Contributions by Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka (4 total)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi ya kwanza kukushukuru wewe mwenyewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia Maazimio yote mawili yaliyopo mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu Afrika na dunia nzima imeshuhudia upendo usio na mfano ulioonyeshwa na Watanzania walipojitokeza kumsindikiza, kumuenzi na kumuombea Hayati mpendwa wetu Dkt. John Pombe Joseph magufuli. Upendo waliouonesha Watanzania katika maeneo ulikopitishwa mwili wa Mheshimiwa Dkt. John Pomba Joseph Magufuli na maombi na dua yaliyofanyika nchi nzima katika maeneo ambapo mwili wa mpendwa wetu haukuweza kufika ni ushahidi tosha kwamba Watanzania walikuwa na imani kubwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyekuwa Rais wetu wa Awamu ya Tano alifanikiwa kujijengea uhalali wake mara alipochaguliwa na Watanzania kuwa Rais wa nchi yetu. Rais hayati Mzee Benjamin William Mkapa aliwahi kusema: “Kazi ya uongozi ni kuonyesha njia na watu wanakufuata si kwa sababu wanakuogopa ila kwa sababu wanakuamini na imani ya kweli haitokani na maneno bali matendo”. Mwisho wa kunukuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, matendo ya hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli yalimjengea heshima, imani ya Watanzania kumfuata. Kazi aliyoifanya kwa miaka mitano akisaidiana na Mheshimiwa Samia Suhulu Hassan amekijengea chama chetu na Taifa letu uhalali wa kuendelea kuheshimika Barani Afrika na duniani kote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninyi nyote ni mashahidi na Watanzania ni mashahidi kwamba ukiacha kufanya maombolezo tuliyofanya kwa kujitokeza kila mmoja wetu lakini siku ya kumuaga Afrika ilileta Rais wapatao 16 na Mabalozi wasiopungua 51 waliotoka kote duniani. Pia nchi zote dunia ambazo hazikuweza kuleta Mabalozi na Rais walituma salamu kwa Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kufuatia kuondoka kwa shujaa wa Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inaonesha kwamba maisha ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli siyo tu yaliwagusa Watanzania yaligusa Afrika na dunia yote. Kinachosikitisha ni kwamba wakati mataifa haya yakitupa pole na kuomboleza pamoja nasi bado kuna Watanzania wenye passport za Tanzania wanaobeza kazi iliyofanywa na hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Kazi yetu ni kuendelea kuwaombea msamaha kwa Mungu awafunulie ili siku moja waweze kuijua kweli na warudi kuungana nasi katika kuweka Utanzania mbele hata kama kwa sasa wanalishwa na hao wenye nia ovu na Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii tena kueleza bayana kwamba tunamuenzi Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri aliyofanya na tunampongeza mama Samia Suluhu Hassan kwa kupokea kijiti cha kuendelea kuongoza Taifa letu. Wote wawili hawa wamepata uongozi bila ya kuwa na makundi, bila kutoa hata shilingi. Dkt. John Pomba Joseph Magufuli alichaguliwa na Mkutano Mkuu wa Taifa bila kuhonga hata shilingi moja naye alimteua mama Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea mwenza na hatimaye wakaongoza jahazi la nchi yetu kwa muda wa miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya miaka hiyo mitano mmeshuhudia kiwango cha kura ambacho CCM imeweza kupata katika uchaguzi wa mwaka 2020. Huu ni ushahidi tosha kwamba tulitekeleza Ilani ya Uchaguzi chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe Joseph Mgufuli na mama Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme tu uhalali wa uongozi wowote na hasa kwa mujibu wa Mwongozo wa Chama cha Mapinduzi wa mwaka 1981, ibara ya 107 unatokana na uongozi huo kuendelea kuwa tetezi wa kuaminika kwa maslahi ya makundi au kundi lililokuwa kubwa katika nchi yetu. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba kijiti kinapokabidhiwa kwa mama Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa kiongozi kutoka kwenye ngazi za msingi hadi ngazi ya Taifa ya chama chetu na ameongoza Serikali zote mbili, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano na hatimaye Makamu wa Rais, tuna uhakika kabisa nchi yetu ipo salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme la mwisho kwamba…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Kengele imegonga Mheshimiwa.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nina hakika kabisa miaka hii iliyobaki katika ungwe hii ya miaka mitano itakuwa ndiyo miaka mitano ya kwanza ya mama Suluhu Hassan na miaka mitano mingine itakuwa miaka ya ungwe yake ya pili kwa mujibu wa Katiba yetu. Hili tujiandae kifikra na kimtazamo kwa watu ambao walikuwa wanafikiri 2025 uongozi utabadilika. Ni zamu yao, sisi Bara tuliongoza miaka 23 ya Mwalimu, tukaongoza miaka 25 tena mingine siyo dhambi…
NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umeisha.
MHE CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, siyo dhambi sasa kwa Mzanzibar mmoja aliyejipambanua na mwenye sifa kuendelea kuwa Rais katika miaka hii iliyobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi ya kwanza kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nachukua nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Amiri Jeshi Mkuu na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, kwa jinsi anavyoliongoza Taifa letu kwa viwango ambavyo kila mtu anakiri na kazi yetu ni kuendelea kumwombea kwa Mwenyezi Mungu, ampe afya njema. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukupongeza wewe binafsi kwa kuchaguliwa kwa kura zote na Bunge hili la Jamhuri ya Muungano kuwa Spika wa Bunge letu. Hakika Mbeya imetupa mtu, hakika Magufuli alimwona mtu makini, hakika aliyekuteua kuingia kwenye Bunge la Katiba aliona mbali na leo Watanzania watashuhudia uwezo wako katika kipindi cha uongozi wako. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Spika, nisiwe mwizi wa fadhila, niwapongeze Wabunge ambao wamepata dhamana ya kuaminiwa na Rais kwa nafasi mbalimbali; nampongeza Mheshimiwa Shangai kwa kuchaguliwa na wananchi wa Ngorongoro. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nianze mchango wangu sasa kwanza kwa kuwashukuru waliowasilisha taarifa za Kamati zote mbili, lakini nianze na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Mtakumbuka tumekuwa na mgogoro wa muda mrefu kati ya wananchi au watumiaji wa ardhi na Hifadhi zetu za Taifa kwa muda mrefu; na Rais wa Awamu ya Tano aliunda Kamati ya Makatibu Wakuu na Mawaziri na baada ya kazi kukamilika, alisema maamuzi yatatolewa.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alisema kazi inaendelea, alitekeleza uamuzi huo kwa kufanya uamuzi wa haraka na kwa muda mfupi sana aliweka historia ya kuwatuma Mawaziri wapatao nane kuzunguka nchi nzima kutoa maamuzi ya Serikali ya kilio cha muda mrefu cha wananchi wa maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, Mawaziri hawa wanane wakiongozwa na Mheshimiwa Lukuvi, wakati huo akiwa Waziri wa Ardhi, walifika Jimbo la Simanjiro kutokana na mgogoro uliokuwepo kati ya Kijiji cha Kimotoro kwa upande mmoja na Pori la Mkungunero Game Reserve kwa upande mwingine; na pia kushughulikia mgogoro uliokuwepo kwa Vijiji vya Wilaya ya Kiteto kwa maana ya Erikiushi, Bwawani na Katikati, lakini kushughulikia pia mgogoro ulioko kati ya Mkungunero na Jimbo la Kondoa Vijijini la Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji na maamuzi yale yalitangazwa na wananchi walipata faraja na hakika walimsifu sana Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza mpaka sasa, baada ya maamuzi na maelekezo ya Rais ambayo yalikuja kutamkwa na Mawaziri, watendaji na wataalam walioambiwa wafanye kazi hiyo, mpaka sasa wameshindwa kukamilisha kazi hiyo kwa sababu wanazozijua wao wenyewe. Ombi langu kwa Waziri Mkuu na kwa Serikali, wale waliotumwa kufanya kazi hiyo wakamilishe haraka ili wananchi…
SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Venant.
T A A R I F A
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, mchangiaji anaongea vizuri sana juu ya Mawaziri hawa, lakini nataka nimpe taarifa kwamba kweli walitumia fedha nyingi kuzunguka kuja kutatua migogoro hii, lakini cha ajabu wataalam waliachiwa hili jukumu la kusaidia kutatua migogoro hii, wenyewe wanasema wanahitaji maelekezo kutoka kwa wahusika kwa barua. Kwa hiyo nampa taarifa kuwa Serikali sasa ipeleke maelekezo kwa barua ili sasa migogoro hii iweze kwisha.
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
SPIKA: Mheshimiwa Christopher Ole-Sendeka.
MHE. CHRISTOPHER O. SENDEKA: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa yake na ninaungana naye kuiomba Serikali ifuatilie kazi ambayo watendaji walipewa ya kuhakikisha kwamba wanamaliza mgogoro huu ili ahadi ya Rais iweze kuwa ni ya kweli kama alivyoahidi mwenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niende sasa katika suala ambalo ninaliomba Bunge hili lijipe muda wa kuungana na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kupata muda wa kulitafakari, nalo ni suala la mgogoro uliopo katika maeneo mawili ya Wilaya ya Ngorongoro. Kwanza Tarafa ya Ngorongoro yenye kilometa za mraba 8,000 eneo ambalo kuna maisha mseto kati ya wanyamapori, binadamu na mifugo inayofugwa na binadamu ambayo imeanza mwaka 1959.
Mheshimiwa Spika, mgogoro mwingine ni katika eneo la kilometa 1,500 za Tarafa za Loliondo ambayo inatakiwa ifanywe kuwa ama Game Reserve au Game Control Area. Jambo hili ni vizuri sana Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania likaelewa, likapata muda wakati Serikali inafanya tathmini, Bunge lako likapeleka Kamati ya kuyajua mambo haya. Kwa sababu upotoshaji unaoendelea kufanywa na baadhi ya vyombo vya habari na upotoshaji unaofanywa na social media hakika hauwatendei haki wananchi wa Ngorongoro.
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba ninukuu maneno haya ya gazeti la Jamhuri la tarehe 1 mpaka 7 Februari, linasema hivi: “Loliondo na Ngorongoro kwa ujumla wake ni za Watanzania. Hivyo sote tuna wajibu wa kuona ikiendelea kuwepo ili iwe na manufaa kwa Watanzania na walimwengu wote. Haiwezekani kabila moja katika nchi likatae kutii mipango ya Serikali hasa ikizingatiwa kuwa kinachofanywa na dola kina manufaa makubwa kwa Umma na kwa nchi.” (Narudia), “haiwezekani kabila moja likatae kutii.” Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Spika, lugha hii siyo njema hata kidogo. Haiwezekani! Unaposema haiwezekani kabila moja; wanaosemwa hapa, walioko Loliondo na Ngorongoro ni kabila moja linaloitwa Wamasai. Wamasai hawa wamekuwa waungwana kwa uhifadhi. Kama kuna kabila lililoonesha uhifadhi bora na kuweza kuishi na wanyama katika eneo moja bila kuwadhuru ni Tarafa ya Ngorongoro katika Wilaya ya Ngorongoro ambalo wengi wa wananchi wanaoishi hapo ni Wamasai.
Mheshimiwa Spika, wananchi hao hao walitoa ardhi yote ya Serengeti, Tarangire, Ngorongoro na Lake Manyara. Leo unapozungumza kilometa za mraba 1,500 ambayo Mheshimiwa Waziri Pinda aliundia Tume na baada ya Tume yeye mwenyewe alikwenda; CCM iliunda Tume iliyoongozwa na Dkt. Mwigulu Nchemba, nami nilikuwa Mjumbe wake tukaleta taarifa. Waziri Mkuu wakati huo Mheshimiwa Mizengo Pinda akaenda Loliondo akatoa tamko la Serikali, juu ya msimamo wa Serikali kuhusu eneo la Loliondo na msimamo wa Serikali kuhusu eneo la Ngorongoro.
Mheshimiwa Spika, Wakati huo huo Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, baada ya kelele kuendelea alisema hivi akiwa kwenye matibabu; na haya ni maneno yake naomba ninukuu kwa ruhusa yako. Haya ilikuwa ni tarehe 23 Novemba, 2014.
Mheshimiwa Spika, nami naomba ninukuu kwa sababu aliandika kwenye twitter yake kwa Kiingereza: “There has never been, nor will there ever be, any plan by the government of Tanzania to evict the Maasai people from their ancentral land.” Mwisho wa kunukuu. Haya ni maneno ya Rais wa Awamu ya Nne. Baada ya kelele za waandishi wa habari kutumia social media na kutumia magazeti yao kutuma ujumbe usio mzuri kwenye ulimwengu mzima.
Mheshimiwa Spika, hata leo naungana na Kamati, wanaposema mfumo wa matumizi bora ya ardhi, usimamizi hafifu ndiyo unapelekea tishio hili lililoko Ngorongoro. Nataka nikwambie, magazeti haya ambayo nilikuwa nakukuu ambayo ni mengi, ninayo hapa, yalikuwa ni matokeo ya semina iliyofanywa na Dkt. Fredy Manongi, Kamishna wa Uhifadhi wa Ngorongoro kwa kuwaita Wahariri wa Habari ili watoe picha wanayoitaka wao na huku wanasahau kwamba hata log yao Mamlaka ya Ngorongoro ina kichwa cha Faru, ina picha ya ng’ombe hapa, kuonyesha kwamba Ngorongoro ni kwa ajili ya wafugaji wa uhifadhi. Hata hivyo, anasahau section 6 ya sheria iliyoanzisha Mamlaka ya Ngorongoro inasema hivi, naomba ninukuu tena ili hawa wenzetu waelewe kwamba walioko Ngorongoro hawako kwa ajali. Inasema hivi: -
“The functions of the authority shall be to conserve and develop the natural resources of the conservation area;” ya pili, anazungumza: “to promote the tourism; na ya tatu: “to safeguard and promote the interest of Maasai citizens of the United Republic.” Hayo ndiyo malengo makuu matatu.
Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapo kwa sababu ujumbe wenyewe umefika, lakini kwa kukuomba na wewe utupe muda, isaidie Kamati hiyo iende Ngorongoro, ikae na wananchi wa Loliondo na wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro. Serikali nayo iunde Tume yake, tutekeleze maelekezo ya Mheshimiwa Rais, amewaambia wasaidizi wake, nendeni mkakae na viongozi wa mila…
SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, dakika moja, malizia.
MHE. CHRISTOPHER O. SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa dakika moja.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo kwamba viongozi wa Serikali wakakae na viongozi wa Ngorongoro, wakae na viongozi wa mila wa Ngorongoro ili watafute ufumbuzi wa namna ya kuendelezwa kwa ufugaji na uhifadhi katika eneo la Ngorongoro. Ninachoomba Serikali isimamie maelekezo ya Rais kama alivyoelekeza.
Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuichangia hoja hii. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii ya kwanza kabisa kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja za Kamati hizi mbili za Kudumu za Bunge lako tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayofanya ya kuiendeleza nchi yetu. Hakika ustawi wa nchi yetu sasa uko kwenye mikono salama, kutokana na jitihada anazozifanya Rais katika kujenga umoja wa kitaifa, kulinda muungano wetu, kutafuta uwezo kutoka nje na uwezo wa ndani ili kuleta ustawi wa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi Mheshimiwa Rais ameendelea kusaidia nchi yetu kuongozwa katika misingi ya kidemokrasia, misingi ya haki inayojali utu wa binadamu na ndio maana Mheshimiwa Rais amekataza watu wengine kufikishwa mahakamani, bila kesi zao kukamilika au upelelezi kukamilika, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwapongeza Wenyeviti wote wawili wa Kamati zote za kudumu kwa taarifa zao nzuri pamoja na Wabunge wanaounda Kamati hizo zote mbili wamefanya kazi nzuri na taarifa zao zote ni nzuri na nitamke bayana kwamba ninaziunga mkono taarifa zote mbili za Kamati hizo mbili za kudumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee na hata pamoja na malalamiko mengi ambayo yametoka katika ukumbi huu leo asubuhi, kulalamikia baadhi ya maeneo ambayo mambo hayaendi vizuri na hasa baadhi ya taasisi ambazo zimekuwa zimepewa mamlaka ya kutunga sheria hizi ndogo na kwa bahati mbaya wakawa wanatunga sheria ambazo kimsingi zinakinzana na sheria za Bunge na hata wakati mwingine kupingana au kukinzana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Feleshi, kwa kiwango kikubwa tangu ameingia katika ofisi hiyo, kwa kweli naona utulivu mkubwa na ushirikiano wake mkubwa sana wa kuishauri Serikali ipasavyo. (Makofi)
Sisi wengine tunaojua rekodi yake akiwa DPP, akiwa Jaji na hatimaye Jaji Kiongozi tunaamini kabisa ofisi hiyo iko salama na nampongeza yeye pamoja na DPP wa sasa. DPP wa sasa anafanya kazi nzuri na nina hakika haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyazungumza katika Bunge hili la leo zitarekebishwa na viongozi wetu hawa wawili ambao wanaongoza taasisi hizo muhimu sana. Pia kwa namna ya pekee nawapongeza pia Mawaziri wa Wizara hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijielekeze sasa katika baadhi ya maeneo ambayo ni ya maana sana na ni ya msingi pia katika hoja za Kamati zilizowasilisha leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na malalamiko mengi juu ya baadhi ya mambo ambayo hayajakaa vizuri na hasa katika maeneo yale ambayo yanahusiana na dhamana tuliopewa Kikatiba kwamba Bunge lako tukufu lina mamlaka ya kutunga sheria, lakini bahati mbaya sana kwa jinsi ilivyo tena hizi sheria ndogo ndogo wakati mwingine zinatungwa na kutumika kabla hazijaingia katika Bunge lako tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaungana na Waheshimiwa Wabunge kwamba ipo haja ya kubadilisha sheria na kulitizama jambo hilo upya ili sheria hizi ambazo zimegeuka kuwa kero kwa wananchi ziwe zimepitia katika Bunge lako tukufu. Bunge lako tukufu halina nafasi ya kulalamika wala Serikali haina nafasi ya kulalamika. Mimi siamini katika kiongozi anayepewa dhamana au mamlaka yoyote inayopewa dhamana badala ya kukalia kile kiti walichopewa na kujaa, unakaa upande mmoja kama una jipu. Ni vizuri siku zote unapopewa dhamana ukajaa katika kiti chako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na Bunge lako tukufu halina nafasi ya kulalamika kwa sababu kwanza linaongozwa na Spika mahiri, makini, mwanasheria aliyebobea, kiongozi madhubuti na ni kijana ambaye bado akili yake iko vizuri zaidi. Pia ana Wenyeviti wasaidizi na Naibu Spika wa viwango. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hivi kwa sababu mamlaka ya kuisimamia na kuishauri Serikali ni ya kwetu kwa mujibu wa Katiba. Lakini Ibara ya 151(1) inaweka tafsiri bayana ya mamlaka ya nchi kwamba ni pamoja na Serikali na Bunge sisi tumetajwa bayana, Mahakama haikutajwa kinagaubaga katika Ibara ya 151 katika tafsiri ya mamlaka ya nchi. Kwa hiyo, sisi ni mamlaka ya nchi pamoja na executive. Sisi katika Ibara ya 63 tumepewa mamlaka ya kuisimamia na kuishauri Serikali ikiwa sisi ndio chombo kikuu kwa mujibu wa Katiba kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siamini katika Bunge ambalo linaona kuna tatizo pale mbele, tunashauri kupitia Kamati za Kudumu za Bunge, tunashauri kapitia Bunge, bado zipo taasisi na maafisa wa umma ambao wanaelekezwa kubadili sheria zinazokinzana na sheria za Bunge, wanaelekezwa kubadilisha sheria zinazokinzana na Katiba ambazo ni batili moja kwa moja kwa mujibu wa Katiba bado wanaendelea kunyamaza na kupuuza maelekezo ya Bunge lako tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kabisa kwamba siku 30 zilizotolewa na siku 60 zilizopendekezwa na Kamati tutaziheshimu na kuziunga mkono kupitisha maazimio hayo leo na baada ya hizo siku 60 ninaamini kabisa na wale waliopewa siku 30 watarekebisha madhaifu yaliyoonekana na Kamati zetu mbili za kudumu ambazo zimeshughulikia na hasa Kamati inayoshughulikia sheria ndogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kwamba Bunge hili ni Bunge madhubuti na kwa kweli halipaswi kulalamika. Miaka ya 1990 Bunge hili hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipokuwa imekuja na hoja ya Tanganyika ya G55 ambayo ilikuwa ni kinyume na sera za CCM, kinyume na Article of Union, lakini bado ndani ya muda mfupi wana-CCM walisimama na Wabunge walisimama wakakataa na Mkutano Mkuu wa Chimwaga ulikataa, lakini baadaye wakarudi tena na kuleta hoja hiyo kutokana na hasira walizokuwa nazo na kutaka kutuingiza katika muundo wa Serikali tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema hasira zenu zisielekezwe kwenye kutuundia jambo linalokinzana na sera, jambo linalokinzana na Article of Union ambayo ndio msingi wa Muungano wa nchi zetu mbili na Mwalimu alitumia maneno haya yafuatayo na mimi naomba niyanukuu katika kitabu cha Mwalimu cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania na hili nalisema kwa taasisi hii na nalisema kwa taasisi zingine zote naomba kunukuu; “Kukubali kufanywa vikaragosi vya viongozi ni dalili ya woga, si dalili ya heshima na woga na heshima ni vitu viwili mbalimbali. Maadili mema hayatudai tuwaogope viongozi wetu na viongozi makini hupenda kupata heshima ya wananchi wenzao, lakini hawapendi kuogopwa. Kuogopwa ni sifa na ada ya madikteta. Viongozi halisi hawapendi kuishiriki, kujenga mazoea ya kutii viongozi hata katika mambo haramu ni dalili ya woga ni kukaribisha udikteta.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nayatumia maneno haya kwa sababu sifurahii kuona Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania likilalamika juu ya maamuzi ambayo mlikwishayafanya. Ningependa tutoke na maazimio kwamba wale walioagizwa wayafanye tuwajue ni akina nani walipaswa kusimamia katika sekta hizo na Bunge hili lielezwe ni nani hao wanaokaidi.
Kwa hiyo, sisi tuko hapa kwa niaba ya wananchi tuchukue hatua, kama hatuna mamlaka ya kuchukua hatua dhidi ya Waziri mmoja mmoja, dhidi ya mtendaji mmoja mmoja, tuchukue hatua kwa wale ambao tuna mamlaka nao ili wawasimamie hao ambao wamepewa dhamana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Edward Olelekaita, Mbunge wa Kiteto alibainisha juu ya dhahama wanazozipata wafugaji sasa kutokana na tafsiri ambazo hazijakaa vizuri. Nchi yetu au Bunge letu lipitie Sheria Namba 5 ya Uhifadhi ya Wanyamapori ya mwaka 2009 na marekebisho mengine ya mwaka 2022, yapo maeneo ambayo kwa mujibu wa sheria iliyokuwepo hayakuwa yanatajwa kama ni maeneo ya uhifadhi, lakini kwa sheria ya sasa ni maeneo yaliyohifadhiwa, ni ardhi ya hifadhi. Lakini unakuja kuhifadhi wakati tayari kuna binadamu walioko pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tukae pamoja kwa sababu ulindaji, uhifadhi na uendelezaji wa rasilimali za nchi ni jukumu la kila raia wa nchi hii, ni jukumu la kila Mbunge aliyeko katika ukumbi huu, ni jukumu la kila kiongozi. Tukae ili pale ambapo ardhi za vijiji ambazo sasa mnataka kufanya kwa Wildlife Migratory Route, Wildlife Dispersal Area, Breeding Areas mnataka kufanya kuwa Game Controlled Area, katika maeneo ambayo yako kwenye ardhi za vijiji hakuna namna unaweza kuichukua ardhi ya kijiji ambayo imekataliwa na sheria ukaifanya kuwa Game Controlled Area.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiacha hii kwa sababu yako mazungumzo na malalamiko niliyowasilisha nikiamini nitakaa na viongozi wenzangu tuyafikie mwisho, lakini kikubwa ninachosema hamuwezi kuendelea kutoza ng’ombe faini ya shilingi 100,000 badala ya ku-compound kama sheria inavyosema katika kifungu cha Sheria ya TANAPA (National Parks) kifungu cha 20A imeweka bayana kabisa juu ya ku- compound lile kosa na kwa yule muhusika ndio anayepigwa faini, ng’ombe hawezi kupigwa faini, anapigwa mmiliki wa ng’ombe.
Kwa hiyo. rai yangu ni vizuri tukazingatia ushauri uliotolewa na Wabunge ili kuepusha adha hii ya kuwatoza wananchi ada zisizokuwa na sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi sote ni mashahidi juu ya hukumu ya Mheshimiwa Elenina ambaye alimaliza kesi yake mwaka 2018 na akashinda, yule mfugaji ambaye amefilisiwa na mnamwona kwenye mitandao ambaye ameshinda kesi yake Mahakama Kuu. Bado DPP aliweza kung’ang’ania wale ng’ombe kwamba akate rufaa abaki na ng’ombe. Jaji wa Mahakama Kuu Jaji Kalombola alikataa na baada ya kukataa bado walikaidi na wale ng’ombe wamekufa na yule mfugaji alikuja kupewa ng’ombe 90 kati ya ng’ombe 265 ambao walikaa nao kwa muda wa miaka mitatu. Ng’ombe 265 wakizaa kila mwaka kwa miaka mitatu ni ng’ombe wangapi?
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja, nakushukuru kwa kunipa nafasi hiyo, na kwa kweli naishauri Serikali iendelee kuwa sikivu katika eneo hilo, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi ya kwanza kukushukuru wewe mwenye kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Madini.
Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye eneo linalonihusu la madini ya vito. Lakini kabla ya kufika huko niseme, waswahili wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, kwa muda mfupi niliokaa kwenye Bunge hili baada ya kurudi juzi Waziri Biteko amefika katika eneo la Mererani kama mara tatu hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, na nilimnong’onezea juu ya kero zinazowakabili wachimbani wa madini ya vito aina ya Tanzanite pale Mererani. Kwa wale wasiofahamu wachimbaji wapatao kati ya 8,000 au 10,000 wanaingia na kutoka katika eneo la machimbo ya Mererani; 8000 – 10000 kwa siku. Nilimuomba Mheshimiwa Waziri asaidie kujenga shade ambayo ingeweza kusaidia wachimbaji wale kujikinga wakati wa mvua na wakati wa jua. Mheshimiwa Biteko alichukua uamuzi palepale na kutoa maelekezo na tatizo hilo sasa linakaribia kufika ukingoni maana jengo hilo linajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilimuomba Mheshimiwa Waziri aweke utaratibu rafiki unaoweza kuwasaidia wachimbaji wadogo na hasa wale wakipato cha chini kuweza kumudu kuendesha biashara katika eneo la uzio wa Mererani, nilipata majibu positive na alitoa maelekezo ambayo ni rafiki na wachimbaji walimpongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilimuomba sana Mheshimiwa Waziri aliondoshe janga lililokuwa mbele yetu kitendo cha… natafuta lugha ya staha; kitendo cha fedheha cha ukaguzi usio na staha, wanaofanyiwa wachimbaji wa madini ya Tanzanite Mererani ambapo watu wapato 20 au 15 wa rika mbalimbali wanapotoka kwenye uchimbaji wakifika kwenye gate kuna vyumba viwili vya ukaguzi, kimoja cha wanawake na kimoja cha wanaume. Wanaume zaidi ya 20 au 15 kwa wakati mwingine; wanawekwa kwenye chumba hicho na kuvuliwa nguo zote, zote; na katika chumba cha wanawake vivyo hivyo, wanaingia kwenye chumba hicho bila kujali rika, bila kujali nini wanavuliwa nguo zao zote na wanaambiwa waruke kichura kidogo kitendo ambacho ni cha aibu. Haitarajiwi kwa Taifa kama letu ambalo linatambua na kuthamini misingi ya utu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini cha kustaajabisha zaidi, Mheshimiwa Waziri alitoa kauli mbele ya wachimbaji wadogo na mbele yangu kwamba jambo hili likome sasa na ukaguzi wa staha ufanyike. Alisema hivyo katika ziara yake ya kwanza, akarudia mbele ya Kamati ya Madini, baada yake siku iliyofuata ikaja Kamati inayoshughulika na masuala ya Ulinzi na Waziri wa Ulinzi ambaye ndiye anayeshughulikia mambo ya ulinzi wa madini pale getini.
Mheshimiwa Spika, ninapata mashaka, kwasababu Serikali haikuongea lugha moja, Wizara hizi mbili hazikuongea lugha moja na juzi tumefanya kikao cha pamoja kati ya Wizara ya Ulinzi, Wizara ya Madini, Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati kwa pamoja kujadili masuala ya Mererani. Kinachoshangaza hata baada ya ombi langu mbele ya Kamati hizo mbili ya Nishati la Kamati ya Ulinzi; hata jana na leo asubuhi ukaguzi unaoendelea ni ule ule, walichotofautisha ni kwamba wamiliki wa migodi na mameneja wa migodi wamepewa mlango wao wa kutokea na kwamba hawavuliwi nguo hao. Lakini wale maelfu wengine waliobaki wanaendelea na kitendo hicho cha fedheha.
Mheshimiwa Spika, waislam wanasema; “ukiliona jambo ovu liondoshe, kama huwezi kuliondosha lishtakie kwa mwenye uwezo kuliondosha na asipoliondosha endelea kulinyooshea kidole mpaka atakapopita mtu wa kuliondosha.” (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hili ni jambo ovu, ni jambo ambao halijarajiwi litendeke hasa na Serikali ya chama changu Serikali ya CCM. Ninataka maelezo ya Mheshimiwa Waziri leo, kauli ya Serikali itolewe na kwasababu kuna kujikanganya kati ya Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Madini. Waziri wa Madini yupo clear kwenye jambo hili, Waziri wa Ulinzi anapata kigugumizi, Waziri Mkuu atoe kauli juu ya jambo hili, kama Tanzania tumefika mahali ambapo Watanzania wanavuliwa nguo hadharani na kukaguliwa na watoto ambao wanaweza kuwazaa…
SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka nilitaka tu kukuhakikishia kwamba Waziri wa Ulinzi yupo.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana napokea maelekezo yako mkuu.
Mheshimiwa Spika, ninachotaka ni kwamba atoe kauli yeye vinginevyo ushauri wangu utakuwa ni vizuri kila mtu aonje fedheha hii. Tulikataa wakati wa Azimio la Arusha tukasema tumeonewa kiasi cha kutosha, tumenyonywa kiasi cha kutosha, tumepuuzwa kiasi cha kutosha, unyonge wetu ndio uliotupelekea tuonewe, tunyanyaswe na tupuuzwe, sasa tunataka mapinduzi, mapinduzi yatakayotupelekea tusionewe tena, tusipuuzwe tena, tusinyonywe tena. Azimio la Arusha mwaka 1967 na tukaweka kwenye utangulizi wa Mwongozo wa TANU wa mwaka 1971. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tamko letu ni la mwaka 1967, kama mnadhani kitendo hiki ni kizuri na mnadhani watendewe watu wa Mererani onesheni demo, ninyi ambao mmepewa dhamana Mawaziri na Makatibu Wakuu tafuteni chumba cha wanaume peke yenu, bila kujali….(Makofi)
SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, hiyo hairuhusiwa Bungeni kuwashauri Mawaziri waende wakaruke kichura. Aaah dakika zako zimekwisha Mheshimiwa.