Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Soud Mohammed Jumah (22 total)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Ahsante sana Mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu kwamba mifuko hii ya Adaptation Fund pamoja ile ya LDCF yaani Least Developed Country Fund hutengewa fedha maalum na Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi kupitia hii mifuko na fedha hizi hutakiwa zitumike katika muda maalum na ni fungu maalum, na kutokana na utaratibu ambao unaendelea katika Serikali au katika Wizara zetu imekuwa ikichukua muda mrefu sana kutayarisha maandiko na kuweza kuyawasilisha na mpaka kupata hizi fedha.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba, fedha hizi ambazo zinakuwa zinatengwa kwa ajili ya Tanzania zinaombwa kwa haraka na kuweza kupatikana katika muda muafaka ili kupunguza hatari ya kuweza kuja kuzikosa hizi fedha au kuzipoteza?

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, je, kuna utaratibu gani wa uwiano wa fedha hizi kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS,
MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, kumekuwa na, kwa namna moja au nyingine ucheleweshaji wa fedha hizi, lakini tunaendelea kuimarisha utaratibu wa mawasiliano. Fedha hizi kwanza lazima mradi uandikwe, lakini vilevile tunashiriki na wenzetu wa Wizara ya Fedha ambao wana taratibu zao, tunahitaji tax exemption katika jambo hili. Kwa hiyo, lazima wataalam wetu wapitie kwanza halafu kisha wamshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha namna bora ya kuweza kuruhusu mradi uweze kuendelea. Wakati mwingine unalazimika kwenda site, hiyo ndio inasababisha muda unakuwa mrefu kidogo, lakini tunaahidi mbele ya Bunge lako tukufu kwamba tutachukua hatua za haraka na miradi hii itakuwa haichukui muda mwingi sana kutekelezwa, ili tuweze kupata fedha hizo ambazo ni manufaa makubwa kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili ambacho Mheshimiwa Mbunge anataka kujua ni kwamba kuna uwiano. Hii miradi kama nilivyotaja katika miradi mitano mradi ukiibuliwa kule upande wa Zanzibar kiasi hicho cha fedha mradi utatekelezwa fedha zinapelekwa bila kuwa na mgawo, kwa hiyo, hapa kazi kubwa ni kujiimarisha, kuandaa watu wetu, wataalam wetu, waandae maandiko ya kutosha fedha zinapatikana. Sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais ni ku- facilitate na kuratibu mambo haya yaweze kufanyika kwa haraka zaidi. Ahsante sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kama unavyokumbuka kwamba mifuko hii imeweza kuchangia maendeleo makubwa katika masuala ya uhifadhi, hususan kupunguza wimbi la ujangili nchini pamoja na kuongeza wigo wa masuala mazima ya miradi ya wanajamii, halikadhalika kuingiza vivutio ambavyo vimetupelekea kufikia lengo la watalii 1,300,000: Je, kutokana na mabadiliko ya sheria hii, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba mabadiliko haya hayaendi kudumaza maendeleo ambayo yamefikiwa katika matumizi ya mifuko inayoathirika kutokana na sheria hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama tunavyofahamu, mwezi wa Pili mwaka huu Mheshimiwa Waziri Mkuu alifungua maonyesho ya mifuko pale Arusha na alitoa wito wa kwamba mifuko hii iweze kuendelezwa ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Je, tuna mpango gani mbadala wa kuisaidia mifuko hii ili pamoja na mabadiliko haya ya sheria ambayo yamefanyika kuhakikisha kwamba yanakwenda kusaidia mafanikio ambayo yamepatikana hasa tukilinganisha kwamba hivi sasa wenzetu wa CMA wameanza kulalamika kutokana na matatizo ya...?

SPIKA: Ahsante sana. Umeshaeleweka Mheshimiwa.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. kwanza nashukuru kwa swali la Mheshimiwa Soud, lakini nimtoe wasiwasi kwamba Serikali iliona suala hili baada ya mifuko hii fedha zake zilizokuwa zinakusanywa kupelekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina, Serikali ilianza kutekeleza majukumu yake yaliyokuwa yanatekelezwa kwenye mfuko huu kupitia bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi kwamba shughuli sasa ambazo zilikuwa zinatekelezwa na mfuko huu ikiwemo uhifadhi, kudhibiti ujangili na shughuli nyingine za kuendeleza utalii, kukuza na kutangaza utalii, Shughuli zote hizi sasa zinatekelezwa na bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Kwa mwaka wa fedha 2021/2022 shughuli zote zilizokuwa zinatekelezwa kwenye mifuko hii, sasa zimeingizwa kwenye bajeti kuu ya Serikali. Naomba kuwasilisha.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ningeomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa vile tokea mwaka 2012 hadi leo hii ni miaka tisa imepita na idadi ya askari polisi imeendelea kupungua kutokana na askari wengi kustaafu katika maeneo ya Zanzibar.

Vilevile kuongeza kwa vitendo vya uhalifu katika baadhi ya maeneo, je, Mheshimiwa Waziri au Serikali haioni haja ya kuajiri askari zaidi katika maeneo ya Zanzibar na hasa mashambani ili kuweza kuziba hilo pengo kwa haraka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, kwa vile askari jamii katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar, wamekuwa ni msaada mkubwa na tayari kuna good practices katika baadhi ya maeneo. Je, Serikali haioni haja ya kuweza kupanua wigo wa askari jamii kwa kuwapatia mafunzo na motisha, ili kuweza kufanya kazi na kuweza kusaidia kupunguza vitendo vya uhalifu katika maeneo ya Zanzibar? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ili tuweze kufanya uajiri kuna mambo lazima tuyaangalie. La kwanza, lazima tuhakikishe kwamba, tumepata kibali cha kufanya uajiri kitu ambacho nataka nimuambie Mheshimiwa Mbunge, tumeshakifanya na tumo mbioni kuhakikisha kwamba, tunapata ruhusa ya kufanya uajiri.

Mheshimiwa Spika, lingine ili tuweze kufanya uajiri maana yake lazima tuhakikishe kwamba tuna bajeti ya kutosha kwasababu tukisha waajiri lazima tuwalipe. Sasa kikubwa ambacho nataka nitoe wito hapa leo kwa Waheshimiwa Wabunge, hasa Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali na Waheshimiwa Wabunge leo tukijaaliwa hapa tunaenda kupitisha bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, tunaomba bajeti hii tuipitishe kwasababu, ndani ya bajeti hii imezungumzwa taarifa za ajira za vijana hasa kwenye jeshi la polisi. Kwa hiyo, nawaomba tupitishe hii bajeti ili sasa tuweze kufanya hizo harakati za uajiri.

Mheshimiwa Spika, nimeulizwa pia suala kuhusu namna bora ya kuweza kuwaboresha askari jamii. Nimuambie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyozungumza tayari Kamishna anayeshughulika na masuala ya askari jamii na ulinzi shirikishi Zanzibar kwanza, anachokifanya ni kutoa mafunzo kwa masheha na kamati za ulinzi na usalama za shehia na vijiji, ili lengo na madhumuni ni kuona namna bora ya kuweza kuwashirikisha wananchi katika kupata ulinzi. Lakini tayari kuna mfumo mzuri, mwongozo mzuri ambao umeshatolewa umeshaanza kutumika Unguja na Pemba soon inshalah utaanza kutumika. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu yasiyoridhisha ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mpango gani wa kuhakikisha kwamba, malalamiko haya ambayo yamedumu kwa kipindi kirefu sasa yanafikia mwisho?

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akaji-committ ni lini atakutana na wadau wa biashara ya dagaa wanaosafirisha kutoka Zanzibar kwenda Tunduma, ili kuhakikisha kwamba, anazungumza nao kuhusu hizi kadhia na kuzimaliza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, lini yatafika mwisho malalamiko haya ya wafanyabiashara wa dagaa. Nataka nimhakikishie kwamba, tumeweka utaratibu mzuri wa kufunga lakiri. Dagaa wanaotoka Zanzibar kupita katika Bandari ya Dar –es - Salaam wanapita katika utaratibu wa magunia yaliyo wazi. Tumeweka utaratibu ndani ya Serikali kwamba, wanapifika katika Bandari ya Dar - es - Salaam ni lazima tuyafunge lakiri ili kuthibitisha kama huu mzigo tayari ulishalipiwa ushuru kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, nakiri yawezekana wako watumishi, baadhi, wasio waaminifu wanaoleta vitendo visivyokuwa vya kiungwana. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wafanyabiashara wote, tutashughulikia jambo hilo hatua kwa hatua na vyombo vyetu vya dola vitakuwa vikifuatilia ili hao watumishi watakaokuwa wanabainika kufanya vitendo visivyokuwa vya kinidhamu tuwachukulie hatua na kuwarahisishia wafanyabiashara wetu kazi yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu lini nitakwenda kukutana na wadau wetu. Nataka nimhakikishie kwamba, mara baada ya Bunge la Bajeti, ikimpendeza yeye na Wabunge wengine wanaoguswa na jambo hili niko tayari kuandaa mkutano huo kwa ajili ya kukamilisha zoezi hili. Ahsante.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kuna taasisi tatu hapa nchini za NEMC, Wizara ya fedha pamoja na TAMISEMI, zimeanza mchakato karibu miaka sita mapaka kumi iliyopita, na mpaka leo hazijaweza kukamilisha utaratibu wa kuweza accredited.

Je, Wizara au Ofisi Makamo wa Rais Mazingira, ina mpango gani wa kuweza kuzihamasisha na kuzijengea uwezo taasisi hizi ziweze kukamilisha mchakato huu na kuweza kufaidika na fedha hizi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa vile Zanzibar hakuna taasisi hata moja ambayo imeanza mchakato huu. Je, kuna utaratibu gani au mikakati gani ambayo imepangwa na Ofisi ya Makamo wa Rais Mazingira, kuweza kuzijengea uwezo taasisi za Zanzibar na kuzihamasisha ziweze kuanzisha mchakato wa kujiunga na mfuko huu wa taibanchi. Ahsant sana. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS
(MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali na Mhesimiwa Soud Mohammed Jumah kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa mwenyekiti, ni kweli katika hizi fedha za mifuko hii miwili ya Adaptation na Green fund, hizi mara nyingi sana tushindwa kuzi – access kwa muda mrefu, hata hivyo Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira, imeweza kuhakikisha kwamba katika kipindi cha hivi karibuni imejitahidi kufanya kazi yake kubwa vya kutosha, na tushukuru sasa hivi, kwa mfano, NEMC imefanikiwa kupata fedha kutoka mfuko wa Adaptation Funds, ambao ni wastani wa shilingi billion 6 ambazo hizi tupo katika mchakato na Wizara ya fedha kuweza kuzi – access vizuri ili ziweze kufanyakazi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tunaendelea kuzijengea uwezo taasisi hizo. Tunafahamu kwamba TAMISEMI walianza mchakato takriban miaka mitatu, na bado kuna suala la capacity tunaendelea kulifanyia kazi. Kwa upande huu wa Zanzibar, juzi tulikuwa na ziara kule Zanzibar (Unguja na Pemba) na jana tulimaliza. Miongoni mwa jambo kubwa sana tulokubaliana nalo ni suala zima la kuangalia jinsi gani tutafanya kazi kwa pamoja katika upande wa kimazingira, kwa sababu jambo la mazingira linakata maeneo yote mawili.

Mheshimiwa mwenyekiti, hili naomba nikuhakikishie Mheshimiwa mbunge, mimi na dada yangu kule Mheshimiwa Saada Mkuya, ambae anahusiana na upande wa Mazingira kwa upande wa Zanzibar, tutafanya kila liwezekanalo kwa umoja wetu. Na hivi sasa Mkurugenzi wetu wa Mazingira anaitwa Dkt. Andrew Komba hivi muda huu ninayozungumza yuko Zanzibar akifanya kikao na wakuu wa Mikoa kule Pemba, katika ajenda kubwa ya kuangalia jinsi gani tutafanya ajenda ya pamoja ya mazingira ndani ya nchi yetu.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wizi wa mazao ya kilimo na mifugo yamekuwa yakiongezeka pamoja na takwimu nzuri ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri amezieleza hapa. Je, ningependa Mheshimiwa Naibu Waziri alieleze Bunge lako Tukufu tuna-fail wapi?

Swali Namba Mbili, ningeomba vilevile kuuliza kwa sababu kinga ni bora kuliko tiba. Je, hatuoni kwamba kuna haja ya kukinga haya matokeo ya wizi yasitokee ili kuwasaidia wananchi na wakulima wasiweze kupata hasara ya kuibiwa mazao yao. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mbunge wa wananchi wa Jimbo la Donge, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi wajibu wetu mkubwa ni kulinda raia na mali zao. Kwa hiyo katika hili tunajitahidi na tunafika hatua tunakuwa tunakutana na changamoto nyingi zikiwemo zile za wananchi wenyewe kwanza kushindwa kwenda kutoa ushahidi kwamba nani ameiba na nani amechukua mazao na nani amechukua mifugo. Lakini kikubwa ni kwamba tunaendeleza jitihada za kuhakikisha kwamba tunawakamata tunawafikisha kunako vyombo vya sheria hawa wanaohusika.

Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali katika kuzuia haya, tuna mikakati mingi ambayo kama atarejea kwenye jibu langu la msingi moja ni kuendeleza ule ushirikishwaji wa wananchi katika ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ambalo pia tumelifanya kama ni sehemu ya mkakati ni kufanya doria za mara kwa mara katika maeneo haya hasa yale maeneo ya Zanzibar maeneo ya Donge, Muwanda na maeneo mengine ili lengo na madhumuni hivi vituko ama hivi vitendo vya uhalifu visiweze kutokea. Lakini kubwa nataka nitoe wito kwa wananchi wetu wasiendelee kuchukua hatua mikononi mwao, tumepata matukio mengi ya watu wanachinjwa, watu wanachomwa, watu wanachukuliwa hatua mikononi kitu ambacho ni kinyume na utaratibu wa sheria. Ninakushukuru. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na yenye matumaini mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile mchakato wa wenzetu hawa NEMC kujiunga na Mfuko wa Fedha wa Green Climate Fund umechukua muda mrefu kuliko ilivyotaratijiwa; na kwa kuwa sehemu ya mchakato huo ilishafanyika wakati NEMC wanajisajili katika Mfuko wa Adaptation Fund.

Je, NEMC wamejipanga vipi kuweza kuainisha vipaumbele vya miradi kwa kuzingatia maeneo ya kijiografia, Zanzibar na Tanzania Bara ili wakishapata usajili wasije tena kuchelewa kuwasilisha andiko la mradi kwenye sera hizi ambazo nchi mbalimbali zinaomba na hazijatengwa kwa ajili ya Tanzania peke yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa tunaenda kupata taasisi ya pili sasa kwa upande wa Tanzania Bara ambayo imepata accreditation kwa upande wa Mfuko wa Fedha wa Green Climate Fund: Je, Ofisi ya Makamu wa Rais imejipanga vipi kuisaidia Zanzibar angalau kuweza kupata taasisi moja ambayo itapata usajili kwa ajili ya Mfuko huu wa Mabadiliko ya Tabianchi ili Wazanzibar nao wawe na direct access ya kuomba hizi fedha za mabadiliko ya tabianchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Soud maswali yake ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Soud kwa kazi nzuri anayoifanya hasa ya kutoa elimu kwa wananchi katika masuala mazima ya uhifadhi wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo maeneo ambayo tumeshayaainisha au tunayafanya kabla hatujaanza kufanya uteuzi wa hiyo miradi. Kwanza huwa tunatembelea maeneo ambayo tunaweza tukaiibua hiyo miradi ambayo tunaweza kuiingiza huko. Kingine tunachokifanya ni kukusanya taarifa ambazo zinaweza kusaidia na baadaye tunaenda kuziandikia project proposal.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyokuwepo hapo ni kwamba mara nyingi miradi hii inakuwa inasuasua. Kwa hiyo, nataka nichukue fursa hii nitoe wito kwa Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini, wajitahidi wasimamie vizuri miradi hii, kwa sababu kuna baadhi ya maeneo fedha zimepelekwa, lakini bado miradi hii inasuasua haijamalizika utekelezaji wake wakati bado kuna baadhi ya maeneo miradi hii imeshakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuisaidia Zanzibar kupata angalau taasisi; Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira ipo wazi, kikubwa ni kwamba tunawaomba waje, tutawaelekeza, tutawafahamisha, tutawaambia namna ambavyo tunaweza tukawasaidia wakaingiza hizo taasisi. Kikubwa ni kwamba wanaweza wakaandaa pia miradi ili wakija kwetu inakuwa rahisi kuifanyia utekelezaji. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa Herbarium ya TPRI, Arusha ni kituo muhimu cha uhifadhi na utafiti: Je, Serikali ina mpango gani wa kuweza kuajiri na kuzalisha wataalam zaidi ili kuweza kukusanya data nchi nzima badala ya ku-concentrate na mikoa miwili tu hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili: Kwa kuwa wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, hususan misitu, wana utaalamu mkubwa wa usimamizi wa Herberium: Kwa nini tusiangalie uwezekano wa kuhamisha usimamizi wa hii National Herbarium kuipeleka maliasili au angalau kuwa-engage watu wa Maliasili wakasaidiana ili kuboresha au kuongeza wigo wa uhifadhi, utafiti na utalii katika herbarium zetu? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, la kuhusu kuajiri, kwa sababu, nimezungumza pale awali kwenye majibu yangu ya msingi kwamba hii tayari imeshahamia ndani ya Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu, ambayo tumeanza kupitia pia muundo wake na hivi sasa tunahakikisha kwamba tunawapatia nafasi pia kuweza kuajiri wataalamu zaidi kwa sababu muundo huu tunaupitia. Kwa hiyo, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba na hilo pia litakuwa ni sehemu kati ya priorities kuhakikisha kwamba, tunakuwa na wataalamu wa kutosha katika eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuhusu kuhamisha, jambo hili lipo kisheria na hivyo linahitaji marekebisho ya sheria, lakini tumepokea kama Serikali hoja ya Mheshimiwa Mbunge. Nakushukuru sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa nchi yetu Tanzania hivi sasa inakabiliwa na wimbi kubwa la ukataji na uchomaji moto wa misitu ya asili. Je, Wizara ina mkakati gani wa ufuatiliaji kuona mpango huu wa AFR 100 unakwenda kufanikiwa ili kukabiliana na tatizo la uharibifu wa misitu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa utekelezaji wa lengo la mpango huu linajumuisha nchi nzima pamoja na Zanzibar. Naomba tu kujua tumeishirikishaje Zanzibar ili kuona mpango huu tunautekeleza kinchi zaidi ili kuweza kukabiliana na tatizo la uharibu wa misitu kule Zanzibar? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mohammed Jummah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa mhifadhi mzuri kwenye masuala haya ya misitu kwa sababu kwa asilimia kubwa amekuwa anatoa mchango mzuri sana kwenye eneo hili la uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mikakati mingi na mikakati hii tayari ilishaanza kutekelezwa tangu mwaka 2018 ambapo Serikali iliingia mkataba na dunia. Mkakati huu ni wa kidunia lakini kwa Afrika tumeelekezwa kutekeleza jumla ya hekta milioni 100 kuziongoa ili ziingie kwenye uhifadhi. Tanzania ni moja ya nchi ambazo zimeingizwa katika mkakati huo ambapo jumla ya hekta milioni 5.2 tumeziwekea mkakati huo na malengo yetu ni kuhakikisha tunaziongoa.

Mheshimiwa Spika, mikakati hii imeendana sambamba na zoezi la uongoaji na urejeshaji wa maeneo ya hifadhi. Hivi karibuni utashuhudia ziara ya Mawaziri Nane wamekuwa wakitembea kila mikoa kuhakikisha kwamba maeneo yale ambayo yanastahili kurejeshwa, yarejeshwe ili tuweze kuingia kwenye mpango huu wa kidunia ambao tunaongoa jumla ya hekta milioni 350.

Mheshimiwa Spika, swali lake lingine ambalo ameuliza, je, Zanzibar ni miongoni mwa nchi ambazo ziko ndani ya mkakati huu. Zanzibar ni kweli ipo na kwa kuwa Zanzibar ni sehemu ya Muungano zoezi hili linafanyika kama Tanzania Bara na Zanzibar hivi karibuni kuna Mradi wa FAO ambao umeunganisha Zanzibar na Kigoma na tayari wanatekeleza katika maeneo mbalimbali ikiwemo kurudisha maeneo ya hifadhi ili kurejesha uoto wa asili.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba moja; kwa kuwa tayari kuna jitihada ambazo zilishafanyika toka mwaka 2014 za kuanzisha mfumo wa fedha wa mabdiliko ya tabianchi (Tanzania Climate Financing Mechanism), pamoja na tafiti nyingi pia zilifanyika, ili kuanzisha mfuko wa mabadiliko ya tabia ya nchi.

Je, kwa nini Serikali haioni haja ya kutumia taarifa na tafiti mbalimbali ambazo zilifanyika huko kabla ili kuweza kuharakisha utaratibu huu wa kuanzisha mfuko wa mabadiliko ya tabianchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba mbili; kama ninavyokumbuka kwamba dunia inalichukulia suala la mabadiliko ya tabianchi ni janga kubwa kuliko athari nyingine za kimazingira;

Je kwa nini Serikali haioni haja ya kutengeneza mfuko wa mabadiliko ya tabia ya nchi unaojitegemea ili kuweza kuchochea ufadhili na kuweza kuhamasisha wafadhili na wahisani kuweza kuchangia mfuko wa mabadiliko ya tabianchi sambamba na zile jitihada za Serikali kuweza kuji- commit fedha zaidi katika huu mfuko? Ahsnate sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Jimbo la Donge, maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo alilolishauri Mheshimiwa Mbunge, tayari ni jambo ambalo tumeshaanza kulifanyia kazi. Hivi ninavyokwambia tumeshaanza mchakato wa mapitio ya Sheria hii ya Mazingira ambayo imo katika Sura ya 191. Tumeanza mchakato huu lengo na madhumuni ili kuona, kwanza namna gani mfuko huu utaundwa, lakini vipi unaweza ukapokea fedha, namna utakavyozitoa hizo fecha, ni fursa na faida gani na ni athari zipi ambazo zinanweza zikapatiwa msaada ama zikasaidiwa kupitia mfuko huu, baada ya mfuko huu kwa sasa unaanza kutoa hizo. Kwa hiyo kikubwa nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato umeanza na muda wowote unaweza ukakamilika na hiyo hali ikaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge, kwamba lengo na adhma ya Serikali katika kuunda mfuko huu kwanza ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unajitegemea, lakini la pili ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unapata fedha ya kutosha, tatu ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unapata misaada kutoka kwa wafadhili mbalimbali, ili lengo na madhumuni mfuko huu uweze kusaidia wananchi katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na utunzaji na uhifadhi wa mazingira. Hivyo nimwambie tu Mhehsimiwa Mbunge kuwa adhma ya Serikali inaendanana na mawazo yake.

Mheshimiwa Mwenyekti, nakushukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa wananchi wa Jimbo la Donge wanatembea masafa marefu kufuata huduma za kipolisi katika Vituo vya Polisi vya Mkokotoni na Kituo cha Polisi cha Mahonda na kwa kuwa uhalifu na halikadhalika idadi ya watu wameongezeka katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Donge. Je, Serikali haioni haja ya kufanya kazi na wananchi wa Jimbo la Donge kuweza kujenga kituo katika maeneo hayo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Kituo cha Polisi cha Mahonda ni kituo kikongwe toka kipindi cha ukoloni na kituo hiki hakijafanyiwa ukarabati mkubwa kwa kipindi kirefu. Je, Serikali ina mpango gani wa kukifanyia marekebisho makubwa Kituo cha Polisi cha Mahonda pamoja na nyumba za wafanyakazi ili kuweza kukidhi kupambana na masuala ya uhalifu ambayo yanaongezeka siku hadi siku? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu umuhimu wa kujenga Kituo cha Polisi eneo la Donge ambalo ametaja vigezo vitatu vya masafa marefu lakini kuwepo kwa uhalifu, kujenga kituo pale tutawasiliana na Kamisheni ya Polisi Zanzibar wafanye utafiti kuona umuhimu wa kujenga pale ili iweze kuingizwa kwenye bajeti hatimaye ujenzi uweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la kuchakaa kwa Kituo cha Polisi Mahonda, namwomba Mheshimiwa Mbunge, tutaituma Polisi Kamisheni Zanzibar kwa kauli yangu niombe Polisi Zanzibar wafanye uthamini wa Kituo cha Polisi Mahonda kwa madhumuni ya kubaini mahitaji ili tuweze kuingiza kwenye mpango wa ukarabati. Nashukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Katika Jimbo langu la Donge kuna majengo ambayo yamejengwa zaidi ya miaka 20 iliyopita na wenzetu hawa wa Posta na Simu. Majengo yale mpaka leo hayakutumika na yanaendelea kuzeeka na kuchakaa hivi sasa. Sasa namwomba tu Mheshimiwa Waziri kama yuko tayari aidha tufuatane na kumwomba awaachie wananchi wa Jimbo la Donge watumie yale majengo kwa shughuli zingine za maendeleo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Soud, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirika la Posta Tanzania majengo yake mengi ni ya siku nyingi, lakini mpango wa uliopo ndani ya shirika letu ni kuhakikisha kwamba tunaboresha vituo vyetu vya mikoani. Kwa majengo yetu yaliyoko katika upande wa wilaya baada ya kukamilisha awamu ya kwanza ambayo ni mikoa baadaye tutashuka mpaka kwenye wilaya na hatimaye majengo yote yataanza kufanya kazi iliyotajiwa na Watanzania. Ahsante.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini pamoja na kwamba takwimu haziko vema na ningeomba Mheshimiwa Naibu Waziri apate muda akajiridhishe na hizo data au takwimu zilivyochukuliwa, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa magari ya mchanga yanasababisha sana ajali za daladala pamoja na ajali za bodaboda hasa katika maeneo ya Kaskazini A Kule Nungwi na maeneo ya Donge kwa ujumla wake. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mpango gani wa kukaa na Wizara za Mawasiliano pamoja na Wizara husika kule Zanzibar ili kuweza kutatua tatizo hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa tatizo la magari ya mchanga kwenda mwendo wa kasi ni tatizo sugu hivi sasa. Je, Mheshimiwa Naibu Naibu Waziri haoni haja ya kukaa na taasisi inayoshughulikia masuala ya usafirishaji wa mchanga pamoja na maliasili isiyorejesheka ili kukaa na kuratibu utaratibu mzima wa leseni pamoja na utaratibu wa kusafirisha hizi rasilimali za mazao yasiyorejesheka? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza takwimu hizi nimeletewa na Kamisheni ya Polisi Zanzibar, kwa hiyo nina Imani zimetoka kwenye mamlaka sahihi. Hata hivyo, kwa vile amesema tujiridhishe, mimi na yeye tutashirikiana kuzifuatilia, kama ana source nyingine yenye takwimu tofauti na hizi tutasaidiana kuona ni zipi ni sahihi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu magari haya kusababisha ajali kwa wingi kama alivyoeleza, kwa takwimu zetu kunaonekana kuna dalili ya kupungua. Hata hivyo, nieleze hata kama gari inabeba mzigo au ni mfanyabiashara na nini, anapoingia barabarani lazima azingatie Masharti ya matumizi ya barabara na kwa maana ya Sheria ya Usalama Barabarani inamhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu magari haya kusababisha ajali kwa wingi kama alivyoeleza, kwa takwimu zetu inaonekana kuna dalili ya kupungua, lakini nieleze hata kama gari inabeba mzigo ama ni mfanyabishara na kadhalika, anapoingia barabarani lazima azingatie masharti ya matumizi ya barabara na kwa maana Sheria ya barabarani inamhusu. Kwa hiyo, kwa hawa wanaobeba mchanga ninashauri nchi nzima siyo tu lile eneo la Mheshimiwa Soud alilolieleza kwamba, kwanza inatakiwa ule mchanga ufunikwe ili usitoe vumbi wanapokuwa wanaendesha yale magari. Pili wahakikishe magari yale ni mazima yanapoingia barabarani na madereva kwa kweli wawe sober enough wasiwe wamekula vilevi wakasababisha ajali kwa watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, tutaendelea kufuatilia kwa ukaribu na kupitia Bunge lako Tukufu nimwelekeze IGP kupia Kamisheni ya Polisi Zanzibar waimarishe usimamizi wa eneo hili lililobainishwa na Mbunge, eneo la Nungwi na maeneo ya jirani ili kukomesha kabisa ajari za namna hiyo. Nashukuru. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, ili kuzifanya juhudi hizi ambazo Mheshimiwa Waziri amezieleza hapa kuwa endelevu, Je, hatuoni haja ya kuja na mkakati wa pamoja ambao utazishirikisha sekta za maliasili, kilimo, mifugo pamoja na sekta ya maji ili kulimaliza kabisa tatizo hili ambalo ni la muda mrefu?

Swali la pili, kwa kuwa kuna good practices kwa wenzetu Uganda ambao wanawashurutisha wafugaji wenye mifugo wengi kutenga maeneo ya malisho toshelezi kwa ajili ya mifugo yao. Je, Serikali haioni haja ya kuiga mfano huu mzuri ili kuweza kupambana na changamoto hii ambayo inaleta migogoro kati ya wakulima, watu wa maliasili pamoja na mifugo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza ni kwamba mkakati upo wa Wizara zote ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na Wizara ya Maji, tukiungana na watu wa Wizara ya Ardhi, kuandaa mipango endelevu kwa ajili ya kusiadia wafugaji wetu ili kuondoa hii migogoro ambayo imejitokeza. Kwa hiyo, jambo hilo lipo Mheshimiwa Mbunge, na tutaendelea kuliboresha zaidi ili tuondoe hii dhana ambayo imekuwa ikijengeka kila wakati ya migogoro inayotokana na wafugaji pamoja na wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kutenga maeneo, hilo tayari ni agizo ambalo Serikali ilishalitoa katika Halmashauri zote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya wafugaji, hususan wale wenye mifugo wengi ili kuondoa hii kuhamahama kutafuta malisho pamoja na maji. Utaratibu huu kwanza utaboresha mifugo wetu wa kisasa na kuongeza ubora wa malisho na mifugo ambao tunao. Ahsante sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Hifadhi za Taifa, Hifadhi za Misitu pamoja na Mapori ya Akiba, tumeanzisha kwa ajili ya kuhifadhi uoto wa asili na kulinda viumbe hai pamoja na wale ambao wako hatarini kutoweka. Hali kadhalika kwa kuwa hivi karibuni maeneo mengi ya hifadhi na mapori ya akiba, aidha tumeyamega ya kuyateremsha hadhi baadhi yake. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba utaratibu huu wa kumega maeneo na kuteremsha hadhi maeneno ya hifadhi haujirudii tena?

Swali la Pili, kwa kuwa upoteaji wa uoto wa asili unaenda sambamba na upoteaji wa viumbehai, mimea na wanyama ambao wako hatarini kutoweka. Je, Serikali ina mpango gani wa kuainisha na kuwea kutenga utaratibu maalum wa kuweza kuhifadhi viumbe adimu na wale ambao wako hatarini kutoweka? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliridhia kuachia maeneo yenye migogoro vilevile kushusha hadhi baadhi ya mapori na hifadhi zetu baada ya kubaini kwamba ipo migogoro isiyokuwa na tija iliyokuwa inahatarisha usalama wa wananchi wetu. Serikali ilifanya hivyo baada ya kufanya utafiti wa kina kuona kiasi cha matumizi endelevu ya maeneo hayo, jinsi ambavyo yanaweza kutumika na kama yalikuwa yanatumika kwa jinsi ambavyo ilivyokuwa imekusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale inapoonekana kwamba pori au hifadhi imepoteza sifa yake ya awali ya msingi, basi maeneno hayo hushushwa hadhi na kuwa misitu ili tuweze kuendelea kutunza maeneno haya. Katika kujipanga kuhakikisha kwamba hali hii haijitokezi tena, Serikali inajipanga kutoa elimu kwenye maeneo yote yanayozunguka maeneo ya hifadhi zetu na mapori tengefu ili kujenga uelewa wa wananchi kuhusiana na umuhimu wa rasilimali hizi, vilevile Serikali imejipanga kuongeza doria katika maeneo haya ili uvamizi usijitokeze tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, Serikali inajitahidi sana kuhakikisha kwamba pale ambapo mimea imetoweka au wanyama wametoweka Serikali imekuja na mkakati wa kupanda miti kwenye maeneo yale yaliyoathirika, kwa mfano kupitia TFS tumeaza kupanda miti kule Mkoani Geita, vilevile tumeanza kupanda miti Mkoani Kigoma zaidi ya hekta 139,000 zimepandwa ili kuhakikisha uoto ule haupotei.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pale ambapo tunaona kwamba kuna aina fulani ya wanyama inatoweka, tunakuwa na mkakati wa kuweka maeneo maalum ya kuhakikisha tunadhibiti kuzaliana kwa wanyama wale ili wasije wakatoweka. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba moja, kwa kuwa NEMC ndiyo taasisi pekee Tanzania ambayo ina uwezo wa kuomba fedha kupitia huu mfuko wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi. Je, Serikali inashirikishaje taasisi nyingine pamoja na NGO katika kuwajengea uwezo ili waweze kuomba fedha na kuzipata kwa haraka?

Swali namba mbili; Je, kwa kuwa Zanzibar fedha hizi pia zinatumika. Je, Serikali haioni haja ya kusaini memorandum of understanding na taasisi moja Zanzibar kama vile ZEMA ili kuweza kuimarisha uratibu na kuwajengea uwezo Wazanzibar ili fedha hizo ziweze kutumika kwa ufanisi zaidi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano Mazingira hasa kupitia Baraza la NEMC tunao utaratibu wa kutoa uelewa kwa wale ambao wanakuja kuandika miradi na kuileta kwetu, zaidi wale ambao watakuja na miradi endapo miradi hiyo itakuwa haijakamilika taarifa zake, hapo ndipo tunawaita na kuwapa uelewa na kuwafahamisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kama kutakuwa na taasisi inataka kuandika miradi na hasa inataka kuleta kwetu basi tupo tayari kwenda kuwapa uelewa ili lengo na madhumuni wawe na ujuzi na utaalam mzuri wa kuandika miradi ambayo itakwenda kusaidia kutatua changamoto za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Zanzibar tunao ushirikiano na usimamizi mzuri sana wa fedha za miradi na ndiyo maana miradi mingi haijakwama na inaendelea vizuri kwa upande wa Zanzibar na upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendeleza ushirikiano huo ili lengo na madhumuni tutatue changamoto za wananchi hasa za kimazingira na zile ambazo zina lenga katika kubaliana na mabadiliko ya tabianchi. Nakushukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mie kuuliza swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa misitu mingi ipo katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa; je, kuna utaratibu gani wa Serikali kuzihamasisha taasisi za Serikali kuweza kushiriki katika biashara hii ya hewa ukaa?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la kaka yangu Mheshimiwa Soud, mimi namuita encyclopedia ya mambo ya mazingira kwa sababu amebobea sana katika mambo ya mazingira katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kwamba kama tulivyosema ni kwamba katika kushirikisha taasisi hizi hata sasa hivi ukiangalia kwa mfano TFS wana misitu mingi sana, lakini bado hawajanufaika katika hewa ya ukaa, ni halmashauri ya Katavi peke yake na kule kama tulivyosema Simanjiro ambao wao kwa mwaka ile own source collection katika hewa ya ukaa ni kubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ndiyo maana tumeweka mwongozo kwa lengo kubwa ni kwamba taasisi kwa mfano TFS, vijiji vyetu, halmashauri zetu na watu binafsi waweze kushiriki vizuri katika hewa ya ukaa. Kwa hiyo ndiyo jambo ambalo tuliona kulikuwa na gap hapo tunaenda kuya-address gap hii kwa lengo kubwa ni kwamba kujenga uchumi wa nchi yetu katika suala zima la hewa ya ukaa.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la uhalifu limekuwa likiongezeka siku hadi siku katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar na tatizo hili limeshazungumzwa sana hapa Bungeni.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mkakati gani wa kushirikiana na Vikosi Maalum vya SMZ kule Zanzibar ili kuweza kutokomeza na kufanya jambo hili kuwa historia? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Soud Mohammed - Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, makosa ya uhalifu kama ambavyo yanatokea maeneo tofauti, yamebainishwa Zanzibar vikundi vinaongezeka na nilikuwepo kule, viko vikundi vingine vya wavuta bangi. Lakini kinachofurahisha Jeshi la Polisi Kamisheni ya Zanzibar wanafanya kazi nzuri sana na kwa kawaida vyombo hivi hushirikiana na vyombo vingine vya usalama vikiwemo SMZ katika vikao mbalimbali vya ngazi ya Mkoa, kuna Kamati za Usalama za Mkoa, ngazi ya Wilaya kuna Kamati za Usalama za Wilaya na hivyo kupeana ushauri na mbinu za kukabiliana na matukio haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie polisi wetu wako imara kwa kushirikiana na vyombo vingine watakabiri makundi haya yanayoibukia huko Zanzibar kwa madhumuni ya kuyadhibiti. Nashukuru.
MHE. MOHAMED JUMAH SOUD: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Donge limepanuka sana na hivyo vigezo ambavyo amevizungumza Mheshimiwa Naibu Waziri vingi vyake vinakidhi kuanzishwa Kituo cha Polisi katika Jimbo la Donge na halikadhalika uharamia umeongezeka sana kiasi kwamba mazao sasa hivi kulima kumekuwa ni shida, mifugo kufuga imekuwa ni tabu. Swali hili niliwahi kuuliza hapa na Mheshimiwa Naibu Waziri aliniahidi kwamba atafanya tathmini ili kuangalia uwezekano wa utekelezaji. Sasa je, ananiahidi vipi ile tathmini imeshafanyika na kama haijafanyika basi lini itakamilika ili utekelezaji uanze. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la moja la nyongeza la Mheshimiwa Soud, kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kama nilivyosema ameeleza hapa Jimbo la Donge linakidhi vigezo hivyo, kupitia Bunge lako Tukufu nimwelekeze Kamishna wa Polisi wa Zanzibar na Wasaidizi wake waweze kufanya tathmini ya eneo hilo. Wakibaini kwamba linakidhi vigezo, basi hatua za kujenga Kituo cha Polisi liweze kufanyika. Mheshimiwa Mbunge tutapeana ushirikiano ili kuona kwamba jambo hilo linafanyika. Ahsante sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na nimpongeze sana kwa majibu mazuri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kama mnavyojua kwamba, baadhi ya Kamandi au Kambi kumekuwa na tabia ya ukataji wa miti na uondoaji wa misitu ambayo imekuwepo kwa muda mrefu. Sasa, nilikuwa naomba tu kujua Mheshimiwa Waziri, wana mwongozo gani wa kushirikiana na Taasisi za Idara za Mazingira na Misitu hasa kule Zanzibar, ili kuona kwamba miradi hii ikiibuliwa na ikitekelezwa basi haiathiri mazingira?

Swali namba mbili, je, Kamandi au Wizara ina utaratibu gani wa kuwa na mwongozo wa mapato na matumizi kama vile walivyo wenzetu wa Jeshi la Polisi ule mpango wa Tuzo na Tozo, ili kuhakikisha kwamba, mapato yanayopatikana yanatumika katika njia ya ufanisi zaidi? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, miradi hii huzingatia pia taratibu za uhifadhi wa mazingira. Kwa hiyo, tunafuata mwongozo wa Serikali kuhakikisha kwamba, taratibu za uhifadhi wa mazingira zinazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mwongozo wa mapato na matumizi; Miradi hii inaendeshwa kwa kuzingatia kwanza inachambuliwa na Makao Makuu ya Jeshi na umewekwa utaratibu ambao pesa zote zinazopatikana zinafuata Taratibu za Matumizi ya Fedha katika Taasisi za Umma. Kwa hiyo, hakuna wasiwasi kwamba, pesa hizi labda zinapotea na nipende kutoa pongezi kubwa sana kwa Jeshi letu la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, kwa kazi kubwa mabyo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kipindi tulikuwa na ukwasi lakini miradi hii imesaidia katika kutekeleza majukumu ya msingi ya Jeshi. Kwa hiyo, nawapongeza sana Jeshi letu na nikuhakikishie kwamba, taratibu na matumizi ya fedha haya yanafuata taratibu zote, hata audit huwa zinafanywa, ahsante sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuondoshwa kwa maeneo ya kinga (buffer zone) kunasogeza zaidi wananchi karibu na hifadhi na kuwahatarisha na wanyama wakali na waharibifu: Je, Serikali haioni haja ya kuja na mikakati zaidi ya kutoa elimu ili kuwasaidia wananchi hawa kuwaepusha na hiyo hatari? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa buffer zone kitaalam inalenga kuwatenga wananchi na maeneo ya hifadhi na hivyo, kupunguza vitendo vya uharibifu na vitendo vya uvamizi.

Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuhakikisha kwamba, utaratibu huu wa kuondoa buffer zone katika maeneo ya hifadhi haujirudii? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mohammed Soud Jumah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, Wizara inajielekeza sana kwenye kutoa elimu. Sambamba na hiyo, kwenye maeneo ya namna hii vilevile tuna mikakati ya kuwahamasisha wananchi kufuga nyuki kwenye maeneo hayo. Vilevile, kuendesha utalii wa kiutamaduni, kupanda au kutunza misitu ili waweze kuja na mfumo wa biashara ya uvunaji wa Hewa ya Ukaa. Tunaamini wananchi wakijielekeza kwenye maeneo haya, basi huo muingiliano utapungua athari zake.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, ni kweli kwamba maeneo haya ya buffer zone yanalenga kuwatenga wananchi na maeneo ya hifadhi ili kuwaondolea athari ya madhara ya uvamizi na hivi. Pamoja na kutoa elimu, Wizara inajielekeza kwenye kusimamia sheria, kanuni na taratibu za uhifadhi na kutoa elimu kwa viongozi na wananchi. Imani yetu ni kwamba, elimu hii ikiwaingia wananchi na wakazingatia maelekezo haya, basi migogoro hii itaondoka. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na nimpongeze sana kwa majibu mazuri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kama mnavyojua kwamba, baadhi ya Kamandi au Kambi kumekuwa na tabia ya ukataji wa miti na uondoaji wa misitu ambayo imekuwepo kwa muda mrefu. Sasa, nilikuwa naomba tu kujua Mheshimiwa Waziri, wana mwongozo gani wa kushirikiana na Taasisi za Idara za Mazingira na Misitu hasa kule Zanzibar, ili kuona kwamba miradi hii ikiibuliwa na ikitekelezwa basi haiathiri mazingira?

Swali namba mbili, je, Kamandi au Wizara ina utaratibu gani wa kuwa na mwongozo wa mapato na matumizi kama vile walivyo wenzetu wa Jeshi la Polisi ule mpango wa Tuzo na Tozo, ili kuhakikisha kwamba, mapato yanayopatikana yanatumika katika njia ya ufanisi zaidi? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, miradi hii huzingatia pia taratibu za uhifadhi wa mazingira. Kwa hiyo, tunafuata mwongozo wa Serikali kuhakikisha kwamba, taratibu za uhifadhi wa mazingira zinazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mwongozo wa mapato na matumizi; Miradi hii inaendeshwa kwa kuzingatia kwanza inachambuliwa na Makao Makuu ya Jeshi na umewekwa utaratibu ambao pesa zote zinazopatikana zinafuata Taratibu za Matumizi ya Fedha katika Taasisi za Umma. Kwa hiyo, hakuna wasiwasi kwamba, pesa hizi labda zinapotea na nipende kutoa pongezi kubwa sana kwa Jeshi letu la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, kwa kazi kubwa mabyo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kipindi tulikuwa na ukwasi lakini miradi hii imesaidia katika kutekeleza majukumu ya msingi ya Jeshi. Kwa hiyo, nawapongeza sana Jeshi letu na nikuhakikishie kwamba, taratibu na matumizi ya fedha haya yanafuata taratibu zote, hata audit huwa zinafanywa, ahsante sana.