Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Dr. Charles Stephen Kimei (65 total)

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niulize maswali mawili mafupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nashukuru sana kwamba nimepewa jibu la kina na naamini tutaendelea kulifuatilia suala hili. Zaidi ni kwamba hawa operators wanakuja na watu kutoka sehemu nyingine ambao hawajui hii mikataba. Kwa hiyo, hawaajiri wale vijana ambao wanatoka kwenye vijiji karibu na ule mlima, wao hawaelewi mikataba hiyo hivyo wanalipwa kidogo sana. Je, hatuwezi kuweka uwiano fulani hasa kwa zile shughuli ambazo hazihitaji taaluma kwamba hawa operators waweze kuajiri au kuchukua vijana kutoka kwenye kundi la wale ambao wanatoka karibu na mlima kwa sababu hiyo ni njia mojawapo ya kuwapa motosha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni nyeti kidogo ni hili suala la nusu mile. Kwa vile tunajua kwamba watu wanaolinda ule mlima ni wale wanavijiji walio karibu na hifadhi ya mlima ule inakuwaje sasa suala la nusu mile. Nusu mile ni suala nimezungumza na Mheshimiwa Waziri na ni nyeti kidogo lakini nafikiri kwamba tusiliangalie kama watu wanaomba kuingia msituni isipokuwa ni ku-review ile mipaka ya msitu na kuongeza sehemu ndogo ambayo inaweza ikasaidia wale wananchi wanaoishi karibu kuweza kupata kuni na kupata malisho ya wanyama bila kuathiri miti. Siyo suala la kuingia isipokuwa ni suala la kupanua…
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya wageni kupata ajira kwenye maeneo ya hifadhi hasa kwenye Mlima Kilimanjaro. Hata hivyo, katika mwongozo wa waongoza utalii kuna kiwango ambacho wamewekewa waongoza utalii ambapo hawa watumishi kwa maana ya wanaoomba ajira wanaomba kwa kuzingatia mwongozo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto pia kwenye upande wa kiwango kwamba mtu anapokuwa anahitaji ajira basi anapunguza kiwango kinakuwa chini ya mwongozo uliopo. Waongoza utalii (tour operators) wao wanazingatia zaidi kupata faida kwenye biashara zao. Kwa hiyo, huyu mtumishi anapokuwa akiomba ajira na kwa kuzingatia kwamba waombaji wa ajira wanakuwa ni wengi basi anapunguza kiwango ili aweze kupata ajira. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto hii lakini tunawashauri watumishi wanaokutana na changamoto hizi waende kwenye Tume ya Usuluhishi (Mahakama ya Kazi) ambayo inasimamia haki za mtumishi yeyote anapokuwa amedhulumiwa haki yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine ni kuhusu nusu mile, naomba itambulike kwamba maeneo ya hifadhi yanapokuwa yametangazwa kuwa hifadhi hairuhusiwi kufanya kitu chochote zaidi ya uhifadhi. Nimuombe sana Mheshimiwa Dkt. Kimei, sisi kama Serikali tunapokuwa tunahifadhi maeneo haya tunatunza ili yawe kivutio na kwa ajili ya kutuletea mapato.

Kwa hiyo, tunapokuwa tunatunza, hairuhusiwi kufanya kitu chochote ndani ya eneo la hifadhi, hata kama ni kuokota kuni hairuhusiwi. Kuna maeneo mengine ambayo huwa tunawatengea wananchi kwa ajili ya kuendelea na shughuli zingine kama ufugaji, uvuvi pamoja na kilimo lakini maeneo yanayotunzwa kama hifadhi hairuhusiwi kufanya kitu chochote.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi sana kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, kwa kweli nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ambayo imeletwa na Mheshimiwa Dkt. Kimei inahusika pia na masuala ya mikataba ya ajira na stahiki za wafanyakazi na mfumo mzima wa uratibu wa ajira katika eneo la Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Waziri ameliweka vizuri, tayari Wizara ya Maliasili na Wizara yetu tumeweka ule mwongozo. Tunawaomba sana wafanyakazi wote wanapokutana na changamoto zozote ambazo pia zinahusiana na Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, 2004, wajitahidi kuwa wanatoa taarifa mapema sana kwenye ofisi zetu za Idara ya Kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa sasa imeamua kufungua kliniki maalum. Kila Ijumaa ya mwisho wa mwezi wafanyakazi wote ambao wanaona wana changamoto zinazohusiana na sheria za kazi watakuwa wanaripoti kwenye ofisi zetu za kazi ili wakaeleze zile changamoto wanazozipata kama ni za mishahara, mikataba na mambo mengine yoyote ili ofisi ya Waziri ya Waziri Mkuu iweze kuchukua hatua haraka ili kuondoa migogoro katika maeneo ya kazi kati ya mfanyakazi na mwajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamuomba sana Mheshimiwa Kimei kama ana mambo ya ziada aonane pia na ofisi yetu na tutaweza kulifanyia kazi na tutaagiza utaratibu na mwongozo usimamiwe vizuri. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona, nilitaka kunyosha mikono miwili. Naomba niulize swali moja. Kwa vile Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa kwenye kampeni kule Vunjo aliahidi kujenga barabara ya Kilema a.k.a barabara ya Nyerere ambayo ni kilometa tisa; barabara ya Uchira kwenda Kisomachi kilometa nane tu na Mabogini – Kahe na Chekereni ambayo na yenyewe ni kilometa 22 tu kwa kiwango cha lami. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza akatuhakikishia kwamba, barabara hizo zimeingizwa kwenye mpango wa 2021/2022? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi alizosema ni ahadi za Rais na ni ahadi katika kipindi cha uchaguzi wa 2020. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Kimei avute subira kwa sababu, bajeti ndio inaenda kwa hiyo, tutaangalia. Siwezi nikasema kwa sasa kwa sababu, hiyo bajeti bado haijapitishwa, lakini kama ni ahadi ya Rais, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba, ahadi za Rais zitazingatiwa katika kutekelezwa kwa bajeti zinazokuja kuanzia 2021/2022. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa majibu mazuri na ya kina kuhusiana na swali hilo ambalo tumeuliza, lakini naomba niulize maswali mawili za ziada madogo. Swali la kwanza; kwa vile SIDO inalenga watu wa chini watu ambao wapo kwenye vijiji na kadhalika na hawa watu ni vigumu sana waweze kuelewa hivi vitu alivyovieleza kwa sababu hata mimi nilikuwa sivijui. Je, wana mpango gani wa kuiongezea SIDO uwezo wa kujitangaza na kutekeleza maonesho kwenye miji midogo midogo kama Mji wa Himo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kuhusiana na mabanda ya viwanda au majengo ya viwanda. Kasi ya ujengaji wa majengo haya ni ndogo sana pengine tunaenda na too much sophistication, lakini tukienda kwa mtindo mwingine naamini tutaweza tukaharakisha sana ujenzi wa haya mabanda. Je, kama wakienda na kasi hii kweli ni lini wanafikiria watatufikia sisi kule kwenye Mji wa Himo, Uchira na miji midogo midogo kwenye mikoa yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli uelewa wa wajasiriamali wengi kuhusu huduma zinazotolewa na Shirika letu la Kuhudumia Viwanda Vidogovidogo (SIDO) bado si wa kuridhisha sana kwa sababu taarifa nyingi haziwafikii wale wajasiriamali wadogo. Namshukuru Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei kwa mawazo mazuri kwamba sasa tuone namna ya pekee ya kuliwezesha shirika letu la SIDO kujitangaza zaidi kwa wajasiriamali wadogo ili waweze kutambua fursa na teknolojia ambazo zinatolewa na shirika letu la SIDO.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Kimei kwamba tunaenda kuwezesha SIDO na tunaenda kuwatengea fedha zaidi kwa maana ya mwaka ujao wa fedha 2021/2022 kuwatengea fedha zaidi ikiwemo kwa ajili ya kujitangaza ili angalau wajasiriamali wengi waweze kujua fursa na huduma za teknolojia ambazo zinazotolewa na shirika letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu majengo ya viwanda, naomba niwahakikishie Wabunge na Watanzania wote hasa wajasiriamali ambao wanataka kuwekeza katika viwanda kwa maana ya viwanda vidogo vidogo kwamba, tunakwenda kuwaongezea SIDO uwezo ili waweze kujenga majengo mengi zaidi ambapo humo wajasiriamali wetu wataweka viwanda vyao vidogo vidogo au mashine zao ambazo wataweza kuchakata mazao ya kilimo mbalimbali kulingana na mikoa au mahitaji ya sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaenda kuwaongezea uwezo SIDO ili angalau waendelee kujenga majengo mengi zaidi kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya wajasiriamali. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa fursa hii. Niseme kwamba kutokana na jitihada za wananchi wetu kule Vunjo kupanda miti na kuitunza kwenye mashamba yao ya kahawa na ndizi, ngedere na tumbili wameongezeka sana mpaka wamekuwa tishio kwa maisha ya watoto wachanga wanaoachwa nyumbani na ni vigumu sana kupambana na ngedere na tumbili kwa vile wana akili kama binadamu. Sasa nataka nijue, je Serikali ina suluhisho gani kuhusiana na ongezeko hili kuwaondoa hawa ngedere na tumbili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kimei kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli changamoto hii ipo katika Mkoa wa Kilimanjaro na wiki iliyopita tu tulienda kuangalia changamoto hii katika Wilaya ya Rombo na kukawa kuna changamoto ya nyani pamoja na hao ngedere. Wizara ya Maliasili na Utalii ilitoa tamko kwamba tutaenda kuwahamisha hao nyani pamoja na ngedere, tuwapeleke kwenye maeneo ya hifadhi ambako kutafaa zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niulize swali lifuatalo; mafuriko yaliyoikumba Hai na Moshi Vijijini yamelikumba pia Jimbo la Vunjo hususani Skimu za Kahe. Je, Serikali ina mpango gani pia kuhakikisha kwamba Skimu za Kahe nazo zinafanyiwa marekebisho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena, Mkoa wa Kilimanjaro, timu yetu ya wataalam hivi tunavyoongea ikiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo ipo huko. Tunatoa uzito sana athari zilizotokea katika Mkoa wa Kilimanjaro, kwa maana ya Wilaya zote zilizoathirika ikiwemo Jimbo la Mheshimiwa Dkt. Kimei.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie kwamba baada ya ripoti ya tathmini kurudi, skimu zote zitakuwa ni sehemu ya priority. Vilevile athari ambazo wakulima wamezipata ambao tuna uhakika kwamba hawatapata mavuno au chakula mwaka huu, tutatoa kipaumbele kinachostahili na kuweza kutatua hizo changamoto. Kwa hiyo, niwaombe Wabunge wa Mkoa wa Kilimanjaro na hasa wilaya zote zilizoathirika, watuvumilie wakati watu wetu wanaendelea kufanya kazi hii katika maeneo yao. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba niulize hivi, Je, Wizara ya TAMISEMI haioni umuhimu wa kuweka maafisa masoko kwenye halmashauri zetu. Tunajua kwamba tatizo kubwa kwenye halmashauri ni ukosefu wa masoko. Watu hawajaunganishwa na masoko, sasa tungekuwa na maafisa hawa wangetusaidia sana. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika uendeshaji wa shughuli za masoko katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Serikali imeweka utaratibu ambao pamoja na wakuu wa idara wengine, wakuu wa idara ya fedha na biashara kuna maafisa biashara katika halmashauri zetu ambao kimsingi wanafanya kazi kwa karibu ambazo zinafanana sana na Maafisa Masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo tunaendelea kuhakikisha kwamba tunaboresha mfumo huo kuhakikisha kwamba wale maafisa biashara ambao wanasimamia masoko na shughuli nyingine zote za biashara katika halmashauri wanafanya kazi zao kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wazo lake pia la kuwa na Maafisa Masoko tunalichukua, tutalifanyia tathmini na kuona kama tunaweza tukaongeza nguvu katika eneo hilo kuwa na maafisa biashara na pia kuwa na maafisa masoko. Kwasababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kuna ufanisi mkubwa wa biashara na ustawi wa mapato ya ndani lakini pia ya wananchi katika masoko yetu.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ubarikiwe sana. Kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inawajali sana wananchi wake wakiwemo wale wanaoishi kwenye Vijiji vya Kata ya Kirua Vunjo, Kilema, Marangu, Mamba na Mwika na wanaoishi kwenye vijiji vinavyozunguka msitu wa Mlima Kilimanjaro:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutathmini upya msimamo wake na kuwaruhusu wanavijiji hawa kutumia eneo la nusu maili ambalo limeainishwa kwenye mipaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nitoe rai tu kwa Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo ambayo tayari yanakuwa yameshatangazwa kuwa Hifadhi ya Taifa haturuhusiwi kufanya kitu chochote. Isipokuwa kama ana maombi ambayo anahitaji ifanyike tathmini, basi naomba kupitia Serikali ya Wilaya na Vijiji walete maombi kwenye Wizara, halafu tutaangalia tathmini kama itawezekana; na pale ambapo haiwezekani pia, tutawapa majibu. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kituo cha Afya pekee kinachotegemewa na watu zaidi ya 300,000 pale Vunjo ni cha Kilema. Kwenda kwenye kituo hiki, barabara iliyopo ni hiyo ya Mandaka – Kilema au barabara ya Nyerere. Sasa hivi barabara ile haipitiki kabisa, wagonjwa hawawezi kwenda kwenye kituo hiki cha afya. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri, chonde chonde atoe tamko la dharura watu waende kushughulikia barabara hii. Nitashukuru sana akitoa tamko hilo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei ameelezea hiyo barabara inayoelekea katika Kituo cha Afya Kilema kinachohudumia zaidi ya wananchi 300,000 kwamba haipitiki wakati huu na ameitaka Serikali itoe tamko. Niiagize TARURA kwamba waende wakafanye tathmini watuletee katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kusaidia, tuone namna gani tunapata fedha na kuitengeneza hiyo barabara kwa dharura ili wananchi waweze kupita.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru sana. Kusema kweli Serikali imetenga fedha nyingi. Kwenye Jimbo letu la Vunjo Kata 16 hakuna kituo cha afya cha Serikali isipokuwa vituo vikongwe, vichakavu vya Mwika, OPD Himo na Kiruavunjo. Ni chakavu hata havistahili kuitwa vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri atueleze ni lini watakarabati vituo hivi na kuviinua hadhi ili viweze kuwa vituo vya afya vinavyotumika na watu wa Vunjo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi tunatambua sana kwamba katika Jimbo la Vunjo kuna upungufu mkubwa wa vituo vya afya lakini hata vile vituo vya afya ambavyo vipo, vina uchakavu kwa sababu ni vya siku nyingi. Ndiyo maana katika mpango wetu ambao tumeuwasilisha na bajeti yetu ya mwaka 2021/2022 tumeweka kipaumbele kwanza cha kwenda kuhakikisha tunajenga vituo vya afya 211 katika maeneo ambayo hayana vituo vya afya.

Pili, kuhakikisha tunaweka mpango wa kwenda kukarabati na kupandisha hadhi vile vituo ambavyo vina sifa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba Jimbo la Vunjo pia litapewa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunafanyia kazi vituo hivyo vya afya. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri na nampongeza Waziri kwa kutoa majibu haya ambayo yanatoa faraja sana kwa hawa wanaoendesha shughuli hizo. Hata hivyo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, Serikali itakuwa tayari kurejesha kodi iliyokusanywa kutoka kwenye taasisi hizo kwa shinikizo na hatimaye kuzidhoofisha sana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali iko tayari kuchukua hatua za kinidhamu kwa hawa maafisa wa TRA wanaokiuka sheria? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Serikali ina utaratibu wa kurejesha fedha ambazo zilichukuliwa na kwa mujibu wa sheria zinatakiwa kurejeshwa kwa utaratibu ulio wa kawaida wa kufanya refund na refunds hizo huwa zinafanyika kwa mujibu wa sheria. Kwa maeneo ambako kuna makosa ya ukiukwaji wa kisheria, taratibu za kisheria huwa zinafuatwa na hatua stahiki za kinidhamu kuchukuliwa kwa wale wanaokiuka sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna maeneo ambako maafisa wetu wamekiuka sheria, taratibu za kisheria zitafuatwa na hatua za kisheria kuweza kuchukuliwa.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Swali langu dogo ni hili kwamba: Je, Serikali itaanza lini ujenzi wa barabara inayotoka Chekereni – Kahe kwenda Mabogini? Hii ni barabara pekee ambayo ni bypass kwa magari ambayo yanatoka Dar es Salaam kwenda Moshi na hakuna bypass nyingine. Kwa hiyo, ni lini wataanza ujenzi huo ambao pia upo kwenye Ilani? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba eneo ambalo anataja tunalifahamu, lakini tumeweka mipango ya Serikali kutafuta fedha. Tutaanza mara moja baada ya kupata fedha kujenga barabara hiyo ambayo ni muhimu ili kuendeleza shughuli za kiuchumi katika eneo lake. Ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mimi ninauliza swali moja ambalo ni, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi kwenye Soko la Kimataifa la Mwika ambalo liko mbali sana kutoka Himo ambako ndiko kwenye kituo cha polisi?

Mheshimiwa Mwneyekiti, ahsante sana.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nimjibu Mheshimiwa Kimei, swali lake la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kimei, kama ulivyosema, na niseme tu kwamba uko umuhimu wa kuwa na kituo cha polisi. Si maeneo tu haya ya Mwika, lakini maeneo mengi ambayo yanaweza yakawa yanajihusisha na biashara kama ilivyo eneo la Mwika. Nilichukue suala hili ili tuone upande wa Serikali kulifanyia kazi haraka ili tuweze kuleta manufaa makubwa. Ili biashara iweze kushamiri vizuri tunahitaji kwa kweli kuwa na ulinzi wa kutosha katika maeneo haya. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa lakini kusema ukweli matengenezo yanayofanyika hayatoshelezi kitu. Unafanya matengezo mwezi huu, mwezi ujao mvua kubwa ikinyesha unarudia tena matengenezo. Kusema kweli ahadi ambazo zilitupa ushindi sisi wana-CCM ni ahadi hii ya barabara ya Mandaka – Kilema ambayo Mheshimiwa Rais aliitoa. Naomba Mheshimiwa Waziri atueleze ni lini au anafanya commitment gani kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna taswira kwamba kule Kilimanjaro kuna barabara nzuri. Nataka niwahakikishie wananchi kwamba Kilimanjaro hatuna barabara nzuri, barabara zilizokuwepo ni zile za zamani zilizojengwa na Ushirika na zingine zinaenda mpakani. Sasa namuomba Mheshimiwa anayehusika, Waziri wa TAMISEMI, hajawahi kufika kwenye jimbo langu akaona hali ya usafiri ilivyo ngumu, najua kwamba tumeshapewa hela lakini hazitoshi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Kimei uliza swali lako.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa. Je, Waziri atakubali kuongozana nami nikamtembeze aone hali ya barabara za Vunjo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza Mheshimiwa Mbunge amesema anataka kujua commitment ya Serikali juu ya ahadi ya barabara ya Mandaka – Kilema itaanza kujengwa lini kwa kiwango cha lami. Niseme tu kwamba tumelipokea kwa sababu moja ya wajibu wetu ambao tulikuwa tunaufanya hapo awali ilikuwa ni kuchukua ahadi zote za viongozi ili tuziweke katika Mpango. Kwa sababu jana tumepitisha Bajeti Kuu na kuna ongezeko la fedha ambalo limetokea, naamini katika Mpango unaofuata tutakuwa tumeingiza na tutafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili kufika katika Jimbo lake, nimwambie tu hapa katika Bunge lako Tukufu kwamba niko tayari kwa sababu mara baada ya Bunge nitakuwa na ziara ya kuzunguka katika maeneo mbalimbali ikiwemo zile ahadi ambazo nimezitoa hapa kwa Wabunge mbalimbali kufika katika maeneo yao. Kwa hiyo, moja ya eneo ambalo nitafika ni pamoja na Vunjo. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuuliza kuhusu hii reli kutoka Dar es Salaam kwenda Moshi na Arusha ilifufuliwa, sasa imekufa, ni kitu gani kimeiua? Naomba Waziri hebu tueleze. (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hii reli haijafa ila zipo changamoto ambazo tunaendelea kuzifanyia kazi, kuongeza vitendeakazi pamoja na wafanyakazi katika eneo hili. Mheshimiwa Mbunge avute subira tunalifanyia kazi, reli hii itaendelea kufanya kazi ambavyo imekusudia Serikali, ndiyo maana ikaanzishwa baada ya muda mrefu sana. Ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniruhusu niulize maswali mawili madogo ya nyongeza, licha ya majibu mazuri yaliyotolewa na Wizara. Swali la kwanza; Jimbo la Vunjo ni jimbo lililo mpakani. Majimbo yaliyo mpakani yanakuwa na changamoto tofauti kidogo, kwa mfano, magendo na unajua Wachaga wanavyopenda magendo. Dawa za kulevya zinaingia halafu kunakuwa na uhamiaji haramu. Kwa hiyo, kuna umuhimu na tunaomba Serikali ituhakikishie kwamba, itachukua hatua gani ili kuimarisha ulinzi kwenye vituo vya polisi kwa kuongeza polisi pamoja na kuongeza bajeti kwa sababu, wanahitaji kuchukua za haraka wakati mambo kama yale yanapotokea?

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kwamba, kule Vunjo unywaji wa gongo, ulaji mirungi, bangi, dawa za kulevya umekithiri kwa sababu, of course watu hawana ajira wengi, lakini ukweli ni kwamba, imekithiri sana. Najua kwamba, Serikali za Mitaa zinafahamu jambo hili, lakini linahitaji national effort na tunataka tuombe Wizara iweze kutueleza inachukua mikakati gani ya kuweza kushughulikia tatizo hili la unywaji pombe kali, bangi na vitu vyote kama hivyo, otherwise tutapoteza kizazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Dkt. Charles Stephen Kimei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatutasubiri mpaka tufike sasa watu waanze kuandamana. Serikali kupitia Jeshi la Polisi tuna mikakati madhubuti ambayo tumeifanya na tunaendelea kuifanya. Ya mwanzo, ni kuhakikisha kwamba, tunafanya doria za mara kwa mara ili lengo na madhumuni kuweza kukamata na kukomesha hizo tabia pamoja na kwamba, zinakuwa na changamoto kidogo, lakini tutajitahidi katika kuhakikisha kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunaendeleza sasa suala zima la ulinzi shirikishi; lengo na madhumuni sasa jamii iweze kutumia fursa ya kuchukua nafasi ya kuelimisha vijana wao ili sasa vijana waweze kupunguza hii, lakini kikubwa zaidi tunachukua hatua za kisheria. Kwa hiyo, wale vijana ambao wanafanya hili, basi tutawachukulia hatua za kinidhamu, hatua za kisheria, ili vijana waweze kuachana na tabia au vitendo vya utumiaji wa dawa za kulevya na utumiaji wa hiyo gongo kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, nadhani maswali yalikuwa mawili, lakini yote yalikuwa yanaangalia kwenye gongo na bangi na masuala mengine. Nakushukuru sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani nyingi kwa Mheshimiwa Rais wetu kwa fedha tulizopata kwa kujenga vituo vya afya Pamoja na kukarabati kituo cha kule Kirua Vunjo na Marangu headquarter. Nina swali kuhusu kituo ambacho tumeahidiwa pale OPD Himo mji mdogo wa Himo. Kituo hiki kinahudumia watu wengi sana watu zaidi ya 36 elfu lakini bahati mbaya hakina majengo ya upasuaji, mahabara na Mochwari na tulipoahidiwa hili jambo na Mheshimiwa Naibu Waziri wa afya wakati wa kampeni tulijua kwamba tutafanyika na imefanyika lakini haya majengo hayapo. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, ni lini tutapata fedha kwa kujenga majengo haya ili kituo hiki sasa kiweze kutumika na kutoa huduma zote zinazostahili kwa kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei Mbunge wa jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tunavituo vingi nchini vikiwepo vituo vya Jimbo Vunjo ambavyo kwanza vinamiundombinu michache kulinganisha na huhitaji wa vituo vya afya ikiwemo majengo kama mahabara majengo ya upasuaji lakini pia upungufu wa mawodi. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kituo cha afya cha OPD himo ni miongoni mwa vituo ambavyo tumeviahinisha na tumeviwekea mpango kazi wa kutafuta fedha ili kwenda kujenga majengo hayo ambayo yatavifanya vikamilike kuwa vituo vya afya na hatimaye viweze kutoa huduma zile ambazo zinatarajiwa. Kwa hiyo, tunatafuta fedha Mheshimiwa Mbunge na niwahakikishie kwamba fedha ikipatikana tutawapa kipaumbele kitu cha afya cha OPD Himo.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ubarikiwe sana kwa kuniona. Swali langu linahusu Vyuo vya ufundi stadi vilivyopo kwenye Kata zetu kwenye Jimbo la Vunjo Kata ya Mwika, Kata ya Marangu, Kata ya Mamba na Kata ya Makuyuni Pamoja na Kiruavunjo ambavyo vimekufa. Naomba niulize, Serikali ina mpango gani wa kufufua vyuo hivi na kuvipa stadi mpya ambazo zitawawezesha wananchi wa Jimbo lile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mkakati gani kutuonesha kanzidata ya Vyuo vya Ufundi Stadi ambavyo vipo nchini ili tuweze kuwahamasisha wananchi wetu wakasome huko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Serikali ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na vyuo vya ufundi stadi katika kila Wilaya nchini. Vile vile Serikali inajikita kuhakikisha kwamba tunakuwa na vyuo vya ufundi stadi vya Mikoa na Kanda mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu, sasa hivi tumeanzisha vituo, zile center of excellence. Kwa mfano, kwa pale DIT Dar es Salaam tutakuwa na center of excellence katika masuala ya TEHAMA, Arusha eneo la Arusha Technical tuna center of excellence katika masuala ya nishati jadidifu, Mwanza tunaanza center of excellence katika masuala ya ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba Wilaya zote zitakwenda kupata vyuo hivi kwa sababu tumeona umuhimu na uhitaji wa vyuo hivi nchini. Vilevile tunajikita katika maeneo ya Mikoa sambamba na hivi vyuo ulivyovitaja, kwamba tayari sasa tupo katika tathmini ya kuhakikisha vyuo vyote vile ambavyo vilikuwa vimekufa zamani, tunaenda kuvifufua sambamba na kuanzisha vyuo vipya katika Wilaya zote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa biashara ya gesijoto imeshamiri sana duniani na imekuwa inaendelea kwa miaka mingi; na nchi nyingi zimefaidi kwa kuuza gesijoto ambayo inahifadhiwa kwenye misitu; na Tanzania yenyewe hii tunayo misitu mingi iliyohifadhiwa ambayo mojawapo ni ule wa KINAPA na ni mkubwa; naomba nijue mkakati wa Serikali wa kuingia kwenye biashara hii ya carbon trading kwa sababu itatupa fedha kule kwenye vijiji vyetu. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, kwa sababu aliyeuliza swali ni mtu mzito katika Kamati ya Mazingira, licha ya kumwomba alete swali hili kama swali la msingi, kwa faida kubwa ni kwamba tuna success story ndani ya nchi yetu katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika. Jambo hili, watu wa Tanganyika zaidi ya 3.2 billion wanakusanya kutokana na Carbonate Hydrates Program.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nadhani jambo hili tutaenda kulichakata vizuri, lakini litakapokuja katika swali la msingi tutalifanyia kazi vizuri kwa heshima ya Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa nimeshatoa machozi ya kutosha mbele ya viongozi wetu wakuu kuhusiana na uhitaji wa lami kwenye barabara zetu tatu fupi pale Vunjo ambazo ni Barabara ya Uchira-Kisomachi-Kolalie, Barabara ya Pofo-Mandaka-Kilema na Barabara ya Himo Sokoni- Lotima. Nataka nimwombe Waziri kama ataridhia kuambatana nami kwenda kutembelea barabara hizi ili aweze kuona uhalisia wa hadhi ya barabara hizi na kero ambazo wananchi wanapata? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu kwa kifupi swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo tayari kuambatana na Mbunge kwenda kuziona hizo barabara ili tuhakikishe kwamba tunawapatia ufumbuzi wa kudumu. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kuniona. Swali langu litahusu TEMESA na nimeshawasilisha changamoto zake kwa Kamati husika, lakini kwa fursa hii uliyonipa naomba nimuulize Waziri swali moja dogo. Je, kutokana na ucheleweshwaji na gharama kubwa zinazotumiwa na halmashauri zetu wanapopeleka magari na mitambo mingine TEMESA.

Je, Waziri yupo tayari kuiagiza TEMESA kuruhusu halmashauri zenye karakana zake kutengeneza magari yake yenyewe, hasa inapokuwa ni matengenezo madogo madogo?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. FREDY A. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Hili swali la TEMESA ni kwa mujibu wa sheria kwamba magari yote ya Serikali yatengenezwe chini ya TEMESA kwa hiyo, nachukua concern yako kama ambavyo umesema ili nasi tuweze kujadili upande wa Serikali. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Wizara, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. La kwanza; je, Wizara haioni umuhimu wa kuwawezesha halmashauri kutenga maeneo mahususi kwa wajasiriamali na kuyawekea miundombinu stahiki ili wale wanaopokea mikopo waweze kuanzia miradi yao na shughuli zao kwenye maeneo haya ambayo yatakuwa kama incubation center na pia waweze kupewa ushauri nasaha?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; kwa vile tunafahamu kwamba mikopo inayotolewa na NEDF chini ya SIDO inalipika, inarejeshwa kwa kiwango kikubwa cha zaidi ya aslilimia 90. Je, Wizara haioni umuhimu wa kushirikisha SIDO kwenye kutoa mikopo ya halmashauri?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa tunakubaliana na Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge kwamba halmashauri zetu lazima zitenge maeneo mahususi kwa ajili ya uwekezaji na maeneo haya pia wanufaika vikundi ambavyo vinakopa asilimia zile 10 wawe ni moja ya wanufaika katika maeneo haya ambayo yanatengwa mahususi kwa ajili ya uwekezaji. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hili tumeboresha zaidi, tumeshakaa na Wizara ya Kilimo kuangalia hata makundi ya vijana wasomi ambao wanapata asilimia 10 kwenye Halmashauri zetu, Majiji na Manispaa, kuangalia namna bora ya kuweza kuwasaidia maeneo mahususi kama haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo jambo hili tunalifanyia kazi na nitumie nafasi hii kuzielekeza Halmashauri zote nchini, kuhakikisha maagizo ya Serikali ya kutenga maeneo mahususi kwa ajili ya uwekezaji yanashughulikiwa. Tunashirikiana na Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi ili kuweza kuliratibu hili vyema kwa sababu yapo masuala ya fidia. Halmashauri nyingine zimekuwa na nia ya kutenga maeneo, lakini wanakosa fedha kwa ajili ya fidia. Kwa hiyo, yote haya tunayaangalia ndani ya Serikali ili kuhakikisha tunaratibu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuhusu mikopo ya SIDO na mikopo kupokea, hili ni eneo lingine ambalo Wizara Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara tunaangalia namna ya ku-link pamoja ili zile asilimia 10 ambazo tunazitoa kwenye halmashauri na fedha kupitia Mifuko mengine ndani ya Serikali, tunakaa pamoja na kuangalia namna bora ya kuipeleka kwenye makundi ili iweze kuleta tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili kwenye suala la asilimia 10 mikopo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunafanya tathmini ya nchi nzima kuangalia namna bora tutakayoweza kutumia fedha hizi kwa sababu tumetathmini ni takriban zaidi bilioni 60 kila mwaka zinapatikana kupitia halmashauri kupitia vikundi.

Kwa hiyo, tungependa kuona mabilioni haya yanapokwenda kwenye vikundi yanaleta tija, yanasaidia vikundi, lakini vikundi hivi vinasaidia nchi katika kujenga uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya tathmini hii kufanyika, tutaleta hapa Bungeni uchambuzi huo ili Waheshimiwa Wabunge waweze kushauri ili tuweze kwenda vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Swali langu ni fupi. Je, Serikali itatumia mkakati gani na ni lini itaanza kugawa hizo mbegu mnazosema tutagawiwa za ruzuku za miche ya kahawa kwa sababu muda unakwenda?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, zoezi la ugawaji wa miche chotara linaendelea na tumeshagawa katika Mikoa ya Kagera, Mbeya, Songwe pamoja na Mkoa wa Kilimanjaro, pia hata Mheshimiwa Ndakidemi ni shahidi katika eneo lako miche hii imeshagawiwa. Zoezi ambalo tunaendea nalo ni kuhakikisha kwamba, tunazalisha kwa wingi ifikie miche Milioni 20 ili tuweze kubadilisha ile mibuni iliyokaa muda mrefu tui-replace na hii mipya ili kuondokana na changamoto ambayo wakulima wengi wanaipata.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini niseme, tumejua kwamba uwekezaji kwenye TTCL unaweza ukageuka kuwa ni mkakati mzuri wa kuongeza mapato ya Serikali. Tatizo la kuunganisha watu linatokana tu na gharama hizo, njia mojawapo ya kupunguza gharama hizo ni kuiwezesha TTCL kupata mtaji au kupata mkopo kwa kupata dhamana au kwa kutumia dhamana ya Serikali ili iweze kuwaunganisha watu na kuwachaji polepole, kidogokidogo kwa miaka miwili mitatu, hizo gharama zitakuwa ndogo na watu wataomba kujiunga kwenye mkongo huu ambao ni cha msingi sana.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kwamba siku za karibuni tumesikia kwamba TCRA inataka kugawa masafa ya spectrum za 5G na tunajua kwamba nchi hii zama hizi ni zama za internet of things na ni Artificial Intelligence tunaingia na inahitajika sana 5G. Naomba niiulize Serikali, je, imejipanga namna gani kuiwezesha TTCL kupata masafa ya kutosha ya 5G katika ugawaji wa spectrum hizo?
WAZIRI WA HABARI MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza anauliza Serikali kama iko tayari kuliwezesha Shirika la Mawasiliano (TTCL) kupata mtaji. Majibu ni kwamba pamoja na kwamba tumeendelea kuwekeza hata Bajeti hii iliyopita hapa Serikali imetenga zaidi ya bilioni 150 kwa ajili ya kujenga mkongo. Huu mkongo tunaukabidhi sasa kwa TTCL ili waweze kuuendesha kibiashara ikiwemo kutafuta fedha kwenye vyombo vya fedha kwa ajili ya kujenga, kuimarisha na kuwahudumia wateja wao. Uamuzi huu utaboresha huduma na kuipa mtaji TTCL.

Mheshimiwa Spika, swali la pili kama tuko tayari kutoa upendeleo maalum kwenye umiliki wa spectrum. Ni kweli kwamba internet of things ndio dunia inakokwenda na ni kweli kwamba 5G itakwenda kubadilisha matumizi hayo, lakini kama Serikali mauzo ya hizi spectrum tunayauza kwa uwazi na tunataka kila mmoja akashiriki na hatuna mpango wa kumpendelea mtu. Hivi juzi tumefanya mnada, tukapata zaidi dola milioni 187 kwa sababu mnada ulitenda haki, kila mmoja aliingia sokoni, akashindana akapata ambacho alikuwa anastahili kupata.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Je, ni lini Serikali itamalizia kipande kilichobakia kwenye Kawawa Road kufikisha Marangu Mtoni kwa hadhi ya lami, tulipewa ahadi na Mheshimiwa Rais Kikwete awamu zile na iko kwenye Ilani ya CCM?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimwondoe hofu kwa sababu tumeshajenga awamu ya kwanza na kilichobaki nikumalizia katika eneo la pili na uzuri barabara hii iko katika mipango ya TARURA. Kwa hiyo, kwa sasa tunatafuta fedha tutakapopata mara moja naamini kabisa kwa sababu iko katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi barabara hii tutaitengeneza. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nafurahi sana.

Je, Mheshimiwa Waziri anaweza akaniambia ni lini ukarabati wa skimu zilizo kwenye Kata ya Kahe Magharibi na mifereji iliyo kwenye Kata za Marangu Mashariki, Kirua Vunjo na Kilema utafanyika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tuna orodha ya miradi mingi sana ambayo mwaka huu wa fedha tunaifanyia kazi. Hivyo, nitaomba mimi na Mheshimiwa Mbunge tukae tuangalie maeneo ambayo tutayafanyia utekelezaji mwaka huu katika Mkoa wa Kilimanjaro ni yapi, na ya mwaka unaokuja ni yapi, ili kama hayapo katika mwaka huu wa fedha basi tuyaingize kwa ajili ya mwaka ujao wa fedha. Lakini lengo letu ni kuhakikisha mifereji yote hii inafanyiwa kazi na wakulima wa kutoka Jimboni kwa Mheshimiwa Kimei wanapata fursa ya kilimo cha umwagiliaji.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri; je, mifereji iliyo kwenye Kata ya Kilema na Kirua Vunjo na ile skimu ya Kahe wanaifahamu? Mbona haijawahi kuangaliwa siku za karibuni? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, miradi yote ya umwagiliaji nchini inafahamika na ndiyo maana katika maelezo yangu ya awali nilisema tunayo miradi mingi sana. Tumeielekeza Tume badala ya kuendelea kukumbatia miradi mingi ambayo haifanyi kazi, tunaanza ku-take stock kupata mradi ambao unahitaji marekebisho madogo, mradi ambao unahitaji marekebisho makubwa, baadaye tuweke nguvu kukamilisha miradi hii ikiwemo mradi wa Mheshimiwa Mbunge.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Waziri kwa kuwa muwazi na kuwa mtu mzuri. Alitembelea Vunjo baada ya kuahidi hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni hivi, je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuinua hadhi ya OPD Himo kuwa Kituo cha Afya kwa kutekeleza majengo matatu yanayostahili pale, pamoja na watumishi wanaohitajika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambacho anahitaji tu ni kwamba kwenye eneo hilo la Himo tupandishe hadhi, tuongeze watumishi, tujenge jengo la OPD na anachotaka kufahamu tu, ni lini sasa ile huduma ambayo ameikusudia Mheshimiwa Mbunge itatekelezeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Serikali imelipokea na tutalifanyia kazi kwa sababu Serikali ya Awamu ya Sita moja ya ajenda yake kubwa kabisa ni kuhakikisha tunaboresha huduma za afya nchini. Ahsante sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nimpongeze sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nimesikiliza hapa maswali kwenye Ofisi ya Rais, TAMISEMI takribani Wabunge wengi ambao wamekuwa wakiuliza maswali ya nyongeza wamekuwa na hofu ya uhaba wa watumishi na hasa kwenye sekta ya elimu na sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasimama hapa kwa heshima kubwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba niwaarifu Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais na Serikali yake wametambua tatizo hili la uhaba wa watumishi na hasa kwenye miradi ya sekta ya afya na sekta ya elimu. Hivyo basi, Mheshimiwa Rais ametoa kibali. Ahadi ya Serikali kwa mwaka huu wa fedha ilikuwa tuajiri watumishi 44,000; tayari Serikali ilishaajiri watumishi wapya na wa ajira mbadala 12,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais ameridhia na wiki ijayo nitatoa tangazo rasmi la ajira 32,000 na utaratibu wa ajira hizo na mgawanyo wake katika sekta ambazo zinaongoza kwa uhaba wa watumishi, maelezo yote nitayatoa wiki ijayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, Serikali ya Awamu ya Sita inajali tatizo la uhaba wa watumishi nchini. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kuwasaidia wananchi wa Kata ya Mwika Kaskazini kumalizia kituo muhimu sana kwenye Soko Kuu la Mwika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama wananchi wa Kata hiyo wameshajenga kituo wanahitaji kupata msaada wa Serikali kukamilisha tutahitaji tu uongozi wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro waweze kufanya tathmini kuona jengo limefika kiwango gani ili waweze kuliingiza kwenye mpango wa ujenzi kama tunavyofanya kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Kimei, tukupongeze kwa kuhamasisha wananchi na sisi tutakuunga mkono baada ya kupata uthamini huo.
MHE. DKT.CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, kwenye barabara ya Himo kuelekea Rombo, eneo wanalovuka wanafunzi wa Shule ya Korona na maeneo yale yanayokaribia masoko ya Kisambo na Mwika ni hatari sana kwa wapita njia lakini kwa magari pia. Je, Serikali ipo tayari kujenga matuta kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la matuta ni suala ambalo linategemeana na wataalam. Naomba niwaagize wataalam wa TANROADS hasa Meneja wa Mkoa wa Kilimanjaro, aende akafanye usanifu ili aone kama kuna umuhimu wa kufanya suala hilo. Ni vyema akawasiliana na Mheshimiwa Mbunge ili aone maeneo ambayo anahitaji suala hili linakotakiwa kufanyika, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa vile bei za miche ya kisasa ya kahawa, ya miparachichi hiyo tunayozungumza, ya migomba bei zake ni juu sana. Sijui Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku kwa miche hiyo? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka ujao wa fedha tutakapopitisha bajeti hapa mtaona kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo inatoa guidance juu ya subsidy kwenye zao la avocado na baadhi ya mazao na mazao haya kwa muda mrefu yalikuwa hayana guidance, hayajulikani nani mzalishaji kila mtu anajizalishia barabarani.

Kwa hiyo, tunazindua guiding ya uzalishaji wa miche ya avocado na mazao ya miti na kutakuwa kama ambavyo mzalishaji wa mbegu anavyozalisha na hapo mtaona kwenye bajeti tutatenga fedha kwa ajili ya ku-subsidize uzalishaji wa miche milioni 20 kuanzia mwaka kesho kwa uwezo wa Mungu. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, inasikitisha sana, nashukuru sana ametoa majibu ya swali hilo. Hata hivyo inasikitisha sana kwamba mifuko hii inajikita kwenye majiji na kwenye manspaa ambazo zina uwezo mkubwa kwa zile asilimia zao 10 kutoa mikopo kwa vijana, wanawake na walemavu. Wamejikita huko sasa, ni ile ile dhana kwamba watu wanaohitaji zaidi ni vijijini lakini hii mifuko hailengi wale wa vijijini.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuhakikisha kwamba mifuko hii inabadilisha misimamo yake au mitizamo yake na kulenga zaidi Halmashauri kwenye wilaya za vijijini? Hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, je, Serikali haioni umuhimu wa kuunganisha mifuko hii ili kupunguza gharama za uendeshaji na pia kutoa usawa zaidi na ufanisi katika kutoa mikopo yake?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika moja ya mikakati ambayo tunaifanya Serikali ni kuona namna gani mifuko hii ya uwezeshaji itawasaidia zaidi wananchi walioko katika maeneo ya vijijini na ndio maana moja ya mifuko hii au pesa zinazotolewa kwa wajasiliamali ile asilimia 10 ina gusa katika Halmashauri zote ambazo zinagusa pia vijijini. Pia zaidi tutaangalia na hii mifuko mingine ikiwemo ya NEDF, SELFU na TAFF iweze kufika kule vijijini kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameshauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la pili tayari tumeshaanza na kazi hiyo inafanyika, kuona namna ya kuunganisha mifuko inayotoa fedha au inahudumia shughuli zinazofanana na taarifa hiyo tayari inakamilika iko kwenye hatua za mwisho kuona mifuko ipi itaunganishwa ili kupunguza wingi wa mifuko hii, ambayo inahudumia watu wanaofanana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante; swali langu ni je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya utekelezaji wa miradi ya maji kwenye Kata za Mwika Kaskazini, Mamba Kaskazini, Marangu Mashariki, Mwika Kusini na Kilemu kwa sababu miradi hiyo ina matatizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge, maeneo hayo yote uliyoyataja tuna miradi ambayo inaendelea na usanifu na miradi ambayo tunaitafutia fedha na katika mgao ujao na hata Jimbo la Vunjo nalo litakuja kupatiwa fedha ili miradi hii ianze kutekelezwa kwa wakati.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Swali langu, ni lini Serikali itatathimini upya uhitaji wa eneo la zaidi ya eka 35, 30 ili kujenga hospitali za wilaya. Ni sehemu zipi utapata eneo kubwa kiasi hicho, kwanini tusitafute namna ya kujenga hizi hospitali hata kuweka ghorofa moja moja badala ya kutafuta eneo kubwa kiasi hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI katika ujenzi wa hospitali za halmashauri yako ya aina mbili. Kuna maelekezo ambayo yanaendana na halmashauri za vijijini, ambako ardhi ni kubwa wanahitaji kutenga angalau ekari 30 na kuendelea kwa sababu hospitali zile tunazojenga tunatazama miaka 50 au mia moja ijayo, haituangalii miaka mitano au kumi ijayo. Kwa hiyo, tunahitaji kuwekeza katika maeneo makubwa ili hata baada ya miaka 100 miundombinu tu itabadilika lakini eneo litaweza kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ya mijini tunaweka eneo siyo kubwa sana, inategemeana na eneo, lakini tunapendekeza kujenga majengo ya kwenda juu kwa maana ya maghorofa. Kwa hiyo, maeneo yote mawili yametazamwa, maeneo ya mijini, tunakwenda kwa maghorofa, kama eneo halitoshi lakini maeneo ya vijijini tunataka angalau eka 30 kwa sababu tunaona miaka mingi ijayo.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri aliahidi kwamba ataingiza mchakato wa kuingiza LUKU za maji ili kudhibiti gharama zisizo sahihi zinazosomwa na wale wanaosoma. Je, huu mchakato umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kimei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, LUKU za maji tayari katika baadhi ya mikoa imeshaanza kutumika mita hizo ambazo zinatoa uwezekano wa kulipa kulingana na matumizi yako. Mchakato unaendelea kwa mikoa mingine, lakini tayari tuna pilot Mikoa kama Iringa, Mbeya inafanya vizuri kwa baadhi ya maeneo ambayo tayari imefungwa, hivyo tutasambaza maeneo yote ambayo zitaweza kufikia.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara ya Chekeleni – Kahe – TPC – na Mabogini iko kwenye Ilani awamu hii na awamu iliyopita na pia ni ahadi ya Viongozi Wakuu wa Serikali. Nataka kujua ni lini Serikali itaanza sasa kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa? Natumaini hatasema kwamba ni mpaka hela ipatikane.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema ni ahadi ya viongozi lakini pia iko kwenye ilani naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga barabara zote ambazo imeziaidi kuzijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na barabara ambayo Mheshimiwa Mbunge wa Vunjo ameitaja.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii, nina swali dogo gu. Kwa vile Serikali imetuhakikishia kwamba Mamlaka za Hifadhi za Misitu na Wanyamapori wana wajibu wa kutoa CSR kwa vijiji vinavyozunguka hifadhi hizi. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuziagiza mamlaka hizi ziweke bayana kiasi cha ufadhili ambazo zimetolewa kwa vijiji hivyo ndani ya miaka mitatu iliyopita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niwaombe sana wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi waamini kwamba Serikali inatambua umuhimu wa mashirikiano ikiwemo miradi ya ujirani mwema.

Mheshimiwa Spika, bajeti zote tunapozileta hapa Bungeni huwa tunaweka kipengele cha miradi ya CSR. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hata bajeti hii tutakayoisoma hivi karibuni itazingatia hilo. Hivyo, niwaombe wananchi wote na Waheshimiwa Wabunge ambao wanazungukwa na maeneo haya yaliyohifadhiwa watarajie kuona CSR katika maeneo yao. Ahsante sana.
MHE. DKT CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI alituahidi mwaka jana kwamba angetupatia kituo cha afya kwenye Kata ile ya Kirua Vunjo Kusini kwenye Kijiji cha Kohesa. Sijui mtaanza lini kujenga hospitali hiyo kwa sababu tulipata mbadala wa kupata Hospitali ya Wilaya.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ya Serikali itatekelezwa, ni suala la muda tu kwa hiyo Serikali inatafuta fedha ili kwenda kutekeleza ahadi hiyo kupeleka Kituo cha Afya katika Kata aliyoitaja, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba niulize Maswali mawili madogo tu: -

(i) Je, Serikali inaweza ikatudokeza kidogo kitu gani tutegemee kutokana na huo mwongozo?

(ii) Kwa vile Serikali imeweza kutoa ruzuku kwa maunganisho ya umeme, ni nini kinazuwia kutoa ruzuku kwa maunganisho ya maji ilhali tunajua maji ni uhai?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge.

Swali la kwanza, kwa nini tunashindwa kutumia ruzuku kwenye maunganisho ya maji; hili suala naomba nilichukue tuweze kulifanyia kazi. Vilevile swali lake la kwanza naomba niwe nimelipokea nitalifanyia kazi.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba niulize swali moja fupi. Kwa vile Kata ya Mamba Kaskazini na Mamba Kusini kuna shule nyingi za sekondari lakini hatuna shule hata moja ya kidato cha tano na sita.

Je, Serikali iko tayari kuipandisha hadhi Shule yaSekondari ya Mboni kwa kuijengea pia hosteli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye shule hizi ambazo amezitaja Mbunge za Mamba Kaskazini na Mamba Kusini, utaratibu ni ule ule kuweza kujenga miundombinu ambayo inatakiwa ili kupandisha hadhi shule halafu kuiombea usajili kutoka Wizara ya Elimu. Tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona shule hizi kama miundombinu inakidhi vigezo, na kama inakidhi vigezo basi tuone taratibu za kuombea usajili wa kuweza kupata mkondo wa kidato cha tano na sita.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali langu ni hili hili nalirudia kila wakati. Ile bypass road kutoka Chekereni kwenda Kahe – Mabogini na TPC wataifanya nini au wana mkakati gani kwa sababu hii iko kwenye Ilani na ahadi za viongozi wetu wakubwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika bypass road hii Serikali inaifanyia kazi kupitia Wakala wa Tanzania ambao ni TANROADS na tutakaa pamoja na wenzetu wa TANROAD kuona mipango yao ni ipi kuhakikisha barabara hii inatekelezwa kama Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ambavyo ilielekeza.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia utaratibu wa ubia na sekta binafsi katika kujenga mabweni kwenye Vyuo na hata kwenye Sekondari?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kimei ametoa wazo, naomba tulichukue ushauri wake tuende tukaufanyie kazi ili tuweze kuangalia ni nimna gani tunaweza tukajenga hosteli kwa njia ya PPP. Ninakushukuru.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Swali langu ni hili; je, Serikali inaweza ikatoa kauli gani kuhusu uwezekano wa kuingia ubia na taasisi za kidini ambazo zilijenga Vyuo vya Ufundi Stadi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nimtoe hofu Mheshimiwa Kimei, utaratibu huo upo. Naomba tu kwa vile ni suala mahususi, baada ya kikao chetu hiki au baada ya kipindi hiki cha maswali, tunaweza tukakutana ili tuweze kuangalia hilo eneo au hivyo vyuo ulivyovitaja namna gani tunaweza tukatengeneza huo ushirikiano wa kutoa mafunzo kwa pamoja baina ya wawekezaji pamoja na Serikali, nakushukuru sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni je, Serikali inatoa ushirikiano gani kwa vituo vya afya vinavyomilikiwa na sekta binafsi hususan Makanisa ili viweze kutoa huduma kwa wananchi wanaotegemea sana hivi vituo kwa bei nafuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na utaratibu wa Serikali kushirikiana na hivyo vituo kwa mikataba maalum. Kama Mheshimiwa Mbunge anakumbuka hata kwenye jimbo lake kuna kituo ambacho kuna ushirikiano kama huo, naomba kama kuna Kituo ambacho amekiona kinategemewa sana na wananchi na vituo vingine vipo mbali na anahitaji hilo, angeleta ili kupita kwenye mchakato ikionekana inafaa na ikikidhi vigezo, basi Serikali itatafakari la kufanya. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara ya Himo - Sokoni kwenda Lotima ina kilometa 7.5 na Mheshimiwa Waziri Mkuu aliagiza kwamba TARURA waweze kuijenga kwa kiwango cha lami na mmeanza mmejenga mita 800 tu.

Je, mnatoa kauli gani kuhusu kumalizia barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba ni kweli maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imekwishaanza kutekeleza kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema, tumeanza na mita 800 lakini tunafahamu barabara ile ina urefu wa kilometa 7.5 tutakwenda kwa awamu, safari ni hatua tumeanza, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kuweka kipaumbele kuhakikisha kilometa hizo 7.5 zinajengwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES. S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali imetoa majibu mazuri na nimeyafurahia sana, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Bodi ya Barabara ya Mkoa wetu wa Kilimanjaro imeshatuma maombi kwenye Wizara ya kuipandisha hadhi Barabara hii ya Chekereni – Kahe – Mabogini – TPC.

Je, tutapata uthibitisho gani kwamba maombi haya yameshughulikiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nashukuru sana Serikali imeweza kutengeneza Daraja la Marangu Mtoni; lakini tunaomba kauli ya Serikali kuhusiana na kukamilisha kipande kilichobaki cha barabara hiyo kuanzia Kawawa – Nduoni kuja Marangu Mtoni ambayo ipo pia kwenye Ilani ya CCM, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni juu ya Bodi ya Barabara kuipandisha hadhi Barabara ya Kahe – Chekereni. Suala hili ni la kisheria na taratibu za namna ambavyo barabara inatakiwa kupandishwa hadhi na kwenda kwa wenzetu wa Wizara ya Ujenzi zipo wazi. Hivyo basi, tutakaa na Mheshimiwa Kimei kuona ni hatua zipi ambazo maombi haya yamefikia ili kuona kama tayari yamefika kwa Waziri wa Ujenzi mwenye dhamana ya kupandisha hadhi barabara hii. Kama maombi haya hayajafika basi tutaona ni namna gani yanaweza kufika ili timu iweze kwenda kufanya assessment na barabara hii iweze kupandishwa hadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda kwenye swali lake la pili linalohuau Saraja la Marangu Mtoni, ambalo linaunganisha barabara ya Kawawa – Kahe – chekereni. Nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Vunjo, kwamba Serikali ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga zaidi ya shilingi milioni 989 kuhakikisha kwamba barabara katika jimbo la Mheshimiwa Kimei zinafanyiwa ukarabati ikiwemo Barabara hii ambayo inaitwa Fungate – Mabogini – Kahe – Chekereni ambapo kwa sasa kuna shilingi milioni 39. Inasubiri tu daraja lile likamailike ili barabara nayo iweze kuendelea kutengenezwa na iweze kupitika.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize swali la nyongeza fupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Vunjo kuna vituo vya afya vinne tu licha ya kwamba tuna kata 16. Na hivi vituo vya afya vikiwemo Unyika Msae, Marangu Head Quarter ambacho ni kipya, Kilua Vunjo na Kahe havina uwezo wa kutoa huduma ya upasuaji, hususan kwa wanawake ambao ni wajawazito na hivyo wanalazimika kupewa rufaa kwenda kwenye hospitali za Mawenzi ambapo ni mabli au KCMC ambapo pia kuna usumbufu mkubwa;

Je, ni lini Serikali itatoa vifaa na madaktari ili vituo hivi viweze kutoa huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Serikali ya Doctor Samia Suluhu Hassan ilipopeleka vituo vya afya kule kwa kweli lengo lake ni kufika mahali vile vile viweze kufanya upasuaji waweze kuwasaidia akina mama kule kule badala ya kuwapeleka mbali kama hospitali ya Mkoa anavyosema Mheshimiwa. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge kama suala ni ukosefu tutakuja kuangalia vituo vyako specifically kama theater ipo na vitu vingine vipo. Kama ni ukosefu wa vifaa tutashirikiana na wenzetu TAMISEMI tuone namna vitakavyoweza kupatikana ili huduma hiyo iweze kutolewa.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama navyofahamu wafugaji hawaishi mjini sasa vijiji vya Kisimani na Kilimani pale Himo viliingizwa kwenye Mji mdogo wa Himo na hivyo kukosa fursa ya kufurahia umeme wa REA. Je, mnatoa kauli gani kuhusu hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba azma na nia ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha kila Mtanzania popote alipo anapelekewa huduma ya umeme na tayari tumeshaanza kufikisha kwa kila kijiji. Lakini hatua kubwa inayofuata ni ya kupeleka kwenye vitongoji ambavyo hata juzi kwenye bajeti tumevisema na tunatarajia pesa kubwa tutaipata kwenye mwaka wa fedha ule mwingine unaofuata ili vitongoji vyote maana yake wananchi wote waweze kupata huduma ya umeme popote walipo.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri na yenye tija, naomba niulize maswali mawili madogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo la Vunjo kuna mabwawa mawili moja linaitwa Urenga katika Kata Kirua Vunjo Mashariki na nyingine ni Koresa Kata ya Kirua Vunjo Kusini yameharibika sana sasa hivi ni kama vile hayapo. Nataka nijue kama Waziri atakubali kutembelea eneo hili na kuyaona haya mabwawa ili aone kama watafanya nini kuyakarabati? (Makofi)

Swali la pili. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu ukamilishaji wa miradi iliyoanza mwaka juzi kule Mamba Kaskazini na Kusini, Mwika Kaskazini na Kusini na Marangu Mashariki na Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Charles Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kutembelea mabwawa ambayo kwa sasa hayafanyi vizuri. Mheshimiwa Mbunge, naomba nikuhaidi baada ya Bunge hili tutakwenda kuyatembelea na kuona nini kinaweza kufanyika kupitia watalaam wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kukamilisha miradi Mheshimiwa Mbunge pia hili tutakapokuwa tunatembelea tutaona kwa nini miradi hii haijamilika kwa wakati? Nakuhakikishia tutahakikisha inakamilika ili wananchi waweze kupata huduma. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ni lini mtapandisha hadhi barabara ya Uchira – Kisomachi - Kolarie?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge, kuhusu kupandisha hadhi hizi Barabara, kuna taratibu zake, ambapo kama Mheshimiwa Mbunge pamoja na vikao vya kuanzia wilaya, mkoa wataleta maombi, Wizara ya Ujenzi ambayo watakwenda kufanya tathmini na baada ya hapo kama itakidhi vigezo, maana yake ni kwamba hiyo barabara itakuwa imepandishwa hadhi. Pia kama itakuwa barabara hiyo haikupandishwa hadhi, wanaweza kuomba kukasimiwa kukarabatiwa ama kusimamiwa na TANROADS, ahsante.
MHE. DKT, CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, je, Serikali itakuwa tayari kuweka wazi mkeka wa mgawanyo wa minara 758 na hiyo mingine 600 tuliyoahidiwa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko tayari.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, SIDO imepotelea wapi kwa sababu kwenye Jimbo letu sijawahi kusikia SIDO, iko wapi?
NAIBU WAZIRI UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba nijibu swali la Dkt. Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, SIDO bado ipo na inaendelea kufanya shughuli zake, changamoto tuliyonayo ni mtaji mdogo wa kuweza kutoa huduma kama ilivyokusudiwa na shirika letu la kuendeleza viwanda vidogo na biashara ndogo Tanzania. Sasa tutakuja na sheria mahususi ili tuone namna gani ya kuiwezesha SIDO iweze kufanya shughuli zake kibiashara badala ya kutoa huduma ambayo inahitaji mtaji zaidi wa Serikali. Kwa hiyo tunadhani huu utakuwa ndio ufumbuzi ili waweze kuendesha shughuli zao kibiashara ili kuwafikia wajasiriamali wengi na wenye viwanda wengi zaidi kadri ambavyo uchumi wa sasa unataka.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili licha ya majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inaweza ikanihakikishia kwamba wananchi wa Uchira, ambao nao walipisha ujenzi wa upanuzi wa barabara hii inayotoka Arusha – Moshi kwenda Holili, je, nao watalipwa chini ya mchakato huu ulioanza?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, lini sasa barabara hii itaendelezwa toka pale ilipoishia Tengeru, eneo la Arusha kuja Moshi, Himo mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba Mheshimiwa Dkt. Kimei kwa kweli suala la malipo ya fidia kwa hawa wananchi limekuwa ni suala ambalo kila tunapokutana na kuja ofiini analifwatilia, lakini tumelitolea majawabu na kwamba sasa tunakamilisha.

Mheshimiwa Spika, swali lake kuhusu wananchi ambao pia watapisha ujenzi, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa tulifanya tathmini siku za nyuma, tutarudia ku-review zile tathmini ili ziendane na muda wa sasa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Tengeru kuja huku Holili; JICA walishakubali, tumelijibu mara kadhaa, tutajenga hiyo barabara kwa kusaidiana na wenzetu wa Japan, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa vile ujenzi wa barabara ya Chekereni – Kahe - Mabogiri kwa kiwango cha lami ipo kwenye Ilani ya CCM na pia ni ahadi ya viongozi wakubwa wa kitaifa. Je, ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoainisha iPo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika kipindi hiki kuna hatua ambazo tutaanza kuzitekeleza kama tulivyoainisha kwenye Ilani lakini itategemea sana na kadri ya fedha itakavyopatikana. Ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Swali langu ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga barabara kutoka Mji Mdogo wa Himo kupitia Sokoni kwenda Lotimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Mji Mdogo wa Himo ambayo inakwenda kuunganisha na miji mingine ni barabara muhimu na ni barabara ambayo tulishaelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Kilimanjaro na Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Moshi kuhakikisha kwamba wanazifanyia tathmini na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi ili Serikali itafute fedha kujenga barabara hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuwahakikishie kwamba tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya barabara hizo, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo vyetu vya afya kwenye Jimbo letu la Vunjo kuna uhaba mkubwa wa wahudumu lakini pia kuna wahudumu ambao wanataka kujitolea ili wasaidie na wenyewe wamesomea mambo hayo hayo ya ukunga nakadhalika na unesi lakini hawana kazi. Je, Wizara haioni umuhimu wa kuweka utaratibu wa kuwaruhusu hawa ambao wanataka wajitolee kusaidia kutoa huduma bure hata kama watalipwa kidogo na wananchi ili waweze kuchukuliwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza anachokisema Kimei ni kweli kipo na nimetembelea jimbo lake tumeliona hilo na ameshakieleza mara nyingi lakini sasa Mheshimiwa Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu alishaelekeza na tayari utaratibu, muongozo wa ajira ya kujitolea umeshatengenezwa kwa level ya Hospitali za Mikoa na kwenda juu. Sasa tunashirikiana na amesema atashirikiana na Mheshimiwa Bashungwa ili kutengeneza na utaratibu kwa kushuka chini tuone tunafanyaje hilo liweze kutekelezeka kwa urahisi lakini ni jambo jema sana kwasababu hata kwenye shule zetu tumeona kwamba kuna walimu wengi wanajitolea na wanasaidia sana watoto nayo kwenye afya tungetamani tuwe na jambo kama hilo lakini tulitafakari kwa kina kabla ya kutekeleza.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Swali langu nilikaa nikafikiri kwamba ultrasound machine pamoja na x-rays ni muhimu sana kwenye suala zima la Watoto Njiti. Kwa hiyo nilitaka nimuulize Waziri kwamba ni lini watepeleka ultrasound machine na x-ray katika kituo cha Afya Himo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, labda nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mimi na yeye nikimaliza haya maswali kama kituo chake hakina ultrasound tukae chini ili tuweze kuelekeza MSD wapeleke mara moja ultrasound kwenye eneo lake. Pia suala la x-ray kuna fedha zile ambazo Waziri wa Afya amesema zimeokolewa tumefanikiwa vilevile kupata x-ray 33 za ziada, kwa hiyo katika hiyo ziada tutaona tunaelekeza maeneo gani baada ya watalaam kuchakata na kuona vipaumbele.(Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Je, Mheshimiwa Waziri atakubali kuongozana nami kutembelea eneo hili ili aone umuhimu wake na fursa zilizopo kwa kuongeza ajira na biashara kwenye ukanda huu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki?

Mheshimiwa Spika, la pili; kwa vile Serikali imeanza sasa kuboresha mazingira ya machinga huku mjini kwa kuwajengea maeneo mazuri na kuwawekea mapaa kwenye biashara zao.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwezesha wanawake, akinamama, mabinti zetu kule kwenye vijiji ambao wanaenda kwenye magulio kama yale ya Mwika, Kisambo, Marangu, Lyamombi, Kinyange wakinyeshewa mvua mazao yao yakiharibiwa kwakati mvua zinaponyesha ni pamoja na kupigwa na jua kali. Je, Serikali haioni haina mkakati wa kuwajengea mapaa angalau kwenye maeneo machache kwenye masoko haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Charles Kimei, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Dkt. Kimei kwa ufuatiliaji kwa ajili ya maendeleo ya Jimbo la Vunjo amekuwa akifuatilia sana kuhusiana na ujenzi wa masoko.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu kuongozana nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge hili tutapanga na tutaongozana ili tuweze kutembelea maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuhamasisha maendeleo katika Jimbo lake.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ni kweli Serikali inapambana kuhakikisha tunaweka miundombinu wezeshi ikiwemo masoko, maeneo ya kuuzia bidhaa mbalimbali hasa kwa wanawake, vijana na wamachinga na hii Serikali imeshaanza kupitia TAMISEMI kujenga mabanda na kuezeka maeneo mbalimbali ambayo yanatumika kama masoko ili kuhifadhi bidhaa wakati wa mvua na jua ili wakinamama wafanyabiashara waweze kufanyakazi. Naomba halmashauri waweze kufanya hivyo ili kuhakikisha bidhaa hizo zinatunzwa na kuuzwa katika mazingira mazuri, nakushukuru.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali, je ni lini Serikali itaanza ukarabati wa Kituo cha Afya cha Mwika, kwa kuongeza jingo la wodi ya watoto pamoja na jengo la upasuaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Kimei, amefuatilia sana suala la ukarabati wa Kituo cha Afya cha Mwika, na sisi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, tulishamhakikishia kwamba tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga wodi ya watoto, wodi ya upasuaji lakini pamoja na ukarabati wa kituo kile na tutafanya hivyo.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Swali langu ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga barabara kutoka Mji Mdogo wa Himo kupitia Sokoni kwenda Lotimu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Mji Mdogo wa Himo ambayo inakwenda kuunganisha na miji mingine ni barabara muhimu na ni barabara ambayo tulishaelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Kilimanjaro na Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Moshi kuhakikisha kwamba wanazifanyia tathmini na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi ili Serikali itafute fedha kujenga barabara hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuwahakikishie kwamba tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya barabara hizo, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Chuo cha Ufundi Stadi cha Mangaria kilicho kwenye Kata ya Mamba Kaskazini na kukipa vifaa vya kufundishia?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokwishaeleza awali kwamba Serikali bado tunaendelea na mchakato wa utafutaji wa fedha; kwanza tuweze kufanya ujenzi kwenye wilaya ambazo hazina hivi vyuo. Hata hivyo, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Dkt. Kimei, kwa vile ametaja suala la ukarabati katika Chuo hicho cha Mamba, nitamwomba tu baada ya kikao hiki cha leo tuweze kuonana baadaye ili kwanza tuweze kutuma timu yetu ya wataalam kwenda kule Mamba, iende ikafanye tathmini ya kina, tuweze kujua gharama za ukarabati ukaohitajika pale ni kiasi gani ili tuweze kuingiza kwenye mipango yetu na tukipata tuweze kukipa kipaumbele cha ukarabati chuo hiki. Nakushukuru sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Swali langu nilikaa nikafikiri kwamba ultrasound machine pamoja na x-rays ni muhimu sana kwenye suala zima la Watoto Njiti. Kwa hiyo nilitaka nimuulize Waziri kwamba ni lini watepeleka ultrasound machine na x-ray katika kituo cha Afya Himo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, labda nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mimi na yeye nikimaliza haya maswali kama kituo chake hakina ultrasound tukae chini ili tuweze kuelekeza MSD wapeleke mara moja ultrasound kwenye eneo lake. Pia suala la x-ray kuna fedha zile ambazo Waziri wa Afya amesema zimeokolewa tumefanikiwa vilevile kupata x-ray 33 za ziada, kwa hiyo katika hiyo ziada tutaona tunaelekeza maeneo gani baada ya watalaam kuchakata na kuona vipaumbele.(Makofi)

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri: Ni lini atawezesha wananchi wa Mwika Kaskazini kwa kumalizia kituo chao ambacho alikitembelea na akaahidi kwamba tukimaliza kupaua, basi tutapata uwezeshaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya kauli ile kama unavyokumbuka tulikuwa wote Mheshimiwa Dkt. Kimei, tukasema IGP na imewekwa kwenye mpango wa ukamilishaji katika mwaka wa fedha unaoanza 2024/2025. Hiyo ni commitment, tutalitekeleza Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Skimu za mifereji ni skimu ambazo zilikuwepo na kule kwetu Vunjo zimekuwa zinaweza zikaleta matokeo chanya kwenye kuongeza tija kwenye kilimo. Kwa kuwa Tume ya Umwagiliaji imeshafika kutafiti na kuziangalia skimu hizi, je, Waziri anaweza akanihakikishia kwamba wataenda haraka na kuanza kukarabati mifereji ile?

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Vunjo Dkt. Charles Kimei kwamba hiyo kazi tutaifanya kwa haraka iwezekanavyo kwa sababu tumepewa rasilimali zote kutekeleza jambo hili; kwa hiyo, liko ndani ya uwezo wetu. Ahsante sana.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, naomba niulize swali moja la nyongeza, ila niruhusu nijieleze kidogo.

Mheshimiwa Spika, wakati kunatokea moto kwenye mlima watu wanaokimbizana kuuzima ni wale wanaoishi kandokando ya ule mlima; pale Marangu wanabebwa, wanasombwa, wanalazimishwa kwenda kuzima moto. Sasa tulikuwa tunaomba Serikali itoe kauli kuhusiana na uwezekano wa kutoa mwongozo ili wale tour operators wawe na uwiano fulani tuseme asilimia 70 ya wahudumu wanaopandisha watalii wawe wanatoka kwenye eneo lile la pale Marangu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, tumepokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tunaenda kuufanyia kazi tuone ushauri wa kitaalam utatuelekeza vipi. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kuhusu Nusu Maili; Nusu Maili ambayo ni eneo la Nusu Maili kuanzia vijiji kwenda kwenye hifadhi inayozunguka Mlima Kilimanjaro liliwekwa mwaka 1923 na Serikali za wakoloni.

Naomba nijue kwamba hii Kamati ya Mawaziri Nane imefikia muafaka gani kuhusu hilo eneo kwa sababu kuna mkanganyiko mkubwa sana kuhusiana na maagizo ya Waziri aliyekuwepo Mheshimiwa Jumanne Maghembe na hali ilivyo sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo ambayo tunatamani sana wananchi wafahamu kwamba ni maeneo ya muhimu. Eneo hili la Nusu Maili ni eneo ambalo tumeukinga Mlima Kilimanjaro ili barafu yake isiendelee kuyeyuka. Tumeendelea kuwaelimisha wananchi namna ambayo tunaweza tukafanya kama ni mbadala, badala ya kuendelea kuomba Nusu Maili, sisi tumejipanga kugawa miche kwa ajili ya wananchi wapande miti ili iweze kuwasaidia baadae kuwa na mavuno ya zao la miti ikiwemo kupata mkaa na matumizi ya nishati mbadala.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kuwaomba wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro. Mlima Kilimanjaro tunapata faida kubwa sana ikiwemo kupata watalii na hata wenyeji walioko katika maeneo hayo wanafaidika ikiwemo sisi kupeleka CSR kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, hii Half Mile ambayo tumeendelea kuiomba tuwaombe kwamba Mlima Kilimanjaro unahitaji kuhifadhiwa vizuri kwa ajili ya kizazi hiki na vizazi vinavyokuja. Kwa hiyo, niwaombe wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro tuendelee kushirikiana na Serikali kuutunza mlima huu.