Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Jackson Gedion Kiswaga (2 total)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, kwa kuwa suala la Mlima Kilimanjaro ni suala nyeti kwa uchumi wa nchi, na ni maeneo muhimu sana ambayo yanatuletea fedha nyingi pamoja na Ngorongoro na Serengeti; na Jeshi la Kujenga Taifa limeonesha uwezo mkubwa katika operesheni mbalimbali katika nchi hii: -

Je, kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kuwa hata na kambi ndogo ndogo mbili hata za wanajeshi watano au sita, kuzunguka Mlima Kilimanjaro? Kwa sababu kwenda mbele inawezekana kuna wivu mkubwa unajitokeza kwa sababu ya matangazo makubwa ambayo tunayafanya ya kuleta watalii katika nchi hii.

Swali ni kwamba je, kwa nini Serikali isione umuhimu wa kuwa na kambi kambi ndogo ndogo mbili za Jeshi ili kulinda Mlima Kilimanjaro?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tukio hili moto Mlima Kilimanjaro linajitokeza pia na maeneo mengine na linatokana na baadhi ya watu wasiopenda mema ambao pia hawataki hata uhifadhi, huchoma moto maeneo yote yanayotakiwa kuhifadhiwa kama ambavyo ingekuwa kupitia elimu mbalimbali zinazotolewa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sasa tumeona tatizo hilo na katika kipindi cha muda mrefu tulikuwa hatujapata moto kiwango hicho kwenye Mlima Kilimanjaro, lipo jambo tumejifunza. Ushiriki wa majeshi yetu yote; JWTZ, Jeshi la Mgambo, Jeshi la Polisi, na wananchi pamoja na Skauti na makundi mbalimbali yaliyojitokeza kwenda kuzima moto, tayari baada ya zoezi hilo litakapokamilika, tutakaa chini kufanya tathmini.

Swali lako ambalo limeingia pamoja na ushauri, tutauzingatia ili sasa tuwe na mkakati endelevu kwenye maeneo mengi muhimu ambayo yanaweza kujitokeza tatizo la moto, ikiwemo na kuimarisha Kitengo cha Maafa na hasa kwenye maeneo ya moto. Kuwa na vifaa, kuwa na wataalam ambao pia wanapata mafunzo ya mara kwa mara ili tuweze kukabiliana na majanga haya yanapotokea popote pale.

Mheshimiwa Spika, naomba kupokea pia na ushauri aliutoa Mheshimiwa Kiswaga. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kumwuliza Waziri Mkuu swali. Kwa kuwa tabia za watu za uharibifu wa mazingira zimesababisha kuwa na nchangamoto za ukosefu wa mvua na hivyo kuhatarisha pengine usalama wa chakula katika Taifa letu na hivyo kusababisha pia mabadiliko ya tabianchi: Je, ni mpango gani wa Serikali sasa kuzuia kabisha shughuli za kibinadamu kwenye milima yote na vilima vyote ili sasa tuwe na mvua za uhakika na hivyo kulifanya Taifa liendelee kuwa imara katika emneo hilo? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la uhifadhi wa mazingira Serikali yetu tumeliwekea nguvu kwa sababu tunataka tulinde mazingira haya kwa misitu yetu, mito na vyanzo vya maji kwa lengo la kufanya Taifa hili kuwa endelevu na kutoa fursa za upatikanaji wa maji na pia tupate mvua za kutosha kupitia misitu.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais eneo la Mazingira wamefanya kazi kubwa na wanaendelea kufanya kazi kubwa kukabiliana na uharibifu wa mazingira. Kwanza ziko sheria zinasimamia uhifadha wa mazingira ambapo pia wenyewe tumeendelea kushirikisha mpaka kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa; mkoani, wilayani na kwenye halmashauri zote na vijijini ambapo ndiyo misitu ilipo, kila mmoja ashiriki katika uhifadhi wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, pia tumeendelea kutoa elimu kwa Watanzania kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira, misitu yetu pamoja na vyanzo vya maji kwa sababu vyote hivi vina umuhimu mkubwa kwenye maisha ya kila siku ya binadamu. Hata hivyo, tumekuwa tunashirikisha taasisi mbalimbali za umma na zile za binafsi kwenye uhifadhi wa mazingira na kwenye eneo hili tunaungwa mkono sana. Malengo yetu ni kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi ni programu mbalimbali zilizoko ndani ya Serikali zinazosimamia uhifadhi wa mazingira kwenye milima hiyo ya miinuko, kwenye mabonde na maeneo yote ambayo yana misitu ambayo tunaitumia kwa ajili ya kuhifadhi mazingira yetu. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania, kwanza kuona umuhimu wa uhifadhi wa mazingira kwa maslahi yetu.

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya kupatikana kwa mvua yanatokana na uharibifu wa mazingira ambao sasa unaendelea; pia ukosefu wa maji kwenye maeneo ambayo tulikuwa tunatarajia tupate maji kama vyanzo ili tujenge miradi ya maji inatokana na uharibifu wa mazingira. Madhara haya na madhara mengine ndiyo yanasababisha sasa kuwa na mabadiliko ya majira, kuhamahama kwa wanyama kutoka kwenye maeneo yao kuhamia kwenye maeneo mengine wakitafuta maji na aina nyingine yoyote ya usumbufu ambao tunaupata.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, nataka niwakikishie kwamba Serikali inao mpango huo wa kuhifadhi mazingira, kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na tumeipeleka hiyo mpaka TAMISEMI, tusimamie kwa pamoja tuhakikishe kwamba nchi yetu tunakabiliana na uharibifu wa mazingira. Kwa kufanya haya, tunaweza sasa tukaokoa mazingira yetu na tukaanza kunufaika na uwepo wa misitu hii, vyanzo vya maji na aina nyingine yoyote ya uhifadhi ambayo tumeiwekea sheria, na tutaendelea kuimarisha sheria zetu na kusimamia sheria zetu. Vile vile taasisi zote ambazo zinahusika katika uhifadhi zisimamie kikamilifu. Huo ndiyo mkakati wetu tulionao ndani ya Serikali, ahsante sana. (Makofi)