Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jackson Gedion Kiswaga (23 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya kipekee niliyopewa ya kuweza kuchangia hotuba ya Rais. Kwa kweli, kwanza nimshukuru Rais mwenyewe na Chama changu cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi ya kugombea kuwa Mbunge wa Jimbo la Kalenga. Pia niwashukuru wananchi wa Kalenga pamoja na familia yangu kwa kunisimamia, kuniamini, kuniombea, mpaka leo nimesimama hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu ameendelea kuliweka Taifa hili katika hali ya amani. Ndiyo maana hata leo Watanzania tunaweza kufanya mambo yetu kwa uhuru ni kwa sababu, tunaye Rais ambaye anapenda amani na kweli ameilinda amani. Pia namshukuru Rais kwa sababu ya nidhamu kubwa ambayo ameileta kwenye Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, George Washington alisema kwamba imani ni roho ya jeshi. Jeshi dogo katika kukaa kwa pamoja linaweza likafanya mambo makubwa. Ndiyo maana sasa kama nchi tumeweza kuingia katika uchumi wa kati kwa sababu ya ile nidhamu kama Taifa ambayo tumejijengea. Kwa hiyo, nimshukuru sana Rais kwa ajili ya hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi na Watanzania wengi tunamuunga mkono, tuko pamoja naye pamoja na vijembe vinavyoendelea vya watu wasio na macho ya kuona uzalendo mkubwa huu unaofanywa na Rais wetu. Tupo Watanzania ambao tutamtetea usiku na mchana na nchi hii itafika kwenye hatima yake tukufu na sisi tukiwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa habari ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais yako mambo mengi, lakini mimi niliona nianze kujielekeza kwenye kilimo. Upande wa kilimo hii Program ya Pili ya Kuendeleleza Sekta ya Kilimo ukiitizama imejaa majawabu mengi sana ambayo yataleta majawabu makubwa ya upungufu wa chakula katika Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nafahamu kwamba bado haijaanza kupewa pesa. Kama hii Program ya Pili ikianza kupewa pesa tutatatua changamoto nyingi kwenye kilimo. Kwa mfano, tumeeleza kwa mapana sana ni namna gani tutakwenda kutengeneza skimu za umwagiliaji. Tukianza kuipatia pesa tunaweza kuanza kuwapa Maafisa Ugani pesa kidogo, kwa mfano Afisa Ugani mmoja kwa kila kata; tukachagua kata fulani kwamba huyu akatengeneze miche ya korosho, huyu akatengeneze kishamba-darasa chake cha miche ya parachichi watu wakaenda kujifunza pale wakapata ujuzi na wakaendelea. Serikali ina-finance kwa kumpa ruzuku na yeye huyu Afisa Ugani atapata pesa kwa sababu utakuwa ndiyo mradi wake. Tukifanya namna hii tutakuwa tumetengeneza motisha kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni namna gani tunalinda ardhi. Ardhi yetu imeendelea kufa kwa sababu ya sumu kali. Je, hizi mbolea ambazo tunaleta sijui tunazikaguaje kwa sababu nimepita maeneo mengi yalikuwa mazuri unakuta sasa hakuna kinachoota kwa sababu ya mbolea za sumu. Suala hili tuliangalie sana namna gani tunaweza kulinda ardhi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwenye mbegu, hata Rais ameendelea kuzungumza. Ndugu zangu sasa hivi biashara kubwa duniani ambayo itakuwa kama ya mafuta ni biashara ya mbegu. Kuna vita kubwa hawa wakubwa kutuletea mbegu, nimeona sehemu fulani walileta migomba ikawa inazaa sana lakini mwishoni inaoza. Kwa hiyo, kama Taifa ni lazima tujielekeze katika kutunza mbegu zetu za asili ili tusifike mahali tukawa watumwa na tukizembea tutakuwa watumwa kwelikweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni linalohusu masoko kwenye kilimo. Watu wamekuwa wakizungumza kwamba tusiuze bidhaa Kenya. Haya ni makosa makubwa na nisingependa mtu azungumzie habari ya kutokuuza bidhaa Kenya. Mimi nalima parachichi pale Njombe, Wakenya wanakuja shambani kwangu wananunua kilo moja Sh.1,500/= parachichi inayobaki naenda kuuza kiwandani kilo moja Sh.300/= sasa wewe unasemaje Mkenya asije kununua, nikauze wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala la msingi tulete ushindani. Tuhimize wafanyabiashara wakubwa kama ilivyo kwa Coca washindane lakini usizungumzie habari ya kutokuuza Kenya ni kosa kubwa sana hilo. Kwa hiyo, suala la masoko kwanza tuache kuwazuia Watanzania kuuza bidhaa zao nje kwa sababu tunavyowazuia tunapunguza pia tija mazao yanaendelea kuoz. Kwa hiyo, hilo ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine kwenye kilimo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mfupi wa mdomo, napenda nisisitize juu ya uwekezaji kwenye ardhi. Inakisiwa kuwa ifikapo mwaka 2050 dunia itakuwa na watu wapatao bilioni 9.7. Watu wote hawa watahitaji kula, hivyo watahitaji ardhi kwa ajili ya kilimo. Nchi yetu haina umakini wa kutosha namna tunavyowapa wageni ardhi. Wawekezaji wengi wanakuja tunawauzia ardhi kwa maana kuitumia kwa shughuli za kilimo kwa miaka 33, 66 au 99.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania kihistoria haina ardhi tupu. Aidha, itakuwa inamilikiwa na familia, koo fulani au Serikali za vijiji. Mara nyingi wakija hawa wawekezaji tunazichua ardhi hizi kutoka kwa watu wanaohodhi na kuwapa wawekezaji kwa bei ndogo sana na kwa kuwa maeneo ya uwekezaji kwenye ardhi yanazidi kupungua, tusipozingatia tutakuja kujikuta ardhi imekwisha na kundi kubwa vijijini litabaki bila ardhi na hii inaweza kuwa hatari kwa usalama na usitawi wa watu na Taifa lao.

Napendekeza itungwe sheria au miongozo ya kusaidia Watanzania wabaki na ardhi yao ila itambuliwe mahali ilipo, inamilikiwa na nani na kiasi gani na inafaa kwa kilimo cha mazao gani. Mwekezaji akija tumwambie ardhi ya uwekezaji ipo mfano Kalenga ni eka kadhaa inamilikiwa na kijiji au watu binafsi. Unakaribishwa kuwekeza ila ardhi sio yako ingawa unaruhusiwa kuwekeza mfano kwa miaka 40 lakini tutamiliki kwa hisa ardhi hiyo wewe mgeni chukua asilimia 80 kwa kuwa unaleta pesa na ujuzi na kijiji au mtu binafsi wachukue asilimia 20 ya mazao au faida inayotokana na mazao hayo. Jambo hili niliona muhimu sana, litavijengea uwezo vijiji vyetu na watu wetu, itaimarisha uchumi wa vijiji na watu wake. Nimeangalia muundo wa Dubai (Dubai Land for Equity). Alichotakiwa kuwa nacho Mdubai ni ardhi tu iliyopimwa. Wawekezaji walikwenda kutoka Ulaya, Marekani na kwingineko. Iwe hivyo kwenye ardhi yetu kwa faida ya nchi yetu na watu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawasilisha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi uliyonipatia, lakini nianze kuunga hoja taarifa hizi tatu ambazo zimeletwa na Kamati zetu hapa Bungeni. Sisi tunaamini kwamba, Kamati ya PAC, PIC na LAAC, CAG ndiye jicho letu, maana yake ndiye jicho la Bunge. Kwa hiyo, tunapokuwa humu ndani sasa hivi leo, tunafanya kazi sisi wenyewe kama CAG. Kwa hiyo, tunapoona kuna watu wanateteatetea haya mambo tunajiuliza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana mchangiaji wa mwisho hapa, Profesa Kitila, amesema CAG ameshaleta mapendekezo mengi, lakini hayafanyiwi kazi. Hayafanyiwi kazi kwa sababu, sisi wenyewe humu tena tunawateteatetea hawa ambao wamesemwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Bunge ni kutunga sheria. Tunapotunga sheria miongoni mwetu humu kuna Mawaziri wanakwenda kutunga kanuni ili kuiwezesha sheria kufanya kazi. Wanapokwenda kufanya kazi tumepitisha bajeti hapa ya miradi, wao ndio wanaoandaa Bill of Quantity, makadirio ya mradi. Wao ndio wanaoandaa taasisi hiyo, inaandaa mikataba; ikiandaa mikataba inaweka vigezo mbalimbali. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Taasisi ya TANROADS…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kiswaga kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Maganga.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumpa Taarifa mchangiaji. Kwa kweli, wanaojaribu kuteteatetea kuhusiana na hii ripoti, nataka nimwongezee tu mchangiaji, yeye atiririke tu asiwe na wasiwasi tutafikia hitimisho na nawaandika hapa wale wanaotetea, tutakuja kumalizana mwishoni. (Kicheko/Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kiswaga unapokea Taarifa?

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea Taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na miradi ya bilioni 664 ya ujenzi wa barabara. Bilioni 600 hizi wakandarasi walicheleweshewa kulipwa na kufanya Serikali kuingia hasara ya jumla ya bilioni 68.7. Huu ni udhaifu wa usimamizi wa mikataba. Kama ambavyo nilisema sisi ndio tunaandaa makadirio, sisi ndio tunaandaa mikataba, halafu tunashindwa kusimamia mikataba, kulipa kwa wakati mkandarasi akiwa amemaliza kazi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili halikubaliki kwenye dunia hii. Hatuwezi kukubaliana na jambo hili. Nchi hii ni tajiri, lakini inataka kufilisiwa na watu ambao kimsingi wanaangalia maslahi yao. Inaingiaje akilini kwamba, tuliweka sheria ya siku 28, tukaweka sheria ya siku 56 ili mkandarasi awe ameshamaliza kulipwa, jumla ni siku themanini na ngapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuangalie, tuwafuate mmoja mmoja ambaye amesababisha hasara hizi, kwamba, mkandarasi alipo-raise certificate ilikaa kwake siku ngapi ili tumwone nani ameingiza hasara hizi. Haya yamekuwa ni mazoea, huu ni mradi mmoja tu wa taasisi moja ya TANROADS; miradi mingi ya Serikali yote ina riba, kwa nini tuwe na riba? Kwa nini tuwe na riba wakati kuna wataalam waliobobea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewapa ofisi nzuri, tumewapa magari, tumewapa kila linalowezekana ili wafanye kazi hizi, haiwezekani hata siku moja. Kwa hiyo, Bunge tuangalie ni nani aliyesababisha hasara hizi, awe ni mtoto wa shangazi, awe ni mjomba, awe ni mke wangu, wote wachukuliwe hatua. Haiwezekani nchi hii watu wakatengeneza kichaka cha kupigia kwenye miradi na sisi tupo, haiwezekani. Tumekuja hapa Bungeni kufanya kazi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tulikuwa tunajadili kuleta Muswada hapa wa bima na Wabunge tunalalamika kwamba, wananchi hawana uwezo wa kuchangia, kumbe fedha ambazo zingeweza kulipa zimekwenda kulipa riba na sisi tupo, haiwezekani! (Makofi)

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, Taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nampa taarifa mzungumzaji kwamba, hata hizi riba ambazo zimelipwa bilioni 68 hazikulipwa kwa wakandarasi wazawa, zimelipwa kwa kampuni za nje. Hakuna mkandarasi mzawa anayedai fidia kwenye Serikali, maana yake riba na mimi nikiwemo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kiswaga unapokea Taarifa?

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea Taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo maana yake nini? Ni kwamba, hawa wataalam wetu walioko ofisini wanakaa wanazungumza na hizi kampuni, tukucheleweshee certificate, tukulipe riba, halafu na mimi uje unipe cha kwangu, ndivyo inavyoonekana. Halafu Serikali imeshindwa kuweka utaratibu wa kisheria wa kuteua bodi, Executive Board, inateua bodi ya ushauri ilimradi iwe na mkono wake na yenyewe au kuna namna gani humo ndani, Serikali watueleze haya maneno haya? Kwa hiyo, Bunge tuchukue hatua kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili nakwenda kwenye Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Imezungumzwa hapa, bahati nzuri Mheshimiwa Songe jana alizungumza kwamba, kuna watu wanapewa mikopo ambao hawana sifa, ni zaidi ya bilioni mbili, ngoja niangalie hapa. Ni zaidi ya bilioni 2.5 hivi, bilioni 2.255, hawana sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wataalam wamebobea wako kule ofisini wanatoa kwa watu ambao hawana vigezo, watoto wa walalahoi wanakosa hela hizi. Nilimsikia Mheshimiwa Spika, jana anasema hawa wataitwa, hivi bado wapo? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata Mheshimiwa Waziri mwenyewe wa Elimu alipouona huu uozo akateua Kamati, Kamati ikaenda kukwamishwa maana yake nini? Unajua Sheria haina mbadala na sisi ndiyo watunga Sheria, akikwamishwa Waziri Kamati yake maana yake Serikali imekwamishwa kufanya kazi, hao bado wapo? Waziri, tena Profesa mbona tunataka kuchelewa nchi hii, hao hawana mjadala, hao anzeni kuchukua hatua mara moja. Haiwezekani Serikali inakwamishwa na taasisi ambayo imeiweka yenyewe, halafu Bunge tuko hapa, CAG leo sasa anafanya kazi yake lazima tuamue, haiwezekani! Tuliomba Ubunge ili tuwasaidie wananchi, Hapana! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine mmetupa Kamati ngumu kweli! Kamati ya PAC ya kuangalia wezi, usiku na mchana wezi! tena Kamati hii inamaliza vikao kila siku usiku Saa Mbili, hizi Kamati ni nzito kweli halafu tuache hawa,tumeumia migongo hawa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Azimio letu tuchukue hatua iwezekanavyo hawa hawapaswi hata kukawia kama ni Jumamosi wangeitwa, sijui waitwe lini, sijui kesho asubuhi ili kwanza Kamati iwanyonge, halafu sasa azimio letu nalo Jumamosi tukamalizie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, PAC ilipendekeza Bodi za Wakurugenzi kwamba zikimaliza muda wake ziendelee, hili nalo siyo sawa kwa sababu inafahamika bodi hii inamaliza muda wake lini, kama inafahamika wale wanaopendekeza majina kwenda kwa mamlaka ya uteuzi wanaweza wakawa wanachelewesha, kwa sababu yupo mtoto wa Shangazi, Mjomba, yupo mate wangu, wanachelewesha hata kama bodi hii haitoi matokeo chanya, Hapana! Wale wanaopendekeza majina kama tutabaini wanachelewesha kupeleka kwa mamlaka ya uteuzi tuchukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu, Bodi hizi…… samahani niongeze muda kidogo. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya dakika moja hitimisha hoja yako.

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Bodi siyo mahala pakwenda kupumzikia. Kuna utaratibu wa kuchagua watu ambao wanaelekea kustaafu sikatai, lakini kuna wengine ukiwaona wakitoka PAC wengine PIC pale, unaona wamechoka, unaweza kutafakari sijui wanaomba msaada huyo au namna gani! Lakini nataka niwaeleze Bodi hizi ni za kwenda kuweka akili ili Shirika au Taasisi iendelee. Haiwezekani tunao vijana wazuri wa miaka 30 au 45 wanashindwa kuteuliwa kwenye Bodi tunateua watu ambao kimsingi wanapaswa kupumzika, tusifanye hisani kwenye Mashirika yetu na Taasisi zetu tupelekeni akili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru kwa kupata nafasi hii kwa ajili ya kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Mwaka Mmoja na Miaka mitano. Kwa kuwa mimi ni mfuasi sana wa Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli, kwa uzalendo wake napenda niendelee kumpongeza kwa kazi nzuri anayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe Watanzania na wenzangu waliomo humu kwamba baba yetu huyu amefanya kazi kubwa. Wakati anaingia mwaka 2015 nilimsikia akisema ninyi TANESCO acheni mchezo, nafahamu huu mgao wa umeme mnafanya biashara. Mnafungulia maji ili watu waweze kuuza majenereta halafu wauze mafuta. Alivyokemea, kweli sisi tuliokuwa tunaishi Mbeya na Dar es Salaam, taabu ya umeme tuliyokuwa tunapata na kelele za majenereta ziliisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuendelee kumtia moyo. Hao wanaombeza, waendelee kubeza, lakini kwa sababu hata Mungu aliyetuumba wengine tunamkataa, tunampenda shetani. Kwa hiyo, ni jambo la kawaida. Kwa hiyo, namtia moyo aendelee hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mpenzi wa kilimo, siku ile kwenye hoja nilizungumza kidogo sikumaliza. Wakati tukiwa kwenye mpango kazi wa Wizara, mimi pia kama Mjumbe wa Kamati tulizungumza baadhi ya mambo. Moja ambalo linanigusa sana ni kuona Serikali sasa inakwenda kuwekeza kwenye suala la maabara za utafiti wa udongo. Ni muhimu sana. Wajerumani walifanya portioning ya nchi hii, wakasema hapa tutalima pareto, hapa tutalima kahawa, kwa sababu walipima udongo katika nchi hii na wakaweza kutoa mawazo yao kwamba tukilima hiki hapa tutafanikiwa. Najua ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba tunainua kilimo, lakini naona kwamba tuwekeze kwenye maabara za utafiti wa udongo, ni muhimu sana kwa sababu tutatoa mwongozo na tutaweza kuelekeza watu walime namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia upande wa mifugo, tumekuwa tuna shida ya chanjo. Chanjo nyingi ambazo tunazileta nchini zinatengenezwa kutoka katika nchi mbalimbali na hizi chanjo wanasema kwamba zinatibu magonjwa mengi na magonjwa mengine ambayo zinatibu hapa Tanzania hayapo. Sasa ningependa kuona Serikali inashirikiana na hiki Kiwanda cha Health Bioscience kuona kwamba kinakamilika kwa haraka, kama kuna vikwazo vyovyote vya kikodi au vya kivibali, basi viondolewe ili kiwanda hiki kianze kutengeneza chanjo hapa hapa nchini kwa sababu tutatengeneza chanjo zinazolingana na mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo, tutaweza sasa kuzalisha mazao ya wanyama ambayo tunaweza kuyauza hata Nchi za Ulaya pamoja na Nchi za SADC, kwa sasa tunashindwa kwa sababu ya ubora wa mazao yetu. Kama hizi chanjo tutazizalisha hapa, tutadhibiti magonjwa na tutaweza kuongeza tija kwenye mifugo. Najua muda utafika, baba yetu akishamaliza hii miradi ya umeme tutakwenda kumwomba fedha za kimkakati ili tuwekeze kwenye utafiti wa chanjo, kwenye maabara, kwenye mifugo pamoja na mazao, najua haya mambo yatakwenda vizuri, kwa sababu haya mambo ni ya kupanga tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tumesema kwamba utalii, ecology kule Arusha inaharibika. Sasa naona sasa ni wakati muafaka tuweze kufungua milango ya utalii wa Nyanda za Juu Kusini. Baba yetu Magufuli pale Iringa ametuletea pesa, tutajenga Kituo cha Utalii (Tourism Hub). Sasa ili haya mambo yaende vizuri tungehakikisha kwamba hizi barabara, kwa mfano ya Ruaha, ya kutoka Udzungwa kuja Iringa Mjini pale, tutengeneze ring fence tunavyotoka Mikumi tunaingia Udzungwa, tunaingia Kalenga kwenye Jimbo langu tunakwenda Ruaha Mbuyuni. Kwa hiyo haya mambo yatakwenda vizuri tukifanya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la umeme, kaka yangu Mheshimiwa Muhongo alisema kwamba tuwe na vyanzo vingi vya umeme. Sasa kaka yangu pale Mheshimiwa Kalemani tuliongea juu ya hawa RP Global ambao wanataka kuleta umeme kwenye jimbo langu umeme wa solar. Namshukuru amelipokea, nimwombe watakavyokwenda kumwona…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii adhimu kuchangia katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya tabia nchi yanakwenda haraka sana. Nchi lazima iwe tayari kuchukua hatua za kukabiliana nazo. Ziko fedha nyingi duniani zinazotolewa kwenye nchi zinazozalisha hewa ya ukaa inayotokana na kutunza misitu. Nchi hii bado ina misitu mingi. Hivyo nashauri hamasa ya kutunza hii misitu na vijiji vinavyozungukwa na misitu hiyo zipewe fedha ili iwe hamasa kwao.

Mheshimiwa Spika, misitu mikubwa kama ya Kitonga na Nyang’oro mkoani Iringa ukipita wakati wa kiangazi utakuta moshi. Hii inamaanisha watu wanachoma mkaa. Hili likiendelea litaharibu zaidi mazingira na kusababisha ukame kuendelea. Serikali ione namna ya kuongeza ulinzi hata ikibidi kujenga kambi za ulinzi.

Mheshimiwa Spika, ujenzi kwenye miinuko na vilima vyote kwenye miji kama Morogoro, Iringa, Mwanza, Mbeya na kadhalika uzuiwe. Misitu hii inasaidia miji kupumua kwa maana tunapata oxygen nyingi. Binadamu na misitu tunategemeana. Wizara ione namna ya kufanya ili kuzuia kabisa kupima viwanja kwenye maeneo hayo. Nawasilisha.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nipate kuchangia kwenye hoja hii muhimu. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja iliyoko mbele yetu. Sina mashaka na nia ya Serikali ya kuweza kuboresha hali yetu ya uchumi hasa ukizingatia bajeti imeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka sasa tuna shilingi bilioni 44.4 nyongeza ya 7% kutoka bajeti ya mwaka jana lakini ninashukuru kwamba kiasi kikubwa cha Bajeti hii karibu 71% inatoka kwenye mapato yetu ya ndani lakini kabla sijaendelea nitoe shukrani zangu kwa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu mpendwa kabia anayefanya kazi ya kutukuka katika nchi hii kwa kutoa fedha nyingi katika miradi mbalimbali inayoendelea hata hivi juzi katika Jimbo langu la Kalenga tuliweza kusaini mkataba wa kujenga barabara mpya inayokwenda vijijini kutoka Wenda kwenda Mgama kwa shilingi bilioni 29.8 ni fedha nyingi kujengwa barabara kwenda vijijini lakini nashukuru zaidi alituongezea fedha kwa ajili ya kujenga kipande cha lami kinachokwenda kwenye Makumbusho ya Mkwawa. Kwetu sisi jambo hili ni la heshima kubwa kwa hiyo, nipende kumshukuru kwa niaba ya Wananchi wa Kalenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitoe pole kwa Wananchi wa Jimbo la Kalenga hasa Kata ya Maboga na Kata ya Mseke ambako wamevamiwa na simba na mpaka sasa simba zimeshakula ng’ombe zaidi ya 10. Niwape pole wote waliovamiwa lakini Serikali inafanya kazi. Tumesha shauriana na vyombo vinavyohusika na wako site wanajaribu kulikomesha kabisa tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia hasa kwenye eneo la utalii. Eneo la utalii ni eneo muhimu sana kwenye uchumi wetu wa Taifa linachangia 25% ya pato la kigeni (fedha za nje) lakini 17.5% kwenye Pato la Taifa na Nyanda za Juu Kusini kama tunavyojua, Nyanda za Juu Kusini bado ni kama bikra katika eneo hili la utalii kwa sababu maeneo mengi hayajapata kufunguliwa na tunaamini Mpango wa Serikali wa kuanzisha ile miradi ya regrow Nyanda za Juu Kusini itakwenda kusaidia utalii kuweza kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, rai yangu ni kwamba niiombe Serikali sasa iweze kuharakisha mipango yake ya kujenga hii miradi ya regrow pale Iringa kile kituo cha utalii kiweze kujengwa kama Serikali ilivyoahidi pia na maeneo mengine ambayo yatakwenda kurahisisha watalii kuweza kwenda Nyanda za Juu Kusini ikiwa ni pamoja na kumalizika kwa ule uwanja wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunapokwenda kumalizia Uwanja wa Ndege wa pale Iringa ambao unaitwa Nduli ambao hauna sifa sana kwenye Taifa hili la Tanzania; maana Nduli Iddi Amini kwetu huku tukimzungumza kwa kweli ni kichefuchefu. Ningependa, kwa ushauri wa wananchi wa Mkoa wa Iringa kwamba ule Uwanja wa Ndege wa Iringa unaoitwa Nduli sasa uitwe Mkwawa, kwa sababu Mkwawa ni jina la kitaifa katika nchi hii kwa mambo mengi ambayo yalifanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzungumzie pia kwenye utalii. Nilikuwa nashauri kwa sababu Mbuga ya Ruaha imekuwa ikikauka mara nyingi kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi na shughuli za kibinadamu zinazoendelea katika maeneo mbalimbali, kwa hiyo ile mbuga imekuwa ikikosa maji. Sasa kuna mpango wa kujenga lile Bwawa la Lyandembela au Lugodaluchali, ambalo bwawa lile ni kubwa kama likijengwa inaonekana litakuwa na kina kirefu sana hata kuliko haya mabwawa mengine tunayojenga, kama Bwawa la Kidunda, ambalo ujazo wake unakisiwa kuwa utakuwa na mita za ujazo milioni 350. Kwa hiyo hili bwawa tukilijenga litaweza kutiririsha maji angalau mita sita kwa mwaka ambayo yataweza kutiririka kwenda katika maeneo ya Madibila kwenye yale mashamba ya mpunga. Maji mengine pia yatakwenda Mtera, Bwawa la Kihanzi na hatimaye Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Serikali itaamua kujenga bwawa hili itakuwa ni rahisi kwanza kudhibiti ule mtiririko wa maji. Kwa hiyo ushauri wangu ni kwamba, kwa kuwa Wizara ya Maji imefikiria kulijenga bwawa hili ningeweza kushauri pia hata wenzetu wa utalii katika hii miradi ya REGROW wafikirie namna gani wanaweza kushirikiana kwa sababu bwawa lile ni likubwa na linagharimu fedha nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kwa kuwa sasa nchi yetu inakuwa katika eneo la utalii, changamoto tuliyonayo nchi hii ni katika kutoa huduma hasa kwenye maeneo ya hoteli. Huduma zinazotolewa na hasa wafanyakazi wetu hawana ujuzi wa kutosha. Ningeomba Serikali ione namna gani tunaboresha huduma (hospitality) ambazo kwenye hoteli si nzuri. Sasa ukuaji wa uchumi katika maeneo haya ya utalii uendane sambamba na zile huduma ambazo tunazitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumza kwenye eneo la kilimo. Tunaishukuru Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa ruzuku ya mbolea, wananchi wengi wamepata. Lakini ushauri wangu kwenye hilo, ili tuendelee kuongeza uzalishaji ambao utakula fedha nyingi kaka yangu Mwigulu ningeshauri yafuatayo. Kwenye upande wa mbolea tuhakikishe kwamba vituo vya kusambazia mbolea tunavisogeza viwe karibu na maeneo ya wakulima lakini mbolea pia iweze kupatikana kwa wakati. Kwa kufanya hivyo tutaweza kuzalisha zaidi na tutaweza kukupa fedha nyingi ili wewe uweze kutekeleza miradi mingi ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeshauri, ukiangalia kwenye Kata ya Nzihi katika Jimbo la Kalenga ndiyo kata kame kwenye Jimbo langu la Kalenga. kwa hiyo kulikuwa kuna mpango wa kujenga bwawa miaka mingi iliyopita. Tangu mwaka 2008 utafiti ulishafanyika, walishafanya angalau upembuzi kwa kiasi fulani. Kwa hiyo ningeiomba Serikali iendelee sasa na mpango wake wa kulijenga lile bwawa na kukarabati skimu mbalimbali zilizoko kwenye Jimbo la Kalenga. Tuna skimu takriban 19 ambapo tutakuhakikishia kwamba tutaongeza kilimo lakini utaweza kupata pesa nyingi kutokana na hili eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye wakulima; mwaka jana tunashukuru tulifanya usajili wa wakulima wengi, lakini wapo wakulima ambao kwa bahati mbaya hawakuweza kusajiliwa. Ningeomba Serikali iweze kuchukua hatua sasa waanze kusajili wakulima sasa ili wakulima wengi waingie katika hii fursa ya kupata mbolea za ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulishauri ni kwa upande wa ulipaji kodi. Wapo Watanzania wenzetu wengi ambao wamekuwa wakikwepa sana kodi na wakati mwingine kuisingizia TRA, kwamba TRA wamekuwa brutal, lakini wao wengi wanaongoza katika kukwepa kulipa kodi. Sasa kama ukikwepa kulipa kodi tutatekelezaje miradi hii mikubwa namna hiyo? Kwa hiyo mimi ningeomba Watanzania wenzangu wafanyabiashara, suala la kulipa kodi ni suala la lazima na suala la kutoa risiti za eletroniki ni suala la lazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ione namna gani inaweza kufanya mifumo mbalimbali ya ukusanyaji wa fedha iweze kusomana ili kuziba mianya ambayo inapelekea leakages, fedha kuvuja katika maeneo mbalimbali. Hili nalo liweze kuangaliwa, Serikali iharakishe sana mifumo yake ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali isomane na iwe rahisi. Hili ni jambo ambalo ni muhimu sana tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri, kwa kuwa umefanya marekebisho ya kupunguza na kuongeza kodi katika maeneo mbalimbali, ningeshauri katika eneo la majengo na eneo la ardhi hasa eneo la viwanja; huku kuna fedha nyingi sana ambayo imelala. Watu wengi hawalipi kwa sababu kama mnavyojua hali ya uchumi imeathirika sana duniani hata mfukoni namo mmepata changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningependa kushauri kwamba, zile faini ambazo zinatolewa kwenye kodi za majengo na kwenye kodi za viwanja ziondolewe angalau kwa kipindi cha miaka miwili, na tuendelee kuhamasisha watu waweze kulipa hizi kodi. Hata kwenye majengo ya Serikali hata taasisi nyingine zinadaiwa fedha nyingi sana na hizi faini zimelimbikizwa, zipo nyingi. Tafuteni namna ya kulifanya hili. Mkifanya hivyo ninaamini mtakwenda kupokea makusanyo mengi sana na yataweza kusaidia kuingia kwenye mfumo na hizi fedha tuweze kuzitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kama Mwenyekiti wa Mazingira ningependa kushauri, hakuna uchumi bila kutunza mazingira. Suala la mazingira katika nchi hii ni baya zaidi. Tafiti zanasema kwamba ifikapo mwaka 2030 asilimia 66 ya ardhi inayolimika, itakuwa hailimiki kwa sababu ya uharibifu wa mazingira. Ukiangalia kile kilichotokea Malawi, mmomonyoko wa ardhi na mafuriko ambao umeleta hasara ya karibu trilioni moja na milioni mia mbili, watu takriban elfu moja wamekufa ni kwa sababu mazingira yameharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nitoe rai katika eneo hili kama tunataka kuendelea kuwa na uchumi suala la uharibifu wa mazingira lichukuliwe kipaumbele na Serikali itumie nguvu zake za kisheria kuzuia ukataji wa miti na kuhimiza upandaji wa miti. Ukipita kwenye ndege hapa utakuta kwenye vilima vingi ni mawe tu ndiyo yanayoonekana. Hii inaonesha ni kiasi gani mazingira yameharibiwa. Kwa hiyo kwa hili niwaombe sana hatuna uchumi bila mazingira kwa hiyo Serikali iweke sheria kali. Hakuna kukata mti katika mlima wowote katika nchi hii. Kama kuna watu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: …itapaswa ijengwe kwa mikataba maalum, nakushukuru sana napenda kuunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii muhimu ya bajeti kuu ya Serikali. Kwanza nianze kumshukuru Rais kwa kazi nzuri anayoifanya hasa kwa kutengeneza ile filamu ya Royal Tour ambayo tumeshuhudia na tumepata taarifa kwamba tayari wageni wengi wanaanza kumiminika hasa Kanda hii ya Kaskazini kwa sababu ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimnukuu Isaac Newton alisema, “an object will remain at its original state or rest until a relevant force is applied.” Kwamba kitu kitakaa katika hali yake ya kawaida au katika eneo lake la asili mpaka nguvu fulani itumike kukisukuma na ndiyo hicho ambacho Rais amefanya, amesukuma utalii wetu na sasa tunaona matokeo. Ni kweli kulikuwa kuna sababu ya kuutangaza utalii kwa sababu katika sehemu nyingi za dunia wenzetu wamekuwa wakitumia fursa hasa ya kutangaza Mlima Kilimanjaro na maeneo mengine kupita njia za nchi za jirani ili kuingia kwenye nchi yetu. Kwa hiyo, hiki ni kitu kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wamekuwa wakilalamika kwamba sasa kwa nini utangazwe utalii kwa wakati huu na tuko kwenye mfumuko wa bei na mambo mengi? Nimnukuu tena mwanaharakati mwingine ambaye anaitwa John Mason wa Insight International, yeye alisema hivi, “in trying times we should not stop try.” Katika nyakati ngumu na nyakati za majaribu tusiache kuthubutu wala tusiache kujaribu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namshukuru Rais kwa hilo, amethubutu na kwa vile maisha hayaishi leo, ni lazima tuendelee kufanya mambo ambayo yatakayosaidia Taifa liende mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukiangalia hapo hapo kwenye utalii, kule Iringa tunayo ile Mbuga ya Ruaha National Pack, ukiangalia kitakwimu ni kwamba ile mbuga ni ya pili hapa Tanzania ikiwa na eneo kubwa la kilomita za mraba 20,226 ambayo ni ya pili kwa Tanzania. Ilikuwa ya kwanza, lakini sasa Mwalimu Nyerere imeizidi, mwaka 2008 tulivyoongeza lile Bonde la Usangu ilikuwa ya kwanza, lakini sasa ni ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia duniani ni mbuga ya sita, lakini pia wanasema kwamba ni ya 10 duniani kwa kuwa na simba wengi. Hata hivyo mbuga hii ya wanyama inatembelewa na jamii ya ndege wapatao 574; kabila za ndege mbalimbali duniani ambao wanatoka Ulaya, Australia, Madagaska na nchi nyingine za Afrika, wanakwenda Mbuga ya Ruaha kwa nyakati tofauti. Kwa hiyo, kuna kuhama kwa hawa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ukiangalia katika nchi hii ndiyo mbuga ambayo haitembelewi kabisa. Sababu ni nini? Sababu ni miundombinu, lakini tunamshukuru Rais, sasa amesaini mkataba ambao utakwenda kujenga barabara ya kwenda Ruaha National Pack na hivyo huu utalii utakwenda kukua hata Nyanda za Juu Kusini. Na kama ambavyo tumekuwa tukizungumza mara zote, ni muhimu sana sasa watalii wakatawanywa katika nchi yote ili sasa kupunguza uharibifu unaoendelea kule Kanda ya Kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuhusiana na Royal Tour kwamba amefanya sehemu ya kwanza, ni sehemu ndogo, kwa sababu ya mafanikio ambayo tayari tumeanza kuyaona, nashauri kwamba hii Royal Tour iwe kwenye series, yaani kuwe kuna toleo lingine tena. Hili toleo litakalofuata liingize mbuga za Ruaha ambazo kipekee utakuta kuna mnyama pale anaitwa tandala ambaye hayupo sehemu nyingine; utaingiza Mbuga za Kitulo na maeneo mengine kama Kalambo Falls na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya namna hiyo, tutakuwa tumeutangaza utalii vizuri na utalii wetu utaendelea kukua. Pia kwenye utalii ni muhimu sana sasa kama nchi tusiangalie utalii wa wanyama peke yake, tuangalie utalii wa namna tofauti. Unaweza ukawa utalii wa mavazi. Kwa mfano, kule Iringa tuna mambo yale ya migolole, ni utalii. Kwa hiyo, tuangalie utalii kwa mapana yake, tusiangalie tu utalii wa wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wenzetu walioko kwenye utalii naomba waweze kuangalia kwa mapana yake. Kule kwetu kuna mapango ambayo Mkwawa alikuwa anajificha; nayo yanaweza yakaingizwa kwenye utalii. Viko vitu vingi. Kwa hiyo, tuwaanchie wao, naona watafikiria namna ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ule mradi wa Regrow ambao ulikuwa na mpango wa kuifanya nchi Nyanda za Juu Kusini iwe hadhi ya utalii. Tuna kituo kinatakiwa kijengwe pale Iringa, tunaamini Serikali itakwenda kwa haraka kufanya hivyo, tukiunganisha pamoja na uwanja wa ndege ambao inaonekana kwamba sasa hivi wamegundua kuna mwamba pale chini ambapo inaonesha kwamba tutachelewa kumaliza ule uwanja kwa miezi 36 zaidi. Naiomba Serikali ione namna gani ya kuweza kuharakisha hilo ili tufanye utalii wetu kuwafungamanishi tukiwa na ndege, barabara na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikizungumzia ile Bodi ya Stakabadhi Ghalani. Nimezungumzia kwenye biashara, na pia nilizungumzia kwenye kilimo. Sasa hapa nataka kushauri nini? Wakati tunaanzisha hii Bodi ya Stakabadhi Ghalani mwaka 2005, kulikuwa kuna kipengele katika sheria ambacho kilikuwa kinaipa hii mamlaka kujasili maghala yote yaliyoko nchini. Isipokuwa tulipofanya marekebisho mwaka 2016, hiki kipengele kikaondolewa. Maana yake sasa tumemwondolea mamlaka huyu Mkurugenzi wa Bodi za Maghala, hana meno tena ya kuweza kusajili maghala yote yaliyoko nchini pamoja na yale ya binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini ni muhimu kusajiliwa? Ni lazima kwa sababu tukisajili haya maghala yatatusaidia kujua mazao ambayo tunakuwa nayo tangu kutoka kule chini vijijini. Kwa hiyo, naiomba Serikali na Waziri husika kwa wakati unaofaa wailete hii sheria tuifanyie marekebisho ili tumpe meno huyu Mkurugenzi wa Bodi za Stakabadhi Ghalani aanze kusajili maghala yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia jambo lingine, tunazungumzia suala la bajeti, lakini pia kuna changamoto kubwa ambayo imeanza kujitokeza sasa hivi, watu kutotoa hizi risiti za EFD. Mtu mmoja mwenye hekima alisema, “men were created to be controlled and guided.” Kwa maana gani? Kwamba wanadamu waliumbwa ili wasimamiwe na waongozwe. Tukiwaacha hawa wanadamu, wanafanya mambo wanayotaka. Kwa hiyo, sasa hivi hawatoi risiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna bidhaa nyingi ambazo zinaingia kutoka nje kupitia hii mipaka, ni kama panya road fulani hivi, maeneo ya Bagamoyo, Tunduru na maeneo ya mipaka mbalimbali ya nchi. Kwa hiyo, bidhaa nyingi zinaingia kwa njia ya panya road. Sasa kama tukiacha hii iendelee, tutafifisha nguvu ya Serikali kuweza kukusanya mapato na kuhudumia wananchi wake na kufanya miradi mingi ambayo Serikali inatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, tumeongeza ajira nyingi, tumeongeza mishahara, lakini sasa kama hatuwezi kukusanya kodi, itakuwa ni kazi kubwa sana Serikali kuweza kutima malengo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nigusie hili suala linaloendelea kuhusu Ngorongoro. Najua rafiki yangu Mheshimiwa Shangai tumekuwa tukizungumza mambo mengi, lakini nizungumzie suala hili, kwamba ni kweli mchango mkubwa wa utalii kwenye nchi hii unatokana pia na Kanda ya Kaskazini hasa eneo la Ngorongoro. Katika sheria za nchi hii ni kwamba hakuna Mtanzania, mimi au yeyote mwenye haki ya kusema kwamba hii ni ardhi yangu nitakaa milele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anayemiliki ardhi katika nchi hii ni Rais na Serikali inaweza wakati wowote inavyoona inafaa ikaichukua ile ardhi kwa matumizi ambayo yana faida pana kwenye Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama walivyosema wenzangu, mwaka 1974 nchi hii iliamua kuhamisha watu kutoka katika maeneo waliyokuwa wamekaa, wametawanyika, kuwaleta kwenye vijiji. Sababu zilikuwa nyingi, pamoja na kuwapa huduma kwa karibu na mambo mengine. Ila ili nasi tuweze kuendelea kuutunza utalii wetu, iko sababu ya kuendelea kuilinda Ngorongoro na nchi hii kama unavyosema kwamba hakuna kabila ambalo linaweza lika-claim kwamba hapa ni pakwangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda hata kule Iringa utakuwa Wamasai wengi sana wanaishi kule na wamegombea mpaka Ubunge. Ukiangalia pale Isimani wapo, huwa wanagombea gombea mpaka Ubunge. Kwa hiyo, tusilete chokochoko kuonekana kwamba kuna kabila fulani moja au Wahehe au Wapare wenye uhalali sana kwamba hii ardhi ni ya kwao; Sukuma land or Hehe land au Masai land. Nafikiri tusilete huu mchanganyiko, tunafanya hili jambo liwe gumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweka uzalendo mbele, tujue kwamba nchi hii ni ya kwetu, na kama kuna chokochoko yoyote ambayo inagusa maslahi ya nchi, ni lazima wote tuungane kwa ajili ya kusudi jema la kuhakikisha kwamba nchi yetu inaimarika kiuchumi na tunakuwa wamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia suala lingine kuhusu Bandari ya Bagamoyo. Bandari hii ni muhimu sana katika uchumi wa nchi. Ni kweli kumekuwa kuna malalamiko mengi kwamba namna mikataba hii ambavyo ilikuwa imesainiwa ambayo hata sisi hatuijui, ilikuwa ya ovyo. Hata hivyo, bado kuna sababu ya kuendeleza hii Bandari ya Bagamoyo kwa sababu ziko meli kubwa sana duniani ambazo haziwezi kutua katika nchi yetu ya Tanzania, sasa lile eneo la Bagamoyo lina upana mkubwa ambapo tunaweza tukalipanua na tukaleta meli kubwa na uchumi wetu ukaweza kwenda kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ione ni namna gani inaweza kuendeleza ile Bagamoyo, na mfumo wa uendeshaji wa hizi bandari nashauri uwe kwa mfumo wa kushirikiana kati ya private sector na Serikali ili kuweza kuharakisha maendeleo. Kwa sababu private sector inavyoingia kwenye kuendesha jambo, maamuzi yake yanakuwa ya haraka. Ila mara nyingi kwenye Serikali zote duniani maamuzi huwa yanakuwa ni ya polepole sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia huu mpango wa maendeleo kwa miaka mitano ijayo. Kwanza nashukuru wachangiaji wenzangu wengi wamezungumza katika maeneo mengi, lakini kipekee nataka kumshukuru pia Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Prof. Mkenda na Msaidizi wake kwa kazi nzuri wanaoifanya.

Mheshimiwa Spika, katika michango yangu iliyopita nilikuwa nimezungumzia mambo ya kilimo. Kwa upande wa ugani nilizungumzia habari ya mbegu, habari ya utafiti wa udongo na pia habari ya soko. Nilipopata nafasi ya kuzungumza naye wiki iliyopita tukiwa tunakunywa chai, alinieleza kwa shauku kubwa sana ni namna gani ambapo ameweka bajeti kwanza kuhakikisha kwamba tunapata mbegu bora. Hiyo inatokana na kuwekeza kwenye maeneo ya umwagiliaji, kwamba katika maeneo yanayozalisha mbegu wanasema sasa watazalisha mwaka mzima, kwa sababu tunakwenda kuweka umwangiliaji. Kwenye soko akawa ananieleza kwamba mwaka huu tutafanya maonyesho ya bidhaa zetu China na Oman na mambo mengi alizungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa udongo, alinieleza kwamba wanakwenda kununua vifaa kwa ajili ya Halmashauri 45 ili tuwe tunapima udongo. Kwa hiyo, kwa kweli kwa kazi hiyo nzuri nawapongeza, lakini baada ya hapo acha niendelee na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi hii nimemsikia hata Mheshimiwa Rais akizungumza siku ile kwamba tunaweza tukapata pesa nyingi kwenye madini. Alizungumzia suala la Serengeti, lakini nchi hii ina maeneo mengi sana yenye madini ambayo Watanzania hatujafanya utafiti. Wazo langu nilikuwa nafikiri kwamba Serikali ingeweka bajeti ili tutengeneze kama kitabu ambacho kinaonyesha maeneo yote Tanzania. Tufanye utafiti ili tuandike na mwekezaji anapokuja aambiwe ukienda Kalenga utapata madini haya. Kule Kalenga wazee wameniambia kama maeneo matatu muhimu, kwamba zamani tulikuwa tunachimba madini hapa; na kuna madini mengi.

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa naishauri Serikali, katika mipango yake tuweke alama (marks) kwamba eneo hili na hili unaweza ukapata madini haya, ili hata wawekezaji wanapokuja, ni rahisi sasa tukimpa kile kitabu, achague kwamba mimi nikawekeze Kalenga kwa sababu naweza kupata Shaba au Dhahabu. Kwa hiyo, hilo tulifikirie katika mipango ya baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna eneo la pili ambapo nimejihusisha kidogo katika utafutaji wa hizo wanazoita tunu na malikale. Nimewekeza fedha nyingi, lakini nimefanya katika kipindi cha miaka miwili nikakimbia. Hili eneo inaonekana ni muhimu sana na watu wapo wenye ushuhuda kwamba wamekuwa wakipata fedha na hizi tunu zipo. Sasa ushauri wangu, kuna mambo mawili kwamba ukienda Maliasili, wanataka ulipie ile leseni miezi mitatu mitatu. Sasa miezi mitatu mitatu hii, watafiti wengi wamekuwa wakifanya huko zaidi ya mwaka mmoja mpaka inaendelea hata miaka mitano au sita. Sasa inakuwa ni gharama kulipa laki tano tano kwa miezi mitatu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nafikiri kwa sababu eneo hili lina watu wengi na wengi sasa hivi wanafanya na hawalipi hata leseni, kwa sababu wako huko porini, wanaona hii miezi mitatu mitatu ni gharama. Nilikuwa naishauri Serikali, wenzetu hawa wa Maliasili angalau wangeweza ku-charge hata kwa miezi sita sita ili kuwapa nafasi hawa watu wanaofanya utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine, nimegundua kwenye huu utafiti wa tunu, kuna utamaduni wa Kijerumani katika mambo haya. Nikawa nawaza, kama hawa Wajerumani wanahusika, kwa nini Serikali isifikirie sasa kutafuta hawa wazee wa Kijerumani ambao wanaonekana wana ramani za haya mambo ya malikale, tukafanya partnership kama tunaweza kutoa hizi tunu, basi wao wabakie na asilimia 40, sisi tubakie na asilimia 60. Ili sasa hili jambo liwe wazi, kwa sababu watu wanajitafutia tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina Ushahidi, kuna mzee mmoja ambaye nilikuwa nafanya naye utafiti, hata sasa nimemwacha site, mimi nimemkimbia baada ya kuona gharama zinakuwa nyingi. Anasema yeye alifanya kazi na Wajerumani na hiyo scanner anayoitumia katika kuangalia maeneo ambayo madini yapo, ni ya Kijerumani na alipewa na Mjerumani. Kwa hiyo, maana yake haya mambo yapo, lakini hayajawa wazi sana. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiri katika eneo hilo nalo, tuone; kwanza, kupunguza hizo gharama za kulipia hivyo vibali na pili tuone kama tunaweza tukawatafuta hao Wajerumani ili tushirikiane nao.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nilikuwa najaribu kuliangalia kwamba kwenye mashirika yetu ya Serikali performance yake imekuwa kidogo, lakini nikaja nikawa nafanya utafiti kujua kuna tatizo gani? Kwa nini kuna performance ndogo? Nikaliangalia kama shirika la TTCL ambapo mimi nimefanya kazi kwenye mitandao kwa miaka 20. Yaani hatujalipa nafasi, kama unamteua Mkurugenzi, basi mpe mamlaka ya kufanya maamuzi na kuweza kufanya maamuzi fulani hata kufanya promotions. Kwa mfano, kwenye mitandao tulikuwa tunasema, we copy with pride, kwamba ukionga mwenzako…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana nami kupewa nafasi hii adhimu kabisa kwa ajili ya kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali. Kwanza nami nianze kumshukuru sana Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa upendo wake mkubwa na usikivu mkubwa ambao ameuonesha kwa sisi Wabunge na Watanzania wote kwa ujumla. Namshukuru kwa sababu ya yale ambayo tayari wenzangu wameshayazungumza kwa kupewa zile shilingi milioni 500 kwenye Majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Rais kupitia Waziri wake wa TAMISEMI, Mheshimiwa Ummy Mwalimu ambapo Wabunge tumeelekezwa kwamba tupeleke mapendekezo ya eneo gani tutapenda shule zetu zijengwe angalau shule moja ya Kata. Hii inanifanya niendelee kuamini misemo mingi ambayo imekuwa ikisemwa na majukwaa mengi ya Kimataifa, hata World Economic Forum wakati fulani walisema, nanukuu: “Having women in leadership roles is more important now that ever.”

Nikiendelea kunukuu makala moja iliyoandikwa na mama mmoja anaitwa Lynn Camp ambaye ni CEO wa EVERGREEN, hawa wanajihusisha na biashara za mitandao na digitali, anasema: “Women led Government is taking bigger steps forward on behalf of the state economy, they have shown the real desire to listen to experts in wider world of business.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiendelea kunukuu anasema: “the survival of planet requires new thinking and strategies we are in the pitched battle between the present array of resources and the attitude and the future struggling to be born. Women get it, young get it, they are creating a whole different mindset.” Sasa ukisoma hizi nukuu zote zinaonesha huko tunakoelekea sasa akina mama pamoja na vijana wanachukua nafasi. Inaonekana kwamba wameleta mchango mkubwa sana katika kufikiri na kuleta mikakati mipya ambayo itakwenda kukuza uchumi wetu kama nchi na biashara za dunia kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, hata Deloitte and Tosh walisema kwamba; companies led by women in leadership they have six times innovative than other companies and also, they meet financial targets two times. Kwa hiyo, wakimaanisha kwamba kampuni ambazo zinaongozwa na akina mama inaonekana zina ubunifu mara sita dhidi ya kampuni nyingine ambazo zinaongozwa na akina baba. Kwa hiyo, kwa kweli namshukuru sana Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kutokana na hilo nitumie nafasi yangu ya Kibunge kuishauri Serikali na kumshauri Mheshimiwa Mama Samia, kwa kuwa sasa imeonesha kwamba mwelekeo sasa katika uongozi wanawake na vijana sasa wanachukua hatamu, nilikuwa napendekeza kwamba hata katika miradi mikubwa ambayo tunafanya sasa, tuanze sasa kutaja wanawake ambao walileta mchango mkubwa kwenye Taifa hili…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiswaga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda nimpe Mheshimiwa Kiswaga taarifa. Nampongeza sana kwa jinsi anavyotambua kwamba wanawake na vijana watachukua hatamu. Kwa maana hiyo, mwaka 2025 ni dhahiri kwamba Mheshimiwa Mama Tendega atakuja kwa Jimbo la Kalenga. Ahsante. (Kicheko/Makofi)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hiyo ina utata kwa sababu Jimbo lile la Kalenga lilitawaliwa na Chifu Mkwawa. Kwa hiyo… (Makofi/ Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiswaga, sina hakika kama hii ilikuwa ni taarifa, lakini malizia mchango wako. (Kicheko)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kwa hiyo, nimesema kwamba tuwe na maeneo sasa ambayo yanatajwa kwa ajili ya akina mama. Kwa mfano, wako akina mama ambao walileta michango mikubwa katika Taifa hili kama akina Mheshimiwa Getrude Mongella na Mheshimiwa Anne Makinda. Tunaweza hata tukajenga hospitali fulani ya akina mama tukaiita Anne Makinda au Gertrude Mongella. Tunafanya hivyo ili ku-inspire vijana wengi wa kike. Hata mimi nina binti ambaye ninatamani aje awe mtu mkuu sana. Kwa hiyo, wakianza kuona waliotangulia wanaheshimiwa, basi na wengine watafuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli bajeti hii ina mambo mengi sana mazuri ambayo nimeyaona yametajwa humu. Moja ya jambo muhimu sana ambalo nimeliona ni lile la kuwa na sensa. Ni muhimu sana katika kukuza uchumi wetu, kuwa na data muhimu kwa wakati. Unajua katika mipango mingi ya maendeleo duniani inategemea sana takwimu. Unaweza ukasema kwamba tunahitaji shule 10 katika Jimbo la Kalenga; kwa sababu ya takwimu tulizonazo ambazo siyo za kweli, kumbe takwimu halisi zinataka tujenge shule 20. Kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa kutenga bajeti karibu shilingi bilioni 328 kwa ajili ya kufanya sensa mwakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumpongeza sana Waziri wa Fedha pamoja na msaidizi wake na pia pamoja na Mwenyekiti ambaye ni jirani yangu hapa kwa kuchambua bajeti vizuri na kuzingatia mawazo mengi ya Wabunge pamoja na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti hii kuna mambo mengine ambayo tunataka tuchangie kidogo labda kwa kuboresha. Kama nilivyosema mimi nimekuwa kwenye mitandao miaka mingi; kwenye hii kodi ambayo tumeianzisha kwenye mitandao hasa kwenye laini za simu, tumesema tuna- charge kati ya shilingi 10/= mpaka shilingi 200/= kwa siku. Ukweli ni kwamba ukiangalia kwenye watumiaji wa simu, asilimia 65 ya wateja wao, wengi wana-charge kwa mwezi shilingi 500/=. Asilimia 59 mpaka 65 wanaweka shilingi 500/= kwa mwezi. Sasa ukisema kwamba uta-charge kila siku shilingi 10/=, maana yake unasema shilingi 300/=. Kwa hiyo, maana yake kuna kundi kubwa ambalo linakwenda kuathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda pengine kuna shida kwenye uchapishaji, tuseme kwamba labda tuna-charge shilingi 10/= kwa kadri mtu anavyoweka fedha. Tukiangalia pia kwenye ile miamala, tumesema kwamba tuta-charge kati ya shilingi 10/= mpaka shilingi 10,000/=. Ukiangalia muamala wa juu kwa mfano shilingi 1,000,000/= tuna-charge shilingi 8,000/=. Hili limeleta malalamiko sana wakati hivi viwango vinapandishwa kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili nilikuwa nafikiri Serikali ione uwezekano. Kodi tunaitaka kwa sababu tunataka kufanya mambo mengi na mama ameshaonesha njia kwamba tunataka kufanya transformation kwenye uchumi. Ingekupendeza ungekaa na watu wenye mitandao wakupe uhalisia wa hili jambo, kwa sababu tukiongeza shilingi 10,000/= kwenye shilingi 1,000,000/= inakuwa shilingi 18,000,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa mfano Airtel, imechukua muda mrefu sana kufanya miamala ya bure ili angalau kuchochea watu wengi waweze kufanya hiyo miamala. Wamechukua muda mrefu sana. Sasa leo tukisema tunaongeza kwenye shilingi 10,000/= inaweza ika-slow down na hiyo kodi ambayo tunategemea kuipata tusiweze kuipata. Kwa hiyo, hili ninaomba pia tukaliangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye mambo ya kodi yanayohusiana na ardhi, kuna viwanja ambavyo vimepimwa vingi na Watanzania wengi hawalipi. Tunakushukuru umesema kwamba kwenye Property Tax tutaweka kwenye Luku. Watu wengi wamechangia hapa, najua utapata hekima ya namna gani utaweza ku-charge kama mtu ana kiwanja, ana nyumba nyingi ana Luku nyingi, hiyo hekima Mungu atawaongoza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo hili lingine la viwanja, watu wengi sana hawalipi kwenye land rent, na huko tuangalie tutafanya nini? Kwa sababu kuna kodi nyingi huku zimelala na zinaweza kusaidia sana uchumi wetu na tukafanya mambo mengi ya kimaendeleo. Kwa hiyo, hilo nalo tunaweza tukatengeneza task force ambayo itakwenda kusaidia kukusanya hizi kodi, vyovyote mtakavyoona inafaa naomba tuweze kutupia jicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna jambo lingine ambalo nilikuwa nalifikiria, huko tuendako uchumi mwingi utatoka kwenye kilimo. Sasa ningeomba kwamba, mkakati kwenye kilimo uwe namna hii kwamba, tumekuwa tuki- acquire ardhi kuwapa wawekezaji, sipendi hilo jambo la kuchukua ardhi kwa wananchi kuwapa wawekezaji; napenda hivi kwamba, tuwe na ardhi kwa ajili ya uwekezaji kama walivyofanya Dubai wanasema land for equity. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija pale Iringa kwangu, nina eka zangu 2,000 sijaziendeleza, Chalamila ana eka 2,000 hajaziendeleza, Mkoa naye 5,000 hajaziendeleza, tunazitambua zile eka kwa pamoja tunasema eneo hili lina eka 20,000 wanaomiliki hapa ni Mheshimiwa Kiswaga, ni Mkwawa, ni fulani. Muwekezaji aje awekeze pale na tumeshaiainisha ardhi, lakini sisi tuchukue asimilia 20 ya uwekezaji. Akae miaka 33, miaka mingapi, lakini sisi tuwe na hisa kutokana na ardhi tuliyonayo na yeye anakuja na pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana Dubai leo watu wamekuwa matajiri kwa sababu walikuwa na ardhi. Hili suala la kuichukua ardhi tuwape wawekezaji linaleta shida, unakuta kwamba, muwekezaji anakwenda kwenye kijiji anapewa eka labda 500 eti kwa sababu amejenga ofisi ya vyumba viwili. Baada ya hapo mnakwenda kumuomba pesa ya maendeleo 500/= tu, labda 100,000/=, anasema mpaka muandike barua, hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ile ardhi kijiji kingeamua kushirikiana naye kwamba, wewe njoo wekeza katika eka hizi 500 tunakupa, lakini katika mazao utakayopata utupatie sisi asilimia 20 kwa miaka yote, sisi tutakuwa na uchumi wetu kama kijiji na hatutakuwa na tatizo tena la kwenda kuombaomba. Tukiacha hili jambo ardhi yetu itapotea na Watanzania hawatakuwa na ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja zilizopo mezani. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja zote zilizopo mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijielekeze zaidi kwenye taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali hasa katika Bodi ya Mikopo. Mwalimu Nyerere alitueleza kwamba maadui wakubwa kabisa katika nchi hii ilikuwa kwanza, ni ujinga na wengine wakafuata. Akaweka mifumo ya kufuta huu ujinga kwa maana ya kumtokomeza kabisa huyu adui. Pia Mwenye hekima mmoja Jeff Rich alisema:

“If you think education is expensive, then try ignorance”

Mheshimiwa Spika, anamaanisha, kama unafikiri elimu ni gharama, basi jaribu ujinga. Kwa muktadha huo tunamshukuru sana Rais Wetu Mama Samia Suluhu Hassan ambaye amejipambanua vizuri kabisa kuhakikisha kwamba anaondoa ujinga katika nchi hii. Tumeona mwaka jana alianza kutoa fedha nyingi ili kujenga madarasa ili Watanzania wengi wapate fursa ya kwenda kusoma na kuweza kufuta ujinga. Hata hivyo mwaka huu tena tumeona bilioni 160 zimetolewa ili madarasa 8,000 yakejengwe ili Watanzania wakaweze kusoma. Tunamshukuru zaidi kwenye kuongezea fedha kwenye Bodi ya Mkopo mpaka kufikia bilioni 570. Kwa kweli anajitahidi na anafanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ripoti ya CAG inaonesha kwamba kwa kipindi cha miaka mitano ambacho amefanya ukaguzi ni 72% tu ya wanaostahili kupata mikopo ndio wamekuwa wakipata mikopo. Pia imeonesha kuna wanafunzi 492 ambao wao walishindwa kuendelea na masomo kwa sababu walishindwa kupata mikopo hali ya kuwa wao ni watoto wanaotoka kwenye familia maskini. Hivyo walishindwa kuendelea kusoma.

Mheshimiwa Spika, inaonesha vile vile kuna kiasi cha fedha Sh,1,768,000,000 ambapo katika mwaka 2017/2018 wanafunzi wapatao 5,650 walipokea mikopo ambayo hawakustahili. Tena aliendelea kutaja kwamba kumekuwa na changamoto kubwa kwamba mifumo haisomani. Wanafunzi wanapata shida wanapokwenda kuomba ili wapate mikopo. Kwa mifumo kutoka Baraza la Mitihani ukiangalia pia Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini pamoja na Mamlaka ya Usajili wa Vitambulisho vya Taifa, hii mifumo haisomani. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto kubwa kwa wanafunzi kupata shida katika kuomba waweze kupata nafasi ya kupewa mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, imeoneshwa pia kwamba Bodi kwa muda mrefu kwa kipindi hiki cha miaka mitano imekuwa ikitoa kiwango cha chini cha mikopo kwa kila anayekuwa akiomba. Pia kwa kiwango cha juu kwa kati ya Sh.3,100,000/= kwa wanafunzi kati ya 896, zote hizi ni chanagamoto ambazo CAG amezionesha. Hizi ni chanagamoto kubwa.

Mheshimiwa Spika, taarifa imeonesha katika kipindi cha mwaka 2018/2019, kuna wanafunzi wapatao 6,183 ambao walipangiwa mikopo kwa kiwango cha juu zaidi ya vile walivyostahili ambapo kiasi cha Sh.5,668,843,000/= kilitumika, lakini pia kuna wanafunzi 2,852 walipata kiwango cha chini cha uhitaji wa mkopo kiasi cha Sh.1,147,000,000/=. Kwa hiyo kunaonekana kwamba kuna fedha nyingi ambazo zimekuwa zikitolewa nje ya utaratibu. Kwa hiyo kwa miaka mitano inaonesha kwamba kuna jumla ya Shilingi bilioni 13.7 ambazo zimetolewa kwa watu ambao hawakustahili, ambapo kiasi hiki kingeweza kutosheleza wanafunzi ambao walipata mikopo ya chini kama 10,075 ambapo pia kingeweza kulipia wanafunzi wengine wapya ambao waliomba kama 3001. Kwa kweli changamoto ni nyingi.

Mheshimiwa Spika, nimeamua kuchukua kipande hiki kwa sababu nimekuwa nikipokea malalamiko mengi ya watoto ambao hawana uwezo, maskini kutoka katika Jimbo langu la Kalenga na majimbo mengine ambao wamekuwa hawapati mikopo kwa kukosa umakini kwa hawa wenzetu ambao tumewapa dhamana.

Mheshimiwa Spika, ukaguzi katika kipindi hicho cha miaka mitano, umeonesha kuna wanafunzi 756 ambao waliostahili kupata mikopo lakini hawakupata. Ni mambo mengi yamekuwa yakiendelea. Vile vile tunaoneshwa kuwa kuna ambao walistahili kupata mikopo kiasi cha 192,039 lakini ambapo walitakiwa wapate kiasi cha Sh.569,313,000,000/=, sasa hili sio tatizo la watu wa Bodi ya Mikopo kwa sababu ni uwezo wa Serikali kuwapa hiyo mikopo ulikuwa mdogo kwenye hilo eneo.

Mheshimiwa Spika, tumeona sheria na miongozo katika Bodi ya Mikopo ambayo inawataka wanafunzi ambao wako katika uhitaji wa juu wa mikopo, kwa mfano, wale ambao wanatokana na kaya maskini ambao wanatakiwa wapewe mikopo, kiasi cha wanafunzi 22 hawakupata mikopo hiyo. Hii ni kati ya kipindi cha miaka miwili 2019/2020 na 2020/2021 kiasi cha Sh.84,000,000 zilitakiwa zitolewe lakini hazikutolewa. Pia inaonesha kuna watoto 95 ambao wanatoka katika zile familia za yatima (baba na mama wamefariki) na mwongozo unaonesha kwamba ni lazima wapewe, lakini hawakupewa. Walipoulizwa wanasema kwamba, mfumo hautambui kwamba wale watoto wanaotoka familia maskini au yatima ndio wanaotakiwa kupewa kwanza. Hayo ndiyo majibu ambayo bodi iliyatoa. Hii nayo tunaiona ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo bodi wamekuwa wakiipata ni kwamba, wakishapeleka fedha kwenye taasisi zile za juu kwamba kuna wanafunzi
100 katika pengine Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walitakiwa kupewa mkopo, bodi inapeleka, ikishapeleka kule, wale wanafunzi wasipopewa ndani ya siku 30 mwongozo unasema zile fedha zinatakiwa zirudi kwenye Taasisi ya Bodi ya Mikopo ili waendelee kuwakopesha wengine. Sasa imetokea tatizo kwamba kumekuwa na ucheleweshaji. Kwamba hawarudishi kwa wakati ndani ya siku zile 30, kwa hiyo, kunainyima furs ana uwezo Bodi ya Mikopo kuendelea kukopesha wanafunzi.

Mheshimiwa Spika, sasa nakuja na mapendekezo kulingana na yale ambayo nimeyaona, niombe wenzangu wa Kamati, najua walikuja na mapendekezo yao, naomba wapokee na hii nyongeza ya mapendekezo ambayo nimeona kutokana na kile ambacho nimekisoma kutoka kwenye Taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, pendekezo la kwanza, niombe taasisi zote ambazo zinahusiana na usajili wa wanafunzi yaani mifumo yake iweze kusomana. Nikimaanisha Bodi ya Mikopo, Vitambulisho vya Taifa pamoja na Usajili, Ufilisi na Udhamini mifumo yake isomeke ili iwe rahisi kuondoa matatizo yanayotokana na forgery. Pia bodi ihakikishe wale wanaopewa mikopo ni wale wanaostahili kupewa mikopo kama wale watoto maskini kutoka katika kaya zile zinazohudumiwa na Serikali, watoto yatima, ihakikishe kwamba wanapewa. Wanachotakiwa kufanya ni kubuni tu mbinu za namna gani ya kuwasaidia, wanaweza wakawa pengine na dawati maalum la kuweza kuwasaidia hawa, kama mfumo hauwatambui, basi waweze kuandaa dawati maalum la kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, pia tufanye tafiti kuona nchi nyingine zinafanya nini kusaidia Bodi hizi za Mikopo na taasisi nyingine ambazo zinasaidia watoto kusoma, kuona vyanzo vyake vinatoka wapi ili tutafute vyanzo vingine, lakini tunaweza kujifunza kutoka nchi nyingine. Pia taasisi za elimu ya juu kwa maana ya vyuo vikuu zihakikishe kwamba wanafuata mwongozo wa Bodi ya Mikopo kwa maana kwamba zile fedha ambazo hazijaenda kwa wanafunzi waliotakiwa kupewa na hawakupewa ndani ya siku zile 30 basi zirudishwe ndani ya wakati kama mwongozo unavyosema, ndani ya siku 30.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo mengine, naomba uchunguzi ufanyike kulingana na haya makosa ambayo yameainishwa ni mengi mno. Uchunguzi ufanyike ili waone kama ilikuwa ni maksudi ya kuibia Serikali ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa haraka. Pia kuwe na kitengo maalum kama huduma kwa wateja cha kusaidia kupokea na kutoa ufafanuzi pamoja na kutatua changamoto kwa wakati ambazo zinaikabili Bodi ya Mikopo.

Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine ni kwamba TAKUKURU watumie hii ripoti ya CAG kuhakikisha kwamba wanafuatilia na kuhoji hizi Taasisi za Serikali Bodi ya Mikopo ikiwa mojawapo na nyingine ambazo zimetajwa na kazi yao iwe ya muda mfupi kwa sababu wamerahisishiwa. Suala la TAKUKURU kuchukua miaka miwili miaka mitatu, wakati taarifa hizo wameshatafuniwa hiyo inatia mashaka, kwamba inaweza ikawa kuna coalition pia hata huko ndani ya TAKUKURU pia kwa sababu nao pia ni binadamu.

Mheshimiwa Spika, hivyo, tuombe kwamba ripoti hii waifanyie kazi kwa muda mfupi, hatutaki kusikia miaka miwili miaka mitatu, unachunguza nini wakati tayari umeshatafuniwa. Kwa hiyo, naomba TAKUKURU hili walifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, mimi niliomba nichangie hayo kwa uchache, ni eneo hilo moja tu, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii ya Waziri Mkuu. Kwanza napenda kukupa taarifa pia, mimi humu ndani najuiliakana kama Chifu Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga. Sasa nimeshangaa kwamba sijachangia, lakini umejua nimechangia, lakini nafiri ni error kidogo. Yupo Kiswaga mwingine, lakini humu ninajulikana kama Chifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza nimshukuru sana Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaifanya, hata Jimbo langu limefaidika sana katika kipindi cha mwaka mmoja ambapo Rais huyu ameingia madarakani. Pongezi hizo zinakwenda kwanza kwa kuwa nimeweza kupokea fedha, na kulikuwa kuna kilio kikubwa katika Kata ya Ifunda kwenda Lumuli, watu walikuwa wanashindwa kuvuka wakati wa mvua, lakini kwa fedha za dharura nimepokea kama shilingi milioni 900, tumeshaweza kutengeneza daraja pamoja na kivuko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru kwa sababu nimeweza kupokea shilingi milioni 500, tunajenga Kituo cha Afya pale Kiwele; pia nimepokea shilingi milioni 446, tumeunganisha Kijiji cha Mlanda pamoja na Magulilo ambapo ilikuwa ni shida sana kuvuka. Vile vile nimepokea shilingi milioni 470 kwa ajili ya kujenga Shule ya Sekondari pale Luhota. Pia nimepokea kiasi cha shilingi bilioni moja kutoka kwenye Mfuko wa UVIKO kwa ajili ya madarasa. Kwenye UVIKO pia nimepokea shilingi milioni 500 ambazo zinakwenda kwenye maji pale Magulilo Kijiji cha Nega ‘B’. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengi yametekelezeka, kwa hiyo, nimeona nami niweze kumpongeza. Nilikuwa najaribu kuangalia mambo haya mengi yamefanyika kwa muda mfupi Rais huyu akiwa mwanamama, nasi akina baba tulikuwepo, hatukuweza kufanya haraka haraka namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia dunia kwa ujumla wake, nikaona kwamba wanawake huwa hawapati nafasi sana za kiutawala. Nikiangalia katika mataifa makubwa, kwa mfano, Uingereza, tangu mwaka 1801 kumekuwa na Mawaziri Wakuu 55, lakini kumekuwa na wanawake wawili tu; alikuwepo Margaret Thatcher na baadaye akaja Theresa May. Huyu mama, Margaret Thatcher ambaye alikuwa mwanamke wa chuma, alifanya kazi kubwa sana za kuinua uchumi katika Taifa lile; na ndiye Waziri Mkuu peke yake aliyetawala muda mrefu na tunaamimi na Mama huyu atatawala muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilikwenda pale Ujerumani nikaona kumekuwa kuna ma-chancellor 33 tangu mwaka 1867, lakini ni mwanamke mmoja tu anaitwa Chancellor Angela Merkel, ametawala kwa miaka 16, kwa muda mrefu baada ya Chancellor yule mwanzilishi ambaye alikuwa Otto Von Bismarck. Kwa hiyo, wanawake wanafanya kazi kubwa katika dunia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikija kwenye hoja baada ya kutoa hiyo shukrani, ni kwamba katika Hotuba ya Waziri Mkuu imekuwa ikieleza mambo mengi; inaeleza mipango ya maendeleo katika maeneo mbalimbali na inagusa miundombinu na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikielekea kule kwangu, Jimbo la Kalenga na Mkoa wa Iringa kwa ujumla tuna mambo ambayo tulikuwa tukitamani Serikali iweze kufanya. Kwa mfano, kwenye upande wa miundombinu, tuna barabara mbili muhimu sana na nyingine za kiuchumi. Ukiangalia ile barabara inayotoka Iringa kupita Kalenga ikaenda kule Ruaha National Park kwa ndugu yangu Mheshimiwa Lukuvi, na ile barabara inayotoka Iringa, inapita Jimboni kwangu inaenda kule Kilolo, barabara hizi tumezizungumza mara nyingi, lakini tunaendelea kusisitiza kwa sababu zina umuhimu mkubwa sana katika uchumi wa Mkoa wa Iringa na kwa Taifa kwa ujumla kwa sababu zinakwenda katika maeneo yenye Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru nimefanya vikao na Afisa Mtendaji Mkuu wa TANROADS, amenipa matumaini. Ameniambia hii barabara ya kutoka Iringa kwenda Kilolo tutaanza pengine mwezi wa Saba kwenye bajeti ya RISE; tunaomba hilo litekelezeke. Pia amenipa taarifa kwamba barabara ya kwenda Ruaha National Park, mazungumzo yanaendelea na World Bank, pengine tunaweza tukasaini mkataba mwezi wa sita na ujenzi ukaendelea. Kwa hiyo, tunaomba haya mambo yatekelezeke ili Mkoa wa Iringa uweze kufunguka na uchumi uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana TARURA kwa kazi kubwa ambazo wanaendelea kuzifanya. Bajeti tumeongezewa kwenye Jimbo langu na kwenye maeneo mengine ya Taifa. Changamoto kubwa tulizonazo katika kutengeneza miundombinu ya barabara za vijijini, tumekuwa hatutengi bajeti vizuri kwa ajili ya mifereji pamoja na makalati. Hilo limekuwa ni tatizo kubwa sana. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali na TARURA kwa ujumla, tunapokwenda kuweka hizi bajeti, tuzingatie sana makalavati pamoja na madaraja madogo madogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru pia CEO wa TARURA, ndugu yangu Seif, nimefanya naye vikao kadha wa kadha na amenihakikishia kwamba mwaka huu katika Mradi wa RISE vijijini, tutakwenda kujenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka pale Uwenda, ikatokeze Mgama kilometa 19. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba hilo litekelezwe kama tulivyoongea ili sasa tuweze kuomba mahitaji mengine. Kwa mfano, barabara inayotoka Kalenga kwenda Mafinga kupita Wasa, kupita Maboga, ni barabara muhimu sana ambayo kama mkoa tunaweza kuitumia kama njia mbadala.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa kuna changamoto kubwa sana kwenye nchi yetu, maeneo mengi hayana barabara mbadala. Kwa hiyo, ikitoka kama jam au ajali njiani, unakuta kwamba kunakuwa na ucheleweshaji mkubwa. Kwa hiyo, kama tukitengeneza hii barabara ya Kalenga, ikaingia Uwasa, ikatokea Mafinga itakuwa ni njia mbadala ya Mkoa ili hata ikitokea tatizo, tunaweza kuitumia. Yale mazungumzo nimeshaanza kufanya na TANROAD na TARURA, tumekubaliana kwamba tutaitembelea. Naomba hii iingie kwenye kumbukumbu rasmi za Bunge ili ije itekelezwe baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, Serikali imekuwa ikifanya kazi nzuri sana kwenye miundombinu ya elimu na madarasa mengi tumejenga lakini changamoto kubwa ambayo tunayo ni upungufu wa walimu na mabweni. Tunatamani sana sasa Serikali ijielekeze kwanza kukarabati shule kongwe. Tuna shule kongwe nyingi ambazo zimejengwa tangu miaka 1970 na kuendelea, ambazo zimechakaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna upungufu wa walimu. Kwa mfano, weekend nilikuwa Jimboni, nimekuwa vijiji vya Nega ‘B’ na vijiji vya Mlanda. Kijiji cha Nega ‘B’ Shule ya Msingi ina walimu watano. Mfano tu natolea, Mlanda Shule ya Msingi ina walimu saba. Kwa hiyo, naomba Serikali sasa iweke nguvu katika kupeleka walimu kwenye shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ujenzi wa vyoo; ukiangalia tumepewa fedha kwenye vituo shikizi. Hivi vituo shikizi vimekuja bila fedha ya choo. Kwa hiyo, hilo nalo tuliangalie kwenye bajeti zetu, maana kuna Halmashauri nyingi ambazo hazina uwezo. Hilo tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tukija kwenye Afya, sera yetu inasema kwamba tutakuwa na zahanati kila Kijiji, na nguvu za wananchi zimekuwa zikitumika maeneo mbalimbali, na tuna vijiji vingi ambavyo tayari vimeshakamilisha maboma. Kwa mfano, nilikuwa Ndiwili Jumamosi, wameshakamilisha boma, lakini bado hawajaezeka. Sasa Serikali lazima iwaunge mkono mara moja ili sasa nao waweze kufurahia ile kazi yao ambayo wanaifanya na Serikali kuwaunga mkono kwa haraka. Hata pale Nega ‘B’ tayari wameshakamilisha boma lakini bado hatujaweza kuwakamilishia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwa upande wa vituo vya afya, ni kweli tunayo sera ambayo inasema tuwe na vituo vya afya kila kata. Sasa kazi kubwa imefanyika. Kwa mfano, Jimbo la Kalenga lina vituo vitatu ambavyo vimekamilika. Kwa mfano, kituo cha Nzihi ni cha siku nyingi lakini hakina wards. Kwa hiyo, hiyo ni changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ukienda kwa mfano Kituo cha Mgama; pale Mgama wananchi wameshaweka msingi kwenye kujenga wodi kwa ajili ya akina baba na akina mama, lakini miaka karibu minne hakijamalizika. Kwa hiyo, naomba Serikali kwenye bajeti zake sasa ikamilishe hivi vituo vya zamani ukiacha hivi vipya ambavyo tunavileta ili sasa na wananchi waweze kuifurahia Serikali yao kwa kazi kubwa ambayo inafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambazo nilipenda pia kuzungumzia ni kwenye upande wa umeme. Serikali imeagiza kwamba ifikapo mwezi wa 12 tuwe tumemaliza umeme kwenye vitongoji vyetu vyote, lakini nikiangalia kasi tunayokwendanayo sasa, bado tupo nyuma sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja, mengine nitaandika kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia mchana huu. Nafikiri kwansababu nilikaa Zanzibar ndiyo maana nimefuatia kuchangia baada ya watu wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu kwamba hali ya mazingira katika nchi yetu imeendelea kuharibika sana. Takwimu za dunia zinaonyesha kwamba joto katika miji mikubwa limeendelea kuongezeka sana. Tanzania kwa sababu bado tuna misitu mingi hatujaona yale matatizo makubwa. Nilikuwa na mambo mengi ya kuzungumza lakini kwa sababu ya muda nijielekeze tu moja kwa moja katika ushauri.

Mheshimiwa Spika, ushauri ambao nataka kutoa katika eneo hili la kutunza mazingira, kwanza elimu ya kutunza mazingira kwa Watanzania naomba itolewe kwa wingi sana kwa sababu hali inazidi kuwa mbaya. Sehemu nyingi ambazo zimeanza kuwa kame ni kwa sababu mazingira yameharibiwa mno ndiyo maana unakuta kwamba mimomonyoko inakuwa mikubwa, maji yameacha mkondo yameenda kwa wananchi. Nashauri elimu itolewe kwa wingi kwa sababu sioni kama Serikali inatilia mkazo sana eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna hii kawaida kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanafanya zoezi la kupanda miti kama 100 au 500 halafu vyombo vya habari vingi vinatangaza lakini hatutaki popularity ya aina hiyo. Namshauri Waziri wa Mazingira kwamba katika KPA (Keep Performance Areas) kwa hawa Wakuu wa Mikoa wape malengo ya kupanda miti kila mwaka na wapimwe kwa namna hiyo. Tunaona pale Tabora Mkuu wa Mkoa aliyekuwepo Bwana Mwanri ameubadilisha sana kwa sababu ali-focus sana katika kupanda miti. Kwa hiyo, kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya iwe ni KPA yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka kushauri katika kutunza mazingira tuongeze matumizi ya gesi lakini kama tutaweza tutoe ruzuku kwa vijijini. Kule vijijini tutoe ruzuku kidogo kwa sababu uwezo wa hawa watu wa vijijini kununua gesi ni kazi kubwa. Nashauri tufikirie kwa baadaye siyo sasa ili tutunze mazingira yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kumekuwa na ongezeko la kujenga kwenye miinuko katika miji, kwa mfano Iringa pale kuna miinuko lakini hata Morogoro pale Milima ya Uluguru unakuta watu wanajenga na Serikali ipo! Kwa nini Serikali isipige marufuku kwa sababu mazingira yanaendelea kuharibika na watu wanaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika kutunza mazingira mashamba yaliyoko vijijini, kwa mfano kuna shamba pale Uyole wakati niko pale Mbeya nilisikia watu wanasema hili shamba tunataka tuishauri Serikali ibadilishe kuwa viwanja, hapana! Siyo lazima tufanye hivyo. Unajua maeneo makubwa kama yale ni ya makimbilio, inaweza ikatokea vurugu huko mjini eneo kama lile linakuwa ni eneo la makimbilio. Kwa hiyo, wazo la kusema kwamba ufute shamba lililopo mjini siyo sawa. Kwani nani alisema mijini hatuwezi kuwa na mashamba, ni eneo zuri sana la makimbilio lakini ni source kubwa ya oxygen. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo naliona sasa kumekuwa na ukataji mkubwa wa miti kiholela, watu wanachoma misitu lakini watu wanakata miti kiholela. Hawa Maafisa Misitu tumewaweka huko hawasimamii suala hili. Kwa hiyo, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba Maafisa hawa wanasimamia maana vinginevyo haya maeneo yatakwisha. Kwa mfano, mimi nina Kata za Kihanga na Wasa, miti kule imekuwa ikikatwa hovyo hovyo, Mkuu wa Wilaya na Afisa Misitu yupo na usiku wanasafirisha. Sasa mimi kama Mbunge siko tayari kuona misitu yangu inaharibika niondoke niache wananchi wakiwa katika hali ya ukame. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine Serikali iongeze maeneo ya uhifadhi. Tukifanya hivyo kwa kweli tutaweza kutunza mazingira na uharibifu wa mazingira tutaweza kuudhibiti. Kumekuwa na ukuaji wa miji, vijiji vinageuka kuwa miji na shughuli za kiuchumi zinaongezeka, kilimo cha kisasa kinaongezeka; hivi vitu vyote vinaharibu mazingira.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iyazingatie haya niliyoshauri, nafikiri tukienda hivi tutakwenda vizuri. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia jioni ya leo katika sekta hii muhimu sana ambayo ni sekta mtambuka kabisa katika nchi yetu. Nafahamu kwamba mawasiliano ni muhimu sana ndiyo maana hata ukiangalia Waheshimiwa Wabunge wote hapa wameinamia simu zao kuonyesha kwamba mambo mengi hayawezi kwenda pasipo kuwa na mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia eneo moja, mimi niiombe kwanza Serikali iwekeze sana kwenye TTCL kwa sababu kazi yake ni kutoa huduma. Nimeona mara nyingi hapa watu wanamlazimisha Waziri kwamba waambie watu wa mitandao waende wakajenge hap ana pale, watu wa mitandao hawawezi kujenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimefanya kazi kwenye mitandao miaka 20, nilikuwa Mkurugenzi wa Kanda, unaomba minara 50 unaambiwa useme utaturudishia nini (Return on Investments). Kwa hiyo, unless Serikali wakati inatoa ile license ilimwambia yule mtoa huduma kwamba tunataka uende vijijini utujengee minara vijiji 500 lakini kama ulimkaribisha tu ukampa leseni huwezi ukamlazimisha. Kwa hiyo, ni kazi ya Serikali kuona kwamba inaiwezesha hii TTCL ipate pesa ya kutosha. Tukiiambia Serikali itoe pesa hizo ndiyo tutakuwa na haki ya kuiambia Serikali hapa sina mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kushauri ni kwamba TTCL ijiendeshe kibiashara. Kwenye mawasiliano kuna ushindani mkubwa sana, yaani ushindani kwenye mawasiliano katika nchi ya Tanzania ni mkubwa mno. Huwezi ukasema kwamba TTCL ifanye vizuri kama hujaipa pesa! Hata kuajiri kwenye mitandao huwa kunyangana wafanyakazi, mtandao huu ukiona kuna mfanyakazi mahali fulani anafanya vizuri zaidi unapanda dau unamchukua aje kwako. Sasa na sisi kwenye TTCL kama Serikali tunaweza kuamua kubadilisha kanuni kwamba namna tunavyoajiri iwe tofauti na yanavyoajiri mashirika mengine ili tuwe na ushindani wa kweli. Tusipofanya hivyo hatuwezi kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine ambalo nataka kuzungumzia hapohapo kwenye TTCL, mwaka 2003 niliingia kwenye Task Force ambacho ni kikosi maalum kwa ajili ya kuuza simu za mezani zilikuwa zinaitwa People’s Phone, wengi mtakuwa mnazifahamu. Baada ya kuona haziende Kampuni yangu ya Vodacom kwa wakati huo ikaunda timu ya watu watatu na mimi ikaniweka kitengo cha mauzo. Nikafikiria nifanye nini, mimi ndiyo mwanzilishi wa hao mnaowaita freelancers, ikabidi niishauri kampuni yangu inipe pesa ili mimi nilete vijana ambao watakwenda mlango kwa mlango kuuza simu. Baada ya kunikubalia, tuliuza zile simu ndani ya mwaka mmoja nchi nzima ilikuwa tayari imeshapata hizo simu za mezani. Kwa hiyo, tuipe nafasi pia TTCL ili iweze kutumia huu mfumo wa freelancers. Tukifanya hivyo, itaweza kupata wateja wengi, hilo nilipenda kushauri pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine ni upande wa Shirika hili la Mawasiliano (TCRA). Ninaiomba sana TCRA iimarishe mahusiano na watoa huduma. Kumekuwa kama kuna uadui fulani. Nilizungumza siku moja na Waziri kwamba huyu mtoa huduma akifanya kosa kidogo, anapigwa faini kubwa. Kwa hiyo, kumekuwa kuna uhasama wakati mwingine kati ya watoa huduma na hiki chombo ambacho kinadhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara inahitaji mahusiano duniani, usipokuwa na mahusiano, huwezi kufanya biashara. Kwa hiyo, napenda Waziri hilo alisisitize sana kwa watu wake. Hii TCRA isiwe Polisi. Ikiwa Polisi, itaharibu biashara, nasi tunahitaji biashara. Kama tunataka hawa watu wawekeze, ni lazima tuwabembeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka kuzungumzia ni UCSAF. UCSAF nayo siamini sana kama inapewa pesa ya kutosha. Naishukuru Serikali kwa kuamua kutengeneza huu mfuko ili kusaidia mawasiliano vijijini. Kama nilivyosema kwamba hawa watoa huduma wengine kwenda vijijini hawawezi kwa sababu minara mingi vijijini, unakuta mnara unaleta shilingi milioni moja. Wewe umejenga kwa shilingi milioni 300, lakini kwa mwezi unakupatia shilingi milioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unauhudumia huu mnara kwa shilingi milioni 4.8 kwa sababu mnara mmoja kuweka majenereta unaweka lita 2,000 za mafuta unakuta kwamba unatumia kati ya shilingi milioni 4.8 mpaka shilingi milioni tano kwa ajili ya kuuhudumia, lakini unakupa shilingi milioni moja au shilingi 800,000. Kwa hiyo, hakuna mtoa huduma ambaye atakuwa na hamu ya kwenda huko. Ndiyo maana tunaomba hii UCSAF ipewe pesa ya kutosha ili Watanzania wengi wapate mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nije kwenye Jimbo langu. Jimbo langu nalo lina mawasiliano hafifu katika kata nyingi. Ukiangalia Kata za Magulilo, Wasa, Mgama, Kiwele, Ulanda, mawasiliano yako hafifu. Pia kuna Kata moja ya Masaka, haina mawasiliano kabisa na Kata ya Kihanga pamoja na Kata ya Wasa, naiomba Serikali, kale kasungura kadogo ambako tunakwenda kugawana, nami basi kule Kalenga Waziri unikumbuke kidogo kupitia mfuko huu. Siwezi kusema nikushikie shilingi hapa, siwezi kwa sababu najua huna pesa. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namsaidia tu Mheshimiwa kwa kumwambia kwamba TTCL ilikuwa na minara nchi nzima ikauza kwa American Tower, sasa hivi inakodi. Yaani iliuza kwa gharama nafuu, sasa hivi inakodi minara. Sasa tutapataje mawasiliano? Endelea Mheshimiwa. (Kicheko/Makofi)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninachosema ndugu yangu, Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, ni kwamba nami mwenzako…

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea taarifa hiyo, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitafafanua anachozungumza huyu; anachozungumza ni suala tu la kimazingira kwamba ilikuwa ni makubaliano ya makampuni na Serikali iliridhia kwamba hatuwezi kuwa na minara mingi, kwa sababu mnara ule mmoja siyo mawasiliano, kinacholeta mawasiliano ni zile antenna tunazofunga.

Kwa hiyo, kampuni hata tano zinaweza zikafunga kwenye mnara mmoja na bado watu wakapata mawasiliano ya makampuni tofauti. Kwa hiyo, hilo lisikutishe kuona mahali minara inaondolewa, lakini hata ukibaki mmoja, makampuni hata kumi yanaweza yakautumia mnara mmoja na mawasiliano bado watu wakaweza kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kule Kalenga…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante. Dakika zako saba zimekwisha.
Mheshimiwa Dkt. Kimei. (Kicheko/Makofi)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu. Mwaka 2012 nilipata nafasi ya kuhudhuria mkutano ulioandaliwa na USAID pamoja na SAGCOT pale Ubalozi wa Marekani, wakati huo mimi nilikuwa msimamizi wa Idara ya Ukuzaji Biashara M-Pesa na nilikuwa nimekwenda pale kwa sababu ya kutaka kusaidia sekta ya kilimo ili kuona namna gani kwa kutumia mtandao tunaweza tukawasaidia kutoa taarifa mbalimbali zinazohusiana na kilimo, upatikanaji wa ardhi na pembejeo na vitu vingine kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, katika kikao kile alikuja Mkuu wa USAID duniani wa 16 kwa wakati huo, alikuwa anaitwa Rajiv Shah. Katika mazungumzo yake nilimsikia akisema: “I am not convinced with a progress of SAGCOT and I therefore consider to withdraw.” Akiwa anamaanisha kwamba hakuridhishwa na hatua ambayo SAGCOT walikuwa wameifikia wakati ule na naamini alisema statement hiyo pengine wao walikuwa ni wafadhili wa huo mradi.

Mheshimiwa Spika, Nini ambacho hakuridhishwa nacho? SAGCOT ilitakiwa iandae ardhi kubwa kwa ajili ya uwekezaji, lakini mpaka wakati ule SAGCOT ilikuwa haijafanya hivyo na wawekezaji wa Marekani inaonekana walikuwa wanataka ardhi kubwa. Unajua mwekezaji wa Marekani anaweza akawekeza Mkoa wote wa Dodoma sasa SAGCOT ilikuwa haijafanikiwa kufanya hivyo kwa hiyo, inaonekana USAID walisema wanataka kujiondoa.

Mheshimiwa Spika, sasa ushauri wangu ni nini katika chombo hiki? Hiki chombo ni muhimu na kiliundwa katika Awamu ya Nne ya Serikali yetu na nia yake ilikuwa ni kutaka kusaidia kilimo kiweze kukua, kutafuta masoko na ardhi ya uwekezaji. Sasa nataka niiombe Serikali katika chombo hiki ione uwezekano wa kukifanya chombo hiki kifanye kazi. Kama kwenye umeme kuna Mfuko wa REA, kwenye maji tumeweka RUWASA, lakini pia kwenye barabara tumeweka TARURA na kwenye kilimo tuitumie hii SAGCOT ili iweze kuwasaidia wakulima kutafuta masoko lakini kuleta wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mpango wa maendeleo tumesema hivi, kwamba tunataka tuandae mazingira wezeshi lakini pia tutafute ajira kwa ajili ya vijana pamoja na masoko, ukileta wawekezaji wakubwa huitaji kuisumbua Serikali kutafuta masoko kwa mfano ukienda pale Rungwe nilishakutana na mkulima mmoja anaitwa Robert Kruga yeye alitoka Zimbabwe analima pale anasoko lake yeye mwenyewe kwa wiki nafikiri anatakiwa kupeleka makontena 50 Ulaya ya Parachichi. Kwa hiyo, ametengeneza wakulima wengine wengi out growers hatuhitaji Serikali maana kule jamaa tayari ana soko.

Mheshimiwa Spika, ukienda Iringa pale ipo Asasi yeye anafuga na anatengeneza hizo yogurt lakini sasa hivi anapata lita 40,000 kwa siku na yeye anataka lita 100,000 kwa hiyo ametengeneza wafugaji wengi ili wamsaidie kupata maziwa na bado hayatoshelezi. Kwa hiyo, maana yake hii SAGCOT kama tunaiwezesha ikapata fedha lakini zamani nimeangalia hapa hii SAGCOT imekuwa ina guarantee ya Serikali ukiipa guarantee hii SAGCOT unaiwezesha iende ikatafute wafadhili yenyewe ili ikipata wafadhili wawekeze kwenye kilimo na hawa SAGCOT wakipata fedha hii SAGCOT catalyst fund itaweza kwenda kuwakopesha wakulima, itaenda kutoa elimu na kuweza kuwatafutia masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utakuta kwamba hatuna haja sasa ya kuona kwamba hawa wakulima wanahangaika na soko au wahangaike kwenye mabenki kupata zile riba kubwa na za muda mfupi SAGCOT inaweza kuamua kwamba iweze kutoa riba za muda mrefu na kuwasaidia wananchi. Lakini pia ukitengeneza viwanda vidogo vidogo kwenye kilimo soko litakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe mfuko huu wa SAGCOT uwezeshwe na Serikali na mpango wake wa kwanza ulikuwa kwamba huu mfuko ushughulikie sekta zote Mifugo pamoja na Kilimo, na kwa mpango huo nilikuwa ninashauri ikiwezekana huu mfuko usikae kwenye Kilimo ukae kwa Waziri Mkuu ili aweze kuuratibu kwa sababu sasa ushughulikie sekta zote na uweze kwenda nchi nzima usiende Nyanda za Juu Kusini peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na mengi naona muda wangu hautoshi ni hilo tu moja linatosha kuchangia kwa leo pengine mengine nitaandika ili Serikali iweze kuangalia nini cha kufanya, naunga mkono hoja ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kweli nilikuwa nimejiandaa kuchangia kesho lakini tuendelee. Ni heshima kubwa umenipa, ninashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo moja ambalo nilitaka kuzungumza tumesema kwamba tunataka kuleta umeme wa vyanzo tofauti tofauti. Nilikwenda kumuona Waziri wakati fulani. Namshukuru, alinipokea. Kuna watu walikuwa wanataka kuweka mradi wa umeme kwenye Jimbo langu, mradi wa solar. Nilivyoongea na Waziri alinipokea vizuri lakini nikiangalia utekelezaji wake kwa watendaji wake naona kama iko polepole sana kwa sababu nimekuwa nikifuatilia sioni kama napata majibu vizuri.

Mheshimiwa Spika, nachotaka kusema ni nini? Kama mradi huu wa solar utaweza kujengwa kwenye Jimbo langu la Kalenga kwanza utausaidia Taifa kupata umeme kwa sababu hawa watu wanataka kuleta Megawatt 50 ambazo wataziingiza kwenye grid ya Taifa. Lakini pia kwenye Jimbo langu watu watapa ajira, pamoja na kuongeza uchumi katika maisha yao, hii ni muhimu. Nataka nikuambie Waziri hili jambo nitaendelea kulifuatilia na wewe unisaidie kuhakikisha kwamba huu mradi wa solar kwenye Jimbo la Kalenga unatekelezwa na huyu mtu ambaye ameonesha nia ya kutaka kuweka huu mradi apate hiyo fursa kwa sababu itatusaidia kufikia malengo ya Kitaifa ya kuhakikisha kwamba tunaongeza megawatt na kuwa na vyanzo tofauti tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ningependa kuishauri Wizara na TANESCO kwa ujumla, tunavyopeleka huu umeme wa REA III sasa kwenye vijiji tuhakikishe kwamba tunaangalia Taasisi. Of course, maagizo wewe Waziri umeshatoa lakini nataka kwa watendaji wako wafahamu hili ni suala muhimu sana taasisi kama shule, kama zahanati, hizo ni muhimu sana zipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapokea malalamiko hapa watu wananiambia umeme wa REA umepita lakini kwenye shule tumeambiwa kwamba tununue nguzo. Nafikiri hilo hapana. Kwmaba ni muhimu sana kuona kwamba tunapeleka umeme huko watoto wetu wasome lakini pia na kwenye zahanati watu waweze kupata huduma. Ninavyo vijiji kadhaa hapa ambavyo havina umeme na ninaomba kwamba katika mradi huu wa REA tunaokwenda nao sasa tuhakikishe kwamba vijiji ambavyo havijapata umeme tukiangalia kwenye Kata ya Wasa na vijiji kama Ulata lakini tukija kwenye Kata yangu ya Luhota kuna vijiji kama Wangama, Ikuvila ambavyo tayari kwa miaka mitatu watu wameshasuka umeme, wameshalipia lakini umeme haujawashwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru Waziri kwa sababu Wizara yako kweli imefanya kazi hatuwezi kulalamika lakini ni muhimu kwa sababu kwamba kwa kadri tunavyoendelea kuongeza huduma na matamanio ya watu ndiyo yanakuwa makubwa. Kikubwa kingine ni kwamba kuna maeneo mengine tuna umeme mdogo.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Kijiji nilichozaliwa mimi Kijiji cha Nyamihu kwamba tuna transformer iko mbali sana na wananchi wangu wamekuwa wakilalamika kwamba tunataka transformer isogee hapa kijijini ili sisi tuweze kuwa na umeme wenye phase tatu. Tuweke mashine za kukoboa, za kusaga. Kwa kufanya hivyo, tunavyoongezea hii huduma maana yake tunazalisha ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, rafiki yangu Gambo, siku moja alisema hapa kwamba anashangaa inakuwa kuwaje Serikali imesema itaajiri watu milioni nane. Hapana, Serikali inavyosogeza huduma karibu na wananchi kama umeme maana yake kama tunaweka mashine za kusagia maana yake tumezalisha ajira. Tunavyoweka viwanda vidogo vidogo maana yake ndivyo tunavyozalisha ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana kwamba taasisi tuzizingatie. Kwa mfano katika Kata yangu ya Kiwele nimekuwa nikilalamikiwa hapa kuna kitongoji kimoja cha Kipengele, yaani umeme umeruka lakini eneo hilo ndiyo lenye shule na eneo hilo ndilo lenye makanisa. Ndiyo maana tukasema kwamba focus iwe kwenye huduma za jamii zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuangalie vile vitongoji vilivyoko pembezoni, vile vilivyoko pembezoni tukianza navyo hivyo ni rahisi wakati mwingine kurudi katikati. Kwa hiyo, nikuombe sana kwa hayo machache tuone namna gani tunaweza tukapeleka umeme hasa kwenye jimbo langu. Lakini jambo ambalo pia nataka kusisitiza nikukumbushe tu Mheshimiwa Waziri Jimbo la Kalenga ndilo jimbo ambalo Spika wake hapa ndiyo amekaa muda mrefu kuliko mtu mwingine yeyote. Lakini ukiangalia pia Chifu wetu Mkwawa ndiye Chifu ambaye alitetea nchi hii kuona kwamba isitawaliwe na Wajerumani na wengine waliokuja. Kwa hiyo, ni Jimbo moja muhimu sana. Kwa hiyo mnavyofikiri akupeleka huduma lazima hizi facts zote mziangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Rais wakati anafanya uteuzi wa Wakuu wa Mikoa amewakumbuka waasisi wetu. Amechagua mtoto wa Nyerere, akachagua mtoto wa Sokoine. Maana yake amekumbuka michango ya hawa waasisi walichofanya. Lakini na Jimbo la Kalenga katika nchi hii lina mchango mkubwa sana. Kwa hiyo, wewe pamoja na Waziri mwingine wanavyofikiria kupeleka huduma, Jimbo la Kalenga lipewe kipaumbele kwa sababu ya mchango wake mkubwa sana kwenye Taifa hili la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa hayo machache. Naamini mambo mengine tutaendelea kuzungumza. Ahsante sana Spika kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya na Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula, East African Community Protocol on Sanitary and Phytosanitary Measures – EAC SPS ambalo linalenga Kuwa na viwango ambavyo vitaleta ushindani katika soko la Afrika Mashariki pale ambapo tutakuwa tunapeleka mazao na wanyama wetu kwenye hili soko la Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nchi yetu ya Tanzania imechelewa kwa miaka nane kama ilivyoelezwa tangu mwaka 2013, lakini nafahamu kwamba ilikuwa ni uwoga. Kama nchi tulikuwa hatuko tayari na tulikuwa tuna mashaka kama hizi fursa zitatolewa pengine wenzetu wanaweza kufaidi zaidi kuliko sisi. Hili lilikuwa ni jambo la msingi kwa sababu ukiangalia misingi yetu kama nchi, tumekuwa na mfumo ule wa kiutawala wa kiujamaa, wakati mwingine umekuwa ukijitenga sana na mifumo hii ya kidunia. Tukafikiri kwamba tukiwa sisi peke yetu pengine ndani ya nchi tunaweza tukafanya mambo yetu, lakini ukiangalia mabadiliko yanayoendelea sasa duniani hatuwezi kusimama peke yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata ukisoma katika Maandiko Matakatifu, katika Kitabu cha Mwanzo 11:6 pale, inazungumzia umoja; anasema, watu hawa ni wamoja, lugha yao ni moja na sasa hili ndilo wanalifanya na hakuna atakayewazuwia. Sasa tukifikiri sisi kama Taifa tunaweza tukasimama peke yetu hiyo haiwezekani. Ni kweli, ukiangalia ki-teknolojia kama Taifa hatuko tayari, wenzetu wamesha- advance kwa mambo mengi, lakini sasa tutasubiri mpaka lini? ukiendelea kusubiri baadaye tutafungiwa milango na tukishafungiwa milango inaweza ikawa pengine ni kazi kubwa kuja kuifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi naona hili jambo ni la msingi sana, kama nchi tuchukue hatua tuingie. Yale mapungufu ambayo yapo tuchukue hatua ya kuanza kuyatekeleza na kuziba mianya hiyo ili sasa tuingie kwa miguu miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo naliona katika kutekeleza Itifaki hii ni muhimu sana kuhusisha sekta binafsi. Kwa mfano, ukizungumzia habari ya kulima parachichi kule Njombe, Serikali haiko, lakini watu binafsi wanalima na wanauza kwenye masoko ya nje na haya maparachichi yanakubalika. Ukiangalia wakulima kama akina ASAS wanatengeneza vyakula vyenye viwango vya kimataifa. Kwa hiyo, kama tukihusisha sekta binafsi ni rahisi sana kuwakilisha nchi yetu na kuleta ushindani kwenye soko la Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimeona kwamba kama tutaingia kwenye Itifaki hii kuna manufaa makubwa; kwanza ushirikiano wa pamoja lakini tunaweza kuteteana kama Jumuiya. Kama tunaamua kuuza bidhaa zetu pengine Ulaya, Marekani, kwa kuwa sasa tuna Itifaki ya pamoja kama nchi moja inapeleka kule inazuiliwa nchi nyingine inaweza ikaitetea. Kwa hiyo, unakuta kwamba tukiungana kwa namna hii inakuwa ni kazi rahisi tutaweza kuendelea kwa Pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunaweza kufaidishana kati ya nchi na nchi hasa kimaarifa. Kama tunafanya kazi kwa pamoja tukishirikiana na Wakenya na Warundi na Waganda, tukikaa kwa pamoja tuna-share ile wanasema maarifa. Kwa hiyo, kama tukijenga maarifa na ufahamu wa pamoja ni rahisi sana kujenga nguvu ya pamoja na tukaweza kufanikiwa kama Jumuiya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nishauri kwa kuwa tayari Tanzania ni mwanachama wa Shirika la Biashara Duniani hii Itifaki pia inaweza kuisaidia Tanzania kufanya biashara hata kwenye masoko ya kimataifa. Ukiangalia pia tumeshapitisha mikataba mingine ya kimataifa inayohusiana na usalama wa mimea na wanyama pamoja na mazao. Kama tulishapitisha hii mingine miaka mingi iliyopita hakuna sababu ya kuikataa hii tunakuwa tunajichelewesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nachoomba hii iwe changamoto kwa Taifa, kwamba tuingie, lakini changamoto ambazo tutazikuta huko tukabiliane nazo kwa sababu tukiendelea kuchelewa haitusaidii kama nchi. Tunaweza tukapima matokeo tangu tumeanza kukataa nchi yetu imefika wapi? Tukiangalia kiuchumi tuko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nawashauri Wabunge wenzangu kwamba tuipitishe Itifaki hii, lakini changamoto tutakazozikuta kule mbele tukabiliane nazo na baadaye tutavuka na tutapata manufaa makubwa katika kuuza bidhaa zetu zinazotokana na mazao ya kilimo katika nchi za Afrika Mashariki lakini pamoja na nchi za nje. Ni kweli kumekuwa kuna mashaka, ukiangalia hii miaka nane iliyopita kulikuwa kuna vipengele viwili ambavyo tumeona vilikuwa vinaleta mashaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ilikuwa inaonesha kama tukisaini Itifaki hii tutalazimika pia kufuata mikataba mingine ya EPA ambayo inazungumzia ulinzi wa kimazingira ambayo ilianzishwa na Marekani. Pia kulikuwa kuna mashaka kuhusiana na mambo ya GMO lakini wenzetu wametueleza kwamba hatulazimiki kwenda kutumia hizi GMO, hasa mbegu, kuleta kwenye ardhi yetu. Kwa hiyo, hicho kipengele kimeangaliwa na sisi tumejiridhisha kwamba kama hilo halitakuwa ni kigezo basi tuko tayari kuingia na kuisaidia nchi yetu iweze kupata manufaa ya kibiashara kwanye hili soko la Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa hayo machache, niwashauri Wabunge wenzengu kwamba tuunge mkono halafu twende tukakabiliane na changamoto ambazo tunaziona ziko huko mbele. Nashukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru hata na mimi kunipa nafasi ya kuweza kuchangia jioni ya leo katika mapendekezo haya ya mpango wa bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa ufupi tu kumshukuru Rais kwa kazi kubwa anayoifanya, tumtie moyo kwa hatua kubwa ambazo ameweza kuzifanya, hata pia kukaribisha uwekezaji na kufungua milango, najua nchi itakwenda kufunguka kwa mapana yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia sehemu ya kilimo, kama ulivyosema twende moja kwa moja. Kwa kweli na mimi ninataka nizungumzie kidogo habari ya kilimo. Tukiangalie kweli kilimo, kama Serikali kwa kweli tumekuwa na mipango mingi lakini tumeitawanya mno, kama tunasema kwamba kilimo kinachukua asilimia 66 ya Watanzania wote, basi kwa kweli tuwe na mikakati ambayo baadae itaweza kutuletea matokeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia habari ya ruzuku bado na mimi naona kuna umuhimu wa Serikali kuweka ruzuku kidogo kwa sababu nikiangalia hali ilivyo huko sokoni kwa maana hasa ya pembejeo, kuna sababu ya Serikali kuangalia katika mpango huu. Ruzuku siyo jambo geni, ukiangalia nchi ambazo zinaongoza duniani kwa ruzuku, kwa mfano anasema Ufilipino na Indonesia wao kwenye Pato lao lile la Taifa wanaweka asilimia 3.1. Lakini ukiangalia kwa mfano India asilimia 25.1 ya fedha zote zinazokwenda kwenye ruzuku kwa maana ya kwenye madini, ujenzi, miundombinu, wao asilimia 25 inakwenda kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia Marekani pia kwa miaka minne tangu mwaka 2017 mpaka kufika 2020 walianza na dola Milioni Nne na sasa wamefika dola Milioni 20 wakiongeza ili kuweza kufidia yale mapungufu ambayo yametokea kwenye kilimo na sababu ni kwamba ni lazima kuweza kuboresha uchumi wa nchi unaotokana pia na kilimo kwa sababu pia ni lazima tule, lakini pia inasaidia kuweza kuboresha bei, kuhakikisha kwamba bei zinaendelea kuwa imara na wakulima wanapata kipato chao. Kwa hiyo, Serikali hili iliangalie kwa huruma yake. Najua inafanya mambo mengi lakini na hili la ruzuku iangalie ili mwakani tusiingie kwenye baa la njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi haina shida ya chakula, kwa mfano ukiangalia sasa mahindi ni mengi, lakini shida tuliyonayo ni masoko. Sasa suala la masoko hili ni muhimu sana. Ukiangalia Nchi ndogo kama ya Swaziland ambayo wana ng’ombe kama laki sita, unakuta wao wana mikataba na nchi za Ulaya, wanauza nyama nyingi kuliko sisi ambao tuna ng’ombe milioni karibu 33.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa walichofanya ni nini ni kusiani bilateral agreements, yaani mikataba ya nchi na nchi ya kufanya biashara, lakini sisi ni nchi kubwa tumeshindwa kusaini mikataba ile fungamanishi na nchi mbalimbali ambazo tunaweza tukafanya biashara kubwa zinazotokana na kilimo. Kwa hiyo hilo nalo ni la kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ambayo nilitaka kuangalia ya kuongeza mapato kama ulivyosema, nilikuwa nafikiria hapa kwenye upande wa transfer ya properties, hasa majengo na viwanja. Eneo hili unakuta kwamba kuna pesa nyingi sana ambazo zimeendelea kushikiliwa. Ninaishauri Serikali kwamba ikiona inafaa tunaweza tukapunguza ile asilimia 10 ya transfer ikaenda asilimia tano, siyo lazima iwe ya kudumu, inawezekana tukafanya kwa mwaka mmoja wa bajeti, labda mwaka tu mmoja wa bajeti tukasema kwamba tunapunguza asilimia tano ili tuchochee watu ambao wana mali ambazo hazihamishiki wakahamisha maana ni eneo lingine ambalo pia Serikali inaweza kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumzia habari ya kuongeza gati, kwa mfano pale bandarini. Sasa uchumi wa mbogamboga, matunda, ni uchumi ambao unakua sana duniani. Sababu kubwa ambayo Tanzania tumekuwa tukishindwa kupata soko kwenye hili eneo la uchumi ni mazingira yetu katika bandari zetu. Kwa mfano, ukiangalia Bandari ya Mombasa, wao wana cold rooms - hivi vyumba baridi, zaidi ya 1,000 kama 1,200 na kitu. Lakini ukiangalia kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam nimesikia kuna mia na kitu, yaani hata mia mbili hatufiki. Sasa eneo hili pia Serikali ni lazima tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka huu uchumi wa mbogamboga na matunda uweze kukua, na ni eneo kubwa linalokuwa duniani, ni lazima tuangalie namna gani tunavyopanua bandari zetu, basi na hizi cold rooms, hivi vyumba baridi vya kuhifadhia mazao vijengwe kwa wingi kulingana na hali halisi ya soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia hatuwezi kujenga, kuweka mipango ya maendeleo ya uchumi bila kuangalia mazingira. Tukiangalia mazingira duniani hali ya mazingira imekuwa mbaya, yaani hata hapa Tanzania mazingira yameharibika sana, nimemsikia Mheshimiwa Rais akiwa Glasgow kwenye mkutano wa mazingira anasema kila mwaka tunapanda miti Milioni 276 ni taarifa nzuri Watalaam wanampatia lakini Je, nikiangalia reflection ukitembea huku Dodoma na Iringa ukiangalia kwa macho yako hiyo miti Milioni 276 kwa mwaka unaiona? Kwa hiyo, inawezekana wakati mwingine hawa Watalaam wanaotoa ripoti, sisemi wanaandika siyo zenyewe lakini ukiangalia misitu inavyoteketea, Je, misitu uteketeaji wake na hii miti tunayopanda vinawiana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mnavyokwenda kuangalia suala la maendeleo lazima suala la mazingira tuliangalie kwa ukaribu sana, ni muhimu sana na hili mimi kwa vile pia ni mpenzi wa mazingira siku zijazo nitakuja...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ni kengele ya pili.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Basi naunga mkono haja. Nilijaribu kwenda haraka, nilifikiri nitamaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye mapendekezo ya Mpango wa Bajeti. Nina mambo machache ambayo nataka nichangie. Kwanza ni kwenye kilimo, kwanza nimshukuru sana Waziri kwa mikakati yake ambayo ameanza kuifanya kuhakikisha kwamba kilimo kinakuwa na nafasi katika nchi hii, lakini kuna mambo ambayo tunahitaji kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 nilipata nafasi ya kualikwa Ubalozi wa Marekani alikuwa amekuja, aliyekuwa US Administrator wa USAID alikuwa anaitwa Rajiv Shah na yeye alikuwa na mpango wa kutaka Tanzania iweze kulima zaidi kwa kupitia taasisi moja ambayo tuliianzisha wanaita ile korido ya Kusini. Alitaka tuwe na benki ya ardhi ambapo yeye anaweza akaleta wawekezaji kutoka Marekani waje walime katika eneo kubwa. Akaonesha masikitiko yake, kwamba tangu aanze ku-support mambo ya kilimo, haoni hatua ambayo imeendelea, kwa hiyo alikuwa na mpango wa kujiondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu ni nini? kwa kuwa tunasema kwamba Tanzania ina asilimia zaidi 60 ya ardhi ambayo inaweza kulimika, tunaweza tukafanya mapinduzi makubwa sana kwenye ardhi, kwa kufanya nini? Lazima Serikali iwe na benki kubwa ya ardhi ambayo imeisajili na iko mikononi mwake. Mwekezaji mkubwa anapokuja hapa anataka kuwekeza tumwonyeshe kwamba tuna benki ya ardhi iko Morogoro tuna hekta 500,000, tuna hekta 100,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyojua wawekezaji wakubwa kutoka katika mataifa makubwa hawawezi kuja kuchukua heka 1,000 heka 2,000. Tuone katika mipango yetu ya baadaye, tutakuja kufanya nini katika hilo eneo. Maana vinginevyo tutakuwa na ardhi kubwa, lakini hatuwezi kufaidika nayo. Tuwe na mipango ya muda mrefu ya kuwa na Benki ya Ardhi ambayo tutaweza kuvutia wawekezaji kirahisi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwenye kilimo, kwamba tunafahamu mabadiliko yanayoendelea ya hali ya hewa, mvua zimepungua sana. Naomba Serikali isichelewe, tuwe na mpango endelevu wa muda mrefu. Sehemu nyingi za nchi hii zina mabonde mengi mazuri. Tunaweza tukatengeneza haya mabanio kwa bei ndogo sana. Huhitaji kufikiria mradi wa bilioni 10, 20 au 30, unaweza kutengeneza banio kwa bilioni moja na nusu, unafunga upande huu, upande huu, kwenye mkondo wa maji unatengeneza mabwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa na mabanio mengi katika nchi hii, tutaokoa majanga mengi ambayo yanatokana na wananchi kukosa mahali pa kulima na sasa hivi wananchi wengi wanakimbilia kwenye vyanzo vya maji kwa sababu hawana maji, sasa utafanya nini? Ni lazima wakimbilie tu huko, lakini kama tutatengeneza mabanio mengi, kwa mfano Mkoa wa Iringa of course na mikoa mingine yako maeneo mengi ya namna hiyo. Serikali isichelewe kwenye huo mkakati, vinginevyo itafika mahali tutaanza kulia wakati tutakuwa tumeshachelewa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nione liwe kwenye mpango wa muda mrefu ni namna gani tutaendelea kuboresha mawasiliano vijijini? Unajua biashara nyingi na mifumo mingi sasa hivi ya kibiashara huwezi kuitenganisha na mawasiliano. Mwaka 2012 wakati nasimamia idara ya M-pesa nilipata nafasi ya kuanzisha kitengo cha M-commerce. Sasa kwenye M- commerce kwa maana ya mtandao biashara tuliingiza afya, kilimo na kwenye afya tulitaka kwamba tusajili vituo vyote vya afya, tusajili zahanati zote ambapo kwa kutumia M-commerce, biashara mtandao tulikuwa na uwezo wa kutoa taarifa kutoka katika vituo mbalimbali kusema hapa unaweza kupata dawa hii, dawa hii na mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye M-commerce tulikuwa na uwezo kwenye kilimo wa kujua hali ya hewa ya kuweza kujua ni aina gani ya mbegu, wapi upande nini, ardhi inapatikana wapi, msimu wa kulima na mambo kama hayo. Yote hayo yanafanyika kwa njia mtandao, ndio maana ni muhimu sana kuwa na mipango ya baadaye ya kuboresha mitandao ya simu vijijini kwa sababu ni njia ya uchumi na ya kukusanya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnavyoona sasa hivi ni njia rahisi sana kukusanya mapato kwa kutumia mitandao ya simu. Sasa kama hatujaweza kupeleka mawasiliano huko tutafanyeje? Kwani eneo lingine muhimu sana la kukuza biashara na uchumi wa nchi yetu. Hilo nalo katika mipango yetu ya baadaye hilo tuliweke na tuone tutafanya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye mazingira sio jambo la kuchezea. Tumekuwa tukisema mara nyingi hapa tulinde mazingira, lakini ukipita katika milima mikubwa hata kama Kitonga pale unakuta moshi unafuka katikati ya mlima. Sasa unajiuliza ni hatua gani kama Serikali tunachukua? Sasa kama moshi unafuka pale maana yake kuna watu wanachoma mikaa, sasa hili ni jambo la hatari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi mikaa mingi sana inatoka katika nchi hii inaenda kuuzwa Burundi, Kenya na misitu yetu inazidi kuharibika. Sasa kwenye hili eneo la utunzaji wa mazingira kwa kweli kuna hao watu wa hizi kampuni ambazo zinajihusisha na kutunza mazingira wanasema miradi ya kuhifadhi mazingira pamoja na bioanuwai. Kwa hiyo kwamba ziko fedha nyingi sana ambazo tunaweza tukazivutia kwa kuziingiza halmashauri zetu, zikatengeneza maandiko mengi, tukahifadhi mazingira, tukapata fedha, tukafanya maendeleo kwenye vijiji vyetu, lakini bado tumetunza mazingira at the same time tumepata pesa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda wangu umekwisha, naunga mkono hoja, mambo ni mengi lakini nitachangia kwa njia nyingine, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii iliyopo mezani. Nitajielekeza zaidi katika Kamati ya Kilimo, Maji na Mifugo. Kwanza naunga mkono hoja ambayo imewasilishwa hapo na Mwenyekiti wangu wa Kamati na ameeleza mambo mengi, nitajadili mambo kadhaa.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa Uvuvi haramu ambapo Kamati imeeleza kwamba kuna uvuvi mkubwa haramu ambao unaendelea kwenye Mabwawa yetu kama Mtera pamoja na Maziwa na nini hasa kinafanyika huko na madhara ambayo yamekuwa yakijitokeza kutokana na huu uvuvi haramu. Kwa mfano, tatizo kubwa ambalo limeonekana, kumekuwa kuna uvuvi wa kutumia hizi taa za solar ambapo Serikali iliruhusu aina fulani ya taa, lakini wenzetu kwa sababu ya kupata faida ya haraka haraka wamekuwa wakitumia taa ambazo hazitakiwi na hivyo kupelekea kuvua mazalia ya Samaki, wale Samaki wadogo kwa mfano Sato ambao wanafuata mwanga na hivyo kuendelea kuangamiza kabisa mazalia ya Samaki hizi. Kwa kweli, jambo hilo tungeomba Serikali ichukue hatua madhubuti kwa haraka sana kuweza kudhibiti, maana vinginevyo uchumi huu unaotokana na Samaki hatutakuwa nao.

Mheshimiwa Spika, pia matumizi ya zile nyavu ambazo hazitakiwi kama kokoro ambapo kuna uwanda tu fulani ambao hawa Wavuvi huwa wanakwenda kuvua, ni rahisi sana kwa Serikali kwenda kudhibiti katika ule uwanda ambao haya makokoro huwa yanakwenda kutumika huko. Kwa kweli Serikali isipokuwa makini tutashangaa baadae kwamba uchumi huu wa samaki tutakwenda kuua kabisa na wananchi kuweza kukosa kipato.

Mheshimiwa Spika, imetokea tatizo lingine ambapo samaki wamekuwa wakifa hasa kwenye Bwawa la Mtera, lakini inaonekana kwamba kuna kilimo ambacho kinaendelea kandokando ya Mito ambayo inapeleka maji kwenye haya Mabwawa. Sasa hiki kilimo kwa mfano, kilimo cha Nyanya kuna madawa mengi yanayotumika, haya madawa yanayotumika ndiyo inakuwa sumu ambayo inaingia kwenye mabwawa na kwenda kusababisha samaki kufa. Kwa hiyo, Serikali ione ni namna gani inaweza kudhibiti watu wanaolima kandokando aidha kwenye Mabwawa yenyewe au kwenye mito inayopeleka maji kwenye mabwawa hayo ili kuendelea kutunza uchumi unaotokana na samaki.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kushauri ni ujenzi wa mabwawa. Tunafahamu kwamba mabadiliko ya tabianchi yanazidi kukua na hii imesababisha sehemu nyingi sana maji kukauka, sasa ujenzi huu wa mabwawa ningeshauri kwamba Serikali kwa kushirikisha Wataalam wa Kilimo, Watalaam wa Maji na Watalaam wa Mifugo wakae kwa pamoja, wawe na design moja. Watengeneze design ambayo hii inaweza kuwa shared ili mtu wa maji anavyotengeneza atumie design hiyo, mtu wa kilimo siyo kila mmoja alete design yake, wakati mwingine tumeona changamoto kubwa kwa hawa wajenzi wa haya mabwawa hayajengwi kwa viwango lakini imekuwa ni shida ni malalamiko badala ya kuwa faida inakuwa ni shida.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kushauri tuendelee nalo, lile zoezi la kuweka hereni kwenye mifugo ni zoezi muhimu sana. Kwanza linaisaidia nchi kujua kwa uhakika wake kwamba tunayo mifugo kiasi gani katika nchi. Zoezi lile lilisimamishwa lakini nimekuja kugundua wakati mwingine ni maslahi yetu sisi wanasiasa, pengine mimi Kiswaga nina ng’ombe 200 sitaki wajulikane ninaweza kuleta sababu kwamba hizi hereni hazifai. Tuangalie kuna changamoto zipi, kama ni gharama za hizo hereni tunaweza tukajadili lakini ili tuweze kufahamu kwamba nchi ina mifugo kiasi gani ni muhimu sana hili zoezi la utambuzi wa heleni likaendelea, maana tunasema kuna mifugo kule Ngorongoro asilimia karibu 50 sio mifugo ya Watanzania lakini tukiweza kutambua kwa kutumia hizi hereni tutaweza kujua kama nchi, mifugo yetu ni ipi na ni mifugo ipi inaingia huko Misenyi ikitoka nchi ya jirani. Kwa hiyo, hilo zoezi ningependa kushauri liendelee ili kusaidia tufahamu kwanza tunamifugo lakini kudhibiti hii mifugo haramu ambayo pia inatoka nchi za jirani.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo nimeona ni muhimu pia ni kuendelea kupanga matumizi bora kwenye upande wa vitalu vya mifugo. Hilo liende sambamba na kutunza maeneo ambayo yamehifadhiwa na Serikali kwa ajili ya ufugaji. Kwa mfano, maeneo yote ya NARCO mimi ninasikitika ninapoona maeneo ya NARCO yanaanza sasa kugawiwa kwa Wawekezaji waweke viwanda au pengine kilimo. Kwa sababu ukiangalia wingi wa mifugo tuliyonayo nilifikiri kwamba tunaweza tukatoa mifugo huko inako haribu mashamba ya watu, tukairudisha huku kwenye hizi NARCO zetu, kwenye hivi viwanja kama tutaweka mipango mizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninashauri Serikali na wenzangu mlioko kwenye Baraza la Mawaziri, msijadili kugawa maeneo ya wafugaji kwenda kwa wakulima au kwenda kujenga viwanda haitusaidii! Tuna mifugo mingi inakwenda huko holela, kwa hiyo tuirudishe huko kwenye ranchi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde thelathini malizia muda wako umekwisha.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika ahsante sana. Jambo lingine pengine kwenye kilimo imetokea changamoto kwenye ucheleweshaji wa mbolea. Kwa kuwa, tunafahamu mahitaji ya wakulima, ningependa tufanye planning mapema. Kwa mfano, sasa hivi mbolea ya kukuzia hatuna, sasa kwa vile tunajua mahitaji basi tuwe na stock in advance, tuwe na akiba ili muda unapofika wananchi wasihangaike na mbolea.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwa uchache kwa habari ya hoja iliyopo mbele yetu inayohusu uwekezaji viwanda na biashara, mimi ningependa kuchangia eneo moja tu pengine mawili hasa upande wa stakabadhi za ghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulipata fursa ya kutembelea Mikoa ya Kusini kwa maana ya Mtwara, Ruvuma pamoja na Lindi kujionea ni namna gani mfumo wa stakabadhi za ghala unafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli tulijiridhisha vya kutosha pasipo shaka kwamba mfumo huu ni mzuri na unaweza kuisaidia nchi kuweza kufanya shughuli za uratibu unaotokana na shughuli hasa za mazao. Tulivyoangalia ule mfumo ule kwanza unawasaidia sana wananchi kuweza kupata soko la Pamoja, wanavyojiunga kwenye vikundi inasaidia kutafuta soko kwa haraka lakini kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulichoona kwamba unasaidia utunzaji wa mazao katika maeneo yenye viwango vizuri kwenye maghara na hivyo inasaidia mazao kutokuharibika, kwa sababu ukiangalia katika maeneo mbalimbali namna ambavyo tunatunza mazao yetu imekuwa ikisababisha mazao yetu kupata sumu kuvu. Kwa hiyo, kwa mfumo huo wa kutumia stakabadhi za ghala inasaidia sana mazao yetu kutunzwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho tuliona kwamba huu mfumo unalinda wazalishaji wadogowadogo, kinachofanyika ni kwamba wenye fedha wafanyabiashara wa mazao ni rahisi kwenda kuokotaokota mazao kwa wakulima wadogowadogo mwenye magunia mawili, matatu, kwa hiyo unakuta kwamba inawanyonya kwenye bei, lakini kama wakiweza kuuza kwa pamoja inawasaidia kupata bei nzuri. Kwa hiyo ni mfumo mzuri ambao mimi nimeona unafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninachokiona kwamba kwenye huu mfumo kumekuwa kuna malalamiko mengi kwamba wananchi mazao yao wakati mwingine hayapimwi katika vipimo rasmi lakini kwa kupitia mfumo huu inasaidia sana wananchi waweze kupima mazao yao katika vipimo ambavyo ni rasmi na vinaweza kuwasaidia wao kuweza kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani tulishaweza kusikia Mzee Mangula alikuwa analima viazi akawa analalamika kwamba wananunua kwa lumbesa lakini kwenye mfumo huu sasa inasaidia kwa sababu tunakuwa na mizani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilichokiona kingine ni kwamba wananchi wanaweza kupata elimu ya pamoja, kama watu wamekaa katika vikundi ni rahisi Maafisa Ugani, Maafisa Kilimo kuja kuweza kuwaelimisha kwa hiyo ni jamba zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niliona jambo lingine zuri katika mfumo huu kwamba pembejeo zinaweza kununuliwa katika maeneo ya uhakika kuliko tunavyoona sasa mtaani kuna viuatilifu na pembejeo feki, lakini kwa kupitia mfumo huu wa stakabadhi za ghala ni rahisi sana kuweza kusaidia watu kupata pembejeo katika maduka ambayo ni rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nililiona, kwa sababu katika safari ile pia tulikuwa na taasisi za fedha, kwa hiyo watu wakikaa katika mfumo huu wa stakabadhi za ghala inasaidia sana kuwa accessible kirahisi na hizi benki zinaweza kuwakopesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni changamoto zipi ambazo tuliziona, tulivyotembelea pale wananchi wengi walitoa shuhuda wao kwamba maisha yao yameboreka, wamejenga nyumba wanasomesha Watoto, lakini changamoto kubwa ambayo tuliiona ni kwamba kumekuwa na ucheleweshaji wa malipo ya fedha, kwa hiyo unakuta kwamba wanapeleka bidhaa leo lakini anaweza akalipwa baada ya miezi mitatu, hiyo inawachelewesha wakati mwingine kufanya mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo tuliliona uaminifu kwa wale watunza maghala, unakuta kwamba umeleta mzigo wako labda wa korosho, wale wasimamizi wanasema pengine korosho zako zilikuwa na unyaufu wa asilimia fulani, kwa hiyo ni changamoto nyingine. Lingine ambalo nililiona ni kwamba kuna changamoto ya maghala ambayo hayana viwango, hizo ni changamoto tatu ambazo tuliziona. Sasa ni nini mapendekezo yangu:

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambacho niliona ni kwamba mapendekezo ambayo mimi ninayatoa hivi Vyama Vikuu viwe na mtaji angalau wa kulipa asilimia fulani wakati mkulima anavyoleta mazao yake ili kuweza kumudu yale mahitaji madogomadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninashauri kwamba hivi vyama viwe na uwezo wa kununua angalau pembejeo za kuanzia ili wanachama wao waweze kupata pembejeo kwa wakati angalau zile za kuanzia. Pia benki ziangalie kutoa mikopo kwa wakati, maana hili pia lilikuwa ni lalamiko ambalo nililiona wananchi wanasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutengeneze maghala yenye viwango, kwa sababu unaweza ukaona kwenye kutunza kwa mfano mbaazi haziwezi kutunzwa katika mazingira fulani kwa muda mrefu yanaweza kuharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine vyama viwe na vipimo vya kuangalia unyevu kwenye mazao hiyo ni mapendekezo ambayo naona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wakala wa vipimo wahakikishe mara kwa mara wanapita kukagua ile mizani kuona kwamba inapima vizuri kwa sababu ile mizani imekuwa na tabia ya kuchezewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu pia iendelee kutolewa hasa kwa viongozi na sisi wanasiasa, maana inaonekana kwamba huu mfumo bado hatujauelewa, wakati mwingine pengine interest zetu, wakati mwingine pengine atuelewi tu mfumo, mimi nilivyouona kwanza utawasaidia wananchi pamoja na Serikali kupata zile tozo muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuwa na uhakika kwamba kama nchi fulani inataka mazao ya kiasi fulani ni rahisi kuweza kujua kwamba Songea tuna dengu kiasi fulani tuna mbaazi kiasi fulani ni rahisi kufanya namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuwe na vyama vichache vyenye nguvu badala ya kuwa na vyama utitiri ambao wakati mwingine ni utapeli. Tukiwa na vyama vichache vyenye nguvu vinaweza kufanya mambo yake vizuri. Tumeona vyama kule Mbinga tumekwenda, kule Namtumbo wanajenga sasa hivi kiwanda chao cha kutengeneza vifungashio ni kwa sababu ni viwanda ambavyo vimeimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, riba kwenye Benki angalau ziendelee kuwa chini kwa sababu hii pia ni changamoto kubwa ambayo tuliiona. Mfumo wa stakabadhi za ghala pia napendekeza uende nchi nzima nina fahamu kupokea au adoption mara nyingi ni shida sana hapa nchini, hata wakati tunaanza LUKU walikuwa wanakataa lakini sasa ndio imekuwa kitu kizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naona katika mapendekezo minada iwe ya wazi, yaani minada siyo tu mtu anakuja na karatasi kwenye boksi mnada ufanyike kwa uwazi kama inavyofanyika ukienda wakati mwingine sokoni watu wanauza mia tano, mia sita, mnada ukifanyika wazi ni rahisi watu kupandisha bei. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hoja hii muhimu iliyoko mezani na nianze kwa kuunga mkono hoja ya Waziri Mkuu kwenye Bajeti ya Waziri Mkuu.

Kwanza nimshukuru pia kwa uwasilishaji mpana ambao umegusa sekta mbalimbali lakini pia namshukuru sana Rais kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kutuletea miradi mingi sana siwezi kueleza mmoja mmoja. Nilikuwa namwambia mtu mmoja wakati fulani nilikuwa nampongeza rais, akasema unampongeza Rais kwa nini mbona anafanya kazi yake? Nikasema wewe hujui kinachoendelea acha sisi tumpongeze kwa sababu tunajua aliyotufanyia kwenye majimbo. Kwa hiyo aendelee kupokea hizi pongezi, sisi tunampongeza kwa sababu tunamtia shime ili aendelee kupata moyo wa kuendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikubwa ni hiyo fairness yake ya kuhakikisha kwamba kila jimbo linapata mgao sawia. Zamani haikuwa hivyo unakuta mtu mwenye nguvu ndiyo anapata share kubwa zaidi, kwa hiyo ndiyo maana tunampongeza.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwanza nianze pia kuishukuru Wizara ya Kilimo kwa kutuletea mahindi hata Jimbo langu lilikuwa limeathirika lakini baadhi ya maeneo tumeshapokea hayo mahindi, rai yangu ni kwamba Watendaji wetu wa Serikali waendelee kuwa waaminifu kwa sababu inaonekana sehemu nyingine watu wanaandikisha majina ya watu ambao hawana uhitaji, wakati wao ndiyo wanaochukua hayo mazao kwenda kujinufaisha, kwa hiyo niombe vyombo vinavyohusika Wakuu wa Wilaya na Maafisa Tarafa kwenye maeneo yote siyo tu Jimbo langu na sehemu zingine zote hili jambo walifatilie kwa karibu.

Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba watanzania wenye njaa wanapata chakula siyo watu kwenda kujitajirisha, hii tuwaonye pia hao wanaofanya hivyo kwa sababu watafungwa, Serikali haipo hapa kwa ajili ya kuchezacheza.

Mheshimiwa Spika, kwenye kilimo ningependa kuchangia zaidi, sasa hivi hali ya hewa inaendelea kubadilika sana kwa sababu ya haya mabadiliko ya tabianchi, hapa Tanzania tumezoea sana kulima haya mazao hasa mahindi kama ndiyo zao letu kuu, sasa tuone wenzetu wa kilimo waanze kufanya utafiti hasa kwenye zao la muhogo kama ndiyo kiwe chakula ambacho kinatoa zaidi, tunapozungumzia nafaka.

Mheshimiwa Spika, miaka ya nyuma huko hata kule kwetu Iringa tulikuwa tunalima sana mtama, lakini miaka ya hivi karibuni huu mtama umepotea. Kwa hiyo, wenzetu wa kilimo sasa watusaidie kwanza kutoa elimu pia kufanya utafiti zaidi kama tunaweza tukapata mtama ambao ni mwepesi zaidi wa miezi miwili pia utawanyike katika maeneo mbalimbali ya nchi kwa sababu tunakokwenda hali itakuwa mbaya zaidi.

Mheshimiwa Spika, hapo hapo kwenye kilimo kwenye vyuo vyetu vya VETA kuwe kuna mitaala mahsusi ambayo inaelezea namna gani tunawafundisha vijana kulima kwa sababu ukiangalia kadri tunavyoendelea ardhi inazidi kupungua, kwa hiyo, uhitaji wa kulima kwa tija unakuwa mkubwa zaidi, mtu atumie eneo dogo lakini azalishe kwa tija zaidi. Sasa hii itawezekana tu kama tutajikita katika kutoa masomo yanayohusu kilimo lakini na zile shule zetu za kilimo za zamani ziweze kurudi ili tuanze kuwaandaa vijana kutoka huko, hiyo itasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la mbolea ya ruzuku pia tunaishukuru sana Serikali kwa kutoa mbolea za ruzuku lakini tuwaombe wenzetu wa Wizara ya Kilimo waanze maandalizi mapema. Mwaka huu sehemu nyingi za Tanzania hata katika Jimbo langu la Kalenga wananchi wamechelewa sana kupata mbolea, pamoja na kuwa mvua zimekuwa pungufu lakini pia mbolea zenyewe zilichelewa sana. Kwa hiyo tunawaomba wenzetu wa kilimo maandalizi yaanze mapema ili mbolea zipatikane mapema, pale ambapo mvua zipo basi Watanzania waweze kunufaika na hii ruzuku ambayo Mheshimiwa Rais amewapa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda kuzungumzia eneo lingine la kukuza uchumi hasa upande wa bandari, kwamba bandari tunajua ni lango kuu la uchumi, naipongeza Serikali katika mipango yake ya kutaka kuanza kujenga Bandari ya Bagamoyo. Tanzania inaweza ikawa hub ya uchumi unaotokana na bandari katika eneo la Maziwa Makuu pamoja na Afrika Mashariki kwa ujumla wake pengine hata na SADC, kwa hiyo jambo hili liende haraka.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali kwamba tulishaanza na tulishasikia kwamba kulikuwa kuna mpango wa kutengeneza mfumo wa kusomana kati ya TRA pamoja na shughuli zinazofanywa bandarini. Miaka miwili iliyopita tuliambiwa kwamba wanaanza majaribio, miaka miwili imepita hakuna kinachoendelea. Hii inaonesha kwamba nia ya bandari na nia ya TRA sioni kama iko vizuri! Kama wote wangekuwa na nia moja hii ingekuwa imeshakwisha na tunaweza kama Serikali tukapata fedha nyingi sana mambo yetu yanapopita kwenye mfumo. Kwa hiyo ninawaomba wenzetu TRA, Bandari mharakishe hili jambo la mifumo kusomana ili nchi iweze kunufaika na kazi kubwa. Muoneshe nia vinginevyo mnatutia mashaka kwamba hizi fedha zinazovuja wenzetu mnanufaika nazo. Kwa hiyo, hilo naomba muweze kuliangalia kwa ukaribu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kuzungumza ni kwamba tunavyoelekea bajeti yetu hii mpya, kweli shule zetu za zamani zimechakaa sana, ninaiomba Serikali kwamba katika bajeti zake sasa tuanze kuziangalia shule zetu kongwe, hasa za shule za msingi nilishazungumza tena nalirudia tena, shule hizi ambazo zimejengwa miaka ya 1970, 1980 zimeshaanza kuchoka. Tunavyoweka nguvu katika kujenga shule mpya basi tuhakikishe kwamba ukarabati wa shule za zamani pia tunaendelea kuziboresha. Hilo nalo ni jambo jema Serikali ione namna gani tunafanya.

Mheshimiwa Spika, pia umaliziaji wa yale maboma katika maeneo ya mashule, katika maeneo ya hospitali kwa maana ya zahanati na vituo vya afya, ambapo tayari wananchi walishaanza. Vipo vituo vya afya ambapo vilijengwa siku nyingi unakuta vina wodi moja ya akina mama lakini hata sasa hivi wakina baba wanaumwa sana. Kwa hiyo, tungependa pia Serikali ione umuhimu katika vile vituo vya afya vya zamani kwangu Kalenga na nchi nzima kuanza kujenga pia wodi za wanaume kwa sababu uhitaji upo na tunavyokwenda huko tunakuta wananchi wanatuuliza.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ninapenda kuzungumza ni suala la upimaji wa viwanja. Kwa mfano, Serikali inajitahidi sana kutoa huduma kwa wananchi lakini kwa sababu ya ujenzi holela, mimi niko katika kijiji fulani, nimekaa hapa leo ninaamua naona kuna shamba kilometa 10 nakwenda nafyeka najenga kesho namleta Binamu, kesho namleta na Mjomba baadaye unashangaa eneo lile lina watu watano, lina watu kumi, tayari tunaanza kuisumbua Serikali, hamtuletei maji, hamtuletei shule. Sasa inaonekana kwamba Serikali haifanyi kazi lakini kwa sababu tumeshindwa kudhibiti ni namna gani tunaweka matumizi bora ya ardhi hasa katika eneo la makazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hilo Serikali iwekee mkazo mkubwa ili tusiwe na hizi changamoto tunakwenda kukagua miradi ya maji unaambiwa bwana mahali fulani sisi hatujaletewa maji, kwa nini kuna kitongoji fulani tumeanzisha. Kwa hiyo Serikali kwenye hiyo mipango miji iende pengine kwa haraka zaidi itaweza kuisaidia nchi ili mipango ikae vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la umeme. Serikali imefanya vizuri tunaishukuru, katika Jimbo langu la Kalenga nilibakiwa na vijiji vitatu sasa hivi wanavimalizia tunashukuru Serikali. Vipo vitongoji vingi sana ambavyo ni vikubwa katika bajeti hii Serikali sasa ione namna gani tutakwenda kupeleka kwa kasi umeme katika vitongoji ambavyo tayari maombi hayo kwenye TANESCO na REA. REA sasa kwa kuwa wanakwenda kumaliza vijiji, nguvu zaidi waelekeze kwenye vitongoji ili nako tuweze kukamilisha mambo hayo.

Mheshimiwa Spika, naona muda wangu umeisha ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nipate kuchangia katika bajeti hii muhimu ya kilimo. Kwanza nianze kwa kumnukuu mnenaji mmoja maarufu duniani anaitwa John C. Maxwell anasema, “everything rises and falls depending on the leadership.” Kila kitu kinaweza kupanda au kushuka kinategemeana na uongozi. Nchi inaweza kuzama, kampuni inaweza kuzama, Wizara inaweza kuzama kutegemeana na uongozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza Waziri akitoa hotuba zake kuanzia tarehe 4 siku ile wakati anagawa zile pikipiki, alitoa hotuba moja jiwe sana ambayo ilikuwa kwa kweli ni mwongozo. Kama akiweza kuisimamia, ile ni operating model yake ambayo akiitekeleza nchi hii itakwenda kubadilika. sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Rais, kwa kweli nimekuwa nikiwasikia hawa wenzetu wanaitwa wachache wanasema kwamba political will; maana wakizungua mambo yao wanasema, “political will” kwamba tumemwona Rais ana political will kwenye upande wa kilimo. Hivyo nina uhakika kwamba nchi hii kwenye kilimo itakwenda kubadilika kwanza kugawa zile pikipiki karibu 7,000 na sasa kupandisha bajeti kutoka Shilingi bilioni 294 kwenda Shilingi bilioni 754. Hiyo ni political will.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wenzangu ambao walikuwa wanazungumza kwamba ni maneno; haya sasa siyo maneno tena, kwa sababu tayari jambo limeshakuwa kwenye bajeti na bajeti zimeshatoka. Kwa hiyo, tunashukuru. Pia mwaka jana nilichangia kwa habari ya ruzuku na ninamshukuru sana Rais, pamoja na Waziri kwa sababu ya ruzuku ambayo wanakwenda kuweka sasa kwenye mbolea pamoja na mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii inaonesha namna gani tutakwenda ku-transform kilimo cha nchi hii. Kwa hiyo, kwa kweli niseme Mungu awabariki sana na sisi kama watumishi wenu na wafuasi wenu tutaendelea kuhakikisha kwamba tunafanya kazi ili tuwatie moyo katika kutekeleza majukumu yenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumezungumzia habari ya umwagiliaji, nakushukuru Mheshimiwa Waziri kwamba sasa tunakwenda kubadilisha kilimo chetu kwenye umwagiliaji. Bilioni hizo ambazo zimewekwa kwenye kilimo, sasa naomba hata Jimbo la Kalenga lipate kufaidika pamoja na umwagiliaji huu. Kwenye Jimbo la Kalenga tuna scheme zipatazo 19 ndogo ndogo na za kati. Sasa changamoto nyingi tulizonazo kwenye hizi skimu, nyingi ni za kizamani na kienyeji. Kwa hiyo, unakuta kwamba zinahitaji kutengeneza mabanio tu kidogo ambayo ni bajeti ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kueleza skimu zote hapa. Kwa mfano, kuna Skimu ya Weru iliyoko Kata ya Ulanda, wanasema hii ina ukosefu wa banio, kwani iliyopo ni ya kienyeji fedha za kutengeneza banio na kugawa mifereji; kitu kama hicho, ziko kama 19. Kwa hiyo, utatusaidia na sisi tupate bajeti, siyo kubwa, angalau tutengeneze hizi banio ndogo ndogo hata kwenye huu umwagiliaji mdogo mdogo tuweze ku-maximize tuweze kupata mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna skimu nyingine nilikuwa ianze, tulishafanya usanifu katika Kijiji cha Magubike Kata ya Nzi. Shilingi milioni 40 zilishatumika kufanya usanifu, lakini hatukuendelea. Hili tutaliangalia, nafikiri document ninayo hapa, nitakuja tuzungumze kirefu na Mkurugenzi wa Tume ya Umwagiliaji hapo ili tuone tunakwendaje juu ya hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye vyama vya ushirika, ushirika ni nguzo muhimu sana kwenye ukuaji wa uchumi unaokua kwa wakulima. Hata Mwalimu Nyerere wakati fulani alisema, katika mambo ambayo alishawahi kusikitika sana, alisema alisikitika kuuacha ushirika. Tumeona hata wawekezaji wakubwa ambao ninao kule kwenye Jimbo la Kalenga, ambao walikuja katika kulima tumbaku miaka hiyo, walitokea katika ushirika. Kwa hiyo, ushirika ni nguzo muhimu na inaweza kusaidia nchi hii ikaweza kukua kwa sababu watu wakilima katika ushirika ni rahisi sana kuweza kuratibu hata shughuli zao za kilimo lakini shughuli za kimasoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwenye ushirika kumekuwa na changamoto kubwa. Moja ya changamoto ambazo naziona pia kwenye ushirika ni ukosefu wa vifaa. Kwa mfano, hawana magari. Ni ngumu sana kuweza kufanya uratibu (coordination) wa shughuli za kilimo kama hawana vifaa. Kwa hiyo, Serikali ione namna gani itafanya kuimarisha ushirika kuhakikisha kwamba inawapa vitendea kazi, hasa magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Afisa Ushirika wengi wako chini ya Halmashauri. Sasa napendekeza hawa Maafisa Ushirika wahame kwenye Halmashauri, wawe chini ya Wizara ya Kilimo ili sasa Waziri wa Kilimo awe na nguvu ya kuweza kuwaamuru. Tuliona kwenye ardhi, Waziri wa Ardhi wa wakati huo alihamisha Maafisa Ardhi wakaenda kwenye Wizara ya Kilimo na tumeona ufanisi. Kwa hiyo, na kwenye ushirika tufanye hivyo hivyo, vinginevyo line of reporting zinakuwa nyingi. Kwa hiyo, hakuna mtu mwenye nguvu wa kuweza kuwasimamia. Hili tuliangalie sana ili kama tunataka tukuze kilimo chetu kiweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanzisha Kituo cha Afya ya Mimea pale Arusha. Tunaishukuru Serikali, sasa tunaweza kutoa ithibati; tumepata ithibati ambayo inaturuhusu sisi tuuze mazao yetu kwenye nchi zinazotuzunguka. Sasa changamoto ambayo naiona pale ni kwamba tuna mashine ambazo tulipewa za msaada, mashine moja moja; sasa Serikali ione umuhimu wa kuhakikisha kwamba tunanunua mashine nyingine ili sasa kama hii inaharibika, basi tunakuwa na mashine nyingine za kuweza kuendelea kukagua mazao yetu na kuendelea kuyapa ubora unaotakiwa ili tuweze kuuza nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lingine ambalo nimeliona, hatuna wataalam. Mara nyingi mitambo ikiharibika tunaleta wataalam kutoka nje na gharama za kuwalipa hawa ni kubwa sana. Kwa hiyo, Serikali ione umuhimu wa kupeleka vijana wetu wakajifundishe huko nje ili waje wahudumie hizi mashine zetu, tusiingize hizi gharama za kuleta wataalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye suala lingine ni kwenye maghala. Nilishalizungumza suala la maghala kwenye viwanda, lakini huku nitalizungumza katika mtizamo mwingine. Maghala yatatusaidia sana. Kwanza tumekuwa na tatizo la sumukuvu kubwa sana katika nchi hii na ukiangalia mazao yanavyohifadhiwa katika maeneo yetu mara nyingi wanamwaga chini ardhini, lakini tutakapokuwa na maghala mpaka kwenye vijiji kama Waziri alivyozungumza, yatasaidia sana kwanza kutunza ubora, na pia kudhibiti upotevu wa mazao. Tuna asilimia karibu 30 mpaka 40 ya mazao yetu yanayopotea. Kwa hiyo, tukiwa na haya maghala itasaidia sana kuratibu na pia kuwa na mazao yenye ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kwenye hili atafute pesa, aidha anakopa; hapo ni mahali pazuri pa kuanzia. Hapo utatengeneza alama, utawasaidia Watanzania kupata masoko na utaweza kuratibu mazao yanayozalishwa katika nchi hii na kuwatafutia masoko.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naona kengele imeshagongwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Muswada huu muhimu wa Marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Maji. Nami kama Mjumbe wa Kamati ya Maji, kwanza naunga mkono marekebisho ya sheria ambayo yanakwenda kufanywa na pia naunga mkono taarifa ya Kamati ambayo imemaliza kuwasilishwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza pia kwa kumnukuu Ismail Serageldin huyu mimi namwita ni Balozi wa masuala ya maji duniani. Amekuwa ni sauti kubwa sana kuzungumzia masuala ya maji na namna gani tunaweza tukatunza maji kwa ajili ya vizazi vijavyo. Yeye katika moja wa mkutano wake mwaka 1995 alisema “if the wars of this century were fought over oil, the wars of the next century will be fought over the water.” Anasema kwamba kama vita vya dunia vya karne hii ambayo inamalizika vilipiganwa kwa sababu ya mafuta, pengine na dhahabu na mali nyingine za thamani duniani, anasema kwamba karne inayokuja, vita kubwa duniani itahusisha masuala ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inakadiriwa kwamba kuna watu wapatao milioni kama 400 walio Kusini mwa Jangwa la Sahara ambao wana changamoto kubwa ya kukosa maji. Sababu zimeelezwa zinaeleweka kwamba dunia imeongezeka sana watu, shughuli za kibinadamu zimeongezeka sana, kwa hiyo, inakuwa sasa suala hili ni la lazima hasa kwa nchi yetu kama Tanzania ambayo bado haijapata majanga makubwa kama ambayo yanapatikana katika nchi nyingine ambazo tayari zimeanza kuwa kame kwa sababu zilishindwa kutunza hivi vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Watanzani ni lazima tuchukue hatua sasa kuhakikisha kwamba tunatunga sheria ambazo zitatoa mamlaka kubwa kwa hawa wasimamizi wa mabonde kuweza kusimamia rasilimali za maji kwa ajili yetu sisi wenyewe na kwa ajili ya vizazi vijavyo. Kwa hiyo, ni muhimu sana hili jambo tukaweza kuliangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inaipatia mamlaka za mabonde ya maji; kwanza, kuwa na udhibiti kwenye matumizi ya maji, kwa maana ya kwamba, hata kama mtu anahitaji kuchimba kisima mahali popote, anahitaji apewe kibali. Hiki kibali kitamwelekeza kitaalamu ni nini afanye. Kwa sababu tumeona sehemu nyingi kwamba watu wanachimba maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu kinyume na sheria; na maji haya wakati mwingine wanachimba pengine hawafikii kile kiwango kinachotakiwa na hivyo kusababisha yale maji yawe machafu, yawe na wadudu na kuathiri pia afya za watumiaji. Kwa hiyo, sheria hii ambayo tunaileta sasa itakwenda kuzipa mamlaka za mabonde ya maji, kusimamia hata wale ambao wanachimba visima vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kushauri kwamba kwa kuwa sasa haya mabonde tunaenda kuyapatia nguvu ya kisheria, ni lazima pia wafanye mapitio ya visima vyote ambavyo vimechimbwa katika nchi hii na vinavyotumika, kama vimechimbwa kwa viwango ambavyo vitamsaidia Mtanzania kuwa na afya anapotumia hayo maji. Kwa hiyo, wasimamie hata kule ambako tayari visima vilishachimbwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunapokwenda kutunga sheria hii na kuongeza usimamizi mkali kwenye vyanzo vyetu na maeneo tengefu, maana yake, kuna watu ambao wanakwenda kuathirika. Wengi ambao walikuwa wanalima katika maeneo ya mabonde, wataathirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua hizi sheria zinapokuja kuna mmoja atafaidika na mmoja ataumia. Wale ambao wanalima kwenye maeneo ya mabonde, wanakwenda kuumia kidogo. Sasa mapendekezo yangu ni kwamba pamoja na kusimamia hizi rasilimali za maji, ni lazima pia Wizara ijikite sana katika kuendeleza na kuanzisha maeneo mapya. Kwa mfano, kama tutakwenda kutengeneza mabwawa ambayo yanatokana na kudaka yale maji yanayotokana na mvua; kwa mfano sasa Wizara ya Maji imeshaanza kutengeneza mabwawa, yale maeneo ya mabonde ambayo ni njia kubwa za maji, tukienda kujenga yale maeneo tukatengeneza hivi vidakio, tukatengeneza mabwawa, tutasaidia wananchi wengi ambao tutaweza sasa kuwatoa kwenye mabonde kwa sababu sheria hii itawabana, maana yake tunawapa jambo lingine ambalo ni mbadala. Kwa hiyo, hilo nalo ni jambo la kulizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni namna gani pia sheria hii itakwenda kutekelezwa kwa wepesi? Ni muhimu sana tukaunda jumuiya kwenye vijiji na maeneo haya yenye vyanzo vya maji na maeneo tengefu. Tuwe na jumuiya za wasimamizi wa mabonde kwenye haya maeneo ili sasa kiwe ndiyo chombo ambacho kitakwenda kusaidia kutoa elimu kwa wananchi. Maana kama mamlaka yenyewe ina watu wachache, sasa kama tutatengeneza hizi jumuiya kwenye vijiji, kwenye hivi vyanzo vya maji na kwenye maeneo haya tengefu, itasaidia hii elimu ifike kwa haraka. Kwa hiyo Wizara na mamlaka hizi za mabonde ya maji zijikite sana katika kutoa elimu kwa kutumia hizi jumuiya ambazo tutaenda kuziunda kwenye haya maeneo ya vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tuangalie pia, kumekuwa na uharibifu wa maji kwa ujumla, kwa sababu sheria hii pia inazungumzia uchafuzi wa maji. Tuangalie ni namna gani tunaweza kushirikiana na Wizara nyingine na mamlaka nyingine. Tumeona hivi karibuni kwamba kwenye maeneo ya maziwa na bahari, ni kwamba watu wamekuwa wakijenga, yaani pembezoni kabisa, wengine wanaingia mpaka ndani ya maji. Sasa hii sheria sijui itafanyaje kwa sababu naliona hili pia ni aidha ni uchavuzi wa maji na pia inaweza ikaleta diversion kwenye haya maji na baadaye inaweza kuleta shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona huko duniani, iko bahari moja ilishawahi kukauka. Profesa Muhongo alishatuambia, miaka 400 iliyopita kuna bahari moja ilishawahi kukauka kwa sababu ya matumizi mabaya ya maji. Sasa tunafanyaje kushirikisha hizi mamlaka nyingine? Watu wanaojenga mpaka kwenye haya maziwa ndani, hilo nalo tuangalie namna gani tutashirikisha mamlaka nyingine kuhakikisha kwamba hata haya maji yanatunzwa kwa ajili ya vizazi vingine vijavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye sheria hii nilitaka tu kuweka muhuri kwamba ninaunga mkono mabadiliko ya sheria hii na kwamba Bunge zima tuiunge mkono kwa sababu tutakwenda kuilinda nchi; na nchi hii itakuwa ni ya kutamaniwa na itaweza kuwa endelevu, hata vizazi vingine vitakavyokuja baadaye vitakuta mazingira yametunzwa na tutaendelea kupata uchumi unaotokana na vyanzo vya maji. Kama tutakuwa na vyazo vya maji ambavyo vimeendelezwa, itakuwa ni source nyingine ya uchumi kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeki, kwa hiyo, naunga mkono hoja hii kwa mikono yote miwili kwamba ipite ili nchi hii tuitunze kwa ajili yetu na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)