Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Soud Mohammed Jumah (19 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi kuweza kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi kwa vile ni mara yangu ya kwanza kusimama katika hadhira hii ningeanza kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhana Wataalah, lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein ambaye kwa kweli amenilea na kunikuza na kuniamini kunipa Idara ya Misitu kuweza kuiendesha kwa miaka karibu minne ambayo ndiyo imenijenga na kuwa mtu wa namna hii hapa nilipo.

Mheshimiwa Spika, pia ningependa kumshukuru mama yangu Bi. Jira binti Machano na mke wangu Shufaa binti Suleiman Hamad pamoja na wanangu bila kusahau wanachama wa Chama Cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Donge ambao wamenipa imani kubwa ambayo imenisababisha mimi leo kusimama hapa nikiwawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kwa moja niende kwenye hotuba ya Mheshimwa Rais na nianzie ukurasa namba tisa ambapo Mheshimiwa Rais ameipongeza Tume ya Uchaguzi kwa kuendesha uchaguzi katika hali nzuri, lakini pia kutoa matokeo haraka na kuipongeza kwa kuweza kubana matumizi kwenye bajeti ambayo walikuwa wametengewa ya shilingi bilioni 331 na kutumia shilingi za Kitanzania bilioni 262.

Mheshimiwa Spika, hapa nilikuwa napenda kutoa angalizo maalum kwamba aliyepaswa kushukuriwa zaidi hapa ni Mheshimiwa Rais mwenyewe pamoja na Rais Dkt. Ali Mohamed Shein kwa sababu viongozi hawa wameweka alama katika uchaguzi wa mara hii kwa sababu ni mara ya kwanza Tanzania imeweza kuendesha uchaguzi kwa kutegemea fedha za ndani tofauti na miaka yote iliyopita. Kwa kweli tunawashukuru sana viongozi wawili hawa kwa sababu wameweka alama.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika ningependa kwenda kwenye page number 13 ambayo Mheshimiwa Rais ameweza kuelezea kwamba, atazienzi tunu za Taifa letu ambazo zinajumuisha amani, uhuru, mshikamano, umoja, Muungano pamoja na Mapinduzi ya Zanzibar. Pia ameendelea kwa kusema kwamba, atashirikiana na na Rais Dkt. Mwinyi kuweza kuhakikisha kwamba tunu hizi zinalindwa kwa gharama zozote zile.

Mheshimiwa Spika, hapa ningetoa pia angalizo kwa sababu kuna watu wanapenda kuchezea Muungano wetu na halikadhalika nafikiri juzi mnakumbuka kwamba kuna kiongozi mmoja wa kisiasa amejaribu kuzungumza kumzungumzia kiongozi mkuu wa Serikali kwamba, ana maradhi na lengo lake sote tulikuwa tunalifahamu kwamba ilikuwa ni kuleta mshtuko miongoni mwa jamii ambayo hivi sasa kama tunavyofahamu uchumi wetu umeanza kuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule tulikotoka ndege zilikuwa hazionekani, watalii walikuwa hawaonekani, lakini hivi sasa tumeanza kuimarika, kwa hiyo, nafikiri bado ambao hawapendi mshikamano na umoja wa nchi yetu, Muungano una dumu, basi wanatafuta kila aina ya visingizio kuweza kutumia fursa kuweza kuleta chokochoko. Kwa hiyo, tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutoa angalizo hili kwamba atashirikiana na Dkt. Mwinyi kuweza kuhakikisha kwamba analinda tunu hizi za Taifa kwa gharama yoyote.

Mheshimiwa Spika, lakini ningependa kumalizia kwa kuhusu maliasili na utalii.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SOUD MUHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais katika hotuba yake amesisitiza kuziendeleza na kuhifadhi maliasili za nchi. Katika kumuunga mkono na ili kumsaidia kufikia malengo ni vyema changamoto za sekta za maji, ardhi, kilimo na mifugo ambazo zinachangia moja kwa moja uharibifu wa maliasili zishughulikiwe kwa ushirikiano wa kisekta.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ripoti ya Mawaziri saba kuhusu ardhi iletwe Bungeni na kujadiliwa, kwani kuna michango mizuri ya kujenga kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Serikali iwe makini katika kumega hifadhi na mapori ya akiba kwa lengo la utatuzi wa changamoto za sekta za ardhi, mifugo na kilimo. Huu hauwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia yafuatayo nikianza na sualalal ulinzi na uhifadhi wa vyanzo vya maji. Kuna uharibifu mkubwa wa vyanzo vya maji nchini. Wizara imeweka nguvu nyingi na fedha zaidi kwenye miundombinu na kuliacha suala la uhifadhi wa vyanzo vya maji kwa sekta nyingine hussusan za maliasili. Ni vyema kuanzisha uratibu na miradi ya pamoja na sekta za misitu ili kulinda na kuhifadhi vyanzo vya maji. Tuweke mikakati ya pamoja na sekta za kilimo, mifugo na misitu ili kizitafutia suluhisho la kudumu changamoto zinazotishia uendelevu wa vyanzo vya maji.

Pili ni kuhusu upotevu wa maji; tuongeze fedha zaidi kwa kushirikiana na TAMISEMI ili kukarabati miundombinu ya maji iliyochakaa. Aidha, tuendelee kutoa elimu kwa jamii kujenga tabia ya kutumia maji kwa nidhamu zaidi na kulinda miundombinu yake.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kuhusu mabadiliko ya tabianchi sambamba na makazi holela inachangia sana upoteaji wa maji na uharibifu wa vyanzo vya maji. Tufanye kazi kwa karibu na sekta za misitu na ardhi ili kupanga makazi katika hali bora zaidi itakayozingatia uwepo na uendelevu wa vyanzo vya maji. Aidha, tuimarishe dawati la mazingira na mabadiliko ya tabianchi ili kuweza kupata ushauri na kuzingatia athari za mabadiliko ya tabianchi katika shughuli zote za sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Allah Subhanhu Wataallah kwa kutujaalia uzima, salama na kuendelea kuijalia nchi yetu kuendelea kuwa na usalama na kutamalaki kwa maisha mema nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependaa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya yeye pamoja na Naibu Waziri Ndugu Pinda, pamoja na timu nzima ya watendaji, kwa kweli mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. Tumeona maendeleo makubwa tu katika mabadiliko ya ardhi na hili nafikiria ni register shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifaya na inaonesha wazi Mheshimiwa Rais, kwa kweli anapita katika nyanja zilezile ambazo alipita Hayati Julius Kambarage Nyerere, pamoja na Hayati Abeid Amani Karume, kwa kuweka usalama wa matumizi bora ya ardhi na kuwamilikisha wazawa na wananchi wanyonge kuendelea kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuelekeza mchango wangu katika maeneo matatu makubwa; la kwanza, mwenzangu jana Mheshimiwa Chege aliligusia kidogo kuhusu suala la sera. Nafikiria ni kipindi kirefu kidogo tumekuwa tukizungumzia suala la kukamilisha Sera ya Maendeleo ya Ardhi pamoja na Sera ya Maendeleo ya Makazi nchini, na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri na timu yake wamefanya kazi nzuri katika hili na hadi sasa tayari rasimu ipo na kuna mabadiliko machache ambayo yanasubiriwa hasa katika suala la diaspora pamoja na watu wa real estate kuweza kulikamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nilikuwa nina ushauri hapa; ushauri wangu ni kwamba nimuombe tu Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa zile changamoto ambazo zinaonekana ni ngumu kidogo kuweza kukamilika kwa haraka na kuikamilisha rasimu hii ya sera. Basi tungeendelea na mchakato tukaja tukaweka provision katika maeneo ya sheria katika maeneo ya sheria kwa kuja kuitayarisha kanuni ambayo itakuja kuwasaidia wenzetu wa diaspora pamoja na usimamizi mzima wa masuala la real estate. Hii itafanya tukamilishe hii sera haraka na kuanza kuitekeleza ili iende ikasaidie zile changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge hapa wamekuwa wakizungumza kila mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la pili nigusie kidogo kuhusu suala zima la mipaka ya kimataifa; kazi nzuri imekuwa ikifanywa katika kuainisha na kuweka mipaka katika maeneo mbalimbali lakini bado hatuendi kwa kasi. Kwa hiyo, mimi nilikuwa naomba tu, Mheshimiwa Waziri na hivi zaidi tusimlauimu Mheshimiwa Waziri wa Ardhi ni Waziri wa Fedha, kwa sababu wao wanafanya kazi kulingana na kiwango cha fedha ambazo wanakasimiwa. Sasa ningeomba tu Waziri wa fedha akatenga fedha za kutosha ili hili zoezi la kuainisha na kuweka mipaka ya kimataifa kwa haraka basi likaenda kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunategemea fedha kwa hiyo Mheshimiwa Waziri wa Fedha nafikiri hayupo, lakini anatusikia huko aliko, kwamba tuisaidie fedha hii Wizara ya Ardhi, kwa sababu hawawezi wakafanya miujiza kama hawana fedha za kutosha katika kulifikia hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi pia nilikuwa na ombi moja hapa. Mheshimiwa Waziri najua tunashughulika na mipaka zaidi ya kimataifa lakini na mipaka ya ndani vilevile tuiangalie na haswa masuala ya Zanzibar na Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wenzetu wa usimamizi hasa baharini wanapata shida wakati mwingine katika kusimamizi wa rasilimali za bahari na rasilimali nyingine za uvuvi na ulinzi kwa sababu mipaka ya Zanzibar na Tanzania Bara hasa katika eneo la bahari vilevile nalo ni kiini macho, kwa hiyo, ningeliomba na hili nalo tukaliingiza katika kuweka mipaka, basi na hili pia nalo tukaliingiza katika kubainisha ule mpaka hasa tukajua tukawasaidia watendaji wetu wa uvuvi, watendaji wetu wa kilimo, watendaji wetu wa Serikali kwa ujumla wakajua ile mipaka ili usimamizi wao na utendaji kazi wao tukaurahisisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na suala la tatu nigusie katika suala zima la upimaji na usimamizi mzima wa ardhi; changamoto nyingi zimekuwa zikizungumzwa hapa kwamba mipaka imekuwa ina shida lakini pia upimaji hauendi kwa kasi. Lakini vilevile nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kweli tumeona kuna maendeleo makubwa yamekuwa yakiendelea katika sekta nzima ya upimaji wa ardhi Tanzania na kwa kweli nimpongeze sana mpima na zaidi Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Upimaji ya Ardhi nchini, anafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nilikuwa na mapendekezo machache; kwanza, tukaangalie migogoro ambayo kwa kipindi kirefu imetamalaki Tanzania. Kuna mgogoro wa Tarime. Mipaka inajulikana toka mwaka1968 na wameenda watendaji kule wakiongozwa na mwenyewe mwenye hatimiliki ya kuainisha na kutafsiri mipaka Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, lakini ameondoka kule bado shida ameiacha iko vilevile. Lakini pia juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu amenda Mbarali nako vilevile akaenda akatoa maeneo na maeneo yale kwa kweli maeno oevu, maeneo ya majimaji, ya chemchem, lakini pia tukawa tume–risk, tukawapa wananchi lakini alipoondoka yale maeneo ambayo tumekubaliana watu wakaanza kuvamia tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hali kadhalika kuna hekta karibu 950,000 tumezitoa tukawapa wananchi na tumeyakata maeneo ya hifadhi, hifadhi nyingine tumeziondoa, hifadhi nyingine tumezimega tukawapa wananchi, lakini bado matatizo ya ardhi yanaendelea. Kwa hiyo, hapa tatizo la migogoro ya ardhi tuliweka kama ni suala ambalo litaendelea kwa miaka mingi itakayokuja. Tuweke utaratibu wa watu kuweza kwanza, kuwa wazalendo na kutii sheria hili la muhimu na tukiweka utaratibu Mheshimiwa Waziri wa kwamba kila mtu tumridhishe kwa atavyotaka basi nchi nzima itakuwa ni kama vile uwanja wa mpira tunanyang’anyana tu mpira utacheza wewe kwa atakayekuwa na nguvu ndio atafunga goli, kama Mayele ana nguvu nzuri zaidi ana magoli 16 sasa. Kwa hiyo itakuwa mwenye nguvu ndio anashinda sasa unaona. (Makofi)

Kwa hiyo mimi ninaloomba tuendeleze utii wa sheria kwa wananchi wetu. Mipaka ikishakutafsiriwa na Mheshimiwa Waziri ambaye ndio tumempa nafasi hii ya yeye ndio atafsiri mipaka ya ardhi ya nchi yetu, akishatafsiri basi pande nyingine ziridhike. Lakini leo Mheshimiwa Waziri unaitwa uende na timu yako wanakwenda sio kwamba ukafanye utatuzi, unaitwa uende ukatoe haki kwa upande ambao watu wangependelea uwape, siyo kwa sababu ya kwamba ukafanye haki kwamba tunavyoona mimi mpaka uko hapa, nyie kuweni huku. Kwa mfano, kama Tarime, Tarime Mheshimiwa Rais amefanya favour mpaka buffer area ya zile mita 500 zile amewapa wananchi, baada ya kusema kwamba nusu tuwape hifadhi na nusu tuwape wananchi Mheshimiwa Rais amesema zote wapeni wananchi. Ametoa favour kubwa lakini bado tatizo linaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba mipaka hii ya ardhi itaendelea kuwepo, lakini Serikali isimame katikati, itoe haki kama inavyohitajika na mimi nitoe ushauri nimalizie kwa ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa kwanza huu mradi ambao wa usalama wa miliki za ardhi Mheshimiwa Waziri twende tukaushughulikie na tukausimamie ipasavyo, kwa sababu una malengo mazuri na mimi nimeusoma mradi mzima ule nimeusoma vizuri. Tunakwenda kuandaa hati milioni mbili kwa wakazi wa mijini na tunakwenda kuandaa hati 500,000 zile hati za kimila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunakwenda kuandaa miundombinu ya kidijitali ambayo itarahisisha kufanya shughuli zetu kwa haraka. Sasa hivi ni 10% ya mradi tunaenda kupima, lakini tukiumaliza mradi tutakuwa tumeandaa miundombinu ya kuweza kusaidia upimaji kwa haraka zaidi na hivi Mheshimiwa Waziri ningependa sana utakapokuja hapa ukawaeleza wananchi huu mradi una tija kiasi ngapi? Kwa sababu wananchi wengi hasa Waheshimiwa Wabunge bado hawajaelewa pamoja na semina ambayo umetufanyia pale Msekwa bado hawajaelewa tija ya huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia tija ya matokeo ya huu mradi unakwenda kumaliza tatizo la upimaji wa ardhi nchini, unakwenda kumaliza tatizo la migogoro ya ardhi nchini. Hebu Waheshimiwa Wabunge wenzangu tumpe muda Mheshimiwa Waziri na timu yake wakatekeleze huu mradi kwa sababu tunasema huu mradi fedha nyingi zimewekwa kwenye uratibu. Uratibu ukijenga ofisi nao ni uratibu, ukienda kutayarisha miunombinu ya communication ikawa mawasiliano mikoa kwa mikoa nao ni uratibu. Isionekane kwamba labda shilingi bilioni 45 zinaenda kwenye uratibu kwamba hizi fedha labda ni watu watakuwa wakikaa kitako ndio wanatumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naangalia mradi mzima sikuangalia lile jedwali la fedha tu. Nimengalia mradi mzima in totality, nimeona kwamba kwa kweli mradi huu una tija na Mheshimiwa Waziri tukiushughulikia basi utakwenda kutuvusha katika suala zima la migogoro ya ardhi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu subhanahu wata’ala kwa kutujalia uhai, uzima na salama lakini pia nikimshukuru sana Mheshimiwa Rais ambaye ni mhifadhi namba moja kwa jitihada ambazo amekuwa akizichukua katika kuendeleza masuala mazima ya uhifadhi wa maliasili Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Kwa kweli amechukua ofisi hii muda mfupi uliopita lakini jitihada zake zinaonekana wazi kwamba anakwenda kufanya kitu. Jitihada tumeziona na mimi juzi wakati anazungumza kwenye semina pale niliwaambia wenzangu naona Mheshimiwa Waziri hii tune ambayo ameizungumza hapa leo, hii ndiyo tune ya maliasili. Maana yake kuna tune ambayo unaweza ukaiongea mahali pengine lakini kuna tune nyingine hiyo ndiyo ya kuiongelea kwenye Maliasili na ndiyo ile Mheshimiwa Waziri uliyozungumzia ukamalizia pale kwenye semina juzi, ile ndiyo tune ya kuizungumza katika uendelezaji wa maliasili popote duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia mambo manne kama muda utaruhusu. Jambo la kwanza ninazungumzia kuhusu suala la uendelezaji wa hifadhi zetu. Kama inavyofahamika kwamba hifadhi zetu zimeongezeka kutoka hifadhi 16 mpaka kwenda kuwa hifadhi 22, eneo la hifadhi limeongezeka kufikia karibu kama sijakosea kilometa za mraba sasa hivi 105,000 hivi kama. Eneo ni kubwa lakini bajeti haikuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulizungumzia hili hapa hali kadhalika wakati tunatoa ripoti ya nusu mwaka Kamati pia ilipendekeza kwamba lazima tuangalie uwezekano wa kuongeza bajeti katika hifadhi zetu ili ziweze kukidhi changamoto ambazo zinatokea kwenye uhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mwaka jana wakati ana-conclude speech yake hapa aliahidi kwamba hifadhi atazipatia bajeti ya miezi miwili kwa utangulizi ili bajeti moja ibakie kama spare in case ikitokezea dharura za moto, dharura za uhifadhi zote zile itatumika lakini utatuzi huu haukusaidia sana. Hifadhi zetu bado zinateseka na tatizo la kibajeti na zinahitaji mchango mkubwa kwenye bajeti. Kwa hiyo mimi napendekeza kama alivyozungumza Mheshimiwa Hawa Mwaifunga hapa kwamba pamoja na changamoto za retention ambazo zilipelekea retention kuondoshwa, mimi naomba tena retention tuirejeshe hata kwa asilimia siyo ile iwe pungufu lakini retention ni muhimu katika masuala ya uhifadhi. Hiyo ni kama utaratibu wa kidunia. Masuala ya uhifadhi lazima kuwe kuna retention ambayo inatumika kwa sababu ukifuata utaratibu wa kawaida wa kibajeti basi hutozisaidia sana kwa sababu mambo mengi ya kidharura yakitokezea hutoweza kuyashughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ningependa kuzungumzia kuhusu mwenzangu ambaye amechangia kuhusu Msomera. Nahisi kama tunakwenda kusahau changamoto ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Tulipelekea kufanya maamuzi yale tuliyopelekea watu waende Msomera kwa sababu Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro iko hatarini, hizi hatari zilizungumzwa hapa na watu wakafika mpaka kutoa machozi kutokana na tatizo la Mamlaka ya Ngorongoro lakini sijui ni utaratibu wetu au utamaduni wetu watanzania, jambo tunaweza tukalichukua kwa kasi kubwa lakini baadae tukapoteza mood.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hizi mood ya Ngorongoro imeanza kupungua. Sasa nilichangia hapa katika ripoti ya Kamati ya nusu mwaka nikazungumza kwa sababu wenzetu wameshafanya utafiti wamesema wakipata shilingi bilioni 200 basi hii kazi inakwenda kuisha. Nikazungumza kwamba kwa sababu makusanyo ya Mamlaka ya Ngorongoro yenyewe tu yanakaribia shilingi bilioni 200, sasa kama hatuna fedha basi Mheshimiwa Waziri wa Fedha tuwaruhusu wenzetu wa Ngorongoro wanachokikusanya wakitumie ili tuondoshe hili tatizo, lakini kama kuna uwezekano mwingine basi tuwakopee, tutafute mahali tukope hili jambo tulimalize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waswahili wanasema, “Mchuzi wa mbwa unywewe ukiwa wa moto.” Sasa suala la Ngorongoro tulimalize likiwa liko moto moto, tukikaa hapa miaka mitatu, minne, mitano tutapoteza dira nzima ya masuala ya Ngorongoro ambayo tilishakubaliana nayo hapa. Kwa hiyo niombe Wizara na zaidi Waziri wa Fedha tuwapatie wenzetu Mamlaka ya Ngorongoro, tuwapatie wenzetu wa Maliasili fedha kwenda kumaliza hili suala. Tusifanye kazi zetu kwa vipande vipande, tunafanya kazi nusu, nusu inabakia mwaka mzima, matokeo yake tuna vipande vipande dunia nzima hatuendi hivi. Kwa hiyo mimi naomba hili tukalisaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ni kuhusu Jeshi USU ambalo pia mwenzangu hapa amelizungumzia, sasa hivi limepandishwa daraja limekuwa Jeshi la Uhifadhi. Tunalo tatizo kubwa kuhusu suala zima la Jeshi la Uhifadhi maslahi yao siyo mazuri. Mheshimiwa Waziri amezungumza hapa na alikuwa anakaribia kutoa machozi, Jeshi la Uhifadhi wanapata shida sana. Wanakufa, wanauliwa, wanajeruhiwa lakini maslahi yao hayaendani na kazi wanayoifanya. Watu wa Jeshi USU au Jeshi la Uhifadhi wako kwenye mapambano mwaka mzima, wawe mitaani mwaka mzima anaingia kazini bismillah kwanza ana mapambano na wanyamapori lakini ana mapambano na majangili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuende tukarebishe maslahi ya Jeshi la Uhifadhi na hili mimi nilitegemea, kwa sababu tunaambiwa kwamba watu wa utumishi ndiyo wanalishulikia hili suala, kuna suala sijui waraka tayari umeishapelekwa wapi? jamani tusifanye kwa mazoea hebu tukifanya mambo tuyamalize, hawa watu wanauhitaji. Hapa nitoe ombi maalum vijana wetu wanaomaliza Olmotonyi, Mweka ambao ndiyo tunategemea tuwaajiri kwenda kuwa Jeshi la Uhifadhi, kwa sababu hatuajiri kila mwaka tunakaa miaka miwili, miaka mitatu wanapitwa na umri, sasa hili suala la umri Mheshimiwa Waziri hebu liangalie hili, tusiwaache hawa vijana ambao tayari wameishamaliza chuo na wana vigezo vyote, lakini suala la umri linakwenda kuwasumbua. Kwa hiyo ningeomba tu suala la umri ingawa lipo kisheria, hebu tukaliangalie kwamba wanafunzi wote ambao hawajaajiriwa wanachuo wetu basi ikitokea nafasi wawe na nafasi sawa ya kuomba kuweza kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne ni kuhusu suala la hewa ya ukaa. Nimshukuru sana Mheshimiwa Jafo amepiga hatua kubwa kwa kutayarisha mwongozo wa suala zima la biashara ya hewa ukaa, lakini bado hatuendi kwa hatua kubwa hasa katika uelimishaji. Kwa sababu inaonekana kwamba biashara ya hewa ya ukaa ni kama vile Serikali ndiyo itaongoza kila kitu. Hii ni biashara huria isipokuwa Serikali inatakiwa iweke vigezo na kuwaruhusu wadau kuingia kwenye hii biashara. Kwa hiyo, tuende tukatoe elimu kwa sababu ina faida kubwa katika uhifadhi wa misitu yetu hii ni incentive.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa uharibifu wa misitu ni mkubwa sana kwa Tanzania. Tunapoteza karibu hekta laki nne kila mwaka, sasa watu wanafikiria kwamba ukishakuwa na msitu tayari wewe uko eligible kuweza kupata fedha za hewa ya ukaa. Kupata fedha za hewa ya ukaa ni incentive ya uhifadhi, umehifadhi kwa kiwango gani? kwa hiyo, kile kiwango ambacho kinaongeza (additionality permanence) ya uhifadhi ndiyo inayokwenda kukupa credit ya biashara ya hewa ya ukaa. Kwa hiyo, twende tukatoe elimu kwa wananchi wetu, tukawambie kwamba kuwa na msitu ni jambo moja lakini suala la kuulinda, kuhifadhi usichomwe moto, usikatwe hovyo, usiharibiwe ndiyo utakwenda ku – add value wewe kupata fedha za hewa ya ukaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie katika suala zima la utafiti. Tuna taasisi zetu za utafiti za TAFORI na TAWIRI lakini nazo hizi zina tatizo kubwa la kibajeti na tumelizungumzia hapa, ukienda TAFORI kwa mfano, inafika wakati hata kuweza kulipa umeme hawawezi, ile kulipa umeme hawawezi inamaana inabidi wachangishane ofisini wakalipe umeme wa ofisi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningeliomba Mheshimiwa Waziri, tukazingalie hizi Taasisi za Utafiti, kwa sababu hakuna nchi ambayo itaendelea bila utafiti, hakuna eneo ambalo utalifanyia kazi bila utafiti, ili wafanye utafiti vizuri lazima tuendeleze kibajeti. Sasa ningeliomba tu angalau fedha ambazo zilikuwa zinatengwa tuwaongezee ziongezeke kidogo kadhalika na fedha zenyewe zipatikane kwa wakati, siyo fedha zinatengwa asilimia 100 lakini wanapata asilimia 26 mwaka ukimalizika, hii haitusadii sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, Bismillah Rahman Rahim, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini halikadhalika napenda vilevile kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mulamula pamoja na Mheshimiwa Balozi Mbarouk na timu yao ya Wizara kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakifanya katika kuboresha diplomasia ya uchumi pamoja na kuhuisha mahusiano mema ya Tanzania ya kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika kabla sijaenda mbali naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Hassan Mwinyi kwa kitendo cha uungwana alichokifanya ambacho hakuwa amekipangia cha kuweza kuwahudumia vizuri wale wakimbizi wa Ukraine ambao walikuwa wamekwama kule Zanzibar wakati kwao lilipotokea lile tatizo la vita na wakawa hawana jinsi isipokuwa wabakie Zanzibar, na katika hili pia napenda kuishukuru Wizara kwa sababu Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Tanzania ndiyo ilishirikiana na Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Hassan Mwinyi kuweza kuwahudumia wale wakimbizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo nimpongeze vilevile ndugu yangu Balozi Simbachawene kwa jitihada zake ambazo alizifanya hivi karibuni na kitendo kile kimeonesha mfano wa Mabalozi wetu kwamba wanaweza wakafanya kazi nzuri katika hali ya dharura. Kuna vijana ambao walikuwa wavuvi wetu kule Zanzibar, walipata tatizo baharini na wakaenda wakaokotwa Kenya. Lakini ubalozi wetu wa Kenya ulifanya kazi kwa haraka na vijana wetu wale wakashughulikiwa, wakahudumiwa, wakalazwa na wakasafirishwa mpaka Zanzibar kwa muda muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hiki kinatufundisha kitu, kitu gani tunasoma hapa; kwamba ni muhimu Wizara, Mheshimiwa Waziri Mulamula tutenge fungu la fedha za dharura katika Mfuko wetu wa Maafa ambao unaweza ukahudumia majanga kama haya ambayo hatuyategemei kutokea wakati wowote ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini halikadhalika naomba sasa niende katika diplomasia ya kiuchumi ambayo wenzangu pia wamezungumzia. Diplomasia ya kiuchumi kabla sijazungumzia hapa nafikiri kwanza nipeleke pongezi zangu kwa Mama Samia kwa sababu yeye ameonesha kivitendo na kiuhalisia umuhimu wa diplomasia ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakumbuka kwamba Tanzania ikiwa ni kama nchi inahitaji tuzidi kuifungua. Tayari imefunguka kwa sababu kazi ya kuifungua tofauti na wenzetu wanavyozungumza hapa Tanzania imefunguliwa na toka Rais wa Kwanza Baba Nyerere, akaja Mheshimiwa Mkapa, Ali Hassan Mwinyi, amekuja vilevile Jakaya Mrisho Kikwete, Magufuli na sasa hivi Mama Samia tunaendelea kuifungua nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo kwamba labda nchi ilikuwa imekwama haijafunguka, lakini sasa hivi Mama Samia amekuja katika utaratibu ule mpya ambao mwenzangu amegusia hapa, ile innovative diplomacy kwamba issue ya royal tour imekwenda kuifungua na siyo kuitangaza tu Tanzania, lakini imekwenda kuifungua kiuchumi na ku-unlock zile fursa za maendeleo na kiuchumi ambazo zilikuwa kidogo zimekwama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika hili naomba tu Wizara sasa mama ameanza na mabalozi wetu waichukue hii royal tour katika hatua ya pili. Tungetegemea sasa hivi mwakani tukija tukikutana hapa, tuje tutoe taarifa ya ongezeko la makongamano ambayo yamefanyika katika nchi mbalimbali kutokana na wenzetu hawa mabalozi katika maeneo yao ambayo tutakwenda kupima kutokana na ongezeko la wageni ambao wameongezeka katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuongelea suala zima la ushauri katika maeneo mbalimbali hasa kwa upande wa Zanzibar kwa sababu royal tour bahati nzuri ime-reflect Zanzibar vizuri sana. Sasa wakati royal tour inaongea vizuri kuhusu Zanzibar, nafikiri ni muda muafaka sasa tuongeze wigo wa uwakilishi wa ubalozi na watendaji au Maafisa Ubalozi katika balozi zetu mbalimbali duniani ili tuongeze vivutio au tuongeze wigo wa fedha za maendeleo ambazo zinakwenda Zanzibar kupitia balozi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano hivi sasa watalii ambao wanakuja Tanzania ni kama theluthi moja, hata haifiki vizuri ambao wanakwenda Zanzibar. Sasa kwa kutumia balozi zetu hizi twende tukahamasishe balozi ziweze kufanya kazi za kuweza kusaidia wigo wa kuimarisha maendeleo ya Zanzibar. Lakini pia naomba jambo lingine la muhimu tukaongeza wigo wa wawakilishi katika mikutano yetu ya kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika uwakilishi wa mikutano yetu hii kuna mikutano mingi ambayo Tanzania imeridhia, mfano kuna UNCC-COP yaani Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi, kuna United Nation Conference on Biodiversity, kuna United Nations on Control and Combat Desertification kuna mikutano ya trades ya kibiashara, kuna mikutano mbalimbali ambayo tumeridhia kama Tanzania. Lakini uwakilishi wa Zanzibar hauko vyema na hata tunapokwenda kuwakilisha sijaona kama kuna mkutano ambao Chief Negotiators amekuwa ni Mzanzibar, lakini always Chief Negotiators wanatoka upande wa pili wa Muungano, sasa na hii wakati mwingine kidogo inaminya maendeleo au zile fursa za uchumi kwa upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, naomba hili tukalisimamie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika pengine twende mbali zaidi kwenye masuala ya sera, kwa sababu foreign policy ya Tanzania ina-reflect vilevile United Republic of Tanzania. Sasa iko so generic kiasi kwamba haioneshi Zanzibar hasa inakuwa reflected vipi katika policy ile. Kwa hiyo, naomba Waziri ikiwezekana japokuwa sera yetu ni ya mwaka 2015 lakini tuna uwezo wa kuifanyia marekebisho mapema tukaangalia sasa hivi na Zanzibar ina-fit vipi katika maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye mikutano hii kama kuna Chief Negotiators basi kuwe na Deputy Chief Negotiators ambaye atatoka upande wa pili wa Muungano. Kama Chief Negotiators atatoka Zanzibar basi msaidizi wake atoke Tanzania Bara, halikadhalika kama atatoka upande wa Bara basi msaidizi wake atoke Zanzibar. Lakini halikadhalika katika mabalozi pia siyo lazima tufate utaratibu ambao upo sasa hivi duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile sisi tuna Muungano na Muungano wetu ni very unique, tunaweza tukaamua sasa balozi akawa na msaidizi wake. Kama balozi atatoka Tanzania, msaidizi balozi atoke Zanzibar. Na hii itaisaidia Zanzibar kuweza kujitangaza zaidi na kuweza kutengeneza fursa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kuna mikataba miwili hii ambayo ina reflect kibiashara; kuna mkataba mmoja unaitwa Basel Convention ambao ni International Treaty on Control of Transboundary Hazardous of Waste and their Disposal; halafu kuna mkataba mwingine wa sites ambao ni Convention on International Trade in Endangered Species; mikataba hii yote ni mikataba ya kibiashara. Sasa ombi langu kwa sababu ni ya kibiashara hii, sekta ambazo zinatekeleza hii mikataba zote ziko Tanzania Bara kwa upande wa Basel Conventions sekta ambayo inahusika ni NEMC kwa Bara na kwa upande wa sites ni Maliasili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba tu kwa sababu hizi Mzanzibar akitaka kusafirisha vyuma chakavu au akitaka kusafirisha hizi aina za wanyama ambazo ni adimu inabidi aje Dodoma, aje afuatilie vibali. Kwa hiyo, inapoteza muda na inaingiza gharama zaidi. Naomba tu mikataba ya namna hii tuangalie uwezekano wa kuwa na uwakilishi wa zile institutions za Zanzibar ambazo zinaweza zikatoa vibali vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kama NEMC kuna ZEMA kule Zanzibar inaweza ikafanya kazi hiyo, lakini halikadhalika kwa upande wa Maliasili na Zanzibar vilevile kuna Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka inaweza pia ikafanya kazi hiyo. Kwa hiyo, naomba tukaangalia uwezekano wa kuweza ku-reflect hizi taasisi nazo kwa hii mikataba mbalimbali...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia bajeti ya Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira. Naomba niende moja kwa moja kwenye masuala ya mabadiliko ya tabia nchi.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyokumbuka kwamba, Tanzania imeridhia mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya Tabianchi na halikadhalika katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za mabadiliko ya tabianchi Tanzania mwaka 2000 na kitu Tanzania iliandaa mkakati wa mabadiliko ya tabianchi, lakini kabla ya hapo Tanzania iliandaa mkakati wa kupunguza ongezeko la hewa ukaa kutokana na masuala mazima ya uharibifu na ukataji wa misitu hovyo. Sasa namwomba tu Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje atuambie tu kwa kiasi gani wametekeleza ule mkakati wa mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2012 na wana mpango gani wa kufanya mapitio ya mkakati ule kwa sababu matatizo bado yanaendelea.

Mheshimiwa Spika, halafu pia nataka vilevile kumwomba Mheshimiwa Waziri, kama tunavyojua kwamba, hizi documents zimetumia fedha za Watanzania na kwa kiasi kikubwa inaonekana mara nyingi tukishakuzitayarisha zinabaki kwenye ma-shelf na utekelezaji wake unakuwa ni mtihani. Kwa hiyo, naomba tu hili lifanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, pia kuna suala zima, ambalo wenzangu wameligusia hapa kuhusu fedha za mabadiliko ya tabianchi. Kuna Mifuko hii, Mfuko wa kwanza Mfuko wa Nchi Masikini wa Mabadiliko ya Tabianchi na kuna Mfuko wa GCF wa Green Climate Fund, lakini pia kuna Mfuko wa Adaptation Fund. Mifuko hii yote inasaidia nchi kuweza kutekeleza mikakati yake ya mabadiliko ya tabianchi na kuepukana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Sasa nataka kujua tu kwa kiasi gani Wizara au Ofisi imejitahidi kuweza ku-capitalize hizi fedha na kuweza kutumika. Kwa hiyo, naomba atakapokuja Waziri aje atueleze tu tumepata fedha kiasi gani kwenye Mifuko hii yote mitatu na zimetumika kwa kiwango gani?

Mheshimiwa Spika, kuna sehemu vile vile ambayo ni muhimu pia, niliwahi kuuliza katika swali langu moja hapa Bungeni kwamba, fedha hizi matumizi yake hayako vizuri kimgawanyo baina ya Zanzibar na Tanzania Bara. Imekuwa zaidi ni kama huruma tu kwamba, fedha hizi zitumike Zanzibar na hizi zibaki zitumike Tanzania Bara.

Kwa hiyo naomba Waziri atakapokuja aje atujulishe vilevile kwa kiasi gani fedha hizi zimeweza kutumika upande wa Tanzania Visiwani na upande wa Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, kuna sehemu moja ambayo ni muhimu kuizingatia. Fedha hizi hasa za Adaptation Fund na fedha za Mfuko wa Nchi Masikini kunakuwa kuna allocation maalum ambayo inagawiwa kwa nchi. Allocation ile kama hukuitumia vizuri, basi inakwenda kwa nchi nyingine ambao wako sharp katika matumizi. Sasa nina wasiwasi kwamba, gawio letu la Tanzania hatulitumii vizuri kwa sababu, mara nyingi utaona ufuatiliaji wetu katika…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa. Eeh, sawa nimekuona.

T A A R I F A

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kumpa Taarifa mzungumzaji kwamba, anayosema ni sahihi na sisi kama Taifa tumeshindwa ku-access hizo fund kwa sababu, kuna qualifications; lazima uwe na taasisi ambazo ziko accredited, wakati nchi kama Kenya ina taasisi kama hizo 18 sisi nadhani tuna taasisi moja tu ambayo ni NEMC. Ndio maana tunakosa hizo fedha pamoja na kuwa fungu limetengwa kwa kila nchi. (Makofi)

SPIKA: Nakushukuru kwa intervention hiyo, lakini pamoja na taasisi hiyo moja hata hizo chache ambazo tumepata zinakwama Wizara ya Fedha. Ndio maana Waziri wa Fedha ajiandae siku ya Wizara yake nitakamata shilingi mimi mwenyewe ya mshahara wa Waziri wa Fedha. (Kicheko/ Makofi)

Kabisa, yaani ni kitu ambacho kila wakati nauliza, hivi hata Spika basi mwambieni ili anyamaze. Kwa nini fedha inaombwa inakuja katika nchi yetu, Wizara ya Fedha mnakalia, eti kisa kamati inayoitwa kamati ya nini sijui, nini sijui inaitwa ile, wala sio ya madeni maana yake hii sio deni, hii ni grant; inaitwa kamati ya, sijui kamati gani, ninyi mnaielewa vizuri zaidi, eti haijakaa. Ni kamati ya wataalam ndani ya Wizara ya Fedha, haijakaa.

Fedha zina miaka miwili, zina miaka mitatu, zina mwaka. Hata Mheshimiwa Jafo tunamwonea tu maana hata yeye hazikwami kwake, zinakwama Wizara ya Fedha. Sasa Wizara ya Fedha waipate kabisa mapema, katika jambo hili tunataka badiliko, kwamba mifuko iko, mapesa yako duniani ya kutusaidia mambo ya mazingira, halafu hizo chache zinazokuja kwanza hatupati za kutosha, hizo chache zinazokuja zinakwama Wizara ya Fedha kwa nini? (Makofi)

Tunataka wenzetu wataalam muandike zaidi tupate hizo fedha, hizo fedha ni za dunia nzima ni za mazingira. Tuweze kufaidika na sisi tuna shida kubwa ya mazingira, miti kukatwa hovyo, makorongo kila mahali na matatizo ya fukwe, mmeeleza ninyi wenyewe matatizo mengi sana, tufaidike na hizo fedha. Sio fedha ikifika Wizara ya Fedha, basi ina wenyewe pale Wizara ya Fedha, haiwezekani! Haiwezekani Bunge hili likakubali mambo ya namna hii. (Makofi)

Endelea Mheshimiwa, alikuwa anakuunga mkono kwenye mchango wako. Malizia dakika zako kama bado una ya kusema.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza naikubali Taarifa na Wizara ya Fedha walianza mchakato wa accreditation karibu sasa hivi mwaka wa kumi na mpaka leo hawajafanikiwa kupata accreditation.

Kwa hiyo, ningeomba tu sijui kama hili Mheshimiwa Waziri atakuwa na nafasi nalo, lakini tulikuwa tunataka tupate vilevile ufafanuzi wa Wizara ya Fedha wamekwama wapi?

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, wenzetu nchi mbalimbali…

SPIKA: Wizara ya Fedha au Ofisi ya Makamu wa Rais?

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha wameanza mchakato wa accreditation wa kuweza ku-access fedha za GCF, huu ni mwaka wa kumi na imeshindikana. Tunashukuru Mungu angalau…

SPIKA: Miaka kumi hatujapata hela za Global Climate Facility.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, hatujawahi kupata hata siku moja, labda kupitia kwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa. Kwa hiyo, hili nafikiri Wizara ya Fedha au Waziri wa Muungano, kwa sababu, yeye ndio answerable kwa masuala ya mabadiliko ya tabia nchi, basi ni vizuri wakaja wakatueleza wana mchakato gani kwa sababu, kama alivyozungumza mtoaji taarifa kwamba, kuna nchi zina karibu taasisi zaidi ya tano, sita, ambazo tayari zimeshakuwa accredited na zinaweza ku-access hizi funds, lakini sisi ndio kwanza CRDB na CRDB ilivyo kwa utaratibu wa benki watakopesha hawatatoa msaada moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, wale ambao watakuwa na uwezo wa kuweza kutoa grant moja kwa moja ingekuwa kama Wizara ya Fedha na kule Zanzibar walianza mchakato, lakini mpaka leo nako bado hawajafanikisha. Kwa hiyo, kwa ufupi Tanzania capacity yetu imekuwa ni ndogo na hizi fedha tutakuwa tukiona tu wenzetu wakizitumia, nchi nyingine, lakini sisi tutakuwa hatuna faida nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie mchango wangu katika mchango wa CSOs asasi za kiraia. Kama unavyojua kwamba, asasi za kiraia na asasi za kikanda na za kimataifa nazo zina mchango wa kuweza kutupatia fedha kwa ajili ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi. Kuna tatizo ambalo limekuwa likijitokeza kuna asasi ambazo zina wataalam kutoka nje ambao wamekuwa wakisaidia ku-raise hizi funds, lakini hawa wamekuwa wakipata matatizo ya kuzuiliwa vibali na wengine wameondoshwa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeomba tukazisaidie hizi asasi kuzijengea uwezo na hawa wataalam kutoka nje wakija basi tuwape nafasi kuweza kusaidia kuchangia na ku-raise hizi funds.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa kunipa hii nafasi kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Pia naomba niwashukuru kwa dhati Mheshimiwa Waziri Lukuvi pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri Angelina Mabula na timu yake ya Watendaji ikiongozwa na Ndugu Mary Makondo pamoja na Ndugu Nicholous, Naibu Katibu Mkuu pamoja na timu nzima ya watendaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, hii timu imefanya kazi nzuri sana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na halikadhalika wanaendelea kufanya vizuri. Napenda kuelekeza mchango wangu katika maeneo mawili na kama muda utaruhusu, basi nitaongeza na mawili madogo. Sehemu ya kwanza kabisa napenda kuelekeza mchango wangu katika masuala mazima ya upimaji na umilikaji wa ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyofahamu, wenzangu wengi wamechangia hapa kuhusu umuhimu wa kufanya haraka kupima ardhi yetu ya Tanzania na kuimilikisha ili kuweza kupunguza changamoto ambazo zinakabili ardhi yetu. Kila tukichelewa basi changamoto zinaongezeka na kuna uwezekano, kwa kuwa sasa hivi tuko katika uchumi wa kati wa kiwango cha chini, basi itakuwa Tanzania ni nchi ya mfano ya kuwa na squatters ambao wako katika uchumi wa kati katika daraja la juu. Kwa hiyo, ni vyema tukafanya haraka kuweza kuipima ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu zinatuonesha kwamba kuanzia mwaka 2007 mpaka mwaka 2021 tumeweza kupima ardhi vijiji 2,204 tu. Katika kipindi chote hicho, ni sawa sawa kwamba tumepima vijiji 169 kwa mwaka mmoja na kama trend itaendelea hivi, basi tujue kwamba tunahitaji miaka 58 ili tuweze kukamilisha kuipima ardhi yote ya Tanzania. Yaani ni mwaka 2079 ndiyo tutakuwa tumepima ardhi yote ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 imeelekeza kwamba tuhakikishe tunaongeza wigo wa upimaji wa ardhi ya Tanzania ili angalau kwa kila mwaka tuweze kupima vijiji 826 ambapo kama tutakwenda na trend hiyo, basi itatuchukua miaka 12 kuweza kupima ardhi yote ya Tanzania. Kwa hiyo, tutakuwa tumepiga hatua kubwa kama tutakuwa tumefanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Lukuvi amefanya kazi nzuri sana. Nami nafikiri hatuna zawadi ya kumpa zaidi ya kumsaidia kuweza kufikia lengo la kuipima ardhi ili atakapoondoka katika Wizara hii ionekane kwamba ameacha legacy ya kumaliza au angalau kupunguza tatizo la upimaji na umilikaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa ardhi wamefanya kazi kubwa ikiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo wenzetu wa Halmashauri. Kuna Halmashauri 102 zimejengewa uwezo kati ya Halmashauri zote 135. Ni kazi kubwa. Halikadhalika wameweza kutenga fungu la shilingi bilioni 3.5 na hizi fedha kuzikopesha Halmashauri na Manispaa ili kuweza kuharakisha au kuchochea upimaji wa ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, jambo la kusikitisha, wenzetu wa TAMISEMI nafikiri hawakufanya kama ni core function yao hii ya upimaji na umilikaji wa ardhi. Sasa napenda tuwanasihi sana, tuwaombe na tuwa-task wenzetu wa TAMISEMI waone kwamba suala la upimaji na umilikaji wa ardhi ni core function yao badala ya kuiacha Wizara ya Ardhi kufanya shughuli hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika katika bajeti ambayo amewasilisha Mheshimiwa Waziri hapa, kuna mpango wa kuajiri vijana ambao watakwenda kuongeza wigo wa upimaji wa ardhi. Naomba sana katika ajira hizi, basi tuzingatie sana vyuo vyetu ambavyo vipo Tanzania. Bahati nzuri, namshukuru Mheshimiwa Jafo ameniteua kuwa Balozi wa Mazingira, nashukuru sana kwa nafasi; kwa hiyo, nitumie nafasi hii katika mchango wangu kuweza kunasihi sana Wizara ya Ardhi kwamba wahakikishe kwamba katika upimaji wa ardhi, basi wazingatie masuala ya mazingira kwa sababu ni suala muhimu sana. Bila kuzingatia hilo, inawezekana upimaji huu ukaacha ombwe kubwa sana katika umilikaji na upimaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa Chuo cha Mipango hapa Dodoma wameshatusaidia kazi, kwa sababu nimeangalia ile content yao ya curriculum ya masomo ya certificate, diploma pamoja na degree na masters degree ya kozi ya Chuo cha Mipango wanatoa Urban Planning and Environmental Management Course kuanzia Cheti mpaka Masters Degree. Hawa vijana hawa tukiwatumia, tayari hii kozi imekuwa well contented kwa sababu, masuala ya mazingira yamo ndani humo; watapima, watamilikisha na watazingatia masuala ya ardhi humo ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimesikia kwamba hawa vijana wetu wa kozi ya Mipango katika ajira hizi za Wizara ya Ardhi wanaonekana wao ni kama hawahusiki sana, kwamba wao labda ni sehemu ya daraja la pili au la tatu na zaidi wanazingatia vile vyuo vya ardhi. Napenda tu kuiomba Wizara ya Ardhi, nimeangalia course content yao kwa makini, iko vizuri, imeshiba, mpaka remote sensing imo ndani. Kwa hiyo, nafikiri tutakuwa tunafanya makosa makubwa kama hatutawatumia vijana hawa wanaomaliza Chuo cha Mipango Dodoma katika ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikia vilevile kuna tatizo la Scheme of Service kwamba hawakutajwa huko. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Utumishi akaliangalia hilo kwa haraka kwa sababu tutakuwa tunasomesha watoto kwa gharama kubwa, chuo kile kina walimu zaidi ya 150, tunawalipa Serikali, tunapoteza pesa, halafu itakuwa hatujawafanyia haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haraka haraka kuna suala la wenzetu hawa wanaokwenda kupima visiwa. Naomba tu, visiwa 289 ambavyo vimepimwa, vimekuwa identified, basi hiyo ni step ya kwanza, naomba tuendelee na hatua ya pili kwa kuweza kutayarisha Mpango Kazi na vilevile kutayarisha utaratibu wa kuangalia resource mapping ili tuweze kuona tunaviendeleza vipi kwa sababu kuna uharibifu mwingi wa mazingira katika hivi visiwa vidogo vidogo ambavyo vimo katika maziwa na vilevile katika maeneo ya bahari.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia jambo moja kumalizia mchango wangu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuwasilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuweza kunipa fursa hii kuweza kuchangia katika bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2021/ 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Allah Subhana Wataalah kwa kuweza kutujaalia uzima na kuweza kuendelea na bajeti katika kipindi hiki cha lala salama. Hali kadhalika ningeomba vile vile kumpongeza sana sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wake wa Wizara ya Fedha wakiongozwa na Komandoo Katibu Mkuu Tutuba kwa kazi nzuri ya ukweli ambayo wameweza kuifanya. Kwa kweli, bajeti bajeti hii kama ambavyo wenzangu wamezungumza imezingatia hoja za Wajumbe wa Bunge hili Tukufu na ndiyo maana imekuja kuwa ni bajeti kielelezo, bajeti ya mfano, bajeti ya mkakati ambayo inakwenda kutuvusha katika uchumi ule wa kiwango cha chini tunakwenda katika daraja la juu sasa uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeanza tu kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Alhamis tarehe 10 wakati anawasilisha bajeti speech yake hapa siku ile ile kama nchi tano zilikuwa zikiwasilisha bajeti zao zile za nchi za Afrika Mashariki. Sambamba na hilo pia Zanzibar, siku ileile Alhamisi tarehe 10 iliwasilisha bajeti yake, Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Sasa Mheshimiwa Waziri nikuombe hapa kabla sijaenda kwenye michango ya moja kwa moja kwamba ukimaliza bajeti hii tukimaliza Bunge hili, ningekuomba sana ukae na Waziri wa Fedha wa Tanzania Visiwani (Zanzibar) pamoja na Waziri anayeshughulikia masuala ya Muungano kule Zanzibar, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, muweze kukaa kuangalia vipaumbele vya bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambavyo vina mnasaba wa kuangalia ushirikiano ambao unahitajika kwa upande wa Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hili kwa sababu mara nyingi bajeti ya Zanzibar kuna maeneo ambayo kwa kweli kama haikupata msukumo wa Waziri wa Fedha pamoja na Sekta za Muungano huku Tanzania Bara basi bajeti ile inakuwa ina kasoro na mambo mengi yanakuwa hayawezi kutekelezeka vyema. Kwa hiyo, naomba tu Mheshimiwa Waziri hili ukali-note ukimaliza usisubiri upate mualiko, mtafute mwenzako Waziri wa Fedha muweze kukaa kitako pamoja muangalie vipaumbele ambavyo vinahitaji ushirikiano muweze kuvitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala muhimu ambalo pia ningependa kuligusia. Wakati Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Magufui Mungu amrehemu anazindua Bunge la 12, alisisitiza sana ushirikiano wake kwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na hili kwa kweli mimi siiti ile ni hotuba ya kulizindua Bunge, naiita ni hotuba ya kutuusia kwa sababu kama alijua kwamba anaondoka basi niwausie au niwaase vipi Watanzania wakati naondoka waishi vipi hasa katika masuala ya Muungano. Hali kadhalika wakati anamuapisha Waziri Mkuu kule Chamwino pia alimkaribisha Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kuweza kueleza machache na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar alitumia muda mwingi kuweza kuomba ushirikiano na kuungwa mkono na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, ningependa tuzidishe kuziunga mkono zile sekta na taasisi za Zanzibar katika masuala ambayo yanahitaji ushirikiano wa Kimuungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna Sekta ya Kilimo na Mifugo. Sekta hii siyo ya Muungano lakini kuna changamoto kama wenzetu wa Mambo ya Ndani hawakuisaidia, basi wananchi wataendelea kupoteza nguvu zao bure na tija ya kilimo na mifugo haitaweza kupatikana Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kwa kipindi kirefu na hata Rais wa Zanzibar wakati ananadi sera za Chama cha Mapinduzi aliahidi hili kwamba atajitahidi kuhakikisha kwamba kero za wizi wa mazao ya kilimo na mifugo inapungua. Kwa kweli, kwa tatizo kubwa la wizi wa mifugo na mazao ya kilimo Zanzibar na hata nafikiri Mheshimiwa Abdallah Mwinyi ni shahidi. Jimboni kwake kule kuna mwannachi wake mmoja alipoteza maisha kwa kulinda nazi. Amelinda nazi wakati mtu yuko juu kwenye mnazi anaangua basi yeye wakati analinda kuna mwizi mwingine akaja akampiga kisu na kumuua hapo hapo. Sasa kwa kweli ningeomba tu katika bajeti inayokuja Wizara ya Mambo ya Ndani ije ituambie mkakati ambao imeutumia katika kipindi hiki kuondoa tatizo la wizi wa mazao ya kilimo na mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wameondokana kabisa na suala zima la ufugaji Zanzibar. Mtu alikuwa na mbuzi au ng’ombe wake watano, kule ufugaji wetu sio mkubwa sana lakini zizi zima limeenda kuchukuliwa wakachinjwa hapo hapo. Sasa nataka kuwauliza, hivi Jeshi la Polisi liko wapi? wakati watu wanajitahidi kulima wewe shamba lako zima unaenda asubuhi limeshavunwa lote, kama muhogo umeshavunwa wote. Kama viazi vimeshavunwa zote, kama nazi zimeshaanguliwa zote. Kwa hiyo, ina-disappoint au inakatisha tamaa wakulima kwa upande mmoja. Kwa hiyo, Wizara ya Mambo ya Ndani lazima tuje na mkakati tutalisaidiaje hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kwenda Misri, wenzetu kule ukitembea ndani ya dakika moja utakutana na Askari kwa sababu wanafahamu hali yao. Sasa na sisi Zanzibar Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani lazima uje na mkakati wa kulisaidia hili. Ni miongoni mwa kero ambazo Mheshimiwa Rais wa Zanzibar ameahidi kwenda kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Donge, nafikiri kama ningekuwa Tanzania Bara tungeweka miongoni mwa Mikoa mitano ambayo inalisha nchi. Jimbo la Donge ni miongoni mwa Jimbo ambayo Mungu kayajaalia kuyapa rutuba ni miongoni mwa maeneo ambayo ni big fertile land lakini kwa kweli kumekithiri wizi kiasi kwamba hata ukilima basi huna uhakika wa kuvuna. Mazao yanavunwa usiku, yanavunwa machanga kiasi kwamba tija ya kilimo na mifugo haionekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nazungumzia hilo, ningependa vile vile kuzungumzia suala jingine la kuzishika mkono Sekta za Zanzibar. Zanzibar tuna miundombinu ya barabara ambazo ni main road hazizidi kilometa 700, Zanzibar nzima yaani hiyo. yaani ukitoka Mjini Zanzibar kwenda Nungwi, Mjini Zanzibar kwenda Makunduchi, Mjini Zanzibar kwenda Chwaka na ukitoka Wete kwenda Mkoani, Wete kwenda Makangale, Wete kwenda Micheweni ni kilometa zisizozidi 700. Lakini tumekuwa tukihangaika na barabara hizi kwa miaka sasa hivi, toka mapinduzi hatujaweza kumaliza kwa sababu hali ya Zanzibar kama hatukuishika mkono kuweza kuikamilisha vizuri ile miradi ya kimkakati ni ngumu. Kwa hiyo, ningeomba sana hii miradi ya wahisani ambayo inapitia katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuiangalie sana Zanzibar kwa sababu kinyume chake ina-disappoint maendeleo ya Zanzibar kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Kwanza aliisaidia Zanzibar kuipa eneo Makurunge kule. Lile eneo akasema chukueni fugeni ng’ombe ili Zanzibar iondokane na matatizo ya nyama ya ng’ombe na maziwa. Ile ni spirit ambayo sisi hivi sasa lazima tuiige. Kwa hiyo, naomba Mawaziri na uongozi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivi sasa tuige spirit ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Kwanza ya kupenda kuisaidia Zanzibar kuwa ni kama economic hub kwa East Africa. Tukiitengeneza Zanzibar ikawa ni economic hub itakwenda kuisaidia Tanzania Bara vilevile. Lakini matatizo ya Zanzibar vilevile yatakwenda kuhatarisha na kuongeza changamoto za Muungano vilevile. Kwa hiyo, ningependa tukalisaidia hili nalo kwa sababu lina umuhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Waziri wa Fedha amesaidia zile pesa za Majimbo zile Milioni Mia Tano ukisaidia Zanzibar hutapoteza kitu kwa sababu ndiyo ile spirit Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Kwanza ameifanya kwa kuipa Zanzibar ardhi ndani ya Tanzania Bara. Wewe ukipeleka zile fedha Milioni Mia Tano ni ile ile spirit ambayo ameifanya Mwalimu Nyerere kipindi hicho kwa kuipa Zanzibar ardhi huku.

Kwa hiyo, utakuwa hujafanya kosa kubwa Mheshimiwa, iga huo mfano ili na wewe uache legacy ambayo Zanzibar itakukumbuka miaka 50 inayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kumalizia kuhusu fedha za mifuko. Nimeshukuru sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuweza na mimi kutoa mchango wangu katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi, lakini kadhalika ningependa kwanza kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake Ndugu Ulega, kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika Wizara hii. (Makofi)

Ningependa kuwapongeza watendaji wa Wizara hii kwakweli wamefanya kazi nzuri na ndiyo maana sasa hivi maeneo mengi yameanza kuimarika hasa yale ambayo yamezalia samaki hasa katika masuala ya matumbawe au coral leaves. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kuelekeza mchango wangu katika maeneo mawili makubwa; la kwanza ni kuhusu suala la usafirishaji wa biashara ya dagaa ambayo jana niliuliza swali langu, lakini la kwanza ningependa kumpongeza vilevile Mheshimiwa Ulega kwa kweli toka jana ameanza kulifuatilia hili suala na imenitia moyo sana na huu ndiyo uwajibikaji haswa wa Serikali hii ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kusisitiza tu kwamba tusiwategemee tu sana watendaji wetu wakati mwingine wanakuwa wanatuangusha kwa sababu wanaporipoti inakuwa sivyo wanavyofanya, kwa hiyo nashukuru hili ambalo tulikuwa tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia ningependa tu kuwaomba wenzetu watendaji hawa wakajaribu kuwasaidia hawa wafanyabiashara na dagaa kwa sababu ni nieneo ambalo linaajiri watu wengi sana na hasa wanawake, na hivi sasa biashara hii imekuwa inafanywa sana na wageni ambao wanakwenda mpaka kwenye madiko na kununua dagaa; ingekuwa vyema kama tukawapa-incentives watu wetu wakaweza kufanya biashara wao moja kwa moja na wakasafirsha dagaa badala ya wageni kuja moja kwa moja kwenye mwalo na kununua dagaa.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ningechangia kuhusu masuala mazima ya maeneo ya mazima ya maeneo ya mazalia ya samaki hasa masuala ya mikoko au mangroves yaani mikandaa kwa jina lingine. Kuna uharibifu mkubwa sana katika maeneo ya mikoko au mikandaa, ukaenda Rufiji na maeneo ya kanda mbalimbali za fukwe za bahari, mikoko imekuwa ikiathirika sana na nimaeneo ambayo ni mazalia makubwa ya samaki. Sasa hapa ningewaomba wenzetu wa uvuvi mkashirikiana na Wizara na Maliasili kwa sababu ingawa mikoko au mikandaa ni miti, lakini ni mazalio na ni malisho ya samaki.

Mheshimiwa Spika, sasa tukiwaachia wenzetu wa Maliasili peke yao, sisi tukaendelea zaidi kwenye masuala ya uzalishaji wa samaki au uvunaji na biashara moja kwa moja basi tutakuwa tunaacha eneo muhimu ambalo linaweza likasaidia. Kwenye Mradi wa MANCEP ulifanya kazi nzuri ya kuendeleza mikandaa, lakini Mradi wa SWIOFish bahati mbaya umeliacha hili eneo haukuliendeleza, kwa hiyo hizi resources tunavyozipata tuangalie maeneo haya kwa sababu nayo ni maeneo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Semesi katika mwaka 1992 alifanya utafiti wa mikoko au mikandaa na akaandaa management plans ikiwemo uzalishaji na ulishaji au malisho ya samaki. Lakini bahati mbaya hizi management plan zote ziko kwenye ma-shelf, hazikufanyiwa kazi toka mwaka 1992 mpaka hii leo. Ningeomba wenzetu wa uvuvi mkaziangalia hizi management plans na tukaangalia tukazi-review ili kuona uwezekano kuziendeleza tujue tunaanzia wapi katika kuendeleza mikandaa au mikoko iwe ili iwe ni sehemu salama zaidi ya kuweza kuwasaidia kuzalisha samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho ningependa kugusia vilevile suala zima la mabadiliko ya tabia nchi. Mabadiliko ya tabia nchi yanaathiri sana wafugaji na kipindi cha ukame maeneo mengi ya maji na malisho yanaathirika na kuna miradi kama Mradi wa Decentralize Government Finance ulianzishwa ili kuzisaidia Halmashauri kuweza kusimamia maeneo ya malisho na kuzitafuta fedha kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji. Sasa mradi ule umemalizika mpaka hii leo zile jitihada hatukuziendeleza, kwahiyo miradi hii inakuwa ni mizuri lakini sasa stability inakuwa haipo. Kwa hiyo ningeliomba tu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, na mimi nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhana Wataalah kwa kutujaalia na kutupa afya njema na kuendelea na Bunge sasa hivi karibu mwezi wa pili.

Lakini pia nikushukuru wewe kwa kuweza kunipa hii nafasi kuweza kutoa mchango wangu muhimu katika Wizara hii muhimu ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Hali kadhalika niwashukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri Sheikh Mbarouk pamoja na watendaji wa Wizara hii kwa kweli wamekuwa wakifanya kazi nzuri na tumeanza kuona mabadiliko chanya katika maeneo mengi. Kwa mfano, kule Zanzibar hivi sasa hivi tayari tuna mchoro wa bandari na nafikiria kwamba Wizara yetu hii itafanya hima kuweza kuhakikisha kwamba utekelezaji wa ujengaji wa bandari unafanyika haraka ili yale matokeo chanya yanayokusudiwa kutokana na bandari zile basi yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuchangia mchango wangu katika maeneo mawili makubwa; la kwanza ambalo Mheshimiwa Fakharia amelianza ni kuhusu ofisi yetu ya Zanzibar. Kwa kweli Ofisi ya Zanzibar kama alivyosema Mheshimiwa Fakharia, sio ofisi kwa kweli na ni nyumba ambayo ni ya muda mrefu sijui kama tulijenga au tulihamia tu lakini haina hadhi ya kuwa ni Ofisi ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Ofisi ile imechoka na hivi sasa tuna taarifa kwamba inafanyiwa marekebisho. Sio kujengwa mpya, inafanyiwa marekebisho.

Kwa hiyo, ningewaomba tu wenzetu wa Wizara kwa kweli aidha, sahihi kama tunafanya marekebisho au matengenezo haya ya dharura basi tuendelee na matengenezo ili tuweze angalau kupata pa kuanzia, lakini tuwe na utaratibu wa muda mrefu wa kuangalia uwezekano wa kujenga ofisi mpya aidha pale kwa sababu pale sasa hivi pameshakuwa kama ni museum, ni eneo la mji lile sasa hivi. Kwa hiyo, sio mbaya tukatafuta eneo nje ya mji, kiwanja kizuri tukaenda tukajenga ofisi kubwa ambayo itakuwa na hadhi ya Ofisi ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyojua kwamba ile ofisi ndiyo sehemu kubwa ambayo mabalozi wakienda Zanzibar ile ndiyo sehemu yao kubwa ya kufikia. Lakini pia hata viongozi mbalimbali wenye hadhi ya Kimataifa ile ndiyo ndiyo center yao ya kuweza kufikia, lakini sasa hivi viongozi hawa wengi wanafikia hotelini. Kwa hiyo, ningeomba Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri Sheikh Mbarouk tukajitahidi katika kipindi chenu hiki Inshallah tukaweza kushuhudia kwamba angalau katika kipindi hiki cha miaka mitano tunapata eneo na miaka mitano inayokuja tunajiandaa kwa kujenga ofisi yenye hadhi ya kimataifa ambayo itakuwa ina-represent Umoja wa Mataifa kule kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala zima la uratibu na taratibu za ofisi zetu za kikanda na za kimataifa. Kama tunavyojua kwamba kwamba Zanzibar ni kisiwa na inategemea sana ndugu zao wa upande wa pili wa Muungano kuweza kuwawakilisha katika mambo ya kikanda na ya kimataifa. Lakini kidogo kuna changamoto mbili kubwa ambazo zinakabili katika maeneo haya; changamoto ya kwanza ni uwezo wa taasisi za Zanzibar kuweza ku-access fursa za mbalimbali zinazopatikana katika maeneo ya kikanda na maeneo ya kimataifa.

SPIKA: Hebu rudia hapo hujaeleweka.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, uwezo au capacity ya Taasisi…

SPIKA: Tangu ulipoanzia kwamba Zanzibar…

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, naam!

SPIKA: Rudia kidogo hapo ulipoanzia hoja yako.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, nasema kwamba changamoto mbili ambazo zinakabili ya kwanza ni uwezo wa taasisi za Zanzibar kuweza ku-access fursa zinazopatikana katika maeneo ya kikanda na maeneo ya kimataifa. Nitatoa mfano, ya kwanza kama tunavyojua kwamba kuna mifuko ya fedha mbalimbali, lakini hali kadhalika kuna balozi zetu hizi kama mfano ukienda Ubalozi wa Japan kuna Shirika la Maendeleo la JICA, ukienda Shirika kama USAID, kuna mashirika mbalimbali ya kikanda, kuna ADB lakini ningependa kuwashauri wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje wakatusaidia kutujengea uwezo zile taasisi za Zanzibar kuweza kutafuta hizi fursa kwa sababu sasa hivi kuna malalamiko mengi, lakini ukiangalia wakati mwingine changamoto vilevile sio kama iko katika upande wa Wizara peke yenu, lakini pia wale wenzetu wa Zanzibar bado uwezo wao sio mzuri sana kuweza ku-access hizi fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ni urasimu au wenzetu wa upande wa pili kwa sababu kama tunavyojua kwamba Zanzibar hata kama ni jambo sio la Muungano kwa mfano jana mwenzangu Mheshimiwa Ravia alizungumzia hapa suala la michezo. Suala la michezo sio suala la Muungano lakini tukitoka nje ya nchi ni lazima tuweze kuungana. (Makofi)

Sasa tukienda kwenye masuala ya CAF, FIFA lazima tuwe tuko pamoja. Sasa wenzetu wa upande wa pili wa Muungano kama ni Wizara hizi zote lazima washike mkono wenzetu wa Zanzibar vizuri, kwa sababu mimi mwenyewe nimeshawaji kupata changamoto kipindi fulani. Kulikuwa kuna mradi ambao nilikuwa nauratibu Zanzibar kule na nikaomba mradi mimi mwenyewe ambapo ilitangazwa call for proposal, nikaomba na ile call ilikuwa call ambayo ni competitive ya kupambana mwenyewe. Tukaomba ile pesa na tukawa tumeshapata, lakini wakati tunatafuta zile fedha ilikuwa lazima kwa sababu pesa tumezipata through ADB lazima Waziri wa Fedha wa Muungano ndiyo asaini ule mkataba. Ilichukua miezi sita nahangaika kutafuta signature ya Waziri wa Fedha, mpaka tulipomtumia Waziri wa Fedha wa Zanzibar pia naye alishindwa kuweza ku-fast track kuweza kupata signature ya Waziri wa Fedha haraka. (Makofi)

Sasa wakati mwingine changamoto zinakuja kwa sekta za Bara, Wizara za Bara hizi zinakuwa zinashindwa kuzishika mkono zile taasisi za upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, ningependa tujitahidi fursa kuweza kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kumaliza kwa upande wa mikutano ya kikanda hasa ya Afrika Mashariki. Kuna mikutano ambayo tunashiriki sisi kwa upande wa Tanzania, lakini kuna wenzetu wa Tanzania Visiwani inabidi tuwaalike tuwe nao pamoja lakini taarifa hizi zinakwenda Zanzibar late, inawezekana mkutano uko kesho taarifa zinakwenda leo.

Pia inawezekana mkutano ule unafanyika either Arusha, Kigali, Entebbe na kadhalika katika Afrika Mashariki au SADC. Lakini taarifa zinakuja late, Wazanzibari wanashindwa kujiandaa mapema na ukienda kwenye mikutano wanakuwa ni wasikilizaji tu hawana mchango wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna tatizo la kwamba kwa sababu hakuna maandalizi inawezekana taarifa zile zikienda hata bajeti kule hakuna ya kuweza kumpeleka mwakilishi. Pia kuna mikutano ya maandalizi ambayo aidha inafanyika Dodoma au Dar es Salaam, mikutano ile mara nyingi Wazanzibari hawahudhurii kwa sababu hawapati taarifa mapema na hata wakija kwa sababu inaonekana ni gharama matokeo yake inakuwa ni Tanzania Mainland peke yao ndiyo wanahudhuria kwenye vile vikao na inakuwa havina tija kwa upande wa Zanzibar. (Makofi)

Kwa hiyo, ningeomba tu Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na Wizara kwa ujumla wakajitahidi kuondoa urasimu vile vile kusaidia kujenga uwezo Zanzibar na kuwashika mkono ili waweze kuweza kupata hizi fursa au kuzi-access fursa za kikanda na za kimataifa. Ahsante nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Ndumbaro pamoja na Naibu wake, Mheshimiwa Mary, pamoja na watendaji wa Wizara hii wakiongozwa na Dkt. Allan Kijazi, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo amekuwa akiifanya. Kwa kweli wameacha alama katika kipindi kifupi hiki ambacho wameikamata hii Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Wizara ya Maliasili na Utalii katika kipindi cha miaka mitano iliyopita wamefanya kazi kubwa sana. Nami ni shahidi, tumeweza kutembea katika baadhi ya hifadhi na tumeona mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na kuona hivi sasa wanyama wameongezeka sana na wale tembo ambao ilikuwa hata ukienda kwenye hifadhi zetu kuwaona ni nadra, basi hivi sasa wamekuwa ni wengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeelezwa hapa kwamba kabla ya kupata Uhuru tulikuwa na tembo waliokuwa wakifikia 200,000 lakini hivi sasa tembo wamepungua mpaka kufika 40,000. Hivi sasa wameongezeka mpaka wamefika karibu 60,000. Haya kwa kweli ni matokeo mazuri ya uhifadhi ambao unafanywa na wenzetu hawa wa Maliasili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, tumekwenda kwenye Hifadhi ya Ruaha, wenyeji wametueleza pale kwamba kwa miaka kumi iliyopita Mto Ruaha kilikuwa kinafika kipindi maji yanakata karibu miezi miwili au mitatu, lakini hivi sasa Mto Ruaha kwa mwaka uliopita haukukata maji hata mara moja, umeweza kutiririsha maji kwa mwaka mzima. Haya ni matokeo ya juhudi za uhifadhi ambazo wenzetu wamekuwa wakizifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wenzetu hawa wamefanya kazi nzuri hata katika masuala mazima ya uhifadhi wa maliasili, yaani miti. Kwa sababu wenzetu wa TFS hivi sasa ukiangalia mapato ambayo wameweza kuyapata katika kipindi kilichopita pamoja na maradhi ya Covid, lakini wamevunja rekodi katika vipindi vyote vilivyopita. Yaani wakati sekta nyingine zinahangaika kwa ukusanyaji hafifu wa mapato, wao wameweza kufanya kazi nzuri na kuweza kukusanya mapato kwa kiasi kikubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kidogo katika suala muhimu la usimamizi shirikishi wa maliasili zetu nchini. Kama tunavyojua, juzi na jana, nimesikiliza kwa makini wakati michango ikitolewa katika Wizara za Maji na Nishati, tumekuwa tukizungumzia sana kuhusu uhifadhi na uvunaji wa rasilimali zaidi, yaani vipi tutapata nishati, vipi tutaunganisha tupate umeme? Ila hatuangalii na tija: Je, haya maji sustainability yake itaendelea kuwa vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukizungumza masuala yote ya uhifadhi, ningependa tu kuwaomba wenzangu kwamba tuka-adopt ile approach ile integrated natural resources management, yaani usimamizi shirikishi. Tusiwaachie watu wa maliasili tu kwamba ndiyo wahifadhi rasilimali za misitu au rasilimali za wanyamapori. Kwa sababu tukizungumza maji wanategemea vilevile sustainability ya hifadhi ya misitu. Tukizungumza nishati wanazitegemea vilevile sustainability wa hifadhi wa misitu; tukija utalii, wanategemea vilevile sustainability ya rasilimali za misitu, hata tukija kwenye masuala mazima ya food security, pia kama hatukuweza kupata kuni na makaa katika njia endelevu, basi hata usalama wa chakula nao hautakuwa mzuri. Kwa hiyo, lazima tuje na usimamizi shirikishi ambao utajumuisha sekta zote hizi muhimu ili tuweze kuhakikisha kwamba maliasili zetu zinahifadhika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunakuja hapa tunazungumza kwamba tunataka kuifanya Tanzania kuwa ni nchi ya tembo. Hii siyo kauli nzuri sana kwa sababu, kama tunavyojua hivi sasa tuna tembo 60,000, huko nyuma tulikuwa tuna tembo zaidi ya 200,000 na tuliweza kuishi katika hali endelevu zaidi na wanyama hawa. Kwa hiyo, nafikiri ni pahala pa kujipanga kisekta tukashirikiana katika uhifadhi wa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunazungumza kuhusu Bwawa la Mwalimu Nyerere. Tunategemea pale tukapate Megawatt za umeme karibu 2100, lakini tunategemea kuanzia mwezi Aprili tuwe tumeshalijaza maji lile bwawa; na kuanzia mwezi Juni tunategemea tuanze kuchaji na kupata umeme. Wakati nazungumzia kuhusu kupata maji, hatuzungumzi kuhusu haya maji, potential threat yake ikoje kama maji hayatatiririka vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tuwa- support wenzetu wa maliasili ili wahifadhi vyanzo vya maji ili kuhakikisha kwamba bwawa letu la Mwalimu Nyerere linaweza kupata maji katika hali endelevu na kuweza kupata matunda ambayo tunakusudia. Kinyume na hivyo, tunaweza tukazungumza hapa bila kuangalia zile threats ambazo zinakabili suala hili zima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la taaluma kuanzia kwa Wabunge na wanajamii. Kwa kweli kinachoonekana ni kwamba elimu ni hafifu. Kwa hiyo, naomba wenzetu wa maliasili tujipange vizuri kuweza kuelimisha kuanzia wanajamii hapa pamoja na Wabunge kuweza kupata taaluma muhimu kwa sababu michango tunayokuwa tunaitoa hapa wakati mwingine ni kutokuwa na taarifa za kutosha katika masuala mazima ya uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa mfano mdogo tu; kule Zanzibar miaka ya 1970 tulikuwa na Chui zaidi ya 1,000 na kidogo hivi, lakini hivi ninavyokwambia Chui wale wamemaliza na hakuna tena hivi sasa. Chui wameisha. Pia tulikuwa na Paanunga zaidi ya 6,000 kipindi cha miaka ya 1970. Hivi sasa Paanunga wamebakia 300 tu Zanzibar nzima. Kwa hiyo, unaweza kuona athari ya viumbe kuweza kutoweka. Tukifanya masihara tutapoteza viumbe kwa kutokuzingatia uhifadhi sahihi na kutokuwapa nguvu wenzetu wa maliasili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie suala la mifuko ya fedha. Kwa kweli mifuko ya fedha tumeamua kwamba fedha zikusanywe na watu wa TRA na ziende kwenye mfuko mkuu na baadaye ndizo zirejee tena kwa wenzetu hawa waweze kutumia. Vilevile naomba tu kutoa indhari, wenzetu katika kipindi hiki cha fedha wamepokea asilimia 32 tu ya fedha. Kwa hiyo, kama tutaendelea na utaratibu huu, zile kazi ambazo tumezipanga hazitaweza kufanyika.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala kwa kutujaalia afya njema, hali kadhalika nikushukuru na wewe kwa jinsi unavyoliendesha Bunge hili na hata sisi wa form one tumekuwa tunajisikia vizuri wakati tukitoa michango yetu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji wake mzuri pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Masauni hali kadhalika ningependa vilevile kuwapongeza Watendaji wa Wizara hii ya Fedha wakiongozwa na Mtendaji Mkuu Katibu Mkuu Ndugu Emmanuel Tutuba Rafiki yangu ambaye kwa kipindi fulani tulikuwa tuko pamoja kule Ufaransa tukishughulikia masuala mazima ya mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba wakati nikiwapongeza kwa jitihada kubwa alizokuwa akizifanya lakini pia ningeomba nitoe mchango wangu katika maeneo mawili makubwa, kwanza ni kuhusu masuala mazima ya fedha za maendeleo au miradi ya maendeleo hususan katika fedha za maendeleo kwa kupitia wadau wa maendeleo au wahisani.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kuna tatizo changamoto kubwa ambayo imekuwa ikiikabili hii miradi ya maendeleo na zaidi ni ucheleweshaji wa fedha kupitia Wizara ya Fedha. Kama tunavyojua kwamba tumefanya mabadiliko kidogo hivi sasa tunazitaka taasisi au sekta mbalimbali kwenye utararibu mzima wa fedha za wahisani zipitie Wizara ya Fedha kwa ajili ya kuratibiwa na ndipo ziende katika sekta husika kwa ajili ya utekelezaji wa miradi. Lakini kwa kweli kumekuwa na tatizo kubwa la ucheleweshaji na ambalo limekuwa liki-disappoint au likikatisha tamaa wahisani na pia watekelezaji wa miradi. Kwa mfano, kuna mradi wa equal PRC ambao ulikuwa ukitekelezwa na wenzetu wa Chuo cha Misitu Olmotony, mradi ule kwa bahati nzuri mimi nilikuwa ni miongoni mwa Board Member badala ya kutekelezwa mradi ule kwa miaka mitatu mradi ule ulitekelezwa kwa miaka minne na nusu na sababu kubwa ilikuwa ni ucheleweshaji wa fedha kupitia Wizara ya Fedha, kwa hiyo ningeliomba sana Mheshimiwa Waziri eneo hili akalifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi sasa kuna mradi ambao wenzetu wa NEMC na niwapongeze kwa hili, wenzetu wa NEMC wameomba miradi miwili, mradi mmoja wa Tanzania Bara ambao utatekelezwa kule Bunda na mradi mwingine ambao utatekelezwa Zanzibar unaitwa mradi wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi kwa jina la Climate Change Resilience for Coastal Community for Zanzibar. Sasa mradi huu una jumla ya dola milioni moja na mkataba wake umesainiwa tarehe 2/7/2020 na hapana mkataba wake umepitishwa rasmi na Bodi ya Adaptation Fund tarehe 2/7/ 2020 halafu mkataba rasmi umesainiwa taehe 7/11/2020 na fedha zimeingizwa katika akaunti ya NEMC ambayo iko BOT mwezi 11 mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ni mwezi wa Tisa fedha ambazo zimeingizwa kwa ajili ya utekelezaji wa mwaka wa kwanza wa mradi bado fedha hazijakuwa released kwenda kwenye sekta husika na kwa ajili ya matumizi au ya utekelezaji. Delay hii itatugharimu baadaye tuje tuombe no cost extension kwa ajili ya utekelezaji wa mradi kwa uzembe wetu sisi wenyewe.

Mheshimiwa Spika, Katibu Mkuu unakumbuka wakati tuko Ufaransa mwaka 2015 nchi masikini zilivyokuwa zikihangaika kutetea mfuko wa Adaptation Fund na unakumbuka vilvile nchi masikini zimekuwa zikihangaika kuweza kuomba fungu la Adaptation Fund liongezwe ili ziweze kusaidia kukabiliana na kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi. Sasa kama leo fedha zinaingia mwezi wa Tisa hivi sasa bado hazijakuwa released kwa ajili ya kwenda kutekeleza miradi nafikiri hapa itakuwa hatujifanyii sisi haki na vilevile hatufanyi haki hawa wenzetu wa NEMC ambao wamehangaika kuweza kuzitafuta hizi fedha na zimeshafika nchini fedha, tuna delay kuzitoa kwa ajili ya utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapa ningeliomba vilevile kupeleka mchango wangu kwenye suala zima la Kamati ya Madeni. Kuna Kamati ya madeni ambayo iko Wizara ya Fedha ndiyo inayoratibu na inajumuisha wadau mbalimbali, lakini kuna shida kubwa napo hapa kwa sababu imekuwa miradi mingi au bajeti nyingi ambazo zinapelekwa Wizara ya Fedha za kupitia wahisani wa maendeleo hawa, unaambiwa kwamba mradi hauanzi kwa sababu Kamati ya madeni haijakaa sijui utaratibu wa hii kamati ya madeni ukoje kwasababu hata ile miradi ambayo ni grant siyo madeni lakini pia unaambiwa tusubiri Kamati ya Madeni ikae.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka mwaka 2014 binafsi nilikuja Wizara ya Fedha mara saba kufuatilia mradi wa ADB (African Development Bank) mabadiliko ya tabianchi na kila nikija kuuliza naambiwa Kamati ya Madeni haijakaa, huu mradi ulikuwa una dola laki 360 tu ni fedha ndogo mno, kiasi kwamba mpaka unaambiwa kwamba mpaka Kamati ya Madeni ikae na inaweza ikawa miezi mitatu miezi sita haijakaa. Kwa hiyo, ningeomba tu hii kamati ya madeni nayo vilevile tupate utaratibu ukoje, hizi fedha za ruzuku kwa nini tusiziondoe kwenye Kamati ya Madeni tukazitafutia utaratibu mwingine wa kuweza kuzipitisha badala ya kutumia Kamati ya Madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naiomba Wizara ya Fedha kwa sababu fedha kama hizi laki 350 hivi mpaka zije zipate signature ya Waziri wa Fedha Tanzania Bara? Hatuwezi tukaweza tuka-apportion haya madaraka kwa Waziri wa Fedha Zanzibar fedha kama hizi ndogo akasaini yeye yakaisha? Kwa sababu signature ya Waziri wa Fedha ilituchukua karibu miezi sita! signature tu ya Waziri wa Fedha unakuja Tanzania Bara na kurudi bado signature hujaipata sasa kwa nini tusiangalie uwezekano wa hizi fedha za ruzuku na hasa kama asilimia ndogo kama hii laki 350 tusiangalie uwezekano Waziri wa Fedha Znzibar akasaini badala ya kutumia Waziri wa Fedha wa Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeliomba vilevile kuendelea na suala moja la accreditation. Niliwahi kuchangia hapa katika Bunge lako Tukufu kuhusu suala zima kwamba Wizara ya Fedha walikuja na suala la registration karibu miaka 10 iliyopita, mpaka leo hii Tanzania ukiondoa CRDB ambao wamejitahidi kwa upande wao lakini hakuna taasisi ya Serikali ambayo imeweza kupata accreditation kwa ajili ya mfuko wa mabadiliko ya tabianchi wa dunia (Green Climate Change Fund). Kwa hiyo, ningeliomba Waziri wa Fedha atakapokuja hapa aje atuambie wapi Wizara ya Fedha wamekwamba, kwa sababu wenzetu Ethiopia Wizara ya Fedha sasa hivi imekuwa accredited na inaweza kuomba fedha moja kwa moja kwenye huu mfuko wa GCF.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika Rwanda Wizara ya Kilimo wao wameomba wamekuwa accredited na wanaweza kuomba fedha moja kwa moja Mfuko wa GCF. Tanzania tumekwama wapi? Suala hili zaidi ni suala la uzalendo, kwa sababu bila kujituma, bila watu kuwa dedicated, kuwa committed, nchi ikawauma, wakaweza kuomba kusimamia vitu kama hivi siyo rahisi, wenzetu wa Wizara ya Fedha mnakwama wapi uzalendo uko wapi mpaka leo mmeshindwa wakati wenzetu nchi nyingine wamefanya hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala zima la ucheleweshaji wa miradi hasa mradi huu wa Zanzibar na Bunda ningeliomba kama sikupata majibu ya kuridhisha nitazuia kifungu hapa, kwa hiyo ningeliomba kabisa nitazuia mshahara wako Mheshimiwa Waziri kama sikupata majibu ya kuridhisha katika suala zima la ucheleweshaji wa fedha za mradi hasa wa mabadiliko ya tabianchi kwa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala kwa kutujalia uzima, salama na afya njema.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru pia wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika ripoti hizi mbili muhimu za Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii pamoja na ile ya wenzetu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kuwapongeza wenzetu wa Maliasili, Waziri, pamoja na Ardhi, Mawaziri pamoja na timu zao. Kwa kweli wamefanya kazi nzuri katika kipindi hiki cha utekelezaji wa kipindi cha miezi sita na tunaona matokeo chanya katika sekta zetu zote hizi za ardhi pamoja na maliasili.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni ombi langu kwa Wizara ya Fedha; sekta hizi tumezipelekea fedha kidogo. Maliasili kidogo wao wana afadhali, lakini sekta ya ardhi bado hali haijaridhisha, kwa hiyo tunaweza tukawalaumu utekelezaji siyo mzuri, lakini sababu kubwa ni kwamba kiwango cha fedha ambazo tunawapelekea hawa wenzetu hakiwezi kukidhi utekelezaji wa shughuli ambazo tumewapangia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo namwomba sana Waziri wa Fedha ajitahidi kwa sababu tuna malengo tumeyapanga katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi, tuweze kuyafikia katika miaka mitano na nyota njema huonekana asubuhi. Mpaka hivi sasa bado haionekani kwamba kuna uwezekano mzuri wa kuweza kuyafikia haya kama hatutaweza kuzipatia hizi sekta fedha za kutosha.

Mheshimiwa Spika, nami niungane na wenzangu na napenda kumfuata kaka yangu, ndugu yangu, Mheshimiwa Omar King. Kuna maneno ya maandishi yanazungumza “idha dhwaharal-bidaa washarus-swahaba famankanalahul-ilma falyudh-har. Wamankudhwiat alayhi laanatu-llah” kwamba unapodhihiri ufisadi au uzushi na kubughudhiwa au kutukanwa kwa wanazuoni, basi wale ambao wana utaalam wanatakiwa waudhihirishe na watakaoficha basi laana ya Mwenyezi Mungu inatakiwa iwaandame. Sasa mimi binafsi sitaki laana ya Mwenyezi Mungu ije iniandame kwa sababu tayari nina ujuzi katika haya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo suala la Ngorongoro nafikiria tatizo kubwa kwamba tumewaacha wataalam wetu na sasa tunaongozwa na vichwa vyetu. Kwa sababu wataalam toka mwaka 1959 wamefanya tafiti za kutosha za kutupa dira ya kufanya maamuzi sahihi vipi tutalifikia hili suala, lakini matokeo yake vitabu tumeviweka pembeni na tunaongozwa na hisia na vichwa vyetu. Kwa hiyo kama walivyozungumza wenzangu kwa kweli tunakwenda kuipoteza Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kama hatutachukua hatua sahihi hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika masuala ya uhifadhi, suala la muda ni suala muhimu sana. kama muda ukiuacha, nakumbuka kuna Profesa mmoja, Profesa Kajembe, alifanya utafiti kule Duru-Haitemba katika kuwashirikisha wanajamii katika kuhifadhi msitu. Wananchi wale walikabidhiwa msitu katika kipindi cha mwaka mmoja walienda msitu ukawa umepotea wote umekwisha. Nafikiri wale ambao ni wenyeji wa Duru-Haitemba wananisikia hapa watakuwa wanafahamu kule Babati ukweli jinsi ulivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo na sisi katika hali halisi ya Mamlaka ya Ngorongoro kama hatutachukua hatua hivi sasa basi tujiandae Tanzania kwenda kupoteza urithi wa dunia. Kwa sababu kila sababu zinaonekana kama tulikuwa watu 8,000 sasa hivi tupo zaidi ya 120,000; tulikuwa na ng’ombe 12,000, sasa hivi kuna ng’ombe zaidi ya 800,000. Hapa projection ya ndani ya miaka 20 hadi 40 inayokuja unaitegemea itakuwaje; tutakuwa na ng’ombe zaidi ya bilioni moja na kuendelea, tutakuwa na watu zaidi ya 300,000 hadi 500,000. Kwa hiyo naomba tu, muda wa maamuzi ni sasa, lazima tuchukue hatua.

Mheshimiwa Spika, katika uhifadhi huuhuu ambao tunauzungumza ndani ya Ngorongoro tulikwenda tukapoteza faru mpaka wakabakia faru watano. Jitihada zimefanyika sasa hivi tumeweza kurejesha faru angalau idadi inatia matumaini.

Mheshimiwa Spika, sambamba na suala la Mamlaka ya Ngorongoro, kuna hali ambayo inafanana na hiyo ya Bonde la Kilombero. Bonde la Kilombero nako hali siyo salama kwa sababu tumeshaweka fedha, trilioni sita pale na hizi fedha kama hatukwenda kulishughulikia Bonde la Kilombero nako hatari inatunyemelea.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu maji ambayo yanatoka katika Mto Kilombero ni asilimia 60 mpaka 65. Kuna vijiji kama Kijiji cha Ngombo; kuna vitongoji karibu vinane katika Wilaya ya Malinyi; kuna vitongoji vitatu katika Wilaya ya Ulanga na kuna kitongoji kimoja katika Wilaya ya Kilombero kutokana na data za wataalam wetu vinatakiwa viondoke. Kama tukichelewa kuviondosha hivi, basi tusitegemee Mradi wa Stiegler’s Gorge wala tusitegemee Mradi wa SGR kwa sababu hii miradi miwili inategemeana.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nimalizie tu kwa kuwapa pongezi wenzetu wa maliasili hasa TAWIRI kwa kuweza kufanya ile International Conference ambayo ilikuwa ikifana vizuri na ninampongeza sana Mkurugenzi wa TAWIRI na Mkurugenzi wa Wanyamapori pamoja na Waziri. Namwomba Profesa Mkenda tuwahamasishe vijana wetu wa Vyuo Vikuu, basi waweze kuhudhuria katika makongamano hayo kwa sababu yana tija kubwa na yataweza kuwasaidia Watanzania kuweza kukuza vipaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia katika taarifa hizi mbili za Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii pamoja na Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninamshukuru Mwenyezi Mungu, Subhanahu Wa Ta'ala, kwa kutujalia uzima, afya njema na kuweza kusimama hapa mbele yako leo na kuweza kuchangia taarifa hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja ninapenda kuanza katika Taarifa hii ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa kuomba twende tukaongeze azimio moja la kuzitaka taasisi watekeleze takwa la kisheria la kuanzisha desks za climate change (mabadiliko ya tabianchi) katika kila Wizara. Kwa sababu kuna azimio ambalo la utekelezaji wa mpango kabambe kwa kutoa elimu zaidi, lakini nafikiria itakuwa na tija zaidi tukiliacha hili azimio lakini pia tukaongeza na azimio lingine la kuzitaka taasisi zote zitekeleze hili azimio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo; kwa sababu taasisi zote hapa zimekuwa zikiripoti matatizo ya mabadiliko ya tabianchi kama ni changamoto ambayo inatatiza utekelezaji wa bajeti, utekelezaji wa miradi ya maendeleo, utekelezaji wa shughuli zote za huduma za kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tuweze kutekeleza vizuri takwa hili la kisheria ambalo limewekwa katika sheria na sera yetu ya mazingira basi ni vyema tukazitaka sasa kwa sababu hizi sekta zimekwisha kushajihishwa, zimeshapewa elimu lakini sidhani kama kuna angalau desk officer au focal person mmoja katika taasisi zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu, Rais, Mheshimiwa Samia, ame-commit hekta milioni 54 katika Mkutano wa Glasgow na Mkutano wa juzi wa Sharm El Sheikh kule Misri, kwamba tunazitenga kwa ajili ya carbonsink Tanzania. Hili ni azimio na vilevile ni commitment ambayo tumeifanya kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna huu mpango kabambe, hali kadhalika kuna matakwa mengi ya Kitaifa na kimataifa ambayo tunataka tutekeleze na kuisaidia Tanzania kuweza kuepukana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi. Kwa hiyo, ninaomba hili takwa la kisheria tukaliongeza hapa, na tukaliongeza hili azimio katika maazimio ambayo wenzetu wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira wamekuja nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitakwenda moja kwa moja katika sekta ya maliasili na utalii. Mwenzangu amezungumzia kuhusu TANAPA. Na ni kweli, kwamba TANAPA wana jukumu kubwa sana na kama alivyozungumza kwamba tulikuwa tuna hifadhi 16 na hivi sasa zimeongezeka na kuwa 22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa na hifadhi 16 tulikuwa tuna eneo kama kilometa za mraba 54,000 tu, lakini hivi sasa tuna kilometa za mraba 104,000 wakati eneo la uhifadhi limeongezeka na hizi hifadhi zimeongezeka lakini bado bajeti imebakia ileile tuliokuwa tukiitumia wakati tuna hifadhi 16. Kwa hiyo, ninaomba tu kwamba wenzetu wa Wizara ya Fedha waliangalie hili na ninafikiri sasa ni wakati mwafaka hili azimio la kusaidia, pamoja na bajeti ambayo tunakuwa tunawapa lakini angalau ku-retain, ile retention ya asilimia angalau 20 zibakie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kuna majukumu ambayo wakati mwingine inakua ni vigumu hizi taasisi zetu kuyatekeleza kama vile majanga ya moto, majanga ya maradhi n.k. kwa kutegemea fedha za bajeti. Mpaka uombe Wizara ya Fedha zije inakuwa ni ngumu. Kwa hiyo, ninaomba tu kwamba tubakishe angalau asilimia 20 za fedha katika ile retention au makusanyo yao wakaweza kutumia kwa masuala mbalimbali, hasa yale ambayo yanakuwa hayana mpangilio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ni Hifadhi ya Ngorongoro; tuwapongeze sana wenzetu wa Maliasili, wanafanya kazi nzuri. Lakini pamoja na hayo, Waswahili wana usemi kwamba mchuzi wa mbwa uliwe ukiwa wa moto. Sasa na sisi hili jambo tulifanyie harakati kidogo kwa sababu kama tukichelewa mpaka 2025 inawezekana tukajikuta kuna ugumu kuweza kulitekeleza hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wana bajeti ya karibu bilioni 200 na kidogo ambazo wakizipata hizi wataweza kutekeleza kuhamisha wananchi kwa hiari kutoka Ngorongoro kwenda Msomera kwa ukamilifu. Kwa hiyo, ninaomba tu kwamba tujitahidi kuwapatia hizi fedha, na hata ikiwezekana kwa sababu makusanyo ya Ngorongoro kwa mwaka mmoja yanafika milioni 150. Sasa kama tukijitahidi tukiachilia labda fedha zisiende Treasury kwa miaka miwili basi hatutakuwa na haja ya kuchangisha fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niongelee kuhusu Jeshi Usu; Jeshi Usu linafanya kazi kubwa sana. Na hivi karibuni tumekuwa tukisikia kuna vifo vingi vimekuwa vikitokea vya askari wetu hawa wa Jeshi la Uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba tu kwamba tujitahidi inavyowezekana kwamba mafao yao hivi sasa yarekebishwe kwa sababu sasa hivi Jeshi la Uhifadhi kutoka TANAPA wana skimu yao, Jeshi la Uhifadhi na WMA wana skimu yao na Jeshi la Uhifadhi la TFS nao wana skimu yao. Kwa hiyo ninaomba tu tukarekebisha utaratibu huu haraka inavyowezekna ili ikiwezekana wawe na utaratibu kama vile wa Jeshi la Polisi, Jeshi la Wananchi wa Tanzania, nao watambulike na mafao yawe mazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu hii ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Niende moja kwa moja katika michango yangu kutokana na uchache wa muda. La kwanza ningependa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake kwa uwasilishaji mzuri ambao wameufanya.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana wakati nachangia bajeti kuu ya Serikali nilitoa indhari hapa kwamba kama sikuona mabadiliko katika matatizo ya wizi wa mazao ya kilimo na mifugo kule Zanzibar kama sikuona ufumbuzi wa kudumu katika bajeti hii ya Mheshimiwa Waziri basi nitashika mshahara wake, sasa Mheshimiwa kwa masikitiko makubwa kwa kweli katika bajeti hii sikuona sehemu ambayo kuna mkakati maalum kwamba tunakwenda kuondoa tatizo la wizi wa mazao ya kilimo na mazao ya mifugo kule Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aje aniambie kuna mkakati gani wa kwenda kuondoa tatizo la wizi wa mazao, kwa sababu hili tatizo limekuwa ni kidonda sugu kule Zanzibar, wananchi wanalima sana, wanajitahidi kufuga, lakini wizi umekuwa mkubwa unawarudisha nyuma na hakujakuwa na suluhisho la kudumu ambalo linatia matumaini kwa wakulima wetu ambao wanajituma siku hadi siku kuweza kulima.

Mheshimiwa Spika, tukizungumzia food security tunakusudia kwamba usalama wa chakula ambao unategemea asilimia zaidi 70 ya wakulima wetu ambao wanalima. Sasa wewe unakwenda kwenye kilimo unalima, unakuta shamba lako limevunwa lote. Unakwenda kwenye mifugo unakuta mifugo yako kama ni kuku au ng’ombe wameondoka wote. Hapa juzi Mheshimiwa Mbunge wa Chambani aliuliza swali hapa na akaelezea changamoto za Chambani, kwa hiyo nazungumzia katika Jimbo langu la Donge, lakini hili tatizo ni tatizo sugu kwa Zanzibar nzima. Kwa hiyo ningependa Mheshimiwa Waziri aje anipe majibu ya kuridhisha hapa, tunakwenda kutatua vipi tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, suala lingine katika Jimbo langu la Donge ni sehemu ya machimbo ya mchanga, mchanga asilimia 90 unatoka katika Jimbo langu la Donge na Jimbo la Mheshimiwa Mbunge wa Bumbwini. Sasa kuna ajali nyingi zimekuwa zikitokea kutokana na magari ya mchanga kwenda kwa kasi na hivi juzi nimeenda kwenye hizi sherehe za sikukuu, nimezika wananchi wangu wawili kutokana na ajali za barabarani. Kwa hiyo ningeomba vile vile Mheshimiwa Waziri atakapokuja aniambie ana mpango gari wa kupunguza ajali katika eneo langu la Jimbo la Donge, lakini katika barabara ya Bububu - Mkokotoni ambayo kwa Zanzibar ndio inayoongoza kwa ajali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tatu niongelee kuhusu Kituo changu cha Mahonda, Kituo cha Polisi Mahonda kimeanza kukarabatiwa na kuna ujenzi unaendelea hivi sasa lakini huu ujenzi unasuasua sana. Kwa hiyo, vile vile ningeomba Mheshimiwa Waziri aje aniambie kwamba je, ujenzi huu utaratibu ukoje isije ikawa unasema zile Tuzo na Tozo ambazo mpaka zipatikane ndio ujenzi uendelee, ningependa ujenzi huu uwe endelevu na umalizike kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho ni suala la ajira ambazo Mheshimiwa Simai hapa amelizungumzia. Kwa kweli ni tatizo kwa sababu imekuwa kama vile hii ajira wenzetu wa Makao Makuu wana mpango wao maalum ambao kwa kweli Majimbo, Wilaya na Mikoa hawaujui unaendaje. Nafasi za Polisi, Uhamiaji yaani utaratibu haufahamiki vema, kwa hiyo ningependa Mheshimiwa Waziri angejitahidi kuwe na uwazi katika masuala ya ajira kwa nafasi hizo za Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara kwa uwasilisho mzuri wa bajeti pamoja na mikakati ambayo wameiweka katika bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maeneo matatu na kama muda utatosha nitaongeza moja la nne haraka haraka katika michango yangu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ya kule Zanzibar kwa kuweza kuifanyia marekebisho makubwa Ofisi ya Zanzibar ya Mambo ya Nchi za Nje ambayo kwa sasa angalau ina mwonekano wa kweli wa Ofisi ya Mambo za Nchi za Nje. Ni tofauti na ilivyokuwa zamani, miaka mitano iliyopita, kwa kweli ilikuwa inatia aibu kama ni ofisi ya mambo ya nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ombi langu, kwamba pamoja na marekebisho tuliyofanya kwenye ofisi hii, naomba sasa twende kwenye changamoto ambazo zinakabili hiyo ofisi. Changamoto ya kwanza hiyo ofisi ina upungufu mkubwa wa watendaji. Kwa hiyo ningeomba tukaongeza idadi ya watendaji katika Ofisi ya Mambo ya Nchi za Nje ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala zima la vifaa na usafiri. Kwa kweli ni aibu Ofisi ya Zanzibar ukienda suala la usafiri ni gumu katika Ofisi ya Mambo ya Nchi za Nje ya Zanzibar na halikadhalika vitendea kazi. Kwa hiyo ni tegemeo langu kwamba Mheshimiwa Waziri na timu yake wataionea huruma Ofisi ya Zanzibar kwa kuipatia vifaa na usafiri ili iweze kuonekana kuwa na hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ningeomba pia kama kuna uwezekano tukatenga eneo hasa, sababu tumefanya marekebisho, lakini tutenge eneo tujenge Ofisi ya Zanzibar katika maeneo mengine sio katika eneo lile ambalo kidogo limejikunja hata parking za magari ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, wenzangu wameongelea kuhusu sera hapa na mimi vile vile niweke mkazo kwenye marekebisho ya sera, tuyafanye kwa haraka kwa sababu sera ya mwaka 2011, ni kipindi karibu miaka 23 sasa toka sera hii imetayarishwa. Sasa naomba tu kwamba tuweke mkazo kwenda kuitayarisha na kuitengeneza Sera ya Mambo ya Nchi za Nje ili kuweza kuakisi hii diplomasia ya uchumi ambayo tunaizungumza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni suala zima la mambo ya royal tour. Mheshimiwa Waziri amefanya kazi nzuri kuzihamasisha baadhi ya balozi zetu nchi za nje na zimefanya kazi nzuri, lakini ombi langu sasa ni vyema tukawa tuna mkakati wa pamoja na miongozo ambayo itazitaka balozi zote ziwe na target ziwe na miongozo maalum ya kuweza kuifanyia kazi hii ripoti au hii video ya royal tour ili kuweza kutangaza na kufikia ile target au lengo la kufikia watalii elfu tano ifikapo mwaka 2025, kama ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyozungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niongelee suala zima la ushiriki wa Tanzania katika taasisi na mikutano ya kikanda na ya nchi za nje au ya kimataifa kwa ujumla. Kama unavyojua kwamba ili kuweza kupata hizi fursa kusema vizuri za mambo ya nchi za nje, ni lazima tuwe na watendaji wazuri ambao wameandaliwa, lakini pia tuandae mazingira ya Tanzania kwa ajili ya kupata hizi fursa ambazo ziko katika taasisi pamoja na mikutano ya kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano hapa, kuna mikutano ya kikanda ya mabadiliko ya tabianchi ambayo kuna fursa nyingi za kiuchumi, lakini ukienda hivi sasa kuna tatizo kubwa kwamba hizi fursa hatujajiandaa vizuri kwa sababu kama ukiangalia, kuna accreditation institution moja tu Tanzania ambayo ni Bank ya CRDB, lakini bado wenzetu kuna baadhi ya nchi wana institutions ambazo zimesajiliwa zaidi ya nne, zaidi ya tano ambazo zinaweza zikatafuta hizi fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo na sisi Tanzania tuandae watendaji, tuandae na hizi institutions zetu ziweze kuchangamkia hizi fursa za kifedha na shughuli nyingine mbalimbali katika hizi Jumuiya za Kikanda pamoja na mikutano ya umoja wa kimataifa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji asubuhi hii katika Wizara yetu hii ya Nishati. Awali kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu Wa Ta'ala kwa kutujalia afya njema, uzima lakini pia kuendelea amani kutamalaki katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri January Makamba, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara kwa kweli wanafanya nzuri na mwenye macho haambiwi tazama kwa sababu ukienda kwenye maonyesho pale unajione mwenyewe. Kama leo Mtanzania Mheshimiwa Mbunge ambaye hajawahi kufika kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere lakini ameweza kulionia akiwa Dodoma na ameliona si kwamba ameliona picha ameona kwa uhalisia kabisa. Kwa hiyo kweli huu ni ubunifa mkubwa na ni mapinduzi ya kiteknolojia na kiutendaji katika sekta yetu hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, mimi niende kwenye maeneo matatu makubwa na nianze tu kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuendeleza ushirikiano mzuri baina ya TANESCO na ZECO Zanzibar hali kadhalika baina ya Wizara ya Nishati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Tanzania Visiwani, ambayo ni Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ushirikiano ni mzuri na ndiyo haya mwenzangu Kaka yangu Pondeza ameyazungumza hapa. Kwamba hivi sasa tumeweza kufika kile kilio chetu ambacho tulichangia hapa mwaka jana kwa sauti kubwa kwamba bei za Tanzania Visiwani na za Tanzania Bara ambao wote hawa ni raia wamoja na ni ndugu – kulikuwa kuna tofauti kubwa sana, na sasa hivi ni furaha kwamba tumeambiwa kwamba hii kadhia imeweza kutatuliwa.

Mheshimiwa Spika, sasa ni ombi langu tu, kwamba tuwasiliane na wenzetu wa ZECO tukaone tafsiri ya haya mazungumzo na makubaliano tafsiri yake ikaonekane kwenye bill. Kwa sababu mimi nikiwa kama mtumiaji wa umeme bado ile tafsiri na mabadiliko hali sijayaona bado. Sasa ningeliomba tu kwamba haya mabaliko ambayo yanaonekana kwamba bei imekwenda kuwa negotiated na hadi sasa bei zinafanana basi ikaonekane kwenye bill ya mwananchi, kwa sababu siyo fair kwa Mtanzania huyu huyu ambaye kwenye Tigo, kwenye Zantel, kwenye Vodacom analipia sawasawa baina ya Tanzania bara na Tanzania Visiwani lakini umeme kuwe kuna tofauti. Nafikiri tunaamini kama hilo limekaa sawa ni vizuri na kama bado kuna tofauti ndogo tukarekebishe.

Mheshimiwa Spika, suala jingine ni kwanza nitangulize shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Waziri kutokana na jitihada na tafiti ambazo zinaendelea katika vyanzo vingine vya umeme. Kwa sababu ni hatari kuendelea kutegemea vyanzo vya maji peke yake. Kama tunavyojua kwamba nchi hii iinakabiliwa kama ilivyo dunia kwa ujumla na mabaliko ya Tabianchi na hatujui siku gani utakuja ukame wa kutisha na vyanzo vyetu vya maji vije viweze kuteteleka na hapa itakuwa hatuna msalia Mtume isipokuwa tukangalie vile vyanzo ambavyo havitegemei maji moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningelimuomba tu Mheshimiwa Waziri hapa atengeneze jitihada. Mwenzangu Mheshimiwa Sanga jana amezungumza hapa, kwamba kuna maeneo tayari ameshafanyia tafiti kama Makambako, lakini yapo maeneo mengi Tanzania kuna maeneo ambayo yana-potential ya umeme wa jotoardhi, umeme wa solar na umeme wa upepo. Sasa nafikiria maeneo ambayo tayari tafiti zimeshakamilika sasa nafikiri tuende tuka-invest ili angalau tupate megawatt chache za kuweza kuziweka kama akiba ili siku ambayo tutateteleka kwenye maji basi angalau tutakuwa tuna sehemu ya kukimbilia.

Mheshimiwa Spika, sehemu ya tatu ya mchango wangu niende kwenye ile ambayo jana alizungumza hapa Mheshimiwa Waziri, ile kuhama kutoka kwenye nishati chafu ya kupikia na kwenda kwenye nishati safi na salama ya kupikia. Na hapa tena niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anayaifanya, na niombee Mungu mradi wa LNG nao uende ukafanikiwe haraka ili uende ukaongeze ufanisi katika hili.

Mheshimiwa Spika, hapa pia nafikiria nimuombe tu Mheshimiwa Waziri tujitahidi kadri inavyowezekana, kwa sababu kama tunavyojua, kwamba bado kuna jitihada nyingi zinaendelea katika nchi hii katika suala la kuhama au shifting kutoka kwenye kutumia nishati chafu hii na kwenda kwenye nishati safi na salama. Wenzetu wa misitu wanafanya kazi hiyo, wenzetu wa mazingira wanfanya kazi hiyo. Sasa hivi jitihada twende tukazichanganye kwa pamoja ili tuweze kupata ufanisi mzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Tanzania inapoteza takriban hekta laki nne kwa mwaka. Na hekta hizi laki nne ambazo zinapotea kwa mwaka ndizo ambazo zinahifadhi na zinatiririsha maji kupeleka kwenye vyanzo vyetu vya umeme vya Kihansi, Pangani, Mtera, hali kadhalika na chanzo cha umeme ambacho sasa hivi tunakitegemea cha Bwawa la Mwalimu Nyerere. Sasa iwapo misitu hii itaendelea kupotea basi ni hatari kubwa kwa investment kubwa ambayo inafanywa na Serikali kwenye miradi yetu ya maji. Kwa hiyo, ningeliomba tu Mheshimiwa Waziri akajitahidi kukaa na wenzake hawa wa sekta ya TAMISEMI ili kuangalia wanafanya jitihada hizi kwa kiasi gani ili kuzichanganya kwa pamoja ili ziweze kuleta tija.

Mheshimiwa Spika, lakini pia ombi langu, tusije tukavamia tukachukua register kwamba hizi nishati mbadala ziende kwa kila mahali Tanzania zienee. Ningeliomba tu kwamba tukaangalie uwezekano wa maeneo mbalimbali ambayo yako very strategic, ambayo ni potential. Kuna maeneo ambayo yana misitu na kasi ya kupotea kwa misitu ni kubwa; twende huko tukashambulie kwanza kabla hatujaenda kuangalia kila mahali. Kwa hiyo kwa utaratibu wetu sisi hasa Wizara ya Nishati tukaangalie maeneo ambayo yanatuhusu zaidi kwanza halafu tena baadaye ndipo tukaangalie upande mwingine.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa promotion ambayo anaendelea kuifanya. Waheshimiwa Wabunge hawa walifanya kazi kubwa kipindi cha sensa, walifanya promotion ya sensa na Tanzania nzima ilisimama na matokeo yake matokeo ya sensa sisi tunayajua. Kwa hiyo nafikiria na hii promotion ambayo unajumuisha Wabunge katika uendelezaji wa nishati safi na salama basi hii inakwenda kuzaa matunda makubwa, kama ambayo ulitufunza.

Mheshimiwa Spika, nishukuru na niunge mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi kuweza kuchangia katika Wizara yetu hii muhimu ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Kwa kuanza na mimi ningependa vilevile kumshukuru sana Mwenyeezi Mungu Sub-hanallah Wataallah kwa kutujaalia uhai uzima na salama lakini halikadhalika kumshukuru Jemedari Mkuu au Amiri Jeshi Mkuu wetu, Mama Samia kwa jitihadi ambazo amekuwa akizichukua katika kuliendeleza Taifa hili. Mheshimiwa Rais ametuletea jembe Waziri wetu ambaye kwa kweli anatusaidia sana katika kuiendeleza Wizara hii na mimi nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri muda mfupi lakini ameweza kufanya makubwa katika Wizara hii pamoja na timu yake, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja katika mchango wangu mimi nikiwa kama Balozi wa Mazingira na nimpongeze sana Mheshimiwa Jafo kwa kunipa nafasi hii, ili niende kuitendea haki ningekwenda moja kwa moja kwenye mchango wangu katika page 13 ambayo inaelezea utunzaji wa mazingira katika speech yake Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri umepanda miti 147,000 katika makambi yetu kwa kweli hiki kiwango kidogo tukizingatia mahitaji ya nishati ya kupikia, miti ya kujengea katika makambi yetu. Kwa hiyo, ningeomba tu kwamba katika bajeti hii inayokuja tukaongeza kidogo kiwango cha upandaji miti katika makambi yetu kwa sababu miti 100,000 ni kidogo Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili Mheshimiwa Waziri kule Zanzibar kuna uharibifu mkubwa wa mazingira katika makambi yetu na zaidi kuna Kambi ya Ali Khamis Camp ambayo ilipanda miti mingi kipindi cha nyuma, lakini pia kuna kambi ya Mwanyanya ambayo ilipanda miti mingi kipindi cha nyuma lakini hivi sasa miti ile inavunwa lakini bila ya kurejeshewa miti mingine. (Makofi)

Kwa hiyo, ningeomba tu katika kipindi kinachokuja tukajikita zaidi katika upandaji miti katika makambi yale haya ile miti ambayo tunavuna basi tuirudishe tena. Lakini kuna Kambi ya Makuwe na Bububu kuna uharibifu mkubwa wa mazingira Mheshimiwa Waziri, ningeliomba pia ukaweka jicho lako kule kwa sababu Idara ya Misitu na Maliasili kwa miti isiyorudishwa wamekuwa wakigombana mara kwa mara na kambi hizi kwa ukataji miji hovyo. Kwa hiyo, ningelipenda tu pia tukawaelimisha kambi zetu kwamba wakachukua jitihada za kutunza mazingira kama ulivyoahidi katika hotuba yako hapa kwamba miti hii ya asili inalindwa na kutunzwa. Kwa hiyo, nafikiri kambi hizi kwa sababu vilevile kuna miti ya asili basi tungeitunza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika Mheshimiwa Waziri katika suala la uwekezaji katika kambi zetu hizi za Zanzibar kumekuwa na uwekezaji ambao siyo sahihi, kwa sababu mfano kama kuna msitu mdogo katika Kambi ya Bavuai, ulikuwepo msitu ambao ni mzuri na umetunzwa kipindi kirefu, lakini hivi karibuni tumeanza kuumega, tumejenga vituo vya mafuta (shell) pale na tukitoka Kiembesamaki, Uwanja wa Ndege mpaka Mwanakwerekwe kuna karibu vituo vya mafuta (shell) saba. Sasa sijui kama kulikuwa na umuhimu wa kuwa vituo vya mafuta (shell) nyingine pale.

Kwa hiyo, mimi ushauri wangu tu Mheshimiwa Waziri tunapowekeza katika Kambi zetu hizi tuangalie uhalisia na tuangalie vilevile ramani za Manispaa na Miji yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini halikadhalika, tukiangalia katika Kambi ya Mtoni kuna vi-garage pale vya ajabu ajabu, sasa sijui kama kulikuwa na umuhimu wa zile garage pale kwa sababu zinaharibu haiba ya Mji; tunataka vikosi vyetu viwekeze kiuchumi, lakini vilevile tufanye tathmini ya kuangalia huu uwekezaji kama una tija. Lakini halikadhalika kuwema mazingira ya mji kwa sababu katika Mji wa Zanzibar kuna Kambi karibu tano na Kambi zote hizi zipo ndani ya mji. Sasa kama tutakuwa tunawekeza katika lengo siyo zuri tunaweza tukaaribu mazingira. Lakini pia kuna Kambi ya Welezo, ndani kule wamechimbisha mchanga ni mashimo matupu. Kwa hiyo, pia ningelikuomba Mheshimiwa Waziri ikiwekana ungefanya ziara ukaenda Zanzibar...

MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Soud kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Asya.

T A A R I F A

MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, naomba ni mpe taarifa mchangiaji siyo tu kwamba kuna uharibifu wa kimazingira kwenye kambi, lakini kuna wananchi wanaishi pembezoni mwa kambi, yaani Kambi ya Jeshi kwa mfano kambi anayozungumza Mheshimiwa Soud ya Mtoni watu wanaishi hapa ndani ya Kambi. Kwa hiyo, ni hatari zaidi hata mabomu muda mwingine yanaporipuka madhara huwa yanatokea kwa wananchi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Soud unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, naipokea hiyo taarifa. Naomba niendelee haraka haraka muda wangu nafikiri utakuwa umenichungia kidogo.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika kuna Kambi ya Welezo kuna Mheshimiwa mmoja pale alijenga jengo na akaambiwa kwamba lile jengo litakuwa sio salama na ikabidi afidiwe aondoke. Sasa utashangaa sasa hivi yeye ameondoka, lakini sasa hivi pana maduka ya miti, pana maduka ya garage, yameanzishwa pale sasa utashangaa kama je, ilikuwa ni usalama ndio tukamuondosha yule. Sasa je, huu uwekezaji tunaouweka sasa hivi nao ni sahihi? (Makofi)

Kwa hiyo, ningemuomba tu Mheshimiwa Waziri ukafanya ziara ukaenda Zanzibar na ikiwezekana ikikupendeza, ukafuatana na Mkurugenzi wa Mazingira, Mkurugenzi wa AZEMA…

SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa, muda umekwisha.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, na Mkurugenzi wa Misitu ili waweze kushauri. Ahsante sana. (Makofi)