Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Nashon William Bidyanguze (17 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, na mimi naomba nichangie hotuba ya Mheshimiwa Rais zote mbili, lakini pia naomba nichukue nafasi hii kwanza niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini kwa kunileta Bungeni kwa kura nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba niseme na niungane na wananchi wengine ambao wanasema kwamba Rais Magufuli ni chaguo la Mungu na ni kweli Rais Magufuli ni chaguo la Mungu. (Makofi)

Mimi kwenye Jimbo langu eneo kubwa ni eneo la maji, lakini Mheshimiwa Rais amekubali kukarabati meli ya Mv Liemba. Hivi sasa imeanza kukarabatiwa, lakini Mheshimiwa Rais siyo hivyo tu amekubali kutengeneza meli mbili moja itabeba watu na mizigo yao, lakini moja itabeba mizigo peke yake. Jimbo langu ni wahanga wa usafiri wa maji kwa maana hiyo wanatumia usafiri wa mitungwi ambayo inatumia mbao, kwa maana hiyo kumekuwa na ajali nyingi sana, lakini meli hizi zikitengenezwa zikikamilika tutakuwa wananchi wa Kigoma Kusini tumepata ufumbuzi na watu watasafiri kwa raha mstarehe kwa maana kutakuwa hakuna ajali lakini pia watasafirisha mizigo yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wakati anapita jimboni kunadi sera za Chama cha Mapinduzi kuomba kura na kuniombea kura mimi alikubali kuongeza zahanati, kuongeza Hospitali ya Wilaya nyingine kwa maana Jimbo langu ni kubwa sana katika majimbo ya Mkoa wa Kigoma, alikubali kuongeza hospitali nyingine ya Wilaya maana yake mimi nakwenda kuwa na hospitali mbili za Wilaya ni jambo la kumshukuru sana Mheshimiwa Rais katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie katika habari ya uvuvi. Katika jimbo langu wananchi wanajishughulisha na uvuvi, namshukuru Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi aliweza kuwasikiliza wananchi wangu waliotoka jimboni kuja kuzungumzia malalamiko ya suala zima ya kanuni zilizokuwa siyo rafiki na wao na Mheshimiwa Waziri alionesha kabisa kusikitishwa kwa nini hizo kanuni ziliwekwa vile, kwa hiyo, nina imani Mheshimiwa Gekul ambaye ni Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi hili jambo anakwenda kulitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili jambo litakwenda kuleta uchumi mzuri katika Jimbo la Kigoma Kusini kwa maana ya uvuvi, lakini pia Mheshimiwa jimbo langu wananchi wanajishughulisha na kilimo cha mpunga pamoja na mahindi na mihogo. Lakini ipo changamoto moja ambayo kwa kweli naomba Serikali iweze kusaidia, ni wanyama kwa maana ya mamba katika majaruba yale ya mpunga kwa mfano Kyala yaani watu wanakufa kwa sababu ya mamba ni wengi sana, tumejaribu kuwaambia watu wa mifugo wajaribu kupunguza wale mamba yaani mamba wale wana uwezo wa kuchukua binadamu yaani mmoja kwa kila siku, sasa fikiria kwa mwaka mzima ni watu wangapi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mpango kwa taarifa nzuri aliyoleta mbele yetu na naomba nichangie eneo la kilimo na uvuvi kama muda utanitosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichukue nafasi hii niwashukuru Wanajimbo la Kigoma Kusini kwa kunichagua, lakini pia nikishukuru Chama Cha Mapinduzi kuweza kurudisha jina langu ili niweze kupeperusha bendera ya kutetea Jimbo la Kigoma Kusini ambapo nilishinda kwa kishindo na pia Mheshimiwa Rais alipata kura nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwashukuru familia, hawa watu kama wasingeweza kunipa support nisingeweza kufika hapa nilipo; mke wangu pamoja na watoto lakini zaidi sana ndugu yangu mmoja ambaye anaitwa Gervas; Mkurugenzi wa World Worth. Huyu mtu alilfika kwenye mkutano wa kampeni wakati mimi nazindua tarehe 11 Oktoba, 20. Aliwaambia wananchi, mkimchagua huyu bwana Bidyanguze mimi nitamchangia milioni 50 kuongezea kwenye Mfuko wa Jimbo wa Serikali. Jambo la ajabu sana, kwa hiyo nataka nikwambie kuanzia sasa tayari katika Mfuko wa Jimbo ule ambao nilifadhiliwa na mwanaume yule tayari nilishapeleka milioni 12 mifuko ya cement 600 ya thamani ya milioni 12. Huyo mtu lazima nimpongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nichangie Mpango huu kwenye eneo la kilimo. Kilimo ni kweli ndiyo uti wa mgongo, lakini kwa bahati mbaya sana naomba nishauri Serikali, bado haijaweka miundombinu mizuri yaani ile ambayo inatamanisha wananchi waweze kupenda kilimo. Serikali bado inasaidia tu wale ambao wameitikia kilimo, mimi najiuliza wako vijana wengi wanaingia shule za sekondari wanamaliza vyuo vikuu, wote hawa plan yao ni kuajiriwa. Naamini Serikali haina uwezo wa kuajiri wote hao, sasa tufanyeje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Serikali ije na mpango wa kushawishi wananchi, hawa vijana ambao ni kundi kubwa, waweze kupenda kilimo. Kilimo wanakikimbia, si tunao majimboni kule, wapo ambao wamesoma wamemaliza vyuo vikuu lakini hawana kazi, lakini ukiwaambia twende tujiajiri kwenye kilimo hawana habari na hicho kitu. Sasa nadhani katika eneo hili la kilimo, yuko mchangiaji mmoja amezungumza vizuri na sikumbuki vizuri, hivi tathmini ya wanafunzi ya wanaokwenda kujifunza kilimo kusoma masomo ya kilimo hivi ni wangapi? Naona kama ni wachache sana, kwa sababu gani? Kilimo wanakikimbia na wale ambao wanalima wanakwenda kuchoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nadhani Wizara ya Kilimo ije na mpango ambao utatengeneza ushawishi ili watu waweze kulima. Kilimo kimetafsiriwa kwamba ni kwenda na jembe la mkono kwenda kulima, mtu aliyesoma hawezi kwenda kulima kwa kilimo hicho. Kwa hiyo tunatakiwa Serikali ije na mpango wa kusaidia kutoa mashamba maana mashamba yenyewe kuyapata ni kazi. Mashamba yapatikane kwa njia nyepesi kama vile ambavyo Serikali inahamasisha uwekezaji tuhamasishe uwekezaji ndani ya kilimo kwa watu wetu hawa vijana, tukishafanya hivyo, watu watakipenda kilimo, lakini mwisho wa siku lazima kilimo kile Serikali iweke utaratibu wa kupata masoko kwa ajili ya mazao hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mkulima kwa kiasi fulani, niliwahi kulima maeneo ya Tanga kule, lakini tuliwahi kupata mahindi mengi wakati fulani nadhani ilikuwa elfu mbili kumi na ngapi sijui, lakini Serikali kwa sababu ya kuhitaji kutunza chakula ndani ya nchi ilikataza watu kusafirisha mazao nje ya nchi. Hata hivyo, yenyewe Serikali haikuwa tayari kuyanunua. Sasa wewe fikiria, mtu amekwishalima na amekwishavuna, asafirishe akauze, apate fedha anazuiliwa na Serikali ni jambo jema, lakini basi yanunue hayo mazao. Kwa hiyo nafikiri kwenye eneo la kilimo tukilifanyia kazi ni sehemu nzuri sana ya kuajiri watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ufugaji pia; ufugaji ni kama kilimo. Sisi Kigoma tunalo Ziwa Tanganyika lina samaki wengi sana lakini elimu haipo ya uvuaji wa samaki, ni eneo moja ambalo kama Serikali ingejikita kufundisha na kutoa nyenzo kwa ajili ya watu waweze kuvua, nadhani vijana wetu hawa ambao wako katika shule na wanaingia kwenye shule na vyuo vikuu wangeweza kujikita baada ya kutoka kule, kuja kuingia kwenye habari ya uvuaji wa samaki. Habari hii ni ajira kubwa sana na ingeleta tija kubwa sana na fedha nyingi kwenye kuongeza kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nafikiri hili nalo lazima tuliangalie sana, kuliko kufikiria tu kwamba lazima mtu asome awe nani. Nasema hivi, watu wengi sasa hivi wanafikiria kila mtu awe Mbunge, wanafikiri kwamba kwenye Ubunge kidogo kuna nafuu, lakini Jimbo la Kigoma Kusini, Jimbo la Mwibara na mengine, hivi wote kama watafikiria kuja huku ni kwa nini? Ni kwa sababu inaonekana kidogo Mbunge akirudi kutoka Bungeni, anakuja amevaa vizuri, anaonekana anafaa. Kwa hiyo, nadhani Serikali iwekeze katika kilimo na uvuvi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuchangia hayo. Ahsante (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Waziri wa Maji. Waziri wa Maji huyu ametokea kwenye nafasi ya Naibu Waziri, inaonekana Mheshimiwa Rais alimwona pale alipokuwa akitenda kazi kwenye nafasi yake ya Unaibu Waziri ndipo akaona ampandishe daraja awe Waziri kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Meneja wa RUWASA pale kwenye Jimbo langu la Kigoma Kusini, pale Uvinza, naye ni mpya, lakini ameanza kazi vizuri. Ameanza kwa kutembelea kata zote na kuhakikisha anaona vijiji ambavyo havina maji aweze kuona namna ambavyo anawapatia maji wananchi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na Wabunge wenzangu waliojaribu kusema namna ambavyo Wizara inaweza ikatengeneza miradi ya maji ya kitaifa. Jimbo langu liko pembezoni mwa Ziwa Tanganyika. Jimbo langu lina kata 16, lakini ni kata tatu tu ndio zina maji, lakini vijiji viko 61, vijiji ambavyo vina maji havifiki 10. Pia ni jambo la kushangaza sana kwamba, maji wananchi wanayaona, lakini uwezo wa kuyachukua hawana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama ambavyo Serikali kupitia Wizara ya Maji imeweka utaratibu wa kuchukua maji katika Ziwa Viktoria na kuyafikisha katika mikoa mbalimbali na hapa Dodoma yanakuja. Kwa nini Mheshimiwa Waziri asione namna ya kubuni mpango wa kuanzisha mradi mkubwa katika eneo lile kwa kutumia maji yale ya Ziwa Tanganyika ambayo mradi ule ungeenda mpaka kwenye Wilaya ya Nkasi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi katika jimbo letu, kama nilivyotaja, tuko karibu sana na maji, lakini iko miradi ambayo ilipelekwa ambayo mpaka sasa haijakamilika. Kwa mfano, Lukoma; uko mradi mmoja mzuri sana wa maji ulianzishwa mwaka 2010. Mpaka leo tunavyozungumza mradi ule ulikuwa na asilimia 80, lakini mpaka sasa haujaanza. Kijiji cha Lukoma watu wanasubiri maji hawayaoni, lakini fedha ya Serikali ilikwenda kwa hiyo, unaweza ukaona kwamba, miradi hii ambayo Wizara inaianzisha wakati mwingine ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anatakiwa awe na mpango madhubuti, mpango ambao utampelekea kuonesha kwamba, amefanya maamuzi magumu. Miradi ambayo ni ya pesa nyingi, lakini itakuwa na matokeo mazuri kuliko vimiradi vidogovidogo ambavyo vinakuwa na pesa kidogokidogo na mwisho wa siku miradi ile haikamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fikiria Kata hiyo ya Lukoma ambayo ina mradi wa maji huu wa mwaka 2010 ambao mpaka sasa haujakamilika na kata ile ina vijiji saba. Hivyo vijiji vyote havina maji, ila nashukuru tu kwamba, Mgambazi ndio kijiji kimoja ambacho katika vijiji saba ambacho kina maji. Pia Mwakizega uko mradi ambao ulianzishwa mwaka 2020, lakini mpaka sasa mradi huo haujaanza. Mabomba yapo, lakini tatizo ni viunganishi kama Waheshimiwa Wabunge wenzangu walivyozungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mlela pia upo mradi wa maji, kisima kilishachimbwa, lakini mradi ule wananchi wanaendelea kusubiri hawapati maji. Kandaga vile vile ndio kijiji ambacho mimi natokea, kijiji hicho kilichimbiwa visima, lakini bahati mbaya kumbe visima vile vilivyochimbwa inaonekana upembuzi yakinifu haukufanywa vizuri, vile visima havina maji, lakini fedha ya Serikali ilitumika katika eneo lile. Kwa hiyo, leo tunasubiri labda Mradi ule wa Mlela ambao tayari umeshachimbwa kisima na wataalam wale wanasema inawezekana yale maji wakayasogeza pale Kandaga ambapo ni vijiji vinafuatana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasubiri hiyo neema kama itapatikana na naomba nimwombe Mheshimiwa Waziri kwa kweli katika eneo hili, tukiweza kumpitishia bajeti yake basi aweze kuniona, atembelee katika jimbo langu aone hiki kilio ninachokitoa kwa uhalisia kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile pana mradi pale Ilagala. Ule Mradi wa Ilagala bahati mbaya sana ni mradi ambao haukushirikisha wananchi. Walichimba kisima na bahati mbaya sana kile kisima kina maji ya chumvi wakati Ilagala kuna Mto Malagarasi, mto ambao una maji baridi. Sasa wananchi wanajiuliza, Wizara ya Maji kwa nini watuletee maji ya chumvi wakati sisi tuna maji baridi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mradi ule ni kama vile hauwezi kufanya kazi kwa sababu, wananchi hawataki kabisa yale maji. Kwa hiyo, tukienda kule Mheshimiwa Waziri nina imani atapata uchungu mkubwa kuona namna ambavyo anaweza kubadilisha ili tuweze kuwatengenezea pump ili wapate maji yale ya Mto Malagarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwambao mwa Ziwa Tanganyika lina kata nane, lakini katika kata zile ndio kata ambazo kwa kweli, kimsingi mvua zinaponyesha wananchi wanapata shida ya tatizo lile la kipindupindu, kwa sababu ziwa liko bondeni wananchi wanaishi juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati mwingine kutokana na mazingira yalivyo lazima walazimike kuchota maji ya ziwani ili waweze kujikimu na yale maji yanakuwa yameshachafuka kutokana na vinyesi ambavyo, maana vyoo vipo, lakini vyoo wakati mwingine vikifurika maana yake lazima choo kile kiende kule ziwani. Kwa hiyo, kuondoa tatizo la kipindupindu katika Kata za Sunuka, Sigunga, Helembe, Buhingu ni kuhakikisha kwamba tunapata miradi ya maji mikubwa ambayo inatokana na maji ya kutoka Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fikiria Sigunga ina vijiji vitatu lakini hakuna hata kijiji kimoja kina mradi wa maji. Hiyo Sunuka ambayo nimeitaja ina vijiji nane, lakini kuna kijiji kimoja tu kina ndio mradi wa maji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nirudie kumwomba Mheshimiwa Waziri, tuongozane kwenda Jimboni, ili niweze kwenda kumwonesha matatizo yaliyoko jimboni kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu, Wizara ya Miundombinu. Naomba nilete masikitiko yangu kwa barabara kubwa hii ambayo inatoka Tabora kwenda Kigoma. Kwanza, naomba nichukue nafasi hii nimpongeze na kumshukuru Rais wa Awamu ya Nne, ndiye aliyetuunganisha na mikoa mingine sisi Kigoma pale alipotutengenezea Daraja la Mto Malagarasi na likaitwa Kikwete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipo kipande kilibaki cha kilometa 51 ambacho kinatokea Mpeta baada ya kuvuka Daraja la Mheshimiwa Kikwete mpaka Uvinza ni kilometa 51, hili eneo limekuwa ni tatizo kwa muda mrefu sana. Unatoka Dar-es-Salaam, Dodoma, Tabora, unakwenda mpaka Kigoma lakini eneo hilo ndilo limebaki na vumbi, ni jambo la ajabu sana. Wananchi wanajiuliza hivi kuna nini? Kwa hiyo, naomba Waziri pamoja na kwamba nimeona kwenye bajeti yake ameitaja, lakini naomba nisisitize na wananchi wasikie kwamba barabara hiyo nimeitaja, ni kero kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ipo barabara nyingine ya Uvinza kwenda Kasulu nayo ni kero sana na ni barabara fupi sana. Kwa kweli, naomba katika bajeti hii hii barabara nayo iweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ipo nyingine inatoka Uvinza kwenda Mpanda kupita Mishamo. Hii nayo ni barabara ambayo kwa kweli ni ya kimkakati, ikiwekwa lami na sisi Kigoma tutakuwa tumeondokana na lawama na malalamiko kama ya wale wenzetu waliokuwa wanasema wametengwa. Sisi tumetengwa kwa sababu tumetengenezewa barabara za lami lakini vipande vimebaki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Kigoma Kusini, wewe ni shahidi, ulipokuwa ukitokea kwenye msiba wa marehemu Mbunge wetu ambaye alitangulia mbele ya haki, Mheshimiwa Nditiye, wakati unarudi kutoka Kigoma kwenda Mbeya ulipotea. Ulichukua barabara ambayo sio yenyewe, ile barabara ni ya Simbo – Kalya, ulikwenda kurudia kwenye kivuko cha pale kwenye Mto Malagarasi, pale ndiyo uliposhtuka kwamba barabara ile sio yenyewe, nakupa pole sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuja kuambiwa kwamba Naibu Spika alipotea alidhani hii barabara inakwenda Mbeya. Ukweli barabara ile kama itajengwa vizuri inayo access ya kwenda Mbeya, ulikuwa hujakosea, sema kule mbele ungepata shida sana. Barabara ambayo ungepita badaye ni kutoka Rukoma kwenda Ikuburu na Rubalisi baadaye inapita Mwese halafu ndio ungeingia sasa Mpanda kwenda sasa Kalya. Hii barabara ni muhimu sana kwa sababu ni barabara ya mkoa lakini inakwenda kuishia Kalya peke yake. Ni barabara nzuri bado tunatumia changarawe na kwa kweli kupitia nafasi hii nimpongeze Meneja wa TANROADS wa Mkoa wa Kigoma Bwana Eng. Choma, hii barabara anaingalia sana lakini bado kuna vipande ambavyo vina shida.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema tu kwamba Daraja la Mto Malagarasi pale ulipokwamia ni tatizo, lakini nashukuru Wizara imetenga shilingi milioni 250 kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Nina imani daraja hilo litaenda kujengwa. Naomba niunge mkono hoja. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, uliniita mchangiaji wa tatu, nipo hapa William Nashon.

MWENYEKITI: Ulipoitwa hukuwepo.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwepo.

MWENYEKITI: Haukusimama lakini.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisimama, nilikuwepo.

MWENYEKITI: Haya endelea.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu sana ambayo ni Wizara ya Mawasiliano. Kwanza naomba nimpongeze ndugu yangu Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya. Wizara hii ni Wizara nyeti sana, kwa sababu sasa hivi kwa kweli wananchi wameshaelimishwa na wanazo simu zao na njia nyingi ni kutumia simu. Ukitaka kulipia maji, ni lazima utumie simu, lakini pia ukitaka kulipia umeme lazima utumie simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna shida kwenye mtandao huu wa kulipia umeme. Nadhani mnaweza mkaona kabisa, yaani hakuna namna ya kulipia umeme, kuna shida sana. Kwa hiyo, bado Wizara ina kazi kweli ya kufanya hii shughuli ili iweze kuwa na ufanisi mkubwa kuliko ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea Wilaya ya Uvinza ambayo kwa kweli ni Wilaya ambayo watu waliitikia sana katika utaratibu huu wa wananchi kuwa na simu, kwa sababu hakuna namna nyingine, maisha ni simu. Kwa hiyo, Wizara hii ni Wizara ambayo inawagusa watu. Kwangu ninazo kata 16, lakini zipo kata nne, zote zina matatizo ya mawasiliano. Yaani ukienda kule Mbunge unafanya ziara, hata kama ningekwenda na Waziri, yaani siku hiyo tunashinda hakuna mawasiliano kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, ni Kata ya Mtegowanoti, yaani haina mawasiliano kabisa na hakuna mnara hata mmoja; ya pili ni Kata ya Kandaga hasa katika Kijiji cha Kandaga chenyewe. Kwa kweli na Kijiji kile ndipo ninapotokea; mimi nikishaingia kijijini pale, hakuna mawasiliano mpaka kesho nitoke kule, niende eneo lingine ambalo lina mawasiliano. Ni aibu sana. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kwakweli jambo hili Mheshimiwa Waziri aweze kuliangalia hasa katika eneo langu hilo la Kandaga na vijiji hivi ambavyo nimevitaja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Herembe ina vijiji vitatu, lakini vyote havina mawasiliano; Kata ya Igalula ina vijiji saba lakini vijiji ambavyo vina mawasiliano ni viwili; ambavyo ni Lukoma pamoja na Igalula yenyewe, vilivyobaki vyote, havina mawasiliano. Sasa kwa kweli ukiangalia hili ni tatizo. Ukienda kule wananchi wanamlalamikia Mbunge kwamba ni vipi sisi tumetengwa? Mbona wengine wana mawasiliano, sisi inakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nadhani, kwa kuwa na sisi Serikali inao mtandao wa TTCL, kwa nini basi tusiweze kupata minara ya TTCL ili tuweze kuondokana na hilo tatizo? Kwa sababu makampuni mengine haya yanafanya kazi kibiashara zaidi, lakini mtandao wetu huu wa kampuni ya TTCL, pamoja na kwamba na yenyewe inafanya kazi kibiashara, lakini pia mtandao ni wa Serikali. Kwa maana hiyo, ina huduma pia. Wenzetu hawa hawana huduma; wakiweka eneo mtandao au huo mnara, wakiona hali siyo nzuri ya mapato, wanahamisha. Sasa wakihamisha wale wachache maana yake wanaobaki, hawana huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, katika Jimbo langu eneo la mawasiliano, tukimaliza bajeti yake yeye mwenyewe Waziri twende Pamoja. Haiwezekani tuwe marafiki, halafu mimi nyumba inaungua. Mheshimiwa Waziri nitafurahi sana tukienda wote huko ili uone. Simu zako utazima, kwa sababu hutakuwa na uwezo wa kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja. Kama Mheshimiwa atanifanyia hivyo, basi hata shilingi yake sitashika. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimpongeze Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayofanya. Lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa jinsi alivyoweza kutatua mgogoro wa wavuvi katika Mkoa wa Kigoma kwa maana ya Majimbo matatu; Kigoma Kaskazini, Kigoma Mjini na Kigoma Kusini ambalo ndilo jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ametusaidia sana pale ambapo walikuja wale wavuvi na wakaja na agenda zao zilizosababisha Mheshimiwa Waziri kifuta baadhi ya kanuni ambazo hazikuwa rafiki. Mheshimiwa Waziri, nakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali kupitia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo mpango wa Serikali uliopo ni wa kuhakikisha kwamba inanunua meli za uvuvi katika Bahari Kuu ili nasi tuweze kufaidi samaki wale ambao watatusababishia kuongeza Pato la Taifa katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli tunasikitika sana wananchi tunapoona kwamba tunalo ziwa kuu lakini tumekuwa hatupati faida itokanayo na samaki wale katika ziwa kuu. Lakini inaonekana mpango wa Serikali ni kwamba sasa itanunua meli nne ambazo zitahakikisha kwamba zinavua samaki ambao watasababisha tupate mapato makubwa kutoka kwenye chanzo hiki cha mapato ambacho tumekiacha kwa muda mrefu. Hii naomba niwapongeze Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri kwa hii ambayo itakwenda kuongeza uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, alivyomaliza kutatua ule mgogoro katika zile kanuni kwenye jimbo langu pamoja na majimbo ya wenzangu wa Kigoma ambayo nafahamu kabisa utatuzi ule alikuwa anaendana na wavuvi wale wa Ziwa Tanganyika lakini katika Mkoa ule wa Katavi pamoja na Wilaya ile ya Tanganyika, na wenyewe walikuwemo katika ule ujumbe. Nina imani kwamba ukanda wote ule tatizo sasa hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo moja; naomba uige mfano wa Wizara ya Madini ambayo ina wachimbaji wadogo. Lakini wachimbaji wadogo wale wamewekewa utaratibu ambao Serikali imewatambulisha kwenye mabenki na sasa wanakopesheka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wetu katika Ziwa Tanganyika wanatumia vifaa ambavyo ni duni. Na ndiyo maana wakati mwingine samaki hawawezi kupatikana vizuri kwa sababu hakuna utaalam wa kisasa. Naomba katika eneo hili wavuvi wa Ziwa Tanganyika, pamoja na maeneo mengine waweze kukopesheka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atengeneze utaratibu kama ambavyo Wizara ile ya Madini imeweza kufika mahali sasa wachimbaji wadogo wanaweza kukopesheka. Hii sekta ya uvuvi pia ni sekta muhimu. Wakopesheke. Pia Wizara iweke utaratibu namna ambavyo baada ya kupata samaki wale waweze kuhifadhika kwenye majokofu ili waweze kuuzwa hata baadaye, lakini samaki wanapopatikana bado wabichi wanalazimika kuwauza harakaharaka ili wasiweze kuoza. Sasa wanapoteza fedha kwa sababu hawawezi kuweka, lakini kama wataweka maana yake watauza wakati ambao soko lipo. Hili naomba Mheshimiwa Waziri ulichukue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye eneo la ufugaji wa ng’ombe kwa maana ya mifugo. Amezungumza mchangiaji mwenzangu kwamba Wasukuma ndio watu ambao kwa kweli wanajishirikisha na mifugo. Jimbo langu lina vijiji 61; wote wanaofuga ng’ombe pale wao wanaochunga ng’ombe kule katika vijiji vile ni Wasukuma, sisi Waha hatufugi ng’ombe. Kama vile Mheshimiwa Spika alivyokuwa akizungumza kwamba Serikali haifugi ng’ombe na sisi Waha hatufugi ng’ombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba, ng’ombe wale ni wengi. Katika wilaya yangu ile, kwenye jimbo langu, tuna ng’ombe takribani 200,000 na hawa ng’ombe wamezagaa. Hakuna mpango wowote lakini wanasumbua wananchi ambao wanajishirikisha na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika eneo hili naomba nimshukuru Waziri kwa sababu alifika jimboni kwangu akaenda kutatua mgogoro ambao kwa kweli ulikuwa ni mkubwa katika eneo moja, ingawaje maeneo mengine hakufika, pale ambapo aliruhusu kwamba kwenye eneo ambapo alitoa hekta 6,000 ziweze kutumika kwa wafugaji. Hilo ni jambo ambalo wananchi wamelifurahia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona bado kuna eneo lingine, kwa mfano kata nane za ukanda wa maji, bado hukufika na hukutoa maelekezo yoyote, na huko ndiko kwenye matatizo ya kuingiliana wale wafugaji wanapoingia kwenye maeneo ya wakulima. Kesi ziko nyingi mno na ng’ombe wakishaingia kwenye shamba, hata ungeenda mahakamani, kesi inaamuliwa kwamba ng’ombe ndio wamekula; sasa unashitakije ng’ombe? Inakuwa ni ngumu sana. Kwa hiyo, naomba katika eneo hilo Wizara iweze kuja na mpango wa kuhakikisha kwamba hizi ranchi ambazo zipo ambazo hazitumiki basi ziweze kutumika sasa katika kipindi hiki ambacho hazitumiki Wizara iweze kuwapa wananchi waendelee kuzitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tunajinasibu kwamba sisi nchi yetu ni nchi ya tatu katika mifugo. Sasa Serikali katika eneo hili imefanyaje? Imewatengea maeneo gani? Unakuta ni migogoro. Kwenye maeneo ya wakulima kuna migogoro ya wakulima, lakini kwenye maeneo ya ranchi wakati mwingine pia wakiingia kwenye ranch kuna matatizo tena katika maeneo hayo. Sasa nadhani Wizara ingekuja na mpango ikatenga maeneo kwa ajili ya hawa ambao nao ni wafugaji na ni eneo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimalizie kwa kusema kuwa eneo hili Serikali bado haijawekeza. Kwa sababu jiulize; hawa ng’ombe 200,000 katika jimbo langu, kuna majosho mawili tu. Sasa tunasema nchi yetu ni nchi ya tatu katika mifugo kwa Afrika, sasa kwa nini tusifike mahali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hotuba ya Waziri wa Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya katika wizara hii pia na Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini pia naomba nimshukuru Katibu Mkuu wa Wizara hii kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya. Tunao ushahidi mkubwa kwamba nchi yetu ilikuwa na giza, lakini sasa mwanga unaonekana, pamoja na kwamba zipo changamoto. Lakini nipongeze Serikali kwa kazi nzuri ambayo imefanywa ya kuhakikisha kwamba tunapata megawatt 2115 katika bwawa lile la Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli huo utakuwa ni ufumbuzi wa kudumu kuondokana na giza tuliokuwa nalo katika nchi yetu, lakini pia ni kwamba kutokana na umeme ni mwingi ambao utakwenda kuuzwa katika nchi jirani maana yake bwawa lile litakwenda kuongeza pato la Taifa pale ambapo tutakwenda kuuza umeme katika nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili jambo la kupongeza sana Awamu ya Tano ambayo iliingia mkataba na ilifanya maamuzi magumu kwa kuhakikisha kwamba bwawa lile linajengwa pamoja na kwamba mipango ile ilikuwepo kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia niipongeze Serikali kwa kuingia mkataba wa kuona namna ya kujenga ile eneo la Malagarasi pale Igamba ambayo kwa kweli ni katika Jimbo langu la Kigoma Kusini huu mradi unakwenda kutekelezwa kulingana na hotuba ya Waziri wa Nishati naomba Mheshimiwa Waziri mradi huu unaonekana utaanza Septemba mwaka huu na utakwenda kuisha Septemba tena 2024, maana yake ni miaka minne.

Mheshimiwa Spika, naomba Mkoa wa Kigoma umekuwa ukitumia mafuta, umeme wa mafuta kwa muda mrefu sana na ndiyo maana unaweza kuona kwamba kimkoa hatuna viwanda, isingewezekana kupata kiwanda au viwanda katika eneo ambalo tunatumia umeme wa mafuta. Ambao umeme wa mafuta una gharama kubwa sana katika uendeshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninayo imani, kwamba mradi huu ambao una megawatt 49.5 utakwenda kuwa ufumbuzi na wa Mkoa wa Kigoma kwa ujumla, lakini ninayo imani kutokana na bajeti yako na ulivyoonyesha, umeonyesha kabisa kwamba umeme wa grid ya Taifa utawahi kuingia Kigoma kabla ya mradi huu ambao utajengwa pale, pale Igamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona ulitakiwa kufanya ziara kwenye Mkoa wa Kigoma pale Nguruka ambapo tayari kumeshaandaliwa na palishajengwa kwa ajili ya kupokelea umeme ambao ndiyo utakuwa unapoozewa pale. Lakini ninayofuraha kuona kwamba mpango wako Mheshimiwa Waziri kuingiza umeme wa grid ya Taifa Kigoma maana yake upande mmoja wa Tabora unaingilia Nguruka ambapo ni kwenye Jimbo langu pale katika Kijiji cha Mgaza pameshajengwa tayari, compound imeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, lakini pia umeme mwingine wa grid ya Taifa unaingilia Kankoko kutokea Nyakanazi hii mipango miwili ikikamilika Mheshimiwa Waziri kwa kweli na sisi Kigoma tutakuwa tumepata ukombozi kutoka kwenye giza. Na ninayo imani sasa wawekezaji watakuja kwa ajili ya kuwekeza viwanda katika mkoa wetu ili na sisi mkoa wetu uweze kuinuka kiuchumi na wananchi wetu wa Kigoma waweze kupata ajira, kwa sababu bila viwanda ni vigumu sana kupata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika eneo hili la Ujenzi wa Igamba nimefurahi kuona kwamba tayari fedha zimekwisha patikana kwa ajili ya fidia, wananchi katika eneo hili walitwaliwa maeneo yao kwa muda mrefu na walizuiliwa wasiendelee kwa hiyo walikuwa hawawezi kufanya chochote kwa sababu ya mradi huo, lakini naona kabisa kwamba sasa fedha ya fidia nayo pia imepatikana. Naomba Mheshimiwa Waziri jambo hili uende kulifanyia kazi ili wananchi wale waweze kupata fidia katika maeneo ambayo waliyaachia kwa ajili ya mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu kuna vijiji 61 ni kweli vipo vijiji 17 tayari vimekwishapata umeme na maana yake kuna vijiji 14 bado havijapata umeme kabisa, lakini kwamba hata hivi vijiji 17 ambavyo vimekwishapata umeme ni katika maeneo tu kama Waheshimiwa Wabunge wenzangu wanavyoongea. Na hii imetuletea malalamiko makubwa sana sisi Wabunge, tunalalamikiwa sana kwamba kwanini umeme unakuja hapa na baadaye kwenye vitongoji vingine umeme haufiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapata wakati mgumu katika kujibu maswali tunaomba Mheshimiwa Waziri hili jambo lifanyie kazi. Nafurahi kuona kwamba unao mpango mzuri kwamba tayari makandarasi wameshapatikana na nimekuwa nikikusumbua sana, lakini mpango wa Serikali ni kwamba umeme utapatikana 2022 kwa maana ya nchi nzima, kwa maana ya vijiji vyote.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba wakandarasi hawa ambao sasa wameteuliwa waweze kwenda kuondoa hizi kero pamoja na kwamba tunatakiwa tuendelee kumaliza vile vijiji 14, lakini pia huku kwenye vijiji 17 ambavyo tayari vina umeme lakini kuna maeneo mbalimbali hayana umeme katika vijiji hivi kwenye vitongoji na hiyo kazi pia iendelee kupunguza malalamiko.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu la Kigoma Kusini zipo Kata nne, Sigunga, Mgambo, Kalya na Igalula, kata hizi zinatumia umeme wa jua, wananchi hawa wamekuwa wakilalamika sana kila siku napigiwa simu kwamba kwanini mkandarasi huyu ambaye ni Jumeme kwanini anawauzia umeme unit moja shilingi 4000. Shilingi 4000 tunakuwa na bei mbili kwenye nchi moja hivi hawa wananchi tunawaonaje, tunawasaidiaje Mheshimiwa Waziri, nimekwisha kuja kwako mara nyingi sana, lakini ulionyesha kutatua tatizo hili na leo pia umetoa tamko, lakini pia bado nakuomba ziara yako ya kwenda Kigoma kutokea Tabora iendelee kuwepo na nitaomba nishirikiane na wewe unipe taarifa lini utakwenda nione uende kutoa tamko ili kusudi hawa watu wakome, wakome kabisa. (Makofi)

SPIKA: Ahsante, Ahsante Mheshimiwa Bidyanguze.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naoamba basi niweze kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niunge mkono hoja kwa sababu Kamati hii ni yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anafanya kazi vizuri na pia kwenye jimbo langu amenijengea madarasa 196. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimshukuru na kumpongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati kwa kuwasilisha taarifa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najikita kwenye eneo moja kulingana na dakika ambazo ni chache; eneo la watoto wanaopata mimba katika shule zetu za Sekondari na Msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo imeruhusu sasa watoto wale ambao wamepata ajali ya kupata mimba watarudi tena shuleni kusoma baada ya kuwa wanaendelea kunyonyesha. Hilo ni jambo jema na wananchi wamelifuarahia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili isije kuonekana Serikali sasa imeruhusu mimba za shuleni. Hili ni jambo la kuangalia sana; kwamba kwanza kwenye familia zenyewe ambako hawa watoto ndiyo wanatoka, tuvunje ukimya, tuzungumze hili suala la mimba, tusiwafiche watoto wetu. Kama mwanaume utashindwa kuongea na kijana wako, basi tafuta namna ambavyo ujumbe utamfikia kijana wako, lakini kama huna uwezo wa kuongea na msichana basi tafuta hata shangazi aweze kuongea na huyu msichana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ni vizuri pia ije na mpango mwingine. Niliwahi kuzunguza wakati fulani kwenye semina nikasema Serikali ilete mtaala ambao utasababisha kufundishwa wale watoto wafikie hatua ya kujua kwamba mimba inapatikana wakati gani. Kwa sababu ile ni ajali. Ni ajali. Hakuna mtoto anayetegemea kupata mimba, hakuna. Anakwenda kusoma ilia pate elimu. Kwa nini anapata mimba; anapata mimba kwa sababu ni ajali. Na anapata mimba kwa sababu wakati mwingine hajui kwamba ile mimba anaipatapataje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa wale ni wanafunzi na wanasoma, basi wafikishwe kwenye eneo la kalenda, kwamba ukitaka kuthubutu kufanya jambo hilo, basi tarehe hii na hii usithubutu hicho kitendo. Kabisa. Kama mwenzangu aliyechangia aliposema kwamba…

T A A R I F A

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, taarifa.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kitendo cha ngono kwa mila na desturi za Mtanzania na kwa imani za dini zetu zote haipaswi mtoto kufundishwa namna ya kukifanya na kwamba kufanya hivyo ni sawa na kuhalalisha dhambi hiyo ya uzinzi. Ahsante. (Makofi)

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo lazima tulizungumze kwenye familia zetu lakini pia tulipeleke na shuleni. Bila kufanya hivyo Serikali itaonekana sasa kuruhusu hawa watoto waliopata mimba shuleni na warudi tena kusoma shuleni, itaonekana imehamasisha wanafunzi kupata hizo mimba. Naamini kabisa mimba zile zinapatikana kama vile ajali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niishauri Serikali; habari ya kukataa kufundisha somo hili tutakuwa tunajipotezea muda kwa sababu tunaposema kwamba kujamiiana ni dhambi, ni sawa ni dhambi, lakini lazima tufikie mahali kwamba no, usifanye ngono kipindi hiki na hiki, ndiyo. Tufike mahali hilo tuliseme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja tena. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kukushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini pia naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya ya kuweza kusimama hapa Bungeni niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya Waziri wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya yote naomba nimshukuru Rais wetu mpendwa Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika nchi yetu na hasa katika Jimbo langu la Kigoma Kusini. Nimeshuhudia na wananchi wameshuhudia kupata madarasa 196 kwenye eneo la Sekondari na madarasa kwenye shule shikizi. Ni jambo kubwa sana na shule hizi zimekuwa ni mpya zaidi sasa kuliko shule zile za msingi. Naomba katika eneo hili shule za msingi nazo Mheshimiwa Waziri uzione kwamba zimebakia chini sana na zimebaki na majengo mabovu sana nimeona kwenye hotuba yako ya bajeti umeonyesha kutenga fedha kwa ajili ya shule kongwe naomba na mimi kwenye Jimbo langu liangalie sana ziko shule nyingi ambazo kwa kweli zina majengo mabovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano iko shule moja katika Kata ya Itebula na ni shule yenyewe ya Itebula kwa kweli mpaka watoto wamehama kujaribu kusomea kwenye vyumba vichache ambavyo kidogo kuna nafuu na mimi kwenye mfuko wangu wa Jimbo nimepeleka fedha pale angalau nijaribu kuokoa hali ya shule ile na hali ya wale watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwenye eneo la ahadi za viongozi wakuu. Nakumbuka Mheshimiwa Hayati Magufuli wakati anaomba kura kwenye Jimbo langu eneo lile la Uvinza aliahidi kilometa tano za barabara ya lami lakini nashukuru kwamba angalau kuna kilomita mbili zinaendelea kujengwa. Lakini pia aliahidi kilomita tano Nguruka bado hata kilomita moja haijajengwa, sasa naomba Mheshimiwa Waziri kwenye eneo hili la ahadi za Viongozi wetu Wakuu kwa kweli uweke nguvu sana kwa sababu inapunguza imani ya wananchi na Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Magufuli aliahidi kutoa Shilingi Milioni 10 kwenye kituo cha afya pale Kazulamimba wananchi wanashangaa hivi ni kweli Milioni 10 inaweza ikashindikana kupelekwa pale Kazulamimba ambapo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ni jambo la kushangaza sana na mimi wamekuwa wakinisumbua sana wanasema Mheshimiwa Mbunge ni namna gani Milioni 10 haijafika. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri upeleke Milioni 10 Kazulamimba kwa sababu tayari wameshajenga boma wanahitaji kuendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa alitoa ahadi ya kupandisha hadhi kituo cha afya cha pale Nguruka na kilishapanda hadhi kwa hiyo tunasubiri Mheshimiwa Waziri uweze kuleta fedha kwa ajili ya kujenga sasa majengo kwa ajili ya kuendeleza sasa hospitali ile ambayo ilishapandishwa hadhi. Nilijenga hoja wakati ule naomba kura wananchi na Mheshimiwa Rais alikuwepo kwamba Nguruka mpaka kwenye hospitali ya Wilaya ilipo ni umbali wa kilometa 100 kwa hiyo Mheshimiwa alikubali kuongeza hadhi ya kituo kile na kilishapanda hadhi naomba uweke fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna ahadi ambazo alipokuja Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Ummy Mwalimu alikubali kujenga kituo cha afya chenye hadhi ya hospitali zaidi kidogo ya kituo cha Afya kule ukanda wa maji, eneo moja linaitwa Lukome na ninashukuru Serikali fedha Shilingi 250,000,000 zimeshakuja na ujenzi unaendelea naomba kwenye bajeti hii Mheshimiwa Waziri uongeze fedha ili tuweze kumalizia ujenzi wa hospitali ile kwa sababu inakuwa ni hospitali ya rufaa kwa sababu eneo lile na Mheshimiwa Ummy alitengeneza historia kutoka Makao Makuu ya Wilaya kwenda Kalya ni kilometa 300 kwa hiyo unaweza ukaona ni eneo kubwa sana ambalo linahitaji huduma hiyo ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri Ummy alikubali kufungua barabara ambayo inatoka Kalya kwenda Sumbawanga, alikubali kutoa Shilingi Bilioni Moja na Milioni Mia Tano, naomba ahadi hiyo uiandike ili kusudi mwaka huu wa fedha tuweze kupata hiyo fedha tuweze kufungua hiyo barabara. Pia aliahidi kujenga jengo moja la wodi ya wanaume na watoto pale kwenye kituo cha afya cha Kalya, naomba ahadi hizi Mheshimiwa kwa sababu wewe sasa ndiyo umeingia kwenye kiatu ambacho alikuwa amevaa Waziri Ummy hili jambo uweze kulichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo kwakweli mambo yanaenda vizuri na naomba nipongeze…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze kwa mchango wako.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii na mimi nikupongeze kwa kuchaguliwa kwako lakini naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende moja kwa moja katika kumpongeza Waziri wa Elimu pamoja na Naibu wake pamoja na staff yake nzima kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nijikite kwenye eneo moja lakini yatakuwa maeneo mawili. Moja ni kwenye shule mbili ambazo zimetelekezwa pale kwenye Jimbo langu ambazo ni shule za Wizara hii ya Elimu ni shule moja ya Lugufu Boys na shule moja ya Lugufu Girls. Hizi ni shule za Wizara ya Elimu, shule hizi zimetelekezwa kwa sababu hazijapata miundombinu ya maji pamoja na umeme. Naomba Mheshimiwa Waziri unisaidie kwenye jambo hili kwa sababu hizi hazipo chini ya Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi Jimbo langu lina Tarafa tatu. Nilikuwa naomba Tarafa ya Nguruka tupate high school kwa sababu tuna sekondari nyingi. Lakini pia naomba kwenye Tarafa ya Buhingu, Buhingu Sekondari ipandishwe hadhi iwe shule ya high school kwa sababu eneo langu la Jimbo ni kubwa sana. Kutoka mwanzo wa jimbo mpaka mwisho wa jimbo ni kilomita 400. Kwa hiyo unaweza ukaona kabisa kwamba kila tarafa kuna haja ya kuwa na high school. Kwa hiyo watu wa Nguruka wako tayari kupokea high school kwenye Shule yao ya Nguruka Sekondari lakini pia Buhingu wako tayari kupokea high school kwenye Shule yao ya Buhingu. Naomba Mheshimiwa jambo hili unisadie.

Mheshimiwa Naibu Spika, liko jambo ambalo mimi ninaomba nilizungumze; ni jambo la kitaifa. Kwanza naomba nipongeze Serikali kwa kukubali kuwarudisha shuleni wanafunzi waliopata ujauzito; kwamba baada ya kuwa wamejifungua basi warudi kusoma na huku wakiendelea kunyonyesha. Hili ni jambo jema sana na naomba nikuhakikishie wananchi wamelifurahia sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo hili mimi ninaona bado kuna hatari kubwa sana, kwa sababu kwa taarifa ya mwaka jana, mimba za shuleni zilikuwa 8,000, ni nyingi sana! Kwa hiyo, Serikali lazima iweke mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba inapunguza hizi mimba shuleni. Lakini hili ambalo Serikali imelifanya la kuona namna ya kuwarudisha waliopata mimba, baada ya kujifungua warudi shuleni huku wakinyonyesha watoto wao. Mimi naona kama hili jambo litaongeza idadi ya mimba. Kwa sababu wale 8,000 walipata mimba lakini wakiamini kwamba hawawezi kwenda shuleni kwa sababu wamepata mimba. Sasa watakapokuwa wamepata mimba na wakarudi shuleni kusoma huku wakinyonyesha mimi ninaona kabisa kuna hatari ya mimba kuongezeka shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, kwa kuwa pia hata Kamati yangu imelizungumza hili na kuona, kwamba kuwe na elimu kwenye eneo lile la mimba shuleni. Kwa maana itapunguza sasa kile kitendo cha kuongeza mimba shuleni.

Mheshimiwa Waziri hili jambo usipoliangalia litaleta shida kwa sababu pamoja na kwamba wananchi wamefurahia lakini mimba zitakapoongezeka wananchi wataandama. Kwa hiyo itakuwa kashfa kwa Serikali kuona yenyewe imechochea mimba shuleni kwa sababu imeruhusu sasa watoto waliokuwa wamepata mimba wajifungue na warudi shuleni wakiendelea kunyonyesha watoto wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kitakachotokea mle darasani yawezekana ikawa ni darasa ambalo linafundisha wazazi waliojifungua. Kwa hiyo, naomba hili nizungumze kwa msisitizo. Nakumbuka hili jambo kuna kikao cha Bunge wakati fulani niliwahi kulizungumza, nadhani lilikuwa Bunge la mwezi wa tisa. Kwa kweli naomba nirudie ili kusudi lisije kuleta taharuki baadaye kwa wananchi wetu watakapokuja kuilaumu Serikali kuona kwamba yenyewe ndiyo imesababisha mimba za shuleni kuweza kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nichukue nafasi hii nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameweza kutupa afya kuweza kuingia hapa Bungeni tuweze kujadili mambo ya Kitaifa, mambo ya maendeleo ya wananchi wa nchi yetu ya Tanzania na kwenye Majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi kwanza niseme kwamba naunga mkono hoja Wizara hii. Vilevile nimpongeze Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya katika nchi yetu na katika majimbo yetu. Pia nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na Katibu Mkuu na wote wanaoendelea kumsaidia kwenye Wizara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nijikite katika maeneo ambayo fedha zimekuja na zimeweza kutatua matatizo katika Jimbo langu. Zimekuja milioni 645 katika Vijiji vya Mwakizega na Kabeba; huu Mradi ulikuwa umekwama kwa muda mrefu. Imekuja milioni 43 kwa Kijiji cha Sunuka kwa ajili ya ujenzi wa tenki la maji lita 150,000. Pia imekuja milioni 992 kwa ajili ya Vijiji vya Sigunga na Kangwena Mkandarasi amepelekwa pale tarehe 07 mwezi huu wa Tano. Lakini pia 1,600,000,000.00 kwa ajili ya Vijiji vya Herembe pamja na Kaparamsenga. Mradi huu bado unafanyiwa vetting.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia milioni 281 kwenda Kijiji cha Mdabazi kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati huu Mradi ni wa muda mrefu lakini ulikuwa kidogo hautoi maji lakini mpaka leo nilikuwa naongea na Diwani bado kuna shida kidogo. Lakini kuna milioni 281 ambayo imetengwa kwa ajili ya kufanya ukarabari. Milioni 450 ni kwa ajili ya Kijiji cha Kashaguru. Pia milioni 495 Vijiji vya Mlela na Kandaga. Mkandarasi yupo site; ingawa fedha ilichelewa kufika lakini juzi niliambiwa wamelipwa na wanaendelea na Mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, milioni 650 kwa ajili ya Kijiji cha Malagarasi Mkandarasi yupo anaendelea. Milioni 87 kwa ajili Vijiji vya Basanza na Msebeyi hivi sasa gari za kuchimba visima viwili ziko pale kwa ajili ya Basanza na Msebeyi. Milioni 132 Kijiji cha Rukoma ukarabati, huu Mradi ni wa mwaka 2012, ni mradi wa muda mrefu sana. Ulikwama kwa sababu ya ubadhirifu wa wale wanaopewa kazi ya kutengeneza mradi huu, lakini nashukuru kwamba hii milioni 132 tayari hata nilikuwa naongea na Mwenyekiti leo wa Kijiji kuna baadhi ya sehemu maji yameanza kutoka. Hata hivyo kwenye tenki lenyewe yalikuwa hata hayafiki lakini Mwenyekiti amethibitishia Kijiji kwamba maji yanaingia kwenye tenki na limejaa; kwa bado sasa namna ya kuepeleka maji kwenye magati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili kwa kweli inasikitisha sana kwa sababu tangu mwaka 2012 ni muda mrefu sana ni miaka 10 wananchi wanasubiri maji na fedha imepelekwa pale. Yaani unaweza kuona jinsi ambavyo watendaji wanavyoichonganisha Serikali na wananchi, kabisa, haipendezi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba tukimaliza Bunge hili twenda ukaone kabisa wananchi watafurahi sana na mimi nitafurahi sana, mimi naomba niende na wewe mwenyewe Waziri kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia 2,400,000,000.00 Kijiji cha Kaziromimba Mradi uko pale lakini bahati mbaya sana Kijiji kile, Mheshimiwa Waziri jambo la kusikitisha sana, naomba unisikilize. Kuna tenki ambalo liliagizwa kwa ajili ya Mradi ule liko Bandarini sasa hivi ni mwezi wa tatu. Wananchi wanajiuliza hivi lile tenki ambalo tuliahidiwa kwamba linakuja, limetoka nje ya nchi limekuja mpaka Bandarini mbona bado liko pale Bandarini? Na mimi Mheshimiwa Waziri nataka nikwambie kabisa pamoja na kwamba nimekushukuru na kukupongeza lakini kwenye eneo hili nakusudia kushika shilingi yako kama hukutoa maelezo mazuri ni lini tenki hili litatoka Dar es Salaam Bandarini kwenda pale Kazuramimba ili wananchi wakazi wanaokaribia kufika 48,000 waweze kufaidi maji. Lakini pia katika eneo la Kijiji cha Uvinza ambacho ndiyo chenye jina ambalo kimebeba Makao Makuu ya Wilaya. Kijiji kile Mheshimiwa Makamu wa Rais juzi juzi alisimamishwa pale wakalalamika kwamba Kijiji kile hakina maji, lakini mimi nilivyofuatilia ni kweli kijiji kina maji, lakini Vitongoji vyake ndiyo bado havijapelekewa maji. Na hili Mheshimiwa Makamu wa Rais alinipigia simu kunipa taarifa kwamba Mbunge angalia kwa nini wananchi wa Uvinza wanalalamika maji. Maji yapo lakini kwenye maeneo ya Vitongoji ndiyo maji hayajafika. Lakini pia pale Makao Makuu ya Halmashauri bado kuna shida ya mtandao wa maji mradi wa maji pale bado kuna shida, ni kizungurumkuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Nguruka, Mradi ule ulikamilika vizuri lakini bahati mbaya sana haufanyi kazi vizuri na wananchi wameshindwa kuupokea kwa maana ya matumizi kwa sababu ule mradi chanzo chake kwa maana ya pump inatumia mafuta ya petrol.

Kwa hiyo sasa unaweza ukaona kwamba gharama ni kubwa mimi nilikuwa nakuomba Mheshimiwa Waziri kwenye chanzo kile cha maji basi kwa kuwa umeme haujafika basi tuweke miundombinu ya solar ili wananchi waweze kufaidi maji ambayo kidogo yatakuwa na nafuu pale Nguruka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nguruka imebeba Kata mbili, kwa maana ya Kata ya Nguruka yenyewe na Kata ya Itebula, kwa hiyo unaweza ukaona kwamba Mradi huu ni mradi mzuri sana na umeshakamilika lakini wananchi wameshindwa ku-afford bei kwa sababu ya mafuta ile pump inayosukuma yale mafuta. Lakini pia ninajua utatuletea fedha mwaka huu wa fedha lakini bado kuna Vijiji vingi sana havijapata maji kwa mfano Vijiji vya Kata ya Mgabo vyote vitano havijapata maji, Kata ya Mtego wa Noti vyote havijapata maji Nachakulu haijapata maji ni Vijiji vingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi nilikuwa nadhani katika eneo hili wengi wamesema na mimi naomba niseme lakini nashukuru kwamba kwenye Hotuba yako umeongea vizuri kwamba unakusudia kutumia vyanzo vya maji yanayotokana na Ziwa ili yaweze kusaidia kwenye maeneo hayo. Kwa mfano Ziwa Tanganyika ni chanzo kizuri cha maji kwa nini kisitumike hiki? Wabunge wengi wamelalamika ametoka kuzungumza Mbunge mwenzangu wa Sumbawanga kule, lakini Wabunge….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Bidyanguze, muda wako umekwisha.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: … kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri katika eneo hili chanzo cha Ziwa Tanganyika kiweze kutumika. Ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia na mimi nichukue nafasi hii nikushukuru kwanza wewe Mwenyekiti kwa nafasi hii ambayo umenipa, pia nichukue nafasi hii nimpongeze Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa hotuba nzuri aliyoitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wewe ni rafiki yangu, umekuja Kigoma mara nyingi sana, Kigoma unaifahamu, hasa eneo la uvuvi. Kwenye eneo la Mifugo kwa kweli hujafanya vizuri. Wewe umekuwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi lakini umekuja kwenye Jimbo langu hasa kushughulikia kwenye eneo la uvuvi. Kwenye hilo naomba nikushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri naomba nizungumzie mambo mawili, kwanza kwenye eneo la mifugo. Eneo la mifugo Mheshimiwa Waziri ninakupongeza Waziri aliyekutangulia alikuja Wilaya ya Uvinza kutoa eneo kwenye Ranchi ya Taifa ili liweze kutumika kwa ajili ya wafugaji. Hilo ni jambo jema sana. Ni baada ya mimi kuja kuomba Bungeni hapa na Wizarani, Waziri aone namna ya kutenga eneo ambalo litasababisha wananchi wale ambao ng’ombe zao zinazagaa katika vijiji vyote 61 waweze kupeleka ng’ombe huko. Hili jambo nashukuru lakini Mheshimiwa Waziri utekelezaji kwa maana ya kuhamisha wale ng’ombe kwenye vijiji 61 haujafanyika.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuja Kigoma kwenye ziara, alipoandamana na Naibu Waziri wako huyo Mheshimiwa Silinde ambapo naye ndiyo aliteuliwa kuingia kwenye Wizara hiyo akiwa Kigoma, nilimwambia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba naomba Naibu Waziri aje aweze kutatua huu mgogoro ahamishe kwa kushirikiana na Serikali ya Mkoa na Wilaya waweze kuweka mikakati mizuri ya kuondoa hizo ng’ombe katika vijiji hivyo ili wananchi wabaki salama wale wanaojishughulisha na kilimo, kwa sababu kilimo ndiyo uti wa mgongo lakini kilimo ndiyo kinachosaidia wananchi wetu wadogowadogo kwa ajili ya kujikimu na maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wale ng’ombe wanapoendelea kubakia kwenye vijiji, maana yake kwa kweli habari ya kilimo haipo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri unaona jinsi ambavyo unapingana na Wizara ya Kilimo. Sasa hili nakuomba, lakini ng’ombe wale wamezagaa kwenye misitu ya TFS kwa hiyo unapingana pia na Serikali kwa upande huo mwingine. Itakapohamishwa hiyo mifugo maana yake kule itabidi uweke miundombinu kwa ajili ya majosho ambapo kule vijijini hakuna josho hata moja. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri hilo ni la kwanza, naomba sana kwenye eneo hilo nadhani baada ya Bunge hili la bajeti nakuomba ama wewe ama Naibu Waziri aje kule Jimboni ili tuweze kufanya mikakati ya namna ambavyo tunaweza tukahamisha hiyo mifugo kupeleka kwenye eneo lililo rasmi, naamini Serikali itapata mapato kulikoni ambavyo ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine Mheshimiwa Waziri ni kwenye eneo hili ambalo limezungumzwa na Wabunge wenzangu kwenye eneo la samaki. Mheshimiwa Kilumbe ameongea vizuri sana, Mheshimiwa Aida amezungumza vizuri sana. Kwa kweli kwenye eneo hili Wabunge wa Mikoa mitatu ya Kigoma, Katavi, Sumbawanga, ndio ambao tuko kwenye ukanda wa hilo Ziwa Tanganyika, Mheshimiwa Waziri nataka nikuambie kwamba ziwa Tanganyika ndiyo chanzo kikuu cha mapato katika Mikoa hii mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hata hizi Halmashauri zetu zipo kwa sababu ya uvuvi, hakuna namna nyingine. Nataka nikuambie, nimekwenda kufanya ziara kwenye Kata mbili, Sigunga na Mgambo nilichokiambulia ni hiki. Kata ya Sigunga waliniambia Mheshimiwa Mbunge tunaomba kama Ziwa linakwenda kufungwa tuandalie makaburi, hatuna kazi nyingine ya kufanya, kazi yetu ni hapo ziwani. Sasa hebu niambie hiyo kauli ni nzuri kwa wananchi ambao ni wapiga kura? Nikasema siwezi kuwaandalia makaburi lakini Serikali lazima iwe makini namna ya kutekeleza hili jambo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kule kwenye Kata waliniambia kama Ziwa linakwenda kufungwa niwatafutie kazi nyingine ya kufanya.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nashon kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Askofu Gwajima.

TAARIFA

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa anayezungumza kwamba Ziwa Tanganyika linategemewa na nchi nne, sehemu kubwa ya Ziwa hili ipo Congo na mtaalam Waziri anafahamu kwamba samaki huwa wanahamahama katika kuzunguka zunguka. Ukifunga kwetu huku kule Congo wanaendelea kuvua. Utakuwa umefanya uamuzi wa kijinga wa kuisaidia nchi nyingine kile ambacho ungekipata wewe, kinatumiwa na nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zingine zote zitaendelea kuvua halafu wewe utaacha kuvua, wale watapata wewe utakuwa maskini. Kwa hiyo namjulisha mzungumzaji kwamba ni uamuzi usio wa kisayansi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nashon taarifa unaipokea?

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo iko sahihi lakini nadhani haelewi ni kwamba hili Ziwa linafungwa kwa maana ya nchi zote hizo zinazozunguka eneo la Ziwa, lakini mimi nazungumzia upande wangu kwamba wananchi wa Kata ya Buhingu wanasema niwatafutie kazi nyingne ya kufanya, maana yake ni kwamba kazi yao wao ni hiyo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza kutokana na kwamba jambo hili halikuwa na ushirikishwaji, Wabunge wenyewe hatukuwa tumelijua, pamoja na kwamba wananchi wetu kule Majimboni walikuwa wanajua kwamba Wabunge tumeshazungumza hili huku Bungeni au tumekwisha zungumza na Waziri jambo hili, hatukuwa tumezungumza na Waziri jambo hili, nasi kama wananchi ambavyo walikuwa hawalijui nasi pia Wabunge tulikuwa hatulijui. Kwa hiyo, jambo ambalo linatakiwa hapa ni kuona namna ya kutushirikisha Wabunge, wadau wa uvuvi na wananchi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna haja ya kufanya siri ya jambo hili, Ziwa ni la wananchi na Ziwa ni la Serikali na wananchi lazima watii sheria za nchi Serikali ambazo zipo ni jambo la kawaida lakini lazima kuwe na ushirikishwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza ipo timu kubwa ya wavuvi ambao wako hapa Dodoma, wamekuja kukutana na Waziri na leo baadhi yao wataingia humu Bungeni wakati Waziri atakuwa ana-wind up watakuwa wanamsikia. Kwa hiyo, naomba jambo hili….

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa, muda wako umeisha.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Serikali ilichukulie kwa umakini sana na Wabunge hoja yetu siyo kukataa Serikali isifunge Ziwa, lakini hoja yetu ni kushirikishwa.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa nafasi hii ambayo umenipa. Kabla sijanza kuchangia nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu hii hoja ni hoja kubwa, Wizara ambayo inashika wananchi wote wa kawaida na tumekuwa tukisema kilimo ni uti wa mgongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe, naomba nianze kwa masikitiko kuonesha kwamba mimi msimu wa kilimo uliopita kwenye Wilaya ya Uvinza, Jimbo la Kigoma Kusini sikupata mbolea kabisa. Mheshimiwa Bashe tulikutana pale airport Dodoma nikakueleza jambo hili, ulinifahamisha kwamba mbolea ilikwenda pale Nguruka lakini baadae mbolea ile iliondolewa, ni kweli nilifuatilia mbolea ile iliondolewa. Sababu ya kuondolewa mimi sikuwa naijua, kwa hiyo naomba sana Mheshimiwa Bashe kwa kweli msimu huu wa kilimo naomba unikumbuke Wilaya ya Uvinza kwa sababu ni Wilaya ambayo kwa kweli inajishughulisha kwa kilimo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto iliyopo ya mifugo kwa sababu mifugo inapingana na kilimo, wenzetu wale wa mifugo hata mahindi, hata muhogo, chochote kinacholimwa na binadamu wao wanasema ni majani pia, kwa hiyo wanafyeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilete masikitiko yangu kwa mara ya kwanza, nadhani kwenye Wilaya zote msimu uliopita nimepata njaa kwa sababu debe la mahindi lilifika shilingi 30,000. Nilimuona Naibu Waziri kujaribu kuona na mimi nipelekewe mahindi kwenye Wilaya yangu lakini masharti aliyonipa ni kwamba Mkuu wa Wilaya aandike barua. Ni kweli Mkuu wa Wilaya nilimwambia aandike barua lakini sijui kama barua iliandikwa na ikaja. Kwa sababu tatizo ni kwamba Mkoa wa Kigoma ni Mkoa ambao haujawahi kuingia kwenye njaa tangu tumepata uhuru. Sasa nadhani Serikali walipata kigugumizi kuandika barua kwamba Mkoa wa Kigoma una njaa, kwa maana ya Wilaya ya Uvinza, lakini wananchi wangu kwa kweli walipata shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu ruzuku ya mbolea ya tumbaku. Wenzangu wamezungumza sana, tumbaku ni kilimo. Kwa nini tumbaku isiwekewe na yenyewe mfumo wa kupata ruzuku ya mbolea, kwa sababu ni kilimo. Naomba sana kwenye jambo hili kwa sababu Wilaya yangu pale Nguruka wanalima sana kilimo cha tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri lingine ni kwenye eneo la mbegu ya mchikichi. Mheshimiwa Waziri Mkuu amepambana kuhakikisha kwamba Mkoa wa Kigoma unakuwa miongoni mwa mikoa ambayo inazalisha chikichi kwa wingi kwa sababu kwa kweli kimsingi ndiyo Mkoa ambao una historia na chikichi, kwa bahati mbaya sana pamoja na juhudi za Serikali mbegu hizi bado. Kwa sababu mimi mwaka jana niliomba miche 7,500 kwa sababu mimi nina shamba la ekari 200, kwa kuzingatia kwamba ekari moja ni miche 58, niliomba nipatiwe 7,500 sikupata, niliambulia miche 1,000, unaweza kuona kwamba bado.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili Mheshimiwa Bashe lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba chikichi pamoja na alizeti yanakuwa ni mazao ambayo ni mkombozi ili tuweze kupata mafuta sisi wenyewe wananchi kwa maana ya nchi yetu ili tupunguze fedha ambayo inatumika kuagiza mafuta nje, bado Mheshimiwa Bashe wananchi hawa ni kweli wana vishamba vidogovidogo, nakuomba sana. Mpango wa kuhakikisha unapata wawekezaji kwa ajili ya zao hili kama ambavyo Serikali imekuwa ikihakikisha inashawishi wawekezaji kuweza kuchukua maeneo kwa ajili ya kilimo cha miwa ili tuweze kupata sukari na kwenye eneo hili naomba sana Mheshimiwa Bashe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi tukiwategemea sana uwezo wao ni mdogo. Utawapa miche lakini uwezo wa kifedha wa kulima na kupalilia hawana. Kwa hiyo kwenye eneo hili naomba sana Mheshimiwa uone namna ya kuweka wawekezaji waje kuwekeza kwa ajili ya kilimo ili sasa hawa ambao ni wakulima wadogo waweze kuuza kwa hao wawekezaji ambao nao najua lazima kutakuwa na viwanda vikubwa kwa ajili ya kuchakata hayo mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ni eneo la kilimo cha umwagiliaji. Mimi nashukuru mwaka 2016 jimbo langu lilipata bilioni mbili kwa ajili ya skimu za umwagiliaji, lakini kwa bahati mbaya sana Mheshimiwa Bashe, skimu hizo zilikwenda kujengwa kwenye mashamba ya watu, hili ni jambo la kusikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, skimu ya Kalya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Bidyanguze kwa mchango wako, na muda wako umekwisha.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami naomba niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya katika Taifa letu. Pia naomba nimpongeze Waziri, amesoma bajeti yake vizuri, pia wanaomsaidia kwa maana ya Naibu Mawaziri, wanachapa kazi vizuri. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niende moja kwa moja kwenye eneo moja la Bandari ya Lagosa na Sibwesa. Mheshimiwa Waziri, hizi bandari zilitengewa fedha na zilishajengwa kwa kiasi kikubwa tu, bado kidogo kumalizia. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, peleka fedha katika eneo la Lagosa na Sibwesa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi, pamoja na kwamba tunahitaji bandari hizi zianze kufanya kazi pamoja na kwamba meli hazijakamilika, lakini wananchi wa maeneo yale, wanawadai wakandarasi fedha nyingi sana. Yaani watu wamefilisika, watu waliamini kwamba watalipwa lakini baada ya Serikali kusitisha kupeleka fedha pale kwenye zile bandari, wananchi wanapata shida sana. Nakumbuka juzi kwenye semina niliwahi kuongea jambo hili na majibu niliyopata ni kwamba fedha tayari Mkandarasi wa Lagosa ameshapata na kwa hilo naomba nikushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo naomba nilete shukurani ni kwenye daraja la Malagarasi Chini. Ni kweli fedha ilikwenda kwa ajili ya upembuzi yakinifu na kwa sasa hivi taarifa ya Serikali ni kwamba mwezi Novemba Mkandarasi yule atamaliza kazi. Naomba sana amalize kazi mapema iwezekanavyo ili tuanze kuweka mchakato wa kuona namna ya kwenda kujenga hilo daraja kwa sababu ni kiunganishi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, sisi Mkoa wa Kigoma tuko pembezoni na ile barabara ni kubwa ambayo inaweza kututoa kwenye Mkoa mwingine wa Katavi na Mkoa wa Sumbawanga pia. Sasa unaweza kuona kabisa kwamba barabara ile ni muhimu sana na hasa hilo daraja. Viel vile, kwenye barabara hiyo hiyo ambayo ni barabara ya Nsimbo – Kalya, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri, inaendelea kutengewa fedha mara kwa mara, na inasimamiwa vizuri sana na Meneja wa TANROAD ambaye anaendelea kuisimamia na kwa kweli inapitika. Nashukuru sana kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye barabara ya Kalya - Sibwesa, Mheshimiwa Waziri barabara ya Kalya - Sibwesa ni barabara ambayo inakwenda bandarini kwenye hiyo bandari ambayo nimesema ya Sibwesa. Naomba sana, uliweka fedha kwa ajili ya kuifungua na mimi kwenye Mfuko wa Jimbo ile milioni 500 aliyotupatia Mheshimiwa Rais, nikaweka pale, TARURA wakaenda pale kujenga madaraja pamoja na fedha za TANROADS, barabara ile imekwishafunguka, lakini bahati mbaya bado haijakamilika. Naomba sana unapoendelea kujenga na kukamilisha bandari hiyo ya Sibwesa na hii barabara ni vizuri uiwekee fedha ili iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, lakini pia iko barabara hii kubwa ambayo inotoka Tabora. Sisi kipande cha Mpeta – Uvinza ni kilometa 51. Naishukuru Serikali, Mheshimiwa Waziri uliweka fedha na mkandarasi yuko kazini lakini anasuasua, tatizo ni nini? Mheshimiwa Waziri hebu nenda uone inawezekana vifaa ni vichache, lakini inawezekana fedha pia hapati vizuri. Naomba sana kwenye jambo hili kwa sababu kwenye kipindi hiki cha mvua wananchi wamepata shida sana. Kwa sababu diversion anazotengeneza haziko imara, magari yalikuwa yanakwama sana, nakuomba sana na bado wana umbali mrefu sana, kwa kweli jambo hili naomba nipongeze, lakini naomba nisistize kipande kile kiweze kutengenezwa kwa haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa barabara ya Katavi – Uvinza – Kasulu, barabara hii sijasikia imezungumziwa kabisa. Hii yote ni kufungua Mkoa wa Kigoma. Naomba utakapokuja ku–wind up hili jambo kwa kweli ulizungumze kabisa. Hakuna haja ya mtu wa Kigoma kupita Tabora wakati anakwenda kwa Mheshimiwa Tulia pale Mbeya, njia yetu ndiyo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye habari ya meli; nakushukuru umetoa habari nzuri hapa Bungeni kwamba kuanzia mwezi wa sita ambayo ni kesho kutwa tu, mkandarasi anaanza kukarabati Meli ya Mv Liemba. Huo ndio ukombozi wa sisi watu wa Kigoma, yaani Kigoma, Katavi na Sumbawanga ukweli ni kwamba ziwa lile limetufanya tuwe karibu na nchi tatu kwa maana ya Congo, Zambia na Burundi. Sasa nchi zile tunabaki tunaziangalia tu kwa sababu hatuna usafiri wa kwenda kule. Pia ninataka nikwambie Mheshimiwa Waziri, meli zile ndizo zimekuwa zinasababisha kupata uchumi kwenye Mkoa wa Kigoma na uchumi wa mtu mmoja mmoja kwa wananchi wetu wa Kigoma, kwa hiyo ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye eneo lile la utengenezaji wa meli mpya na mimi niungane na wenzangu, meli kubwa sana nadhani itakuwa haiwezi kusaidia, kwa sababu mizigo sio mingi ni mizigo kidogo kidogo. Kwa hiyo, kwa meli ile ambayo inaweza kuwa na tani 2000 tukipata hata meli mbili za tani 1000 kila meli ni jambo jema sana. Itakuwa inakwenda-inarudi haraka haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nizungumzie kwenye uwanja wa ndege wa Kigoma; Mheshimiwa Mbarawa wewe ulikuja Kigoma, sisi Wabunge tulikuwepo, ulisaini mkataba mbele yetu tuliona, tulitaka tuone kazi inafanyika tusiishie kuona mkataba peke yake, wananchi wasije wakafika mahali wakachoka. Kwa kweli nataka nikwambie, Mheshimiwa Rais wetu wananchi wa Kigoma wanampenda sana na wanamwamini sana kama sisi Wabunge tunavyompenda na kama tunavyomwamini. Kwa kweli kwenye majimbo yetu hali ni nzuri na haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi ya maji, barabara za TARURA yaani huwezi kuamini mimi kule kwenye jimbo langu hata huko bondeni kwenye ziwa barabara zimefika, kitu ambacho kilikuwa hakijawahi kutokea wananchi wanashangaa. (Makofi)

Kwa hiyo, mimi nilikuwa naomba nikupongeze na niseme hayo machache lakini pia nikutie moyo, pambana na fanya kazi vikwazo ni vingi lakini mimi ninaamini Mheshimiwa Mbarawa utashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Nashon wakati unataja zile barabara, ile ya kutoka Uvinza inayounganisha Katavi ndiyo hiyo umeitaja au hiyo haipo?

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, hiyo ni nyingine. Hiyo ya Katavi ni nyingine, hii nyingine inaitwa Simbo- Kalya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. NASHON D. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, naomba na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri wa Nishati, ndugu yetu Mheshimiwa Januari Makamba. Kwanza naomba nichukue nafasi hii kwa kusema kwamba, mimi naunga mkono hoja kwa sababu eneo hili ni eneo kubwa nani nyeti. Na kama mwenyewe Mheshimiwa Januari anavyoendelea kulizungumzia, ni kwamba kwa kweli, bila umeme nchi itasimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nizunguimzie kwenye eneo moja, lile la vinasaba ambavyo kimsingi tulikwishakubaliana kwamba TBS ndio ambao wataendelea kuweka vinasaba kwenye mafuta. Mimi naomba kwenye eneo hili niendelee kusisitiza kwa sababu TBS pia ni Shirika la Serikali. Mheshimiwa Waziri aendelee kusimamia jambo hili kwenye eneo la TBS, TBS waendelee kuweka vinasaba kwenye mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwanza naomba nimpongeze Meneja wa TANESCO Wilaya ya Uvinza, anafanya kazi vizuri sana tena katika mazingira magumu. Kuna kipindi alikuwa hana hata gari la kubadilisha transformer kuweka nyingine; kwa sababu mradi huu wa REA ulianza na transformer ambazo ni ndogo kidogo ambazo zilikuwa ni 100, lakini yeye anaendelea kubadilisha kwa gharama za TANESCO, anapoomba fedha anapewa kufanya miradi na anabadilisha sasa kutoka 100 kwenda 150 mpaka 200. Kwa hiyo ni jambo la kumpongangeza sana kwa sababu, sasahivi wananchi wanaendelea kutumia umeme na wakati kwingine wanatumia kwa ajili ya mashine za kusaga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine, katika jimbo langu kuna vijiji 61, vijiji 29 vilishapata umeme, vijiji 32 bado. Hata hivyo naomba nimshukuru Mheshimiwa Januari Makamba, sasahivi tunavyozungumza kuna vijiji sita vinaendelea kuwekewa umeme, ni jambo la kupongeza sana, na kwa hili naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Makamba. Lakini pia kuna njia ya umeme ambayo ni kilometa 104.6 ambao unatoka Kirando kwenda Karirani, ni umbali mrefu. Na umbali huo ndio ambao vijiji hivyo viliwekewa umeme wa jua, na siku zote wamekuwa wakilalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa unaweza kuona kabisa kwamba, hiyo line ambayo imeanza kujengwa ikikamilika itakuwa na uwezo wa kusaidia kuweka umeme vijiji 13. Kwa hiyo vijiji vyangu ambavyo ambavyo havina umeme vitazidi kupungua. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Makamba kwa kazi hiyo nzuri ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naomba niseme; jana Mheshimiwa Makamba amezungumzia kwenye bajeti yake kwamba mwaka ujao wa fedha kwa eneo lile la Malagarasi, umeme ule wa Kv 49, kama sijakosea 49, utakwenda kuanza kujengwa. Na taarifa nilizonazo ni kwamba mkandarasi alikwishapelekwa site. Mkandarasi wa kujenga alishapelekwa site, lakini pia mkandarasi wa kujenga njia ya kupeleka umeme kule wilayani ameshapatikana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, naomba nipongeze kwamba, umeme ule ambao unatoka Tabora ambao unakuja pale Nguruka kwenye eneo la pale Mganza ambapo sub station imeshajengwa, bado ku-install, naomba nikushukuru. Hata mkandarasi wa kuja kuifanya hiyo sub station ikamilike amekwishaletwa pale, na mimi taarifa ninazo na mimi nilimuona, hilo ni jambo jema sana. Pia mkandarasi wa kuleta njia ya umeme kutoka Tabora kuja hapo amekwishaletwa pale site, lakini wa kutoka hapo tena kupeleka kwenye eneo ambalo limeandaliwa ameshapatikana. Kitu ambacho naomba nimuombe Mheshimiwa ni kwenye hawa watu wanaoathirika na hiyo njia, kwenye kuwathamini. Naomba kusiwe na mgogoro kwenye eneo hilo, hawa wananchi wamekuwa na ridhaa na wameacha maeneo yao. Sasa ninaomba sana hao nao waweze kuthaminiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jingine ambalo ninamwomba Mheshimiwa Waziri, ni kwenye eneo la Kijiji cha Nguruka na Kijiji cha Uvinza. Naomba sana, hili jambo nimekuwa nikimwambia siku zote kwamba hawa watu walipangiwa shilingi 320,000 lakini uwezo huo hawana, mimi ndiye ninayewajua. Nashukuru Mheshimiwa Waziri alituma tume, ilikwenda, na nadhani taarifa anayo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu atamke neno, Nguruka warudi kulipa shilingi 27,000 lakini pia, Uvinza warudi kulipa 27,000. Na kubwa sana hivi leo wako kwenye runinga wanaendelea kusikiliza jinsi ambavyo Mbunge wao anamwomba Mheshimiwa Waziri, na wangetamani aseme, ili waweze kusikia, naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja kwamba, hii bajeti iko vizuri na mimi nitakuwa tayari kuipitisha. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami nichangie kwenye eneo hili la Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Mifugo aliwahi kuja Jimboni kwangu kwa lengo moja la kuhakikisha kwamba anagawa vizimba au blocks kwenye eneo la ranch ya Wizara ya Mifugo ili kusudi watu wanaofuga Ng’ombe waweze kupeleka ng’ombe zao pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa hilo lakini pia kwa kazi ile iliendelea pia kwa sehemu imekamilika. Sasa bado kazi ya kuelimisha wale Wasukuma, na wewe ndiyo uje uongee kisukuma na waondoe ng’ombe katika vijiji vyote 61 vya Wilaya ya Uvinza. Sasa hivi wakulima wanalima na hawavuni kwa sababu ya ng’ombe zilivyotapakaa katika Jimbo na vijiji vyote. Sasa Ng’ombe tunazipenda zina maziwa, zina nyama lakini sasa utakula nyama na maziwa bila ugali? Haiwezekani! Sasa uje.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa tu taarifa mchangiaji anayeendelea kuchangia aondoe neno Wasukuma maana anagusa kabila la watu wengi ambao tumo hata humu ndani. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa hiyo siyo, ungesema kuhusu utaratibu kwa sababu umetumia Kanuni tofauti, lakini na wewe Mheshimiwa Bidyanguze jaribu kuji-refrain kutumia majina ya watu. (Makofi)

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, sizungumzi hivyo kwa nia mbaya lakini ndiyo wafugaji na ndiyo matajiri wa ng’ombe, Waha hatufugi ng’ombe sisi ni wakulima. Kwa hiyo, akija yeye ana lugha ambayo ataweza kuongea nao ili waweze kuondoa ng’ombe katika vijiji na waweze kupelekwa katika eneo ambalo Waziri alikuja kuliandaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niondoke kwenye eneo hilo la mifugo ambayo mifugo yetu katika eneo la Wilaya ya Uvinza inakaribia takribani mifugo Laki Mbili na mifugo haiharibu tu mazao ya wakulima inaharibu na reserve ya misitu ya Serikali ambayo imewekwa pale, ambayo lengo la Serikali kuacha misitu ile ni kuendelea kuwa na mvua na sifa ya Mkoa wa Kigoma ni kweli kwamba hatujawa na ukame hata siku moja, sasa kwa ujio wa hizi ng’ombe Laki Mbili maana yake kama Serikali haikufanya juhudi ya kuhamisha hizo ng’ombe maana yake na Kigoma tunakwenda kuwa na jangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nihamie kwenye eneo la uvuvi. Naomba nikupongeze Mheshimiwa Waziri pia Naibu Waziri nikupongeze. Mheshimiwa Waziri, ulipokea ujumbe wa Wavuvi kutoka Mkoa wa Kigoma kwa ujumla wake wavuvi wa Jimbo la Kigoma Kaskazini na Kigoma Mjini Pamoja na Kigoma Kusini. Ulitoa elimu nzuri na sasa hivi Waziri au Naibu Waziri anapokwenda katika Jimbo la Kigoma Kusini au Kigoma kwa ujumla haendi tena kuchoma nyavu hafanyi hiyo kazi tena, kwa sababu tayari elimu ilikwisha patikana. Juzi alikuwepo Naibu Waziri, kwakweli hakuna nyavu alizooneshwa ili achome, kwa hiyo Waziri elimu ile uliyotoa wakati wale viongozi wa uvuvi wamekuja ile elimu iko vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo bado tunahitaji Wizara iweze kuwasaidia wavuvi wetu vifaa vya kisasa vya uvuvi. Sasa hivi wavuvi wa Ziwa Tanganyika katika Majimbo Matatu wanakwenda kuvua na wanarudi bila samaki, wanarudi bila dagaa na vyombo wanavyotumia ni vilevile walivyokuwa wakitumia zamani wakati samaki zikipatikana na dagaa zikipatikana. Kwa hiyo, nadhani imefika wakati sasa Wizara ilete wataalam, iweze kubuni ni vyombo gani vya kisasa viweze kuletwa katika Mkoa wa Kigoma kwa maana ya wavuvi wetu waweze kufaidi matunda ya nchi ili waweze kuvua. Siamini kwamba samaki katika Ziwa Tanganyika hawamo! Kwa mujibu wa tafiti zilizopita samaki bado ni wengi ingawaje nimeongea na Afisa Uvuvi ameniambia kwamba TAFIRI wamefanya utafiti mwingine, tunaomba Wizara utafiti huo uletwe tujue samaki wapo kiasi gani na wapo katika maeneo gani? Tumechoka wavuvi wetu kwenda kuvua kwa kubahatisha gharama ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipongeze shirika moja linaloitwa ‘TUUNGANE’ hili shirika linawasaidia wananchi wa jimbo la Kigoma Kusini sijui kama majimbo mengine kama wapo lakini hawa ndiyo ambao kidogo wanawasaidia wavuvi katika Ziwa Tanganyika. Nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri amekuja mara mbili mfululizo pale Buhingu, Nakatumbi, wamejengewa vyombo vya uvuvi viwili vya thamani ya Milioni 38, jambo la kuunga mkono na jambo la kupongeza sana hawa watu wanaojiita tuungane ni shirika zuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Buhingu pia wanajenga mwalo wenye thamani ya Milioni 300 unaweza ukaona kama ni shirika …

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Bidya kengele ya pili.

MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, basi naomba kwa hayo machache niunge mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii naomba nichangie na mimi kwenye hotuba hii ya Waziri wa Nishati ambayo ameileta kwetu ili tuweze kufanya uchambuzi, lakini kabla sijaendelea naomba nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba nimpongeze mdogo wangu Mheshimiwa January kwa kazi nzuri anayofanya kwenye Wizara hii na mimi lazima niwaambie na nimwambie kwamba Mheshimiwa January ninamfahamu na kwa kweli Mheshimiwa January yupo makini katika uongozi wake lakini ninaimani kabisa kwamba Wizara hii ipo kwenye mikono salama pamoja na Naibu wake Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiit, sisi Wabunge wa Kigoma naamini tulikuwa tuwe wakali sana kama Mheshimiwa January hakuja na mpango wa kuhakikisha kwamba tunapata umeme wa Gridi ya Taifa katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wa Gridi ya Taifa imekuwa ni kizungumkuti kwa maana ya kwamba Wabunge wengi waliopita walikuwa wakizungumza na kulalamika sana kuhusu Gridi ya Taifa kutokuingia katika Mkoa wa Kigoma na imepelekea Kigoma kuendelea kubakia nyuma sana kimaendeleo kwa sababu tuliendelea kukosa umeme wa uhakika, haiwezekani kukawekezwa viwanda katika Mkoa wa Kigoma ambao unaendelea kutumia mashine zinazotumia dizeli, isingewezekana kupata maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa January kwa kuja na mkakati wa kuhakikisha kwamba kabla ya mwaka huu haujaisha tumepata umeme wa Gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma mimi ninakuhakikishia sisi Wabunge wa Kigoma sasa tunakwenda kukuunga mkono katika kupitisha bajeti yako hii ili kusudi tupate huo umeme wa Gridi ya Taifa ili na sisi tuweze kupata viwanda sasa kwa sababu tunaenda kuhakikisha kwamba tunakwenda kuwekeza kwenye kilimo cha michikichi, sasa je, michikichi itakapolimwa, je, bila umeme kiwanda kitakwenda kupatikana namna gani, kwa hiyo hili jambo ni jema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba nizungumzie kwenye eneo la umeme wa maji wa Mto Malagarasi. Mheshimiwa Waziri eneo hili huu mradi umekuwa ukitajwa katika miaka mbalimbali iliyopita, lakini nafurahi kuona kwamba Mheshimiwa January anakwenda kuandika historia katika mradi huu kwenda kuanzishwa mwaka huu wa fedha, naomba nikupongeze sana Mheshimiwa January na jambo hili ukilifanya kwa kweli utakuwa umeandika historia kwa wananchi wa Kigoma kwa sababu huu mradi utakwenda kutusaidia sisi Kigoma lakini pia na Mkoa wa Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye eneo hili naomba uhakikishe wananchi wanafidiwa maana yake huu mradi unakwenda kuutekeleza kwenye Jimbo langu la Kigoma Kusini, wananchi walisimamishwa katika maeneo yao wasiendeleze kilimo, sasa naomba uhakikishe kwamba unapokwenda kutekeleza mradi huu wananchi hawa wawe wamefidiwa. Ninayo taarifa kwamba Gridi ya Taifa inapopita kote tayari wananchi wamekwisha tambuliwa wa maeneo yale wanaokwenda kupoteza baadhi ya mazao na maeneo kwamba tayari, lakini sina taarifa ya kwamba tayari wamelipwa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba eneo hilo waweze kulipwa fidia wananchi, wasibaki wanalalamika, mradi wanautaka lakini tafadhali sana Mheshimiwa Waziri fidia itolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la umeme wa REA mimi nina vijiji 61 lakini nashukuru kuona kwamba kusema kwamba tunavyo vijiji 29 tayari vimeshapata umeme, lakini bado vijiji 32 havijapata umeme, lakini ninavyo vitongoji 350. Sasa unaposema umeme unakwenda kupatikana mwishoni mwa mwaka huu, mimi siamini kwamba vitongoji hivi vitakuwa vimekwenda kupata umeme kwa sababu kuna Mbunge mwenzangu alizungumza juzi kwamba yeye alipata t-shirt ambayo inaonesha kwamba sasa tunakwenda kwenye vitongoji wakati kumbe hata vijiji vyenyewe bado hatujakamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina vijiji 32 ni vingi sana, lakini ukienda kwenye vitongoji 350 yaani vitongoji vyenyewe vina ukubwa sawa na vijiji, sasa kama umeme umechelewa kwa muda huu kwa vijiji 61 tu, je, vitongoji 350 itachukua muda gani, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri wananchi tuwaambie ukweli kwamba ni lini umeme utapatikana katika vijiji vyetu, lakini ni lini umeme utapatikana kwenye vitongoji. Lakini tukizungumza kwamba ni mwaka huu mwezi wa 12, mimi siamini kwamba hilo jambo litawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika Jimbo langu pia wapo wawekezaji wa umeme mmoja anaitwa Jumeme na mwingine anaitwa Power Corner; hawa watu wamechukua baadhi ya kata kwa maana ya vijiji wamepeleka umeme lakini wananchi wanalalamika sana, wanalalamika mambo mawili, kwanza moja umeme haupo yaani umeme haupo wakati wa mvua umeme haupo, hata wakati wa kiangazi umeme haupo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaweza ukajiuliza hivi hawa wananchi kupewa huu mradi kwa hawa watu wa Jumeme na Power Corner maana yake ilikuwa ni nini, wanahisi kwamba Serikali iliwadanganya, lakini kero nyingine ya pili ina maana wao wanapewa unit mbili kwa wiki, sasa unit mbili ni ndogo sana na ukilinganisha kwamba umeme wenyewe haupo, kwa hiyo wananchi wanalalamika, wakati mwingine wanaweka vitu vyao kwenye deep freezers zao, lakini mwisho wa siku vinaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini makampuni haya ofisi zao hazijulikani, wananchi hawajui waende kulalamika wapi, lakini pia lipo jambo ambalo limelalamikiwa na Wabunge wengi hili ambalo baadhi ya vijiji vimeongezewa kutambuliwa kwamba ni miji waweze kulipa shilingi 320,000 kuingiza umeme; kwa kweli ni jambo la kushangaza sana.

Mheshimiwa Waziri unafahamu Nguruka na unafahamu Uvinza hivi ni vijiji, imekuwaje na hawa Nguruka na Uvinza waweze kuwekwa kwenye tariff ambayo inalipwa na mijini? Naomba hili jambo uende kuliangalia, nimefurahi kwenye taarifa yako ulipokuwa unatusomea bajeti kwa kweli imeonesha kwamba lalamiko hilo limefika kwako Wizarani, lakini umetuma Tume ya kwenda kuchunguza uhalisia huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba jitahidi sana Mheshimiwa Waziri Nguruka watu waende waone na Uvinza wafike, hawa wakifika Uvinza au wakifika Nguruka hakuna sifa ya kuongezewa ikawa shilingi 320,000 hawana hiyo sifa hata Uvinza hawana hiyo sifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nimpongeze Mheshimiwa Waziri, lakini nakuomba sana umeme wa Gridi ya Taifa ufike Kigoma, lakini na huu mradi wa umeme wa Malagarasi tuanze kuona kazi ikiendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo mimi naomba niunge mkono hoja nasema kazi iendelee, ahsante kwa nafasi. (Makofi)