Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Francis Leonard Mtega (16 total)

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, pamoja na TANROADS kujitahidi kukarabati barabara ile, lakini nyakati za masika imekuwa ikikata kabisa mawasiloiano; na kwa kuwa, amekiri kwamba, ni muhimu sana kwa kusafirisha mazao na isitoshe wananchi wale wanaitegemea sana barabara ile kwa huduma mbalimbali za kijamii kupeleka wagonjwa hospitali, lakini bidhaa mbalimbali za matumizi ya kila siku. Je, Serikali haioni kwamba, sasa ipewe kipaumbele ili ujenzi wa barabara ile kwa kiwango cha lami uanze haraka iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mkoa wa Mbeya tuna uwanja mkubwa wa ndege wa kimataifa na Mheshimiwa Rais amenunua ndege kubwa, Dreamliner na barabara ile inapita kandokando mwa lango kuu la Kusini kuingia Hifadhi ya Ruaha (Ruaha National Park), sasa watalii wangepitia lango lile la Kusini kwa urahisi kabisa. Je, Serikali haioni kwamba inakosesha pato la Taifa hasa pesa za kigeni? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwa sababu ya umuhimu wa hiyo barabara ndio maana tayari taratibu za kuanza kujenga kwa kiwango cha lami zimeshaanza na zimeshatengwa tayari bilioni 3.38 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mbarali kwamba, kwenye bajeti zinazofuata nina hakika barabara hii itatengewa fedha zaidi, ili iweze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya umuhimu huu kama alivyosema kwenye swali lake la pili kuhusu uwanja wa ndege nasema ndio maana tayari hii barabara kwa Serikali kutambua umuhimu wake ikiwa ni kupokea wageni kutoka uwanja wa Songwe, lakini na kuwapeleka kwenye mbunga, ndio maana tayari taratibu za Serikali zimeanza za kukamilisha ama kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Moja, hivi tunavyoongea, juzi makundi makubwa ya tembo wamevamia vijiji vyote vitano vya Kata ya Igava na wameshambulia mazao yote; mahindi, mpunga na maboga. Sasa wananchi wale wapo hatarini kupata janga la njaa. Ni lini Serikali itawalipa fidia wale wananchi kuwanusuru wasipatwe na janga la njaa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa ng’ombe wakiingia hifadhini kwa bahati mbaya, ng’ombe mmoja huwa anatozwa shilingi 100,000/=, sasa makundi ya tembo wale wametetekeza mazao yote na nimeenda juzi nimekuta ni mashimo matupu mashambani: ni kigezo gani au ni thamani gani watalipwa wale wahanga ambao ni wafugaji na wakulima wa sehemu ile? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuhusu fidia, tumekuwa tukifanya uthamini pale ambapo kunatokea changamoto hiyo ya tembo kuingia kwenye maeneo ya kilimo na tunapofanya uthamini tuna-compensate wananchi kulingana na uthamini ulivyofanyika.

Mheshimiwa Spika, kuna uthamini wa aina mbalimbali; kuna mwananchi kuwa amepoteza Maisha, na upande mwingine kupoteza mazao na pia wananchi kujeruhiwa. Kwa hiyo, tunalipa fidia kulingana na athari ilivyojitokeza.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu changamoto ya namna ambavyo tunatoza ng’ombe shilingi 100,000/=; kwanza naomba sana wananchi watambue kwamba sisi tupo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hifadhi hizi zinalindwa na zinatunzwa kwa ajili ya manufaa ya nchi kwa ujumla na wananchi waliopo kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, mara nyingi kumekuwa na sintofahamu hasa kwa wafugaji kwamba wanaingiza ng’ombe zao kwenye hifadhi kwa makubaliano ya watumishi walioko kwenye maeneo husika na matokeo yake wanyama ambao wanahifadhiwa kwenye maeneo yale wanakutana na changamoto za magonjwa. Sasa Serikali inajikuta inagharamia gharama kubwa kufanya utafiti wa gonjwa lililoingia kwenye hao wanyama na kuwatibu. Kwa hiyo, tunajitahidi sana kuzuia wafugaji wasiingize mifugo yao kwenye maeneo ya hifadhi. Tutambue kwamba sheria ni sisi wenyewe tulizitunga, kwa hiyo, sisi ni watekelezaji wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kiwango hiki kipo kwenye sheria, siyo kwamba sisi tumekiamua; kipo kwenye sheria ya Wanyama kwamba wananchi wanapoingiza mifugo yao kwenye maeneo ya hifadhi, basi tunatumia hiyo sheria kuhakikisha kwamba inatumika sawa sawa. Ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na zaidi nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Hata hivyo, nina swali la nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wakulima wale mpaka sasa hivi tunavyoongea, bado mazao ya mahindi na mpunga ni mengi sana na kwa kuwa, wanaelekea msimu mpya wa kilimo na bei ya mbolea iko juu na wengine wanashindwa kufanya marejesho ya benki.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami kwamba muda umefika sasa wa kuunda task force maalum ya Waheshimiwa Mawaziri. Pengine ikijumuisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wa Kamati za sekta husika, ili waende mahsusi kutafuta masoko kabla ya msimu mpya wa kilimo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA
AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbarali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi anavyofuatilia upatikanaji wa masoko ya bidhaa ikiwemo mchele, na mahindi. Lakini pia, ninakubaliana na wazo la Mheshimiwa Mbunge kwa kuunda hiyo task maalum kwa ajili ya kutafuta hayo masoko. Lakini pia ninaomba kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba, juhudi nyingi sana hivi sasa zinachukuliwa na Serikali katika kutafuta masoko ya bidhaa hizo. Hivi sasa ninavyosema kuna timu ya Wizara ya Kilimo ambayo iko nchini Comoro, mahsusi kwa kutafuta soko la bidhaa ya mchele na mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni juzi tu, timu hiyo ilitoka South Sudan kwa nia hiyo hiyo ya kutafuta soko la mahindi na mpunga na mwisho ninapenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba, TANTRADE wana utaratibu maalum wa kuwasiliana na Balozi zetu ambazo ziko nje mahsusi kwa ajili ya kutafuta soko kwa bidhaa za Tanzania ikiwemo za mpunga na mahindi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushuruku sana lakini pia nashukuru sana majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwanza, kutoka barabara kuu kufika Kitulo pana mlima wenye kona 54 na nyani wa kutosha. Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ile kwa kiwango cha lami ili watalii wakafurahie nature ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; je, Wizara ina mpango gani wa kujenga ofisi walau ndogo pale Chimala ili kuamsha ari ya wananchi pale kujenga mahoteli ya kitalii jambo ambalo litaleta fursa ya ajira kwa vijana na kuinua uchumi wa Wanambarali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbalali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna changamoto ya barabara hii na tutazungumza na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi ili tuone namna ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami na hii itasaidia kuvutia utalii katika maeneo yanayozunguka Hifadhi ya Kitulo.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la ujenzi wa ofisi ninaomba nilichukue tukafanye tathmini kuangalia namna iliyo bora ya kufikika kiurahisi, lakini pia kuwepo na hicho kituo ambacho kinawezesha muendelezo wa utalii. Naomba kuwasilisha.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Wakulima wa skimu za umwagiliaji Matebete, Chosi, Herman, Isenyela wanapata shida sana wakati wa uhaba wa mvua kwa kupeana zamu usiku, na wengi wao wanazunguka na mapanga usiku kucha.

Je, Serikali itawaboreshea skimu hizi lini ili kuondoa adha hii na waweze kulima kwa tija?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Mbarali tuna miradi ya umwagiliaji ambayo tumeitengea fedha ya kiasi cha shilingi bilioni 61 ambayo inahusisha Herman Chosi, Bonokuva Gigolo na kwenda katika Matebete, tunakwenda Ifenyela na Uturo. Haya yote niliyoyataja wakandarasi wameshapatikana na muda wowote kazi ya utekelezaji wa miradi hii unaanza.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na napongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa maboresho makubwa, hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, moja; ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha hasa madaktari na wauguzi?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; ni lini Serikali itapeleka vifaa vya kutosha katika Kituo cha Afya Chimara lakini pia Kituo cha Afya Igurusi ili waweze kutoa huduma za upasuaji? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshapeleka vifaa tiba vya shilingi milioni 418 katika Halmshauri ya Mbarali, lakini katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 69.65 kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba kwenye vituo vya afya na hospitali za halmashauri pamoja na zahanati zilizokamilika. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la kupeleka vifaa tiba kwenye vituo vyetu ni endelevu, lakini pia vituo hivi vya Mbarali vitapata vifaa tiba hivyo.

Mheshimiwa spika, lakini pili katika mwaka wa fedha uliopita Serikali iliajiri watumishi 10,462 na Halmashauri ya Mbarali ilipata watumishi 51 wakiwemo madaktari na wauguzi na Seriakli itaendelea kupeleka watumishi hao katika halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu maziuri ya Mheshimiwa Waziri, na ya kueleweka nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa mchakato wa huu ni mrefu, je, Serikali itakubaliana nami kwamba kuna ulazima wa kuongeza vyombo vya usafiri katika Halmashauri ya Mbarali, hasa kwenye sekta ya elimu, afya, TASAF na kadhalika ili waweze kuwahudumia wananchi kikamilifu?

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa TARURA ipo chini ya TAMISEMI, je, Mheshimiwa Naibu Waziri haoni kuwa kuna ulazima wa kuhamasisha hii TARURA sasa ikarabati zote zilizoharibiwa na mvua kubwa iliyokuwa inanyesha kipindi kilichopita, ili wananchi waweze kupata huduma za kijamii kwa urahisi na pia kusafirisha mazao yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA
MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Leornard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni kuhusu usafiri. Nimhakikishie tu kwamba Ofisi ya Rais TAMISEMI tumeshaanza huo mchakato. Mwaka jana tuligawa magari, kwa maafisa elimu sekondari, na mwaka huu vilevile tumeshaagiza magari mengine 184 kwa ajili ya maafisa elimu wa shule za msingi ambayo tumeshapata awamu ya kwanza 35 na mengine yanakuja, lakini yote yameshalipiwa.

Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo tunatoa magari kwa ajili ya wahandisi wa TARURA wa halmashauri, lakini vilevile tutapeleka ambulance katika halmashauri zote nchini ambazo zina hospitali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jukumu hili la kusadia Halmashauri nchini ikiwemo ya Mbarali lipo katika utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusu kumalizia ukarabati wa barabara za TARURA, tumelichukua hilo katika bajeti yetu na kwamba tutahakikisha kwamba zinajengwa kulingana na mahitaji. Ahsante sana.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mabwawa sita Wilayani Mbarali ili kuboresha kilimo cha mpunga?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika miradi yetu yote sita iliyoko Mbarali tumemaliza taratibu zote na miradi mingine wakandarasi tayari wako site. Miradi kama ya Utuo, Isenyera, Gonakuvagogoro, Helmanichosi yote yana mkandarasi na kazi inaendelea. Nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imedhamiria kujenga miradi hiyo na kazi inaendelea.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali; lakini hata hivyo nina swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa barabara ni moja ya barabara ambazo wananchi wa Mbarali wanazitumia sana kusafirishia mazao na sasa barabara nyingi zimeharibiwa mno na mvua hali inayopelekea ugumu wa kufanya shughuli hizi.

Je, ni ipi kauli ya Serikali kwa wanambarali kuhusu adha hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyozungumza Mheshimiwa Mbunge, barabara nyingi ambazo zimeharibika kutokana na msimu huu wa mvua zimewekewa kipaumbele cha matengenezo katika mwaka huu wa fedha tunaoenda kuuanza Julai, Mosi mwaka huu.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na uchambuzi mzuri uliofanyika na Serikali, wananchi wa Igurusi wanapata shida hasa wazazi wanapokuwa na uzazi pingamizi: Je, ni lini sasa maboresho yataanza kufanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Je, kuna mpango gani wa kupeleka vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Chimala ili waweze kusaidiwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali lake la kwanza la lini maboresho yatafanyika, kama nilivyoshasema kwenye majibu yangu ya msingi, ni kwamba tumefanya tathmini na kugundua kuna vituo vikongwe hapa nchini 193, na hivi sasa tuko katika mchakato wa kutafuta fedha na kuhakikisha tunavikarabati na kuviongezea majengo vituo hivi vya afya ambavyo ni vikongwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili tutapeleka fedha kadiri ya upatikanaji wa fedha hizo na tutaangalia katika mwaka wa fedha huu ambao bajeti imepitishwa, kama kuna vituo ambavyo viko allocated Mkoa

wa Mbeya, basi tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona ni namna gani Mbarali nao wanaweza kupata. (Makofi)
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa baadhi ya halmashauri malipo au stahiki za Madiwani zinapishana sana mathalani malipo ya simu kwa wenyeviti wa halmashauri na kadhalika, je, nini kauli ya Serikali katika hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, aina za posho za Madiwani zimeainishwa ambazo ziko wazi. Posho ya kwanza, ni posho ile ya mwezi ambayo nimetoka kuitolea majibu katika swali la msingi. Posho ya pili, ni posho ya madaraka ambayo posho hii pia inatolewa kwa mujibu wa waraka wa viwango vya posho vya Serikali. Posho ya tatu ni posho ya kuhudhuria vikao na posho ya kujikimu na safari mbalimbali za ndani ya halmashauri husika na nje ya halmashauri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hizi posho za ndani zinategemeana na uwezo wa halmashauri husika. Kwa hiyo, hili tutaendelea kuwaasa wakurugenzi wa halmashauri mbalimbali nchini kuangalia walau wanatenga posho ya mawasiliano na kadhalika kulingana na uwezo wa mapato yao wenyewe ya ndani.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, baadhi ya maeneo yale wamesharudishiwa wananchi kwa matumizi yao. Sasa ni lini Serikali itayaratibu na kuyapanga upya maeneo yale kwa maana ya vijiji, vitongoji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ikitokea wananchi wamechoka jina la mtaa, je, wanaweza wakabadilisha jina? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali la kwanza; eneo ambalo limerudishwa katika vijiji tutashirikiana kwa sababu yanagusa Wizara mbalimbali, tutashirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, tutashirikiana na Wizara ya Ardhi, lakini vilevile tutashirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ili kuona jinsi ya kulifanyia kazi na pale ambapo tutajiridhisha kwamba limesharejeshwa kweli, basi anuani za makazi zitawekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa pili, swali la pili, pale ambapo wananchi au Serikali inataka kubadilisha jina la mtaa au jina la barabara; kuna utaratibu ambao unapitiwa. Lazima vikao vifanyike kwa ngazi ya chini na wananchi washirikishwe na pale ambapo Serikali itajiridhisha kwamba ndani ya kata moja kuna jina la mtaa linalofanana na mtaa mwingine basi Serikali itawashirikisha wananchi ili kubadilisha, lakini hata pale ambapo wananchi wanalalamika katika maeneo hayo yote hayo yatafanywa kulingana na utaratibu uliowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kesi iko pale Goba, kwenye utaratibu ambao walishirikishwa mwanzoni waliamua kwamba jina lao liitwe Maghorofani, lakini baada ya kuwa wanatumia ile anuani wakajikuta kwamba jina lile linaitwa Janguo. Sasa tumeshatuma timu yetu kwenda kuhakikisha kwamba ni nani mefanya ujanja huo wa kubadilisha jina la mtaa bila wananchi wenyewe kujua kwamba utaratibu upi umetumika katika kubadilisha hilo jina.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuwa Kituo cha Polisi Chimala ni duni na makazi ya askari wale ni duni je, lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo hicho pamoja na makazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua jinsi ambavyo Chimala kunaendelea kwa kasi kule Mbarali na niwapongeze wananchi wa Chimala pamoja na uongozi wao akiwemo Mbunge na DC kuanza Ujenzi wa Kituo cha Polisi Chimala na hatua itayofuata ni kuingia ujenzi wa nyumba za makazi ya askari. Serikali itawaunga mkono pamoja na wadau kama ambavyo RPC ameanza kufanya ili kuhakikisha kwamba Chimala wanapata nyumba bora za kuishi, ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, hususan katika kata hizi tatu, lakini nina swali dogo la nyongeza: Je, Serikali iko tayari kupeleka mawasilino katika maeneo mengine yenye shida kama vile Ihahi, Azimio Mswiswi, Mapula, Ilaji, Igalako, Uhambule, Chamoto, Mbaliro na Matebete? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kata ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja zina mitandao isipokuwa jambo ambalo lipo kwa sasa ni kwamba, unakuta kata moja ina mtandao wa Halotel lakini wananchi wanahitaji Airtel, na kata nyingine wana Airtel lakini wananchi wanahitaji Vodacom.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote Na. 11 ya Mwaka 2006 lengo lake lilikuwa kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma ya mawasiliano, hata angalau kwa mnara mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Sheria yetu ya EPOCA Na. 3 inampa Mheshimiwa Waziri mamlaka ya kutunga kanuni. Sasa ili tutatue changamoto ya kuwa na minara mingi ndani ya eneo moja na kuwa na utitiri ndani ya eneo moja, tumeamua sasa kuingia kwenye kanuni ambayo inaelekeza watoa huduma; cha kwanza tuwe na infrastructure sharing, maana yake tukiwa na mnara mmoja watoa huduma wote watakwenda kuweka huduma ya mawasiliano pale ili Watanzania wote waweze kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tumeliongeza kuhakikisha kwamba tuna-share ile spectrum (masafa), badala ya kila mtoa huduma kuja na masafa yake, basi tumeruhusu ambapo sheria hapo kabla ilikuwa inazuia, sasa tumeruhusu ili kuhakikisha kwamba Waheshimiwa wote wenye changamoto za mawasiliano tuweze kuwapatia huduma kwa urahisi bila kuleta utitiri wa minara ndani ya nchi yetu, ahsante sana.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Barabara ya Igawa – Kinyanambo – Mafinga huko imefanyiwa upembuzi yakinifu kwa muda mrefu na iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi pia: Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Igawa – Kinyanambo ipo kwenye ilani na kwa kweli, inatakiwa ijengwe kwa kiwango cha lami hasa tukizingatia umuhimu wa barabara hii inayopita maeneo yanayozalisha sana hasa mpunga. Serikali inaendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mpango uliopo ni kuhakikisha kwamba inafanyiwa ukarabati iweze kupitika kwa kipindi chote cha mwaka. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imeendelea kujitahidi sana kuhakikisha barabara hii inafanyiwa matengenezo mara kwa mara na kupitika kwa muda wote wa mwaka, ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Rujewa – Madibila – Kinanyambo - Mafinga ni muhimu sana kwa wananchi wa Mbarali na upembuzi yakinifu ulishafanyika; je, ni lini sasa Serikali itaanza rasmi ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Francis, Mbunge wa Mbarali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii ni barabara moja muhimu sana na ya kiuchumi na ni fupi kutoka Igawa – Rujewa kuja Mafinga. Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami kwa ajili ya kuboresha usafiri kati ya Mbarali na Mafinga. Ahsante.