Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Joseph Anania Tadayo (3 total)

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa Serikali imetumia nguvu nyingi sana katika kupambana na uvuvi haramu na kulinda hifadhi zetu na kama sehemu ya mafanikio ya juhudi hizi idadi ya wanyamapori imeongezeka na katika maeneo mengine wanyamapori hawa wamesambaa na kuingia katika makazi ya watu na hivyo kuathiri sana maisha ya watu na shughuli za uzalishaji. Kwa kuwa tatizo hili sasa limeonekana kuwa la kudumu, Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya suluhisho la kudumu la tatizo hili? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali hili linafanana sana na swali ambalo mwanzo nimetoa ufafanuzi wake kwamba yako maeneo yana migogoro kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi. Swali la awali lilikuwa linazungumzia ule mgongano wao na hili linzungumzia wanyamapori walioko.

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo haya tuliyoyahifadhi yana hawa wanyamapori na maeneo haya ya wanyamapori pia tumeendelea kuwahifadhi na kutoa tahadhari kwa wananchi walioko jirani na maeneo haya. Mkakati wa kuzuia wanyamapori hawa kuja kwenye makazi ya wananchi upo na unaendelea pale ambapo kwanza tumetoa elimu kwa wananchi wanaokaa karibu na maeneo haya ya wanyamapori kuwa na tahadhari. Wanapofanya shughuli zao wasiingie kwenye eneo la wanyamapori, pia tumewawekea buffer ya mita kama 500 ambazo wao wananchi walioko huko hata wanapoingia eneo hili lazima wawe na tahadhari ya kutosha. Tunaamini wanyama walioko kwenye lile pori wanaweza kuja mpaka kwenye mpaka wa kijitanua kidogo wanaingia kwenye hili eneo la mita hizi 500, wanaweza wakazunguka hapo na kurudi. Inapotokea wakija huku sasa Idara ya Maliasili kupitia kikosi chao cha wanyamapori tumekiweka maeneo yale ambayo wanyamapori huwa wana tabia ya kutoka na kurudi huku kwa ajili ya kuwazuia kurudi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, jambo hili tunalifanya kwa kushirikisha pia vijiji vyenyewe, tunawapa elimu tunaanzisha ulinzi wa kijiji ambako pia ikitokea hilo nao wanasaidia kuwarudisha. Bado tunao wanyama wanatoka wanakuja lakini bado tumeendelea kuimarisha vikosi vyetu kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yana wanyamapori wanaotoka sana kuweka kambi dogo la kuhakikisha kwamba wanarudishwa kwenye maeneo hayo na makambi hayo tumeamua tuyaweke katika maeneo yote ambayo tunaona wanyama kama tembo ambao wameongezeka sana kwa sasa waweze kudhibitiwa.

Mheshimiwa Spika, nimeliona hili pia nilipokuwa nafanya ziara wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, nimeona pia nikiwa Bariadi Mkoani Simiyu, nimeenda pia hata Tarime na maeneo mengine ambayo nimepita, nimepata malalamiko haya na tumeshawasiliana na Wizara ya Maliasili kujiandaa vizuri kwenye maeneo haya. Kwa hiyo, tumeshaanza kusambaza vikosi vyetu, kulinda maeneo hayo ili pia wananchi wasiweze kusumbuliwa.

Mheshimiwa Spika, wito kwa wananchi walioko kwenye vijiji ambavyo viko karibu na maeneo ya hifadhi, wasiingie sana kwenye mapito ya mara kwa mara ya wanyama. Tunao wanyama kama tembo ambao wao wana mapito yao miaka yote. Kwa hiyo, maeneo hayo kwa sababu tunaishi kwenye vijiji hivyo, tunayafahamu. Ni muhimu kuwa na tahadhari kwenye maeneo haya ya mapito ili tusije tukawa tunaingiliana na hawa wanyama, lakini bado mkakati wetu ni ule ule. Kwa hiyo, tushirikiane pamoja kuhakikisha kwamba tunawahifadhi wanyama wetu na madhara ambayo yanajitokeza pia tunaendelea kuyadhibiti ili yasiweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati wa kudhibiti hatari hii unaendelea chini ya maliasili kwa kuweka makamanda kwenye maeneo hayo na kila wilaya iliyoko kwenye mpaka tuna kitengo hicho ambacho pia kinafanya kazi hiyo kubaini kwenye mipaka yake kwamba wakati wote tunakuwa salama. Lengo ni kuwalinda wananchi wanaoendelea na shughuli zao, lakini pia kuwalinda wanyamapori ambao pia na wao watatupatia tija kwa shughuli za kitalii na uhifadhi wa wanyama wetu kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni Serikali yetu imeonesha uwezo mkubwa sana wa kushughulika na masuala na miradi mikubwa katika hali ya dharura na kwa mafanikio makubwa sana. Mfano mojawapo ikiwa ni miradi mbalimbali iliyoendeshwa kwa hizi fedha za UVIKO na hata linaloendelea sasa hivi la kudhibiti madhara ya bei za mafuta kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu lipo tatizo la muda mrefu la uchakavu wa Shule za Msingi ambazo nyingine zilijengwa wakati wa ukoloni nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba je, Serikali haioni kwamba kwa uwezo huu ulionao kwamba sasa ichukulie suala la uchakavu wa hizi shule za msingi kwamba ni jambo la dharura ili shule hizi zikarabatiwe na elimu yetu iendelee kuwa bora.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tadayo Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna shule za muda mrefu sana na wala siyo shule za msingi tu, ziko shule za sekondari, vyuo vya elimu ya kati hata vyuo vikuu. Nakiri kwamba tunahitaji mkakati wa Serikali wa dharura lakini utaratibu wa kukarabati shule hizi kongwe tayari ulishaanza kwa kupeleka fedha kwenye shule zetu ili kukarabati miundombinu yake irudi katika hali inayoweza kutumika kisasa zaidi. Tulianza zoezi hilo mwaka 2013 kwa kupeleka milioni 50, kila shule ili kukarabati na kuongeza fedha, tukaongeza uwezo zaidi wa Serikalini, tumeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ukarabati shule za msingi kongwe, sekondari kongwe, FDC kongwe lakini pia hata VETA ambazo zilianza kujengwa muda mrefu na vyuo vikuu vyote vilivyo vikongwe nchini.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili ni endelevu ndani ya Serikali ya Serikali. Kwa hiyo, udharura ni pale ambapo labda kutatokea madhara makubwa moja kati ya miundombinu hiyo tunaweza tukapeleka fedha, lakini kila mwaka tunatenga fedha. Hata Wizara ya Elimu jana wameshatoa bajeti zao moja kati ya fedha ambayo jana tumeitisha hapa ni ya kukarabati shule zote kongwe na taasisi zote za elimu ili miundombinu hii iweze kutumika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Waheshimiwa Wabunge wote ambao pia kwenye majimbo yenu kuna hizo shule hizo kongwe na Watanzania naona pia kuna vijana wetu wa shule, shule zotte na taasisi zote zitakarabatiwa. Waheshimiwa Wabunge mmeshapitisha bajeti zetu hapa na naomba muendelee kupitisha bajeti za Wizara zote ili Serikali ifanye kazi yake ikiwemo na ukarabati wa shule hizo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi hii ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nchi yetu kupitia Bunge hili ilitunga sheria nyingi nzuri za kulinda uhifadhi hapa nchini na hasa kuzuia uwindaji haramu kwa ajili ya kukuza utalii, kulinda ikolojia na pia kuongeza Pato la Taifa kupitia mapato yanayotokana na utalii. Hivi karibuni Mheshimiwa Waziri Mkuu, wanyamapori hawa ambao tumewahifadhi kwa mujibu wa sheria zetu na pia kwa kuheshimu mikataba ya Kimataifa katika eneo hili wamegeuka kuwa janga kwa kuharibu mali za watu, kuvuruga miundombinu na hata kusababisha watu wengi kupoteza maisha.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba tunapitia upya sheria hizi ambazo tuliziweka kwa ajili ya kulinda uhifadhi ili pia ziwalinde wananchi wetu na hata ikibidi kujitoa kwenye baadhi ya mikataba ya Kimataifa ambayo inatushurutisha kuweka sheria za namna hii ambazo zinawadhuru wananchi wetu na mali zao? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kupitia vikao vyetu vya Bunge hapa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakieleza usumbufu ambao wananchi kwenye maeneo yetu wanaupata kwa wanyama waliohifadhiwa kwenye maeneo mbalimbali kwenye misitu yetu kuhamia kwenye makazi ya watu na kusababisha uharibifu wa mali, lakini pia hata maisha ya watu, na tumepata taarifa hizi mara nyingi kwenye miji iliyoko kando kando na hifadhi zetu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunazo sheria zinazosimamia utekelezaji huu wa kuhakikisha kwamba wanyama wanabaki porini na wananchi wanaendesha maisha yao kwenye maeneo yao rasmi. Pia kumekuwa na wimbi kubwa la ongezeko kubwa la wanyama kwenye misitu yetu na hii ilitokana na jitihada tulizozifanya kupitia sheria zetu hizo hizo za kulinda uwindaji haramu, hili ndiyo limepelekea kuwa na idadi kubwa ya Wanyama.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Wizara ya Maliasili imekuwa ikifanya taratibu kadhaa kukutana na vikao na Wizara ambata zinazohusika kwenye uhifadhi wa mazingira yetu, wa misitu yetu, wanyama wetu na kuona kuwa wanyama wanabaki huko, jitihada kadhaa ambazo zimechukuliwa ni pamoja na kuongeza idadi ya Maaskari ambao pia wameweka vituo kando kando ya maeneo haya ili kuzuia wanyama kuingia, lakini pia tumeona jitihada za kutumia hata ndege kufukuza wanyama kuingiza porini.

Mheshimiwa Spika, tunajua ziko sheria zinalinda haya na Mheshimiwa Mbunge ametaka tubadilishe sheria, lakini muhimu sasa ni Wizara kuhakikisha kuwa maeneo yote yaliyohifadhiwa kwa ajili ya kuweka wanyama yanaendelea kusimamiwa na sheria zake, lakini na taratibu hizo ambazo wamezipanga kwa ajili ya kudhibiti wanyama hawa kuingia kwenye makazi. Hii ni pamoja na kulinda ile buffer ambayo tuliitenga kilometa tano kutoka makazi kuingia kwenye msitu na baadaye tukaruhusu wananchi wafanye shughuli zao za uzalishaji mali, shughuli za maendeleo kwenye hifadhi ile ya kilometa tano, lakini sasa inaonekana pia wanyama wanavuka hifadhi hiyo na kuingia kwenye makazi ya watu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ziko jitihada zimechukuliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii na wameunda timu ya kufanya ukaguzi wa maeneo haya na kubaini tatizo exactly ni nini hasa kinapelekea wanyama kutoka kule kuingia huku, baada ya kamati ile kukamilisha kazi yao tutapata majibu. Kwa hiyo, niwaahidi kwamba hili ilimradi Wizara imeshaanza kuunda timu ya kwenda kukagua na kugundua tatizo ni nini, baada ya kubaini tatizo, kama tatizo hilo pia litagusa kwenye sheria basi Wizara itatuongoza katika kuleta sheria hapa tufanye mabadiliko ili tuweze kuhifadhi, lakini pia tuhakikishe kwamba wananchi wanaendesha shughuli zao na maisha yao yanaendelea kuimarishwa na kulindwa kama ambavyo tuliweka sheria hizi awali na hatukuwa na tatizo hili hapo mwanzo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilitaka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa ushauri wake kwa Serikali sisi tunauchukua, lakini kwa kuwa timu ilishaanza kazi, tuipe muda timu yetu ikamilishe kazi, halafu ije na mkakati ambao imeuweka na tutaona mkakati huo na jinsi ambavyo utaweza kulinda maisha ya watu, utaweza kulinda pia na hawa wanyamapori wakiwa kwenye maeneo yao. Hii ndiyo njia sahihi ambayo itatusaidia katika kuzuia madhara yaliyojitokeza kwenye makazi ya watu hasa yale makazi yaliyopo karibu na sehemu za hifadhi. Ahsante sana. (Makofi)