Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Charles Muguta Kajege (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami naomba niende moja kwa moja kwenye hoja zangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nilipata bahati ya kuwa katika Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa tukapitia baadhi ya gharama katika baadhi ya mikoa. Kitu cha kwanza nilichogundua ni kuwa kuna ugawaji wa rasilimali ambao hauendani na hali halisi ya wananchi. Kwa mfano, kuna ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kishapu gharama yake itakuwa 1.5 billion, lakini ukiangalia gharama hizi zinazidi mara tatu ujenzi wa vituo vya afya ambavyo vimekubaliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, nataka nijielekeze katika Jimbo langu la Mwibara kwa sababu muda ni mfupi. Naomba katika Jimbo la Mwibara tupate maji kwa sababu licha ya kuzungukwa na robo tatu ya Ziwa Viktoria lakini maeneo mengi bado hayana maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya vilevile ni tatizo kubwa. Katika Kata za Nasimo, Kibara, Chitengule, Igundu, Nampindi, Kwilamba, Namuhula, Butimba na Nyamiholo bado hakuna huduma nzuri za afya. Katika maeneo hayo wananchi wamejitahidi sana kujenga maboma ya zahanati. Serikali iliahidi kwamba ingemalizia, naomba Serikali itekeleze na yenyewe wajibu wake.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni katika barabara. Barabara nyingi za Mwibara hazipitiki lakini hasa nitazungumzia barabara moja ambayo inatoka katika Kijiji cha Buguma - Chigondo haipitiki kabisa kwa sababu mkondo wa maji umekatisha katikati ya barabara. Kama leo nikiongozana na Waziri wa TAMISEMI akienda kuona jinsi ambavyo wanawake wanavuka pale sidhani kama atafurahi. Kwa hiyo, naomba barabara hii na yenyewe ipewe umuhimu katika kujengwa.

Mheshimiwa Spika, lingine ni elimu. Tuna matatizo ya vyumba vya madarasa, maabara, maktaba na nyumba za walimu. Vilevile maboma mengine ambayo wananchi wamejenga hajayakamilika, naomba Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ni kivuko kati ya Nasimo na Kisiwa cha Nafuba. Naomba Serikali itufikirie kutusaidia katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini tatizo lingine ni fidia kwa wananchi ambao walipisha mradi wa barabara ya kutoka Bulamba - Kisorya. Hawa nao bado hawajalipwa, naomba vilevile tufikiriwe.

Mheshimiwa Spika, lingine ni wakulima wa pamba. Hawa ni karibu mwaka wa tatu sasa hivi hawajalipwa pesa zao. Nafikiri Wizara husika inaweza kuangalia namna ya kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu ajira ziko katika maeneo makubwa mawili, kwanza ni kilimo. Bahati nzuri tunazungukwa na Ziwa Viktoria, naomba tupewe skimu za umwagiliaji maji na vilevile tupate mikopo ya matrekta.

Mheshimiwa Spika, lakini sekta nyingine ni uvuvi. Sasa hivi samaki wamekuwa wajanja huwezi ukawavua kwa kutumia zana za kizamani. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie namna ya kutusaidia kupata zana za kisasa kuliko Maafisa Samaki au Maafisa Uvuvi kuendelea kuwakamata wavuvi wetu kwa kutumia zana za zamani.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine naiomba Serikali kuangalia ulipaji wa madeni kwa wale waliotoa huduma Serikalini. Kwa mfano, nina kampuni mbili za jimboni kwangu; moja ni Swahili Ceramics, hawa wanaidai TBA zaidi ya milioni 139 kuanzia mwaka 2017 hawajalipwa, naomba Serikali ichukue hatua. Kampuni nyingine ni Wajenzi Enterprises ambao wanaidai Halmashauri ya Gairo milioni 10.5. Hawa nao wanasumbuliwa, naomba nao waangaliwe.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia halmashauri ya kwetu ambayo ni ya Majimbo mawili ya Mwibara na Bunda Vijijini; ili uweze kwenda katika Jimbo la Bunda Vijijini inabidi uvuke Jimbo la Bunda Mjini. Ushauri wangu naomba Bunda Vijijini na Bunda Mjini wawe katika halmashauri, moja sisi Mwibara tubaki peke yetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa muda huu, naomba na mimi niunge mkono hoja hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Vilevile nichukue fursa hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mwibara sasa hivi limeanza kung’ara, namshukuru sana. Pia, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Waziri wa TAMISEMI na wasaidizi wake pamoja na Katibu Mkuu wa TAMISEMI kwa kazi kubwa na jukumu kubwa sana walilonalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia katika maeneo yafuatayo: Kwanza ni katika sekta ya afya. Huduma za afya katika Jimbo langu la Mwibara bado haziridhishi. Tunavyo tu vituo vitatu vya afya vya Kasahunga, Kisorya na Kasuguti, lakini bado huduma zinazotolewa siyo za kiwango cha vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza ni kwamba, hivi vituo vimejengwa kwa muda mrefu sana. Kwa mfano, Kituo cha Kasahunga kina zaidi ya miaka 20, lakini bado hakijakamilika. Kituo cha Kasuguti kina zaidi ya miaka 15 bado hakijakamilika na Kituo cha Kisorya kina zaidi ya miaka saba bado hakijakamilika. Naiomba Serikali yangu sasa hivi iweze kutufikiria vizuri sana na kutupa kipaumbele iweze kukamilisha vituo hivyo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusia na Mfuko wa Jimbo. Naipongeza sana Serikali kwa kuongeza fedha katika mfuko huu, lakini nataka niishauri Serikali, pesa hizi naomba zigawanywe sawa sawa katika kila Jimbo.

Hakuna formula ambayo tutatumia hapa ambayo itafanya Jimbo lingine liweze kupata inavyostahili. Hakuna formula nakwambia! Fedha hizi zigawanywe kama ambavyo zimegawiwa pesa za TARURA, kila Jimbo lipate pesa sawa sawa. Tukishagaiwa hivyo sasa, kila Mbunge atakwenda kupambana na mambo yake huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo letu la Mwibara lina ardhi ya kutosha na lina maji ya kutosha, tunachohitaji ni elimu sahihi na mafunzo sahihi ili tuweze kutumia fursa zilizopo katika sekta hizo za uvuvi na kilimo. Jimbo letu tumeshaenda hatua moja mbele katika kutafuta Chuo cha VETA. Kata yetu ya Butimba imetoa ekari 57 kwa ajili ya ujenzi wa VETA hiyo. Naomba Serikali sasa itufikirie katika mgawo wa VETA katika kipindi hiki ambacho kinakuja nasi tuweze kupata Chuo cha VETA katika Jimbo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shule kama tatu kongwe za msingi ambazo majengo yake yameshachakaa na baadhi ya viongozi wa elimu wamekuja na wamesema kwamba, hayo majengo sasa hivi hayastahili kutumiwa tena. Naomba Serikali yetu sasa iweze kufikiria namna ya kujenga shule hizi kongwe za zamani ili ziweze kuwa salama na ziweze kuendelea kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala la posho za Madiwani limezungumzwa na wenzangu wengi waliotangulia. Wakati wa kampeni tunasema tunakwenda na mafiga matatu, yaani Rais, Mbunge na Diwani, lakini baada ya uchaguzi sisi wengine tunawafungia nje hawa Madiwani, tunakuwa tena hatuwatendei haki. Pamoja na mapendekezo ambayo yametolewa kwamba posho zao ziongezwe angalau ziwe shilingi 800,000/= kwa mwezi, mimi naona kama bado hazitoshi. Nashauri angalau wapate shilingi milioni moja kila mwezi ili waweze kufanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hao Madiwani ndio first responders wetu. Ndio wanaotatua matatizo ya wananchi sisi tukiwa huku Bungeni. Vilevile tusisahau kwamba na wao wanatumika kama ATM huko majimboni mwetu. Kwa hiyo, naomba nasi tuweze kuwafikiria waweze kupata posho ya kutosha waweze kufanya kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni zaidi ya miaka 13 sasa hivi tangu mradi wa ujenzi wa barabara ya Bulamba hadi Kisorya ufanyike. Kuna wananchi ambao walitoa nyumba zao zikabomolewa kwa ajili ya kupisha mradi huu, lakini bado mpaka sasa hivi hawajalipwa.

Naomba Serikali yetu sasa iharakishe malipo ya hawa wazee ambao wengi wao sasa hivi maisha yao yamekuwa magumu; wengine walipoteza nyumba zao na kwa hiyo, wameshindwa kujenga nyumba zao upya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na kaka yangu kwa mchango wake mzuri. Ni kweli, hiyo barabara ni ya muda mrefu na ni kweli kwamba sio wananchi tu wa upande wa Jimbo la Mwibara, hata wa Bunda Mjini mpaka kwenda kule Nyamuswa na wenyewe mpaka sasa hivi hawajapisha na wametenga maeneo yao kwa sababu Wilaya ya Bunda wanahitaji barabara ya lami ambayo itaenda kuunganika na Arusha. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kajege, unapokea Taarifa?

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naichukua kabisa na kuikubali hiyo Taarifa. Nami nasisitiza tena kwamba, haya malipo yafanyike mapema sana.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapo. Naunga mkono hoja hii ya TAMISEMI. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia katika hotuba ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Kama walivyofanya watangulizi wangu na mimi napenda nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ambayo amefanya katika kipindi hiki kifupi. Katika kipindi hiki kifupi tumeona miradi yote mikubwa inaendelea kutekelezwa kawa kasi kubwa na kwa ubora wa hali ya juu, mahusiano yetu na nchi zingine za nje yamepanuka zaidi na kukua zaidi, biashara yetu ya nje na ya ndani imekua na kupanuka zidi yote hii katika kipindi kifupi hiki cha utawala wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa TAMISEMI na timu yake kwa uongozi mzuri ambao wamefanya katika kipindi hiki kifupi. Kama walivyozungumza wezangu imekuwa ni raisi zaidi kumpata Mheshimiwa Waziri Kairuki, muda wote ukimpigia simu anapokea simu na bado anakuletea mrejesho ambao ni mzuri. Nakupongeza sana Waziri wetu Kairuki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Mwibara nitazungumzia baadhi ya changamoto ambazo ndiyo kikwazo kikubwa katika maendeleo yetu. Changamoto ya kwanza ipo katika Sekta ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitembelea katika shule za Mwibara nyingi hasa shule za msingi utakuta kuna upungufu mkubwa sana wa vyumba vya madarasa na hata vile vyumba vya madarasa viliyopo bado vimechakaa sana, wanafunzi katika chumba kimoja utakuta ni zaidi ya mia moja, vilevile vyumba hivi vingi havina sakafu kwa hiyo watoto wanasoma katika vumbi. Shule hizi ni kama Shule ya Msingi Gundu, Chitengule, Nampangala, Igundu, Buyomba, Susi, Bwanza, Shabirizi, Visambu, Bunele, Mlagata, Kinkombe na Kabaija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kutembelea katika hizi shule ni kama hazipo, kwa sababu majengo ni mabovu na mengine sasa hivi hawaruhusiwi hata watoto kuyatumia, kwa hiyo ni kama majengo hayapo. Vilevile upungufu wa madawati madarasa mengi hayana madawati kwa hiyo wanafunzi wanasomea chini. Sasa ukiangalia kwamba madarasa kwanza wanafunzi wako wengi katika darasa moja vilevile ni kwamba hawana madawati plus kwamba hata sakafu hazipo, ni chafu, ni vumbi kwa hiyo mazingira ya kusomea hawa wanafunzi yanakuwa ni magumu sana. Sasa inakuwa ni vigumu kumchukua mwanafunzi anatoka katika madarasa haya aka–compete na wanafunzi wengine ambao wanatoka katika mazingira mazuri sana ya elimu, kwa hiyo lazima naiomba Serikali iweze kuangali hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kingine ni upungufu wa walimu. Katiba hotuba ya TAMISEMI Mheshimiwa Waziri amesema kuna upungufu wa Walimu zaidi ya 89,932 katika shule za msingi wanaokuja kuajiriwa mwaka huu tunaona ni kama 13,000 peke yake ambayo ni sawa sawa na asilimia 14 hawa walimu ni wachache sana hawatoshi. Nilikuwa naomba Serikali yetu ifikilie namna ya kuongeza walimu, kwa sababu kama hatuna walimu hizi shule tunatoa elimu ya namna gani kama hatuna walimu na tulikubaliana kuanzia mwanzo kwamba mojawapo ya maadui wetu ni ujinga sasa hatutoweza kutoa ujinga kama walimu hawatoshi katika mashule yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ambayo ina changamoto ni katika sekta ya afya. Kwa sasa hivi ninavyo vituo Vitatu vya Afya Kisolya, Kasaunga, Kasuguti lakini bado havijakamilika, hivi bado havina majengo kutosha, vifaatiba havipo na wauguzi hawatoshi. Ningeomba sana Serikali ifikirie namna ya kuvikamilisha vituo hivi ili viweze kutoa huduma inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna maeneo ambayo sasa huduma ya afya iko mbali sana, kwa mfano Kata ya Igundu na Kata ya Namuhula nilikuwa nasikia kwamba Serikali ifikirie kujenga vituo vya afya katika Kata hizo mbili. Vilevile mwaka jana wakati ziara ya Mheshimiwa Rais katika Wilaya ya Bunda Tarehe Saba Februari, alielekeza kwamba hospitali ya Halmashauri nyingine ijengwe katika Jimbo la Mwibara, hilo agizo bado halijatekelezwa naomba hii Wizara ifikirie namna ya kujenga hiyo hospitali mapema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni michango ya wananchi kusaidia katika miradi ya maendeleo. Sina tatizo na michango, lakini tatizo langu ni kwamba michango mingine imekuwa ya holela. Kwa mfano, juzi nilipokuwa Jimboni, nilipita katika Kijiji kimoja cha Busambara. Hawa wameletewa pesa shilingi 54,824,000 kujenga matundu 20 ya choo. Wananchi wameombwa kuchangia tena shilingi 15,000 katika kila kaya. Nikawauliza, hivi gharama ya choo kimoja, tundu moja ni kiasi gani? Wakasema ni shilingi 1,500,000. Sasa kwa hesabu rahisi ni shilingi milioni 30. Nikawauliza, hizi Shilingi milioni 24 zinazobakia zinakwenda wapi? Hawakuwa na jibu. Nikawaambia wananchi msichange, hizo pesa zinatosha. Nilikuwa naomba, Serikali yetu iangalie vilevile kuhusu uchangishaji holela kutoka kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, bado kuna upotevu wa pesa katika Jimbo langu. Kuna wizi tuseme, kwa mfano, kuna shilingi milioni 300 ambazo zimepelekwa katika Kituo cha Afya cha Kasuguti, hazijulikani zilipo; kuna shilingi milioni mbili nilitoa katika Kata ya Nyamihoro kutoka katika mfuko wangu wa Jimbo, hazijulikani zilipo; kuna Shilingi milioni moja ilikuwa kwa ajili ya ujenzi wa choo katika Shule ya Msingi ya Msambara, VEO kakimbia nazo hazijarudi; na vilevile nilitoa shilingi 500,000 kwa ajili ya Nyamihoro na zenyewe hazijulikani zilipo. Naomba sasa wakati wa majumuisho nipate majibu ya nini kinafanyika au tutapataje hizi pesa ziweze kufanya maendeleo katika jimbo langu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kuanzishwa kwa kidato cha tano katika Shule za Sekondari za Nansimo na Buramba. Katika Shule ya Nansimo miundombinu imetosha, yaani kuna mabweni na madarasa, yanatosha; lakini katika Shule ya Buramba kuna madarasa lakini hakuna bweni. Nilipoongea na Afisa Elimu, akasema kwamba haiwezekani kuanzisha Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Buramba kwa sababu hamna bweni. Mimi naona hilo siyo tatizo, haya mambo tumeambiwa kuanzia miaka mitano iliyopita mpaka leo na shule haijaanzishwa. Naomba tuanzishe Kidato cha Tano, bweni litatufata baadaye. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWNEYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Charles Kajege.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja Ofisi ya Rais, TAMISEMI. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Vile vile kama ilivyokuwa kwa watangulizi wangu, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaifanya. Nataka niwahakikishie Watanzania kwamba kazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ndio ameianza, Watanzania tutegemee makubwa huko mbeleni tutakapokwenda. Pia, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wa Wizara hii kwa utendaji wao wa kazi nzuri ambazo wanafanya mpaka muda huu. Wameweza sasa hivi kuifanya Tanzania ipitike kwa urahisi angani, ardhini na majini, nawapongeza sana. Lakini vile vile nampongeza Engineer Mativila Mtendaji Mkuu wa TANROADS na Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mara Engineer Maribhe kwa kazi nzuri sana ambayo wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza tena Wizara hii kwa kuweza kukamilisha ujenzi wa Barabara ya Nyamuswa – Bunda - Bulamba – Kisole kwa kiwango cha lami. Kwa sasa tunasafiri na kusafirisha mizigo yetu kwa raha mustarehe, nawashukuru sana. Vilevile naishukuru Wizara kwa kupanga kukamilisha vipande vya barabara kati ya Kibara na Kasaunga na pia Kisole na Kisole Kivukoni kwa kiwango cha lami. Ukamilishaji wa vipande hivi utasaidia kuunganisha barabara nzima kutokea Kisorya mpaka Nyamuswa kwa kiwango cha lami, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nitumie fursa hii kuiomba Wizara sasa kuipandisha hadhi Barabara ya Kisambala…

MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: … Mugala na Musoma Vijijini. Barabara hii ina traffic kubwa sana ya watu pamoja na mizigo, na vile vile barabara hii ni shortcut ya watu waendao Musoma na vile vile watokao Musoma kwenda sehemu za Ukerewe naomba sana Wizara ifike kupandisha barabara hii.

SPIKA: Mheshimiwa Kajege, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba wakati anazungumza barabara ya ile ya kuunganisha Kisorya, amesahau kusema barabara ya kutoka Balili kwenda Mugeta nayo inapaswa kuunganisha.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Kajege, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, huyo ni Comrade, naipokea taarifa yake. Kuna changamoto ambazo bado Wizara inatakiwa kuzitatua ili kuweza kufanikisha malengo ya Serikali yetu. Kwa mfano, kuna Shirika la Air Tanzania Limited, shirika hili limekodisha ndege kutoka Shirika la TGFA, lakini nikiangalia kwa sababu nimepata bahati kwamba nipo katika Kamati ya PIC, na Viongozi Wakuu wa ATCL wamekuwa wanakuja katika Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika kuangalia tumekuta kwamba tatizo kubwa katika ATCL ni mkataba kati yake na TGFA, mkataba huu kwa kweli si rafiki. Ninaiomba sana Serikali iuangalie tena mkataba huu ili uweze kufanywa kuwa rafiki. Lakini tatizo lingine katika ATCL ni madeni iliyorithishwa, madeni hayo hayalipiki. Ningeomba Serikali iangalie namna nyingine ya kuweza kuchukua madeni haya. Vilevile kuna mwingiliano mkubwa wa Serikali kuipatia ATCL namna ya kufanya kazi, yaani waliache sasa Shirika la ATCL lifanye kazi kibiashara, lihudumie njia zenye faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano siku moja nilikuwa Mwanza, ndege ya ATCL ilikuwa inatoka Chato. Ndani ya ile ndege nilipoingia niliikuta ina abiria watatu lakini utakuta abiria wengi wapo hapa Dodoma wanasubiri ndege za ATCL kuweza kuwasafirisha. Ningeomba sana Serikali iliache Shirika hili liweze kufanya kazi yake ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni utitiri wa vituo bubu vya ukaguzi wa malori na mizigo katika barabara zetu. Ukitoka Dar es Salaam mpaka kufika Tunduma kuna vituo bubu zaidi ya 100. Haya malori yenye mizigo yakitoka Bandarini yanasimamishwa kila sehemu, yanakaguliwa kila sehemu na wakati mwingine yanchukua muda mrefu. Mfano mmoja siku moja nilikutana na dereva mmoja ambaye alikuwa anatoka Dar es Salaam kwenda Tunduma saa mbili nikamkuta akiwa amesimamishwa pale Kibaha lakini wakati narudi saa 12 jioni kutoka Morogoro nilimkuta bado amesimama pale. Wahusika walikuwa wanadai kwamba kuna cheti ambacho kilikuwa kimesainiwa lakini aliyekuwa amekisaini yuko kwenye mkutano. Kwa hiyo hakumruhusu huyo dereva aendelee na safari mpaka tena wapate aliyesaini kile cheti (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi vituo ni mojawapo ya vikwazo vikubwa sana vya biashara kati ya Tanzania na nchi zingine, lakini vile vile ni chanzo vile vile cha kuwafanya watumiaji wengine wa bandari zetu washindwe kutumia bandari yetu. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie sana hivi vituo bubu, ikiwezekana viondoke vyote vinafanya nini? Kama mizigo ikishakaguliwa bandarini kwa nini iendelee tu kukaguliwa tena njiani? Itakaguliwa kule mwishoni. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu kuna Kivuko cha Mugala - Musoma Vijijini ni kibovu, hiki kivuko kimekuwa ni kibovu kwa muda mrefu. Wananchi wanaotaka kusafiri kwenda Musoma Vijijini na wanaotoka Musoma Vijijini kuja Jimboni kwangu Mwibara wanapata tabu sana. Naomba sana Serikali sasa ikamilishe ukarabati wa hicho kivuko.

Mheshimiwa Spika, kingine ni tunahitaji kivuko kwenda katika Kisiwa cha Nafuba. Kisiwa hiki kina watu wengi sana na ni kikubwa sana, watu wengi mahitaji yao wanachukua katika nchi kavu huku. Kwa hiyo, ningeomba sana Serikali sasa iweze kutafuta kivuko kwa ajili ya kusafirisha wananchi kwenda Nafuba na kuja sehemu zingine za Jimbo la Mwibara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo jingine liliopo ni vibali vya kusafirisha mitambo ya ujenzi, kwa mfano inapotokea mkandarasi anataka kusafirisha mtambo mmoja kwenda katika mkoa mwingine kibali lazima akipate kutoka Dodoma. Hiyo inachukua muda mrefu sana kuweza kupata hivi vibali, inapoteza muda wa biashara na inakuwa kabisa ni usumbufu mkubwa, naomba kuwa na decentralization ya kutoa hivi vibali vya kusafirisha mitambo ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni malipo ya waliopisha Mradi wa Barabara ya Bulamba – Kibara – Kisorya. Barabara hii imeshakamilika muda mrefu lakini wahusika bado hawajalipwa. Jana wakati natoa taarifa kwa mzungumzaji mmoja niliomba Serikali iingilie kati kuweza kuwalipa wahusika fidia zao ili na wao waweze kuendesha maisha yao vizuri.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema haya machache naomba niunge mkono hoja hii na nawapongeza sana Wizara na Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri. Ahsante sana. (Makofi)