Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Exaud Silaoneka Kigahe (92 total)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa kumpata mwekezaji katika Shamba la Chai la Kidabaga?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile nami ni mara ya kwanza leo kusimama katika Bunge lako Tukufu, naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema ambaye ametujalia mema mengi. Pili, nakishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniamini na kunipa nafasi kuwakilisha katika Jimbo la Mufindi Kaskazini. Tatu, nawashukuru wananchi wenzangu wa Jimbo la Mufindi Kaskazini ambao waliniamini na kunipa kura nyingi ili niweze kuwa mtumishi wao. Mwisho, kwa niaba ya familia yangu, nawashukuru sana, lakini kwa namna ya pekee mke wangu kwa kunipa ushirikiano ili niweze kuendelea kutekeleza majukumu yangu ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kumpata mwekezaji mahiri katika Kiwanda cha Chai cha Kidabaga. Maandalizi ya kumpata mwekezaji huyo yameanza ikiwa ni pamoja na kukamilishwa kwa Andiko linalohusu Viwanda 17 vilivyokuwa vimebinafsishwa lakini baadaye kurejeshwa Serikalini, kikiwemo Kiwanda cha Kidabaga.

Mheshimiwa Naibu Spika, andiko hilo kwa namna ya pekee kuhusu Kidabaga linajumuisha mapendekezo ya muundo mpya wa uendeshaji wa kampuni utakaozingatia maslahi ya wakulima wa chai wa Kidabaga na kwa Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara inaandaa Waraka wa Baraza la Mawaziri kwa ajili ya viwanda vilivyorejeshwa Serikalini ikiwa ni pamoja na Kiwanda cha Chai cha Kidabaga. Hivyo, Serikali itakamilisha mchakato huo mapema iwezekanavyo ili mwekezaji mahiri aweze kupatikana kwa ajili ya kuwekeza katika shamba hilo la Kidabaga.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawalipa wakulima wa tangawizi Mamba Myamba, Wilaya ya Same Mashariki ambao walifungiwa na SIDO mashine zisizo na kiwango cha kuchakata tangawizi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirika wa Wakulima wa Mamba Myamba uliopo Wilaya ya Same, tarehe 21/05/2010 uliwapa SIDO kazi ya kutengeneza mtambo wa kuchakata tangawizi kupitia Halmashauri ya Same ambao ulikuwa unahusisha hatua tano za uchakataji ambazo ni kuosha, kukata, kukausha, kusaga na kufungasha. SIDO iliingia mkataba na Halmashauri ya Same na Chama cha Ushirika cha Msingi cha Mazao na Masoko. Mradi huo ulikuwa na thamani ya shilingi 88,895,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtambo huo ulikamilika na kulisimikwa tarehe 29/10/2012 na ulifanya kazi. Hata hivyo katika ufanyaji kazi wake kulikuwa na changamoto mbalimbali ambazo baadaye zilirkebishwa na mtambo huo tena kusimikwa upya tarehe 27/2/2015.

Aidha, SIDO ilinunua tangawizi kutoka kwa wakulima na kufanya majaribio katika mtambo huo ambao ulionekana kufanya kazi vizuri. Mpaka sasa mtambo huo unaendelea kufanya kazi vizuri na wana ushirika wanaendelea na shughuli zao za uchakataji wa zao la tangawizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mkataba ulioingiwa na SIDO, majukumu ya SIDO yalikuwa ni kutengeneza na kufunga mtambo kazi ambayo ilikamilika. Hata hivyo, baada ya changamoto zilizojitokeza Serikali imeielekeza SIDO ishauriane na Halmashauri ya Same namna bora ya kutatua changamoto ambazo zimejitokeza kwa kushirikiana na Ushirika wa Mamba Myamba ili kuona changamoto walizonazo zinatatuliwa.
MHE. TUNZA I. MALAPO Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafufua viwanda vyote vya kubangua Korosho vilivyopo Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kabla ya zoezi la Ubinafsishaji, Serikali ilikuwa na jumla ya viwanda 12 vya kubangua korosho nchini. Kati ya viwanda hivyo viwanda viwili vilikuwa katika Manispaa ya Mtwara. Hiki ni kile kilichokuwa kinajulikana kama Likombe Cashew Factory na hivi sasa ni Micronics Systems Company Limited; na kile kilichokuwa kinaitwa Mtwara Cashew Company Limited, sasa hivi ni Cashew Company (2005) Limited.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi vyote viwili vinafanya kazi. Kiwanda cha Micronics Systems Company Limited kina uwezo uliosimikwa wa kubangua korosho tani 5,000 kwa mwaka. Hata, hivyo kutokana na changamoto ya malighafi kiwanda hicho kinabangua wastani wa tani 2,000 kwa mwaka. Pia Kiwanda cha Mtwara Cashew Company Limited kinaendelea na uzalishaji katika kutoa huduma za kupanga madaraja (grading) na kufungasha (packaging) kwa korosho zinazobanguliwa na viwanda vidogo vilivyopo katika maeneo hayo ambavyo havina mitambo ya grading na packaging.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuvutia uwekezaji na kuwezesha sekta binafsi kuwekeza katika viwanda vipya na kufufua viwanda vilivyopo vya kubangua korosho hapa nchini.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutafuta soko la uhakika la matunda ndani na nje ya nchi pamoja na kuanzisha viwanda vya kusindika matunda ili kufanya kilimo cha matunda kuwa chenye tija?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa utafutaji masoko ya ndani na nje kwa mazao na bidhaa mbalimbali, ikiwemo masoko ya matunda ni jukumu endelevu. Utekelezaji wa jukumu hilo huhusisha taasisi zetu kama TanTrade, Balozi za Tanzania nje ya nchi, Bodi za mazao, Soko la Bidhaa za Mazao na sekta binafsi. Lengo la kutumia balozi zetu nje ni kupata taarifa za kina kuhusu mahitaji ya masoko ya mazao na bidhaa za Tanzania katika nchi husika.

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Serikali katika kutafuta masoko unahusisha uhamasishaji wawekezaji wa ndani na nje kujenga viwanda vidogo, vya kati na vikubwa kupitia taasisi zetu za uwekezaji TIC, EPZA, Balozi zetu nje pamoja na Serikali ngazi za Wilaya na Mikoa. Uhamasishaji huo unaenda sambamba na kutoa vivutio vya kikodi na visivyo vya kikodi kupitia sheria za uwekezaji pamoja na zile za Uendelezaji Maeneo Maalum ya Uwekezaji yaani EPZ na SEZ. Aidha, Serikali kupitia Taasisi za SIDO, NDC na EPZA inaendelea kutoa ushauri wa namna ya kuanzisha viwanda vidogo, vya kati na vikubwa vya aina mbalimbali ikiwemo vya kusindika matunda na kuvilea ili viweze kukua na kuweza kuwa soko kwa matunda yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, Juhudi za Serikali ni kuhamasisha uanzishaji wa viwanda na ambapo juhudi hizo zimezaa matunda ambapo kwa sasa kuna viwanda viwili vikubwa vya kusindika matunda katika Wilaya ya Bagamoyo ikiwa ni vya Elven Agri Co. Ltd na Sayona Fruits Co. Ltd vyenye uwezo wa kusindika tani 28 za matunda kwa siku na kuajiri jumla ya wafanyakazi 755.

Mheshimiwa Spika, viwanda hivyo hutoa soko la uhakika la matunda kwa wakulima mbalimbali hapa nchini. Aidha, ili kuwa na uhakika wa malighafi za kutosha kwa mwaka mzima, tunashauri Mheshimiwa Mbunge kuendelea kushirikiana na Serikali kuhamasisha uzalishaji wa aina mbalimbali za matunda yatakayotumika katika viwanda hivyo ili viwanda hivyo viweze kupata malighafi za uhakika kwa kipindi kirefu.
MHE. LUCY J. SABU Aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa kiwanda cha vifaa tiba vinavyotokana na zao la pamba Mkoani Simiyu utaanza kwa kuwa upembuzi yakinifu ulishafanyika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya viwanda vya dawa hapa nchini ina jumla ya viwanda 17 ambapo viwanda 12 vinatengeneza dawa za binadamu, viwanda viwili vinatengeneza vifaa kinga na viwanda viwili vinatengeneza dawa za mifugo na kimoja vifaa tiba. Viwanda 17 hivyo vinauwezo wa kuzalisha dawa chini ya asilimia 12 tu ya dawa zote zinazohitajika nchini. Hivyo zaidi ya asilimia 88 ya dawa za binadamu zinazotumika zinaagizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mkakati na mbinu za makusudi kuwezesha uwekezaji wa viwanda vya dawa vilivyopo na kuongeza ufanisi ili kufikia asilimia 60 ya uzalishaji wa dawa na vifaa tiba hapa nchini ifikapo mwaka 2025. Mikakati na mbinu hizo inahusisha pia kuongeza idadi ya viwanda vya vifaa tiba nchini. Aidha, Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwenye sekta hiyo ili kuvutia wawekezaji wengine katika sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada hizo, kuna umuhimu pia wa kuanzisha Kiwanda cha Vifaa Tiba Simiyu ambapo malighafi ya pamba inayolimwa kwa wingi nchini itatumika. Taratibu zote za kuanzisha kiwanda husika zimekamilika ikiwa ni pamoja na upembuzi yakinifu kama alivyobainisha Mheshimiwa Lucy John Sabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa kiwanda hicho unategemea kuanza mara tu baada ya Serikali kukamilisha utaratibu bora wa kugharamia mradi huo. Nashukuru.
MHE. JULIANA D. MASABURI Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Kiwanda cha MUTEX kilichopo Wilaya ya Musoma Mjini kinafunguliwa na kurudisha ajira kwa vijana wa Mkoa wa Mara?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Didas Masaburi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ina jumla ya viwanda 12 vya nguo na mavazi na viwanda vitatu kati ya viwanda hivyo havifanyi kazi ikiwemo Kiwanda cha Musoma Textiles.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha MUTEX ni moja kati ya viwanda vilivyobinafsishwa na Serikali kwa wawekezaji kwa lengo la kuviendeleleza ili viweze kukuza sekta ndogo ya nguo na mavazi, kutoa ajira kwa wananchi, kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi na kuleta ustawi kwa jamii. Kiwanda hiki kimekuwa kinafanya kazi kwa kusuasua na mara kadhaa kimesimamisha uzalishaji. Kiwanda cha MUTEX ni moja kati ya viwanda 20 ambavyo vimerejeshwa Serikalini baada ya wawekezaji wa awali kushindwa kuviendeleza na kukiuka masharti ya mkataba.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhamira ya dhati ya Serikali ni kuona viwanda hivyo vinafanya kazi kwa tija na ufanisi mkubwa ili kuongeza ajira kwa ajili ya maendeleo ya watu, kuchochea shughuli za kiuchumi, na kuongeza mapato ya ndani ya nchi. Serikali imeshatoa Tamko la kuvitafutia wawekezaji wapya wa kuviendeleza kwa tija viwanda vyote vilivyorejeshwa Serikalini ili vilete manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla. Ni matumaini ya Serikali, kuona kuwa wawekezaji makini watajitokeza kwa lengo la kutumia fursa hii adhimu kuwekeza katika viwanda hivi. Serikali inaandaa utaratibu maalum utakaowezesha kupatikana wawekezaji wapya kwa njia ya zabuni ya kiushindani na wazi kwa kuzingatia vigezo vitakavyowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kuwakaribisha wawekezaji wenye nia na uwezo wa kuwekeza katika Kiwanda cha MUTEX na viwanda vingine vilivyorejeshwa Serikalini kuwasilisha maombi yao mara baada ya utaratibu utakapotangazwa rasmi. Nashukuru.
MHE. SOPHIA H. MWAKANGENDA aliuliza:-

Je, ni kwa nini wananchi wa Wilaya ya Rungwe wanalazimishwa kuuza chai na maziwa kwa mnunuzi mmoja hali inayosababisha mnunuzi kupanga bei kitu ambacho ni kinyume na Sera ya Ushindani wa Biashara?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kifungu cha 10(1) cha Sheria ya Ushindani ya Mwaka 2003, uwepo wa mnunuzi mmoja katika soko siyo kosa, kosa ni endapo mnunuzi huyo atatumia nguvu ya hodhi ya soko aliyonayo katika kufupisha ushindani kwa kuzuia washindani wengine waliopo sokoni kufanya biashara. Kufifisha ushindani kwa kuwaondoa washindani wengine waliopo sokoni na kufifisha ushindani kwa kuzuia makampuni au watu wengine kuingia kwenye soko husika.

Mheshimiwa Spika, iwapo itathibitika kuwa kuna kosa la kupanga bei ya huduma au bidhaa Tume ya Ushindani kwa maana ya FCC kuchukua hatua kwa kutumia Kifungu Namba 9 cha Sheria ya Ushindani. Kwa mujibu wa Kifungu hiki ili kosa husika lifanyike ni lazima kuwe na washindani katika soko, ambapo washindani hawa hukutana na kupanga bei ya bidhaa au huduma wanayotoa au kupanga kiasi cha kuzalisha au kugoma kusambaza bidhaa na huduma husika au kupanga zabuni.

Mheshimiwa Spika, hivyo Wizara kupitia FCC inafanya uchunguzi wa suala hili ili kubaini uwezekano wa kuwepo kwa uvunjifu wa Sheria ya Ushindani. Katika hatua za awali za uchunguzi FCC imeshawasiliana na Bodi ya Chai Tanzania, Bodi ya Maziwa Tanzania na Ofisi ya Katibu Tawala, Mkoa wa Mbeya ili kupata taarifa muhimu kwa ajili ya kujiridhisha kuhusu changamoto hii katika soko la chai na maziwa Wilayani Rungwe. Ikiwa itabainika kuwa kuna uvunjifu wa sheria ya ushindani, hatua stahiki zitachukuliwa dhidi ya wahusika.

Mheshimiwa Spika, nipende kutumia fursa hii kuwajulisha wafanyabiashara wote nchini kuzingatia sheria zilizowekwa ili kuwa na ushindani wa haki katika soko.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kiwanda cha Mbolea katika Mji wa Kilwa Masoko kitakachotumia malighafi inayotokana na gesi asilia ya Songosongo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mpango wa Matumizi ya Gesi Asilia kwa maana Gas Utilization Master Plan imepanga kutumia kiasi cha futi za ujazo trilioni 0.7 za gesi asilia kwa uzalishaji wa Mbolea. Utafiti unaonesha kuwa Tanzania ina kiasi cha akiba ya gesi asilia kilichogunduliwa na kuthibitishwa takribani futi za ujazo trilioni 57. Hazina hii ya gesi tuliyonayo kwa sasa katika visima vyetu vya gesi asilia inatosha kwa matumizi ya viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na kiwanda cha mbolea kwa kutumia malighafi ya Gesi Asilia. Hivyo, Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC) na TPDC, Tume imeendelea na juhudi za kupata wawekezaji kwa ajili ya kuwekeza kwenye viwanda vya mbolea. Hapo awali Serikali iliwahi kufanya majadiliano na kampuni ya Ferrostaal na Helm kutoka Ujerumani. Serikali imeendelea kufanya majadiliano na wawekezaji wengine akiwemo Dangote, Elsewedy kutoka Misri na Minjingu Mines Limited ambao wameonesha nia ya kufanya uwekezaji huo.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC), TPDC, PURA, EWURA na Wizara inaharakisha kukamilisha majadiliano hayo na hatimaye kupata wawekezaji wenye uwezo wa kujenga viwanda vya mbolea kwa lengo la kumaliza tatizo kubwa la uagizaji mbolea nje ya nchi. Pindi majadiliano hayo yatakapokamilika ni imani ya Serikali kuwa ujenzi wa kiwanda hicho utaanza mara moja. Nakushukuru.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-

Je, Serikali imeweka mkakati gani wa kuanzisha viwanda vya dawa na vifaa tiba hapa nchini ili kuacha na kuagiza vifaa hivyo nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Jimbo la Singida Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Viwanda vya Dawa na Vifaa Tiba ina jumla ya viwanda 14 ambapo viwanda 12 vinatengeneza dawa za binadamu viwanda viwili dawa za mifugo; na kiwanda kimoja kinatengeneza Vifaa Tiba. Wizara imeendelea kuchukua hatua za makusudi ili kuhakikisha Sekta hiyo inaongeza uwekezaji kwenye Viwanda vya Dawa na Vifaa Tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hiyo inakwenda sambamba na kuongeza ufanisi wa viwanda vilivyopo ili kufikia asilimia 60 ya uwezo wa uzalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini ifikapo mwaka 2025. Hatua hizo ni pamoja na kuunda Kamati ya Kitaifa inayoshughulikia Sekta ya Viwanda vya Dawa na Vifaa Tiba (National Pharmaceutical Coordination Committee - NPCC); na kuweka vivutio vya uwekezaji kwa lengo la kuhamasisha wawekezaji wa ndani na Nje ya Nchi ili kuwekeza katika sekta hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ili kuvutia wawekezaji katika sekta hiyo, Serikali imeondoa VAT kwenye vifungashio vya dawa zinazozalishwa nje na ndani ya nchi; imeshusha kodi ya mapato kwa asilimia 30 ambayo imesaidia kuhamasisha uwekezaji mpya na upanuzi wa viwanda kwa muda wa miaka miwili kwa miradi mipya ya viwanda vya dawa na kuweka upendeleo maalum kwa ununuzi wa dawa zinazozalishwa na viwanda vya ndani kupitia MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imeendelea kufuatilia uwekezaji na ambapo sasa hivi kuna viwanda 11 vinavyoendelea na ujenzi wa Viwanda vya Dawa na Vifaa Tiba na ujenzi umefikia katika hatua mbalimbali. Lengo la Serikali ni kuokoa fedha zinazotumika kuagiza dawa na vifaa tiba hivyo kutoka nje ya nchi kwa kuzalisha na kuwezesha upatikanaji wa uhakika wa dawa hizo nchini na hivyo kuendelea kutengeneza ajira hapa nchini. Aidha, lengo hilo linakusudia kuhakikisha afya za Watanzania zinakuwa ni suala la kipaumbele wakati wowote.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza: -

Maeneo ya wananchi wa Kata ya Zinga, Kitongoji cha Mlingotini na Pande, yalichukuliwa na Serikali ili kupisha Mradi wa EPZ lakini hawajalipwa fidia:-

Je, ni lini wananchi hao watalipwa fidia?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Muharami Shabani Mkenge, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Bagamoyo Special Economic Zone ni moja ya miradi wa kielelezo na kimkakati ambao umepewa kipaumbele nchini na umeainishwa katika Mpango wa Miaka Mitano wa Kwanza, wa Pili na wa Tatu na katika Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mradi huo, Serikali ilichukua hatua mbalimbali za uendelezaji ikiwemo kulipa fidia kwa baadhi ya watu waliopisha mradi kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo lilifanyiwa tathmini ni hekta 5,743 ambazo fidia ilikuwa ilipwe jumla ya bilioni 58.5 na katika hekta hizo zilizolipwa fidia ni hekta 2,339.6 ambazo jumla ya fidia iliyolipwa ni takriban bilioni 26.6. Serikali inatambua uwepo wa maeneo yanayodaiwa fidia katika eneo maalum la kiuchumi la Bagamoyo yakiwemo maeneo yaliyoko katika Vitongoji vya Mlingotini na Pande katika Kata ya Zinga, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza azma ya ujenzi wa uchumi wa viwanda, Serikali inaendelea kuangalia namna bora zaidi ya utwaaji wa maeneo ya namna hii na kuweka utaratibu wa fidia wenye kuleta tija ya uwekezaji kwa Taifa kwa ujumla. Taratibu hizo zitahusisha ulipaji wa fidia kwa maeneo yaliyotathminiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali na fidia hufanywa kwa mujibu wa Sheria. Pia utaratibu huo unalenga kuyamiliki na kuyaendeleza maeneo hayo ili yawe na tija kwa Taifa letu. Hivyo, fidia kwa wananchi ambao bado wanadai katika eneo hilo la Mlingotini na Pande itafanyika kwa kuzingatia utaratibu hu una Serikali italipa wadai hao haraka iwezekanavyo.
MHE. IRENE A. NDYAMKAMA aliuliza:-

Je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kuendeleza kilimo cha zao la miwa kwa Wananchi wa Wilaya ya Kalambo na Nkasi na baadae kujenga kiwanda cha sukari ambacho kitatoa ajira kwa Vijana na Wanawake ndani ya Mkoa wa Rukwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Irene Alex Ndyamkama, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sukari ni kati ya bidhaa muhimu sana nchini na matumizi yake kwa maana ya majumbani na viwandani. Kwa sasa Tanzania ina uwezo wa kuzalisha wastani wa tani 320,000 kwa mwaka kwa ajili ya matumizi ya majumbani na wakati mahitaji halisi tani 485,000 na mahitaji ya sukari kwa matumizi ya viwandani ni tani 145,000. Pengo la takriban tani 165,000 kwa ajili ya matumizi ya majumbani na tani 145,000 kwa matumizi ya viwandani huagizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua ongezeko la mahitaji ya sukari lisiloendana na uwezo wa uzalishaji wa sukari nchini, Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika miradi mipya na upanuzi ya uzalishaji wa mashamba ya miwa uzalishaji katika viwanda vya sukari ikiwemo viwanda vikubwa na vidogo vilivyopo nchini. Mwaka 2015, Bodi ya Sukari Tanzania ilifanya utafiti na kubaini uwepo wa maeneo yanayofaa kwa ajili ya wakulima wadogo na wa kati kwa ajili ya kilimo cha miwa na hatimaye tuweze kuongeza uzalishaji wa sukari. Aidha, Mkoa wa Rukwa ulibainisha maeneo kwa ajili ya uwekezaji wa kilimo na viwanda ili tukipata wawekezaji katika sekta ya sukari waweze kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kitabu cha Mwongozo wa Uwekezaji cha Mkoa wa Rukwa, Mkoa umetenga jumla ya hekta 20 na hekta 15.65 katika Wilaya ya Kalambo na Nkasi Mtawalia kwa ajili ya uwekezaji wa kilimo cha miwa. Hivyo, Serikali inaendelea kuhamasisha kilimo cha zao la miwa katika maeneo yote yenye sifa za uzalishaji ikiwemo Wilaya ya Kalambo na Nkasi. Pia tunaendelea kuhamasisha kujenga viwanda kwa ajili ya kuchakata miwa ili kukidhi mahitaji ya sukari na pia kutoa ajira kwa Watanzania. Vile vile, Serikali kupitia Bodi ya Sukari inawahamasisha wawekezaji wakubwa na wadogo kuzalisha sukari ili kukidhi mahitaji yaliyopo hapa nchini.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani kupitia SIDO kutengeneza mashine zitakazosaidia kuchakata mazao ya Wakulima, kama vile mashine ya kutengeneza chips za ndizi, muhogo, sauce za nyama, karoti, pilipilihoho na mbogamboga kwa gharama nafuu?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali ni kuendeleza viwanda hususan viwanda vidogo sana na viwanda vidogo vinavyolenga kuongeza thamani ya mazao ya kilimo. Serikali imeendelea kulijengea uwezo Shirika la kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) ili kubuni na kuendeleza teknolojia mbalimbali kutokana na mahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) lina Vituo vya Uendelezaji Teknolojia (Technology Development Centres) katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Kigoma, Lindi, Iringa, Mbeya na Shinyanga kwa ajili ya kutengeneza mashine za kuchakata na kusindika mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mashine hizo ni pamoja na za kutengenza chipsi za ndizi, chipsi za viazi na muhogo, mashine za kukausha mboga mboga na matunda mashine za kusindika nyanya, karoti na mashine kusindika pilipili kwa ajili ya achali kulingana na mahitaji. Aidha, mashine mbalimbali zinazotengenezwa na shirika la kuhudumia viwanda vidogo SIDO zinapatikana katika tovuti ya SIDO na husambazwa katika Mikoa yote ya Tanzania Bara kupitia ofisi za SIDO.

Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya SIDO kutengeneza mashine hizo pia imekuwa ikitoa mafunzo ya usindikaji wa muhogo, ndizi, nyanya, karoti, pilipili na mbogamboga katika Mikoa yote ya Tanzania Bara. Bei za mashine hizo hutegemea na uwezo wa mashine yenyewe kwa maana ya capacity na pia mahitaji halisi ya mjasiriamali.

Mheshimiwa Naibu Spika, SIDO imeendelea kutafuta teknolojia mbalimbali za kisasa na nafuu ndani na nje ya nchi hii, ambazo zinaweza kutumika kutengeneza mashine kulingana na mahitaji ya wajasiriamali. Vile vile SIDO inasimika mitambo ya kisasa yenye uwezo wa kutengeneza mashine kwa wingi na huisambaza kwa wajasiriamali kwa gharama nafuu kwenye vituo vya kuendelezea teknolojia katika Mikoa ya Kigoma, Lindi na Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanikisha hili katika mwaka huu wa fedha tunaoendelea nao, Serikali imeweza kuliwezesha SIDO zaidi ya bilioni nne kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo kwa ajili ya wajasiriamali ikiwemo maendeleo ya teknolojia na ujenzi wa majengo ya viwanda vya wajasiriamali wadogo. Naomba kutoa wito kwa wananchi wenye uhitaji wa mashine za kuchakata na kusindika mazao ya kilimo wakiwemo wananchi wa Jimbo la Vunjo, kuwasiliana au kuwasilisha mahitaji yao kwenye Ofisi zetu za SIDO zilizopo katika Mikoa yote ya Tanzania Bara.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge wote kuwahamasisha wajasiriamali kwenye maeneo yetu kutumia fursa zilizopo za uwepo wa vituo vya kuendeleza teknolojia yaani TDC vya SIDO ili kujinufaisha kiuchumi.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA aliuliza:-

(a) Je, Serikali inawatumia vipi wanafunzi wanaohitimu Shahada ya Science in Industrial Engineering Management katika Uchumi huu wa kati wa Viwanda?

(b) Je, ni wanafunzi wangapi waliohitimu katika fani hiyo wameajiriwa Serikalini tangu mwaka 2019 hadi 2020?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Shahada ya Sayansi katika Menejimenti ya Uhandisi wa Viwanda (Bachelor of Science in Industrial Engineering Management), ilianzishwa mwaka 2015/2016 katika Chuo Kikuu cha Mzumbe. Shahada hiyo ilianzishwa ikilenga kuzalisha wataalam wa kusimamia shughuli za uzalishaji katika viwanda ambavyo vinamilikiwa na Serikali na vile vya mashirika na makampuni binafsi.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017/2018 mpaka 2019/2020, wahitimu wengi katika fani hiyo wameajiriwa katika sekta binafsi hususan katika viwanda vya kuzalisha bidhaa kama vile viwanda vya saruji, vinywaji, nguo, sukari, vyakula, mbao, vifungashio, mafuta na kadhalika na katika uchimbaji wa madini. Pia, wahitimu hao wameajiriwa katika taasisi za Serikali zinazoshughulikia masuala ya ubora kwa mfano Shirika la Viwango Tanzania - TBS, Shirika la Utafiti wa Maendeleo ya Viwanda-TIRDO, Chuo Kikuu cha Mzumbe, Taasisi ya Uhandisi na Usanifu wa Mitambo -TEMDO, huduma za viwanda vidogo Vidogo-SIDO na mengineyo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali yetu inatekeleza azma ya ujenzi wa viwanda, yaani uchumi unaoongozwa na viwanda, wahitimu katika fani hiyo walioajiriwa wanatumika katika usimamizi wa shughuli mbalimbali za viwanda vilivyopo katika sekta ya umma na sekta binafsi na hivyo kuleta tija katika uzalishaji na uendeshaji wa taasisi za umma na za binafsi.

(b) Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017/2018 mpaka 2019/2020 jumla ya wahitimu wa shahada hiyo walikuwa 228. Kati ya hao, wahitimu 55 walipata ajira. Aidha, kati ya hao 55 waliopata ajira, katika mashirika na taasisi za Serikali ni wahitimu saba.
MHE. HAMIS M. MWINJUMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha kuwa kunajengwa Kiwanda cha Kuchakata Viungo Wilayani Muheza?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamis Mohamed Mwinjuma, Mbunge wa Jimbo la Muheza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa viwanda katika kuchangia ukuaji wa uchumi nchini, Serikali imeendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa Sekta Binafsi ili iweze kuanzisha na kuendeleza shughuli za viwanda hapa nchini. Aidha, Wizara kupitia Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) inaendelea kutoa huduma mbalimbali zinazohusiana na uanzishwaji wa viwanda vidogo na vya kati ikiwa ni pamoja na mafunzo juu ya usindikaji wa mazao ya kilimo, uendelezaji teknolojia rahisi za uongezaji thamani mazao ya kilimo, utafutaji wa masoko ya bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali na kutoa mikopo kwa masharti nafuu kupitia Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Wajasiriamali Wananchi (NEDF).

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Muheza ina viwanda vidogo vitatu kwa ajili ya kuchakata viungo. Viwanda vinavyofanya kazi ni viwili ambavyo ni Trianon Investment Limited kilichopo eneo la Lusanga, Muheza Mjini, ambacho mwaka 2020 kimeuza nje jumla ya tani 120 za viungo ambavyo vimechakatwa katika kiwanda hicho. Kiwanda cha pili ni G.F.P Organic Limited kilichopo barabara ya kuelekea Pangani ambacho mwaka 2020 kiliuza nje jumla ya tani 80 za viungo.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivyo vinahudumiwa na Shirika letu la SIDO na vimetoa ajira za kudumu zipatazo 30 na vibarua zaidi ya 50. Viungo vinavyochakatwa ni pamoja na iliki, mdalasini, pilipili manga, karafuu, mchaichai, binzari, maganda ya machungwa na limao. Aidha, kiwanda cha Raza Agriculture Limited kilichopo katika Kijiji cha Muungano, Muheza, kinatarajia kuanza uzalishaji hivi karibuni.

Pamoja na viwanda hivyo wilayani Muheza kuna wajasiriamali wadogo wengi ambao husindika viungo katika ngazi za kaya (household level). Serikali kupitia Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Biashara Tanzania (TANTRADE) inawasaida wajasiriamali hao kuwapatia mafunzo na ushauri ili waweze kuzalisha kwa ubora unaotakiwa na kuuza bidhaa zao katika masoko ya ndani, kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, napenda kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha Sekta Binafsi kuwekeza zaidi katika ujenzi wa viwanda vya kuchakata viungo nchini ikiwemo katika Jimbo la Mheshimiwa Hamis, Jimbo la Muheza.
MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango wa kupunguza bei na kuongeza muda wa mkopo wa Matrekta waliokopeshwa Wakulima wa Jimbo la Kiteto na Shirika la NDC?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edward Kisau Olelekaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Matrekta wa URSUS unatokana na mkataba wa ushirikiano wa kiuchumi baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Poland, uliosainiwa tarehe 28 Septemba, 2015. Serikali ya Jamhuri ya Poland iliiteua kampuni ya URSUS na Serikali ya Tanzania iliiteua SUMA JKT kama watekelezaji na baadaye mradi huu ukahamishiwa Shirika la la Taifa la Maendeleo (NDC) kwa utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkataba huo, Serikali ya Poland ilitoa mkopo nafuu wa dola za Kimarekani milioni 110 kwa riba nafuu ya asilimia 0.3 kwa mwaka, ukiwa na kipindi cha mpito cha miaka mitano na utarudishwa katika kipindi cha miaka 30. Lengo la mkopo huo ilikuwa ni kugharamia maendeleo ya Sekta ya Kilimo nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kupanga bei ya matrekta, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), ilifanya uchambuzi wa gharama na kupanga bei kulingana na uchambuzi huo. Bei hizi zilipangwa kwa kuzingatia gharama za uagizaji, kutolea bandarini, kuunganisha na gharama nyingine za usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilipanga bei nafuu ambapo wakulima wengi wanaweza kununua na kukopa matrekta hayo kutokana na mchango wake katika kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula, biashara na kuzalisha malighafi za viwandani.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ili kurahisisha uuzaji wa matrekta hayo, mkopo uliotolewa haukuwa na riba. Lengo kuu la Serikali siyo kupata faida, bali kuwawezesha wakulima kujikwamua kutoka kwenye matumizi ya jembe la mkono na kuongeza tija zaidi. Hivyo bei ya matrekta hayo kwa sasa inarejesha gharama tu za matrekta hayo pekee bila kupata faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kurahisisha ulipaji wa mkopo kwa wakulima, kuanzia mwaka 2020, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) iliongeza muda wa kulipa mikopo kwa wakopaji ambao muda wa mikataba yao umeisha. Utaratibu unaofanyika ni kuwapa mikataba ya nyongeza wakopaji wote wa matrekta ya URSUS nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikataba ya nyongeza inahusisha bakaa ya deni na haitozwi riba. Utaratibu wa kupewa mikataba ya nyongeza unahusisha mkulima na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) kwa kukaa pamoja na kufanya majadiliano ya namna mkulima atakavyolipa deni lililobaki. Zoezi hili limeshaanza kwa wakulima wa Kiteto katika kipindi hiki na linaendelea ili kuwafikia wale wote ambao muda wa mikataba yao umepita.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza Mradi wa Liganga na Mchuchuma ili uweze kuchangia katika kukuza Uchumi wa Taifa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi unganishi wa madini ya chuma na makaa ya mawe ya Liganga na Mchuchuma uliopo katika Wilaya ya Ludewa, Mkoani Njombe ni mradi wa kimkakati na upo katika hatua za awali za utekelezaji.

Aidha, mradi huo unategemea kutekelezwa kwa ubia kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ambalo litakuwa na 20% na Kampuni ya Sichuan Hongda Group Company Limited ambayo itakuwa na 80% ambayo ni kampuni ya China baada ya majadiliano kuhusiana na baadhi ya vipengele katika mkataba wa utekelezaji wa mradi huo kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa mradi huo, utafiti wa kina umeshakamilika na kubaini kuwepo kwa tani milioni 428 za makaa ya mawe katika eneo la Mchuchuma na tani milioni 126 za chuma katika eneo la Liganga. Aidha, uwekezaji katika mradi huo utagharimu kiasi cha Dola za Kimarekani bilioni tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za awali ambazo zimeshafanyika ni pamoja na utafiti wa athari za mazingira zitakazotokana na utekelezaji wa mradi huo pamoja na njia ya kupunguza athari hizo. Uthamini wa mali na fidia kwa wananchi watakaopisha mradi umeshafanyika, lakini pia, tumeshatoa elimu ya kujenga uwezo wa wananchi kuweza kutumia kiuchumi katika eneo la mradi (Local Content) pale ambapo mradi huu utaanza kutekelezwa. Pia, uboreshaji wa kilometa 221 za barabara kutoka Itoni, Njombe, hadi maeneo ya mradi na ukamilishaji wa utafiti wa reli ya kisasa kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na matawi yake kwenda hadi Mchuchuma na Liganga.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuendelea na utekelezaji wa mradi huu, mwekezaji aliomba vivutio (incentives) ambavyo vilishindwa kutolewa na Serikali kwa sababu vinakinzana na baadhi ya sheria za nchi. Kwa sasa, Serikali ipo katika hatua za uchambuzi wa mradi na kujiridhisha zaidi kuhusu namna bora ya kutekeleza mradi huo ili kukidhi matakwa ya Sheria mpya Namba 5 na 6 za mwaka 2017 zinazolinda rasilimali za nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia uchambuzi huo, Timu ya Serikali ya Majadiliano (Government Negotiation Team) ilishaundwa na inaendelea kujadiliana na mwekezaji. Hivyo, utekelezaji wa mradi huo utaendelea mara baada ya kukamilika kwa majadiliano baina ya Serikali na Mwekezaji.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa masoko ya Kimataifa ya Kitega Uchumi ya Murongo na Nkwenda ili kuongeza chachu ya maendeleo ya Wilaya ya Kyerwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na masoko ya Kimataifa ya kimkakati kwa ajili ya kukuza biashara na mauzo nje ya nchi kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wake. Kutokana na umuhimu huo, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuhakikisha masoko ya kimkakati hususan ya mipakani yanaanzishwa, kuboreshwa na kuendelezwa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mpaka kati ya Tanzania na Uganda, Serikali iliamua kuanzisha masoko ya kimkakati ya Kimataifa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa masoko ya Nkwendana Murongo yaliyopo Wilaya ya Kyerwa Mkoani Kagera chini ya Mradi wa Uwekezaji wa Sekta ya Kilimo Wilayani, (DASIP) uliokuwa unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Mheshimiwa Spika, Masoko hayo bado hayajakamilika kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo ufinyu wa Bajeti. Aidha, Serikali imeunda timu ya wataalam ili kufanya uchambuzi wa kina kuhusiana na changamoto katika miradi hiyo na hatimaye kuja na mapendekezo ya namna bora ya kukamilisha ujenzi wa masoko hayo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya tathmini na uendelezaji wa masoko ya kimkakati ya mipakani. Kazi hiyo itafanywa kwa pamoja kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara ya Kilimo. Aidha, Serikali inaendelea kushirikiana na wadau wengine kutafuta fedha za kukamilisha ujenzi wa masoko ya Murongo na Nkwenda kwa wakati.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO K.n.y. MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza:-

Je, ni kwa namna gani Serikali imetumia fursa ya makubaliano ya TICAD kati ya Tanzania na Japan ili kupata wawekezaji nchini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkutano wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD) ni chombo kilichoanzishwa na nchi ya Japan mwaka 1993 kwa lengo la kukuza mahusiano, maendeleo na kuondoa umaskini Afrika. Vipaumbele vya TICAD vinaenda sambamba na agenda ya 2063 ya Umoja wa Afrika na agenda ya 2030 ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa.

Mheshimiwa Spika, kupitia TICAD Serikali ya Tanzania imeweza kuandaa mfumo wa blueprint unaoboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini na hivyo kupelekea kukuza sekta za uzalishaji, ujenzi wa miundombinu na huduma ikiwemo nishati na kujenga uwezo wa wajasiriamali. Sekta hizo huandaa miradi mbalimbali na kuiwasilisha TICAD, ili kupata ufadhili wa kifedha chini ya uratibu wa Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, miradi ya kiuwekezaji ambayo imetekelezwa nchini kutokana na TICAD ni pamoja na maboresho ya Bandari ya Kigoma, uendelezaji wa huduma za usambazaji wa maji Zanzibar, ujenzi wa kituo cha uzalishaji na usambazaji wa umeme kwa kutumia nishati ya gesi mkoani Mtwara, maboresho ya barabara jijini Dodoma na utoaji wa mikopo nafuu kwa wajasiriamali.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kukuza mahusiano mazuri ya kibiashara baina ya Tanzania na Japan ili kuendelea kunufaika na TICAD katika kuvutia wawekezaji zaidi wa ndani na nje ya nchi.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafufua Viwanda vya Korosho vilivyopo katika Wilaya za Masasi na Newala ili kuchakata korosho ghafi na kuongeza bei ya zao hilo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya za Masasi na Newala zilikuwa na viwanda vitatu vitatu vya kubangua korosho vilivyokuwa vikimilikiwa na Serikali na hatimaye kubinafsishwa. Viwanda hivyo ni Masasi Cashew Factory, Newala l Cashew Factory na Newala ll Cashew Factory.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Korosho cha Masasi kilichopo Masasi kilibinafsishwa na kuuzwa kwa Kampuni ya BUCCO Investments Holdings Limited ambayo ilishindwa kukiendeleza kutokana na Benki ya CRDB kuzuia mali za kiwanda baada ya kiwanda kushindwa kurejesha mkopo waliokopa. Hatimaye Kiwanda kiliuzwa na Benki ya CRDB kwa Kampuni ya Micronix Export Trading Co. Ltd kwa njia ya mnada. Kampuni ya BUCCO Investments Holdings Limited hawakuridhika na utaratibu uliotumika kuuza kiwanda hicho. Walifungua kesi mahakamani na kuishtaki Benki ya CRDB. Kesi hiyo bado ipo mahakamani hivyo uendelezaji wa kiwanda hicho umesimama kusubiri maamuzi ya Mahakama.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Newala I Cashew Factory kilinunuliwa na Kampuni ya Micronics System Ltd, kiwanda hiki kinaendelea kufanya kazi. Kiwanda cha Newala II Cashew Factory kilinunuliwa na Kampuni ya Agrofocus (T) Ltd. Tangu kibinafsishwe, Kiwanda hicho hakijawahi kufanya kazi. Hivyo, mwaka 2019 kilirudishwa katika umiliki wa Serikali chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina. Kiwanda hicho kama vilivyo viwanda vingine vilivyorudishwa Serikalini kipo katika utaratibu wa kupatiwa mwekezaji mwingine mwenye uwezo wa kukiendeleza.
MHE. KENNETH E. NOLLO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kiwanda cha Chumvi katika Kata ya Ilindi, Wilayani Bahi kitakachosaidia kuongeza mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Bahi na kutoa ajira kwa wananchi hasa akina mama?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Ernest Nollo, Mbunge wa Bahi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya vipaumbele vya Serikali katika kipindi hiki ni kuhamasisha ujenzi na kuendeleza viwanda vinavyoongeza thamani ya rasilimali zinazopatikana kwa wingi nchini ikiwemo madini ya chumvi inayopatikana katika Kata za Ilindi na Chali katika Wilaya ya Bahi ili kukuza uchumi na kuongeza ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu zilizopo zinaonesha kuwa, shughuli za uchimbaji na ukusanyaji wa chumvi Wilayani Bahi, zimeajiri takribani watu 400 hasa vijana na akinamama. Serikali inafanya utafiti wa kujua kiasi cha chumvi kilichopo yaani salt deposit ili utafiti huo ukikamilika utumike katika kuhamasisha wawekezaji katika viwanda vya chumvi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inashirikiana na Wizara nyingine za kisekta ikiwemo Wizara ya Maji ili kuhakikisha upatikanaji wa maji ya uhakika katika eneo hilo na Wizara ya Madini kujua kiasi cha madini ya chumvi kilichopo yaani salt deposit ili kuona kama kitakidhi kiwango cha uzalishaji kinachotakiwa kuendesha na kiwanda hasa kiwanda vya kati.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) inafanya utafiti wa teknolojia rafiki ya kuwasaidia wajasiliamali wadogo ili kuzalisha chumvi kwa tija katika eneo la Ilindi, Bahi.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza: -

(a) Je, ni lini wananchi wa Ludewa ambao maeneo yao yamechukuliwa na Serikali kwa muda mrefu kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa Liganga na Mchuchuma watalipwa fidia?

(b) Je, ni lini Mradi wa Liganga na Mchuchuma utaanza kufanya kazi ili kuinua uchumi wa Mkoa wa Njombe na Taifa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi unganishi wa madini ya chuma na makaa ya mawe ya Liganga na Mchuchuma uliopo katika Wilaya ya Ludewa, Mkoani Njombe ni Mradi wa Kimkakati na upo katika hatua za awali za utekelezaji. Mradi huu unategemea kutekelezwa kwa ubia kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa - NDC ambalo litakuwa na 20% na Kampuni ya Sichuan Hongda (Group) Kampuni hii ya China yenye 80% baada ya majadiliano kuhusiana na baadhi ya vipengele katika mkataba wa utekelezaji mradi huu kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ili kuanza utekelezaji wa mradi, mwekezaji aliomba vivutio ambavyo vimeshindwa kutolewa na Serikali kwa sababu vinakinzana na Sheria mpya Na. 6 na 7 za mwaka 2017 ambazo ni Natural Wealth and Resources Contracts (Review and Renegotiation of Unconscionable Terms) Act, 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hadi sasa, majadiliano na mwekezaji huyu yanaendelea ikiwemo suala la ulipaji wa fidia kwa maeneo yote ya mradi yaliyothaminiwa. Utekelezaji wa mradi huo utaanza mara baada ya kukamilika kwa majadiliano hayo.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza: -

Mihimili muhimu ya uchumi wa soko ni Mamlaka za Udhibiti, Tume ya Ushindani na Mamlaka ya kulinda haki na maslahi ya Watumiaji: -

(a) Je, ni lini Serikali itaunda mamlaka yenye nguvu ya kulinda haki na maslahi ya watumiaji nchini?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutunga Sheria ya kuwalinda Watumiaji?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kumlinda Mlaji/Mtumiaji na inatekeleza jukumu hilo kupitia Sheria ya Ushindani Namba 8 ya Mwaka 2003 (The Fair Competition Act). Sheria hiyo ndiyo iliyounda Tume ya Ushindani (Fair Competition Commission – FCC) ambayo ndiyo mamlaka ya kuwalinda walaji/watumiaji wa bidhaa na huduma nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Sheria hii, Serikali imekamilisha uundaji wa Baraza la Kumtetea na Kumlinda Mlaji (National Consumer Advocacy Council) ambalo litakuwa na jukumu la kisheria kusimamia haki za mlaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kukamilisha taratibu za kuhakikisha Baraza hilo linaanzishwa ili liweze kujitegemea nje ya FCC, ili liweze kufanya kazi zake kwa ufasaha.

Aidha, Serikali inakamilisha maandalizi ya Sera ya Ubora ambayo pia ni muhimu katika kulinda haki za walaji/ watumiaji.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inazo sheria mbalimbali za kumlinda mlaji. Sheria hizo ni pamoja na Sheria ya Ushindani Namba 8 ya Mwaka 2003, Sheria ya Viwango ya Mwaka 1975, Sheria ya Vipimo ya Mwaka 1982, Sheria ya Usalama Mahali pa Kazi ya Mwaka 2003, Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 na Sheria ya Chakula, Madawa na Vipodozi ya mwaka 2003. Chini ya sheria hizo walaji mbalimbali hulindwa.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Soko la Kimkakati la Rusahunga Wilayani Biharamulo litakalogharimu shilingi bilioni 3.5 kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri Mkuu Bungeni?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na masoko nchini kwa ajili ya kukuza biashara na mauzo ndani na nje ya nchi kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wake. Kutokana na umuhimu huo, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuhakikisha masoko yanaanzishwa, kuboreshwa na kuendelezwa ili kutoa fursa kwa wakulima wadogo pamoja na wafanyabishara kuuza mazao na bidhaa zao katika masoko hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kipindi cha mwaka 2017/2018, Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo ilitenga eneo la uwekezaji katika Kata ya Lusahunga lenye ukubwa wa ekari 65 ambalo lina thamani ya shilingi bilioni 3.5. Eneo hili limetengwa kwa ajili ya kujenga viwanda vya kusindika mazao ya kilimo, kujenga maghala ya kuhifadhia mazao, miundombinu ya majengo ya kibiashara kama mahoteli, ujenzi wa soko la kimkakati, kituo cha afya, viwanja vya makazi, na kituo cha mafunzo ya wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) imeendelea kusisitiza Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo kutenga fedha katika bajeti yake ili kufanikisha ujenzi wa soko hilo. Aidha, Serikali inaendelea kutafuta wadau mbalimbali ikiwemo Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ili iweze kufanikisha ujenzi wa soko hilo.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA aliuliza: -

Je, Serikali ina mikakati gani ya kuanza uzalishaji katika Kiwanda cha Chuma Mang’ula?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga, Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa uchumi wa viwanda hapa nchini, pamoja na mambo mengine unalenga kufufua na kuendeleza viwanda vilivyobinafsishwa ambavyo havifanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mang’ula Mechanical Workshop ni karakana iliyoanzishwa kwa msaada wa Serikali ya China mwaka 1969. Karakana hiyo ilianzishwa kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa vipuri mbalimbali ya mitambo iliyokuwa inatumika wakati wa ujenzi wa Reli ya Tanzania-Zambia (TAZARA), pamoja na utengenezaji wa vipuri sehemu ya eneo la karakana hiyo ilitumika kujenga kiwanga cha Pre-Fabricated Concrete Manufacturing kwa ajili ya kutengeneza mataruma ya zege kwa maana ya concrete slippers na nguzo za zege.

Mheshimiwa Naibu Spika, karakana ya Mang’ula Mechanical and Machine Tools Company Limited ilirejeshwa Serikalini mwaka 2019 kutokana na mwekezaji wake kushindwa kuendeleza kiwanda hicho kwa mujibu wa mkataba wa mauziano. Kufuatia urejeshwaji huo Wizara ya Viwanda na Biashara na Ofisi ya Msajili wa Hazina imeandaa utaratibu wa kutafuta wawekezaji wapya watakaoviendesha viwanda hivyo kikiwemo kiwanda cha Mang’ula Machine and Mechanical Tools Limited.
MHE. SHALLY J. RAYMOND K.n.y. MHE. ESTHER E. MALLEKO) aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kufufua Kiwanda cha Magunia Moshi Mkoani Kilimanjaro ili kukuza ajira na uchumi kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, magunia yanayotokana na zao la mkonge ni moja ya vifungashio muhimu vya mazao ya kilimo hapa nchini. Tanzania ina viwanda nane vinavyoongeza thamani zao la mkonge. Kati ya viwanda hivyo, viwanda vitatu 3 ni vya kuzalisha magunia ya mkonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Magunia cha Moshi (Tanzania Bag Corporation – TBCL) kilibinafsishwa na Serikali kwa kampuni ya Mohamed Enterprise Tanzania Limited (METL). Hata hivyo, kutokana na changamoto mbalimbali kiwanda hiki kimeshindwa kuzalisha na kujiendesha kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto za viwanda vya magunia ya mkonge ni mtambuka na Serikali inazishughulikia kiujumla kwa tasnia yote ya mkonge. Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo na Wizara ya Fedha na Mipango na Taasisi zake inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za utatuzi wa changamoto ikiwemo kulinda wazalishaji wa ndani na kuwatengenezea mazingira bora ya ufanyaji biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini ya Serikali kuwa jitihada hizi zinazoendelea zitakuwa ni chachu ya kuinua kilimo cha mkonge na ufufuaji wa viwanda vya magunia ya mkonge kikiwepo kiwanda cha magunia cha Moshi na hivyo kukuza ajira na uchumi wa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. ASSA N. MAKANIKA aliuliza: -

Je, Serikali imefikia hatua gani katika kurekebisha vifungashio vya mafuta ya mawese kwa kuwa wananchi wanaumizwa na kunyonywa kupitia vifungashio vinavyotumika sasa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Assa Nelson Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo, Mkoa wa Kigoma limeshatengeneza sampuli za vifungashio vya mafuta ya mawese vitakavyotumiwa na wakulima. Kwa kuanzia SIDO imetengeneza sampuli za vifungashio hivyo vya lita tano na lita ishirini. Vifungashio hivyo viko katika mfumo wa ndoo ya chuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua inayofuata ni sampuli hizo za vifungashio kuwasilishwa kwa Wakala wa Vipimo kwa ajili ya uhakiki wa ujazo huo. Aidha, baada ya Wakala wa Vipimo kuhakiki vifungashio hivyo, itawasilisha sampuli hizo za vifungashio kwa SIDO ili viweze kuzalishwa kwa wingi kwa maana ya kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshatoa maagizo kwa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) na Wakala wa Vipimo kuharakisha zoezi hilo la urekebishaji wa vifungashio hivyo ili wakulima wa mawese Kigoma wasiendelee kunyonywa. Aidha, SIDO wataanza kuzalisha kwa wingi vifungashio hivyo na kuviuza kwa bei nafuu kwa wazalishaji wa mafuta ya mawese nchini ili kutekeleza kwa vitendo agizo la Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, alilolitoa wakati alipokuwa katika ziara yake Mkoani Kigoma mwezi Februari, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza: -

Serikali imewekeza kiasi cha Shilingi Bilioni 20 kwa ajili ya kutengeneza miundombinu ya ukaguzi wa magari nchini (Destination Inspection).

Je, ni sababu zipi zilisababisha Serikali kubadilisha mfumo huo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirika la Viwango Tanzania (TBS) lilianza kukagua magari yaliyotumika yanayoingia nchini kuanzia tarehe 01 Machi, 2021 katika Bandari ya Dar-Es-Salaam. Sababu za kusitisha utaratibu uliokuwepo awali (Pre-Shipment Verification of Conformity to Standards – PVOC) ni pamoja na changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa mfumo huo na pia, faida tarajiwa baada ya kutekeleza mfumo wa Destination Inspection (DI).

Mheshimiwa Spika, changamoto za PVOC ni pamoja na Mosi; ukosefu wa ufanisi, gharama kubwa za ukaguzi na upimaji. Mawakala kutokutokuwa na ofisi za ukaguzi katika maeneo yote, mawakala kushindwa kufanya ukaguzi inavyostahili, nchi kupoteza fedha za kigeni, upotevu wa ajira kwa Watanzania, nchi kushindwa kujenga uwezo wa miundombinu ya ukaguzi na wataalam wa ukaguzi na ugumu wa kuhudumia Wajasiriamali Wadogo wanaonunua bidhaa nyingi za aina mbalimbali zenye thamani ndogo.

Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, tangu ukaguzi huu uanze hapa nchini mwezi Machi hadi tarehe 25 Agosti, 2021 jumla ya magari 13,968 yamekaguliwa na TBS na kuliingizia Taifa jumla ya Shilingi 4,888,800,000 ikiwa ni tozo za ukaguzi. Aidha, wateja wengi wameridhika na kufurahia utaratibu huu wa DI. Nashukuru.
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: -

Je, ni lini akina Mama zaidi ya 300 waliokuwa Wafanyakazi wa Kiwanda cha Kiliflora Wilayani Meru watalipwa stahiki zao baada ya Kiwanda hicho kufungwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Zaytun Seif Swai, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mgogoro uliopo baina ya wafanyakazi na mwekezaji wa Kampuni ya Kiliflora Ltd. Hivyo, Serikali ilifuatilia mgogoro huo na kubaini kuwa Tanzania Investment Bank (TIB) ilirejesha fedha iliyokopesha kwa kuuza mali za Kiliflora Ltd zilizowekwa dhamana ili kulipa deni la mkopo uliochukuliwa na Kampuni. Hivyo, kisheria Wafanyakazi wanapaswa kulipwa na Kampuni ya Kiliflora kwa kuwa kilichofanyika ni ufilisi kabidhi na siyo kufunga kampuni. Mfilisi Kabidhi (Receiver and Manager) ni tofauti na Mfunga Kampuni (Liquidator).

Mheshimiwa Spika, aidha, wafanyakazi wa Kiliflora Ltd, Wilson Samwel na Wenzake 502 walifungua Kesi ya Labor Na. ARS/ARM/305/2020, 152/2020 dhidi ya Kampuni ya Kiliflora Ltd na Frank Mwalongo ambaye ni Mfilisi Kabidhi ambayo ilianza kusikilizwa tarehe 30/10/2020. Shauri hili lilikwishatolewa maamuzi na Mahakama kwamba, masuala ya madai ya wafanyakazi yanapaswa kufanyiwa kazi na Kampuni ya Kiliflora Ltd maana haijafilisiwa kama ilivyoonekana kwenye taarifa za BRELA kwamba, Kampuni bado ipo hai.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango inaendelea kuhimiza mmiliki wa shamba la Kiliflora kuwalipa akina mama hao. Nakushukuru.
MHE. SYLVESTRY F. KOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Kiwanda cha Viuadudu cha Kibaha kinazalisha bio-larvicides za kuangamiza viluilui vya mbu kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sylvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kiwanda cha viuadudu Kibaha, Tanzania Biotech Products Limited ni mali ya Serikali kwa asilimia 100. Kiwanda hiki kinao uwezo wa kuzalisha lita milioni sita za viuadudu vya kibaolojia (bio-larvicides) kwa mwaka vinavyotumika kuua viluilui wa mbu waenezao Malaria na aina nyinginezo.

Mheshimiwa Spika, kiwanda kinaendelea kuzalisha viuadudu vya kibaolojia ambapo tangu kiwanda kilipoanza uzalishaji mwaka 2017 hadi mwezi Agosti, 2021 kimeweza kuzalisha jumla ya lita 700,286.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali kupitia Shirika letu la Maendeleo ya Taifa (NDC) ni kuhakikisha kiwanda hiki kinazalisha kwa ukamilifu wake (full installed capacity) kwa kutafuta masoko zaidi ya viuadudu ya ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
MHE. NG’WASI D. KAMANI Aliuliza: -

Je, Serikali imefikia hatua gani katika kuunganisha Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi hususan Vijana na kuwa na eneo moja la wazi la utoaji huduma?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa ridhaa yako kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu anayetujalia uhai tuendelee kutekeleza majukumu yetu ya kila siku. Lakini pili, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpenda wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuniamini na kuweza kuniendeleza kubaki katika nafasi ya Naibu Waziri katika Wizara hii ya Uwekezaji Viwanda na Biashara, ili niweze kuendelea kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara inasimamia Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya Mwaka 2004 na Sheria ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004. Aidha, Serikali inaratibu utekelezaji wa mifuko na programu za uwezeshaji 62 ambapo mifuko na proramu 52 zinamilikiwa na Serikali na mifuko na programu 10 zinamilikiwa na taasisi za sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, kati ya mifuko hiyo na proramu 52 zinazomilikiwa na Serikali, mifuko 21 inatoa mikopo ya moja kwa moja kwa walengwa, mifuko tisa inatoa dhamana ya mikopo, mifuko 17 inatoa ruzuku na programu tano ni za uwezeshaji ambazo zinatoa huduma mbalimbali ikiwemo ujenzi, urasimishaji ardhi na uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha taarifa ya tathmini ya mifuko hiyo na taarifa hiyo itawasilishwa hapa Bungeni baada ya kukamilika. Nakushukuru sana.
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Viwanda vya Kusindika Maziwa katika Mkoa wa Arusha?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Arusha ni moja ya mikoa yenye uzalishaji mkubwa wa maziwa ambapo unazalisha takriban lita 30,550,500 kwa mwaka. Mkoa wa Arusha una jumla ya viwanda 18 viwanda ambavyo ni vikubwa na vidogo vya kusindika maziwa vilivyosajiliwa na Bodi ya Maziwa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo uliosimikwa wa kusindika maziwa kwa viwanda tajwa ni kiasi cha takriban lita 43,789,200 kwa mwaka. Lakini hata hivyo, usindikaji halisi ni lita 6,315,400 kwa mwaka. Maziwa mengi hayaingii kwenye soko rasmi na kushindwa kupelekwa viwandani kwa ajili ya kuchakatwa, kutokana na ukusanyaji mdogo wa maziwa yanayozalishwa na wafugaji katika maeneo hayo. Jambo linaloathiriwa na ukosefu wa mifumo mizuri ya ukusanyaji wa maziwa (collection centres).

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali ni kushirikiana na sekta binafsi kuendelea kuhamasisha ujenzi wa miundombinu ya kukusanyia maziwa ili viwanda vyote vipate maziwa ya kutosha katika mkoa wa Arusha na mikoa mingine nchini, yenye uzalishaji mkubwa wa maziwa. Hii itasaidia kuongeza tija kwenye mnyororo wa thamani wa maziwa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. DAVID M. KIHENZILE Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga Kiwanda cha Parachichi Mkoa wa Iringa hususan Mufindi Kusini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Waziri Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara namba kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea na azma ya kuhamasisha ujenzi wa viwanda katika nchi yetu. Moja ya mikakati ambayo Serikali imeweka ni pamoja na kutenga maeneo katika kila Wilaya na kuweka miundombinu wezeshi ili kuvutia uwekezaji wa viwanda kulingana na malighafi zinazopatikana katika eneo husika.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Mufindi, Serikali imetenga maeneo mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa viwanda ikiwemo eneo la Igowole katika Jimbo la Mufindi Kusini. Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji kujenga viwanda vinavyotumia malighafi zinazopatikana Tanzania ikiwemo zao la parachichi Wilayani Mufindi, nakushukuru.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia akinamama wafanyabiashara ili wafanye biashara zenye tija?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuhamasisha wafanyabiashara wadogo wakiwemo akinamama kufanya shughuli zao katika maeneo rasmi na kuchukua vitambulisho vya wajasiriamali na kurasimisha biashara zao. Mikakati ya Serikali ni kuendelea kuwasaidia akinamama wafanyabiashara kupitia mikopo inayotolewa na Mifuko ya Uwezeshaji ukiwemo Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Wafanyabiashara Wananchi (NEDF) chini ya Shirika letu la Kuendeleza Viwanda Vidogo (SIDO) na Mfuko wa Dhamana ya Mikopo kwa Wajasiriamali (SME Credit Guarantee Scheme) unaoratibiwa na pia SIDO kwa kushirikiana na Benki ya CRDB.

Mheshimiwa Spika, pia tunaendelea kuboresha na kujenga miundombinu ikiwemo majengo ili wapate sehemu tulivu za kukuza biashara zao. Kuanzia Julai, 2015 hadi Machi, 2021, Serikali kupitia Mfuko wa Dhamana ya Mikopo kwa Wajasiriamali pekee imekwishawapatia akinamama wafanyabiashara mikopo yenye thamani ya Shilingi milioni 310. Aidha, Wizara inakamilisha mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo ya mwaka 2003 ili iweze kuendana na mabadiliko ya kijamii na kiuchumi ya sasa. Nakushukuru.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua Kiwanda cha Tembo Chipboard kilichopo Kata ya Mkumbara Wilayani Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tembo Chipboards Limited ni kiwanda kilichokuwa kikimilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ikiwa na hisa asilimia 80 na Kampuni ya Grewalls Saw Mills asilimia 20. Mnamo tarehe 13 Aprili, 2004 Serikali ilibinafsisha kiwanda hicho kwa kuuza hisa zake zote asilimia 80 kwa mwekezaji wa kampuni ya MELJON Bf ya Uholanzi na baadaye tarehe 13 Machi 2015 Kampuni ya Grewalls Saw Mills ilisaini makubaliano na MELJON Bf kwa kuuza hisa zake asilimia 20. Hivyo kampuni ya MELJON Bf iliendelea kuwa mmiliki wa kiwanda kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, kufuatia zoezi la ubinafsishaji wa viwanda, mwekezaji MELJON Bf alitakiwa kuwekeza kulingana na mkataba. Kutokana na uwekezaji huo kutofanyika, tarehe 16 Oktoba, 2018 Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina ilifanya maamuzi ya kukirejesha kiwanda na mwekezaji alipewa barua ya kuvunja mkataba.

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina anamalizia taratibu za kukirejesha kisheria kiwanda hiki Serikalini. Urejeshaji huu ukikamilika ndipo uwekezaji mpya utafanyika ili kuwezesha kukifufua kiwanda hicho. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED aliuliza: -

Je, kuna viwanda vingapi vya kuchakata taka ngumu nchini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asya Mwadini Mohammed, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tanzania hadi sasa tuna jumla ya viwanda 137 vya kuchakata taka ngumu hapa nchini. Viwanda hivyo vimegawanyika katika makundi manne ambayo ni viwanda vinavyotumia taka zitokanazo na chuma viko 16; viwanda vinavyotumia taka za plastiki viko 70; viwanda vidogo vya kutengeneza mkaa mbadala kutoka kwenye mabaki ya kilimo viko 50; na tuna kiwanda kimoja cha kutengeneza mbolea aina ya mboji inayotokana na mabaki ya vyakula. Nakushukuru.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha uwekezaji wa miradi 294 yenye thamani ya dola bilioni 8.04 inatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Jimbo la Lulindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha kuwa uwekezaji wa miradi 294 yenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 8.04 inatekelezwa, Serikali imeendelea kufanya ufuatiliaji na kuhakikisha kuwa mazingira ya uwekezaji nchini yanaendelea kuboreshwa ili kurahisisha utekelezaji na kuvutia mitaji zaidi. Aidha, kuimarisha Kituo cha Huduma ya Mahala pamoja, kutoa huduma za mahala pamoja kwa njia ya kieletroniki lakini pia kuendelea kuwahudumia wawekezaji baada ya kukamilisha uwekezaji. Nakushukuru.
MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza: -

Je, kwa miaka kumi ni wawekezaji wangapi wa nje walionesha nia ya kuwekeza na kufanikiwa na upi mkakati kwa ambao hawajafanikiwa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC) jumla ya miradi 4,543 ilisajiliwa katika kipindi cha miaka kumi kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2021 ambapo mitaji yenye thamani ya dola za Marekani bilioni 53.1 ilitarajiwa kuwekezwa na kutoa ajira 654,260. Kati ya miradi hiyo, miradi 3,304 ilitekelezwa sawa na asilimia 72.7 ya miradi yote iliyosajiliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kufanikisha uwekezaji ikiwemo kuimarisha matumizi ya TEHAMA, dirisha moja la kuhudumia wawekezaji, kuboresha na kujenga miundombinu wezeshi, vivutio vya kikodi na visivyo vya kikodi na kutenga maeneo kwa ajili ya wawekezaji. Nakushukuru.
MHE. JAFARI W. CHEGE K.n.y. MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawawezesha wananchi wa Jimbo la Tarime Vijijini, Tarime Mjini na Rorya kupata bidhaa kutoka nchi jirani ya Kenya?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ni miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na inatekeleza makubaliano ya hatua ya pili ya ushirikiano ya Soko la Pamoja ambapo wafanyabiashara kutoka nchi wanachama wameruhusiwa kusafirisha bidhaa kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa katika nchi husika. Hivyo, kutokana na mazingira hayo, Serikali haijaweka zuio lolote la bidhaa kutoka nchi jirani ya Kenya kuingia Tanzania. Nakushukuru sana.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza: -

Je, ni lini mifuko ya kuwezesha wananchi kiuchumi itaunganishwa ili kuleta tija na manufaa kwa Watanzania hasa waishio vijijini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara inaratibu utekelezaji wa mifuko na programu 62 za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekamilisha tathmini ya mifuko na programu za uwezeshaji ishirini. Napenda kutumia fursa hii kukujulisha kuwa, Serikali inafanyia uchambuzi wa kina taarifa ya tathmini hiyo na kuja na hatua za kuchukua ili kuboresha utoaji wa huduma wa mifuko husika. Nakushukuru sana.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta Mwekezaji wa Kiwanda cha Saruji katika Wilaya ya Uvinza?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Vieanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ili kuhamasisha na kuvutia wawekezaji ikiwemo kwenye sekta ndogo ya saruji. Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kwa kushirikiana na Uongozi wa Mkoa wa Kigoma kimeweza kuvutia mwekezaji (Itracom Fertilizers Company Limited) kujenga kiwanda cha saruji na tayari tumeshampa ekari 47 katika Eneo la Uwekezaji la Kigoma (KiSEZ). Wilaya ya Uvinza pia itanufaika na mwekezaji huyu. Serikali inaendelea kuvutia wawekezaji zaidi ili kuwekeza katika Mkoa wa Kigoma ikiwemo Wilaya ya Uvinza. Nakushukuru.
MHE. MOHAMED SAID ISSA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wigo wa biashara baina ya Zanzibar na Tanzania Bara ili kuongeza mapato?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Said Issa, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ina Mipango na Mikakati mbalimbali ili kuendelea kupanua wigo wa Biashara baina ya Tanzania Bara na Zanzibar ikiwemo: -

(i) Kuendelea kutoa elimu na kuongeza hamasa zaidi kwa makampuni ya Tanzania Bara na Zanzibar kushiriki katika Maonesho mbalimbali yanayofanyika ndani ya Tanzania Bara na Zanzibar;

(ii) Kufanya tathmini na kubaini vizuizi visivyo vya kikodi;

(iii) Kuzishirikisha Mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka za Mapato za Tanzania Bara (TRA) na Zanzibar (ZRA) kwenye majadiliano ya pamoja ili kupanua wigo wa Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Upanuzi wa ushirikiano wa kibiashara unazingatia na kuheshimu sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Ninakushukuru.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza: -

Je, ni zipi sababu za Kiwanda cha Pamba na Mafuta cha Kasamwa kusimamisha uzalishaji kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Pamba na Mafuta cha Kasamwa kilisitisha shughuli za uzalishaji mwaka 2012 kutokana na changamoto mbalimbali zikiwemo teknolojia iliyopitwa na wakati, ukosefu wa vipuri, gharama kubwa za uendeshaji hususani maji na umeme, uhitaji wa idadi kubwa ya wafanyakazi na ukosefu wa malighafi. Ninakushukuru.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kuwanunulia mitambo ya kisasa na kuwapa mikopo wanawake ambao wanazalisha pombe za kienyeji?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushuru. Kwa niaba ya Waziri wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshiniwa Condester Michael Sichalwe Mbunge wa Jimbo la Momba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uzalishaji na uuzaji wa pombe za kienyeji unaofanyika vijijini na katika baadhi ya maeneo ya mijini. Kwa sasa Serikali haijaanzisha mpango wa kuwanunulia mitambo ya kisasa na kuwapa mikopo wanawake wanaozalisha pombe za kienyeji. Hata hivyo, wanawake wajasiriamali wataendelea kupata mikopo kupitia mifuko na programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi. Nakushukuru.
MHE. JULIANA D. MASABURI aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kufanya ukaguzi wa kudhibiti uingizaji na utengenezaji wa vipodozi fake nchini?
NAIBU WAZIRI UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Didas Masaburi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Shirika la Viwango Tanzania yaani TBS imeendelea kudhibiti uingizaji na utengenezaji wa vipodozi visivyokidhi viwango vya ubora kwa mujibu wa Sheria ya Viwango Na. 2 ya Mwaka 2009 na Sheria ya Fedha Na. 8 ya Mwaka 2019. Pia Serikali imeendelea kudhibiti bidhaa fake kupitia Tume ya Ushindani (FCC) kwa mujibu wa Sheria ya Ushindani Na. 8 ya Mwaka 2003.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kufanya utafiti kuhusu hali ya biashara na uchumi wa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kupata matokeo ya tafiti zinazolenga kuboresha biashara na uchumi wa wananchi pamoja na kuwaunganisha wananchi na fursa za masoko kupitia maonesho ya mifuko na programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, aidha, pamoja na hiyo mikakati mingine ni kutoa tuzo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya tafiti bora kwenye masuala ya uchumi na biashara.
MHE. KAVEJURU E. FELIX aliuliza: -

Je, kuna mpango gani kuweka Mazingira bora ya uwekezaji kilimo cha Michikichi pamoja na kiwanda cha kuchakata mafuta – Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Felix, Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika juhudi za kuongeza uzalishaji wa mbegu za michikichi, Serikali imeanzisha Kituo Maalum cha Utafiti wa Zao la Michikichi cha TARI Kihinga, mkoani Kigoma ili kuendeleza zao hili kwa ufanisi. Vile vile, Serikali kupitia Wizara yangu, imepanga kujenga viwanda viwili vidogo vya kuzalisha mafuta ya mawese katika Kijiji cha Nyamuhoza kilichopo Wilaya ya Kigoma (DC) na Kijiji cha Sunuka kilichopo Wilaya ya Uvinza.

Mheshimiwa Spika, juhudi zote hizo zimelenga kuweka mazingira bora ya uwekezaji kwenye zao la michikichi mkoani Kigoma.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. HAMIS M. MWINJUMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha upatikanaji wa soko la machungwa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamis Mohamed Mwinjuma, Mbunge wa Jimbo la Muheza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha upatikanaji wa masoko ya uhakika ya machungwa ambayo huzalishwa kwa wingi katika Mkoa wa Tanga hususan Wilaya ya Muheza, Wizara kupitia Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) imeendelea kutafuta masoko katika nchi mbalimbali, ambapo mwaka 2021/2022 liliweza kupatikana soko la machungwa katika nchi za falme za Kiarabu. Vile vile, Serikali inaendelea kutoa elimu ya ufungashaji na usindikaji wa matunda ya aina zote kwa wazalishaji ili kuyaongezea thamani na kuweza kunufaika na fursa hiyo ndani ya nchi ambayo itaongeza soko kwa matunda yakiwemo machungwa. Nakushukuru sana.
MHE. CECILIA D. PARESSO aliuliza: -

Je, nini kauli ya Serikali kwa wakulima wa vitunguu maji katika Bonde la Eyasi juu ya upatikanaji wa masoko pamoja na bei ya zao hilo?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuhakikisha mazao yanayozalishwa nchini yanapata soko la uhakika, na kuwa mkulima anapata bei nzuri na kunufaika.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kupitia Idara ya Maendeleo ya Biashara na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TanTrade) inaendelea kutafuta masoko ya uhakika ya zao la vitunguu maji vinavyolimwa hapa nchini, ikiwa ni pamoja na vitunguu kutoka Bonde la Eyasi ili kupata bei nzuri itakayo wanufaisha wakulima wa zao hilo hapa nchini. Nakushukuru.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA K.n.y. MHE. MOHAMED SAID ISSA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kuhakikisha TBS na ZBS zinafanya kazi kwa ushirikiano?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Said Issa, Mbunge wa Jimbo la Konde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS) wana hati ya makubaliano (Memorandum of Understanding) iliyosainiwa Mei, 2015 kwa kipindi cha miaka mitano na pia imehuishwa tena mwaka 2020.

Mheshimiwa Spika, katika makubaliano haya yanajikita katika maeneo yafuatayo: -

(i) Uandaaji wa viwango vya Kitaifa;
(ii) Udhibiti wa ubora na usalama wa bidhaa;
(iii) Huduma za metrolojia na upimaji;
(iv) Mafunzo ya kitaalam kwa maafisa wa ZBS; na
(v) Kutambua bidhaa zilizothibitishwa ubora baina ya mashirika haya mawili.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kuondoa changamoto ya Lumbesa kwa wakulima wa zao la viazi nchini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA aljibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali kupitia Sheria ya Vipimo, Sura 340, mapitio ya mwaka 2002 na marekebisho yake ya mwaka 2018 wa kuondoa changamoto ya lumbesa ni kuendelea kutoa elimu kwa umma juu ya matumizi sahihi ya vipimo. Mazao ya mashambani ikiwemo viazi yatafungashwa kwa uzito usiozidi kilogramu 100 na hatua zitachukuliwa kwa wote watakaobainika kuvunja sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI aliuliza: -

Je, wananchi wa Vunjo wamenufaika vipi na Mifuko ya Uwezeshaji ya Wajasiriamali kama NEEC, NEDF, SELFU na TAFF?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mifuko na programu za uwezeshaji zimetoa manufaa makubwa katika kuwezesha mikopo, ajira, kipato kwa wananchi wakiwemo wananchi wa Vunjo. Mifuko na programu za uwezeshaji zimetoa jumla ya mikopo yenye thamani ya shilingi trilioni 5.68 tangu kuanzishwa kwake. Mathalani katika Jimbo la Vunjo, kwa kipindi cha mwaka 2019/2020 hadi 2021/2022 mfuko wa NEDF umetoa mikopo 11 yenye thamani ya milioni 25.2 na Mfuko wa TAFF umetoa ruzuku yenye thamani ya shilingi milioni 20, nakushukuru.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa mradi wa Liganga na Mchuchuma?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kuona mradi unganishi wa Linganga na Mchuchuma unatekelezwa mapema iwezekanavyo. Serikali imefanya uthaminishaji mpya katika eneo la mradi baada ya ule wa kwanza kwisha muda wake kwa mujibu wa sheria na zoezi la kuhuisha tathmini ya taarifa za wananchi lilikamilika mwezi Disemba, 2022. Pia tumehuisha majadiliano na mwekezaji wa mradi ili kuhakikisha majadiliano yanakamilika kwa wakati pasipo kuleta hasara kwa Taifa na kutoa fedha za kutengeneza miundombinu kwa maana sehemu korofi za barabara katika eneo la Milima ya Kemilembe Mchuchuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu mkubwa wa Mradi huo kwa Taifa letu, napenda kuwahakikishia kuwa juhudi zinazofanyika hivi sasa zitawezesha utekelezaji wa mradi huo haraka.

Mheshimiwa naibu Spika, nakushukuru.
MHE. EDWARD O. KISAU K.n.y. MHE. ABDULLAH ALI MWINYI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa taarifa ya utekelezaji wa Blueprint for Regulatory Reforms za mwaka 2018 ili zijadiliwe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdullah Ali Mwinyi, Mbunge wa Jimbo la Mahonda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianza rasmi utekelezaji wa mpango wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini (MKUMBI) ujulikanao kama blueprint hapo Julai Mosi, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba tarehe 24 Oktoba, 2022, Wizara iliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa MKUMBI kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira. Katika taarifa hiyo ambayo inaonesha utekelezaji wa hadi kufikia Agosti, 2022 ilijadiliwa, ambapo Kamati ilitoa maelekezo mbalimbali ya kufanyiwa kazi ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa mpango huo, maelekezo hayo yanaendelea kuzingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.
MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza vyanzo vya mitaji kwa akina Mama wajasiriamali mbali ya fedha zinazotolewa na Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu Swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikiwawezesha kimtaji akina mama kupitia Mifuko ya Uwezeshaji inayoratibiwa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Serikali ilianzisha Mifuko hii ili kuwasaidia wananchi wake hasa makundi maalum kwa lengo la kupunguza changamoto ya upatikanaji wa mitaji yenye masharti nafuu.

Mheshimiwa Spika, vilevile, Serikali ilianzisha Benki ya Wanawake Tanzania na ili kuboresha huduma shughuli za Benki hiyo zilihamishiwa katika Benki ya Tanzania Postal Bank sasa hivi inaitwa Tanzania Commercial Bank. Aidha, katika mwaka wa fedha wa 2020/2021 Benki hiyo kupitia dirisha la wanawake imeendelea kutoa mikopo kwa wanawake, ambapo kiasi cha Shilingi Bilioni 22.3 kimetolewa kwa wanawake 6,327. Nakushukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali imeshindwa kukamilisha ujenzi wa soko la kimkakati la Kimataifa la Remagwe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na masoko ya Kimkakati kwa ajili ya kukuza biashara na mauzo nje ya nchi, kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wake.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliamua kuanzisha masoko ya kimkakati ya Kimataifa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa soko la Remagwe katika mpaka wa Sirari chini ya Mradi wa Uwekezaji wa Sekta ya Kilimo Wilayani, District Agricultural Sector Investment Project (DASIP) uliokuwa unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kukamilisha ujenzi wa soko hilo.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza: -

Je, mazungumzo ya Serikali na wawekezaji kujenga Kiwanda cha Mbolea Kilwa Masoko kwa kutumia gesi asilia yamefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa viwanda vya mbolea na namna uzalishaji wa mbolea nchini utakavyoongeza tija kwa wakulima na hatimaye kupata mavuno mengi na viwanda kupata malighafi za kutosha kwa ajili ya kuchakata. Serikali inaendelea na majadiliano na wawekezaji mbalimbali wakiwemo Kampuni ya Dangote, Elsewedy na PolyServe ili kuharakisha uwekezaji wa Kiwanda cha Mbolea Kilwa Masoko.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Kituo cha SIDO Wilayani Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Bajeti ya mwaka 2022/2023 Wizara kupitia shirika la kuendeleza viwanda vidogo (SIDO) imetenga jumla ya shilingi milioni 950 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya mitaa ya viwanda. Kati ya fedha hizo, kiasi cha shilingi milioni 100 ni kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Mafunzo na Uzalishaji cha SIDO Wilayani Nyasa. Hivyo, pindi fedha hizo zitakapopokelewa, ujenzi wa kituo hicho utakamilika. Nakushukuru.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italipa fidia wananchi waliotwaliwa ardhi yao kwa ujenzi wa viwanda maeneo ya Liganga na Mchuchuma?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa uwekezaji Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi Unganishi wa Mchuchuma na Liganga unatarajiwa kutekelezwa kwa ubia kati ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) kwa niaba ya Serikali na Kampuni Binafsi, ambaye ni mbia. Katika kutekeleza mradi huo, Serikali imetenga fedha katika bajeti ya mwaka 2022/2023 kwa ajili ya kufanya uthaminishaji upya na hatimaye kulipa fidia kwa wananchi wanaopisha mradi huo kwa mujibu wa Sheria.
MHE. JUDITH S. KAPINGA aliuliza: -

Je, Serikali kupitia Tume ya Ushindani (FCC) ina mkakati gani wa kumlinda mlaji katika biashara za mtandaoni?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Judith Salvio Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha biashara ya mtandaoni inalindwa, Tume ya Ushindani (FCC) ina Mpango mkakati wa kutekeleza jukumu la kumlinda mlaji wa biashara mtandaoni 2021/2022 - 2025/2026. Mkakati huo ni kupitia njia ya elimu kwa walaji kuhusu haki na wajibu wao na mambo ya msingi ya kuzingatia wakati wakifanya biashara za mtandaoni ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa taarifa zilizotolewa kwenye mtandao kuwa ni sahihi. Nakushukuru.
MHE. TARIMBA G. ABBAS aliuliza: -

Je, nini juhudi za Serikali kuweka mifumo rafiki ya kurahisisha ufanyaji wa biashara ili kuvutia zaidi uwekezaji nchini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kufanya maboresho ikiwa ni pamoja na kurekebisha sheria, kuweka mifumo ya kielektroniki, kufuta au kupunguza tozo na ada kero, kuondoa muingiliano wa majukumu katika baadhi ya taasisi, kuunganisha mifumo ya kielektroniki katika taasisi mbalimbali ili iweze kuwasiliana, kuweka miongozo na taratibu za utoaji huduma katika mamlaka za udhibiti, kuanzisha vituo vya pamoja vya kutoa huduma, kusogeza huduma karibu na watumiaji, kuboresha mifumo ya ukaguzi wa pamoja, kuweka utaratibu wa ukaguzi unaozingatia vihatarishi, kujenga uwezo katika mamlaka za uthibiti na kuweka taratibu na kanuni za kujidhibiti. Nakushukuru.
MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya uendeshaji wa Mabaraza ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Subira Khamis Mgalu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikiendesha Majukwaa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi tangu mwaka 2017. Lengo kuu la majukwaa hayo ni kuwakutanisha wanawake ili waweze kujadili fursa za kiuchumi na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wakati wa utekelezaji wa shughuli za kiuchumi nchini.

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwaka 2021/2022, mikoa yote 26 imezindua majukwaa ya wanawake katika halmashauri 140 kati ya halmashuri 184 na kata 1,149 kati ya kata 2,404. Lakini pia mitaa na vijiji 1,776 kati ya mitaa na vijiji 7,613.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Serikali ilitenga fedha zaidi ya milioni 72 na katika mwaka wa fedha unaokuja 2023/2024, Serikali imetenga shilingi milioni 200 kwa ajili ya uendeshaji wa majukwaa hayo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ASYA SHARIF OMAR aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kuongeza viwanda vya kusindika ngozi za mbuzi na ng’ombe?

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asya Sharif Omar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa uwekezaji katika sekta ya ngozi unaongezeka. Mikakati hiyo ni pamoja na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi lakini Vilevile, Serikali katika kuhakikisha inavutia na kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya ngozi, imehakikisha viwanda vya ngozi vya ndani vinapata malighafi za kutosha hapa nchini kwa kuongeza ushuru kwa ngozi zinazouzwa nje ya nchi. Mfano, asilimia 80 kwa ngozi ghafi na asilimia 10 kwa ngozi iliyoongezwa thamani hadi kufikia kuwa ya “wet blue”. Aidha, Serikali imekuwa ikitoa vivutio mbalimbali ikiwa ni sehemu ya kuvutia uwekezaji kama vile kusamehe kodi kwa mitambo inayoingizwa kutoka nje ya nchi kwa lengo la kusindika na kuzalisha ngozi na bidhaa za ngozi hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mikakati hiyo, Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya ngozi kwa kuweka mazingira bora ya ufanyaji biashara nchini kupitia MKUMBI. Ninakushukuru.
MHE. KAVEJURU E. FELIX aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi katika Ziwa Victoria na Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Jimbo la Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina Mkakati wa Kuendeleza Sekta ya Uvuvi 2022/2023 – 2025/2026, pia Mkakati wa Taifa wa Kuendeleza Ukuzaji Viumbe kwenye Maji 2018 – 2025, na Mpango Kabambe wa Sekta ya Uvuvi 2021/2022 –2036/2037 ambayo imelenga kuongeza viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi kupitia Mkakati Jumuishi wa Kuendeleza Viwanda Nchini.

Mheshimiwa Spika, kupitia mikakati hiyo, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya uvuvi na viwanda na uboreshaji wa mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji ambayo utekelezaji wake utaendelea kuvutia uwekezaji wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi nchini ikiwa ni pamoja na eneo la Ziwa Victoria na Tanganyika.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanzisha Special Economic Zone ili kuchochea viwanda vya uchakataji Njombe Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Programu ya Special Economic Zones na Export Processing Zones ina jumla ya maeneo ishirini na nne ambayo yametangazwa kuwa Maeneo Maalum ya Uwekezaji (Special Economic Zones). Serikali imeendelea na jitihada za kuanzisha Kanda Maalum za Kiuchumi katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kuchochea ukuaji wa uchumi. Katika kufanikisha azma hiyo, Mamlaka ya EPZ imekuwa ikizihamasisha Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kutenga na kuwezesha uendelezaji wa maeneo ya Special Economic Zones.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya EPZA iko tayari kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Njombe Mjini na Uongozi wa Mkoa wa Njombe kufanikisha uanzishaji wa Kanda Maalum ya Kiuchumi katika Mkoa huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukiongezea mtaji kiwanda cha Kahawa cha TANICA?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Jimbo la Muleba Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua mwenendo wa kibiashara usioridhisha wa Kiwanda cha Tanganyika Instant Coffee Company Limited (TANICA) unaochangiwa na changamoto ya ukosefu wa mtaji, uchakavu wa mitambo, matumizi ya teknolojia iliyopitwa na wakati na kiwanda kuwa na madeni makubwa. Kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, Serikali imefanya upembuzi yakinifu wa mahitaji ya rasilimali fedha kwa ajili ya kuendesha kiwanda hicho, ambapo imebainika kuwa zinahitajika takribani dola za Marekani milioni 1.31.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali inafanya mashauriano na wanahisa wa kiwanda ili wawekeze kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kukiboresha na kuendesha kiwanda hicho. Serikali ina nia ya dhati kuhakikisha kuwa kiwanda hicho kinafanya kazi kwa ufanisi na tija ili kuendeleza zao la kahawa ambalo linalimwa kwa wingi katika Mkoa wa Kagera, nakushukuru.
MHE.CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: -

Je, lini Serikali itafufua Mradi wa Chumvi Ivuna – Itumbula Momba?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe, Mbunge wa Jimbo la Momba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Chumvi cha Itumbula kilichopo Kata ya Ivuna Wilaya ya Momba kilianzishwa na wananchi ambao wameungana pamoja kutoka Kijiji cha Ivuna na Itumbula ili kuanzisha mradi wa kuzalisha chumvi kwenye bwawa la maji ya chumvi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua juhudi na jitihada za Wananchi wa Kijiji cha Itumbula na itahakikisha kuwa kiwanda hicho kinaanza uzalishaji. Serikali imeshatoa Shilingi milioni 120 kwa kuelewa kuwa ni mradi wa kimkakati lakini pia Halmashauri ya Wilaya ya Momba imetoa shilingi milioni 50 ili kusaidia katika kutekeleza mradi huo.

Mheshimiwa Spika, aidha mikakati ya Serikali ni kuhakikisha tunahamasisha wawekezaji wengine kuwekeza katika kiwanda hicho.
MHE. NORAH W. MZERU aliauliza: -

Je, ni lini Kiwanda cha Mazava Winds Group – Morogoro kitapatiwa eneo kubwa la uwekezaji?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Mazava Fabrics and Production East Africa Limited kinajishughulisha na uzalishaji wa nguo. Kiwanda hiki kipo chini ya mamlaka ya EPZ na kinafuata taratibu za uwekezaji zilizowekwa na Mamlaka hiyo. Kiwanda hiki kinatumia majengo ya kupanga kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya EPZ kwa kushirikiana na Mkoa wa Morogoro waliwezesha kupatikana kwa eneo la uwekezaji linalofahamika kwa jina la Star City lililopo Manispaa ya Morogoro, lenye ukubwa wa mita za mraba 20,000. Mwekezaji alikubaliana na eneo hili kuwa linafaa kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, vilevile Mkoa wa Morogoro umetenga eneo la uwekezaji ambalo pia linafaa kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda liitwalo Kiyegera. Eneo hili linafaa kwa uwekezaji Mkubwa na Mdogo.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani Mkoa wa Mtwara umewekeza na unanufaika na uchumi wa Bluu?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kuufanya Mkoa wa Mtwara kunufaika na uchumi wa bluu, Serikali imeimarisha miundombinu ya Bandari ya Mtwara na kuifanya kuwa ndiyo kituo kikuu cha usafirishaji wa bidhaa na malighafi mbalimbali. Serikali pia imejenga Kituo cha uzalishaji wa mbegu za mazao ya baharini (majongoo bahari, pweza, kamba na kadhalika) ili kuwasaidia wananchi wa mkoa huo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA) inatoa mafunzo ya ufugaji wa majongoo bahari na kujenga vizimba vya ufugaji. Aidha, Serikali ya Mkoa wa Mtwara imeelekeza nguvu zake kwenye kilimo cha Mwani katika eneo la Naumo Wilayani Mtwara bila kusahau kilimo cha chumvi ya Bahari.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuvutia wawekezaji katika uchumi wa Bluu nchini hasa katika sekta za usafirishaji baharini, kilimo, uvuvi, na utalii kwa ajili ya mikoa ya pwani ukiwemo Mkoa wa Mtwara.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza: -

Je, Serikali imejiandaaje kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji nchini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kuna mazingira wezeshi Serikali imeendelea kutekeleza Mpango wa Kuboresha Mazingira ya kufanya Biashara Nchini (MKUMBI) lakini pia kuboresha sera na sheria mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako tukufu, Serikali ilitunga Sheria mpya ya Uwekezaji Tanzania ya mwaka 2022 ambayo pamoja na masuala mengine imeboresha na kulinda maslahi ya wawekezaji na uwekezaji, kuboresha huduma kwa wawekezaji katika kupata vibali na leseni mbalimbali kupitia mfumo unganishi wa kielektroniki katika kuhudumia wawekezaji, kuboresha utoaji wa vivutio vya kikodi kwa wawekezaji kwa kuongeza muda kutoka miaka mitatu hadi mitano na kutoa vivutio katika miradi ya upanuzi na ukarabati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia inaendelea kuboresha miundombinu wezeshi kama barabara, reli, bandari, viwanja vya ndege na umeme, nakushukuru.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kufufua jengo la viwanda vidogo vidogo – Lwosaa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha tathmini ya jengo hilo na kupata gharama za ukarabati wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo ambazo ni jumla ya shilingi 293,986,850. Pia Serikali kupitia SIDO inaendelea kufuatilia suala la umiliki wa eneo hilo ili kuanza ukarabati na kumalizia ujenzi. Aidha, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati na kukamilisha ujenzi wa jengo hilo ili shughuli kusudiwa zianze kufanyika kwa manufaa ya wananchi wa Lwosaa na Taifa kwa ujumla. Nakushukuru.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza: -

Je, kuna mpango gani kufanya utafiti na kurasimisha pombe ya mwiki inayotokana na mabibo ili kuongeza thamani ya zao la korosho?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto kadhaa zinazowakabili wazalishaji wa pombe za kienyeji hivyo kushindwa kukidhi matakwa ya viwango na kukosa ithibati ya ubora, Serikali kupitia Shirika la Viwago Tanzania (TBS) pamoja na Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) imeweka utaratibu wa kutoa mafunzo kwa wazalishaji wa pombe za kienyeji kuhusu matumizi ya teknolojia bora na matumizi sahihi ya viwango katika kuzalisha pombe za kienyeji ikiwemo pombe aina ya mwiki ili ziweze kukidhi viwango vinavyokubalika na hivyo kuruhusiwa kuingia sokoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia mwezi Oktoba, 2022, jumla ya leseni 43 za ubora zimetolewa kwa bidhaa mbalimbali za pombe za kienyeji, na maombi mengine mapya 22 yapo kwenye hatua mbalimbali za tathimini kuelekea kwenye kupata ithibati ya ubora. Aidha, Serikali kupitia Shirika la Viwango Tanzania itaendelea kutengeneza viwango vya pombe za kienyeji kwa kadri mahitaji yatakavyojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. SYLVIA F. SIGULA aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kuwawezesha wajasiriamali kwa kuwapatia ujuzi na mafunzo?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sylvia Francis Sigula, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo nchini (SIDO), lenye ofisi katika Mikoa yote nchini hadi kufikia Februari 2023, imeratibu na kutoa mafunzo na ujuzi kwa wajasiriamali wapatao 12,091, ambapo wanaume walikuwa 5,082 sawa na asilimia 42 na wanawake 7,009 sawa na asilimia 58 kupitia kozi 519 katika maeneo mbalimbali yanayohusiana na uendelezaji wa biashara na shughuli za uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imepanga kutoa mafunzo na ujuzi katika nyanja mbalimbali kwa wajasiriamali nchini. Aidha, Serikali imepanga kuongeza wigo wa kutoa mafunzo ya biashara na ufundi pamoja na ushauri kwa kutumia TEHAMA. Nakushukuru.(Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA aliuliza: -

Je, nini mpango wa Serikali kufufua Kiwanda cha Maziwa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto za kiwanda cha maziwa Njombe Milk Factory Company Limited na Serikali kupitia uongozi wa mkoa imekwishaanza kuchukua hatua za kukikwamua kiwanda hicho. Hatua za awali zilizochukuliwa ni pamoja na kuwakutanisha wanahisa wa kiwanda na uongozi wa Mkoa wa Njombe.

Aidha, ninapenda kumuahidi Mheshimiwa Mbunge kuwa, kwa kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Njombe, Serikali itahakikisha kiwanda hicho kinaweza kufufuliwa kwa haraka ili sekta ya viwanda vya maziwa izidi kukua na kuleta manufaa kwa wafugaji na wanahisa, ninakushukuru.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kutoa mwongozo kwa wawekezaji kuchangia shughuli za maendeleo katika maeneo wanayowekeza?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wawekezaji wanachangia shughuli za maendeleo za jamii katika maeneo wanayowekeza, Serikali ina sheria za kisekta na miongozo inayosimamia wawekezaji katika sekta ya uziduaji ambayo ni mwongozo wa ushiriki wa Watanzania katika sekta ndogo ya mafuta 2019, mwongozo wa kuwasilisha mpango wa ushiriki wa Watanzania katika sekta ya madini wa mwaka 2018 na mwongozo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhusu uwajibikaji kwa jamii wa makampuni wa mwaka 2022. Aidha, Serikali iliandaa mwongozo wa Taifa wa ushiriki wa Watanzania katika sekta mbalimbali wa mwaka 2019 kwa ajili ya kusimamia masuala ya ushiriki wa Watanzania katika miradi ya kimkakati na uwekezaji. Utaratibu huo unaruhusu wawekezaji kuchangia sehemu ya mapato yake kwa jamii ikiwa ni sehemu ya uwajibikaji kwa jamii na kuchangia shughuli za maendeleo katika eneo la uwekezaji kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa. Nakushukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, Wamachinga wangapi wamefuzu kuwa Wafanyabiashara rasmi kwa kipindi cha kuanzia 2016 hadi 2021?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA, alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia Machi, 2023 kuna jumla ya Machinga 1,987,361 nchini. Aidha, kwa sasa Serikali inaanda utaratibu wa kuwatambua Wamachinga waliofuzu kuwa wafanyabiashara mara baada ya kurasimisha biashara zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuhamasisha urasimishaji wa biashara nchini kupitia njia mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya faida za urasimishaji biashara kupitia mafunzo mbalimbali ya biashara ya ujasiriamali. Mikakati iliyopo kwa sasa ni uanzishwaji wa vituo jumuishi vya urasimishaji wa biashara na uandaaji wa mwongozo wa taratibu za kurasimisha biashara nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kufufua Kiwanda cha General Tyre na shamba la mpira Kata ya Mwaya-Kilombero?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga, Mbunge wa Kilombero, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Kiwanda cha Matairi Arusha, uko kwenye hatua ya kukamilisha taratibu za kuutangaza ifikapo mwezi Oktoba, 2023 ili kuweza kumpata mwekezaji mahiri mwenye mtaji na teknolojia ya kisasa inayohitajika. Mradi huu unatarajiwa kutangazwa ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mashamba ya mpira likiwemo shamba la Kilombero, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) imeendelea kuboresha uzalishaji wa mpira kwa kupanda miche mipya, kujenga miundombinu, kununua mashine za kugemea utomvu, uchakataji na vitendea kazi vingine ili kuongeza upatikanaji wa utomvu na mpira mkavu wenye viwango bora, nakushukuru.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha mafuta ya kula yanazalishwa kwa wingi nchini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeendelea kutekeleza mkakati wa kuendeleza Sekta Ndogo ya Alizeti na Chikichi ambayo ndiyo mazao makubwa yanayoweza kuzalisha kwa tija mafuta ya kula hapa nchini kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa mkakati huo, viwanda vipya, kama Qstec na Jeolong vimeanzishwa. Upanuzi wa viwanda kama Mount Meru Millers, lakini pia, Serikali imeongeza nguvu katika taasisi za utafiti wa mbegu na hivyo kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za alizeti na michikichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali inaelekeza nguvu zaidi kwenye kilimo cha kuzalisha mbegu bora, ili kukidhi mahitaji ya malighafi katika viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza: -

Je, Serikali inatambua gunia kuwa kipimo au kifungashio kwa mujibu wa Sheria?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo, The Weights and Measures Act (Amendment) Order, G.N. No. 725 of 2018, jedwali la 10 chini ya kifungu cha 2(b) cha Jedwali hilo ambacho kinasema mazao ya mashambani yatafungashwa kwa uzito usiozidi kilogramu 100. Pamoja na kuelekeza wauzaji au wanunuzi wa mazao kutumia mizani, Serikali haitambui gunia kuwa kipimo bali ni kifungashio.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nitoe wito kwa wadau wote kuepuka matumizi ya gunia kama kipimo kwani kwa kufanya hivyo ni kukiuka Sheria ya Vipimo, nakushukuru.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza:-

Je, lini Serikali itaviendeleza viwanda vya nyama na samaki Mkoani Rukwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uendelezaji wa sekta ya viwanda ikiwemo viwanda vya nyama na samaki katika Mkoa wa Rukwa na mikoa mingine nchini ni endelevu. Serikali inaendelea na juhudi za kuhamasisha uwekezaji wa viwanda vipya na uendelezaji wa viwanda vilivyopo katika sekta ya mifugo na uvuvi hususani viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya upatikanaji wa malighafi ya mazao ya mifugo na uvuvi inayovikabili viwanda vya nyama na samaki katika Mkoa wa Rukwa na mikoa mingine nchini. Kwa sasa Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka nguvu kubwa katika unenepeshaji wa mifugo pamoja na ufugaji wa samaki kwa kutumia vizimba, kutenga na kuboresha maeneo ya ukusanyaji samaki (collection centers) pamoja na minada ya mifugo ili kukidhi haja ya upatikanaji endelevu wa malighafi bora ya viwanda vya nyama na samaki nchini ikiwemo katika Mkoa wa Rukwa.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali inaendelea na juhudi za kukabiliana na tatizo la utoroshaji wa mazao ya samaki na mifugo kwenda nchi za jirani bila kufuata taratibu ili kukidhi mahitaji ya malighafi katika viwanda vyetu vya ndani. Hivyo, nitoe rai kwa wavuvi na wafugaji kuviuzia malighafi viwanda vyetu vya ndani ili viweze kukidhi mahitaji yake, nakushukuru.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa ithibati kwa baadhi ya pombe za kienyeji ambazo zimekidhi viwango?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe, Mbunge wa Jimbo la Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Mwezi Oktoba, 2022 jumla ya leseni 43 za ubora zimetolewa kwa bidhaa mbalimbali za pombe za kienyeji zilizokidhi viwango na maombi mengine mapya 22 yapo kwenye hatua mbalimbali za tathmini kuelekea kwenye kupata ithibati ya ubora. Aidha, Serikali kupitia Shirika la Viwango Tanzania itaendelea kutengeneza viwango vya pombe za kienyeji kwa kadri ya mahitaji yatakavyojitokeza, nakushukuru.
MHE. MWANTUM DAU HAJI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha na kuwainua kiuchumi wanawake wasiojiweza?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakusukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanzisha mifuko na programu za uwezeshaji kwa lengo la kuwawezesha na kuwainua wananchi kiuchumi wakiwemo wanawake wasiojiweza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) imeendelea kutekeleza Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - Awamu ya Pili kwa kuhawilisha ruzuku ili kuwawezesha wananchi wasiojiweza ikiwemo wanawake kupata mahitaji ya msingi ikiwa ni pamoja na kuwawezesha kujiunga kwenye vikundi na kuanzisha shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza wanawake wasiojiweza kutumia fursa za uwepo wa mifuko na programu za uwezeshaji ili kuanzisha na kuendeleza biashara zao, nakushukuru sana.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-

Je, lini mkataba na mwekezaji utakamilika ili Mradi wa Liganga na Mchuchuma uweze kufanya kazi na kuchangia pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imedhamiria kuona mradi unganishi wa Liganga na Mchuchuma unatekelezwa, kwa kuzingatia dhamira hiyo, hatua mbalimbali zimeanza kuchukuliwa ili kuanza utekelezaji wa mradi huo muhimu. Hatua hizo ni pamoja na kulipa fidia ya kiasi cha shilingi za Kitanzania 15,424,364,900 kwa wananchi 1,142 na kuanza upya majadiliano na mwekezaji wa mradi ili kuhakikisha kuwa mradi unatekelezwa pasipo kuleta hasara kwa Taifa, nakushukuru. (Makofi)
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza:-

Je, lini Serikali itawalipa mafao yao watumishi waliokuwa Kiwanda cha Magunia Moshi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kuwa Ofisi ya Msajili wa Hazina ilipokea madai ya waliokuwa wafanyakazi wa Kiwanda cha Magunia Moshi na kuyashughulikia kwa kuunda Kamati ya Uhakiki. Taarifa ya Kamati hiyo ilibainisha kuwa Watumishi hao walishalipwa mafao yao na kujulishwa kwa barua yenye Kumb. Na. CKB.87/406/02/C/80 ya tarehe 3 Mei, 2019. Hata hivyo, pamoja na kuwajibu, wadai wameendelea kuandika barua kwenda kwenye Taasisi mbalimbali za Serikali kuwasilisha malalamiko yao; na kwa upande wetu tumekuwa tukiwajibu na kutoa ufafanuzi kuwa walalamikaji hao walilipwa stahiki zao ipasavyo.
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuvutia Wawekezaji wa Viwanda vya kuchakata Madini ya chumvi Wilayani Kilwa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mkakati wa Serikali kuvutia wawekezaji katika sekta ya Chumvi unaendelea ikiwa ni pamoja na kutenga eneo lenye ukubwa wa hekta 168 katika Wilaya ya Kilwa kwa ajili ya wawekezaji wenye nia ya kuchakata madini ya chumvi.

Mheshimiwa Spika, Aidha, Serikali imeendelea kutoa vivutio mbalimbali vya kikodi na visivyo vya kikodi kwa uratibu wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kwa kushirikiana na Taasisi husika ili kufanikisha azma ya kuwekeza katika sekta husika kwa maana ya sekta ya madini.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua changamoto za Viwanda vya Nguo nchini kwani ni viwanda vitatu tu kati ya 33 vinafanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sekta ndogo ya nguo na mavazi nchini ina jumla ya viwanda tisa vinavyofanya kazi hivi sasa. Serikali inaendelea kutatua changamoto zinazokabili viwanda vya nguo, ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara nchini, kudhibiti bidhaa zisizo na ubora na bidhaa bandia kutoka nje ya nchi, kuongeza ushuru wa forodha kwa kanga na vitenge vinavyotoka nje ya nchi, kuhamasisha Taasisi za Umma na Watanzania kwa ujumla kununua bidhaa za nguo zinazotengenezwa na viwanda vya hapa nchini na kuweka miundombinu wezeshi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ENG STELLA M. MANYANYA aliuliza:-

Je, ni kwa nini Serikali isitoe rasilimali za Kiwanda cha Mang’ula Mechanical and Machine Tools kilichopo Kilombero kwa Taasisi za Ufundi kama DIT na nyinginezo ili ziweze kutumia?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA, alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Jimbo la Nyasa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeamua kukihuisha upya kiwanda cha Mang’ula Mechanical & Machine Tools Co. Ltd. kupitia Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ili kiendelee kutekeleza majukumu yaliyokusudiwa hapo awali. Ikiwa kutakuwa na haja ya kuzihusisha Taasisi za Ufundi Serikali itafanya hivyo.

MHE. CHARLES S. KIMEI aliuliza;

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa soko la Kimataifa katika eneo la Lokolova mpakani mwa Tanzania na Kenya?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA, alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Moshi imetenga eneo lenye ukubwa wa ekari 140 katika eneo la Lokolova kwa ajili ya ujenzi wa soko la mpakani. Hatua inayofuata ni kupata hati miliki ya eneo hilo na hatimaye kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya soko hilo, nakushukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Viwanda vya Mbolea nchini ili Wakulima waongeze tija?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA, alijibu: -

Mheshimwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na Mpango wa Kuratibu Uwekezaji wa Viwanda vya Mbolea Nchini. Matokeo ya uratibu huo ni pamoja na Kiwanda cha Mbolea cha Minjingu na ujenzi unaoendelea wa Kiwanda cha Mbolea cha Itracom Fertilizer Limited, Jijini Dodoma. Nakushukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA K.n.y. MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia wenye viwanda vilivyokufa au havifanyi kazi kwa sababu mbalimbali ikiwemo kiwanda cha kutengeneza mafuta ya kupikia cha Famili kilichopo Salasala katika Jimbo la Kawe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Askofu Josephat Mathias Gwajima, Mbunge wa Jimbo la Kawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali kupitia utekelezaji wa blue print ni kuhakikisha changamoto zote zilizokuwa zinavikabili viwanda visivyofanyakazi zinatatuliwa ili kuwezesha viwanda hivyo kufanya kazi ikiwemo kiwanda cha mafuta ya kupikia cha Famili. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. KHAMIS MBAROUK AMOUR aliuliza: -

Je, Serikali ina mikakati gani ya kuwasaidia wamachinga ili waondokane na umachinga na kuongeza mapato ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khamis Mbarouk Amour, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wamachinga ni fursa sahihi ya kujenga uchumi, Serikali itaendelea kusaidia wajasiriamali kifedha na kuboresha mazingira ya kufanyia biashara, miundombinu na kurasimisha wajasiriamali ikiwemo wamachinga. Nakushukuru.
MHE. TABASAM H. MWAGAO aliuliza:-

Je, lini Serikali itakarabati viwanda vya kuchambua pamba vya Nyakarilo, Nyamirilo na Buyagu vilivyopo Sengerema?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu la Mheshimiwa Hamis Mwagao Tabasam, Mbunge wa Jimbo la Sengerema, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, viwanda vya kuchambua pamba vilivyo na usajili wa Bodi ya Pamba hadi kufikia mwishoni mwa msimu 2022/2023 vilikuwa 92, na kati ya hivyo viwanda 57 vinamilikiwa na kampuni binafsi na 35 ni mali ya Vyama vya Ushirika.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha viwanda vyote vya kuchambua pamba vinafanya kazi. Serikali kupitia Bodi ya Pamba (TCB) mwaka 2020 ilifanya tathmini ambayo imewezesha baadhi ya viwanda vinavyomilikiwa na vyama vya ushirika kupata mikopo kupitia Benki ya Kilimo iliyowezesha kukarabati viwanda vyao. Kupitia utaratibu huo, Serikali itahakikisha pia viwanda vya Nyakarilo, Nyamirilo na Buyagu vinakarabatiwa ili kuongeza tija katika mnyororo mzima wa sekta ya pamba. Nakushukuru.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuelekeza taasisi zake kununua mashine na vipuri katika kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) imekifanyia ukarabati mkubwa Kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools (KMTC) ikiwa ni pamoja na kujenga tanuri la kuyeyushia chuma (Foundry), ukarabati wa miundombinu ya kiwanda na utengenzaji wa mtambo wa kuweka utando katika bidhaa za chuma ili kuzuia kutu (hot dip galvanizing plant).

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kuwa taasisi zake zinazotumia bidhaa na vipuri vinavyozalishwa na KMTC zinaingia mikataba ya kununua mashine na vipuri kutoka KMTC, nakushukuru.