Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Prof. Adolf Faustine Mkenda (12 total)

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii. Nitangulie kusema kwamba naunga mkono hoja na kwa vile ni mara yangu ya kwanza kabisa kuzungumza kwenye Bunge lako Tukufu, naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa Chama Cha Mapinduzi na wapiga kura wa Jimbo la Rombo wa kuniwezesha kuwa Mbunge kwenye Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameniamini kwa kunifanya kuwa Waziri wa Kilimo. Shukrani pekee ninazoweza kumpelekea ni kwamba, nitafanya kazi wa bidii, maarifa na juhudi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu imepitia kwenye simanzi kubwa sana kwa kuondokewa na Mheshimiwa aliyekuwa Rais wetu, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, lakini tunamshukuru Mungu, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametusimamia vizuri, tumeendelea na msiba vizuri ametufariji na kuleta matumaini makubwa sana kwenye nchi yetu. Tunamshukuru sana, tuendelee kumuunga mkono.

Mheshimiwa Spika, kilimo kimezungumzwa sana katika mjadala wa Waheshimiwa Wabunge na masuala yaliyozungumzwa ambayo sitaweza kuyazungumzia yote, mengi tutayaona kwenye majibu ya bajeti yetu, ni umwagiliaji, zaidi ya Waheshimwa Wabunge 10; suala la mafuta ya kula, zaidi ya Waheshimiwa Wabunge saba; pembejeo za kilimo, Waheshimiwa Wabunge 12; huduma za ugani, Waheshimiwa Wabunge watano; utafiti, Waheshimiwa Wabunge wanne; masoko, Waheshimiwa Wabunge watano; sera kwa ujumla, Waheshimiwa Wabunge tisa, mazao na ushirika Waheshimiwa Wabunge 10.

Mheshimiwa Spika, ukijaribu kuangalia, sehemu kubwa wa yale yaliyozungumzwa ukiyatafrisiri yanazungumza kwenye umuhimu wa kuongeza tija kwenye kilimo. Yaani kuongeza kiasi cha mazao ambacho tunaweza kukipata kwa heka moja au kile ambacho tunaweza kukipata kwa juhudi ambazo tunazitoa. Kwa kweli hiyo inaendana sana na maudhui ya Mpango huu wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao moja ya term, flagship statement yake ni kujenga uchumi shindani. Hatuwezi kushindana kwenye mazao endapo gharama ya uzalishaji itakuwa kubwa sana, lakini kwa heka moja tunazalisha kidogo

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwenye mafuta ya kula kwa mfano changamoto yake, ni kwamba sisi gharama ya kuzalisha mazao yanayoweza kutuletea mafuta ni kubwa sana. Mchikichi kwa mfano, kwenye hekta moja sisi tunaweza tukapata mafuta tani 1.6, lakini wenzetu tunakochukua mafuta sasa hivi hayo Mawese Malaysia, Indonesia na kadhalika, wanapata tani 10 kwa hekta na hili ni suala la tija.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake ukiangalia kwa sababu siwezi kuingia kwa detail sana, ukiangalia pato la Taifa letu lote, utaona kwamba kilimo kinachangia takribani theluthi moja tu ya pato la Taifa, lakini nguvu kazi inayoenda kwenye kilimo ni zaidi ya theluthi mbili ya nguvu kazi yote hapa nchini. Maana yake ni kwamba, juhudi zinazozafanywa na mkulima, zinaleta kipato kidogo sana katika nchi yetu tija ipo chini sana na hatuwezi kuingia kwenye ushindani bila kutatua tatizo hili. Kwa hiyo, changamoto kubwa kabisa ya kilimo ni kuhakikisha kwamba gharama ya uzalishaji zinashuka, maana yake ni kwamba na bei ya mazao ishuke, lakini kipato cha mkulima kiongezeke. Hiyo inawezekana tu endapo tunaweza kuzalisha zaidi kwa hekta moja na gharama zikishuka zitatusaidia kujenga viwanda na kuleta ushindani kwenye uzalishaji wa mafuta ya kula na kwenye kuuza kwa nchi za jirani ambazo tunashughulika nazo.

Mheshimiwa Spika, sisi tunachukua maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wameyatoa hapa ambayo ni mengi sana na tumeya-summarize. Mengine mazuri sana, tutayafanyia kazi, lakini niwape matumaini Waheshimiwa Wabunge baadhi ya vitu ambavyo tayari viko kwenye mchakato na tunaomba tutakapokuja hapa na hotuba ya bajeti na maombi ya fedha mtupitishie kwanza.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia suala la utafiti. Tunaongeza fedha kwenye utafiti wa kilimo, kwa sababu bila utafiti hatuwezi kupata mbegu bora na hatuwezi kuwa na kilimo bora katika mazingira yetu. Kwa hilo moja tunaongeza na wataona na tunafanya hivyo kwa kuanzisha Mfuko wa Utafiti ambao tutaulezea hapa na vile ambavyo tutafanya.

Mheshimiwa Spika, katika utafiti tutalenga sana vitu viwili; kwanza mbegu, kupata mbegu bora zinazokidhi mahitaji ya nchi yetu; na pili kilimo bora katika mazingira yetu. Katika suala la mbegu, tutajitahidi sasa kuzalisha mbegu nyingi kwa sababu kilio cha mbegu hata humu ndani ya Bunge lako Tukufu tumekisikia sana. Tunafanyaje? Mashamba yote ya ASA yaliyopo hapa tunayatengea fedha kwa ajili ya kufanya kilimo cha mbegu cha umwagiliaji ili tuhakikishe kwamba tutakuwa tunazalisha mbegu sio kwa kutegemea msimu wa kilimo, kwamba tunaendana na wakulima tunazalisha mbegu wakati tunazalisha chakula halafu zile mbegu tunasubiri mpaka mwaka ujao, lakini tuweze kuzalisha mbegu kwa mwaka mzima na kuzalisha mbegu za kutosha na hizo mbegu ziwe ni matokeo ya utafiti ambao utakuwa unafanywa na taasisi yetu ya utafiti kwa fedha ambazo tutaziongeza kama Waheshimiwa Wabunge watakavyosikia katika bajeti. Hilo tutalifanya pamoja na mambo mengine ya pembejeo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine hata tukifanya utafiti, hasa upande wa agronomy, kilimo bora tunahitaji kufikisha matokeo ya utafiti kwa mkulima. Kama Waheshimiwa Wabunge wengi walivyozungumza ni muhimu sana kuimarisha shughuli za ugani hapa nchini, tuna kazi kubwa sana, kwa sababu namna fulani tumerudi nyuma katika eneo hilo. Maafisa Ugani wengi hawana usafiri, wanahitaji kutoa huduma kwa wakulima na namna ya kufuatilia utendaji wao haujawa mzuri sana, kwa hiyo tunafanya nini? Kwanza, tutanunua, tutakapoomba fedha hapa tunaomba mtukubalie, pikipiki 1500 kwa kuanzia, kwa ajili ya kuwagawia Maafisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatenga mikoa mitatu ya kielelezo ya namna ya kufanya huduma za ugani kwa namna ambayo inaleta tija. Mikoa hiyo tunahitaja wakati tutakapo wasilisha hapo Bungeni. Tunaongeza juhudi za ufuatiliaji, kwa sasa hivi tuna kitu tayari kinachoitwa mobile kilimo. Kila Afisa Ugani ambaye tumemuunganisha naye anakuwa na simu anapomtembelea mkulima, anatoa taarifa na anatuwekea namba ya mkulima. Kwa hiyo tunaweza tukakaa ofisini hapa au kwenye halmashauri unampigia mkulima kumuuliza Afisa Ugani alivyokuja kulikuwa na shughuli gani na amekushauri nini.

Mheshimwa Spika, kwa hiyo tutalifuatilia hilo, tutaongeza sana hasa kwa hiyo mikoa mitatu ambayo tutaitaja siku hiyo kuhakikisha kwamba kweli tunafuatilia shughuli za ugani zinakwenda vizuri. Tutafufua na kuimarisha zile farmers’ fields schools, mashamba ya mfano, lakini kila Afisa Ugani hasa kwenye hii mikoa mitatu tutahakikisha na yeye ana shamba na tutamhudumia, tutamwezesha. Wakati tunamkagua utendaji wake tutaenda kuangalia na shamba lake likoje. Wakati kuna shamba la kielelezo katika eneo lake, tunataka kuhakikisha kwamba na yeye analima, anatuonesha anajua kitu ambacho anataka kwenda kuwashauri wakulima.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni pamoja na kuongeza huduma za kupima udongo kama zilivyosema hapa, kwa sababu matumizi ya pembejeo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, yapo mengi ya kusema, lakini kwa sababu ya muda, nashukuru sana na kama nilivyosema naunga mkono hoja. Tunaomba tukija kuomba fedha Bungeni zipitishwe. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitazungumza kwa kifupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukrani sana kwa Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji, kwa sababu wakati wa kuwasilisha kwa kweli walitukalisha chini kweli kweli, walichambua Itifaki kwa undani kweli kweli, waliuliza maswali mengi sana, walitaka tuwahakikishie kila kitu na maslahi ya nchi yetu yapo wapi, tunashukuru tulielewana nasi kwa upande wetu tunachukua ushauri wao wote nita- highlight baadhi ya vitu ambavyo wamevizungumza hapa. (Makofi

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hesabu zangu za haraka haraka tumekuwa na wachangiaji 16 na wote wameunga mkono hoja na wametoa ushauri ambao ni muhimu sana kwetu kuuchukua. Sasa niweke kwa muhtasari mambo makubwa nitajaribu ku- highlight vitu vichache sidhani kama nitahitaji muda wote ambao umewekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kama kila mtu alivyosema Itifaki hii ni muhimu sana kwetu. Kwanza kwa sababu inatuwezesha sisi kufanya biashara, kuuza nje hapa tunazungumza changamoto ya soko, changamoto kubwa ya soko la mahindi, changamoto kubwa ya soko la mchele na tunazungumzia mboga mboga, na tuliona hapa karibuni tatizo la watu kutoa tafsiri kuhusu usalama wa mahindi yetu. Kuwa na itifaki kama hii kama walivyosema baadhi ya Wabunge, ambayo inatupa vigezo ambavyo vinapimika na vya uwazi za kuhakikisha kwamba hatudanganyani kama nia ya kuzuia biashara yetu isifanyike kutatusaidia sisi kuendelea kutumia soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hakika na nadhani wamezungumza baadhi ya Wabunge hapa, sisi ndiyo wauzaji wakubwa wa mazao ya chakula katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa hiyo, sisi kwa hakika ndiyo tunastahili zaidi kuisimamia Itifaki hii ili uweze kuwa na mafanikio kwa hiyo hilo ni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili; hii Itifaki nayo inatuhakikishia usalama wa vile vinavyoingia hapa nchini kwetu, kwa sababu ni vigezo vya kuhakikisha usalama wa vitu vinavyoingia. Kwa hiyo, kwa kusaini hivi na kudhibiti kwamba nchi jirani kwenye Jumuiya hii haziingizi vitu ambavyo vikivuka kwanye mpaka vinakuja kuumiza afya ya watu wetu, tunakuwa tunajilinda na tunalinda watu wetu, kwa hiyo ni Itifaki ambayo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwa na Itifaki hii inatukumbusha kuendelea kuboresha ubora na usalama wa bidhaa zetu kwa sababu bado tunahitaji masoko ya Ulaya, na kote kuna SPS, kinachozuia sana kuingia masoko ya Ulaya Marekani kwa sababu viwango vyao viko juu sana, walau tunajiwekea viwango sasa hivi vya kwenda mbele na kuhakikisha kwamba baadaye tunaweza tukaongeza ubora wetu na kuuza nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa na la muhumu ni kwamba tayari Tanzania ni signatory ni member wa WTO, na Itifaki ya namna ipo katika agreement ambazo tunazo kwenye WTO. WTO ndiyo inasema nchi mkiwa pamoja na mazingira yanayofanana mnaweza mka- customize na ku-localize agreement ambayo tayari iko WTO. Kwa hiyo, hata kama tusinge saini Itifaki hii bado tunabanwa na itifaki WTO ambayo sisi ni member.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulichofanya sasa ni kuhakikisha kwamba tunazungumza na wenzetu, kwa mfano tu, kwenye Itifaki inasema lazima tubadilishane taarifa kwamba ni taasisi gani huko Tanzania itakuwa inahakiki usalama na taasisi gani ya Kenya, taasisi gani ya Uganda, na kadhalika. Kwa hiyo, hata mfanyabiashara anakuwa na uhakika nasi tunakuwa na uhakika unapotaka kuuza bidhaa zako katika nchi hizo unapitia upande gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Itifaki imechukua miaka minane na sehemu mojawapo ni kwa sababu kulikuwa na mjadala mrefu na kila mtu na kila taasisi imetaka kujihakikishia na baada ya pale ikaonekana umuhimu wa kutunga sheria ambayo ilitungwa mwaka jana ya afya ya mimea kuhakikisha baadaye tutakaporidhia hii tutakuwa tumeajiandaa vizuri. Sisi kwa upande wa kilimo tunaita, sheria ambayo tulitunga mwaka jana ambayo inaitwa Plant Health No. 4, 2020 ambayo imeanzisha taasisi inaitwa Tanzania Plant Health and Pesticides Authority (TPHPA), ambayo ni Taasisi muhimu kwa ajili ya shughuli za SPS.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa upande wa Mifugo na Uvuvi tayari walikuwa na sheria nyingi ambazo ametueleza Naibu Waziri hapa kwa ajili ya shughuli hizo hizo. Kwa hiyo, baada ya kuchukua miaka minane sasa hivi tunajua kabisa tumejiandaa vizuri sana na kila taasisi na kila mdau aliyekuwa na shaka ana uhakika kwamba tumezingatia maslahi na msimamo wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya mambo ambayo yamezungumzwa na Kamati yetu ni kwamba lazima tujenge uwezo na ni kweli, wa maabara yetu na kuongeza uwezo wa kupima kwa haraka, tunakubali. Jambo kubwa ambalo pengine baadhi ya watu wanalitilia shaka ni juu ya suala la GMO, humu ndani Itifaki haisemi kwamba tutaruhusu bidhaa za GMO, kilichosemwa ni kwamba tutakaa chini na kuweka utaratibu na sheria na masimamo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu GMO.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tuna msimamo wetu na tunapokwenda kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki hakuna kinachopita bila kukubaliana wote. Tanzania hatuna sababu na hatuna nia ya kutetereka kuhusu msimamo wetu wa GMO.

Kwa hiyo, tutakapokaa mezani kuweka msimamo, msimamo wa Tanzania lazima tuhakikishe kwamba ndiyo msimamo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, hivyo hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala jingine ni kuwa kulikuwa na wasiwasi baadhi ya watu walihisi kwamba kwa sababu ukisoma inasema hii ni kwa ajili ya kutujengea mkakati wa pamoja ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao vilevile utatuongoza sisi kushughulika na Jumuiya nyingine, baadhi ya watu wakadhani kwamba maana yake kwamba ni kushughulika na EPA. Ukweli ni kwamba unapokuwa na Trade Block, mnapokubaliana taratibu zenu, zile taratibu zinatumika vilevile ninyi kufanya biashara na nchi nyingine na blocks nyingine bila kujali EPA. Kwa hiyo, watu walikuwa na wasiwasi kwamba ni EPA lakini siyo kabisa haina uhusiano wa namna yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vyovyote vile standard za SPS za Ulaya ni kubwa kweli ndiyo maana tunapata shida sana kuuza vyakula vyetu katika Jumuiya ile ya Ulaya. Kwa hiyo ingekuwa tunafanya hivyo kwa sababu ya EPA hizi standard wala sisi wengine tusingeziweza katika nchi za East Africa Community. Kwa hiyo, watu wengi wameliona hilo, taasisi mbalimbali zimeona na zimeridhika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengine ambayo tumeambiwa hapa kwenye kujenga uwezo tunakubali sana, mimi nadhani yote tu kwa sababu discussion yote ilikuwa ni positive. Kwa hiyo, ninapenda kuchukua muda huu kutoa shukrani nyingi sana kwa Kamati inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Ishengoma, ametuongoza vizuri sana, na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Almas Maige na Wajumbe wote wa Kamati, kwa sababu product hii ni pamoja na mchujo na majibizano na scrutiny niliyofanya na Kamati na ninashukuru wamekuwa wa kwanza kuanza kuelezea msimamo wa Serikali, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kujadili hoja muhimu ya Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa ambayo kimsingi ina mambo makuu matatu.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, mikopo inayotolewa inatosha? Watu wanalalamika kwamba mikopo haitoshi, kuna watu wanashindwa kupata mkopo. La pili, mikopo hii, hata kama haitoshi, inatolewa kwa haki? Kwamba watu ambao kwa vigezo vilivyowekwa walitakiwa wapewe mikopo, wanapewa hiyo mikopo? Wako watu ambao hawakidhi hivyo vigezo wanapewa na ambao wanakidhi wanakosa mikopo? La tatu; Serikali ina mpango na mkakati gani?

Mheshimiwa Spika, naomba nijaribu kujadili hoja hii kwa kutoa maelezo kadhaa. La kwanza, tuanze na ugawaji wa mikopo kwa haki. Na Mheshimiwa Eng. Ezra ameeleza na ametoa mfano wa mtu ambaye ukimuangalia kabisa na wazazi wake inaonekana kwa vigezo hivi angetakiwa kupata mkopo lakini hakupata.

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mikopo imeweka vigezo na viko wazi, viko kwenye tovuti vya nani anaweza akapata mkopo kwa hali ya kiifamilia, aina ya masomo unayosoma na kuna clusters za masomo; la kwanza, la pili, la tatu. Viko wazi.

Mheshimiwa Spika, wakati tunajadili bajeti ya elimu hapa Bungeni, Waheshimiwa Wabunge kadhaa walitaka Serikali ipitie kuhakiki kwamba tunapogawa hii mikopo vile vigezo ambavyo tumewaambia waombaji wa mikopo kweli tunavizingatia. Na kulikuwa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa wanasema tunafahamu watu wengine ni yatima na vigezo vinasema kama wewe ni yatima utapata mkopo labda asilimia mia moja usome. Je, linafanyika hilo?

Mheshimiwa Spika, kwenye hilo nimeunda kamati ya watu makini kwelikweli, wataalam wa mifumo wanaoweza wakaingia kwenye kompyuta, huwadanganyi chochote, kutoka Mzumbe University, University of Dar es Salaam na kutoka Zanzibar kukagua, moja tu, vigezo hivyo whether ni vizuri au vibaya, vipo; tunavifuata?

Mheshimiwa Spika, mimi nilichogundua baada ya kuunda hii kamati, resistance ambayo ilikuwepo ya kuzuia isifanye kazi imenishawishi kwamba huenda kuna madudu makubwa sana katika bodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mbinu mbalimbali zinatumika kuvujisha information, kutoa barua kwenye mitandao, kumtumia Kigogo, kuzunguka kuchafua, kuweka ukabila na vitu kama hivyo. Na hiyo kwa hakika inaonesha kwamba huu ukaguzi ni muhimu, unafanyika, utakamilika, na utafanyika kwa muda mfupi sana kwa sababu wanaingia kwenye mfumo, watacheki tutajua nini kinaendelea. Hicho Waheshimiwa Wabunge, tutawaletea taarifa. La pili; mkopo unatosha? Kwa sababu hata kama vigezo hivyo kweli vikifuatwa, unatosha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuangalie historia ya mikopo; tulianza, na nadhani Mheshimiwa Mnzava ametoa takwimu vizuri sana. Tulianza wakati fulani mwaka wa kwanza tunadahili wanafunzi 34,000. Kwa kila tunapoongeza bajeti ya mikopo tunaongeza uwezo wa kudahili wanafunzi wa mwaka wa kwanza. Na nitaeleza baadaye changamoto ya sasa hivi imetokana na nini na hatua gani tunazichukua.

Mheshimiwa Spika, kitu kikubwa ambacho kimefanywa na Serikali, na kwa kweli hii ni credit kwa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa sababu alivyoingia madarakani mnakumbuka, kwa sababu bajeti inapitishwa humuhumu Bungeni, alikuta mikopo ya elimu ya juu ikiwa ni bilioni 464 na akafanya maamuzi matatu. kwanza iongezwe kutoka 464 kwenda 570, na ni nyongeza kubwa sana kwa mkupuo. Pili, akaondoa zile tozo, kuna moja ilikuwa asilimia 10 na nyingine asilimia sita, kuna retention na nyingine kama hujawahi kurudisha unakuwa punished. Kwa hiyo hivyo vyote vilikuwa vinasababisha mzigo kwa wanafunzi kurudisha mkopo kuwa mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maamuzi hayo tumerahisisha mzigo kwa waliochukua mikopo ili waweze kurudisha, lakini vilevile udahili uliongezeka, nafikiri wanafunzi 70 kwa mwaka wa kwanza, kwa mara ya kwanza katika historia tangu tuanze Bodi ya Mikopo. Huo ni umamuzi uliofanyika baada ya Mheshimiwa Rais kuingia madarakani, ile bajeti ya kwanza ilisomwa hapa na mtangulizi wangu, Mheshimiwa Prof. Ndalichako, ndivyo tulivyokwenda huko.

Mheshimiwa Spika, sasa kabla sijaeleza chimbuko la changamoto hii tuliyonayo sasa hivi nieleze na hatua nyingine ambazo zinachukuliwa. Ukiacha mkopo kwamba bajeti sasa hivi imeongezwa kutoka bilioni 464 iliyopitishwa na Bunge kwenda bilioni 570, ilipitishwa na Bunge bajeti iliyopita na mwaka huu ilipitishwa kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, hatua za ziada ambazo zimechukuliwa, kabla sijaenda kwenye changamoto, ni pamoja na kwa mara ya kwanza Serikali kuanza kutoa scholarship, yaani kusomesha wanafunzi bila mkopo, unasomeshwa moja kwa moja. Na hii ilipitishwa na Bunge lako Tukufu, na Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulivyoleta proposal hiyo kuanzisha kuhimiza watoto wanaotaka kusoma science na wanaofaulu vizuri sana, wao wapewe scholarship, wasomeshwe kama tulivyosoma sisi wengine moja kwa moja mpaka wamalize. Na wadau wengi wakasema hii iitwe Samia Scholarship.

Mheshimiwa Spika, tulipewa mapendekezo mengi sana, sisi tumeamua tu sasa inaitwa Samia Scholarship. Kuna wanafunzi 640, kwa kufaulu, na ufaulu huo ni wa wazi, hakuna upendeleo. Unaonekana kuanzia wa kwanza mpaka wa 640. Kama umefaulu vizuri kwenye science kama tulivyosema hapa Bungeni na ukaamua kwenda kusoma science, ama engineering au tiba, utasomeshwa na Serikali moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, Serikali ime-engage private sector kuhakikisha kwamba tunaongeza fursa za mikopo. Kwa mfano NMB, na tulisema wakati tunasema bajeti hapa, tukawapongeza. Tumeongea nao, wametenga bilioni 200 kwa ajili ya mikopo ya elimu.

Mheshimiwa Spika, sasa hiyo inakuwa na masharti yake tofauti kidogo na Bodi ya Mikopo. Kwa sababu anayeweza kupata huo mkopo ni mtu ambaye ana miamala inayopita kwenye NMB. Kwa hiyo hilo tumelifanya, bilioni 200 ina interest rate ya asilimia tisa, lakini ni mzazi ambaye anapokea mshahara kwenye NMB kumsomesha mwanao au wewe mwenyewe unataka kwenda kusoma unaweza ukaitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tuna-engage private sector kwa ajili ya kutoa mikopo. Vodacom kwa mfano, sasa hivi wanatoa scholarships, siyo mikopo, wanatoa scholarships moja kwa moja na tunaendelea ku-engage wadau mbalimbali. Na sisi tunapambana kuhakikisha kwamba tunarudisha fedha nyingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo sasa hivi; baada ya mchakato wa bajeti, maana yake bajeti hiyo ni moja ya Serikali. Humu ndani vuta nikuvute, budget ceiling ikoje, inaongezwa au haiongezwi, mkimaliza tunakuja humu. Bajeti ya mikopo ilikuwa ni bilioni 550, ilikuwa ni ileile ambayo iliongezwa with a big jump kutoka 464 kwenda 570. Sasa kwa ku-maintain constant budget ile maana yake ni kwamba wale wanafunzi ambao udahili uliongezeka wakaingia mwaka wa kwanza, wanakwenda mwaka wa pili wanastahili kupata mikopo. Bila kuongeza hizo bilioni 570 zikaongezeka zaidi, udahili wa mwaka wa kwanza hauwezi kuwa sawa na wale ambao tulikuwa na wanafunzi 70 kwa hiyo momentum ile itakuwa maintained tu endapo bajeti ingekuwa zaidi ya bilioni 570.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi tayari tuna-engage na Hazina na tumezungumza sana na Waziri wa Fedha kuangalia kwamba udahili huu ambao kwa mwaka wa kwanza ume-drop lakini mwaka wa pili umeongezeka sana kwa sababu wale wa mwaka wa kwanza wameendelea na mwaka wa pili, idadi ya wanafunzi wanaopata mkopo mwaka wa pili sasa hivi ni kubwa kuliko ambavyo imewahi kutokea. Sasa kwa sababu wamechukua zile fedha wanaoingia mwaka wa kwanza idadi imepungua. Tuna-engage na Wizara ya Fedha, tuna mazungumzo naona yanakwenda vizuri kuangalia namna ya ku-rescue hii situation, kwamba at least ile status quo ya vigezo vilivyotumika wakati ule tuhakikishe kwamba tunaweza tuka-retain wale wanafunzi wakaendelea kupata mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli mapendekezo hapa ni ya muda mfupi kama hili nililosema. Lakini kuna mapendekezo ya muda mrefu. Moja wapo ni kupitia upya Bodi ya Mikopo, lingine ni ku-engage zaidi private sector na la mwisho ni kuona tunaangaliaje mambo ya kibajeti; haya yote ni ya kwetu. Kwa sababu hata bajeti hii ya 570 tulileta hapa Bungeni Waheshimiwa Wabunge mkaturidhia, tukashukuru, tukasonga mbele. Crisis tumeiona wote, tunazungumza tunaamini baadaye tutajua cha kufanya kwenye short term na long term lazima tutakuja na mkakati kama ambavyo imependekezwa hapa kuhakikisha kwamba tunajaribu kuipunguza hii changamoto kadri inavyowezekana.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa muda wako. (Makofi)

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Waziri nakushukuru. Nilisita kukukatisha, nilitaka umalizie mtiririko wako. Nisaidie jambo moja tu; katika hizi Samia Scholarship ambazo umesema ni watoto ambao wanakuwa na ufaulu mzuri kwenye masomo ya sayansi, kwa hiyo wanaokwenda kusoma udaktari ama tiba ni miongoni mwao. Huyu aliyesomwa hapa amekosaje hiyo Samia Scholarship? Hebu tusaidie au ile 1.7 haijafikia vile vigezo vya kupata hiyo Samia Scholarship?

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwanza udaktari uko kwenye cluster ya kwanza ya watu wanapewa upendeleo kwenye mikopo. Lakini ili uweze kupata scholarship tunaangalia waliofaulu vizuri kuanzia wa kwanza, wa pili, wa tatu, wa nne, wa tano, bajeti yetu imeisha tulivyofikia 640. Wako wenye first class lakini wako chini ya 640. Na ninapenda kusema waliopewa scholarship ni nje kabisa ya hawa wa mikopo.

Mheshimiwa Spika, lakini nitapenda kupata hizo details kwa sababu ndiyo maana tumeamua kui-audit Bodi ya Mikopo. Na inashangaza kupata resistance kwenye taasisi ya Serikali kama hii, kwamba usiguse mkopo, unahangaika, umeajiri watu wako, ndugu zako, na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hao wanaosoma udaktari kama alivyosema Mheshimiwa Eng. Ezra pale, kwa alivyofaulu nitapenda kwenda kuangalia. Ni sehemu ya ukaguzi ambao tutauhakiki kuhakikisha kwamba kweli watu wanapata mkopo kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana kwa fursa hii naomba kwanza niweke kumbukumbu sahihi, kwamba ninaomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 294,162,071,000 kupitia fungu namba 43, Fungu namba 5 na Fungu namba 24 kama ilivyoainishwa katika hotuba ya bajeti ambayo tuliwasilisha mbele yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani nyingi sana kwa Wabunge wote kwa michango yao mingi sana tumepata wabunge 87 waiochangia katika hotuba hii kati yao tumepata vile vile michango kwa maandishi kwa Wabunge tisa. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba kila lililozungumzwa na tuliloletewa tutalitafakari kwa kina, tutalizingatia na pale inapowezekana tutalitekeleza kwa hiyo ninawashukuru sana kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani za pekee kwa Kamati yako ya kudumu ya Kilimo Mifugo na Maji chini ya uongozi mahiri wa Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dkt. Ishengoma na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Almas Maige na wajumbe wote kwa kweli tumefanya nao kazi kwa pamoja na nitatoa mfano mmoja tu. Hivi mnavyoona dodoso la umwagiliaji wakati tunapeleka taarifa yetu ya umwagiliaji kwenye Kamati ndio baadhi ya Wabunge wakatuambia hapa mbona kinachoelezwa hapa sicho hasa tunachokiona kule. Kwa hiyo, tulishapanga na Mheshimiwa Bashe tutawanyike nchi nzima lakini basi hapa katikati mara nzige, mara misiba nakadhalika. Lakini tutaanza safari baada ya Bunge na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge naombeni mjaze haya madodoso tutayafanyia kazi kwa sababu tunahitaji kuwasikiliza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tulianza kuyasikia yale kwenye kama Kamati na tutayafanyia kazi. Kwa namna ya pekee napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Hussein Bashe Naibu Waziri wa Wizara yetu ndio Mheshimiwa anasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi aubebe ninamshukuru Mheshimiwa Rais kunipa Mnyamwezi kama Naibu, tunafanya kazi vizuri kwa ushirikiano ni mbunifu na kadri tunavyojua Mheshimiwa Bashe haja-change tulikuwa tunamsikia hapa Bungeni akiongea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi nafasi aliyopo mengine alikuwa anaongea anayafanyia kazi huku sio kila kitu anaweza akakisema kabla hakijakamilika ninawahakikisha kwamba Mheshimiwa Bashe ni yule yule ana moto ule ule na ubunifu ule ule ninashukuru sana na kumpongeza kwa kufanya nae kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda sana kutoa shukrani kwa Katibu Mkuu Andrew Massawe, Naibu Katibu Mkuu Profesa Tumbo, watumishi wote wa Wizara na Taasisi kwakweli wanafanya kazi kubwa na mimi ninasema tu kama kuna matatizo, matatizo ni kwa Waziri kwa sababu tunachowaambia wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiona hakijakwenda vizuri labda hatujawaambia kwa hiyo lawama anabeba Waziri wa Kilimo, wana roho nzuri sana mambo yakiharibika labda Waziri ndio atakuwa mwenye roho mbaya.

Mheshimiwa Spika, kilimo na hili ni muhimu sana lipo ASPD Ilani ya Chama, lipo kila document na hili lazima tulikumbuke tatizo la kilimo ni tija ndogo na Mheshimiwa Bashiru amelieleza vizuri sana na Waheshimiwa Wabunge wengi sana hapa, na nitalifafanua kidogo kwa sababu mikakati tuliyoichukua kwa bajeti ile ile haijaongezeka na nitawaeleza tumefanya nini kuhakikisha kwamba tunashughulika na suala la tija ndogo ni muhimu sana na sisi tunajitahidi tusishindwe kwa sababu tunachojaribu kukifanya tukishindwa pengine nguvu ya kujaribu kukifanya itapotea.

Mheshimiwa Spika, ngoja ianze ku-aggregate data ukiangalia pato la Taifa tunaona kwamba Kilimo kinachangia, kilimo kwa ujumla wake maana mifugo na kila kitu kinachangia asilimia 26-point somethings. Kwa sababu kilimo cha mazao tu ni takribani asilimia 18 lakini watu walioajiriwa kwenye Kilimo ni takribani asilimia 58 maana yake ni nini?

(i) Maana yake ni kwamba pato la Taifa ambalo uzalishaji wetu takribani theluthi mbili inazalisha theluthi moja tu maana yake uzalishaji ni mdogo sana kwa mtu mmoja mmoja, tija ni ndogo sana;

(ii) Umaskini ni mkubwa kwenye kilimo;

(iii) mgawanyo wa mapato ni mbaya, maana yake ni kwamba pato la taifa ndio keki tunayokula inapokuwa wakulima ambao ni theluthi mbili ya watu wote wanakula theluthi moja tu ya pato la Taifa anayekula theluthi mbili ni nani? Kwa hiyo huo ni mgawanyo mbaya wa mapato, na yote hayo ni kielelezo kwamba tija ni ndogo na Mheshimiwa Rais alivyohutubia Bunge lako Tukufu hapa alizungumzia cha kwanza tatizo kubwa ni tija na kama hatuchukui hatua za kunyanyua tija hatua nyingine sio sexy lakini lazima zichukuliwe ili tuweze kusonga mbele hiyo ni aggregate data. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu twende kwa zao moja moja kabla ya hatujaangalia pale niwasomee hapa pamba, nadhani kuna Waheshimiwa walizungumza hapa sisi tunapolima kwenye hekari moja pamba tunapata kilo 200, 300, 350 kwa hekari moja West Africa kuna nchi zinapata kilo 1000 kwenye hekari moja. Kwa hiyo, hata tukizungumza masoko hapa tutazungumza masoko sana lakini tija ikiwa ndogo unaenda kushindana kwenye soko la Dunia na mtu ambaye kwenye hekari moja anapata kilo 1,000 halafu sisi tunapata hekari moja kilo 200,250 na ndio maana nitaeleza hatua ambazo tunazozichukua tena kwa undani zaidi.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kusogea ebu tuchukue michikichi na Mheshimiwa Waziri Mkuu atatusaidia sana kwenye hilo sasa hivi tuna matatizo ya mafuta ya kula wanasema michikichi ilitoka Kigoma. Sisi kwenye hekta moja ya michikichi tunapata mafuta ya mawese tani 1.6 lakini huko tunaponunua mafuta ya mawese sasa hivi kwenye hekta moja wanapata mpaka tani 10 za mafuta. Kwa hiyo, tunaweza tukazungumza masoko sana na tutayazungumza kwa hiyo, kipaumbele cha kwanza kitakuwa nini. Kwa hiyo, soko la mafuta lipo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku zote tunatumia mafuta hapa hatujaacha kutumia mafuta shida iko wapi sio kwamba tu kila mara likiwepo soko basi uzalishaji unakwenda soko mafuta halijawahi kuondoka lakini uzalishaji ndio huo. Hatuwezi kushindana tumeongeza import duty kwenye mafuta wanasema bora kuletwe refine oil sasa import duty unaiongeza pale wananunua mafuta refine wanaleta hapo wanauza kwasababu kwenye hekta moja wanapata almost tani kumi ya mafuta hilo tatizo tusipolitatua hatuendi popote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua kitu kingine hapa juzi nilienda Kongwa, nilienda mchana kidogo nimeangalia mtama, sijui kama picha ipo hapa niliona mtama huwezi kuamini kwa utafiti wetu tu tumegundua mtama aina ya Masiha ambao kwa mkulima sasa hivi kwa hekta moja mtama anapata tani 0.9 akilima vizuri 0.9 kwa mbegu mpya tuliyoipata kwa utafiti wetu sisi hekta moja unapata tani 3 hadi tani 3.8. Kwa hiyo, ukiingia kwenye soko uzalishaji wako tija ni dogo utahangaika kweli kweli kama wenzako tija nzuri na sisi Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano tumesema ni kujenga uchumi shindani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake kuzalisha kwa gharama ndogo ili uweze kuuza, sasa naweza nikatoa mfano mmoja hadi mwigine hadi mwingine hadi mwingine. Lakini hili suala la tija ndio kubwa katika kilimo tusipolitatua tutaendelea kuzungumza kilimo ni uti wa mgongo kilimo ni oxygen tutalizungumza hilo lakini ufumbuzi upo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spia, sasa tunafanya nini? Kwanza kwenye tija na hiki ni vizuri tukisema tunapokuwa tunataka kujenga uchumi wa Viwanda hapa nchini kwa kweli tunataka malighafi iwe ni bei ndogo maana yake ni kwamba tunataka tuweze kupata mazao kwa bei ndogo. Lakini tunataka mkulima apate fedha nyingi na njia pekee unayoweza kutimiza hilo ni kuwa na tija kubwa huyu mkulima wa Pamba tunataka kuanzisha Textile Industry tungependa aweze kuzalisha kilo 1,000 kwa ekari moja ili hata kama bei imeshuka yule mwenye Textile anunue pamba kwa bei nzuri bado kipato cha mkulima kiongezeke.

Mheshimiwa Spika, na hata mishahara sisi kilimo tunaweza tunaongeza mshahara tunaita mshahara halisi real wage tunaongezaje bei ya chakula ikishuka kwa kipato chako hicho hicho unaweza ukala na kununua vitu vingi zaidi kuliko kabla bei ya chakula haijashuka walio-industrialize wote walihakikisha bei ya chakula ndani ya nchi inashuka, tunafanyaje? Tija kwa njia zote hizo mbili; to pathways to industrialization; the cost of raw material that used in the country should go down, the price of food should go down lakini challenge yetu vile vile tunataka kipato cha Mkulima kiongezeke jibu lake tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunafanya nini? Kipaumbele cha kwanza utafiti na Mheshimiwa Rais alivyotoa hotuba hapa alizungumzia hicho hicho na niwaeleze ni kwa nini nimewaeleza hapa kilimo cha Mtama hapo Kongwa ninawaalika mkaangalie kuna mashamba yapo side by side kilimo ambacho ni tradition na kilimo kinachotumia utafiti agronomy nzuri na mbegu nzuri unaona kwa macho huna haja ya kuambiwa.

Mheshimiwa Spika, mihogo tunapata soko sasa hivi la Mohogo China lakini tuna mbegu pale Kibaha tumeigundua inaweza sasa hivi kwa hekta moja kupata kuanzia tani 22 hadi tani 50 na hauwezi kudanganya ule muhogo ukiushika unauona. Sasa hivi tunapata tani tatu tukienda sana tani nane. Kwa hiyo ninashangaa soko linafunguka soko lipo tunashindwa kulishika kwa sababu ya tija ndogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utafiti ni kipaumbele cha kwanza na kitasaidia hata kwenye soko kwa sababu ni suala la ushindani tu. Hapa kuna nchi moja tulipata matatizo mpakani unasikia minong’ono labda wamenunua mahindi kutoka Latin America bei ndogo kuliko mahindi yaliyoko hapa na gharama yote ya usafiri, inakuwaje, tija ndogo, sasa tumefanyaje hapo? Bajeti ya Wizara ya Kilimo iko pale pale, haijaongezeka lakini sisi ndani ya Wizara kwa panga pangua tumeongeza bajeti ya utafiti kutoka shilingi bilioni 7.35 mpaka shilingi bilioni 11.63 ongezeko la asilimia 63. Ndiyo maana nasema watumishi wetu wana roho nzuri, tumekaa hapo mimi na Naibu Waziri nawaambia tutafuteni hela tumeongeza hela hizo za utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumegundua kwenye sheria tunaruhusiwa kuanzisha Mfuko wa Utafiti, haujaanzishwa kulikuwa hamna kanuni. Kanuni tunazikamilisha inawezekana fedha hizi tulizozipata tukaziongeza kutokana na Mfuko wa Utafiti. Tutaongea na wadau wa maendeleo tuongeze hela ili vituo vyetu vyote vya utafiti vifanye vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano sasa hivi kwenye korosho, kila mahali tunataka kuzalisha korosho safi lakini ukiangalia tija yetu ya korosho bado iko chini. Tunaweza tukazalisha twice as much pale Mtwara peke yake, kwa hiyo, tunaenda extensive lakini intensive we are not doing anything. Nasikia Ivory Coast they are doing the best kuliko sisi hapa kwa sababu ya utafiti. Ukiviangalia vituo vyetu vya utafiti vimechoka, kwa kweli ni sawa na yule yule dada daktari alivyosema it is not sexy kwa sababu utafiti ni pata potea, unaweka hela unajaribu unakosa, unaweka hela unajaribu unapata. Nadhani Prof. Ndakidemi yeye alishagundua mbegu moja, kwa hiyo inachukua muda lakini lazima tufanye. Hicho ni kipaumbele cha kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika utafiti la kwanza utafiti kuhusu mbegu, tumeona wataalam wetu wamegundua mbegu nyingi na nzuri; za mtama, mihogo na michikichi inayooteshwa chini ya uongozi wa Waziri Mkuu.

Wananiambia ile mbegu ikiota sasa hivi kwa hekta moja tunaweza tukapata mafuta takriban tani tano, kwa hii michikichi mipya ambayo tunaotesha hapa. Kwa hiyo, tutakomaa na utafiti tu inawezekana tukaondoka Wizarani hatujamaliza lakini tunaanza nalo, tunakomaa nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili kwenye utafiti ni kilimo bora. Kwenye pamba tunaambiwa hata spacing tu inaweza ikaongeza tija zaidi ya asilimia 50 na hiyo ni matokeo ya utafiti. Kwa hiyo, kipaumbele cha kwanza kinabaki utafiti haina maana kwamba masoko siyo kipaumbele kwa sababu haina maana kwamba tutafanya utafiti tukimaliza ndiyo twende kwenye masoko, vyote hivyo tunavibeba. Pia kuna vipaumbele vingine hivi tumeviita vipaumbele vikuu vya mkakati, yako mambo ya kujenga vihenge, sumu kuvu na kila kitu. Hivi ni vipaumbele vikuu vya kimkakati ukiona kimekuwa cha kwanza na kile cha masoko tutakwenda navyo hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele kikuu cha mkakati cha pili uzalishaji wa mbegu. Bajeti ya Wizara imebaki vilevile, panga pangua tumeongeza fedha kwa ASA kutoka shilingi bilioni 5.42 kwenda shilingi bilioni 10.58. Kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri hela za umwagiliaji tutakazozipata kwenye Mfuko wa Umwagiliaji, cha kwanza mashamba yote 13 ya ASA mengi yapo tu ni mapori yanatuletea ugomvi na wananchi tunaenda kuyafufua na tutayafanyia umwagiliaji ili tuweze kuzalisha mbegu throughout the year. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeanza kwenye ngano, tumehamasisha kilimo cha ngano, tumeingia makubaliano na importers; ngano kilo moja sasa hivi itakuwa Sh.850, the best price, wanasema wenyewe wanatudai mbegu ziko wapi? Nimetoa kibali tumeagiza mbegu kutoka Zambia, just across the border, hatuna!

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia alizeti hapa, record ime-improve sana sasa hivi haitoshi. Kwa hiyo, hata kwenye mkakati wa mafuta ya kula ambao nitauzungumzia hapa tuta-import mbegu na tutatumia revolving fund kuwapa wakulima kuhakikisha tunazidi kuzalisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunahitaji mbegu ya kila kitu. Nimesikia Waheshimiwa Wabunge hapa wanazungumza mbegu za mahindi zinakuja kinyemela kutoka Zambia, za viazi zinakuja kinyemela kutoka Kenya na matokeo yake tukiwa tegemezi kwenye mbegu uhakika wa chakula (food security) utakuwa mashakani sana. Kwa hiyo, tumeongeza hilo, mashamba yote ya ASA tutayafufua tutayafanyia umwagiliaji. Tutatumia na sekta binafsi na tutapambana na mazingira mazuri ya kibiashara waongeze uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya utafiti umepata mbegu nzuri, unapata kilimo bora kinamfikiaje mkulima, huduma ya ugani. Bajeti ya Wizara haijabadilika. Bajeti tunayomaliza nayo shughuli za ugani tulitenga shilingi milioni 603 tu. Kwa hiyo, wakati unazungumza idadi ya Maafisa Ugani wachache lakini hata fedha zenyewe ndiyo hizo.

Mheshimiwa Spika, sasa panga pangua, bajeti ceiling ni ileile tumetoka kutoka kwenye shilingi milioni 603 za ugani kwenda mpaka shilingi bilioni 11.5. Wakati tunafanya haya unaambiwa sasa Waziri, Naibu Waziri Maafisa Ugani wako TAMISEMI, kwa nini tukate huku tupeleke TAMISEMI, tunapeleka hela hiyo Maafisa Ugani wawe TAMISEMI wawe popote wanatumikia Serikali moja kwani hatutasogea bila kuboresha ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako wakulima wakubwa, viko vyama vya ushirika kama Kahama wameajiri Maafisa Ugani na unaanza kuona matokeo lakini sehemu nyingi mtu hajui afanye nini. Hapa Dodoma tukisema tulime alizeti watu wengine wanavuna mbegu ile ile wanaenda kuotesha, productivity inakuwa ndogo sana, unaotesha lini na kwa utaratibu gani?

Mheshimiwa Spika, tutakachofanya kwenye ugani hicho hasa ndiyo tunasema tunataka tusishindwe na tutajitahidi tusishindwe, tutafanya nchi nzima mambo mengi na tunashirikiana na vyama vya ushirika na makampuni binafsi kama ile NOSC – Njombe Out Growers Services Organization na Kahama Cooperative Society na nchi nzima tutapeleka huduma nyingi. Hata hivyo, pamoja na yote tutakayofanya katika nchi nzima tumechagua mikoa mitatu ambayo tunataka kufanya huduma za ugani kwa namna ambayo pengine hatujaifanya kwa muda mrefu au tangu tupate uhuru. Tumechagua Dodoma, Singida na Simiyu, tumeongozwa na umuhimu wa kuzalisha mazao ya mafuta, alizeti at the heart of it. Tunajua tukifanikiwa tutarudi kwa Waziri wa Fedha ule mwaka unaokuja, unaona matokeo haya, unaona shughuli za ugani zinavyolipa hebu twende tukafanye kote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika hii mikoa mitatu pamoja na baadhi ya Maafisa Ugani wengine tunawapa mobility (pikipiki). Nilishasema hapa tunawasaidia kwa fedha za Serikali wawe na mashamba yao, walime, tuweze kukagua unalimaje wewe, mashamba darasa yote yanafufuliwa na ya mwanakijiji ambaye anaonekana anaweza akawasaidia. Pia tutawapatia mafunzo rejea, wengine wameshafunzwa miaka 20, 25 wanafanya kazi hawajafundishwa upya new technics na new discoveries ambazo tunazo.

Mheshimiwa Spika, tutahakikisha tunawapa spark smartphone ambazo zitasaidia vitu vingi. Moja watakuwa wana-monitor masoko lakini pili sisi tutawa-monitor wanafanya nini. Kila siku kuanzia Jumatatu mpaka Ijumaa lazima ajaze kwamba amefanya nini kwenye mobile kilimo. Umeenda kumtembelea Mheshimiwa Gambo lazima ujaze ulienda saa ngapi, tatizo lake lilikuwa nini, umemshauri nini na simu yake. Kwa hiyo, tunaweza tukakaa ofisini tukapiga tukamuuliza Mheshimiwa Gambo eti alikuja bwana shamba hapa? Kwa hiyo, tunafanya hayo katika mikoa hii mitatu.

Mheshimiwa Spika, vilevile tutawapa soil tool analysis kits kwenye kila halmashauri na kadhalika. Katika suala la alizeti ambalo nitalizungumzia mbegu hazitoshi kwa hiyo tutatoa huduma ya ugani na hii huduma ya ugani kwenye alizeti na pamba kwa Simiyu na alizeti itaongeza masuala kama mtama na mazao mengine yote pamoja na Mheshimiwa Mavunde alivyosema suala la kilimo cha zabibu. Kwa hiyo, mazao yote mabwana shamba watafundishwa upya namna ya kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya mwaka mmoja tutapima matokeo ya hiki tunachojaribu kwenye mikoa mitatu. Tutafanya kazi na Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya na tutafuatilia kwa karibu na Waheshimiwa Wabunge tunawa-invite muangalie.

Mheshimiwa Spika, sasa labda nilisemee hapa hapa kwamba katika hiyo mikoa mitatu nguvu kubwa sana itaenda kwenye alizeti na mazao mengine, mbegu tutapata wapi? Sasa hivi tumeshazungumza na taasisi moja ya kimataifa nadhani tumeshapata hela ya kuanzia. Juzi nimefanya mkutano kwa Zoom inaweza ikaongezeka, hela hiyo ikija tunaita mkutano wa wakamua mafuta, tutazungumza nao na ma-bankers kuhakikisha kwamba wakulima kwenye vyama vyao vya ushirika wanapata contract farming tunawapa mbegu ya chotara (hybrid) ambapo kwa sababu hatuna record ya kutosha tutawaletea wakati wa mawazo tuta-recovery halafu tutakuwa revolving fund. Kwa wakulima wakubwa bila kujali Mikoa ya Dodoma, Singida na Simiyu iwe ni Kiteto, Simanjiro, Manyara au Morogoro tutawa- encourage na sisi wapate mbegu waingie kwenye contract farming ili sasa viwanda vya kukamua mafuta ambavyo sasa hivi vinafanya kazi miezi miwili, mitatu, minne vinafungwa kwa uhaba wa mbegu za mafuta viweze kuingia kwenye mikataba na wakulima katika mikoa hii.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele kingine sitavitaja vyote tulizungumza ni umwagiliaji. Kwenye umwagiliaji bajeti tumeongeza kutoka shilingi bilioni 17.7 kwenda shilingi bilioni
51.5. Pili tumeanzisha Mfuko wa Umwagiliaji ambao tunaamini tutautumia kwa ajili ya kuimarisha shughuli za umwagiliaji na tutajaribu kuongea na wadau mbalimbali tuhakikishe kwamba tunapata fedha nyingi na kuchukua hatua ambazo Naibu Waziri amezieleza.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kidogo kuhusu masoko. Kwanza nianze na tumbaku na Mheshimiwa Naibu Waziri nakushukuru sana kwa maelezo, tunazungumza na ile kampuni ambayo iliondoka hapa, prospect ni kubwa watakuja kurudi kwenye biashara. Wamewasiliana na Mheshimiwa Bashe na tumekubaliana. Walitaka kutuma consultant tumesema hapana tunamtaka yeye mwenyewe aje tuzungumze kwa sababu tunakosa ushindani. Tumbaku ni zao pekee ambalo nilikuta watu wamekamatwa huko Katavi wanaambiwa eti umelima tumbaku bila kibali wakanyang’anywa hela zao, nimetoa amri warudishiwe hela zao. Halafu unapewa pembejeo na makampuni hayo unalima tumbaku ukitaka kuuza unambiwa wewe hukupewa contract ya kulima tumbaku yako ni makinikia wananunua kwa bei ya kutupa, hilo tutalishughulikia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu chai, tunaanzisha mnada wa chai kama ambavyo tumeshaeleza.

Mheshimiwa Spika, sasa twende kwenye mahindi. Tumebarikiwa sasa hivi tuna ziada kubwa ya mahindi. Kwanza niwahakikishie hata kabla ya changamoto ya mpaka na Kenya tuliita mkutano mkubwa wa wafanyabiashara wa nafaka hapa Dodoma kuhimizana twendeni tukatafute masoko kwa sababu haya masoko kazi ya private sector kazi yetu ni ku-facilitate. Tulizungumza tukaunganisha na Mabalozi wote wa nchi jirani za DRC, Zambia, Malawi, Burundi, Rwanda, Kenya, tukazungumza na kuweka mikakati ambayo mingine tumeanza kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kenya niseme mahindi yetu yanayoenda Kenya tunapima sisi ni salama. Nadhani hata wakati yamezuiwa bado kwa namna fulani yalikuwa yanaenda. Sasa Mheshimiwa Rais ameenda Kenya tumesikia wote tangazo mahindi yanakwenda. Natoa wito kwa wafanyabiashara sombeni mahindi pelekeni Kenya maana yanapendwa sana kule. Natoa wito tena kwa vyombo vyetu vya usalama barabarani mmetusaidia sana, tukiona mtu anasafirisha mahindi na ufuta siyo bangi watu wetu wamekuwa harassed sana kule mpakani acha yaende yauzwe kwa vyovyote na yauzwe popote, nendeni Serikali itasimama na nyie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi ninavyozungumza rate ya kupeleka mahindi Kenya ni wastani wa tani 2,000 kwa wiki. Kwa hiyo, mahindi yanakwenda na tunafuatilia mpakani. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa safari yake ya kwenda Nairobi na mimi nilikuwa kwenye msafara wake na nilipata fursa ya kuongea na Waziri wa Kilimo wa Kenya alikuja mwenyewe mpakani Namanga na alinipigia simu. Kwa hiyo, biashara ipo na ni soko kubwa tulichangamkie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya Kenya ni tani 600,000 ya mahindi bado tunacho-supply kule ni tone tu. Twendeni tukauze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imetoka Sudan ya Kusini, wamefanya mazungumzo mazuri sana na wafanyabiashara wa Sudan ya Kusini watakuja hapa kwa ajili ya kukamilisha maelewano ya namna ya kuuza mahindi na mchele na mazao mengine Sudan ya Kusini. Mimi binafsi nimepanga tunaenda na msafara wa wafanyabiashara baadaye Sudan ya Kusini na tutaenda DRC, mchele Zimbabwe na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Zimbabwe wana mahindi ya kutosha wanahitaji mchele. Humu ndani kuna Mbunge mwenzetu ni mfanyabiashara, namsifu sana ametusaidia kufungua soko la Eswatini Swaziland, consignment ya kwanza imeenda. Kwa hiyo, tunataka kufungua masoko South Afrika na maeneo kama hayo. Tumekubaliana Wizarani mtu anapoomba kibali cha kusafirisha mazao akishasema nia yake hata asiporudi tunamtafuta na tumekubaliana utamfuata popote umsaidie kujaza online apate kibali bidhaa zetu ziende. Kwa hiyo, tunaendelea kuchakarika kupeleka mazao sehemu nyingine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwahakikishie mahindi sasa hivi Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imepata shilingi bilioni 10 tumewaambia waingie sokoni bei ya mahindi ni ndogo wale wanafanya biashara nunueni mchangamshe soko nendeni mkauze. Kwa hiyo, tumekubaliana wataanza kufanya biashara hiyo. Tuna mazungumzo vilevile na World Food Program, tuna mkataba pamoja na hivyo kuna mahitaji mengine ya mahindi ambayo yanaendelea. Pamoja na changamoto hii tunaamini kwamba sasa soko litatulia na hasa wafanyabiashara wakiona fursa ipo na mambo yanakwenda.

Mheshimiwa Spika, kwenye mchele sasa hivi tunauza sana Uganda. Tunataka kwenda Saudi Arabia na nchi nyingine kwa ajili ya kufanya kitu kama hicho. Niishie hapo ili nisiache mambo mengine muhimu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna changamoto ya ushirika, ni kweli kumetokea wizi mkubwa na ubadhirifu Mheshimiwa Waziri Mkuu amelisimamia sana. Mali za ushirika ziliibiwa mchana kweupe lakini chini ya uongozi wa Waziri Mkuu na Ikulu wakati huo na sasa hivi mali nyingi imerudi. Kweli tumekuwa na majizi humo lakini siyo wote ni majizi kwenye ushirika.

Mheshimiwa Spika, tulimualika Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika cha Kahama, nitamualika hapa siku moja ananunua pamba kwa bei nzuri kuliko mtu mwingine yeyote. Kahama sasa hivi pamba inatoka sehemu nyingine inakimbilia kule, analipa hela na baadaye analipa na nyongeza na wameajiri na Maafisa Ugani. Tusimame na ushirika na Waheshimiwa Wabunge naomba tusaidiane tujenge ushirika ndiyo nguvu ya mnyonge Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matatizo hayo ni pamoja na aliyosema Mheshimiwa Saashisha. Mheshimiwa timu ilishaenda kufanya uchunguzi, ripoti ilikuwa haijafika kwangu ilikuwa kwenye Tume nimeipata na nimepitia tusipuuze anachosema Mheshimiwa Saashisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Bashe nimemuomba ajipange aende Kilimanjaro kwenye ziara mojawapo atakwenda kulishughulikia hili. Mambo ambayo nimeyaona siyasemi sasa hivi lakini hatutapuuza alichosema Mheshimiwa Saashisha watu wasije wakadhani kwamba unaropoka, umetusaidia sana kutueleza hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu stakabadhi ghalani, narudia tena Mheshimiwa Bashe amelieleza vizuri sana na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote walioeleza changamoto na faida. Kwa hiyo, tutamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye hili mamlaka ibaki Wizara ya Kilimo. Pamoja na kwamba kuna maduhuli kwenye mazao tusianzishe stakabadhi ghalani kwa lengo la kukusanya maduhuli ya Serikali hata kama tunahitaji maduhuli hayo. Hii ni kwa sababu tunamuadhibu yule anayepeleka kwenye ghala halafu tunaacha hao wengine. Vilevile kuna geographical factors na wingi wa mazao yanayozalishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi ndiyo tutakaotoa kibali kwamba zao hili liingie stakabadhi ghalani. Napenda kuwahakikishia tutafanya hivyo consultatively, tutakaa chini wote na Waheshimiwa Wabunge na wawakilishi wananchi mtashirikishwa pale ambapo tunaona inaweza ikafanya kazi tutapenda tuje tusishirikiane tufanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie mambo mawili harakaharaka; moja nashukuru Waheshimiwa Wabunge na napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wetu wote wa Siha, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Longido, Monduli, Simanjiro na Mwanga wakati tunapambana na nzige tulijifunza mambo mengi tukagundua kwamba kilimo anga ni kama vile hatukukiendeleza. Mheshimiwa Waziri Mkuu ulitoa maelekezo na sasa tumetoa, tulikuwa na shilingi milioni 150 za kilimo anga sasa hivi kwa bajeti ileile narudia bila kuongeza ceiling panga pangua tumeweka bilioni tatu na humo ndani mojawapo tutanunua ndege, hizi ndege za mashirika mengine ni zetu pamoja.

Mheshimiwa Spika, Shiriki la Ndege la Jangwani sisi ni wanachama na naamini ni nchi mbili tu Tanzania na nchi nyingine ndiyo zimelipia ada. Kwa hiyo, mlivyosikia tunapiga kelele ndege irudi ni ndege yetu kama ilivyo ya Kenya, Ethiopia, Sudan na kadhalika lakini tunahitaji moja ya akiba hapa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapambana na kwereakwerea na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao tulishirikiana, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, mwisho suala la mitaji limezungumzwa sana humu, Benki ya Maendeleo ya Kilimo imesemwa na kadhalika. Tutaomba tuwe na siku ifanyike semina, tutakuomba kwa sababu modules ya ile benki sizo ambazo kila mtu anavyoiamini. Halafu kama kuna mawazo tutaongea lakini ukweli ndiyo hivyo kuna namna inavyofanya kazi na kuna maeneo mengi sana imefanya kazi kubwa sana; nimeenda Minjingu nimekuta wamewekeza vizuri sana kwenye upanuzi wa viwanda. Tumeenda maeneo mengine wamekopesha wakulima wadogowadogo, kwa hiyo tutawale hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeunda kamati, high level panel na nimemchagua Mheshimiwa Bashe awe chairman nawashukuru sana wakuu wa mabenki wote pamoja na Mkuu wa PAS yupo pale kwenye Speakers Gallery pale, wamekubali watakaa kwenye hiyo kamati watafanya kazi kwa takribani miezi minne. Watapata fursa ya kuongea na kila mtu ili tuweze kupana namna ya ku-fund kilimo kwa namna ambayo sio ya gharama kama hii.

Mheshimiwa Spika, labda la mwisho ambalo nimelisahau nimalize kwenye ushirika tunapitia sheria upya na kabla hatujaja na sheria hapa tutahitaji kuwa-consult Wabunge wote. Tunataka twende kwa makini sana kwa sababu tunataka ushirika ukue, AMCOS zifanye vizuri, hatutaki zife lakini tunataka tujue ni nini vikwazo ambavyo tunavipata sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda huu, Waheshimiwa Wabunge nawashukuru sana…

SPIKA: Kabla hujamalizia kuna Wabunge walikulaumu kidogo kwamba kwenye hotuba yako hukugusa masuala ya horticulture kabisa na kwenye majibu hapa pia umesahau horticulture ama una neno moja mawili ya kusema. (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nimeongea strategic intervention bila kutaja zao lolote. Tuliposema utafiti hatukusema kwenye zao gani ni mazao yote. Kwenye hotuba ya bajeti nadhani tunaweza tukaonesha hapa alivyosema Mheshimiwa Dkt. Kimei tulimpelekea kitabu na kumuonesha reference na sio kwa bahati mbaya tulimualika Dkt. Mkindi hapa kama mgeni wetu kwa sababu horticulture ni kati ya mazao ya mkakati na Mheshimiwa Waziri Mkuu ametu-guide. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda nitoe na mfano, Arusha tutakuwa na kikao cha investment forum into agriculture European watakuja Arusha. Suala kubwa ambalo tunataka kuongea nao ni kurudisha ile logistical arrangement ambayo inasaidia sana kwenye ku-export horticulture. Kulikuwa na call chain system walikuja hapa kwa namna fulani wakashindwa wameenda Ethiopia wanafanya vizuri sana. Niliongea na Balozi nadhani wa Uholanzi alivyonieleza nikasema nataka tuwaite tena tukae nao tuone kama wanaweza wakarudi ili mkulima wa parachichi Njombe pale aweze kuli-export haraka sana na bila uharibifu. Kwa hiyo, kwa kweli hatuwezi kupuuza horticulture.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa sababu nami ni mara yangu ya kwanza kuzungumza baada ya Mheshimiwa Rais kuniteua kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kutoa shukrani nyingi kwa Mheshimiwa Rais kwa uteuzi huu na kumwahidi kwamba tutafanya kazi kwa bidi, timu yote, kwa ajili ya kuleta mabadiliko ambayo sote tunayatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa fedha hizi za ahueni ya UVIKO ambazo sekta ya elimu kwa ujumla wake ndani ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na TAMISEMI tumepata zaidi ya bilioni 300 ambayo kwa kweli inatusaidia sana kusonga mbele, hasa katika suala la miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeisikiliza vizuri Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. Tunamshukuru sana Mwenyekiti, Mheshimiwa Stanslaus Nyongo na Wajumbe wote kwa taarifa nzuri ambayo tutazingatia sana ushauri ambao wameutoa. Napenda kukuhakikishia vilevile tutazingatia ushauri ambao umetolewa na Waheshimiwa Wabunge kwa mapana yake katika utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda kueleza vitu vichache ambavyo vinahitaji ufafanuzi. La kwanza ambalo linaweza likawa linazusha taharuki ni kuhusu transition ya wanafunzi kutoka darasa la kwanza mpaka la saba kuanzia form four kwenda form five, form six, kwamba tuna dropout kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zetu hazioneshi kama net enrollment rate hata gross enrollment rate Tanzania ni mbaya. Tulipata peak kubwa sana ya enrollment baada ya Serikali kutangaza kutoa elimu bure, na enrollment iliongezeka sana mwaka 2016. Ili tuweze kuona picha vizuri najaribu kutoa takwimu za wanafunzi waliofanya mtihani Darasa la Nne na waliofanya mtihani Darasa la Saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wanafunzi waliofanya mtihani Darasa la Nne mwaka 2018, walikuwa ni 1,362,642 na walipofika Darasa la Saba 2021, waliofanya mtihani ni 1,132,084. Noteworthy alarming lakini haturidhiki na transition hiyo na hao ambao wame-drop hapo katikati. Hata hivyo, figure siyo kubwa kama ambavyo imekuwa alluded to, hapo mwanzoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hizi takwimu ni vizuri kama tunataka kuziangalia kwenye NBS, net enrolment rate ambayo inaonesha watu ambao kwa umri fulani walitakiwa wawe darasa fulani, na wangapi bado wapo katika darasa hilo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo, ningependa nieleze kwamba Serikali hasa chini ya Uongozi wa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, imejikita sana kuhakikisha kwamba wale wote ambao wana-drop shuleni kwa sababu mbalimbali, wanarudi shuleni. Ndiyo maana ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais tumetoa mwongozo, tumeusambaza, kuonesha namna gani ya kuwarudisha tena wanafunzi ambao waliacha shule kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na wale ambao walipata ujauzito; na wengine kwa sababu walikuwa na changamoto ambazo hawakuzijua. Kwa mfano, mwanafunzi alikuwa na matatizo ya kusoma hakujua kwamba anahitaji miwani, akaacha shule. Baadaye akagundua kumbe nahitaji miwani, anataka kurudi shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunajaribu kutoa fursa kwa kila mwanafunzi ambaye hata kama alikuwa ameshaacha shule, aweze kurudi shule na kuendelea kusoma ili tuhakikishe kwamba namba zinaongezeka kutoka hizi namba ambazo nilikuwa nimezieleza hapo katikati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeshauri sana suala la kuongeza ajira hasa ya walimu; na ni kweli kuna upungufu mkubwa wa walimu. Serikali imewekeza sana sasa hivi kama tulivyoona katika miundombinu ya ufundishaji hasa madarasa na vifaa vilevile vimenunuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ukweli ni kwamba bado tuna upungufu mkubwa wa walimu. Wengine mtakuwa mlimsikia Mheshimiwa Rais wakati anapiga simu kuongea na walimu na wanafunzi wa Benjemin Mkapa Secondary School pale Dar es Salaam. Alieleza kwamba baada ya miundombinu, kazi kubwa sasa hivi ni kuajiri walimu ili kuhakikisha kwamba tunapata walimu wa kutosha.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja nielezee suala la mitaala ambalo kidogo ni muhimu, niache haya mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati vilevile imeeleza na Waheshimiwa Wabunge wamesisitiza tumalize mapema iwezekanavyo mapitio ya mitaala na ndicho tunachojaribu kukifanya. Hata hiyo tarehe ambayo imewekwa tungetaka tumalize kabla ya hapo. Pia ningependa tuzingatie kwanza kwamba mitaala hii inaongozwa na Sera. Sera ya 2014 inafanyiwa mapitio, Sheria, halafu mitaala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia Sera ya 2014 inaelezea miaka sita ya elimu ya msingi; elimu ya lazima mpaka Form Four. Maana yake ni kwamba hata mitaala inapotengenezwa lazima izingatie suala hili, endapo sera itakapofanyiwa mapitio, tutabaki na vigezo hivyo hivyo. Kwa hiyo, tunafanya mapitio ya sera na wakati huo huo tunapitia mapitio ya sheria na tunapitia vilevile mitaala. Pia kama Kamati ilivyoshauri, tunapitia mitaala siyo kwenye elimu ya msingi tu, ni pamoja na Vyuo na Vyuo Vikuu, na miongozo imetolewa na kazi inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naona kengele imeshagongwa, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kushukuru sana kwa fursa hii ili kuchangia taarifa hizi za Kamati tatu. Napenda kupongeza sana Kamati zote tatu, Wenyeviti na Wajumbe kwa ripoti zao nzuri sana ambazo kwa kwa kweli kama nitakavyoeleza baadaye maazimio yao, recommendations zao tunazikubali kwa Wizara ya Elimu na nyingine tumeanza kuzitekeleza. Napenda vilevile kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia mjadala huu na maoni yao ambayo yamegusa Sekta ya Elimu hasa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia tumeyabeba na mengine nitajaribu kuyatolea maelezo kidogo. Kwa hiyo mchango wangu pengine utakuwa nia mfupi kidogo.

Mheshimiwa Spika, naomba niungane na wenzangu vilevile kumpongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan hasa katika Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mambo makubwa sana ambayo yamefanyika kwa kipindi kifupi ambacho amekuwa Rais wa Nchi yetu, ujenzi wa shule nyingi wote tunauona, ujenzi wa vyuo kwa mfano sasa hivi najua kila Mbunge tukiongea naye anaulizia kuhusu VETA, lakini makubaliano tumeshafanya na Hazina kwa maelekezo ya Rais wetu ni kwamba fedha tuliozonazo za VETA zitajenga VETA katika kila wilaya ambayo sasa hivi haina VETA mradi tupate ardhi. Vilevile ujenzi wa campus ya Vyuo Vikuu katika mikoa 14 ambayo ilikuwa haina campus ya Vyuo vikuu. Kwa hiyo mafanikio haya na yenyewe ni mazuri sana yanaleta vilevile changamoto kwa sababu tunaongeza idadi ya wanafunzi ambao wanahitaji fursa ya kusoma na kazi yetu kubwa ni kupambana na hizo changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala kubwa ambalo limezungumzwa hapa ni kuhusu Bodi ya Mikopo kwa Elimu ya juu na nitajaribu kuelezea kwa kifupi yale ambayo yameelezwa na Kamati na yale ambayo tunakusudia kuyafanya. CAG mwenyewe ametoa recommendation kubwa kwamba tufanye maboresho ya Sera na Sheria ya Bodi hii na vilevile tuhakikishe kwamba Wizara inaongeza usimamizi na kuimarisha mfumo wa kitaasisi kwa ajili ya kuimarisha bodi hii. Mambo mengine ambayo yametajwa na CAG ambayo yamerudiwa na PAC ni masuala kama vile kugundua yatima ambao waliomba mikopo ambapo kwa vigezo ambavyo vilitakiwa vitumike, walitakiwa wapate mikopo, vilevile kasi ya kushughulikia rufaa kwa mtu ambaye ameomba mikopo, lakini hakuweza kupata na nadhani kwamba kwa vigezo ambavyo vimetangazwa angeweza akapata na vilevile kuangalia wale wanaostahili.

Mheshimiwa Spika, CAG vilevile amezungumzia kuhusu endapo mini testing yaani mfumo tunaotumia kutambua nani apewe mkopo na apate kiasi gani kama kweli tunatumia taarifa za kutosha kuweza kuhakikisha kwamba kweli tunawalenga wale ambao tunahitaji kuwapata.

Mheshimiwa Spika, taarifa vilevile ya PAC imepitia humo humo na maazimio ambayo wameyapendekeza yapo katika mfumo huo huo. Mambo kwa mfano ya sera na sheria, vilevile mfumo wa usimamizi na kwa sababu taarifa zote mbili zinazungumzia umuhimu wa Wizara kuhakikisha kwamba inafanya usimamizi wa bodi na kusimamia vilevile mfumo wa kitaasisi na PAC ina- recommend vilevile Msajili wa Hazina naye a-play role yake katika kuimarisha suala hili.

Mheshimiwa Spika, mengine ambayo yamezunguzwa na PAC ni pamoja na hilohilo la mini testing ambayo inatumika wanaona kwamba pengine inahitaji taarifa nyingi zaidi na imetambua kwamba mahitaji ya mikopo kwa kweli yanaongezeka sana na yameongezeka zaidi baada ya nyongeza kubwa ya bajeti ambayo ilifanyika mwaka jana.

Mheshimiwa Spika, kuna lingine moja hapa ningependa nilizungumzie kidogo, kwenye taarifa ya PAC nili-clarify kidogo tu, kwa sababu katika ripoti pameelezwa kwamba mini testing inaangalia needs kwa ajili ya kujua nani anaweza akapata mkopo na haiangalii aina ya shahada mtu anayeisoma na tutahitaji kuweka maelezo vizuri zaidi kwa sababu ziko cluster tatu. Cluster ya kwanza inapewa upendeleo zaidi; ya pili upendeleo wa pili; na ya tatu. Kwa hiyo inaangalia mahitaji ya kaya na mtoto anakotoka na vilevile ni masomo gani anaenda kuyasoma? Hivyo ndiyo vigezo vinavyotumika, tunahitaji pengine kuweka ufafanuzi ili viweze kueleweka vizuri zaidi hapa.

Mheshimiwa Spika, wakati wa mjadala huku kumekuwa na masuala mengi vilevile ya kuelezea umuhimu wa kuhakikisha kwamba kuna haki katika kugawa mikopo. Kwanza nianze kusema kwamba tangu tuanzishe Bodi ya Mikopo kumekuwa na uboreshaji wa namna ya kugawa mikopo na nitatoa mfano.

Mheshimiwa Spika, hapo mwanzo taarifa zilizokuwa zinatumika zilikuwa haziingizi taarifa kwa mfano ya TASAF, sasa hivi Bodi ya Mikopo inaruhusu kuchukua taarifa moja kwa moja kwa mwombaji wa mkopo ambaye anatoka kwenye kaya ambayo imeonekana ina mahitaji ya kusaidiwa na TASAF moja kwa moja achukuliwe kama ni anatoka kwenye kaya yenye uhitaji mkubwa kwa hiyo, anapewa upendeleo hivyo hiyo ni taarifa ya ziada ambayo inatumika sasa hivi. Pia Bodi ya Mikopo sasa hivi imefungamana na RITA kwa mfano kwa ajili ya kutambua watoto ambao ni yatima kwa hiyo, ukitoa taarifa yako inaweza ikawa verified mara moja na hali ikaenda vizuri. Hivyo, kumekuwa na improvement mwaka hadi mwaka ikiwa ni pamoja na jitihada za kuongeza makusanyo kwa wale ambao walinufaika na mikopo kuhakikisha kwamba wanarudisha mikopo yao.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa Taarifa Mheshimiwa Waziri kwamba, katika hicho anachoongelea kuhusu uboreshaji wa utoaji mikopo na amesema moja ya improvement yao ni kuingiza taarifa za TASAF. TASAF bado yenyewe kule kuna shida kubwa kwamba mpaka hata hao wanaopewa hiyo fedha au ule unafuu wa kusaidia kaya maskini kule kwenye TASAF kwamba, wapo wanaopewa ambao siyo wenyewe ama wanapewa ambao siyo walengwa. Wapo ambao wanao uwezo na bado wanaingizwa kwenye TASAF. Tunayo malalamiko hayo mengi, kwa hiyo, nadhani pia taarifa za TASAF haziwezi kufanya improvement kubwa kwenye mikopo. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, unaipokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba niipokee taarifa hiyo kwa maana kwamba, Serikali tuna haja ya kuboresha maeneo yote kuhakikisha kwamba, taarifa ambazo zinakusanywa ziko sahihi, lakini hii hatua ya bodi ya kuanza kutumia Taarifa ya TASAF ni attempt ya kuhakikisha kwamba tunapata taarifa nyingi zaidi kumtambua mtoto mwenye mahitaji, lakini kwa kweli mfumo mzima unahitaji kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie suala lile la sera ambalo naona liko katika mapendekezo ama maazimio hapa. Kweli, kwamba, kuna haja ya kupitia sera na matokeo ya kisheria ya higher education financing hapa nchini pamoja na mfumo wa kitaasisi. Sasa hivi tunapitia sera ya elimu na ninapenda kutoa taarifa kwamba ni kama tumeshamaliza mapitio ya sera sasa hivi, tunasubiri tu mfumo wa approval ndani ya Serikali halafu tutatoa almost like a white paper kwa ajili ya majadiliano ya mwisho kabla ya kwenda kufanya maamuzi kupitia Serikali nzima na suala hili la namna ya ku-finance higher education ni suala ambalo limezingatiwa katika mapitio ya sera na kwa hiyo, liko kwenye azimio hapa nasi tayari tumeshatangulia tunakwenda hukohuko. Hiyo, itaendana vilevile na kupitia mapitio ya Sheria ya Elimu pamoja na sheria nyingine ambazo zinahusiana na utoaji wa mikopo kwa elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika, vilevile suala la Wizara kuongeza oversight kwenye Bodi. Progress imekuwa ikiongezeka lakini sasa hivi tutazingatia zaidi, vilevile kupitia mfumo wa kitaasisi ambao utatuhakikishia kwamba kwa kweli tuna- improve kwa sababu kila siku kuna room ya ku-improve. Suala moja kubwa ambalo ningependa nilizungumzie kama ambavyo limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi hapa ni suala la kuhakikisha kwamba mikopo inagawanywa kwa haki.

Mheshimiwa Spika, wengi wamelizungumza na kwenye taarifa ya CAG ameeleza, watu ambao wanapewa mikopo ambao yeye alivyowaangalia kama sample ameona kwamba hawakustahili kupata mikopo, wengine wamepata mikopo zaidi kuliko walivyostahili, hili ni suala ambalo na sisi tunalitilia umakini sana. Wakati nilipozungumza hapa mara ya mwisho, nilizungumza kwamba tumeweka Kamati ya wataalam wa mifumo na takwimu, wanaweza wakafanya programming kuweza kuchukua takwimu zote na kuzichakata na kuzi-cluster kuangalia vigezo na kuhakikisha kwamba, tunahakiki kweli wale waliopata mikopo kama wanakidhi vigezo ambavyo vilitangazwa. Inawezekana vigezo hivyo tusiridhike navyo, lakini madhali ndiyo vilivyotangazwa tunataka kuangalia compliance yake ikoje.

Mheshimiwa Spika, Pili, Kamati hii itaangalia vilevile ni taarifa zipi za ziada ambazo tukizitumia zitaongeza ubora wa mini-testing kama ambavyo CAG mwenyewe amesema tunahitaji kuboresha taarifa hizi.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa hapa kwamba Kamati imeshaanza kazi, inaendelea na kazi kwa bidii kabisa na itafanya kazi hiyo itamaliza. Kamati hii kwa sababu ina wataalam wa mifumo, takwimu na programing, siyo watu wa kwenda kufanya sampling, ni watu ambao wanaweza wakakaa kuandika program na kuchakata takwimu zote za watu ambao wameomba mikopo na kuhakikisha kwamba, wanajua kama tumekuwa tukizingatia vigezo ili tuweze kupata recommendations tujue tunakwendaje.

Mheshimiwa Spika, sote wote kama Serikali tunajua umuhimu kwamba fedha zilizopo kwa ajili ya mikopo kila mtu anasema hazitoshi, zitaongezwa zitakuwa hazitoshi, zitaongezwa hazitoshi, basi kile ambacho tunacho kigawanywe kwa haki, anayepata mkopo awe kweli yule anayestahili na ambaye kwa kweli anajiwezaweza kama fedha hazitoshi asije akaingia kule.

Mheshimiwa Spika, suala hili tusipolizingatia malalamiko yatakuwa makubwa sana. Kwa hiyo, napenda kusema Kamati iko kazini na imeongezewa nguvu leo, vilevile itakuwa na fursa ya kutangaza kwa watu wenye taarifa za kupeleka kwenye Kamati, nje ya takwimu zilizopo kule watazipeleka kwenye Kamati tutapata taarifa hatimae tutajua tuweze kuongeza nini katika yale tunayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo mengine ya ziada ni pamoja na kama nilivyosema pale kwamba, mikopo ya elimu ya juu kama CAG alivyosema ni kweli tunahitaji kutafuta vyanzo vingi zaidi. Kulikuwa na recommendations huko mwanzo kwamba tuweze kutoa mikopo hata kwa wale wanaofanya Diploma. Kwa sasa hivi tumeznza na NMB tumepata Bilioni 200 na masharti yake, ingawaje masharti nafuu sana kwa mikopo ya elimu, lakini tutaendelea kufanya hivyo kuhakikisha kwamba, tunaboresha education financing hapa nchini, hasa higher education financing na financing hasa kwa hivi vyuo vya kati kama VETA na vingine vya ufundi.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa muda. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii. Nami naungana na wenzangu wote kupongeza Kamati zote mbili kwa kazi nzuri na ushauri mzuri sana na pongezi kubwa kwa Kamati inayotusimamia, Kamati ya Huduma za Jamii chini ya uongozi wa Mheshimiwa Nyongo, tunafanya nao kazi vizuri sana. Wanatuelekeza na kutushauri na kwa kweli hapa tulipofika kwa sehemu kubwa ni kufanya kazi pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nampongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Wizara ya Elimu tunajivunia kuona kipaumbele cha elimu katika Serikali. Nitoe mifano miwili tu. Mfano, sasa hivi tunazungumzia kujenga VETA katika wilaya zote Tanzania, shughuli ambayo inaanza kabla ya mwisho wa mwaka huu, nadhani mwezi huu wa Pili tutakuwa tumeanza kazi hiyo. Hazina tayari wametuambia tunachukua fedha zote, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametuambia na kazi itaanza.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunasambaza Kampasi za Vyuo Vikuu katika mikoa 14 ambayo ilikuwa haijawahi kupata Kampasi ya Chuo Kikuu. Haya yote ni maelekezo ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nawapongeza sana na ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao, kwa kweli tutazingatia. Tumekuwa tukichukua kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi sana ya kusema kwa sababu mengi ya ushauri tutayabeba kama ambavyo tumeyapokea. Ila kuna jambo moja kubwa ambalo limezungumzwa napenda nilisisitize, hili ambalo tumelisikia wote hapa Bungeni kuhusu umuhimu wa walimu. Imeelezwa umuhimu wa kuwa na walimu wa kutosha na umuhimu wa walimu katika elimu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alilianzisha asubuhi kwa kueleza umuhimu wa kuwaenzi walimu wetu, nasi hilo tunalizingatia. Kama mnavyojua, Rais wetu tangu aingie madarakani, wakati tulikuwa tume-freeze employment kwa ujumla alipoingia madarakani tu tumeanza kuona, kama alivyosema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ajira za Walimu zimeanza na zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, tumekamilisha mwongozo sasa hivi wa kuhakikisha kwamba Walimu wanaojitolea tunaweza tukawa-engage vizuri kwa ajili ya kuchangia idadi ya walimu ambao watatosha kutoa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaangalia vilevile suala la ufundishaji wa walimu. Katika mageuzi ya elimu ambayo yanakuja, jambo ambalo ni wazi kwamba tutakuwa tunazingatia sana suala la ufundi stadi; hawa wenzetu wa Zanzibar wanasema mafunzo ya amali. Kwa hiyo, tutangalia vilevile tunavyo-train walimu kuelekea huko. Nilikuwa Mtwara juzi, kuna hili moja limesemwa, nimeangalia Vyuo viwili vya Ualimu vya Mtwara. Kimoja kinaitwa Mtwara Kawaida na kingine kinaitwa Mtwara Ufundi, vimekaa vimeshikana vimepakana, lakini vyote ni Mtwara kawaida, kwa sababu ufundi haufundishwi.

Mheshimiwa Spika, tutarudi huko kwenye ufundi na kuangalia namna ya kufanya vyuo vyote viwili iwe Kampasi moja ambayo inafanya kazi na Vyuo Vikuu lakini kwa ajili ya kufundisha masomo ya kuandaa walimu kwa ajili ya Mafunzo ya Elimu ya Amali kwa sababu na fursa ile ni kubwa, karakana zipo lakini hazijatumika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake, suala la kuwaenzi walimu ni zuri sana. Napenda niseme hivi kwa sababu najua walimu wengine watakuwa wanasikiliza. Wamesikiwa Waheshimiwa wabunge wanavyowasemea vizuri, wamemsikia Mheshimiwa Waziri Mkuu anavyowasemea vizuri, tunajua kabisa kwamba hapa karibuni kumekuwa na clip zinatoka ambazo zinasababisha mpaka watu waanze kuwa na jicho tofauti kuhusu walimu. Walimu wetu popote mlipo sikilizeni Waheshimiwa Wabunge wanavyowasemea na kuwatetea na hasa tukizingatia alichosema Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kazi inayofanywa na Walimu wetu ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kuna mwalimu mmoja mfano clip yake inazunguka na napenda nimtaje hapa, anaitwa Mwalimu Yusuph Mohamed Yusuph. Huyu ni Mwalimu wa Shule inaitwa Ikorongo, iko Wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara. Huyu Mwalimu anaitwa Yusuph Mohamed Yusuph, maarufu kama Yusuph Pangoma. Ana ubunifu mkubwa sana wa kufundisha, na ninatarajia wakati wa kusoma bajeti tutamwalika hapa kwa ajili ya kupewa pongezi na walimu. Wako walimu wengi sana wanafanya kazi kubwa, wanajitolea na ubunifu kwa kutegemea mazingira yale yale ambayo wanafanyia kazi. Tutaendelea kuwaenzi sana walimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizi clips ambazo zimekuwa zikizunguka kama Kamati yetu ilivyosema na Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyosema hapa, kuna suala kubwa la malezi shuleni na suala la maadili ambalo ni jukumu letu vilevile. Tunashirikiana na Wizara mbalimbali; tunashirikiana na Mheshimiwa Dkt. Gwajima, TAMISEMI, tunashirikiana na Wizara mbali mbali chini ya uongozi wa Waziri Mkuu, lakini ndani ya Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia tuna jukumu la kufanya vilevile.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kusema, pamoja na kwamba tumeona hizo clip, walimu wetu wengi karibia wote ni wazuri sana na wanalea Watoto wetu vizuri sana kama alivyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuendelee kuwaenzi walimu hao.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa wale wachache ambao wanakiuka maadili, unyanyasaji wa watoto kwa namna yoyote ile, kesho Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Francis Michael atatangaza sasa namba ambazo zitatumika kama call center ili kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge mmoja hapa kwamba hivi sisi tutaripoti wapi kama tukiona matukio kama haya.

Mheshimiwa Spika, mtu yeyote hasa walimu wengine ambao mkiona kuna unyanyasaji wa aina yoyote, vitendo vya uvunjaji wa maadali katika shule yoyote hapa nchini, unapiga ile namba whether unataka jina lako litajwe au lisitajwe, Serikali ipo kila mahali mpaka vijijini na kwenye vitongoji. Tukipata hiyo namba sisi tutafuatilia na kuhakikisha kwamba tunadhibiti hali kama hiyo na kuhakikisha kwamba hivi vitendo vichache sana ambavyo vinaondoa taswira kwa sababu sisi wenyewe tunafundisha kwamba samaki mmoja akioza kwenye tenga wote ameoza. Kwa maana hiyo hawa wachache wanaoharibu taswira ya walimu tutahakikisha kwamba tunawadhibiti na kwa ajili ya kulinda watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo limezungumzwa sana hapa ni umuhimu wa hasa masomo ya hisabati na sayansi, kwa hakika. Kwa kuangalia matokeo, tukiangalia trend kwa mfano form four sio kwamba imeenda chini ukilinganisha na miaka mingine lakini bado hairidhishi. Tungependa ufaulu uongezeke hasa katika masomo ya sayansi na hisabati na nitawakumbusha tu Waheshimiwa Wabunge, ninyi mliridhia hapa Bungeni kuanzisha scholarship maalum kwa wanafunzi wanaofanya vizuri sana kwenye masomo ya sayansi. Wakimaliza form six wanasomeshwa na Serikali full time, baadaye ile scholarship tumeiita Samia Scholarship. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ilikuwa ni njia mojawapo ya kuhakikisha kwamba tunahimiza watu wasome na tumesikia na tunapata mrejesho mashuleni kwamba sasa watoto wanasema ili kumwondelea mzazi wangu shida ngoja nisome sayansi na nitajitahidi ni faulu vizuri sana ili nihakikishe kwamba kweli nipata scholarship ya kwenda kusoma.

Mheshimiwa Spika, tayari wameshapata scholarship, wapo vyuoni, tutakuwa na siku moja ya kutangaza na kuonesha majina, kuonesha jinsi tulivyowachagua kwa sababu tulisema tutawachagua kwa njia ya haki kabisa kuhakikisha kwamba kila moja ambaye anaweza kupata nafasi hiyo atapata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile tutazingatia katika hii walimu wa kujitolea, mwongozo na vilevile ajira zinazokuja kuhakikisha kwamba tunatoa kipaumbele kwa ajili ya walimu wa sayansi na hisabati kwa sababu kwa kweli maeneo hayo ni muhimu sana kwa maendeleo ya elimu ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Waziri, swali moja tu. Hizi taarifa za huyu Mwalimu Yusuph kutoka Serengeti umezipataje?

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, huyu mwalimu nimezungumza naye vilevile na nawasiliana naye.

SPIKA: Aah, yaani yeye alikupigia akakuambia kuhusu ubunifu wake ama alijirekodi ukaona kitu? Ama ni kata iliripoti? Shule iliripoti? Kata? Yaani taarifa zake ulizipataje? Ni hicho tu.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, aliwasiliana na mimi mapema sana na baadaye niliziona hizo ambazo zimekuwa recorded anavyofundisha, nikawasiliana na wenzetu wa TAMISEMI tukam–track down, tukahakiki kweli ni mwalimu na mimi nipo constant in touch with him. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kutofuata Maelekezo ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii ya kuchangia hoja ya Kamati yetu na naishukuru Kamati kwa kazi waliyoifanya na mambo waliyoibua.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe maelezo kidogo; la kwanza, Kamati inasema kwamba nanukuu kwenye taarifa; “kwamba wakati akitoa maelekezo yake Mheshimiwa Waziri alisema kwamba, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu inamkwamisha.”

Mheshimiwa Spika, niliyosema hapa yapo kwenye Hansard, sikusema maneno hayo nadhani ni kughafirika, naomba iondolewe kwenye taarifa.

Mheshimiwa Spika, nilipokutana na Kamati tulizungumza, niliwaeleza kwamba ile Kamati ya Kupitia Mikopo ilishaanza kazi na kwa kweli ilianza kazi kabla hoja iliyotolewa hapa kuhusu mikopo ya elimu ya juu na mtoa hoja wakati ule Mheshimiwa Ezra alinukuu siku naongea na vyombo vya habari, kwamba atakayekwamisha kazi ya Kamati hii nitakula kichwa. Nilisema vile kwa sababu nilikuwa nataka nione speed ya kazi inaongezeka. Sasa hata ukienda kwa whatever explanation kuanzia tarehe 12 Julai mpaka 31 Oktoba, 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati ile ilikuwa tayari kufanya kazi mwezi Septemba, on record na ilipeleka proposal na ilikuwa tayari kufanya kazi mwezi Septemba, haikuanza kufanya kazi na wale watu wameajiriwa sehemu nyingine wakawa wametawanyika. Kamati iliniuliza, wewe Bodi imekukwamisha? Niliwaambia Bodi naimudu, ikinikwamisha mimi nitaishughulikia siji kushtaki Bungeni hapa na sikuishtaki Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakaniuliza ulitumia neno resistance, kwamba resistance uliyoiona inasababisha uamini kwamba huenda kuna madudu, ulikuwa unamaanisha nini na resistance? Kwa sababu sikusema Bodi wala sikuitaja, niliwaambia moja, sikuridhika na speed, nitaeleza kidogo.

Mheshimiwa Spika, pili, nilieleza na nilieleza hapa leakages za taarifa mitandaoni, ya barua zinazotoka kwenye Bodi na maelezo kwamba hapa Mkenda anafanya witch-hunting anataka kuweka Mchaga kuongoza, aache kufuatilia huku, yeye atafute hela ziongezeke zaidi. Sasa ile hisia huwezi kujua na hata sasa hivi siwezi kujua leakage inatoka wapi, lakini fact of the matter is, mimi kazi yangu na CAG ameeleza kwamba oversight ya Wizara kwenye Bodi ya Mikopo si nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kazi yangu ya ku- exercise oversight sio witch-hunting na uzuri clip zipo. Mara ya mwisho nilivyokutana na Bodi tarehe 5 Septemba nadhani, niliwaeleza sina haja ya kumuumbua mtu hii ripoti ni ya Waziri na ni ya Bodi. Tunataka kuangalia wapi tunaweza tuka-improve. Ripoti ni ya Waziri na ni ya Bodi, tunataka kuangalia wapi tunataka…

Mheshimiwa Spika, sasa mtu anapodhani kwamba ni witch-hunting au nataka kumwondoa mtu siwezi kuelewa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri ngoja nikuongoze kidogo, ukitoa maelezo yale ambayo hayako kwenye hii taarifa na michango ya Waheshimiwa Wabunge kwenye hoja hii, utataka tena tufungue, watu watataka kujibu tena hoja hizo.

Na ile Bodi haitapata tena fursa ya kuanza kujibu haya, kwa hiyo, tutakuwa tunaenda mbele, tunarudi nyuma. Kwa hiyo, nikuombe ufafanuzi umepewa muda, hoja zile zilizotolewa na Wabunge hapa baada ya kuwa Kamati imeleta taarifa na zile za kwenye taarifa ambazo wewe unataka kuzitolea ufafanuzi ili tuwe tumejielekeza kwenye jambo lililo mbele yetu.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante na nitafanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwanza sikuja kuishtaki Bodi humu, sina haja ya kuishtaki Bodi, ninaimudu na wala sikusema kwamba Bodi inanikwamisha kama ilivyoandikwa hapa. Neno resistance nililieleza vizuri kwenye Kamati na nilieleza mambo ya speed, nilieleza mambo ya mitandao. Vilevile maelezo ambayo nilikuwa nimeyapata ambayo sikuridhika nayo na Kamati niliwaeleza vilevile kwamba waliambiwa na Kamati fulani ya Bunge kwamba Kamati yangu ivunjwe, tulipotafuta maandishi hatukuyapata.

Mheshimiwa Spika, kitu cha muhimu ni kwamba kazi imeanza tarehe 31 na lazima niseme ukweli Kamati inapata ushirikiano mkubwa sana na Bodi na nimeongea nao hata leo kwamba kazi inaendelea vizuri sana, wanaendelea. Watanzania wote wanaosikiliza wajue kwamba tutajaribu kuchambua na kuelewa kwamba tunavyogawa mikopo kama kweli tunagawa kwa haki, mahali ambapo pana upungufu tutaweza kuparekebisha.

Mheshimiwa Spika, lazima niseme vilevile kwamba suala kubwa ambalo hata CAG alizungumza na kila mtu alizungumza hapa ni suala la kugawa mikopo kwa haki. Kamati yenyewe hadidu za rejea kama ulivyouliza ya kwanza, kwa sababu ni wataalam wa mifumo na ni wataalam wa programming ni kwenda kuangalia takwimu na kuzi-program, kuhakikisha kwamba kila aliyeomba mkopo, sio some...

T A A R I F A

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, hii taarifa siipokei na nimeeleza kwamba at some point nilikuwa sijaridhika na speed ya utekelezaji. Ile Kamati ilikuwa tayari kufanya kazi mwezi Septemba…

T A A R I F A

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa sijaridhika na speed ya kazi, nikatoa onyo public, siyo humu Bungeni na kazi ikaanza na ushirikiano ni mkubwa na ndio jukumu langu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilizungumza in public na labda ni-quote maneno; “kwamba atakayekwamisha Kamati hii nitakula kichwa” iko ndani ya uwezo wangu na nilizungumza hivyo…

T A A R I F A

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimekuelewa na nakushukuru kwa mwongozo wako.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo yako mambo yangu ya kazi yangu niliyasema nje ya Bunge, wakati naongea na press na yale niliyoyasema humu na yale niliyoyasema humu nilijaribu kuyafafanua kwenye Kamati kwamba yalikuwa na maana gani kama nilivyoeleza ni hayo nilikuwa najaribu kuyaeleza. Lakini bado tunarudi tena kwenye hoja ya msingi kwamba, kazi ya ile Kamati ni kujaribu kuhakikisha kwamba mikopo ya wanafunzi inagawanywa kwa haki. Nadhani hata ukiangalia kwenye ripoti ya CAG imesema wako yatima ambao wamekosa mikopo. Kwa hiyo, kazi ile na Waheshimiwa Wabunge wakati tunajadili bajeti yetu hayo mambo yalikuwepo na Wabunge wengi walipenda tuyafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha muhimu sasa hivi ni kwamba kazi inafanyika na ushirikiano upo na ile Kamati imetoa communication strategy, mtu yeyote mwenye taarifa za ziada atapeleka kwenye Kamati. Naamini kazi itakapokamilika tutakuwa na fursa nzuri sana ya kuboresha namna ya kutoa mikopo. Kwa hiyo, hilo ni kubwa na nadhani hatutakiwi kutoka kwenye reli.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, labda nieleze kidogo tu kuhusu TOR ambazo ulikuwa umesema hadidu za rejea, sijui kama ni wakati wake wa kuzieleza hapa, kwa sababu kazi kubwa ile ni compliance, kwamba vigezo ambavyo vimetangazwa, mwombaji anapoomba mkopo anavisoma kwenye tovuti, kwamba nikiwa na hivi naweza nikapata mkopo. Je, ukiomba na unakidhi hivyo vigezo unapata mkopo? Kama nilivyosema wakati ule hata kama vigezo hivyo bado vina mashaka, ni vizuri kwanza tuvitendee haki tufanye hivyo.

Mheshimiwa Spika, la pili, tunahitaji na iko kwenye CAG Report kuangalia taarifa zipi za ziada tunaweza tukazitumia kwa ajili ya ku-improve means testing na hii wanaifanya. Tumefanya kazi na Bodi kama ninavyosema na wenyewe wameongeza TOR zao kwa sababu kuna kazi wanataka kuifanya na niliridhia na nataka kutoa tena taarifa hapa, Kamati ipo kazini, inafanya kazi vizuri, speed nilikuwa sijaridhika nayo, sasa hivi ninaridhika na kazi inavyokwenda na Bodi. Nisiporidhika hatua za kuchukua zipo ndani ya mikono yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii. Naomba nianze kwanza kwa shukrani.

Kwanza naomba kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja yetu hii. Tumehesabu, tuna Wabunge 43 waliochangia na Wabunge kadhaa wameleta kwa maandishi. Tunaomba kuwahakikishia kwamba kila mchango uliotolewa hapa tutauzingatia sana tunavyosonga mbele na maoni mengi ambayo tumeyapata kwa kweli ni ya kufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa, naomba niishukuru sana Kamati yetu inayotusimamia, Kamati ya Kudumu ya Bunge, maoni yao takribani yote tutayafanyia kazi. Wamekuwa wakitusimamia vizuri sana na kutuongoza. Hapa tulipofika kwa kweli, ni kwa sababu tumekuwa tukifanya kazi kwa pamoja. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na ninaishukuru sana Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba vilevile nimshukuru Naibu Waziri, Mheshimiwa Kipanga. Nina bahati sana kupata Naibu Waziri mchapa kazi kama huyu, ananisaidia sana. Hii kazi ni teamwork ikiwa pamoja na Katibu Mkuu Prof. Sedoyeka pamoja na Manaibu Katibu Wakuu Prof. Mdoe na Prof. Nombo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais. Mtakumbuka wakati anahutubia Bunge hapa mwezi wa nne mwaka 2021 katika vitu alivyovisema ilikuwa ni kutoa maelekezo kwamba, Serikali sasa ipitie mitaala ili iboreshe elimu na kuhakikisha kwamba elimu hii inaakisi mahitaji yetu na kweli inamwandaa mhitimu kuweza kuishi katika mazingira yetu na katika mazingira ya utandawazi. Amekuwa akirudia maelekezo hayo mara kadhaa na hata mimi aliponiteuwa kwenye Wizara hii alinipa maagizo kwamba kipaumbele chako ni kusimamia mageuzi makubwa kwenye sekta ya elimu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais aliliona hili mapema, Waheshimiwa Wabunge wameliona na takribani kila Mbunge aliyezungumza amegusia suala la mageuzi ya elimu. Sasa dunia nayo imeliona, dunia imetukuta tumeshaanza kazi kwa sababu Rais wetu tayari alikuwa ahead of the time. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, na kwa kweli, nashukuru sana vilevile kwa sekta yetu ya elimu kwa ujumla wake, kwetu sisi pamoja na wenzetu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kwa mfano, kwa upande wa mikopo ya elimu ya juu Mheshimiwa Rais alivyoingia ofisini alikuta tunatumia Shilingi bilioni 464 kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu, aliagiza iongezwe kufikia Shilingi bilioni 570 kwa mkupuo. Ndani ya mwaka mmoja tumeweza kuongeza vile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, aliagiza tuondoe zile tozo; 6% ya kutunza fedha na 10% ya adhabu ili kumpunguzia mzigo mtu aliyenufaika na mkopo huu wakati wa kuweza kurudisha na vilevile fedha zile ambazo zilikuja kutoka IMF alizielekeza katika sekta ya elimu vile vile. Sisi kwetu tulipata takribani Shilingi bilioni 65, lakini kwa ujumla wake sekta nzima ya elimu ilipata takribani robo ya fedha hizi kwa ajili ya kusaidia elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naona tunapoenda legacy ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wetu inawezekana itakuwa katika eneo la elimu. Namshukuru sana Makamu wa Rais vile vile na Waziri Mkuu wanamsaidia Rais vizuri sana kutusimamia sisi katika utendaji wetu wa kazi. Naomba nikushukuru sana nakupongeza tena wewe kwa kazi nzuri unayofanya kutusimamia kuendesha Bunge letu na Naibu Spika wetu na Wenyeviti wote wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani vile vile kwa wapiga kura wote watu wa Rombo kwa kunihakikishia kwamba naendelea kuwa hapa.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu hoja zile specific, na ni nyingi. Nyingine Waheshimiwa Wabunge wanaswma kwamba mimi nahitaji VETA, hapa tunahitaji High School; tumeziandika na tutaenda kuziangalia namna ya kutekeleza kwa sababu tutaangalia kwenye bajeti tumeweka kiasi gani. Kuna mahali pengine tunaambiwa twende; kwa mfano Mheshimiwa Maganga, kwenda kuona kule katika maeneo yake, hayo yote tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi sitaenda sana kwenye specific nitaenda katika masuala mapana ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, la kwanza; hoja ilitolewa kwamba na ilitolewa na Mheshimiwa Sanga na nadhani kila mtu alipiga makofi kwa sababu kila mtu anaamini hivyo; kwamba katika sekta ya elimu tusiwe tunabahatisha na kukurupuka na kubadilisha. Kwamba, akija huyu twende kushoto akija huyu twende kulia akija huyu songa mbele akija huyu rudi nyuma. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, kwanza mimi binafsi kunieleza hivyo its like preaching to the Pope himself; kwa sababu hatuamini kwamba Wizara hii inahitaji kufanya maamuzi bila kutafakari vya kutosha na bila kushirikisha wadau vya kutosha. Hii si Wizara ya kubadilisha badilisha mambo bila kuwa na utafiti wa kina. Hii si Wizara ya kusema kuna la Mkenda la Ndalichako wala la Kawambwa. Hii ni Wizara ya Serikali ya Watanzania na jukumu letu ni kuhakikisha kwamba tunatumia mifumo yetu yote kwa ajili ya kufanyia maamuzi, na ndivyo tunavyokwenda; na ndiyo maana suala la mageuzi ya mitaala nimelikuta halikuanza na sisi lilikuwa limeanza na Mheshimiwa Ndalichako.

Mheshimiwa Spika, tunapitia Sera; hii ilipita wakati wa Mheshimiwa Kawambwa. Mambo mengi ambayo tunayafanya sasa hivi yako katika ripoti ya Jackson Makweta 1982. Kwamba tunarudi nyuma kuangalia ni nini ambacho hatukutekeleza? Lakini pamoja na yote hayo tunaendelea kushirikisha wadau. Waheshimiwa Wabunge tulikuwa na semina pamoja, tulikuwa na ya kutosha kueleza Wabunge, tukasema hatuji sisi kueleza tunakuja elezwa. Kwa hiyo tuliweka kila kitu kilichoko pembeni tukasikiliza maoni tumeahidi tutarudi tena, uturuhusu tukishakamilisha tutakuja sasa kueleza tumekusanya nini kabla kuingia kwenye mchakato wa kufanya maamuzi.

Mheshimiwa Spika, la pili labda niseme hili highlight moja kubwa, na ninaisema hii kwa sababu nataka kuhimiza wadau wengi watusaidie. Nimesema Mheshimiwa Rais ametusaidia kuongeza mkopo wa elimu ya juu, na ilikuwa ni big jam pamoja na kuondoa zile tozo ambazo zilikuwa zinasababisha kurudisha mkopo unakuwa kazi kubwa sana. Lakini vile vile Wizara imeamua kuongea na taasisi mbalimbali kuhakikisha kwamba tunaongeza fursa za mikopo kwa ajili ya elimu.

Mheshimiwa Spika, hapa nataka niitaje NMB, na nimtaje specifically mkuu wa NMB Ruth Zaipuna. Kwa sababu yeye baada ya mazungumzo amekubali kutenga bilioni 200 kwa ajili ya mikopo. Yapo masharti, tunaendelea ku- negotiate tuone unafuu utakuwa mkubwa kiasi gani. Fursa hii itatuwezesha sisi si kutoa tu mikopo kwa elimu ya juu itatoa fursa kwa wafanyakazi wanaotaka kwenda kujiendeleza kielimu na itatoa fursa kuhakikisha kwamba hata wazazi wanaweza kupeleka watoto wao kwenye elimu ya juu. Tumeshatoa maelekezo kwenye Bodi ya Mikopo kuhakikisha kwamba wanaangalia kwenye bajeti itakayokuja 2023/2024. Bajeti ambayo itafuata baada ya hii kukamilika tuwe tumeshajipanga kuhakikisha kwamba tunatoa scholarship kwenye vyuo vyetu vya ufundi na pengine VETA katika hali ya juu ili tuhakikishe kwamba yale maeneo ambayo mtu akipata mkopo anaweza akaajirika kirahisi na kurudisha fedha basi tunapeleka fedha kule. Kwa hiyo nawashukuru sana NMB, naomba benki nyingine zote tuendelee na mazungumzo, kwa sababu tunaendelea. Bado kuna fursa ya kuongeza wigo kwa kutoa mikopo kwa wanafunzi wetu.

Mheshimiwa Spika, tunaongea na Private Sector ambayo siyo banking. Na wakati nawasilisha hapa jana alikuwepo bwana mmoja anaitwa Rupin Rajani alikaa pale juu pale. Huyu tulizungumza, nikamwambia hebu jaribu kutengneneza aina fulani ya private foundation watu binafsi ambao wanaweza wakatafuta fedha kusaidia Watanzania kwenda kusoma nje kwenye Vyuo vya hali ya juu kama MIT Harvard na kadhalika. Alienda Marekani amerudi akaniona akanipa brief nzuri sana; na tutakuwa na mkutano tarehe 14 jioni nyumbani kwake Dar es Salaam. Amenieleza kuna matumaini makubwa sana watu binafsi wa ndani na nje kukaa chini na kuangalia uwezekano wa kuanzisha foundation ya kukusanya fedha kusaidia Watanzania wanaotaka kwenda kusoma nje hasa katika maeneo ya sayansi teknolojia na tiba.

Namshukuru sana ndugu yangu Rupin Rajan na alikuja hapa Dodoma nikamualika akarudi Dar es Salaam akaja asubuhi hapa kuja kusikiliza hotuba yetu ya bajeti naomba wadau wengine wote ambao tutakutana nao tushikane mkono kwa sabbu private sector ina nafasi kubwa sana ya kufanya hapa.

Mheshimiwa Spika, lakini si hivyo tu, vile vile sisi ndani ya Wizara tumetenga fedha kwa ajili ya scholarship, tuna bilioni tatu. Nyingi zitaenda kwa vijana wanaomaliza Form Six watakaofanya vizuri sana katika masomo ya sayansi watakaotaka kwenda kusoma elimu tiba, sayansi na teknolojia watapata 100% scholarship kutoka kwa Serikali kama zawadi ya kufanya vizuri darasani.

Kwa hiyo wakati matokeo ya Baraza la Mitihani yatakapotoka wale watakaofanya vizuri sana kwenye PCM, watakaofanya vizuri sana kwenye PCB, masomo ya sayansi wakaotoka kwa wazazi wajue haijalishi mzazi ni tajiri ni maskini tutawasomesha asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, lakini tutatoa fursa vile vile, upendeleo maalum, scholarship kwa watu wenye ulemavu watakaomaliza form six na ambao watakuwa wamefanya vizuri vya kutosha kwenda kuendelea na masomo ya shule. Kwa hiyo hizi hela tunaamini zitatusaidia wenzetu kwa ajili ya kwenda kusoma.

Mheshimiwa Spika, tumetenga fedha vile vile kwa ajili ya scholarship kwa ujumla wake kwa Wahadhiri wa Vyuo Vikuu Watanzania; Vyuo Vikuu vyovyote, Private na Government; ambaye atapata nafasi ya kwenda kusoma nje ya nchi yetu katika masomo ya sayansi teknolojia na tiba. Kiasi hicho cha fedha, kati ya hizo bilioni tatu tulizotenga pamoja na fedha za mradi wa HEET ambao tunakaribia kuanza kuutumia, tutatoa scholarship kwa hawa watanzania kwenda kusoma nje kwa sababu itatusaidia sana kupunguza tatizo la ajira katika Vyuo vyetu Vikuu. Kwa hilo kubwa tunakwenda nalo.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo saba tuliyoyazungumza kwenye bajeti yetu katika kuendeleza elimu, na Wabunge wengi wameongelea humo humo. Niyaseme haraka haraka halafu nitoe ufafanuzi katika maeneo kadhaa.

Mheshimiwa Spika, moja, tulisema lazima tupitie hii sera, nitaeleza kidogo, mbili sheria, tatu mitaala, nne idadi ya waalimu, wakufunzi na wahadhiri, tano ubora wa walimu wakufunzi na wahadhiri, sita miundombinu na saba ni vitendea kazi.

Mheshimiwa Spika, tukisema tunabadilisha mitaala ni jambo zuri sana, tukisema tunabadilisha sera ni jambo zuri sana suala la idadi ya walimu na ubora wao miundombinu vitendea kazi hatutopuuza; na hiyo nimesikia Wabunge wengi sana wamesema. Kwamba sasa tukienda huku hatuna walimu wa kutosha hapa na kandalika.

Mheshimiwa Spika, twende kidogo kwenye Sera. Sera yetu sasa hivi ukiondoa pre-school sasa hivi unaweza ukai- define kwa structure tu ya elimu ni 7, 4, 2, 3 plus. Maana yake ni kwamba, miaka saba ya lazima, miaka minne ya 0-level, miaka miwili high school, miaka mitatu plus ya Chuo Kikuu, minimum Chuo Kikuu ni miaka mitatu kwenda juu.

Mheshimiwa Spika, labda niliseme hili kwa sababu limezungumzwa sana. Kenya walikuwa na utaratibu wa 8, 4, 4. 8 elimu ya lazima, 4 Sekondari na 4 Chuo Kikuu. Na ile ilikuwa inawafanya washindwe kuingia vyuo vikuu kwetu sisi kwa sababu sisi nasi tuna viwango na wakenya wengi walikuwa wanapeleka watoto nchi nyingine hasa Uganda ili waweze kupata access kwenye vyuo vingine vya nchi nyingine kwa sababu wao ili uweze kwenda Chuo Kikuu lazima ukae Chuo Kikuu miaka minne; sisi Chuo Kikuu minimum miaka mitatu. Kwa hiyo huwezi kuchukua mtu aliyesoma kwa utaratibu huu Kenya halafu ukamlete Tanzania asome miaka mitatu ilhali elimu yake haijamuandaa kufanya miaka mitatu ya Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Spika, lakini wenzetu wa Kenya na wenyewe wamebadilika sasa hivi wanaenda six elimu ya msingi, three jumla miaka tisa elimu ya lazima three Sekondari na three Chuo Kikuu kwa hiyo wana six three three sasa hivi wamebadilisha na naamini kwa utaratibu huo itakuwa ni rahisi kuwapata wanafunzi kutoka Kenya.

Mheshimiwa Spika, sasa turudi kwa upande wetu sisi. Kwa upande wetu Sera yetu ya Elimu na Mafunzo ya 2014 inasema nchi yetu itatoa elimu ya lazima (compulsory education) miaka 10; na ndicho tulichosaini kwenye Sustainable Development Goal duniani, wakuu wa nchi wote walisaini. Na structure yake ni kwamba, tutakuwa six basic education, four secondary education. Kwa hiyo six plus four ni lazima kila mtoto asome pale. Halafu two high school three plus Chuo Kikuu, ndivyo Sera ilivyo, haijabadilishwa, ndiyo Sera iliyoko sasa hivi, haijabadilishwa. Tunachotekeleza sasa hivi, ni seven, four, two, three plus. Tunaposema tunafanya mapitio ya Sera, pamoja na mambo mengine tunataka kujiuliza, ile Sera ilivyokuwa tuitekeleze ilivyo? Kuna sababu ya kubadilisha? Economic necessity zake ni zipi, budgetary implication zake. Kwa hiyo kwenye timu inayofanya ile kazi kuna wachumi sasa hivi wanaangalia miundombinu yetu yote, human resource zetu zote tulizonazo na mfumo ambao tunataka kwenda nao kwa ajili ya kuangalia Sera yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Sera ipo ni six, four, two, three plus utekelezaji tofauti, ni seven four two three plus. Lazima tufanye maamuzi, hatuwezi kuwa na Sera hapa na utekelezaji hapa sera yetu lazima tufanye maamuzi na baadhi ya mambo mengine ambayo wameyazungumza hapa.

Mheshimiwa Spika, kwa uapnde wa Sera, hii ya structure ya elimu kama tukienda kwa sera ya elimu na mafunzo 2014, dhana yake, kama tukienda nasema maana maamuzi lazima yatafanyika, kama tukienda dhana yake basic education miaka sita, compulsory education miaka 10, basic education miaka sita punguza idadi ya masomo focus kwenye masomo ambayo wanafunzi wataeleza build strong foundation. Ukitoka pale wanafunzi kutakuwa na michepuo miwili wanaopenda vitabu sana na kusoma sana pengine asilimia 20 au wachache wataendelea huku watasoma trigonometrically complex number na kadhalika, na masomo mengi. Majority wataenda kwenye elimu ujuzi kwa miaka minne. Na watakapofanya mitihani masomo labda mawili, matatu manne, itakavyoamuliwa ndiyo watafanya chini ya NECTA; masomo mengine ni on the spot. Umejifunza ufundi magari, wiring, ya nyumba, uashi, useremala pengine, namna ya ku-repair ma-fridge na kadhalika utafanyiwa mtihani pale na mafundi wengine on the spot. Kwa hiyo utakapomaliza cheti chako cha miaka 10 kama ni kilimo unajua kilimo, kama ni kufuga wale nini aliosema Mheshimiwa pale wale wanaoliwa na kuku wale utafunzwa huko kama ni kufuga samaki na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo dhana iliyo kwenye elimu ya mafunzo ya 2014 ambayo kwa kiasi kikubwa imechukua mfumo wa Ujerumani wenzetu wa Zambia wanatekeleza something along those lines, kwa hiyo sisi lazima sasa tufanye maamuzi hatuwezi kuwa na Sera ikakaa kapuni halafu tukaenda kana kwamba hatukutunga Sera sisi wenyewe na Sera hii ilikuwa shirikishi sana lakini kama ambavyo nimesema sisi ni waumini wa utulivu kwa hiyo pamoja na kwamba kulikuwa na consultation tumeanza tena consultation na tunataka tuzimalize mwisho wa mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, pengine tuna kitu cha kutosha kwenda kwenye maamuzi lakini tunadhani haitatusaidia sana. Tuendelee na consultation; na naomba Wabunge waendelee kutoa maoni pamoja na ile semina ambayo tulikuwa tumeifanya, lakini tutakapoyafanya haya kwa kweli nawaambia yatakuwa ni mageuzi makubwa katika historia ya nchi yetu katika elimu ni mageuzi ambayo yataitikia wito na maelekezo ya Rais. Kwamba elimu yetu iongeze ujuzi. Ni mageuzi ambayo yatakidhi kiu ya Wabunge wetu; kwamba elimu yetu iongeze ujuzi. Ni mageuzi ambayo hayatatuondoa kwenye utandawazi; kwamba wanaotaka kwenda kuwa marubani wa ndege au wanaotaka kuwa madaktari bado kutakuwa na mrengo wa kwenda kufanya masomo hayo na kuyasoma vizuri sana ili kuweza ku-compete katika dunia. Kwa hiyo hatutapoteza chochote tutakachofanya ni kwamba wanafunzi wote watakapomaliza kusoma; kwanza watamaliza wakiwa miaka 15, 16, 17 ni umri ambao unaweza ukaanza kutafuta ajira sasa hivi wanamaliza miaka 13, 12, 14 ni umri hata kwa sheria za ILO huwezi kutarajia huyu mtoto aende akaajiriwe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili la kwanza, la Sera. La pili ni kuhusu Sheria. Huku kwenye Sheria bado tutakuja kujadiliana nanyi. Lakini mojawapo lazima tufunge, kuhakikisha kwamba utaratibu wa kubadilisha mambo usiwe wa ghafla ghafla katika sekta ya elimu kama ambavyo imesemwa hapa.

Mheshimiwa Spika, la tatu ni suala la mitaala. Kazi ya mitaala imeshafanyika na imeenda mbali sana. Na juzi wakati wa semina ya Wabunge, nawahakikishia takribani asilimia 98 ya maoni ya Wabunge tulishayapata, tulikuwa nayo. Na ndiyo nikashukuru kwamba niliwaambia wenzangu wataalam tusiende sisi na kueleza kwamba tuna nini tuweke chini tuwasikilize Waheshimiwa Wabunge tukawasikiliza tukawa tunafurahi tukasema inaonekana tuko on the right track; haiwezekani haya mambo tumeshayakusanya watu zaidi ya 100,000 wametoa maoni na Wabunge wakati fulani kulikuwa na semina ya kukusanya maoni hayo hayo; kwa hiyo tunayasikia hata baada ya one year down the road we have the same views. Kwa hiyo kwa kweli it seems we have a stable system ya kwenda kubadilisha mitaala.

Mheshimiwa Spika, lakini tunaendelea kukusanya maoni; na Waheshimiwa Wabunge tunaomba tuendelee; ukiwa na maoni njooni tuendelee kuangalia. Ikifika Desemba tunataka tuwe na tuna rasimu zetu za mitaala na tuna rasimu ya Sera. Januari mwakani tunataka tuanze kuingia kwenye maamuzi ili tuhakikishe kwamba baadhi ya haya mambo yanatekelezwa mapema 2024 kuelekea 2025. Na mitaala hiyo inaangalia sana suala la ujuzi. Kuna mambo mengi tunajiuliza, nasema lakini siyo maamuzi, tunajiuliza tuna shule shikizi sasa hivi kwani miaka minne mwanafunzi hawezi kuwekwa kwenye kituo shikizi? Kama kuna eneo lenye shughuli kubwa ya ufundi wakajifunza darasani kidogo wakafanya on the field wakapelekwa kwenye field for four years akitoka pale anakuwa amekamilika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunapozungumza kwenda kwenye michepuo mchepuo mwingine kwenye kilimo. Kwa nini tusitumie maeneo yetu na vyuo vyetu vya kilimo; akienda kukaa pale mtoto akajifunza kilimo, akajifunza uvuvi, akajifunza mifugo biology kidogo na kadhalika akitoka pale ameshakamilika? Lakini hatutoacha kufundisha yale mengine physics, chemistry, biology, additional mathematics, advance mathematics kwa wale wachache ambao wana attitude na ambao tunawahitaji kwa sababu nchi hii inahitaji engineer vile vile; kwa hiyo kwenda huko hatuta-compromise kwenye quality ila itatoa fursa kwa kila mtu kuchagua mrengo anaotaka kwenda unaoona unamnufaisha. Watakaoenda kwenye ujuzi lazima tuwape path way ya kwenda Chuo Kikuu. Kutakuwa wana masomo machache ambayo ukiyasoma na ukiamua kwamba unataka kuendelea basi chukua hayo hayo nenda high school au tumia utaratibu ambao umeelezwa hapa; nadhani Mheshimiwa Mbunge mmoja alikuwa anasema lazima tuwe na utaratibu wa kuandaa foundation course. Tumtengenezee mtu foundation course akitaka kwenda kuchukua degree aende kwa sababu bila ya hivyo baadhi ya wazazi watasema mtoto wangu lazima aende kwenye ma-physics na chemistry na biology na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, la nne ni idadi ya walimu, wakufunzi na Wahadhiri ambao limezungumzwa sana hapa hilo nalo muhimu hata ukiwa na mitaala mizuri hata ukiwa na sera nzuri usipokuwa na walimu wa kutosha na kadhalika. Humu ndani kuna suala la distribution. Ukichukua - Basic Education Statistic of Tanzania (BEST) ipo available, kaangalie tu pupil per teacher ratio, mwalimu mmoja na wanafunzi Kasulu 104, Kinondoni takriban 31, wote wanafanya mtihani ule ule. Uyui 74, sawa, ukienda Arusha 31, wote wanafanya mtihani huo huo na nchi hii ni moja na wote wana haki. Kwahiyo distribution ya walimu lazima itumike kwanza kwa kupunguza makali haya. Lakini na mengine kwa sababu ajira zinaendelea tunaamini tutaenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, la tano ni ubora. Unakuwa na mwalimu wanakuwa na Mhadhiri wanakuwa na Mkufunzi. wanahitajika ku-update knowledge wanahitajika kuwa na fursa ya ku-exchange wanahitajika kukutana pamoja kuongeza ubora na huko mbele kuangalia tunapo-recruit walimu tuna-recruit vipi. Kwa sasa hivi kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu sana tumetumia 2.1 bilioni kufanya semina katika maeneo maalum ya walimu. Tumefanya Tanga, Bagamoyo na Morogoro nchi nzima; na Morogoro nimeenda kufungua mafunzo hayo kwa walimu wa kilimo na sayansi kimu. Wanakusanywa tena, wanakaa kama darasani wanabadilishana idea na kuongeza ujuzi. Tumeweka tena kiasi hicho cha bajeti naomba Waheshimiwa Wabunge mpitishe bajeti hii kwa sasa tutakuwa tunaendelea na mfumo huu huu.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kushirikiana na TAMISEMI tunaimarisha sasa Teachers Resources Centers sehemu za walimu kwenda kukaa pamoja walimu wa hesabu wakae pamoja wapate na mtaalam wakae wa-update uwezo wao. Walimu wa kiingereza wakae wazungumze kiingereza kizungumzike maana yake kinafundishwa shuleni kwa hiyo tunaposema wanafunzi wana challenge ya kiingereza wakati tunafundisha maana yake ufundishaji wenyewe ndiyo challenge yenyewe, changamoto. Kwa hiyo huko tunakwenda lakini hata vyuo vikuu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia tu kwa vyuo vikuu sasa hivi tutaanza na ubora wa walimu. Tumesema tuwapeleke nje kwenda kusoma. Vyuo vikuu vyote duniani vinajaribu kupeleka watu mbali kwenda kusoma. Kachukue elimu hata China leta nchini mwako, hilo tunalifanya. Lakini lingine, tumesema, sasa hivi watu wanapanda vyeo kwa ku- publish kwenye journals ambazo hazitambuliki na haziko juu sana katika impact factor, hazikubaliki sana. Kwa hiyo tumesema kwa upande wa sayansi na tiba mwalimu wa Chuo Kikuu uki-publish kwenye journal top five zile kubwa ambazo zinafahamika ambazo mhadhiri wa pale aki-publish chuo kinapandishwa rank; wewe mwalimu ukiweza kufanya vile una milioni 50 cash una ondoka nazo na utazitumia unavyotaka.

Mheshimiwa Spika, tumetenga bilioni moja, na nina- challenge wahadhiri, hela hizo hapo bilioni moja tusije tukarudi nazo Bungeni mwakani. Tunataka tuone publication za Watanzania kwenye nature, kwenye landset, kwa sababu kule uta-publish kitu ambacho umekifanyia utafiti vizuri na kinaanza kuleta matokeo. Tumezungumza hapa, Mheshimiwa Abbas Tarimba umezungumza; tulikuwa na covid hapa, sasa tunataka hawa wafanyiwe research sasa hatutaki unafanya research unakimbilia kwenda kuangalia unafuga kuku halafu una daladala yako huwezi ku-concetrate. Unafanya research kwenye medicine ukifanya vizuri breakthrough milioni 50 cash mfukoni tumia unavyotaka. Tutaona inavyofanya ikifanya vizuri tutasonga mbele zaidi. Lakini tunaanzia hapa; South Africa uki-publish popote kwenye journal za juu unawekewa fedha kwenye akaunti yako kwa ajili ya kufanya research ku-recruit assistance na kusafiri sisi tunakupa cash tumia unavyotaka milioni 50.

Mheshimiwa Spika, lingine ni miundombinu. Ni kweli lakini Mheshimiwa Kipanga ameelezea kwamba tunahitaji kuendelea kuboresha miundombinu ya vyuo pamoja na shule zetu. Namshukuru tena Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwakweli maamuzi yake ya kusema kwamba fedha hizi zimekuja kwa ajili ya kupambana na UVIKO-19 na alisema Mbunge mmoja hapa tunaweza tukaondoa barakoa zote tukanunua na chanjo na kadhalika, tukasema tumefanya hivyo, na zipo nchi zimefanya hivyo, lakini alisema sisi tunataka kuondoa msongamano wa watu, kama tunataka kuondoa msongamano wa watu tuanzie shuleni, tujenge madarasa na wenye fedha zao wakaona kweli ni hoja nzuri, lakini dhana ya Rais wetu ilikuwa kwamba hizi fedha tutakapoziweka ziwe na impact long term zibaki. Kwa hiyo, hata COVID ikiisha tutabaki na madarasa yetu hiyo imetupeleka mbali sana.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuna miradi kadhaa katika Wizara yetu ya kuendeleza ujenzi na napenda kusema tu kwamba na maelekezo hayo mradi wa HEET ambao unajenga miundombinu kadhaa katika vyuo mbalimbali hapa nchini, Vyuo Vikuu mbalimbali 14 sasa tumetenga katika kila fedha, tutakuwa tunatenga kiasi fulani kijenge Kampasi katika Mkoa ambao sasa hivi hauna Chuo Kikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kampasi hiyo tunataka itumike for technical education isimamiwe na chuo for technical education, kwa sababu kilio chetu sasa hivi ni elimu ya ufundi tutaongea na ma-Vice Chancellor kwamba sawa hata kama ipo chini ya chuo chako basi itoe Diploma, au kitu kidogo pale ili watu wakitoka pale wameimarika vizuri wanaajirika. Kwa hiyo fedha hizo mazungumzo yamekubalika tunasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, tutakuwa na Mikoa mingi sana sasa hivi ambayo haijaonja level hiyo ya elimu nadhani naweza nikataja Rukwa hapa, nadhani Kigoma mingi tu Mheshimiwa Sanga, kwa hiyo huko tunapokwenda tutakwenda vizuri kwenye miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika yale mambo saba kuna vitendeakazi, Walimu wanaandaliwaje kwa ajili ya kwenda kufundisha. Dhana iliyokuwepo na Mheshimiwa Ndalichako mimi nakushukuru sana umeniacha pazuri, dhana iliyopo ni kuhakikisha sasa tunaenda na tablets kwa Walimu huko tunapokwenda, kwa sababu kila mmoja anazungumza TEHAMA hapa, tunazungumza mitaala maoni ni vilevile tufundishe vijana wetu coding. Tunasikia Kenya wame-adopt lakini humu tumeshaipata tayari na kama tunaenda vile ina maana lazima tuwe tumejiandaa na vitendeakazi, huwezi kumfundisha mtu mambo ya computer kwenye ubao wa chaki, uanze kumwambia hii ndiyo nini, kwa hiyo huko tunakwenda na nina matumaini huenda mambo hayo yakatekelezeka haraka sana kwasababu maelekezo hayo yamekubaliwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mambo hayo saba lazima ni muhimu tuende nayo yote bila kupuuza hata moja. Nimesema la kwanza sera, sera nimetaja kitu kimoja tu kuna mengine hapa yamezungumzwa lugha nini na kadhalika na hayo yote tutaenda kwa kushirikiana na watu halafu tuende tuamue.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili tunazungumzia sheria. Sheria hii pamoja na kubadilisha Sheria ya mwaka 1978 ni pamoja na kukazia baadhi ya maeneo tusiwe tunabadilisha kiurahisi sana, yaani tuwe na utaratibu mzuri wa kubadilisha mambo ili wakati wa kubadilisha tuwe kweli tuna improve mabadiliko lazima yatakuja mbele ya safari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimezungumza tatu ni mitaala, kazi ambayo imeshaanza takribani mwaka mzima, halafu nimesema tunahitaji idadi ya Walimu, ubora wa Walimu, miundombinu na vitendea kazi.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie baadhi ya vitu vingine haraka haraka, liliulizwa swali moja hapa labda ningependa nilielezee na Mheshimiwa Abbas Tarimba, aliuliza vyuo vikuu kazi yao ni kufanya research, na vyuo vikuu siyo High School, hatuwezi kufanya Wahadhiri wa vyuo vikuu kazi yao ni kufudisha tu haiwi tena Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kazi ya Vyuo Vikuu ni production of knowledge and dissemination of knowledge, siyo dissemination of knowledge ivumbuliwe kwingine wewe kazi yako hapa ni kuwapa wanafunzi.

Mheshimiwa Spika, Mhadhiri wa Chuo Kikuu, Mhadhiri wa Chuo Kikuu lazima afanye research, push to the front of knowledge. Kuna baadhi ya maeneo tulipowekeza kwenye research matokeo yake yamekuwa mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimetoka kilimo juzi hapa, tuna mbegu nyingi zilifanyiwa utafiti na TARI na ukienda Kongwa pale kulikuwa na mashamba, hata Mtama wa mbegu za kawaida hapa Mtama wa mbegu za masia, zimefanyiwa research na watalam wetu unaziona zinavyobeba tofauti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajua juzi hapa kwenye bajeti tulimwalika Researcher mmoja kutoka Zanzibar, alifanya research kuhusu mbegu bora za mpunga duniani anatambulika, alikuwa hapa amekaa na sisi, kwa hiyo kuwekeza kwenye research kunalipa.

Mheshimiwa Spika, tunayo chanjo ya kideri ni matokeo ya research na sasa hivi tunaweza tukaangalia katika tafiti kwa sababu sasa hivi wanakusanya zaidi za COSTECH lakini lazima twende beyond that, tuna miradi 145 ya tafiti ya kuangalia utafiti umeenda tumepata nini.

Mheshimiwa Spika, kinachohitajika huko tunapoenda lazima kwenye bajeti tuangalie Wahadhiri kuna bajeti ya research, Waheshimiwa Wabunge mmezungumza vizuri sana, kwamba sisi tusipoweka bajeti wafadhili ndio wataweka bajeti. Kulikuwa na mradi mkubwa sana wa research Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nakumbuka ulikuwa unaangalia dawa itokanayo na mitishamba, ulifadhiliwa na nchi moja ya Ulaya, matokeo yake yote yalikuwa yanachukuliwa kwenda Ulaya. Aliyekupa fedha ndiye mwenye haki miliki, walifanya research wapo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wenye taarifa zote wapo nje ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sisi lazima tutoe fedha, ndiyo maana nimesema leo nawaombeni sana, Waheshimiwa Wabunge mtupitishie bajeti yetu, hizo fedha kidogo za research ambazo tunawapa hawa ni stimulus package tutaomba na watu wengine watoe fedha kwenye research zitatusaidia Wahadhiri wakiwa Chuo Kikuu wasiwe na mambo mengi kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani wewe umeajiriwa kufanya research kwenye medicine ili baadaye likija janga lingine kama UVIKO uweze kututafutia dawa lakini huna fedha ya kutosha kazi yako ni kutafuta shamba Kiteto na kwenda kufuga ng’ombe, huku unakwenda kuwa na daladala na kuangalia miradi halafu hujui ukistaafu unakwendaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unakuta wako Maprofesa, tupo maprofesa publication zetu ukizitafuta uki-google huziona katika ma-journal ya hali ya juu lazima tubadilike! Kwa hiyo, naomba hiki kwa mfano Shilingi 50,000,000 kwa kila research ni hela ndogo, wenzangu walisema zitaisha Bilioni Moja, zinaweza zikabaki kwa sababu tumeshaanza na trend mbaya, naomba sana mtusaidie kupitisha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda jingine kwa muda uliobaki, maoni mengine kwa mfano Vyuo Vikuu tunaajiri vipi, una mwajiri mtu Chuo Kikuu vipi? Tunalipokea. Mimi niliajiriwa baada ya muda fulani kwenye Idara yangu unafanya mtihani matokeo yanatoka unaambiwa wewe tunakubakisha hapa unaendelea kufundisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo watu wengi Waafrika, Wachina, Wahindi wanakwenda kusoma Marekani na kadhalika, wanaonekana wanafanya vizuri sana ndiyo unaambiwa wewe tunakutaka ubaki hapa usiondoke, sasa na sisi lazima tujiulize maswali tunataka tuajiri vipi, kwa mkupuo, kutangaza tunachukua cohort moja, Wahadhiri nimepata fursa ya ajira niliambiwa nikasema kwa Vyuo Vikuu punguza idadi tunataka tuajiri taratibu kwa performance na hatutaki kuajiri cohort ambayo yote inakuja kustaafu wakati mmoja.

Mheshimiwa Spika, hivyo niliongea na Mheshimiwa Mhagama nikasema hivyo vingine sasa Vyuo Vikuu napenda yule aliyefanya vizuri wa 4.6 tumwajiri kipindi hichi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuwekeeni akiba mwakani ikija akifanya vizuri mwingine tumchukue na tusipomchukua akiondoka anaenda huko anapata kazi nyingine matokeo yake kumrudisha haiwezekani siku unapoajiri you don’t get the best, kwa hiyo hizi hoja tutazibeba tutazifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba Waheshimiwa Wabunge mpitishe bajeti yetu na naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii ya kuchangia na kutoa hoja.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kutoa shukrani zangu za dhati kwa Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kuzungumza na kwa maandishi, rekodi inaonesha tumepata michango jumla ya 51 na shukrani za kipekee nazipeleka kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo chini ya Mwenyekiti Mheshimiwa Profesa Kitila Alexander Mkumbo na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Husna Sekiboko. Michango yote ya Kamati tumeipokea mingi ni muhimu sana kwa asilimia kubwa tutayafanyia kazi na mahali tutakapohitaji kujadiliana tutajadiliana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla tunashukuru sana kwa kuungwa mkono kwa sehemu kubwa mno kwa hoja yetu hii tuliyoileta, kwa ushauri na maelekezo ambayo Waheshimiwa Wabunge wametupa, naomba niseme ahsanteni sana Waheshimiwa Wabunge na ahsante hizi ni kutoka kwangu na kutoka kwa wenzangu wote wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana mpitishe bajeti hii kama tulivyoomba. Kabla sijazungumza hoja na masuala mbalimbali ningependa kumshukuru sana kwanza Mheshimiwa Omari Kipanga, Naibu Waziri wa Wizara yetu na Katibu wetu Mkuu Profesa Nombo, Naibu Katibu Mkuu Profesa Mdoe, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Rwezimula pamoja na Kamishna wa Elimu Dokta Mtahabwa na watumishi wote wa Wizara na taasisi zote kwa kufanya kazi pamoja nasi, kwa sehemu kubwa na chochote ambacho tutakuwa tumefanikiwa kwa kweli ni kazi imefanyika kama team work. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niitumie fursa hii vilevile kuwashukuru wananchi wetu wa Rombo kwanza kwa kumuunga Rais wetu mkono, wanaendelea kumuunga mkono kwa asilimia kubwa sana. Wanaiunga mkono Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dokta Samia Suluhu Hassan na vile vile wanaendelea kuniunga mkono katika shughuli zangu za Ubunge na wanatambua kwamba muda mwingi nipo huku kwa shughuli za Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee sana naomba nikushukuru wewe na uongozi wote wa Bunge letu. Naibu Spika na Wenyeviti kwa kutuongoza vizuri sana katika shughuli hizi. Natoa shukrani zangu za dhati sana kwa Walimu wote, Wakufunzi na Wahadhiri hapa nchini na nadhani tuliwaleta wale walimu wanaofundisha kwa namna ya ubunifu na hamasa sijui kama wapo humu ndani. Sasa hivi clip zao zilikuwa zinatembea, labda wangesimama sijui kama mimi naruhusiwa kutambulisha watu lakini walimu hawa katika mazingira hayo hayo wako Mikoani wanafundisha kwa namna ambayo kwa kweli inatia hamasa unatamani ungerudi kuwa mtoto ufundishwe na walimu kama hawa, wako wengi lakini tumewaalika wawili hapa kwa kuwapa heshima na wengine tutaendelea kukutana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao wadau wengi wa elimu. Wadau wetu wa elimu kwa ujumla tunashukuru sana na wengine wako hapa, wengine ni local kwa mfano nadhani Meneja Mkazi Roselyn Marik wa ‘So they can Tanzania’ ambaye tunashirikiana nadhani yuko humu ndani vilevile tuko naye, na Rais wa Tanzania Academy of Sciences Profesa Yunus Mgaya ambaye nadhani yuko humu ndani. Wamiliki wa shule binafsi ambao kwa kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mulugo na ninakushukuru sana kulisema hili, nakushukuru sana kwa dhati ya moyo wangu, kwamba tumefanya nao kazi kwa karibu sana sekta binafsi, tumeshirikiana nao sana kama nitakavyoeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja zilizotoka hapa nyingi kama nilivyosema tutazibeba. Zipo hoja nyingine ambazo zinagusa sekta ya elimu zote lakini nyingine za TAMISEMI, nyingine Utumishi na kadhalika lakini zote zinagusa sekta ya elimu, nitajaribu kuzieleza zote nyingine tutazifanyia kazi ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kimsingi Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia wote kabisa wote kabisa wamempongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, wamempongeza sana kwa jinsi ambavyo ametoa kipaumbele kikubwa sana kwa ujasiri mkubwa sana kwa utashi mkubwa sana wa kisiasa kwa sekta yetu ya elimu kama ambavyo nitajaribu kueleza kidogo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaona kama alivyosema Naibu Waziri hapa VETA sasa hivi katika Wilaya 64 pamoja na mikoa, kumaliza wilaya zote ambazo hazina VETA. Mradi wa HEET Mikoa 14 inanufaika kupata kampasi za vyuo vikuu ambavyo vilikuwa hamna. Hakuna Mheshimiwa Mbunge yeyote hapa ambaye kwake katika jimbo lake hakuna shule mpya, madarasa mapya, pengine kampasi ya chuo kikuu, kuna VETA inajengwa na kadhalika. Hakuna Mheshimiwa Mbunge yeyote ambaye hana suala la elimu ambalo analo la kujivunia na kulisemea kwa wananchi na kwa sababu kwa kweli haya ni maelekezo specific ya Rais wetu Mheshimiwa Dokta Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Walimu, Walimu ndiyo watumishi walio wengi zaidi Serikalini, kwa walimu ujasiri wa Rais wetu kusema kwamba tuende kwenye sensa, tutumie vishkwambi ili vishikwambi hivyo vianze sasa kutumika katika kufundisha na vimegawanywa kwa walimu wote kabisa wote Tanzania Bara na Visiwani pamoja na Maafisa Elimu na wakufunzi wa vyuo vyetu vya FDC, VETA pamoja na Wadhibiti Ubora hapa nchini, yalikuwa maamuzi ya Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu wanafunzi wa vyuo vikuu, pamoja na kukutana uongozi wa wanafunzi wa vyuo vikuu kuwaongezea maslahi yao lakini ameendelea kuongeza fursa ya mikopo kubwa sana kwa wanafunzi wote. Kwa hiyo, kwa kweli ninaelewa kabisa ni kwa nini kila kila kila Mbunge aliyezungumza hapa bila kukosa na tumerekodi wote kila mmoja alianza kwa kusema tunampongeza na kumshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kubwa kuliko yote na ninadhani Mwenyekiti wetu wa Kamati Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo alilieleza vizuri sana. Kubwa kuliko yote ni maamuzi magumu ya Rais wetu kwamba tufanye mageuzi makubwa sana kwenye elimu, kwa kufanya mapitio ya sera na mabadiliko ya mitaala. Mageuzi haya yana gharama na mara nyingi ni rahisi sana kutafuta kitu ambacho matunda yake yanaonekana katika miaka miwili, mitatu, minne, mitano, lakini mageuzi haya ya elimu matunda yake halisi yataonekana kwa muda mrefu zaidi.

Mheshimiwa Spika, inahitaji utashi mkubwa sana wa kisiasa kuingiza Taifa katika maamuzi haya mazito, kufanya mabadiliko yatakuwa na gharama zake na matokeo yake makubwa yatakuja mbele ya safari. Kwa jambo hili kubwa hata mimi binafsi na yote aliyoyafanya Rais wetu, naungana na Waheshimiwa Wabunge wote kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa kweli mimi na wenzangu wote katika Wizara tunajisikia tuna bahati kubwa sana kupata fursa ya kuhudumu kipindi hiki ambacho Rais wetu ameelekeza jicho lake, ameelekeza maono yake katika sekta ya elimu.

Mheshimiwa Spika, chochote kitakachotokea hapa pengine wengine watatutaja mimi, wengine watamtaja Ndalichako kwa sababu tulikuwepo lakini yalikuwa ni maelekezo ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Rais tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana vilevile viongozi wetu Wakuu Mheshimiwa Dkt. Isdor Mpango, Mheshimiwa Dkt. ` Hussein Mwinyi kwa sababu suala la elimu kuna sehemu inaenda across the border na Rais wetu na kutupa miongozo mingi mizuri kutuwezesha kusonga mbele na Mawaziri wenzangu ambao tunafanya kazi vizuri kwa pamoja kumsaidia Rais wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo moja ambalo limezungumzwa kubwa sana ni kuhusu muingiliano na mgongano wa majukumu kati ya sekta ya elimu na TAMISEMI. Kamati imezungumza, nadhani Mheshimiwa Mulugo ndiyo amelifafanua zaidi specific maeneo ambayo yanaumiza na mapendekezo yametoka kwamba kuwe na chombo maalum cha kusimamia elimu nchi nzima au pengine elimu yote iwe chini ya Wizara moja na kadhalika. Sasa kuna suala la ugatuaji na suala la kuendesha ugatuaji kwa ufanisi nadhani suala linahitaji mjadala.

Mheshimiwa Spika, suala la kuwa na chombo cha kusimamia elimu ni pendekezo ambalo nadhani limeletwa katika mapitio ya sera na ninajua tutapata fursa Waheshimiwa Wabunge wote kupitia mapitio hayo na kulizungumza, vilevile tukumbuke kwamba ugatuaji wa madaraka una sababu zake, msingi wake na umuhimu wake.

Mheshimiwa Spika, nitalizungumza suala moja ambalo lilizungumzwa hapa na Mheshimiwa Mulugo. Tunajua kwamba TAMISEMI inamiliki shule kama ambavyo BAKWATA inamiliki shule, Baraza la Maaskofu linamiliki shule, sekta binafsi zinamiliki shule. Wizara ya Elimu iko pale inasimamia sera, sheria na kadhalika. Kama ambavyo Waziri wa Kilimo anaweza asiwe na mashamba lakini kuna watu wana mashamba na kuna mashamba mengine ya Serikali mengine ya watu binafsi anamiliki pale.

Mheshimiwa Spika, sasa changamoto moja aliyoisema Mheshimiwa Mulugo na ninaitolea utatuzi hapa hapa ni kwa TAMISEMI kuchukua wakati mwingine jukumu la kutoa amri kwa shule binafsi kwamba sasa kuna mitihani wote lazima mfanye, lazima mfanye leo, keshokutwa mfanye na mlipie. Nimeongea na Kamishna wa Elimu kwa sababu na mimi naheshimu mamlaka yake japokuwa mimi ni Waziri na ameniambia atatoa tamko, maelekezo kuanzia sasa hivi, kuanzia leo shule binafsi hazitalazimishwa kufanya mitihani ambayo inapangwa na Halmashauri na kadhalika kwa amri na kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahimiza zishiriki kwa hiari kufanya mitihani hiyo lakini hazitolazimishwa kufanya mitihani, taratibu za mitihani na kadhalika zinatolewa na Kamishna wa Elimu kwa mujibu wa Sheria yetu ya Elimu ambayo ipo, nadhani hilo tunaweza tukalimaliza. Yako mambo mengine chungu mzima ya ufanisi tu kati ya TAMISEMI na Wizara ya Elimu kwa sababu na tunafanya kazi vizuri sana kwa kweli na nadhani tutaendelea kufanya hivyo lakini suala la mitihani Kamishna ameniambia atalileta, tutaliona, tutalimaliza kwa namna hiyo. Mengine tutaendelea kuyajadili katika sera na sheria.

Mheshimiwa Spika, wengi wamezungumzia sana kuhusu mapitio ya sera na mitaala. Mmoja alisema kwanza tuanze kubadilisha sheria. Kimsingi sheria inatokana na sera. Ni vigumu sana kubadilisha sheria ya mwaka 1978 sasa hivi ya elimu kabla ya kubadilisha sera. Kwa mfano, sera ya mwaka 1978 ndiyo inasema elimu ya lazima ni miaka saba. Huwezi kwenda kubadilisha sheria kwanza ukasema kwamba sasa sheria iseme elimu ya lazima miaka 10 bila kuwa na sera inayosema elimu ya lazima ni miaka 10. Nawahakikishia na mtakumbuka mwaka jana wakati nilivyokuja hapa mbele yenu kwenye Bunge lako Tukufu, nilieleza kwamba kuna mambo saba ambayo tutakuwa tunayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nilisema ni sera, nikasema mitaala, nikazungumzia sheria, nikazungumzia idadi ya walimu, nikazungumzia ubora wa walimu, nikazungumzia miundombinu, nikazungumzia vitendea kazi na kadhalika. Vitu saba tuliweka kwenye bajeti ambavyo bado tunavifanyia kazi. Kwa hiyo, suala la sheria litakuja tukishamaliza tu sera hii, kuna masuala chungu nzima ambayo itabidi tuende tukabadilishe kwenye Sheria ya Elimu ya Mwaka 1978, ama kuifumua yote upya au kufanya mabadiliko kulingana na jinsi ambavyo sera itakuwa imepita.

Mheshimiwa Spika, kadhalika mitaala, kwa kawaida mitaala mingi inapita Waheshimiwa Wabunge haiji Bungeni, haiji kujadiliwa hapa. Sasa hivi tumeileta hapa kwa sababu mitaala hii inaendana na structure mpya ya sera ambalo ni jambo kubwa sana, hatuwezi kulibeba wenyewe tu kama Wizara na kwenda nalo. Kwa hiyo, naona tumeleta tutakapopeleka hata cabinet paper itakuwa na mapitio ya sera na itakuwa addendum ya mitaala jambo ambalo mara nyingi linamalizwa kwenye taasisi ya elimu tu huko nyuma tulivyokuwa tunakwenda. Kwa hiyo, ndivyo ambavyo tutakuwa tunakwenda katika kufanya hilo.

Mheshimiwa Spika, sasa yako masuala chungu mzima yamezungumzwa hapa kuhusu mapitio ya sera. Pengine nisingependa niyajibu yote, kwa sababu gani? Tuliomba na ulitupa ruhusa tukafanya semina kwa Waheshimiwa Wabunge, tukawapitisha kwenye mapitio ya sera na mitaala, lakini tulifanya wakati wa break baada ya kukutana asubuhi halafu tulikuwa turudi mchana. Wabunge wengi wakasema; najua Mwenyekiti wa Kamati ambaye alikuwa ana-chair pale, akasema atakuona, kwamba ni vizuri tutafute siku ya weekend, tuwe na kutwa nzima ya kupitia mapitio ya mitaala tuliyoyafanya pamoja na sera hiyo ili tuweze kupata maoni kamili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baadhi ya maoni niliyokuwa nayasikia hapa kwa kweli, naamini kwa sababu kumekuwa hakuna muda wa kutosha kupitia, na tutaomba tupate kibali hicho hapa tunavyoendelea, na ninaomba sana tuweze kupata kabla ya tarehe 31 Mei, 2023.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, pamoja na kwamba tutaomba tuwapitishe tupate maoni yenu, kwa sababu tunaamini sana nyie ni wawakilishi wa wananchi wote wa Tanzania, lakini hata mwenye maoni tutaendelea kuyapokea, kwa sababu baada ya kufanya kongamano lile kubwa tulitangaza hadharani makusudi ili kuchochea watu wengi zaidi walete maoni, na watu wengi sana walifuatilia na wengi wanaendelea kuleta maoni. Tunaendelea kupokea maoni. Tunatarajia kwamba tukifika tarehe 31 Mei, 2023, kwa kweli kila mtu atakuwa ameshaleta maoni yake, tutayachakata na kuandaa cabinet paper kwenda kupata approval kwa Mheshimiwa Rais kupitia washauri wake ambao ni Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata baada ya mambo tuliyoyazungumza hapa, japokuwa nitayazungumza tena kidogo, kwa mfano suala la lugha, bado kuna fursa ya kutoa maoni, kuyaleta na kuona namna ambavyo tunaweza tukayachakua. Nitafafanua kidogo kuhusu suala la lugha, lakini umuhimu wake ndiyo huo, bado safari ya kukusanya maoni ipo. Ilianza mapema wakati Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako akiwa Waziri wa Elimu, tumeendelea nayo. Ndiyo maana nasema haya mageuzi ni makubwa sana, na hatufanyi kwa kukurupuka.

Mheshimiwa Spika, kuna suala limezungumzwa sana kuhusiana na sera na sheria, kwamba sasa hii sheria mkifanya, kuna uhaba wa walimu na uhaba wa miundombinu. Hatuwezi kukataa ukweli wa uhaba mahali ulipo, takwimu zenyewe zipo. Tuna kitabu kinaitwa Basic Education Statistics of Tanzania, kiko hadharani, kila mtu anaweza akaangalia. Pupil Teacher’s Ratio katika kila Halmashauri ni kiasi gani? Ni facts ambazo tunazo na sisi Wabunge tunafahamu maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, upo upungufu tunaweza tukaukiri, lakini shukrani zote tulizompa Mheshimiwa Rais hapa ni kwa sababu speed ya kuongeza miundombinu mashuleni sasa hivi wote tumeiona. Kwa kasi hii, tunatarajia kwamba tunaweza tukaendelea na safari hii ya mageuzi tunayoyafanya wakati tuna-catch up na miundombinu. Tunaona jitihada za Rais wetu sasa hivi za kuanza kuajiri. Ujue kwamba ajira ilikuwa frozen kwa muda fulani ambayo inaleta changamoto kidogo kwa sababu kuna watu wengi walimaliza shule hawajaweza kuajiriwa, lakini tunaona kwa kuangalia budgetary implication jitihada za kuajiri zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, zaidi niseme vilevile kuna suala limezungumzwa hapa la mwongozo, Mheshimiwa mmoja alisema hapa, mwongozo wa walimu wa kujitolea. Wiki hii tunautoa na tumeanza kuzungumza na watu ambao wanaweza wakatusaidia kuhakikisha kwamba kweli, tunaweza kuhakikisha kwamba hawa wanaweza wakatusaidia kufundisha. Tutatumia teknolojia vilevile kuhakikisha kwamba tunapambana na uhaba huu wa walimu. Kuna mambo mengi sana tunaweza tukayafanya wakati ambapo Serikali inaangalia budgetary implication inaongeza ajira za walimu, nasi tutajitahidi kufanya hivyo hivyo. Hii ni pamoja kwa wakufunzi na Wahariri wa Vyuo Vikuu.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi unaweza kuona kuna Mhadhiri wa Econometrics, yuko Dar es Salaam anafundisha darasa la UDOM. Tumefanya hivyo, najua nilivyokuwa nafundisha pale, watu wanafundisha kwa zoom, unafundisha watu wako Ghana, unafundisha kutokea Dar es Salaam. Nadhani tunaweza tukajitahidi hivyo kwenda mbele. Hata hivyo, Rais wetu kwa mwendo anaoenda nao, tunaamini kwamba tunaweza tukasogea mbele kuhakikisha kwamba tutapata hivyo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine kubwa ambalo limezungumzwa sana ni tahadhari, kwamba mageuzi haya tumejiandaa vipi? Tunaendaje kutekeleza mageuzi haya? Yupo Mheshimiwa mmoja, nadhani ni Mheshimiwa Shigongo kama sikosei, alisema, tusijadili sana, dunia inaenda kwa kasi sana. Tutakuwa na mitaala, kabla haijatekelezwa utakuta tumeshapitwa na wakati. Wako wengine nadhani Mheshimiwa Tabasam alisema, tuwe tahadhari. Alitupa historia sana ya mageuzi ya mitaala tangu wakati wa Ujerumani mpaka sasa hivi. Kwa hiyo, haya yote ni muhimu, kwenda kwa kasi ili tusichelewe na kuchukua tahadhari ili tusiboronge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kalenda ile ya utekelezaji ambayo tuliileta kwenye semina kwenu, tulisema kwamba mwezi Januari mwakani tunaanza na pilot. Tunaishi kwa matumaini kwamba kwa kweli pendekezo letu litapita, rasimu hizi zitakubaliwa, iwe ni sera ya elimu na mafunzo 2014, Toleo la 2023 na mitaala yake itapita. Sisi tumeamua tunaanza kidogo kidogo mafunzo ya amali kwa sababu tunataka mafunzo ya amali tusiharibu. Hatutaki anayekwenda kwenye mafunzo ya amali ajisikie ni failure. Hatutaki kujenga mazingira ya mwanafunzi ambaye angependa kwenda upande wa mkondo wa mafunzo ya amali, aone kwamba kila mtu atamwona ni failure. Ndiyo maana tumeweka pathway ya mikondo yote miwili.

Mheshimiwa Spika, ukienda elimu jumla unaweza ukaenda mafunzo ya amali baadaye, ukienda mkondo wa mafunzo ya amali, utapunguza masomo, lakini bado kuna pathway ya kwenda high school na kwenda chuo kikuu kama kawaida. Tunataka tuhakikishe kwamba wote wanajisikia ni Watanzania bila kubaguliwa. Tutajenga mkakati baadaye wa namna ya kuwashauri wanafunzi kwamba wewe umefika Darasa la Sita, tunadhani itatusaidia sana, wewe unapenda sana michezo ukichukua masomo yako manne, matano halafu ukaenda Shule ya Michezo A-Level, utaenda mbali sana kwenye michezo, lakini unaweza ukaenda Chuo Kikuu kupitia yale masomo machache ambayo unachukua, halafu baadaye ukaenda ukafanya Diploma ukaendelea. Kadhalika mwingine anaweza kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa tulichofanya, tumechagua shule ambazo ni prestigious. Zamani kila mtu anajua tuliosoma enzi hizo, kwamba walikuwa wanaenda zile shule zilikuwa zinaitwa Tanga Tech., Ifunda Tech., Bwiru Boys Tech., Moshi Tech., ndio wale waliofanya vizuri sana darasani. Tena uwe mzuri sana kwenye hesabu, lakini yale mafunzo ya amali, ukisoma form one ukiingia form two unapata cheti. Hata ungeacha shule, unaweza ukaajiriwa kwa sababu una cheti. Ukifika form five unapata cheti cha level fulani unaondoka.

Mheshimiwa Spika, sasa tumeamua kwamba sisi tunaanza na vyuo vya ufundi vile tisa. Tumeweka bajeti hii ambayo tunaomba muipitishe sasa hivi, ili vyuo vifuatavyo tunaenda kuviwekea miundombinu. Tunavifahamu, tumevikagua ili mwezi Januari vichukue wanafunzi, waanze mwaka wa kwanza kwa mitaala mipya ambapo watakuwa na masomo machache ya elimu jumla. Watafanya shughuli nyingi zaidi ambazo ni mafunzo ya amali, wakimaliza pale, ni full technician, wako very qualified, wanaweza wakaajiriwa, lakini wakitaka, wanaweza kwenda kwenye diploma, wakitaka yale masomo machache wanaweza wakaenda high school. Shule hizo ni Bwiru, Chato, Ifunda, Iyunga, Moshi, Mtwara, Musoma, Mwadui na Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda niseme, hapa yuko mdau, nilimtaja Rose Mariki makusudi kabisa ambaye alitusaidia sana kujenga chuo kule Babati, wamesema na wenyewe wanataka kuweka hela kuhakikisha kwamba tunaweza tukaanza shule ya mafunzo ya amali. Sekta binafsi pia, wengine wameshajitolea sasa hivi wanasema tuko tayari. Sijui kama naweza nikawataja, walisema tuko tayari, tupate maelekezo na mitaala hiyo na sisi tuhakikishe na sisi tuna shule zetu za mafunzo ya amali ambazo zinafuata mitaala yetu, halafu tunasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaanza kwa pilot, lakini tunavyoenda kufanikiwa, tutasonga mbele. Zaidi ya hapo, tunaanza na walimu. Tumetenga bajeti. Kwenye bajeti hii ambayo tunaipitisha sasa hivi, tumetenga bajeti za kuandaa walimu wa kwenda kufundisha. Tunaangalia shule za ufundi, zina walimu, lakini hawatoshi, kwa hiyo, tunafanya juhudi za kuwafundisha lakini training, re-training, and re-orienting kwa walimu wetu itakuwa ni kazi kubwa sana mbele yetu kwa sababu baada ya document hizi kupita ambazo nadhani baadhi ya Wabunge walisema ni one of the best kwa kweli, tunaweza tukaharibu kama tusipokuwa na very good management ya process ya implementation. Kwa hiyo, tunakwenda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie kidogo suala la lugha kwa sababu limeleta mjadala hapa. Kwanza niseme, hatujafunga mjadala, hatujafunga maoni, kwa hiyo, siyo uala la kusema kwamba tumeshapitisha. Zile zinaitwa rasimu na tumesema maoni mpaka tarehe 31 Mei tutapokea maoni. Tuna semina ya Wabunge inayokuja na kuna nafasi ya kuzungumza sana.

Mheshimiwa Spika, kwenye lugha kuna vitu viwili ambavyo vimefanyika ambavyo ni vizuri sana tuvione. Kwanza, kwenye sera yenyewe imetoa fursa ambayo ipo sasa hivi, kwamba ukitaka kuanzisha shule yako hii iwe english medium ambayo ni primary, wakati huo itakuwa kuanzia elimu ya awali mpaka darasa la sita, unaomba kibali maalum, unakaguliwa, umejiandaaje, unaweza ukapata. Ukifika form one kwenda juu ni Kiingereza, ila ukitaka form one kwenda juu kufundisha Kiswahili, unaomba kibali maalum, ukaguliwe kama umejiandaaje. Kama umejiandaa vizuri unaweza kufundisha unaendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, hatuwezi sisi kama Taifa tukasema tumefungia Kiswahili, lakini najua mwendo wa kwenda kwenye Kiswahili utakwenda kwa tahadhari kubwa hata wazazi wengi, kama alivyosema Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, kwa tahadhari kubwa kwa sababu tutapenda kuhakikisha kwamba kweli tunapokwenda kule hatutashusha kiwango cha elimu. Milango iko wazi, nasi kama Serikali tutajitahidi kuhakikisha kwamba hata watakaokwenda kule, kweli wakatoe elimu ya viwango. Kwa hiyo, hilo lipo.

Mheshimiwa Spika, la pili ambalo tumelifanya kubwa, na maoni yametolewa na Mheshimiwa Husna, na Mheshimiwa wakati unaongea nilijua ulisoma document thoroughly, kwa hiyo, nilikuwa very excited wakati unaongea. Kwa sababu ufundishaji wa lugha umebadilishwa kwenye mitaala, na ninaomba msome mitaala hiyo. Hatufundishi tena sijui syntax, sijui nini; rules nyingi sana, halafu unamaliza darasa la saba huongei Kiingereza. Unafundishwa Kiingereza cha kuongea, ukimaliza darasa la saba ni aibu uanze kusoma Kiingereza, unamaliza huwezi kuongea, darasa la saba. Kadhalika unamaliza darasa la saba, unaboronga Kiswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, hata tunaposema kwamba vijana wetu wanamaliza darasa la saba sasa hivi hawaongei Kiingereza, ina maana ufundishaji wetu hauendi vizuri. Kwa hiyo, tumefanya mapitio, tutumie wataalam wa lugha, ufundishaji huu uache kukazia rules ambazo ni so boring, mwanafunzi hajui kama anajifunza lugha, ajifunze straight namna ya ku-communicate na kuongea, kwa sababu watu wanajifunza Kimasai, wanajifunza Kiusukuma, wanajifunza Kinyakyusa, wanaelewa ndani ya miaka mitatu. Utakaaje shuleni miaka minne unajifunza Kiingereza utoke huwezi kuongea Kiingereza chenyewe!

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, sasa hivi somo la Kiingereza litaanzia darasa la kwanza. Litafundishwa kama somo moja na tutahakikisha kwamba ukimaliza Darasa la Sita, kweli uweze kuongea Kiingereza. Hizo rules zitakwenda tu kwa sababu huko mbele ya safari tutazungumza suala la communication na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa alipokuwa anazungumza hapa, kwa kweli na mitaala iko huko. Nakuomba usome, kama kuna comments zaidi tutazipokea na comments nyingine kutoka kwa watu wote mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Kiswahili, kwa sababu tusije tukadhani kwamba watu wanaongea Kiswahili fasaha kwa Tanzania. Kwa sababu tunasema kwamba tuongee Kiingereza fasaha, Kiswahili chenyewe tunaboranga. Sikilizeni tu watu wanapoongea, hata tafsiri tu na lafudhi na kadhalika, ni vitu ambavyo lazima shuleni tujaribu kuviimarisha na kuvifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumze suala lingine; je, Serikali inaona sekta binafsi ni washindani? Yaani shule binafsi ni washindani wa Serikali? Narudia tena, yaani Wizara inaona shule binafsi, vyuo binafsi ni washindani? Never, hapana, haijawahi kutokea, haitatokea na haiwezi kutokea chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, na haitatokea baadaye. Hii ni Serikali ya wananchi na hizi shule zinafundisha Watanzania.

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi, bosi wangu alikuwa Mheshimiwa Charles Mwijage, alikuwa Waziri wangu, ndio aliniagiza tutengeneze blueprint ya kuimarisha sekta binafsi. Tulifanya kazi hiyo, siyo kwa sababu nilielekezwa na bosi wangu, we had passion ya kusimamia na kuendeleza sekta binafsi. Blueprint mpaka sasa hivi inazungumziwa. Haiwezekani leo, mimi binafsi kwa mfano, niko Wizara ya Elimu halafu nianze kufanya kazi dhidi ya sekta binafsi. Hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shule binafsi pamoja na vyuo vikuu vimekuwa msaada mkubwa sana Tanzania, na nadhani Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, sikumbuki nani alisema hili. Tulikuwa tunaona watoto wetu wadogo wanaondoka wanaenda kusoma Kenya na Uganda. Leo mabasi shule zikifunguliwa, huoni wanakwenda, shule zimetufuata nyumbani. Tunazifurahia, tutazilinda, tutazitetea. Narudia tena Mheshimiwa Mulugo kwa kusema ukweli hapa, kwamba tumekutana mara nyingi sana na kuongea. Kwa kweli ndiyo mwendo wetu, na tutakwenda kufanya kazi hivyo hivyo mbele ya safari. Tutakaa pamoja na tutaendelea.

Mheshimiwa Spika, niwaambieni ukweli maelekezo ya Rais wetu. Hivi vyuo binafsi, tumetenga hela kwa vyuo binafsi kuwasomeshea wahadhiri wao. Mara ya kwanza Serikali inatoa hela kwenda kusoma. Wataenda kusoma Wahadhiri binafsi South Africa. Unalipiwa na Serikali kwa sababu unafundisha chuo binafsi. Kwa hiyo, Serikali hii haioni kabisa sekta binafsi kama ni wapinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi tulipokutana mara ya mwisho, alikuwa Mwenyekiti wa Wamiliki wa Shule, alisema kitu kimoja, na nitakirudia, kwamba na sisi sekta binafsi tusaidiane na Serikali, kwa mfano katika kupambana na wizi wa mitihani. Tusionekane sisi tunalalama kwamba Serikali kwa nini tunapambana na wizi wa mitihani, na sisi tusaidiane kupambana na wizi wa mitihani. Yeye mwenyewe ni owner wa shule akasema, mimi binafsi niligundua nilikuwa natoa motisha kwa walimu wanaofanya vizuri wakawa wana- organize wizi wa mitihani, nimechukua hatua. Hiyo ilitoka sekta binafsi yenyewe. Kwa sababu sisi tunapopambana na wizi wa mitihani, hatupambani na sekta binafsi wala sekta ya umma.

Mheshimiwa Spika, sisi tuliofanya mapitio ya mitaala katika mikutano yetu yote kabisa, tumekuwa tukiita sekta binafsi, wamiliki wa shule, walimu kutoka sekta binafsi, wote wameshiriki na ukweli wametoa mchango mkubwa sana hapa. Sasa vitu vingine ambavyo vimesemwa kwamba pengine ni dalili kwamba sisi tunapambana na sekta binafsi. Hili sikutarajia nitatoa tena maelezo. Ranking of schools, ooh mmeondoa kumi bora kwa sababu hamzipendi shule binafsi. Nilieleza vizuri hapa, lakini sasa niulize swali, kwamba ooh, mmeondoa ushindani, kwa hiyo, shule zetu zitaboronga. Ushindani gani tumeondoa?

Mheshimiwa Spika, bado tunatoa A, tunatoa B, tunatoa C, si ushindani huo! Tunatoa first class, second class na tunatangaza, si ushindani huo? Samia Scholarship, unapewa kulingana na performance yako na watu wanatangaza, si ushindani huo! Kwenye Samia scholarship wako wanafunzi wametoka private sector ambao wamepata Samia scholarship, si ushindani huo! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachosema sisi, ushindani lazima tutegemee kigezo kinachokubalika. Sisi tunashindanisha wanafunzi waliosoma masomo ya science na tumewapa full scholarship ambayo sisi Wizara ndio tumeamua iitwe Samia Scholarship. Tunaangalia wame-perform vipi na tunakutaja. Tumesema hivi kuhimiza watu washindane, kwa sababu wanafunzi wamekaa kwenye mtihani wa physics, wanafanya mtihani huo wa physics wote wanakwenda.

Mheshimiwa Spika, kushindanisha shule ni tofauti na kushindanisha wanafunzi. Kwani Kenya haipendi private sector! Mbona imefuta kutoa best school kwa kutegemea vigezo vya mitihani? Uganda je? UK je? Sasa sidhani kama nina haja ya kurudia tena maelezo tuliosema. Tunachosema, tutaangalia vigezo bora vya kushindanisha shule, siyo vigezo vya kusema kwamba wewe tu kwa sababu wanafunzi wanafanya vizuri sana, wewe ni shule bora.

Mheshimiwa Spika, nilitoa mfano mdogo sana hapa, na nirudie tena, hivi shule ambayo imechukua wanafunzi wenye C, C, D, halafu wale wanafunzi wakatoka wote A; na shule nyingine imechukua wanafunzi wote A, wakatoka wote A, wewe unadhani shule gani ni bora? Je, mnafahamu kuna shule zina matawi mawili; moja huku, anayefeli anahamishwa kwa nguvu, mzazi hapewi choice. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtoto ameugua, tunatarajia shule sasa imlee, imsaidie, badala ya kumsaidia, inamtoa ili wabaki kupata A. Ushindani huo hauna afya sana, lakini wanaotaka kutangaza, matokeo yako hadharani. Serikali haiwezi yenyewe ikasema hii shule bora kwa vigezo ambavyo wanataaluma wamevikataa, na machapisho yako mengi, na nchi nyingi zimeacha.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema ni kwamba, Association of Private School Owners, wakitaka kusema haya, wasituweke sisi, matokeo tunatoa hadharani. Sidhani kama nina sababu ya kuelezea hili. Kwa nini watu wanadhani hii ni kupambana na private sector? Kwa hiyo, hizi nchi ambazo kwa kweli ndiyo private sector, zimekubuhu, wameacha. Sasa watu wanawahitaji. Sisi hatuwezi kupambana na private sector kwa sababu hiyo. Hata kidogo, na hatuna sababu ya kufanya vile.

Mheshimiwa Spika, tunafurahi wanapofanya vizuri, na ndiyo maana Samia Scholarship wapo watu walisema, angalia watu waliosoma private wasipate. No! Tumesema tunataka wanafunzi waliofanya vizuri waje wawe madaktari wazuri sana, waje wawe ma-engineer wazuri sana. Kwa hiyo, haijalishi wametoka wapi? Wametoka wengine Feza School, wametoka private schools, wameenda mpaka Samia Scholarship kwa mashindano hayo. Kwa hiyo, mashindano hatujayakataa, kabisa, naombeni dhana hiyo tuache.

Mheshimiwa Spika, lingine ni mitihani. Kwa nini Olympio kulikuwa na wizi wa mitihani hamkufungia shule kama kituo cha mitihani, lakini shule binafsi mnakuwa na haraka sana ya kufungia? Cha kwanza, wanafunzi wote wanaohusika na wizi na udanganyifu wa mitihani, tunafuta matokeo. Haijalishi anatoka shule ya umma au binafsi. Nyaraka zinaonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shule inayofungiwa kuwa kituo cha mitihani, ni shule ambayo tumeona kulikuwa na organized effort ya ku-cheat ndani ya shule. Mfumo wa kitaasisi wa kufanya udanganyifu, sio mwanafunzi mmoja mmoja. Hata shule binafsi ambazo unakuta mwanafunzi mmoja mmoja ame-cheat hatuzifungii. Nitatoa mifano miwili, mmoja mnaufahamu. Iko shule moja mlisikia binti mmoja analalamika, mimi namba yangu ya mtihani nilibadilishiwa, nikawa nalalamika hawataki. Mtihani wa kwanza, wa pili, wa tatu, wa nne. Ule wa mwisho ndiyo wakatubadilishia namba, wakarudisha ile namba yangu ya mwanzo, halafu akaitwa na walimu wote wakaambiwa msiseme kilichotokea.

Mheshimiwa Spika, tusingejua kama yule binti asingetoa taarifa. Siyo jamani! Alivyotoa taarifa, tukachunguza, tukagundua ni ukweli. Hiyo shule ilikuwa one of ten best at some point. Shule hiyo nadhani iliongoza kwenye mkoa, ikawa one of the best.

Mheshimiwa Spika, siyo kwamba mwanafunzi ame- cheat, lakini walimu wameshirikiana, wamebadilisha namba za mitihani, wamempa huyu na huyu, for whatever reasons, halafu baadaye wanabadilisha, halafu wanaita wanafunzi wanaambiwa msiseme.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hata watumishi wa umma walikuwepo tumewachukulia hatua na wale wa nani tumewachukulia hatua alafu tumefunga kama kituo, sasa hiyo tumefunga kwa sababu ya kuchukia private sector.

Mheshimiwa Spika, mfano mwingine iko shule mwanafuzi kaingia na simu, hairusiwi lakini ame–manage kuingia na simu, ameingia kwenye mtihani akawa anapiga picha maswali halafu amemtumia mwenye shule halafu mwenye shule nje akapanga watu wa ku–solve matokeo. Sasa huyo tuna mtetea private sector mtakuwa mnafanya kazi nzuri sana, msitetee hiyo private sector msitetee hiyo, kwa sababu private sector inafanya kazi nzuri sana. Hawa wachache wanaweza waka tarnish image huo ni mfano lakini kwani private sector tu tunakwenda?

Mheshimiwa Spika, hapa navyozungumza wako watumishi Shinyanga wako ndani, alikuwa Afisa Elimu kwanza alihamishwa haraka haraka akakimbia nadhani akapelekwa Tukuyu tumemfuata, tumemdaka, tumemrudisha yupo mahabusu kwa reason tu organized. Wako polisi, wako ndani, kwani polisi ni private sector? Afisa Elimu ni private sector? Na sisi tuna deal zaidi kwa nguvu kubwa zaidi na Maafisa wetu ambao tunagundua wanaiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hao ambao tumewakuta, tuliwakutaje? Mtihani umeibiwa Serengeti, kwa kufungua mtihani mapema kwa kufanya mchezo kupiga picha, umetumwa kwenye simu Kahama. Sasa hamuwezi kujua system tuliyonayo sasa hivi ukiiba mtihani rahisi sana kukudaka, Kahama watu wamedakwa simu zimekamatwa, tumeangalia zimetoka wapi? Tumekwenda kule tumegundua, polisi aliyehusika kulinda mtihani hao wako ndani, Afisa Elimu yuko ndani na hili hawa ni Maafisa wa Serikali walikuwa wanafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, isihusishe vita dhidi ya private sector nakuombeni sana. Kwa nini tufanye vita dhidi ya private sector? Kwa nini? Kwa hiyo, Olympio hatukupata mfumo wa kitaasisi wa wizi ni kweli, walikuwa wana–cheat wamepatikana, wamefutiwa matokeo kama ambavyo kuna shule za private ambazo tumekuta watu wame–cheat zikafutiwa matokeo. Shule moja ya Mwanza ilichukua muda kabla ya kuiondoa kama kituo cha mitihani kwa sababu tulikuwa tunafanya uchunguzi.

Mheshimiwa Spika, kwa hilo nilipenda nilizungumze sana, kwa sababu nisingependa private sector ione kama tuna pambana nayo ili iweje? Lakini wizi wa mitihani hakuna mtu atakae vumilia mahali popote kabisa. Tushikamane private sector na public sector tushikamane, tupambane na wizi wa mitihani. Then shule hizi za private ni nzuri sana, nyingine wala hazifanyi mtihani wa NECTA ndiyo wanachukua mtihani wa Cambridge wanafanya. Kwa hiyo, tushikamane jamani namna wanafanya kazi nzuri na mimi I can promise na Rais wetu, kwa sababu Rais wetu kwanza yuko hivyo hatuwezi kupambana na shule binafsi hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ningependa nilizungumze labda niseme tu mambo mengine ambayo kwa kweli ni operational nadhani alikuwa Mheshimiwa Tabasam alizungumza hapa kuhusu wananchi wamejiunga, wamejenga shule zao, wamemaliza karibu wamekamilisha wanaomba usajili halafu sisi hiyo lazima niseme sisi kwa sababu mimi nachukua jukumu. Tunakwenda pale tunasema haa hapa kimepunguka maabara kwa hiyo, hatutoi usajili.

Mheshimiwa Spika, tumeishakubaliana wale wananchi ambao wameishajipanga wamefanya kazi imebaki kitu kidogo sana baada ya sisi kukatalia usajili tunapeleka hela tunamalizia shule, shule isajiliwe ianze kufundisha wanafunzi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Tabasamu na wengine wote katika mazingira hayo na tukifanya hivyo tutaimiza wananchi maana yake hamuwezi kuwaambia wananchi hebu changieni tena, tukifika mahali Serikali itakuja itatushika mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuacha kusajili shule kwa sababu haina maabara tu, haina kichomea taka na kadhalika lakini tuna Taasisi yetu ya Elimu na Mamlaka ya Elimu ambayo kwa kweli tunaweza tukai–direct bwana peleka kule kwa sababu wananchi wameisha pambana na tuone na tushafanya hivyo naomba hilo twende nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala jingine lilizungumzwa na baadhi ya Waheshimiwa nadhani suala la recognition power learning actually ukisoma Sera ndiyo utapenda zaidi. Ipo sasa hivi lakini, ipo ilikuwa inafanya chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ipo vijana wapo mtaani wanafanya shughuli zao, VETA wana wa–trace, wanawafatilia, wanasimamia, wana–observe vizuri wanakuja wanawapa cheti kwamba kwakweli wewe uwe fundi magari ni mzuri sana cheti hiki ili uweze hata kufanya kazi hata za Serikali ipo sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kwenye Sera kuna utaratibu nyumbufu, mzuri zaidi wa kuwawezesha watu kupata kila kitu na hata ile nadhani alisema Mheshimiwa Kishimba, kuwafundisha vijana sijui house girl na kadhalika lakini iko kwenye hospitality ukarimu, ukarimu unafundishwa kutandika kitanda, kupiga pasi, kupika chakula na kadhalika, kufagia nyumba na vitu vyote vile ambavyo ni muhimu lakini tunachohitaji tumefanya tracer study kuangalia wanafunzi wetu waliyotoka kwenye vyuo vyetu wanakubalika vipi? Ili tuweze kubadilisha mitaala kazi yetu kubwa ni kuimarisha tunavyo fundisha kule ili kila mtu aone kweli hawa wanafaa kwa cheti kile waweze kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jingine kubwa niliseme mabweni chini ya darasa la tano. Waraka wa kamshina unasemaje? Unasema kama mwongozo wa 2020 unavyosema yeyote haruhusiwi kuanzisha mabweni chini ya darasa la tano bila kibali maalum cha kamshina. Kama huna hicho kibali maalum, ulipewa deadline ambayo tu baada ya kukaa na private sector tumesogeza tunaongeza jitihada za kukagua.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mtoto elimu ya awali siyo kwamba anaenda shuleni tu, hata kwenda choo kujisaidia nini care yake ni kubwa zaidi ni more vulnerable. Kwa hiyo, lazima ukaguzi wake na vigezo vyake view vikubwa zaidi, tunatambua kwamba kuna mahitaji lakin vilevile tuna wajibu sasa sisi tukishatoa kibali kitakachotokea kule tutaulizwa sisi na sasa hivi tunafanya utafiti wa kuangalia ni namna gani ya kubana zaidi kuhakikisha kwamba kwakweli wale watoto wanalindwa lakini kwa kibali maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekutana na private sector tukasema na wapo wenye vibali, tukasema mnaendelea lakini tutawakagua, tutawakagua kuhakikisha kwamba kweli hawa watoto wanakuwa well taken care of na tuna– encourage zaidi watoto wakae na familia lakini tunatambua wako yatima wamechukuliwa na vituo mbalimbali, wako wengine walikuwa nao hawana vibali wamekuja wametuletea document tumewapeleka kwa kamishna. Peleka timu kubwa ika kague kule kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hawa yatima wanakuwa supported wataondoka wataenda wapi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo tunalijua lakini walioko huko very clear na maneno yako vilevile bila kibali maalumu cha kamishna haijasema hairuhusiwi. Kwa hiyo, kibali chake ni kigumu kuliko kuanzisha bweni tunaomba tu mtusapoti kwenye hilo na tutafanya kazi vigezo hivyo na private sector kuhakikisha kwamba ni vigezo ambavyo kweli vinaleta na. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la mwisho, mwisho hapa kuna hoja nzuri sana ya vyuo vikuu imezungumzwa sana hapa Mheshimiwa Profesa Ndakidemi, Mheshimiwa Dkt. Chamuriho na Mheshimiwa Profesa Muhongo wamezungumza vizuri sana, vyuo vyetu kuhusu sasa hapo ndiyo rank ipo, unataka ku–rank vipi? Hatu–rank vyuo vikuu kwa matokeo ya darasani. Vyuo Vikuu vina heshimika kwa utafiti, namba moja na utafiti mzuri ni mwalimu mzuri.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana Bunge lako Tukufu lilipitisha fedha shilingi 50,000,000. Kwa muhadhiri yeyote, sasa hivi tunaanza na wahadhiri watakao fanya kazi kwenye natural science au medicine waka–publish kile alichosema Mheshimiwa Profesa Muhongo kwenye high impact factor journal na mwenyekiti wa kamati ya kuweka mwongozo ni Profesa Yunus Mgaya ambaye tuko nae hapa nae ni mtafiti.

Mheshimiwa Spika, akifanya akipata anaondoka na kitita cha milioni 50. Mwanzoni niliona watu wanasema kwa nini usi–support local journals Mheshimiwa Profesa Muhongo amezungumza vizuri sana namshukuru sana, sasa hilo linaeleweka. Hatuwezi kuleana hapa kuanzisha journal na kupandishana vyeo tutakuwa ni kichekesho, unaweza ukaitwa profesa hapa nchini ukienda nje ukikutana na watu wanavyoongea unawaambia msaidizi hebu usinite profesa hapa mpaka nirudi nyumbani, kwa sababu hapa nitahadhirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka maprofesa wetu wapande na ushindani wa kimataifa na tunataka kama ambavyo tungependa wachezaji wetu wa mpira kama wale wa simba na wale wengine waweze kucheza kimataifa wakubalike. Tunataka wote Simba na Yanga, wote tunataka wahadhiri wetu wachapishe kwenye ma–journal hayo huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuta ku–reward kwa kuchapisha huko na yako nje kwa sasa hivi, wenzetu wame catch up kwa kuanzia huko leo India wana journal nzuri sana lakini walianza kuchapisha huko. Kwa hiyo, siyo matumizi mabaya ya fedha, kwa hiyo, fedha mlipitisha Waheshimiwa Wabunge, nawashukuru sana, muongozo tunao nadhani tarehe Katibu Mkuu atatangaza na tutatangaza lini tutatoa tuzo hiyo kwa wale ambao wamechapisha kule na imehamasisha sana utafiti wetu kufanya vile.

Mheshimiwa Spika, nakadhalika tumefanya kitu kingine ambacho ni kikubwa kwenye Tuzo ya Mwalimu Nyerere ambapo na Waheshimiwa mlitoa hela. Tumefanya, tumeshangaa, Miswada iliyokuja mingi kweli kweli washapewa. Namba moja amepewa milioni 10 na Miswada ile inaenda sasa kwa wachapishaji itachapishwa na kuhamasisha publish industry hapa nchini unaweza kushangaa hata tuna vitabu vyetu, nexty tutaongeza na vitabu vya watoto tusiwe kama watu wa kubana tu, kubana tu vitabu lakini tunahimiza uandishi wa vitabu vile tulivyosoma wagaga gigi koku lakini tuwe na vitabu vya kisasa hivi vinavyo changasha watu.

Mheshimiwa Spika, lingine na hili litakuwa la mwisho kabla ya kengele ya pili. Kuhusu English Medium, yako mengine mengi lakini sikujipanga kuyajibu yote labda yaulizwe, English medium kamishna anaporuhusu kwamba umeenda halmashauri umeomba shule hii iwe English medium hasemi kwamba kachaji watu. Shule za Serikali hazichaji ni free, free ni elimu bila ada kuifanya English Medium hakukupi wewe kibali cha kuleta ada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hayo ya ada nimeuliza kidogo yanakuja kwenye Baraza la Madiwani ambapo sisi wote ni madiwani, hebu twende tukaangalie tunafanya hivyo kwa sababu gani? Kwa sababu kwakweli tunahitaji kwenda na mwongozo wa Serikali kwamba shule za Serikali zitoe elimu bila ada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda wako, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii na mimi ya kuchangia Hotuba hii ya Bajeti Kuu ya Serikali. Naomba nitangulie kusema naiunga mkono 100% na ni matumaini yangu kwamba Wabunge wote kabisa tutaunga mkono hoja hii ya Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwanza kwa kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa mapendekezo mazuri sana yaliyoko kwenye Bajeti Kuu pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Hamad Hassan Chande, Katibu Mkuu Dkt. Natu, Naibu Makatibu Wakuu, Kamishna wa Bajeti na wengine wote kwa sababu wameleta mapendekezo mazuri na nitazungumzia kidogo kwenye Sekta ya Elimu na baadaye nitajibu hoja moja tu iliyotolewa ambayo ni kubwa kwenye suala la elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote hawa katika maandalizi yao kwa kweli wamejitahidi sana kulenga yale maono ya Mheshimiwa Rais aliyoyaelekeza na kama tunavyoona katika Bajeti na kama alivyosema Mheshimiwa Waziri hapa kuna vipaumbele ambavyo Mheshimiwa Rais aliviweka. Elimu ni kati ya kipaumbele kikubwa sana cha Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa hilo kwa kweli nadhani tumpongeze sana Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua ni rahisi sana kutafuta vitu ambavyo matokeo yake unayaona sasa hivi lakini katika mageuzi ya elimu kama nitakavyosema hapo baadaye matokeo yake huwezi kuyaona mapema. Wanasema kwamba a politician focuses on the next election; a state man focuses on the next generation. Rais wetu anaangalia na vizazi vijavyo kwa jinsi ambavyo ameamua kuwekeza katika elimu. Baadhi ya matokeo ya mageuzi haya yatakuja wakati 2030 ameshamaliza urais wake amepumzika na matunda yake yataonekana mbele ya safari. Kwa kweli Rais wetu lazima tumpongeze sana kwa maono yake haya na hii Bajeti kwa kweli inazingatia maelekezo ya Rais wetu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba nakushukuru na kukupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitataja baadhi ya maeneo ambayo wote tunajua. Tunafahamu na wote tumesikia elimu bila ada. Kuna baadhi ya watu wanadhani ile ada ni ndogo sana na wengine wanadhani kwamba pengine kuondoa ada kuna madhara katika elimu lakini tukumbuke tulivyoanza tu Serikali ilivyoanza kuondoa ada kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne, tulishangaa wanafunzi waliosajiliwa mashuleni idadi iliongezeka kwa ghafla sana kuonyesha kwamba kumbe tulikuwa tunaacha baadhi ya wanafunzi wanashindwa kwenda shuleni kwa sababu ya ada hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alivyoingia madarakani mara moja aliamua kuongeza elimu bila ada kwenda form five na form six na vilevile kuondoa ile ada ya mitihani ambayo kwa kweli inanufaisha familia nyingi ambazo vinginevyo baadhi ya wazazi walikuwa wanajaribu kushawishi watoto kwamba jitahidi usifaulu sana kwa sababu sina hela za kukupeleka shuleni. Tunamshukuru sana Rais wetu na tunashukuru sana Waziri wa Fedha kwa kutekeleza maagizo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengine tunajua kwa mfano, ongezeko la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. Tunajua kwamba wakati Mheshimiwa Rais alivyoingia alikuta ni shilingi bilioni 464. Hakuacha nyongeza iende progressively, jump kubwa imeshafanyika sasa hivi mikopo ya elimu ya juu imefikia shilingi bilioni 731. Hilo ni ongezeko kubwa sana lakini zaidi ya hapo katika bajeti hii inabeba ongezeko la fedha ambazo wanafunzi wanazipata kwa siku kutoka shilingi 8,500 mpaka shilingi 10,000 na haya yalikuwa maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Rasi baada ya kukutana na uongozi wa wanafunzi wa elimu ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kingine ambacho kinaonekana ni fedha kidogo sana, Samia Scholarship. Mnakumbuka wakati tulivyokuja hapa mwaka jana kuomba fedha hapa tuliomba tutenge fedha kwa ajili ya kutoa scholarship kwa wanafunzi wanaofanya mtihani wa form six kupitia Baraza la Mitihani wafaulu vizuri sana kwenye masomo ya sayansi na wakubali kwenda kusoma sayansi (engineering au medicine). Mliipitisha Waheshimiwa Wabunge hapa tumeiweka ile sisi baadaye Wizarani tukasema tuiite Samia Scholarship. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni shilingi bilioni tatu tulipitisha mara ya kwanza na sasa hivi tumetengewa tena fedha nyingine. Kwa hakika imetushangaza jinsi ambavyo wanafunzi sasa hivi wanaonyesha mwamko mkubwa wa kusoma masomo ya sayansi na Taifa haliwezi kuendelea bila kuwekeza katika sayansi, teknolojia na ubunifu. Kwa hiyo, hata hilo nashukuru sana Waziri wa Fedha kwa sababu maelekezo ya kutoa fedha hizi kwa ajili ya scholarship yalikuwa maelekezo ya Rais wetu. Kuiita Samia scholarship tuliamua sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hii ni Bajeti ambayo inaenda kutekeleza kazi ya ujenzi wa zile kampasi mpya za vyuo vikuu katika maeneo chungu mzima ambayo yalikuwaga hayana kampasi ya vyuo vikuu. Mikoa kama Tabora, mahali kama Singida, sehemu kama Tanga. Mikoa yote hiyo sasa hivi itaenda kuwa na kampasi za vyuo vikuu, tunaenda kutekeleza ujenzi wa vyuo vikuu 14, mchakato unaenda vizuri sana. Kuna mchakato mrefu kidogo katika taratibu hizi na World Bank lakini tunaenda vizuri na utekelezaji wake umebebwa na Bajeti hii ndiyo maana naomba sote tuiunge mkono na tuiunge mkono kwa 100%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Bajeti hii inayotusaidia kwenda kuendeleza ujenzi wa vyuo vya VETA ambavyo tunavijenga katika nchi nzima katika takribani wilaya 64 pamoja na Chuo cha VETA cha Mkoa wa Songwe. Najua Wabunge wengi wote ni wanufaika wanafahamu ujenzi unaoendelea kule sasa hivi na Waziri wetu wa Fedha kwanza mwaka jana alipewa maelekezo na Rais wetu tena baada ya Bajeti ya Wizara ya Elimu kwamba hebu kaongeze ujenzi wa vyuo vya VETA na sasa hivi ametenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huo. Tunampongeza sana Waziri wetu huyu kwa kutekeleza maelekezo ya Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona katika Bajeti hii, kilio kikubwa kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba tuanze kuwaangalia wanafunzi wanaoenda vyuo vya kati ambavyo tunasema vinatoa elimu ya amali (mafunzo ya kazi moja kwa moja) ili wanafunzi wengi waweze kumudu kwenda kusoma kule. Waziri wa Fedha ametenga fedha kwa kuondoa ada katika baadhi ya course wanafunzi wanaotoka kidato cha nne kwenda kusoma DIT, kusoma Arusha Technical, na MUST. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wanaweza wakaenda kusoma kule bila ada tunapongeza sana Wizara ya fedha na mnaelekezwa na Rais wetu ni mwendelezo wa kukuza elimu ya amali ambao wako katika moyo wa mageuzi ya elimu na kadhalika. Kuanzisha programu ya kutoa mikopo sasa kwa vyuo kadhaa vya kati ambavyo ni ubunifu mwingine umeletwa na Wizara yetu ya Fedha kutekeleza maelekezo ya Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda kusema, kwa upande wa mageuzi ya elimu bajeti hii vilevile imebeba bajeti ya kuanza safari ya mageuzi ambayo tumekuwa tukiyajadili hapa. Mageuzi haya kama mnavyofahamu yalikuwa ni maelekezo mahususi ya Rais wetu. Alivyoapishwa tu, nadhani wakati alifanya mabadiliko kidogo katika Baraza la Mawaziri, alianza kuelezea anachotaka kuona katika elimu. Siku ile alikuwa anapitia wizara moja hadi nyingine, wakati huo Mheshimiwa Profesa Ndalichako alikuwa Waziri wa Elimu alisema hapa Wizara ya Elimu nataka nione mageuzi ya elimu, mitaala na bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ndalichako ananiona pale kazi hiyo inatekelezwa. Kwa hiyo watu wakisikia tunamsifu Rais wetu wajue tunamsifu hata wenyewe wanaweza waka-verify. Maelekezo mengine hamuyasikii wote lakini haya yalisemwa hadharani na alikuja akaahidi hapa Bungeni kwamba Serikali anayoiongoza itafanya mageuzi makubwa. Bajeti hii itatuanzishia safari hiyo, kwa hiyo naombeni sana tuiunge mkono kwa asilimia 100 utekelezaji wa mageuzi hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa labda niseme kitu kimoja na hili suala lililetwa na Mheshimiwa Janejelly James kuhusu wanafunzi wanaorudi kutoka nchi ambazo zina matatizo ya vita. Wanafunzi waliotoka Ukraine kwa sababu ya vita kati ya Ukraine na Urusi na wanafunzi wanaotoka Sudani kwa sababu ya machafuko ya hali ya hewa. Nitangulie kusema nchi yetu imebaki ya amani hili tulikumbuke siku zote, tunapoona changamoto hizo, wanafunzi wanarudi hapa wanatafuta mahali pa kusoma, tukumbuke vilevile nchi yetu ina amani na amani hii inatokana na jinsi tunavyoendesha siasa zetu, kwa ustarabu, kwa kuheshimiana, kwa kuunga mkono viongozi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa alichouliza Mheshimiwa Janejelly James ilikuwa ni kwamba sasa tumeona wanafunzi chungu mzima wameenda Muhimbili kutoka Sudan. Wale wa Ukraine vipi? Kwa nini wale hawajapata fursa ya kujiunga na vyuo vikuu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitolee maelezo kidogo jambo hili na Watanzania wengine wote wasikie. Wanafunzi waliokuwa wanasoma Ukraine, baadhi yao, si wote, waliomba kujiunga na vyuo vyetu na utaratibu unaoitwa credit counselor ukafanyika. Baadhi yao wameweza kujiunga na vyuo vyetu, si wote. Kwa sababu utaratibu wa kuhamisha masomo unayosoma Chuo Kikuu kimoja kuja chuo kikuu cha ndani unasimamiwa na TCU. Kuna vigezo vingi sana vinaangaliwa baadhi yao ya wale walioomba walienda kusoma Ukraine wamejiunga na vyuo vyetu na sio wote walioomba kuja huku. Kwa wale waliotoka Sudan mpaka sasa hivi hakuna hata mmoja ameweza kujiunga na chuo chetu. Mchakato unaendelea najua kesho kuna vikao vinaanza kwa wale ambao wanataka kujiunga na vyuo vyetu ili tuangalie utaratibu wa credit transfer waweze kuhamisha masomo yao kutoka Sudan kuja hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale walioonekana kwenye picha walipokelewa na Profesa Janabi Hospitali ya Muhimbili sio MUHAS. MUHAS Vise Chancellor anaitwa Profesa Pembe. Wale wanafunzi waliotoka University of Medical Science and Technology Sudan; wameshasoma miaka mitano wamekuja kwa ajili ya clinical trial kwa ajili ya clinical training na huu ni utaratibu. Tumepokea wote wanafunzi kutoka Zimbabwe ambao wamemaliza masomo yao ya medicine wanakuja hapa kuomba kufanya kazi kwenye hospitali zetu wapate certification halafu wanaenda ku-graduate kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wanafunzi tuliowaona wameenda Muhimbili tunawatakia kila la heri tunafurahi wamekuja nchini kwetu, watafanya clinical training hapa Tanzania, na watakapomaliza watarudi kwenda kuhitimu kwenye vyuo vyao. Hao wengine walioomba tutajitahidi kwa kadri ya uwezo wetu. Tungependa wote tuweze kuwa- integrate of course kuna changamoto. Kuna wengine kuna criteria zilizotumika kuwa-admit katika vyuo vyao kule sio criteria ambazo sisi tunatumia kuwa-admit wanafunzi huku. Kwa hiyo ni changamoto ambayo TCU inafanya. Najua kutakuwa na vikao kushirikiana na Wizara ya Elimu ya Zanzibar na kwetu na TCU kuona kwa wale wanaotaka kujiunga na vyuo vyetu tutatumia utaratibu gani. Kwa hiyo mpaka sasa hivi kwa kweli hatujaweza kuwachukua wale wanafunzi lakini navyojua nina taarifa kwamba kuanzia kesho kuna vikao vitaanza kuona namna ya kuwa- integrate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalize hapo narudia tena naunga mkono hoja hii ya Waziri wa Fedha na naomba wote tuiunge mkono asilimia 100, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa fursa hii kwanza naomba nisimame kumshukuru sana Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Husna Sekiboko na Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima na wajumbe wote wa Kamati kwa taarifa nzuri na kwa usimamizi mzuri wa Sekta yetu ya Elimu kwa kutuongoza na kutusimamia vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa sababu kazi kubwa iliyo mbele yetu sasa hivi ni mageuzi makubwa ya elimu. Wamesimama kidete na sisi na wamekuwa wakiuliza maswali mapendekezo kutufuatilia mpaka hapa tulipofika. Kwenye hili la mageuzi ya elimu niseme mambo machache kwanza. Moja, hii ilikuwa ni ahadi ya Rais wetu Mheshimwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliiotoa hapa Bungeni kwa Watanzania kwamba Serikali yake italeta mageuzi makubwa ya elimu kukidhi matakwa ambayo yapo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hiyo imefanyika na imeanza na Mheshimiwa Profesa Ndalichako na tumeendelea nayo hadi sasa hivi. Tunayo sera sasa hivi inayotuongozo na tuna mitaala mipya. Nataka tu kuotoa taarifa kwamba tumeendesha mafunzo kwa zaidi ya walimu 10,000 kwa ajili ya mitaala mipya na tumepeleka mafunzo kwenye kata zote hapa nchini kwa ajili ya mitaala mipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati ambao tunaufanya ni utekelezaji kwa awamu kwa sababu tulijua na haya mapendekezo ya wajumbe wengine na Wabunge kwamba tukifanya kila kitu kwa mkupuo tunaweza tukajikuta hatutekelezi kwa ufanisi mkubwa. kwa maana hiyo tuliamua kwamba mitaala mipya inaanza kwa elimu ya awali, darasa la kwanza, darasa la tatu, kidato cha kwanza kwa mafunzo ya amali ambapo mpaka sasa hivi ni shule 96 zinatekeleza mafunzo ya amali na baadae tutakuwa na kidato cha tano na mafunzo ya uwalimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo si kwamba madarasa yote yanatekeleza mitaala mipya tutakwenda taratibu tukifika Mwaka 2027 tutakuwa tumefika turning point ya utekelezaji huo lakini mafunzo yanaendelea vizuri yanakwenda kwa walimu wote na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme vile vile kwamba kupitia Bunge lako Tukufu na hasa kwa Kamati yetu Serikali imewekeza sana katika miundombinu ambayo ni muhimu sana katika mageuzi. Sitaweza kusema yote, natoa mfano tu; kupiti mradi wetu wa Higher Education for Economic Transformation, HEET, sasa hivi mikoa ifuatayo kwa mara ya kwanza kabisa itapata kampus ya vyuo vikuu. Naanza na Kagera ambapo Mheshimiwa Mwijage amesema tumepeleka elimu ambapo inastahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mikoa hiyo ni pamoja na Kagera, Shinyanga, Simiyu, Mwanza, Lindi, Manyara, Ruvuma, Njombe, narudia tena Njombe, Singida, Kigoma, Katavi, Rukwa, Tabora, Tanga na Mtwara. Vilevile tunakaribia kutoa tangazo kwa maalum kwa Mtwara. Hayo yote ni maelekezo ya Rais wetu na usimamizi wa Bunge lako tukufu kwamba tutekeleze yale yote ambayo Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliahidi akaagiza tuyatekeleze. Yajayo yanafurahisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika, na kama ilivyosemwa hapa sasa hivi tunaendelea na juhudi za kujenga vyuo vya VETA kwa wilaya zote 64 ambazo sasa hivi hazina vyuo vya VETA. Ujenzi huo unaendelea, na kupitia Wizara yetu ya Fedha najua tutakuwa tunapata fedha kwa speed inayotakiwa ili tuweze kukamilisha ujenzi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kumalizia ujenzi wa VETA ya Mkoa wa Songwe ambao ndiyo mkoa pekee ambao tulikuwa hatujaanza ujenzi wa VETA kwa ajili ya mkoa huo tutakuwa tumekamilisha kila kitu katika shule zote. Kazi kubwa itakuwa ni hiyo ambayo mapendekezo ya Kamati na Waheshimiwa Wabunge kwamba tuhakikishe tuna wakufunzi na vifaa vya kufanyia kazi katika vyuo vyote. Serikali imejipanga vizuri tutahakikisha kwamba tunatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa sasa hivi napenda kutaja tu baadhi ya taasisi ambazo zinasaidia kwa mfano, NBC Bank na KCB Bank. Wao wameamua kumuunga mkono Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha kwamba si tu wanatoa ufadhili kwa wanafunzi kusoma kwenye vyuo vya VETA klakini wanawaandaa kwa ajili ya kuwa wajasiriamali. Kwa hiyo kila mmoja ambaye anapata ufadhili wa NBC Bank au KCB Bank anaenda anasoma VETA akitoka pale anasaidiwa yeye mwenyewe kuanzisha shughuli zake kwa kupewa, kama alivyosema Mheshimiwa mmoja hapa, mtaji mbegu na usimamizi ili elimu aliyoipata iweze kumsaidia siyo tu kujiajiri lakini vilevile kuongeza ajira kwa wengine hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imezungumzia suala la kuongeza bajeti ya elimu ya juu na kwa Wizara kwa ujumla wake. Ni vizuri wakati tunazungumzia hilo ambalo ni muhimu sana vilevile tuone muelekeo wa kibajeti ambao umekuwepo kwa sababu ni vizuri tukatoa maua panapostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2019/2020 bajeti ya mikopo ya elimu ya juu ilikuwa ni shilingi bilioni 450, 2019/2020 bajeti hiyo ikaongezeka kidogo kufikia shilingi bilioni 464. Alivyoingia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na mmesikia hapa Bungeni, aliagiza kwamba haridhiki na ongezeko hili. Akaagiza tuongeze kwa kiasi kikubwa sana mpaka kufikia shilingi bilioni 570, hiyo ilikuwa 2021/2022 na hivyo sasa hivi bajeti kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu ni shilingi bilioni 738.7.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vyovyote vile hakuna mtu anayesema bajeti inatosha lakini cha muhimu ni kwamba kwanza kwa maelekezo ya Rais wetu kwa kweli tumekuwa tukiongeza bajeti vizuri sana. Kazi iliyopo kwetu sisi ni kuhakikisha kwamba tunapambana kuhakikisha wale ambao wamepata mikopo warejeshe. Hatua mbalimbali zinafanyika ikiwa ni pamoja na kushirikiana na mifumo mbalimbali kama NIDA kuhakikisha kwamba tunamtambua nani amepata mkopo na vilevile kutangaza ambao wanadaiwa ili kama ameajiriwa kwenye sekta isiyo rasmi watu wajue by naming and shaming kwamba rudisha fedha watoto wa Tanzania wengine wasome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi limesemwa hapa na ni vizuri Watanzania wajue. Kupitia mapendekezo ya Kamati yetu na kwa kibali na maelekezo ya Rais wetu sasa hivi tumeanza kutoa mikopo kwa vyuo vya kati. Tumeanza na shilingi milioni 48 na tumechagua maeneo yale ambayo kwa kweli Serikali ikitangaza ajira tunakosa wataalam. Kwa hiyo tuna uhakika hawa tunaowapa mkopo sasa hivi wakimaliza watapata ajira na watarudisha fedha hizo kwa ajili ya kuweza kuwapa watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la Samia Scholarship. Ndiyo, kama ilivyopendekezwa tuongeze bajeti lakini vilevile tupeleke maua panapostahili. Tulianza na shilingi bilioni tatu na sasa hivi tuna shilingi bilioni 6.7.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya Samia Scholarship ilitokana na maelekezo ya Rais wetu kwamba hebu wale vijana wanaosoma sayansi ambao wamefaulu vizuri sana, ambao ni vizuri tuhakikishe kwamba wakienda vyuo vikuu wanasoma mambo ya TEHAMA, hisabati, sayansi, uhandisi na elimu tiba hebu tuwape ufadhili wa asilimia 100 ili kuwashawishi waende huko, ili kile ambacho Profesa Muhongo alikuwa anasema kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaandaa wataalam wa big data, machine learning, block chain, artificial intelligence tuweze kufikia kwa kasi tuweke fedha hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tulipewa maelekezo, Wizara tukakaa tukasema kwa sababu ni maelekezo ya Rais wetu tutaita Samia Scholarship. Fedha zinaongezeka lakini tunazipeleka kwa wale ambao wamefaulu vizuri sana katika masomo ya sayansi kwa masharti kwamba watakwenda vyuo vikuu kuendelea kusoma sayansi, hisabati, TEHAMA, uhandisi au elimu tiba. Kwa hiyo, hata kama tunaona kwamba kiasi hiki ni kidogo tukipiganie kiongezeke lakini basis yake ndiyo hiyo, sababu ni kuendeleza masomo ya sayansi; kati ya hatua kadhaa; tunaona muda ni mfupi; ambapo tunachukua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda umeisha malizia.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda umeisha nakushukuru sana. Naomba kusema moja tu, la mwisho ambalo linaleta taharuki kidogo kuhusu maji katika Chuo Kikuu cha Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Aweso yuko hapa, tuliwasilana naye mara ya kwanza akapeleka wataalam kule, tulivyoona mambo hayaendi kwa kasi tukawasiliana naye, amekwenda mwenyewe pale, amebadilisha mfumo na ametuhakikishia kwamba tutapambana kuhakikisha kwamba UDOM inapata maji ya kutosha. Naomba tumpe Mheshimiwa Aweso maua yake. Nashukuru sana. (Makofi)