Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Samweli Xaday Hhayuma (48 total)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Naitwa Eng. Samweli Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la maji lililopo Butiama lipo pia kwenye Mji wa Katesh kwenye Jimbo langu; na kwa kuwa Serikali imeshawekeza shilingi bilioni 2.5 kuleta maji mjini na maji yale sasa yapo tayari kutumika. Je, Wizara iko tayari kuongeza fedha kidogo ili maji yaweze kusambazwa kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuongeza fedha katika miradi ambayo ipo katika hatua za utekelezaji ni jukumu la Wizara. Hivyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge fedha zitakuja kwa awamu kama ambavyo imekuwa kawaida yetu kuhakikisha mradi huu unafikia lengo la kupata maji bombani. Lengo la Wizara siyo tu kujenga hizo structures ambazo zipo tayari, tutaleta fedha kuhakikisha maji sasa yanafika bombani.
MHE. SAMWELI H. XADAY: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kwa kuwa kwa sasa Serikali haina utaratibu wa kufuata mipaka ya kiutawala katika kutoa huduma za umeme, kwa mfano, Kata ya Masakta iko kwenye Wilaya ya Hanang kiutawala lakini inahudumiwa na TANESCO Babati na hii imekuwa ikisababisha usumbufu kwa wananchi kufuatilia huduma. Je, Serikali ina mkakati gani kurekebisha tatizo hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali imefanya kazi kubwa kwenye mradi wa REA kupeleka umeme vijijini lakini kwenye vijiji husika maeneo yanayofikiwa au watu wanaopata umeme ni wachache. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba wananchi wengi zaidi wanapata umeme na kufika kwenye hatua ya vitongoji hasa kwenye Jimbo langu la Hanang? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya maeneo ambapo mikoa au wilaya za ki-TANESCO haziendani na mikoa au wilaya za kiserikali na nia kuu ya Shirika la TANESCO chini ya Serikali ilikuwa ni kuhakikisha kwamba huduma zinawafikia wananchi katika maeneo ambayo yanafikika kirahisi. Kwa kutoa mfano katika Mkoa wa Manyara, Wilaya ya Kiteto inahudumiwa na Mkoa wa Dodoma lakini tunayo wilaya ya ki-TANESCO inaitwa Simanjiro na wilaya nyingine inaitwa Mererani. Wilaya ya Simanjro ki- TANESCO inahudumiwa na Mkoa wa Kilimanjaro lakini wilaya ya ki-TANESCO ya Mererani inahudumiwa na Arusha.

Mheshimiwa Spika, kwa wanaofahamu ni rahisi sana kutoka Simanjiro kwenda Kilimanjaro, ni rahisi sana kutoka Mererani kwenda Arusha kuliko kurudi Makao Makuu ya Mkoa wa Manyara ambapo ni Babati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nia ya Serikali ilikuwa ni kuhakikisha kwamba huduma zinawafikia wananchi kirahisi wanapohitaji kwenda ofisini kupata huduma lakini pale ambapo TANESCO inatakiwa iende kuwafuata wananchi kuwahudumia au kwenda kufuata vifaa katika bohari.

Mheshimiwa Spika, Serikali imepiga hatua kubwa sana ya kuhakikisha miundombinu inafika karibia kila sehemu na hivyo ni rahisi sana kufikisha huduma kwa wananchi mbalimbali kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo, kila inapowezekana Serikali imeamua sasa ipeleke utawala wa ki-TANESCO sawasawa na utawala wa kiserikali ili kuhakikisha mtu anapata huduma kutoka kule ambako anategemea kuipata na maendeleo hayo ataendelea kuyaona kadri muda unavyozidi kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili ni kweli na kama tunavyofahamu maendeleo ni hatua. Kwa harakaharaka tu mwaka 2007 wakati REA inaanza ilipita vijiji 506 ndio vilikuwa na umeme lakini taarifa zinaonyesha kufikia 2015 tulikuwa tuna vijiji 2018 vyenye umeme na kufikia mwaka huu 2021 taarifa zetu zinaonyesha tuna vijiji 1950 kati ya 12,268 ambavyo viko Tanzania kwa ujumla wake. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba maendeleo ya kupeleka umeme ni endelevu na kadri Serikali inavyoendelea kupata pesa kwa kujibana na kwa kujihamasisha yenyewe inaendelea kuepeleka huduma hii na tutahakikisha inamfikia kila mwananchi anayehitaji kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali yenye kutia matumaini, nina maswali mawili madogo. Swali la kwanza; kwa kuwa barabara hii inategemewa na wananchi, upande wa Hanang’ tu zaidi ya 100,000 wa Kata za Gisambalang, Bilmaa, Simbai, Isilo, Wareta na Nangwa yenyewe na kulikuwa na Daraja la Mungurwi B. Daraja lile limechukuliwa na mafuriko ya mvua iliyonyesha 2019/2020. Ni kwa nini Serikali daraja lile lilivyochukuliwa halikuwekwa kwenye mpango wa dharura wa kulirudishia?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa daraja lile la Mto Bubu limekuwa likigharimu Maisha ya watu na kupoteza mali kwa kusombwa na maji. Je, Serikali ina mpango gani wa dharulra ili kuhakikisha wananchi wanaendelea na shughuli zao za kijamii pamoja na biashara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samwel Hhayuma, Mbunge wa Hanang’, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba daraja la Mungurwi B lilisombwa na maji na ni daraja ambalo liko sehemu ya bonde ambapo baada ya kusombwa lilitengeneza umbali wa mita zaidi ya 200 na hivyo ilikuwa ni ngumu sana kulijenga kama lilivyokuwa na badala yake, daraja hili linafanyiwa usanifu kutoka ilipokuwa kupanda eneo la juu ambalo tunaamini litakuwa ni eneo fupi, lakini pia hakutakuwa na changamoto ya mafuriko. Kwa hiyo linafanyiwa usanifu na baada ya kukamilika tutaanza kulijenga daraja hilo. Hiyo ndio sababu kubwa ambayo hatukuweka daraja la dharura.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la huo Mto Bubu nadhani nimelijibu pamoja na swali la kwanza kwamba baada ya fedha kupatikana na baada ya usanifu kukamilika, basi hilo daraja litakamilika ili kuunganisha wasafiri kutoka upande wa Kondoa kwenda upande wa Mkoa wa Manyara. Kwa sasa tunawashauri wananchi waendelee kupita kutoka Kondoa kupitia Babati kwenda Katesh na kutoka Sambalang kwenda Babati bila kupita kwenye huo mto. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Changamoto ya barabara iliyopo Mbinga ni sawa sawa na changamoto iliyopo kwenye Jimbo langu la Hanang hasa Mji wa Katesh. Ule ni Mji ambao una umri zaidi ya miaka 30 na kitu ukiwa ni Makao Makuu ya Wilaya lakini hakuna kilometa hata moja ya lami :-

Je, Wilaya ina mpango gani angalau kuweka kilometa 10 za lami ambayo pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge amejaribu kuainisha hapa barabara ambazo ni ahadi za viongozi na sasa hivi nikuhakikishie tu kwamba Serikali ipo katika Mpango wa Kukusanya ahadi zote na kuziweka pamoja, kuzifanyia tathmini pamoja na kuzitengea bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hicho ambacho amekieleza katika Mji wa Katesh ambapo mahitaji yao yapo, nimhakikishie kuwa ahadi zote za viongozi tutaziainisha, tutazitenga katika bajeti kwa ajili ya utekelezaji ikiwemo katika mji wake wa Katesh.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa, swali la msingi nami pia nina wakulima kwenye jimbo langu la Hanang wanasumbuliwa vivyo hivyo; na malalamiko makubwa ya wakulima hawa ni ubora wa matrekta ambayo wamepewa na pia kukosa usaidizi pale ambapo matrekta haya yanaharibika, kwa maana ya matengenezo na matengenezo kinga na vipuri:-

Je, sasa Serikali iko tayari kuwasimamia hawa NDC pamoja na URSUS, kampuni iliyouza matrekta kuhakikisha kwamba matrekta haya yanahudumiwa kadri ya mikataba ya wakulima?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto kidogo kwa baadhi ya wakopaji kwa wakulima ambao walikopa matrekta haya ya URSUS katika suala la ubora. Kweli suala la teknolojia ambayo ilikuja na matrekta haya kulikuwa kidogo kuna changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara kupitia NDC tulishaligundua hilo na hivyo tumeshaanza kulifanyia kazi kuona namna gani tunaweza kuwa na utaratibu mzuri wa kuwasaidia ili matrekta hayo yanayopata changamoto ya ubora kwa maana ya utekelezaji wa dhana nzima ya kuhakikisha trekta lile linafanya kazi, tumeshaanza kuainisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kwamba wenzetu wa NDC wameshaweka utaratibu mzuri wa kuwa na mafundi maalum ambao watapita kuwasaidia wakulima wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na vipuri, ni kweli matrekta haya kidogo yalikuwa na changamoto ya vipuri kwa sababu ni mapya na ile kampuni ya URSUS ilikuwa bado inaendelea kuleta baadhi ya spare. Kwa hiyo, hili nalo tunalifuatilia kuhakikisha kwamba matrekta haya yanaendelea kuwa na vipuri ili pale ambapo yanapata hitilafu au yanaharibika, basi angalau vipuri vya kurekebisha hitilafu hizo vinapatikana.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi naomba kufahamu Serikali lini itaanza ujenzi wa uwanja wa ndege wa Manyara ili kurahisisha usafiri na usafirishaji kwa wakulima wafugaji na wafanyabiashara wa Mkoa wa Manyara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge la nyongeza juu ya uwanja wa Manyara kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali nililoulizwa na Mheshimiwa Phillip Mwanyika kutoka Njombe Mjini, nimesema kwenye jibu la msingi kwamba viwanja 11 vimefanyiwa tathmini na upembuzi yakinifu, tunajua gharama zilizopo, uwanja wake Mheshimiwa Mbunge na Mkoa wa Manyara kwa ujumla upo kwenye mpango huu, tunatafuta fedha na zikipatikana wakati wowote uwanja wake wa Manyara, pamoja na viwanja vingine 11 ambavyo nimevitaja hapa vitajengwa ili ndege iweze kutoa huduma katika mikoa hiyo. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

La kwanza, kwa kuwa Serikali imesema upembuzi yakinifu wa barabara ya Katesh – Hydom unakamilika Juni, yaani mwezi huu; na kwasababu mfumo wa sasa ni wa kusanifu na kujenga. Je, baada ya mwezi wa sita ambapo upembuzi utakamilika Serikali iko tayari kuanza ujenzi mara moja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye barabara hiyo kuna maeneo mawili korofi moja ni daraja ambalo lipo Njia Panda ya Dawar kwenye hiyo barabara ya kwenda Hydom, lakini lingine ni ule Mlima Chavda ambao unakwaza usafiri na usafirishaji kwa kata za Bassodesh, Garawja, Hirbadaw, Getanuwas, Bassotu, Murbadau, Dawar yenyewe na Mogitu na mara nyingi wananchi wamekuwa wakipoteza maisha yao na kupoteza mali.

Je, Serikali itakuwa iko tayari sasa kuweka lami wakati tukitarajia ujenzi uanze kwenye eneo la Mlima Chavda na kujenga daraja imara pale kwenye ule mto uliopo kwenye njia panda ya Dawar?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Samwel Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna aina mbili, ya usanifu na kujenga ama kusanifu halafu baadaye kujenga. Kwa kuwa tayari tunafanya upembuzi yakinifu, itategemea na upatikanaji wa fedha kama utaruhusu tufanye utaratibu wa kusanifu na kujenga. Lakini kama fedha itakuwa haipo, kwa maana ya bajeti ya mwaka tunaoanza kutekeleza baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu tutafanya usanifu wa kina ili barabara hiyo sasa iwe tayari kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa kiwango cha lami kwa hela hiyo ya mfadhili kutoka benki ya Ujerumani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu daraja na maeneo korofi tayari tulishatoa taarifa kwa mameneja wote barabara zote ambazo zina maeneo korofi waweze kuyaainisha ili tuweze kuyafanyia mkakati wa kuyatengeneza si tu kwa barabara hii ya Hydom – Katesh bali ni pamoja na barabara zote ili tuweze kuyatengeneza, hata ikiwezekana kuweka lami nyepesi ili yaweze kupitika kwa kiwango chote. Kuhusu madaraja wataalamu wako barabarani wakiwa wanaangalia uharibifu wa madaraja hayo yote na kuweza kuyatengeneza ili baada ya kipindi hiki cha mvua kukatika basi barabara zote ziweze kupitika bila kuleta bugudha. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi.

Naomba kufahamu, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi wa maji wa Ziwa Basutwa ambao utasambaza maji kwa vijiji tisa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma Mbunge wa Hanan’g kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote ambayo inapatikana kupitia maziwa makuu, mito na vyanzo vikubwa vya maji vyote vimepewa kipaumbele na Wizara. Na kama tulivyowahi kumsikia hapa ndani Mheshimiwa Waziri yeye mwenyewe ameshaji-commite kwa Serikali, kwamba lazima tutajitahidi kutatafuta fedha ili tuweze kuona maziwa makuu na vyanzo vikubwa vya maji vyote tunakwenda kuvitumia kadri fedha tutakakuwa tunazipata.
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Changamoto ya maji inayoikumba Jimbo la Mwibara ni sawasawa na ambayo tunaipata kwenye Mkoa wetu wa Manyara na sehemu kubwa huwa tunapata changamoto kubwa hasa kwenye eneo la kuchelewa kwenye suala la manunuzi. Pale Mkoani hatuna Afisa Manunuzi.

Je, Wizara iko tayari kwa kushirikiana na Utumishi kupeleka Afisa Manunuzi pale Mkoani ili kuharakisha manunuzi? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Hanang kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake. Sisi kama Wizara ya Maji tutaendelea kumpa ushirikiano katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji katika Mkoa wa Manyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la Maafisa Manunuzi ni kweli tumeanzisha Taasisi yetu ya (RUWASA) Wakala wa
Maji Vijijini, hii ni mahususi kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji vijijini. Lakini tumekuwa na changamoto ya watumishi hususani katika eneo la manunuzi. Tumeshafanya mazungumzo na wenzetu wa Utumishi na hivi karibuni tutapata Maafisa hao katika kuhakikisha tunakwenda kutatua matatizo ya maji. Eneo ambalo tutalipa kipaumbele kabisa ni Mkoa wa Manyara katika kuhakikisha hii changamoto tunaifanikisha kwa haraka. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, la kwanza; baada ya ujenzi wa Kituo cha Afya Bassotu, Endasak na Gisambalay kukamilika bado tutakuwa na upungufu wa vituo vya afya 25 kwenye Wilaya ya Hanang’. Je, Serikali iko tayari kutufanyia upendeleo mahususi, ili tupate vituo vya afya viwili kwenye bajeti hii tunayoenda kuianza ya 2022/2023?

Mheshimiwa Spika, lakini la pili; Serikali imetupatia fedha milioni 300 kwa ajili ya kujenga jengo la magonjwa ya dharura kwenye hospitali ya wilaya, lakini wananchi pia, wamehamasishana tumechanga vifaa vinavyokaribia milioni 200. Je, bado tuna upungufu mkubwa wa majengo; Serikali iko tayari kutupatia fedha ili tujenge jengo la wodi kwa ajili ya wanaume? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Hanang’, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Hhayuma kwa kazi kubwa anayoifanya ya kufuatilia ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya kwa ajili ya Jimbo la Hanang’ na nimhakikishie kwamba, Serikali tutaendelea kushirikiana nae kuhakikisha wananchi wa Hanang’ wanapata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Spika, upungufu wa vituo vya afya hivi sasa tumeweka mkakati badala ya kujenga kituo cha afya kila kata, tuna kata zaidi ya 3,500 kwa hivyo, kwa sasa tunajenga vituo vya afya vya kimkakati kwenye tarafa, lakini pia kwenye kata zile ambazo zina uhitaji mkubwa kwa maana ya idadi kubwa ya wananchi, umbali mrefu zaidi kutoka kwenye kituo cha karibu, lakini na idadi ya magonjwa.

Mheshimiwa Spiika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutafanya tathmini ya mazingira yale ambayo kimsingi pale Hanang’ tunaweza kujenga vituo vya afya ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, pili; ni kweli Serikali yetu imefanya kazi kubwa ya kupeleka fedha ya ujenzi wa miundombinu ya majengo ya dharura, ikiwepo Hanang’ wamepata milioni 300 na kazi ya ujenzi wa wodi na miundombinu mingine tutaendelea kuitekeleza kwa awamu, ili hospitali ile ya Hanang’ iwe na miundombinu yote inayofanana na hospitali ya wilaya. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka 2021 alifika kwenye Barabara ya Haydom - Katesh na amejionea hali ya ile barabara ambayo inategemewa na wananchi kwa shughuli za kilimo pamoja na huduma mbalimbali: -

Je, ni lini wananchi wa Jimbo la Hanang na Mbulu watawaona wakandarasi wakiwa kwenye kazi kutengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samweli Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tutafuatilia na kuona kwamba wakandarasi hawa wanakuwepo site haraka inavyowezekana. Ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Wilaya ya Hanang, Kata ya Basutu, tuna mgodi wa dhahabu, lakini uzalishaji wake uko chini sana. Je, Serikali iko tayari kushirikiana na mwekezaji ili kuongeza uzalishaji wa dhahabu kwenye eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara, tunashirikiana na wawekezaji na wachimbaji wadogo. Vilevile sisi kama Wizara lengo letu kubwa ni kusimamia upande wa sera, kanuni na sheria, lakini pia kutoa elimu na kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata fursa za kufikia taasisi za kifedha ili waweze kukopeshwa vifaa ama fedha baada ya kukidhi vigezo ili uzalishaji uweze kuendelea na waweze kupata tija kwa juhudi ya uchimbaji wa madini.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Wilaya ya Hanang tunachangamoto kubwa sana ya umeme kukatika mara kwa mara, na suluhu ya tatizo hili ni kujengwa kwa kituo cha kupooza umeme pale Mogitu. Serikali iliahidi kutoa zaidi ya shilingi bilioni mbili ili ujenzi huo ufanyike.

Je ujenzi huo utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye maswali mengine, Serikali imefanya utafiti na kubaini maeneo yanayohitaji kujengwa vituo vya kupooza umeme kwa ajili ya kuhakikisha huduma inawafikia wananchi, na eneo hilo ni mojawapo kati ya maeneo ambayo yametengewa na muda utakapofika huduma hiyo itatekelezwa kwenye jimbo lake.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa
Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi barabara ya kutoka Bashineti – Lukumanda – Seche – Basodeshi – Ibadalu – Zinga, kutoka TARURA Kwenda TANROADS? Kwa sababu barabara hii upande wa Singida iko TANROADS na upande wa kutoka Babati kwenda Mbulu iko upande wa TANROADS.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo yetu katika halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Hanang na mikoa yote, ni kuhakikisha zile barabara ambazo zinaunganisha kati ya halmashauri moja na nyingine, mkoa mmoja na mwingine ambazo zinaangukia katika upande wa TARURA ili ziunganishe mkoa, ni kuanza mchakato wa kuhakikisha sasa zinakuwa na vigezo vya kupandishwa hiyo hadhi.

Mheshimiwa Spika, maelekezo yangu kama katika swali la msingi na kwa Waheshimiwa Wabunge ni hayo na tutafuatilia maelekezo hayo kwa nia moja tu ya kutaka kuwasaidia wananchi katika maeneo yenu.
MHE. ENG. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Haidong - katesh imeshatengewa milkioni 300 kwa ajili ya ujenzi na milioni 280 kwa ajili ya usanifu wa kina. Je, Serikali ina mpango gani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pilli, Barabara ya Nangwa – Kondoa ina daraja ambalo limekuwa likikwamisha wananchi, daraja la Munguli, ilitengewa milioni 600. Je, ujenzi wake utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Xaday, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Hydom – Katesh ipo kwenye mpango na imepangiwa fedha. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa utekelezaji ni mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, Daraja la Munguli linalounganisha Kondoa na Hanang pia limetengewa fedha kwa ajili ya kulijenga Mwaka huu wa fedha. Ahsante.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu kwa kuwa mashamba ya Murujanda, Sechet ambayo yako chini ya Mwekezaji kwa sasa uzalishaji uko chini ya kiwango na aliahidi kwamba ndani ya mwaka mmoja ataboresha.

Wizara ina kauli gani katika kuhakikisha kwamba tunapata Wawekezaji ambao wako makini au kuwapatia wana Hanang’ maeneo hayo?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Hanang’ kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna mashamba yalichukuliwa na Wawekezaji mojawapo ni Ngano Limited katika Mkoa wa Manyara Wilaya ya Hanang’ na uwezo wake wa kuyatumia hauzidi asilimia 30. Aliingia makubaliano nasi kama Wizara ya Kilimo na kutuambia kwamba tumpe span ya mwaka mmoja, ataweza kufanya matumizi kwa kiwango cha asilimia 100 mpaka sasa amefeli.

Mheshimiwa Spika, hivyo, Wizara sasa hivi tunawasiliana na wenzetu wa TIC na kuwasiliana na wenzetu wa Hazina ili tumuite Mwekezaji huyu, tukae naye aweze ku- offload hekari zaidi ya 30,000 ambazo ameshindwa kuzitumia mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninatumia Bunge lako Tukufu kuwaambia Halmashauri ya Hanang’ kwamba eneo la Basutu lisibadilishwe matumizi litabaki kuwa eneo la uzalishaji wa ngano. Hili ni jambo muhimu sana na Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani, wahakikishe hawabadilishi eneo la Basutu kulipelekea matumizi mengine isipokuwa kwa ajili ya matumizi ya ngano. (Makofi)
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Barabara ya Nangwa- Gisambalang-Kondoa inayotegemewa na Kata ya Gisambalang, Dirma, Simbai, Sirop na Wareta ina daraja ambalo limekatika toka mwaka 2019.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga hilo Daraja la Muguri B?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja alilolitaja ambalo liko sasa hivi kwenye usanifu na tunategemea kwenye mwaka wa fedha ujao daraja hilo lianze kujengwa. Ahsante.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Ni lini Serikali itahamisha barabara ya Bashnet – Bassodesh – Hirbadaw - Singida kutoka TARURA kwenda TANROADS kwa kuwa upande wa kutoka Bassodesh - Hirbadaw ipo TANROADS na Singida ipo TANROADS matengenezo yake huwa yako tofauti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Xaday Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nizielekeze tu halmashauri zenye mahitaji hayo zifuate taratibu na utaratibu unaeleweka unaanzia ngazi za halmashauri baadaye zinaenda katika Bodi ya Barabara Mkoa halafu zinapelekwa Wizara ya Ujenzi kwa ajili ya uthibitisho. Kwa hiyo sisi tunapokea tu kama ombi ili hizo taratibu ziweze kufuatwa, ahsante sana.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, changamoto ya ufinyu wa maeneo ya kutolea huduma ya afya ya mama na mtoto hasa eneo la kujifungulia ipo maeneo mengi ndani ya Wilaya yangu ya Hanang.

Je, sasa Serikali haioni ni wakati muafaka kufanya tathmini ya jumla wakati tukiendelea kupanga mpango wa kujenga kituo cha afya kila Kata ili kufanya maboresho katika maeneo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili fedha zilizotengwa kwa zahanati ya Laghanga, milioni 10. Je, Serikali haioni kwamba hizo fedha ni kidogo haiwezi kutosheleza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba zahanati zile ambazo zilijengwa miaka ya nyuma zilikuwa ndogo na vile vyumba vya kujifungulia vilikuwa finyu lakini kwa sasa Serikali imeboresha sana ramani zetu, ramani zetu ni kubwa zina vyumba vya kutosha vya kujifungua, lakini pia vya kupumzika wakina mama baada ya kujifungua. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba kwa ramani za sasa tutajenga zahanati zenye nafasi za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kujenga vituo vya afya kila Kata utaratibu wa Serikali tutajenga vituo vya afya vya kimkakati katika maeneo ya kimkakati ambayo yana idadi kubwa ya watu lakini umbali mkubwa kutoka kituo cha huduma cha Jirani zaidi. Lakini hii shilingi milioni 10 imetengwa kutoka mapato ya ndani na chumba kinakwenda kuongezwa katika jengo lile ambalo linatumika kwa sasa, kwa hiyo tunaamini itatosha na kama haitatosha basi Serikali itaongezea kuhakikisha kwamba chumba hicho kinakamilika. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itajenga Barabara ya Mogitu - Hydom kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, barabara aliyotaja Mheshimiwa Hhayuma, ni link kati ya Barabara ya Babati - Hydom kwenda Sibiti. Kwa hiyo itakavyoanza kujengwa, hicho kipande kitakuwa ni sehemu ya hiyo barabara.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba nifahamu ni lini Serikali itakamilisha usambazi wa maji Ziwa Basutu ambako imefikia tu eneo moja kwa sasa na maeneo yaliyotarajiwa ni 12?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, kwanza anafanya kazi kubwa nzuri na nimekwishafika katika Jimbo lake. Kikubwa ahadi ni deni, Serikali na dhamira ya Rais wetu tutahakikisha kwamba tunakwenda kuyatumia maji yale ya Ziwa Basutu na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi maneno ya usanifu wa kina au upembuzi yakinifu hawayaelewi vizuri;

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Mogitu – Hydom kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, swali lililoulizwa na Mheshimiwa Hhayuma lilikuwa ndilo swali la msingi lililohusu Mogitu – Haydom na nimeshalijibu kwamba tayari mkandarasi yupo anafanya usanifu wa hiyo barabara tujue gharama halafu fedha itafutwe kwa ajili ya kuijenga, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza: -

Je, Serikali iko tayari kutenga fedha kwa ajili ya kutengeneza Daraja la Sanjawe, Mara na Daraja linalounganisha Basodeshi na Gietamo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika,
naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samweli, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kutenga fedha ya barabara hii ya Sandawe. Na ninaamini katika mwaka huu wa fedha tayari TARURA, kupitia Meneja wa Mkoa na Meneja wa Wilaya, watakuwa wameiwekea fedha barabara hii na tutampatia Mheshimiwa Mbunge Taarifa hiyo.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Nangwa – Gisambala – Kondoa ikiwepo Daraja la Munguri kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja tuna mpango nayo kwa ajili ya kukamilisha na ku-review usanifu na baada ya hapo gharama zitajulikana ili tuweze kuipanga sasa kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, hii barabara ili ilete tija inayokusudiwa, ni muhimu kufungua barabara ya Mashaw - Waranga, barabara ya Masusu – Gisambalang – Mhanda; je, Serikali iko tayari kutenga fedha haraka ili barabara ziweze kufunguliwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wilaya ya Hanang’ ina maeneo mengi ambapo mvua ikinyesha yanakuwa kama kisiwa. Mfano Mara, Uteshi, Merekwa, Gaulol, Ghetaghul na Gijetamogh; je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kuingozea TARURA Wilaya ya Hanang’ bajeti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza; la kwanza, hii barabara ambayo ameitaja ya Marang, Masusu, Gisambalang na maeneo ya kule Hanang’ Serikali itaendelea kutenga fedha kadiri ya upatikanaji wa fedha hizi. Vile vile kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, barabara hii ilikuwa ni ya kupita mifugo (Pario). Kwa jitihada kubwa za Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na TARURA kuongezewa fedha, imeanza kufunguliwa na sasa zaidi ya kilometa 30 tayari zimetengenezwa na kadiri miaka inavyokwenda tutazidi kuhakikisha barabara hii inafunguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii za Katesh, Berekwa na maeneo yale ya kule Hanang ambayo ameyataja Mheshimiwa Hhayuma, TARURA kwa mwaka wa fedha huu unaomalizika ilitengewa shilingi bilioni 2.33 kwa Wilaya ya Hanang peke yake. Hii ni zaidi ya mara tatu ya bajeti ambayo ilikuwa 2020/2021 ya barabara katika Wilaya ya Hanang’. Hivyo Mheshimiwa Mbunge awe tu imani kwamba katika bajeti inayofuata hii, vilevile TARURA wametengewa bajeti hiyo hiyo ya shilingi bilioni 2.33 kule Wilaya ya Hanang na barabara nyingi zitafunguliwa kuhakikisha kwamba wananchi wake kule wanapita bila matatizo yoyote.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kituo cha Afya cha Endasaki miundombinu yake ni chakavu sana; je, ni lini Serikali itatoa fedha zote zinazohitajika ili kukarabati miundombinu ya kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Endasaki pale ambapo upatikanaji wa fedha hizo utakuwepo. Tutaangalia katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 kama kituo hiki kimetengewa, ili fedha hizo ziweze kwenda mara moja. Kama hakijatengwa katika mwaka huu wa 2023/2024, tutahakikisha mwaka 2024/2025 kituo hichi kinatengewa fedha.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuambatana na Mheshimiwa Ally Kassinge kutembelea eneo la Kilwa Kivinje ili kujiridhisha na mahitaji ya soko hilo na kuharakisha ujenzi wake?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Ziwa Bassotu ukanda upande wa Kata ya Mulbadaw miundombinu ya msingi imeishajengwa ya mwalo. Je, yupo tayari kutoa tamko ili watendaji wake ndani ya Wilaya Hanang’ wafungue Mwalo huo mara moja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge mara baada ya Bunge hili kuhairishwa na ratiba yetu tutapanga kuanzia mwezi ya saba kwa hiyo hilo limekubalika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tamko la ziwa niseme tu kwamba, nimelipokea jambo hilo na ninakwenda kulifanyia kazi na baada ya hapo tutatoa tamko rasmi, ahsante.
MHE ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, mbegu za kisasa tunazozitumia unaweza kuzitumia mara moja tu na ni bei ghali. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuendeleza mbegu zetu za asili ambazo unaweza kuzitumia zaidi ya mara moja ili kupunguza gharama kwa wakulima?

Swali la pili, mwaka 2020 Wizara ya Kilimo ilikuja Jimboni Hanang’ na baadaye wakanunua ngano, tukielezwa kwamba zile ngano zilizoko Hanang’ ni bora na zinafaa kuwa mbegu. Je, Serikali ina kauli gani juu ya upatikanaji wa mbegu bora za ngano Nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la kwanza mbegu za asili, mbegu hizi zimeendelea kutambuliwa na Taasisi ya Utafiti ya Kilimo Tanzania (TARI) inaendelea kuzifanyia utafiti, vilevile Mamlaka ya Afya, Mimea na Viuatilifu Nchini (TPHPA) na yenyewe sasa iko mbioni kwa ajili ya kutunga Sheria ya Nasaba za Mimea ili kuzitambua, kuzitunza na kuzitumia kwenye utafiti. Kwa hiyo, Serikali inaipa umuhimu suala hili la mbegu za asili.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli mwaka 2020 tulifanya utafiti huo na tulichukua sampuli ya mbegu 22, tano zikiwa kutoka nje ya nchi na 17 za ndani ya nchi, kwa ajili ya kwenda kuangalia ubora wake. Katika tafiti hii zaidi ya mbegu 10 zimeonekana zinafanya vizuri na zina kiwango kikubwa cha gluten kwa maana ya protein ambayo inazidi asilimia 10, hivi sasa zimeanza kusambazwa katika baadhi ya maeneo kuweza kutumika ili kusaidia upatikanaji wa mbegu bora za ngano.

Mheshimiwa Spika, katika mbegu hizi ziko mbegu za Kariege, Sasambua, Sifa, Chiriku pamoja na mbegu nyingine ya Mbayuwayu ambayo imeonekana kuwa na soko kubwa sana.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika; je, Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga Barabara ya Hydom – Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hiyo ilishafanyiwa usanifu na Serikali inatafuta fedha kuijenga hiyo Barabara ya Hydom Mogitu kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi; ujenzi wa stendi Mji Mdogo wa Katesh unasuasua; je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kuwa stendi hiyo inakamilika haraka ili ianze kutumika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natoa maelekezo na nasisitiza kwa Mkurugenzi wa Halmashauri hii ya Hanang. Tulishafanya ziara pale, mimi na Mheshimiwa Mbunge lakini pia tuliona kweli stendi ile inasuasua. Tulitoa maelekezo na Halmashauri ilitoa commitment ya kuongeza fedha kwa ajili ya kukamilisha. Kwa hiyo, tunatoa maelekezo kwamba wahakikishe wanakamilisha stendi ile haraka iwezekanavyo na sisi Ofisi ya Rais-TAMISEMI tutafika kukagua na kuona kazi imetekelezwa kwa wakati, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara hii ambayo inapita Lukhumeda – Setet kwa upande wa Babati, ambayo kwa Hanang inapita Bassodesh – Dang’aida – Hilbadaw, lakini ukienda upande wa Singida inaenda Singa – Ilongero – Singida, imejadiliwa kwenye kikao cha Bodi ya Barabara mwaka 2021. Hapa Bungeni nimeshaisema hii barabara zaidi ya mara tano; je, Serikali ina kauli gani juu ya nini kifanyike ili barabara hii iweze kufanyiwa kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022, tuliongeza bajeti ya TARURA kwa uwiano kwa majimbo yote, lakini kwa majimbo yale makubwa ambayo mtandao wa barabara ni mkubwa, fedha hizi ni kidogo; kwa mfano kwa Hanang tuna kata 33 na vitongoji 414; je, Serikali ina kauli gani kuziongezea bajeti zile Halmashauri kubwa au majimbo makubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Hhayuma, hili la kwanza la kauli ya Serikali juu ya barabara hii ya Hilbadaw – Bashnet iliyopo kule Hanang kupandishwa hadhi; kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi, hili ni takwa la kisheria la kupitisha barabara hii kwenye vikao hivi. Mheshimiwa Mbunge ameshasema barabara hii ilipitishwa mwaka 2021, hivyo basi, kwa sasa litakuwa chini ya Waziri mwenye dhamana na barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilitakiwa timu ije kufanya tathmini ya barabara hiyo kabla ya kuipandisha hadhi na kumshauri Waziri wa Ujenzi. Kwa hiyo, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na kuona hili limekwamia wapi? Pale lilipokwamia basi hatua ziweze kuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu uwiano wa bajeti ya barabara za TARURA katika majimbo mbalimbali hapa nchini, ikiwemo na Jimboni kwake Hanang; hapa wakati najibu swali mojawapo la nyongeza, nilisema tayari kuna timu ambayo inafanya tathmini ya maeneo yetu hapa nchini juu ya bajeti ya barabara ambayo inatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa TARURA ilirithi mfumo ule ule uliotoka kwenye Bodi ya Barabara wakati taasisi hii inaanzishwa. Tathmini ile itakapokamilika kuangalia maeneo ya kijiografia, kiuchumi na masuala ya kilimo yanayotokana na maeneo mbalimbali hapa nchini, basi formula mpya itatolewa. Kama nilivyosema, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, analifanyia kazi na timu yake muda siyo mrefu itamshauri.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga barabara ya Haydom -Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara ya Mogitu - Haydom ni barabara ambayo ni link kwenye ile barabara ya Karatu - Mbulu – Haydom kwenda Lalago. Kwa hiyo, ni link ya hiyo barabara. Kwa hiyo, ni sehemu ya hiyo barabara, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kufahamu Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga barabara ya Kondoa – Gisambalang – Nangwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ambayo ameitaja kwa kweli mpango mkubwa hasa ni kuhakikisha kwamba kuna daraja kubwa ambalo linaleta changamoto kati ya Kondoa na Hanang. Tunachofanya sasa hivi, kwanza ni kufanya usanifu wa lile daraja, tulijenge, halafu tuimarishe hiyo barabara ili iweze kupitika kipindi chote cha mwaka. Sasa hivi kwa kweli inapotokea masika hiyo barabara haipitiki, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza naishukuru sana Serikali kwa fedha ambazo zimewekwa kwa ajili ya barabara ya Mogitu – Dawar – Ziwa Chumvi, lakini pia kwa shilingi milioni 53 ambayo imetengwa kwa ajili ya Dawar – Endasak. Pamoja na pongezi hizo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza maeneo ya Mara – Getaqul ambayo iko Kata ya Measkron, na Merekwa – Gauror ambayo iko Kata ya Dirima na Sosomega ambayo iko Kata ya Hirbadaw kipindi cha mvua huwa yanakuwa kama yako kisiwani.

Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka kufikisha mkono wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan maeneo hayo ili nao waweze kufurahia maisha kwenye eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tuna changamoto kubwa ya daraja kule Sirop. Serikali imeshatenga fedha shilingi milioni 568; je, ni lini ujenzi wa daraja hilo utaanza ili wananchi waachane na adha ya daraja hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hhayuma. Swali lake la kwanza hili la Kata ya Dirima aliyotaja na vijiji ambapo barabara hizi zipo katika kata ambayo mvua ikinyesha wanakuwa wako kisiwani, naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Hanang’ kwenda kufanya tathmini ya barabara hii na kisha kuiwasilisha Makao Makuu ya TARURA ili kuona ni namna gani tunaweza tukai-accommodate katika bajeti zifuatazo kuitengeneza barabara hii ili wananchi hawa wasiwe kisiwani kipindi cha mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Hhayuma kwa sababu amekuwa akifuatilia sana upatikanaji wa fedha wa daraja hili ambalo linaenda kujengwa kwa Shilingi milioni 568 ambalo amelitaja yeye mwenyewe, nimhakikishie kwamba mara tu tutapoanza mwaka wa fedha wa 2023/2024 ujenzi huu utaanza kwa kutangaza kazi hii ili apatikane kandarasi kwa ajili ya kujenga daraja hili.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka vifaa tiba vya kisasa katika Hospitali ya Wilaya ya Hanang kama ventilator, anesthesia machine na diathermy ili koboresha huduma za afya ya mama na mtoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za Wilaya zinakuwa zina vifaa tiba vya kisasa na tayari tumeshapeleka fedha kwa wenzetu wa MSD kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. MSD imeanza kupeleka vifaa hivi katika Hospitali za Wilaya mbalimbali hapa nchini. Nitakaa na Mheshimiwa Hhayuma kuweza kuona Hospitali ya Wilaya ya Hanang ipo katika awamu ipi ya kupokea vifaa tiba hivi vya kisasa katika Hospitali ya Wilaya ya Hanang.

MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Tarafa ya Balangaralu Makao Makuu yake yako Kata ya Balanga na pale hakuna Kituo cha Afya.

Je, Serikali ni lini itapeleka fedha ili kituo cha afya kijingwe pale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha katika Tarafa aliyoitaja Mheshimiwa Hhayuma kule Hanang kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mipango iliyopo katika mwaka wa fedha unaofata 2023/2024 kuona kama fedha yoyote imetengwa kwa ajili ya kwenda Halmashauri ya Wilaya ya Hanang ili tuweze kuhakikisha inaenda haraka kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kufahamu kwenye mikataba iliyosainiwa, barabara ya Hydom – Mogitu yenye urefu wa kilometa 68, ipo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Haydom – Mogitu ilikuwa ni sehemu ya barabara ya Serengeti Southern Road wakati wa design ya awali, lakini katika mpango huu wa EPC + F barabara hii kwa sasa tunaifanyia usanifu, maana ilikuwa imefanyiwa usanifu wa awali, sasa tumeiingiza tuifanyie usanifu ili tutakapokamilisha hiyo barabara ambayo ni ya EPC + F tuweze kuijenga hiyo pia kwa sababu ndiyo inayounganisha barabara ya Hydom kwenda Sibiti na barabara ya Singida kwenda Babati, ahsante.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mamlaka ya Mji mdogo wa Katesh ni ya muda mrefu na Mji wa Katesh umepanuka sana. Je, Serikali lini itachukua hatua ya kuanzisha Mamlaka kamili ya Mji wa Katesh?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, Serikali kwa sasa bado inaweka kipaumbele katika kumalizia ujenzi wa miundombinu kwenye maeneo ambayo ni mapya na maeneo yale ambapo Halmashauri zilihamia kwenye maeneo yale ya kiutawala na pale Serikali itakapomaliza ujenzi wa miundombinu hii muhimu, tutaanza kuangalia tena namna ya kuweza kuanza kupandisha hadhi maeneo mengine ya Mamlaka za Miji.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza maji ya Ziwa Bassotu kwa siku za karibuni yamekuwa yakisambaa na kuingia kwenye mashamba ya watu na nyumba:-

Je, Wizara ya Maji iko tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, (Mazingira) kuangalia na kufanya tathmini ya tatizo linalofanya hayo maji yasambae na hatimaye kulitatua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mradi huu karibu miaka mitatu ya fedha imekuwa ikitengewa chini ya Shilingi bilioni moja na tathmini ya awali ni Shilingi bilioni 12:-

Je, Wizara sasa iko tayari kutenga fedha zaidi ili mradi huu ukamilike kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Hhayuma, Mbunge wa Hanang’ kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara tunafanya kazi kwa ushirikiano na Wizara ambazo tunakuwa tunaingiliana kikazo. Hivyo tupo tayari kushirikiana ili kuondoa hiyo adha kwa wananchi na vilevile kutenga fedha zaidi. Tutaendelea kufanya hivyo na pale tunapoendelea kupata fedha tutaongeza bajeti kwenye eneo hilo ili miradi hii ikamilike.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itapandisha Mamlaka ya Mji Mdogo wa Kateshi, kuwa Mamlaka kamili ya Mji wa Kateshi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eng. Samweli Mbunge kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachohitaji katika Halmashauri yake ya Hanang’ ni kufuata tu vile vigezo halafu baada ya kumaliza hivyo vigezo watuletee nasi tutakuja kufanya tathmini tuone kama inakidhi ili tuweze kupandisha hadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi pamoja na mpango mzuri wa Serikali kupeleka magari ya wagonjwa kila halmashauri.

SPIKA: Taja kituo cha afya ama hospitali na uliza swali lako.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, na kwa kuwa Wilaya ya Hanang kuna upande wa juu ambapo kuna kata nane na tumejenga vituo viwili vya afya vya Basutu na Hirbadaw, je, Serikali ipo tayari kutuletea gari la pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Hhyuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang kama ifuatavyo; nimhakikishie kwamba tufanya tathimini na kuona uhitaji wa magari katika vituo hivyo na tutapeleka kadri ya upatikanaji wa magari hayo. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga barabara ya Nangwa - Kisambara - Mkondoa ambayo vinaunganisha Mkoa wa Manyara na Kondoa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Samweli Hhyuma, Mbunge wa Hanang kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kati ya barabara ambazo zipo kwenye mpango wa kuzijenga kwa kiwango cha lami, lakini ujenzi huo utategemea na upatikanaji wa fedha. Ahsante.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali kwanza, tarehe 29 Septemba, 2022, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alitutembelea na kati ya miradi aliyokagua, alikagua ujenzi wa barabara za lami Mji wa Katesh aliahidi kwa mwaka ule wa fedha 2022/2023 ameshaongea na Mheshimiwa Rais angeongeza fedha kwa ajili ya kilometa moja na hizo fedha hazikuja kwa mwaka huo wa fedha.

Je, Serikali sasa iko tayari kwa mwaka huu wa fedha 2023/2024 kutupa fedha za kilometa moja?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; mradi huu kidogo hauendi kwa kasi ili kufikia kilometa 10; je, Serikali ina mkakati gani mahususi ili kujenga barabara za lami katika Mji wa Katesh? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samwel Hhayuma. Swali la kwanza na la pili yote nitayajibu kwa pamoja. Ahadi hizi za viongozi ni lengo la Serikali kuzikamilisha zote kwa wakati na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anafahamu tayari asilimia 30 ya ahadi hii ya barabara ya kilometa 10 imeshafikiwa mpaka hivi tunavyozungumza.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha ahadi hiyo ya kilometa 10 iliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ahadi pia iliyotolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutahakikisha fedha inapopatikana ahadi hizi zinaenda kutekelezwa kwa ujenzi wa barabara hizi za lami.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Baadhi ya zahanati ambazo zimejengwa Makao Makuu ya Kata hasa Sirop, Dirma, Laghanga, Getanuwas na Ishponga hazina jengo la mama na mtoto; je, Serikali ina kauli gani ili kuboresha afya ya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Samweli Hhayuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati zote ambazo zimejengwa na zina upungufu wa majengo ya Huduma za Afya ya Mama, Baba na Mtoto, tumeshatoa ramani nyingine kwa ajili ya kuongeza majengo hayo kwenye zahanati hizo ili huduma hizi ziweke kupatikana. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zahanati ambazo amezitaja hapa tutazipa kipaumbele pia kuhakikisha kwamba zinajenga majengo hayo, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Baadhi ya zahanati ambazo zimejengwa Makao Makuu ya Kata hasa Sirop, Dirma, Laghanga, Getanuwas na Ishponga hazina jengo la mama na mtoto; je, Serikali ina kauli gani ili kuboresha afya ya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Samweli Hhayuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati zote ambazo zimejengwa na zina upungufu wa majengo ya Huduma za Afya ya Mama, Baba na Mtoto, tumeshatoa ramani nyingine kwa ajili ya kuongeza majengo hayo kwenye zahanati hizo ili huduma hizi ziweke kupatikana. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zahanati ambazo amezitaja hapa tutazipa kipaumbele pia kuhakikisha kwamba zinajenga majengo hayo, ahsante.
MHE. SAMWELI X HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; kwa kuwa, ahadi hii ni ya muda mrefu toka 2005 na utekelezaji wake tukienda hivi utachelewa sana na tumeleta maombi maalum Wizarani.

Je, Serikali ina kauli gani juu ya maombi maalum tuliyoleta?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Mji wa Basutu ni Makao Makuu ya Tarafa ya Basutu n ani mji ambao una wananchi wengi sana.

Je, Serikali itakuwa tayari kutenga fedha ili kujenga barabara chache za lami ndani ya mji huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maombi maalum ambayo tayari yamefika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tupo kuyafanyia kazi. Kwa sababu unapoleta maombi na sisi tunatafuta fedha na tutakavyopata maana yake tutatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa swali la pili, kuhusu Mji wa Basutu, na lenyewe tumelipokea na tutaliweka katika mipango yetu. Ahsante sana.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kijiji cha Mrelu ni eneo kame sana na kimeshachimbwa kisima. Je, ni lini Wizara italeta fedha ili maji yale yaweze kusambazwa?

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba arudie swali.

SPIKA: Mheshimiwa Hhayuma hujasikika vizuri.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kijiji cha Mrelu ni eneo kame sana na sasa hivi kisima kimeshachimbwa na wananchi wanaishukuru sana Serikali. Je, ni lini fedha zitapelekwa ili maji yale yaweze kusambazwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mara tunapopata chanzo cha uhakika, kusambaza ni moja ya wajibu wetu mkubwa na hiyo ndio tija ya dhima ya Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Mbunge mwaka ujao wa fedha mapema kabisa miezi ya mwanzoni tunaenda kusambaza maji katika eneo hili ambalo tumechimba kisima.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, naomba kufahamu, je, Serikali imefikia hatua gani kwenye maandalizi ya kujenga barabara ya Hydom – Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ilishafanyiwa usanifu na tayari Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.