Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Exaud Silaoneka Kigahe (11 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia afya ya kufanya kazi ya kujadili na kupitisha Bajeti za Wizara mbalimbali hapa Bungeni. Lakini pia kwa namna ya pekee, naomba niwashukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, wewe Mwenyekiti na Wenyeviti wenzako wenza, Wabunge kwa namna ambavyo mnatuongoza katika Bunge hili kwa weledi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nianze kwa kuunga mkono hoja ya bajeti ya Wizara na Viwanda na Biashara iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Profesa Kitila Alexander Mkumbo, Mbunge wa Jimbo la Ubungo ambaye ndiye Waziri wa Viwanda na Biashara. (Makofi)

Naomba pia Wabunge wenzangu wote tuunga mkono bajeti hii ambayo imezingatia miongozo mikuu ya Kitaifa hususan Dira ya Taifa, Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa ya Miaka Mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea baadhi ya hoja kidogo kulingana na muda. Lakini, hoja nyingine nitamuachia Mheshimiwa Waziri ambaye ndiye mwenye Wizara yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niongelee kuhusu ukaguzi wa bidhaa (destination inspection) hususan imeongelewa kuhusu magari hasa yaliyotumika. Utakumbuka kuwa ukaguzi huu sio mara ya kwanza sasa kufanyika katika nchi yetu, umeshakuwa unafanyika huku nyuma, lakini kutokana na baadhi ya changamoto ndiyo tulibadilisha baadaye kuanza kuwa na ile pre-verification of conformity to standards (PVOC) kwa maana ya kukagua nje bidhaa hizo kabla ya kuingia nchini na hasa magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuona changamoto ambazo tumekuwa tukizipata na Waheshimiwa Wabunge wanajua, kwanza kulikuwa kuna ukosefu mkubwa sana wa ufanisi katika ukaguzi wa magari yao huko nje. Kwanza tozo iliyokuwa inatozwa kodi zile zilikuwa nyingi, muagizaji alikuwa anatakiwa kulipa takribani dola 150 kwa ajili ya ukaguzi ule. Lakini zaidi ya hapo, usumbufu zaidi anapotuma kule, walikuwa wanatuma hela zaidi ya dola 100 kwa hiyo, unatuma dola 150 ya ukaguzi lakini pia unatuma na dola 100 kwa ajili ya handling ya yale makampuni ambayo yanafanya kazi ya ukaguzi kule. Kwa hiyo, unakuta mtu anatuma dola 250 badala ya dola 150. Kwa hiyo, gharama kubwa ya ukaguzi na upimaji ilikuwa ni moja ya changamoto ambazo zilikuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mawakala wengi kutokuwa na ofisi na hivyo kuwa na changamoto kidogo kwenye ukaguzi huo. TBS sasa imeanza kukagua magari hapa nchini kuanzia mwezi Machi, 2021 na hakika kazi hii inaenda vizuri na nikutaarifu tu na Bunge lako kwamba kazi ya ukaguzi wa magari yaliyotumika nje unaenda vizuri na baadhi ya changamoto za kawaida ambazo ndizo tunategemea kwa mfano sasa tunapokagua pale baadhi ya magari ambayo hayakidhi viwango yanapewa muda wa kwenda kutengenezwa, halafu yanarudishwa kupata ile certificate ya TRA. Tumeshapata eneo la UDA pale ambapo magari yale ambayo yanahitaji kutengenezwa yanakaa pale yakishatengenezwa taarifa zile zinarudishwa TBS, TBS wanapeleka TRA wanapata ile certificate ya ukaguzi wanaendelea. Nina uhakika asilimia 80 ya magari yaliyokuja sasa yako vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na utaratibu uliokuwepo sasa hivi ni kwamba TBS wanashirikiana na wameshatoa maelekezo kwa kampuni yanayouza magari kule nje kuhakikisha kwamba wanaleta magari yenye ubora. Kwa hiyo, na sisi tunatoa rai kwa waagizaji wote wa magari kutoka nje watumie kampuni ambazo zinafahamika. Wasiagize kwenye kampuni ambazo hazifahamiki kwa sababu zile kampuni zimeshapewa maelekezo ya namna ya ubora ambao tunautaka sisi kama nchi kwenye magari ambayo yanaingizwa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili suala la ukaguzi wa magari au bidhaa za kutoka nje, lengo kubwa ni kuhakikisha tunakuwa na bidhaa zenye ubora na hivyo tukishamaliza hili tutajiimarisha tayari zaidi ya shilingi bilioni 60 zimeshatengewa kwa ajili ya kuweka mitambo ambayo itafanya ukaguzi wa magari lakini baadaye kukagua bidhaa nyingine ambazo zinaingizwa kutoka nje. Kwa hiyo, lengo ni kuona kwamba bidhaa nyingi zinakaguliwa sasa nchini ili kuepuka baadhi ya kampuni huko nje kutumia udanganyifu lakini pia na wafanyabiashara wengine kuingiza bidhaa ambazo hazina ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameongelea kuhusu Electronic Tax System. Huu ni mfumo ambao ulianzishwa kwa ajili ya kukusanya kodi kwa njia za kielektroniki. Lengo kubwa la mfumo huu lilikuwa ni kukusanya kodi ya Serikali. Makampuni au wafanyabiashara wengi hasa wenye viwanda walikuwa na questionable integrity. Ndiyo maana Serikali ikaona sasa ili kuondoka na tatizo hili la kutokuwa waadilifu kwa wafanyabisahara integrity kati ya Serikali na wafanyabiashara ilikuwa chini. Kwa hiyo, tukaanzisha mfumo hu una ufanisi wa mufumo huu umekuwa ni mkubwa ambao kimsingi umdhibiti udanganyifu uliokuwepo unafanywa na wafanyabiashara wasio waaminifu ambao walikuwa hawaripoti taarifa kamili ili waweze kulipa kodi stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makusanyo kutokana na mfumo huu yameongezeka, lakini tukubali kwamba katika kufanya kazi yoyote au katika ufanyaji kazi huo kuna changamoto na changamoto kama ambavyo Waheshimiwa wameongelea ni kuhusiana na ile kampuni ambayo inafanya kazi hii kuchukua mapato mengi zaidi kuliko ambavyo Serikali inakusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikutaarifu tu kwamba Serikali sasa inafanyia kazi hili na kwa sababu tulikuwa tumekubaliana, tumeingia mkataba na ile kampuni, kwa hiyo, cha muhimu tunaona namna gani tutakavyofanya ili kuhakikisha baada ya mkataba ule kuisha basi tuweze ku-review ile kampuni, lakini pia ikiwezekana tufanye sisi wenyewe hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala unyaufu wa korosho; niliongelee kidogo hili. Ni kweli kuna changamoto hiyo lakini tumeshakubaliana kwamba sasa tunaenda kufanya utafiti ambao utaangalia namna gani tuweze viwango vya unyaufu katika korosho. Utafiti huo utaongozwa na TARI kwa kushirikiana pia na shirika letu la Tanzania Bureau of Standards, lakini pia na Bodi ya Korosho na Chuo Kikuu cha Sokoine, lakini pia na wadau wengine kwa maana ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Vyama Vikuu, TAMISEMI lakini pia na waendesha maghala. Kwa hiyo, hilo pia tuanenda kuliangalia ili tuweze kuona namna gani sasa ya kutatua changamoto hii ya unyaufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo pia kuhusu vifaatiba na dawa za binadamu. Limeongelewa kuhusu viwanda vya vifaatiba na dawa; tuna viwanda zaidi ya 14 sasa; kati ya hivyo, viwanda 12 vinatengeza dawa za binadamu lakini viwanda viwili vinatengeneza vifaatiba na vingine viwili vinatengeneza dawa za kinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kamati ya Kitaifa ambayo inaendelea na upembuzi yakinifu kuhusiana na uanzishwaji wa kiwanda cha vifaatiba katika Mkoa wa Simiyu. Kamati hiyo, iko katika hatua mbalimbali za kuona namna gani ya kuanzisha kiwanda hicho ikiwemo maoni ya hawa Waheshimiwa Wabunge ambayo leo wameyatoa nayo yataingizwa kwenye Kamati hiyo ya Kitaifa ili tuweze kuwa na uhakika sasa wa kuanzisha kiwanda hicho katika Mkoa wa Simiyu. Kusudi ni lile lile kuhakikisha tunatumia malighafi zilizoko nchini kwa maana ya pamba angalau zianze sasa kutumika katika viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba tena kuwasihi Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono hoja bajeti hii iliyobeba ajenda kubwa ya Kitaifa na hasa ujenzi wa Tanzania ya viwanda. Hakika, kazi hii ni kubwa na sote tuunge mkono ili iweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye hoja hii muhimu ya kuridhia Azimio la Eneo Huru la Biashara Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nianze kwa kuunga mkono hoja, na kimsingi kama ambavyo wajumbe wengi wamesema labda na mimi niseme tu kidogo. Eneo Huru la Biashara Afrika ni utaratibu wa pamoja wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Afrika unaolenga kuchochea uchumi na biashara miongoni mwa nchi wanachama.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kama walivyochangia wachangiaji wengi na kukubaliana na Azimio hili, lengo hasa litakuwa ni kufunguliana masoko ya biashara ya bidhaa na huduma, kuondeleana ushuru wa forodha, pamoja na kulegeza vikwazo na masharti mbalimbali ili kuhakikisha Afrika tunafanya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji wengi wamekubaliana, lakini wametoa baadhi ya maoni kwa upande wa Serikali. Na mimi kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba maoni haya tunayachukua na moja ya mikakati ambayo tunaenda kuitekeleza ni kuhakikisha tunaendeleza kuimarisha mazingira bora au wezeshi ya kufanya biashara katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika hilo kweli kulikuwa kuna changamoto kidogo, kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge, na tuliona baadhi ya hata wafanyabiashara wakubwa wakiondoka, wakiondoa mitaji yao na kuwekeza katika nchi zingine, lakini sasa baada ya maboresho yanayoendelea hasa kupitia blue print kama mlivyosema Waheshimiwa Wabunge tunaona tayari wawekezaji wengi wanaanza kurudi kuwekeza hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, maana yake hili ni move nzuri ambayo na sisi tuitumie nafasi hii sasa kuvutia mitaji mingi kwa kuweka mazingira wezeshi ili tuanze kuzalisha nchini na kuuza katika eneo hili la biashara la Afrika kwa faida zaidi kulingana na utaratibu tunaoendana nao sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, wameongelea kuhusiana na kuhakikisha sekta binafsi inawezeshwa au inashirikishwa. Hili tunalichukua na kuhakikisha kweli sasa tunaenda ku-engage; na kama ulivyosema wengine tayari sekta binafsi imeshasema faida kubwa ambayo wataenda kuipata au manufaa makubwa ya Tanzania kuridhia mkataba huu wa eneo huru la biashara Afrika, kwamba wao wataenda kufaidika Zaidi, na ni wengi wamesema.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tutaendelea kuimarisha uwezo wa uzalishaji wa ndani na hasa kwenye kukidhi viwango, kwa maana ya kuhakikisha unahamasisha uzalishaji wa tija kwenye bidhaa zetu lakini na mazao. Kama walivyosema wengine, kwamba angalau sasa bidhaa zetu na mazao yetu yawe shindani kulingana na soko la sasa, lakini hasa kwenye hili soko la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, wameongelea kuhusiana na sekta ya biashara ndogo, kwamba lazima hawa nao pia tuendelee kuwawezesha. Ni kweli, tuhakikishe sasa sekta ndogo kwa maana wajasiliamali waweze kuzalisha kibiashara kwa kuhakikisha kwamba vifungashio vyao vinakuwa vya viwango, lakini pia hata ubora; na hii tunaenda kuhakikisha tunafanya hivyo kwa sababu sasa hivi tunaenda kuandaa sera ya ubora. Tuwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba tutaenda kutekeleza au tutaingia tukiwa na nguvu katika soko hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa ujumla wake Waheshimiwa Wabunge wameongelea sana kuhusiana na umuhimu wa sisi kama Bara la Afrika kuanza sasa kuishi pamoja, kwa maana ya kufanya biashara pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli changamoto mojawapo kubwa sana katika kufanya biashara katika bara letu ni miundombinu. Kwa mfano; utakuta mtu anataka kwenda labda hata Kongo tu hapo, kama kwa njia ya ndege maana yake lazima uende Ethiopia au hata nchi za nje ili kesho yake ulale, uje Kongo, DRC. Sasa unakuta miundombinu hii ndiyo imekuwa na changamoto kubwa sana ya sisi kwenye kufanya biashara katika Bara la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo moja wapo ya vitu ambavyo vitaenda kutupelekea kuhakikisha sasa tunaimarisha miundombinu yetu hii ni moja ya fursa ambayo naamini, kama alivyosema Mheshimiwa Mwijage na mwingine, kwamba sasa miundombinu hii itajengwa kwa sababu tunajua tunakwenda kufanya biashara kati ya nchi na nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili pia, naona kwa mfano; hata kwenye njia tu za barabara watu wanaouza mazao mbalimbali ikiwemo hata mbao kupeleka Kongo badala ya kukatisha hapa tunaenda mpaka Zambia halafu uanze kurudi hivi. Maana yake kwa miundombinu hii inapelekea bidhaa zetu kuwa uncompetitive, kwamba zitakuwa sasa haziwezi kushindana na bidhaa hata za kutoka ulaya kwa sababu ya miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe, kama ambavyo wote wamekubali, kwamba tuunge mkono Azimio hili kwa sababu lina manufaa mengi kwa nchi yetu, lakini pia kwa Bara zima la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja hii muhimu ya Mheshimiwa Waziri wa uwekezaji viwanda na biashara. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema ambaye ametujaalia kukutana siku hii ya leo tukiwa na afya njema kuhakikisha tunapitisha Bajeti hii muhimu ya Wizara ya uwekezaji viwanda na biashara.

Mheshimiwa Spika, pili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini, niendelee kutumikia nchi hii katika nafasi ya Naibu Waziri katika Wizara ya uwekezaji viwanda na biashara.

Mheshimiwa Spika, tatu nishukuru sana viongozi wetu Wakuu, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu lakini pia nikushukuru sana na wewe Mheshimiwa Spika, Naibu Spika lakini na Wenyeviti wa Bunge hili lako tukufu kwa kuendelea kusimamia na kuhakikisha tunatekeleza na majukumu yetu vyema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Waziri wangu Dkt. Ashatu Kijaji Kwa kuendela kunisimamia vizuri na kunielekeza katika kutimiza wajibu wangu. Naanza kushukuru sana Kamati ya Kudumu ya Viwanda, Biashara Kilimo na Mifugo kwa namna

pekee mwenyekiti wetu Mheshimiwa Kihenzile lakini pia na Makamu na wajumbe wote. Pia kwa namna ya pekee niwashukuru sana wajumbe wa kamati lakini pia na waheshimiwa wote Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendela kushirikiana nasi katika sekta hii ya uwekezaji, viwanda na biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bajeti iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri imebeba dhamana kuu ya kuendeleza kasi ya uwekezji na ujenzi shirikishi na unganishi wa uchumi wa viwanda kwa kutambua nafasi ya sekta binafsi kama injini ya ujenzi wa viwanda na shughuli za ubia kwa sekta binafsi na umma na hii dhahiri kuwa mfumo huu na maboresho mengine yanayoendelea katika nchi hii ikiwemo utekelezaji wa mpango wa kuboresha mazingira ya biashara Mkumbi au blue print unalenga kuboresha mazingira ya biashara na kuchochea hali ya ujenzi wa uchumi wa viwanda na kuleta maendeleo endelevu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba sasa na mimi nichangie hoja kwa kutoa maelekezo au ufafanuzi kwa baadhi ya hoja zilizowasilishwa kuhusiana na Bajeti ya uwekezaji, viwanda na biashara kwa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda na Biashara Kilimo na Mifugo imetoa maoni mengi na maelekezo katika maeneo kadhaa na ambayo kimsingi mengine yameshatekelezwa na yanaendelea kutekelezwa ikiwa ni matokeo ya kazi kubwa ya kamati hii kutuwezesha sisi kama wizara kutekeleza majukumu hayo. Mosi, ni kuhakikisha tunalipa fidia ya eneo lile la mradi huu mkubwa ambao umeongelewa na wabunge wengi Mchuchuma na Liganga.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru Serikali ya Awamu ya Sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upenzi mkubwa kuhakikisha sasa anaweka historia kama ambavyo Wabunge wamesema kwamba sasa tunaweza kutekeleza mradi huu ametoa hizo fedha bilioni 15.4 ambazo zinaenda kulipa fidia ya wananchi wale ambao sasa ni hatua ya awali ya kutekeleza mradi ule mkubwa katika mkoa wa Njombe katika Halmashauri ya Ludewa. Ambapo tunaamini katika zoezi hili la kulipa fidia, mosi ni kitu kikubwa uchumi wa nchi hasa wana Ludewa, lakini pili tutatoa elimu ili fedha hizo malipo haya yanayolipwa yawe na faida yawe na manufaa ili wananchi wale waweze kutumia vyema na siyo baada ya hapo warudi tena kwenye umasikini kama ambavyo baadhi ya wabunge walisema katika maeneo mengine fidia hizi zikilipwa wananchi wale wanatumia fedha vibaya halafu wanarudi kwenye hali ngumu na kuwa masikini zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali.

Mheshimiwa spika, pili kulikuwa na suala la kiwanda la viuwa dudu. Tunajua changamoto kubwa ilikuwa ni kuona namna gani kiwanda kile kinaendela kuzalisha kadri ambavyo kilipangwa na sisi kama Serikali tumeishakubaliana kupitia Wizara ya Afya lakini na wenzetu TAMISEMI kuhakikisha lile soko la awali ambalo ni sisi watanzania kutumia dawa zile zinatumika na katika mwaka huu wa fedha tunaenda kutekeleza hayo lakini zaidi tunatafuta masoko ya nje, zaidi na haya yameshaanza na tumeanza kuuza katika badhi ya nchi dawa hizi katika nchi za majirani kwa upande wa SADC na EAC na tunaamini kiwanda hiki kwa mwendo huu wa mauzo sasa na utaratibu unaokwenda kwa kuzalisha viuwa wadudu lakini viwatilifu na amini kwa kuwa sasa fedha zimeanza kupelekwa katika kiwanda hiki na uzalishaji umeanza na kwa historia ya kwanza walikuwa wanapewa fedha na Serikali.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi kuanzia mwaka huu wa fedha wameanza kujilipa wao kutokana na mapato ndani ya kiwanda hicho, kwa hiyo tunaamini huko tunakokwenda tukikamilisha haya tutaweza kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini kulikuwa na hoja ambazo Kamati ya Kudumu ilielekeza kuhusiana na eneo la Engaruka nalo hili tunalifanyia kazi na kutakuwa na fidia kwa wananchi zaidi ya 599 ambao tukisha kamilisha uhakiki kama ambavyo tumeanza kwenye Mchuchuma na Liganga na huku pia tutaenda kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, vilevile kulikuwa na hoja ya nini tunafanya kuhakikisha Shirika letu la Maendeleo la Taifa NDC wanaendelea kutimiza wajibu wao au uwepo wao. Nitoe taarifa kwamba Shirika letu la Maendeleo ya Taifa NDC kwa sasa lina jumla ya miradi 13 ambayo moja ni hili la Mchuchuma na Liganga lakini kuna Mradi wa Engaruka Soda ash au Magadi ya soda lakini Maradi wa Makaa ya Mawe Ngaka ambako ndiyo kuna ile Kampuni ya Tancol Mheshimiwa Kapinga amesema.

Mheshimiwa Spika, pia tuna Mradi wa Chuma Ghafi cha Maganga Matitu lakini tuna kongane za viwanda lakini zaidi pale TAMCO, Nyanza Grass, Kange na KMTC lakini pia tuna Kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools pale kwa Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, tuna Kiwanda cha Mang’ula Mechanical Machine Tools ambacho hiki kilikuwa mboni ya viwanda vile ambavyo vilikuwa vimebinafsishwa amavyo tumevirudisha Serikalini kikasimamiwa na Shirika letu la Maendeleo ya Taifa NDC lakini pia tuna Mradi wa Bandari Kavu ambao unaendelea lakini pia Kiwanda hiki cha Viua dudu pale Kibaha na Mradi wa Umeme wa Solar Singida, Mradi wa Upepo Singida lakini pia tuna Mashamba ya Kihui na Kalunga ambayo ni Mashamba ya Mpira.

Mheshimiwa Spika, katika miradi hiyo 13 miradi ambayo inaenda vyema kwa sasa au tunatekeleza kwa hatua ya awali ni mitano ambayo inafanya kazi ikiwemo ni kongane za viwanda pale TAMCO Nyanza grass kiwanda cha Machine Tools Mradi wa Bandari Kavu lakini pia Kiwanda cha Viua dudu na Mashamba ya Mpira ya Kiuwi Muheza Mkoa wa Tanga lakini pia Kalunga Kilombero Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kuanzisha Kituo cha Ugavi wa Biashara cha Kurasini au Kurasini Logistical Centre. Ni kweli mradi huu ulikuwa utekelezwe chini ya Wizara lakini ninyi ni mashahidi kutokana na msongamano mkubwa pale bandarini, kwa hiyo, kulikuwa na maelekezo maalum kwamba sasa lile eneo liweze kutumika katika upanuzi wa huduma ya bandari pale Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, lakini mradi ule bado unaendelea na dhamana ya kuendeleza mradi ule ni kuhakikisha kituo hicho cha bishara ya ugavi kinafanya kazi chini ya mamlaka yetu ya EPZ. Na dhamira hiyo bado ipo kwa sababu, tulikuwa na changamoto na sasa bado tunayo changamoto ya masoko ya mazao ya kilimo ikiwemo chai.

Mheshimiwa Spika, na kwa sababu hiyo, mradi huu mpango wake ni kuhakikisha tunatumia eneo lile la Bandari Kavu la Kwala, ambapo kule sasa kutakuwa pamoja na viwanda vingine, lakini pia kutakuwa na hii agro-processing na mambo mengine ambayo yatatekelezwa katika eneo lile la Kwala. Kwa hiyo ule mradi haujafa, lakini tumehamisha eneo kwa sababu ya umuhimu wa Bandari yetu pale Dar-es-Salaam ili iweze kufanya kazi vizuri kupunguza msongamano ambao nao ni changamoto kubwa katika kuhakikisha uchumi wa nchi hii unasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya lumbesa. Nitoe taarifa, kulingana na kanuni na sheria kwa kutumia Sheria ya Vipimo Sahihi na Kanuni za Ununuzi na Uuzaji wa Mazao, The Weight and Measures Act, tunataka vifungashio visizidi kilogram 100 pamoja na kiasi cha uhimilivu asilimia kama tano. Na kwa mujibu huo kwa hiyo maana yake tafsiri sahihi ya ufungashaji ni kwamba tusifungashe tofauti na vifungashio ambavyo vimewekwa, iwe ni kilo 100 au ni chini ya hapo.

Mheshimiwa Spika, na kwa sababu hiyo, tumesema lumbesa, kwa maana ya kuongeza kilemba au kofia ni marufuku kwa sababu inaleta dhana potofu ya kuwalinda au kuwanyonya wakuluma au wazalishaji wa mazao katika nchi yetu. Kwa hiyo tutahakikisha tunasimamia sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, tumeshakubaliana Wizara yetu, Wizara ya Kilimo na wenzetu TAMISEMI, ambao wao ndio wako kule kwenye masoko, kuhakikisha tunakuwa na collection centers au masoko, maeneo ambako kutakuwa na uuzaji wa bidhaa au mazao haya ili kuhakikisha vipimo sasa, ili Wizara yetu kupitia wakala wa vipimo wawe na mizani pale ambayo itawasaidia kupima mazao haya yanayouzwa kwa wakulima au kwa wanunuzi badala ya wanunuzi kwenda mashambani kwa wananchi au wakulima na kuwanyonya. Kwa hiyo, hili ni elekezo; na tumekuwa na fine kadhaa kwa wale ambao wanakiuka sheria hii.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala la uhuishaji wa leseni. Kwa mujibu wa Sheria ya Leseni za Biashara, leseni zote za biashara kundi A na B zinatakiwa kuwa hai muda wote. Kwa hiyo, kwa sasa tunahuisha kwa sababu ziko manually, tunakokwenda tutaenda kwenda automation kwa maana ya kuwa electronic. Hiyo itatusaidia kuhakikisha tunafuatilia kwa urahisi zaidi. Tunaamini hata kama kutakuwa na gharama basi itakuwa ni ndogo zaidi kuliko hivi sasa, lakini badaye kadiri maendeleo yanavyoenda tunaamini hii tutaitoa ili kuhakikisha biashara inafanyika vema na kupunguza usumbufu kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala la uingizaji wa bidhaa mbalimbali, vikiwemo vyakula hapa nchini, kuhakikisha tunasimamia ubora wa bidhaa hizo. Ikumbukwe kuwa madai ya uwepo wa mchele wa plastic si jipya na lilishakuwepo hata huko nyuma, lakini kupitia taasisi yetu, shirika letu la viwango, tumepitia na kubaini kwamba bado si taarifa sahihi. Lakini tutaendelea kufanya hivyo pamoja na vyakula vingine au bidhaa nyingine ambazo hazina ubora ili viweze kukidhi viwango ambavyo tumejiwekea kama nchi na kuhakikisha wananchi hawadhuriki kutokana na bidhaa ambazo hazina viwango.

Mheshimiwa Spika, kuliongelewa kuhusu masuala ya ubunifu. Nitoe taarifa kwamba, kulingana na mwongozo wa ubunifu ambayo ni Sheria ya COSTECH, Sura ya 5, ambao wameanzisha Mfuko wa Taifa wa Uendelezaji wa Sayansi na Teknolojia; mfuko huu tayari umesaidia wajasiriamali wengi kupitia COSTECH, lakini pia TIRDO; na Waheshimiwa Wabunge wengine wamefika pale TiRDO; tunawalea vijana hawa. Kuna wengine ambao kwa mfano wabunifu wa mita za maji, hapa Dodoma, Mvumi, lakini pia kuna wengine wazalishaji wa mbolea ambayo inatumika kwenye parachichi na wengine. Tunaamini Serikali inaendelea kuwapa motisha na kuwapa fedha, na wengine wamepata fedha kupitia Global Fund, ambao wanajihusisha na utekelezaji wa ubunifu mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi tunaendelea kuwalea wabunifu na tutaendelea kuhakikisha wanapata uwezeshaji zaidi kadiri ambavyo tunaendelea na maboresho haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kulinda viwanda vya ndani. Lazima sisi kama nchi tujielekeze kuhakikisha tunalinda viwanda vya ndani. Na sisi kama Wizara tumeshaanzisha mchakato wa maandalizi ya Sera ya Taifa ya Ushiriki wa Watanzania kwa maana ya a local contents policy.

Mheshimiwa Spika, sasa kuliongelewa kuhusu kiwanda cha magari pale…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa hiyo, tunaenda kuwalinda wazalishaji wa ndani.

Mheshimiwa Spika, lakini nimalizie kidogo kuhusu hoja ya pombe zinazotengenezwa kienyeji. Kama utaruhusu kwa dakika moja niweze kuelezea kidogo nini tunafanya. Kwa mujibu wa viwango vya pombe kali, pombe kali inapaswa kuwa na kiwango cha pombe, ethanol, kuanzia asilimia 37 hadi 42 volume, ambayo inammanisha kwamba mchanganyiko wa pombe na maji na haipaswi kuwa kiwango kikubwa zaidi ya hapo. Sisi kama Wizara tumeendelea kusaidia wazalishaji wa pombe hawa wa ndani, wa kienyeji, wengi ikiwemo na mimi kule nyumbani kuna pombe ya ulanzi, tayari wameshapata ithibati ya kutengeneza. Pia kuna Kampuni moja ya Businde Distillers, Rubisi, kule karagwe, tayari wamepitishwa kupitia Wizara hii kwa kusaidiwa na TIRDO, TBS na SIDO, ambao wanawasaidia.

Mheshimiwa Spika, tunaamini wajasiriamali wengine kupitia SIDO wajiandikishe na sisi tutaendelea kuwasaidia kuhakikisha kwamba nao wanazalisha kwa tija, ili kuondokana na dhana kwamba hatuwalindi wazalishaji wa ndani na hasa kwenye sekta hii ya vinywaji ambayo inachangia pato kubwa sana la Taifa kwa maaba ya kodi katika uchumi wetu wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda na mimi nakushukuru sana kunipa nafasi. Baada ya kusema hayo machache naomba kusema naunga mkono hoja na ninaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuweze kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri, ili tuweze kutekeleza majukumu yake katika mwaka wa 2023/2024. Naomba kushukuru kwa nafasi hii. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza na mimi nichukue nafasi hii kukushukuru sana na kukupongeza kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi kuwa Naibu Spika wetu katika Bunge hili tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara nipende kwa namna ya pekee kushukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Wajumbe wote kwa vile ambavyo wanatupa ushirikiano katika kuhakikisha kwamba tunatekeleza mipango ya Serikali, na hivyo basi imekuwa desturi ya Kamati hii kutushauri kwa umakini mkubwa kwa nia ya kuhakikisha kwamba tunatekeleza masuala mbalimbali yanayohusu Sekta ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kwa weledi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inathamini sana ushauri wa Kamati hii, na tutandelea kufanya nao kazi kwa ukaribu kuhakikisha yale ambayo wanatuelekeza tunayatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara tunaendelea kupitia sera zetu, kuanzia Sera ya Uwekezaji, Sera ya Viwanda Vidogo (SMEs) na biashara ndogo na biashara ili ziendane na mazingira ya sasa ikiwa ni pamoja na kujumuisha vipaumbele na mipango ya maendeleo ya Taifa kwa ajili ya mabadiliko yanayoendelea katika dunia ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara tunatekeleza mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba tunatekeleza blue print. Baadhi ya vitu ambavyo vimelalamikiwa sana ni kuwa na sehemu moja ya kuhudumia wawekezaji. Tanzania tunatengeneza sasa kitu inaitwa Tanzania Electronic Investment a single window ambayo hiyo itawezesha sasa wawekezaji kuwa na sehemu moja ambako watapata huduma nyingi ambazo zinatolewa na taasisi zetu. Kwa kuanzia tutaanza na BRELA, TIC na TRA ambazo zitaunganishwa pamoja katika mfumo huo ili kupunguza usumbufu kwa wawekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunaendelea pia kuhamasisha ujenzi wa viwanda vidogo kwa maana ya kuwa na kungani za viwanda ambazo zitasaidia sana, unajua sekta kubwa ya viwanda ni viwanda vidogo, vya kati, lakini pia hatusahau viwanda vikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali tunaendelea kuhakikisha tunaweka mazingira wezeshi ili kuwe na ujenzi wa viwanda katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunaangalia pia kwa namna ya pekee kuona mifuko ya kuwezesha wajasiriamali inaongezewa fedha, lakini kuhakikisha pia inaboreshwa kwa kuunganishwa ile ambayo inawezekana ili iweze kuwa na tija kwa ajili ya kuwasaidia wajasiriamali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa hili muhimu sana la utekelezaji miradi ya kimkakati ambayo imeongelewa sana. Nia ya Serikali hasa ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu mpendwa Samia Suluhu Hassan, ameelekeza tuone sasa namna ya kukwamua miradi hii mikubwa ambayo itakuwa na impact kubwa sana katika maeneo ya nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuhakikishie tutaenda kuishughulikia kwa haraka iwezekanavyo, lakini kwa kuangalia kwa weledi ili kuhakikisha tija na manufaa ya nchi nzima kwa kizazi hiki na vizazi vijavyo ili utajiri huu na maliasili hii tuliyonayo katika hii miradi ya kimkakati ambayo iko chini ya sekta hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara inakuwa na tija kwa ajili ya maendeleo endelevu ya nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini pia nashukuru Kamati na Wabunge wote ambao wametushauri, ushauri wao tunaenda kuufanyia kazi ili kuhakikisha tunaendelea kuhakikisha tunajenga uchumi wa viwanda kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii. Nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia katika taarifa hizi za kamati hizi mbili ambazo zimeletwa mbele ya Bunge lako. Kuna mengi yameongelewa ambayo ni ya kujenga kwa hiyo niendelee kushukuru kwa michango mizuri ya Waheshimiwa Wabunge lakini mahususi kwa kamati hizi mbili ambazo zinaendelea kuhisimamia na kuielekeza Serikali katika kutekeleza majukumu yake mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, yameongelewa mengi lakini kubwa ni kuona namna gani kuboresha au kuziwezesha taasisi ambazo zinatoa huduma katika maeneo tofauti tofauti ikiwemo taasisi yetu ya ABZA CAMATEC, SIDO, TEMDO, TIC na taasisi zingine ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ukamilifu. Tunachukua mawazo haya ya Waheshimiwa Wabunge lakini kamati hizi mbili kwa umakini mkubwa kuhakikisha kwamba tunatekeleza majukumu hayo ili tuweze kunufaisha Taifa hili kupitia huduma zinazotolewa katika Taasisi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, imeongelewa suala la utekelezaji wa Blue Print ambalo Mheshimiwa Tarimba amemalizia sasa Serikali inaendelea kuhakikisha kutekeleza hilo lakini tunaangalia na mapungufu mengine ambayo yanaendelea kujitokeza wakati tunatekeleza. Siyo kweli kwamba tunafungia katika kabati lakini tunaendelea kutekeleza hatua kwa hatua na nikuhakikishie Bunge lako liwe na imani nia ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu mpendwa Samia Suluhu Hassan ni kuona tunaweka mazingira wezeshi na bora Zaidi ili kuwahakikisha sekta binafsi inakuwa ni kiongozi katika kujenga uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumeongelewa mambo mengi kuhusiana na miradi ya kimkakati ambayo inatekelezwa chini ya Taasisi zetu. Serikali inaendelea kufanya bidi na haraka zaidi lakini kwa uweledi ili miradi hiyo iweze kutekelezwa kwa haraka lakini kwa tija kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. Imeongelewa miradi ya Mchuchuma na Linganga, lakini kuhusu viuwadudu na mengine tutahakikisha tunatekeleza miradi hii kwa uweledi lakini kuona maslahi mabana ya nchi yanazingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Serikali tunachukua maoni yote na tuhakikishie Waheshimiwa Wabunge lakini kamati zetu mbili ambazo zinatusimamia kwamba tutatekeleza maoni yao na ushauri wao na tutaendelea kushirikiana nao kuhakikisha wanatekeleza majukumu ya kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kamati hizi mbili. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia katika hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, katika mijadala inayoendelea moja ya hoja kubwa ambayo imejadiliwa ni kuhusu mfumuko wa bei za bidhaa mbalimbali hapa nchini na hasa katika kipindi hiki ambapo tupo katika majanga mbalimbali ikiwemo iliyokuwa UVIKO pia na yale yanayoendelea huko katika nchi za Ukraine na Urusi.

Mheshimiwa Spika, changamoto hii ya mfumuko wa bei siyo ya Tanzania tu ni maeneo yote au dunia nzima na Serikali tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali kuona namna gani tunapunguza makali ya maisha ya wananchi katika kuhakikisha bidhaa nyingi zinapatikana kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, mwelekeo wa sera ya nchi yetu ni kuona tunaachia nguvu za soko huria katika kuendesha biashara. Hiyo haiachi jukumu la Serikali la kuhakikisha tunalinda ushindani wa haki kwenye soko pia kuhakikisha mlaji nae analindwa.

Mheshimiwa Spika, tutakumbuka sote kwamba bei za bidhaa mbalimbali kuanzia mbolea pia bidhaa muhimu kama sukari lakini pia na vifaa vya ujenzi, mafuta ya kula na kadhalika vilipanda bei sana, ilianza mwaka jana mwezi wa Desemba.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali tulianza kuchukua hatua za awali za haraka kuhakikisha tunapunguza makali hayo ambayo yanatokana na bei hizi kuwa juu.

Mheshimiwa Spika, moja ya vitu ambavyo tumefanya kwanza ni kukaa na wazalishaji kuongea nao hasa wale wanaoanzisha bidhaa za ndani. Bidhaa ambazo zilikuwa zimepanda bei sana mwaka jana na hata hivi karibuni zimeendelea nyingine ni pamoja na vifaa vya ujenzi. Mtakumbuka vifaa vya ujenzi vilikuwa vimepanda sana pia vinywaji baridi, tulipokaa na wazalishaji tulikubaliana na kuona maeneo mahsusi ambayo yalikuwa si sahihi na hasa kupitia Tume ya Ushindani ambao wanajukumu la kuhakikisha sheria ya ushindani inatumika kudhibiti vitendo vya kuvuruga mwenendo wa soko au bei ya bidhaa sokoni.

Mheshimiwa Spika, ninyi ni mashahidi Waheshimiwa Wabunge wataona kwamba bei za saruji angalau zimepungua kidogo, ingawaje bado tunaendelea kufanyia kazi lakini pia na bei za vinywaji baridi zilipungua lakini pia tunaendelea na kazi hiyo kwa sababu kazi ya kuhakikisha ushindani wa haki na kulinda mlaji ni endelevu siyo kazi ya siku moja.

Mheshimiwa Spika, hivyo tunaendelea kuhakikisha kwamba bei za bidhaa mbalimbali zikiwemo, sasa tumeona bei za vyakula vya kawaida kwa maana ya mchele, maharage na kadhalika navyo pia vimepanda bei. Moja ya changamoto tuliona katika kukaa na wazalishaji na wasafirishaji ilikuwa kwenye eneo la usafirishaji ambalo kimsingi tunaendelea kulifanyia kazi ili tuone ni namna gani ya kuhakikisha tunadhibiti upandaji holela wa bei za bidhaa katika soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mfupi ni hizo lakini pia hatua za muda wa kati ni pamoja na kuendelea sasa kuhakikisha tunaendelea kuweka vivutio au motisha maalum kwa ajili ya uzalishaji wa ndani, kuhakikisha tunawezesha viwanda vyetu vya ndani vinavyozalisha ili viweze kuendelea kuzalisha kwa tija, hii tumeendelea kuchukua hatua ikiwemo tarehe 25 Machi tuliweza kutia saini mikataba ya utekelezaji kati ya makampuni ambayo yapo kwenye miradi ya kimkakati au mahiri hii ikiwemo Intracom ambao wapo hapa Dodoma watazalisha mbolea, pia Bagamoyo Sugar ambao wataenda kuzalisha sukari pia Taifa gas, Kagera Sugar, Mtibwa Sugar na wale wenzetu NAFO ambao watazalisha Gypsum Board na Gypsum Powder.

Mheshimiwa Spika, hii mahsusi kuhakikisha uzalishaji wa bidhaa unaoweza kufanyika ndani ufanyike kwa tija ili kuhakikisha tunapunguza utegemezi wa kuagiza bidhaa kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha tunakuwa na uhakika wa kuwa na bidhaa hizi muhimu tunaendelea sasa kuhakikisha tunaweka mazingira wezeshi na bora ili tuweze kupata wawekezaji wengine kutoka nje kuhakikisha kwamba bidhaa nyingi tunakuwa na uwezo wa kuzalisha nchini badala ya kutegemea kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumeona kwamba mfumuko huu wa bei maeneo makubwa mengi yametokana na tunasema imported inflation ambao umetokana na kupungua kwa uzalishaji wa bidhaa mbalimbali huko nje, hata kwa malighafi ambazo zinatumika katika viwanda vya ndani lakini ambazo zinatoka nje, zile malighafi ambazo zipo ndani tutaona ni namna gani tutahakikisha tunaweka mazingira ili ziweze kuzalisha bidhaa ambazo zitakuwa hazina bei ghali.

SPIKA: Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja iliyoko mezani. Kwanza, tuweke wazi kwamba Serikali hatujazuia na hatujafunga wafanyabiashara kuuza mazao nje hasa zao hili la mahindi.

Mheshimiwa Spika, hoja kubwa ambayo Serikali tunakuja nayo ni kuona namna gani tunarasimisha biashara zote kwenye sekta zote ikiwemo hii ambayo imekuwa na changamoto kubwa sana, sekta ya kilimo, kwa maana ya zao hili la mahindi.

Mheshimiwa Spika, wewe ni shahidi, mwaka jana kama ambavyo wachangiaji wamesema kulikuwa na changamoto kubwa sana ya bei ya mazao mbalimbali ikiwemo mazao ya chakula kupanda bei na kukithiri vile ambavyo tumezoea. Sababu mojawapo ilikuwa ni hii ya kutokuratibu vizuri biashara ya mazao ya kilimo na hasa mazao ya chakula.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Serikali tunataka tuhakikishe kwamba tunarasimisha biashara zote ikiwemo ya kuuza mazao ya chakula ili wafanyabiashara waweze kuwa na bei nzuri ya kununua kwa wakulima. Kwa sababu kumekuwa na taratibu za walanguzi na hasa wengine kutoka nje ya nchi kwenda kununua kwa wakulima kule chini kwa bei ya chini ambayo haina maslahi wala tija kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, pili, tunataka tuone kwa uratibu huu maana yake na yule mkulima wa chini anakwenda kuuza kwa vipimo na si kwa zile njia ambazo tulizoea za lumbesa, ndonya, ndoo na kadhalika. Hii imeenda kumuumiza mkulima kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, la tatu, tunataka tu–formalize kwamba, sasa hawa wanaofanya biashara wawe na leseni na sasa hivi tumerahisisha kupitia kituo cha pamoja kutoa leseni ambazo zinawasaidia wafanyabiashara kufuata taratibu zote ili pia waweze kuchangia pato la Taifa katika kulipa kodi, lakini pia kumwezesha mkulima aweze kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, nne, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, tunadhani sasa ili kusaidia wakati huu kabla ya taratibu kukamilika, NFRA nao waendelee kununua kwa bei ambayo tunadhani itakuwa haimuumizi mkulima, lakini pia ni faida kwa mfanyabiashara ambaye atakuwa amefuata taratibu zote ili aweze kuuza kokote atakakoweza kuuza. Vile vile, hata mkulima mwenyewe, kuna wakulima ambao wana mazao ya kutosha wanaweza kuuza hata nje kama watafuata utaratibu huu ambao tumesema.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai kuweza kusimama hapa mbele na kuwasilisha bejeti hii; lakini kwa namna ya pekee nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini na kuendelea kufanya kazi kama Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara kumsaidia Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nipende kushukuru sana michango ya Waheshimiwa Wabunge kwa kuchangia kwa mtazamo chanya kwenye bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kuendeleza kutimiza adhma ya ujenzi wa uchumi wa Viwanda nami nasimama hapa ili niweze kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi kubwa na umakini ambao anaoufanya katika kuendelea Sekta hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Mheshimwia Mwenyekiti, bajeti iliyowasilishwa imebeba dhamira kuu ya kuendeleza kasi ya uwekezaji na ujenzi shirikishi na unganishi wa Uchumi wa Viwanda kwa kutambua nafasi ya Sekta Binafsi; kama ambayo Waheshimiwa Wabunge wameeleza kama injini ya ujenzi wa Uchumi wa Viwanda na shughuli za ubia kwa Sekta Binafsi ya Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kuwa mfumo huu wa maboresho na mengine yanayoendelea nchini likiwemo kutekeleza mpango wa kuboresha mazingira ya biashara kwa maana Blue Print unalenga kuboresha mazingira ya biashara na kushushia ari ya ujenzi wa uchumi wa viwanda na kuleta maendeleo endelevu katika nchi na wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya ya awali na mimi niweze kuchangia kidogo kwanza kwenye hoja zilizotolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira katika kuchangia bajeti hii. Kulikuwa na hoja kuhusu Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara ya TanTrade ambayo imechangiwa pia na Wabunge wengi sana, kuhusu kuona namna gani tunaweza kuisaidia ili kuhakikisha inatimiza wajibu wake kwa kufanya kazi ya kutafuta masoko ya bidhaa hasa mazao ya kilimo na bidhaa nyingine. Serikali inafanyakazi kubwa kuhakikisha tunawezesha taasisi zote ikiwemo hii ya TanTrade.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na katika bajeti hii tunayoendelea nayo sasa tulikuwa tumewapa fedha kidogo lakini mwaka huu tumeongezea kufikia bilioni 1.8 hii maana yake ni kuiwepo kwa dhamira njema ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu mpendwa Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha masoko ya bidhaa na hasa mazao ya kilimo yanapata masoko ya uhakika kwa kuhakikisha TanTrade inafanyakazi yake vizuri. Lakini Serikali itaendelea kuweka fedha zaidi kuhakikisha TanTrade inafanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kulikuwa na hoja kuhusu uandaaji wa kanzidata ya viwanda. Ni kweli Kanzidata ya viwanda ni moja ya matokeo ya utafiti na utambuzi wa viwanda ambayo huwa ni fursa kwa uwekezaji na wa rasilimali inayopata hapa nchini.

Kwa hiyo, kanzidata ni kweli itakuwa na taarifa sahihi za viwanda ikiwemo maeneo viwanda vilipo, ukubwa na uwezo wa viwanda hivyo na ajira ambazo zinatokana na viwanda hivyo. Lakini zaidi itaweza kutusaidia kujua malighafi zinazotakiwa kwa ajili ya kuzalisha bidhaa katika viwanda hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa taarifa hizo zitatusaidia pia kuona namna gani tunajua wapi kwa kuwekeza kwenye maeneo yapi, pia ambapo tunaamini yataleta tija. Sasa Wizara kupitia TIRDO tumeshaanza kazi hiyo kwa kushirikiana na taasisi zingine kama vile Ofisi ya Rais, TAMISEMI, NBS, BRELA na SIDO wanaendelea na uhakiki wa kukusanya takwimu za taarifa mbalimbali ambazo zitajumuishwa kwenye kanzidata ya viwanda katika Mikoa mbalimbali hapa nchini na sasa wameanza katika Mikoa ya Kanda ya Mashariki ikiwemo Morogoro na Mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja pia kwenye Kamati kuhusu uboreshaji wa mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji hapa nchini, ambao pia imechangiwa pia na Waheshimiwa Wabunge wengi. Wizara kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC) inakamilisha mfumo wa kielektroniki wa kutoa huduma ya mahali pamoja kwa wawekezaji (Tanzania Investment Electronic Single Window), ambayo itasaidia kuhakikisha tunaondoa baadhi ya changamoto na kupunguza urasimu usio wa lazima ambao umesababisha ucheleweshwaji kwa upatikanaji wa vibali kwa wawekezaji ikiwemo kujaza fomu nyingi na kujirudiarudia kwa sababu ya taasisi nyingi ambazo zinafanya kazi zinazofanana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo ni hoja chache kutoka kwenye Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie kidogo kwa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia katika bajeti hii hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate ambayo aliongelea kuhusu umuhimu wa kuwezesha Bodi ya Maghala ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa uhakika na kwa ufanisi zaidi. Ni kweli nasi Wizara na Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha tunawezesha Bodi hii iweze kufanya kazi yake. Kwa sasa hivi inasimamia baadhi ya shughuli lakini pia tutaleta nadhani maboresho ya Sheria kuona sasa inasimamia maghala yote nchini ili yaweze kufanya kazi zake vizuri, lakini tumeendelea kuwawezesha kwa kuwapa fedha zaidi kila mwaka ili waweze kukamilisha majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alisema hoja ya Bodi hii ihakikishe inaweza kujenga maghala kwenye vijiji na maeneo mengi. Nia ya Serikali ni kuona sasa tutashirikisha sekta binafsi ili nao waweze kufanya kazi zao vizuri lakini pia na sisi kama Serikali tutaendelea kuwezesha ujenzi wa maghala hayo maeneo tofauti tofauti na hasa vijijini ambako ndiko kuna haja kubwa ya kuwa na maghala haya ili wananchi waweze kuhifadhi mazao yao yawe katika ubora unaotakiwa lakini pia kuweza kudhibiti kupata bei bora ya mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Subira Mgalu kuhusu SIDO kuwezeshwa mitaji ya fedha lakini pia kuwezeshwa na vitendea kazi. Ni kweli SIDO ambayo ndio inahudumia viwanda vidogo vidogo na biashara ndogo ndogo kama Waheshimiwa Wabunge wengi walivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kuona sasa tunaimarisha sekta hii ya viwanda vidogo vidogo ili viweze kusaidia wananchi wengi zaidi kwenye ngazi ya chini ambako ndiko wananchi wengi wanashiriki katika kukuza uchumi wa nchi hii. Kwa hiyo, tutaendelea kuwawezesha SIDO na kuhakikisha teknolojia muhimu katika maeneo tofauti mikoani mpaka kwenye Halmashauri ili angalau zisaidie maendeleo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja ya kuhakikisha kufanya tathmini ya vile viwanda mia moja vya kila Halmashauri ambavyo tulikuwa tunaendelea navyo. Ni kweli tutaendelea kufanya zoezi hilo la utambuzi wa viwanda vile na kuhamasisha ujenzi wa viwanda vingine ili kuhakikisha kila Mkoa unapata fursa ya kuongeza thamani hasa kwenye eneo hili la mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja nyingine pia ya kuona namna gani tunaendeleza kuhakikisha tunahamasisha ujasiriamali. Kama nilivyosema SIDO ndiyo wanasaidia sana katika eneo hili lakini pia na vyuo vingine kama VETA na Taasisi zingine TCCIA na CTI ambao wapo kwenye sekta binafsi kuhakikisha tunawawezesha wajasiriamali katika elimu kwa maana ya ujuzi lakini pia teknolojia lakini na mitaji kuhakikisha nao wanashiriki vizuri katika kuendeleza sekta ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo naomba kusema tena naunga mkono hoja na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wote, tuunge mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri ili kuhakikisha Wizara inaweza kutimiza majukumu yake katika Mwaka, 2022/2023. Ninakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kutoa machache kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri katika kuridhia itifaki ya biashara ya huduma ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) ya mwaka 2012.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuendelea kutupa uzima na hadi leo kutufikisha hapa kujadili itifaki hii muhimu. Lakini pili nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kuendelea kutumikia nchi yangu katika nafasi ya Naibu Waziri katika Wizara ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuruni nanyi pia Viongozi wetu wa Bunge, wewe Mwenyekiti lakini Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote ambao mmeendelea kutuongoza vizuri hapa Bungeni lakini pia ushirikiano mkubwa mnaopata kutoka kwa Wabunge wenzetu katika kujadili masuala mbalimbali ambayo ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itifaki ya biashara ya huduma ni mwongozo unaotoa wajibu wa kila nchi mwananchama wa SADC namna ya kushughulikia sekta ya huduma katika nchi yake na hii ni matokeo kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema ni matokeo ya utekelezaji wa itifaki ya biashara ya mwaka 1996 ambayo nayo iliendelea kujadiliwa na utekelezaji wake ukaanza Januari mwaka 2000. Nasema hili kwa sababu kumekuwa na hoja ya kwamba labda sisi tumechelewa sana kuridhia itifaki hii ya huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutia saini itifaki hii mwaka 2012 pale Maputo Msumbiji kulikuwa na muda wa majadiliano katika nchi zote ambayo majadiliano hayo yalikamilika mwaka 2019. Kwa hiyo, katika muda huo ilikuwa kila nchi inafanya majadiliano ili kuona namna gani wataweza kunufaika au kushiriki katika itifaki hii ya huduma ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nchi zile kumi na moja ambazo zimeiridhia ni kwamba ni baada ya hapo. Kwa hiyo, ni takribani kuanzia mwaka 2022 takribani mwaka mmoja ndiyo utekelezaji hasa wa hii itifaki umeanza. Kwa hiyo, Watanzania, Waheshimiwa Wabunge hatujachewelewa ni muda muafaka lakini pia kuchelewa huko kwa mwaka mmoja ni muda mzuri ambao na sisi tumejitafakari kuona namna gani tunaweza kushiriki kikamilifu katika itifaki hii ya huduma au biashara za huduma katika Jumuiya ya SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na hoja nyingi sana ambazo zimetolewa hapa lakini muhimu kwanza nikuona namna gani tunaboresha sera zetu, sheria na kanuni lakini na mipango mbalimbali ambayo itawezesha sisi kama nchi kuweza kunufaika baada ya kuridhia itifaki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni hoja muhimu na sisi tumeishaanza kufanya hivyo pamoja na mambo mengine sera zetu zinauhushwa na ziko katika ngazi mbalimbali baada ya muda siyo mrefu italetwa hapa Bungeni ili nazo ziweze kupitishwa naamini hiyo itasaidia kuhakikisha tunapoanza baada ya kuridhia, naamini baada ya kuridhia itifaki hii zitatuwezesha kutekeleza vizuri maazimio ambayo yatakuwa yamepitishwa katika azimio hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na hoja muhimu sana ambayo sisi kama Serikali kuona namna gani tunawezesha sekta binafsi ili iweze kuwa shindani tuandae baada ya kuridhia itifaki ya biashara za bidhaa protocol on trade ya 2000. Sasa wafanyabiashara na wafanyabiashara na bidhaa mbalimbali lakini changamoto imekuwa katika sasa huduma kwamba sasa huduma kwamba mtu anaweza akawa anatoka na bidhaa zake hapa kupeleka Afrika Kusini lakini sasa hauwezi kusafirisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo tunayofanya sasa huduma hizi zilizopo ni baina ya nchi na nchi bilateral kama ni benki kati ya Tanzania na Burundi au DRC mfano hiyo lakini hizi ni bilateral agreement kati ya nchi na nchi au makampuni ama makampuni katika kufanyia biashara. Sasa tunataka tuseme katika Jumuiya tuweze kufanya makubaliano namna ya kushiriki katika huduma za biashara. Kwa hiyo, Serikali tunaona ni muhimu sana ndiyo maana nimeleta hapa turidhie ili tuweze kuwahusisha wafanyabiashara wetu waweze kufanya biashara zao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi haja kubwa, hoja kubwa ambayo imeelezwa ni namna ambavyo sisi kama nchi kama Serikali tunaendelea kutoa elimu kwa wadau mbalimbali ili kuweza kushiriki fursa zinazotokana na Jumuiya zetu zilizopo ikiwemo hii ya SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tunaendelea kufanya hivyo na tunaendelea kutoa elimu kwa wadau wote ikiwemo wafanyabiashara, sekta binafsi lakini pia kwa wananchi kwa ujumla ili wajue nini tunafanya kama Serikali ili kuhakikisha tunainua uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuweze kuridhia itifaki hii ambayo ni muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge sisi siyo kisiwa kwa hiyo hatuwezi kujetenga kusema tutashindwa, tutakaa peke yetu wakati wenzetu wanakwenda katika kuridhia itifaki hii na tayari nchi kumi na moja zisharidhia. Kwa hiyo, ni sisi ni muda muafaka baada ya kutathimini na kutafakari kwa kina tunaamini sasa ni muda muafaka kuridhia tuweze kuendelea na sisi kufaidika na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana, nakushukuru. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia katika bajeti hii ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea na juhudu za dhati za kuhakikisha tunafikia kujenga uchumi shindani na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu ambayo ni adhma ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kuungana na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha Daktari Mwigulu Nchemba ambaye kwa kweli anafanya kazi kubwa sana katika kuhakikisha nasi tunajenga uchumi wa viwanda ambao kimsingi unategemea ushirikishwaji kati ya Serikali na sekta binafsi na Serikali tumeendelea kufanyakazi kubwa ili kuweka maboresho mbalimbali ambayo tunaamini yanaendelea kusaidia kupunguza urasimu katika ufanyaji biashara lakini pia katika uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo nitumie nafasi hii kueleza kidogo kuhusiana na mpango wa kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji nchini ambayo Wizara yangu inaendelea kuratibu lakini kwa kushirikiana na sekta zote muhimu katika nchi hii ili kufikia azma ya kuwa na uchumi shindani kama nilivyosema na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2019 hadi 2023 jumla ya marekebisho 307 ambayo yameondoa na kupunguza tozo mbalimbali yamefanyika lakini katika kipindi hicho Sheria 48 zimefanyiwa marekebisho ambapo kwa mwaka 2022/2023 pekee zaidi ya Sheria 12 zilifanyiwa marekebisho ili kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumekuwa na maboresho jumla ya 105 yanayohusu ada, tozo na kodi mbalimbali ambazo zilikuwa kero katika kufanyabiashara na uwekezaji nchini lakini kubwa zaidi katika hili ni mfano wa usajili kuanza kutumia fedha za Kitanzania badala ya dola ambazo zimekuwa kero katika kuhakikisha tunatoa huduma kwa Watanzania. Moja ya mfano huo ni usajiri wa chakula cha watoto wachanga na formula za ukuzaji kabla ya maboresho ilikuwa inatumia dola za Kimarekeni 900 ambayo ilikuwa ni sawa na shilingi 2,120,400 lakini sasa tunatoza kwa shilingi milioni moja pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea pia kuboresha, kuondoa na kupunguza tozo katika maeneo mbalimbali muhimu, moja ni sekta ya kilimo, afya, mifugo, utalii pamoja na taasisi za udhibiti zilizoko hapa nchini. Pia maboresho mengine ni uimarishaji wa mfumo TEHAMA ambao Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia kwamba tuendelee kuboresha. Kwa mfano, sasa hivi mifumo 58 ya kutoa vibali na leseni zinatumia njia za kielektroniki katika mamlaka mbalimbali za udhibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mfumo wa malipo ya Serikali wa kielektroniki ambao umeimarishwa kwa maana ya GePG ambao unatoa huduma zaidi ya 900 ambazo zimeunganishwa na kurahisisha walipaji kodi na huduma mbalimbali wanazolipa Watanzania ili kupata huduma kutoka Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na mfumo unaowezesha mifumo mbalimbali ya Serikali kuwasiliana na kubadilishana taarifa, maana yake kulikuwa na hoja kwamba ndani ya Serikali hakuna mawasiliano lakini tunaendelea kuboresha, hadi sasa zaidi ya mifumo 50 katika taasisi 45 zimeweza kubadilishana taarifa ambazo zinasaidia ufanyajikazi ili kuhakikisha tunaendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo tumeendelea pia na kuanzisha sasa vitengo maalum, changamoto kubwa tuliyonayo ni katika ngazi za Halmashauri. Sasa tunaenda kuanzisha kitengo ambacho kitashughulikia masuala ya uwekezaji, viwanda na biashara ili shughuli hizo ambazo wengine wanalazimika kuja Makao Makuu kwa maana Wizarani sasa waweze kuapata huduma kule katika ngazi ya Halmashauri. Hii yote ili tuweze kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa matokeo ya haya ambayo tunaendelea nayo kumekuwa na angalau sasa kupunguza malalamiko kama si kumaliza, angalau tumepunguza kwa asilimia 71. Matokeo ya kupungua kwa siku za kuhudumia kwa mfano katika taasisi zetu, mfano OSHA wamepunguza muda wa kupata vibali kutoka siku 14 mpaka siku tatu. Pia muda wa kutoa leseni na kukabidhi matakwa ya Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kutoka siku 28 mpaka siku tatu, muda wa kupata cheti cha usajili wa sehemu za kazi kutoka siku 14 mpaka siku moja. Muda wa usajili wa hospitali binafsi kutoka miezi 12 hadi miezi mitatu. Muda wa usafirishaji wa mizigo umepungua kwa mfano kutoka Dar es Salaam mpaka Tunduma ilikuwa wastani wa siku saba na sasa hivi imeenda kuwa siku tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi tumepunguza kushughulikia maombi ya vibali vya kazi kutoka zaidi ya siku 14 hadi siku tatu mpaka saba. Pia tumepunguza mchakato wa ushughulikiaji wa maombi, mfano taasisi ya OSHA hatua ambayo imepunguza kutoka hatua 33 mpaka hatua saba, zaidi tumepunguza foleni ya kuomba huduma katika taasisi zetu ambazo zilikuwa ni foleni kubwa ukifika kwa mfano pale BRELLA na maeneo mengine utakuta msururu wa watu wanasubiri kupata huduma katika Taasisi za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka niseme haya kwa sababu kwa kweli pamoja na changamoto tulizonazo kwenye uwekezaji na viwanda wamesema hapa kuna viwanda vingine ambavyo vimefungwa lakini tunahakikisha sasa sababu zile au changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia Serikali tunazichukua kwa umakini kabisa ili tuendelee kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara ili nasi sasa tuendelee kuwa nchi shindani katika Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki lakini pia katika SADC lakini katika Eneo Huru la Biashara la Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeendelea kufanya marekebisho ya Sheria na Kanuni mbalimbali ambazo kwa kweli tunadhani ni muhimu katika kutekeleza shughuli za Serikali. Kwa mfano, Serikali imepitia na kurekebisha Sheria na Kanuni 12 hususani katika sekta za uwekezaji, viwanda na biashara, kilimo, ufugaji, afya na maliasili na hii imeenda kuboresha katika kuhakikisha tunaimarisha mifumo ya taasisi, kama nilivyosema tumeanzisha dawati au kitengo maalum cha viwanda, biashara na uwekezaji katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ngazi ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii muhimu, nashukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hii hoja muhimu ya Muswada huu wa Sheria ya Marekebisho ambao ni muhimu sana. Kwanza nianze kwa kuunga mkono mapendekezo yaliyowasilishwa katika Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, aidha, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: Umuhimu wa kutunga sheria hii mpya ya uwekezaji ulizingatia sana maoni ya wadau mbalimbali ambao ni wa ndani na nje ikijumuisha na taasisi za Kimataifa ikiwemo Benki ya Dunia na Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo (UNCTAD) ambao pia kwa vipindi tofauti wamekuwa wakifanya tathmini ya utekelezaji wa sheria yetu.

Mheshimiwa Spika, pia sheria hii ni sehemu ya utekelezaji wa blueprint. Wachangiaji wamesema wengi, na mimi niseme ile Blueprint for Regulatory Reforms to Improve the Business Environment in Tanzania, moja ya changamoto zilizokuwepo ni pamoja na kuwa na sheria na sera mbalimbali ambazo zimepitwa na wakati.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu wa sheria unachangia katika kuhakikisha tunaweka mazingira ambayo yanatabirika kwa wawekezaji wa ndani na wa nje katika nchi yetu. Katika Muswada huu tumeona kwa kuzingatia umuhimu wa Watanzania kupata au kuwekeza kwa kunufaika na vivutio hivi, moja ya maeneo ambayo yameangaliwa ni hayo na kupunguza mtaji au fedha zinazohitajika kupata vivutio kutoka Dola za Kimarekani 100,000 mpaka 50,000. Hii ni moja ya maeneo ambayo yameangaliwa katika Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka sheria hii kama walivyosema wachangiaji wengi, ni ya muda mrefu; ya tangu mwaka 1997 na katika kipindi hiki kuna marekebisho mengi yamefanywa na sasa ikafikia wakati kwamba hatuwezi kuendelea tena kurekebisha, kwa hiyo, lazima tulete itungwe upya kama sheria ya mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli moja ya maeneo ambayo yameangaliwa katika Muswada huu ni kuona namna gani tunaweka sheria hii iwe inatabirika. Moja ya viashiria vilivyokuwa vinavunja moyo wawekezaji hasa kutoka nje, ni kutokutabirika kwa sheria zetu. Ila katika Muswada huu tumeona wameweka sharti la muda wa mradi, miaka mitano. Maana yake mwekezaji akiwekeza anakuwa na uhakika kwamba katika muda ule aliyopewa wa vivutio wa miaka mitano, maana yake hakutakuwa na mabadiliko katika uwekezaji wake. Kwa hiyo, hili ni eneo ambalo wadau wengi walikuwa wanachangia kuhakikisha kwamba tunaboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Mheshimiwa Spika, sheria hii inaipa nguvu zaidi TIC. Waheshimiwa wachangiaji wa Muswada huu wamesema tuweke kama mamlaka. Ni kweli, moja ya maeneo makubwa ambayo Muswada huu umeangalia pia ni kuipa jukumu la kuratibu na kuandaa jam za uwekezaji nchini (National Investment Branding) Kituo cha Uwekezaji. Kwa hiyo, maana yake imeongezea nguvu tofauti na hapo awali kabla ya Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, sheria inataka tuwe na mfumo wa kielektroniki wa kuwezesha usajili wa miradi utakaounganishwa na mifumo ya taasisi nyingine muhimu zote zinazohudumia wawekezaji hapa nchini. Maana yake Muswada huu unaweza kutusaidia sasa kupunguza malalamiko ya wawekezaji kwenda kutafuta huduma kwenye taasisi tofauti tofauti. Maana yake tukiitekeleza itarahisisha angalau kupunguza ule usumbufu ambao wanapata wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, moja ya maeneo ambayo yameongelewa na wachangiaji ni kuhusiana na suala la One Stop Centre. Ni kweli, katika changamoto mojawapo ambazo wawekezaji walikuwa wanakutananazo ni pamoja na hili la kutokuwa na taasisi ambayo ina mfumo unaohudumia watu wengi kwa mahali pamoja (One Stop Centre).

Mheshimiwa Spika, taasisi nyingine ambazo tunadhani baada ya kukamilika kwa Muswada huu na mfumo huu wa kielektroniki, utapunguza ule usumbufu wa kwenda kwenye taasisi tofauti tofauti ambazo tunaamini katika mfumo huu utawezesha kuwa na sehemu moja ya kupata huduma, au tunasema huduma ya mahali pamoja.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wamechangia ni kuona namna gani ya kupunguza usumbufu au tuangalie mindset. Mheshimiwa Tarimba amesema kwa wawekezaji, lakini mtazamo kwa ujumla wa Watanzania kwamba Muswada huu utusaidie sasa pia na sisi wengine kuelewa umuhimu wa kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini kupitia Muswada huu, sheria hii, pia tunapitia na sera ambazo zitatusaidia kuhakikisha Watanzania wengi wananufaika na sheria hii ya uwekezaji na mazingira haya rafiki ya kuwekeza katika sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, umeongelewa umuhimu wa kuangalia sekta nyingine ambazo hazisimamiwi na sheria hii. Tunaamini tutaendelea kufanyia kazi kwa maana ya kuhakikisha pia uboreshaji kwenye utendaji wetu wa kila siku katika utekelezaji kupitia Muswada huu na sera ambazo zinatumia uwekezaji, tunaweza kuweka mazingira ambayo yatasaidia na sekta zote ambazo ni muhimu zisiwe changamoto kwa wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kuunga mkono hoja, na niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote tuunge mkono hoja ya Muswada huu ili uweze kupitishwa.

Mheshimwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)