Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Masache Njelu Kasaka (15 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri Mkuu. Niungane na wenzangu kutoa pole kwa familia na Watanzania kutokana na kifo cha Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. Pia nampongeza Rais wetu wa Awamu ya Sita, mama yetu Mheshimiwa Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri Mkuu kwa hotuba hii nzuri ambayo nitapenda kujikita kwenye Sekta ya Madini. Kama ambavyo tunajua, Serikali ya Awamu ya Tano wakati inaingia madarakani ilirekebisha mazingira ya uchimbaji na tukaweza kutoka pale tulipokuwa na kupata mapato kutoka shilingi bilioni 150 mpaka kufikia takribani shilingi bilioni 550, kwa kiwango hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi watu wa Wilaya ya Chunya tuliweza kutoka uzalishaji wa kilo 20 kwa mwezi mpaka sasa hivi tunafika kilo 230 kwa mwezi. Haya ni mafanikio makubwa ambayo yanaweza kupelekea kulipa kodi. Mwanzoni wakati Serikali Awamu ya Tano inaingia madarakani tulikuwa tunalipa kodi ya shilingi milioni 150, lakini sasa hivi tunaweza kulipa kodi zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa mwezi. Haya ni mafanikio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima twende mbele zaidi, tusiridhike na hapa tulipofika. Ili tuweze kwenda, kuna sheria mbalimbali ambazo kubadilishwa; na moja kati ya sheria ambazo zimebalishwa iliweza kuwataka wale wanaofanya utafiti kwenye madini, kuhakikisha majibu ya tafiti zao yanapelekwa kwenye Taasisi ya Jiolojia (GST).

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wetu ni nini? Ushauri wetu ni kwamba zile tafiti ambazo zimeshapelekwa GST, zinyambuliwe katika lugha nyepesi ambapo wachimbaji wetu wazipate na kuweza kuzitumia ili uchimbaji wao sasa ufanyike vizuri. Badala ya uchimbaji huu wa ramli unaofanyika kwa wachimbaji wadogo, itatuwezesha sasa kupata mapato mengi zaidi na mapato haya yatasaidia kuongeza wigo wa mapato ya Serikali na kuleta mapato makubwa zaidi kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa GST hawa wenzetu, bado ofisi zao ziko Dodoma. Nchi nzima huku tukitaka kupima viwango vyetu vya madini, ni lazima tuje Dodoma. Nashauri sasa kwa Wizara kuhakikisha kwamba washuke chini zaidi kwenye level ya kanda ili GST wawepo kwenye kanda na wachimbaji wetu wadogo wasifunge safari kutoka Chunya kuja Dodoma, waishie kwenye kanda. Hiyo itaweza kutusaidia sana. Ni imani yangu kwamba Serikali itawasaidia wachimbaji wadogo na uzalishaji wao kuongezeka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongezee pia kwa upande wa kodi. Kwa sisi wachimbaji wadogo, kodi imekuwa siyo Rafiki. Tunaomba Serikali iangalie namna gani ambavyo itaweza kutusaidia. Leo hii kwa mchimbaji huyu anaweza akapata leo kiasi cha shilingi milioni 50, lakini akiipata leo, inawezekana mwaka mzima asipate tena. Sasa nini cha kufanya? Namna nzuri ya kufanya na kuwasaidia wachimbaji wetu wadogo, tuone namna bora zaidi ya kubadilisha sheria, ili wakati ambapo mchimbaji anaenda kuuza madini yake na kodi hii aweze kukatwa pale pale; kama ambavyo kodi hii inakatwa kwenye mrabaha wa 6% na inspection fee 1%, unapouza unakatwa pale pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia yale malalamiko tuliyonayo wafanyabiashara na wachimbaji wetu kwa akaunti zetu kufungwa na TRA, hili suala halitakuwepo. Maana nikienda kuuza madini yangu, pale pale nitakwa na kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, itawasidia wachimbaji wetu. Kwa kauli ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Mama yetu Samia amesema tusifungiwe akaunti. Kwa hiyo, akaunti za wachimbaji hazitafungwa na sheria hizi zikibadilishwa, hawataweza tena kupata matatizo yoyote ya kikodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ninaloweza kulielezea ni namna ambavyo ile Service Levy tunavyoilipa kwenye Halmashauri. Service Levy tunayolipa kwenye Halmashauri ni asilimia 0.03, ndivyo wachimbaji wanavyoilipa. Sasa kwa maeneo ya Wilaya, kama Wilaya ya Chunya ambako ndiko tunakochimba madini, tunalipa kodi zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa mwezi, lakini malipo yanayobakia kwenye Halmashauri ni asilimia 0.03. Ni kiasi kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kuona namna bora zaidi ya kubadilisha hii sheria angalau kiwango hiki sasa hivi kiweze kupanda kutoka 0.03% iweze kwenda 1% au 2% ili mapato mengi yaweze kubaki kwenye Halmshauri zetu kule ambako wachimbaji wanafanya uchimbaji huu. Hiyo itaweza kusaidia haya matatizo madogo madogo tunayokimbizana nayo sasa; ya madarasa, madawati na kadhalika, kile kiwango ambacho tunakipata kitaweza kufanya kazi vizuri zaidi kwenye Halmashauri zetu kule na Serikali haitakimbizana na hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kusema hayo, naiunga mkono hoja iliyoko mbele yetu na ninampomgeza sana Waziri Mkuu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi kupata nafasi niweze kuchangia kwenye hotuba nzuri sana ya Ofisi ya TAMISEMI.

Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake, vijana mahiri, wachapakazi, wanaokimbia huku na huku na mimi nawashukuru sana Waziri pamoja na Naibu Mawaziri wote wameshafika Chunya, tunawashukuru sana kwa kazi nzuri ambayo wamendelea kufanya, lakini pia tuipongeze Serikali yetu ya Awamu ya Sita kwa namna ambavyo imeweza kushusha miradi mingi kupitia TAMISEMI, imeweza kushusha fedha nyingi sana kupitia TAMISEMI, tumpongeze sana Mama yetu Samia Suluhu kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kufanya na ninyi kama wasaidizi wake mmekuwa mnaweza kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote tumekuwa mashahidi namna ambavyo fedha hizi zimekuwa zinakwenda kwenye majimbo yetu na kwenye Wilaya zetu. Nianze tu kuzungumza kwenye upande wa TARURA. Tumeona namna ambavyo kila mmoja hapa ameweza kuguswa na pesa nyingi sana ambazo zimekwenda kwenye upande wa kujenga barabara hasa barabara ya TARURA. Pesa hizi zimeshuka nyingi ambazo zimeweza kwenda kule kwenye vijiji vyetu, kwenye kata zetu, kwenye Wilaya zetu na ameweza kuchechemua uchumi wa kwenye maeneo yetu yale na kwa mara ya kwanza sisi tumeweza kupata fedha nyingi, kwa Wilaya ya Chunya peke yake tumepata zaidi ya shilingi bilioni 2.3. Ni fedha nyingi ambazo tumezipata kipindi chochote ambacho Wilaya hii imeumbwa, tuipongeze sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeendelea kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pesa hizi pamoja na kufika huko tumeona namna ambavyo zimeweza kuchechemua uchumi wa nchi, namna ambavyo wakandarasi wameweza kuzidiwa kwa miradi mingi waliyokuwanayo. Leo hii wakandarasi tunawadai kazi siyo pesa, pesa zimekwenda huko nyingi za kutosha, lakini wao ndiyo wamekwama kutekeleza kwa wakati. Aidha, hawana vitendea kazi, hawana wataalam wa kutosha ambao imepelekea mpaka hii miradi kwenda kwa kusuasua. Lakini kwa upande wa Serikali tumeona kwamba fedha zimeweza kwenda kwa wakati. Zimeweza kwenda kwa wakati, tunaweza kuipongeza sana Serikali hii imeweza kufanya mambo makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja nakufanya mambo makubwa haya tuwapongeze tumeona kwenye hotuba yako hapa ya bajeti yale mawazo tuliyokuwa tukiishauri Serikali mara kwa mara mmeweza kuyachukua. Tulikuwa tunawaambia kwamba mwaka wa fedha unaanza Julai, ninyi mlikuwa mnakaa mnasubiri Julai mwaka wa fedha unapoanza ndiyo mlikuwa mnaanza kutangaza tender kwa ajili ya kufanya hizi kazi za ujenzi wa barabara. Lakini tumewashauri mara kadhaa, nimeona kwenye bajeti yako umesema. Sasa haya mmeyapokea na mmeweza kuyafanyia kazi. Sasa hivi mnaanza kutangaza hizi tender ili kuanzia mwezi Julai mwaka wa fedha unapoanza maana yake watu wanapewa sasa mikataba hii na kazi zinaanza kwenda kwa wakati. Hii tunawapongeza sana na kwa kweli ule utaratibu wa nyuma ule ulikuwa unatukwamisha sana. Leo hii sisi kwa Chunya unakuta fedha zilitoka toka mwaka jana mwezi wa nane wa tisa leo ndiyo miradi ya barabara inatekelezwa. Watu wamepata shida kipindi chote cha masika wakati fedha zipo. Lakini kwa utaratibu huu ambao mmeanza nao mmetuambia leo kwa kweli tunawapongeza sana mmechukua ushauri wetu uliokuwa mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo tumeona kwamba sasa TARURA pamoja na kazi nzuri ambayo wanafanya lakini na wao pia kuna changamoto wanazo, wana changamoto za wafanyakazi, za ma-engineer, sisi Wilaya yetu ya Chunya tuna ma-engineer watatu almost kama wanne, Wilaya ni kubwa sana kwa Mkoa wa Mbeya tunakaribu ya eneo la ukubwa zaidi ya asilimia 40 ya Mkoa mzima wa Mbeya, sasa unapotupa wahandisi watatu, na bosi wao mmoja pale Mkuu wa Idara maana yake unatulinganisha sisi na Wilaya nyingine, sisi tunakuwa kwenye wakati mgumu kwenda kusimamia hii miradi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo yake kule barabara za vijijini zinakosa usimamizi mzuri wa ma-engineer hawa waweko kule kwa wakati barabara zinajengwa wakati mwingine wakati mwingine zinajengwa mkandarasi anajenga chini ya kiwango, lakini mainjinia wetu hawa wanashindwa kufika maeneo husika kwa wakati kuweza kusimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nishauri kwenye ajira ambazo zinakuwa zinatolewa hizi pamoja na kuajiri ma- engineer hawa tuajiri pia na wale ma-engineer wa kati wale ma- technician wawepo, wawe ndio wanashinda kulekule site muda wote, wataweza kutusaidia sana kuhakikisha kwamba thamani ya fedha inayotolewa inakwenda sambamba na kazi ambayo inakwenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine kwenye upande wa TARURA ni vitendea kazi hasa magari. Wilaya zetu hizi zinatofautiana Wilaya za mjini na wilaya za vijijini, Wilaya ya mjini ukiwapata magari ya kawaida, ukiwapa pickup za kawaida, wao zinaweza zikawasaidia sana, lakini kwa Wilaya zetu sisi zenye miundombinu mibovu ya barabara kama Wilaya yetu ya Chunya kuweza kuwapa pickup ya kawaida ni ngumu sana utekelezaji wake kwenda kusimamia hii miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana wakati ugawanyaji huu wa rasilimali hizi za magari unafanyika Wilaya sisi hizi zenye miundombinu dume tuweze kupata yale magari ambayo yanaweza yakahimili, tuweze kupata landcruiser pickup ziweze kufanya kazi kule. Leo tunapozungumza hapa sisi pale Wilaya ya Chunya tuna pickup moja ambayo pickup yenyewe bado ni mbovu, leo ni spana mkononi matokeo yake ma- engineer wanashindwa kwenda kufanya kazi kufikia miradi kwa wakati, kila siku wanabisha hodi kwa Mkurugenzi kwenda kuomba magari pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana kwenye bajeti zenu hizi mnapotenga vitendea kazi muone miundombinu ya Wilaya za vijijini hizi tuweze kupata magari ambayo yataweza kutusaidia kuweza kufikia na kuweza kusimamia hii miradi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine lakuweza kuchangia ni kwenye upande wa elimu, niipongeze Serikali imefanya kazi kubwa, imeweza kujenga miundombinu ya majengo vizuri sana, sisi sote tumekuwa mashahidi tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita ya Mama Samia, tunashukuru sana viongozi wa Wizara, pamoja na kazi kubwa hii iliyofanyika leo hii majengo yetu kule yanakuwa hayajaweza kutumika ipasavyo, majengo yamekamilika watoto wapo lakini hatuna walimu wakuweza kwenda kuwafundisha watoto wetu. Lakini pamoja kwamba shule shikizi zimejengwa kule na leo hapa naona umezungumza kwamba zitaendelea kwenda kujengwa, tuone namna ambavyo hizi shule shikizi tuwapeleke walimu ambao wanaweza wakakaa kwenye mazingira yale, na walimu wanaweza kukaa kwenye mazingira yale tunao sasa hivi walimu wapo wanaojitolea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ajira zinapotoka hizi wao ndio tuwape kipaumbele kwa sababu tayari wameweza kumudu yale mazingira, ajira zilizopita awamu iliyopita tumeona walimu wanaojitolea wameachwa, sasa tunaomba sana awamu hii walimu wanaojitolea wale waweze kupewa kipaumbele cha kwanza hii itaweza kutusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niwapongeze mnasema mnakarabati shule kongwe sisi pale Chunya tuna shule zetu kongwe za miaka mingi toka enzi hatujapata uhuru, shule ya msingi ya Chunya kati, shule ya msingi ya Mjini pale tumerithi kutoka kwa Wamisionari, zimechakaa zimeharibika zimekuwa za muda mrefu sana sasa shule shikizi zinakuwa ni nzuri kuliko zile shule ambazo zilikuwa muda mrefu na ziko katikati ya mji. Tuombe sana mnapotenga kwenye bajeti yetu zile shule kongwe muweze kuzikumbuka na hizi shule tutaweza sana kuendana sambamba ya utoaji wa elimu bora tunayoendelea nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na haya walimu tutawapeleka kule tuone namna ya kuweza kuwasadia kuwajengea nyumba kule kwenye shule shikizi kule kuna maeneo mengine sisi wanakokaa wafugaji kule hata nyumba ya kupanga mwalimu hakuna, sasa tuone namna ambavyo kupitia Wizara yenu, mkishirikiana pamoja na Wizara ya Elimu kuona namna ambavyo mtaweza kujenga nyumba za walimu ili walimu wetu hawa waweze kufanya kazi katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho nizungumze habari ya afya na yenyewe tunaipongeza Serikali mmefanya kazi vizuri, miundombinu ya afya imejengwa vizuri vituo vya afya vinajengwa, zahanati tunaona zinajengwa na kwa kweli kazi inayofanyika maana yake tunaenda kuwajali Watanzania kuhakikisha kwamba wana afya bora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja kwamba miundombinu hii ya majengo yanajengwa lakini bado tuna changamoto ya vifaatiba; vifaatiba kwenye zahanati zetu na kwenye vituo vya afya hatuna mimi nikupe mfano tuna Kituo cha Afya cha Mtande kimekamilika toka mwaka 2019 lakini mpaka leo hakina vifaatiba pale, sasa hiko ni kimoja ambacho ni Kituo cha Afya cha Mtande, lakini tuna Kituo cha Afya cha Makongolosi kimekamilika, tuna Kituo cha Afya cha Matwiga, na sasa hivi tunaenda kukamilisha Kituo cha Afya cha Kambikatoto vyote hivi havina vifaatiba, tuombe sana Serikali inapofanya mambo haya...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana ya pili hiyo kwa mchango mzuri sasa mchangiaji wetu wa mwisho.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana kwenye uchumi wa nchi yetu lakini kwenye maendeleo ya nchi yetu kwa sababu taasisi zote muhimu ambazo zinakwenda kuboresha uchumi wetu zipo chini ya Wizara hii. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, pamoja na wakuu wa taasisi zake zote wanafanya kazi nzuri sana na kazi ambazo tunaziona na ule usemi wa kwamba kazi iandelee, hapa kweli kazi inaendelea. Tunawapongeza sana ninaimani huu ni utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi chini ya Jemedari Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, hakika kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mambo kadhaa ya kuweza kuchangia kuhusu Wizara hii na nitapenda nianze na suala la barabara. Tumeona kwenye bajeti hii namna ambavyo barabara nyingi zimeoneshwa kwenda kutengenezwa na barabara nyingine ujenzi wake unaendelea na nyingine tayari zimekwisha zinduliwa. Tunaipongeza Serikali kwenye hili na nina imani zile barabara ambazo bado zimebakia zitakwenda kufanyiwa kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini moja kati ya barabara ambazo bado hazijaweza kujengwa barabara ya mkoa ni barabara ambayo inaunganisha kati ya Mkoa wa Mbeya pamoja na Mkoa wa Tabora na Singida. Barabra hii inapita ndani ya Wilaya ya Chunya ambako ndipo jimbo langu lilipo. Barabara hii ni muhimu sana kiuchumi kwa sababu barabara hii inakwenda inafungua Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, Mikoa ya Kanda ya Kati na Kanda ya ziwa. Kwa hiyo, muiangalie barabara hii kwa jicho la kipekee. Maana yake ukiifungua barabara hii kwa kiwango cha lami maana yake sasa utakwenda kuifungua mikoa ya nyanda za juu kwa maana ina mipaka miwili kule, Mpaka wa Tunduma na mpaka wa Malawi unakwenda kutuunganisha sasa na Mkoa wa Tabora na Singida ambapo tunakwenda moja kwa moja mpaka mikoa ya kanda ya ziwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri barabara hii ina umuhimu mkubwa sana, naomba uweze kuiangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia hapa kwenye bajeti yako namna ambavyo miradi inaendelea. Mheshimiwa Waziri na hii barabara na yenyewe naomba uweze kuiweka kwenye mpango wa EPC + F ili na yenyewe iweze kujengwa. Tumeona mmeanza upande wa Mkiwa kilometa 56 lakini hizi ni kidogo sana. Kwa sababu barabara hii ina kilometa zaidi ya 350. Ukianza kilometa 56 upande wa Mkiwa mpaka uje ufike Makongolosi huku inaweza ikachukua miaka mingi sana. Niombe sasa, unapoanza upande wa Mkiwa kule ambako kazi inaendelea, sasa tuanze upande wa Makongolosi kwa maana ya Wilaya ya Chunya ili tuweze kwenda huko angalau tupate kilometa 100, tutaweza kwenda vizuri sana na barabara hii itaweza kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna barabara nyingine kuanzia Makongolosi ambayo inakwenda kutuunganisha na Mkoa wa Songwe na Wilaya ya Songwe. Barabara hii inaanzia Makongolosi inapita kwenye Mji wa Mkwajuni inakwenda kutuunganisha na Mbalizi. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Songwe lakini kwenda kutuunganisha na Mkoa wa Songwe pamoja na Mkoa wa Mbeya. niombe Mheshimiwa Waziri, anapokwenda kupanga mipango yake na hii barabara pia aweze kuiweka kwenye mipango pia iweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo barabara za mwendokasi. Barabara hizi zimeanza kujengwa kwenye Mji wa Dar es salaam lakini baadae zitaenea katika maeneo mbalimbali kwenye nchi yetu hii ya Tanzania. Barabara hizi ni nzuri, sasa hivi Mji wa Dar es Salaam unapendeza. Lakini, zinapokuwa zinajengwa hizi barabara kunakuwa na changamoto kwenye ujenzi wake. Tumeona, wakati wa awamu ya kwanza ya barabara inajengwa tumeona kwa maana ya kuanzia Barabara ya Morogoro, lengo kubwa lilikuwa ni kwenda kuzitoa daladala ambazo tumekwishazoea kuzitumia siku zote. Hata hivyo, lengo hili lilishindwa kutimia kwa sababu wakati wanajenga havikujengwa vituo vya kusimamia dala dala za kawaida. Leo hii dala dala za kawaida zinasimama katikati ya Barabara, hali ambayo inapelekea foleni kubwa sana. Lengo la barabara ya mwendokasi ni kupunguza foleni lakini kwa sababu tulishindwa kuzitoa dala dala za kawaida na zenyewe zinasimama kwenye vituo zilivyozoea kusimama kule. Hii barabara inakuwa tena haitusaidii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilitegemea Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalamu wake hasa wa TANROADS, kwamba baada ya kuona awamu ya kwanza tumeshindwa kuzitoa dala dala , awamu zinazofuata kwa maana ya kuanzia Barabara ya Kilwa Road kwenda Mbagala na hii ya Nyerere Road kwenda Gongo la Mboto tuweze kuweka provision ya vituo vya dala dala hata kama dala dala hizi tutakuja kuzitoa baadaye, hii provision ya vituo hivi vya dala dala itatumika pale mtu atakapokuwa amepata emergence gari itasukumwa itakwenda kusogezwa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunavyosema na wewe gari inapopata tatizo lolote mtu anaweza kutembea kilometa mbili mpaka kikometa tatu ndipo aweze kupata mahali pa kuweza kujibanza. Hii tunaomba sana mlichukue na huko mbele mnapoendelea kujenga, na hata sasa hivi kwa kuwa bado ujenzi unaendelea, muone namna ambavyo mnaweza kulirekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia Uwanja wa Ndege wa Songwe. Tunaishukuru Serikali imefanya kazi nzuri sana uwanja wetu sasa hivi umekuwa ni mzuri, jengo letu la abiria sasa limefikia zaidi ya asilimia 98 na kwa kweli jengo linapendeza sana, lakini pia uzio kwenye uwanja wetu wa ndege umekamilika tunaipongeza Serikali kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hili, mimi niombe sasa, ule uwanja jengo la abiria pale imeshakamilika, sasa, hizi asilimia zilizobakia ziweze kukamilika na baadae sasa jengo hili lizinduliwe ili sisi wananchi wa Mbeya na wananchi wa Nyanda za Juu Kusini tuweze kufaidika na huduma bora ambazo zinapatikana ndani ya uwanja huu wa ndege, na hasa ukizingatia sasa hivi ndege zinaanza kutua usiku, kwa hiyo wananchi wengi sana hapa wanatumia ule uwanja. Nina imani jengo lile litakapokamilika huduma nyingine zitazidi kuboreka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bei yake, ule uwanja sasa hivi hauna cold room; niombe wakati ujenzi huu unaendelea iweze kujengwa cold room kwa ajili ya perishable goods. Tuna amani, kwamba sasa hivi kuna parachichi pale zinazalishwa kwa wingi sana zitahitaji kusafirishwa kwenda nje, tuna mazao ya horticulture na mazao ya maua yatasafirishwa kupelekwa nje. Haya yote yanahitaji sana ile cold room. Kama ulivyosema kwenye hotuba yako, sasa ndege ya mizigo iko njiani inakuja, sasa, ndege ya mizigo hii kama iko njiani inakuja itashindwa kufanya vizuri kwa ufanisi kwa sababu cold room sasa hivi hatuna pale. Niombe sana hivi vyote viwili viweze kwenda kwa pamoja, vitaweza kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo na upande wa ATCL, wanafanya kazi nzuri, lakini kumekuwa na changamoto kubwa sana ya cancellation ya safari. Sisi watu wa Mbeya mara nyingi sana tumekuwa tunasafiri kwa ndege hizi usiku. Tiketi inakuonyesha saa kumi na mbili jioni, mara saa mbili usiku unakuja kuondoka saa saba za usiku; na hii yote inakwenda hata taarifa haupewi, na baadaye unakuta tu hata kuombwa radhi inakuwa ni changamoto. Lakini sisi abiria ambao leo ukipata changamoto kama hiyo ukataka Kwenda kubadilisha tu tiketi yako, bei ya kubadilisha tiketi ni kubwa sana, ambapo ni bora ukate tiketi mpya kuliko kubadilisha tiketi ambayo inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili wananchi wengi wakaosa mahali pa kusemea. Sasa sisi tuwaombe kupitia Wizara lakini kupitia watu wa ATCL, ninaimani Engineer Matindi ni msikivu sana, waliangalie kwa jicho la peke yake. Wananchi wanapotaka kubadilisha tiketi basi bei iwe reasonable ambayo kila mwananchi anaweza akafanya hivyo, lakini bila hivyo wananchi wengi wanaumia kiasi kwamba inafikia hatua mtu anaona ni bora aiche tiketi iende apate tiketi upya kuliko kubadilisha tiketi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ili kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Madini. Pia nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri, yeye pamoja na Naibu Waziri, lakini pia na timu yote nzima ya Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya. Kwa kweli tuwapongeze Wizara hii kwa kuweza kuchangia pato la Taifa na mpaka kufikia mwezi Septemba, 2020 iliweza kukua kwa asilimia sita. Kwa hiyo, tunaipongeza kwa kazi kubwa sana ambayo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile niipongeze pia Wizara kwa namna ambavyo iliweza kusimamia uanzishwaji wa masoko. Masoko haya makubwa takribani masoko 39 yalianzishwa, masoko madogo zaidi ya 41 na mengine yanaendelea kuzalishwa, yanaendelea kujengwa. Pia vituo vya ununuzi vidogo vidogo vile katika vijiji, vinaendelea kujengwa katika vijiji vyetu na hili linaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa sana namna nzuri ambavyo tunaweza tukazuia utoroshaji wa dhahabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hivi vituo kuna changamoto kidogo ambayo wananchi wetu wanaweza kuipata kule. Moja ya changamoto ambayo wanaipata ni masoko haya kutofanya kazi siku za Jumamosi na Jumapili, lakini pia siku za Sikukuu. Kwa sababu, wachimbaji wetu wadogo wengi uchimbaji wao na kipato chao kinategemea kwa siku, aende asubuhi achimbe na jioni aweze kuuza. Sasa mchimbaji huyo anachimba vizuri, lakini akienda muda wa kwenda kuuza anaambiwa kwamba, sasa leo weekend soko limefungwa. Kwa hiyo tuone njia nzuri aidha haya masoko madogo kwa maana ya brokers na hizi buying station hizi ziweze kufunguliwa siku saba za wiki na hata siku ambazo ni za sikukuu pia, ziweze kuweza kufanya kazi ili wachimbaji wetu hawa wawe na uhakika wa kuuza dhahabu zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine, tumeona hapa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna vipaumbele ambavyo ameviweka, kipaumbele kimojawapo ni kuweza kuwaendeleza wachimbaji wadogo. Kweli juhudi kubwa zinafanywa, Wizara inafanya jambo kubwa kuwaendeleza wachimbaji wadogo na sisi sote tumekuwa mashahidi tunaona namna iliyokuwa bora ambavyo wachimbaji hao wanaweza kuendelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikumbuke hapo nyuma kidogo wakati Wizara imetengeneza utaratibu wa kuweza kuwasaidia wachimbaji wadogo iliweza kutengeneza mfumo wa kuwapa ruzuku. Wachimbaji wadogo walikuwa wanapewa ruzuku. Nakumbuka miaka kadhaa walikuwa wanapenda ruzuku na mara ya mwisho nadhani kama 2017 au 2018 ndiyo ruzuku hii ilikoma. Sasa hivi tukitaka kuweza kuwasaidia hawa wachimbaji wadogo, tuweke mazingira mazuri ya kuweza kurudisha tena ile ruzuku. Ile ruzuku inawasaidia sana wachimbaji hawa, inawasaidia kimitaji na wao wanaweza kukua. Waliokuwepo Wizarani watakumbuka, wachimbaji wengi waliopata ruzuku ile miaka ya nyuma, leo hii wamekuwa wachimbaji wa kati, wameweza kukua na wao wameweza kuajiri wachimbaji wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Wizara iweze tena kuweza kutoa ruzuku kwa wachimbaji hawa wadogo, ili na wao waweze kukua na wao wataweza kutoa ajira, lakini pia pato kwa Serikali kwa sababu wataweza kulipa kodi vizuri zaidi. Nizungumzie suala la GST, GST hii Taasisi inategemewa sana sana na wachimbaji kwa sababu inafanya kazi kubwa na sisi wachimbaji tunaiona kazi ambayo wanaifanya. Nikiangalia kwenye taarifa hapa aliyokuwa anasoma Mheshimiwa Waziri, fedha zilizotengwa kwa ajili ya kuendeleza utafiti kwenye hii taasisi ni takribani bilioni 3.4 tu. Kwa kweli fedha hizi ni kidogo mno, ukiangalia kazi kubwa ambayo taasisi hii inafanya na sisi wachimbaji tunategemea iendelee kufanya. Nashauri tuone namna iliyokuwa bora zaidi kuweza kuongeza fedha kwenye Taasisi ya GST, ili na wao sasa waweze kuwa na nguvu kubwa Zaidi, waweze kufanya kazi vizuri, waweze kuwafikia wachimbaji wetu huko na zile tafiti zao ziweze kuwasaidia wachimbaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hii GST tunafahamu kwamba wako hapa Dodoma, tunashauri waweze kupewa fedha ili washuke chini huku mikoani maeneo ambako uchimbaji huu unafanyika. Wakiweza kushuka huku itatupunguzia gharama kwa wachimbaji wetu, mchimbaji anatoka Chunya, anatoka Itumbi aweze kuja mpaka Dodoma kuja kuleta mawe yake ili yafanyiwe utafiti, gharama inakuwa kubwa lakini pia inachukua muda, angalau ikisogezwa kwenye maeneo yetu ya mikoani kule itaweza kutusaidia sana sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye GST hii vile vile, ikumbukwe kwenye mabadiliko ya sheria ya mwaka 2017, iliyataka makampuni yote yanayofanya utafiti yakimaliza tafiti zao, copy ya tafiti zile ziweze kupelekwa GST. Sasa nishauri pia GST, zile tafiti wanazozipata waweze kuzinyambua katika lugha ambayo ni rafiki kwa sisi wachimbaji wadogo, ili baadaye wachimbaji hawa wadogo wakihitaji zile tafiti waweze kupewa, ziweze kuwasaidia katika uchimbaji ambao wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji ambao wapo hapa wanafahamu namna ambavyo wachimbaji wadogo wanachimba kwa kubahatisha, ni kama vile wanapiga ramli tu. Sasa tuondoke kwenye uchimbaji wa kupiga ramli, sasa twende kwenye uchimbaji ambao umefanyiwa utafiti mzuri ili wachimbaji wetu wanapochimba wawe na uhakika na kitu kile ambacho wanakifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la kodi, kuna wachimbaji wetu wa ndani lakini pia tuna wachimbaji wetu wa nje. Wachimbaji wetu wa ndani ambao wanachimba nje wakitoka na mali kule kuingia nazo ndani, bado TRA wanawakata kodi wanavyoingia na ule mzigo hapa ndani. Hata carbon wakitoka nazo nje, wakiingia nazo ndani bado TRA wanawakata kodi na bado wakija kuchenjua, baadaye wakipeleka mzigo sokoni bado wanaendelea kukatwa kodi kwa maana ya kwamba zile tozo ya mrabaha asilimia sita na inspection fee asilimia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri sasa tuone namna iliyokuwa nzuri zaidi ya kwamba, kama mtu anatoa mzigo nje anatuletea ndani, tusiwe tena tunamkata hiyo kodi kule. Ibakie kodi ya ndani, hii itawasaidia wachimbaji wa kwetu ambao wako nje, waweze kutoa mali kule kuleta ndani na sisi tutapata kodi kubwa zaidi hapa ndani. Kwa hiyo, upande wa kodi niishauri pia namna iliyokuwa bora zaidi ya mchimbaji huyu wakati anauza dhahabu zake tumkate kodi kwa asilimia, pale anapouza tumkate kodi kwa asilimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itaweza kuwasaidia sana kwanza itasaidia Serikali kuweza kupata mapato ya uhakika, maana yake kila anayeuza dhahabu yake au madini yake atakatwa kodi pale pale. Pia itaweza kuwasaidia wachimbaji wetu, mchimbaji leo anachimba, anapata leo, lakini mwisho wa mwaka anakuja kulipa kodi. Kipindi ambacho anaambiwa alipe kodi fedha nayo hana, matokeo yake anakuwa na malimbikizo ya kodi na anashindwa kulipa hii kodi. Tukiweka utaratibu huo kwa asilimia utaweza kusaidia zaidi kwa wachimbaji hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna wale wachimbaji ambao huwa wanachimba lakini hawana eneo, hawana claim, hawana PML, sasa huyu mchimbaji huyu kila anachokipata, maana yake kama amekipata shambani kwake, huyo hawezi kulipa kodi kabisa. Sasa tukiweka utaratibu huu, maana yake hata huyu ambaye amepata dhahabu yake kwenye shamba lake, ataweza kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa upande wa TASAC. TASAC...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba nzuri iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri. Nimpongeze kwa hotuba nzuri, nipongeze Manaibu Waziri pamoja na watendaji wote. Sina shaka na uzoefu wa Mheshimiwa Waziri kwa kuwa alikuwepo kwenye Wizara hii kama Mtendaji Mkuu, kwa hiyo, ninaimani mambo mengi ambayo ameyaeleza hapa anayafahamu vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuongea kwenye barabara, kwa kweli kwenye bajeti hii ambayo imesomwa leo, barabara yetu ya Mbeya - Chunya - Makongorosi zimetengwa takribani bilioni 13, lakini hizi bilioni 13 hizi zote, zitaenda kuishia kwenda kulipa madeni ya wakandarasi ambao wamefanya hii kazi. Barabara hii imekamilika kutoka Mbeya mpaka Chunya na sasa hivi inaendelea Chunya – Makongorosi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipande cha Mbeya – Chunya kimeshakuwa na mashimo, tumeshakuwa na viraka. Mheshimiwa Waziri alikuja wiki mbili zilizopita alikuja akaona na nilimwambia kwamba, standard za barabara anazojenga inakuwaje na hii barabara toka imekamilika ina miaka karibu mitatu tu na hii bado iko chini ya uangalizi wa mkandarasi, lakini tayari imeshakuwa na viraka, sasa sijui miaka mitano mbele itakuwaje. Kwa kweli sisi watu wa Chunya tulihitaji sana hii barabara kwa kiwango cha lami, lakini kiwango ambacho kilijengwa mpaka sasa hivi tuna wasiwasi zaidi ya miaka mitano inayokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo na mimi nitoe ushauri standard za viwango vya barabara za TANROADS ziwe kimoja ile layer ya juu inayojengwa iwe moja kwa barabara zote za TANROADS. Sio barabara hii inawekwa tabaka hili na barabara nyingine inamwagwa tu lami na baadaye zinawekwa kokoto juu, kwa hiyo magari yakija kupita barabara zile zinakuwa na mashimo. Pia tujue kwamba barabara ya lami inapokuwa imetengenezwa eneo Fulani, maana yake matumizi ya ile barabara yanaongezeka, kama ilivyo kwa barabara ya Mbeya – Chunya – Makongorosi. Barabara hii waliweka makadirio ya chini ya kupita magari, sasa hivi magari ni mengi mno ndio maana imeanza kuwa na viraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ujenzi wa barabara ya kuanzia Makongorosi – Rungwa – Mkiwa, hii imekuwa story sasa ya muda mrefu, kila siku inazungumzwa hii barabara, kila siku upembuzi yakinifu unaendelea. Kwenye bajeti hii zimetengwa hapa kuanzia Makongorosi – Rungwa wameonyesha hapa kilomita 50, lakini bado wanasema mpaka fedha zitakapopatikana! Pia kama hiyo haitoshi, hata upande wa kuanzia Ipole kuja mpaka Rungwa hivyo hivyo zimetengwa kiasi cha kilometa 56, lakini mpaka fedha zitakapopatikana. Kwa hiyo, kwa mtindo huu hatuwezi kwenda tukafika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi barabara zimeahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, tumeinadi Ilani hii kwa nguvu zote, tumewaaminisha na kuwaambia wananchi wetu. Kama fedha hazipatikani maana yake tutarudi kule kule kila siku. Sasa najiuliza hapa, sisi watu wa Mkoa wa Mbeya sisi tulikosea wapi? Maana yake barabara ya kuanzia Igawa - Mbeya Mjini mpaka Tunduma, hivyo hivyo fedha hakuna. Barabara za kuanzia Mbeya Mjini kwenda Makongorosi mpaka Rungwa, fedha hakuna. Vilevile ya Makongorosi, Mkwajuni mpaka Mbalizi, fedha hakuna na ndugu yangu Mheshimiwa Ally amezungumza ya kwenda mpaka Kasumulu kule, fedha hakuna. Sisi Mbeya kuna mradi gani wa barabara ambao fedha imetengwa kwa mwaka huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, sisi watu wa Mbeya tuna shida sana ya hizi barabara. Naomba waangalie vizuri bajeti hii angalau na sisi watu wa Chunya kuanzia Makongorosi ili na sisi watu wa Tarafa ya Kipembawe kule nao waweze kuona lami kwa mara ya kwanza. Naomba sana Waziri akayafanyie kazi haya, atakapokuwa anahitimisha hoja yake tuweze kupata majibu mazuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumze kidogo kwenye upande wa kiwanja cha ndege. Nimeona hapa kwenye bajeti hii nzuri ambayo Mheshimiwa Waziri ameisema ina maneno mazuri sana. Kiwanja chetu cha Songwe kimekuwa kila mwaka kinaongelewa habari ya kuwekwa taa, kila mwaka inaongelewa habari ya kuweka tabaka la juu, kila mwaka inaongelewa habari ya jengo la abiria na mwaka huu pia takribani karibu bilioni tisa zimetengwa, hatuna uhakika kwa maelezo ya miaka ya nyuma, je, hizi fedha zitatoka?

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba, kwa kiwango hiki cha pesa ambacho kimetengwa, badala ya mambo mengi kufanyika kwenye kile Kiwanja cha Songwe, basi angalau mambo mawili tu yafanyike. Liboreshwe jengo la abiria, lakini pia ziweze kutengenezwa zile taa za kutua ndege pale, hayo mambo mengine ya kutengeneza fensi na mambo ya matabaka mengine yatafuata baadaye, ili twende awamu kwa awamu, kuliko fedha hiyo kidogo ambayo inatolewa yote iende kufanya kazi pale haitaonekana nini ambacho kimefanyika. Hii iende pia kwenye viwanja vingine ambavyo vimetengewa fedha kwa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo upande wa bandari. Bandari yetu hii kuna uwekezaji mkubwa sana umefanyika na kama tunavyojua, bandari ni lango kubwa la uchumi. Geti Na.1 mpaka Na.7 limeweza kutengenezwa, kina kimeweza kuongezwa na sasa hivi tunaona geti la Na.7 na Na.8 yanaendelea na Geti Na. 12 na Na. 13 yanaendelea na usanifu wake. Hii ni kazi nzuri, tuipongeze Serikali kwa namna nzuri ambayo inafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyojua kwa kuwa bandari ndio lango kuu, linachangia kwenye uchumi lakini pia linachangia kuleta ajira, pale kwenye bandari kuna taasisi nyingi takribani zaidi ya 30 ambazo zinaizunguka bandari yetu hii. Kwa hiyo bandari inaweza ikaonekana kwamba ufanisi wake ni mdogo kwa sababu tu hizi taasisi nyingine hazina ofisi palepale bandarini. Kwa hiyo, nashauri hizi taasisi nyingine hizi ziweze kuweka ofisi zao palepale bandarini na ikiwezekana kuwe na dirisha dogo moja ambalo taasisi zote zitakuwepo pale. Hapo ndipo ufanisi wa hii bandari utaweza kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru Waziri Mkuu alikuja juzi pale na akawaambia watu wa TRA wawe na ofisi palepale bandarini, sio mtu anatoka pale chini bandarini mpaka apande juu kule, tena arudi chini, tunapoteza muda pasipokuwa na sababu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, kwa kuwa hii bandari inatoa mizigo na nchi jirani pia, nitoe angalizo, wenzetu wa Zambia wametengeneza sheria, hii sheria inataka mizigo yote inayosafirishwa kwenda Zambia iweze kutolewa na makampuni ya Kizambia yaani zile clearing and forwarding lazima ziombewe zikiwa Zambia, mana yake kampuni za Kizambia ndio ziweze kupata hizi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kana kwamba hiyo haitoshi mpaka makampuni ya usafirishaji pia yale ya logistic lazima na yenyewe ya kutoka Zambia yaweze kufanya hivyo. Maana yake sasa sisi hapa makampuni yetu ya clearing and forwarding hayataweza kupata kazi, lakini pia na makampuni ya logistic hayawezi kupata kazi, sisi tutabakia na barabara yetu kuharibika, makampuni yote yatafanya kazi huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kengele ya pili imegonga, mengine nitaandika kwa maandishi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Kwanza nimpongeze Waziri pamoja na Naibu Waziri na Wizara kwa ujumla kwa wasilisho zuri lakini pia kwa mwelekeo mzuri kwamba sasa tunaanza kuona dira namna nzuri ya kilimo chetu tutakavyokwenda kukupeleka.

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia kwa kuongelea zao la tumbaku. Zao la tumbaku sasa hivi limekuwa halina tija tena kwa mkulima, wakulima wetu sasa wanalima kwa mazoea maana yake hawanufaiki nalo tena. Kama tunataka kuwakomba wakulima wetu hawa lazima tujielekeze kwenye masoko ya uhakika. Makampuni ya ununuzi yanapokuja huwa yanaweka makisio ya kununua na kulima. Kwa hiyo, huyu mkulima wetu hata alime vipi kama atakuwa amelima zaidi ya yale makisio aliyowekewa maana yake tumbaku yake haiwezi kununuliwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi kwa wakulima wetu hawa wadogowadogo kwa mkulima mmoja wao wanaruhusiwa kulima heka mbili tu pekee lakini kwa gharama anayotumia kulima kwa heka mbili hana uwezo wa kulima heka tatu. Shida ni kwamba hata akilima kwa heka tatu maana yake ni kwamba tumbaku yake ambayo itanunuliwa ni ile ya heka mbili. Huyu mkulima ili kumsaidia maana yake lazima aweze kulima zaidi ya heka mbili kwa msimu ndiyo aweze kupata kipato cha kumtosheleza na aweze kupata faida. Namna pekee na tuishauri Serikali ili kuwasaidia wakulima wetu hawa ni kutafuta masoko ya uhakika, makampuni yawepo mengi ili makisio ya hawa wakulima yaweze kuongeza. Hii ndiyo njia pekee ambapo tunaweza tukawasaidia hawa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine kwenye suala hili la tumbaku ni haya madaraja yanayopangwa na makampuni kwa ajili ya wakulima wetu. Wakulima hawa wanapokuwa wamelima tumbaku yao wao wenyewe huwa wanai-grade sasa makampuni yanapokuja na yenyewe yanakuja tena kui-grade upya tumbaku ile. Kitengo hiki huwa kinapelekea sasa hapa katikati wale wanaokuja ku-grade kule kwetu wanaonekana kama Mungu amefika, akifika siku hiyo mkulima lazima umnyenyekee, umlishe kuku vizuri ili sasa aweze kui-grade tumbaku yako vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bila kufanya hivyo tumbaku yako inaweza ikawa kwenye grade nzuri lakini yeye akai-under grade. Bahati mbaya sana kwenye zao letu hili ukishindwa kuuza kwenye kampuni ile maana yake huwezi kuuza tena. Kwa hiyo, tunaishauri sana Serikali ione namna nzuri sana ya kukaa na makampuni haya au wanao-grade tumbaku wawe na watu wao lakini sisi kama Serikali pia tuwe na watu wetu waweze kuhakikisha kwamba hiki ndiyo kiwango ambacho kinatakiwa.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la tumbaku pia wafanyakazi wa haya makampuni na wenyewe wanajiingiza kwenda kulangua tumbaku hii. Wanachofanya ni kwenda kununua tumbaku hii kwa wakulima kwa bei ndogo ili baadaye na wao waweze kuja kuuzia makampuni ambayo wanafanyia kazi. Hawa wakulima wasipowauzia tumbaku hii wale wafanyakazi ndiyo baadaye wanashindwa kupata grade bora zaidi na wengine hawapati kabisa masoko katika kununua. Kwa hiyo, naishauri Serikali iweze kuangalia jambo hili.

Mheshimiwa Spika, nizungumze kidogo kwa Wilaya Chunya, lilianzishwa zao mbadala la tumbaku la korosho. Zao hili lililetwa miche, kwa maana Serikali ilitoa ruzuku kuleta miche hii, lakini ilikuja tu awamu ya kwanza baada ya hapo ile miche tena haikuja. Baadaye halmashauri na yenyewe ilijitahidi kutoa fedha zake kununua miche na kuwapatia wakulima wetu hawa lakini na wao wamefika hatua nao wameshindwa. Sisi wakulima wetu wa Wilaya ya Chunya wanashindwa kuipata hii miche mizuri zaidi ili wawekeze kwenye zao hili la korosho.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye zao hili la korosho kwa kuwa ni zao jipya Maafisa Ugani wetu ambao wapo kule Wilaya ya Chunya bado na wao hawajaweza kupata elimu ya kutosha kuhusu zao hili la korosho. Mimi niishauri Wizara kupitia TARI-Naliendele waweze kuleta wataalam wao mara kwa mara kwa Maafisa Ugani wetu hawa ili waweze kuwapa hii elimu na wao Maafisa Ugani wetu kwa kuwa ndiyo wanakaa kulekule na wakulima hawa waweze kuwapa hii elimu ya mara kwa mara. Hii itaweza kutusaidia sana na hili zao liweze kwenda vizuri zaidi. Sisi tunaamini zao mbadala la tumbaku ni korosho, kwa hiyo, lazima tuwekeze kwa kiasi kikubwa ili hili zao liweze kuwasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, pia nizungumizie suala la umwagiliaji. Wilaya yetu ya chunya tulipata bahati ya kuwa na skimu ya umwagiliaji katika Kata ya Ifumbo. Skimu hii ilianza zaidi ya miaka kumi iliyopita, ilianza kwa za ufadhili wa nje baadaye Serikali ikaja kutoa fedha zake lakini mara ya mwisho Serikali kutoa fedha mwaka 2013, fedha zilizowekezwa pale ni zaidi ya bilioni moja lakini mpaka leo tunasema zile fedha tulizitupa pale. Niiombe Serikali kupitia Wizara ya Kilimo iweze kuipitia hii miradi ambayo ilisimama kwa muda mrefu, ione tatizo lilikwamia wapi ili baadaye waweze kuweka fedha na lile dhumuni kubwa ambalo lillikuwa limekusudiwa kwa ajili ya kujenga hizi skimu liweze kuwasaidia wananchi wa maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Ifumbo tunaitegemea sana kwa Wilaya ya Chunya kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Skimu ile ikiweza kupata fedha za kutosha na ikianza kufanya kazi maana yake mbogamboga na vyakula vyote vinavyozalishwa kwenye skimu za umwagiliaji tutaweza kupata kutoka Kata hii ya Ifumbo. Wilaya ya Chunya ambayo tunaona kama kame nako tutaweza kupata mazao mengi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu sana inayogusa wananchi wengi. Kwanza niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri lakini kwa mipango mizuri sana iliyokuwepo kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tushukuru kwa namna ambavyo tumepata namba za wakandarasi ambao wanaenda kujenga umeme wa REA III na sisi wananchi wa Chunya kwa namna yake kwenye kata zote 20 tunaenda kupata umeme katika kata zote. Umeme huu utaenda kufika kwenye Vijiji cha Lupa Market, Kambi Katoto, Sipa, Lualage, Mwigi, Liheselo, Bitimanyanga, Mazimbo, Kalangali, Magunga pamoja na Shoga. Sasa hapa Chunya tutaenda kuwa tumewaka vizuri. Tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo anaenda kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mazuri anayofanya Waziri bado kwa Wilaya ya Chunya tuna changamoto ya umeme mdogo ambao unafika ndani ya wilaya yetu. Kwa kuwa tunaenda kupeleke umeme mwingi kwenye vijiji vyetu changamoto hii Wizara iweze kuichukua na kuitatua kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwenye Wilaya ya Chunya kama tunavyofahamu uchumi wetu mkubwa tunategemea uchimbaji kwa hiyo tuna viwanda vingi vidogovidogo ambavyo vinachenjua dhahabu maarufu kama co-elution. Viwanda hii vinazidi kujengwa kila siku umeme ambao wanautumia ni umeme mkubwa, sasa inafikia hatua watu wengine wanashindwa kutumia umeme huo inabidi wawashe majenereta ili kuweza kukidhi mahitaji ya umeme ambayo yanahitajika. Naomba tuone namna ambayo ni nzuri zaidi kuweza kuongeza umeme wa msongo mkubwa uweze kufika kwenye Wilaya yetu ya Chunya ili mahitaji haya yaweze kuwafikia wananchi wetu vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia umeme huu ambao unatoka kwenye kituo cha Mbeya unafika Chunya lakini pia unaenda wilaya jirani ya Songwe ambapo kule kuna mgodi mkubwa sana wa Shanta. Mgodi huu na wenyewe bado wanatumia umeme ambao unapita Wilaya ya Chunya, kwa hiyo, inafikia hatua umeme huu haukidhi mahitaji ya wananchi wa Wilaya ya Chunya. Kwa hiyo, naomba kama ikiwapendeza na bajeti ikiwepo tuweze kujenga power station plant pale kwenye Mji wa Makongorosi ili sasa umeme huu uweze kugawiwa vizuri kwenye Miji ya Chunya, Mkwajuni, Lupa mpaka Kambi Katoto ili sasa kuweza kukidhi mahitaji vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na vijiji hivi kupata umeme lakini pia tatizo kubwa tunalo kwenye REA awamu II, vijiji kadhaa viliweza kupata umeme lakini umeme ambao uliweza kufika ilikuwa takribani kilometa moja au moja na nusu, kwa hiyo, wananchi hawa walikuwa wanaonjeshwa tu ule umeme. Unakuta kwenye kijiji kuna nyumba 20 mpaka 25 ndizo zilizopata umeme, wananchi wengi wameomba na wamelipia lakini mpaka sasa hivi bado hawajaweza kupata umeme. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ni msikivu sana naomba tuone namna bora xaidi kushughulikia suala hili. Pamoja na mambo mazuri yanayoendelea tuweke bajeti ya kutosha ili vile vijiji ambavyo vilikuwa havijaweza kufikiwa kwa maana kuongeza kwenye mitaa umeme huo ziweze kufikiwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna vijiji ambavyo vilikuwa kwenye mradi wa TANESCO havikuwa kwenye mradi wa REA kama Igundu, Sangambi, Godima pamoja Itumbi. Mradi huu ulianza zaidi ya miaka mitatu na nusu iliyopita toka 2018/2019 nguzo zimefika kwenye vijiji hivi lakini mpaka leo umeme haujaweza kuwaka. Kwa hiyo, tuiombe Wizara kuona namna ambavyo tunaweza tukapata vifaa kwa maana ya transformer pamoja na mita ili sasa wananchi wale waweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, vijiji nilivyovitaja hapa ni vikubwa lakini umeme haujaweza kuwaka na kuna baadhi ya vitongoji vimepata lakini vijiji havijapata. Kwa hiyo, malalamiko ya wananchi yamekuwa makubwa na wanaanza kuona kama Serikali hii haiwajali. Kwa hiyo, niombe sana wakati Mheshimiwa Waziri ana wind-up aone namna iliyokuwa bora zaidi na hivi vijiji pia viingizwe kwenye mpango ikiwezekana kwenye hii REA III ili na wao waweze kunufaika na umeme huu na baadaye waweze kuona matunda mazuri zaidi ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshmiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia; na nitajielekeza sana kwenye miundombinu. Nitapenda nianze na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa barabara zetu hizi kila mwaka Serikali imekuwa na mipango na imekuwa inatenga fedha kwa ajili ya kuwezesha barabara hizi kuweza kujengwa, lakini kiasi cha fedha kinachotengwa ni kidogo sana ukilinganisha na kazi ambayo inatakiwa kufanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani barabara ya kilometa 100, lakini unakuta inatengewa shilingi bilioni mbili kwa mwaka. Sasa hapo tunakaa tunajiuliza: Je, itatuchukua muda gani mpaka barabara hii kukamilika? Mwaka wa fedha uliopita ambao tunaendelea nao, kuna barabara ambazo zimetengewa fedha, lakini ni kiasi kidogo sana na nyingine nyingi hazijaanza kujengwa na ndiyo tunaelekea kumaliza mwaka wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuiombe Serikali iweze kuona namna gani ya kuzikamilisha hizi barabara na kuzitengea fedha za kutosha. Zikitengwa fedha za kutosha walau sasa wananchi wetu nao wataweza kunufaika na kwa muda mfupi wataona barabara zao zinajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, kwenye upande wa barabara, tuishauri Serikali iweze kutenga, kuwa na mipango ya muda mrefu kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Leo hii kila mzungumzaji hapa ni kuhusu habari ya mradi kukwama kwa sababu ya fidia. Sasa inakwama kwa sababu hatuna mipango ya muda mrefu. Sisi mipango yetu ni ya muda mfupi. Tunaishauri Serikali hasa kwenye upande wa miundombinu iweze kuwa na mipango ya muda mrefu; miaka 50 mpaka miaka 100 mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunazungumza barabara za mzunguko. Tumeona juzi tukisaini hapa Dodoma barabara za mzunguko. Hizi barabara za mzunguko tunataka mipango yake iende kwenye miji na majiji karibu nchi nzima. Kila mkoa huwe na mipango ya miaka 50 au 100 mbele ndiyo tutaweza kutoka hapa tulipo tuweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, leo kwenye Jiji la Mbeya kuna changamoto ya barabara. Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kutengeneza barabara ya bypass. Sasa badala ya kujenga barabara ya bypass kwanini isiweke mpango kujenga sasa barabara za mzunguko ambazo zitakaa kwa muda mrefu zaidi? Hata kama ujenzi wake hautaanza sasa hivi, lakini tuna imani ndani ya miaka 10, 15, 20 hizi barabara zitaanza kujengwa; na kwa kuwa tayari kunakuwa na hiyo mipango ya muda mrefu ambapo tunakuwa tumeshirikisha majiji kwenye masterplan zao, fedha itakayokuwa inapatikana tutaendelea na ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ile bypass ya Uyole kwenda kutokezea Songwe, fedha yake imeshatengwa tayari. Sasa badala ya kuanza kujenga bypass, plan iwekwe barabara ya mzunguko ili hii fedha iingie sasa kuanza kujenga barabara ya mzunguko badala ya kujenga barabara ya bypass. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzungumze sasa pia kwenye upande wa mizani zetu. Leo tunaona magari yanayotoka kuanzia Dar es Salaam kwenda mikoani mpaka nchi jirani, kila kwenye mizani inapopita inatakiwa isimame. Sasa unajiuliza leo, tenki la mafuta linaloondoka Dar es Salaam linaenda Mwanza, Bukoba au nje ya nchi, lina sababu gani ya kupita kila mzani na kupima uzito? Wakati tenki la mafuta likishajazwa kutoka Dar es Salaam likapimwa, lina lita labda 30, haliwezi kupungua njiani mpaka linafika Bukoba au Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuone namna iliyo bora zaidi, hii mizani yetu, baadhi ya magari mengine kama ya matenki yanaweza yasipite kwenye mizani. Hii itaweza kusaidia sana kupunguza foleni. Haya matenki mengi yameshafunga vehicle tracking system, hata ule mfuniko tu ukiugusa, tayari unapiga kelele kule. Maana yake hawezi kufanya chochote njiani hapa. Kwa hiyo, magari kama ya matenki ya mafuta yapime yanapoanza kuondoka na mwisho wa safari ili kurahisisha na kupunguza msongamano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hata kwa upande wa mabasi hasa ya safari ndefu; basi linatoka Kigoma, Mbeya au Mwanza; kila kituo ikipita inapima uzito. Inapita Mwanza, inapima uzito; inafika Morogoro, inapima uzito; inafika Mikese, inapima uzito. Sasa akifika Mikese akapima uzito, hana sababu tena ya kupima uzito pale Vigwaza, tunaongeza foleni isiyokuwa na sababu. Kwa hiyo, tuone namna ambavyo Wizara na Serikali itayachukua haya iweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, naunga mkono hoja na ninaomba sana Wizara iyachukulie haya na iweze kuyafanyia kazi. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango huu wa Bajeti wa Mwaka ujao wa Fedha kama ulivyowasilishwa na Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa ambayo imeletwa hapa ya mpango tumeona ukuaji wa uchumi katika kipindi cha Januari mpaka Juni 2022. Tumeona uchumi wetu umekua kwa asilimia 5.2 katika nusu mwaka hii na kuna sekta ambazo zimeongoza katika ukuwaji huu ni sekta ya maji safi na maji taka ambayo imekua kwa asiliamia 10.7, bima asilimia 10, umeme asilimia 8.5, madini na mawe asilimia 7.1 na nyinginezo. Ukuaji huu kwa robo hii umekwenda vizuri lakini ukuaji huu hauendani sambamba na mfumuko wa bei ulivyo. Tunaona kipindi cha Agosti, 2022 mfumuko wa bei kwenye upande wa vyakula na vinywaji ilikuwa ni asilimia 7.8 ambapo hii ni ongezeko kubwa, ambapo kipindi cha Agosti mwaka uliopita mfumuko wa bei ulikuwa 3.6 kwa hiyo, mfumuko wa bei umekwenda mara mbili zaidi ya hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachotaka kusema ni nini? Nikwamba uchumi wetu unakua lakini auendi sambamba na mfumuko wa bei, kitu ambacho ni hatarishi sana kwenye uchumu wa nchi yetu. Nikiangalia kwenye mpango hapa hakuna namna yeyote ile yakuweza kukabili mfumuko huu wa bei. Tunaacha tu nature iweze ku-take place kitu ambacho ni kibaya, niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, uangalie wewe pamoja na Wachumi wa kwako ambao amekuzunguka, namna ambavyo tuwe na mipango endelevu ya kuhakikisha kwamba mfumuko wa bei huu tunaenda kwenda kuutatua kwakuwa na mipango ya muda mfupi na mipango ya muda mrefu, bila hivyo tutakuwa hatuwezi kufika kule tunakotaka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango huu wa Bajeti, tumeona kwenye msimu wa 2021/2022 uzalishaji wa chakula ulikuwa tani milioni 17.4 na kwenye mpango huu wa bajeti wamekadiria mahitaji ya chakula ya kwetu sisi hapa ni tani milioni 15. Hata hivyo hawajaonesha namna ambavyo uzalishaji wa kwetu sisi utakavyokuwa. Sasa tuna mipango mingi ambayo inakwenda, tunawekeza kwenye kilimo lakini hatuna mpango wa kuonesha kwamba uwekezaji wetu huu utazalishia kiasi gani? Kitu ambacho kwenye uendeshaji wa uchumi wa kwetu tunakuwa tunakwenda kwa sababu tu tulitakiwa twende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tu Wizara fedha, pamoja na Wizara ya Kilimo, muweze kukaa muwe na mipango kuonyesha kwamba kiasi ambacho tunakwenda kuwekeza kwenye upande wa kilimo tunategemea uzalishaji wetu utakua kiasi hiki na matumizi yetu yatakuwa kiasi hiki na hii ziada itatuwezesha sasa kuweza kuuza nje, kama mnavyojua, fedha nyingi ambazo tumeweza kuwekeza kwenye bajeti ambayo imepita tunaimani utekelezaji kwenye kilimo ukienda vizuri uzalishaji utakua zaidi na ukikua zaidi hii ni fursa kwetu kwa hizi bidhaa zetu za mazao kwenda kuuza nje ya nchi na tukaweza kupata fedha za kutosha na badae uchumi wetu ukakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tukifanye kilimo chetu hiki kuwa cha kibiashara. Tumekuwa tunakizungumza kwa nadharia kwamba tunawekeza kwenye kilimo lakini tunaenda kufanya kilimo hiki kwa mazao ya kuweza kujikimu. Tutoke hapa tulipo twende kwenye mazao ya kibiashara ili haya tunayoyasema yaweza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze pia kwenye upande wa Miundombinu. Naona hapa kwenye bajeti na kwenye mpango huu wa bajeti kuna mambo makubwa yameelekezwa kwenye miundombinu. Nichukulie mfano kwenye SGR tunajenga hapa, tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kujenga na mambo yanaendelea vizuri lakini bado hatujawa na mpango endelevu kuweza kuhakikisha kwamba reli hii itaweza kuwa na tija kwetu sisi. Leo tunajenga reli hii kwenda Mwanza, kule Mwanza hakuna mzigo wa kututoa Dar es Salaam kutupeleka Mwanza, sasa hivi hapa ili reli iweze kutulipa, iweze kulipa tunapoweza kusafirisha mizigo mingi na ya kutosha na mizigo pekekee ambayo inaweza kututosheleza na uchumi wetu kuweza kukua ni kututoa Dar es salaam kwenda Kigoma na baadae DRC ndiyo inachukua mzigo wa asilimia Sabini ya unaopita Bandari ya Dar es salaam lakini sisi tumeelekeza reli yetu kwenda Mwanza kusafirisaha abiria badala ya kupeleka Kigoma ambapo tutapeleka kule mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Serikali iweze kupitia upya ione namna nzuri zaidi reli hii sasa tuwekeze nguvu ambayo itapeleka mizigo hii na badae itaweza kutusaidia. Hii ni reli ya kati lakini pia kwenye mpango tuone namna ambavyo tunaweza tukaiboresha reli yetu ya TAZARA. Reli ya TAZARA siyo kuboresha tu miundombinu peke yake. Reli hii tuone namna ambavyo, namna ya uwanzishwaji wake, namna uendeshwaji wake baina ya hizi nchi mbili. Tukiweza kutatua hili ndivyo ambavyo baadae tutaenda kwenye miundombinu na baadae tuone namna ambavyo itaweza kutusaidia. Kuna mizigo mingi inatoka hapa inaenda Zambia, kuna mizigo mingi inatoka Zambia shaba inatoka kule inakuja Dar-es-Salaam leo hii awatumia TAZARA wanatumia barabara, barabara hizo wanazotumia zinaishia kwenda kuharibu barabara zetu kwa malori haya na sisi tunakuwa hatunufaiki wakati reli tunayo na kusudi kubwa la reli lilikuwa kuhakikisha kwamba miundombinu hii inakua vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda wenyewe siyo rafiki. Nitakuandikia kwa maandishi ili niweze kuleta mchango wangu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami kupata nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Madini.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya kuhakikisha kwamba sekta hii ya madini inazidi kukua siku hadi siku. Pia niipongeze Wizara kwa kazi nzuri ambayo inaendelea kuifanya katika kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waendelee kushiriki kwenye uchumi wa madini ambao unawawezesha kushiriki kwenye uchumi huu na katika kujitafutia riziki na kuweza kulipa kodi.

Mheshimiwa Spika, lakini wachimbaji wadogo hawa wameweza kuendelea na kuwezeshwa katika kupata maeneo ya kufanyia kazi, kupata ama kupewa leseni kwa maeneo ambayo yanaonekana yana madini. Lakini pia tuwapongeze Wizara kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya katika kutoa semina mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo tumeona kwamba kazi nzuri inaonekana kufanyika, na kazi hii inayofanyika na Wizara inasababisha hata maduhuli ya Serikali kuongezeka. Tukiangalia mwaka wa fedha uliopita kiasi cha fedha ambazo kiliingizwa na mwaka huu wa fedha zaidi ya asilimia nne zimeongezeka. Hii ni kazi kubwa sana na kwa hiyo Wizara maana imechangia kwenye Pato kubwa la Taifa.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na kazi kubwa hii nzuri inayoendelea kufanyika tunawapongeza pia Wizara kwa kuhakikisha kwamba wanaendelea kuzishirikisha taasisi za kifedha ambazo zimeonana na wachimbaji wadogo ili kuhakikisha kwamba wanapata mikopo midogo midogo itakayowawezesha kupata vifaa na vifaa hivi vinawawezesha wao kuweza kurahisishia uchimbaji wao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na taasisi za kifedha kuwapatia wachimbaji wadogo lakini bado masharti ya taasisi hizi yamekuwa magumu kuwawezesha wachimbaji wadogo hawa kuweza kunufaika. Tuiombe Wizara, pamoja na kwamba wameendelea kufanya kazi kubwa katika hili lakini pia waendelee kuongea na taasisi za kifedha hizi ili benki na taasisi nyingine walegeze haya masharti waliyonayo ili kuwawezesha wachimbaji wengi wadogo hasa wale wa chini kabisa waweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, leo hii wachimbaji wadogo ambao wananufaika ni wale ambao wanaweza wakapata mascaveta, mabuldoza pamoja na ma-tipper, yale makubwa.

Mheshimiwa Spika, leo hii wachimbaji wadogo ambao wananufaika ni wale ambao wanaweza wakapata ma-excavator, bulldozer pamoja na tipper kubwa, lakini tunataka tushuke chini zaidi kwa wale wachimbaji wadogo ambao wanaweza wakapata fedha ya kuwanunulia makarasha, wakapata fedha ya kujenga plant na vitu vingine kama hivyo ili mzunguko huu wa fedha uweze kwenda kwa wachimbaji wengi zaidi na wao pia waweze kujiwezesha kiuchumi waweze kulipa kodi zitakazoisaidia nchi yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo pamoja na kuwezeshwa huko wachimbaji lakini taasisi ya GST iendelee kufanyakazi yake kuhakikisha kwamba inaendelea kufanya tafiti hizi na tafiti hizi ziweze kushuka kwa wachimbaji wengi wadogo na walio wa chini.

Mheshimiwa Spika, leo hii tafiti nyingi ambazo zinafanyika zinaishia kwenye makabrasha ofisini ninaomba sana taasisi ya GST iweze kufanya kazi hii na ihakikishe inatohoa kwenye lugha nyepesi na rahisi ambazo zitaweza kuwafikia wachimbaji wetu wa kule chini, ziweze kufika kwenye ngazi za Mkoa, kwenye ngazi za Wilaya na wachimbaji wetu wa kule Nyang’hwale wachimbaji wetu wa Chunya, wachimbaji wetu wa Matundasi Sangapi na maeneo mengine waweze kuzipata hizi na waweze kunufaika pamoja na hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona taasisi ya GST ilichukua ushauri wetu, mwaka jana tuliwaambia hapa waanzishe maabara kwenda kwenye Mikoa yetu, nashukuru sana nimeona kwenye taarifa hapa maabara hizo sasa zimeanza kuanzishwa tumeona Geita kule zimefunguliwa maabara hizi. Ninaomba sasa Serikali kwa kuwa imeanza kufungua maabara hizi na sisi watu wa Nyanda za Juu Kusini, watu wa Mkoa wa Mbeya na hasa Wilaya ya Chunya ambako ndio wachimbaji wakubwa sana wa dhahabu tuhakikishe kwamba maabara hizi sasa zinaenda kuanzishwa haraka zaidi ili wachimbaji wetu hawa wapeleke sampuli zao pale, wawe na uhakika na kile ambacho wanaenda kukichimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo pia hata ule uchorongaji, nimeona hapa wameagiza mashine za uchorongaji, mashine hizi zitakapofika tuhakikishe kwamba zinaweza kuwafikia wachimbaji wetu hawa.

Mheshimiwa Spika, wachimbaji wengi wanachimba sasa hivi katika hali ya kubahatisha hasa wale wachimbaji wadogo, leo GST wanasema kwamba wanaboresha kanzidata yao ya miamba ni jambo zuri sana, lakini kuboresha peke yake haitoshi! Waboreshe hizi kanzidata na taarifa hizi za miamba ziweze kuwafikia wachimbaji wengi wadogo, wachimbaji hawa watakapoweza kupata taarifa ambazo ni nzuri na sahihi ndivyo watakavyoweza kuongeza uzalishaji wao na wakiongeza uzalishaji wao ndivyo ambavyo wataweza kulipa kodi kwa Serikali na Serikali itazidi kupata mapato na tutaona nchi yetu itazidi kupaa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia …

SPIKA: Sekunde thelathini.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, basi nitaleta mchango wangu kwa maandishi lakini ninapongeza na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ambayo tunategemea ukuaji wake na mchango wake ni mkubwa sana kwenye maendeleo ya nchi yetu hii na kwenye Pato la Taifa. Nakupongeza Mheshimiwa Waziri na wataalam wako wote Wizarani; mnafanya kazi kubwa na nzuri na kila mwananchi wa Tanzania anaiona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini imeendelea kukua miaka hadi miaka. Kwenye uchangiaji wa Pato la Taifa pia imeendelea kufanya vizuri na ukuaji wake kila mtu anauona. Tunawapongeza sana kwa hili na kwa kweli tuna imani kwamba ile mipango ya kufikia zaidi ya asilimia kumi na itaweza kufika kwa wakati na pato lake kwa Taifa litakuwa linaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapowapongeza hawa lazima pia tuwapongeze wachimbaji wadogo, wachimbaji wetu wadogo nao pia wameendelea kufanya vizuri. Wameweza kuendelea kuongeza uzalishaji na kuweza kuchangia kwenye pato la Taifa. Katika madini yote ambayo yanapatikana, asilimia 40 yanapatikana kutoka kwa wachimbaji wadogo; lazima tuwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachimbaji wadogo hawa ambao wanachangia zaidi ya asilimia 40, maisha yao ambayo wanaishi hayaakisi kile ambacho wao wanakizalisha. Na hayaakisi hivi kwa sababu ya kodi nyingi na ada mbalimbali ambazo wao wanatozwa. Leo hii baada ya Wizara na mfumo mzima wa uchimbaji kuwa vizuri, sasa taasisi nyingine zote za kimapato zinaangalia uchimbaji huu mdogomdogo kama vyanzo vyao vya kutafuta mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapozungumza kodi ambazo zinamkabili mchimbaji mdogo ni nyingi sana kiasi kwamba inasababisha mchimbaji huyu anazalisha kwa nguvu kubwa sana lakini tija kwake yeye binafsi inakuwa ndogo sana. Niombe kama Serikali muweze kukaa muone namna bora zaidi za kumpunguzia kodi mchimbaji huyu mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi hizi pia ziweze kukaa ziwe na utaratibu mzuri zaidi wa kumuwezesha badala ya kuwa wao kazi yao ni kuzuia. Leo mchimbaji mdogo anapoanza kufanya kazi yake zinakuja taasisi nyingine, badala ya kumsaidia, kumshauri vizuri, wao kazi yao wanakuja pale kumuwekea vikwazo ambavyo vinasababisha mchimbaji huyu ashindwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anakuja kudai jambo dogo tu anakwambia sasa hapa tunasimamisha uzalishaji wako mpaka ulipe hii kodi au ulipe hii ada. Na hiyo inakwenda kwenye ngazi kuanzia ya TRA wenyewe, hizi taasisi zinazozunguka mpaka kwenye ngazi ya kijiji. Leo mpaka mtendaji wa kijiji anafika pale anakwambia kwamba hujalipa service levy au ada hii hapa ndogo, uzalishaji usimame mpaka ulipe. Namna hii hatutaweza kumkomboa mchimbaji mdogo, lazima hizi sheria pia ziweze kubadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo upande wa STAMICO. Wamefanya kazi nzuri, tunawapongeza sana. Kutoka kuwa shirika mfu ambalo lilikuwa linataka kufutwa mpaka ilifikia hatua wanashindwa kulipa mishahara yao. Lakini sasa hivi wameweza kupiga hatua kubwa sana na wameweza kuzalisha faida ya zaidi ya bilioni 70 kwa mwaka; hii ni hatua kubwa sana. Tuwapongeze na tuwape moyo, wanaweza wakafanya mambo makubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri, Serikali iliangalie sana Shirika la STAMICO, linaweza likafanya miradi mikubwa na ya kimkakati na uzalishaji ukaongezeka na uchangiaji kwenye pato la Taifa ukawa mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza habari ya STAMICO, tuangalie sheria ya uanzishaji wake. Tunaweza tukaibadilisha sheria ya uanzishaji wa STAMICO na yenyewe ikawa wasimamizi badala ya Serikali kwenye ule uchimbaji wa madini mwingine wowote ambao Serikali inaingia, badala ya kuanzisha kampuni ndogondogo za kila siku, yenyewe sasa ikasimama badala ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikwenda ikulu pale kushuhudia makubaliano na kusaini mikataba lakini kulikuwa na makampuni mbalimbali ambayo yameanzishwa na Serikali ambayo yameingia ubia na hayo makampuni ya nje kwa ajili ya uzalishaji. Sasa badala ya kuanzisha makampuni madogo madogo mengi kila tunapotaka kuanza uchimbaji sasa tuipe jukumu hili STAMICO ili waweze kuifanya kazi hiyo. Nina imani STAMICO wanaweza wakafanya kazi hiyo vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia kwenye STAMICO hapa namna ambavyo wameendelea kwenda na ubunifu na sasa wamekuja na mkaa rafiki. Ni teknolojia ambayo wameanza nayo na ni nzuri, na ikiendelea hivi itasaidia sana mkaa huu kwenda kuwa mbadala wa ile mikaa ambayo inatumiwa ya miti na kuhakikisha kwamba mazingira yetu yanaendelea kuwa safi na salama kwa muda mrefu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mkaa rafiki ambao unazalishwa na STAMICO, hii teknolojia ambayo wao wameifanya, mimi nishauri kwamba badala ya kuendelea nayo wao waiuze kwa Taasisi nyingine kama SIDO au VETA ili wao sasa waje waipeleke kwenye jamii huku chini na baadaye uzalishaji wake uweze kufanyika huko. Badala ya wao kuibuni na wao pia waendelee kuweza kuzalisha na kuuza huko mtaani. Wao wabakie na mambo makubwa makubwa kama ambayo wanaendelea nayo sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakiendelea na mambo makubwa haya ambayo sisi tunayasema ili kuweza kuifanya STAMICO ikue kwa uwanda mpana zaidi. Leo mfano tunazungumza makaa ya mawe, haya makaa ya mawe ndiyo ambayo leo yanazalisha umeme. Je, sisi kutumia STAMICO tunaisadia vipi hii nchi yetu STAMICO iweze kuzalisha umeme mkubwa zaidi uweze kuingia kwenye Gridi yetu ya Taifa ili uweze kutusaidia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kwamba sasa badala ya STAMICO kwenda kuzalisha hii miradi mingine midogo midogo, ijiwekeze kwenda kwenye kuzalisha umeme uwe mkubwa zaidi, tutoke sasa hivi tunataka tuzalishe kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere megawati elfu mbili na, twende kupitia makaa ya mawe chini ya STAMICO tufikirie miaka 10, 20 mbele uzalishaji wa umeme uweze kufikia megawati 10,000 mpaka 15,000 kupitia makaa ya mawe. Jambo ambalo linawezekana, ni kuwawezesha tu STAMICO waweze kufanya kazi hiyo vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa STAMICO wakati Mheshimiwa Rais anapokea Ripoti ya CAG tuliona alisema kuna baadhi ya mashirika na taasisi nyingine yamekuwa hayana faida kwa sasa hivi. Tutolee mfano NDC; NDC imekuwa inasimamia Mradi ule wa Liganga pamoja na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu imekuwa ni stori ya miaka nenda rudi, niombe sana kuishauri Serikali iweze kubadilisha sheria ili ule Mradi wa makaa ya mawe wa Mchuchuma uweze kutoka kule ulipokuwepo kwa maana ya Wizara ya Viwanda na Biashara chini ya NDC uweze kuja sasa Wizara ya Madini na isimamiwe na STAMICO ili sasa uchimbaji uweze kufanyika na baadaye iweze kuleta tija kubwa sana kwenye nchi yetu hii. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeisaidia STAMICO na itakuwa ina miradi mikubwa na sisi tutakuwa tumeweza kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie habari ya GST, GST pamoja na kazi nzuri ambazo wanaendelea kufanya bado wanapata bajeti ndogo na mazingira yao ya kazi siyo mazuri. Tukiweza kuwekeza vizuri kwenye utafiti maana yake wachimbaji wetu hawa wadogo wadogo na wa kati wataweza kufanya kazi zao kwa kujua nini ambacho wanakifanya, nini ambacho watakipata chini badala ya sasa hivi tunafanya uchimbaji wa kupiga ramli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwawezeshe hawa GST waweze kufanya kazi yao vizuri zaidi, wawe na vifaa vya kutosha. Leo wameagiza mitambo ya kuchoronga mitano na mingine inakuja, ni mwanzo mzuri lakini tuweze kwenda mbali zaidi na taarifa zao za GST ziweze kuwafikia wachimbaji wadogo hawa, ndiyo itakuwa ukombozi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumza hapa kwenye mapato haya ambayo yamepatikana ya uchimbaji asilimia 40 yamezalishwa na wachimbaji wadogo lakini wachimbaji wadogo hawa hatujaweza kuwawezesha vizuri kuhakikisha kwamba uchimbaji wao utakuwa na tija na kuweza kuwasaidia.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kasaka, malizia mchango wako.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kwa kuweza kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii, moja kati ya Wizara muhimu sana kwenye ustawi wa nchi yetu, kwa namna ambavyo inaendelea kufanya kazi vizuri. Lakini pia niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri hakika anafanya kazi vizuri sana na sisi kama vijana wameendelea kutuheshimisha kwenye taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo ambazo tunawapa Wizara na Wizara hii ukizingatia kwamba ndiye mkombozi wa wananchi wengi, hasa wakulima wadogowadogo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba ustawi wa chakula katika nchi yetu unaendelea kuwa imara zaidi. Na ustawi wa chakula katika nchi yetu unategemea sana wakulima hawa wadogowadogo ambao takribani wanachukua asilimia 70 ya Watanzania wote. Hivyo tuweke jicho la kipekee kwa wakulima wadogowadogo hawa. Tunashukuru Serikali kwa kweli, tumeona ilileta ruzuku ya mbolea ambayo imepelekea wakulima wetu wadogo hawa uzalishaji wao kwenda vizuri zaidi na uhakika wa chakula kwa wananchi umekuwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mbolea hii kuwekewa ruzuku kumekuwa na changamoto ya mbolea hii kuweza kufika kwa wakati. Mbolea kwa wakulima wetu imechelewa sana kwenye msimu uliopita. Mbolea ya kupandia imeweza kufika mwezi wa 12 mpaka mwezi wa kwanza, hali ambayo ilisababisha wakulima wetu wengi, hasa wadogo hawa, kuweza kupata changamoto ya kuweka mbolea hii ya kupandia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai na nitoe wito sana kwa Serikali ihakikishe mbolea hii ya ruzuku inafika kwa wakati kwenye maeneo husika ili wananchi wetu wengi hawa waweze kunufaika, na hasa ukizingatia na maeneo tunatofautiana kutokana na msimu. Sisi watu wa Nyanda za Juu Kusini tunajua kwamba msimu wetu ni kuanzia mwezi wa 11 na 12 ndipo tunapanda; lakini maeneo ya kaskazini huko pia wana msimu wao, na ile mbolea iweze kufika kwa wakati ili wakulima hawa waweze kunifaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la bei yake; mbolea hii imakuja kwenye package ya kilo 50. Wakulima wetu wanauwezo wa hali tofauti ya kununua mbolea hii. Tuiombe serikali kupitia Mheshimiwa Waziri iongee na wale mawakala wanaoleta mbolea hii ili waweze kuweka kwenye parkage tofautitofauti, kuanzia kilo 50,20,10 mpaka kilo tano, ili hata mkulima ambaye analima bustani nyumbani kwake, anayelima matuta matano nyumbani kwake aweze kununua mbolea hii na aweze kunufaika nayo kwa uzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili mbolea hii kwenye maeneo mengi imeweza kufika kwenye makao makuu ya wilaya. Sisi ndani ya Wilaya yetu ya Chunya ilifika makao makuu ya wilaya; na sisi kama unavyojua, kwa jiografia, kwa ukubwa wa Wilaya ya Chunya ukienda kwenye Kata za mwisho za Kambi Katoto na Mafyoko kule ni takribani kilometa zaidi ya 200 kutoka Makao Makuu ya Chunya Mjini. Na bahati mbaya sana mbolea hii wale mawakala hawakuweza kuifikisha kule, kwa hiyo ilipelekea sasa upatikanaji wa mbolea hii kuwa ni wa gharama kubwa ambayo wananchi wetu wengi walishindwa kuipata kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa Wizara, kwenye Wilaya yetu ya Chunya na baadhi ya maeneo mengine ipeleke mbolea hii. Si makao makuu ya wilaya peke yake bali na kwenye baadhi ya maeneo ya centers zile kubwa kubwa ili wananchi wetu hawa wengi waweze kunufaika sawasawa na mbolea hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie suala la zao la tumbaku. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali kwa ujumla chini ya Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kweli wameweza kusikia kilio cha Wabunge. Zao la tumbaku ambalo lilikuwa ni kilio kwa wakulima sasa hivi limekuwa neema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masoko sasa hivi yanafunguliwa, huko sasa hivi ni chereko chereko, sasa wanamwimba Mheshimiwa Bashe, wanamwimba Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ambayo wanaifanya. Naomba sana, kampuni ambazo zimeletwa kwenye msimu huu, ambazo zinaendelea kufanya kazi ziendelee kufanya kazi vizuri na zilindwe. Vilevile, ikiwezekana kampuni nyingine pia ziweze kuja ili ushindani uweze kuwepo na baadaye mkulima aweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana wanaposhindana sokoni kwa wakulima ndivyo bei inavyokuwa nzuri zaidi na wakulima wetu hawa wanaweza kunufaika. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kwenye upande wa tumbaku, kama yalivyokuwa mazao mengine, tumbaku ni moja kati ya zao ambalo halijapata mbolea ya ruzuku. Niombe sana kupitia Wizara hii na Serikali kwa ujumla ione namna ya kuweka ruzuku ya mbolea kwenye zao hili la tumbaku ili hawa wakulima wetu nao waweze kunufaika kama ambavyo wakulima wengine wa mazao wanaweza kunufaika kupitia kilimo hiki hili litaweza kutusaidia sana. Lakini bei yake, wakati msimu huu wa mbolea unaendelea; mbolea waliyoleta mara ya kwanza ilikwisha. Walipoleta mbolea mara ya pili walileta mbolea kwa wakulima wa tumbaku ikiwa ina nembo ya mbolea ya ruzuku, hali ambayo imeweza kuleta mkanganyiko mkubwa sana kwa wakulima wetu. Hii ni kwa sababu mifuko ina nembo inayoonesha kwamba hii mbolea ni ya ruzuku lakini wao wanauziwa kwa bei ambayo si mbolea ya ruzuku. Hali hii imewanyong’oneza sana wakulima wetu kwa sababu sasa hivi imeleta hali ya sintofahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri anapokuja kuhitimisha uje utupe na majibu. Kwamba ile mifuko ambayo imekuja ina nembo ya mbolea ya ruzuku je, wakulima hawa watalipa kwa bei ya ruzuku au watalipa kwa bei ambayo itaendelea kuwanyonya wakulima wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu nizungumze ni suala la block farming au BBT. Sisi Wilaya yetu ya Chunya ni moja kati ya wanufaika wa mpango huu wa BBT kwa sababu tuna eneo la takribani hekta 47,000 ambalo limeshatengwa kwa ajili ya mpango huu. Mpango ni mzuri na tunapongeza Serikali kwa kuja na mpango huu tuna Imani kubwa sana mpango huu ukitekelezeka vizuri utakuwa ni mkombozi kwa nchi yetu na kuifanya Tanzania kuwa hub ya chakula kwa nchi zote za Afrika Mashariki na ikiwezeanika mpaka nchi zote mpaka Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linavyokuwa linakwenda lazima pia tuweze kutoa maangaliazo ambayo tunakuwa tunayaona. Moja kati ya mambo ambayo sisi tunaishauri Serikali, Serikali imeweka utaratibu mzuri wa kuwachukua vijana na kwenda kuwapekea kwenye kambi, mpango ni mzuri. Lakini, mnapochukua vijana hawa na kwenda kule kwenye kambi kule pia tuweze kuangalia vijana ambao wao tayari wamesha jiajiri kwenye kilimo hiki, tuweze kuwapa kipaumbele. Hawa vijana ambao tutawapa kipaumbele wataweza kutusaidia sana kwenye maeneo yale pale ili na wao waweze kunufaika. Hata benki huwa wanamkopesha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana…

MHE. MASACHE N. KASAKA: …mtu ambaye tayari anafanya biashara, sisi wale ambao tayari wameshaaanza kulima tukiwawezesha hii itaweza kuwasaidia na wao watazalisha kwa wingi zaidi na baadae tuwachukue hawa ambao tumewapeleaka…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Njelu Kasaka muda wako umekwisha.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana ya maji ambayo tunasema maji ni uhai. Nasi watu wa Chunya tunaitegemea sana Wizara hii kuhakikisha kwamba mji wetu unakuwa na maji ya kutosha. Tuna imani kubwa sana na Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake wote wa Wizarani, wakiongozwa na Naibu Waziri. Pia tumpongeze Mheshimiwa Rais, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba anatoa fedha ya kutosha ili waweze kufanya kazi yao vizuri sana. Tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, kwenye Wilaya yetu ya Chunya, katika Mkoa wa Mbeya sisi ndio tunapata wastani wa maji ya chini sana. Sisi tunapata maji kwa wastani wa asilimia 40, ambayo ni kiasi kidogo sana ukilinganisha na mikoa mingine na ndani ya Mkoa wetu wa Mbeya. Kwa hiyo, hili jambo ambalo linafanyika hapa lazima tuliseme ili kuhakikisha kwamba maji yanapatikana ndani ya Wilaya ya Chunya. Tuwapongeze kwa kweli kwenye upande wa RUWASA, wanafanya kazi yao vizuri sana. Kuna miradi Chunya inaendelea ambapo pesa zinaletwa pale, na miradi mingine imeweza kufanyiwa kazi. Kwa hiyo, tunapongeza kwa kazi bora inayofanywa. Tunampongeza Engineer Hans pamoja na Engineer Ismail kwa ushirikiano wao, juhudi zao zinaonekana na wananchi wanaona kazi ambayo inafanyika.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi hiyo ambayo inaendelea kufanyika, tunashukuru pia Serikali kwa kutuletea mtambo wa kuchimba maji kwenye Mkoa wetu wa Mbeya, na gari hili limeweza kufanya kazi kwenye Wilaya ya Chunya. Tayari katika vijiji 14, vijiji vinne vimeshafanyiwa kazi. Kijiji cha Itumbi wameshachimba maji, kikiwemo na Kijiji cha Matondo, Kijiji cha Igundu na Kijiji cha Shoga. Tunapozungumza sasa hivi, tayari fedha zote zilishalipwa, zaidi ya takribani Shilingi milioni 250, lakini wale watu wa mamlaka ya kuchimba maji, DCCIA hawapo eneo la site. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri uwasisitize, pesa wameshalipwa, warudi site ili waweze kuchimba vijiji kumi ambavyo vimebaki.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri kama anakumbuka wakati anasaini mradi wa maji wa Kiwira alituahidi kutuletea Shilingi milioni 250 kwa ajili ya mradi wa maji wa Itumbi. Kisima kimeshakamilika tayari, na tayari Engineer wa Maji Wilaya alishakuandikia barua ya kukukumbusha, naomba nami nikukumbushe kwa niaba ya wananchi wa Chunya na wananchi wa Itumbi utuletee hizi pesa ili mradi huo uweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri ambayo inaendelea, naishukuru tena Wizara, imetuletea pesa kwa ajili ya mradi wa maji wa extension ya Makongorosi zaidi ya Shilingi milioni 200, kazi inaendelea, na mradi wa Matwiga pia wametuletea pesa ya kumalizia. Naomba kupitia Wizara yako, wasisitize mradi huu wa Matwiga uweze kukamilka kwa wakati. Fedha ipo, na mradi huu kutokana na kuwa ni wa muda mrefu sana, naomba sana uwasisitize mradi huu uweze kwisha ili vile vijiji vya mwanzo viwili; Kijiji cha Matwiga pamoja na Kijiji cha Isangawana, viweze kutumia maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumze kuhusu mradi wa maji wa miji 28. Sisi watu wa Chunya ni moja kati ya wanufaika wa mradi wa maji huu katika miji 28, na mradi huu wa maji, tuna imani ukikamilika utakuwa mkombozi mkubwa sana kwa wananchi wa Chunya hasa Chunya Mjini.

Mheshimiwa Spika, Sera ya Maji ya mwaka 2022 inasema kwamba, ushirikishaji wa wadau ambao ni wanufaika wa maji, lazima uzingatiwe. Kwenye Wilaya yetu ya Chunya, ukiwaza kuwashirikisha wadau, utamshirikisha Mbunge, Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkurugenzi, Mabaraza ya Madiwani pamoja na wananchi kwa ujumla. Kwa huu mradi wa maji ambao unaenda kwenye miji 28, tunasikitika sana kwamba ushirikishaji wake ni mdogo sana kwa sisi wadau wa Wilaya yetu ya Chunya. Katika mradi huu wa maji, sisi tuna maoni yetu namna ambavyo tunataka kushirikishwa.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Chunya ni moja kati ya Wilaya kame, na uchimbaji wa Visima umeweza kuchimbwa kwa muda mrefu na matunda yake yameonekana ni madogo sana. Mwaka 2017/2018 uliletwa mradi wa maji wa Nyatura. Kilichimbwa kisima cha maji na lilijengwa tenki la lita karibu 500,000, lakini mpaka leo tunapozungumza, maji hayapo kwenye ule mradi. Kwa hiyo, tuna experience ya kutosha kuhakikisha kwamba miradi ya maji kwa kutumia visima kwa Wilaya ya Chunya sasa hivi haifai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Chunya tulishauri na tukapendekeza kwamba ili kutatua changamoto ya maji ndani ya Wilaya ya Chunya, tuweze kutumia maji ya Mto Bwaziva na Wizara ilifanya kazi hiyo. Mheshimiwa Naibu Waziri ni shahidi, ametembelea mara kadhaa kile chanzo cha maji na mwaka huu pia aliweza kutembelea pamoja na wataalam wake wa maji kuonesha kwamba kile chanzo cha maji kitaweza kutufaa kwa muda mrefu zaidi.

Mheshimiwa Spika, matumizi ya maji ya Chunya kwa sasa hivi ni takribani lita milioni mbili na nusu, na kile chanzo kina maji zaidi ya lita milioni saba na nusu kwa siku. Kwa hiyo, ni chanzo cha uhakika kwa miaka mingi zaidi. Masikitiko yetu, kupitia Mradi wa Maji wa Miji 28, wataalam wa Wizara wanataka wautekeleze mradi huu kupitia visima, kitu ambacho tayari huko nyuma kimeshaonesha kimefeli.

Mheshimiwa Spika, watu wa Chunya wamenituma tuwaambie Wizara, sisi watu wa Chunya hatuko tayari kuona mradi huu unatekelezwa kwa takribani zaidi ya Shilingi bilioni 11 kuchimba visima vya maji ambavyo tuna uhakika kwamba havitakuwa na tija kwa muda mrefu. Nawaomba sana Wataalam wako, wiki iliyopita nilikuja Wizarani nikaonana nawe, nikaonana na Katibu Mkuu, tunashukuru wameweza kulifanyia kazi, amewatuma kule wataalam, wameshaenda kule, naomba mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Chunya wamesema hawako tayari kuona kwamba mradi huu unatekelezwa kwa visima hivi vinavyoenda kuchimbwa kwa sababu wanajua hautaweza kuwanufaisha. Wataalam wa maji wanaishi Dar es Salaam, wanaishi Dodoma, sisi kule ndio wahanga wakubwa wa maji. Watatekeleza wanavyoona wao, lakini wakiondoka sisi ndio tutakaopata shida.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana, sisi watu wa Chunya ndio tunaojua adha. Mheshimiwa Waziri ana usemi wake mmoja unaosema kwamba, anayelala na mgonjwa, ndiye anayejua mihemo yake. Sisi ambao tuko Chunya, ndio tunaojua hii adha. Hao wataalam ambao wako Dodoma na Dar es Salaam, hii adha hawaijui. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, unapokuja ku-wind up hapa utupe jibu la swali hili ili wananchi wa Chunya kule nao waweze kuwa tayari kupokea mradi huu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu. Kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutuletea bajeti hii ambayo sasa imeakisi kwamba Serikali imekuwa na dhamira ya dhati kabisa kuweza kumkomboa mkulima wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza pia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote wa Wizara kwa ujumla kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Pamoja na dhamira kubwa ambayo Serikali imeendelea kuifanya kwenye Wizara hii, tunaona namna ambavyo kule kwetu ambako tunalima zao la tumbaku wameweza sasa kuona umuhimu wa zao hili na kuhakikisha kwamba tunakwenda kupata makampuni mengine zaidi kwa ajili ya kununua zao la tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Serikali imepata kampuni, kampuni ya AMIS ambayo nayenyewe tayari imeshachukua kiwanda cha kichakata tumbaka pale Morogoro na wametuhakikishia kwamba kwenye mwaka huu wataweza kununua tani milioni 10, tunawapongeza kwa kazi kubwa ambayo mmefanya, yale ambayo tulikuwa tunawashauri mmeyachukua na mmeenda kuyafanyia kazi, tunawapongeza kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hivyo hii kampuni imetuhakikishia kwamba mwaka ujao wa kilimo itanunua tani Milioni 30, hii maana yake tunaenda kuongeza makisio kwa wakulima wetu wa zao la tumbaku na tutakapoongeza makisio watalima zaidi na wanapolima zaidi maana yake uchumi wao utakukua. Ninawaambia wakulima wangu wa Tarafa ya Kipembawe Wilaya ya Chunya wajiandae sasa kampuni hii inakuja, makisio yataongezeka hivyo uchumi wa eneo husika utaenda kukuwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo bado kuna changamoto kwenye mbegu na miche ya tumbaku. Tumeona kwenye hii bajeti upande wa utafiti, maeneo mengine wamewekewa fedha lakini upande wa mbegu za tumbaku na miche ya tumbaku hawajawekewa fedha, hii kampuni ya utafiti ya TORITA haijawekewa fedha. Ninaiomba Serikali kama ina dhamira ya dhati kabisa ya kuhakikisha kwamba zao hili linaenda kumkomboa mkulima mwaka ujao waweke fedha ili ziweze kuwasaidia kupata mbegu ambayo ni bora na tunaweza kupata tumbaku ambayo ni nzuri zaidi.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu watu wa Malawi pamoja na Zimbabwe wamewekeza kwenye utafiti, wamewekeza kwenye mbegu bora za tumbaku. Wao wanapata tumbaku yenye daraja la juu zaidi. Sisi tumbaku yetu iko chini na ndiyo maana hata bei ya tumbaku Tanzania iko chini. Tuna wastani wa dola 1.4 mpaka wastani wa dola 2.2 ambayo iko chini, wakati wenzetu wananunua kuanzia dola mbili na kitu na bei ya juu ni dola nane. Kwa hiyo, tukiwekeza huko tutaweza kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nizungumze habari ya pembejeo. Serikali imeongeza ruzuku kwenye bajeti hii kwa ajili ya pembejeo, ni jambo zuri sana, nasi tunapongeza kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya. Tunampongeza sana Waziri kwa ubunifu wake huo. Tuna imani wakipata fedha ambazo wameziomba, bei ya pembejeo inaenda kushuka. Sisi sote tumekuwa mashahidi huu musimu wa kilimo uliopita hapa, bei za pembejeo zilikuwa hazishikiki. Kila Mbunge hapa alikuwa analalamika kwamba pembejeo ziko juu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi kupata nafasi ya kuweza kuchangia. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wataalam wote wa Wizara hii. Kutokana na ufinyu wa muda nijielekeze moja kwa moja upande wa mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa ya Waziri ambayo ameitoa hapa ameeleza kwamba kwenye huu mwaka wa fedha ambao tunaendelea nao kuna takribani Kata 85 ambazo zilikuwa zimepangwa kuweza kujengwa kwenye huu mwaka wa fedha. Kata hizi ni chache sana kulingana na ukubwa wa jiografia ya nchi hii na tukienda kwa mtindo huo maana yake, hatutoweza kuyafikia maeneo yote kwa kuweza kujengwa minara ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, minara hii inajengwa kupitia Mfuko wa Mawasiliano wa UCSAF minara ambayo inajengwa kwa UCSAF minara mingi wamepewa TTCL na TTCL hawa wanakwenda kwa hali ya kusuasua, tukienda nao hivi tutafikia hatua ambayo hatutaweza kufikia lengo la kujenga hii minara na kuifikisha kwa wananchi kwa wakati. Kutokana na minara hii na TTCL kwenda katika maeneo ambayo kibiashara siyo rafiki sana ambayo Maopareta wengine wanaiogopa hii, sasa tunavyokwenda na TTCL maana yake hata ule ushindani na kukua kwao kuweza kupata faida inakwenda kuwa ni ngumu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na TTCL kwenda maeneo ambayo kibiashara hayana faida kwao ni kama wanatoa huduma matokeo yake TTCL wanakuwa hawafanyi vizuri sana sokoni. Nikiangalia kwenye takwimu ambazo tunazo, kwa watoa huduma saba ambao tuko nao, Telephone Operators TTCL ni wa pili kutoka mwisho. Kwenye market share wa kwanza anaongoza Vodacom ana asilimia 30.5, Airtel ana asilimia 27, tiGo 25.4, Halotel 13.3, Zantel asilimia Mbili na TTCL ana asilimia 1.7. Kwa hiyo, kuweza kushindana kwenye soko imekuwa ni gumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kushindana huku kunakuwa kugumu tuone namna ambavyo tunaweza kubadilisha Sheria kwa TTCL ambayo itaweza kuwabeba ili na wao waweze kufanya kazi yao vizuri. Ninashauri Serikali ili kuweza kuwasaidia TTCL tuweze kubadilisha Sheria zetu, TTCL wabakie kuwa ni wajenzi wa miundombinu peke yake, wasiingie kama Telephone Operators kuweza kushindana na haya makampuni mengine kwa sababu, kwenye ushindani tayari wameshaonesha kwamba hawawezi wameshindwa. Tukiweza kubadilisha sheria wao wakawa wanamiliki miundombinu minara hii wanapewa na minara mingine waendelee kuijenga, baada ya hapo hawa Telephone Operators wengine wawe wanapanga kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnara mmoja utaweza kupangwa na makampuni matatu mpaka manne, kwanza itasaidia minara kuwa michache, lakini mnara huo mmoja na makampuni mengine yakipanga hapo na huduma zote maana yake hazitaweza kupatikana vizuri na kwa wakati. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam, Mbunge wa Sengerema, taarifa.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa tu mchangiaji kwamba TTCL hata hiyo minara wameshauza.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Masache Njelu Kasaka, unaipokea taarifa?

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo. Tuseme tu TTCL wakiweza kumiliki hii minara lakini hata pia kwa usalama wa nchi itaweza kutusaidia sana, maana yake tutakuwa tuna uhakika na usalama na udhibiti mzuri ambao tuko nao. Tukienda hivi tuliona hapa miaka kama miwili iliyopita, wenzetu baadhi ya kampuni fulani tulishindwa kupata mawasiliano hapa, lakini tukiwa na uhakika wa TTCL kuweza kumiliki hii hapa hakuna mtu ambaye ataweza kufanya chochote kwenye minara ambayo tunayo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana kwa hoja yako ambayo nafikiri pia yamepokelewa na Wizara.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.