Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Francis Leonard Mtega (8 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. FRANCIS I. MTEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana ya uhai wa wananchi, suala la maji.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ukomo wa bajeti nafahamu kwamba ipo miradi katika jimbo langu ambayo imeachwa kutokana na ukomo, ambayo ni miradi muhimu sana inayohudumia wananchi wengi, takribani wananchi 10,000,000. Mheshimiwa Waziri mfano wa miradi hiyo, mfano Mradi wa Mirade karibu milioni 500, Mradi wa Mbigigi milioni karibu 520, Mradi wa Ndala karibu milioni 350. Miradi hii yote imeachwa kutokana na ukomo wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba upo mpango wa Wizara hii kuongezwa fedha hasa kutokana na agizo la Mheshimiwa Rais kwamba Wizara hii anaingalia kwa makini sana na akamwambia Waziri akizingua na yeye atamzingua. Sasa pale pesa zitakapoongezwa, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri miradi hii irudi kwenye bajeti. Kwa sababu ni miradi muhimu, wengine naona wanaongelea miradi ya miji yao kupata maji, lakini sisi wa vijijini na Wilaya yangu ya Mkalama ni wilaya mpya, haina vitendea kazi na shida ya maji ni kubwa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri atakapoongezwa pesa, miradi hii irudi ili wananchi hawa wa Mirade, Ndala na Mbigigi katika Wilaya ya Mkalama nao waweze ku-enjoy maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, pia Meneja wangu wa RUWASA pale Mkalama anafanya kazi nzuri sana Engineer Mark, ni msikivu, anafuatilia lakini tatizo kubwa hatuna vitendea kazi. Wilaya yetu iligawanywa kutoka Iramba na vitendea kazi vingi vilibaki kwenye Wilaya Mama. Hatuna gari, nimwombe Waziri katika bajeti zake atupatie Mkalama gari ili Engineer huyu na watu wake na Ofisi yake waweze kufanya kazi nzuri zaidi ya wanayoifanya sasa ya kuhudumia Wilaya yetu ya Mkalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuongelea jimbo langu sasa nishauri pia Wizara hii kitaifa. Kwa kushirikiana Wizara ya Maji na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wanaweza kutengeneza sera ambayo itawafanya Watanzania wawe na tabia ya kuvuna maji ya mvua. Unajua kila Mtanzania mwenye nyumba ya bati tayari ana chanzo cha maji, kinachobaki ni storage tu. Kwa hivyo kama tutatengeneza sera vizuri ya kuwashawishi Watanzania, wakaweka umuhimu kwenye ramani zao za nyumba wanapojenga kuwe kuna tank angalau la lita 50,000 za maji.

Mheshimiwa Spika, ukiwa na lita 50,000 za maji una mapipa zaidi kama 250 hivi. Kwa mwananchi wa Tanzania akiwa anatumia pipa moja lenye ndoo 12 anaweza akatumia miezi nane ya kiangazi. Kwa hivyo kama Watanzania wenye nyumba za bati wakatambua kwamba tayari wana chanzo cha maji na hivyo wakatengeneza storage tank, tutatumia, tutapata maji ya mvua ya kutosha na tatizo hili tutalipunguza kama siyo kulimaliza katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo ikiwepo sera maana yake kutakuwa na miongozo, kutakuwa kuna uhamasishaji na mambo mengine na hii tabia itaingia taratibu kwa Watanzania kujua kwamba tayari wana chanzo cha maji na hivyo kinachobaki ni kutengeneza storage tank angalau ya lita 50,000 na kuendelea. Mimi hapa nina ma-tank zaidi ya matatu yenye lita laki 200, na-enjoy, kwa hiyo naamini hiki kitu kikienda kwa Watanzania wengi shida hii itapungua kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, niiombe pia Wizara, badala ya kusubiri kila wakati maji yazame kwanza ardhini halafu ndiyo tuyafuate, unajua maji haya ya visima ni maji ambayo ni ya mvua, yakishazama yanaenda kwenye miamba yanatuama ndiyo tunafanya kazi ya kuyafuata chini. Hebu tujielekeze zaidi kwenye mabwawa kwa sababu mabwawa maji yanakuwa bado yapo juu na tukiyatega mabwawa ya maji yanakuwa na faida zaidi ya kunywa maji peke yake, kwa sababu bwawa la maji utapata maji ya kunywa, tutapanda samaki, tutavua samaki lakini na sehemu nyingine pia itamwagilia hata mazao. Kwa hiyo bwawa hili linakuwa lina kazi zaidi ya moja kuliko kusubiri yaende chini ndiyo tuyafuate kwa gharama kubwa kuyaleta juu.

Mheshimiwa Spika, ipo mipango mikubwa ya mabwawa, mimi nilikuwa Mkuu wa Wilaya ya Chemba, kuna mradi wa Farukwa pale umeoongelewa, ni mradi mkubwa ambao lengo lake lilikuwa ni kulisha Dodoma, sijaona kama umepewa kipaumbele kikubwa. Bwawa lile likijengwa linakuwa hadi na kisiwa ndani, sasa hatuoni kwamba mipango hii ya mabwawa ikifanywa vizuri italeta faida mara mbili, mara tatu zaidi ya kupata maji ya kunywa. Kwa hiyo niombe wizara ijielekeze zaidi kwenye mabwawa kwa sababu fedha nyingi na miradi hii itakuwa multipurpose itafanya kazi kubwa zaidi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia …

SPIKA: Ahsante sana muda wako umeisha.

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Aweso; na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Maryprisca Mapunda. Pia niwapongeze sana Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na wataalam wote wa Wizara ya Maji kwani wamefanya kazi kubwa sana na tunajua nchi yetu hii ni kubwa sana lakini kwa jitihada zao kwa kweli wamejitahidi mpaka hapo walipofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo naomba nijikite kuchangia mambo mawili tu. Moja ni kuwajibika na la pili ni kuwajibishana, kwani naamini hizi ndizo nguzo kuu kabisa kujenga nidhamu kwa wafanyakazi ili waweze kutimiza lengo la kuwapa maji wananchi wote kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba nitoe changamoto kadhaa zinazowapata wananchi wetu kule vijijini. Yawezekana kwa kuwa hii ni Wizara kubwa na inajumuisha Wizara nyingine, zile changamoto ambazo zitahusu moja kwa moja Wizara hii Mheshimiwa Waziri atazijibu anapojumuisha, lakini zile ambazo zitahusu labda Wizara zingine na wenyewe watapata nafasi kujibu watakapokuwa wanatoa hotuba zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa mambo ya washirika na mamlaka zilizo chini ya Wizara. Nimeona katika hotuba ukurasa wa 80, Waziri ameelezea namna anavyoshirikiana nao na ametoa miongozo. Hata hivyo, kanuni hizo zinafanya baadhi ya mamlaka hizo pengine kwa kutofahamu au kwa makusudi kabisa kufanya changamoto kubwa sana kwa watumiaji wa maji kule vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na maji safi na mazingira. Wananchi wanapata mfadhili awasaidie kujenga tenki kubwa la maji, naenda RUWASA, RUWASA wana masharti yao. Wanasema kwanza maji yale yapimwe na Mkemia Mkuu, lakini pia bonde waje waidhinishe, wapime kina cha maji. Sasa ukienda bonde wao watasema tunasubiri kwanza mvua zinyeshe tuone maji huwa yanajaa kiasi gani. Ukienda wakati wa mvua wanasema tusubiri kiangazi tuone maji huwa yanapungua kiasi gani. Hivyo wananchi wanakosa huduma ya maji. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, maji yale wananchi huwa wanayatumia muda wote. Sasa mfadhili anataka kuongeza wingi wa maji hivyo kumbe wangeweza kutoa kibali, tenki likajengwa huku wanasubiri vipimo hivyo viendelee kwa vile maji yale yanatumika moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika umwagiliaji. Wakulima wale huwa wanahangaika sana. Wanaenda Mamlaka ya Bonde, Bonde wanasema sisi tumesitisha vibali, hatutoi vibali kabisa, lakini unakuja kwa Sekta ya Umwagiliaji, wao wanasema sisi tunaruhusu mfereji upite hapa lakini kule kibali hawatoi. Sasa wananchi hawa wanaendelea kupata changamoto kubwa sana. Wananchi hawa muda wote wanapita mamlaka zingine za mifereji wanawatoza ada ya maji. Ukienda Mamlaka ya Bonde wanasema sisi hatujapata ada yoyote na hawa hawana control number, leo watapita na counter book jipya, kesho watapita na ki-note book, anakusanya fedha na hazieleweki zinaenda wapi. Huku analipa elfu 50,000 kwa heka moja, fedha haziingii Serikalini, lakini, mkulima huyu anauza gunia moja shilingi 45,000, kwa hiyo ni changamoto kubwa sana kwa watumiaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye kuwajibishana. Kuwajibishana kwa upande wa Wizara. Utendaji kazi kwa upande wa Wizara mambo ni mazuri sana, mambo yanaenda vizuri kama nilivyopongeza lakini kule kwa watendaji wa chini kwenye vijiji namwomba Mheshimiwa Waziri akae na wadau mbalimbali aongee nao. Hii itampa picha namna gani mambo yanaenda kule kwa sababu nimeona katika ukurasa wa 80 wa kitabu ametaja anavyoweza kushirikiana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema kwamba ushirikiano wa Waziri na Wizara ya TAMISEMI, ningeomba hizi Mamlaka zote ziwajibike kwa Waheshimiwa Madiwani. Waheshimiwa Madiwani kwenye Baraza lao ndiyo pekee wanaoweza kuhoji na wanaweza angalau wakafuatilia miradi ile kwa ukaribu Zaidi. Tumeona akienda Waziri mwenyewe na Mheshimiwa Naibu Waziri wanakuwa wakali lakini hawa Madiwani wanaweza kusimamia kwa ukaribu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayofanya, lakini nimpongeze sana Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ningependa nichangie kuhusu migogoro ya ardhi na mipaka, hususan mipaka. Migogoro ya ardhi imekuwa mingi kwa nchi yetu kwa ujumla, lakini Mheshimiwa Lukuvi amekuwa hodari sana na mahiri kwa kuitatua, nampongeza sana. Hata Mbarali tulikuwa na mgogoro baina ya mwekezaji wa Kapunga na wananchi, lakini mwaka ule 2015 alikuja haraka sana na kuumaliza mgogoro ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mgogoro mkubwa sana wa mipaka kati ya TANAPA na vijiji 55 katika Jimbo la Mbarali. Huu mgogoro kwa kweli ni mkubwa sana na una athari nyingi. Namwomba Mheshimiwa Waziri aupe kipaumbele kuutatua mgogoro huu, vinginevyo Wana-Mbarali hawatakuwa na amani na utulivu kabisa. Mpaka huu wa GN Namba 28 bahati mbaya sana umepita vijijini, mawe mengine yako katikati ya vijiji. Sasa wananchi wale wanaishi kwa matamko; atakuja kiongozi huyu anasema msiwe na wasiwasi, endeleeni na shughuli zenu kama kawaida, Serikali inafanyia kazi. Anakuja kiongozi mwingine anasema mko ndani ya hifadhi hamruhusiwi kufanya kitu chochote. Sasa hii inawapa shida wananchi wale, hawajui wafanye nini, kwa sababu, shughuli nyingi wanazifanya ndani ya maeneo yao wanayoishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna mashamba mazuri kule Mnazi na mashamba yale yanatoa mpunga kwa wingi na tuna viwanda vikubwa pale Ubaruku vinachakata mpunga tena wa hali ya juu. Sasa kuwaambia wasifanye shughuli yoyote, maana yake ni kuwarudisha nyuma kiuchumi na kukosesha pato la Taifa. Kwenye Ilani imeainishwa kabisa kwamba tunaenda kuboresha kilimo na kuhakikisha wananchi hawa wanakuwa na kipato cha kutosha na vilevile Taifa linakuwa na akiba ya chakula. Sasa wanapozuiwa wasifanye shughuli zao za kila siku, kwa kweli hatuwatendei haki wananchi wale wa Mbarali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna shughuli mbalimbali, kwa mfano kule Luhanga kuna ujenzi wa Shule ya Msingi na ujenzi wa Zahanati. Sasa kiongozi huyu anakuja anasema endeleeni na ujenzi msiwe na wasiwasi, kesho kiongozi mwingine anakuja kuzuia kwamba msifanye jambo lolote la kuendeleza kwa sababu mpo ndani ya hifadhi, subirini Serikali itoe maamuzi yake kwamba wapi kutakuwa ni mpaka ndipo mtakapoendeleza ujenzi. Sasa hii inawavunja moyo wananchi wale, wamepoteza nguvu zao na sasa hawaendelei na ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba Mheshimiwa Waziri, maamuzi ya Serikali yaharakishwe ili kubainisha mpaka sahihi ni upi? Yawezekana kuna vijiji vitaambiwa viondoke, yawezekana kuna vitongoji vitarekebishwa, sasa hii ingefanyika haraka ili wananchi wawe huru kufanya kazi zao za kila siku wajipatie kipato na vilevile waweze kuliongezea pato Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije upande wa GPS. Zamani mipaka ilikuwa inawekwa mawe tu, kiasi kwamba wazee wanakuwepo ni mashuhuda kwamba mpaka ulikuwa hapa na viongozi wa eneo lile wanashuhudia, lakini sasa ni GPS. GPS hii ni wataalamu peke yao wanaoweza kutafsiri. Sasa naomba Waziri atakapojumuisha, atuambie ni nani ata-cross check kuona kwamba hawa wataalam wetu wanaotafsiri coordinates zile kuweka mawe, je, hawawezi wakawa wanaingia ndani zaidi au pengine kutoka nje zaidi? Kwa sababu, wananchi pale hawana utaalamu wowote, wao wakishaona jiwe limewekwa ni kulalamika tu kwamba, sisi mpaka tunajua ulikuwa kule, sisi mpaka haukuwa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo tuna migogoro mingi sana kuhusu GPS katika tafsiri yake na mawe yanavyowekwa, wananchi hawawi na uhakika, wanakuwa na wasiwasi mkubwa sana. Kwa kweli, Mbarali tuna uhaba mkubwa sana wa ardhi, Mbarali tuna mifugo mingi, Mbarali tuna mashamba ya mpunga, Mbarali tuna hifadhi ya TANAPA; ile hifadhi ni kubwa mno kiasi kwamba eneo linalotumika kwa wanyama liko upande wake, lakini eneo la wananchi ambapo linaonekana ni oevu, kwa kweli ni kubwa mno na kwa sasa hivi ule u-oevu haupo. Nimezunguka sehemu nyingi ni vumbi tupu na mashamba, lakini Ihefu kwa kweli bado ni sehemu oevu na inahifadhiwa na wananchi hawaruhusiwi kwenda kule. Sehemu nyingine zote ni kavu, zina mashamba, hakuna uoevu, hakuna maji; maji yanapita tu mtoni, yanatoka Makete, pale ni mapito ya maji, wala hakuna madhara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa kweli aende mwenyewe kule ashuhudie, aone haya mawe yaliyopandwa vijijini yanavyoathiri wananchi na kwamba, sehemu zile kwa kweli hazihusiani kabisa na uoevu unaoongelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika bajeti hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu anayetujalia uhai na anayezidi kulinda Taifa letu na ustawi wa wananchi wake. Pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazofanya, nimshukuru sana Makamu wa Rais, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Baraza lote la Mawaziri kwa kazi nzuri wanazofanya. Hii imetuletea bajeti nzuri, bajeti ambayo imegusa kila eneo, kila kundi kwa kweli ni bajeti ambayo inaenda kuinua hali za Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mchango wangu ujikite katika kilimo; kwa vile asilimia 65 ya Watanzania wanajihusisha na kilimo, lakini pia vijana wetu ambao hawana ajira wanaweza wakajiunga na kilimo. Vile vile Bunge lako Tukufu hili Bunge la Kumi na Mbili limebainisha kwamba linaenda kujikita zaidi katika kufanya mageuzi makubwa katika sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona katika bajeti ukurasa wa tano, ukurasa wa 16 na wa 17 namna ambavyo Serikali inaenda kuboresha kilimo, namna Serikali inavyoenda kuleta tija na kutafuta masoko ya ndani na nje ya nchi. Hata hivyo, nilitarajia kuona kwamba Serikali inaweka fedha nyingi kama mtaji kuinua hii sekta; kwanza kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya umwagiliaji, lakini pili, kwa kutafuta masoko na kuboresha ya ndani na nje na kikanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kabla ya kuanza mtaji huu naona kuna tozo mbalimbali zimewekwa pale. Kwa mfano katika ukurasa wa 33 kuna tozo ya zuio, sasa pale imefafanuliwa vizuri kwamba tozo hii inaenda kutozwa kwa NFRA kama Wakala wa Ununuzi, lakini bahati mbaya kinachotokea kule ni tofauti kabisa, ni wakulima ndio wanaotozwa tozo hii. Wakulima wale hawajafafanuliwa vizuri, tozo hii inatozwa wakati gani kwa sababu kuna ushuru wa halmashauri na wakulima wanatozwa njiani wanavyotoka shambani wakati wanarudisha mazao nyumbani, wanatozwa barabarani, lakini pia wakulima wanatozwa wanapopeleka gulioni wanatozwa mara ya pili na tatu wengine wanatozwa pale wanapouza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Waziri aje na ufafanuzi, kwamba muda sahihi wa kumtoza mkulima hasa mdogo ni wakati gani? Anaposafirisha au anapouza? Ni wakati gani atozwe na kwa kiasi gani? Tumeona nyuma huko, ilikuwa kawaida ni kwamba anayebeba chini ya tani moja hatozwi chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ukurasa wa 33 imebainishwa kabisa, hii haitahusu wakulima wadogo wadogo magulioni, itahusu tu wakala wa ununuzi, lakini kinachotokea kule ni tofauti kabisa; wale wazabuni wanaotakiwa watoze njiani, hata wakiona gunia chini ya tani moja, wanatoza. Wanatoa visingizio mbalimbali; watasema umeweka mfuko haufai siyo wenyewe, watasema sijui sasa hivi tunatoza tu kwa vile umechelewa kurudi toka shambani, ili mradi wao wapate kodi kubwa. Wanapiga hesabu ya kutosha kupeleka Halmashauri na nyingine ibaki kwa ajili yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tungependa ufafanuzi, tujue hali halisi, inatakiwa itozwe kwa nani? Kama ni mkulima, basi ni wakati gani? Je, ni pale anapofanya biashara au wakati gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, changamoto nyingine kwa wakulima hawa ni mbolea. Mbolea ina ruzuku lakini kwa kweli ruzuku ile inafika mahali haiwezekani, bado ni bei kubwa sana. Nitoe mfano, mwaka jana 2020, Jimbo la Mbalali mbolea aina ya CAN imeadimika kabisa. Huwa bei ya kawaida uwa ni shilingi 45,000/=, imepanda mpaka shilingi 55,000 kwa mfuko mmoja wa kilo 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine kwa wakulima ni skimu zile. Kwa kweli skimu zilizo nyingi zina hali mbaya sana. Kwa hiyo, wakulima wanakosa pato kwa sababu skimu zile hazijakarabatiwa kwa muda mrefu. Kule Mbarali kuna skimu moja inaitwa Mwendamtitu, imekuwa ikijaa mchanga mara kwa mara. Halmashauri kupitia mapato ya ndani imejaribu kuzibua, imeshindikana na wale wameomba mkopo kutoka TAB Bank mpaka sasa hivi hawajapata mkopo wowote na baadhi yao hawajavuna kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ni mtaji. Wakulima wadogo wale hawana mtaji wa kutosha. Mtaji kwa maana ya kwamba wanaenda benki wanaahidiwa kukopeshwa, lakini ukifika msimu kwamba wanaenda shambani, benki hawatoi mikopo kwa wakati na pengine hawatoi kabisa. Wamekuwa wakinilalamikia. Mwenyewe nimeenda benki kuulizia, mbona hamuwapi wakulima hawa mikopo na msimu unapita? Wananijibu kwamba mtandao haupatikani, waombaji ni wengi, tunaendelea kuchambua, tutawapa tutakapoona majina yao, lakini muda unazidi kwenda, wengi wamekosa mikopo, wachache wamebahatika kukopa na wengine wameenda kukopa kwa watu binafsi, kitu ambacho ni gharama kubwa, kwani riba ni kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wamehangaika, wamepata mikopo, wamepata shida zote hizo, lakini masoko hakuna. Wamevuna mipunga, imejaa ndani na soko hakuna. Kwa mwaka uliopita Mbarali tumevuna tani 275,000 uzalishaji, lakini mahitaji yetu ni tani 125,000 tu. Kwa hiyo, tuna ziada ya tani 150,000; na hizo tani zimekutana na mavuno ya mwaka huu. Kwa hiyo, wamekopa, hawajauza, wamelipa ushuru, tozo mbalimbali, mpunga umekwama ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka haraka nije kwenye suala la masoko ya ndani. Naiomba Serikali iwape NFRA fedha nyingi wanunue mazao yote ya wakulima. Njia nyingine katika kuimarisha masoko ya ndani ni kuanzisha mradi wa Liganga uanze kufanya kazi, watauza mazao yao kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo kubwa sana la Tume ya Umwagiliaji, inafanya kazi kule bila mawasiliano na Halmashauri. Wanaenda site, wanaongea na wakulima moja kwa moja; sehemu nyingine wanafukuzwa na sehemu nyingine kuna miradi ya ajabu kabisa ambayo Halmashauri haijui na mingine iko chini ya kiwango. Kwa mfano, tuna bwawa moja Rwanyo pale Igurusi la miaka mingi halifai na ni hatari kwa wananchi pale. Tuliomba Chuo Kikuu Mzumbe waje kutathmini namna ya kurekebisha, wakasema gharama ya marekebisho itazidi gharama hata ya ujenzi. Sasa fedha ya Serikali ndiyo imeisha hiyo, ni hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba, ili tuwe na usimamizi mzuri kwa Wilaya ya Mbarali, kwa kweli jimbo lile ni kubwa mno, tunaomba ligawike yawe majimbo mawili au Halmashauri mbili, kwa sababu inapitia mikoa mitatu; imeanzia Mbeya, Njombe, hadi Iringa; na ukiwa katikati pale kwenda upande wa mashariki ni kilomita 97, kwenda magharibi ni 134, jumla ni urefu wa kilomita 231. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mtaalam kwenda kufanya supervision, akienda anarudi usiku kabisa na inabidi anywe Panadol ndiyo alale usingizi na akirudia analazwa. Sasa kwa kweli tuna hali ngumu sana. Kuna miradi mikubwa na mizuri ya ujenzi wa madarasa; mnaenda kule mnaambiwa cement tulimwazima Mwenyekiti wa Kijiji, tuliona itaganda. Mbao, kiongozi fulani tuliona azitumie, fedha hatuna. Kwa kuwa ni mbali mno, tunaomba sana igawanywe iwe Halmashauri mbili na ikiwezekana na Mji wa Lujewa iwe mamlaka kamili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS L. MTEGA Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote ninaipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, pamoja na viongozi wote waandamizi ngazi ya taifa kwa kuendelea kutoa fedha nyingi katika miradi mbalimbali ya afya kwa Watanzania.
(Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Katibu wa Wizara pamoja na Watendaji wote kwa usimamizi wao mahiri na Wizara inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo nitajikita zaidi kuelezea uhaba wa rasilimaliwatu namna unavyoathiri uadilifu na ufanisi katika kazi. Kabla sijaingia kwenye mchango wangu niongelee kidogo kuhusu ajira. Nashukuru na kuipongeza Serikali kwa ajira hizi 10,285 lakini kwenye Kamati yetu tulishauri kwamba ajira hizi zizingatie usawa, haki na kijiografia pia kwa kuona kwamba mchakato mzima wa ajira zenyewe kwa kuwa ni mfumo basi angalau kila sehemu, kanda, iwe na waliochaguliwa. Sisi kama wawakilishi kwa kweli tumekuwa tukipigiwa simu nyingi na waliomba nasi kama sauti zao naomba kusisitiza hili kwamba, kwa kuwa wanaomba kwa mfumo labda Waziri aangalie namna ya kuunda Posts Selection Committee ambayo atachagua wataalam baadhi kutoka Wizarani na wengine kutoka hospitali mbalimbali ili kuhakiki kuona kwamba malengo yaliyowekwa yamefikiwa.

Mheshimiwa Spika, nina wasiwasi mifumo wakati mwingine inaweza kuwa tampered, badala ya kuchagua kama ilivyoainishwa kwenye mpango, idadi na aina za wale wanaochaguliwa ikawa tempered badala yake wakachaguliwa wa sehemu moja au ukanda moja na pengine wengi kupitia kanda moja kuliko nyingine kama ilivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili niendelee na mchango wangu kuhusu uhaba wa Rasilimaliwatu. Kwenye Kamati tumeshauri kwamba hawa watumishi wasimamiwe vizuri katika kuziba mapengo yaliyopo katika Idara mbalimbali. Lakini kukiwa na uhaba wa Rasilimaliwatu mara nyingi sana kama tulivyoona michango ya Waheshimiwa waliotangulia kwamba wengi wao kufuatana na maadili yao na viapo vyao siyo walalamishi wanavumilia, anazidiwa kufanyakazi lakini anajituma anaendelea kujitahidi kwa kadri ya uwezo alionao. Tofauti na sekta zingine kama walimu utaona athari zake moja kwa moja, amezidiwa wanafunzi wengi wanapiga kelele, hata akichoka anaweza akawapa assignment akaenda kunywa chai, akaenda kupumzika kidogo, lakini huyu wa Idara ya Afya hana nafasi hiyo, atajitahidi mpaka pale atakapotimiza kumaliza wagonjwa wote walio mbele yake.

Mheshimiwa Spika, kazi nyingi hazihitaji presha, hata kama ni kazi ndogo kiasi gani iwe ya kutafuta mshipa wa damu, kama ana presha ana haraka hiyo kazi badala ya kutumia dakika mbili atatumia nusu saa. Halikadhalika upasuaji mdogo na kadhalika, hivyo tunahitaji rasilimali watu ya kutosha ili wafanye kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, athari nyingine ni wale wagonjwa wanaosubiri watahisi kwamba huyu mtu labda hahudumiwi ili apewe rushwa, kumbe yule mtumishi amezidiwa. Sasa wanashawishika kutoa rushwa wakidhani kwamba wanacheleweshwa maksudi lakini kumbe ni uhaba wa rasilimaliwatu.

Mheshimiwa Spika, pia wapo wanaotumia nafasi hiyo kuchukua rushwa, kwamba atajifanya amezidiwa na kazi mpaka ndugu wa mgonjwa aende amuone atoe chochote ndipo amhudumie. Imetokea hospitali fulani ipo barabara sintaitaja hapa, na ni Hospitali ya Mkoa ya Rufaa. Kijana alipelekwa usiku pale anavuja damu, amevunjika mfupa unaonekana, hahudumiwi, ndugu wanaambiwa nendeni barabarani mkatafute Panadol na baadaye wale vijana wanashangaa wanaulizwa je, mna fedha zozote mtupatie? Kama hamtoi mgonjwa wenu atafariki, wanaambiwa waziwazi. Wale ndugu baada ya kushauriana ilibidi wamtoe mgonjwa usiku ule wakaondoka naye kwenda hospitali nyingine ambako walihudumiwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda unakwenda mbio, niongelee athari katika upimaji physical examination. Pale kuna takiwa wafanyakazi wa kutosha wa jinsi tofauti tofauti kwa sababu kuna hatari kama anayepima ni jinsi nyingine na ni peke yake, akamdhalilisha yule mgonjwa akamfanyia visivyo lakini kumbe wakiwa wengi basi atafanya kwa uhakika na bila matatizo yoyote wala wasiwasi kwa mgonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee Hospitali zetu za Rufaa. Sina shaka ngazi ya Taifa zinafanya vizuri, wabobezi wapo wengi, wanafanya kwa umakini, lakini hizi za Mikoa nina wasiwasi nazo huduma kwa kweli labda zichunguzwe ziitwe Rufaa zile zinazotoa huduma nzuri kabisa. Pamoja na ubobezi walionao lakini kama mtu anavuja damu anaambiwa akanunue Panadol halafu inaitwa Hospitali ya Rufaa kwa kweli hii inatia shaka sana. Wale wa Hospitali za Rufaa tulizotembelea kule Muhimbili, Taasisi ya Mifupa MOI na Taasisi ya Magonjwa ya Moyo, kwa kweli waliomba kwamba tunaomba tufikiriwe, tunaomba mtupigie kelele tuongezewe angalau tupate fedha zaidi kwa sababu tunajituma na kazi ni kubwa. Nami leo hapa natumia nafasi hii kuomba Wizara i- top up kwa kuwa Mkurugenzi kule alituambia kwamba yeye anatoa motisha kulingana na mapato ya ndani. Lakini Serikali, Wizara naomba i-top up kwa kweli kuwapongeza wale wanafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia zipo kazi ambazo zinatumia umakini zaidi. Kwa mfano, tulifika MSD tukakuta kijana amekaa pale muda wote ana-check kidonge kwa kidonge kwenye mizani, kina uzito gani, kina ugumu gani, kiko bora kiasi gani? Lakini tulivyotoka pale wanalalamika kwamba sisi hapa hatuna mgahawa. Sasa motisha ya aina hii kukosekana kwa watu wanaofanya very tedious work kwa kweli inakatisha tamaa na hawa wakati mwingine ndiyo wakuibua maovu yanayofanyika pale. Sasa wasipoangaliwa vizuri, wanahudumiwa vizuri hawatatoa taarifa yoyote na ni rahidi kurubuniwa wakapewa kitu kidogo mambo yakaenda hovyo. Mara nyingi wale wanaotoa siri, waadilifu wanapigwa vita.

Mheshimiwa Spika, tumefika Butimba tukakuta Muuguzi mmoja anasota pale Butimba kwa kosa dogo tu la kukosea kuingiza data kwenye mfumo, hasara ya Shilingi 8,000 imemuweka muuguzi yule Butimba, kwa kweli, inasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja.(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia. Niungane na wenzangu kwa kumpongeza sana Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Bashe kwa kazi nzuri anayofanya lakini hasa hasa msimamo wake thabiti kabisa kuhusu bei ya mazao ya wakulima ili wasipunjwe wauze kwa tija. Mheshimiwa Waziri ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Naibu Waziri, Mheshimiwa Anthony Mavunde, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Serikali kwa ujumla kwa kazi wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye item namba 33 ukurasa wa 14 kwenye Hotuba ya Waziri, Kuhusu Kilimo cha Umwagiliaji kama walivyosema wenzangu kwa sasa hivi ndiyo jawabu la kudumu kwa mapinduzi ya kilimo Tanzania kama ambavyo tuliazimia Bunge hili la kumi na mbili kwamba tuhakikishe kuna kuwa na mageuzi makubwa kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Tume ya Umwagiliaji ya Taifa kwa mipango mizuri, ambayo kwakweli inaainishwa vizuri sana kwenye randama yao, tatizo pale ninaloliona ni bajeti. Kwa mfano walitengewa bajeti ya shilingi bilioni 257.5 kwa mwaka uliyopita, lakini mpaka mwezi Februari ni shilingi bilioni 46 tu ndiyo zimeweza kutolewa sawa na asilimia 18. Sasa hii ni fedha kidogo sana kwa mipango mikubwa waliyonayo ya umwagiliaji katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekit, tuchukulie Mbarali tuna mabonde makubwa mazuri katika Milima ya Ulanji ambayo kama Serikali itatengeneza mabwawa na naamini katika mabwawa 22 ambayo yamefanyiwa utafiti. Naamini mabwawa sita yanatoka Mbarali sasa kama tutakuwa na mabwawa hayo sita nina uhakika kilimo cha umwagiliaji Mbarali kitastawi sana na nishukuru Serikali imeashaanza ukarabati wa miundombinu ya umwagiliaji Mbarali sasa tukijengewa na mabwawa nina hakika kilimo kitakuwa bora sana na tutalisha nchi hii mchele bila wasi wasi wote na tutauza nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mbarali shida kubwa tuliyonayo ni mashamba, mashamba kwakweli ni haba sana. Kwa mujibu wa sensa, wananchi Mbarali sasa hivi tumefikia takribani 446,336 karibu laki nne na nusu kutoka laki tatu lakini mashamba ni yale yale. Sasa mashamba yakipungua maana yake nguvu kazi tutaipoteza, wananchi hao wameongezeka sana, mashamba yanapunguzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali hebu iangalie kwa jicho la uhuruma Mbarali, Mbarali tunahitaji tujengewe mabwawa ili wananchi wale waendelee na kulima yale mashamba, maji yawe yanapitiliza yanaenda Mtera yanaenda Bwawa la Mwalimu Nyerere bila wasi wasi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la mabadiliko ya tabianchi kwakweli ni global si Mbarali tu tunaosababisha kama walivyosema wenzangu na nchi jirani zinachangia na pengine ulimwengu kwa ujumla. Tulitembelea na Kamati TMA pale Mamlaka ya Hali ya Hewa Dar es salaam, naipongeza Serikali imewekeza mitambo mikubwa sana yenye kiwango cha kimataifa na accuracy yake kwakweli ni nzuri sana na watalamu wale wana weredi wa hali ya juu, wana mawasiliano na nchi mbali mbali ulimwenguni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametupa mfano kwamba sasa hivi wanachopata tabu sana ni sura ya mabadiliko ya tabianchi inakuja kivingine tofauti na tulivyo zoea nyuma kuona mvua zinakuwa haba, zinachelewa kunyesha, zinaondoka mapema lakini sasa zinanyesha kwa wingi lakini kwa kipindi kifupi walitupa mfano tarehe 12 mwezi wa kwanza juzi 2021 Mtwara waliweza kupima kiwango cha milimita 369.7 wakati wastani huwa ni milimita 133. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa muktadha huo, utaona kwamba kumbe sasa hivi tuelekeze nguvu kubwa kwenye mabwawa fedha nyingi zipelekwe kwenye Tume ya Umwagiliaji waweze kujengwa mabwawa ili tuwe na maji ya kutosha ndipo sasa tuweze kupanda miti istawi turudishie uhalisia. Lakini tukiendelea kupanda miti huku mvua za wasiwasi miti yenyewe inakauka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijaribu kupanda Mbarali mikorosho, mikorosho ilikauka kutokana na mvua haba na maji hakuna. Kumbe kukiwa na maji ya kutosha na wananchi hawa wataendelea kulima huku tunapanda miti, tunamwagilia na maji haya bila shaka tutapata majibu chanya kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti na nisisitize Serikali, kwamba sisi Mbarali tuko tayari kupokea maelekezo ya Serikali, na huku wanavyojipanga kuweka MKUZA, kutathmini maeneo, nani walipwe fidia kiasi gani, tunaomba Serikali iruhusu wananchi hawa wa Mbarali waendelee kuyatumia mashamba haya wakati Serikali inaendela kujipanga. Kwa maoni yangu nadhani mabwawa ni kipaumbele namba moja, hebu mambo mengine yasimame, tuboreshe haya mabwawa ili tupate tija kwa kilimo cha mbarali na maji kwa ujumla, yanayoenda Bwawa la Nyerere na Mtera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niongelee kidogo ugonjwa wa mnyauko uliotokea Mbarali kuhusu mpunga. Nashukuru wataalamu wa TARI wamefanya utafiti na wanaendela kutoa elimu kwa wakulima. Lakini niombe wataalamu hao wafanye mambo mawili; moja, ni kutathmini mbolea tunayoitumia kwa sasa. Nashukuru mbolea ya ruzuku wananchi wamenunua kwa bei nafuu na wameitumia kwa wingi, lakini sehemu ile waliyoweka mbolea kwa kweli kwanza ndio iliyoathirika zaidi kuliko mashamba ambayo hayakuwekwa mbolea kabisa au yaliwekwa mbolea kidogo. Wafanyie utafiti hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niombe wafanye utafiti wa dawa ambayo inatibu, kama ni dawa ya ukungu au kama ni dawa gani ambayo itatibu ugonjwa huu kwa haraka kwa sababu unaathiri kipato cha wakulima Mbarali. Nirudie kusisitiza kwamba kwa kweli Mbarali tumeongezeka tumekuwa watu wengi sana, tuna shida ya mashamba; hivyo basi niombe Serikali itujengee mabwawa kwa kuanzia yawe sita, kama Bwawa la Mtera, ili tuendelee kulima bila wasiwasi wowote na maji yaende mabwawa ya Mtera na Nyerere. Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kutoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayofanya kwa watanzania wote hasa hasa ile ziara ya Royal Tour kwa kweli imeleta watalii wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka tulifika Arusha, Mkuu wa Mkoa alikiri kwamba changamoto kubwa sasa ni namna ya ku-manage magari yanavyomiminika kule Ngorongoro. Ukizingatia kwamba tulitoka kwenye Covid-19 basi hayo yalikuwa mafanikio ya hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa shukrani za dhati kwa viongozi wakuu, Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Phillip Mpango, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri wanazofanya lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, Nimpongeze Naibu wake Mheshimiwa Mary Masanja. Niwapongeze watendaji wakuu wa Wizara Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, watendaji wote na wafanyakazi wote kwa ujumla kwa kazi nzuri wanazoendelea kufanya kuhifadhi, kulinda uhifadhi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita zaidi kutatua migogoro baina ya TANAPA na wakulima, TANAPA na wafugaji lakini wanyama dhidi ya wananchi. Kabla sijaanza mchango wangu nina salamu za pekee kutoka kwa wana Mbarali kwa Mheshimiwa Rais. Wanamshukuru sana kwa uamuzi wake thabiti wa kumaliza mgogoro wa DN Na. 28. Ni mgogoro uliodumu kwa miaka mingi sana, umesumbua sana wananchi wa Mbarali wamesita kuendeleza kuwekeza kwenye maeno yenye mgogoro hivyo kurudisha nyuma maendeleo yao, lakini Serikali ya Awamu ya Sita wanakwenda kuumaliza kabisa wanasema ahsante sana mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jumla ya vijiji 29 vinaenda kurudishwa kwa wananchi ambalo ni eneo lenye ukubwa wa hekta 74,000 kwa hiyo wananchi wa Mbarali kwa kweli wanashukuru sana kupewa eneo hili. Pia wanashukuru kwa uthamini unaoenda kufanywa kwa vijiji vitano tuna baadhi ya vitongoji ambavyo vitabakia kwenye hifadhi na process nzima inavyoendelea na wanafurahi kwamba watalipwa fidia na kuoneshwa maeneo mengine ambayo watayatumia kwa kilimo na ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo sasa nianze mchango wangu kwa kumsihi Mheshimiwa Waziri kwamba namwamini sana. Kama walivyosema wenzangu ameonesha maajabu makubwa kwenye Wizara ya Michezo tuko juu sana. Pia ameenda Serengeti kule ametatua vizuri mgogoro na mimi namwomba tuongozane Mbarali ili akajionee mwenyewe vizuri tushirikiane kutatua migogoro ya Mbarali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa kwanza unasababishwa na vijana wale walioaminiwa kwenda kufanya doria kwenye mipaka na uhifadhi. Badala ya kufanya kazi waliyotumwa wanaenda kuingia kwenye maeneo ya wananchi na kufanya vitendo visivyokubalika. Wengi wao wanaswaga mifugo na kuiingiza hifadhini, sasa hii inachochewa na taratibu au Sheria iliyowekwa ya kutaifisha mifugo ya wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu Mheshimiwa Waziri hebu angalia utaratibu huu vizuri kama unatija kweli kwa sababu inawezekana wale ambao sio waadilifu wanatumia mwanya huu kupora mifugo makusudi pengine wajinufaishe wao wenyewe badala ya kuingiza fedha Serikalini. Hivyo nakuomba sana tuongozane ukachunguze mwenyewe nikuoneshe wahusika walifanyiwa vitendo vile. Muda ule ambao ulivyokuwa mfupi ikauzwa haraka haraka wanunuzi wenyewe kwa kweli inatia shaka nakuomba tuongozane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa pili, vijana wale huwa wanakuja mitaani na kufanya vitu ambavyo havistahili, kupiga watu kwa tuhuma ndogo ndogo ambazo hazina uhakika. Wakiona mtu amebeba kuni barabarani wanamkamata wanampiga eti umetoa hifadhini kitu ambacho sio kweli lakini pia huwa wanaweza wakafika wakaizuia mifugo sehemu na kuiingiza mashambani wanasimamia ili ile mpunga wa watu kitu ambacho kwa kweli kinatia huzuni sana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri kwa hiyo, nakuamini sana, ni mchapakazi, ni hodari, ni mbunifu twende Mbarali ukatatue hii migogoro naamini itaisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimefurahi sana kuona kwamba kuna azimio linaletwa Bungeni la kuridhia mipaka mipya baina ya Hifadhi ya Ruaha na wananchi wa Mbarali kwa kweli ni jambo la kheri. Tunaamini ikifikia hatua hii migogoro yote itakua imeisha Mbarali sasa tutalala na usingizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha niombe kwamba baada ya kufika Mbarali baada ya kujiridhisha mwenyewe, niko tayari kutoa ushirikiano wa hali ya juu kwako na kwa Serikali yangu yote. Nipo tayari kujitolea kutetea, kulinda maslahi ya Serikali lakini pia maslahi ya wananchi wa Mbarali kama walivyonituma mwakilishi wao. Nikizingatia kiapo cha uaminifu na kiapo cha kulinda na kutetea Katiba ya Jamhuri yetu ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru Mheshimiwa Waziri na timu yako yote nina Imani kubwa sasa na wewe kwamba tutaenda Mbarali. Tutaenda kumaliza migogoro yote ya wana Mbarali.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Niwashukuru sana viongozi wakuu wa kitaifa, nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Naibu Waziri, watendaji wote wa Wizara kwa kuwa na sera nzuri ya upimaji ardhi, urasimishaji na utoaji wa hati za ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nioneshe masikitiko yangu makubwa kuhusu migogoro ya ardhi; na kwa kweli mgogoro sugu wa ardhi uliopo Wilayani Mbarali ni GN namba 28. Ninamshukuru Mheshimiwa Bahati Ndingo ametoka kusema muda si mrefu; vijiji ambavyo vilihamishwa rasmi taratibu zote zilifuatwa na malipo yalifanyika. Isitoshe walilipwa mara mbili walipofanya uthamini mara ya pili, kwa hiyo tunashukuru kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilipeleka miundombinu sehemu ambazo wana Mbarali wanatakiwa sasa waishi kwa amani na bila bughudha yoyote. Cha kushangaza na kusikitisha, wataalam wamekwenda kinyemela kuongeza mipaka bila ushirikishwaji wowote kwa wananchi. Kwa kweli kitendo hiki kimetuumiza sana, na mpaka sasa hivi ni mateso yanaendelea kwa wananchi wa Mbarali, achilia mbali vitendo vya kutisha, kama vile mauaji; mara tuokote nywele, mara kichwa, mara mifupa na viongozi wetu kupigwa sana na kuumizwa sana.

Mheshimiwa lakini pia ziko athari za kimaendeleo. Kwa mfano Mheshimiwa Rais ametoa fedha za kujengea Shule ya Sekondari Luhanga, shilingi milioni 600, lakini pia akatoa fedha kwa ajili ya vituo shikizi zaidi ya vine. Cha kushangaza ni kwamba wateule wake wamezihamisha zile fedha bila taarifa yoyote kwa wananchi. Wananchi wameshikwa na taharuki kubwa, wanashangaa; Mheshimiwa Rais anavyopenda wananchi wake, ameleta fedha halafu tena zimehamishwa, kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na majibu rahisi huwa wanasema kuwa haya ni maamuzi ya Mheshimiwa Rais. Sasa, matumizi mabaya ya jina la Mheshimiwa Rais kwa kweli hii inasikitisha sana na haikubaliki. Nimetembelea Luhanga, nimefanya kikao pale, nimeshuhudia mwenye wananchi kwa nguvu zao wamejitoa, wamechangishana; na ugumu walio nao lakini wameweza kujenga majengo ya shule ya sekondari, na wamekamilisha vyumba vitatu na ofisi moja; na matundu ya vyoo ilikuwa bado kidogo kukamilisha, mimi nikajitolea mifuko ya saruji ili wakamilishe kwa dhumuni la kunusuru watoto wale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu iliyopita watoto 60 hawaku-report shuleni katika kata ambayo iko jirani. Kwa kweli ni umbali mrefu, zaidi ya kilometa 60 kwenda na kurudi; sasa, watoto wanashindwa kuhudhuria. mwaka huu kati ya watoto 2019 waliochaguliwa kwenda kidato cha kwanza ni Watoto 49 tu wame-report, wengine wote wamepotelea mitaani na wanachunga ng’ombe. Kwa kweli wanakosa haki yao ya msingi ya kupata elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, cha kushangaza ni kwamba, eneo lile wao wanasema ni hifadhi, mimi wiki iliyopita nilimfuata Mheshimiwa Waziri, kwamba hebu tuangalie kwenye kitabu, eneo lile sikuliona. Wakati huo huo ninafanya kikao pale kuna kijana alisimama, anauliza, anasema, hapa ardhi imeuzwa kwa matajiri, sisi vijana hatujapewa hata ekari moja. Mimi nimewasimamisha wenyeviti wa vijiji pale wajibu hoja, kwamba kwa nini mmeuza ardhi na imekuwaje vijana hawajapewa hata ekari moja. Viongozi wale walianza kuvutana vutana pale; haieleweki nani ameuza. Mheshimiwa Diwani akasema Mheshimiwa Mbunge tunaomba utuachie, hili tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, cha kushangaza, iwapo eneo lile ni hifadhi, imekuwaje matajiri waende wakanunue na kisha watengeneze mashamba? Wao hawaogopi kuhamkishwa?

Mheshimiwa Mwenyikiti, lakini madhara mengine ni kwenye anuani za makazi. Sote tunaelewa, sensa ya tarehe 23 Agosti itajumuisha pamoja na anuani za makazi. Sasa pale Mbarali kuna kata tatu ambazo sehemu kubwa ya vijiji havijawekwa kwenye mpango wa anuani za makazi mpaka sasa hivi ninavyoongea. Hata hivyo, cha ajabu ni kwamba, viongozi wangu walipolalamika kwamba mbona vijiji vingi havijaingizwa kwenye anuani za makazi mimi niliwajulisha kwamba hebu kaeni kwenye kamati ya siasa mje na muhtasari huku Dodoma mtakapokuja kwenye Mkutano Mkuu wa Chama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikaa kwenye kamati ya siasa, majibu yakawa ndiyo hayo, kwamba ni maamuzi ya Mheshimiwa Rais. Viongozi wale wa chama wakasema kama ndivyo hivi sisi kesho tunakwenda Dodoma na muhtasari huu tukaoneshe. Cha kushangaza, asubuhi ile tunapigiwa simu kuwa baadhi ya vijiji wametumwa wataalam Kwenda kuandikisha anuani za makazi. Sasa tunashangaa, kwamba Mheshimiwa Rais anaamua kwa namna hiyo, kama si kumchafua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana kwamba wanancho walikabidhiwa yale maeneo ili waendelee kufanya kazi zao kama kawaida. Wapo waliojenga nyumba nzuri za maana, wako wanaobabaika mpaka sasa wanashindwa kujenga nyumba ilhali wana haki kabisa. Ingalikuwa wao wamehamishwa au wamelipwa fidia sasa hapo ni kweli wasingeweza kupewa anuani za kamakazi. Taratibu hazijafuatwa, sasa kwa nini wasipewe anuani za makazi? Na kama Serikali itaamua kulichukua eneo hilo basi taratibu zifuatwe. Kwamba wajulishwe, washirikishwe, walipe fidia halafu waondoke, kuliko kubaki wanateseka, kwamba hawana uhakika na maisha yao, kwamba tutabaki au tutaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kinachosikitisha zaidi ni usiri mkubwa katika jambo hili. Tumeona Mheshimiwa Waziri Mkuu, mwadilifu, mzalendo mkubwa kabisa, amekwenda pale Ngorongoro, amekaa na wananchi wale wafugaji, amewaelekeza hali halisi, baadhi yao wamekubali na wanaondoka vizuri tu kwa hiari yao. Kwa nini Mbarali kuna siri? Kuna nini nyuma ya pazia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile tume ya mawaziri nane walikwenda Mbeya; viongozi wa chama walipigiwa simu kwamba kesho wanakuja mawaziri, nami wakanijulisha. Jioni yake wakapigiwa simu kuwa ile ziara imeahirishwa, msije, lakini kumbe wanakuja. Sasa, kwa nini watufiche? Wawakilishi wa wananchi tunatakiwa tuwepo, tusikilize ili tutoke na majibu sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vyombo vya habari ziliandika habari za kutisha wananchi, kwamba sasa vijiji 31 vinakwenda kwenye hifadhi, wananchi wakashangaa. Mimi nimekuja kufuatilia kwa Mheshimiwa Waziri, kwa kweli Mheshimiwa Waziri alikanusha habari za ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi ya shamba humaliziwa shamba, tunaoumia ni wana-Mbarali. Wanapokwenda Mkoani Mbeya, Mbeya wenyewe wanashangaa kama ambavyo huku wanavyoshangaa. Lakini maumivu tunaopata ni sisi wana-Mbarali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.