Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Geophrey Mizengo Pinda (43 total)

MHE. ZAINAB A. KATIMBA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha baadhi ya Sheria kandamizi kwa Wanawake ili ziendane na wakati?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu nasimama mbele ya Bunge lako kwa mara ya kwanza. Pia niwashukuru wananchi wa Kavuu kwa kunidhinisha kuwa Mbunge wao. Vilevile nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniona nafaa kuwakilisha Wizara hii ya Katiba na Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum kupitia Mkoa wa Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kabla ya kujibu swali la msingi, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kuwa Serikali haina sheria kandamizi. Sheria zote zinazotumika nchini zilitungwa na Bunge lako Tukufu ambalo halijawahi kutunga sheria kandamizi. Aidha, Serikali kwa kuzingatia mahitaji ya wakati na watu wake, imekuwa ikiwasilisha mapendekezo ya marekebisho ya sheria mbalimbali ili kuziboresha sheria hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na wakati tulionao na mahitaji ya sasa, Serikali imeanzisha mchakato wa kuzipitia baadhi ya sheria ili ziweze kufanyiwa marekebisho kuendana na wakati. Hivi sasa, Serikali kupitia Wizara imeandaa Muswada wa Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria ya Ndoa utakaowasilishwa katika Bunge lako Tukufu ili kuiboresha, kwa lengo la kulinda makundi ya wanufaika na sheria hii. Aidha, Serikali inaendelea na hatua mbalimbali za kupitia Sheria ya Usimamizi wa Mirathi na Sheria za Kimila. Hatua hizo zikikamilika, Muswada wa Mapendekezo ya kuzirekebisha sheria hizo utawasilishwa kwenye Bunge lako Tukufu ili Wabunge wapate nafasi nzuri ya kujadiliana na kuyapitisha marekebisho hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa Wizara ipo katika mabadiliko makubwa ya kuhakikisha kunafanyika maboresho makubwa ya sheria zetu ikiwemo kuzitafsiri kwa Kiswahili lakini pia kuweka vipengele kwenye sheria hizo vya kutoa hukumu kwa lugha ya Kiswahili jambo ambalo litaleta tija kubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Tunawaomba Wabunge kuunga mkono juhudi za Serikali katika eneo hili kwa lengo la kuimarisha utawala wa sheria na upatikanaji wa haki nchini.
MHE. ALMAS A. MAIGE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Uyui?
NAIBU WAZIRI YA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi ni mara ya kwanza kusimama hapa baada ya uteuzi, nipende tu kutumia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini vilevile kumshukuru Mama yangu Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini katika nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria nipende kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama ya Tanzania kwa muda mrefu imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya uhaba na uchakavu wa majengo na miundombinu ya Mahakama. Katika maeneo mengi Mahakama imekuwa ikitumia majengo ya kuazima kutoka taasisi nyingine na kupangisha ili kuweza kutoa huduma kwa wananchi. Aidha, katika baadhi ya Wilaya wananchi wamekuwa wakipata huduma za Mahakama ya Wilaya katika Wilaya za jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Tabora Wilaya tatu; Uyui, Kaliua na Sikonge hazikuwa na Mahakama. Hivyo, wananchi wa Wilaya hizo wamekuwa wakipata huduma katika Wilaya za jirani ambapo Wilaya ya Uyui na Sikonge wanahudumiwa na Wilaya ya Tabora na Wilaya ya Kaliua wanapata huduma za Mahakama Wilayani Urambo. Mwaka 2020 Mahakama ilianzisha Mahakama ya Wilaya za Uyui na Kaliua katika Majengo ya Ofisi za Wakuu wa Wilaya ili kusogeza huduma karibu na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, utatuzi wa changamoto hii ya majengo inafanyika kwa awamu kadiri bajeti inavyoturuhusu. Katika mipango yake, Mahakama ya Wilaya ya Uyui itajengwa mwaka wa fedha 2022/2023 kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Mahakama ya Wilaya ya Kaliua itajengwa mwaka wa fedha 2021/2022 na tayari zabuni imetangazwa. Vilevile Mahakama inaendelea kukamilisha ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Sikonge, pamoja na ukarabati mkubwa wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Tabora.
MHE. HUSSEIN N. AMAR Aliuliza:-

Je, Serikali ina Mpango gani wa kujenga Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar Mbunge wa Nyang’hwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale ni moja ya miradi itakayojengwa katika mwaka wa fedha 2021/2022. Zabuni ya kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hiyo imekamilika na ujenzi unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Septemba mara baada ya kusainiwa kwa mkataba wa kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza programu iliyojiwekea ya kujenga na kukarabati majengo yote katika ngazi mbalimbali za Mahakama ili kusogeza huduma karibu na wananchi na kuboresha mazingira ya kazi ili kufikia lengo la kuwa na Mahakama za Wilaya katika Wilaya zote hapa nchini ifikapo 2025. Ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA Aliuliza:-

Je, ni kwa nini Mahakama isipewe jukumu la kugharamia chakula cha mahabusu ambao wapo gerezani kutokana na ucheleweshaji wa kesi kupatiwa hukumu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Magereza wapo kwenye wajibu wao wa kisheria wa kutoa huduma ya chakula kwa mahabusu. Hivyo kwa mujibu wa Sheria ya Magereza Sura ya 58 (105) ambacho kinatoa mamlaka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kutunga Kanuni (The Prison Management Regulations) ambapo Kifungu cha 23 cha kanuni iliyotokana na sheria hiyo kimemuelekeza Mkuu wa Magereza kusimamia chakula kwa wafungwa na mahabusu wanapokuwa gerezani kama sehemu ya wajibu wa Magereza.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Mahakama haijawahi kuchelewesha utoaji wa maamuzi ya mashauri mbalimbali bila uwepo wa sababu muhimu zinazochangia kucheleweshwa kwa kesi husika. Wote tunafahamu kuwa vipo vyombo mbalimbali vinavyohusika katika suala la kesi. Vyombo hivi ni kama Polisi, Magereza, TAKUKURU, Ofisi za Mashtaka, Ofisi ya Mkemia Mkuu na kadhalika, kabla ya kuifikia Mahakama.

Mheshimiwa Spika, hivyo katika sura ya kawaida huonekana kuwa Mahakama ndizo zinazochelewesha utoaji wa hukumu, lakini ukweli ni kwamba kesi huchakatwa na vyombo nilivyovitaja; na wakati mwingine mchakato huchukua muda mrefu kabla ya kutoa nafasi kwa Mahakama kutoa maamuzi. Hata hivyo ninatoa wito kwa vyombo husika kuharakisha michakato inayopita kwenye vyombo vyao ili kufanya Mahakama kutoa hukumu kwa wakati na hivyo kufanya wananchi kupata haki zao kwa wakati. Ahsante. (Makofi)
MHE. WANU HAFIDH AMEIR aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha elimu ya Sheria zinazowapa kinga na haki Wanawake inatolewa kwa Wanawake wote Mijini na Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Wanu Hafidh Ameir, Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mipango iliyopo ya kutoa elimu ya sheria si tu kwa wanawake, bali ni pamoja na makundi mengine maalum katika jamii, wakiwemo watoto, watu wenye ulemavu na wazee. Na kuendelea kutoa mafunzo na kusajili watoa huduma ya msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria. Kuanzisha madawati ya huduma ya msaada wa kisheria katika Mahakama, kutekeleza Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili zidi ya Wanawake na Watoto. Mkakati huu unalenga kuimarisha na kulinda haki za wanawake na watoto, kuanzisha madawati ya msaada wa kisheria katika Vituo vya Polisi na Magereza, kutafsiri sheria zote kwa lugha ya Kiswahili na kuendelea kutoa mafunzo ya sheria kwa wananchi kupitia mikutano na mihadhara mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2017 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilitunga Sheria ya Msaada wa Kisheria, Na. 1 ya Mwaka 2017. Madhumuni ya Sheria hii pamoja na mambo mengine ni kuhakikisha msaada wa kisheria, ambao una maana ya utoaji wa elimu na ushauri wa kisheria, uandishi wa nyaraka za kisheria/kimahakama na/ au uwakilishi mahakamani kwa watu wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za mawakili. Tangu kutungwa kwa sheria hii hadi Machi, 2021, takribani wanawake 3,162,421 kutoka mijini na vijijini wamepatiwa elimu na msaada wa kisheria kupitia madhimisho ya wiki ya sheria, wiki ya msaada wa kisheria ambayo inaadhimishwa kila mwaka katika mikoa yote hapa nchini, vipindi vya redio na luninga, ziara za viongozi na wataalamu wa Wizara katika magereza na mahabusu za polisi na majukwaa mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kutimiza azma ya kuhakikisha kuwa wananchi wanapata haki kwa gharama nafuu na kwa wakati. Aidha nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuwahamasisha wananchi kuwatumia watoa huduma wa msaada wa kisheria, wakiwemo wasaidizi wa kisheria, walio katika maeneo yao nchi nzima wanapokabiliana na changamoto mbalimbali za kisheria ili kuifikia haki iliyokusudiwa, ahsante.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itasomesha wataalam wa Court Reporter na Stenographer ili Mahakama zetu ziwe na wataalam hao?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Katavi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa sasa haina mpango wa kusomesha wataalamu waandishi wa Stenographer (Stenographer na Court Reporters) ambao hufanya kazi za uandishi wa maelezo ya mijadala ya wakati wa uendeshaji wa kesi Mahakamani. Kazi hizo kwa sasa zinafanywa na Waheshimiwa Majaji na Waheshimiwa Mahakimu.

Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kuangalia utaratibu mzuri wa kuwatumia wataalamu hawa ambao kwa sasa hawapo katika Muundo wa Utumishi wa Mahakama. Baada ya kukamilika kwa utaratibu unaoangaliwa na kuingizwa kwenye Muundo wa Utumishi wa Mahakama, Wizara itaandaa mpango wa mafunzo kwa wataalamu hao kuanza kuwasomesha rasmi tayari kwa kuanza kuwatumia kwenye Mahakama zetu hapa nchini. Ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA (K.n.y. MHE. NANCY H. NYALUSI) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Tarafa ya Mahenge Wilayani Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa Mahakama ya Tarafa ya Mahenge iliyopo Wilaya ya Kilolo ni miongoni mwa Mahakama za Mwanzo hapa nchini zitakazoanza kujengwa kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022.

Napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kupitisha Wizara ya Katiba na Sheria ambayo ndiyo inayokwenda kutekeleza ujenzi wa Mahakama hiyo. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge avumilie kidogo kuanzia Julai, Mahenge wanakwenda kushuhudia kuanzwa kwa ujenzi huo. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga Mahakama Hydom katika Jimbo la Mbulu Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Ujenzi wa Mahakama ya Hydom ni moja ya miradi ambayo Mahakama imesaini mkataba Machi, 2021 na tayari Mkandarasi ameanza kazi. Mradi huu utakamilika ifikapo mwezi Agosti, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka mitano 2016/2017 – 2020/2021, Mahakama inafanya maboresho makubwa ili kukabiliana na changamoto ya uhaba na uchakavu wa majengo. Maboresho hayo ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa majengo katika maeneo mbalimbali kwa ngazi zote za Mahakama. Ahsante.
MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza: -

Kumekuwepo na mkanganyiko wa tafsiri ya umri wa miaka 18 katika Sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Mtoto na Sheria ya Kanuni za Adhabu na kupelekea kuvunja misingi ya Katiba: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuzifanyia mapitio Sheria hizo hususan kifungu cha 131 (2) ya Sheria ya Kanuni za Adhabu?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Cyprian Tweve Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, mtu aliye na umri chini ya miaka 18 anatambulika kuwa ni mtoto. Pamoja na kwamba kifungu cha 4(1) cha Sheria ya Mtoto kinabainisha kuwa mtoto ni mtu mwenye umri chini ya miaka 18, Kifungu cha 131(2) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu hakitoi tafsiri ya mtoto bali kinatoa adhabu kwa mtu mwenye miaka 18 au chini ya hapo anayekuwa na hatia ya kosa la kubaka na kupewa adhabu mbalimbali ikiwemo kuchapwa viboko kwa mkosaji wa mara ya kwanza, kufungwa jela kwa miezi 12 pamoja na viboko kwa mkosaji wa mara ya pili, au kifungo cha maisha kwa mkosaji kwa mkosaji anayejirudia kwa mara ya tatu. Kitaalamu hawa wanaitwa young offenders’ au wakosefu wenye umri mdogo.

Mheshimiwa Spika, Sheria zetu mbalimbali nje ya sheria ya Mtoto, zinaweka umri wa mtoto kulingana na muktadha na mazingira ya jambo mahsusi kama vile mikataba, jinai, kupiga kura, leseni za udereva na kadhalika. Kufuatia kutungwa Sheria ya Mtoto mwaka 2009, iliyotokana na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Mtoto wa 1989 pamoja na masharti ya Ibara za Haki za ujumla za Binadamu kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, na kwa kuwa Kifungu cha 131(2) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kilifanyiwa marekebisho mwaka 2009 na baada ya kutungwa kwa Sheria ya Mtoto, ni dhahiri kuwa hakivunji misingi ya Katiba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, Serikali sasa inapoendelea kuzipitia sheria mbalimbali, itakipitia pia kifungu hicho cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ili kufanya marekebisho kutokana na uhitaji uliopo kwa kuzingatia ushauri uliotolewa na Mheshimiwa Mbunge, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Majengo ya Mahakama za Mwanzo katika Kata za Nkoanrua na Nkoaranga ambazo majengo yake yamebomoka?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jengo la Mahakama ya Mwanzo Nkoanrua lilichomwa moto na wananchi na hivyo kushindwa kuendelea kutoa huduma katika eneo hilo. Aidha, jengo la Mahakama ya Mwanzo Nkoaranga katika Tarafa ya King’ori ni chakavu na hivyo kuhitaji kujengwa upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, maandalizi ya Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Miundombinu ya Mahakama wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) yanaendelea ambapo utajumuisha mahitaji yote ya ujenzi na ukarabati wa Mahakama katika ngazi zote. Mpango huu utaweka kipaumbele zaidi kwenye ujenzi na ukarabati wa Mahakama za Mwanzo nchini. Lengo la Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha kuwa Tarafa zote 570 zilizopo nchini zinakuwa na Mahakama ya Mwanzo ifikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Mahakama za Mwanzo za Nkoanrua na Nkoaranga zitapewa kipaumbele katika ujenzi na ukarabati kwenye mpango huo.

Napenda kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa Mahakama katika maeneo yetu, kwani kitendo cha kuchoma moto majengo ya Serikali hasa Mahakama, ni kitendo cha kulaaniwa na hakipaswi kurudiwa tena. Ahsante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Mahakama ya Mwanzo katika Tarafa ya Mambwenkoswe ili kuwapunguzia wananchi adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta haki?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kalambo ina Tarafa tano ambazo ni Mambwenkoswe, Matai, Mwimbi, Kasanga na Mwazye. Kati ya hizo, ni Tarafa nne ambazo zina huduma ya Mahakama ya Mwanzo isipokuwa Tarafa ya Mambwenkoswe.

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inao Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Miundombinu ya Mahakama wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) ambao unajumuisha mahitaji yote ya ujenzi na ukarabati wa Mahakama katika ngazi zote za Mikoa, Wilaya na Makao Makuu yote ya Tarafa nchini.

Mheshimiwa Spika, napenda kumwahidi Mheshimiwa Mbunge kuwa katika kipindi hicho Tarafa yake hiyo moja iliyosalia pia itazingatiwa katika mpango huo. Ahsante.
MHE. SALMA R. KIKWETE K.n.y. MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ndoa Bungeni ili kurekebisha Vifungu vya Sheria vinavyohusu Mtoto wa Kike kuolewa akiwa na umri chini ya miaka 18?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali wa yote, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa juhudi za ufuatiliaji kuhusu marekebisho ya Sheria ya Ndoa na kutaka kujua ni lini Muswada huu utawasilishwa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kuwa Muswada wa Sheria ya Ndoa ulifikishwa kwenye Kamati ya Katiba na Sheria mwezi Februari, 2021 kufuatia maamuzi ya Mahakama ya Rufani katika Kesi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali dhidi Rebecca Gyumi, Rufaa Na. 204 ya 2017 na Na.5 ya 2016 ya Mahakama Kuu iliyotaka Sheria ya Ndoa ifanyiwe marekebisho ili mtoto wa kike aolewe akiwa na miaka 18. Kamati baada ya mapitio iliona upo uhitaji wa ushirikishwaji wa wadau wengi zaidi ili kupata maoni zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na zoezi la kushirikisha wadau ambapo hadi sasa Serikali imeweza kufanya mikutano na Viongozi wa Dini katika Mkoa wa Dar es Salaam mwezi Machi, 2021.

Mheshimiwa NaibU Spika, mMkutano wa pili ulifanyika Jijini Dodoma tarehe 2 Julai, 2021 uliojumuisha Wabunge wa Mkoa wa Dodoma na Viongozi wa Halmashauri ya Mkoa wa Dodoma. Kurejeshwa kwa Muswada huu Serikalini kulitokana na unyeti wa jambo lenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa, Serikali itakapokamilisha michakato iliyoelekezwa na Kamati ya Bunge lako Tukufu, Muswada huu utawasilishwa kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kisha kuwasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu kwa ajili ya Kutunga Sheria husika. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa kipaumbele kwa Wilaya ya Busega kujengewa Mahakama ya Wilaya ili kuondoa usumbufu ambao wananchi wanaupata kwa kusafiri hadi Wilaya ya Bariadi kufuata huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mahakama ya Busega ni moja ya miradi itakayojengwa katika Mwaka wa Fedha 2021/2022. Mkandarasi wa ujenzi wa Mahakama hii amepatikana ambaye ni United Builders na kukabidhiwa eneo la ujenzi mwezi Oktoba. Kazi za ujenzi zimeanza na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Aprili, 2022.

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza programu ya maboresho ya majengo ya Mahakama zake na kukarabati majengo ya Mahakama katika ngazi mbalimbali za Mahakama hapa nchini ili kusogeza huduma karibu na wananchi na kuboresha mazingira ya kazi. Ahsante.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza: -

Wanawake na Watoto wanapata shida Baba wa familia anapofariki; pamoja na Sheria ya Mirathi;

Je Serikali ina mpango gani zaidi wa kumsaidia mjane katika masuala ya mirathi?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi anavyofuatilia na kusemea kwa nguvu kuhusu dhuluma wanazofanyiwa wanawake na watoto mara baada ya baba wa familia kufariki.

Mheshimiwa Spika, sheria zinazohusiana na mirathi, zinatamka wazi kuwa wanufaika wa mirathi ni mke wa marehemu, watoto wa marehemu na wazazi wa marehemu. Vilevile inaelekeza kuwa msimamizi wa mirathi si mrithi wa mali za marehemu labda atokane na makundi tuliyoyataja hapo juu. Uteuzi wa msimamizi wa mirathi hufanywa na kikao cha familia na baadaye kuthibitishwa na Mahakama.

Mheshimiwa Spika, kuendelea kwa vitendo vya dhuluma, udhalilishaji wa familia ya marehemu akiwemo mke na watoto, Serikali imeanza kupitia upya Sheria ya Usimamizi wa Mirathi hiyo katika kubaini mapungufu ili iweze kurekebishwa. Kwa kuwa mchakato huo uhusisha taasisi za dini, mchakato umeanza wa kukutana nao na pia kukutana na viongozi wa makabila mbalimbali ili kupitia mila zao ambazo nyingi ni za udhalilishaji.

Mheshimiwa Spika, ikibainika kutokea vitendo vya dhuluma kwa wanafamilia waliopoteza baba wa familia inaelekezwa kwenda Mahakamani kutafuta haki zao. Nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge kutoa ushirikiano wa familia hizo ambazo nyingi hazina uelewa mkubwa wa masuala ya kisheria kufikia ili huduma hii na waweze kupata haki zao. Ahsante.
MHE. CECIL D MWAMBE K.n.y. MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza: -

(a) Je ni lini mikataba ya miradi mbalimbali ya migodi ya madini, ujenzi wa Bandari Bagamoyo, ujenzi wa Reli (SGR), ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, Bomba la Mafuta na Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam italetwa Bungeni ili kupata ufahamu wa miradi hiyo?

(b) Je, katika mikataba hii ni mingapi imewahi kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za mikataba ya ujenzi wa Reli ya SGR, ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, Migodi ya Madini, Bomba la Mafuta na Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam kwa nyakati tofauti Taasisi na Mashirika yanayosimamia miradi hii yamekuwa yakiwasilisha kwenye Kamati za Kudumu za Bunge taarifa za mikataba ya miradi hiyo. Aidha, Kamati zina mamlaka kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge kupata taarifa zozote kuhusiana na mikataba ya miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili, miradi hii imekuwa ikikaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali yaani CAG. Kwa kuwa baadhi ya miradi Serikali inamiliki kwa asilimia 100 na mingine Serikali ni mbia, hivyo taarifa zake huwasilishwa katika Bunge lako tukufu kupitia Ripoti ya CAG. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Sura ya Tano na Sita inabainisha kwa kina taarifa ya ukaguzi ya miradi ya ujenzi wa Reli SGR kwa Lot. 1 na Lot. 2 na Mradi wa Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere. Aidha, mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam umekuwa ukifanyiwa ukaguzi wa kawaida kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumuarifu Mheshimiwa Mbunge na pia Bunge lako tukufu kuwa Bunge limekuwa likipokea taarifa za mikataba na Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kama nilivyoeleza hapo juu. Ahsante.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Mahakama kutoa hukumu ya pande mbili hasa mtuhumiwa anaposhinda kesi kuepuka usumbufu kufungua kesi mpya ya kulipwa fidia?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kanuni na taratibu za madai ya fidia, kuachiwa huru kwa mshtakiwa katika shitaka la jinai hakumpi haki ya moja kwa moja ya kulipwa fidia. Ili mshtakiwa aweze kulipwa fidia kutokana na kushinda shauri la jinai, ni lazima athibitishe Mahakamani kwamba mashitaka dhidi yake yalikuwa ya hila; na kwamba hakukuwa na sababu za msingi za kumshtaki. Kuachiwa pekee kwa mshtakiwa katika shitaka la jinai hakumaanishi mashtaka dhidi yake yalikuwa ya hila na waliomshitaki hawakuwa na sababu ya kuamini alitenda kosa.

Mheshimiwa Spika, kifungu cha 345(2) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kinaipa mamlaka Mahakama kutoa amri ya mtuhumiwa aliyeshinda shauri lake la jinai kulipwa gharama za shauri iwapo shauri hilo liliendeshwa na Mwendesha Mashtaka wa Kujitegemea (Private Prosecutor).
MHE. KENNETH E. NOLLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kuleta mikataba ya madini na nishati ijadiliwe Bungeni kabla ya kuingia makubaliano na wawekezaji?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Ernest Nollo, Mbunge wa Bahi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Utajiri Asili na Maliasilia za Nchi Sura ya 450 kifungu cha 5 inatoa wajibu wa Bunge kwa mujibu wa ibara ya 63 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, katika utekelezaji wa jukumu lake la kuishauri Serikali linaweza kuitisha mikataba inayohusu masuala ya utajiri na rasilimali za nchi na kuweza kupitia kwa lengo la kuishauri Serikali na kutoa azimio la kuondoa masharti hasi katika mikataba. Takwa hili la sheria linazingatia misingi iliyowekwa na sheria, kwamba mikataba au makubaliano yaliyoingiwa kati ya Serikali na wawekezaji yanazingatia haki, usawa na nia njema kwa pande zote na kuzingatia maslahi ya wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiwasilisha mikataba kupitia kamati za kudumu za Bunge na Kamati kuzitolea maelekezo na ushauri kutoka kwa sekta husika. Pale Kamati husika inapoona umuhimu wa kufikisha mkataba mbele ya Bunge lako Tukufu maelekezo hutolewa na kwa kuzingatia Sheria husika.
MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI K.n.y. MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza: -

Je, ni kwa nini kusiwe na Mahakama ya Rufaa Tanzania Kanda ya Zanzibar badala ya kesi kusikilizwa kwa mwaka mara moja?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Rufaa Kanda ya Zanzibar ipo kwa sasa na inaendesha shughuli zake kupitia Masijala ndogo iliyopo Jengo la Mahakama Kuu ya Zanzibar. Hata hivyo, Serikali inaona umuhimu wa kuwa na jengo la Mahakama ya Rufani Zanzibar na inaendelea kulifanyia kazi.
MHE. VINCENT P. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama ya Mwanzo Chala?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Chala yenye Kata nne; za Chala, Nkadasi, Kipande na Mkwamba, ina Mahakama za mwanzo mbili za Chala na Kipande. Katika kuimarisha majengo ya Mahakama kwa kuzingatia mpango uliopo wa ujenzi na ukarabati wa Mahakama nchini, Mahakama ina mpango wa kukarabati jengo la Mahakama ya Mwanzo Chala katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA aliuliza: -

Je, ni lini Mahakama ya Wilaya ya Korogwe itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alfred James Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza mpango wake wa miaka mitano wa Ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama katika ngazi mbalimbali. Kutokana na mpango huo wa Mahakama, jengo la Mahakama ya Wilaya ya Korogwe, limepangwa kujengwa katika mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, Mahakama ya Tanzania ipo katika mpango wake wa ujenzi na ukarabati wa Mahakama zake hapa nchini. Hivyo basi, ujenzi wa Mahakama za Makao Makuu ya Tarafa zote nchini utakamilika ifikapo 2025.
MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, lini Serikali italeta muswada wa sheria wa kuweka ukomo wa upelelezi kwenye kesi za mauaji nchini?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kesi za mauaji zinaangukia katika makosa makubwa (capital offences) zikiambatana na adhabu kubwa ambayo ni kunyongwa hadi kufa au kifungo cha maisha pale mtu anapopatikana na hatia. Hivyo upelelezi wake unahitaji muda na umakini mkubwa ndiyo maana kwa sasa upelelezi haujawekewa ukomo wa kisheria.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Mkurugenzi wa Mashtaka kwa mamlaka aliyopewa chini ya Sheria ya Mashtaka katika kuratibu na kusimamia upelelezi wa makosa ya jinai ametoa Mwongozo wa Mkurugenzi wa Mashtaka Na. 1 wa mwaka 2022 kuhusu ufunguaji wa mashtaka na ukamilishaji wa upelelezi wa kesi za jinai uliotolewa tarehe 30 Septemba, 2022 na kuanza kutumika tarehe 1 Oktoba, 2022. Mwongozo huo unataka upelelezi wa kesi za mauaji ambazo hazihitaji utaalam kutoka taasisi nyingine usichukue zaidi ya siku 60 na zile zinazohitaji utaalamu kutoka taasisi nyingine usichukue zaidi ya siku 90. Ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya katika Halmashauri ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Iramba Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza mpango wake wa kuhakikisha kuwa kila Wilaya inakuwa na jengo la Mahakama. Aidha kwa sasa miradi inayoendelea ni ujenzi wa majengo ya Mahakama za Wilaya 18. Ujenzi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Mkalama umepangwa kufanyika katika mwaka huu wa fedha 2022/2023. Kwa sasa taratibu za kumpata Mkandarasi wa ujenzi zinaendelea. Ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Mahakama ya Wilaya ya Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshmimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza kwa awamu Ujenzi na ukarabati wa majengo yake sehemu mbalimbali hapa nchini. Katika mpango huu, yapo majengo ambayo yanahitaji kujengwa upya kutokana na hali yake na ufinyu wa jengo ikilinganishwa na mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kulingana na hali ya jengo la Mahakama ya Wilaya ya Lushoto, imeamuliwa kuwa jengo hili lijengwe upya badala ya kukarabatiwa lile jengo lililopo kwani ni la zamani sana, finyu na baadhi ya miundombinu yake hairuhusu ukarabati mkubwa. Hivyo, kulingana na Mpango, jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Lushoto litajengwa kwenye kipindi cha fedha 2024/2025. Aidha, kwa sasa jengo lililopo litaendelea kufanyiwa matengenezo madogo madogo hadi litakapopatikana jengo jipya.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa adhabu kali kudhibiti vifo vya akina mama vinavyosabishwa na waume au watoto wao?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Kanuni ya Adhabu imeweka adhabu ya kosa la mauaji ya kukusudia kuwa ni kunyongwa hadi kufa. Aidha, kwa makosa ya mauaji bila kukusudia Mahakama inaweza kutoa adhabu nyingine yoyote kulingana na mazingira na namna kosa lilivyotendeka. Hata hivyo kwa kosa la mauaji ya bila kukusudia sheria imeweka adhabu ya juu ya kifungo cha Maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Adhabu ya Kunyongwa hadi kufa ndiyo adhabu kali kuliko zote hapa nchini pamoja na ulimwenguni kote. Ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO aliuliza: -

Je, Serikali inawasaidiaje wajane ili kuondoa mila na desturi potofu zinazomkandamiza Mwanamke kwenye suala la mirathi?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo Mbunge wa viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa wajane na katika kulinda haki zao kwa kutunga Sheria mbalimbali na Kanuni za kulinda haki za Wanawake wajane katika uuala zima la mirathi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mila na desturi potofu ni eneo ambalo Serikali imeanzisha mchakato wa mapitio ya sheria za kimila ili kuondoa aina yoyote ya ukandamizaji kwa wajane katika suala la mirathi. Serikali inaendelea kutoa elimu kuhusu Sheria ya Mirathi hususani umuhimu wa kuandika wosia ili kuondoa changamoto zinazotokana na mila na desturi potofu.
MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, nini mpango wa Serikali katika kuharakisha kesi za mauaji ambazo huchukua muda mrefu kusikilizwa?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enossy Swalle, Mbunge wa Lupembe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kupitia Ofisi ya Taifa ya Mashtaka imeunda kikosi kazi kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai cha kupitia majalada ya kesi za mauaji zenye muda mrefu kuanzia miezi miwili na kuendelea. Majalada hayo yanafanyiwa mapitio na kutolewa uamuzi. Kikosi kazi hiki kinaendelea na kazi ya kupitia majalada ambapo kazi hii inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2022.

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kuwa na subira ili kutoa muda hadi mwishoni mwa mwezi Mei, 2022; kesi zote za muda mrefu zitakuwa zimeshughulikiwa.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kufuta Hati ya Umiliki wa Shamba la Mwekezaji katika Kijiji cha Mawalla - Kilolo ambalo limetelekezwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, shamba lililotelekezwa katika Kijiji cha Mawalla, ni shamba lenye Hati Na.16633 lenye ukubwa wa ekari 639 ambalo linamilikiwa na Ndugu Mbaraka Mazrui. Mmiliki wa shamba hili alitelekeza shamba tangu mwaka 1980. Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kwa kushirikiana na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa wa Iringa, imelitambua shamba hili kama shamba lililotelekezwa.

Mheshimiwa Spika, kufuatia hali hiyo, Serikali imeanza hatua za awali za ubatilishaji wa shamba husika na pindi hatua hizo zitakapokamilika, mapendekezo yatawasilishwa kwa mamlaka husika kwa ajili ya ubatilishaji.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha bei ya ardhi inayotwaliwa na Migodi ili iendane na thamani ya ardhi ya eneo husika?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya soko la ardhi huandaliwa kwa kuzingatia Kifungu Na. 70 cha Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini ya mwaka 2016 pamoja na Kanuni Na. 53 ya Kanuni za Uthamini na Usajili wa Wathamini za mwaka 2018. Kanuni hiyo imeelekeza bei ya soko la ardhi kuzingatia visababishi vinavyoathiri bei ya soko la ardhi kati ya eneo moja na jingine na namna ya kufanya tafiti kwa kukusanya taarifa za soko la ardhi katika maeneo mbalimbali. Aidha, Kifungu cha (2) cha Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999 kimetafsiri kuwa petroli na aina zote za madini yanayopatikana chini ya ardhi siyo sehemu ya ardhi bali ni mali ya umma na hivyo umiliki wa ardhi hutolewa tofauti na leseni ya uchimbaji wa madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa kuhuisha viwango vya thamani ya ardhi na mali ili viendane na wakati, viwango vya bei ya soko la ardhi vimeboreshwa kwa kuzingatia sheria na kanuni za ardhi. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI K.n.y. MHE. SUMA I. FYANDOMO aliuliza: -

Je, lini Serikali itapeleka Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi Wilaya ya Rungwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niamba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, taratibu za ajira zinaendelea kuchakatwa ili kupata Wenyeviti 57 watakaoweza kukamilisha uhitaji wa Wenyeviti 139 ambayo ni idadi ya Wilaya zote hapa nchini. Kwa sasa tuna Wenyeviti 82 tu ambao wanalazimika kuhudumia Wilaya zisizo na Mabaraza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Wilaya ya Rungwe inahudumiwa na Mwenyekiti kutoka Wilaya ya Kyela.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka alama za mipaka kutenganisha maeneo ya hifadhi na vijiji 975 vilivyotolewa kwenye Hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kuweka alama za mipaka kutenganisha maeneo ya Hifadhi na Vijiji 975 vilivyotolewa kwenye hifadhi imefanyika katika baadhi ya hifadhi na bado kazi hiyo inaendelea. Hifadhi zilizowekewa alama za mipaka mpaka sasa ni pamoja na eneo la kilomita za mraba 1,500 za Hifadhi ya Pori Tengefu Loliondo vigingi 422 vya alama vilishawekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Pori la Akiba la Wamimbiki alama 277 na kilomita 156 za mkuza zimetengenezwa. Hifadhi ya Pori la Akiba Swagaswaga alama 226 kati ya 250 na kilomita 27 za mkuza zimetengezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Pori la Akiba Mkungunero alama 99 kati ya 157 na kilomita 35.8 za mkuza zimetengenezwa. Hifadhi ya Taifa ya Ruaha alama 650 na kilomita 177 za mkuza zimeishatengenezwa pamoja na Bonde la Usangu, alama 632 zimewekwa kwenye eneo lenye urefu wa kilomita 316 kati ya 350 na mkuza wenye kilomita za mraba 177 umechongwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoani Tabora, alama za mipaka zimeshawekwa kwenye vijiji vitano vya Mwendakumila, Mwaharaja, Chemkeni, Uhindi na Nsimbo vya Wilaya ya Kaliua vilivyokua kwenye hifadhi ya Ulyankulu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa kwa kushirikiana na Taasisi zinazohusika na usimamizi wa hifadhi, kuendelea na utekelezaji wa uamuzi wa Baraza la Mawaziri ikiwemo kazi ya kuweka mipaka kwa kutumia alama za kudumu zinazoonekana ili kuimarisha ulinzi katika maeneo hayo, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa nyumba za Watumishi nchini hasa katika Halmashauri mpya?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Peter Cherehani, Mbunge wa Ushetu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2012 hadi 2014, Serikali kupitia Shirika la Nyumba la Taifa ilijenga nyumba za gharama nafuu 1,189 katika halmashauri 31 kwa ajili ya kuziuza kwa watumishi waliopo katika Halmashauri hizo. Aidha, kuanzia mwaka 2013 hadi sasa, jumla ya nyumba 983 zimejengwa na taasisi ya Watumishi Housing Company katika mikoa 19 na kuuzwa kwa watumishi wa umma na wanachama wa mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Serikali kupitia taasisi zake ikiwemo Shirika la Nyumba la Taifa na Watumishi Housing itaendelea kujenga nyumba bora kwa ajili ya watumishi wa umma ili kuwaongezea tija katika utendaji kazi.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga Mahakama katika Makao Makuu ya Tarafa za Nalasi, Lukumbule na Namasakata – Tunduru?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama inaendelea na utekelezaji wa Mpango wa ujenzi wa Mahakama hizi ambapo Mahakama ya Mwanzo ya Nalasi inajengwa katika mwaka huu wa fedha 2023/2024 ikiwa ni sehemu ya Mahakama za Mwanzo 71 zitakazojengwa nchi nzima. Tayari Mshauri Mwelekezi ameanza kufanya kazi, na mradi unatarajiwa kuanza Oktoba, 2023 na kukamilika kabla ya Juni, 2024. Mahakama za Mwanzo za Lukumbule na Namasakata zitaingizwa kwenye mpango ujao wa miaka mitano sambamba na tarafa nyinginezo nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika bajeti ya mwaka huu wa fedha moja ya Mahakama za Wilaya zitakazojengwa ni Wilaya ya Tunduru, ahsante.
MHE. STELLA S. FIYAO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa Hati kwa maeneo yote ya Umma katika Halmashauri za Mkoa wa Songwe?

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri tano za Mkoa wa Songwe, jumla ya maeneo ya umma 1,679 yanatumika kwa ajili ya matumizi mbalimbali kama vile Shule, Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali, Vyuo, Ofisi, Vituo vya Polisi, Mahakama, Maeneo ya Majeshi, Hifadhi za Misitu na Wanyama na Maeneo ya Makumbusho yanayotumiwa na Serikali au Taasisi. Aidha, maeneo 892 yameshapimwa ambapo kati ya hayo, maeneo 637 yameshakamilishwa na kutolewa Hatimilki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuongeza kasi ya umilikishaji wa maeneo ya matumizi ya umma, Serikali imefanya jitihada madhubuti ikiwemo kuondoa au kupunguza baadhi ya gharama za umilikishaji wa maeneo hayo. Hata hivyo, baadhi ya Taasisi za Serikali zikiwemo Halmashauri zetu zimeshindwa kutenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya umilikishwaji wa maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa viongozi wa Serikali na Wakuu wa Taasisi nchini wakiwemo viongozi wa Halmashauri za Mkoa wa Songwe kuhakikisha wanatenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya kugharamia upimaji na umilikishwaji wa maeneo yao, ahsante.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni ni kwa nini Serikali pindi inapotwaa maeneo ya wakulima isiwatengee maeneo mengine mbali ya kulipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI, alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingston Kaboyoka Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi, Sura 113 kifungu cha 3 Kifungu kidogo cha (1)(g), malipo ya fidia ni takwa la kisheria pindi Serikali inapotwaa ardhi kutoka kwa wananchi. Kimsingi, fidia kwa mujibu wa Sheria inajumuisha thamani ya ardhi na maendelezo yaliyopo juu ya ardhi. Fidia yaweza kulipwa kwa fedha au kupewa ardhi mbadala au vyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza fidia ya ardhi mbadala au fedha au vyote kwa pamoja kutokana na mazingira ya eneo la mradi, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI K.n.y. MHE ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza migogoro ya ardhi maeneo ya Chasimba, Chatembo, Chachui, Nkasangwe na Mabwepande – Kawe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Askofu Josephat Mathias Gwajima, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, migogoro ya ardhi katika Jimbo la Kawe kwa ujumla inahusu wananchi wa Chasimba, Chatembo na Chachui kuvamia eneo la Kiwanda cha Wazo, wananchi kuvamia mashamba ya wananchi wengine katika eneo la Nkasangwe na wananchi kufanya maendelezo katika mashamba yenye miliki likiwemo Shamba la Shirika la DDC katika eneo la Mabwepande.

Mheshimiwa Spika, kwa nyakati tofauti Serikali imekuwa ikishughulikia migogoro hii kwa kuwashawishi wamiliki wa maeneo yaliyovamiwa kuyaachia maeneo hayo ambapo wananchi tayari wameshavamia na kufanya maendelezo na wanapaswa kulipa fidia kwa wamiliki. Hata hivyo, pamoja na jitihada hizo za Serikali kutatua migogoro hiyo kiutawala, kumekuwa na mwitikio mdogo kwa wananchi kulipa fidia kwa maeneo waliyovamia na hivyo kuchelewesha upatikanaji wa suluhisho la kudumu la migogoro hii.
MHE. KAVEJURU E. FELIX aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe ili wananchi waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe ni moja kati ya miradi ya Mahakama inayotekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/2022. Kupitia programu ya maboresho ya Mahakama, Mkandarasi wa ujenzi wa Mahakama hii amepatikana ambaye ni Lucas Construction na kukabidhiwa eneo la ujenzi mwezi Oktoba, 2021. Kazi za ujenzi zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Julai, 2022.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: -

Je ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Momba na lini huduma za Mahakama za Mwanzo zitaanza kutolewa katika Tarafa ya Msangano?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA aliibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Momba ni moja ya Wilaya ambazo zimepewa kipaumbele kwenye Mpango wa ujenzi wa Mahakama katika mwaka wa fedha 2023/2024 ili kuhakikisha kuwa Mahakama inakuwa na majengo yake yenyewe na mazuri.

Mheshimiwa Spika, vilevile, ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo ya Tarafa ya Msangano umepangwa kufanyika katika mwaka wa fedha 2022/2023 ikiwa ni pamoja na kufanya maandalizi ya mahitaji kama watumishi ili huduma zitolewe mara baada ya ujenzi kukamilika.
MHE. JUDITH S. KAPINGA aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kuchapisha sheria za Tanzania katika nakala ngumu na nakala laini ili kurahisisha upatikanaji wa sheria hizo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Judith Salvio Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mara tu baada ya Miswada ya Sheria inaposainiwa na Mheshimiwa Rais kuwa Sheria, Serikali imekuwa ikihakikisha nakala laini zinapatikana kwenye tovuti za Wizara na taasisi zake. Vilevile Bunge na Mahakama wamekuwa wakiweka sheria zote ambazo zimetungwa kwenye tovuti zake ili kurahisisha upatikanaji wake. Aidha, Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali amepewa jukumu la kuchapisha na kuuza nakala ngumu za sheria ili wananchi waweze kupata nakala sahihi na kwa urahisi.
MHE. KAVEJURU E. FELIX aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe ili wananchi waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Buhigwe ni moja kati ya miradi ya Mahakama inayotekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/2022. Kupitia programu ya maboresho ya Mahakama, Mkandarasi wa ujenzi wa Mahakama hii amepatikana ambaye ni Lucas Construction na kukabidhiwa eneo la ujenzi mwezi Oktoba, 2021. Kazi za ujenzi zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Julai, 2022.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya Uvinza?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Kigoma Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Uvinza ni moja ya miradi ya Mahakama inayotekelezwa katika kipingi mwaka wa fedha 2021/2022 kupitia programu ya maboresho ya Mahakama. Mkandarasi wa ujenzi wa Mahakama hii amepatikana ambaye ni Lucas Construction na kukabidhiwa eneo la ujenzi mwezi Oktoba, 2021. Kazi za ujenzi zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Julai, 2022.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza:-

Je, lini Serikali itamaliza mgogoro wa ardhi kati ya mwekezaji wa Shamba la Malonje na wananchi wa Kata ya Muungano na Mollo Kwela?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dues Clement Sangu, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shamba la Malonje linalojulikana kama Shamba Namba 48/1 Malonje katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga na Manispaa ya Sumbawanga lenye ukubwa wa hekta 10,002 liliuzwa na Serikali kwa mwekezaji ambaye pia ni Bodi ya Wadhamini wa Efatha Ministry. Mgogoro wa ardhi katika shamba hili unasababishwa na baadhi ya wananchi kutoka katika vijiji vya Msanda Muungano, Sikaungu na Songambele Azimio katika maeneo ya shamba hili yaliyo ndani ya mipaka kutwaliwa kinyume cha utaratibu.

Mheshimiwa Spika, katika kushughulikia suala hili, Serikali iliwasilisha maombi kwa mwekezaji kumega sehemu ya shamba ili igawiwe kwa wananchi na vijiji vinavyozunguka shamba hilo kwa ajili ya shughuli za kilimo. Pamoja na mwekezaji kuridhia kumega sehemu ya shamba lenye ukubwa wa ekari 3,000 ili angalau kila kijiji kipate ekari 1,000 bado wananchi wameendelea kuvamia shamba la mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa uongozi wa Mkoa na Wilaya kusimamia upangaji na ugawaji wa ardhi iliyotolewa na mwekezaji kwa vijiji hivyo ili kuondoa mgogoro uliopo. Aidha, uongozi wa Mkoa na Wilaya uwaelimishe wananchi juu ya kuheshimu mipaka ya ardhi ya mwekezaji kwa kuwa anamiliki eneo hilo kisheria.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI aliuliza: -

Je, lini Serikali itarejesha eneo lililokuwa linamilikiwa na RUBADA kwa wananchi wa Utengule – Mlimba?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shamba Namba 949 linalojulikana kwa jina la Ngalimila lina ukubwa wa hekta 5,128.483 (sawa na ekari 12,820). Shamba hili lipo Mkoa wa Morogoro katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba katika Kata ya Utengule. Shamba hili limezungukwa na Vijiji vya Ngalimila, Ipugasa, Ngombo, Mpanga, Miembeni na Viwanja Sitini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya mwaka 2009 ardhi hii ilikuwa inamilikiwa na Kijiji cha Ngalimila ambapo tarehe 18 Mei, 2009 kilifanyika kikao maalum kwa ajili ya kujadili maombi ya ardhi kwa ajili ya RUBADA kutoka kijiji cha Ngalimila kwa ajili ya uwekezaji. Wanakijiji walikubali kutoa ardhi hiyo kutokana na manufaa ambayo walielezwa yangepatika na kutokana na uwekezaji mkubwa katika kilimo cha mpunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 16 Aprili, 2014 iliandaliwa taarifa ya kusudio la kuhaulisha ardhi ya kijiji kuwa ya kawaida. Baada ya RUBADA kufutwa, mali mbalimbali ikiwemo shamba la Ngalimila zilirejeshwa Wizara ya Fedha na Mipango na kuwa chini usimamizi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia ardhi ya shamba hili kutoendelezwa kwa muda mrefu, Serikali ilipokea maombi ya wananchi kurejeshewa shamba hili. Hata hivyo, uchambuzi wa maombi hayo ulibaini kuwa eneo lenye ukubwa wa hekta 1,820.494 sawa na asilimia 35 ya shamba hilo lipo katika eneo la Pori Tengefu la Kilombero. Aidha, ili kufika katika shamba hili, sharti kuvuka Mto Mpanga na Mto Mnyera ambayo ndiyo chanzo cha kupeleka maji katika mradi wa ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme wa maji wa Julius Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa wananchi wanaotumia shamba hili kwa sasa ambao ni wavamizi kutokuweka miundombinu ya kudumu ili kuepusha hasara inayoweza kujitokeza endapo Serikali itatoa maamuzi tofauti na maombi yao. Aidha, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa suala hili litashughulikiwa na kutolewa maamuzi kwa uharaka unaohitajika kwa maslahi mapana ya jamii na Taifa kwa ujumla, ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza:-

Je, lini Serikali itafanya maboresho ya Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, rasimu ya Sera ya Taifa ya mwaka 1995, Toleo la 2023 liliwasilishwa na kujadiliwa katika Mkutano wa Baraza la Mawaziri, tarehe 18 Agosti, 2023. Aidha, Wizara imekamirisha maboresho ya rasimu ya sera kwa kuzingatia maoni ya Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, hatua inayofuata ni rasimu hiyo ya sera kujadiliwa katika Mkutano wa Kazi wa Baraza la Mawaziri kwa tarehe itakayopangwa, ahsante.