Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Innocent Edward Kalogeris (8 total)

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuvuna mamba katika Mto Ruvu hasa katika Vijiji vya Kigamila, Bwila juu, Magogoni, Bwila chini, Kongwa, Tulo, Lukuhinge, Kata za Mvuha na Serembala katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini, ili kupunguza vifo vinavyosababishwa na mamba hao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kufanya tathmini ya mamba katika mito iliyopo katika Mikoa ya Katavi, Rukwa na Morogoro. Baada ya tathmini hiyo kukamilika na kubainika kuwa idadi ya mamba waliopo ni kubwa, mamba hao watavunwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, endapo itabainika kuwa idadi ya mamba katika maeneo husika ni ndogo, Serikali itabaini mamba wanaosababisha adha kwa wananchi na kuwavuna ili wasiendelee kuleta madhara makubwa kwa wananchi. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, ni lini ahadi ya ujenzi wa uwanja wa mpira Dodoma iliyotolewa na Mfalme wa Morocco itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana na kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefuatilia utekelezaji wa ahadi ya ujenzi wa uwanja wa mpira Dodoma iliyotolewa na Mfalme wa Morocco. Mawasiliano kuhusu utekelezaji wa mradi huo baina ya Serikali ya Tanzania na Morocco bado yanaendelea. Vilevile katika kuhakikisha kwamba mradi huu unatekelezwa Serikali imedhamiria kutafuta fedha kutoka katika vyanzo mbalimbali vikiwemo sekta binafsi na wabia wa maendeleo.
MHE. DENNIS L. LONDO K.n.y. MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, ni lini TFS itaanza kutoa vibali vya malisho kwa wafugaji kama inavyotoa vibali vya kuvuna mbao na mkaa ili Serikali ipate mapato?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Misitu, Sura ya 323, Kifungu cha 26(n) kinakataza kuingiza au kuchunga mifugo kwenye maeneo ya hifadhi. Aidha, Kanuni za Misitu za mwaka 2004, Kifungu cha 14(4) kimeweka katazo la kutoa vibali vya kuchunga au kulisha mifugo au kufanya shughuli za kilimo kwenye hifadhi za misitu.

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kuwa kuchunga, kulisha mifugo au kufanya shughuli za kilimo kwenye maeneo ya hifadhi za misitu ni kuvunja sheria. Hivyo, sheria zimewekwa ili kulinda rasilimali zilizomo hifadhini kwa matumizi endelevu ya rasilimali za misitu kwa kizazi cha sasa na vijavyo.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kujenga vyumba vinne vya madarasa na bweni katika Shule ya Sekondari Matombo Kata ya Konde?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Sekondari Matombo iko katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro. Shule hii ni ya kidato cha kwanza hadi cha sita, hivyo, kutokana na ongezeko la wanafunzi wanaofaulu mtihani darasa la saba na kidato cha nne kila mwaka shule inahitaji miundombinu ya kutosha ikiwemo bweni na madarasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI alitembelea na kuona hali halisi ya miundombinu ya Shule ya Sekondari Matombo tarehe 22 Septemba, 2021 na kuahidi kujenga madarasa manne na bweni moja mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia programu zake mbalimbali ikiwemo SEQUIP na EP4R zinazojenga miundombinu ya elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, kuruhusu Benki kuwa Wakala wa Bima Serikali haioni kuwa Mawakala wengine watafunga biashara kwa kukosa wateja?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) pamoja na wadau wa bima ilianzisha BenkiWakala wa Bima ili kuongeza wigo wa usambazaji na upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi. Idadi ya Mawakala wa Bima wa Kawaida imekuwa ikiongezeka sambamba na BenkiWakala wa Bima kwa sababu hali hii imechochea ushindani, ubunifu na kutegemeana. Takwimu zinaonesha BenkiWakala waliosajiliwa kwa mwaka 2020 wako 14; mwaka 2021 wako 23; mwaka 2022 wako 27; na hadi 30 Machi, 2023 walishafika 30. Aidha, Mawakala wa Bima wa Kawaida waliosajiliwa kwa mwaka 2020 walikuwa 745; mwaka 2021 walikuwa 789; mwaka 2022 walikuwa 910; na kwa mwaka 2023 hadi Machi, 2023 wameshafika 960.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa takwimu hizi, ni dhahiri kuwa Mfumo wa BenkiWakala wa Bima umesaidia kukuza biashara ya Bima hapa nchini.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga shule ya msingi ya watoto wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Halmashauri ya Morogoro ina watoto wenye mahitaji maalum. Hadi sasa halmashauri imeanza kujenga bweni kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum katika shule ya msingi Mvuha. Shule hii ina jumla ya wanafunzi 24, Serikali tayari imekwishapeleka kiasi cha shilingi milioni 100 katika shule hii katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya ujenzi wa bweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga na kupeleka fedha katika Halmashauri ya Morogoro kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza:-

Je, lini Serikali itaiongezea fedha TARURA kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Jimbo la Morogoro Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. NDUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TARURA imeendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini. Bajeti ya utekelezaji wa miundombinu ya barabara imeongezeka kutoka kilometa 51.5 kwa shilingi milioni 660.95 kwa mwaka wa fedha 2020/2021 hadi kilometa 65.90 kwa shilingi bilioni 1.88 kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2023/2024 jumla ya shilingi bilioni 2.2 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya barabara yenye urefu wa kilometa 85.9. Serikali itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya uimarishaji wa miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Mahakama za Mwanzo katika Tarafa za Bwakira, Mvuli na Matombo – Morogoro Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu sasa swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango na Bajeti ya mwaka 2023/2024, Mahakama ya Mwanzo katika Tarafa ya Bwakira, Kata ya Bwakira Chini itajengwa ili kuwawezesha wananchi katika maeneo hayo kupata haki kwa wakati. Tayari zabuni imetangazwa kwa ajili ya kumpata mkandarasi wa ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mahakama za Mwanzo; Matombo na Mvuha, majengo yaliyopo ni chakavu sana na hivyo kuhitaji ujenzi mpya. Hata hivyo, kutokana na mahitaji makubwa yaliyopo katika maeneo mbalimbali, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Matombo na Mvuha utazingatiwa kwenye Mpango ujao wa ujenzi wa Mahakama, ahsante.