Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Geophrey Mizengo Pinda (98 total)

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Aidha, nina swali moja la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama vile Serikali ilivyoona umuhimu wa kuanzisha Mahakama kwa mfano za Kazi (Labor Courts) au Mahakama za Mafisadi (Economic Crimes Courts) au Commercial Courts (Mahakama ya Biashara) kwa ajili tu ya kutengeneza mazingira wezeshi ya kiuchumi lakini pia ya uwekezaji. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuanzisha Divisheni ya Familia (Family Division) katika Mahakama itakayoshughulika na masuala ya ndoa, talaka na mirathi ili kuharakisha mashauri haya na kuwaondolea wanyonge adha wanayopata ya kuchelewa kwa mashauri haya katika mfumo wa kawaida wa mahakama na hasa ukizingatia wanyonge hao ni wajane? Sisi tunajua kuna legal maxim ambayo inasema justice delayed is justice denied (haki iliyocheleweshwa ni sawasawa na haki iliyonyimwa). (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab, Mbunge Viti Maalum kutoka Kigoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wake ni mzuri sana na chombo hiki ndiyo chombo chenye kazi ya kutunga sharia kwani sheria zote zinatungwa hapa Bungeni. Tusema tu tumepokea wazo lake na tutalipitisha katika mamlaka mbalimbali za kuangalia ile modality ya kuanzisha chombo kama hiki ili tuweze sasa kufikia maamuzi halisi. Naamini Bunge lako Tukufu litapata nafasi ya kupitia na kutoa maoni mbalimbali juu ya muundo utakaowezesha kutoa haki kwa makundi husika. Ahsante.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwanza niishukuru Serikali kwa majibu mazuri kwamba na matumaini kwamba tutajengewa Mahakama yetu mwaka 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini je, kwa kipindi hiki ambacho Mahakama ya Wilaya ya Uyui iko ndani ya chumba kidogo sana katika jengo lile la DC. Je, Serikali ina mpango gani wa kutafuta jengo kubwa ili kutatua tatizo hilo la jengo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa vile yako majengo ya Mahakama ya awali ya Mwanzo ya Upuge yametelekezwa na ni makubwa yana nyumba za wafanyakazi na sasa kuna umeme wa REA, lakini pia kuna maji ya Ziwa Victoria na barabara nzuri; je, Serikali haioni ni busara kuanza kutumia majengo yale ya Mahakama ya Mwanzo ya Upuge kwa shughuli za Mahakama ya Wilaya ya Uyui?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria nipende kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maige kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza hili la kutumia chumba kidogo hili tutalifanyia kazi haraka sana, nadhani mamlaka zinanisikia huko ni muhimu kuanza kufanya tafiti ili kujua tunaweza tukapata chumba wapi kikubwa ambacho kinaweza kikatoa huduma hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii Mahakama ya Mwanzo Upuge nitaifuatilia kwa karibu kuona inaanza kazi mara moja kwa sababu kwanza, tunasema tunaupungufu wa vyumba halafu kumbe kuna nyumba zingine zimekaa hazifanyi kazi, kwa hiyo nadhani hili tumelichukua na tutalichukulia hatua haraka sana, ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kuniona na mimi niulize swali la nyongeza kwa Wizara hii yetu ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la Mahakama ya Wilaya ya Uyui ni sawasawa na tatizo lililoko pale kwetu Wilaya ya Busega na kesi za Mahakama ya Wilaya zimekuwa zikienda kusikilizwa Wilaya jirani ya Bariadi.

Je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kutumia jengo lililopo la Mahakama ya Mwanzo ili litumike kusikiliza kesi za Mahakama ya Wilaya, lakini hivyo hivyo ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa…

NAIBU SPIKA: Swali ni moja Mheshimiwa, swali la nyongeza ni moja.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba Waziri wa Katiba na Sheria nipende kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kutumia jengo la Mahakama ya Mwanzo inategemea sana sifa ya hilo jengo kwa sababu vingine ni vyumba vidogo ambavyo haviwezi kuhimili huduma ambazo zinatakiwa kutolewa kwenye ngazi ya Wilaya, lakini tutalichukua na kulifanyia utafiti ili kuona kama hiyo Mahakama ya Mwanzo ina sifa zinazostahili kuwa kwenye kiwango cha matumizi ya Wilaya na tukijiridhisha huduma itaanzishwa mara moja kwenye eneo husika, ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali.

Kwa kuwa, Wilaya ya Nyang’hwale ina upungufu mkubwa sana wa Mahakama za Mwanzo, napenda kuiomba Serikali ianzishe Mobile Court katika Kata za Busolwa, Nyang’hwale, Kaboha na Shabaka; kwa kuwa Wilaya ya Nyang’hwale ina upungufu wa watumishi kama vile Mahakimu na Makarani.

Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Mahakama hizo?

Swali la pili; je, Serikali ipo tayari kutuongezea Mahakimu pamoja na Watumishi kama vile Makarani?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nassor Amar Hussein, Mbunge wa Nyang’wale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza hili la mobile court tumelipokea na tutalifanyia kazi ili kuona uwezekano wa kata hizo ambazo hazijapata majengo ziweze kufikiwa na huduma hii.

Mheshimwia Spika, lakini vile vile, kuhusu watumishi tunaendelea kutegemeana na nguvu ya Serikali katika kupata uwezo wa kuajiri. Tunachoweza kuahidi tu ni kwamba tutakapopata nafasi ya kuajiri basi tutaangalia na suala la kupeleka watumishi katika maeneo haya ambayo Mheshimiwa Mbunge anayaeleza. Ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wilaya ya Rungwe Mahakama yake ya Wilaya ni jengo la siku nyingi sana. Ni lini Serikali itatusaidia kujenga jengo jipya ambalo litakidhi vigezo vya kuweka wafanyakazi na kuwa na nafasi nzuri ili waweze kufanyakazi kwa weledi na kwa ufasaha zaidi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda ambalo anataka kujua lini Serikali itajenga Mahakama katika Wilaya ya Rungwe.

Mheshimiwa Spika, Mahakama iko kwenye mpango ambao ni wa kipindi hiki tulichonacho cha mwaka wa fedha kuanzia mwaka 2021 mpaka 2025. Katika kipindi hicho tutahakikisha maeneo yote ambayo hayana Mahakama za Wilaya majengo mapya yanaenda kujengwa kwenye maeneo yote ambayo hayana Mahakama za Wilaya.

Kwa sasa hivi kwenye eneo hilo la ujenzi ni matarajio yangu kwamba ifikapo mwaka 2025 eneo hili la Mahakama tutakuwa tumeshamaliza kabisa shughuli za ujenzi. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kwamba, tunakwenda kukujengea hii Mahakama katika kipindi cha awamu hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Hapa ningependa kuikumbusha Serikali, kwamba si mara moja, mara mbili, mara tatu; na hata hivi karibuni tarehe 25 Agosti tulimsikia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akilisemea eneo hili la ucheleweshaji wa kesi kufikia hukumu na idadi kubwa ya mahabusu. Vilevile, tulishamsikia Jaji Mkuu wa Mahakama zetu hapa nchini akilisemea pia suala hili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo maswali yangu mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hivi sasa idadi ya mahabusu ni 17,000 ukilinganisha na idadi ya wafungwa ambayo ni 14,000; na wakati huo huo Serikali haitoi bajeti ya aina yoyote kwa ajili ya chakula; kwa sababu Magereza imepewa maelekezo kwamba ijitegemee kwenye chakula, sasa wale wafungwa 14,000 wanazalisha chakula kwa ajili ya kujilisha wao wenyewe na pia kulisha wale mahabusu 17,000. Je, Serikali haioni ipo haja ya kupitia upya Sheria ile ili itafute namna ya kuwawezesha hawa mahabusu angalau wazalishe chakula chao wenyewe wanachokula?

Mheshimiwa Spika, na swali langu la pili, kwa kuwa majibu ya Serikali wamesema kwamba viko vyombo mbalimbali ambavyo vinahusika kwenye kutoa hukumu hizi za kesi. Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuweka ukomo wa muda ambao utatumika kuanzia upelelezi mpaka kutolewa kwa hukumu kwa kulingana na uzito wa kesi zenyewe? Kwa sababu, ukweli ni kwamba, tuchukulie mfano mtu amebaka halafu kesi yake inaendelea kwa miaka 10...

SPIKA: Mheshimiwa Neema inatakiwa swali. (Kicheko)

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, sawa. Kwa hiyo swali langu ni kwamba, je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kupitia upya mfumo mzima wa Mahakama na kuweka ukomo wa muda wa upelelezi mpaka kutoa hukumu? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Lugangira kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hili la kupitisha sheria ili mahabusu waanze kufanya kazi wakati wakisubiri kesi zao kimsingi ni jambo ambalo tutakuwa tunavunja vile vile haki za binadamu. Kwa sababu wakati mtu anasubiri upelelezi wake wa kesi hajahukumiwa kuwa mfungwa, ukianza kumfanyisha kazi maana yake umemhukumu kabla ya wakati wake. Kwa hiyo, mahabusu huwa wanafanya kazi ndogo ndogo tu za usafi wa mazingira waliyopo, lakini si kuwafanyisha kazi kama wafungwa. Kwa sababu, mfungwa kifungo chake kinamruhusu sasa kufanyishwa kazi kwa ajili ya kurekebishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu hili suala la ukomo wa upelelezi, tunao ukomo wa upelelezi kutegemeana na mazingira ya kesi yenyewe. Kwa mfano, kesi nyingine zimepewa siku 60, kesi nyingine zina miezi sita, lakini kesi nyingine kulingana na mazingira yake zinaweza zikaenda muda mrefu; kwa mfano kesi za mauaji. Kwa hiyo hili linatekelezwa Kisheria.

Mheshimiwa Spika, isipokuwa kama nilivyotoa maelezo yangu kwenye jibu la msingi, kuvitaka vile vyombo vinavyohusika na michakato kuharakisha michakato. Hiyo itasaidia sana kupunguza baadhi ya kesi ambazo kimsingi zinapelekwa pale lakini zinakuwa hazina mashiko ya kuendelea kuwa Mahakamani. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wakati anajibu swali alisema kwamba, kesi zinachelewa kwa sababu kuna vyombo mbalimbali vinachakata. Lakini labda nikuulize Mheshimiwa Waziri, hivi kuanzia mwaka 0 mpaka miaka 7, vyombo kuendelea kuchakata wakati watu wako magereza, unadhani ni sawa? na kama si sawa, kwanini sasa, badala ya kutoa maagizo hapa Bungeni usiwe ni wakati muafaka kwa Serikali kufanya kazi ya ziada kwenda kuchunguza kinagaubaga ili kuja na majibu ambayo yatasaidia wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, muda wa kukaa mahabusu utategemea mwenendo wa upelelezi, na hivyo ni halali kabisa wakati mtu anapelelezwa, ambaye atakuwa yuko nje ya vigezo vya dhamana kuendelea kuwa chini ya Magereza. Kwa hiyo muda unaangaliwa na uzito.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, kuhusu uchunguzi, kwamba tuunde timu ambayo itasaidia kuangalia kwa ukaribu na kwenda kufanya utafiti wa kina badala ya kutoa maagizo Bungeni; hapa nilikuwa natoa kama msisitizo tu lakini ukweli Serikali tulishaanza hiyo kazi na ukweli kwa kipindi hiki cha kuanzia Januari mpaka sasa naamini wazi watu wote mnaona kasi ya kuondoa mahabusu wasiokuwa na kesi zenye mashiko imeongezeka sana na mahabusu zimeanza kupumua. Ahsante. (Makofi)
MHE. WANU HAFIDH AMEIR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kumuuliza swali moja la nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyotambua kwamba, kuna kazi nzuri ambayo inafanywa na wasaidizi wa kisheria nami natambua kazi nzuri hiyo na ya kizalendo ambayo wamekuwa wakiifanya wasaidizi wa kisheria katika kusaidia wanawake na wananchi kwa ujumla katika level ya chini kabisa katika nchi yetu. Swali, Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kuweka utaratibu maalum wa kuwasaidia hawa wasaidizi wa kisheria, ili kuwafikia wananchi wengi zaidi Tanzania, lakini hasa kuwafikia wanawake ambao hasa ndio wanaingia katika matatizo ya kisheria katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa anachokieleza, lakini Wizara imekuwa na utaratibu mzuri sana wa kutoa mafunzo mbalimbali katika maeneo mbalimbali kwenye haya makundi ya watoa msaada wa kisheria. Tumekuwa tukipita katika kila mkoa kujaribu kutoa hii elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ombi lake kwamba, wanawake wengi washirikishwe kwenye suala hili ni ombi muhimu, lakini nipende tu kuwaarifuni kwamba, kumekuwa na shida moja ya akinamama kushiriki kwenye hili zoezi. Tulitembelea Mwanza akinamama walikuwa wanalalamika kwamba, hawaruhusiwi na waume zao kwenda kushiriki kwenye shughuli hii kwasababu, sehemu kubwa sana ya shughuli hii ni kujitolea. Kwa hiyo, kama mtatusaidia Waheshimiwa Wabunge kuwahamasisha akinamama, hii ni kazi huru ambayo mtu yeyote anaweza akaifanya kulingana na kuguswa kwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nipende tu kusema Wizara haina kizuizi kwa akinamama kushiriki kwenye hili zoezi la utoaji wa huduma za kisheria, lakini sisi wenyewe tuna chuo chetu cha sheria pale Dar-Es-Salaam (Law School) inafanya kazi hiyo. Kwa hiyo, wataalamu wengi ambao wanatoa huduma hizi katika maeneo mbalimbali nchini wanapita kwenye hicho chuo, lakini tuna watu wa Legal Service Facility; ni taasisi binafsi ambayo nayo imeendelea kutusaidia kuwapa elimu wananchi ambao wamejitolea kutoa msaada wa kisheria katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Wizara tumefanya ziara katika maeneo ya Simiyu, Tanga na sasa hivi maafisa wetu wapo Shinyanga na wengine wako Kasulu. Nia ya msingi ni kuwakusanya hawa watoa msaada wa kisheria na kuwapa mbinu mbalimbali za jinsi ya kuwasaidia wananchi wetu, ahsante.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amesema kwamba Serikali haina mpango wa kusomesha Stenographer nchini Tanzania; na kwa kuwa kazi hizi zimekuwa zikifanywa na Majaji na Mahakimu wenyewe; swali langu kwa Serikali: Je, Serikali haioni kwamba inawaongezea mzigo Majaji na Mahakimu wasome, watoe hukumu na pia wanachukua jukumu la kuandika? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na malalamiko mengi sana nchini Tanzania kwamba baada ya hukumu unakuta mwananchi inamchukua muda, hata mwezi mmoja kupata ile hukumu yake; hii yote ni kwa sababu hatuna stenographer mle Mahakamani: Je, Serikali haioni kwamba inawakosesha wananchi haki yao ya kupata hukumu zao mara tu kesi inapohukumiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Mheshimiwa anasema Waheshimiwa Mahakimu na Majaji wanakuwa na mzigo mkubwa sana wakati wanasikiliza kesi na wakati huo huo wanachukua uandishi, ni kweli lakini katika mazingira ya kawaida Serikali kama nilivyoeleza mwanzo kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba hawa watu hawajaingizwa kwenye mfumo wa utumishi wa Mahakama. Kwa maana hiyo, Serikali inapitia utaratibu mzuri utakaowezesha hawa watu, kwa sababu itakuja kama idara mpya kama zilivyo idara nyingine za kiutendaji kwenye Serikali hii. Utaratibu wa kuanzisha idara mpya una milolongo yake katika kuangalia masuala mbalimbali. Tunajua wazi kwamba ni mzigo, ni kweli, ndiyo maana Serikali imeendelea kuupitia mchakato wa kuanzisha section hii Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, kuchelewa kwa hukumu siyo kwa sababu tu hatuna hawa watu, hili ni jambo ambalo lina mambo mbalimbali ambayo yanajitokeza pale Mahakamani. Nikuhakikishie tu kwamba mpaka sasa hukumu hazichelewi zaidi ya mwezi mmoja. Tumeendelea kukaa na Mahakimu na kuona uharakishaji wa utoaji wa hukumu zao.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa sasa hivi tunaelekea kwenye Mahakama ya Kiswahili, kwa hiyo, vitu vingi vitarahisishwa baada ya muda siyo mrefu na mambo yote yatakaa sawa. Ahsante. (Makofi)
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri yaliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Wilaya ya Kilolo haina majengo ya Mahakama na hivi sasa majengo yanayotumika ni ya Mahakama ya Mwanzo. Je, ni lini Serikali itajenga majengo ya Mahakama ya Wilaya ya Kilolo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Tarafa ya Mazombe kuna Mahakama ambayo ilijengwa enzi za mkoloni na haijawahi kufanyiwa ukarabati wowote. Je, ni lini Serikali itakarabati majengo hayo ili yaweze kuendana na hadhi ya sasa na haki iweze kutolewa katika mazingira mazuri?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Wilaya ya Kilolo itaingizwa kwenye mpango wa ujenzi Kwa kipindi cha mwaka 2022/2023. katika kipindi kijacho cha fedha tunajenga ile Mahakama ya Mwanzo ambayo ipo Tarafa ya Mahenge na kwa ile ya Wilaya tutaanza kuiweka kwenye mpango nilioutaja.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu ukarabati wa ile Mahakama ya Mazombe, hii nayo tutaiweka kwenye mpango wa 2022/2023. Hii itaendana na ukarabati wa maeneo mengine yote ambayo tumeendelea kuweka mikakati kwa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, napenda tu kusema, katika kipindi cha mwaka 2021/2022 baadhi ya miradi yetu ambayo itaendeshwa katika kipindi hicho tumeiainisha tayari na katika ngazi ya wilaya tutakuwa na Mahakama nyingi sana ingawa kwenye mpango huo wilaya yake haipo. Kutokana na muda ningeweza kuziorodhesha wilaya hizi lakini kwa sasa inatosha kusema hivyo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwanza nionyeshe furaha yangu kwa Serikali kwa kukubali kujenga hii Mahakama ya Mwanzo ya Hydom. Swali, Mahakama ya Wilaya bahati mbaya eneo lake limepitiwa na barabara, je, Wizara ina mpango gani wa kuingiza kwenye bajeti zao ili Mahakama ile ipate kujengwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Waziri amesema Mahakama imeanza kujengwa, je, yupo tayari sasa kwenda Hydom kuona ule ujenzi unaendeleaje ndani ya Jimbo la Mbulu Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtoe wasiwasi kwenye mfumo huu wa Mahakama asicheze ile sarakasi aliyokuwa ameiahidi kwenye Wizara ya Kilimo. Kwa hiyo nipende tu kumuhakikishia kwamba kwenye swali lake la kwanza la nyongeza kuhusu ile Mahakama ya Wilaya kupitiwa na barabara hilo tutalifanyia kazi na kwa kushirikiana naye tutajua namna ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili la kutembelea Mahakama inayoendelea kwenye ujenzi, nipo kwenye ratiba leo ninapomaliza kujibu swali hili nakwenda huko Hydom. Kwa hiyo nimualike tu Mheshimiwa Mbunge tufuatane naye kwa sababu tunahakiki yale majengo yanayoendelea kujengwa. Ahsante sana.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nitaomba kuuliza swali moja la nyongeza, ila naomba pia kwamba Serikali isiwe inatoa majibu tu kwa ajili ya kutuliza Wabunge, lakini kwa kweli ije na kutekeleza yale ambayo wanayasema kwenye majibu yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu; jiografia ya Jimbo langu la Arumeru Mashariki ni ngumu, kwa maana ya kwamba Mlima Meru ambao ni mlima mrefu wa pili hapa nchini uko katikati ya jimbo na kuwafanya wananchi walioko Mashariki na Kaskazini mwa mlima huo, kupata shida kufuata huduma ambazo zinapatikana Kusini mwa mlima pamoja na kufika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya.

Je, sasa hivi Serikali haioni kwamba ni muhimu sasa kujenga Mahakama ya Mwanzo Kata ya Ngarananyuki ili wananchi walioko Kaskazini mwa mlima huo waweze kupata huduma za Mahakama? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, tuko kwenye mkakati maalum wa kuhakikisha kwamba ifikapo mwaka 2025/2026 nchi nzima itakuwa imefikiwa na Mahakama za Mwanzo kwenye ngazi za Makao Makuu ya Tarafa zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Ngarananyuki kupata Mahakama, tunalichukua ingawa katika kipindi hiki cha fedha ambacho tunakijadili sasa kilishapita, tutalipa umuhimu kwenye kipindi kijacho cha fedha. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Makete.

Mheshimiwa Naibu Waziri Tarafa ya Ikuo haina huduma kabisa ya Mahakama; na ni umbali wa kilometa karibu 170 kwenda kufuata huduma ya Mahakama kwenye Tarafa ya Matamba:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama kwenye Tarafa ya Ikuo kwa sababu kwa muda mrefu tumekuwa tukiomba huduma hiyo na hatujapewa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi na jibu la nyongeza la Mheshimiwa, tutakuweka kwenye kipaumbele kwenye bajeti baada ya hii tunayoijadili leo. Ahsante. (Makofi)
MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza. Wilaya ya Songwe ni Wilaya mpya toka mwaka 2016 na nimekuwa nikiahidiwa hapa kila mwaka kwamba tutajenga Mahakama ya Wilaya, lakini mpaka sasa Serikali haina mpango wowote. Viwanja vipo, hati ipo, lakini mpaka leo hakuna jengo la Mahakama. Nirudie tena kwa mara ya tano:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Wilaya ya Songwe?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mulugo naomba tu asiwe na wasiwasi. Katika kipindi kijacho hiki cha fedha ambacho mmetupitishia bajeti yetu Songwe imo kwenye huu mpango. Kwa hiyo, muda mfupi ujao tutaanzisha hii miradi ya ujenzi katika eneo lake kwa kupitia fedha ambazo mmeziidhinisha wenyewe hapa.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mahakama ya Mwanzo ya Liuli ilijengwa toka kipindi cha mkoloni na ikawa imeharibika sana na kilichotokea ni Mahakama kuhama kabisa eneo hilo na kwamba shughuli za Mahakama haziendelei:-

Je, ni lini Mahakama hiyo itarejeshwa katika nafasi yake kama ilivyokuwa mwanzo hapo Liuli?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tunakiri kwamba Mahakama nyingi zimechakaa. Kama nilivyoeleza katika maelezo yangu ni kwamba, mkakati wa kukarabati na kujenga majengo mapya kwenye maeneo ambayo hayana Mahakama, ukomo wake ni 2025 ambapo namwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo la Liuli tunalichukua na katika kipindi kijacho cha fedha tutahakikisha tunawasogezea hii huduma ya ukarabati wa Mahakama yao. Ahsante.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hitaji la Nkoaranga ni sawa sawa na hitaji la Wilaya ya Buhigwe. Wananchi wa Buhigwe wanapata huduma za Mahakama ya Wilaya kwenye Wilaya nyingine ya Kasulu:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mpango wa mwaka 2021/2022 ambao tayari bajeti yake imeshapitishwa Buhigwe ipo katika mpango wa kujengewa Mahakama ya Wilaya. Kwa hiyo, asubiri tu mageuzi kwenye eneo lake. Ahsante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri yanayotia matumaini ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hizi Tarafa ambazo zimetajwa zenye Mahakama kwa maana ya majengo; Mahakama kujenga ni jambo moja na kutoa huduma ni jambo la pili: Je, Serikali ipo tayari kuhakikisha kwamba Mahakimu wanakuwepo muda wote katika hizi Tarafa nne ambazo zina Mahakama tayari? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mahakama ya Wilaya ya Kalambo sasa hivi wanatumia jengo la CCM na hivyo sisi kama CCM tunaona kama wanatunyima mapato: Je, Serikali ipo tayari katika mpango wa kujenga Mahakama za Wilaya, Wilaya ya Kalambo ikapewa kipaumbele kujenga Mahakama ya kisasa yenye kulingana na hadhi ya Wilaya yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu Mheshimiwa Kandege, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza linahusu masuala ya watumishi, Mahakimu. Ni mpango wa Mahakama kuendelea kuongeza idadi ya Mahakimu ili waweze kutosheleza ingawa kwa kweli bado watumishi ni tatizo kubwa katika sekta mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni la kuhama kwenye majengo ya CCM na kurudi kwenye majengo ya Mahakama. Kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi ni kwamba tunao mkakati ambao kufikia 2025/2026 nchi nzima, Makao Makuu ya Wilaya zote yatakuwa na majengo mapya ya Mahakama zetu na Makao Makuu ya Tarafa zote nchini yatakuwa yamepata hayo majengo. Kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa awe mvumilivu kidogo. Ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Najua Serikali mna mkakati wa kujenga Mahakama kila Wilaya. Wilaya ya Bunda haina jengo la Mahakama, imepanga kwenye nyumba ya Mzee Wasira muda mrefu, sasa hivi wamehamia kupanga eneo lingine. Ahadi mlitoa tangu enzi ya Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe akiwa Waziri wa Katiba na Sheria. Nataka kujua ni lini Mahakama ya Wilaya ya Bunda itajengwa ya kwao?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu Mheshimiwa Ester Bulaya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kama mnavyofahamu nchi inapitia changamoto mbalimbali. Kwa sasa kama nilivyoahidi, kufikia 2025 sehemu zote ambazo hazina Mahakama za Wilaya na Makao Makuu ya Tarafa zote katika ngazi ya Kata zitakuwa na majengo mapya. Tuvumilie, tutaendelea kuazima majengo lakini mwisho wetu tumeuweka kwenye 2025 iwe ni mwisho wa habari hii. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, niishukuru sana Serikali kwa hatua za haraka ilizochukua. Ninavyozungumza sasa tayari msingi wameshaanza kuchimba. Pamoja na hayo, kwa kuwa kutoka Busega kwenda Bariadi ambako sasa kesi hizi zinaendeshwa za Kiwilaya ni kilometa takriban 70 na pale Makao Makuu ya Wilaya tuna jengo la Mahakama ya Mwanzo.

Je, Serikali sasa haioni haja ya kuturuhusu kutumia jengo lile angalau kwa hiki kipindi ambapo bado tunasubiri jengo letu kukamilika, kusikiliza kesi za kiwilaya ili kuondoa huu usumbufu wa wananchi kwenda Bariadi na kutumia gharama kubwa ambazo wakati mwingine wanashindwa kuzimudu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe, Mbunge wa Busega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli, pale kuna Mahakama ya Mwanzo, lakini vigezo vile vya kuitumia kama Mahakama ya Wilaya ndiyo kidogo vinakinzana, kwa hiyo waendelee kuvumilia ili tutakapokamilisha jengo lenye sifa, waweze kuanza kulitumia rasmi. Ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Changamoto ambayo inawapata wananchi wa Busega inafanana kabisa na changamoto ambayo inawapata wananchi wa Jimbo la Momba.

Je, ni lini Serikali itaona kuna haja ya kutupa upendeleo ili tuweze kupata Mahakama yenye hadhi ya wilaya ili kuwapunguzia wananchi changamoto ya mwendo mrefu kufuata huduma za Mahakama kutoka Jimbo la Momba mpaka Mji wa Tunduma? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Condester Sichalwe kutoka Jimbo la Momba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kimsingi katika Mpango Kazi wa kuendeleza ujenzi wa hizi Mahakama zetu za wilaya, 2022/ 2023 tunakwenda kuanza ujenzi wa Mahakama yake ya Momba ili kumpunguzia hiyo adha ambayo wananchi wanaikabili kwa sasa.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza nishukuru kwa majibu hayo lakini naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa msimamizi wa miradhi kwa mujibu wa sheria ya sasa anachaguliwa kwenye kikao cha familia ya marehemu ambacho katika kikao hicho mjane anakuwa ni mgeni, wengi wanakuwa ni ndugu wa marehemu, na hivyo anakosa kauli ya kuweza kuchagua au kupitisha mrithi au msimamizi wa mirathi hali inayopelekea familia kwa maana ya mjane na watoto kutaabika pale ambapo aliyechaguliwa kujimilikisha mali hizo. Je, ni lini sasa Serikali inatuletea marekebisho ya sheria hii ili tuweze kuondoa changamoto hizi?

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na sheria ambayo inakwenda kurekebishwa, je, Wizara inachukua hatua gani za dharula ili kuondoa hizi changamoto kwa sababu tunajua mchakato wa kurekebisha sheria inaweza kuchukua muda kidogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Husna kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa inatokea wakati wa vikao vile vya familia za marehemu wajane hawa wamekuwa hawahusishwi kwa asilimia 100 katika kufika muafaka wa kupata yule Msimamizi wa Mirathi. Lakini kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba msimamizi wa mirathi, si mrithi wa mali za marehemu. Na kwa bahati mbaya sana, kwa kuwa sheria hii ya mirathi ina sura tatu yaani kuna sheria ambayo inaruhusu mfumo wa kidini katika kugawa mali, kuna kimila na kuna sheria ile ya Serikali; kumekuwa na mkanganyika mkubwa na ndiyo maana Serikali sasa kwa makusudi kabisa tumeamua kuzipitia hizi taratibu zinazosimamia mgao wa mirathi ili kuondoa huu mkanganyiko ambao kwa sasa unakabili familia nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, lakini ni hatua gani za dharula ambazo tunazichukua, kwa sasa tunaendelea kila tunapopata nafasi ya kwenda katika maeneo mbalimbali ya nchi kuelekeza na kutoa elimu kwa wahusika wote. Kwamba ni muhimu wakatambua kuwa wasimamizi wa mirathi si warithi wa mali za marehemu, labda atokane na wale wanaotajwa kwenye orodha ya mirathi, na yeye anaingia kwenye ule mgao wa kawaida wa mali za marehemu. Lakini vinginevyo tumekuwa na tafsiri ambayo asili yake inatokana na mfumo wa kikabila na mila na desturi zao; yaani mtu akishaambiwa yeye ni msimamizi wa mirathi anajimilikisha haki zote za usimamizi wa mirathi na kuanza kutumia mali za marehemu.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwaomba na Waheshimiwa Wabunge po pote mtakapokwenda kuendelea kuelimisha, wakati sheria inakuja kuendelea kuelimisha juu ya nafasi ya msimamizi wa mirathi. Na inapobainika, kwamba, msimamizi wa mirathi ametumia kula mali ya marehemu kinyume cha utaratibu afikishwe kwenye vyombo vya sheria na hatua zichukue mkondo wake. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, kwa kuwa matatizo na changamoto ambazo wanapitia wanawake kwenye masuala haya ya kifamilia yamezidi kukithiri, na tarehe 6 Oktoba, 2021 Mheshimiwa Rais alilikazia hili, na hata Jaji Mkuu alielezea umuhimu wa kuwa na Mahakama ya Familia. Ningependa kuiuliza Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria. Je, ni lini ambapo itakuja na Mahakama ya Familia ili masuala yote haya ya mirathi matunzo na kadhalika yaweze kuangaliwa kwa utaratibu na haki iweze kutolewa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa mapendekezo mbalimbali yalitolewa kwa ajili ya kuanzisha Mahakama ya Familia, na bado tunaendelea kufanyia kazi, kwa sababu ni taasisi ambayo inahitaji kuwa kwenye muundo sasa wa utendaji kama zilivyo Mahakama nyingine. Kwa hiyo, ni imani yangu kwa kuwa tunakwenda sasa katika kurekebisha sheria yenyewe na muundo wake tunadhani tutakapokuwa tunakuja tutakuja na sura sasa ya kuwa na mahakama hii ambayo itashughulikia masuala ya mirathi. Ahsante. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utakumbuka mwaka jana mwishoni, Mheshimiwa Spika aliunda Kamati Maalum kabisa ambayo ilikuwa ni Kamati ya Viwanda na Biashara pamoja na Kamati ya Bajeti na tulikaa kwa nia ya kutaka kupitia mambo mbalimbali kwa sababu tulipokea taarifa za malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara kuhusiana na bei kubwa za stamp za kielektroniki. Lakini nimesimama hapa nikwambie tu kwamba pamoja na mazungumzo yale Serikali au TRA waliendelea kusaini mkataba huo ambao umekuwa wa kinyonyaji kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuulize Waziri wetu wa Katiba kwamba je, yupo tayari sasa kuleta mkataba kati ya SICPA na Serikali unaohusisha masuala ya stamp za kielektroniki ili tuweze kuwasaidia wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, pamoja na hiyo mikataba mingi uliyoisema na sisi kama Wabunge wengi tunatamani kujifunza na wengine siyo wahudhuriaji kwenye Kamati hizo ulizozitaja. Hauoni sasa ni wakati mikataba hiyo kwa mfano hiyo SGR, mkataba wa Bandari ya Bagamoyo, mkataba wa gesi wa kule Mtwara na mingine mingi kuwa wazi kwa Wabunge wote kuisoma na kupata uelewa wa kina kuweza kuishauri Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali la nyongeza la kwanza la Mheshimiwa Mwambe hili linalohusu stamp, nadhani tutafanya mawasiliano na taasisi inayohusika ili tuweze sasa kujiweka sawa katika eneo hili ambalo limeonesha mashaka ya mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili kuhusu suala la kuwasilisha mikataba katika Bunge lako tukufu kama nilivyoeleza mwanzo, mikataba hii huwa inapita kwenye Kamati kwa sababu ndiyo taratibu zilizowekwa. Kama Bunge lako tukufu litataka mkataba ufikishwe mbele ya Bunge lote basi maamuzi yanatoka kwenye Kamati baada ya kupitia zile taarifa zinazowasilishwa. Ahsante.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa mchakato uliopo unapoteza haki ya watu wengi kwa kutokupata haki zao kwa wakati, lakini wakati mwingine kwa watu wengine kushindwa kurudi Mahakamani kwa hofu na woga: Je, ni lini Serikali itakuja na sheria ambayo inatoa haki kwa wakati huo huo wa hukumu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia swali la pili; kumekuwa na utaratibu kwa watu kufunguliwa kesi baadaye kesi hizo zinafutwa, anafunguliwa kesi nyingine mbadala; je, ni vigezo gani vinatumika kumbadilishia mtu kesi kutoka ile kesi ya awali kuja kesi ya pili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kufanya marekebisho madogo ya sheria kwenye eneo hili tunalichukua na tunakwenda kulifanyia mchakato ili tuone kama kuna sababu zozote za kufanya hivyo na Bunge lako Tukufu litajulishwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mabadiliko ya kesi wakati umeshitakiwa kwa kosa hili na baadaye unapelekwa kwenye kosa lingine, hilo linategemea sana mwenendo wa upelelezi ambao unaweza ukabaini uhusiano wa tukio lile na tukio lingine ambalo linakupeleka kwenye mashtaka mapya. Ahsante. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Mkoani Mbeya Wilayani Rungwe maarufu kama Tukuyu hakuna Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi yapata miaka minne sasa ambapo Halmashauri ya Busekelo inategemea hapo na tatizo hilo Mbarali kuna tatizo hakuna pia Mwenyekiti na Chunya, ukizingatia wananchi wa Chunya wanatoka mbali kabisa Kambi Katoto wanakwenda Mbeya Mjini ambapo ni karibu na Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Sasa je, Serikali ni lini itatupelekea Wenyeviti Baraza la Ardhi kwenye Wilaya hizo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Wizara inaendelea na utaratibu, ni maeneo mengi hayana Mabaraza haya, kwa hiyo Wizara inaendelea kufanya matayarisho kwa ajili ya kuajiri Wenyeviti wa Mabaraza na moja ya watakaoajiriwa tuta-consider hilo eneo la Tukuyu, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo kama Njombe ambayo ni Miji inayokua inauhitaji mkubwa sana wa makazi kwa sasa na maofisi. Ni lini, Shirika la Nyumba litakwenda kuanza mpango wa kujenga nyumba katika maeneo hayo ya Njombe?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Deo, Mbunge wa Njombe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi National Housing inafanya mabadiliko makubwa sana ambayo yanakwenda kuanzisha ujenzi katika maeneo mengi sana ya nchi na hasa pembezoni mwa miji ambayo kwa kweli ilikuwa imesahaulika. Nikuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwenye eneo lako hilo muweze kuandaa maeneo ambayo shirika litakapofika lipate ushirikiano wa kupata maeneo ya kujenga nyumba, ahsante.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Shirika la Nyumba lina nyumba nyingi ambazo ni chakavu na ukarabati wake umekuwa ni changamoto kubwa sana hususani kwenye Mkoa wa Tabora hasa Manispaa ya Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kukarabati nyumba hizi na kama wameshindwa basi waziuze? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Tabora, Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi ukarabati unaendelea nchi nzima na kwa sababu hawawezi kufanya vitu vyote kwa pamoja, ndio maana unaona kama Tabora wamechelewa kidogo. Hatuna mpango wa kuuza nyumba zile kwa sababu zinaendelea kuwasaidia watumishi mbalimbali ambao wanazitumia kwa ajili ya kupunguza ile uwezekano wa kukosa nyumba katika maeneo ambayo wanakwenda.

Kwa hiyo, nipende tu kusema kwamba ukarabati unaendelea nchi nzima na muda mfupi ujao mtafikiwa Tabora, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, kimsingi ninaishukuru Serikali baada ya kupiga kelele kwa muda mrefu imetuletea Mpima mmoja katika Wilaya ya Rungwe.

Swali langu la kwanza; ni kwa nini msiongeze Mpima mwingine kwa sababu Wilaya ya Rungwe ina vitongoji 502 hivyo uhitaji wa Wapima ni mkubwa sana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili tuna shughuli inayoendelea katika Wilaya ya Rungwe ya upimaji wa vijiji 11 katika upimaji huo tunashukuru Serikali mmeleta shilingi milioni 500 na inafanya revolving fund kwa wananchi kulipa shilingi 30,000 ili wapimiwe.

Ni kwa nini Serikali msiongeze fedha ili wananchi hawa watoe angalau shilingi 15,000 kuwapunguzia makali katika upimaji wa viwanja hasa kwenye vijiji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA K.n.y. WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nipende kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakagenda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na lile swali dogo la kwanza ambalo linaomba nyongeza ya watumishi katika sekta ya wapima kwa sababu wanaye mmoja. Wizara inalichukua na bado inaendelea kulifanyia kazi na upo uwezekano wa kuongeza maofisa hao kulingana na jinsi tutakavyokuwa tumejijengea uwezo wa ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili kuhusu suala la kuongeza fedha ni kweli kabisa kwamba jambo hili ni muhimu na tumelipokea kwanza kwa uzito wa kutosha ili baadae tukalifanyie kazi na kuona uwezekano wa kupata vyanzo vya fedha kwa ajili ya kuongeza nguvu ingawa hatutarajii wapunguziwe thamani ile wanayolipa sasa kwa sababu nayo vilevile inasaidia kuongeza uharakishwaji wa zoezi hili. Ahsante.
MHE.KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya maeneo yanayolalamikiwa katika nchi zenye utajiri wa mafuta ya gesi ni kukosekana kwa utawala bora katika kuwa na uwazi kwa mikataba hii kwa umma; je, ipi mikakati ya Serikali katika kuenzi jitihada za kufikia lengo hili la kuwa na uwazi wa mikataba kwa ujumla katika umma wa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili pamoja na kwamba mikataba imekuwa inakuja bungeni kupitia Kamati; je, Serikali haioni kama kuna umuhimu wa kubadilisha utaratibu huu ili kuwe na utaratibu ambao Bunge litaweza kuona kwa maana ya Bunge zima hata kuwe kwa kipindi cha mwisho wa mwaka ili waweze kuona ni maeneo gani ambayo Serikali imeingia mkataba na waweze kupata uelewa wa pamoja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nollo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwazi katika mikataba upo na kimsingi kwa sababu muuliza swali ni sehemu ya Wabunge na Kamati za Bunge zimeundwa kwa mujibu wa sheria na utaratibu wa Kibunge, zinapopata nafasi ya kupitia mikataba hii huwa ni kupunguza lile jambo katika mazingira ambayo yanaweza upotofu wa jumla katika suala la mikataba. Hivyo basi mikataba inapojadiliwa na Kamati za Bunge ni kisheria kabisa unakuwa tayari maelekezo yanayotolewa na Kamati zile yanakuwa ni halali na ni sawa kufikishwa mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu lile suala la kubadilisha mfumo, ni Bunge hili lililokaa na likaweka utaratibu huo, na ni Bunge hili hili linaweza likabadilisha mfumo. Hivyo basi ni jambo ambalo ningemshauri Mheshimiwa Mbunge kutoa hoja ili sasa vyombo vinavyohusika katika kubadilisha mifumo viweze kuchukua nafasi yake. Lakini kwa namna tunavyokwenda kwa sasa ni jambo ambalo linazingatia taratibu na sheria tulizojiwekea. Ahsante.
MHE. ZAHOR MOHAMED HAJI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naomba niongeze swali moja la ziada.

Wanasema justice delayed is a justice denied, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, Serikali iko tayari sasa kuongeza uharaka wa jambo hili kwa sababu wananchi wamekuwa wakipata matatizo kwa muda mrefu? Nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu swali la nyongeza la ndugu yangu pale Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli uharaka upo na kwa sababu ni sehemu ya mchakato wa kupatikana kwa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa majengo hayo, naomba Mheshimiwa Mbunge atupe nafasi tu na muda wa kutosha na ataona kinachoendelea kwa sababu kimsingi Mahakama ya Tanzania iko kwenye mabadiliko makubwa sana katika uwekezaji wake, kwenye majengo ya kutolea huduma. Kwa hiyo hata hili ndio maana tumelitolea maelezo kwamba tunalifanyia kazi na kazi itakwenda kwa kasi sana. Ahsante.
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nina swali moja la nyongeza. Jimbo la Nkasi Kusini Tarara ya Kate, huduma za kimahakama wanatumia godown; upande mmoja magunia, upande mmoja Mahakama inaendelea.

Mheshimiwa Spika, nilimpigia simu Mheshimiwa Naibu Waziri, akafika, tukatembelea Tarafa ya Kate yeye mwenyewe akajionea mazingira magumu, jinsi gani huduma za haki za kimahakama zinatolewa katika mazingira ambayo siyo mazuri. Ni godown, wakiweka dawa kwenye mazao, Mahakama haikaliki, ni harufu tupu: Je, ni lini serikali inakuja kujenga jengo la kisasa Tarafa ya Kate? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa
Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vincent Mbogo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akifuatilia sana masuala haya kwa ajili ya kuwasaidia wananchi kupata eneo sahihi la kupata huduma za haki. Ni kweli kabisa nilitembelea Kate, na nilikuta ni kweli wanatumia godown ambalo ndiyo linakuwa kama Mahakama.

Mheshimiwa Spika, vile vile nilimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba hili jambo tumelichukua na kwa sasa hivi katika ule mpango kazi ambao Mahakama imejiwekea, tunamwahidi Mheshimiwa Mbunge, katika kipindi hiki tunachoendelea nacho mpaka kufika 2025, Makao Makuu yote ya Tarafa nchini tunakwenda kujenga majengo ya Mahakama ya Mwanzo. Kwa hiyo, kwa sababu Kate ni Tarafa, inaenda kupata upendeleo wa pekee katika kipindi kijacho cha fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, lakini kwa sasa hivi hatuna Mahakama ya Wilaya na shughuli za Mahakama ya Wilaya zinafanyika kwenye Mahakama yetu mojawapo ya Mwanzo ambayo haikidhi mahitaji ya Mahakama ya Wilaya: Huoni kuna haja sasa ya Serikali kuharakisha ujenzi wa Mahakama yetu ya Wilaya ya Korogwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza shughuli za Mahakama ya Wilaya ambazo zilitakiwa zifanywe na Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Korogwe, mwanzo zilikuwa zinafanyika katika ofisi ndogo sana ya Mkuu wa Wilaya ya Korogwe. Kwa sasa tumeweza kukarabati jengo ambalo tumepewa na Halmashauri ya Korogwe ambalo kimsingi linakidhi mahitaji ya Mahakama hiyo. Hivyo basi, kama tulivyokwishatoa maelezo ya msingi kwenye jibu la msingi kwamba, ifikapo kipindi kijacho cha fedha, tunakwenda kuanzisha ujenzi wa Mahakama ambayo sasa itakuwa ni ya Wilaya ya Korogwe. Ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Waziri wa Katiba na Sheria na Naibu Waziri, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kupanua wigo wa haki za binadamu nchini Tanzania, nina swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa mwongozo huu ni mwarobaini mzuri wa kusimamia haki za raia wetu nchini. Ni kwa nini mwongozo huu sasa usiingie kama sheria rasmi za nchi yetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kimsingi wazo lake tunalichukua na tutakwenda kulifanyia kazi kuona tuilete kama sheria au iendelee kusimamia kwenye kanuni hizi. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika,ahsante. Kwa mara ya pili ninaomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, Tarafa ya Ikuwo haina Mahakama ya Mwanzo, wananchi wanalazimika kusafiri zaidi ya kilimita 100 kwenda kupata huduma za kimahakama kitu ambacho kinawafanya wananchi wakate tamaa wasiendelee kufuatilia haki zao. Ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Mwanzo kwenye Tarafa ya Ikuwo ili wananchi wangu waweze kupata huduma hiyo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika hali ya kawaida nimuombe Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane baada ya kikao hiki ili niweze kumpa mkakati ambao tumeuweka, kwa sababu katika kipindi hiki tuna miradi Sitini ambayo iko katika hatua mbalimbali na kwa sababu katika kipindi hiki tunayo miradi 60 ambayo ipo katia hatua mbalimbali na kwa sasa, kwa vile sina kumbukumbu sahihi hapa niwasiliane naye ili niweze kumsaidia kujua Mahakama yake inaenda kuanza lini ujenzi. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa, Serikali inaendelea na ujenzi wa Mahakama za Wilaya na kule Wilayani Mkinga Mahakama yetu ya Wilaya iko tayari na imeanza kazi wiki iliyopita. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kukarabati zile Mahakama za Mwanzo ambazo ni chakavu sana. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mhesimiwa Spika, ahsante sana, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu, Mbunge Viti Maalum kutokea Mkinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sasa hivi katika mpango wetu tunaoendelea nao, tunaendelea kukarabati na kujenga majengo mapya katika maeneo mbalimbali. Hivyo nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba majengo yaliyochakaa yataendelea katika utekelezaji wa mpango tulionao katika kipindi hiki tulicho nacho na kipindi kijacho kwa sababu mwisho wa mradi huu ni 2025 kuhakikisha kwamba huduma za Mahakama zote nchini katika ngazi mbalimbali tutakuwa tumezikamilsha. Ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri sana ya Serikali yanayotia moyo, naomba naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Katika Kata ya Iguguno kuna Mahakama ya Mwanzo ya kisasa kabisa na ya kidigitali. Je, Serikali sasa haioni haja ya kuanza Mahakama ya Wilaya kwa muda katika Kata hii, kwani wanachi wanapa shida sana kwenda Wilaya ya Iramba kwenda kufuata Mahakama ya Mwanzo?

Swali la pili, iwapo Serikali itaridhia kutumia Mahakama hii; je, itakuwa tayari sasa kutumia mahabusu ya Singida Mjini badala ya kwenda Kiomboi kwani uhakika wa usafiri wa Singida Mjini ni rahisi na ni karibu zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Iramba Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kimsingi maoni yake yote tunayachukua na tunakwenda kuyafanyia kazi kuona Je, kuna uwezekano wa kuanza kutumia huduma zote hizi mbili ambazo Mheshimiwa Mbunge amependekeza. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wananchi wa Jimbo la Geita Vijijini wanalazima kufuata huduma za Mahakama ya Wilaya kilometa 60. Je, ni lini Wizara itakuwa tayari sasa kwenda kujenga Mahakama ya Wilaya kwenye Jimbo hilo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuko kwenye mkakati wa kuendelea na utekelezaji wa ujenzi wa Mahakama za Wilaya katika Wilaya 18. Ninapenda tu kumwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba ujezi wa jengo ambalo linahitajika katika Wilaya yake linaenda kuanza katika kipindi cha fedha kijacho kwa ajili ya kutekeleza mpango huu wa maboresho ya Mahakama nchini. Ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ni miaka minne sasa nikiendelea kutetea ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbulu. Kwa kuwa, sasa mahakama ya Wilaya inapitiwa na ujenzi wa barabara ya lami. Je, ni lini Serikali itatekeleza azma yake ya ujenzi wa Mahakama yetu hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kutoka Mbulu. Wilaya ya Mbulu ni miongoni mwa Wilaya ambazo ziko kwenye mkakati wa kujengewa Mahakama kwa kipindi hiki cha fedha cha 2022/2023. Kwa hiyo taratibu za kupata Mkandarasi kwa ajili ya zoezi hilo zinaendelea. Ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Uyui iko kwenye chumba kidogo sana tulichopewa na Ofisi ya DC.

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Uyui? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kutoka Uyui kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika jibu la msingi, ni kwamba sasa hivi Mahakama ya Tanzania imeendelea katika shughuli za ujenzi wa Mahakama mbali mbali hapa nchini. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge, tuwasiliane baada ya kipindi hiki ili niweze kumuweka katika kumbukumbu zilizo sahihi juu ya lini tunaenda kuanza ujenzi katika eneo lake. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, napenda kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kujenga Mahakama mpya nzuri ya Wilaya ya Kilombero. Swali, je, ni lini Mahakama ile itazinduliwa katika Kata ya Kibaoni pale ili wananchi wawenze kupata huduma za Mahakama Mpya?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kutoka Kilombero. Ni kwamba wakati wowote atajulishwa utaratibu wa uzinduzi wa ile Mahakama kwa sababu haijaisha muda mrefu sana. Sasa hivi tunaharakisha uzinduzi wa Mahakama zote ambazo zimekamilika hapa nchini kwa ajili ya kuzizindua. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuzijenga na kukarabati Mahakama za mwanzo za Nkwaranga na West Meru, kama ilivyoahidi mwaka wa fedha uliopita 2021?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Pallangyo tuwasiliane ili niweze kumpa mkakati halisi, lakini mpango kazi wote umeshakamilika katika kukarabati na kujenga majengo mapya ya maeneo ambayo hayana mahakama. Kinachokosekana hapa ni kumbukumbu sahihi tu, kwa sababu swali linakuwa limekuja kwa sasa hivi. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa mwenyekiti, nakushukuru, pia namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa majibu mazuri. Nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lushoto lina Mahakama za mwanzo mbili, kwa maana Mahakama ya Mlola na Mahakama ya Gare. Lakini hii ya Gare takribani miaka 20 sasa haifanyi kazi yani jengo lake limekeuwa ni gofu.

Je, Serikali in ampango gani wa kujenga upya Mahakama ya Gare pamoja na kata jirani ili waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshmimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo: -

Mheshmimiwa Mwenyekiti, kimsingi Mahakama ya Tanzania katika mpango wake inajenga Mahakama za Mwanzo katika Makau Makuu ya Tarafa zote hapa nchini.

Kata ya Gare haipo kama sehemu ya Makao Makuu ya kata kwa sababu iko ndani ya Tarafa ya Lushoto yenyewe. Hivyo tunaangalia uwezekano wa kuzipa umuhimu kata ambazo zina uhitaji maalum. Baada ya Bunge hili tutawasiliana na Mheshimiwa Mbunge kujua uhalisia wa tatizo la Gare lakini kwa sasa tunaelekeza nguvu zetu Makao Makuu ya Tarafa hapa nchini.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Mahakama ya Mwanzo ya Mbagala ambayo ina hali ngumu sana, mazingira yake na idadi ya watu wanaopata huduma pale ni wengi sana?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi tumelichukua ombi lake na tutakwenda kulifanyia kazi ili tuweze kuiweka katika mazingira mazuri ya matumizi, ahsante.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza;

Kwa kuwa watuhumiwa wa matukio haya wanaachiwa huru kwa kigezo kwamba ushahidi haujapatikana.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha kitengo cha ushahidi na uchunguzi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nini mpango wa Serikali wa kuzuia mauaji haya ili kuwanusuru wanawake hawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza linaonesha kwamba kumekuwa na muda mrefu wa kesi hizi zikiwa na visingizo vya kupatikana kwa ushahidi wa haraka. Kesi za mauaji zina utaratibu wake katika upelelezi wake. Walio wengi wanafikiri ni jambo la mara moja katika kufikia maamuzi ya upelelezi unaohusisha mauaji, lakini kwa namna yeyote ile muda uliowekwa na mahakama na vyombo vya upelelezi umekuwa ukizingatiwa sana katika masuala ya kesi hizi za mauji na hivyo hatuna kumbukumbu sahihi za watu ambao wamekaa magerezani muda mrefu kuliko kile kipindi ambacho tumekiweka kama dhamirio la kuwapa nafasi wapelelezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu namna ya kuzuia mauaji haya; hili ni jambo la kijamii. Mambo haya mengi yamekuwa yakitokea kwenye jamii zetu na sisi wanajamii ndio tunastahili kuyakemea maana ni maisha yetu ya kila siku ambayo yanasababisha mauaji haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende tu kumpa maelezo muuliza swali; ni kwamba si mauaji tu kwa kina mama na watoto ukienda pale Njombe, nimetembelea Gereza la Njombe, asilimia 75 ya akina mama waliopo mle jela wakisubiri hizo kesi wanahusishwa na mauaji ya kuwaua waume zao. Kwa hiyo unaweza ukaona jinsi ambavyo mauaji haya yanajiografia zake; na mengine yote haya yanayojitokeza kweye jamii zetu wakemaji namba moja lazima tuwe sisi wenyewe wanachi katika maeneo yetu.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa kwa miaka ya hivi karibuni kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya wanafunzi kupewa adhabu kali ya viboko shuleni inayosababisha majeraha, kuzimia, kulazwa na hivyo kushindwa kuhudhuria shule ipasavyo.

Je, Serikali haioni ipo haja ya kuweka adhabu kali kwa waalimu wanaofanya vitendo hivi ili kuwalinda watoto wetu shuleni?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ongezeko la adhabu zisizo na kiasi kwa wanafunzi kule shuleni, na kwamba anaomba adhabu kali zitolewe kwa waalimu wale ambao wanachukua sheria mkononi; kimsingi limekuwa ni tatizo. Kila siku naona kwenye mitandao hatua ambazo walimu wanachukua. Mimi niwasihi, hasa walimu, kwa sababu tunayo sheria ya elimu inayotoa utaratibu wa adhabu kwa watoto wetu. Pale mtu anapochukua sheria mkononi atashtakiwa kama mhalifu mwingine yeyote ambaye ametumia nguvu katika kutoa adhabu kwa watoto wetu.
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nishukuru majibu mazuri ya Serikali. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali bado tuna changamoto nyingi hasa kwenye upande wa magari katika taasisi hii ili waweze kufanya kazi zao vizuri na kurahishisha kazi zao;

Je, Serikali ina mpango gani kuhusiana na masuala mazima ya magari ya usafiri kwa Taasisi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu la pili;

Je, Seriikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi katika Taasisi hii, ambao bado maeneo mengi tuna changamoto kubwa ya watumishi kwenye taasisi hii, ili waweze kufanya kazi vizuri na tukiangalia Taasisi hii ina - deal na masuala ya rushwa na bado tuna changamoto nyingi sana katika nchi hii kuhusu suala la rushwa?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu changamoto ya usafiri, hili linachukuliwa umuhimu wa pekee, na hata kwenye bajeti ijayo tunaomba nafasi ya kuongeza vyombo vya usafiri, ili kuwasaidia maafisa wetu wa TAKUKURU kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile suala la kuongeza watumishi tunaendelea nalo ni zoezi endelevu. Kwa ushahidi Waheshimiwa Wabunge wote mnajua hata mwaka huu TAKUKURU ilipata nafasi na mpaka sasa kwenye kipindi hiki, bado wanaendelea na mchakato. Tangazo lao la mwisho lina kama wiki mbili hivi bado wanaendelea kufanya mchakato wa kupata watumishi zaidi. Kwa hiyo hili zoezi la kuongeza watumishi ni zoezi endelevu kulinganna na upatikanaji wa fedha na namna Serikali itakavyopata nafasi ya kuongeza nafasi zaidi.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa maswali madogo mawili ya nyongeza.

Je, Serikali inampango gani kuajiri wanasheria ambao wanaweza kusaidia kuleta elimu ya mirathi katika ngazi ya kata?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana na inatia huzuni wanawake wajane baadhi yao wamejikunja hawajui hatima yao kwasababu wanadhurumiwa haki zao za mirathi, hivyohivyo wanakuwa wanateseka kwa namna hata ya kusomesha Watoto wao;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inaleta sheria ambayo itasaidia kuleta mpango mkakati kwa ajili ya kunusuru ndoa na mirathi ili kuepusha changamoto za mirathi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kuajiri wanasheria katika ngazi ya kata, kimsingi kule tuna Mahakama ambapo shughuli zote za kimahakama zinafanywa katika maeneo yale, na wale mahakimu ni watalamu ambao wamehakikiwa. Tunakwenda kubadili Sheria ile ya Wazee wa Baraza na badaye kuruhusu wanasheria binafsi vilevile kwenda kusimama kwenye mahakama hizo ili kuwasaidia wananchi wengi ambao wangehitaji msaada wa kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo suala la ule mkandamizaji napenda nitumie nafasi hii kuanza kuwafahamisha wananchi wote; kumekuwa na mkanganyiko tu wa akili za wananchi wachache wenye tamaa, unapopewa nafasi ya kuwa msimamizi wa mirathi huko ndiko kunako anzia tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimamizi wa mirathi si mrithi. Msimamizi wa mirathi kazi uliyopewa ni kukusanya mali za marehemu na kusimamia warithi kupata kwa kuzingatia haki zao na mrithi namba moja kwenye haki za mirathi ni mke wa marehemu, watoto wa marehemu ndilo kundi la pili na kundi la mwisho ni wazazi wa marehemu, kama wapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kinachotokea sasahivi ni kwamba mtu akipewa tu nafasi ya kusimamia mirathi, anaanza kujirithisha yeye mwenyewe. Huyu ni mwizi na anastahili kushtakiwa kama mwizi wa kuaminiwa. Hili ndiyo jambo ambalo kimsingi linakera sana kwenye jamii zetu. Akina mama wengi wananyanyasika katika mazingira kwamba shemeji aliye aminiwa na ile familia kusimamia na kukusanya mali za marehemu yeye mwenyewe ndiye anabaki katika mazingira ya kurithi na kuila ile mali ya wale walengwa ambao kimsingi wanakuwa ni familia ile ya marehemu iliyoachwa baada ya kifo cha wazazi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili ni jambo tu la uelewa, hakuna mtu mwingine yeyote mwenye haki ya kurithi mali iliyoachwa na marehemu nje ya hao niliowataja. Kuna mila nyingine ni potofu sana; kwa mfano kuna mila ambazo zinamfanya mtu anaitwa mrithi awe na sauti asilimia mia kwenye mali zile. Ile si urithi wa kisheria. Urithi wa kisheria unaotambuliwa ni mke, watoto na mzazi wa marehemu; na katika mgao mzazi wa marehemu anapata kiasi kidogo sana kuliko watoto na mke wa marehemu kwasababu mke wa marehemu anakuwa bado anaendelea kuilea ile familia ambayo imeachwa na yule marehemu, ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza niipongeze sana Wizara ya Katiba na Sheria kwa hatua mbalimbali ambazo wanachukua za kuboresha mfumo wa katiba na sheria nchini.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa watuhumiwa wengi wa makosa ya mauaji wanakaa rumande kwa muda mrefu sana wakisubiri mashauri yao kusikilizwa na watuhumiwa wengi wengine wanafia rumande wakisubiri kesi zao. Naomba kujua ni kwa nini Serikali isiteue Majaji wa muda mfupi ad hoc judges au acting judges wakasikilize mashauri haya kwa haraka?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa kesi nyingi za mauaji zinacheleweshwa kwa sababu ya Idara ya Upelelezi kuchelewa kufanya wajibu wake, aidha kwa makusudi au kwa bahati mbaya. Je, ni lini Serikali italeta Bungeni sheria ya kuweka ukomo wa makosa ya mauaji ambayo upelelezi haukamiliki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nipende kumjibu Mheshimiwa Mbunge maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza pamoja na uhaba wa Majaji tulionao, bado sisi kama Serikali Waziri wakishauriana na Mheshimiwa Jaji Mkuu, wamefanya zoezi la kuwaongezea mamlaka wale Mahakimu ambao ni wa mahakama hizi za ngazi mbalimbali ambazo zinaendesha kesi ambazo hazina mamlaka wao kusikiliza kesi za mauaji. Kwa hiyo, tunao Mahakimu nje ya Majaji 153 ambao wameongezewa mamlaka za kusikiliza kesi za mauaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ukiliangalia suala la kesi hizi upande wa mahakama haina kuchelewesha kesi, isipokuwa kwenye eneo hili la upelelezi ambalo kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi, tumeamua kuunda timu kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ambapo tumemshirikisha Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, pamoja na Ofisi ya DPP, kuharakisha upelelezi wa hizi kesi ili kuhakikisha kwamba zinaisha kwa wakati. Mpaka sasa tayari timu iko mikoani na inafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha mpaka kufikia mwishoni mwa Mei, hili suala la mrundikano wa kesi utakuwa umekwisha.

Mheshimiwa Spika, hili suala la kuja na sheria, bado tuna taratibu na kanuni na sheria vilevile zinazoonyesha kipindi cha upelelezi cha kesi, lakini matukio ni mengi sana kwa sasa hivi, kwa hiyo, kila siku kesi za mauaji nyie wenyewe mtakuwa mashahidi zinazaliwa kila siku. Kwa hiyo, ndiyo maana tumekuja na huu mkakati ambao tutakuwa tunatumia hawa Mahakimu ambao hawapo katika vigezo vya kusikiliza kesi za mauaji kuwaongezea nguvu. Vile vile tutahakikisha kwamba tunakimbiza hizi kesi na zinakwenda kumalizika kwa wakati, bila kuchelewesha aina yoyote kesi za mauaji.
MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningetamani pia kujua kwa niaba ya muuliza swali Je, ni Balozi ngapi ambazo walau zimeshakuwa na viwanja japokuwa hazijafungua ofisi rasmi kuelekea kuwa na Ofisi rasmi katika Makao Makuu ya nchi?

Mheshimiwa Spika, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Balozi zote nchini zimegawiwa viwanja Dodoma na Taasisi zake na kila Ubalozi ulitengewa karibu heka tano tano kwa ajili ya kuwekeza makazi yake pale. (Makofi)
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa swali. Mheshimiwa Waziri ametuambia kwamba Balozi zote nchini zimepewa viwanja Dodoma.

Je, ni changamoto gani kubwa inayosababisha Balozi hizi zishindwe kuja kuendeleza viwanja hivyo na kuhamia Dodoma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza utaratibu wa kuhamisha makazi ya Kibalozi kutoka iliyokuwa makao makuu ya nchi yetu kuja Dodoma ni utaratibu sawa na nchi nyingine zilivyofanya wakati huo. Kwa mfano, sisi tulihama kutoka Borne kwenda Berlin lakini tulichukua muda mrefu sana kwa sababu, hili ni suala la mipango ya kila nchi kujiwekea mpango wa uhamisho ambao unahitaji fedha. Kwa hiyo, upo uwezekano kabisa mkubwa wa nchi hizi ku-delay kuhamia hapa Dodoma kwa sababu, lazima ziingie kwenye mipango yao ya fedha na ziruhusu katika utaratibu wa kawaida Balozi zao kuhamishia makazi yake hapa makao makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo tukumbuke wakati tunafanya mchakato wa uhamisho baadhi ya Balozi zetu hapa ambazo zinawakilisha nchi zao hapa ndio zilikuwa zinamaliza majengo yao mapya Dar es Salaam. Kwa hiyo, unaweza ukaona namna ambavyo kunakuwa na misukosuko ile ya kimaandalizi kuanza kufikiria upya kuhamia Dodoma, ahsante. (Makofi)
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza: Serikali haioni haja ya kufanya tathmini ya mashamba yote yaliyotelekezwa na kupata orodha yake ili taratibu za kubatilisha ziweze kufanyika katika Wilaya ya Kilolo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hili shamba limetelekezwa tangu mwaka 1980, lakini hadi sasa halijaweza kubatilishwa: Je, Serikali haioni umuhimu wa kulibatilisha kwa haraka ili liweze kukabidhiwa kwa Halmashauri na kupangiwa matumizi mengine ili wananchi waweze kunufaika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mashamba ambayo yametelekezwa kwa muda mrefu ni mamlaka za Halmashauri kubaini hayo maeneo na kuyaanzia michakato ya kuomba yabatilishwe. Hivyo, nitoe wito kwenye Halmashauri zote hapa nchini, kupitia maeneo ambayo yamesahauliwa na wale ambao walimilikishwa huko nyuma ili sasa hii michakato ya haraka iweze kufanyika na kubadili yale matumizi ya maeneo kupitia hizi mamlaka za juu.

Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la pili, kwa kuwa jambo hili lilichukua muda mrefu, kama nilivyosema mwanzo, inawezekana Halmashauri ilikuwa haijabainisha na kuanza ile michakato, lakini kwa sasa kwa hatua tulipofikia, hili jambo linakwenda kukamilika kwa sababu mwenye maamuzi ya mwisho katika ubatilishaji wa maeneo haya ya ardhi ni Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, tutakapomfikishia, tunaamini wazi kwamba atalitolea maamuzi ya haraka kadri inavyowezekana, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nina maswali mawili ya nyongeza. Wananchi wa maeneo yote ambayo yanazunguka mgodi wa Barrick North Mara hawajui kwamba ardhi ndiyo ya kwao kilichopo chini siyo cha kwao.

Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kwenda kufanya mkutano katika eneo lile ili kutoa elimu hii kwa wananchi ili wajue kwamba hawahusiki na dhahabu iliyoko chini ya ardhi ile?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, pamoja na manung’uniko makubwa sana ya eneo hilo ni nili wananchi wa eneo la Nyamichele, Murwambe, Nyabichune na Kiwanja watalipwa fidia yao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Waitara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwenda kwenye eneo, yaani uwandani Wizara tuko tayari kwenda na tutawasiliana nae kwa ajili ya kupanga utaratibu wa jinsi ya kufika kule kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fidia ya maeneo aliyoyataja nitawasiliana nae kujua viwango vya hatua zilizofikiwa hadi sasa. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa sababu tatizo hili limekuwa kubwa karibu katika Wilaya zote nchini, kuna mlundikano wa kesi nyingi, lakini Wenyeviti hao wa Mabaraza ni wachache sana. Kwa nini Serikali isiwe na mkakati maalum kuhakikisha kwamba mabaraza yote ya ardhi katika Wilaya zetu yanapata Wenyeviti hawa? Swali la pili, Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ina mlundikano mkubwa wa kesi, ina migogoro mingi inayohusu ardhi: Je, Serikali haioni haja ya kupeleka Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi atakayekaa pale kwa ajili ya kuondoa migogoro na kutatua kesi zilizopo zinazohusu masuala ya ardhi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia jibu la msingi ambalo nimelitoa, ni kwamba sasa hivi tunaendelea na michakato kama nilivyoeleza, ya kuziba pengo la Wenyeviti 57 ambao utaratibu wake ukikamilika, tutakuwa tumekamilisha Wilaya zote hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Ukerewe, kutokana na mlundikano wa kesi, hili tutaliangalia kwa umuhimu wake na tutalifanyia kazi, ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mwaka 2018 Waziri wa Ardhi alitembelea mipaka ya Wilaya ya Monduli - Longido, Monduli - Arumeru, na Monduli - Babati na kuagiza mipaka hii iainishwe: Je, ni lini Serikali itaenda kutembelea mipaka hii na kuibainisha ili kupunguza migogoro isiyo ya lazima kwa wananchi inayopelekea mapigano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza swali la msingi lilihusu masuala ya Mabaraza. Kwenye eneo hili la mipaka, tayari tumeshaanza hiyo kazi na katika kipindi cha kama miezi miwili iliyopita, tulikuwa Mkoa wa Arusha ambapo tulitembelea ile mipaka inayotenganisha nchi na nchi. Kwa maana ya migogoro iliyopo kati ya wilaya na wilaya, tayari timu mbalimbali zimeshaundwa na zinakwenda kufanyia kazi haraka sana na Monduli na Arusha zitakuwa ni moja kati ya maeneo ya kupitiwa.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Wilaya ya Kahama ina Halmashauri tatu, lakini ina mwenyekiti mmoja tu wa Baraza la Ardhi. Sasa Serikali ina makakati gani wa kupeleka Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi katika Halmashauri ya Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi kama nilivyolieleza katika jibu la msingi, tunaendelea na michakato ya kupata Wenyeviti katika kuziba pengo la karibu Wilaya 57, na tukishafanikisha, Ushetu nayo itapewa umuhimu wa pekee nao katika kufikishiwa Mwenyekiti wa Baraza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu, katika maeneo yote hapa nchini ambayo mabaraza hayajafika, Mamlaka za Miji husika, kama kuna majengo ambayo tayari yapo, ambayo tunaweza tukayatumia katika kipindi hiki, basi tuarifiane, na Waheshimiwa Wabunge kwenye maeneo yenu mtupe taarifa ili tuweze kuona uharaka wa kuwaleta wenyeviti wetu katika maeneo husika, ahsante sana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza la kwanza baada ya ziara ya mawaziri nane kwenye maeneo yetu ya Wilaya Sikonge. Serikali ilituma timu ya watalamu ambao ilifanya kazi na viongozi wa vitongoji, vijiji na kata na mimi kazi hiyo waliyoifanya narizika. Kwa sababu waliweka mipaka na rangi kwenye hiyo mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo nitayataja Luseseko, Isenga na Manzagata, Misulu, Simbaudenga, Ngakaro, Kawemimbi na Manyanya ya 2,567 zina wakazi 25,000. Sasa swali la kwanza je, ni lini hasa kwenye maeneo haya yenye wakazi wengi watakuja kuweka bikoni ili kuwaondolea wasiwasi wananchi wangu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kwa kuwa uamuzi wa Serikali wa mwaka 2019 uliondoa zile mita 500 za bafa zone ambazo zilikuwa chini ya hifadhi kipindi kile sasa zikawa chini ya halmashauri ili waweze wananchi kuzitumia je, hizo mita 500 kuzunguka maeneo yote ya hifadhi wananchi watakabidhiwa lini kwenye halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza suala la lini hasa bikoni zile zinaenda kuwekwa, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika eneo lako watalamu wanakwenda kuendelea na shughuli hizi. Kwa sababu mpaka sasa watu wako uwandani wanaendelea na kazi. Kitu cha msingi kikubwa kuweka msukumo mkubwa ambao watawezesha sasa alama zote katika maeneo husika ziweze kufikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote katika maeneo yenu yanayopitiwa na hii miradi tuwaombe wananchi wawe watulivu sana katika zoezi hili kwa sababu wakati mwingine linapotoshwa katika ile tafsiri halisi wakati utekelezaji umesimama imara kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; hii bafa zone ambayo tumeiyondoa katika maeneo yetu, wakati zoezi la upimaji wa vijiji unao endelea ndiyo wakati ambao utabainisha hizi mita 500 za eneo ambalo zinatakiwa zirudishwe kwenye halmashauri, naomba tu tuwe watulivu wakati zoezi hili likiendelea, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa shirika hili limekuwa linajenga nyumba katika halmashauri mpya zilizoko mjini. Je, ni lini sasa shirika hili litaanza kujenga nyumba za watumishi katika halmashauri zilizoko vijijini hasa katika Halmashauri ya Ushetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa Serikali inakuwa inapeleka fedha nyingi za ujenzi wa madarasa, zahanati na hospitalini lakini watumishi hawana nyumba kabisa. Ni lini mkakati wa Serikali kuwajengea nyumba watumishi hawa hasa walioko vijijini?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Shirika la Nyumba la Taifa (National Housing) limeendelea kujenga nyumba katika maeneo mbalimbali. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu kwa kuwasemea watumishi wetu walioko katika maeneo na hasa Ushetu huko, kitu kikubwa kabisa ambacho tunaweza tukaahidi ni kwamba tunaendelea katika hatua mbalimbali za ujenzi na katika muda wowote ule tutafika huko Ushetu.

Mheshimiwa Spika, ombi letu sisi kama Wizara nikuomba halmashauri zote kutenga maeneo ambayo wangependekeza kujenga nyumba hizi zinazosimamiwa na mashirika kama hiyo National Housing na Watumishi Housing.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili; fedha nyingi zimepelekwa katika hizi mamlaka zetu za halmashauri kupitia TAMISEMI, na nimeona kwa sehemu kubwa sana fedha zinazopelekwa zinakuwa na kiambata cha nyumba za watumishi.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika swali la msingi kwa kupitia mashirika yetu haya taasisi zinazojenga nyumba zetu za watumishi. Sisi kama Wizara ya Ardhi tutaendelea kusimamia ujenzi wa nyumba hizo lakini niwahimize tu vilevile kwenye halmashauri wanapopata fedha zinazotoka Serikali kuu basi katika ile matumizi wajibane waweze kuweka na nyumba kiasi za watumishi wao katika maeneo wanapo pokea fedha zao. (Makofi)
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Kakonko na halmashauri yake ni mpya na hivi watumishi hawana nyumba za kuishi je lini Serikali sasa itajenga nyumba kwa ajili ya watumishi waliyoko katika Wilaya ya Kakonko? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kakonko na maeneo yote ambayo ni halmashauri mpya niwaombe kama nilivyosema kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu kwamba tutenge maeneo. Kwa sababu wakati mwingine mkienda kwenye maeneo hayo unakuta hakuna hata maeneo yaliyotengwa na halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za taasisi kama National Housing na Watumishi Housing.

Mheshimiwa Spika, hata hizi nyumba zilizopo bahati mbaya sana inatokea watumishi wengi hawaendi kukaa kwenye hizi nyumba na badala yake mashirika haya yamekuwa sasa yakipangishwa watu wa kawaida na hiyo ni mifano ipo hata hapa Dodoma tunazo nyumba nyingi pale Iyumbu lakini watumishi hawaendi pale kwa ajili ya kuzitumia. Ahsante.
MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Tumeshuhudia hivi karibuni nchi ya Afrika Kusini wametangaza uhitaji wa walimu wa lugha ya Kiswahili katika nchi hiyo; je, Serikali sasa inatumiaje fursa hii katika kuhakikisha kwamba walimu wetu waliobobea katika lugha ya Kiswahili wanafaidika na fursa hii hususan walimu kutoka Tanzania Bara na Tanzania Visiwani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Miongoni mwa Balozi ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika kuikuza lugha ya Kiswahili ni Ubalozi wa Tanzania nchini Italy, tayari wameshasajiisha Vyuo Vikuu vitatu ndani ya nchi hiyo, vinafundisha lugha ya Kiswahili, kikiwemo Chuo Kikuu cha Torino, Chuo Kikuu cha Roma na Chuo Kikuu cha Napoli. Vilevile nauliza swali; je, Serikali haioni haja kwamba Balozi zetu ambazo zinatuwakilisha katika nchi mbalimbali ziweze kufuata modality hii ya Ubalozi wa Italy nchini Tanzania, ambapo kwa muda mfupi tu tunaweza tukafaidika kwa hali ya juu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna uhitaji wa Serikali ya Afrika Kusini kuanza kufundisha Kiswahili. Hizi ni juhudi za Serikali vile vile kwa ushirikiano na Serikali ya Afrika Kusini. Kama nilivyoeleza katika jibu la msingi, kimsingi walimu wetu wamenufaika na hizi fursa na wanapelekwa kwa kasi sana kwa sababu ni matangazo yanakuwa ya hadhara kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Balozi zetu kuiga mfano wa Italy, tumepokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tunasisitiza kabisa kabisa. Yapo mambo mengi ambayo katika hali ya kawaida sisi kama Watanzania tunatakiwa kujivunia, Kiswahili chetu kinauzika duniani kote. Tuna redio zaidi ya 13 nje ya Tanzania ambazo zinatumia Kiswahili. Kwa mfano, tuna Idhaa ya Kiswahili ya BBC, tuna Sauti ya Amerika, tuna Redio Japani, Tuna Sauti ya Ujerumani, tuna Sauti ya Umoja wa Mataifa, tuna Redio China na nchi zetu zote hizi za Afrika Mashariki zote zinatumia Kiswahili katika baadhi ya matangazo yake. Kwa hiyo, ni sisi Watanzania kujitangaza katika mazingira yote tunapokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naziomba Balozi zetu huko nje zianzishe majukwaa mbalimbali yakiwepo matamasha ya Kiswahili katika nchi wanazotuwakilisha ili kukitangaza Kiswahili katika uhalisia wake.
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine kusuasua kwa utekelezwaji wa changamoto inapelekea kuibuka kwa changamoto mpya za Muungano. Ni nini commitment ya Serikali kuweza kuzuia changamoto yoyote nyingine ya Muungano isijitokeze?

Swali langu la pili, Serikali inatoa commitment gani ya kutatua changamoto hizi nne zilizobakia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nikianza na swali la kwanza la Mheshimiwa Mbunge namna ya kuzuia changamoto nyingine mpya zisijitokeze, hili ni juhudi ya Serikali zote mbili kuhakikisha wakati wote mara baada ya maamuzi yale yanayojitokeza katika vikao vile vya majadiliano vilivyotatua ile migogoro kuanza utekelezaji mara moja wa yale makubaliano waliyofikia.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, hizi changamoto nne zilizobaki mkononi tunatarajia kwamba kikao chetu kitakuwa mwezi wa Agosti, ambapo katika mazingira ya kawaida hizi zilizobaki ni chache sana tunaweza tukafika mahali, Mungu jalia tutazimaliza zote nne na watu tutaanza kufaida matunda ya Muungano wetu. Ahsante.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa kero za Muungano zina zungumzika, Je, vile vikao vya Wizara moja moja baina ya SMT na SMZ ambao hukaa kuzungumza kero zao bado vinaendelea au vimefunikwa na hivyo vikao vikubwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza kwa msingi wa mazungumzo ya utatuzi wa migogoro hii ambayo iko kati yetu, kitu cha kwanza kabisa ni Wizara zile zenye matatizo yanayosababisha tukasoma kama tatizo kuu kukutana mara kwa mara, kwa sababu hawa ni kama Technical Committee ambazo zinatafuta majibu kwa ajili ya kupeleka kwenye kile kikao kikuu. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunaendelea na vikao vya Wizara kati ya Wizara na Wizara. Kwa mfano, katika haya yaliyobaki Wizara ya Fedha Zanzibar na Wizara ya Fedha Tanzania Bara wanaendelea kuchakata mambo mbalimbali ambayo mwisho wa yote yatatuletea majibu ya utekelezaji. Ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri sana, na tunaomba waendelee kumalizia hiyo Mahakama. Nina swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa maeneo ya Lukumbule na Masakata na Nalasi yamekosa kabisa huduma za kimahakama: Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kuweka Mobile Court katika tarafa hizi ili ziweze kupata huduma za kimahakama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tunashukuru kwa pongezi na shukrani hizo. Kwa sasa Mhimili wa Mahakama una magari mawili (mobile courts) ambazo zinafanya kazi Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Mwanza. Katika bajeti yetu tunategemea kuongeza hizi mobile courts sita Mikoa ya Kagera, Tanga, Dodoma, Arusha, Mara na Morogoro. Tunafanya hivi kwa maeneo ambapo population ni kubwa. Tunatamani tungefika kwa kila Kata, lakini mwenendo wetu wa huu mpango wa Mahakama ni kujenga Mahakama hizo kwa sababu hizi mobile courts ni gharama kuziendesha na wakati mwingine management ya mahabusu na mambo mengine yanaweza yakawa yanaleta gharama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Kata zake hizi ambazo amezitaja, tutaingiza katika mwaka ujao wa fedha, na tutafikia Kata zake na tutazijenga kwenye maeneo ambapo uhitaji upo, ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mahakama ya Wilaya ya Mbulu ni Mahakama chakavu sana iliyojengwa toka enzi za mkoloni; na ni miaka mitatu nimekuwa nikiendelea kuomba ujenzi wa Mahakama hiyo: Je, Serikali ina mpango gani wa kutujengea Mahakama Wilaya ya Mbulu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nijibu swali la Mheshimiwa Issaay Mbunge wa Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa fedha, miongoni mwa maeneo tutayokwenda kujenga, tunategemea kujenga Mahakama 18 za Wilaya. Wilaya ya Mbulu ni miongoni mwa Wilaya ambazo tutajenga Mahakama hii. Kweli eneo lao lile, jengo la Mahakama lipo pembeni ya barabara na kimsingi linatakiwa litoke pale. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba huu mpango tunao na tutajenga katika mwaka huu wa fedha. Upo kwenye list yetu. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niwe na maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Swali langu la kwanza, Taasisi nyingi za Umma zimejikita katika kutoa huduma na hazifanyi biashara: Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka kuondoa kodi ya ardhi ili kuziwezesha taasisi nyingi kuweza kupata hati? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, nataka kujua: Ni lini Serikali itakamilisha kutoa hati katika maeneo 787 yaliyosalia katika Halmashauri za Mkoa wa Songwe ili yaweze kupatiwa hati na kuepusha migogoro ya ardhi isiyokuwa na ulazima baina ya wananchi na Serikali? Nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu hizi Taasisi za Umma kuziondolea kodi, hili tumelichukua na tutakwenda kulichakata na kuona namna nzuri ya kufanya. Mara nyingi sana taasisi zinazoomba kumilikishwa maeneo haya zinakuwa na makusudio maalum pamoja na miradi maalum. Kwa hiyo, kwao inakuwa ni rahisi sana kutumia vyanzo vyao vidogo kwa ajili ya kumilikishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la lini maeneo yaliyobaki katika Mkoa wa Songwe yatakwenda kukamilishiwa umilikishwaji wake? Niwaombe hizo taasisi kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, waanze mchakato wa kuomba namna ya umilikishwaji. Hatua zote ziko wazi na taasisi hizo zote zinaelewa utaratibu ambao tumejiwekea katika uratibumzima wa kumilikisha ardhi hapa nchini.
MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa vile Waziri amekiri kwamba kituo hiki kutokana na uchakavu tayari kimeondoka; na tayari kutokana na mahitaji na eneo lile ni kubwa, kuna miradi mikubwa ya Serikali ambayo ipo sasa: -

a) Je, Serikali haioni haja ya kuweka kituo cha dharura katika eneo hili la Tumbe?

b) Je, Wizara iko tayari kwenda kukaa na ofisi ya mkuu wa wilaya pamoja na halmashauri kuangalia eneo kubwa au kupatiwa eneo ambalo litatosha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omar Issa Kombo, Mbunge wa Wingwi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, ni kweli kabisa kwamba eneo hili lina matumizi makubwa kwa kuwa pia kuna miradi mikubwa ambayo inahitaji kituo cha polisi. Lakini kituo cha polisi cha dharura kinaweza kikapatikana endapo tu mamlaka za halmashauri husika zitatenga jengo ambalo litakuwa na sifa ya kutumika kama kituo cha polisi.

Mheshimiwa Spika, suala la eneo; kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni jukumu la halmashauri sasa kutafuta eneo ambalo tunakwenda kujenga kituo kipya. Na Wizara iko tayari kutoa ushirikiano kwa mamlaka za halmashauri hiyo ili kituo hicho kiweze kujengwa haraka sana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza, kwa vile kumekuwa na malamaiko ya wananchi ambao wananyang’anywa mashamba yao halafu wanapewa hela. Katika harakati za kuhangaika kutafuta mashamba mpaka ile hela inaisha. Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kuelimisha wananchi kuhusu Sheria hii ili pale wanapopewa fedha waombe pia wapewe na shamba?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kutokana na kwamba ardhi kubwa ya Tanzania haijapimwa. Je, Serikali itakapowapa mashamba mbadala hawa wananchi walionyang’anywa itawahahikishiaje kwamba hawatahamishwa tena maana haya yameshatokea na wananchi wanahangaika sana katika kuji-establish mara ya tatu. Naomba nipate majibu.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa swali lake la kwanza kwamba tutoe elimu ya hii Sheria kwa wananchi ili waweze kupata fidia zote mbili kwa pamoja au kwa namna yoyote ile.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, suala la fidia linazingatia sana mazingira ya eneo ambapo mtu anafidiwa. Kwa hao wenzetu wa kulima kimsingi mamlaka za Mkoa huwa zinashirikishwa kwa karibu sana katika suala zima la namna ya kuwapa fidia ya maeneo mengine wale wananchi na kumekuwa hakuna matatizo makubwa sana. Usalama wa mashamba pale wanapofidiwa yale mashamba kwa vyovyote kama ni mkono wa Serikali umekwenda kuwaondoa pale. Yale mashamba mapya watakayopewa lazima yatolewe kwa utaratibu wa kupimwa na wapewe zile hati ambazo zitawasaidia kuwaweka kwenye usalama wa maeneo mapya waliyopewa.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nilitaka kujua ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa shamba la EFATHA ambalo unavikumba vijiji vya Msanda, Muungano, Kaungu, Sandulula, Malonje, Ulinzi na Mawenzusi. Ni lini sasa mgogoro huu utaisha wananchi wanapata tabu sana sana hawana pa kulima. Tunaomba Serikali imalize mgogoro huu. Ni lini sasa Serikali itamaliza mgogoro huu? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza Waheshimiwa Wabunge ni wape angalizo. Vyanzo vingi vya migogoro ni matumizi ya nguvu yasiyozingatia utaratibu. Tunapotoa shamba kwa mwekezaji, mwananchi mwingine yeyote haruhusiwi kwenda kulivamia lile shamba bila kuzingatia taratibu. Kama unaona kabisa kwamba zile taratibu za umiliki wa yule mmiliki zimekiukwa fuata taratibu tulishatoa maelekezo. Halmashauri zianzishe ule mchakato wa kumjadili huyu muhusika wa shamba hilo ambaye amelitelekeza.

Mheshimiwa Spika, wananchi kuanza kuvamia maeneo haya kwa kweli sio kitu cha busara sana. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge sisi ni viongozi wote tushirikiane kwenye hili kuwaelimisha wananchi juu ya taratibu zinazoweza zikafatwa ili kupata kile ambacho tunakihitaji kwa matumizi yetu.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri anataka kujua mgogoro utamalizwa lini maana yake mgogoro upo wewe umeelezea kuzalishwa kwa mgogoro sasa kwa kuwa mgogoro tayari upo utakwisha lini ndio swali la Mbunge.(Makofi)

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kusema maelezo haya tayari tumekwishaanza na tumeunda timu ya ufatiliaji ili makundi ya pande mbili zote yakutane ili kuona uwekezekano wa kulimaliza hili tatizo.

Mheshimiwa Spika, kama mninavyosema vyanzo vikubwa vya migogoro hii ni matumizi ya nguvu zisizozingatia taratibu.

SPIKA: Hilo umeshaeleweka, hoja ni kwamba mgogoro ukisha kuwepo lazima umalizwe, lazima umalizwe. Ukishakuwepo mgogoro umeshatengenezwa lazima umalizwe sasa aliyepelekea huko. Naona Waziri amesimama.

Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa kwa ajili ya kujibu suala hili na nimshukuru pia Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, mgogoro huu wa EFATHA na wananchi wa Sumbawanga kama alivyosema. Mgogoro huu ni wa siku nyingi na mgogoro ulisha wahi kufika mahakamani lakini ulitokana pia na mgawanyo wa maeneo katika lile eneo ambapo mwekezaji alipewa. Mwekezaji alifata taratibu zote katika kupewa yale maeneo. Changamoto inapokuja ni kwamba kadri mahitaji ya wananchi yanavyozidi kuwa makubwa basi wanaona kama vile mwekezaji pengine amekiuka taratibu katika kupewa, lakini taratibu zote zifuatwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie wananchi wa Jimbo la Sumbawanga ambako ndiko kuna mgogoro huo, nitakwenda mwenyewe kule kwa ajili ya kuzungumza nao ili tuweze kuumaliza kwa sababu umekuwa ni wa muda mrefu. Tutapanga na Mbunge kwenda kuumaliza mgogoro huo. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri, kwanza naipongeza Serikali kwa niaba ya Mheshimiwa Askofu Gwajima, kwa kweli alikuwa huko na amelishughulikia suala hili na Serikali imelipokea na imelifanyia kazi. Pongezi sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, Serikali imejipanga vipi sasa kuhakikisha inadhibiti migogoro yote iliyopo katika jimbo hilo ili isijirudie tena? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha Mgogoro wa Shamba la Malolo upande wa Jimbo la Kibamba Halmashauri ya Ubungo nao unaumaliza kama vile walivyomaliza kwenye Wilaya ya Kinondoni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza udhibiti wa migogoro isiweze kujitokeza, ni juhudi za Serikali na tumekuwa tukishirikiana na taasisi mbalimbali katika kuhamasisha migogoro hii isiendelee kujitokeza. Hata hivyo, suala la Malolo, Kibaha nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwamba baada ya Bunge lako Tukufu kumalizika, tutaanza ziara za kutembelea maeneo haya na kukutana na wananchi na taasisi zile ambazo zinagongana kwenye migongano hii ili kuitafutia suluhisho la kudumu, ahsante. (Makofi)
MHE. NANCY H. NYALUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sheria imeweka wazi na inakataza lumbesa, lakini lumbesa bado inaendelea: Je, Serikali ina mkakati gani wa ziada kuhakikisha kwamba inakomesha ujazo wa lumbesa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli lumbesa ni jambo ambalo siyo la kisheria. Nitoe wito tu kwa wasimamizi wa hizi biashara za vijijini hasa maeneo hayo ambayo wananchi wanakiuka utaratibu, hatua za kisheria zichukuliwe dhidi ya wale ambao wanaweka nje ya kipimo halisi na hasa kwenye mamlaka hizo za Halmashauri ambako Maafisa Biashara wanasimamia mazoezi haya.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, eneo linalotumiwa na Kituo Kidogo cha Polisi cha Ngaramtoni linatumiwa tangu mwaka 1984 ambalo liko chini ya Wizara ya Kilimo; je, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, haioni ni vizuri sasa wakaomba eneo hilo ili waweze kurasimishiwa moja kwa moja badala ya kusema hawana eneo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa Jeshi la Polisi ndiyo limepewa mamlaka ya kuangalia raia na mali zao: Je, Serikali inaona ni vizuri Askari kukaa kwenye makuti bila nyumba wala Kituo cha Polisi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA, NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mambo ya Ndani kuzungumzia suala ambalo limetengwa kwa ajili ya shughuli za kilimo na sasa limekosa kibali cha watu wa Polisi kujenga, mazungumzo yanaendelea kati ya Wizara hizi mbili ili kupata kibali cha kuhalalisha hilo eneo ili liweze kujengwa Kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili eneo la usalama wa mali za wananchi, Polisi wanatambua umuhimu mkubwa kabisa wa usalama wa wananchi na mali zao, na hivyo basi ndiyo maana msukumo wa mazungumzo unaendelea kati ya hizi taasisi mbili ili kuweza kuhalalisha hiyo eneo na badae kujenga kwa ajili ya usalama wa wananchi.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nilitaka tu nimshauri Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru wakakae na Halmashauri yao watafute eneo. Eneo la Wizara ya Kilimo linatumika kwa ajili ya wafanyakazi wa utafiti na pale tuliwapa hifadhi ya muda, watafute eneo lingine. Wizara haitatoa kipande cha ardhi cha uzalishaji wa mbegu. (Makofi)
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali ina mikakati gani ya kutujengea mahakama ya Mwanzo katika Tarafa ya Manyovu na Muyama?

Pili, kwa kuwa Tarafa ya Manyovu ina Kata 14 ambazo kijiografia zimesambaa umbali mrefu, Kata Saba zina umbali kwenda Makao Makuu ya Tarafa kati ya kilometa 50 – 84. Je, Serikali inaweza kutusaidia Mahakama mbili za mwanzo katika Tarafa moja ya Manyovu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusu ujenzi wa Mahakama hizi mbili alizoziomba katika Tarafa ya Manyovu na Muyama hizi zipo katika mpango ambao tulikwishaueleza huko nyuma kwamba tunakwenda kujenga Mahakama katika Tarafa zote nchini na program hii itakwisha 2025 ambapo tuna uhakika Tarafa zote zitakuwa zimepata Mahakama.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Kata ambazo zipo mbali na Makao Makuu ya Tarafa, ofisi yangu imeweka utaratibu wa kufanya assessment kutoka kwenye Makao Makuu ya Tarafa na itatoa upendeleo kwa Kata zile ambazo ziko mbali. Kwa hiyo, nina uhakika kabisa kwa sababu baada ya Bunge hili ziara yangu ya kwanza ni Kigoma, tutakwenda kuangalia hiyo na kuipa umuhimu unaostahiki.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Mahakama za Mwanzo hasa zilizopo Vijijini ambazo miundombinu yake imechakaa sana, ikiwepo Mahakama ya Gonja Maore, Jimbo la Same Mashariki katika Mkoa wa Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mahakama nyingi za mwanzo zilijengwa katika mfumo ambao ni wa kizamani sana, na kwa sasa tunaendelea kuziondoa zingine katika sura kabisa ya Mahakama ulivyo sasa ili tujenge Mahakama nyingine nzuri zaidi. Kuhusu ukarabati kwa zile ambazo tunaziangalia kama zinaweza zikarekebika hizo ndizo tunaziwekea mpango wa kwenda kuzifanyia ukarabati na zoezi hilo linaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Gonja, Mahakama za Mwanzo kama nilivyoeleza kwamba tutazipitia nazo kuangalia namna ambavyo tunaweza tukazifanyia kazi. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye bajeti iliyopita tulitengewa fedha kwa ajili ya kujenga Mahakama ya Wilaya ya Kyerwa lakini mpaka sasa Mahakama hiyo haijaanza kujengwa. Ni lini Serikali itaanza ujenzi ili kuondoa adha wanayoipata wananchi wa Wilaya ya Kyerwa.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; nipende kujibu swali la Mheshimiwa Bilakwate Mbunge wa Kyerwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika mpangokazi wa Wizara yangu tulipanga kuanzisha ujenzi wa Mahakama hii, iko kwenye mpango wa 2021/2022. Ninapenda tu kumuahidi kwanza Mheshimiwa Mbunge kwamba baada kikao hiki tutawasiliana kuona kama kuna uhakika wowote mradi huo haujaanza kwa sababu ofisi yangu haijapokea taarifa za kutoanza kwa mradi huu. Ahsante.
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Nachingwea ni chakavu na limejengwa tangu enzi za wakoloni. Je, nini mpango wa Serikali wa kujenga jengo jipya litakaloendana na hadhi ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Nachingwea kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwamba ni kweli kama nilivyoeleza kwenye swali ambalo nimetoka kulijibu muda siyo mrafu, tunayo majengo ambayo yamechakaa lakini tunayo majengo ambayo yamekosa hadhi, kwa maana ya uhalisia wa miradi tuliyonayo kwa mwaka huu ambao unakwenda kumalizika tulikuwa tulikuwa na miradi 22, mwaka ujao tutakuwa na miradi 13 na inawezekana kabisa katika mwaka ujao ukawa umeingia kwenye mpango wa kuangalia uwezekano wa kujengewa Mahakama nyingine. Kwa hiyo, naomba tu Mbunge awe na utulivu katika kipindi hiki kwa sababu miradi yote mpaka kufikia 2025 tutakuwa tumekamilisha majengo yote ya ngazi ya Wilaya asante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, asante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali kupitia Mahakama zake imejenga Mahakama za Wilaya kwa kiwango safi kabisa. Je, ni lini Serikali itakamilisha kujenga Mahakama za Wilaya zote Tanzania kwa kiwango kama kile ambacho wameshajenga? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma (Mshua) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza sehemu zote zenye Mahakama, zenye majengo ambayo yanaendelea kutumika hatuna mpango wa kwenda kuvunja na kuanza upya. Tuna mpango wa kujenga mahakama katika maeneo ambayo hayana mahakama kabisa lakini tutakarabati kwa kiwango bora zaidi kwenye yale majengo ambayo sasa yameendelea kutumika asante.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria ameendelea kuyatoa kuhusiana na miundombinu ya Mahakama. Ningependa kuongeza taarifa ya uhakika kwamba Mahakama ya Tanzania ilishafanya utafiti wa hali ya miundombinu ya Mahakama nchi nzima kwa ngazi ya Mahakama za Wilaya, Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama Kuu. Kwa hiyo, upo mpango wa miaka mitano unaohusu ujenzi wa miundombinu ya Mahakama. Mpango ambao unaendana na mpango mkakati wa Mahakama ambao unaendana na kiasi cha fedha kilichotengwa kwa mahala ambako hakuna jengo la Mahakama kabisa, vilevile fedha iliyotengwa kwa Mahakama zinazohitaji ukarabati.

Mheshimiwa Spika, nitaomba labda Wizara ya Katiba na Sheria inachoweza kufanya ni kuwasilisha ule mpango ofisini kwako ili baadae mpango huo uweze kufikika kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Pia tutaangalia uwezekano vilevile nakala kwa njia laini kama itawezekana ukaweza kuwa accessible na kila Mbunge. Nashukuru. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali iliahidi kujenga jengo la Mahakama katika Tarafa ya Heru, tarafa maalum ambayo alikuwa akiishi Mwami Theresa Ntare. Je, ni lini sasa Serikali itajenga jengo kumuenzi Mwami Theresa Ntare? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kwamba tunapopeleka miradi kwenye maeneo mbalimbali tunapeleka kwa ajili ya mahitaji ya watu, sina uhakika sana kama tutakuwa tukipeleka kwa majina ya watu. Mimi ninapenda tu kumhakikishia kwamba eneo hilo kwa mahitaji yake tutakwenda kulipitia na kuona umuhimu wa kuweka hilo jengo lakini siyo kwa sababu aliishi mtu Fulani. Ahsate.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Jengo linalotumika katika Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Meatu halikidhi hadhi kwa sababu lilikuwa ni Mahakama ya Mwanzo tukiwa Wilaya ya Maswa. Je, Serikali iko tayari kutujengea jengo jingine kwa kuwa eneo la kujenga Mahakama ya Wilaya tunalo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kujenga jengo la Wilaya kama tu wanaendelea kutumia majengo ambayo hayakuwa mahsusi kwa ajili ya Mahakama za Wilaya. Kama tulivyoeleza hapo mwanzo tayari wako kwenye mpango na tutakapowasilisha ofisini kwako na kuwatumia wao wataona kila mtu kwenye position yake Mahakama yake inajengwa lini. Asante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kalambo ni miongoni mwa Wilaya ambazo hazina Mahakama za Wilaya na tayari kiwanja kilishapatikana kwa ajili ya ujenzi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya. Je, Serikali ina kauli gani kwa ajili ya kujenga Mahakama katika Wilaya ya Kalambo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephati Kandege Mbunge wa Kalambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika maelezo yangu ya utangulizi ni kwamba Serikali iko kwenye mkakati wa kujenga Mahakama za Wilaya na mradi huu utachukua kama alivyouleza AG unaishia 2025/2026. Kwa hiyo napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba anakwenda kujengewa Mahakama ndani ya kipindi hiki nilichokitaja na nitawasiliana nae kumpa uhalisia wa mwaka ambapo tunapeleka mradi wake.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kweli kuniruhusu na mimi niulize swali la nyongeza. Mahakama ya Wilaya ya Uyui inafanyakazi katika chumba kidogo kilichoazimwa kutoka kwa DC. Je, lini Serikali itajenga jengo la Mahakama ya Uyui?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maige Mbunge wa Uyuwi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kule tuna mradi tayari unaendelea na tutafuatilia kuona unakamilika lini.
MHE. ESTHER L. MIDUMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Itilima ni Wilaya mpya haina jengo la Mahakama.

Je, ni lini Serikali itajenga jengo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kwimba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kwimba ni Wilaya mpya na katika maelezo yangu ya utangulizi nimeeleza uhalisia wa mpango kazi ambao tunakwenda nao. Mimi nitapenda tu kuwasiliana nae baada ya kipindi hiki leo hii ili nimpe kalenda ya ujenzi utakavyoanza katika eneo lake la Kwimba. Ingawa katika mazingira ya kawaida Kwimba ipo katika mpango wa 2021/2022 program ambayo nina uhakika kabisa Kwimba kuna jengo linaendelea.
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mahakama ya Wilaya ya Lushoto ni ya zamani tangia mkoloni. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati au kujenga Mahakama mpya Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi Mbunge wa Lushoto kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Lushoto nilifanya ziara hivi karibuni na tayari wataalam walishafanya assessment juu ya ukarabati ule. Kwa hiyo, muda wowote jengo lile la Wilaya linaweza likaanza ukarabati. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza nishukuru Serikali kwa kujenga Mahakama ya Hydom imekamilika kabisa. Je, ni lini sasa Mheshimiwa Waziri mnafungua Mahakama ile ya Hydom ili ipate kutumika?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hydom tayari jengo limeshakamilika na utaratibu wa matumizi unaweza ukaanza wakati wowote. Lini tutakwenda kuzindua rasmi ni mpango wa Mahakama ambao huwa wana utaratibu ambao wanautumia katika kwenda kuzindua na uanzishwaji wa matumizi ya Mahakama. Juzi Waziri wangu alikuwa pale Hydom kuangalia hilo jengo na nina uhakika kabisa Mheshimiwa Mbunge alikubaliana jambo na Mheshimiwa Waziri. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Katika Wilaya ya Songwe, ujenzi wa Mahakama umeshaanza tangu mwaka jana, je, lini Serikali itamaliza ujenzi katika Wilaya hii? Hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini changamoto za Mahakama katika Wilaya ya Ileje ni nyingi sana katika Tarafa zote mbili Mbundali na Ulambia, sasa nilitamani kufahamu ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha katika tarafa hizi zote kutakuwa na majengo ya Mahakama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katibu na Sheria, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, umaliziaji wa jengo la Songwe kimsingi upo mwishoni kabisa, ni matarajio yetu katika muda mfupi ujao jengo lile litaweza kukamilika na kwa sababu lilikuwa kwenye mpango huu unaoishia mwezi wa sita na baada ya kikao hiki cha Bunge tutakwenda kuliangalia ili tujue wapi wamekwamia kwa sababu ilikuwa limalizike haraka.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu Mahakama za Ileje, mpango wa Serikali hadi kufikia mwaka 2025 makao makuu yote ya tarafa nchini tutakuwa tumejenga Mahakama ambazo zitakuwa ni bora na nzuri kabisa. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mwandabila baada ya kikao hiki cha Bunge tuwasiliane ili nimpe detail ya mpango kazi ambao tumeuweka kwenye suala la ujenzi wa Mahakama zetu, ahsante. (Makofi)
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina utaratibu wa kuchapisha sheria na marekebisho yake kwa kuziunganisha pamoja kama ilivyo kwa law reports. Sasa tangu mwaka 2002 mchakato huo ulifanyika tena 2019.

Swali langu, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha utaratibu huu unafanyika mara kwa mara ili kuepusha matumizi ya sheria zilizopitwa na wakati?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili, sheria zinaporekebishwa huwekewa RE yaani Revised Edition. Mwaka 2019 siyo sheria zote ziliwekewa Revised Edition. Serikali ina mkakati gani wa kuwekea sheria zote Revised Edition ili kuweza kurahisisha matumizi kwa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Judith kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ule mchakato swali lake la kwanza la nyongeza, nipende tu kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeendelea kujaribu kuziweka hizi sheria katika mfumo ambao ameusema, lakini sehemu kubwa sana ni mkwamo wa fedha kwa ajili ya process nzima ya kuzi-¬combine. Lakini haya marekebisho mengine ambayo ameyazungumza, tumechukua wazo lake na kimsingi tutaendelea kufanya michakato mbalimbali kwa ajili ya kuziunganisha. Ahsante.
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa kufanya tafsiri kwenye sheria zetu kutoka lugha ya Kiingereza kwenda Kiswahili ili wananchi wetu waweze kupata uelewa wa sheria zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumjibu Mheshimiwa Bahati kwamba sasa hivi Serikali imeendelea na mchakato. Wataalam wetu wako kambini wanaendelea kuzitafsiri hizi sheria ili ziweze kuja sasa kwa sura ya lugha ya Kiswahili. Lakini ni matarajio yetu kufikia mwaka 2023 tutakuwa tayari tumekamilisha kwa sababu kuna miainisho mbalimbali ambayo ni process za kutengeneza hizi sheria kuziamisha kwa lugha mbalimbali. Ahsante.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali ina mikakati gani ya kutujengea mahakama ya Mwanzo katika Tarafa ya Manyovu na Muyama?

Pili, kwa kuwa Tarafa ya Manyovu ina Kata 14 ambazo kijiografia zimesambaa umbali mrefu, Kata Saba zina umbali kwenda Makao Makuu ya Tarafa kati ya kilometa 50 – 84. Je, Serikali inaweza kutusaidia Mahakama mbili za mwanzo katika Tarafa moja ya Manyovu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusu ujenzi wa Mahakama hizi mbili alizoziomba katika Tarafa ya Manyovu na Muyama hizi zipo katika mpango ambao tulikwishaueleza huko nyuma kwamba tunakwenda kujenga Mahakama katika Tarafa zote nchini na program hii itakwisha 2025 ambapo tuna uhakika Tarafa zote zitakuwa zimepata Mahakama.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Kata ambazo zipo mbali na Makao Makuu ya Tarafa, ofisi yangu imeweka utaratibu wa kufanya assessment kutoka kwenye Makao Makuu ya Tarafa na itatoa upendeleo kwa Kata zile ambazo ziko mbali. Kwa hiyo, nina uhakika kabisa kwa sababu baada ya Bunge hili ziara yangu ya kwanza ni Kigoma, tutakwenda kuangalia hiyo na kuipa umuhimu unaostahiki.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Mahakama za Mwanzo hasa zilizopo Vijijini ambazo miundombinu yake imechakaa sana, ikiwepo Mahakama ya Gonja Maore, Jimbo la Same Mashariki katika Mkoa wa Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mahakama nyingi za mwanzo zilijengwa katika mfumo ambao ni wa kizamani sana, na kwa sasa tunaendelea kuziondoa zingine katika sura kabisa ya Mahakama ulivyo sasa ili tujenge Mahakama nyingine nzuri zaidi. Kuhusu ukarabati kwa zile ambazo tunaziangalia kama zinaweza zikarekebika hizo ndizo tunaziwekea mpango wa kwenda kuzifanyia ukarabati na zoezi hilo linaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Gonja, Mahakama za Mwanzo kama nilivyoeleza kwamba tutazipitia nazo kuangalia namna ambavyo tunaweza tukazifanyia kazi. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye bajeti iliyopita tulitengewa fedha kwa ajili ya kujenga Mahakama ya Wilaya ya Kyerwa lakini mpaka sasa Mahakama hiyo haijaanza kujengwa. Ni lini Serikali itaanza ujenzi ili kuondoa adha wanayoipata wananchi wa Wilaya ya Kyerwa.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; nipende kujibu swali la Mheshimiwa Bilakwate Mbunge wa Kyerwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika mpangokazi wa Wizara yangu tulipanga kuanzisha ujenzi wa Mahakama hii, iko kwenye mpango wa 2021/2022. Ninapenda tu kumuahidi kwanza Mheshimiwa Mbunge kwamba baada kikao hiki tutawasiliana kuona kama kuna uhakika wowote mradi huo haujaanza kwa sababu ofisi yangu haijapokea taarifa za kutoanza kwa mradi huu. Ahsante.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Nachingwea ni chakavu na limejengwa tangu enzi za wakoloni. Je, nini mpango wa Serikali wa kujenga jengo jipya litakaloendana na hadhi ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Nachingwea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwamba ni kweli kama nilivyoeleza kwenye swali ambalo nimetoka kulijibu muda siyo mrafu, tunayo majengo ambayo yamechakaa lakini tunayo majengo ambayo yamekosa hadhi, kwa maana ya uhalisia wa miradi tuliyonayo kwa mwaka huu ambao unakwenda kumalizika tulikuwa tulikuwa na miradi 22, mwaka ujao tutakuwa na miradi 13 na inawezekana kabisa katika mwaka ujao ukawa umeingia kwenye mpango wa kuangalia uwezekano wa kujengewa Mahakama nyingine. Kwa hiyo, naomba tu Mbunge awe na utulivu katika kipindi hiki kwa sababu miradi yote mpaka kufikia 2025 tutakuwa tumekamilisha majengo yote ya ngazi ya Wilaya. Ahsante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, asante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali kupitia Mahakama zake imejenga Mahakama za Wilaya kwa kiwango safi kabisa. Je, ni lini Serikali itakamilisha kujenga Mahakama za Wilaya zote Tanzania kwa kiwango kama kile ambacho wameshajenga? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma (Mshua) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza sehemu zote zenye Mahakama, zenye majengo ambayo yanaendelea kutumika hatuna mpango wa kwenda kuvunja na kuanza upya. Tuna mpango wa kujenga mahakama katika maeneo ambayo hayana mahakama kabisa lakini tutakarabati kwa kiwango bora zaidi kwenye yale majengo ambayo sasa yameendelea kutumika asante.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria ameendelea kuyatoa kuhusiana na miundombinu ya Mahakama. Ningependa kuongeza taarifa ya uhakika kwamba Mahakama ya Tanzania ilishafanya utafiti wa hali ya miundombinu ya Mahakama nchi nzima kwa ngazi ya Mahakama za Wilaya, Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama Kuu. Kwa hiyo, upo mpango wa miaka mitano unaohusu ujenzi wa miundombinu ya Mahakama. Mpango ambao unaendana na mpango mkakati wa Mahakama ambao unaendana na kiasi cha fedha kilichotengwa kwa mahala ambako hakuna jengo la Mahakama kabisa, vilevile fedha iliyotengwa kwa Mahakama zinazohitaji ukarabati.

Mheshimiwa Spika, nitaomba labda Wizara ya Katiba na Sheria inachoweza kufanya ni kuwasilisha ule mpango ofisini kwako ili baadae mpango huo uweze kufikika kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Pia tutaangalia uwezekano vilevile nakala kwa njia laini kama itawezekana ukaweza kuwa accessible na kila Mbunge. Nashukuru. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali iliahidi kujenga jengo la Mahakama katika Tarafa ya Heru, tarafa maalum ambayo alikuwa akiishi Mwami Theresa Ntare. Je, ni lini sasa Serikali itajenga jengo kumuenzi Mwami Theresa Ntare? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kwamba tunapopeleka miradi kwenye maeneo mbalimbali tunapeleka kwa ajili ya mahitaji ya watu, sina uhakika sana kama tutakuwa tukipeleka kwa majina ya watu. Mimi ninapenda tu kumhakikishia kwamba eneo hilo kwa mahitaji yake tutakwenda kulipitia na kuona umuhimu wa kuweka hilo jengo lakini siyo kwa sababu aliishi mtu Fulani. Ahsate.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Jengo linalotumika katika Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Meatu halikidhi hadhi kwa sababu lilikuwa ni Mahakama ya Mwanzo tukiwa Wilaya ya Maswa. Je, Serikali iko tayari kutujengea jengo jingine kwa kuwa eneo la kujenga Mahakama ya Wilaya tunalo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kujenga jengo la Wilaya kama tu wanaendelea kutumia majengo ambayo hayakuwa mahsusi kwa ajili ya Mahakama za Wilaya. Kama tulivyoeleza hapo mwanzo tayari wako kwenye mpango na tutakapowasilisha ofisini kwako na kuwatumia wao wataona kila mtu kwenye position yake Mahakama yake inajengwa lini. Asante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kalambo ni miongoni mwa Wilaya ambazo hazina Mahakama za Wilaya na tayari kiwanja kilishapatikana kwa ajili ya ujenzi wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya. Je, Serikali ina kauli gani kwa ajili ya kujenga Mahakama katika Wilaya ya Kalambo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephati Kandege Mbunge wa Kalambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika maelezo yangu ya utangulizi ni kwamba Serikali iko kwenye mkakati wa kujenga Mahakama za Wilaya na mradi huu utachukua kama alivyouleza AG unaishia 2025/2026. Kwa hiyo napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba anakwenda kujengewa Mahakama ndani ya kipindi hiki nilichokitaja na nitawasiliana nae kumpa uhalisia wa mwaka ambapo tunapeleka mradi wake.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi. Kwanza kabisa niwapongeze Serikali kwa kutujengea Mahakama Kuu nzuri na ya kisasa katika Jimbo la Shinyanga Mjini. Swali langu Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya Mwanzo na Mahakama ya Hakimu Mkazi imechakaa sana, actually ilijengwa tangu kipindi cha ukoloni. Nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba Mahakama hizo zinakarabatiwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Makamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama tulivyoeleza katika mpango wetu kwamba tumetenga fedha za kukarabati majengo yote chakavu nchini na kujenga mapya katika maeneo yale ambayo yana uhitaji huo. Ninakuahidi tu Mheshimiwa Mbunge uvute subira kidogo utaona kazi inaendelea kule kwa ajili ya ukarabati.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kweli kuniruhusu na mimi niulize swali la nyongeza. Mahakama ya Wilaya ya Uyui inafanyakazi katika chumba kidogo kilichoazimwa kutoka kwa DC. Je, lini Serikali itajenga jengo la Mahakama ya Uyui?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maige Mbunge wa Uyuwi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kule tuna mradi tayari unaendelea na tutafuatilia kuona unakamilika lini.

MHE. ESTHER L. MIDUMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Itilima ni Wilaya mpya haina jengo la Mahakama.

Je, ni lini Serikali itajenga jengo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kwimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kwimba ni Wilaya mpya na katika maelezo yangu ya utangulizi nimeeleza uhalisia wa mpango kazi ambao tunakwenda nao. Mimi nitapenda tu kuwasiliana nae baada ya kipindi hiki leo hii ili nimpe kalenda ya ujenzi utakavyoanza katika eneo lake la Kwimba. Ingawa katika mazingira ya kawaida Kwimba ipo katika mpango wa 2021/2022 program ambayo nina uhakika kabisa Kwimba kuna jengo linaendelea.

MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mahakama ya Wilaya ya Lushoto ni ya zamani tangia mkoloni. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati au kujenga Mahakama mpya Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi Mbunge wa Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Lushoto nilifanya ziara hivi karibuni na tayari wataalam walishafanya assessment juu ya ukarabati ule. Kwa hiyo, muda wowote jengo lile la Wilaya linaweza likaanza ukarabati. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza nishukuru Serikali kwa kujenga Mahakama ya Hydom imekamilika kabisa. Je, ni lini sasa Mheshimiwa Waziri mnafungua Mahakama ile ya Hydom ili ipate kutumika?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hydom tayari jengo limeshakamilika na utaratibu wa matumizi unaweza ukaanza wakati wowote. Lini tutakwenda kuzindua rasmi ni mpango wa Mahakama ambao huwa wana utaratibu ambao wanautumia katika kwenda kuzindua na uanzishwaji wa matumizi ya Mahakama. Juzi Waziri wangu alikuwa pale Hydom kuangalia hilo jengo na nina uhakika kabisa Mheshimiwa Mbunge alikubaliana jambo na Mheshimiwa Waziri. Ahsante. (Makofi)