MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: -
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Chuo cha VETA katika Wilaya ya Manyoni?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Jimbo Manyoni Mashariki kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inayo azma ya kujenga Chuo cha Ufundi Stadi katika kila Mkoa na Wilaya nchini. Katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mia moja kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi katika Wilaya 62 kwa Wilaya ambazo zilikuwa hazijajengewa Vyuo vya Ufundi Stadi. Aidha, Wilaya ya Manyoni ni miongoni mwa Wilaya hizo 62 ambazo zipo kwenye mpango wa kujengewa Vyuo vya Ufundi Stadi kwa mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa ambapo Serikali inaendelea na hatua hizi, nashauri wananchi wa Wilaya ya Manyoni wakiwemo wa Jimbo la Manyoni Mashariki waendelee kutumia Chuo cha Ufundi Stadi cha Mkoa wa Singida, na Chuo cha Wilaya ya Ikungi, Pamoja na Vyuo vya Singida vya FDC na vyuo vingine vya ufundi stadi vilivyopo hapa nchini. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -
Je, ni lini Serikali itafufua Shule za Msingi za Ufundi Wilayani Hai na kurejesha mfumo wa wanafunzi kufanya mitihani na kupewa vyeti?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elinikyo Mafuwe Saashisha, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali iko katika mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na uboreshaji wa Mitaala ya Elimu ili iweze kuwajengea wanafunzi stadi na ujuzi mbalimbali ikiwemo ufundi utakaowawezesha kuhitimu na kuhimili ushindani katika soko la ajira ndani na nje ya nchi. Mara baada ya mitaala tajwa kukamilika ikiwa ni pamoja na manunuzi ya vifaa na mashine mbalimbali za ufundi, Elimu ya Ufundi itatolewa katika Shule za Msingi na Sekondari. Aidha, utaratibu wa kufanya mitihani ya Elimu ya Ufundi na kupata vyeti utaandaliwa kwa kushirikiana na mamlaka husika kama vile Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET).
Mheshimiwa Spika, pamoja na mapitio ya Sera na Mitaala, Serikali inaendelea kufanya maboresho makubwa katika Chuo cha Ualimu Kleruu pamoja na Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Morogoro (MVTCC) kwa kufanya ukarabati wa miundombinu ikiwemo ujenzi wa mabweni ya wanafunzi kwa lengo la kuongeza fursa ya mafunzo kwa Walimu wa masomo ya Ufundi.
Mheshimiwa Spika, pia Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Mbeya kimeanza maandalizi ya utoaji wa mafunzo hayo katika ngazi ya Stashahada katika Elimu ya Ufundi, (Diploma in Technical Education na Postgraduate Diploma in Technical Education). Kwa sasa mitaala ya masomo hayo inafanyiwa kazi na Tume ya Vyuo Vikuu ili kuidhinishwa na kuanza kutumika katika Chuo hicho. Ahsante sana.