Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Robert Chacha Maboto (10 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nafasi ili na mimi niweze kuchangia bajeti yetu ya mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niwashukuru wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini kwa kuendelea kuniamini ili mimi niweze kuwatumikia lakini pia ninaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa kazi kubwa inayofanya, inayoongozwa na Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza pia Serikali kwa sababu imetuwezesha sisi Wabunge kwenye majimbo yetu kwa kutupatia zaidi ya shilingi 500,000,000 kwa ajili ya kushughulika na barabara ambazo zimekuwa kero kubwa sana kwa Watanzania.

Pia naipongeza Serikali kwa sababu ilisikiliza kilio cha Wabunge na mawazo yao kwa muda mrefu ambayo tumekuwa tukiyazungumza hapa. Kwa mfano mimi Jimbo langu la Bunda Mjini, takribani muda mrefu uliopita nyuma barabara zangu za mitaa zilikuwa haziwezi kupitika kwa namna yoyote ile hata kama ungeenda na trekta zilikuwa haziwezi kupitika. Lakini kwa sababu Serikali ya Awamu ya Sita ni Serikali sikivu imetoa fedha na sasa barabara zimeanza kupitika hata kama sio zote lakini mwanzo umeshaanza kuonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Sita imetufanyia mambo makubwa pale Bunda Mjini. Kwa muda mfupi huu tumeshapata taa za barabarani pale mjini, tumeshapata fedha za kujenga shule za sekondari zaidi ya sita, na kwa muda mfupi tumeshazifungua lakini pia na shule za msingi ziko zinaendelea kujengwa. Kwa hiyo kwa bajeti hii ambayo imewasilishwa na Wizara ya Fedha Mheshimiwa Mwigulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo muhimu sana ambalo mimi ninaliona hapa ni kuhakikisha kwamba Wizara ya Fedha inasimama vizuri katika kuhakikisha kwamba makusanyo yale yanayopatikana yanatumika vizuri kwa ajili ya shughuli za maendeleo za wananchi. Wananchi wa nchi yetu tuzipowazoesha suala la kulipa kodi wakalijua, kwamba kila mfanyabiashara anayefanya biashara kulipa kodi ni wajibu wake kuna siku watakuja kudai maendeleo pasipo wao kutaka kutoa kodi. Kwa hiyo hili nilipenda niishauri Wizara ya Fedha ikasimame nalo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, kwa sababu ya makusanyo yetu tunayoyakusanya hayatoshelezi mahitaji yetu, bajeti yetu kwa mwaka ni trilioni 36 lakini makusanyo yetu yako chini. Kwa maana hiyo, fedha hii tunayoikusanya kidogo ni vizuri Wizara ya Fedha ikazilinda vizuri fedha hizi ziweze kutumika kwa shughuli mahsusi. Wasipofanya hivyo, fedha tunayopata ni kidogo na matumizi yakaenda nje na utaratibu unaotakiwa, kile tunachokilenga kwenye shughuli za maendeleo hatutakifikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Wabunge tumesema hapa tukaiomba Wizara ya Fedha kutusaidia fedha kwenye TARURA na wametupa fedha. Lakini kama watu hawatalipa kodi fedha hizo pia tunaweza tukazungumza hapa kuanzia asubuhi mpaka jioni na fedha zisipatikane. Kwa hiyo muhimu ni kuwajenga wananchi wetu kwenye maeneo yetu ili wafahamu kwamba kulipa kodi ni sehemu ya maisha yao ni sehemu ya biashara zao. Wakilipa kodi wanarudi kuidai Serikali maendeleo. Kama hawatalipa kodi kuidai Serikali maendeleo haitawezekana. Lakini pia hatuwezi kupata maendeleo kwenye nchi yetu tukifikiri tu kwamba tunaweza tukapewa fedha za misaada halafu zikatuletea maendeleo kwenye nchi yetu. Hiki kitu hakitawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kuishauri Wizara ya Fedha; Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA inafanya kazi nzuri lakini suala kubwa ambalo mimi ningewaomba wajitahidi kutoa elimu kwa wafanyabiashara. Waweke mazingira ya kodi wazi, kila yule anayetaka kulipa kodi ajue uwezo wake wa kulipa kodi na kodi anayotakiwa kuilipa ni ipi. Wakishafanya hivyo, watu walio wengi wataenda kulipa kodi wao wenyewe kwa hiari yao. Lakini na wao wananchi wakishalipa kodi kwenye Serikali wanaidai Serikali maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo hilo ni muhimu sana ambalo Wizara ya Fedha inapaswa kulishika vizuri ilisimamie vizuri na kwa sababu fedha yetu haitoshi shughuli zetu za maendeleo kwa mwaka, kidogo tunachokipata tuweze kukitumia vizuri. Mimi nimeshangaa kuja kuona kwamba wapo watu baadhi wanaweza kwenda kwenye bomba la mafuta la Serikali wakaenda wakachimbua kwenye bomba la mafuta ya Serikali halafu wao wakapeleka yale mafuta kwenye maeneo yao wakaenda kuuza, raia wa nchi hii. Kama tunataka maendeleo kwenye nchi hii ni lazima sisi wenyewe Watanzania tuwe wazalendo kwa mali zetu sisi wenyewe. Wale watu wanaofanya hayo kwa kuhujumu miundombinu ya Serikali, wanatuambia sisi Wabunge tunachokizungumza hapa au kile ambacho Serikali inakipanga hakitafanikiwa kwa sababu wao wanakihujumu. Kwa hiyo, lazima Serikali isimame kidete kwenye jambo hili ili kwamba wale watu wanaofanya mchezo ule wauache mara moja kwa sababu sio jambo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mtazamo wa nchi kwa sasa wana mpango mkubwa wa kufanya ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kuja Tanzania ambalo wao leo wakiona watu wa Dar-es-Salaam au watu walioko bandarini wanafanya vitu vya namna hiyo, kuna watu watajifunza vitu viovu kupitia kwao, halafu matokeo yake kile tunachokikusudia tusikifikie kwa makusudi ya watu wachache, kundi la watu wachache wasiozidi 10 au 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mtazamo wa nchi kwa sasa wana mpango mkubwa wa kufanya ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kuja Tanzania ambalo wao leo wakiona watu wa Dar-es-Salaam au watu walioko bandarini wanafanya vitu vya namna hiyo, kuna watu watajifunza vitu viovu kupitia kwao, halafu matokeo yake kile tunachokikusudia tusikifikie kwa makusudi ya watu wachache, kundi la watu wachache wasiozidi 10 au 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Wizara ya Fedha, leo tunazungumza na Mheshimiwa Waziri hapa, tunaipongeza sana bajeti yake ni nzuri na imekidhi vigezo vizuri vya wananchi wetu, lakini itakuwa nzuri pale yale yote tunayoyatarajia yafanyike kwa wananchi yatakapofanyika. Nje na hapo tutakaporudi mwaka kesho au kwa muhula mwingine tutaanza kumsema Waziri vibaya, lakini fedha ikipatikana bajeti itakuwa nzuri na shughuli za maendeleo za wananchi zitakwenda vizuri na kile tunachokusudia kitafikiwa. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri kudhibiti suala hilo kupitia Serikali ili kwamba, yale mapato yetu madogo tunayoyakusanya yaweze kutusaidia kwenye shughuli zetu za maendeleo. Nje na hapo Mheshimiwa Waziri, leo tutampongeza na kesho tutarudi kuja kulaumu kwake tena kwamba, mbona hakufanya yale ambayo tulikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipenda nichangie hayo mambo machache katika bajeti hii ili niweze kusema hilo nililoliona. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru, halafu nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata fursa hii asubuhi hii ya leo kwa kunipa pumzi ili niweze angalau kuchangia na mimi kwenye Wizara hii ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya kuhusiana na wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mimi leo nachangia kwenye jambo moja tu kubwa ambalo ni mahususi kwangu, linalohusiana hasa na kata ile ya Nyatwali ambayo wananchi wangu pale takribani 13,000 wanahamishwa kutoka katika eneo lile. Lakini wahusika ambao wanatarajia kuwahamisha wananchi hawa ni Wizara mbili, Wizara ya Ardhi ambayo ndio inafanya tathmini na Wizara ya Maliasili ambayo ndio yenye Mbuga ya Serengeti, hawa ndio wahusika wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi imepewa nafasi ya kufanya tathmini na kufanya valuation kwa ajili ya majengo ya wananchi wetu na kuwafanya ili waweze kupata stahiki zao vizuri. Wizara ya Maliasili ndio mlengwa na muhusika ambaye ndio anapaswa kuwalipa hawa wananchi wetu. Nyatwali sasa jambo lile la wananchi wa Nyatwali kuhama kutoka katika kata yao ile ya Nyatwali ni jambo ambalo mimi nimelisikia kwenye mahusiano yangu zaidi ya miaka 20 leo na nimelikuta likiwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa sababu pia jambo hili limekaa muda mrefu sana kwenye vichwa vya wananchi wetu, kwanza lilishawaumiza kisaikolojia, wananchi walishapoteza direction, kwa hiyo, hata leo ukiwauliza wanananchi wa Nyatwali kwamba mnatakiwa kufanya nini? Jibu la ndio wanaweza kusema hapana na jibu la hapana wanaweza kusema ndio kwa sababu lile jambo lilishawaumiza kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili tumeshawahi kukutana na Mawaziri pale walikuja kwenye kata yetu ya Nyatwali, Mawaziri wale nane. Walisikiliza maoni ya wananchi wao wenyewe kwa michango yao. Sasa jana niliona Mheshimiwa mmoja anachangia hapa anatoa taarifa kwamba wale wananchi wa Nyatwali wao walikuwa tayari kuondoka kwenye eneo lao. Mimi nasema hapana wananchi wa Nyatwali hawakuwa tayari kuondoka kwenye eneo lao isipokuwa wametakiwa kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametakiwa kuondoka kwa sababu ya manufaa makubwa ya nchi yetu. Kwa maana ya kuhakikisha kwamba ile Mbuga ya Serengeti imeongezwa kwenye eneo lao hilo ili Wanyama wetu wawe wanaenda kupata maji kwenye Ziwa letu la Victoria. Sasa wananchi wetu walioko pale Nyatwali wengi wameshaumia na sasa hivi akili yao imebaki tu Serikalini kwamba Serikali lazima itumie utu, kwa sababu wale wananchi ni wananchi wake, wanaipisha Serikali pale kwenye eneo lao ili Serikali ifanye uwekezaji wa kutosha pale ndio maana yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Serikali imeenda kununua eneo kwa wananchi, siyo kwamba wananchi walivamia hapana. Inaenda kununua eneo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unapokwenda kununua eneo kwa mwananchi ambaye yeye alikuwa hayuko tayari kununua eneo lake, siyo kwamba wewe unayekwenda kulinunua ndio unatakiwa kumpangia bei isipokuwa yeye mwneyewe anayetaka kuuza ndio atapanga bei. Sasa Wizara ya Ardhi na Wizara ya Maliasili inawapangia wananchi wa Nyatwali bei ya kununua eneo lao badala ya wananchi wa Nyatwali wao wenyewe kupanga bei yao kwa yule anayetaka mali yao wamuuzie kwa bei wanayoitaka wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya muda mrefu wananchi wetu wa Kata ya Nyatwali wameridhia kukubali wakaona hakuna sababu ya kuendelea kubishana na Serikali wakasema walitoe eneo lao lile ili waache shughuli za Serikali ziendelee na shughuli za hifadhi zifanyike. Lakini pia ufahamu tu kwamba Halmashauri ya Mji wa Bunda ndio Halmashauri kubwa pia inayopata athari kubwa kupitia Mbuga ya Serengeti kwa wananchi wake, kwa sababu pale wananchi wanalishiwa mashamba yao na fidia yenyewe kutoka katika Wizara ya Maliasili na Utalii inaweza kuchukua miaka mitatu, bei yenyewe anayolipwa heka yake ya shamba ni shilingi 100,000. Lakini hiyo fedha mwananchi ataidai zaidi ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwananchi huyohuyo anayeishi pembezoni mwa Mbuga ya Serengeti, ng’ombe wake wakiingia kwenye Mbuga ya Serengeti kila ng’ombe mmoja atakuwa–charged kwa shilingi 380,000 kila ng’ombe aliyekanyaga kwenye Mbuga ya Serengeti. Huku yeye heka moja ya shamba analipwa shilingi 100,000 tena kwa kuidai kwa muda wa miaka mitatu.

Sasa mimi nilikuwa nawaomba watu wa Wizara ya Ardhi na Maliasili wale wananchi wa Bunda wakihamishwa kwa viwango vyao hivi walivyovipanga, pamoja na umaskini wao walionao watu wa Nyatwali, watazidi kuwaongezea umaskini mara tano Zaidi kuliko vile walivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu wale wanachi wa Nyatwali na wao Mbuga ya Serengeti ni mali yao, wala sio mali ya mtu mwingine, ni mali yao, kwa hiyo wanapisha ili wao wafanye maendelezo kwneye mali yao. Sasa kama wanapisha kwa nini wasilipwe fedha stahiki zinazoweza kuwafanya waridhike kwamba mali wanayoiondokea pale ili wanufaike nayo ni mali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wafanya tathmini wale wa Serikali walioko pale, wanafanya tathmini kwenye majengo ya wananchi wetu. Nyumba zile ni nyumba zimejengwa toka miaka ya 1968, leo wale wananchi wanaambiwa wahame kwenye eneo lile ambalo wamekaa toka mwaka 1968.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mwaka 1968 mpaka leo kwamba yule mwananchi alijenga nyumba yake ya majani. Kipindi hicho majani ya kukata kwa mikono yalikuwepo maeneo hayo, leo hii majani yale hayapo, halafu unamwambia leo huyo mwananchi utamfanyia valuation kwenye nyumba yake ya majani, utamlipa fedha kulingana na nyumba yake ya majani halafu yeye ataenda huko atakapokwenda, ataenda kutafuta majani aezeke nyumba yake kwa majani atayatoa wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan, kila mwananchi, kila raia wa nchi hii sasa hivi kule alikokuwa anataka kutoka ili aende mahali pengine, hivi leo unawezaje kumfanyia valuation mwananchi kwenye nyumba yake ya majani, halafu ukamwambia ukitoka hapa ukajenge nyumba ya majani hiyo hiyo wakati kila mmoja anatakiwa kufanya kila jitihada akajenge nyumba ya bati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi, Wizara ya Maliasili na Utalii, wananchi wa Kata ya Bunda Mjini, wananchi wa Kata ya Nyatwali katika Halmashuri ya Mji wa Bunda, lolote litakalowapata katika haya, machozi yao yatabaki Wizara ya Maliasili na Wizara ya Ardhi. Wale wananchi wameshaumia kwa kiasi kikubwa, ni mategemeo yangu, ni maombi yangu na tumeshazunguka nao mara kadhaa kila sehemu kwenda kupeleka jambo hili kusema ili Serikali iweze kuwasikia, lakini bado jambo halijakaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe watu wa Wizara ya Maliasili na Ardhi wahakikishe kwamba wanawatendea wananchi wa Nyatwari haki yao ili wapate fedha stahiki ambazo zinaweza kuwafanya pale wanapotoka na huko wanakokwenda wakanunue eneo, na kwa sababu katika kuwahamisha kwao pale hawakuwatengea eneo maalum ambalo watakwenda kuishi wao wanawalipa fidia, wanawaambia nenda mtanunua ninyi wenyewe huko mnakokwenda kitu ambacho ukija kuangalia kwa sasa hivi mfano kwa mazingira ya sasa hivi ndoa nyingi baba na mama wanaishi, lakini hawako pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo fedha zile zinaenda zinawekwa kwa baba aidha zinawekwa kwa mama kati ya hawa wawili mmoja anaweza akaondoka nazo halafu wale Watoto wakabaki wanarandaranda pale mjini na hawatapata sehemu nyingine ya kwenda. Hawa watakapokuwa wanaanza kulia watakuwa wanaililia Serikali kwa sababu Serikali ndio ilichukua eneo lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna wajane, kuna nini na watu wengi unajua Watanzania wameshaathirika kisaikolojia sana wale wananchi, Serikali ikapata eneo maalum ambalo itawapeleka wale wananchi wa Nyatwali, hautakuja ukaa ukasikia Kata ya Nyatwali na ukajua raia yoyote wa Nyatwali baada ya kuwa wamelipwa walihamia wapi hutakuja kukaa ukapasikia eneo hilo, kwa sababu watakuwa wamepotea katika mazingira ambayo hayawafanyi wao waende kutafuta sehemu nyingine ya kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia wanayopewa ni kidogo sana, nimuombe sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan anaamini kutokana na michango mingi ya Wabunge wenzangu hapa ameliona na amelisikia jambo hili alishike na alifanyie kazi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Robert Chacha Maboto kwa mchango wako. (Makofi)

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kupata nafasi hii jioni hii ya leo lakini pia naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai huu alionipa siku hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimshukuru Mheshimiwa Rais Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya katika Majimbo yetu kwa sababu kazi ambayo Rais anaifanya ni kubwa na ambayo sisi Wabunge wake na wananchi wake kwa ujumla tunamuunga mkono kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda mrefu sana uliopita wananchi wengi wamekuwa wakihadithiwa shughuli za maendeleo bila kuziona kwa macho lakini Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan wananchi wengi wameona shughuli za Serikali zinavyowafikia katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo jambo hili ni la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu anafanya kazi kubwa. Kwa hiyo, hata pale ambapo wananchi wanaambiwa kwamba walipe kodi naamini kwamba wanaweza kuwa wanahamasika kwa sababu wanaona vitu vinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mfanyabiashara na sisi huwa hatuendi darasani kujifunza namna ya kuweza kufanya biashara. Isipokuwa kufanya biashara ni namna tu ya mazingira uliyoyatokea nyumbani kwenu. Wakati mwingine umesoma au hujasoma na ukiona fursa ya kusoma hukuipata lazima uvamie fursa ya biashara. Sasa mimi ni mfanyabiashara, pia tupo wafanyabiashara wengi katika nchi hii ambao tunafanya biashara lakini hatukupata elimu ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa najaribu kufikiria na kuiomba Serikali kwamba hizi kodi nyingi, mtiririko mwingi wa kodi ni kwa nini Serikali isizitengenezee utaratibu wale wafanyabiashara wakawa wanazilipa kwa installment? kwa sababu watu wengi wanapokwenda kwa wafanyabiashara, huyu akaenda leo kwaa jambo fulani kwa ajili ya kumwambia mfanyabiashara alipe kodi ya jambo hilo, kesho akaenda mtu mwingine, keshokutwa na mwingine; zile kodi ziko zaidi karibia ya kumi ambazo mfanyabiashara mmoja anatakiwa kuzilipa. Sasa na kwa sababu pia hatuna elimu ya biashara yule mfanyabiashara anakuwa anachanganyikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi huwa najaribu kufikiri ni kwa nini Serikali haiwezi kuona kwamba zile kodi ambazo zinaweza zikaziunganisha pamoja, kwa nini zisiunganishwe pamoja na wale wafanyabiashara wakaambiwa kuwa wanazilipa kwa wakati? Kuliko hizi ambazo wanaruhusiwa watu wengi kwenda kuwasimamia wafanyabiashara aidha kuwadai vyanzo fulani vya mapato ya Serikali ambavyo na wao wenyewe wao waliotumwa kwenda kuvidai vyanzo vile vya mapato hawajui kuvielezea vizuri kwa wafanyabiashara. Lazima mamlaka ya mapato Tanzania ambayo ndiyo imepewa mamlaka hiyo ya kukusanya kodi inaweza kuwaelewesha watu vizuri wakaelewa namna ya kulipa kodi kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninachoamini ni kwamba hawa wafanyabiashara wakieleweshwa vizuri kuhusiana na suala la kodi naamini watalipa vizuri. Serikali ili ikusanye kodi vizuri lazima iwaeleweshe wafanyabiashara wake vizuri waelewe ni kwa nini wanalipa kodi. Bahati nzuri kitu ninachokisema kwa sasa ni kwamba watu wengi hata mimi nimekuwa nikilalamika huko nyuma kwamba inawezekana nalipa kodi halafu kazi zinazofanywa na Serikali sizioni lakini kwa awamu hii kazi zinaonekana. Kwa hiyo hata namna ya kumwelezea mtu kwamba unalipa kodi ili kifanyike kitu gani inakuwa ni rahisi. Sasa ni kwa nini Serikali isiviunganishe vitu hivi, vyanzo vyake hivi vya mapato kuliko Serikali moja inatengeneza vyanzo vingi karibia 30 halafu unawapa watu tofautitofauti kwenda kuwaelezea hao wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wafanyabiashara kwa sababu tulio wengi hatujasomea biashara ila tumeingia tu kwenye biashara kutokana na ukata wa maisha, namna ile unavyokuja kuni-treat mimi inakuwa ni vigumu kukuelewa. Lakini kukitengenezwa mfumo mzuri ambao wafanyabiashara hawa wa chini wakaambiwa kiwango chake cha kulipa kodi kwa mwaka ni hiki kikagawika kwa awamu kama nne, ikawa kila baada ya awamu analipa kiasi kile anachokijua yeye Serikali haiwezi kupata usumbufu na wala haiwezi kuhangaishana na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hata wakati nyingine mnapoona wafanyabiashara saa zingine wamegoma, wanagoma kwa sababu ya kuchanganyikiwa, yaani vitu vinakuwa vingi ambavyo vinaingia vichwani mwao na namna ya kuweza kulifanyia kazi inashindikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambaye wewe ni daktari wa fedha ni vizuri utusaidie sisi, uwasaidie walipa kodi wako ambao wewe unaamini kwamba unatoza kodi kwa watu ambao hawajasomea biashara lakini ndio wanaokulipa kodi. Sasa wewe lazima utumie namna yoyote inayoweza kuwezekana ili wale wafanyabiashara waweze kulipa kodi katika utaratibu ambao ni mzuri na ni nafuu na ambao ni rafiki. Bila hivyo wafanyabiashara wale bado wataendelea kukuhangaisha na bado watu wataendelea kukwepa kodi. Lakini kumbe kitu kikubwa kilichopo ni kwamba wakishaeleweshwa vizuri wakajua vizuri, na bahati nzuri sasa wanaona shughuli za maendeleo zinavyofanyika katika nchi yao kwa hiyo kigugumizi kinakwisha, na watu watakuwa wanaambiwa kulipa na wanalipa katika utaratibu ambao nil aini kabisa bila kuhangaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo jambo hilo nilikuwa naliomba sana, kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambaye ni mtaalam wa fedha atusaidie jambo hilo. Pia na juzi niliona hapa mchangiaji mmoja anasema kwamba mimi na taasisi yangu labla kampuni yangu nina miaka 20 nayo, halafu leo nikiambiwa kwenda kuisimamia ile taasisi yangu au kuisajili kwa ajili ya kufanya biashara labda ya microfinance naambiwa kwamba mimi siwezi kuwa kwenye bodi ya ma-director kwa sababu elimu yangu mimi haikidhi vigezo hivyo. Wakati huo huo taasisi hiyo nimeanza zaidi ya miaka 20. Sasa kwa akili za kawaida hata ukijiuliza unaona haiwezekani. Uzoefu nao una-matter katika kazi. Ingekuwa tu kusoma peke yake ndiko kunakosababisha kila jambo liweze kufanyika vizuri mimi naamini saa nyingine tusingekuwepo hapa tunahangaika na mambo mengi ambayo saa zingine yamekwenda na saa zingine hayakwenda vizuri. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri hili nalo ni jambo ambalo unapashwa kuliangalia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jambo lingine nilitaka kusema tu kwamba wananchi wangu wale wa Kata ya Nyatwali wameshafanyiwa tathmini ya maendelezo yao kwenye kata yao ile ya Nyatwali. Na kwa vyovyote vile itakavyokuwa muda mfupi uliobaki watahama katika eneo lile. Sasa na kwa sababu wananchi wetu wale na unawajua wananchi walio wengi ni wakulima na wafugaji; ni ombi langu kwa Serikali kwamba ni vizuri yake malipo yao kwenye bajeti hii wakalipwa mapema ili wakajipange mapema kwa ajili ya kilimo katika maeneo mengine. Wakilipwa nje ya muda ule ambao unaendana na muda wa kilimo itawatesa kwa sababu pale walipo hawaruhusiwi kulima, pale walipo hawaruhusiwi kuendeleza chochote. Pia yule anayetakiwa kuwalipa hajawalipa, halafu anawaambia bado wako pale pale. Sasa hao watu wataishi katika mazingira gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naamini kwamba kwenye bajeti hii wale wananchi wetu watalipwa fedha zao mapema na wataondoka kwa wakati ili wakaanze maisha yao huko wanakokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni lile jambo la kifuta machozi. Wananchi wetu wale maskini, wakulima, tena wakulima wa heka moja moja ya chakula na chakula chenyewe wanachokilima hata hakiwatoshi kukila kwa mwaka. Halafu chakula hicho hicho kimekuja kimeliwa na tembo halafu kulipwa fidia analipwa laki moja, halafu laki moja yenyewe anaisubiria baada ya miaka miwili, mitatu. Kwa kweli watu wale wanaumia kwa kiasi kikubwa. Ni ombi langu pia kwa Serikali kwamba jambo hili ni vizuri Serikali ikalifanyia mkakati mpya kuhakikisha kwamba kilimo cha mwaka kile ambacho hao wananchi wamekilima, mazao yao yamelishwa na tembo, muda huo huo mwaka ukiisha wawe wamepewa fedha zile ili na wao waende watafute chakula cha kununua. Hicho chakula ambacho wenzetu wanasema kwao gunia limeshuka mpaka 35,000 mikoa ya kusini. Sisi Mara gunia la mahindi ni 120,000 au 100,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakipata fedha hizo mapema wataenda huko ambako chakula kinauzwa 40,000 gunia wakanunue, halafu kitawasaidia, kuliko ile sasa kwamba fedha za mwaka huu atalipwa baada ya miaka miwili au miaka mitatu. Mwananchi huyu anakuwa ameshaumia kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba Halmashauri yangu ya Mji wa Bunda ilitoa eneo pale kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi za TANAPA kanda ya magharibi; na halmashauri ile ilishatoa eneo lipo kwa muda sasa. Ni imani yetu kwamba kwa sababu tunapisha ile Kata nzima ya Nywatali ni vizuri pia Serikali na yenyewe ikahakikisha kwamba ofisi ile iliyokuwa imetengewa pale fedha za kuanza ujenzi ni vizuri ikajengwa kwa wakati kwa sababu ndio itakayokuwa inasimamia mambo hayo ya Mbuga ya Serengeti na mambo mengine. Malalamiko mengi ya wananchi wetu wakati mwingine yataishia hapo kuliko vile ambavyo tunakuwa tunapata wakati mgumu wa namna ya kupata suluhisho la matatizo hayo ambayo tunakuwa tumeyapata katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kusema kwamba fedha zile zitolewe mapema ili kwamba Ofisi ile ya TANAPA Kanda ya Magharibi ziweze kujengwa kwa wakati ili ziweze kusaidia katika Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la fedha za miradi ya barabara. Niishukuru Serikali kwa sababu imeendelea kufanya kazi kubwa lakini bado sisi kwetu Bunda pale eneo la barabara za mitaa bado tatizo lipo ni kubwa.

Ombi langu ni kuiomba Serikali iendelee kutoa fedha kwenye TARURA ili kwamba uboreshwaji wa barabara zile za mitaa uweze kukaa vizuri; na kwa sababu maeneo hayo muda mwingi yamekuwa hayapitiki kwa muda mrefu lakini kwa sasa ramani imeanza kuonekana. Ombi langu ni kwa Serikali kuhakikisha kwamba wanawapa fedha za kutosha ili kwamba barabara zetu zile ziweze kulimika vizuri na wananchi wetu waweze kupita katika maeneo yao kwa wakati wote wa masika na kiangazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nakushukuru kwa kupata nafasi; ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi hii ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara ya TAMISEMI. Awali ya yote, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kwenye Taifa letu ambapo mwezi wa Pili mwaka huu alipokuja Mkoa wa Mara pamoja na shughuli zote alizokuwa anazifanya, alizindua mradi mkubwa wa maji katika Mji wa Bunda.

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa ambalo naiomba Wizara ya Maji ni kuhakikisha kwamba zile Kata 14 zote zinapata maji kwa sababu mradi huu aliouzindua Mheshimiwa Rais ulikuwa ni mradi wa fedha nyingi na wa muda mrefu. Wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini, ni takribani kilometa tano kuona ziwa pale lakini maji bado yanatusumbua. Kwa hiyo, nawaomba watu wa Wizara ya Maji wahakikishe kwamba mradi huu unamaliza tatizo kubwa la maji ambalo tunalipata pale Bunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kuhusu fedha za UVIKO-19 ambazo kwenye Jimbo langu la Bunda Mjini lilipata takribani vyumba 51 vya madarasa ambavyo vimetekelezwa ndani ya miezi mitatu, na sasa vinafanya kazi, kwa sababu vimechukua watoto wetu kuingia madarasani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kikubwa ambacho nilitaka kukisema hapa ni kwamba watu wa TAMISEMI ni vizuri wakachukuwa mfano huu uliotumika kwenye hizi fedha za UVIKO-19, kuhakikisha kwamba miradi mingi ya vyumba vya madarasa inakuwepo kwenye Halmashauri zetu kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Spika, hapo nyuma kabla ya fedha hizi za UVIKO-19 chumba cha darasa kilikuwa kinaweza kujengwa takribani miaka 15 ambapo leo kwa fedha hizi tumeona chumba hicho kinaweza kujengwa kwa muda wa miezi mitatu. Kwa hiyo, TAMISEMI pamoja na fedha zote hizi ambazo wanazipeleka kwenye Halmashauri, wao watoe kauli kwenye Halmashauri wakati wanapotuma fedha zao kwenda kutekeleza miradi kule.

Mheshimiwa Spika, watu wetu walioko kule chini uwezo wao wenyewe unaonyesha kwamba kujisimamia ni kazi, kwa hiyo, ni vizuri maelekezo mahususi yakatoka ili vyumba vya madarasa badala ya kujengwa kwa muda wa miaka 15 kumbe vinaweza kujengwa kwa miezi mitatu ili kupunguza tatizo hili; na kwa sababu vyumba vya madarasa vya kumalizia vipo vingi sana kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa sababu bado inaendelea kutoa fedha kwa maana ya kumalizia vyumba vile, lakini bado tatizo ni kubwa. Tunaomba TAMISEMI iendelee kutoa fedha ili vyumba hivyo viweze kukamilika na tatizo hili liendelee kupungua kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie kuhusiana na TARURA. TARURA wanafanya kazi nzuri sana na hasa kwenye Jimbo langu la Bunda Mjini, muda mrefu uliopita barabara za mitaa zilikuwa hazipitiki kabisa; mitaro na barabara zake zilishaotea mpaka majani. Barabara ambayo magari yalikuwa yanaweza kuitumia Huwezi kuamini kama kuna gari lilikuwa linapita pale. Fedha tunazozipata zinapunguza tatizo, lakini bado tatizo ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine lililokuja kujitokeza kwenye suala hili la TARURA ni wale wakandarasi wetu wanaopewa miradi ile kuitekeleza kwenye Halmashauri zetu. Kwa mfano, Bunda Mjini pale, Mkandarasi wangu yule aliyepewa kazi pale, kasi yake bado ni ndogo sana. Vile vile fedha hizi za ujenzi wa barabara, leo unaambiwa barua ya kwanza fedha zimekuja shilingi milioni 150 kwa maana ya utekelezaji wa barabara za mitaa. Bado hizo hujajua zimeelekezwa kwenye barabara gani, kuna fedha zingine zimekuja.

Mheshimiwa Spika, bado hizo hujajua zimeelekezwa kwenye barabara gani kuna fedha zingine zimekuja. Wakati mwingine unapata wakati mgumu kwa sababu, siwezi kujua ni fedha zipi katika mradi huu na ni fedha zinazotekeleza mradi huu. Kwa hiyo, niwaombe watu wa TARURA wasimame vizuri na kwa sababu uwezo wa watu wetu hawa umeonekana bado upo chini, hivyo ni vizuri TARURA wao wenyewe wasimame imara kuzihakikisha kwamba fedha hizi zinafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais anatoa fedha kwa maana ya kuhakikisha kwamba barabara za mitaa zinakaa vizuri, halafu unapokuja kufika mwisho, atakapokuja kuangalia zile barabara akute wananchi wanamlalamikia kwenye maeneo hayo hayo, kwamba barabara hazitengenezwi, kumbe saa zingine fedha zipo na Mkandarasi hajafanya kazi hiyo. Kwa hiyo ni jambo ambalo nawaomba TARURA wasimame vizuri hapa na Wizara hii ya TAMISEMI, wasimamie wakandarasi wetu vizuri ili waweze kutekeleza miradi yao vizuri ili iendane na thamani halisi ya fedha zile ambazo zinazotolewa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine hapa ni kuhusiana na vyumba vya madarasa. Vyumba hivi vya madarasa vimekuwepo kwa muda mrefu ambavyo wananchi wao wenyewe walivianzisha, tunaishukuru Serikali kwa sababu inakuwa ikitoa fedha kwa maana ya kwenda kupunguza tatizo lile, lakini bado tatizo ni kubwa. Tuiombe tu TAMISEMI iongeze fedha ili vyumba vile viweze kumaliziwa na kukamilika vyote ili watoto wetu wote waweze kusoma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kuhusu vituo vya afya. Niishukuru TAMISEMI kwa sababu tumepata fedha hapa kwa ajili ya utekelezaji wa vituo vya afya, tumepata shilingi milioni 250 ambazo tulipeleka kule kwenye Kata yetu ya Waliku ambayo sasa tunaelekea kumaliza jengo lile. Niiombe tu TAMISEMI kwamba tutakapomaliza ujenzi wa lile jengo watuletee vifaa vile ambavyo vitaendana na lile jengo ili kwamba huduma ya afya iweze kutolewa kwa wananchi wetu wale, kwa sababu jiografia ya eneo lile Kata ywa Waliku ipo pembeni, wananchi kutoka kule waje Bunda Mjini ni takribani kilomita 16.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Getere, taarifa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa kwamba siyo tu kwamba wapeleke vifaa, ni kwamba tumepewa shilingi milioni 250 kujenga vituo vya afya na bado kuna milioni 50 inakuja. Kwa hiyo tunaomba watayarishe milioni 250 zilizobaki ziwahi mapema kumaliza majengo yaliyobaki.

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na Mheshimiwa Getere kwa sababu tunatoka Wilaya moja taarifa yake naipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, hayo matatizo ya vituo vya afya ni pamoja na zahanati ambazo zimejengwa kule Mcharo na Kijambiga ambazo na zenyewe ziko kwenye hatua ya mwisho, ambazo tutaiomba TAMISEMI itusaidie kuzikamilisha vizuri na vifaa tiba viweze kupelekwa kwenye maeneo yake yale ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiografia ya Mji wa Bunda haijakaa vizuri sana na bado barabara zile za mitaa kama nilivyosema na zenyewe bado ni tatizo hasa barabara ile ya kutoka Guta kuja Kinyambiga, kutoka Kinyambiga kuja Kabasa, Kabasa kuja Bunda Mjini, hizo na zenyewe Wizara iweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mara baada ya kusema hayo, nakushuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Lakini mimi ninayechangia sina elimu ya juu, nina elimu ya chini, kwa maana ya elimu ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Juzi alikuwa anazindua suala la utalii kwenye nchi yetu, ambapo ukija ukiangalia kwenye Mkoa wa Mara, Mbuga ya Serengeti kwa sehemu kubwa iko upande wetu; kwa hiyo tunampongeza kwa kazi kubwa hiyo anayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Wizara hii ya Elimu, Sayansi, na Teknolojia, mimi nilitaka kuzungumza jambo moja tu kuhusiana na suala la vyuo vya ufundi. Kwamba, vyuo vya ufundi vikiboreshwa aidha vikaongezeka vikawa vyakutosha kwenye maeneo yetu, ikiwezekana kila Wilaya au Jimbo kutokana na wingi wa vijana wetu vitatusaidia kuwafanya wao wafundishwe vitu ambavyo wanaviishi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimekuja kupata shida hapa kwenye nafasi hizi zilizotolewa za ualimu. Kwamba shule moja inahitaji mwalimu mmoja, lakini waliyotuma maombi pale kwenye nafasi hiyo ya mwalimu mmoja ni walimu zaidi ya 800; halafu anachukuliwa Mwalimu mmoja, wale 790 wanabaki. Halafu kila wanapobaki muda wao wa kustaafu unazidi kuwasogelea. Najiuliza muda wao utakapoisha hawa watu watakuwa wanafanya nini? Lakini pia najiuliza hawa watu wakifundishwa kwenye vyuo vya ufundi kwa mfano Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Kisangwa kile kilichopo pale Bunda, kikaboreshwa vizuri na Serikali kikaweza kuchukua vijana wetu wengi, wale waliomaliza Darasa la Saba hata wengine waliomaliza Kidato cha Nne ambao hawakupata nafasi ya kuendelea; wakaenda pale wakafundishwa shughuli zao za mikono ambazo wao kwenye maeneo yao wanayoishi hazitawafanya zitawafanya waweze kumudu maisha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sasa ukija ukiangalia walimu wamepata elimu yao ya ualimu lakini nafasi zinazotoka ni kidogo na hawawezi kuitumia nafasi hiyo. Kwa hiyo, mimi nikawa napenda kuishauri Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kwamba kwenye Mpango wake mkubwa ni vizuri ikaboresha vyuo vya ufundi. Ili kwamba tukiwa na wimbi kubwa la watu ambao wamekaa hawawezi kufanya kazi, lazima tuwe tunajiuliza mara mbili mbili matokeo yake ni nini? Lakini hata wale wanaosoma sasa leo lazima waone wale wenzao waliotangulia wanachokifanya ni kitu gani au ninafasi gani wanayoipata na kama wanaona nafasi ni kidogo lazima watafute njia ya pili ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia mimi sidhani kama ingewezekana Taifa zima hili la Tanzania watu wote tukawa tuna degree; atakayeweza kumbebea mwenzake mzigo atakuwa nani? Haiwezekani. Kwa hiyo mimi ninaishauri Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu kuboresha vyuo vya ufundi tena kwa speed kubwa kwa sababu vijana wetu wakipata utaalam wao pale utawawezesha wao kuishi mitaani kwa kufanya shughuli zao wao wenyewe na kwa kujiajiri wao wenyewe. Na kujiajiri kwao wao wenyewe kutawafanya shughuli yao wao wanayoifanya wachange kwenye mfuko wa Serikali kwa kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu vijana wetu wa bodaboda, kwa mfano leo hii tusingekuwa na mpango huu wa bodaboda kwamba vijana wamejiajiri kwenye bodaboda, wale wote wangekuwa wako mitaani wamekaa wanasubiri kuomba ajira Serikalini ilhali nafasi zenyewe zinazotoka za ajira ndiyo hizo; kwamba kati ya watu 800 anatakiwa kuchukuliwa mtu mmoja na wale wangeongezeka ingekuwaje? Kwa hiyo wimbi la watu ambao hawana kazi lingekuwa ni kubwa kuliko uhalisia wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana mimi nilikuwa nashauri kwamba ni vizuri Wizara hii ikaboresha vyuo vya ufundi na kuviongezea upana wake ili iweze kuchukua wanafunzi wengi zaidi ili hawa vijana wetu watakapomaliza kujifunza utaalam wao watajiajiri wao wenyewe kama vile ambavyo vijana wetu wa bodaboda walivyojiajiri wao wenyewe. Tofauti na hapo kwa kweli itakuwa hata hawa ambao wamepata elimu zao wanafika sehemu wanataka kuchukia kile alichokisomea.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine najiuliza, mtu wakati mwingine anakuja ana degree yake, amemaliza shule ana degree; lakini hata ukimuuliza ile namna ya kujieleza baadhi yao hata kujieleza tu hawezi. Sasa unajiuliza wewe hata kama umesoma ni kweli una degree, degree hii hata huwezi kwenda kuiishi mitaani au kwa mazingira yako unayoyaishi wewe huweizi kuitumia inakuwa inakusaidiaje? Ndiyo maana nasema, watu wakifundishwa katika uhalisia wao wa maisha yao utawaondolea umasikini kwa sehemu kubwa. Lakini pia itawafanya wao wajiajiri wao wenyewe, vilevile wao pia watakuwa fundisho kwa wenzao. Kwamba nikiona njia hii ya ajira imebana nitakwenda njia nyingine ya pili ambayo itanifanya na mimi niishi kama fulani anavyoishi yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukisema watu wote wafanye kazi aina moja naamini kwamba nafasi hizo pia hazitaweza kupatikana. Mwisho watu watakaa kubaki kulalamika Serikali kwamba Serikali haitoi ajira lakini Serikali itatoa ajira baada ya kuwa ina income ya kuweza kuwalipa watu Mishahara. Na Serikali kupata mishahara ya kulipa watu ni lazima watu wawe wanafanya kazi, wanapata pato, wanalipa kodi na Serikali inapata fedha ya kuwalipa watu mishahara. Kwa sababu Serikali haiwezi kulipa watu mishahara kwa kupitia fedha ya kukopa, haiwezekani; ni lazima watu wafanye kazi, wazalishe wapate fedha kwao wao wenyewe na fedha zao zitumike kuwalipa mishahara wananchi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi niliona kwenye suala hili la Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia nitoe mchango wangu huo ili kwamba Wizara hii ikituboreshea chuo chetu kile cha Maendeleo ya Wananchi pale Bunda, ikakipanua, itaweszesha vijana wetu wengi waende kupata mafunzo yao pale na mafunzo yale yatawawezesha kuishi vizuri kwenye eneo lao baada ya kuwa wanafanya shughuli zao ndogondogo za mikono na zitakazowezesha kuendesha maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya kusema hayo, nakushuruku kwa kupata nafasi hii, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru na nimshukuru Mungu kwa kupata nafasi hii mchana huu wa leo ili niweze kuchangia. Naishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo imeendelea kuifanya katika Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda ambapo kwa kipindi hiki cha takribani miaka miwili na sehemu tumeshapata fedha za maendeleo kwenye idara ya elimu, afya na TARURA, zaidi ya shilingi biloni 10, tunaipongeza Serikali. Pamoja na kwamba bado kwenye maeneo hayo kwenye barabara za TARURA bado tuna changamoto, tuiombe Wizara iendelee kuwasaidia hao watu wa TARURA kwa kuwatengea fedha za kutosha ili miundombinu yetu ya barabara kwa wananchi yetu iweze kutekelezwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kuhusu TACTIC. Halmashauri ya Mji wa Bunda tupo kwenye ile miji 45 inayoendelezwa. Wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini mradi huu wanausubiri kwa hamu kubwa; na kwa sababu tulishawapa matumaini makubwa na kadri ambavyo viongozi wetu wamepita katika Wilaya yetu wakatoa ahadi kwenye mradi huu, ningeiomba sana Serikali ya Awamu ya Sita na Wizara ya TAMISEMI kuhakikisha kwamba mradi huu unatekelezwa kabal aya 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Bunda tulipata katika mradi huu lami kilomita 25.3, soko jipya la kisasa, machinjio, stendi na dampo la uchafu. Sasa, vitu hivi visipotekelezwa kwa kipindi hiki vinaenda kuwakatisha wananchi wetu tamaa. Kwa sababu jiografia ya Mkoa wa Mara mtu yeyote anayetokea Mwanza Kwenda Mkoa wa Mara anapitia Bunda. Kwa hiyo jiografia ya Mji wa Bunda ikikaa vizuri inaleta jiografia nzima ya Mkoa wa Mara kaukaa vizuri. Kwa hiyo ni ombi langu kubwa kwa TAMISEMI kuwaomba kwamba mradi huu wa TACTIC uwewze kutekelezwa vizuri. Kwa sababu jambo hili…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mhehsimiwa Robert Maboto, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Cosato David Chumi.

TAARIFA

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi naomba kumpa Mheshimiwa anayezungumza taarifa kwamba, kufanikiwa na kutekelezwa kwa haraka kwa mradi wa TACTIC katika miji 45 likiwemo Jiji la Mbeya, pamoja na kuboresha miundombinu itasaidia halmashauri hizo kuwa na miradi ambayo itakuwa chanzo cha mapato ambayo baadaye itaipunguzia Serikali mzigo kwa hiyo ni muhimu ikatekelezwa kwa wakati, naomba kuwasilisha.

SPIKA: Mheshimiwa Maboto, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa sababu na yeye ni mhanga kama mimi hapa. Kwa hiyo jambo hili kwa wananchi wetu ni jambo muhimu sana na ni vizuri kwa Serikali kwa sababu ilishatoa ahadi kwa wananchi ikatekelezwa. Pia itasaidia kuifanya halmashauri iweze kupata vyanzo vya mapato. Kwa mfano, stendi yetu ya Bunda Mjini mabasi yote ya Mkoa wa Mara yanayokwenda Mwanza yanayotoka nje ya Mkoa wa Mara lazima yapite kwenye Halmashauri ya Mji wa Bunda. Kwa hiyo ni hakika kwamba mradi huu ukitekelezwa utawafanya Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda na wananchi wote wa Bunda kwa ujumla kuona kwamba wamepata mapato ya kutosha katika Halmashauri yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni maombi maalumu kwa ajili ya jengo la Makao Makuu ya Utawala Halmashauri ya Mji Bunda. Jengo hili lilishajengwa, lakini tatizo la jengo hili halina uzio. Kwa hiyo kwa sababu jengo hili limejengwa na halina uzio kwa hiyo mtu anaweza akatokea mahali pengine popote kuingia katika Halmashauri ile. Kwa hiyo hata namna ya kufanya ulinzi kwenye eneo lile inakuwa ni ngumu. Ombi langu ni kuiomba Wizara iendeleee kutenga bajeti kwa ajili ya ukamilishwaji wa eneo hili. Bado tunahitaji uzio, tunahitaji mitaro ya uturirishaji maji na hakuna ghala la kutunzia vifaa. Ukiingia kwenye lango la Halmashauri kwenye jengo hilo pale kwenye mlango unapoingilia ndipo unakuta Halmashauri wamelaza nondo hapo na cement kwa ajili ya maendelezo mengine ya shughuli za maendeleo katika Halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Spika, ombi lingine ni kuhusu maboma ambayo yalijengwa na wananchi katika Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda ambayo bado haijakamilishwa. Wananchi walijitolea nguvu zao, wakafanya kazi kubwa na sasa wanaomba ukamilishwaji.

Mheshimwia Spika, kuna Shule ya Msingi Bigwitu yako majengo mawili, Shule ya Msingi Bikole lipo jengo moja, Shule ya Msingi Kabarimu yako majengo mawili na Shule ya Sekondari Mpya ya Kata ya Nyamakokoto mbayo Serikali imeweka pale fedha zaidi ya milioni 500, lakini kulikuwa pia kuna na nguvu za wananchi pale ambazo wao walikuwa wameshajenga majengo yao pale. Ukamilishwaji wake; tuiombe TAMISEMI sasa itusaidie kuhakikisha kwamba jambo hili linakamilishwa ili Halmashauri ya Mji wa Bunda uweze kukaaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ni kuiomba Serikali. Suala la ajira hizi ambazo zimetolewa na Serikali, nimalizie, kwa kumalizia tu; iligawanywa katika mikoa yote. Hapa tulipo simu za wananchi ambazo tunazipata kwa ajili ya kutuambia tuwafanyie mpango ili wapate ajira Serikalini ni simu ambazo hatuna majibu. Ukitengenezwa mgawanyiko wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia Wizara ya Maji, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata fursa hii kwa kunipa pumzi mchana huu wa leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo ameendelea kutusaidia katika Halmashauri ya Mji Bunda katika kuhakikisha kwamba, Mradi mkubwa wa Maji wa Nyabehu umekamilika, ambapo mpaka sasa Mradi wa Nyabehu umekamilika kwa asilimia 99, ulikuwa una thamani ya karibia shilingi bilioni 10 na sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wananchi ambao wananufaika na mradi huu ni zaidi ya wakati 178,000. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa sababu, wakati anaingia kwenye nafasi hii, mradi huu bado ulikuwa hautoi matokeo ambayo wananchi wa Bunda Mjini wanayategemea. Kwa sasa tumeshapata matumaini kwa sababu, mradi huu unatoa maji safi na salama kwa kiwango kikubwa. Sasa ombi letu kwa Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii ya Maji, ndugu yangu Mheshimiwa Aweso, ni kuhakikisha kwamba, atusaidie mambo madogo madogo yale yaliyobaki ya usambazaji maji kwenye maeneo yale ambayo bado maji hayajafika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna Mradi wa Ujenzi wa Tanki la Maji Misisi-Zanzibar ambapo tenki hili litahakikisha kwamba, wananchi wote wa Kata ya Sazira na wengine wa Kata hii ya Kabasa watapata maji mara baada ya kuwa tenki hili limekamilika. Mpaka sasa tumepata zaidi ya shilingi milioni 733 ambazo naamini Mheshimiwa Waziri tumeshapokea kwako fedha milioini 583 kwa ajili ya utekelezaji wa tenki hili ambalo litabeba maji zaidi ya lita laki moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba, jambo hili likishakamilika maeneo hayo tutapunguza uhaba mkubwa wa maji na malalamiko kwa wananchi wetu ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakiona mradi mkubwa wa maji kwao na maji yako karibu kilometa tatu, tano hivi kuingia Ziwa Victoria, halafu wakawa wanashangaa maji hawayaoni, lakini sasa wananchi wa Bunda Mjini wameanza kunufaika na mradi huu mkubwa ambao unatekelezwa pale Bunda. Mradi huu nakumbuka mwaka jana Mheshimiwa Rais alikuja kuuzindua na baada ya kuuzindua umeleta matokeo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, ni ujenzi wa tenki la maji ambalo litasambaza Manyamanyama na Mugaja. Lenyewe hili lina thamani ya shilingi bilioni moja na milioni 65 ambazo sasa mchakato unaendelea. Ombi langu ni kwamba, Waziri aweze kutuwezesha sisi ili tuweze kupata fedha hizo Halmashauri ya Mji wa Bunda, ili mradi huu uweze kutekelezwa na wananchi wetu waendelee kunufaika na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni ujenzi wa tenki la maji ambalo litasambaza maji Kata ya Balili, Rubana na Kunzugu. Maeneo haya tukishawatengenezea tenki la maji, mradi ambao utakuwa unagharimu karibu zaidi ya milioni 759, naamini Mheshimiwa Waziri anafuatilia jambo hili vizuri, tunamwomba tuendelee kupata fedha ili tenki likamilike na wananchi wetu wale wapate maji vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jiografia ya Mji wa Bunda ilivyo na jinsi ambavyo tuko karibu na ziwa, lilikuwa ni jambo la kushangaza kwamba, sisi ndio tulikuwa tunakuwa walalamikaji wa kwanza kukosa maji, lakini sasa namhakikishia kwamba, atakapokuja Bunda kwa mara nyingine ataona furaha iliyopo kwa wananchi wake kutokana na kwamba, wamepata huduma nzuri ya maji wanapata maji safi na maji salama kwa wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu ni kuhakikisha kwamba, jambo hili…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa mzungumzaji Taarifa kwamba, anapozungumza Bunda azungumzie Jimbo la Bunda Mjini. Jimbo la Bunda la kwangu bado lina ukame mkubwa sana wa maji. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Robert, Taarifa hiyo.

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Mheshimiwa Getere anafahamu jimbo lake na mimi nafahamu jimbo langu. Mimi Jimbo langu ni la Bunda Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni suala la upotevu wa maji na jambo hili nimeona tatizo kubwa liko kwenye ile mipira ya kuvutia maji. Hawa ndugu zetu wenye viwanda vya kusambaza mipira hii naamini mipira hii haiko katika viwango vile ambavyo vinatakiwa. Yale mabomba yale ya maji wananchi wanayanunua, wakiyatumia kwa muda mfupi, ndani ya miezi mitatu mabomba yalishapasuka ambayo yanawaingiza wananchi kwenye gharama nyingine tena ya kununua mabomba mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naamini jambo hili na kwa sababu, wale ni wadau wa maji ni vizuri Waziri akawawekea mkazo kwenye mabomba haya ya maji. Yawe mabomba ambayo yanalingana na thamani halisi ya fedha ambazo wananchi wetu wanazitoa. Kwa sasa jambo ambalo litakuja kujitokeza pale kubwa ambalo ni baya ni hilo la mabomba ya maji kupasukapasuka kwa sababu, tumekuwa tukipata malalamiko mengi sana kwa wananchi wetu kwamba, mabomba wanayoyatumia kwa muda mfupi yanakuwa yalishapasuka, halafu wanaingia tena gharama za kununua mabomba yale kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, nimwombe Mheshimiwa Waziri, tuna mradi pale wa kutibu majitaka na maji safi, pale Bunda, lakini tulishapata eneo pale karibu eka 100, kule Butakare, kilichobakia tu ni kupata fedha za fidia ili kwamba, eneo lile na kutokana na mwingiliano wa wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini, ni vizuri tukapata fedha hizi za kulipa fidia maeneo haya, ili mradi ule uweze kutekelezeka ili uweze kuleta manufaa makubwa katika Mji wa Bunda. Kwa sababu jiografia ya Mji wa Bunda ndio picha halisi ya Mkoa wa Mara kwa mtu yeyote anayekwenda Mkoa wa Mara, picha nzuri ya Mkoa wa Mara anaianzia kwa kuona Bunda. Kwa hiyo, akikuta jiografia ya Bunda imekaa vizuri hasa kwenye miundombinu ya maji anajua hata huko anakokwenda lazima atakuta hali halisi ni nzuri zaidi. Kwa hiyo, ombi langu ni kuhakikisha kwamba, jambo hili linafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia jambo lingine nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba, yule Mkurugenzi wetu wa BUWASA aliyeko pale Bunda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii mchana huu wa leo ili na mimi niweze kuchangia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya kwa ajili ya kupeleka fedha za maendeleo katika majimbo yetu ili kukamilisha miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niishukuru Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi inayoongozwa na Mheshimiwa Makame Mbarawa na Naibu wake kwa kazi kubwa ambayo wameendelea kuifanya, lakini pia kwa namna ambavyo wametekeleza mradi mkubwa wa barabara ya kiwango cha lami kutokea Jimbo la Mwibara, Jimbo la Bunda Mjini, na Jimbo la Bunda Vijijini. Barabara hii ilisumbua kwa muda mrefu lakini kwa sasa imeendelea kukamilishwa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Wizara ni kuhakikisha kwamba barabara hii wakati inajengwa tuta lile lililowekwa kwenye barabara ile limekuwa juu sana kuliko makazi ya wananchi wetu. Niwaombe sana Wizara ikumbuke kuwawekea wananchi wetu barabara zile zinazoingia katika makazi yao ili ziweze kuendana na hali halisi ya barabara yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine katika barabara hii. Wizara ituwekee taa za barabarani ambazo zitakuwa zinatokea kwenye maungano ya barabara pale kuelekea barabara ya Kibara na hii barabara inyokwenda Nyamuswa, watuwekee taa za barabarani. Lakini pia katika barabara hii tuna taa za upande mmoja kutokea Balili Kwenda Nyasura, ambako taa hizi zimewekwa upande mmoja na upande mwingine hakuna taa. Kuhusiana na jambo hili mimi nilishajaribu kuzungumza na Meneja wa TANROADS wa Mkoa, nikamuomba, kwamba, katika meneo mengine mengi ambayo mimi nayaona taa zote za barabarani zimewekwa kwa pande zote mbili, ni kwa nini, Bunda tu peke yake kuwe upande mmoja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri atusaidie kwenye jambo hili ili liweze kuendana na hali halisi; ambapo taa zinawekwa katika maeneo yetu. Lakini jambo jingine, Mheshimiwa Waziri nikushukuru katika Jimbo letu la Bunda Mjini katika Bajeti tumepata taa za kuongozea magari kwenye makutano yale ya barabara ya Kisorya, Nyamuswa, Mwanza na Musoma; tumepata taa za kuongozea magari. Na jambo hili mimi nililisema nikasema kwenye eneo lile tukisema tuweke ule mzunguko eneo lile ni dogo kwa sababu litatulazimisha kwenda kubomoa makazi ya wananchi wetu. Naishukuru Wizara, na kwa sababu imekubaliana na hili jambo lile likifanyika naamini kwamba litaufanya Mji wetu wa Bunda uweze kukaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia jambo jingine tunaishukuru Wizara kwa sababu wanatekeleza miradi mikubwa pale ya kujenga mizani katika Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda Kata ya Balili na kata ya Buta. Sasa mizani hii ina muda mrefu. Niwaombe sana Wizara muhakikishe kwamba viongiozi wetu wa Mkoa wa TANROADS wanasimamia miradi hii ili iweze kukamilika vizuri, lakini mizani hii ikikamilika kwa wakati itatusaidia kulinda zile barabara zetu, hasa hii barabara mpya inayokwenda Kisorya na inayokwenda Nyamuswa, ya lami, mzani ule utatusaidia kulinda sana ule ulioko kule Buta; na hii barabara kuu ambayo inakwenda Mwanza na Musoma. Mizani hii ikamilika kwa wakati ili iweze kulinda barabara hizi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Mheshimiwa Waziri jambo jingine ni kuhusiana na Mfuko wa TARURA. Tuiombe Wizara iendelee kuwaongezea fedha watu hawa wa TARURA ili waendelee kutusaidia katika barabara zetu zile za mitaa ili zikamilike. Kazi imefanyika Mheshimiwa Waziri lazima tukuthibitishie hilo lakini bado tatizo lipo, kwa sababu barabara zile kwa muda mrefu zimekuwa hazifanyiwi matengenezo. Kwa kipindi hiki tumeona matenegenezo yanafanyika na wananchi wanaona hatua zinachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana tuendelee kuwapa TARURA nguvu kwa kuwapitishia bajeti ya kutosha ili kwamba weze kutusaidia kuhakikisha kwamba barabara hizi zinapitika kwa muda wote, na hasa kwa sababu mji wa Bunda ndio sura halisi ya Mkoa wa Mara. Utakapokaa vizuri mji wa Bunda ndiyo picha halisi ya Mkoa wa Mara, na kwa sababu pia tuko pembezoni mwa Mbuga ya Serengeti. Mtu yoyote mtalii anayekwenda Mbuga ya Serengeti lazima apite Bunda. Mtu yoyote anyetoka Mwanza nakwenda Silali Kenya lazima apite Bunda. Anaweza asipite mahali pengine popote lakini Bunda Mjini lazima apapite. Kwa hiyo ni vizuri Mheshimiwa Waziri jambo hili la taa za barabarani, taa za kuongoza magari zikawekwa katika Halmashauri ya Mji wa Bunda ili iweze kuleta mvuto mzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jambo jingine ni suala la Barabara ile ya Manyamanyama, Kabulabula, Muhoji, Masinono Kwenda Bugwema ambayo inakwenda kwenye shamba la kilimo la Bugwema. Barabara ile ni pamoja na barabara ile ambayo inatoka Musoma Mjini kwenda Majita ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo Barabara hii nayo ya Manyamanyama, Kabulabula, Muhoji, Masinono ikijengwa kwa kiwango cha lami itawasaidia wale watu wenye magari makubwa ambao wanalazimika kwenda kupita kuzunguka kule mbali, wakapita hapa ikawa ni rahisi kwenda kwenye shamba letu la Bugwema na kwenda kuchukua mazao ya wananchi huko. Kwa hiyo niwaombe sana Wizara jambo hili na lenyewe waliangalie ili waliweke kwenye mpango wao ili liweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii itakapokamilika vizuri itaufanya Mji wetu wa Bunda ukae vizuri. Na sasa hivi tatizo kubwa ambalo tunalo pale lililobakia ni hizo barabara za mitaa. Niwaombe sana Wizara, na kwa sababu bahati nzuri tumepata Meneja mzuri pale wa TARURA wa Wilaya ndugu yangu Baraka na Meneja wa TANROADS wa Mkoa, tunashirikiana nao vizuri kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo hili la uchakavu wa barabara katika maeneo yetu. Niwaombe sana Wizara watu hawa twende nao vizuri ili waweze kutusaidia kuhakikisha kwamba changamoto zetu hizi za wananchi tunazitatua vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushukuru na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya. Pia nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya kwa ajili ya Taifa letu. Juzi ameongeza asilimia 23 ya mishahara ya watumishi wa Serikali, ambao naamini ametimiza wajibu wake kwa nafasi yake, lakini na watumishi wa Serikali kwa sehemu yao na wao wana sehemu yao ya kutimiza wajibu wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo maji ni uhai, chakula nacho ni uhai, lakini pia huduma za afya nazo ni uhai. Kilimo ni uti wa mgongo wa kwetu sisi Tanzania, lakini pamoja na kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu, wakulima wetu uwezo wao wa kulima chakula chao, tofauti na mikoa mitano, mikoa mingine wananchi wetu wanalima chakula chao ambacho hakiwezi kuwatosheleza hata kwa mahitaji yao kwa mwaka, jambo ambalo ni hatari kubwa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo matatu ni mambo muhimu kwa afya ya binadamu. Leo mimi Mbunge nasimama Bungeni kuzungumza bila ya kuwa na afya bora, bila ya kunywa maji, bila kula chakula, uwezo wa kuzungumza sitaupata. Kwa hiyo, najaribu kuishauri Wizara ya Kilimo kwamba suala la chakula ni suala muhimu. Jambo muhimu hapa Taifa letu litengeneze utaratibu au Wizara na wataalam wetu wa kilimo, nchi yetu iwe na uwezo wa kujiwekea akiba ya chakula kwa muda angalau miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi za wenzetu wao wana mafuta yao kwa sababu uwezo wao ni mafuta yao wamejiwekea akiba ya kutosha, wanaweza wakaamua kuyafungia mafuta yao halafu sisi huku Tanzania tukawa tunalalamika, wakati hatuzalishi. Sasa na sisi kwa nchi yetu kwa sababu Mungu ametupa ardhi, na mvua tunapata kwa kiasi cha kutosha, ningeishauri Wizara ije na mpango wa kuhakikisha kwamba nchi inajiwekea akiba ya chakula kwa muda wa miaka mitano, angalau ikitokea siku moja au miaka miwili au mitatu mvua hainyeshi, wananchi wetu waweze kupata chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi tunayo, mvua tunapata ya kutosha, lakini bado wakulima wetu chakula wanachokilima hakitosheleza mahitaji yao ya mwaka. Napata tabu sana kwenye jambo hili. Kila jambo sisi kama nchi au Wizara hatutakuwa na uwezo wa kujitosheleza, ardhi tunayo mvua tunapata, halafu wakulima wenyewe wanalima chakula kidogo ambacho hata wao wenyewe hakiwatoshelezi. Kwa hiyo Wizara itengeneze utaratibu au mkakati wa kuhakikisha kwamba wananchi wote wanahamasishwa kuhakikisha kwamba wanajilimia chakula ambacho kinawatosheleza kujilinda kwa mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Mara hasa Wilaya ya Bunda zao kuu la kibiashara pale lilikuwa ni pamba, lakini leo pamba takribani miaka 10 haifanyi vizuri. Sio kwamba wakulima wale walikuwa hawana uwezo wa kulima isipokuwa tatizo ni soko, soko limeleta tabu, kwa hiyo limesababisha wale wakulima, badala ya kulima pamba sasa na kwa sababu wanalima pamba halafu uwezo wa kupanga bei hawana, anayewapangia bei mtu mwingine, wao wamekata tamaa ya kulima pamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo wananchi wetu wamerudi kuwa maskini. Naiomba Wizara ya Kilimo kwa sababu ina wataalam wa kilimo ambao wao wanaweza kutusaidia kututafutia zao mbadala hasa Mkoa wa Mara ambao sisi zao letu kuu la kibiashara lilikuwa ni pamba ili kwamba zao lile Wizara itakalotuletea lipate kuwasaidia wananchi wetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kwa mchango mzuri.

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza kwa kupata nafasi hii ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara ya Fedha na Mipango. Awali ya yote namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya kwa ajili ya Taifa letu. Suala la bajeti yetu ya nchi 2022/2023, imeenda mpaka shilingi trilioni 41. Fedha hizi, shilingi trilioni 41, kuna fedha ambazo zinakwenda kwenye Wizara ya Kilimo na Chakula.

Mheshiiwa Spika, juzi wakati Wizara ya Kilimo inawasilisha bajeti yake hapa nilitoa mchango wangu na nikashauri kwamba ikiwezekana Wizara ya Kilimo na Chakula ijiweke tayari au ijipange ili kutuwekea akiba ya chakula nchini takribani miaka miwili.

Mheshimiwa Spika, bajeti yetu hii ili iwe imara, na iwe yenye uhakika, lazima wananchi wetu wawe na uwezo wa kupata chakula; na nchi kama nchi iwe na uwezo wa kujiwekea akiba ya chakula kwa muda walau hata miaka miwili ijayo. Leo kukitokea tatizo la njaa kwenye nchi yetu, kwa bajeti hii tunayoipanga leo hapa au tunayoipitisha hapa leo, kukitokea njaa kwa wananchi wetu, mipango yote itakayokuwa imepangwa kutekelezwa kati ya 2022/2023 haitafanyika kwa sababu wananchi watakuwa na njaa na nchi itaingia kwa ajili ya kuwanusuru wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Wizara ya Kilimo na Chakula wamepewa bajeti kubwa kwa mwaka huu, lakini bado jambo la akiba ya chakula nchini ni la muhimu sana. Tusipolizingatia hili, kuna siku Bunge litakaa, litatoa maamuzi na kupitisha bajeti, lakini katikati ya safari wakati tunaendelea kukitokea njaa kwa wananchi wetu, bajeti ile itavurugika kwa vyovyote. Leo tukipata shida ya chakula hapa, lazima mipango mingine yote ile ambayo ilikuwa inapangwa kwa ajili ya utekelezaji wa maendeleo ya wananchi kwenye nchi yetu itavurugika. Taifa litageuka kufanya na kutafuta suluhu kwa ajili ya kuwapatia wananchi wake chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wizara ya Kilimo na Chakula jambo hili ilichukue na ilifanyie kazi. Wenzetu wa nchi za nje wamejiwekea akiba kwenye mambo yao; mafuta na vitu vingine, sisi Tanzania ardhi tunayo, mvua tunapata ya kutosha, na watu wapo. Tunakosaje kujiwekea akiba ya chakula cha nchi cha miaka miwili? Tukijiwekea akiba ya chakula cha miaka miwili, aidha miaka mitatu, yale yote ambayo tutakuwa tunakaa kwenye Bunge humu tukayapitisha, tuna hakika yatatekelezwa kwa sababu hatutapata mtikisiko katikati ya safari. Haiwezi kutokea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni Mamlaka ya Mapato Tanzania. Mimi ni mfanyabiashara, lakini wafanyabiashara walio wengi hapa nchini kwetu sio wafanyabiashara ambao wamesomea mambo ya biashara. Sisi tunafanya biashara kutegemeana na kile ambacho umekiona kiko mbele yako, aidha kwa namna ambavyo umepata mtaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Wizara ya Fedha kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania na kwa sababu wafanyabiashara wetu walio wengi hawakusomea mambo ya biashara, ni vizuri mamlaka ikaweka zile kodi za wafanyabiashara wazi ili kuongeza tija kwa walipakodi. Ila wafanyabiashara wale kwa sababu hawana elimu ya biashara, halafu yule anayekuja kuwafanyia hesabu ya kulipa kodi amesomea, kwa hiyo, anabaki kumsikiliza kila atakachomuamulia yeye. Wizara ikitengeneza mpango wa kutengeneza kodi ya uwazi, kwanza itawavutia wafanyabiashara wengi na kujua viwango halisi vya kodi zao wanavyotakiwa kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huwa najiuliza, kwa mfano, kwenye bajeti hii ya Shilingi trilioni 41, labda fedha ambazo zinatoka kwa wafanyabiashara labda ni Shilingi trilioni 12 au 13, halafu wafanyabiashara na walipakodi wale wote ambao wanalipa, kama ni wafanyabiashara mle kwenye idadi yao, inajulikana wako wangapi? Kila mtu analipa kiasi gani? Kama kweli tunataka kuondoa hii sintofahamu iliyopo kati ya wafanyabiashara na Mamlaka ya Mapato, pangewekwa utaratibu kila mmoja akawa anajua kodi yake atakayoilipa kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine linatolewa jedwali tu ambalo linamwonyesha Maboto mwaka huu fedha zitakazotakiwa kuchangia kwenye kodi ya Mamlaka ya Mapato ni kiasi fulani kwa mwaka, na ikishatolewa hiyo hakutakuwepo na mazungumzo tena na mtu mwingine. Watu wa Mamlaka ya Mapato watabaki kuja kukaa kufuatilia namna ya ulipaji wa zile fedha ambazo zimetolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili linapoachiwa tu kwao wenyewe wakaenda kuzungumza na watu ambao wao kwenye biashara wameingia tu kufanya biashara, jambo hili wakati mwingine linaleta sintofahamu kwa wafanyabiashara, halafu linawafanya pia nao wasione kwamba kile wanachofanyiwa ni haki kwenye kodi zile wanazokuwa wanakadiriwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, nataka kuzungumzia suala la madini. Jambo hili naona bado lina matatizo makubwa, kwa sababu wananchi wetu kwenye maeneo yao wanayoishi, wanakuwa ndio wa kwanza kuvumbua sehemu hii kama ina madini. Wao wenyewe wananchi wa kawaida tu, wakishavumbua lile eneo ambalo lina madini, hawa wataalam wetu wakijua kwamba wananchi wamegundua eneo ambalo lina madini, wanachokifanya ni kwenda kutafuta watu ambao wanakata leseni kwenye eneo lile, bila kuwahusisha wananchi wenyewe, wahusika. Jambo ambalo bado linaleta mgogoro mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ukija kuangalia, kiongozi wa wasimamizi wa wachimbaji wadogo wa madini nchini, yeye mwenyewe ni mfanyabiashara wa madini, halafu yeye ndio anawasimamia wachimbaji wadogo, halafu yeye mwenyewe huyo ndio akawatafute wenye mashamba akazungumze nao. jambo hili halikai vizuri.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kama Kiongozi wa Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini, anatakiwa atokane na watu ambao hana interest yoyote na uchimbaji wa madini ndiyo ataweza kuleta haki kati ya wenye mashamba, wenye leseni na wachimbaji wadogo. Anapewa mtu kusimamia wachimbaji wadogo aidha wenye mashamba na sehemu ya kuchimba madini ambaye yeye mwenyewe ana-interest na uchimbaji wa madini.

Mheshimiwa Spika, jambo hilo linaleta migogoro mikubwa sana kwa wananchi wetu linawafanya wao waone, wao kama raia wa kawaida wamevumbua eneo lile la uchimbaji wa madini, huyu yeye kwa sababu anakuwa yupo ngazi ya juu anakwenda anatafuta leseni anakuja kuwaambia kwamba eneo hili tulishapata leseni miaka mitano iliyopita. Wakati madini yamevumbuliwa labda zaidi ya mwaka mmoja au miaka miwili iliyopita. Sasa jambo lile linaleta mgogoro mkubwa sana kati ya wananchi na Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, wale Wasimamizi wao na Viongozi wa Wachimbaji Wadogo nchini, wanasababisha migogoro iendelee kuwa mikubwa jambo hili lisipowekwa vizuri kuna siku ninaamini litaleta mgogoro mkubwa kwa sababu wale wananchi wanaona kama wananyimwa haki zao, madini ya kwao, eneo la kwao, ardhi ya kwao, Babu yake na Bibi yake wamezikwa hapo halafu leo… (Makofi)

SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa kengele la pili imeshagonga.

MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)