana ujio wako uliokuja kule Mvomero. Kazi kubwa ambayo tunaifanya ya kutoa maji kule Bunduki - Maguruwe yanapita Homboza – Mlali halafu yanakwenda Kipela, Kinyenzi, Mkuyuni, Lukuyu, Mgeta. Vijiji vingi vitapata maji kutokana na huu mradi isipokuwa kuna vijiji viwili ambavyo viko kwenye kata ya Mlali, Kijiji cha Vitonga na Lugono hamjaweka kwenye huu mradi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana ule mradi haiwezekani watu wa Kipela wapate maji, watu wa Mkuyuni wapate maji lakini watu wa Vitonga na Lugono wasipate maji wakati maji yatakuwa yamefika karibu kabisa na maeneo yao. Mheshimiwa Waziri, niombe sana tufanye marekebisho kidogo, mkandarasi aongezewe fedha aweze kufikisha maji kwenye hivi vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, Mheshimiwa Waziri, Tuliani tuna mradi mkubwa wa maji wa shilingi bilioni 3 na milioni 600, mkandarasi yupo site. Lakini nina wasi wasi na huyu mkandarasi atakuwa ni msanii mjanja mjanja. Kwa sababu mpaka sasa hivi amefanya kazi chini ya asilimia 10. Mradi wa bilioni 3.6 atamaliza mwaka gani? Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri, Wizara yako imchunguze huyu mkandarasi nina wasi wasi nae.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye Mradi wa TUILIWASA ambao huyu mkandarasi wa bilioni 3.6 anakwenda kusambaza maji kwenye Tarafa nzima ya Tuliani. Tatizo la ule Mradi wa TULIWASA bili ambazo wananchi wanalipa, wanaletewa bili mwisho wa mwezi baada ya kutumia ni kubwa sana. Huu mradi haya maji ni ya mseleleko sio maji ya kuvuta na umeme. Hayana gharama kubwa sana kuyapata haya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa mwezi wanapewa bili kubwa kiasi kwamba wanashindwa kulipa, wengine sasa hivi wanaanza kutumia visiwa. Watu wa TULIWASA wanaanza kuwakamata watu ambao wanataka kuwasaidia wananchi kuwachimbia visima. Sasa kama wao wanashindwa kuja na bei ambayo mwananchi wa kawaida ataweza kulipa mwisho wa mwezi, wawaache hawa wananchi wakitaka kutumia visima watumie visima. Kama wanataka washushe unit moja ya maji iende mpaka 840 ili wananchi waweze kulipa mwisho wa mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna mradi mkubwa pale Dakawa wa bilioni 2.3. Mkandarasi amesaini mkataba huu mwezi wa pili anasuasua tu hatujui tatizo ni nini? Leo nimezungumza na Injiania wa Mkoa amenihakikishia wiki ijayo ataanza kazi wako kwenye makabidhiano. Sasa miezi miwili fedha za Mheshimiwa Rais zimeletwa ziko pale mkandarasi haeleweki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana mmetupatia fedha za kuchimba vizima tisa kwa milioni 378, tumechimba kule Msongozi. Kata ya Msongozi ina tatizo kubwa sana la maji. Pia pale Magali, Melela, lugono, Makuyu kule Mvomero, Milama, Manza na Sokoine.

Mheshimiwa Spika, kipekee nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, nilikuomba utusaidie kutupatia fedha kwa ajili ya kutatua tatizo la Maji pale Sokoine. Wananchi wa Sokoine walikwa wanakunywa maji na Wanyama. Ziko clip ambazo nilikutumia Mheshimiwa Waziri na nilikuomba utusaidie, ukatupatia mitambo imechimba visima virefu na sasa hivi wanaendelea na ujenzi, wanajenga chumba kikubwa kwa ajili ya kuhifadhi mashine lakini wanajenga pia na tank kwa ajili ya kuhifadhia maji waanze kusambaza kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, niombe sana msukumo wako kwa sababu wananchi wa Sokoine wameteseka kwa muda mrefu kwenye adha ya maji. Niombe msukumo wako kwa huyu ambae anasimamia pale mradi, ahakikishe kwamba mradi huu ikiwezekana mwezi wa saba kama ulivyotuahidi ulivyokuja Mvomero ili wananchi waanze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda Mvomero tuna shida ya gari. Mheshimiwa Waziri, hatuna gari, injinia wetu ana gari bovu halijapata kutokea. Tunaomba utupe gari ili injia aweze kukimbia kimbia. Kwa sababu ya jiografia yetu nafikiri unaijua vizuri…

SPIKA: Mheshimiwa Jonas, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa na mimi nafasi niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Maliasili, pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi hii ya uzima. Nami nielekeze mchango wangu moja kwa moja bila kupoteza muda kwenye Wizara yetu hii ambayo ni muhimu sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze na mimi kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa Royal Tour ambayo imefanya vizuri na imeongeza watalii wengi sana katika nchi yetu. Pia nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wako kwa kazi kubwa na nzuri ambazo mnazifanya katika nchi hii, katika kipindi kifupi nafikiri miezi mitatu na siku kadhaa tumeona mabadiliko makubwa na sisi tunaimani sana na wewe. Nikuambie Mheshimiwa Waziri nilipanga kushika shilingi leo lakini kwa namna ambavyo nakuamini nina imani yote ambayo umetuambia yatakwenda kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu nataka kuboresha tu kwenye hotuba yako ili uweze kuona namna nzuri ya kutusaidia watu wa Mvomero. kwanza ni suala la Tembo.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2021 nilichangia kwenye Wizara hii ya Maliasili kwenye upande wa tembo, mwaka 2022 nilichangia na leo 2023 hakukuwa na utekelezaji wa aina yoyote lakini nina imani kama nilivyosema sasa unakwenda kutusaidia na kutatua changamoto tulizo nazo katika Wilaya yetu ya Mvomero.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri sasa hivi tembo katika nchi hii wana thamani kuliko binadamu, wenzangu wengi waliochangia hapa wameeleza kwenye maeneo yao namna ambavyo tembo wanawasumbua wananchi. Mvomero tumepakana na Hifadhi ya Mikumi, mpaka nazungumza hapa Mheshimiwa Waziri, tembo wameshaua wananchi 37. Wananchi wameshapoteza Maisha 37 kwa kipindi kifupi tu, wiki mbili zilizopita tumetoka kumzika ndugu yetu pale Mkata ameuawa na tembo.

Mheshimiwa Spika, pia wananchi ambao mashamba yao yameharibiwa na hawa wanyama ni zaidi ya 2,500, hakuna chochote walicholipwa. Tunajua hakuna fidia kuna kifuta machozi na kuna kifuta jasho ambacho kwanza ni kidogo sana, leo mwananchi shamba lake likiharibiwa na tembo anatakiwa ekari moja alipwe laki moja, tunafahamu gharama za kutayarisha shamba, gharama za kupanda, kulima, mpaka kuvuna, leo shamba likiharibiwa na tembo anatakiwa kulipwa kiasi kisichozidi laki moja.

Mheshimiwa Spika, pia mwananchi ambaye ameuawa na tembo familia yake inatakiwa kulipwa kifuta machozi kisichozidi milioni moja. Hizi ni kanuni zilizopitwa na wakati Mheshimiwa Waziri, tunawaumiza wananchi na hawa wananchi siyo kwamba wanataka hizi fidia, siyo kwamba wanataka hiki kifuta machozi na kifuta jasho, wanataka kuishi kwa amani hawataki kuishi na tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashangaa naomba leo nizungumze kwa kawaida tu, hivi Serikali imeshindwa kweli kuwarudisha tembo na kuwapeleka kule kwenye hifadhi? Ina maana kwamba hawa watalii ambao wanakuja kwenye hizi hifadhi zetu hawariziki na wale tembo ambao wako mle kwenye zile hifadhi? Sasa hawa tembo ambao wako nje ya hifadhi wanafanya nini Mheshimiwa Waziri? Watu wanaisha, watu wanapotea na hawo ni Watanzania wenzetu! Kifuta machozi chenyewe na kifuta jasho ni kidogo na hawalipwi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mvomero toka mwaka 2019 mpaka leo hakuna mtu aliyelipwa, lakini inaonesha Serikali inathamini sana tembo kuliko binadamu. Niliona kwenye hotuba yako kwamba utakuja sasa na sheria mpya ambayo itaweza kuwasaidia wale wananchi ambao wanakutana na hii adha ya tembo na tuondokane sasa na haya mambo ya kikoloni, haya mambo ya kulipana laki moja na milioni moja yalishapitwa na wakati. Tembo akienda kufanya uhalibifu kwenye maeneo ya wananchi kuwe na sheria ya kumlipa mwananchi fidia siyo kifuta machozi na kifuta jasho kama vile hisani, kuwe na fidia ambayo atakwenda kulipwa huyo mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Waziri, mimi nina ushauri na sidhani kama Serikali mnashindwa, hivi ile Hifadhi ya Mikumi, sisi tuna Kata Saba ambazo zimepakana na Hifadhi, wale tembo waliopo kwenye hizi Kata Saba kwenye hii Tarafa ya Mlali, hivi mkiwarudisha kule halafu mkaweka fensi kwenye ile hifadhi hata zile fensi za umeme ambazo mnazipa umeme baadae mnyama akitaka kwenda kugusa fensi anapigwa shot anarudi, hivi Serikali na yenyewe inashindwa kuweka hizi fensi?

Mheshimiwa Spika, mbona wananchi wa kawaida katika maeneo mengine wanaweka hizi fensi? Ama kuchimba mtaro mkubwa ili wanyama wasiweze kuvuka na lenyewe linashindikana hili? Wako wakulima wetu katika Tarafa hii ya Mlali wana mashamba lakini wamezungusha fensi wamechimba mifereji hakuna mnyama anayeingia katika mashamba, sasa nashindwa kuelewa Serikali inashindwaje kuweka fensi hata ya waya wa umeme wa kuzuia wanyama hawa wasiende kwenye maeneo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tembo ni wengi sana, wananchi sasa hivi hawalimi Kata ya Doma pale Kijiji cha Doma kule Mahalaka hali mbaya, hakuna mwananchi anayelima na kule tunajua wananchi wetu wanajishughulisha na shughuli za kilimo, kuna kilimo cha biashara wanalima nyanya na kuna kilimo cha chakula, pale Msongozi, Mkata, Mangaye Kata nzima ile hakuna mwananchi analima, Merela hakuna mwananchi yeyote analima, Rubungo na Mlali yote kwa ujumla hakuna mwananchi anayelima. Sasa Mheshimiwa Waziri ninakuomba na kwa sababu ninakuamini na hata ulivyoteuliwa kwenye Wizara hii mimi nilinyoosha mikono juu na kumshukuru Mungu kwamba matatizo haya sasa yanakwenda kuisha. Nimeona kwenye hotuba yako umesema Tanzania kwa Afrika tumekuwa watu wa tatu kama sikosei kwa kuwa na tembo wengi, Kimataifa huko tuna sifa kubwa ya kuhifadhi tembo lakini hawa tembo ambao huko nje tuna sifa huku ndani wanaua wananchi.

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana, naomba shughulikia masuala haya ya tembo. Pia nikupongeze nilikuomba siku moja unisadie tuweze kukutana na watu wa TAWA na ukatoa maelekezo tukakutana na watu wa TAWA tukafanya kikao kama wiki tatu zilizopita. Kikao kile nina imani kama yale tuliokubaliana yatatekelezeka hii changamoto kama siyo kuisha inakwenda kupungua kwa kiasi kikubwa, ninakupongeza sana kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Waziri sisi Mvomero tuna hifadhi ya Wami Mbiki na kuna Hifadhi ya Msitu. Hifadhi hii ya Wami Mbiki ni hifadhi ambayo ina migogoro na wananchi wanaopakana na hii hifadhi kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema toka nimekuwa Mbunge na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais ile timu ya Mawaziri Nane, pamoja ya kwamba hii timu imekwenda kukagua yale maeneo na kuanza kupima. Mimi kama Mbunge sijui na wananchi hawajashirikishwa lakini tuna imani itakwenda kututendea haki, nimeona kwenye hotuba yako ulisema utawaagiza Wakuu wa Mikoa haraka iwezekanavyo waende wakamalize haya matatizo ya mipaka katika hizi hifadhi. Mimi nina imani pale katika Hifadhi yetu ya Wami Mbiki tunakwenda sasa kumaliza yale matatizo ili wananchi wetu sasa waweze kulima kwa uhuru. Wamekuwa wakinyanyasika miaka yote, wamekuwa wakinyanyasika kila siku wanashindwa kujua hatma yao lakini kwa maelekezo yako nina imani mambo yanakwenda kukaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuna Hifadhi ya Msitu wa Magote, hii hifadhi ilianzishwa mwaka 1940. Wananchi wameishi ndani ya hii hifadhi katika kipindi chote, kuanzia mwaka 1940 mpaka leo wananchi wapo kwenye ile hifadhi na watu wamezikana mababu na mababu katika ile hifadhi. Leo Serikali inataka kuwaondoa hawa wananchi ili hifadhi hii sasa waanze kupanda miti watu wa TFS, wakati hifadhi hii eneo lote la hifadhi kuna shughuli za kijamii na watu wamejenga, watu wamezikana, hakuna eneo lililobakia. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri hifadhi hii ni hifadhi ndogo sana, ipo pale Jongoya. Ninaomba busara zako utusaidie hifadhi hii wapewe wananchi ili tuweze kuondokana na adha. (Makofi)

SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)