Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo (31 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi hii kumshukuru Rais wetu Dkt. John Joseph Magufuli. Pili, niunge mkono hotuba mbili zote alizozitoa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda ukurasa wa 12 wa hotuba ya kufungua hili Bunge, Rais alisema: “Nataka Watanzania wote washiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa nchi yao.” Tunapoongelea uchumi jumuishi hii ndiyo falsafa yenyewe ambayo Rais anatuelekeza katika hotuba yake. Hata hivyo, hatuwezi kuwajumuisha Watanzania wote katika kujenga uchumi wa nchi yao kama hatujawawekea miundombinu ya kutosha. Ili kuhakikisha kwamba Watanzania wote wanashiriki katika uchumi wa nchi yao, lazima tuangalie sekta za kimkakati ambazo ni pamoja na kilimo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiongelea kilimo, nchi yetu bado inategemea kilimo katika kuzalisha mazao ambayo tunauza nje. Tunayo mikoa ya kimkakati ambayo ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo na biashara. Hatuwezi kuwa na kilimo chenye tija kama tunaendelea na kilimo cha jembe la mkono na cha kutegemea mvua, jua na kiangazi, lazima twende kwenye kilimo cha umwagiliaji maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Muleba Kusini tunayo miradi miwili ya umwagiliaji maji. Tunao mradi wa Kyamyorwa ambao Serikali yetu Tukufu imeugharamia kushirikiana na wadau wengine, tekeo tayari, mfereji umejengwa, tumebakiza banio. Niiombe Wizara ya Kilimo ikamilishe mradi huu ili wananchi wa Kyamyorwa na Muleba na Mkoa wa Kagera kwa ujumla wake waweze kufaidi na kuendeleza kilimo cha umwagiliaji maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mradi mwingine wa Buhangaza ambao umejengwa lakini haujakamilika. Hii miradi imetumia fedha za walipa kodi, niisihi, kuiomba na kuishauri Wizara ya Kilimo, miradi hii ikamilishwe ili iweze kuzalisha kulingana na pesa tulizoziwekeza pale ili wananchi wanufaike na miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera unapakana na nchi nyingi jirani kama Rwanda, Uganda na Burundi. Tukitumia fursa tulizonazo katika Mkoa wa Kagera ambaapo tunalo bonde la Mto Ngono ambalo linafaa kwa ajili ya kilimo na uzalishaji mkubwa wa chakula, tukiweza kuwekeza katika bonde hilo Mkoa wa Kagera unaweza ukawa soko la chakula kwa ajili ya nchi zote zinazozunguka mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye sekta ya uvuvi. Sekta hii inaajiri vijana wengi na nitajikita katika Ziwa Victoria ambako mimi natoka. Ukiangalia kazi zinazoendelea katika Ziwa Victoria sisi kama Tanzania tunamiliki asilimia 51 ya ziwa lile, wenzetu wanamiliki asilimia 49, Uganda wana asilimia 43, Kenya wana asilimia 6 lakini ukiangalia mauzo nje ya nchi inaonekana sisi tunauza kidogo kuliko wenzetu ambao wanamiliki eneo dogo la Ziwa Victoria. Kwa nini inakuwa hivyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, jana kuna Mbunge hapa alichangia kuhusu sekta ya mifugo, ukiangalia kwa nini hatufanyi vizuri katika mauzo ya nje kama Rais anavyotuambia biashara ni vita, mfumo wa tuzo zinazotozwa kwenye mazao yanayotokana na uvuvi na ukilinganisha na nchi za jirani, sisi tozo zetu ziko juu sana. Niishauri Wizara ya Uvuvi kuhakikisha kwamba tunapitia tozo zote ambazo zinatozwa kwenye mazao ya samaki. Tuhakikishe kwamba zile tozo aidha zinalingana na nchi jirani au kwa kuwa tuna eneo kubwa la ziwa tunaweza tukafanya ujanja tuka under cut tuwe na tozo za chini ili tuweze kuvuna na kuuza nje mazao mengi ya uvuvi. Vinginevyo tutabaki nyuma, tutabaki kulalamika lakini jambo la msingi tupitie tozo kama nilivyoshauri ili tuweze kupata pesa za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye sekta ya uvuvi, Wilaya yangu ya Muleba ina visiwa 39 na visiwa 25 vinakaliwa na wavuvi. Ilipokuja hii ya sera ya kukamata wavuvi haramu, siwaungi mkono lakini nawaomba na nishauri Wizara ya Uvuvi, busara itumike tunapokwenda kwenye zoezi la kuwakamata wavuvi haramu. Kinachoendelea sasa imekuwa kama kukomoana na kuna kesi nyingi ambazo zinaendelea watu wanakamatwa, wanafunguliwa kesi na wakati mwingine kesi zenyewe ukiziangalia hazina hata ushahidi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bukoba tumejengewa Chuo cha VETA. Nimshukuru Rais wetu na Serikali yetu Tukufu. Nategemea Waziri wa Elimu, kati ya mitaala itakayoendeshwa kwenye Chuo kile cha VETA tuwe na mtaala ambao unawafundisha vijana wetu kutengeneza nyavu na vifaa ambavyo tunavitumia katika sekta nzima ya uvuvi kwa sababu Mkoa wa Kagera na Mikoa ya Kanda ya Ziwa inategemea sana uvuvi katika uchumi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga hoja mkono hotuba zote mbili na hotuba zote zilizotangulia kabla ya hizo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, zao la kahawa mkoa wa Kagera limegubikwa na tatizo la mfumo wa soko. Soko linaua zao la kahawa Kagera. Mfumo wa AMCOS ni hatari kwa ustawi wa zao la kahawa Kagera. Nashauri tufungue milango kwa wafanyabiashara, turuhusu wafanyabiashara binafsi kwa ajili ya kukuza ushindani wa zao hili. Stop protectionism ya AMCOS. Serikali kupitia Tume ya Ushindani iweke mazingira shindani kwa ustawi wa soko na uchumi wa nchi yetu.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii niweze kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Wabunge wenzangu kumshukuru Rais wetu, hasa kwa pesa ambayo imeletwa kwenye majimbo yetu. Wakati unatoa takwimu za wanafunzi ambao wako darasa la nne nikawa naangalia kwenye Wilaya yangu ya Muleba, tunao zaidi ya wanafunzi 19,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwaka huu kabla Mheshimiwa Rais hajasema neno lolote, tulikuwa tunajiuliza Muleba kule hivi tunafanya nini na watoto ambao wamemaliza darasa la saba. Tukawa tumeanza ujenzi wa vyumba vya madarasa. Nashukuru kwa pesa ambayo ametuletea sasa tunao uhakika kwamba vijana wetu wa darasa la saba watapata madarasa wote na tuendelee kumshukuru Rais wetu kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru Waziri wa Fedha na Mipango kwa hotuba yake. Pamoja na pongezi hizo, zaidi niwapongeze Kamati yetu ya Bajeti. Nimesoma maandiko yao yote na nipende kuwapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza zaidi kwenye sekta ambazo zinachochea uchumi katika majimbo yetu, hasa sisi tunaotoka vijijini. Mimi naomba nitoe ushauri wangu; kwa vipaumbele ambavyo napendekeza kwenye bajeti ijayo naomba tuangalie sekta ya kilimo, tuangalie sekta ya mifugo, tuangalie sekta ya uvuvi na usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamechangia sekta ya kilimo na wengi wamesema inachukua zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania ambao ni karibia milioni 22 ya Watanzania, wanajihusisha na masuala ya kilimo. Na tumeona mchango wa sekta ya kilimo kwenye uchumi wetu. Lakini ukiangalia bajeti ambayo tunaipatia kilimo, nadhani hatukitendei haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti imependekeza kwamba bajeti tuliyonayo ya mwaka huu tuiongeze mpaka ifike zaidi ya bilioni 400. Kama tunataka kutoka hapa tulipo, sikubaliani na mapendekezo ya Kamati ya Bajeti, mimi napendekeza twende zaidi ya trilioni moja kwenye sekta ya kilimo ili tuweze kunusuru uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uzalishaji wa mazao mengi per hector, mazao mengi tunazalisha chini ya kiwango kwa sababu hatujawekeza vya kutosha kwenye sekta ya kilimo. Ukiangalia mpango wa miaka mitano ambao tulijadili hapa mwaka jana tulikubaliana kwamba tunakwenda kuongeza eneo la umwagiliaji kutoka ekari 500,600 kwenda milioni moja na laki mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia tulipo leo, tuna miaka mitatu kufikia mwaka 2025 ambako ndiyo target yetu, bado tunaekari 569,000 lakini lengo letu ni kufikia ekari milioni moja na laki mbili, kwa miaka mitatu iliyobaki tunakwenda kufanya muujiza gani ili tuweze kufikia hilo lengo letu. Tusipoongeza bajeti ya kilimo tutabaki tunaimba wimbo uleule, tutabakia hapohapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia uzalishaji kwa mfano wa mafuta ya kula. Mpaka leo tunapoongea ni aibu kwa nchi hii ambayo tunasema wakulima ni zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wote, bado tunaagiza mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Naomba kwenye mpango huu Waziri wa Fedha atupatie mkakati wa nchi ili kuinusuru nchi hii kutokana na kuagiza mafuta kutoka nje wakati tunalima na wakati nchi hii tunasema ni nchi ya wakulima na ni nchi ya wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya mikoa wamekuja na mazao mapya. Kwa mfano Kagera kule tuna mazao mapya ya vanilla, kwa mfano. Wakulima wamejitahidi wanalima lakini hatuna masoko. Na Wabunge wengi hapa wamesema tunapowekeza kwenye kilimo tuhakikishe kwamba tunawekeza kwenye utafiti, tunawekeza kwenye kutafuta masoko tusije tukatumbukia kwenye janga ambalo tulinaswa nalo hapa juzi wakati tunahangaika kutafuta pesa ya kununua mahindi kutoka kwa wakulima. Naomba tunapohamasisha wakulima wetu wazalishe kwa wingi na Serikali ihakikishe kwamba inatafuta masoko kwa ajili ya mazao ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya uvuvi; mwaka jana wakati nachangia hapa nilisema nchi yetu imebahatika kuwa na maziwa na bahari, lakini ukiangalia mchango unaotokana na mazao ya uvuvi na yenyewe bado ni aibu. Ni aibu kwa nchi kama Tanzania tunapoagiza samaki kutoka nje ya nchi kwa kutumia pesa ya nje ni aibu kwetu. Naomba atakapokuja Mheshimiwa Waziri kwenye mpango tutakaokwenda kutunga sasa kutengeneza bajeti, atuambie tuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba sekta ya uvuvi na mazao ya uvuvi yanachangia kwenye pato la Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea mwaka jana hapa, na ninaomba nirudie niliyoyasema; tumejifunga na kanuni na sheria ambazo zinarudisha uchumi wetu nyuma. Ukiangalia tozo tulizonazo kwenye sekta ya uvuvi, ukilinganisha Tanzania na nchi jirani, hasa zile tatu ambazo tuna-share Ziwa Victoria kwa mfano, kodi zetu hazikubaliki na hazibebeki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache tu, ukiangalia tozo ambazo sisi Tanzania tunatoza na wenzetu, majirani zetu, kwa mfano ukiangalia VAT Tanzania tozo yetu ni shilingi 552 wakati jirani yetu Uganda anatoza 115, mwenzetu Kenya anatoza shilingi 34. Matokeo yake ni nini; mazao mengi ya uvuvi yamekuwa yakielekezwa upande wa pili na sisi tumekuwa tukikosa kazi, na hasa vijana wetu ambao wame- invest kwenye sekta ya uvuvi hawawezi kufanya kazi kwa sababu hawawezi kushindana na wenzao ambao wako nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata viwanda vya kuchakata minofu ya samaki. Miaka ya nyuma Tanzania tulikuwa na viwanda vingi lakini kutokana na hizi sheria tulizojiwekea, tozo, sheria mbalimbali, vibali na nini, viwanda vyote vimehamia nchi za jirani, tumebaki na viwanda vichache hapa. Ni lazima tujiulize tumejikwaa wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunapoongea tumebaki na takribani viwanda nane. Uganda wana viwanda zaidi ya 20, Kenya wana zaidi ya viwanda vitano, na vyote vimehama vimekimbia kutoka hapa kwa sababu ya mfumo tulionao wa biashara, mfumo wa tozo na mfumo wa sheria tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najiuliza kwa nini mpaka leo tunapoongea unapotaka kusafirisha mazao ya uvuvi lazima yasafirishwe kupitia Viwanja vya Ndege vya Entebbe na Viwanja vya Jomo Kenyatta, Kenya, mazao ya uvuvi yanayotokea Tanzania. Tuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba sasa badala ya kusafirisha kwenda Entebbe na Nairobi, kwa nini tusitumie Viwanja vyetu vya Mwanza, Dar es Salaam au KIA? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Mwanza tumejenga facility kwa pesa ya walipa kodi, facility nzuri hata inazidi Jomo Kenyatta International Airport, lakini hatuitumii. Na sote tuko hapa tumekaa hatujishughulishi na hatujiulizi kwa nini hiyo facility ambayo tumeigharamia haitumiki. Na mwaka jana niliongekea hapa lakini tumemaliza tumerudi nyumbani, kila kitu kimeendelea business as usual. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tubadilike, kama tunataka kuingia kwenye soko la ushindani na kwenye mpango tumesema tunakwenda kujenga uchumi shindani na uchumi shirikishi, tunaujengaje kama hatuwezi ku-strain our minds tukafikiri nje ya boksi ile tuweze kunusuru nchi yetu na kuhakikisha kwamba hii sekta ya uvuvi ambayo tumebarikiwa, ni mali ya Watanzania, ili iweze kutusaidia kuchangia uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo kundi la vijana, sijaona kwenye mpango. Ukienda huko vijijini tunakundi la vijana ambao wakiamka asubuhi hawana kazi ya kufanya, mchana hawana kazi ya kufanya, mpaka jioni hawana kazi ya kufanya. Naomba kwenye mpango huu Serikali ije na mkakati hawa vijana tunawafanyaje.Vinginevyo tunatengeneza bomu ambalo miaka kumi, sihirini ijayo, litakuja kutulipukia wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima mpango uangalie kama ni mikopo ambayo tunaitoa kwenye halmashauri zetu ya kuwasaidia hawa vijana, hii asilimia nne ambayo tumejipangia haitoshi. Lazima tuangalie mkakati wa kuwanusuru hawa vijana na kwa kufanya hivyo tuweze kuwashirikisha kwenye uchumi wetu…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii nami nichangie hoja ambayo iko mbele yetu. Kwanza kabisa nikupongeze wewe kwa kazi unayofanya ya kuliongoza Bunge letu. Vile vile nimpongeze Rais wetu kwa kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana wachangiaji wengi waliongelea mambo makubwa ambayo Taifa letu linayapitia. Sisi kama Kamati ya PIC, kazi tunayoifanya ni kupitia uwekezaji wa mitaji unaofanywa na Serikali yetu kwenye mashirika yetu ya Umma. Katika mashirika ambayo yako chini ya TR yanafika zaidi ya 237 na haya yote Serikali inawekeza pesa ya walipakodi kwa lengo la kuboresha hayo mashirika na kutengeneza fedha.

Mheshimiwa Spika, katika uchambuzi wetu tumepitia mashirika na baadhi ya ripoti za TR na ripoti ya CAG, takwimu zinaonesha kwamba mashirika yetu yanafanya vizuri. Mpaka mwaka 2021 mitaji ambayo imewekezwa na Taifa letu kwenye hayo mashirika inanafikia Shilingi trilioni 67.95. Huo ndiyo utajiri ambao uko chini ya mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Spika, ukisoma takwimu, thamani ya uwekezaji wetu katika mashirika haya umekuwa ukipanda lakini ongezeko hilo limekuwa likipungua. Kwa mfano, mwaka 2016/2017 thamani ya mashirika yetu ilikuwa ni Shilingi trilioni 49.6, imeendelea kupanda mwaka 2017/2018 imekwenda Shiligi trilioni 57.79, mwaka 2018/2019 imekwenda Shilingi trilioni 60.3, mwaka 2019/2020 Shilingi trilioni 65.19, na mwaka 2021/2022 Shilingi trilioni 67.79.

Mheshimiwa Spika, kwenye ukuaji wa ongezeko la thamani ya mifuko imekuwa ikishuka. Tunayo sababu ya kujiuliza, kwa nini uwekezaji unaongezeka lakini ongezeko au ukuaji wa ongezeko unashuka? Mwaka 2016/2017 ongezeko lilikuwa ni 63.8%, mwaka 2017/2018 ilishuka ikaja kuwa 13.6%, mwaka 2018/2019 ilishuka mpaka 8.1%, mwaka 2019/2020 ilibaki pale pale 8.1%, na mwaka 2021 ilishuka ni 4.2%. Tunao wajibu wa kujiuliza kwa nini inashuka hivyo? Tusipojiuliza leo, baada ya miaka miwili au mitatu inawezekana tukaja zero tukaanza kwenda kwenye hasi tusipochukua hatua leo.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia haya mashirika yote, yako chini ya usimamizi wa Treasure Registrar (TR). Ukiangalia sheria inayomwanzisha wa Treasury Registrar ya Tanzania ni ya mwaka 1957, ni ya zamani sana, ni sheria kongwe. Imefanyiwa marejeo chini ya Miscellaneous Amendments Act, 2010. Ila yaliyofanyiwa marekebisho hayampi TR wetu uwezo madhubuti wa kusimamia haya mashirika. Ukiangalia, TR anatoa vigezo vya utendaji wa haya mashirika ya Umma lakini haimpi nafasi; haya mashirika ya Umma yasipotekeleza vile vigezo anavyoviweka, TR hana mamlaka ya kuwajibisha haya mashirika ya Umma. Hicho ni kikwazo kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukirejea hiyo sheria ambayo nimeiongelea, ni kongwe, ni ya zamani, na ukiangalia umuhimu wa uwekezaji kwenye haya mashirika, TR anapaswa kuwa na nguvu madhubuti ya kuyasimamia haya mashirika. Taasisi yoyote ambayo inashindwa kutekeleza hivyo vigezo alivyoviweka, lazima ayawajibishe ipasavyo, vinginevyo yataendelea kushuka na tutaendelea kupoteza mitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mashirika ambayo tusipoyaangalia vizuri ni cash cow ya Taifa hili. Mashirika kama TPA; mashirika mengi ambayo tukiwekeza vya kutosha, tutaweza kutengeneza mitaji na Taifa litaweza kujitegemea kwenye uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viko vikwazo vingi ambavyo vinafanya mashirika yetu yasifanye vizuri. Mojawapo ya hivyo vikwazo ni sheria yenyewe. Napendekeza Bunge hili liitishe hiyo Sheria ya TR, Tuifanyie marekebisho. Kwa upande wangu ningependa tuifute kabisa hiyo sheria tuanze upya, TR apewe mamlaka kwenye haya mashirika ambayo anayasimamia, awe na nguvu kiasi kwamba bodi ambazo zinashindwa kufanya vizuri, wakurugenzi ambao wanashindwa kufanya vizuri awawajibishe yeye mwenyewe, akisubiri mamlaka za uteuzi kuteua bodi mpya na kuteua wakurugenzi wapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mamlaka nyingine, kwa mfano, Ofisi ya TR Malaysia, TR ana uwezo uwezo mkubwa sana kusimamia mashirika ya Malaysia. Ukiangalia performance ya mashirika hayo yanafanya vizuri kiasi kwamba TR ana uwezo wa ku-suspend mamlaka yoyote ambayo iko chini yake bila kuuliza mtu yeyote. Ana mamlaka ya kufanya hivyo, baadaye anaandika ripoti kwa mamlaka za uteuzi, zinachagua mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Spika, ripoti yetu imebaini pamoja na mambo mengine, kuzorota kwa utendaji wa mashirika ya Uumma kunasababishwa na mambo kadha wa kadha. Mojawapo, limetokea kwenye ripoti ya CAG ukurasa wa 13 kwamba mashirika mengi uteuzi wa bodi unachelewa. Baadhi ya mashirika yanafanya kazi chini ya wakurugenzi ambao hawana bodi na baadhi ya mashirika yametajwa. Kwa mfano, Mfuko wa Kulinda wanyamapori Tanzania; Hospitali ya Rufaa Mbeya, Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania. Hayo ni baadhi ya mashirika ambayo yametajwa na ripoti ya CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukijiuliza kwa nini tunakuwa na mashirika ambayo hayana Bodi za Wakurugenzi? Mnajua fika, kama taasisi haina Bodi ya Wakurugenzi, Mkurugenzi na Watendaji wote hawawezi kufanya maamuzi ya kuliendeleza hilo shirika, watabaki tu ku-suspend maamuzi kwa sababu hawana chombo cha kuwa-guide. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ambalo limebainika ni mwingiliano wa majukumu kwenye baadhi ya taasisi. Jana nadhani Mheshimwia Dkt. Chaya aliyasema hapa. Baadhi ya taasisi zetu zinaingiliana kimajukumu. Jana ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Chaya alisema, TANROADS na TAA, kwamba tuna mamlaka mbili; tuna TANROADS ambayo kazi yake kubwa na ya msingi ni kutengeneza barabara. Ila hapo nyuma tumefanya maamuzi tukaipa TANROADS kutengeneza viwanja vya ndege, lakini tuna Mamlaka ya Kutengeneza Viwanja vya Ndege ambayo ni TAA.

Mheshimiwa Spika, utengenezaji wa viwanja vya ndege na usafiri wa anga kwa ujumla, kwa wataalam mnajua, usafiri wa anga unaendeshwa kwa misingi ya Kimataifa pamoja na miundombinu yake TAA na ujenzi wa viwanja vya ndege uko chini ya mamlaka ambayo inaitwa ICAO, ni mamlaka ya Kimataifa. Hii ndiyo inatoa viwango na vigezo. Kama unavyojua TAA inakuwa regulated na Mamlaka ya Usafiri wa Anga. Sasa unashangaa, ukijiuliza huyu TANROADS anajenga viwanga vya ndege kwa mamlaka ipi na kwa vigezo vipi?

Mheshimiwa Spika, nimesikia wakati tunaongea kwenye Kamati, TANROADS walikuja pale, wakasema wamechukua wataalam wote kutoka TAA wamewapeleka TANROADS. Najiuliza, kwa nini uchukue wataalamu kutoka TAA uwapeleke TANROADS? Kwa nini hiyo kazi ya kujenga viwanja vya ndege ambayo kisheria ipo chini ya TAA, wewe unafanya kazi ya kuhamisha watumishi na kuwapeleka kule. Hii inatupa wakati mgumu na inawapa mamlaka za udhibiti wakati mgumu hasa TCAA ambayo imekasimiwa jukumu la kuhakikisha kwamba viwanja vya ndege vinajengwa kulingana na mikataba ya Kimataifa ambayo inatolewa na ICAO kupitia Chicago Convention Annex 14 ambayo inakwambia viwanja vya ndege vijengwe kwa viwango vipi na ubora upi? Sasa hii tumeikasimisha TANROADS.

Mheshimiwa Spika, naomba ujenzi wa viwanja vya ndege urudi TAA na TANROADS wafanye kazi yao ya msingi ya kujenga barabara, siyo viwanja vya ndege. Kuna maeneo wanasema pale kwamba uwanja wa ndege ni sawasawa na kujenga barabara, siyo hivyo. Kila mwaka tunakuwa na ukaguzi ambao unafanywa na ICAO, tutakwenda mbele, tutafika wakati ICAO itatu-blacklist, ndege za Kimataifa zitashindwa kuja hapa na tutakuja kufanya marekebisho tumechelewa.

Mheshimiwa Spika, nadhani wakati wa kufanya marekebisho ni sasa, ujenzi wa viwanja vya ndege urudi TAA na TANROADS iendelee na majukumu yake ya kisheria. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Niwapongeze Serikali yetu ambayo iko chini ya Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambazo zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukiwa kwenye Kamati tulitembelea Mradi wa Ujenzi wa Meli ya Kisasa ya MV Mwanza Hapa Kazi tu. Katika maelezo tuliyopewa na Wakandarasi, tuliambiwa ujenzi wa meli unatumia chuma zaidi ya asilimia 60. Chuma chenyewe ambacho kinajenga meli yetu ya kisasa ambayo itaigharimu Serikali yetu zaidi ya shilingi bilioni 108 kinaagizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia gharama ya ujenzi wa meli, bilioni 108, kama tungekuwa na mkakati wa dhati wa kuchimba chuma chetu cha Liganga na Mchuchuma ina maana zaidi ya shilingi bilioni 64 zingebaki hopa nchini, zingechochea uchumi na zingeongeza ajira. Niishauri Serikali yangu suala la kuchimba chuma cha Liganga na Mchuchuma nadhani kwa sasa hatuhitaji mjadala mpana zaidi, ni suala ambalo lazima tulifanye kama tunataka kujenga uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa kanda ya Ziwa suala la meli ni suala la siasa ni suala la uchumi. Tunaishukuru Serikali kwa meli hiyo na tunamwombea Rais wetu na Mtendaji wetu Mkuu Waziri Mkuu wetu, wasukume kuhakikisha kwamba hiyo meli imekamilika na twende kuitumia kwa ajili ya uchumi wa kanda ya ziwa na Taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma Hotuba ya Waziri Mkuu ameongelea huduma kwa wazee. Kuna wachangiaji wameongelea wazee ambao ni wastaafu lakini tuna wazee ambao walitumikia Taifa hili katika nyadhifa mbalimbali. Vile vile, tuna wazee kama baba yangu ambaye alikuwa mkulima akizalisha kahawa ikiuzwa na kuchangia pato la Taifa. Hao wazee ni wengi na kusema kweli nimesoma hotuba ya Waziri Mkuu amewaongelea, lakini tatizo kubwa la wazee wetu wanahitaji na wao kutambuliwa. Kwa kutambuliwa huko hawahitaji tuwatambue kwa maneno, wanataka na wenyewe watambuliwe kwa kupewa ka- pension hata kama ni kadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewasahau sana hawa wazee wetu, wanahangaika, wanateseka, tunataka yanayotendeka Zanzibar, kama Zanzibar wanaweza wakawapa pension hawa wazee ambao hawakuwa wafanyakazi wa Serikali, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na wazee wa Tanzania Bara tuwaangalie. Ni wazee ambao wametulea, wametumikia Taifa hili katika nyanja mbalimbali kilimo, uvuvi, ufugaji naomba tuwape heshima yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewasikiliza wachangiaji wengi hapa tangu hotuba ya Waziri Mkuu tuanze kuichangia wachangiaji wengi wameongelea migogoro ya ardhi kati ya Taasisi za Serikali na wanavijiji na wananchi kwa ujumla. Kama tutapata majanga mbele ya safari matatizo haya yatatokana na umiliki wa ardhi tusipochukua hatua leo. Wachangiaji leo asubuhi alianza Mheshimiwa Ezra, jana tulikuwa na Mheshimiwa hapa Ndugu yangu Mheshimiwa Kwezi anaongelea kwao Sikonge kule, kila sehemu kuna matatizo makubwa sana ya ardhi na matatizo mengi unakuta ni kati ya Taasisi ya Umma aidha Hifadhi ya Misitu au NARCO ni matatizo ambayo yanasababishwa moja kwa moja na Serikali yenyewe au Taasisi zake, matatizo ya namna hiyo lazima tuchukue hatua za haraka sana kukabiliana nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana niliongelea suala la Mwisa hapa na Kaka yangu Mheshimiwa Mwijage ameongelea Rutoro, tunaongelea vijiji ambavyo vimesajiliwa kisheria, Taasisi ya Serikali inakuja kwenye hivyo vijiji kwa mantiki hiyo NARCO wanapima vitalu kwenye ardhi ya vijiji ambavyo vimesajiliwa kisheria na wanagawa hivyo vitalu wanamwachia mtu ambae amepewa kitalu kazi ya kuhamisha wananchi, hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatengeneza ukaburu mwingine, mwenye pesa mpishe na ukishakuwa kwenye vile vijiji mtu anakuja anakuhamisha hakuna chochote anachoondoka nacho. Hili tatizo lazima tutafute suluhu vinginevyo tutasabaisha matatizo makubwa kwa wananchi wetu na zaidi wananchi maskini, hawa ndiyo kazi kubwa ya Serikali ni kuwatetea na kuhakikisha kwamba wanaishi na wanapewa heshima kama wananchi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwisa ambayo ipo Muleba, wakati naingia kwenye Ubunge niliambiwa ni hekta 133,000 ni eneo kubwa sana ambalo kwa Wilaya ya Muleba na Mkoa wa Kagera lile eneo ndilo linazalisha chakula cha kulisha Wilaya ya Muleba. Watu wakaja pale kwenye ardhi ya vijiji vya wananchi wakapima vitalu, sasa wanataka waondoe wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sasa ukiondoa wananchi hilo eneo kutokana na ukubwa wake, linapakana na Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato na upande wa Magharibi kuna Ziwa Burigi lazima tuangalie na masuala ya ekolojia ya lile eneo, ukishawaondoa misitu itakatwa tutatengeneza jangwa lakini kikubwa zaidi lile eneo ndilo linalisha Wilaya ya Muleba na Mikoa Jirani, tutatengeneza baa la njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu na kuishauri lile eneo badala ya kupima vitalu twendeni tukalipime upya, tukatenge maeneo ya kilimo, tukatenge maeneo ya ufugaji tukatenge maeneo ya makazi ya wananchi, eneo ni kubwa hatuna haja ya kugombana gombana na watu hapa ni suala la kufanya matumizi bora ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho lile eneo ni eneo la Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, siyo suala la sijui la mifugo Hapana! hatujawahi kufanya taratibu za kisheria za kuhaulisha lile eneo kutoka kwenye miliki ya Hamlashauri ya Wilaya ya Muleba kulileta kwenye Wizara nyingine yoyote Hapana! Hapa tunavyoongea naishukuru Serikali yangu wameshatupa mpaka na Hati za Vijiji vimesajiriwa na havijawahi kufutwa huyu NARCO anatoka wapi? Mamlaka kapewa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa tumekuwa tukicheza na namba, leo hekta 130, kesho hekta 76 leo naambiwa ni hekta 43 hizi nyingine zimeenda wapi? Ndiyo maana naishauri Serikali tukapime lile eneo upya tujue lina ukubwa kiasi gani tukapange matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho. Sasa hivi tupo kwenye mfumo wa mavuno ya kahawa Kagera, nashukuru Waziri mkuu amefanya kazi nzuri na natumaini ataendelea kutufanyia kazi nzuri na nimeongea naye juzi hapa, tunaomba sasa msimu unapoanza wakulima wapewe ili vyama vya msingi vianze kununua kahawa yetu mapema, Mheshimiwa Bashe naona ameniangalia pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kukimbiana wakulima eti kahawa ni magendo, katika nchi ya Tanzania kati ya Kata na Kata naomba mwaka huu nitafurahi nisipo lisikia. Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Bashe uliniambia, ulisema kahawa ni mali mkulima siyo mali ya Serikali, inakuwa mali ya Serikali pale ambapo imenunuliwa kutoka kwa mkulima imeingizwa kwenye maghala itakuwa mali ya Serikali. Sikubaliani na magendo ya kutorosha kahawa kuipeleka nje ya nchi kwa sababu tutakuwa tunakosa kodi, lakini biashara ndogondogo za humo kwa humo kati ya Kijiji na Kijiji, Kata na Kata tuwaruhusu wakulima wakauze kahawa yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana tunaendelea na kazi ya kusafirisha abiria wetu Mkoa wa Kagera. Niliongea mwaka jana na nalirudia na litakuwa la mwisho na nitaendelea kulisema kwamba Uwanja wa Ndege wa Mkajunguti ni suala ambalo haliepukiki kwa sasa kutokana na wingi wa abiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi niliongelea suala la kiwanda cha Kahawa cha TANICA, kiwanda hiki kina miliki kati ya Serikali na Vyama vya Msingi, lakini kile kiwanda hakiwezi kuzalisha kwa uwezo wake na Kagera tunazalisha kahawa, kile kiwanda ndiyo kiwanda pekee ambacho kinaweza kutusaidia ku-process kahawa inayozalishwa Kagera ninakuomba Serikali itupatie mtaji wa kutosha ili kiwanda hiki kiweze kuzalisha at full capacity, sasa hivi kinazalisha under five percent sasa kiwanda gani hiki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kahawa ipo tunakimbizana na wauza kahawa, sasa hivi wanapeleka Uganda sijui wapi? Ni kwa sababu tumeshindwa kuingiza mtaji katika kile kiwanda. Serikali inaweza ikanunua zile hisa ambazo haijanunua mpaka leo ni Bilioni 8.6 ni hela ndogo! Mheshimiwa Bashe una hela nyingi na hicho kiwanda kipo chini ya Wizara yako, hebu tupeni hiyo hela tukaiongeze mtaji, tunanunulie teknolojia mpya tuweze kuzalisha, itakusaidia wewe na itatusaidia vijana wetu ambao mnawapa mtaji ili waweze kuzalisha lakini itaajiri vijana wetu na kuongeza pesa ya kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga hoja mkono na niwatakie mfungo mwema. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano. Kwanza kabisa nitamke tu kwamba naiunga mkono hoja, lakini mimi ni muumini wa uchumi wa soko na ninashukuru kwenye mpango tulioletewa sura ya tatu unaongelea ushiriki wa sekta binafsi kama chachu ya uchumi shindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo nitaongelea sekta ya kilimo. Kilimo kama tunavyosema ni uti wa mgongo wa nchi hii au Taifa letu, lakini ukiangalia maendeleo ya kilimo chetu hayaoneshi kwa vitendo kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa hili, nikiangalia kwenye mpango wenyewe tumeambiwa kilimo mpaka sasa kinachangia asilimia 27 ya GDP, lakini pia kinachangia asilimia 24 ya mauzo nje ya nchi. Nikilinganisha na nchi jirani nchi nyingine ndogo ambazo ukiangalia ukubwa wa Taifa lenyewe wao kilimo kinachangia asilimia 35 ya GDP na asilimia 40 ya mauzo nje ya nchi. Tunayo kazi kubwa ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo chetu kimebubikwa na mambo mengi ambayo nadhani katika mpango huu lazima tuyapatie wajibu, mojawapo ya haya matatizo tuliyonayo Taifa letu limekumbwa limekumbwa na ugonjwa wa kanuni na tozo nyingi kwenye sekta hii, kanuni zetu zimekuwa mnyororo zimekuwa broke ya kutufanya tusonge mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya yangu ninayotoka zao kubwa tulionalo ni zao kahawa, lakini zao hilo wakulima wanalima, wanajitahidi, wanakwenda kuuza na kanuni tuliyonayo mpaka leo kwamba mkulima akishalima lazima auze kwenye vyama vya msingi/ vyama vya ushirika na anapokwenda kuuza anayo matatizo yake, lakini awezi kulipwa pesa itabidi asubiri mwezi moja, wa pili, wa tatu na wakati mwingine miezi minne, lakini wakati huo huo tunavyo viwanda vinavoongeza thamani ya kawaha.

T A A R I F A

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO:Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongelea zao la kawaha Wilaya Muleba na Mkoa wa Kagera kwa ujumla kwamba kulingana na kanuni tulizonazo kwamba mkulima hawezi kuuza kahawa yake moja kwa moja kwa wafanyabiashara katika mkoa huo, lakini wakati Naibu Waziri wa Kilimo akijibu swali baadhi ya mazao wanaruhusiwa na pale Muleba wapo wafanyabiashara ambao wamewekeza kwenye kusindika zao la kahawa, lakini hawaruhusi kuuza kahawa hiyo moja kwa moja kwenye vile viwanda na kama tunavyofahamu kilimo na viwanda lazima tuvioanishe, matokeo yake wenye viwanda wanalazimika kununua kahawa hiyo kutoka vyama vyetu vya msingi kwa bei ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inayo madhara makubwa sana kwa uchumi, kwanza bidhaa wanayozalisha kutokana na kupata malighafi kwa bei ya juu haiwezi kushindana kwenye soko, lakini pia wakulima ambao wanauza bidhaa yao kwenye vyama vya msingi hawapati bei nzuri na wakati mwingine inawachukua muda kulipwa pesa yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni muda muafaka sasa kuruhusu wafanyabiashara ambao wamewekeza kwenye viwanda ambavyo vinasindika mazao yanayopatikanika katika maeneo mahalia badala ya kufungwa na kanuni ambazo zinazorotesha na kuumiza uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo taasisi ambazo zinashughulika na masuala ya ushindani, tuziruhusu kampuni binafsi zishindane na vyama vyetu vya ushirika na vyama vyetu vya msingi ili kuleta tija katika masoko yetu na kuhakikisha kwamba wakulima wanapata bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine na lamsingi na nzuri tukiwaruhusu wafanyabiashara hao kununua mazao moja kwa moja kutoka kwa wakulima ambao ni zao la kahawa, watahakikisha kwamba wanawapa pesa nzuri lakini pia wanaweza kuwafuatilia wakulima wale kuhakikisha kwamba wanazalisha na wanapatia msaada kuhakikisha kwamba mazao yao na mashamba yao yanakuwa bora muda wote na kilimo kinakuwa endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipatia fursa hii niweze kuchangia kwa dakika tatu kwenye hoja iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuja hapa Bungeni nilimueleza Mheshimiwa Waziri kwamba katika Jimbo la Muleba na Wilaya ya Muleba kwa ujumla tunayo changamoto kubwa ya mawasiliano na kwa heshima kubwa nilimpatia maeneo yote ambayo yana matatizo ya mawasiliano. Hata hivyo, leo wakati nasoma hotuba ambayo ameiwasilisha mbele yetu nimeshangaa sana, hakuna hata kata moja ambayo imezingatiwa kwenye bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri, kati ya kata zote ambazo nimempatia, kama mchangiaji aliyetangulia kusema Mkoa wa Kagera tunalo tatizo kubwa la mawasiliano, naomba chonde chonde atusaidie. Kata zote ambazo tumekupatia na sisi kama Mkoa wa kagera tunapaswa kuwa na usikivu wa mitandao, redio ambazo zinachangiwa na walipa kodi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo unakwenda ukipotea tu huwezi kupata msaada. Tunapoongelea Kata za Karambi, Mmbunda na Buhigi hakuna mawasiliano hata kidogo. Nilikuwa na dhamira ya kushika shilingi lakini najua Mheshimiwa Waziri ni msikivu nakuomba utakapokuja kuhitimisha bajeti yako useme neno ili wakazi wa Mkoa wa Kagera roho zao zitulie kwamba tunakwenda kuwawekea mitandao au mawasiliano ili na wao wajisikie wanaweza kuwasiliana na Watanzania wenzao na dunia nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipatia fursa ya kuchangia Wizara ya Elimu. Niwapongeze Mheshimiwa Waziri Mkenda, Naibu wake Ndugu yangu Kipanga, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Rais wetu kwa kazi kubwa anayoifanya hasa kwenye sekta ya elimu kwa kuwapatia pesa kubwa na nyingi inadhihirisha nia aliyonayo katika kuboresha elimu yetu. Naomba kutofautiana kidogo na wachangiaji waliyonitangulia, naongelea suala la mtaala ambao uko mbioni kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina wasiwasi tunapotengeneza mtaala kwenye ukachukua maandiko matakatifu yanasema “mvinyo mpya kwenye kiliba cha zamani haifai”. Tunayo Sheria Na. 25 ya Elimu ya Mwaka 1978 ilifanyiwa marejeo na Sheria Na. 10 ya Mwaka 1995. Sheria imepitwa na wakati, kama tunataka kuboresha elimu yetu lazima tuanzie huko kwenye sheria ndiyo chimbuko kubwa la kuboresha elimu yetu hata tufanye nini? Tubadilishe mitaala, tufanye nini? Hatutaweza kuboresha elimu. Turudi kwenye chanzo kule, tuboreshe elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo? Ukiangalia Wizara ya Elimu leo inaendeshwa kwa nyaraka. Zipo nyaraka nyingi sana na hizi nyaraka zinazotolewa na Wizara ya Elimu kila siku ni ishara kwamba kwenye sheria kuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye sheria, zipo nyaraka nyingi sana hapa ukisoma unahitaji unaweza ukafanya research ya PHD. Kwenye maeneo kumi na tatu mahususi ya elimu zipo nyaraka rukuki kwa mfano ukiangalia nidhamu na malezi zipo nyaraka tisa, ukiangalia kamati ya bodi za shule nyaraka sita, udahili wa wanafunzi nyaraka kumi na saba, ukienda mihula na siku za masomo nyaraka tatu, michezo nyaraka tano, elimu ya ualimu nyaraka tisa, kufukuza kurekebisha na kuamisha wanafunzi nyaraka kumi na moja. Uendeshaji wa mitihani nyaraka kumi na sita, ukienda masharti ya usajili wa shule nyaraka sita, kukuza uzalendo hapo kuna nyaraka moja sijui kwa nini? Nyaraka ya ajira za nje moja, ada na michango nyaraka kumi na nne, taaluma ufaulu na ufundishaji wa rula nyaraka ishirini na nane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti sasa ukiangalia hizo nyaraka nane anazitoa kafanya utafiti wapi? Unatoa nyaraka kwa sababu wanataka ku–supplement kuna madhaifu makubwa katika Sheria ya Elimu. Sasa nadhani tunapoongelea mitaala tuangalie sera yetu, tuangalie sheria yetu tuweze kuioanisha, tuweze kupata kitu ambacho ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuishauri Wizara ya Elimu, zimetoka nyaraka nyingi sana na juzi juzi hapa ilitoka nyaraka ya watoto wa bweni, nursery school wasiende boarding, waingie bweni wakiwa darasa la tano. Tunaenda wapi? Tunakwenda mbele, tunarudi nyuma? Hebu tuangalie uchumi wetu, kadiri uchumi unavyokua watu wanavyokuwa na pesa ndivyo watu wanavyo wajibika zaidi kwenye sekta za uzalishaji. Sasa kupanga ni kuchagua, Serikali kazi yake ni kudhibiti ni kufanya kazi ya regulatory regulations siyo kupangia watu waishije? Wasomesheje watoto wao? Hiyo siyo kazi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifikiri kadri tunavyotarajia kwenda kwenye uchumi wa kati, ndivyo watu wanavyokwenda kuwajibika zaidi kwenye sekta binafsi na sekta nyinginezo. Sasa mtu anaamua mtoto amwachie nani? Amwachie maid hawapatikaniki siku hizi. Kwa hiyo, chaguo halisi ambalo mzazi analiona kwa wakati huo ni kumpeleka shuleni bweni ambako ana uhakika na malezi ya mtoto wake. Niwaombe Wizara ya Elimu tulitafakari hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tena kuishauri Wizara ya Elimu tuiangalie private sector. Private sector ina shule nyingi, inaajiri watu wengi na imewekeza mitaji kwenye elimu hii lakini kwa macho ambayo unaiangalia private sector ni kama mshindani wa Wizara ya Elimu si kweli. Private sector ina supplement pale ambako Serikali haiwezi kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia private sector imewekeza kiasi gani kwenye Wizara hii? Tukiangalia private sector inaajiri walimu wangapi katika Taifa hili? Inalipa mishahara walimu wangapi kwenye sekta hii ambao wengekuwa redundant kama wasingekuwepo? Nashauri, Mheshimiwa Waziri private sector tuichukulie kama ndugu yetu siyo mshindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia mahusiano kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara ya TAMISEMI, mahusiano yale hayana tija. Ukiangalia kule TAMISEMI tuna wadhibiti ubora mikoani, tuna wadhibiti ubora wilayani, hao wote wanawajibika kwa Waziri wa TAMISEMI, lakini wanafanya kazi ya Waziri wa Elimu. Kuna mpingano, kuna mkorogano hapo katika mahusiano kati ya Wizara ya Elimu na TAMISEMI. Lazima tuliangalie; na ndiyo maana mimi nashauri badala ya kwenda kwenye mitaala tuangalie kwanza sera na sheria zinasemaje kama tunataka kuleta utulivu kwenye sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda huko hata kwenye shule binafsi, unakwenda TAMISEMI wanasema ya kwao, Wizara ya Elimu wanasema ya kwao. Tumefanya hivyo kwenye sekta ya maji, tumefanya hivyo nadhani na sekta ya TARURA. Nashauri watendaji wote ambao ni wadhibiti ubora ambao wako TAMISEMI warudishwe Wizara ya Elimu. Tuwe na Wizara moja ambayo inafanya kazi ya kusimamia elimu na TAMISEMI wabaki na suala la kusimamia miundombinu tu, masuala ya kisera yote yarudi Wizara ya Elimu, vinginevyo tutakuwa tunacheza mdundiko hapa. (Makofi)

Mheshimwia Mwenyekiti, yanatoka maagizo, yanatokea TAMISEMI; Wizara ya Elimu hawayakubali. Mengine ya Wizara ya Elimu, TAMISEMI hawayakubali; tunakwenda wapi? Nadhani tunapaswa kuoanisha haya mambo. Serikali ni moja, Taifa ni moja na ni Serikali ya Awamu ya Sita ya mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nawaomba mkae chini mkayangalie haya mambo, tuwe na Wizara moja mahsusi inayo–regulate na inayoratibu masuala yote ya elimu kama sera na sheria zinavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nirudi kwenye jimbo langu. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana, tunakushukuru sana hasa Mkoa wa Kagera, na salamu zetu tunaomba umfikishie mama yetu Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan; kwa miaka nenda-rudi Mkoa wa Kagera tumepigania kupata chuo kikuu. Tumejaribisha kupitia private sector tulishindwa, vikaja vyuo ambavyo vilianzishwa na mashirika ya dini vinajikongoja. Kama mnavyofahamu, Mkoa wa Kagera ni mkoa wa elimu, upende usipende ndivyo ilivyo, ndiyo historia yetu. Kwa kutupatia chuo kikuu chini ya mradi wa HEET tunakushukuru sana na tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi niende kwenye Wilaya yangu ya Muleba, Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana, juzi hapa tumepewa taarifa wametupelekea takribani milioni 900 kwa ajili ya chuo chetu cha VETA. Kulikuwepo na chuo kidogo hakikuwa na heshima ya Wilaya ya Muleba. Tunakushukuru sana na tunakuomba sasa hicho chuo kijengwe haraka sana. Lakini kama wengine walivyosema, tunapojenga hivi vyuo vya VETA na tunavyotoa elimu yetu, mwaka jana kuna mchangiaji mmoja alichangia hapa, tuangalie tunachofundisha watoto wetu. Walikuwa wanaongelea mambo ya historia, eti tulifundishwa mwanadamu ni evolution, alitokea kwenye nyani na bado tunaendelea kufundisha haya mambo kwa watoto wetu. Hivi kwa nini tusikae chini tukatafakari tukaja na mfumo wetu wa elimu wa kuwafundisha watoto wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nilikuwa naangalia kwenye mtaala ambao wameutoa, Mimi naomba nishauri, ukiangalia mpangilio wa yale masomo mliyoyaweka bado tuna mentality ile ile ya miaka ya 1960. Mimi nilitarajia tuangalie dunia inakwenda wapi, na uchumi unaelekea wapi. Sasa hivi unapoongelea kufundisha watoto unakwenda kuwafundisha historia zilizopitwa na wakati, haina tija kwa watoto wetu na haina tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninadhani tungeelekeza nguvu zetu kwenye kufundisha TEHAMA, kufundisha innovation, consumer protection ili watoto wetu wakue wanajua mambo gani ya msingi ya Taifa lao. Taifa letu linasimamia nini? Ukienda nchi za wenzetu unamuuliza mtoto kwa mfano Tanzania inasimamia nini, ukiwauliza watoto wa Kimarekani watakwambia Marekani inasimamia nini miaka 100 ijayo, lakini sisi hapa ukituuliza itategemea tu kama mvua imenyesha, kama kuna maji mito imefurika, tuje na kitu mahususi cha kuwafundisha watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye VETA zetu; hivi hizi taasisi zetu ambazo ziko chini ya elimu sijui SIDO, sijui nini, zinafundisha nini watoto wetu? Hii mitaala kweli inaendana na hali halisi ya maisha yetu Watanzania? Sioni. VETA iko Kagera unawafundisha sijui vitu gani? Badala ya kuwafundisha kutengeneza nyavu, kuwafundisha kuvua samaki, tunafundisha vitu ambavyo tumevi-import kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga hoja mkono.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru sana kupewa fursa ya kuchangia bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze viongozi wa Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi; Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri mnafanya kazi kubwa na kusema kweli mnapeleka kicheko kwenye mikoa na wilaya zetu na Majimbo yetu. Niwapongeze watendaji wakuu na taasisi zote zilizoko chini ya Wizara hii, kusema kweli bila wao hata Waziri hii kazi ambayo inaonekana haiwezi kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nazipongeza Wizara zote ambazo ziko chini ya Serikali ya Mama yetu Samia Suluhu Hassan, zinafanya kazi nzuri. Katika Jimbo langu na Wilaya yangu ya Muleba Wizara zote zinafanya kazi nzuri isipokuwa Wizara moja tu ambayo badala ya kutuletea kicheko wanatuletea kilio na hiyo si wengine ni watu wa NARCO, hawa wanatuletea kilio kwenye Jimbo langu la Muleba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa barabara; Mheshimiwa Waziri tumeongea sana hii barabara ya Muleba – Muhutwe – Nshamba - Muleba ni barabara yenye kilometa 54 tangu awamu ya nne tumekuwa tukijenga hii barabara kipande kwa kipande. Mheshimiwa Waziri uliniahidi kwamba mwaka huu, mwaka jana nilikuona lakini mwaka huu ukasema barabara hii tutaipatia kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma bajeti yako Mheshimiwa Waziri nimekuta umetupatia kilometa sita tu, Mheshimiwa Waziri kwa kilometa sita tutaimaliza barabara labda tutachukua miaka 50. Chonde chonde Mheshimiwa Waziri hebu angalia kwenye bajeti yako Mheshimiwa, hii barabara imejengwa kwa muda mrefu, tunaomba katika awamu hii tumalize hii barabara huu wimbo tufunge ukurasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii nimesoma mmetutengea pesa kwa ajili ya madaraja mawili Kyabakoba na Kamashango na haya ni madaraja makubwa ambayo katika Bonde la Mto Ngono. Lakini kilichowekwa pale tumeweka feasibility study, upembuzi yakinifu sijui na usanifu nini. Lakini na hii mwaka jana ilikuwa imetengewa pesa kwa ajili ya usanifu na upembuzi yakinifu, lakini hakuna kilichofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaimani kubwa na Waziri ninaimani kubwa watendaji wa Wizara hii, ni watu makini, Mtendaji wa TANROADS Engineer Aisha Amour ninamuamini na utendaji wa kazi unaonekana, Ndugu yangu Migire nawaamini sana. Nawaomba barabara hii na madaraja haya mawili tukayamalize mwaka huu. (Makofi)

Lakini kuna daraja lingine mmelisahau Mheshimiwa Waziri kuna daraja la Marahara na lenyewe linahitaji kufanyiwa kazi kwa sababu ni sehemu ya hiyo barabara. Ninatumaini kwa kazi na mwendo wenu hii kazi mtaifanya na itakamilika kwa wakati.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba Mtendaji wa TANROADS Engineer Mativila na Katibu Mkuu ndiyo Engineer Aisha, ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Ishengoma.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunikumbusha na naipokea taarifa yake kumbukumbu zikae salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera na hususan Wilaya ya Muleba tuna visiwa 39 na katikati ya Ziwa Victoria tuna kata tano ambazo zinaundwa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba na hizo kata mpaka tunaongea hazina usafiri wa uhakika. Lakini niishukuru Wizara inayo mpango wa kutuletea meli ya Clarias kuanzia Mwanza kwenda kutembelea visiwa vya Ziwa Victoria, niwashukuru. Lakini huo mpango wa kutuletea hiyo meli ulianza kuasisiwa tangu mwaka jana, lakini mpaka sasa tunavyoongea tunasubiria hiyo meli ianze kufanya kazi. Na taarifa nilizonazo ni kwamba tunaisubiri TASAC itoe okay ili meli hiyo ianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimweleze Mheshimiwa Waziri kuwa wananchi wanaisubiria hiyo meli kwa hamu kubwa, tunaomba hao TASAC ambao wako chini ya Wizara yako kawahimizehimize najua watachangamka na najua ni vijana wazuri sana, wakatoe kibali hiyo meli ianze kufanya kazi kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika kupanga utaratibu wa hiyo meli, awali ilikuwa itoke Mwanza iende Godziba, iende Kerebe, iende Bumbile iishie Kyamkwiki. Lakini tuna bandari yetu ndogo ya Katembe Magarini ambako tumepata kibali cha kuanzisha soko la kimataifa la kuuza dagaa. Kwa kuwa pale kuna mzigo mkubwa na hiyo bandari ndogo iko chini ya TPA na hapa tunavyoongea nawashukuru TPA wanaendelea kuijenga na kuikarabati hiyo bandari yao kwa sababu gati ilikuwa imezama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale tutatengeneza pesa kwa sababu kuna mzigo mkubwa wa dagaa lakini itatusaidia ku-promote hata bandari yetu na soko letu la kimataifa ambalo limeanza kufanya kazi kwa sasa. Kwa hiyo naomba katika mpango wa awali tukaingize na hiyo kituo cha Katembe Magharini ili hiyo meli yetu tutapoanza na kuchakata na kufanya kazi itoke Katembe Magarini na mzigo wa dagaa ikawalishe watu wa Mwanza. Tutakuwa tumefanya biashara, lakini tutakuwa tumeongeza kwa ajili ya Wilaya yangu ya Muleba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Katemba Magarini watu wa TEMESA tangia mwaka jana wamekuwa wanasema wanajenga gati kwa ajili ya kuegesha vivuko kwa ajili ya Katembe Magarini hadi Ikuza. Lakini na huu umekuwa wimbo wa Taifa Mheshimiwa Waziri na hakika kwenye bajeti hii na hapo kwenye bajeti yako umeitaja na umeitengea pesa. Naomba sasa hii kazi ifanyike na ikamilike kwa wakati ili wananchi wetu waendelee kufaidi matunda ya uhuru wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la mwisho. Ndugu yangu Kyombo ameongelea uwanja wa ndege wa Omukajunguti. Nimeona kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri ametenga pesa kwa ajili ya kujenga jengo la VIP uwanja wa ndege wa Bukoba, kukarabati mita 200 kuongezea njia ya kuruka na kutua ndege na kuongeza kujenga taa za kuongozea ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwa kutupatia hivyo vyote, lakini kwa wakati tulionao ukichukua mazingira ya Mkoa wa Kagera, mahitaji ya sasa ya Mkoa wa Kagera tunahitaji uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Omukajunguti, huu uwanja tuendelee kufanya haya tuliyoyafanya lakini kule kutokana na jiografia ya Mkoa wa Kagera, Kagera sasa baada ya DRC kuingia Afrika Mashariki tutakuja kuleta hoja hapa Kagera ndiyo ipo katikati ya Afrika Mashariki kwa sasa. (Makofi)

Kwa hiyo tutahitaji uwanjwa wetu wa Omukajunguti na tutaendelea kuisemea na tunaomba Mheshimiwa Waziri na leo wakati tuko mapumziko nimeongea na Mtendaji wako kijana machachari Wakili Mbura. Tukaliongelea hili akasema watakwenda kuliangalia, nakuomba Mheshimiwa Waziri mliangalie uwanja wa ndege wa Omukajunguti ni wa siku nyingi na wakazi wa Mkoa wa Kagera tunahitaji uwanja huo. Naendelea kuwashukuru kwa utendaji mzuri wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni la utawala bora; Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ina taasisi zake ambazo zinafanya kazi vizuri, lakini na taasisi nyingine ndogo ambazo ziko chini ya Wizara ya Uchukuzi; moja iko chini ya LATRA na nyingine iko chini ya TCAA. Tuna mabaraza ya ushauri wa watumiaji wa huduma zinazodhibitiwa na mamlaka hizo. Lakini kwa bahati mbaya nilikuwa naangalia bajeti na huu umekuwa uzoefu wa muda mrefu sana hayo mabaraza hayatengewi bajeti, yanabaki kwa utashi wa Wakurugenzi ambao wanaongoza hizi mamlaka, na matokeo yake imekuwa kwamba Mkurugenzi akikuangalia vibaya asubuhi ataamua akutengee kiasi gani cha pesa.

Nashukuru Wizara ya Mawasiliano huwa wanawatengea pesa, Mheshimiwa Waziri unajua mchakato tuliyokuwa nao na ugumu tunaopitia na hizi taasisi ndogo ndogo naomba kuanzia labda bajeti ijayo nashauri tu haya mabaraza yatengewe bajeti na tuione kwenye bajeti ya Serikali inayoletwa hapa Bungeni kwa sababu na zenyewe ni taasisi za umma. Hatuwezi kuziacha mtu mmoja apange bajeti kwa ajili ya hizi taasisi ni makosa makubwa Mheshimiwa Waziri.

Kwa hiyo nashauri na kupendekeza haya mabaraza yanafanya kazi kubwa, yanafanya kazi nzuri ya kuelimisha umma na yenyewe tuone bajeti yake katika haya, kwa sababu na yenyewe yanakuwa audited na CAG, kwa hiyo, wana wajibu na wana haki ya bajeti yao kuonekana hapa. Yameanzishwa kwa sheria na yanafanya kazi yana bodi zake lakini nashangaa kwa nini yabaki huku yakilelewa na mtu mmoja ambaye wakati mwingine anaamua tu kuya-suffocate na kufanya anavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa kazi nzuri wanayoifanya nawaunga mkono hoja na naomba Wabunge wenzangu tuunge mkono hii bajeti ipite waende wakafanye kazi, nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Mimi natokea Kamati ya PIC. Nitaongelea ufanisi…

MWENYEKITI: Waheshimiwa, naomba tupunguze sauti tuwasikilize wachangiaji wetu.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea ufanisi wa mashirika yetu ya umma. Kamati imepitia mashirika ambayo Serikali yetu imewekeza zaidi ya trilioni 73.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa mitaji katika mashirika yetu, pamoja na uwekezaji mkubwa ambao Serikali imeweka lakini ukuaji wa mitaji unatia shaka na wasiwasi. Kwa kipindi cha miaka mitatu, ukuaji wa mitaji katika mashirika yetu ya umma ni asilimia nane tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama watangulizi waliochangia walivyosema, Serikali imewekeza fedha nyingi katika mashirika yetu ya umma lakini return katika uwekezaji ni mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kuwekeza trilioni 73 katika mashirika ya umma hayo mashirika ya umma yanayo matobo mengi sana. Asubuhi tumesikiliza ripoti tatu ambazo zimesomwa na Kamati tatu, kwa kweli inahitaji moyo mgumu kuzipokea na kuzikubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uwekezaji katika mashirika yetu ya umma; mashrika yetu mengi yanasuasua. Serikali inawekeza fedha ya walipakodi lakini mapato yanayotokana na uwekezaji huo ni madogo. Tunayo kazi kubwa mbele yetu ya kufanya ili kuhakikisha kwamba uwekezaji unaendana sambamba na mapato tunayoyapata kutokana na uwekezaji huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya PAC imetoa taarifa yake asubuhi, kati ya mashirika 66 ambayo yalipaswa kutoa gawio ni mashirika 25 ambayo yametoa gawio, mashirika 41 hayajachangia chochote. Ni kana kwamba Serikali kwa kipindi cha miaka mitatu haijawahi kuwekeza fedha yoyote ya walipakodi; lakini tunajua Serikali imewekeza fedha nyingi lakini mashirika yanafanya vibaya na tumenyamaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo mashirika 25 ambayo yamesema yamechangia mfuko mkuu wa Serikali ni mashirika matatu tu ambayo yamechangia zaidi ya asilimia 38, na hayo yametajwa hapa; ni BOT imechangia bilioni 200, Airtel imechangia bilioni ishirini na kitu na NMB; mashirika mengine yote yanasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimenangalia hata kwenye mchango wa GDP mashirika yetu haya ambayo tumewekeza zaidi ya trilioni 73 kwa kipindi cha miaka mitatu mwaka 2019/2020 kwenye GDP yamechangia 0.6, yaani hata asilimia moja haifiki. Tumewekeza fedha nyingi lakini tunachokipata kama Taifa ni kidogo mno. 2020/2021 yamechangia 0.5, 2021/2022 ni 0.6 kwenye GDP, 2022/2023 0.6; kwenye bajeti yanachangia asilimia tatu kwa miaka mitatu mfululizo. Sasa tunajiuliza tunawekeza ili iweje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapowekeza kwenye kitu chochote; amesema mchangiaji wa mwisho kwenye TANOIL; tunapowekeza fedha ya walipa kodi tunatarajia baada ya mwaka mmoja au miwili tuweze kuvuna; na kama tunawekeza bila kuvuna haina maana yoyote ya kuwekeza kwenye haya Mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeangalia gawio, haya Mashirika ambayo hayakuleta gawio ni hatua gani zinachukuliwa na Serikali? Lakini kwa kipindi cha miaka mitatu hakuna hatua yoyote imechukuliwa dhidi ya mashirika ambayo hayakutoa gawio. Tunachokisikia ni Mkurugenzi anahamishwa anatolewa shirika moja anapelekwa shirika jingine na anapopelekwa kwenye shirika jingine ni business as usual.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo tunalijua, mwaka jana nilichangia hapa, kwamba tatizo la mashirika yetu ni sheria ambayo tunayo ambayo inaongoza mashirika haya. Mwaka jana nilisema na nikashauri, kwamba kama tunataka ufanisi kwenye mashirika ya umma lazima twende kubadilisha sheria ambayo ni kongwe sheria ambayo haimpi pia uwezo wa kuyasimamia mashirika haya ya mmma…

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Oscar kuna taarifa.

TAARIFA

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri wa Mheshimiwa anayechangia nataka tu nimpe taarifa kwamba siyo sahihi kusema kwamba hakuna hatua yoyote inayochukuliwa kuhusu mashirika ya umma ambayo hayafanyi vizuri. Mnafahamu mwaka jana na mwaka huu Mheshimiwa Rais aliagiza mashirika ambayo yanasuasua yachukuliwe hatua na mnafahamu mwaka huu Msajili wa Hazina ametangaza hadharani kwamba yapo Mashirka ambayo yanakwenda kufutwa, yapo ambayo yanakwenda kuunganishwa. Lakini muhimu zaidi tumetangaza hadharani kwamba tunaanzisha sheria mpya ya kuyaangalia mashrika haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nakubaliana naye kwamba kuna Mashirika yana changamoto lakini siyo sahihi kusema kwamba hakuna hatua zozote ambazo zimechukuliwa. Kuna hatua zipo zinachukuliwa, ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilitoa ushauri huo kama umechukuliwa na kama hatua zimechukuliwa tumshukuru Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ku-merge mashirika au kuunganisha mashirika bila kutibu ugonjwa unaotafuna mashirika yetu ni kazi bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria iiliyopo ya sasa ambayo wanasema wanakwenda kuifanyia marejeo kimsingi hatupaswi kufanya marejeo kwenye sheria iliyopo tunapaswa kutunga sheria mpya. Mwaka jana nilisema, kama Maandiko Matakatifu yasemavyo huchukui wine mpya ukaweka kwenye viriba vya zamani. Sheria iliyopo haifai, sheria iliyopo ni ya mwaka 1959, kipindi ambacho Taifa hili lilikuwa halijapata uhuru mpaka sasa bado tunatembea na sheria kongwe ya namna hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashuri na kupendekeza kwenye Sheria itakayotungwa ihakikishe inampatia uwezo TR kuyasimamia mashirika haya ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri au kupewa uwezo wa kuteua bodi kuzisimamia bodi na kuwasimamia watendaji wakuu wa hayo. Kama tunataka kufanya biashara tuondokane na tabia ya uteuzi wa Wakurugenzi kwenye mashirika yanayofanya biashara. Kama tunataka kwenda kufanya biashara kufanye biashara kama kampuni nyingine zinavyofanya; kwamba watendaji wakuu wapatikane kwa njia ya ushindani badala ya uteuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haya mashirika yenyewe haya TR mpaka wakati huu tunapoongea hana mfuko wa kuyasaidia haya mashirika katika mizania ya uwekezaji. Tumeona mashirika mengi yanapotokea matatizo yanakosa uwezo wa kukabiliana na matatizo ya kibiashara; TR hana uwezo wa kifedha kuyasimamia wanabaki kusubiri Serikali iwapatie fedha na wakati mwingine fedha ya Serikali inaendana na bajeti ambayo Bunge lako limeipitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kamati yetu tumebaini baadhi ya matatizo ambayo mashirika yetu yanakabiliana nayo; mojawapo ni kuchelewesha kumaliza miradi ya maendeleo. Tumeangalia kipande cha SGR kutoka Dar es salaam mpaka Morogoro kwa kipindi cha miaka mitatu tumeongelea hili tatizo tunasubiri nini? Tunaambiwa kipande kimekamilika asilimi 98.9 lakini kwa kipindi cha miaka mitatu tumekuwa tukisikiliza maneno yaleyale kutoka kwa watu walewale, hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi mingine ya TANROADS; tuna Mradi wa Nyakanazi stopover tulikuwa na mradi wa kusuka magari pale Nyakanazi na mwingine upo pale Manyoni, hii miradi imesimama tangu mwaka 2016. Serikali imewekeza fedha yake pale ya walipakodi lakini hakuna kinachoendelea. Tunajiuliza, hivi wakati tunakwenda kuwekeza pale tulifanya upembuzi yakinifu au tulifanya due diligence au watu waliamua tu wakaamka wakaenda kufanya uwekezaji pale? Fedha ya walipa kodi imesimama, fedha ya walipa kodi imetumika na hakuna tija katika uwekezaji huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi napenda nishauri Serikali, tunapoamua kutekeleza miradi ya maendeleo, tunapoamua kuwekeza katika sekta yoyote kwanza tumalizie miradi viporo ndio twende kwenye miradi mipya vinginevyo miradi ya zamani haikamiliki na tunayoendea mipya haikamiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili la mwisho tumeongelea miradi ya maji; Serikali hususani Wizara ya Maji ilishatoa kiwango cha upotevu wa maji hapa nchini isizidi asilimia 25, wengi wamelisema hili, nitaomba nimalizie na hilo. Lakini ukiangalia mamlaka zetu za maji, mamlaka nyingi upotevu wa maji unakwenda zaidi ya asilimia 38 na tusipochukua hatua mapema, na muona Mheshimiwa Waziri wa Maji yupo, tusipochukua hatua mapema kwa uzembe ambao nauona watu mamlaka zinaanchaia mabomba hata leo nyumbani kwangu pale maji yanamwagika siku saba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: …tusipochukua hatua mapema maji tunayozalisha asilimia 50 yatapotea na tutakuwa tumewekeza fedha lakini wananchi hawapati maji kadri inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupewa fursa hii ya kuchangia Mpango huu. Nitajikita kwenye maeneo mawili; nitaongelea kilimo na uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mpango, umeongelea kwa kina suala zima la kilimo. Kama Wabunge wengi walivyochangia, kilimo ndiyo sekta pekee ambayo inaakisi uchumi jumuishi; inaajiri Watanzania zaidi ya asilimia 65. Kama Waheshimiwa Wabunge wengi walivyosema, kilimo hatujakipatia msukumo ambao kinastahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea zao moja. Kama Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma wanavyosema, kwa Mkoa wa Kagera zao la kahawa ni siasa, zao la kahawa ni elimu, zao la kahawa ni kila kitu. Miaka ya 1970 Mkoa wa Kagera ulibahatika kuwa na wasomi wengi kwa sababu ya zao hili la kahawa. Leo tunapoongea, Kagera zao la kahawa limekuwa kama laana. Bei imeshuka na wanapouza hata bei kama ni ndogo, bado kupata hela zao inawachukua zaidi ya miezi mitatu kama dada yangu Mheshimiwa Conchesta alivyosema pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la kahawa kwa Mkoa wa Kagera linahusisha kaya nyingi kama ilivyo kwa Taifa zima. Nilikuwa naangalia takwimu hapa. Zaidi ya 90 percent ya kahawa inazalishwa na wakulima wadogo wadogo. Hawa wakulima wadogo wadogo ndio wazazi wetu, kaka zetu, wadogo zetu, ambao wanahangaika usiku na mchana kuhakikisha kwamba wanapata pesa ya kusomesha watoto wao, kutunza familia zao na kuhakikisha kwamba wazazi wao wanaendelea kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo liko wapi? Naishukuru Serikali, kwa miaka mitano iliyopita walifuta tozo karibia 20 kwa zao la kahawa, tunawashukuru kwa hilo, lakini walipofuta hizi tozo, hatujatafuta suluhisho la bei na mauzo ya zao la kahawa, tumeviachia vyama vya msingi vinunue kahawa kutoka kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna sekta binafsi, tunaihusishaje kuhakikisha kwamba na wao wananunua kahawa kwa Mkoa wa Kagera ili kuleta ushindani? Tumeviachia vyama vya msingi peke yao, vinafanya kazi vinavyotaka vyenyewe, vinalipa wakati vinapotaka vyenyewe. Hata hivyo, kuna wazawa wa Tanzania ambao wamewekeza kwenye viwanda vya kusindika kahawa, tunawaambia hao kama unataka kununua kahawa, kanunue kwenye vyama vya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri atuambie, tunaoanishaje kilimo na Sekta ya Viwanda? Unapowaambia wanunue kwa vyama vya msingi, watanunua kwa bei ya juu kuliko wangekwenda moja kwa moja kununua kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna maneno hapa yanasemwa, eti watakwenda kuwalangua wakulima. Ndiyo! Wakalangue kule, lakini Serikali ihakikishe kwamba inaweka mazingira sahihi na mazingira huru kuhakikisha kwamba vyama vya msingi vinanunua na wafanyabiashara wananunua bila kuwaathiri wakulima wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mpango namshukuru Waziri, amesema tunakwenda kujenga uchumi shirikishi na uchumi shindani. Tunayo Sheria ya Ushindani hapa nchini, tuweke mazingira huko kwenye vijiji vyetu kuhakikisha kwamba hata huyu; vyama vya msingi na vyama vya ushirika vishindanishwe na wakulima na wanunuzi binafsi ili kuleta uwiano na ushindani kwenye masoko yetu. Tusimlinde huyu. Mnajua madhara ya uchumi hodhi? Mnajua matatizo ya protectionism? Tumevilinda kwa muda mrefu vyama vya ushirika na vyama vya msingi na tunajua matatizo yake kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaporuhusu ushindani, tunakaribisha ubunifu, tunakaribisha teknolojia na tunakaribisha wakulima wapate a fair deal kwa mazao yao wanayoyalima huko kwenye majimbo yetu. Nawaomba ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tushirikiane kuhakikisha kwamba baadhi ya sheria na Mashirika ambayo hayatuongezei ufanisi kwenye maeneo yetu tunakotoka, aidha, sheria zao wazilete hapa tuzipitie upya kuona kama zinatuongezea ufanisi au tufute. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi nilikuwa nasoma kitabu kimoja wachumi wanakifahamu vizuri sana, “Why Nations Fail? The Origins of Power, Prosperity and Poverty.” Mwandishi anatuambia na kutushauri, kama tuna mashirika ambayo hayana ufanisi, tunakaribisha umasikini kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, nishauri kwenye hili, Wizara kwa kushirikiana na sekta binafsi tuhakikishe suala la zao la kahawa Mkoa wa Kagera lipatiwe ufumbuzi wa haraka, watu wapate bei nzuri na sekta binafsi ihusishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo, tatizo tulilonalo kwenye hili zao lenyewe la kahawa kutoroshwa kuuzwa nchi za nje litakwisha. Pia, tutakuwa tumeboresha Sekta ya Viwanda; kwenye jimbo langu tunavyo viwanda viwili vinasindika mazao ya kahawa, lakini wanalazimika kununua tu kwenye vyama vya msingi kwa bei ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni uvuvi. Tunalo Ziwa Victoria ambalo linazalisha, lakini ukiangalia takwimu za uvuvi na faida tunayoipata kutoka katika ziwa hili ni aibu. Sisi kama Tanzania, niliwahi kulisema hapa mwezi wa Pili. Tunamiliki eneo kubwa zaidi ya kilomita za mraba 35,000 ambazo ni sawa sawa na asilimia 51 na wenzetu asilimia 43; lakini ukiangalia tunachokipata na tunachokiuza nje, hakuna uwiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hapa nilikuwa nasoma ripoti moja, tumeambiwa sisi tunauza nje kwa asilimia 51 ukilinganisha na majirani. Kwa uchumi wetu tunachangia only two percent ya GDP, Uganda 3%, Kenya 2% na wenyewe. Ukiangalia viwanda ambavyo vimejengwa, Uganda wanaongoza, wana viwanda zaidi ya 20; sisi ambao tuna asilimia 51 tuna viwanda vinane tu na Kenya wana viwanda vitano. Tunaambiwa viwanda vinazidi kuporomoka kwa upande wetu na vinazidi kuongezeka Kenya na Uganda wenye eneo dogo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tunafanya hayo na sisi tuko hapa? Kazi kubwa tunayopaswa kuifanya kama tunataka kuchochea uchumi, ni kuhakikisha tunavuna hizi fursa ili wananchi wetu waweze kuchangamkia uchumi wetu. Hata mazao tunayoyapata kutokana na uvuvi ili yasafirishwe kupelekwa kwenye masoko ya nje, yanapitishwa Uganda na Kenya; Entebe na Jomo Kenyatta International Airport. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka ya nyuma tulifanya maamuzi mabaya, tuliweka a five percent surcharge kwa total consignment ya minofu ya samaki kutoka Mwanza. Ilifikia mashirika yote ya ndege yakakimbia. Mpaka leo ili tusafirishe minofu ya Samaki, lazima twende Entebe au Jomo Kenyatta International Airport. Kwa nini, Mheshimiwa Naibu Waziri? Ukiangalia chanzo chake ni tozo tulizojiwekea sisi wenyewe na tulizipitisha hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naongea tu, mabondo; ili usafirishe mabondo tuna tozo ya shilingi 7,500/= kwa upande wa Tanzania; Uganda ni shilingi 436/= na Kenya ni shilingi 34/=. Ukipitia tozo zote kwa upande wa samaki na mazao ya uvuvi, sisi tuna tozo ambazo hazibebeki na hazihimiliki na matokeo yake tunapoteza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nitachangia zaidi kwenye sekta.

Mheshmiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami nichangie kidogo hii hoja ambayo iko mbele yetu. Niwapongeze Mawaziri kwa kazi yao nzuri, lakini ninazo hoja mbili. Nitaongelea Sheria ya Bima, tunapoisoma pamoja na Sheria ya Usalama Barabarani. Sheria ya Bima hasa inapokuja kwenye makosa yanayotokana na ajali za barabarani, inayo matatizo makubwa sana na ukiisoma hii sheria ya bima, ajali inapotokea barabarani, Jeshi la Polisi watakwenda watapima, kesi itapelekwa mahakamani, tutasubiri hukumu itoke na wote tunajua, ni mashahidi hukumu zetu zinachukua muda gani! Hukumu ikishatoka yule muhanga wa ajali ya barabarani ndio anaweza akaambatanisha ile hukumu kwenda kudai fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa ni kwamba anapokwenda kudai ile fidia, Sheria ya Bima iko kimya anakwenda kulipwa kiasi gani, ni maamuzi ya kampuni ya bima. Tumeshuhudia ndugu zetu wengi wakipoteza maisha yao kwa sababu, ajali inapotokea baadhi ya familia zetu tunazijua ni masikini, hawana hata pesa ya kumtibia huyu muhanga wa ajali ya barabarani. Wanaanza kuchangishana ukoo mzima ili kupata hela ya kumpeleka hospitalini. Anapokwenda sasa kudai ile fidia/compensation ambayo inalipwa na kampuni ya bima, anakwenda pale wanamwambia tunakupa shilingi laki tano. Ni maamuzi ya kampuni ya bima ndio inaamua amlipe kiasi gani, mtu ametoka Kagera na tunajua makampuni makubwa ya bima yapo Dar es Salaam au hapa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anatoka Kagera analipa nauli anakwenda Dar es Salaam anaambiwa tunakupa shilingi laki tano, hatuwatendei haki watu wetu. Niwaombe Sheria ya Bima ya Tanzania itoe kima au kiwango cha chini, ambacho mtu anapopoteza maisha katika ajali ya barabarani anapaswa kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria nyingine si kwamba hatuna mifano, tunayo mifano. Usafiri wa anga mtu anapokufa akiwa kwenye ndege, sheria zetu pamoja na kanuni za TCAA za usafiri wa anga za mwaka 2008 zinatoa kima cha chini ambacho mtoa huduma anapaswa kumlipa muhanga wa ajali anapokuwa kwenye ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma regulation 24 ni 120,000 USD tunajua hiyo hatuna shida nayo. Lakini usafiri wa majini, nayo ukisoma Shipping Merchant Act kipengele cha 352 kimetoa kima cha chini ambacho muhanga wa ajali ya usafiri wa majini anapaswa kulipwa endapo atapata kifo au ajali au kupoteza mali zote akiwa kwenye meli.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo Sheria ya Usafiri wa Majini (Merchant Shipping Act), ukiisoma ni kichekesho tu, haitekelezeki. Niwaombe Tume ya Kurekebisha Sheria; twenda tukaipitie hiyo Sheria. Unaposema mtu akifa kwenye meli anapaswa kulipwa units wanasema laki 333 units of account nikalifuatilia kuangalia hizi laki 333 units of account maana yake ni nini? Nikaenda kupata kwamba hizo ni sawasawa na one special drawing like the SDR. Na SDR moja ni sawasawa na Euro moja, ni kampuni gani ya Kitanzania inayoweza ikalipa hizi fedha? Haipo!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, na Sheria hiyo tunayo, likitokea la kutokea, hatuwezi kuya-enforce kwasababu ya ugumu wake. Lakini tunajua kwamba hii Sheria ukiisoma na Sheria ya Australia ni cut and paste. Kwa hiyo, niiombe Tume ya Kurekebisha Sheria ipitie hii sheria iweze kuiweka katika viwango ambavyo ni vya kitanzania ambavyo ikitokea ajali hii inaweza ikalipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudi kwenye masuala la ajali za barabarani. Naomba niishauri wizara, twenda tukapitie Sheria ya Bima tuioanishe na Sheria ya Usafiri wa Barabarani Road Traffic Act, tuje na mapendekezo au kiwango ambacho kinahimilika ili watanzania wenzetu wanapopata ajali waweze kulipwa kama sheria inavyosema to compensated adequately lakini sheria ilivyo hatuwatendei haki Watanzania. Tusiyaachie Makampuni ya Bima yaamue juu ya maisha ya Watanzania wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa ushauri mwingine kuhusiana na hii, wananchi wetu wanapopata ajali wakati wanasubiri kesi iende mahakamani ihukumiwe, hapa katikati hatuna chombo cha kuwahudumia tunajua wengi hawawezi kujihudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri wizara tuunde chombo ambacho kitachangiwa na makampuni yote ya Bima mtu anapopata ajali leo, kile chombo kitoe fedha zikamuhudie huyu mhanga wa ajali wakati tunasubiri Shirika/ Makampuni ya Bima kumlipa, atakapolipwa zile fedha ambazo tutakuwa tumempatia kumuhudumia basi tutazikata kurudisha kwenye mfuko ambao nashauri na kupendekeza uundwe chini ya sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo janga lingine, tunayo Sheria ya TASAC. Tulitunga hapa Bungeni lakini ukiisoma leo katika mazingira ambayo leo tunasema tunakwenda kujenga uchumi shindani; ile sheria ni janga la Kitaifa. Nashauri hii sheria tukaipitie upya, haileti ustawi wa sekta binafsi kwenye usafiri wa majini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema TASAC ni mdhibiti na tunajua udhibiti tulionao Tanzania tuliochagua kuuchukua ni udhibiti wa pamoja; lakini TASAC yenyewe ukiiangalia imeunganisha shughuli za kiudhibiti na shughuli za kutoa huduma. Huwezi ukawa referee wakati huo huo unacheza mpira uwanjani ni makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza na kushauri, shughuli za kiudhibiti ambazo ziko chini ya hii sheria zitenganishwe tuwe na mamlaka na chombo ambacho kinaangalia masuala ya udhibiti wa usafiri wa majini na tuwe na kampuni ambayo itatuangalizia kwa nia ileile ambayo tulikuja na hii sheria ya TASAC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua zamani tulikuwa na NASACO, turudishe mfumo uleule lakini tuwe na chombo ambacho kinafanya kazi ya udhibiti peke yake na chombo ambacho kinafanya biashara. Na misingi ya udhibiti, mdhibiti ana hadhi ya kimahakama na hawa wengine wote ambao wanafanya zile shughuli wanapokuwa na matatizo wanakuja kwa mdhibiti ili akawapatie suluhu ya matatizo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunapokuwa na Taasisi ambayo kimsingi ni mdhibiti, ni mahakama, lakini na yeye anafanya zile shughuli inakuwa ni kinyume na utawala bora inapokuja kwenye kusuluhisha matatizo yanayojitokeza kwenye hiyo sekta. Niiombe Tume ya Kurekebisha Sheria, iiangalie hii sheria; badala ya kuleta ustawi nadhani maoni yangu inakwanza ustawi wa sekta hii ya usafiri wa majini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache naomba niunge hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupewa nafasi hii kuchangia Wizara yetu muhimu ya Elimu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nipeleke salamu kwa Waziri, Wilaya ya Muleba inakupenda na inakupongeza sana, kuna shule yako inaitwa Profesa Ndalichako; wamenituma nikuambie usiwasahau. (Makofi)

SPIKA: Imekuwa ya ngapi kwenye matokeo? (Kicheko)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, anajua mwenyewe Waziri wa Elimu. (Kicheko)

SPIKA: Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, lakini hizo salamu ni kwamba bado wanamhitaji sana na wanahitaji ulezi wake wa kimama na wa kiuwaziri.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwenye COSTECH. Jana kwenye mjadala hapa liliibuka suala la gongo na konyagi kwamba hao watu wanaotengeneza gongo na konyagi mara nyingi wanakimbizana na polisi kwamba ile ni bidhaa ambayo haitakiwi.

Mheshimiwa Spika, tunao vijana wengi wa Kitanzania ambao wamevumbua vitu vingi. Miaka mitatu iliyopita tulikuwa na maneno hapa, kuna vijana ambao walivumbua helikopta, sijui wako wapi leo? Kuna vijana ambao walivumbua magari, wako wapi leo? Serikali yetu kupitia Wizara hii imewapa msaada gani? Tumewaacha hawa vijana wanahangaika wao kwa wao, wanatumia pesa yao na muda wao na ile end product, kama Serikali, hatui-own. Tunawaacha tu na haya mambo yanapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna kipindi nilisoma siku za nyuma Mwalimu Nyerere alikuwa na wazo la kuanzisha vijiji vya sayansi ambavyo vingewasaidia vijana ambao wana ubunifu wa aina yake waende kwenye vijiji vile wakapate muongozo na ku-shape yale mawazo yao tuweze kupata wabunifu ambao wanaweza kutengeneza vitu. Tunavyoviona vinaelea Ulaya; ndege tunaziona zinatembea na magari, yalibuniwa na kuasisiwa na vijana ambao walikuwa na ubunifu kwenye mioyo yao. Huu ubunifu haufundishwi vyuoni wala shuleni, ila ni mtu anazaliwa ni mbunifu haijalishi amesoma kiwango gani, ana elimu kiasi gani, lakini anao ubunifu ule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kazi yetu kupitia Wizara ya Elimu, hasa ile Taasisi ya COSTECH nadhani ndio kazi yake hiyo. Mwalimu alikuja na wazo la vijiji vya sayansi tukaja na COSTECH, lakini sasa ukiangalia pesa wanayopewa COSTECH hawawezi kuendeleza ubunifu ambao mbele ya safari ungeweza kusaidia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudi kwenye jimbo langu. Tunayo kazi kubwa mbele yetu. Nilikuwa naangalia maoteo kwenye jimbo langu tu, mwaka huu vijana ambao wamesajiliwa kidato cha kwanza walikuwa 9,041. Mwaka 2023 watakuwa 21,159, mwaka 2024 tutakuwa na vijana 30,025, lakini ukiangalia miundombinu ya shule tulizonazo ni ileile. Naomba Wizara ijipange, vinginevyo kufika mwaka 2025 tutafukuzana kwa sababu wanafunzi walio kwenye shule za msingi ambao tunatarajia waingie kidato cha kwanza ni zaidi ya mara tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Elimu ihakikishe kwamba mikoa ambayo iko pembezoni mwa nchi kama Kagera na mikoa mingine waiangalie kwa jicho la pekee. Ukienda kwenye mikoa mingi ya pembezoni walimu hawapo, unakuta shule ya msingi au shule ya sekondari ina wanafunzi 1,200 ina walimu sita halafu tunaongelea ubora wa elimu, tunajidanganya. Naomba Wizara ya Elimu tujipange kuhakikisha kwamba mikoa ya pembezoni tunaipatia kipaumbele na kuhakikisha ina nyumba za walimu otherwise walimu wote wanaopelekwa kule wanakimbia kwa sababu ya mazingira magumu.

Mheshimiwa Spika, lakini nipendekeze, kwa mikoa ambayo iko pembezoni mwa nchi tuangalie kuwapatia motisha au allowance, ile wanaita hardship allowance iweze kuwa-sustain kule kwenye mazingira magumu ambako hakuna umeme, wakati mwingine hakuna barabara na ukienda kule kwa kweli wengi wanakataa kwenda maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja mkono na nawapongeza Mawaziri wetu kwa kazi kubwa wanayoifanya, ila Mheshimiwa Waziri asisahau Ndalichako Secondary School. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nampongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa miradi mikubwa Wilayani Muleba katika nyanja za afya, elimu, maji, miundombinu, umeme na kadhalika. Kwa niaba ya Wanamuleba namshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake, namshukuru kwa mkutano wake alioufanya Wilayani Karagwe kwa ajili ya kuboresha bei ya zao la kahawa, hakika wakulima wa zao la kahawa wanatoa pongezi nyingi sana kwa kufuta tozo 42.

Mheshimiwa Spika, nachangia hoja ya Waziri Mkuu katika ukurasa wa 42 kifungu cha 75 kuhusu ardhi. Wilaya ya Muleba ina migogoro miwili mikubwa ya ardhi baina ya Kampuni ya Ranchi (NARCO) na wakulima katika Kata ya Rutoro na eneo la MWISA II. Nitajikita kwenye mgogoro wa MWISA II.

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa MWISA II ulianza mwaka 2016 baada ya NARCO kuvamia eneo la MWISA II na kuanza kupima vitalu kwa ajili ya kukodisha wafugaji. Upimaji huo ulihusisha na kuathiri ardhi ya vijiji na vitongoji ambavyo vimepimwa na kusajiliwa kisheria. Huu mgogoro unahusisha kata saba (Kyebitembe, Karambi, Kasharunga, Mubunda, Burungura, Ngenge na Rutoro) vijiji 12 na vitongoji 19. Upimaji huu unakiuka Sheria ya Ardhi ya Vijiji, kuna taaruki kubwa.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana mwezi Julai 2021, Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi alifika Muleba kwa ajili ya kutafuta suluhu ya mgogoro huo. Baada ya mkutano na kwenda kujiridhisha na hali halisi, tulifikia maridhiano kuwa NARCO wasiingilie maeneo ya vitongoji na vijiji ambavyo vimesajiliwa kisheria. Hii ilikuwa faraja kwa wananchi wa vijiji hivyo 12 na vitongoji 19.

Mheshimiwa Spika, NARCO wameanza na wanaendelea kuingilia mashamba ya wananchi katika vitongoji vya Kabwensana na Mahigabili katika Kijiji cha Kakoma, Kata ya Burungura na kuanza kuhamisha watu kwa nguvu, kuwanyang’anya mashamba yao na/au kuwagawia watu wengine heka sita kwa kisingizio cha kupanga makazi. Kuna sintofahamu na taharuki kubwa sana. Kulingana na mila na desturi zetu, tunazika wapendwa wetu kwenye mashamba yetu karibu na nyumba zetu. Hamishahamisha hii haizingatii hata sheria ya kuhamisha makaburi ya wapendwa wetu “The Graves (Removal) Act, Act No. 9 ya 1969.

Naomba Ofisi ya Wazir Mkuu itusaidie kumaliza mgogoro wa MWISA II ambao unahusisha kata saba, vijiji 12 na vitongoji 19. Ni mgogoro unaohushisha eneo kubwa na watu wengi sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi nami nichangie hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na jambo moja dogo. Asubuhi wakati Mbunge mmoja anachangia, aliongelea Wizara kutaifisha mifugo wa watu wetu. Katika wilaya yangu ninakotoka, natumaini Mheshimiwa Waziri ananisikia, kuna mwananchi tangu mwaka 2017 ng’ombe wake 111 na kondoo tisa walitaifishwa kwa kisingizio kwamba wameingizwa kwenye Hifadhi ya Burigi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi ilikwenda Mahakamani, akafunguliwa Kesi Na. 155 ya 2017 akashinda. Huyo mwananchi siku hiyo hiyo akakamatwa tena akafunguliwa Kesi Na. 56 ya mwaka 2017, akashindwa. Akakata rufaa Na. 35 ya 2019 Bukoba, Mahakama ikaamuru arudishiwe mifugo wake. Mpaka leo tunavyoongea, tangu mwaka 2017 hadi leo anafuatilia ng’ombe wake 111 na kondoo tisa, hajapewa mifugo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Waziri anatoa majumuisho, nitaomba kauli ya Serikali, hiyo mifugo iko wapi? Kwa nini Wizara haitaki kumrudishia mwananchi ng’ombe wake?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, subiri. Taarifa Mheshimiwa Silaa.

T A A R I F A

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kama mwaka 2017 walikuwa ng’ombe 111 watakuwa wamezaa. Kwa hiyo, madeni ya huyo mwananchi wake aweze kuyaongeza na wale ndama watakaokuwa wamezaliwa kwa muda huo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, unapokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea na huko ndiko nilikotaka kuelekea. Mheshimiwa Waziri huyu mwananchi anaitwa Dunstan kutoka Kata ya Kyebitembe. Naomba wakati unatoa majumuisho utupe kauli ya Serikali. Whether Serikali iko juu ya sheria au utatuambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa mjadala wa asubuhi ilikuwepo hoja ya NARCO. Wakati Mheshimiwa Spika anasitisha shughuli za Bunge asubuhi, naye ametoa maoni yake kuhusu NARCO.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, subiri. Taarifa; Mheshimiwa Esther.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hoja anayoiongea ni valid sana; na siyo mwananchi wake tu. Tukitaka kusimama hapa kila mmoja, kuna wananchi wengi sana ambao wanapitia hiyo adha. Kwa hiyo, Serikali tu labda ije na mkakati madhubuti kuhakikisha kwamba wale walioshinda kesi warudishiwe mali zao, ikiwezekana na fidia juu. Siyo kwa Muleba tu, ni karibia nchi nzima kuna matatizo kama haya. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni suala la kisera na Kitaifa, naipokea taarifa yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Spika anasitisha shughuli za Bunge asubuhi, naye alitoa maoni yake kuhusu NARCO na Mheshimiwa Rweikiza amesema asubuhi. Katika Wilaya ya Muleba tunao mgogoro mkubwa na shirika letu la NARCO. Katika Wilaya ya Muleba pekee, katika Kata ya Rutoro, tuna mgogoro na NARCO wa hekta 50,000. Katika kata zipatazo sita katika Jimbo la Muleba Kusini; Kata za Kyebitembe, Karambi, Mbunda, Kasharunga, Kakoma na Ngenge, tuna mgogoro na NARCO, mgogoro wa Mwisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu, tumeliongelea hili kwa muda mrefu, lakini kutokana na remarks alizotoa Mheshimiwa Spika leo asubuhi, namwomba Mheshimiwa Waziri, hii ardhi hekta 50,000 ukiongeza hekta 70,000 ambazo tuna mgogoro nazo, atuachie Wilaya ya Muleba tukapange matumizi bora ya ardhi. Wao kama NARCO wabaki kama regulator watupe regulatory oversight tukapange matumizi bora ya ardhi yetu, tukalete wafugaji ambao tunao katika Wilaya ya Muleba, wanatosheleza. Hatutaki wafugaji kutoka nje, tunao wa kutosha na tutafuga…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, pokea taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikao pia cha Waziri Mkuu cha tarehe 26 Februari, 2016 pale Kagera alitoa maelekezo kwamba NARCO wabainishe mpango bora wa matumizi ya ardhi na kama NARCO imeshindwa kuendesha waweze kuipendekeza Serikali wananchi waweze kugawiwa, hasa hilo nilikuwa naomba kumpa taarifa mzungumzaji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba ulinde dakika zangu ninaona nina taarifa nyingi leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wizara na kwa maana hiyo tunaiyomba Serikali suala la Mwisa II kwa Mkoa wa Kagera watuachie, uwezo tunao, watu tunao, na ng’ombe tunao. Wakatupatie utalaam na uangalizi kidogo na ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Muleba inazungukwa na Ziwa Victoria, nashukuru mzungumzaji wa mwisho amesema Kagera, Ziwa Victoria tumepewa pesa kwa ajili ya mikopo kwa wavuvi wetu, niishukuru Serikali kwa hilo. Lakini Waziri wa Fedha yupo hapa Tanzania tumebarikiwa kuwa na fursa nyingi kwa upande wa bahari, maziwa, lakini ukiingalia tunavyotumia hizo fursa ni aibu ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa bahari tuna fukwe yenye urefu wa zaidi ya kilometa 1424 zenye kufaa kwa uvuvi ni kilometa 854 ambayo ni sawasawa na asilimia 60 zinafaa kwa ufugaji wa Samaki. Kwa upande wa Ziwa Victoria ninakotokea, tuna ufukwe wa kilometa 3450 ambapo kilometa 2587 sawasawa na asilimia 75 zinafaa kwa ufugaji wa Samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shughuli za uvuvi zinazoendelea na mazao tunayoyapata ni aibu, mahitaji ya Samaki kwa upande wa Tanzania kwa mwaka tunahitaji kati ya tani 700,000 mpaka 800,000 kwa mwaka. Lakini pamoja na fursa tulizonazo, pamoja na bahari tuliyonayo, pamoja na maziwa tuliyonayo tunazalisha tani 389,455 hata hatutoshelezi soko la ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walichukua dakika zangu, naomba niongezee mbili.

MWENYEKITI: Dakika moja na nusu nakupa.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaagiza Samaki kutoka nje mpaka sasa na tunalo tatizo la vijana kukosa ajira, sasa tunaomba wizara ituambie ina mkakati gani kuhakikisha kwamba hilo gap la Samaki tunaoagiza kutoka nje kwa pesa ya kigeni tunalipunguzaje na kuhakikisha kwamba tuna-involve vijana wengi zaidi ili tuweze kwanza ku-create ajira, wakati huo huo kupunguza uagizaji wa Samaki nje wakati tuna maziwa, tuna bahari ambavyo vipo, tumepewa tu na Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongezea suala la kanuni na tozo, niliongelea hapa wakati nachangia Mpango wa Tatu, nimuombe wizara wapitie tozo zote ambazo tunatoza kwenye mazao ya uvuvi wa Samaki. Lakini tunapoongelea tozo tuangalie tunalinganisha na nchi jirani za Kenya na Uganda ambao wote tuna-share kwa mfano Ziwa Victoria kwa upande wa bahari tuna-share na Kenya na wenzetu Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiishi kama tunaishi kwenye kisiwa, tunapotengeneza kanuni tuangalie na wenzetu, mchangiaji aliyemaliza kusema, amesema kina cha Ziwa Victoria na kina cha Ziwa Tanganyika vinatofautiana, kwa hiyo tunapotengeneza kanuni, tusitengeneze kanuni kwa nchi nzima tuangalie na mazingira ya maziwa yetu, tuangalie mazingira ya bahari, havifanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, lakini naomba Waziri atakaposimama atuambie hatma ya ng’ombe wa wampiga kura wangu 111 na Kondoo 9 wapo wapi? na wameshazaa wangapi? na faida yake ni nini? na anamrudishia huyo mpiga kura lini hao ng’ombe wake. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi hii kuchangia Wizara hii. Niungane na wenzangu Wabunge kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameongea mazao mapya ambayo wameyaongeza kwa ajili ya kuongeza chachu na ufanisi katika Wizara ya Utalii, nayo ni utalii wa uvuvi na kujiburudisha, utalii wa kula Wanyama pori, utalii wa kula chakula porini na utalii wa kupiga makasia. Nawapongeza sana kwa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani wengi tumetembea katika nchi za wenzetu. Kwa mfano ukienda Misri, pamoja na kuangalia zile pyramids lakini jioni mkitoka kuangalia yale ma-pyramids mtakwenda Mto Nile, mtapiga ma-cruise, kuna ngoma za asili, mtakula chakula, inaongeza value kwenye package ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Tanzania tutumie na sisi akili zetu jamani, tusibakie kwenda kuangalia wanyama sijui wapi, kuangalia sijui Tarangire, sijui Serengeti, tuongeze value kwenye kuangalia wale Wanyama, jioni hawa watalii wanaangalia nini, wanafanya nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Hongkong pale ile Hongkong ilivyokaa ina vilima mithili ya Mji wa Mwanza, lakini vile vilima wamehakikisha wamevitunza na ni sehemu ya vichocheo vya utalii, ile jioni mnapanda kwenye mlima mnaangalia Hongkong pale chini. Angalia Mji wetu wa Mwanza tunautumiaje kwenye sekta ya utalii, tumebaki na sekta ya utalii ambayo hatujaijumuisha na mazingira ya maeneo ya utalii wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna ziwa Victoria pale na maziwa mengine tunayaunganishaje kwenye sekta ya utalii kwa mfano Ziwa Victoria, Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi yupo pale, kuna kipindi pale Bukoba walikuwa wameandaa kuwa na cruising party kipindi cha mwisho wa mwaka, lakini ukienda kuazima meli ile ya Victoria wanakwambia hii siyo kazi yetu, siyo kazi ya utalii hii, ni kana kwamba Wizara ya Utalii inajitegemea, Sekta ya Uchukuzi inajitegemea lakini tunapaswa kuwa holistic approach tunapokuja kwenye sekta ya na masuala yote ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Burigi Chato, nawashukuru Serikali ile hifadhi ilikuwa ni majanga miaka ya nyuma, tusingepita mle, lakini kwa kuanzisha hii hifadhi imetuongezea usalama watu wa kanda ya ziwa. Nimwombe Waziri Burigi ndiyo imebeba maana ya ile hifadhi. Tuna Ziwa Burigi pale ambalo kwa bahati nzuri kama hawajawahi kufika, lakini najua hawawezi kufika kwa sababu lile eneo la Burigi halifikiki, hakuna barabara nzuri, lakini pili kama mchangiaji mmoja alivyosema hakuna mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, wakati anakuja ku-wind up atuambie wana mkakati gani kuhakikisha kwamba lile Ziwa Burigi linafikika. Watalii watakapokuja na nina uhakika, watalii wengi watatokea Bukoba kwenda kwenye Hifadhi ya Burigi Chato, tuhakikishe upande wa Muleba tunakuwa na gate kubwa la kuhakikisha kwamba watalii watakapotoka Bukoba kwenda Burigi Chato wanapata sehemu ya kuingilia, badala ya kuzunguka kwenda Biharamulo kwenda sijui Chato, waingilie eneo la Muleba. Mheshimiwa Waziri atatupa maneno yakeo atakapokuja kuhitimisha hoja yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, wakati nachangia Wizara ya Mifugo, niliongelea hili suala la kuchukua mifugo. Bahati nzuri wewe mwenyewe ni Mwanasheria, Waziri ni Mwanasheria, wanajua maana ya sheria. Inapokuja katika Wizara hii, mifugo imeingizwa kwenye Hifadhi mwananchi wangu nilimwongelea katika Wizara ya Mifugo…amekamatwa, amefunguliwa kesi ya kuingiza mifugo kwenye hifadhi, ameshinda. Siku hiyo hiyo amekamatwa kwa kosa lingine eti ameharibu uoto wa asili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mahakama imesema arudishiwe mifugo yake kwa nini watu wa Wizara hii wanakaa na mifugo ya wananchi jamani! Wanafanya wananchi wachukie Serikali yao kana kwamba Serikali imewaibia mifugo yao, lakini ni watu wachache. Tunaomba Mheshimiwa Waziri atusaidie wanatupatia wakati mgumu kwenye majimbo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga hoja
mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara yake.

Mheshimiwa Spika, jana nilichangia bajeti yako na kwa msisitizo, nimesikitika sana kuona Mradi wa Maji kutoka Ziwa Victoria kwa ajili ya Kata za Gwanseli, Magata Karutanga, Muleba, Bureza, Kikuku na Kagoma. Mradi huu ulianza kuasisiwa mwaka 2009. Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulikamilika mwaka 2020. Nimeulizia mara mbili juu ya mradi huu majibu yalikuwa ni ya kutia moyo kwamba mradi huu utakuwa kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023. Mradi huu, haupo kwenye bajeti yako. Nimesikitika sana, Muleba imesikitika sana. Nakuomba uangalie kwenye bajeti yako, mradi huu ni muhimu sana kwa Muleba.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa nafasi ya kuchangia hoja hii. Nampongeza Rais wetu kwa bajeti hii nzuri, pia nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na Watendaji wote wa Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita kwenye kushauri. Nilikuwa naangalia hizi sekta zetu za kiuchumi na mchango wake katika pato la Taifa. Ukizipitia zote, kwa kweli bado tunayo kazi kubwa ya kufanya. Ukiangalia kilimo kinachangia asilimia 26.9 kama takwimu zangu ziko sahihi; fedha na bima zinachangia asilimia 3.5; madini asilimia 6.9; viwanda asilimia 8.4; umeme asilimia 0.3; ujenzi asilimia 14.4; uchukuzi asilimia 7.5; na biashara asilimia 8.7. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia jiografia ya nchi yetu, mimi nadhani sekta nyingi kwa kweli tuko chini pasipo sababu yoyote ya msingi. Kwa mfano uchukuzi, kwa jiografia ya nchi yetu, bandari zetu, nchi tunazopakana nazo, napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri, tujipe mkakati wa kukatisha baadhi ya sekta mchango wake katika pato la Taifa uende zaidi ya asilimia 10. Tupende tusipende lazima tuwe na mkakati wa namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta ya uchukuzi tuna viwanja vyetu vya ndege, lakini kanda ya ziwa tuna uwanja wa ndege wa Mwanza. Zamani mazao ya uvuvi yalikuwa yanasafirishwa kwa ndege kutoka uwanja wa ndege wa Mwanza kwenda nchi za nje, lakini hivi sasa tunavyoongea, mazao yote ya uvuvi ili yaende kwenye masoko ya nje, lazima tuyasafirishe kwa malori tuyapeleke Entebe au Nairobi. Ukijiuliza, kwa nini mazao yetu ya uvuvi yaende Entebe au Nairobi? Hatuna sababu yoyote ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani uwanja wetu wa ndege haukuwa na facility ya kuhifadhi hii minofu ya Samaki, lakini hivi tunavyoongea, Serikali yetu kupitia TAA wamejenga facility nzuri sana ambayo ukilinganisha na nchi jirani actually facility tuliyonayo pale Mwanza ni nzuri na bora kuliko facility zote za Afrika Mashariki na Afrika ya Kati. Tatizo tulilonalo, hatujaisajili kupata FOB Mwanza na ndiyo maana mashirika ya ndege kama Air Rwanda walipojaribu kusafirisha minofu yetu ya samaki kutoka Mwanza, wameshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, kwa kuwa tumeshawekeza pesa yetu pale Mwanza, tumejenga facility, tutafute registration, tupate FOB Mwanza ili mazao yetu ya uvuvi yasafirishwe moja kwa moja kutoka Mwanza kwenda nchi za nje. Hii kwanza itaongeza chachu kubwa ya kuwekeza viwanda hapo Mwanza au Kanda ya Ziwa. Pili, zile pesa ambazo tunazilipa Entebe na Nairobi zitabaki kwenye nchi yetu, tutaongeza pato kwa sekta ya uchukuzi na sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni kuhusu kilimo. Ukiangalia sekta ya kilimo, mchango wake ni mdogo. Wachangiaji wengi wamesema hapa, tuna vijana wengi huko mitaani hawana kazi, lakini hawawezi kwenda kwenye kilimo kwa sababu ukiwaambia wanasema hawana mitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi letu kitengo cha JKT wanafanya vizuri sana kwenye kilimo. Nashauri tuwaongezee pesa wakajikite kwenye kuzalisha mazao ya kilimo. Kwa sababu wana uwezo, watazalisha, watayaongezea thamani na wanaweza kupata masoko kirahisi kuliko mkulima mmoja mmoja. Hata kilimo ambacho tunakizalisha, hapa tunaongea lakini nadhani hatuna mkakati wa madhubuti kuhakikisha kwamba tunaongeza tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu Kagera tunazalisha kahawa. Tumepiga kelele sana hapa, tumesema hebu ruhusuni wafanyabiashara wakanunue hizi kahawa. Kuna watu wamewekeza kwenye viwanda pale, lakini tunawawekea figisufigisu hatuwapatii vibali. Msimu wa kahawa ulianza mwezi wa Nne, lakini tunavyoongea leo, vyama vyetu vya msingi havijafungua masoko, hata wafanyabiashara binafsi ambao wangenunua kahawa, hawajapewa vibali. Ukijiuliza wakati mwingine, tunadhamiria nini? Tunalenga kufanya nini? Ndiyo maana sekta nyingi kama hizi kutokana na kanuni zetu tulizojiwekea, hatufanyi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwamba hizi posho ambazo walikuwa wanalipwa Madiwani sasa Serikali inazibeba. Hata hivyo nikiangalia hizi posho zao hawa Madiwani wenzetu, pamoja na kwamba naishukuru Serikali kwamba imezibeba, itazilipa kwa wakati, lakini tuziangalie hizo posho, bado ni kidogo mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Madiwani wenzetu ndio tunawaachia majimbo yetu, ndio wanafanya kazi kwenye kata zetu, ndio wanafanya kazi ya kuhamasisha kukusanya mapato ya Halmashauri zetu. Napendekeza kwamba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake, tuiangalie hii posho ya Madiwani, tuwaongezee angalau kidogo nao wakajisikie na wakafurahie kazi wanayoifanya huko kwenye Halmashauri zetu na waweze kutulindia majimbo yetu ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa posho zilizopendekezwa kwa ajili ya Watendaji wa Kata na Maafisa Tarafa. Nawashukuru sana. Hata hivyo, kuna kundi ambalo tumelisahau; kundi la wazee. Nimefurahi kule upande wa pili wa nchi yetu, Zanzibar wanawalipa wazee posho ya shilingi 25,000/= kila mwezi; wanafanya vizuri. Ila kwa upande wa Tanzania Bara tuna makundi ya watu wenye mahitaji maalum; tunaongelea watoto, wanawake na vijana ambao wanapewa mikopo, lakini tumesahau hili kundi muhimu la wazee na ambalo katika maisha yao wamelitumikia Taifa hili na kwa kweli wanaishi kwa kusononeka, baada ya kuingia kwenye hili kundi la wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yetu na tujuwe kila mmoja wetu tunaelekea kwenye uzee, tuwatengee na wenyewe posho kidogo ambayo itawapatia furaha katika maisha yao. Hii inawezekana. Baadhi ya taasisi kwa mfano ninakotoka kwenye jimbo langu, kuna NGO tu; kuna mzee mmoja Mswisi, ameishi pale zaidi ya miaka 10. Aliamua yeye kwa pesa yake kuwaletea raha wazee wenzake, kila mwezi anatumia zaidi ya shilingi milioni 16 kuwapa posho hawa wazee. Anawalipa posho zaidi ya wazee 1,000; na kwa mwaka anatumia zaidi ya shilingi milioni 195 kwa pesa yake na pesa ambayo anaitafuta nje. Huyu mzee amekaa hapa muda mrefu sana, lakini alijaribu hata kuomba na uraia tukamnyima. Naona Waziri wa Mambo ya Ndani yuko hapa. Huyu mzee amefanya mambo mengi mazuri na anawasaidia wazee na anawapa raha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema kuwalipa posho wazee siyo suala la pesa unawalipa kiasi gani? Kinachofanyika ni kwamba, wanajiona wamethaminika, wanajiona wanapendwa, wanajiona wana thamani katika nchi yao, hata tukiamua tuwepe shilingi 10,000/= tu, watafurahi, wataishi maisha marefu zaidi na watafurahia nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili tuliangalie, tulitafakari na tulitathmini. Sasa hivi wazee tunasema ni wachache lakini tuendako zaidi ya miaka 10 ijayo, wazee tutakuwa wengi, tunazidi kuongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga hoja mkono, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nami niungane na Wabunge wengine kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma. Katika ripoti yetu tumeangalia mashirika mengi, lakini nasikitika kusema mashirika yetu mengi hayafanyi kazi vizuri. Tatizo mojawapo, katika ripoti yetu tumeainisha, ukosefu wa mtaji ni tatizo kubwa kwenye mashirika yetu na nijikite kwenye TPA.

Mheshimiwa Naibu Spika, TPA kwa uchumi wa nchi yetu na kulingana na jiografia yetu na nchi zinazotuzunguka, kusema kweli ni cash cow yetu. Hata hivyo, ukiangalia mtaji walionao na uwekezaji wetu na jiografia yetu, nchi zilizotuzunguka zinazohitaji huduma yetu, kulingana na ripoti yetu ambayo tumewasilisha hapa, tumesema TPA utendaji kazi wake ni mdogo kwa sababu hawana mtaji wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia vifaa walivyonavyo ni vya karne iliyopita, siyo vya karne hii. Tanzania siyo peke yetu; au Bandari ya Dar es Salaam siyo peke yake katika ukanda huu. Tunazo bandari nyingi ambazo tunashindana nazo. Kama tuna vifaa hafifu ambavyo vina teknolojia hafifu, hatuwezi kushindana na bandari za nchi zilizo karibu kwenye ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika. Tutaachwa nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza, Serikali i- commit hela ya kutosha kwenye Bandari ya Dar es Salaam ili tuweze kuhudumia mizigo ambayo nchi jirani wanapitisha kwetu. Vinginevyo washindani wetu watatuacha nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, bandari hiyo ina upungufu mkubwa wa wafanyakazi. Ikama yao ni wafanyakazi 3,196, lakini waliopo mpaka leo tunapoongea ni wafanyakazi 2,512. Wanao upungufu wa wafanyakazi 1,404 tunashindwa wapi? Kama hiki ndicho kitega uchumi cha uhakika tulichonacho, tukiwekeza vya kutosha, tuna uhakika wa kutengeneza fedha za kutosha kutusaidia kupunguza matatizo kwenye bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukishakuwa na wafanyakazi wachache, ukawa na mtaji mdogo, madhara yake ni kwamba tunatumia muda mwingi kuhudumia meli na matokeo yake hawa tunaowachelewesha kupakua mizigo yao, tunawalipa fidia na hizo gharama zote zinapelekwa kwa mlaji na matokeo yake ni nini? Bidhaa inayopitia kwenye Bandari ya Dar es Salaam haiwezi kushindana na bidhaa nyingine. Itakuwa ni ya bei ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie na Taasisi inayoitwa TASAC. Wakati Sheria ya TASAC inapitishwa hapa, wengi tuliipigia kelele, lakini tukaipitisha kama Bunge. TASAC anafanya kazi ya udhibiti, lakini wakati huo huo anafanya kazi ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani hii. Kwetu huku tunasema ni sawa sawa na kuchukua rubisi ukachanganya na konyagi, haiwezekani. Kama ni mdhibiti, afanye kazi ya udhibiti na tuunde taasisi nyingine ya kufanya biashara ambayo inafanywa na TASAC. Mdhibiti afanye kazi ya udhibiti na tuwe na kampuni nyingine tofauti na TASAC ambayo itafanya kazi ya clearance, kazi za kusafirisha kidogo kidogo na kutoa mizigo, lakini hizi kazi mbili lazima tuzitenganishe, hatuwezi kuendelea hivi. Vinginevyo tunabaki kama kichekesho tu katika uchumi wa soko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na mama yetu, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuipatia Wilaya ya Muleba mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali kupitia Wizara ilitenga shilingi 500,000,000 kuanza ujenzi huo. Ujenzi ulianza kwa majengo mawili ya OPD na maabara. Nimesoma bajeti nzima ya Wizara kwa mwaka 2023/2024 hakuna sehemu ambayo Serikali kupitia Wizara imetenga fedha kuendeleza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Muleba. Wilaya ya Muleba ni moja ya Wilaya kongwe hapa nchini ambayo ilianzishwa mwaka 1974 lakini hadi leo haina Hospitali ya Wilaya. Namshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha shilingi 500,000,000 kuanzisha ujenzi wa hospitali hii.

Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima, angalia popote, naomba fedha angalau shilingi 500,000,000 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Muleba kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Nakushukuru sana kwa kunipatia hiyo fedha.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maombi ya Hospitali ya Wilaya, naomba fedha kwa ajili ya Kituo cha Afya Kata ya Kimwani. Ni kata yenye watu wengi sana lakini pia inahudumia kata mbili za visiwani za Mazinga na Ikuza.

Mheshimiwa Spika, nina barabara tatu muhimu lakini kutokana na jiografia yake zinahitaji nguvu zaidi nje ya bajeti ya TARURA Wilaya. Baraza hizo Kimeya - Burigi (Kata za Kasharunga na Karambi), Ruhunga -Kiholele (Kata za Magata Karutanga na Bureza), Kasenyi-Rwazi (Kata Ikuza).

Mheshimiwa Spika, pamoja na timu nzima ya Waziri nina imani kubwa na ninyi. Natumaini maombi yangu yatapata kibali machoni pako.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia muda huu nami niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru hoja ambayo ilitolewa na Waziri Mkuu. Zaidi namshukuru Waziri Mkuu kwa mkutano wake alioufanya Mkoani Kagera, Wilaya ya Karagwe kutoa suluhu na mweleko wa zao la Kahawa Mkoani Kagera. Nadhani tunakoelekea ni kuzuri, hasa sisi ambao tunatoka katika mikoa inayolima zao la kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitajikita kwenye migogoro ya ardhi. Ninavyoongea leo kuna watu wamelala nje jana. Tuna Kampuni yetu ya ranchi kwa jina mashuhuri, NARCO. Kama kuna kitu ambacho wamefanikiwa Mkoa wa Kagera, ni kutengeneza migogoro mikubwa baina ya wakulima na wafugaji. Kwa kweli, NARCO ni mtambo wa kufyatua migogoro kuliko ufugaji ambayo ni kazi ya msingi waliopewa na sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera, hususani Wilaya ya Muleba, NARCO wana ranchi mbili. Wana ranchi Rutoro na Mwisa, lakini wamepata hizo ardhi katika Wilaya ya Muleba kwa njia ambayo mimi kama Mwanasheria sijui walipataje. Bahati nzuri Mheshimiwa Spika ni Mwanasheria, na ninamwona Waziri wa Ardhi yupo hapa. Upatikanaji wa ardhi ya Mwisa ambayo ni mali ya Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, hawa watu walivyoipata tuna mashaka makubwa. Nimepitia GN zote, tangu mwaka 1960 mpaka leo, nimetafuta GN ambayo inawapa uhalali NARCO kumiliki ardhi ya Mwisa, sijaipata. Tunapoongea, hawa watu wa NARCO wapo eneo la Mwisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la Mwisa katika Wilaya ya Muleba linahusisha Kata saba; tuna Kata za Kemitembe, Karambi, Kasharunga, Mbunda, Burungura, Ngenge na Rutoro. Ndani ya hizo Kata tunavyo Vijiji 12 na Vitongozi 19. Eneo lote hilo tunavyoongea wananchi hawajui kama leo watalala kwenye nyumba zao, hawajui kama kesho wataamka kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba tuna wasiwasi haya maeneo waliyapataje; kwa sababu haya maeneo ni mali ya Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, ni maeneo ambayo yanakaliwa na vijiji; na vijiji vimepimwa tangu mwaka 1975 na vingine vimepimwa mwaka 2010, lakini hawa watu wanasema ni mali yao.

Mheshimiwa Spika, tunazo sheria za nchi hii; tunayo Sheria ya Vijiji (Land Village Act (No. 5) ya Mwaka 1999, lakini tulikuwa na Sheria ya Land Acquision Act; tunao utaratibu wa kutoa ardhi ya vijiji; tunao utaratibu kwamba Rais akihitaji eneo lolote atalitwaa, lakini kuna utaratibu wa kufanya hivyo. Waziri wa Ardhi ataandaa utaratibu ambao utakuwa gazetted, itatoka GN then hilo eneo litatwaliwa kwa matumizi mapana ambayo yana maslahi mapana kwa ajili ya uchumi na matumizi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachoendelea, nimeangalia kote huko, hakuna kitu kinachofanyika au kilichofanyika. Watu wamekwenda wamepima maeneo ya Halmashauri, maeneo ya vijiji; na leo tunavyoongea, katika Vitongoji vya Kabwensana, Maigabili, NARCO wanahamisha watu kinyume cha sharia. Hawafuati Sheria ya Ardhi ya Vijiji, hawafuati sheria ya kuhamisha makaburi ya wapendwa wetu (Grave Remove Act (No. 9) ya Mwaka 1999, pia hawafuati mila na desturi za Wahaya. Wanakwenda pale, wanafukuza watu, wanawaambia ninyi mnahama, mnatoka hapa mnakwenda kule, hakuna notice iliyotolewa, Waziri wa Ardhi hajatoa notice kwa ajili ya kuhamisha makaburi kama ilivyo kwenye Graves Remove Act. Watu hawana amani, hakuna usalama kwenye eneo la Mwisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili nalisema, nashukuru umekalia Kiti, namwona Naibu wa Waziri ni Mwanasheria, naomba mtusaidie. Hatuwezi kuruhusu vitendo vya namna hii, wananchi wanateseka, wanafukuzwa kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi, naomba niliseme hili: lugha inayotumia kule, wanasema ninyi ni wavamizi. Mimi nashangaa! Mtanzania ambaye amezaliwa Tanzania, amekaa kwenye ardhi tangu mwaka 1975, leo NARCO anamwambia ni mvamizi. Tunalipeleka wapi Taifa? NARCO wanalo tatizo. Naomba, haya mambo yanayoendelea Kagera na Muleba, hayawezi kuishia Muleba tu, yatakwenda hata kwenye mikoa mingine tusipochukua hatua leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo hili lilianza mwaka 2016 kwenye upande wa Mwisa. Wakavamia eneo, wakaanza kupima. Tulipokwenda kwenye uchaguzi wakanyamaza. Tumemaliza uchaguzi, wameendelea na leo wapo wanaendelea. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, ndugu yangu Mheshimiwa Ndaki Mashimba. Mwaka 2021 alikuja Wilaya ya Muleba kwa ajili ya kutafuta suluhu ya Mwisa, tukakaa tukaenda field, tukafanya mikutano na wananchi. Tukawaambia, vijiji ambavyo vimesajiliwa pamoja na vitongoji vyake, kwenye huu mradi wa Mwisa havitaguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetoka kule, hawa NARCO walivyo wa ajabu, wakaanza kuwaambia wananchi msiwasikilize wanasiasa. Mimi nashangaa, kama wanasema msiwasikilize wanasiasa, Diwani ni Mwanasiasa, Mbunge ni Mwanasiasa, wewe Mheshimiwa Spika ni Mwanasiasa; na Bunge hili ni la Wanasiasa; ina maana hawatamsikiliza Diwani, hawamsikilizi Mbunge na hata Bunge lako hawatalisikia. Sasa wengine wa juu yake sitawasemea. Nashindwa kuelewa, hivi NARCO hawa, wanatoka Taifa gani? Wanatumikia Taifa gani? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikubaliana pale, tukaja na kitu tunakiita community ambayo ina maazimio 16. Moja ya Azimio, ambalo ni Na. 16 tukasema Ardhi ya Vijiji pamoja na Vitongoji vyake visiguswe. Tumetoka, leo tunavyoongea, wapo kwenye Vitongoji, wanawahamisha watu kwa nguvu zote. Hapo ukumbuke, hawana GN ya kuwapa hiyo ardhi, kwenye makaburi ya watu wanaleta mifugo kulisha pale. Sasa mila zetu ziko wapi? Sheria ziko wapi? Labda kama Waziri amewapa hiyo ruhusa jana, lakini mpaka leo naongea, hakuna taarifa ya kuhamisha makaburi ya wananchi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipatia fursa ya kuchangia kidogo kwenye hoja ambayo iko mbele yetu. Napenda kuwapongeza Wizara ya Fedha kwa kazi hii nzuri waliyotuletea hapa na ambayo tunaijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Hasunga anasema hapa nilikuwa nasoma kitabu kimoja, kimeandikwa na Professor Keith Penny, Professor of psychology and neuroscience. Kwenye hicho kitabu kuna sentensi moja inasema “it takes money to make money”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunachangia Kamati zetu zile tatu, kulikuwepo tatizo kubwa ambalo tulibainisha. Mashirika yetu mengi yanaendeshwa chini ya mtaji wake, yanahitaji mtaji. Kulingana na hiyo quote ambayo nimeisema, bila kuwekeza kwenye mashirika yetu ya umma tusitegemee miujiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kidogo kwenye kilimo, kwa sababu watu wengi miongoni mwa watu wangu wa Muleba ni wakulima na kama tunavyofahamu zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wamejikita kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tatizo tulilonalo kama nchi, wasemaji wengi wamesema, tunalo tatizo na lazima tutafute tumejikwaa wapi ili tuweze kutoka pale. Nikiangalia mfumo wetu wa Taifa tumejifunga kwenye kanuni na sheria zetu ambazo nyingi zinatukwaza. Kule kwetu Mheshimiwa Bashe anafahamu nimemwona pale, kila ikifika mwezi Julai lazima nimwone Mheshimiwa Bashe. Sisi ni wakulima wa kahawa, lakini ikifika mwezi Julai, Agosti tuna task force nyingi kuliko think tanks za kutuletea suluhu ya matatizo yetu. Tutaunda task forces tunaanza kukimbizana na wakulima wadogo wadogo wenye gunia moja, debe mbili eti magendo, tunawakwaza wakulima na wengi wanakata tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko kwetu watu wengi walingoa mibuni na tunayo Sheria ya Kahawa, inasema eti kahawa ni mali ya Serikali. Kati ya sheria mbovu na hiyo ni moja ya sheria mbovu. Mheshimiwa Bashe wakati tunaongea pale alisema anataka free market, sasa inapokuja free market, let make it a free market for every crop for every business, tufungue soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo taasisi za udhibiti, tunayo taasisi ya Fair Competition katika nchi hii, tuiachie ifanye kazi yake. Wakati mwingine tunakimbizana na hawa watu wadogo wadogo hawa, ukiangalia wakulima wa kahawa kwa mfano Kagera, zaidi ya asilimia 90 ni wakulima wadogo wadogo ambao baada ya kuvuna mazao yao tunaanza kukimbizana nao. Hayo mazao wanayapeleka wapi? kama kule wanakoyapeleka kuna soko zuri, bei nzuri, kwa nini tusije na utaratibu mzuri tukawawekea utaratibu mzuri wakauze kule tukakusanye kodi sisi kama Watanzania? Kuna tatizo gani kwenye hilo? Tuachane na mfumo wa ku-paralyze soko kwa kuwafungia wakulima kana kwamba ni wezi, kana kwamba ni smugglers, kana kwamba yaani hawana; mazao wamezalisha wenyewe lakini tunapambana nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye uvuvi, tatizo ni lilelile. Ukiangalia tozo za sekta ya uvuvi na ukizilinganisha na nchi nyingine, ndio maana ukiangalia nchi jirani Uganda, Kenya wanafanya vizuri kwenye uvuvi. Sisi wenye sehemu kubwa ya ziwa tunapata mapato kidogo kwa sababu ya tozo tulizonazo. Huu siyo muujiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye tozo tulizonazo kwa mfano fillet, Tanzania ile viwango vya tozo kwa kilo tunatoza shilingi 552, wenzetu Uganda wanatoza shilingi 115, Kenya shilingi 34.51 hizi ni hela za Kitanzania. mabondo sisi tunachaji shilingi 7,500, wenzetu Uganda shilingi 460, Kenya shilingi 34. Vichwa vya samaki sisi tuna- charge shilingi 46, wenzetu Uganda shilingi 115, Kenya shilingi 34, ndio maana tunakula vichwa hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni mtu gani ambaye ataingia kwenye ziwa akuletee wewe mazao ya uvuvi badala ya kuyapeleka kule ambako tozo na tozo nyingine ziko much more user friendly. Sisi kwetu tozo ziko juu sana, tuangalie haya mambo Mheshimiwa Waziri wa Fedha tunapokuja kutengeneza hizi. Tunavutiaje haya mazao kwetu? Ndio maana Uganda tunavyoongea wana viwanda 20, sisi tuna viwanda nane, Kenya wana viwanda vitano, lakini ukiangalia ziwa tunalolimiliki sisi ni zaidi ya asilimia 50, liko kwa upande wetu. Hata ukiangalia mauzo ya nje, tunavyongea leo, Uganda wanafanya vizuri zaidi kuliko sisi na nchi ya pili baada ya Nigeria, lakini sisi tuko wapi kwa sababu ya mifumo tuliyojiwekea ya sheria, kanuni, tumejifungia kiasi kwamba tunajitengenezea umaskini sisi wenyewe kwa kujua au kutokujua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana Mheshimiwa Hasunga alikuwa anasema we are living in the cycle poverty na hii tumeitengeneza sisi wenyewe kwa kanuni zetu, sheria zetu. Tukae chini tuangalie ni wapi kanuni zetu zinatufunga, ni wapi sheria zetu sio nzuri, ni wapi competitive advantage tunaweza tukaitumia tukijilinganisha na mataifa jirani, tusijifungie ndani, tukadhani sisi ni kisiwa, sisi tunafanya biashara peke yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga hoja mkono. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PIC ambayo iko chini ya Msajili wa Hazina. Msajili wa Hazina anayo Mashirika zaidi ya 230 ambayo Serikali yetu imewekeza mtaji wa zaidi ya trilioni 67.

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa taasisi hizo yapo makampuni ambayo Serikali yetu ina hisa chache mojawapo ni kampuni ya TANICA ambayo iko Mkoani Kagera. Namshukuru Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa aliyoifanya kuhakikisha kwamba anaboresha zao la kahawa Mkoani Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, juhudi ambazo Waziri wetu Mkuu alizifanya Kagera ningeomba ziende sambamba na kuboresha Kiwanda cha TANICA Mkoani Kagera. Nashukuru sana Kiwanda cha TANICA kagera ambacho Serikali yetu inamiliki hisa asilimia Saba, TANICA kilijengwa mwaka 1963 kwa hiyo teknolojia iliyojenga kiwanda hicho nyakati hizi, hiyo teknolojia haipo imepitwa na wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema tunaboresha kilimo lazima twende sambamba na kujenga viwanda ambavyo vitaongeza thamani ya mazao ya mkulima. Mkoa wa Kagera unazalisha zaidi ya tani 34,000 za kahawa lakini kiwanda hiki ambacho Serikali ina hisa asilimia Saba kinaweza kikaongeza thamani asilimia mbili tu ya kahawa inayozalishwa Mkoani Kagera. Ndiyo maana kila mwaka Serikali inatumia nguvu sana kuweza kupambana na magendo ya kahawa kwa sababu wakulima hawana soko la uhakika la kuuza kahawa yao. Kama Serikali ingeongeza mtaji kwenye kiwanda suala la kukimbizana na kahawa au magendo ya kahawa Mkoani Kagera ingebaki historia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha TANICA ambacho Serikali ina hisa chache, kina mtaji wa bilioni kumi lakini share ambazo zimelipiwa ni bilioni moja na milioni mia nne tu, zaidi ya bilioni 8.6 hazijalipwa. Nakumbuka mwaka jana tulikuwa na Kamati Teule chini ya Viwanda na Biashara, ambayo ilifanya tathmini ya hiki kiwanda na ikatoa mapendekezo kwamba Serikali kutokana na umuhimu wa hicho kiwanda cha TANICA Mkoani Kagera ilipe lile deni la shilingi bilioni 8.6 ili Serikali iweze kumiliki hisa nyingi zaidi kwenye hicho kiwanda na iweze kukipatia mtaji kusudi kiweze kuongeza thamani mazao ya kahawa Mkoani Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwenye hili pamoja na viwanda vingine ambavyo vinaendeshwa chini ya mtaji wake, maana yake vinazalisha chini ya viwango, Serikali itafute pesa iviongezee mtaji ili viweze kuzalisha kwa kiwango kinachotakiwa. Kwa kusema hivyo, tutakuwa tumewasaidia wakulima wetu ambao wanazalisha kwa wingi na wakati mwingine tunakosa masoko kwa sababu hatuna viwanda vya kuongeza thamani kwenye mazao tunayozalisha nchini, kufanya hivyo tutakosa pesa ya nje ambayo tunahitaji sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema kuongeza mitaji kwenye viwanda, tumesikia kwenye Kamati ambazo zimesoma ripoti za leo, pesa ambayo inaibiwa kama tutaweza kuithibiti tunaweza ikatusaidia kuongeza mitaji kwenye viwanda ambavyo vinahitaji hizi pesa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili haya Mashirika ambayo yako chini ya Msajili wa Hazina yanaendeshwa chini ya sheria na utaratibu ambao tumeuweka sisi wenyewe. Lakini cha kushangaza Sheria ya Msajili wa Hazina ni sheria ambayo ilitungwa mwaka 1959, nchi hii kabla haijapata uhuru, lakini bado tunatumia sheria kongwe ya namna hiyo kuendesha uchumi, kuendesha mashirika 237, yenye mtaji wa trilioni 67 kwa kutumia sheria kongwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia utajiri ambao tunao kwenye haya mashirika ambayo tumesema trilioni 67, kama tungekuwa na sheria ya kisasa ambayo inampa nguvu na uwezo Msajili wa Hazina, tungekuwa na utajiri zaidi ya hapo labda zaidi ya mara mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana niliongelea hili kwamba Sheria ya Msajili wa Hazina imepitwa na wakati, ni muda muafaka sasa tuifute na tutunge sheria mpya ambayo inalingana na uchumi wa sasa lakini ambayo itampa nguvu na mamlaka Msajili wa Hazina ili aweze kuchukua hatua pale ambapo inahitajika kuhakikisha kwamba Watendaji wa Mashirika haya ambayo ni ya umma pale ambapo anawapa vigezo KPI wanashindwa kuvitekeleza, pale ambapo mashirika hayana bodi lakini Msajili yupo amebaki tu kama Mshauri, ni muda muafaka sasa kumpatia nguvu, kumpatia meno ili aweze kuyawajibisha mashirika haya ambayo yanasababisha hasara, ambayo hayazalishi, na ambayo yanafanya chini ya viwango lakini kwa sasa kwa sheria tuliyonayo hayo mamlaka hana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia mashirika haya ambayo yanazalisha mali ni mfumo wa kampuni na mengine Mashirika ya Umma, mengi Serikali imewekeza lakini ukiangalia tija tunayoipata ni ndogo mno, kwa maana hiyo naomba nishauri Sheria ya Msajili wa Hazina iletwe Bungeni ifanyiwe kazi na kwa ushauri wangu ifutwe na tutunge sheria mpya na ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kukushukuru kunipatia fursa hii ya kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu. Namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anazozifanya hasa za kuwaletea maendeleo wananchi wetu katika Mkoa wa Kagera na hususan Wilaya ya Muleba. Kusema kweli wananchi wa Muleba wanampongeza sana na tunaomba salamu hizo zimfikie popote alipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake nzima; Naibu Waziri, dada yangu Maryprisca, alitembelea pale Muleba akajionea mahitaji makubwa ya maji wananchi wa Muleba waliyonayo. Pia nawashukuru Watendaji wa Wizara hii, kwa kweli mnafanya kazi nzuri, mnatupa ushirikiano mkubwa na ndiyo chanzo cha mafanikio ya Wizara hii. Tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru watendaji wa MURUWASA Mkoa wa Kagera na Muleba. MURUWASA pale Muleba mwaka huu wamekuwa watu wa nne kati ya Mamlaka Ndogo za Miji Midogo ambao wamefanya vizuri, ambayo inatolewa na EWURA. Kwa kweli wanastahili pongezi kwa kazi nzuri ya kuwahudumia wananchi wetu. Naomba Mheshimiwa Waziri hawa uwe unawaangalia mara nyingi sana. Wanaofanya vizuri hata kwenye bajeti yako uwe unawaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru Mheshimiwa Waziri, Muleba ametupatia karibu Shilingi milioni 328 kwa ajili ya kupanua mradi wa maji wa Wilaya ya Muleba. Pamoja na hizo fedha ambazo ametupatia, bado hazitoshi. Vile vile tunashukuru kwa kazi kubwa inayoendelea, na miradi inayoendelea katika Wilaya ya Muleba. Tuna mradi wa Maji Kata ya Buganguzi, tunaishukuru Serikali; tuna mradi wa maji Kishanda, Bureza, Gwanseli, Kasharunga, Kyebitembe, Kagoma, Rutenge na Ngenge. Kwa kweli tunashukuru kwa kazi kubwa inayoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa Mheshimiwa Waziri, hii kazi ambayo imeanza isije ikafika katikati tukaanza kusuasua au tukaanza kukimbizana. Tunajua kazi mnayoendelea nayo ni kubwa na tunaomba sasa hii kazi ambayo imeanza iendelee kama kauli ya Mheshimiwa Rais kwamba kazi iendelee. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri kwa miradi tuliyonayo Muleba isije ikaanza kusuasua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawashukuru kwa miradi mipya ambayo tutaietekeleza mwaka kesho tunawashukuru. Hata hivyo, ukitembelea Wilaya ya Muleba, tuna ukanda wa juu ambao kwetu tunaita Mgongo; lakini tuna ukanda wa chini Muleba Magharibi, hiyo ukanda wa chini wana matatizo makubwa sana ya maji. Kata za Kyemitembe, Kasharunga, Mbunda, Burungula, Ngenge, Butoro, kwa kweli Mheshimiwa Waziri chonde chonde tunakuomba, Kata zile zina matatizo makubwa sana ya maji. Katika miradi ambayo inatekelezwa, hakuna hata mradi mmoja ambao upo kwenye zile kata za ukanda wa chini ambazo zina matatizo makubwa sana ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri, endapo mtapata fedha kidogo nje ya bajeti, tunakuomba Mheshimiwa Waziri hiyo fedha ielekeze kwenye hizi Kata na wenyewe wakafurahie matunda ya Serikali ambayo inaongozwa na Mama yetu, mpendwa wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Watakushukuru sana na wataishukuru Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wilaya ya Muleba tuna visiwa 39 na tuna Kata tano ambazo zipo katikati ya ziwa, katikati ya maji mengi, lakini hazina maji safi na salama. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri na watendaji wako, hizi kata ambazo ziko visiwani zile huwa zinasahaulika kwa mambo mengi sana. Wana matatizo ya umeme, maji na wana matatizo ya kila kitu. Tunakuomba, Kata za namna hii ambazo kweli zimetengwa kijiografia, zimetengwa sijui na nini, lakini tuzipe faraja kwa kuzingalia kwa jicho la pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwa ajili ya Kata sita. Nimeuliza maswali ya nyongeza hapa Bungeni, na niliwahi kuleta swali la msingi na mara zote nimekuwa nikijibiwa kuwa, “Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huo mradi usanifu umekamilika na huu mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria kwa ajili ya kata sita za Wilaya ya Muleba ambazo ni Kata za Gwanseli, Magatakarutanga, Muleba Mjini, Buleza, Kikuku na Kagoma.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi ulianza kusanifiwa tangu mwaka 2009. Leo nilitegemea niukute kwenye bajeti, nimesoma vitabu vyote, hakuna kitu. Mwaka 2000 usanifu ulikamilika na nikaambiwa kwamba utakuwa kwenye bajeti ya mwaka huu. Kwa masikitiko makubwa; na nikuombe Mheshimiwa Waziri, hebu tuangalie. Wilaya ya Muleba ni Kati ya Wilaya ambazo zina matatizo na changamoto kubwa ya maji, ingawa tupo karibu na ziwa. Sisi tupo karibu na Ziwa, lakini hatuna maji. Ni mambo ya aibu. Najua kwa kazi na speed mnayoenda nayo na kwa mapenzi makubwa ya mama yetu, Rais wetu. Mheshimiwa Waziri ukija kuhitimisha hoja yako kesho, hebu tuambie, huu mradi unaanza kutekelezwa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua mnapata fedha nyingine, sehemu nyingine Mheshimiwa Waziri. Hebu tuangalie watu wa Muleba, tunawapenda sana na tuna matumaini na mapenzi makubwa sana na Serikali yetu. Tunakuomba huu mradi wa maji wa kata sita za Wilaya ya Muleba kutoka Ziwa Victoria uanze kutekelezwa sasa. Ni muda mrefu sana tumesemea haya mambo, tunaomba hili suala la kuja kuongea kila mwaka, kila siku, lipate suluhisho na hitimisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawashukuru sana kwa kazi ambazo zimefanyika. Kwetu wanasema, “Usiposhukuru kwa kidogo hata kile kikubwa hutakipata.” Mwisho, kuna tatizo la bei za maji. Ukiangalia miradi ambayo iko chini ya Mamlaka za Miji Mikubwa na Miji Midogo, ukilinganisha na hii miradi ambayo ipo chini ya RUWASA, kuna tofauti kubwa sana ya bei. Jana nilikuwa naongea na mtaalam wetu mmoja, nikamwuliza, kwa nini?

Mheshimiwa Spika, pale kwangu Muleba bei ya MURUWASA, Mamlaka ya Mji Mdogo; unit moja wanauza kati ya shilingi 800 mpaka shilingi 1,200 kulingana na matumizi; lakini nikienda kijijini kwangu, Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja pale akamtua mama ndoo, unit moja tunanunua kwa shilingi 2,500. Ukiangalia tofauti na pengo lililopo kati ya kipato kwa watu waliopo mjini na vijijini, vise versa nadhani ingekuwa applicable. Kwa watu vijijini kulingana na kipato chao kidogo tulitegemea bei ya maji iwe kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, tutafute namna nzuri ya ku-train hizi Kamati zetu za Maji hasa Makatibu wa hizi Jumuiya za Watumia Maji ili waweze kupunguza matumizi. Hayo matumizi yakishapunguzwa yawe reflected kwenye bei ya unit moja kwa watumiaji kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie tunapeleka fedha nyingi sana vijijini kwenye miradi ya maji, lakini hatuna watendaji ambao tumewaandaa kwa ajili ya kuhudumia wananchi kule vijijini, hasa kuunganisha maji. Matokeo yake tumeishia kupigwa fedha. Tunachukua mtu tumemwokotezea pale, unamweka pale akusanye fedha, wakati mwingine anakimbia hata na zile fedha. Tutafuta namna bora na sahihi ambayo itatusaidia kule vijijini kuhakikisha kwamba hii miradi tunayoijenga iwe endelevu na iweze kutumika kwa vizazi vyetu na vizazi vijavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa fursa hii kuchangia hoja hii ambayo iko mbele yetu. Nami nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuteuliwa na Naibu wake pamoja na timu nzima ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa ridhaa yako nisome kwenye randama ambayo imewasilishwa kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Kulikuwepo hoja nyingi sana ambazo zimejibiwa kwenye randama. Hoja namba sita ilikuwa inahusu ugawaji wa vitalu katika eneo la Ranch ya Mwisa II, na Wizara katika hiyo hoja imejibu. Naomba nisome. Serikali inasema, na ninaomba watu wangu wa Muleba wasikie. “Zoezi la ugawaji wa vitalu katika Ranch ya Mwisa II haliendelei.” Hiyo ni kauli ya Wizara ambayo naamini ni kauli ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendeleo kusoma. “NARCO inasubiri maelekezo ya Serikali baada ya Kamati ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kumaliza kazi yake iliyokuwa ikiifanya katika eneo la Mwisa II.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na ninaomba atakapokuja kuhitimisha hotuba yake, haya maneno ayaseme na ayawekee msisitizo na mkazo ili watu wangu wa Muleba ambao wameteseka sana, wananyanyaswa, wanaambiwa waondoke kwenye hili eneo ambalo ni eneo la makazi yao, kuna babu zao walizikwa pale, kuna makaburi yao, lakini leo unapokuja kuwaambia waondoke, Mheshimiwa Waziri haikubaliki hiyo, na hatutakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru watu wa Kigoma kwa mshikamano wao kuhakikisha kwamba Ziwa Tanganyika halifungwi. Nawapongeza kwa mshikamano wenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Mwisa ni eneo la wananchi wa Muleba. Nimesoma kwenye randama na hotuba ya Mheshimiwa Waziri, anasema, mmiliki wa Mwisa na Rutoro ni NARCO. Tangu lini? Kwa mamlaka ipi? Utakapokuja kuhitimisha hii hoja Mheshimiwa Waziri, naomba utuambie, kama eneo la Mwisa II na Rutoro ni mali ya NARCO, kwa nini tuna Hati za Vijiji ambavyo vimesajiliwa na tumepata hati za mwaka 2000? Inakuwaje Mheshimiwa Waziri? Mheshimiwa Waziri utakuwa mtu wa kwanza kuhamisha watu kutoka kwenye vijiji kuwapeleka mbugani na kuwaleta ng’ombe waishi kwenye vijiji, haikubaliki. Hii tutaiingiza kwenye vitabu vya Guinness sijui ya mwaka gani! Haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mwisa II limechukua muda wetu mwingi sana. Nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri, anaongelea migogoro ambayo imezaliwa mwaka 2022/2023 zaidi ya migogoro 55. Anasema wametatua migogoro 13 tu, ina maana NARCO kazi yake na Wizara ni kuingia na kutatua migogoro ambayo wanaisababisha wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 30 Juni, 2022 tulikaa katika Ofisi ya Waziri Mkuu, alituita kwa ajili ya kujadili suala la Mwisa na suala la Rutoro. Kati ya maazimio tuliyofikia, tulisema suala la Mwisa lisimame mpaka hapo tutakapopata suluhu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu. Nakushukuru umelitamka hilo Mheshimiwa Waziri. Nakuomba hayo uliyoyasema yawe ni maneno ya kweli na hao watu ambao wanapita huko Muleba kwenye hayo maeneo yenye mgogoro, wanawaambia wananchi wahame, sijui wawapishe wawekezaji; Mheshimiwa Waziri nakuomba, utakapokuja kuhitimisha utoe kauli yenye uhakika hapa ili watu waendelee na maisha yao. Naomba Serikali itamke, kama tunasubiri taarifa ya Waziri Mkuu, wananchi ambao waliishi kwenye hivi vijiji, waendelee na kazi zao za kuzalisha mali, na waendelee kulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea hapa nadhani wakati nachangia hotuba ya Waziri Mkuu, nilisema lile eneo la Mwisa ni kubwa. Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake amesema ni hekta 66,000, lakini naweza kusema ni zaidi ya hapo. Ndiyo maana tunaomba hili eneo likapimwe upya, vile vitalu vikapimwe upya, tukafanye uhakiki wa lile eneo. Sisi wakazi wa eneo hilo, tunalijua, siyo hizi hekta 66,000 alizotuambia, hapana, ni zaidi ya hapo. Tukishalipima upya, tukapanga matumizi bora ya lile eneo, tunakubali ndio, kaleteni wafugaji, lakini lazima lile eneo tukishalipanga tuhakikishe kwamba, tunatunza na mazingira ya lile eneo. Tunataka tupate maeneo ya kulima, tupate maeneo ya ufugaji na tupate maeneo ya mifugo kwa kutunza ikolojia ya Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme, lile eneo la Mwisa ndiyo eneo linalozalisha chakula kinacholisha Wilaya ya Muleba na Mkoa wa Kagera. Tunaposema tunakwenda kuweka wafugaji pale, tunautangazia njaa ambayo haitakuwa na ukomo Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hili tuliangalie. Naomba nisisitize na nitaendelea kulisisitiza suala la Mwisa II na NARCO ni maeneo ya vijiji vya wananchi. Ni vijiji vilivyosajiliwa na Serikali hii ambayo inasema ni vitalu. Sasa kupanga ni kuchagua; kama tutasema ni vitalu, then tutangaze. Serikali itoe tangazo kwa wananchi wote kwamba vile siyo vijiji ni vitalu, then wananchi mkawapangie maeneo mengine ya kuishi, siyo kuwaachia wenyewe watafute mahali pa kwenda. Haiwezekani! Hii nchi yao, wamezaliwa kwenye vijiji vyao, lazima tuwaheshimu na tuwape heshima yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye uvuvi, Kata ya Mazinga wamenituma nimwombe Mheshimiwa Waziri ifuatavyo: Kata ya Mazinga tuna kikundi kimoja kinaitwa UWAMAKAMA, wanasema waliomba mkopo, kwenye mikopo iliyotolewa na Wizara, lakini bahati mbaya hawakupata mkopo, hawaku- qualify, lakini wametekeleza vigezo vyote. Wanaomba kwenye mgawo wa mkopo ujao wapatiwe mkopo kwa ajili ya kufuga samaki wa vizimba. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Ishengoma. Muda wako umeisha.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kukupongeza wewe kwa kuongozo kikao hiki. Pia nimshukuru Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, nimshukuru Waziri Bashe kwa kazi kubwa wanayoifanya. Kwanza niombe Waziri, Mheshimiwa Bashe na Naibu wake, wapokee pongezi za dhati kutoka Muleba kwa kumteua ndugu yangu na ndugu yetu Rugambwa kuwa Wakala wa Mbolea, hongera sana. Wametusogezea mbolea karibu na wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo ombi Muleba, naunga hoja mkono lakini tuna ombi. Nimemsikia Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti yake akiongelea pampu na matenki madogo ya kumwagilizia mashamba. Kule Muleba tulikuwa tukilima kahawa na asilimia zaidi ya 40 ya kahawa yote Tanzania inatoka Mkoa wa Kagera na zaidi ya nusu ya kahawa inayotoka Mkoa wa Kagera inatoka Muleba. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri sasa kule Muleba akatusogezee karibu zile pampu. Hatutakubali visima, tunayo mito, tuna Mto Ng’ondo na mito mingine mingi tutavuta maji kutoka kwenye, mito tutamwagilizia kahawa. Nimhakikishie Mheshimiwa Waziri akifanya hili kwa kutuletea pampu pale Muleba sasa mavuno ya kahawa yanakwenda kuongezeka mara dufu. Natumaini Mheshimiwa Waziri amelipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tunazalisha kahawa, tumekuwa na matatizo makubwa sana hasa kwenye Mkoa wa Kagera na pale Muleba, lakini nimshukuru tena Mheshimiwa Waziri, mwaka huu soko la kahawa Wilaya ya Muleba limetulia, namshukuru sana na nimwombe aendelee kutia msisitizo kwenye hili. Kama hakuna utulivu kwa wakulima, kahawa itapotea lakini kwa kuwa tumewekeza na ametoa maelekezo thabiti tunamshukuru sana na aendelee kutusaidia. Wakulima wanamshukuru sana na wanaishukuru Serikali inayoongozwa na Mama Samia kwa kuwapa utulivu kwenye mazao yao. Tunaendelea kulisema na Waziri namshukuru kwa kulisema hili, kahawa ni mali ya wakulima, tuwalinde na tuhakikishe kwamba tunalinda mipaka ya nchi kahawa isitoke nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Profesa Muhongo amesema asubuhi na Kaka yangu Mwijage amechangia. Tukiangalia na tukifanya ulinganisho kati ya wakulima wa kahawa Nchini Tanzania na jirani zetu Uganda ni aibu kwa kweli. Mheshimiwa nakuomba Waziri kwenye hili tubadilishe mizania ya mauzo yetu nje ya nchi. Tunapolinganisha na nchi Jirani, hatupashwi kulingana nao, basically tunapashwa kuwa mbele yao, tukichukulia ukubwa wa Taifa letu, tukichukulia mikakati tuliyonayo na nimshukuru kwa mkakati aliokuja nao. Tunawaomba wakulima wetu hasa Wilaya ya Muleba.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo naongelea Muleba, Jimbo langu, tunaomba miche bora kwa ajili ya kilimo na ulimaji mpya wa mazao ya kahawa. Tunalo eneo kubwa na tumekuwa tukiongelea masuala ya Mwisa, kama utafuatilia mchango wangu kwenye mifugo na kilimo, tulisema badala ya kutuletea vitalu pekee yake tutenge eneo kwa ajili ya kilimo cha kahawa, tutenge eneo kwa ajili ya kufuga. Tunapoongelea kufuga na kulima ina maana tukipata mbolea kwenye vitalu vyetu tunaweka kwenye mashamba yetu ya kahawa na tunaongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili lazima tulifunganishe na uongezaji wa thamani wa kahawa tunayozalisha. Kagera tuna Kiwanda chetu cha TANICA pale. Sasa ni muda muafaka kwa Mheshimiwa Waziri akiangalie hiki Kiwanda cha TANICA ili kahawa inayozalishwa ikawe processed pale, tukiongezee nguvu, tukiongezee mtaji. Namshukuru Waziri nilipouliza swali juzi ameshachukua hatua. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia mizania hapa, Tanzania amesema kwenye Hotuba yake Mheshimiwa Waziri, mwaka jana tumeuza kahawa yenye thamani ya milioni 200 USD, lakini jirani pale ambaye ana eneo dogo ameuza zaidi ya milioni 862. Sasa tuna mkakati gani kuhakikisha kwamba tuna overtake huyu ili na sisi tuonekane, sisi ni wa 26, yeye jirani yetu ni watatu. Lazima tuwe na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba huyu jirani yetu tuna mpiku na sisi tunakuwa mbele yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, Kagera tuna zao la vanila, Mheshimiwa Waziri zao la vanila Kagera ambalo linalimwa na wakulima wengi na linalimwa kwenye mibuni yetu hiyo yaani inter-cropping tuna ndizi, tuna migomba, tuna kahawa, tuna pamba na vanila mle, lakini tuna tatizo moja, hatuna soko la uhakika la mazao ya vanila…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, naongezea mchango wangu wa jana.

Mheshimiwa Spika, nianze na Kiwanda cha TANICA Kagera. Naomba Wizara kupitia Bodi ya Kahawa ilipie hisa ambazo hazijalipiwa zenye thamani ya shilingi bilioni 8.6 katika Kiwanda cha TANICA cha Mkoa wa Kagera. Pia nashauri Wizara itusaidie kutafuta wawekezaji zaidi kwenye kiwanda hicho ili kiweze kupata teknolojia mpya. Kiwanda hiki ni muhimu sana kwani kinaongeza thamani kwenye kahawa yetu, tusikiachie kife Mheshimiwa Waziri.

Pili ni Skimu za Kyamyorwa, Buhangaza na Kyota Wilaya ya Muleba; nashukuru sana, naona Tume ya Umwagiliaji imepeleka wafanyakazi Kagera na zaidi Wilaya ya Muleba. Aidha nawashukuru wamepewa vitendea kazi.

Mheshimiwa Spika, naumba sana Waziri, Skimu za Kyamyorwa, Buhangaza na Kyota, Wizara kupitia Tume ya Umwagiliaji itusaidie kukamilisha skimu hizi ambazo Serikali yetu imeweka pesa nyingi ya walipakodi lakini haina tija kwa wakulima wetu kwa sababu haijakamilika. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, nimechangia sana Bungeni kuhusu skimu hizi, nakuomba uzikamilishe kwa ajili ya watu wa Muleba na Tanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Building Better Tomorrow (BBT), Muleba tuna eneo kubwa la Mwisa II zaidi ya hekta 80 ambazo ndio busket food kwa Wilaya ya Muleba na Mkoa Kagera kwa ujumla. Eneo hili linafaa sana kwa kilimo, sana mahindi, maharage na mchele. Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kupitia NARCO walipima eneo hili vitalu jambo ambalo linatishia usalama wa chakula mkoa wa Kagera. Nawaomba eneo angalau nusu yake litumike kwenye mradi wa BBT.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ya kutuletea maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, Watendaji Wakuu wa Wizara na Watendaji wote wa RUWASA nchi nzima, lakini zaidi Meneja wetu wa RUWASA, Mkoa wa Kagera, Ndugu yangu Warioba, mtani wangu; na Meneja wetu wa Wilaya Muleba, Jerome. Ni watendaji wazuri sana, wanafanya kazi iliyotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea suala la upotevu wa maji. Mheshimiwa Waziri naomba hili uliangalie sana. Ukiangalia standard ya ulimwengu, upotevu wa maji haupaswi kuzidi asilimia 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko kwenye Kamati ya PIC, mamlaka nyingi ambazo tumezitembelea, unakuta wanaongelea upotevu wa maji zaidi ya asilimia kati ya 30 mpaka 40. Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji wakati anachangaia hapa, amesema mabomba mengi yanapasuka, na yanapopasuka hatuchukui hatua za haraka kwenda kuyaziba. Hapa ndipo tatizo lilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi, huu upotevu wa maji, mara nyingi sana sisi ambao tumefanya kazi ya kuwalinda walaji, nimefanya kazi kwenye hiyo sekta. Unakuta unabebeshwa watumiaji kwa makosa ambayo yanafanywa na watu wengine, wanakuja kubebeshwa watumiaji. Naomba Waziri uliangalie hili, uwasisitize watendaji wako wawe wanachukua hatua za haraka kuziba mabomba ambayo yanapasuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri, jana tulikutana na management yake pale Wizarani. Kilichonipeleka pale Wizarani ilikuwa ni Mradi wa Muleba wa kutoa maji Ziwa Victoria. Huu mradi nimeuongelea mara nyingi sana. Tangu nije hapa, ni mwaka wa tatu naongelea mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea mwaka huu nitakuta kwenye bajeti, lakini nashukuru kwa commitment aliyotoa Mheshimiwa Waziri jana, na kwa commitment hiyo nategemea bajeti ya mwaka kesho, tulishauriana tukakubaliana kwamba sasa tutautekeleza kwa awamu. Nami nakubaliana na pendekezo la Mheshimiwa Waziri. Sasa isiishie hapa, au pale mezani ofisini kwake. Naomba mwaka kesho nilione kwa vitendo, na hii itampa heshima sana Mheshimiwa Waziri, na zaidi itampa heshima sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Wilaya ya Muleba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu kuona wilaya ambayo iko pembezoni mwa ziwa tunahangaika na maji. Tuna miundombinu ya maji, tuna maji pembezoni mwa kata zetu, lakini hatuna maji. Mheshimiwa Waziri nakuomba hili ulichukue kwa uzito wake, na tukipata mradi huu wa Ziwa Victoria wa kuhudumia kata sita, itatusaidia, hasa maji yanayotumiwa Kata ya Muleba, sasa yataweza kusaidia Kata za Ikondo, Kata ya Kibanga na Kata ya Biirabo na Kata ya Nshamba, tutakuwa tumehudumia hizo kata nyingi kwa mradi huo mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Wizara, tuna miradi mipya miwili. Tuna mradi wa Chebitembe Kisana kwenye hii bajeti, lakini tuna mradi mwingine wa Bushagara. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Rais kwa miradi hii na miradi mingine ambayo inaendelea. Naomba hiyo miradi mingine ambayo inaendelea isije ikasimama. Kazi kubwa imefanyika, na inaendelea kufanyika, tunaomba sasa kama wachangiaji wengine walivyosema, wakandarasi wale wapewe fedha ili miradi iendelee kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kata zetu ambazo ziko visiwani. Tuna kata tano Wilaya ya Muleba. Tuna Kata ya Ikuza, Kata ya Mazinga, Bumbire, Kerebe na Goziba. Hizi ni kata ambazo ziko katikati ya Ziwa Victoria. Tunakuomba utengenezwe utaratibu mzuri, kwani wenyeji wa kule ni wavuvi lakini hawana maji safi na salama, wanatumia maji ya ziwa ambayo siyo salama kwao. Tunakuomba ututengenezee utaratibu mzuri, angalau bajeti ya mwaka kesho hizi kata ambazo ziko katikati ya ziwa na wenyewe tuwakumbuke, ni Watanzania wenzetu na wanastahili kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa hili, Wilaya ya Muleba, hasa Muleba Magharibi, tulikuwa na matatizo makubwa sana. Mheshimiwa Waziri tuliongea jana ofisini kwako na umetupa commitment kwamba gari likitoka Karagwe liende Wilaya ya Muleba kuchimba visima kwenye hizi kata ambazo zina uhaba mkubwa sana wa maji hususan Kata za Kyebitembe nashukuru kuna Mradi wa Kyebitembe sana.

Mheshimiwa Mweyekiti, umetupa visima kwenye hizo baadhi ya kata. Kata ya Burungura, Kasharunga na Kata ya Karambi, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa commitment hiyo natumaini sasa mwaka kesho tutakapokuja hapa hatutakuja kuimba wimbo uleule, kibwagizo kilekile nakuomba tuendelee kufanya kazi tutakuunga mkono na bajeti yako mimi kwa commitment hii jana nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru na la mwisho kwamba nilikuwa na tatizo sana kwenye kijiji changu cha Msalala. Mheshimiwa Waziri kati ya visima ambavyo tumepata visima 10 Wilaya ya Muleba nakuomba na utoe maelekezo mahususi, kisima cha Chakaseni kuchimbwe Msalala, kule eneo la Msalala wana matatizo makubwa sana ya maji, wananunua ndoo moja ya maji mpaka shilingi 1,000 kwa sababu ya uhaba huo wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mmeishatoa commitment kwamba kisima kinakwenda kuchimbwa pale nikuombe Mheshimiwa Waziri utoe maelekezo wakati unatoa hotuba yako ya mwisho na natumaini na watendaji wako wa RUWASA Kagera wakachimbe kisima cha kwanza lile eneo la Msalala, umetupa kisima kimoja nadhani hakitoshi. Mheshimiwa Waziri kwa busara yako kwa sababu kuna watu wengi sana pale na ni mkusanyiko wa watu wengi hasa wavuvi na wanaokuja kununua dagaa ungetuongezea kimoja viwaka viwili watu wa Msalala watakushukuru sana na tutakutafutia samaki utakapo tembea Mkoa wa Kagera kuna guest house nzuri pale ukalale pale watakuandalia chakula kizuri sana kwa heshima utakayokuwa umewapatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, niwatakie utendaji mwema wa kazi haya maelekezo mahususi ulimpatia Katibu Mkuu dada yangu Nadhifa kuhusu suala la kata sita kutoa maji Ziwa Victoria waandae kazi hiyo kwa haraka iweze kutekelezeka mwaka kesho niione kwenye bajeti. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha mchango wangu kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema. Nampongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi iliyotukuka ya kuliongoza Taifa letu. Nakupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na wasaidizi wao na timu nzima ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, nachangia maeneo matatu nikianza na ujenzi wa barabara ya Muhutwe - Kamachumu - Buganguzi - Kishanda - Nshamba - Muleba (Mujungi Road); barabara hii ina urefu wa kilometa 54. Barabara hii ilianza kujengwa kidogo kidogo tangu Serikali ya Awamu ya Nne, mpaka jana unasoma bajeti yako ya mwaka wa fedha 2023/2024, barabara hii imejengwa kwa kiwango cha lami kilometa 38 tu. Kwa taarifa kilometa 3.8 ziko kwenye maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, sehemu ya barabara iliyobaki ni kilometa 12 tu ili barabara hii ikamilike. Barabara hii imejengwa kwa muda mrefu. Nimeangalia kwa makini bajeti yako ambayo naichangia, barabara hii imetengewa kiasi kidogo cha pesa ambazo zitajenga labda kilometa moja tu. Naomba sana, barabara hii ni muhimu sana, nakuomba uongeze bajeti angalau kilometa saba ili bajeti ya mwaka ujao tumalizie ujenzi wa barabara hii. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri tumalizie ujenzi wa barabara hii kabla ya uchaguzi wa mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, pili ni ujenzi wa uwanja wa ndege wa Omukajunguti; uwanja wa ndege wa Bukoba sio salama kwa kuruka na kutua ndege zetu za ATCL na Precision Air. Ndege hizi zinahitaji kutua kwenye uwanja wa ndege wenye njia ya kuruka na kutua ndege urefu kilometa mbili. Uwanja wa ndege wa Bukoba una njia ya kuruka na kutua ndege wenye urefu wa kilometa 1.5. Kwa bahati mbaya uwanja huu hauwezi kupanuliwa kutokana na jiografia ya eneo letu. Kwa sababu hiyo, nakuomba ujenzi wa uwanja wa ndege wa Omukajunguti ufanyike kipindi hiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupewa fursa ya kuchangia hoja ambayo iko mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kazi kubwa anayoifanya ya kulijenga Taifa hili. Kwa wizara hii niwashukuru kwa kuleta habari njema katika Mkoa wa Kagera kwa vizimba 9 ambavyo wametupatia, na vinne vinakwenda wilaya ya Muleba wanakwenda kututengenezea ajira hii ni habari njema kwa wakazi wa Muleba na wakazi wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru tena kwa kutupatia boti moja na injini moja Wilaya ya Muleba kama ambavyo nimekuwa nikichangia ni wilaya yenye visiwa vingi yenye maji mengi lakini pia yenye matatizo mengi vizimba vinne tunashukuru tukiongezewa vingine viwili tutashukuru zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niende kuchangia suala la migogoro kati ya wakulima na wafugaji katika Wilaya ya Muleba. Naomba niseme ni Mbunge wa Wilaya ya Muleba, Wilaya ya Muleba tuna Kata 43 lakini ni wilaya yenye majimbo mawili ya uchaguzi niko mimi na yupo kaka yangu Charles Mwijage. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi amechangia lakini kilio chetu migogoro au mgogoro mkubwa wa ardhi ambayo NARCO ameichukuwa ameivamia, bila kufuata taratibu za kisheria na ninashangaa sijui kama NARCO wana mwanasheria pale. Hili utengeneze Ranch hii ardhi ya halmashauri ichukuliwe kwa ajili ya matumizi ya umma upo utaratibu. Huwezi kuamka asubuhi unakwenda unavamia ardhi ya halmashauri yeyote kwa kisingio chochote kile bila kufuata utaratibu unasema naanzisha Ranch hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro wa Mwisa na Utoro au hizi Ranch za Rutoro na Mwisa imeanzishwa kinyume cha sheria cha sheria za nchi hii. Rutoro kilikuwa Kijiji tangu mwaka 1976 mwaka 2005 NARCO wakaenda wakapima Ranch pale mwaka 2010 Serikali hii Tukufu ikapandisha hadhi Kijiji cha Rutoro ikawa kata vile vitongoji vilivyokuwa chini ya kile Kijiji ikapandishwa hadhi vikawa vijiji, sasa nashindwa kuelewa NARCO wamepima vitalu mwaka 2005 sijui kwa mamlaka ipi lakini Serikali mwaka 2010 inapandisha vile ambavyo vimepimwa kama vitalu inaipa hadhi ya kata na vitongoji inaipa hadhi ya kijiji sielewi hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria tunazitunga sisi wenyewe na lazima mashirika na taasisi za Serikali zifuate sheria. Katika mgogoro huu wa Mwisa unahusisha kata saba Mheshimiwa kaka yangu Mwijage asubuhi amesema wananchi ambao wako kwenye hizo Kata za Kebitemba, Karambi Kasharunga Mbunda Burungula Genge na Rutoro ambazo zina vijiji 12 vitongoji 19 wako kwenye kilio na kazi ya mama ni kupangusa watu wanaolia machozi namuomba mama awapanguse hao watu wa vitongoji 19 awapanguse machozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamelia sana naomba kilio chao kifike mwisho. Lakini NARCO wamekwendaje kwenye eneo la Mwisa na lenyewe ni kizungumkuti hakuna sheria yoyote ile ambayo wameifuata kama nilivyotangulia kusema ili ardhi yoyote itwaliwe lazima Sheria ya Ardhi ya Vijiji ifuate sheria namba tano ukisoma kipengele cha section 4 subsection one ya sheria ya ardhi ya vijiji ili waanzishe Ranch Rais lazima atwae lile eneo na anapolitwaa kuna hati ambayo inatolewa na nimesoma bajeti ya Mheshimiwa Waziri wakati anasoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma kiambatisho kwenye hotuba yake kiambatisho namba 15 imeongelea migogoro ya NARCO kiambatisho namba 12 ameongelea maeneo ambayo yametwawaliwa na NARCO yametolewa notice ya Serikali lakini kiambatisho 11 ameongelea maeneo ambayo yametwawaliwa bila notice ya Serikali sasa nashangaa unatwaaje maeneo unaanzisha ufugaji bila kufuata sheria hakuna notice hakuna nini tunashindwa kuelewa nchi tunaipeleka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi ardhi yao imechukuliwa kinyume cha sheria hapa tunapoongea kwenye lile eneo ambalo wametwaa kinyume cha sheria hakuna notice na nitamuomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hapa atuambie bila kupepesa macho eneo la Rutoro notice ambayo inakupa mamlaka ya kulichukuwa ni notice ya mwaka gani ya tarehe ngapi, ya siku gani utuambie na wananchi wasikie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utuambie eneo la Mwisa umelipatajepataje kama kuna notice ya Serikali utuambie notice namba ngapi kama hakuna notice uwaambie wananchi wa Mwisa ambao leo wananyanyaswa wanaamishwa na hakuna mtu ambaye anafuata hata sheria ya kuhamisha makaburi mnaleta mifugo mnalishia kwenye makaburi ya wazazi wetu wazee wetu ambao wamepumzika pale hatuwezi kukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kama hakuna notice hiyo tuwatangazie wananchi ambao wanahamishwa waendelee kuishi kwenye maeneo yao mpaka utaratibu utakapofuatwa. Mheshimiwa Rais anayo madaraka akiamua atatwaa ile eneo afuate utaratibu.

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Dkt., Kengele ya pili hiyo, ahsante.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO Mheshimiwa Naibu Spika, sitaunga hoja mkono mpaka nipate maelezo ya kina, tupate zile notice.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa nami kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Nimesoma Bajeti ya Serikali, nimeona kuna mambo mengi mazuri, hongera sana Mheshimiwa Waziri. Naipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia tozo ya Shilingi 100/= kwenye mafuta. Nadhani tunapoweka tozo kwenye mafuta, ina madhara makubwa kwenye uchumi kwa sababu inakwenda kwenye usafirishaji na itasababisha mpasuko, kupanda gharama kwenye sekta nyingine za uchumi. Nashauri, tuna mitandao ya kijamii; Instagram au tuseme social media, tungeangalia huko tukaiepeleka kule kwa sababu unapoipeleka kwenye social media haina madhara makubwa kama ambavyo tumependekeza kuipeleka kwenye mafuta. Huo ni ushauri wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye kilimo. Wachangiaji wengi wamesema na ndivyo hali ilivyo, kilimo kinahusisha watu wengi Tanzania, hasa wenye kipato cha chini. Tunao Mradi wa BBT, lakini huku kwetu tunakotoka tunalima zao la kahawa, ndiyo zao kubwa sana, lakini ni zao ambalo linaiingizia kipato kikubwa nchi hii. Ukiangalia wakulima ambao wanachangia pato la Taifa kupitia zao la kahawa, ni wakulima wadogo wadogo wenye mashamba madogo madogo; ekari moja, nusa ekari na ndio hao wanaochangia uzalishaji wa kahawa hasa Mkoa wa Kagera. Mkoa wa Kagera tunazalisha zaidi ya tani 40,000 na ndiyo hizi tunakwenda kuuza nchi za nje na kutuletea fedha za kigeni, lakini ukiangalia mashamba ya wakulima, yanatia hofu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwenye bajeti hii tuangalie jinsi ya kuongeza uzalishaji wa kahawa kwa kuyahudumia haya mashamba madogo madogo ya wakulima wadogo wadogo, ambao huwa wanawasomesha watoto wao na kutunza familia zao. Haya mashamba tukiyapatia kipaumbele, tukahakikisha kwamba wanapewa mbolea na ruzuku kuhakikisha kwamba haya mashamba yanahudumiwa; na ndiyo yanaweza kutoa kwenye mauzo ya kahawa ambapo mwaka 2022 tulipata shilingi bilioni 240 tukaenda mpaka shilingi bilioni labda 500 tukaanza kushindana na jirani zetu Uganda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Uganda na Tanzania, pamoja na kwamba Tanzania ni nchi kubwa, lakini bado mauzo yetu ya nje ni kidogo. Hili ni eneo ambalo tunaweza tukapata fedha nyingi kutokana na mauzo ya kahawa. Naomba tulifanyie kazi. Ila hatuwezi kulifanyia kazi hivi hivi, lazima tuangalie na kiwango gani cha kahawa tunauza nje ambacho bila kuongezea thamani. Tuna viwanda vidogo vidogo. Kwa mfano, kwenye wilaya yangu pale, vipo viwanda ambavyo vinaongeza thamani zao la kahawa, lakini hatuvipatii kipaumbele kuongeza kiwango cha kahawa ambacho wanakifanyia kazi na kuki-process ili tuuze nje zao ambalo tumeshaliongezea thamani. Kahawa nyingi tunaiuza kama raw material.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo, pale Kagera tuna kiwanda kikubwa cha TANICA. Pamoja na kwamba Mkoa wa Kagera tunazalisha zaidi ya tani 40,000, lakini kiwango ambacho kiwanda chetu cha TANICA kinaweza ku-process ni tani 1,500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naishukuru Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, mwaka huu kupitia Bajeti ya Kilimo, Mheshimiwa Waziri ameahidi kutupatia Shilingi bilioni 8.7 ili kukipatia kiwanda hiki mtaji wa uendeshaji, lakini kukipatia mtaji wa uendeshaji pekee yake, haiongezi lolote. Napendekeza kiwanda hiki tukipatie mtaji wa kuboresha mitambo yake, kwani kina mitambo ambayo imepitwa na wakati, teknolojia wanayoitumia inasababisha kupoteza kahawa nyingi. Ndiyo maana mauzo yetu ya nje kwa kahawa ambayo imeshakuwa processed ni madogo mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile pamoja na kwamba ni madogo, ukiangalia bei ya kilo moja ambayo inazalishwa na TANICA, kwenye soko inauzwa dola 8.5 wakati kahawa inayotoka nje kwa kilo moja hiyo hiyo inauzwa dola nne. Sasa ukiangalia uwiano wa bei, mazao ambayo yanatokana na kiwanda chetu hayawezi kushindana katika soko lolote, kwa sababu tunazalisha kwa gharama kubwa, kwa kuwa teknolojia tunayoitumia ni ya zamani. Kiwanda hiki kilijengwa tangu mwaka 1963 na tangu hapo hatujawahi kukipatia mtaji kuboresha teknolojia. Nadhani ni muda muafaka sasa kukipatia mtaji kiwanda hiki ili tuweze kubadilisha teknolojia kiweze kuzalisha na mazao yake yaweze kushindana na mazao mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kahawa ambayo tunaizalisha hapa nchini, hasa ile inayotoka Bukoba ni kahawa nzuri, na ukiipeleka kwenye Soko la Dunia popote, itapata wanunuzi lakini tatizo tulilonalo ni kwamba hatuwezi kushindana kwa sababu hatuna teknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiachana na suala la kahawa, wakati tunachangia Wizara ya Ustawi wa Jamii, tuliongelea masuala ya ustawi wa jamii na maendeleo ya jamii. Tunalo tatizo kubwa sana nchi hii. Wizara yenyewe inaongelea zaidi masuala ya maendeleo ya jamii na masuala ya maendeleo ya jamii ni Wizara zote. Tumesahau Sekta ya Ustawi wa Jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Mheshimiwa Waziri anapokuja kutoa hitimisho, tuangalie hili suala la ustawi wa jamii. Tumeongelea vijana wetu kuharibiwa, tumeongelea matatizo ya jamii yanayoendelea, ni kwa sababu tumesahau hii sekta muhimu ya ustawi wa jamii. Tunakimbizana na maendeleo, lakini tumeshindwa kuwekeza vya kutosha kwenye ustawi wa jamii. Napendekeza tuangalie kwenye bajeti yetu, tuone kwa jinsi gani tunaweza kuisaidia Wizara tukajenga rehabilitation centers kwenye majiji makubwa ambako kuna mmomonyoko mkubwa sana wa maadili na vijana wetu wameharibiwa, ili wale ambao wamebainika kwamba wamepata matatizo/wameharibiwa waweze kupelekwa kwenye rehabilitation center na kuwarududisha katika hali yao ya kawaida, waweze kubaki kwenye jamii na kuendelea na uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi kwenye jimbo langu, naishukuru sana Serikali, imefanya kazi kubwa sana, imetujengea shule, vituo vya afya na hospitali. Kama wachangiaji wengine walivyosema, sasa ni muda muafaka wa kuhakikisha kwamba Serikali pale ambako imejenga vituo vya afya na hospitali tupatiwe watendaji ili tuweze kupata thamani ya fedha ambayo tumeiwekeza kwenye miundombinu ambayo imejengwa na Serikali kwa fedha nyingi za walipakodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Naishukuru Serikali kwa kazi kubwa ambayo inaendelea kuifanya, namshukuru Rais wetu, Wizara na Watendaji wote wa Wizara husika kwa kutuletea bajeti ambayo nadhani itatuvusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)