Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mohamed Lujuo Monni (14 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya upendeleo kabisa maana nimeomba muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na mimi kwa sababu ni mara ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, naomba niseme maneno yafuatayo. Nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema ambaye muda wote amenipa uhai na afya ya kuwa hapa. Pili, nawashukuru wananchi wa Jimbo la Chemba kwa kunipa kura nyingi za kutosha. Tatu, kwa sababu ya muda nakishukuru Chama cha Mapinduzi kwa kunipa uteuzi na hatimaye kuwa Mbunge na leo niko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nichangie kidogo kwenye elimu. Naishukuru Serikali sana kwa sababu ya elimu bure. Hata hivyo, zipo changamoto ambazo zimesababishwa na elimu bure na moja kubwa ni miundombinu. Tumekuwa na idadi kubwa sana ya wanafunzi wanaoingia kila mwaka. Changamoto ambayo tunapata hasa zile Halmashauri ambazo hazina uwezo kuna matamko yanakuja kwamba lazima muwe na madarasa, madawati lakini Halmashauri zenyewe hazina uwezo wa kujenga madarasa lakini pia hazina uwezo wa kununua madawati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano mmoja wa athari ambazo zinatokana na haya matamko. Miaka mitatu au minne iliyopita Halmashauri ya Chemba ililazimika kutumia fedha zote za own sources kuhakikisha inanunua madawati lakini mpaka leo tunadaiwa kila mahali. CRDB wanatudai, watu walio-supply vyuma wanatudai toka mwaka 2016 mpaka leo. Sasa mimi nafikiria lazima kuwa na mpango maalum wa kuhakikisha tunakuwa na mfuko ambao au kuwa na mkakati wa kuhakikisha Serikali inachangia kwenye zile Halmashauri ambazo hazina uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo sio rahisi sana lina madhara makubwa sana kwa Halmashauri hizi mpya. Ziko Halmashauri zina uwezo zinakusanya shilingi bilioni 9 mpaka 12 kwa mwaka hata ukiwaambia wajenge hospitali wanaweza! Sasa tumekuwa na changamoto kubwa sana hiyo. Naomba sana Serikali iangalie namna bora kwenye hizi Halmashauri ambazo hazina uwezo wasitamke tu, tutafukuza Wakurugenzi, ma-DC lakini ukweli ni kwamba fedha hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoa mfano wa hali iliyotokea na sasa hivi ni hivyo hivyo. Sasa hivi tumeambiwa tujenge madarasa, tununue madawati, Halmashauri yangu zaidi ya asilimia 40 watoto wanakaa chini. Tungependa kila mtoto akae kwenye dawati lakini mimi Mbunge nina uwezo wa kununua madawati ya shule zote za Halmashauri? Haiwezekani! Tumeaambiwa tununue madawati, fedha hakuna na ni kweli fedha hakuna, nini cha kufanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapopanga hii mipango lazima i-reflect hali halisi iliyopo huko. Tusipofanya hivyo mipango yetu itakuwa tunaongea tu. Bahati nzuri niseme ukweli kwamba nimesikia michango mizuri sana ya Wabunge, nilikuwa nafikiria tofauti na hali sasa sijui kama Mawaziri wanachukua hiyo mipango inayoelezwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili naomba niongee kuhusu kilimo. Mimi ni mkulima mzuri kabisa. Hata tunayoyaongea kwamba tumetumia shilingi bilioni 180 kwenye kilimo mimi ambaye ni mkulima mkubwa pale Chemba sijawahi kuona kitu hicho. Pia huo mkakati wetu wa kilimo ukoje? Mimi mwenyewe nikilima hata kutafuta soko mpaka niende Nairobi, sijawahi kuona Afisa Kilimo wala mtu yeyote anayenifuta kuniuliza sasa ndugu yangu umelima tufanye ABC, changamoto kubwa ni masoko ya mazao haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo ni kubwa mno. Tunaongelea kulima, tunaongelea kilimo cha umwagiliaji, Jimbo tu maji ya kunywa hawana, sasa huu umwagiliaji utakuwaje? Hatuna uwezo wa kujenga mabwawa ili tupate maji ya kunywa halafu tunafikiria tujenge kwanza mabwawa kwa ajili ya kilimo. Hii inanipa changamoto kwa kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali na wakati mwingine najiuliza hivi nani ana wajibu wa kutafuta soko la mazao tunayolima? Tunasema asilimia 75 ni wakulima, mimi nalima lakini watu wengi walioko vijijini, leo utasikia gunia la ufuta Sh.90,000 lakini kesho Sh.40,000.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuanza kuchangia naomba niseme maneno machache. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, ambaye amekuwa akitupa uhai na afya njema ya kuendelea kuwatumikia Watanzania. Pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais ameanza vizuri na tuna uhakika wa asilimia zote yale ambayo tumeahidi kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi yatatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda naomba mimi nianze kuchangia. Kwanza kabisa nataka nimpongeze sana Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri. Hotuba hii imegusa kila eneo, lakini kwangu imekuwa nzuri zaidi kwasababu ameeleza namna gani tunaenda kujenga lile Bwawa la Farkwa. Mradi huu wa Bwawa la Farkwa ndio mradi peke yake ambao unaenda kumaliza matatizo yote ya maji kwenye Jiji letu la Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na bahati nzuri mradi huu ukitekelezwa hautamaliza tu changamoto za maji kwenye Jiji la Dodoma, utamaliza pia kwenye wilaya zetu zote za Mkoa wa Dodoma. Bahati nzuri sana Waziri Mkuu mwenyewe ametembelea kwenye huu mradi na yapo maelekezo ambayo aliyatoa, lakini bahati mbaya sana kuna changamoto kwenye maelekezo mengi ambayo ameyatoa hayajatekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya changamoto hizo ni kwamba, tayari Serikali ilitoa 1.8 billion kwa ajili ya kulipa fidia ya watu wote waliokuwa kwenye maeneo yale na fidia hiyo tayari imelipwa. Wametengewa maeneo ambayo wanatakiwa waende kuishi, lakini bahati mbaya sana tumechukua shule zao, lakini kule hatujaenda kujenga shule. Wamelipwa fidia tunawaondoa, lakini wanaenda sehemu ambapo hakuna shule ya msingi, hakuna zahanati, wametengewa eneo waende, lakini miundombinu ile ya kuwafanya waishi haipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri Waziri Mkuu alipofika aliwaambia msiwaondoe hawa, jengeni kwanza shule, jengeni zahanati na akaelekeza fedha zitolewe, lakini mpaka leo hii bado ni changamoto kubwa sana. tunaendelea kuwaondoa watu wahame, lakini tunawapeleka sehemu ambako watoto wao watakaa bila kusoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali, tuna mipango mizuri na sisi watu wa Chemba pamoja na Dodoma kwa ujumla tuna uhitaji kweli huo mradi. Na huo mradi ndio peke yake ambao unaenda kuondoa changamoto yote ya maji kwenye maeneo yote yanayozunguka. Lakini bahati nzuri ukisoma andiko la mradi ule limeeleza namna gani kwenye maeneo yale watatengeneza skimu za umwagiliaji kwa hiyo, kwa namna yoyote ile mradi ule una faida kwetu zaidi. Changamoto ni moja tu ni hiyo ambayo nimeieleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Wizara ya Maji itoe fedha kama tulivyokubaliana kwa ajili ya ujenzi wa shule na zahanati, ili watu wale wahamie kule. Tukiendelea kwasababu, sasa hivi kuna kama kigugumizi cha watu kuondoka, watu wengine wamehamia, lakini watu wengine bado wapo. Na nikifika kule naulizwa Mheshimiwa Mbunge wanatuambia tuje hapa, watoto wetu watasoma wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kuhusu maji ni huu, lakini pia naishukuru Serikali, tuna mradi pia katika ile miradi ya miji 28 Halmashauri yetu ya Chemba ni moja ambayo inanufaika na bilioni 11 zile. Na bahati nzuri watu wale wanaotekeleza ule mradi tumefika tukafanyanao vikao tukawaomba watu wale waliokuwa wanadai fidia za watu kupisha mabomba ya maji wamekubali wanaondoka na hawahitaji fidia. Niiombe sasa Serikali ifanye haraka kwa ajili ya kutekeleza ule mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niongee kidogo kuhusu kilimo. Sisi sote tuliopo hapa tunafahamu asilimia 77 ya ajira za Watanzania zinapatikana kwenye kilimo, lakini si hivyo tu, tunafahamu asilimia 90 ya ardhi iliyopo Tanzania hii inalimwa na wakulima wadogowadogo. Sasa ni mawazo ya kawaida tungefikiria kwamba, huku ambako watu waliko wengi ndiko tuingize fedha nyingi kwa ajili ya matokeo makubwa, lakini ukweli ni kwamba, bajeti ya Wizara ya kilimo ni ndogo sana na hii ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe sana kuwa tuangalie namna sehemu ambako tunatakiwa kuwekeza ni sehemu ambako idadi ya wanaochangia uchumi ni kubwa. Idadi ambayo ya waliojiajiri ni kubwa, ili tuweze kutatua changamoto na kwasababu hiyo, tunaweza tukaongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hivyo kuna changamoto kubwa sana kwa wakulima wangu. Moja ya changamoto kubwa ni kile kitu kinachoitwa stakabadhi ghalani. Serikali ina dhamira njema kwelikweli, lakini changamoto iliyopo unawalazimisha watu mpaka kwa bunduki ili wakauze huko kwenye stakabadhi ghalani, sijui ni nini? Unalima mwenyewe, unavuna mwenywe, unapalilia mwenyewe, Serikali hujapeleka hata mbegu, unashika bunduki ili mtu akauze kwenye stakabadhi ghalani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linaleta kero kubwa sana, kule kwangu sasahivi wameanza kuvuna. Nilikuwa na mkutano weekend hii wameanza kuniuliza tumeambiwa tena tuanze kupeleka mazao kule; hivi kweli kama hiyo stakabadhi ghalani ina faida kwa wananchi kwa nini wao wasihamasike kwenda kuuza huko? Unamlazimisha mtu mwenye debe moja aende akasubiri mwezi mzima ndio aje alipwe fedha yake? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hili haliwezi kuwa sawa, nashauri Serikali kwa baadhi ya maeneo au kwa baadhi ya mazao waachane na huu utaratibu kwa sababu kwa namna yoyote ile ungekuwa na faida wakulima wenyewe wasingeukataa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongee kidogo kuhusu barabara, kuna barabara yetu ambayo na Mheshimiwa Rais, Hayati, alivyofika kwenye Jimbo langu la Chemba aliahidi. Barabara inatoka Kibarashi inaunganisha mikoa minne, Kibarashi – Kiteto – Chemba hadi Singida. Barabara hii kwenye Ilani imekuwa ikiandikwa mara zote, lakini hakuna hata mwaka mmoja ambao imetengewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwasababu ya hayo naomba kuwakilisha. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia bajeti hii muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye mara zote amekuwa akitupa afya njema na uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia kidogo sana. Lakini kwanza kabisa nishukuru Wizara na kumshukuru Waziri kwa namna ambavyo mapendekezo yetu sisi Wabunge yamezingatiwa. Kwa hakika kila Mbunge huku nyuma amesema mambo mengi na mengi yameonekana kwenye bajeti hii. Kwa hiyo namshukuru sana lakini pia nampongeza sana yeye mwenyewe Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalam wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati mkuu, mpango mkuu kwenye bajeti hii unaeleza juu ya kujenga uchumi shindani na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. Hili ni jambo kubwa sana na mimi nataka nichangie ni namna gani sasa tunaweza tukafika huko ambako ndiko ambapo mkakati mkuu wa bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wote wengi wetu tuna Majimbo huko na tunafahamu ili tuweze kufikia mkakati huu lazima tuwe na miundombinu bora na imara. Katika hilo kwanza nimshukuru sana sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kutuwezesha, kwa kuiwezesha TARURA kwa kutoa milioni 500,000,000 kila jimbo. Kwa hakika ametusaidia sana sana kuhakikisha baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa hayapitiki tunaweza tukapambana nayo ili walau yaweze kupitika kwa urahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo yapo mambo ambayo nataka nipendekeze. Nafahamu kila Jimbo linahitaji fedha lakini nafahamu kuna maeneo ambayo kiukweli hayapitiki. Moja ya maeneo hay ani majimbo yetu sisi ya vijijini. Sisemi kwamba watu wa Ilala wasipewe, watu wa Kinondoni wasipewe. Hapana. Nafikiria kwamba tumepewa milioni…

MWENYEKITI: Toa mchango wako huna haja ya kutaja Majimbo mengine.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetaja Ilala kwa sababu wewe ndiyo Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Toa mchango wako ndugu au utakaa sasa hivi hapa. (Kicheko)

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni moja, nafikiria kwamba ili tuweze kufikia malengo ya bajeti hii tunafikiria ni lazima tufungue maeneo yote ili yaweze kupitika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Kanda ya Kati, kwa mfano jimbo langu ni wazalishaji wakuu wa alizeti, na sasa hivi tunaenda kufungua viwanda vya alizeti, kama tulivyosema, kwamba mkakati namba moja ni kuhakikisha tunaweka uchumi shindani na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. Katika mazingira hayo yapo maeneo ambayo wamelima alizeti lakini hawana uwezo wa kuzitoa kule kuingiza sokoni. Au, kwa kufanya hivyo, unayatoa kwa gharama kubwa kweli kweli. Maana yake sasa mkulima anazalisha, anatumia fedha nyingi lakini tija yake inakuwa ni ndogo kwa sababu hana uwezo wa kuyatoa au akiyatoa, anayatoa kwa gharama kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo mimi naomba pale TARURA tumeongezewa fedha. Ninakushukuru sana Waziri wa Fedha namna ambavyo umefikiria na umezingatia namna ambavyo tuliongea huku nyuma. Sasa fedha zile zikipatikana naomba basi mgao ule ulenge mahitaji. Tuangalie ni wapi sasa ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie mimi nimeshindwa. Tulielekezwa zile fedha tulizopewa walau tujenga barabara au tujenge kwa kiwango cha changarawe. Lakini ni ukweli kwamba kuna maeneo ambayo hata watoto hawawezi kwenda shule wakati wa mvua. Watakushangaa sana utato amilioni 500,000,000 zile ukajenge kilometa moja ya lami wakati kuna maeneo ambayo hawapo. Mvua zikianza lazima mvua ziishe ndiyo watoto waende shule. Katika kuzingatia hilo, mimi nimuombe sana Waziri wa Fedha, rafiki yangu wa muda mrefu, rafiki yangu wa muda wote. Naomba mnapotoa hizi fedha basi hebu jaribuni kuangalia ni namna gani tunaweza tukaifungua hii nchi kila eneo walau lifaidi au kila eneo walau liweze kupitika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, mimi nakufahamu ndugu yangu Mwigulu Nchemba, ni mtu mchapakazi, mwerevu, anaweza. Sasa tumeongeza fedha kwa ajili ya TARURA naomba basi zitoke, maana tunaweza tukaziongeza lakini kuziongeza na kuzikusanya ni jambo lingine lakini kuzitoa ziende TARURA pia ni jambo lingine. Nafahamu hilo lipo ndani ya uwezo wako Mheshimiwa Waziri. Sisi ambao tuna Majimbo ambayo yapo vijijini tuna changamoto kubwa sana. Naomba sana, fedha hizo zikikusanywa zipekwe huko ili walau zitusaidie kufungua vijiji na vitongoji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwangu peke yangu kwenye zile kilometa nyingi zinazotajwa nina kilometa zaidi ya 1,000 na zaidi za TARURA, lakini ambazo zinafanyiwa ukarabati au zinaweza kupitika ni asilimia 17 tu. Tafsiri yake ni kwamba maeneo mengi hayapitiki wala hayana uwezo, hata kama una biashara yako huwezi kufanya. Mimi nilitaka kuchangia hilo kuhusu barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba niongee kidodogo kuhusu kilimo. Waziri mwenyewe anakiri kwamba asilimia 65 ya Watanzania wanategemea kilimo, lakini ni ukweli kwamba hakuna namna ambavyo nchi yetu inaweza kwenda mbele bila kuwekeza kwenye kilimo ambacho ndicho kina watu wengi na hakuna formula zaidi ya hiyo. Ukweli ni kwamba ukitaka ku-solve quadratic equation lazima utumie quadratic formula, hakuna namna nyingine.

Nimejaribu kuangalia na kufanya tafiti kote duniani, ukweli ni kwamba lazima uwekeze kwenye nguvu kubwa, lazima uwekeze kwenye shughuli kubwa ya kijamii inayofanyika. Watanzania wengi ni wakulima lakini sisi tunawekeza kidogo mno. Bajeti yetu walau tungeisogeza ikafika asilimia 10 ya bajeti tungekuwa tunaamini kwamba sasa tunaenda kusaidia watu walio wengi ili waweze kuinuka kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika hilo mimi Jimbo langu asilimia 95 ni wakulima, na ukitaka kumuuliza mtu anawezaje kupata fedha lazima asubiri wakati wa mavuno ndiyo anaweza kupata fedha na akatunza kwa ajili ya kuhudumia mwaka mzima. Sasa, katika mazingira hayo kuna changamoto kubwa sana kwenye. Moja ya changamoto kubwa sana ni masoko. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri kaeleza vizuri kwenye bajeti hii. Ameeleza namna gani ambavyo anaweza ku-deal na hilo suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine kubwa, na mimi nafahamu ndugu zangu wenye majimbo hapa idadi kubwa sasa hivi ya watu vijijini ni vijana. Vijana ni wengi sana huko vijijini. Mimi nikienda vijijini nikiitisha mkutano nakutana na vijana wengi sana. Wapo vijana wenye degree mbili (Masters) wapo vijana wana degree moja, wapo vijana ambao hawana elimu, wako vijijini wamezubaa kule hawana cha kufanya. Tufanye nini sasa, kwa sababu tukifikiria kwamba waende kujiajiri, wanajiajiri vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri kama alivyosema kwenye bajeti yake ninamuomba sana Waziri hili jambo alifuatilie, tuangalie namna gani tunaweza kuwekeza mitaji kwenye hawa vijana. Otherwise tunaweza kutengenza mazingira magumu sana kwao na kwetu sisi ambao mara zote wenyewe ndiyo wanatusaidia kutupigia kura. Nilitamani sana niyaseme hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nilitaka kuongea kidogo kuhusu elimu. Niliwahi kusema huku nyuma, kuna changamoto kubwa sana kwenye Halmashauri hizi ambazo ni changa, Halmashauri ndogo kama ya kwangu mimi ambayo ukikusanya fedha mapato yote kwa mwaka ni bilioni 1.2 na ukiangalia uwezo wa ujenzi wa madarasa ni mdogo sana. Bado narudi kwenye hoja ile ile kwamba ni lazima tuangalie ni wapi. Wakati mwingine unajiuliza maswali makubwa sana kwamba kule Wizara ya Elimu wametoa fedha kwa ajili ya maboma lakini wametoa flat rate. Yaani mtu ambaye anakusanya bilioni 100 unampa flat rate na mtu anayekusanya bilioni 1.2 kwa mwaka. Hii haiwezi kuwa sawa na hatuwezi kuwa tunalenga sasa kuendeleza hizi halmashauri changa au watu walioko. Mimi nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, hili ulizingatie vizuri. Mimi naamini wewe unaweza na haya mambo unaweza ukayaweka vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia jambo hili muhimu sana lililopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mola ambaye ametujalia afya njema, uhai, na leo tuko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba nimshukuru kipekee kabisa Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo amekuwa akileta fedha nyingi kwenye majimbo yetu. Nawashukuru na wawasilishaji, Mheshimiwa Mwigulu na Mheshimiwa Prof. Kitila, kwa namna ambavyo wameleta wasilisho zuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujadili huu mpango ulioko sasa hivi, naomba na mimi niseme maneno machache kama alivyosema Mheshimiwa mwenzangu aliyepita. Ni vizuri tunapoleta mpango hapa tukaangalia umefanikiwa kiasi gani, lakini pia tuangalie takwimu ambazo zinaletwa kwenye hii mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye takwimu za maji wanasema upatikanaji wa maji mijini ni asilimia 88. Jambo hili katika logic sio sahihi, sisi wote tuko hapa mjini, Dodoma hapa tulipo tunapata maji siku tatu kwa wiki, siku tatu maana yake ni 3/7 x 100 = 42%, sasa kama Dodoma ni asilimia 42, wananchi wanapata maji siku tatu kwa wiki, tunawezaji kuandika takwimu asilimia 88. Haya mambo tuyaseme vizuri ili tukapange mipango ya kuhakikisha watu wanapata maji, hawa wataalam wetu sijui wanatumia maarifa gani katika ku-calculate haya mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiukweli Jimboni kwangu alisema siku moja hapa Mheshimiwa Condester, kwake ni asilimia 22 kwangu ni asilimia 33. Sasa tunaweka mipango ambayo haitekelezeki lakini kwenye makaratasi inaandikwa kwamba haya mambo ukiangalia wanataja visima ambavyo tayari vinatoa maji. Mwaka 2022/2023, 2021/2022 mimi nimepewa visima, nimepewa visima 11 mpaka leo vimechimbwa viwili, nimepewa visima vitano bajeti imepita havijawahi kuchimbwa, nimepewa mabwawa ambayo hayajawahi kuchimbwa. Halafu ukiangalia kwenye takwimu wanasema kwamba maji yanapatikana vijijini kwa asilimia 78.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi taarifa zinatuchonganisha na wananchi.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mohamed Monni, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji, Mheshimiwa Maryprisca Mahundi.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Naomba nimpongeze anayechangia Mheshimiwa Monni, kwenye eneo la asilimia upatikanaji wa huduma ya maji. Wataalam wanakuletea zile percentage, wanaangalia ni coverage ya miundombinu pamoja na upatikanaji wa maji bombani. Kwa hiyo, suala la visima analoliongelea, visima vyote ambavyo vinaahidiwa tumeendelea kuchimba kadri tunavyopata fedha tunawafikia na yeye mwenyewe kwenye jimbo lake atakuwa shahidi amepata upendeleo mkubwa wa gari lile ambalo Mheshimiwa, Dkt. Samia, amenunua 25, sehemu ya kwanza kuchimba visima ilikuwa ni jimboni kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa aongee kile kitu ambacho anakifahamu kwa dhati, kama hiki kinamchanganya ni vyema asipotoshe umma lakini kama anahitaji maelezo zaidi kama anavyokuwa anakuja ofisini pale Wizarani, basi aje tuendelee kumuelewesha lakini sio kupotosha umma, ahsante.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mohamed Monni, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siipokei taarifa yake, lakini anasikitisha sana halijawahi kuja gari hilo kuchimba maji na tena naomba niseme machache kuhusu haya magari yaliyoletwa. Wabunge ni mashahidi, magari yameletwa lakini hayafanyi kazi, bora wangempa mtu binafsi wamshirikishe yangeleta maji. Kila moa, leo walete takwimu zinazoonyesha magari ya UVIKO, yamechimba visima vingapi? Walete takwimu, kama yamechimba visima, yamechimba visima viwili, vitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Dodoma kwanza sijawahi kupata hilo gari kuja kuchimba hayo maji na huo ndiyo ukweli maana yake Mheshimiwa Waziri, anadanganya na ananitengenezea taswira mbaya kwa wapigakura wangu. Ninachojua, kuna Mkandarasi amepewa kazi ya kuchimba visima 11, tangu mwaka jana gari limekaa pale kwa Mtoro, hawajampa fedha tangu mwaka jana lina miezi 11 mpaka leo. Halafu wale watu hawana maji wanaliona gari la kuchimba maji hili hapa, halafu nauliza nini kimetokea, naambiwa hawajapewa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kusema maneno mengi zaidi. Nikisema maneno mengi zaidi nitakuwa mahali fulani naumiza. Nataka niwahakikishie Wizara ya Maji, imekuwa inaletwa kuwa inapewa fedha kwa asilimia 96, kwenye bajeti hapo ilisema hayo maneno. Hizo fedha zinapelekwa wapi, maana yake zinapelekwa sehemu nyingine, jimboni kwangu haziletwi sio sahihi, sio kweli kwa sababu Jimboni kwangu visima 11 vya 2021/2022 havijachimbwa, vimechimbwa viwili. Visima vitano vya 2022/2023 mpaka leo havijachimbwa na muda umeisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabwawa, Kidoka kulikuwa na bwawa la bilioni tatu, tumeweka bango mpaka leo tuna mradi kule Machija, mpaka Katibu Mkuu, amekuja bado hakuna kitu kilichoendelea, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, tuna mradi wa milioni 600 Chandama, mpaka leo Katibu Mkuu, amekuja tumempeleka, miradi yote haijakamilika, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisimame hapa, wakati watu wangu wanajua hawapati maji, halafu niseme kwamba mipango hii inapangwa na inaenda vizuri, haiwezekani! (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Monni, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namuunga mkono Mheshimiwa Mbunge, kwa mchango wake anaochangia. Nataka nimpe taarifa na niwaombe na Waheshimiwa Wabunge wengine, kwamba wala hatuna haja ya kugombana isipokuwa hali ya masuala ya maji imebadilika sana kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Kwa maana hiyo fedha tumetoa, wakati tuko kwenye bajeti tulitoa bilioni 104 kwenda tu Wizara ya Maji na hizo zilikwenda lakini kwa sababu kila kijiji pana mabadiliko makubwa ya tabianchi wale watu ambao zamani walikuwa wanapata maji, kila Mbunge hapa atashuhudia waliokuwa wanapata maji tu yanatiririka sasa hivi hayapatikani maji ya aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, concentration ya watu wote kutakiwa wachimbiwe maji ni kubwa sana na vijiji vinaongezeka na vitongoji vinaongezeka. Ndiyo maana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameleta gari kila mkoa. Pamoja na kuwa gari liko kila Mkoa WAbunge watakubaliana nami kwamba halitaweza kuchimba kila kijiji siku moja. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, tumepokea hoja yake hiyo na tunaichukua kama special case, tumewasikiliza na Wabunge wengine na juzi hapa Waziri wa Sekta alipokuwa anahitimisha hoja amepokea na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea mchango wa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge, waendelee kuiamini Serikali, hili ni moja ya jambo la kipaumbele kwa Mheshimiwa Rais na sisi kama wasaidizi wake tunaweka uzito huo huo na sisi Wizara ya Fedha, tutaendelea kutoa fedha katika maeneo hayo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, ahsante. Mheshimiwa Mohamed Monni, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kiungwana kwa sababu ametoa maneno ya kunifariji na kwa sababu yeye ndiye Waziri wa Fedha, naamini sasa akirudi ofisini atatoa fedha maalum kwa ajili ya Jimbo la Chemba na Wilaya ya Chemba. Namshukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisiseme tena kuhusu maji. Ukiangalia mpango unaeleza kwamba sasa tunaenda kuchochea maendeleo vijijini na watu hawa ni matajiri. Mimi natoka Jimbo la Vijijini ambapo kura ndiyo rahisi zaidi kuzipata kwa Chama chetu Cha Mapindizi, lakini tunawakwaza. Kwanza nishukuru kwa barabara, ile barabara ambayo tayari Mkandarasi amepewa kutoka Kibirashi – Handeni – Chemba – Singida inakata katikati mwa Jimbo langu, niwashukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba barabara ile kidogo itapunguza namna ambavyo watu wanaweza kusafiri. Hata hivyo, zipo barabara ambazo ndiyo maeneo ya uzalishaji, kuna barabara ya kutoka kwa Mtoro hadi huko maeneo ya mashambani kilometa 56, huko ndiko alizeti zote zinazalishwa, huko ndiyo ufuta wote unaouzwa Dodoma unapozalishwa, lakini gharama ya kuzileta Dodoma ni kubwa sana. Fedha zinazotengwa kwa ajili ya ukarabati wa hizo barabara milioni 30, nataka niwaombe kwenye mipango hii lazima takwimu zionyeshe uhalisia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Kamati ya Bajeti, wameeleza wazi kwamba takwimu zilizowekwa sio halisia, wanaomba watu wa mipango wakafanye upya tafiti ya takwimu zilizopo kwenye makaratasi ili sasa tuweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina jambo lingine la muhimu sana. Sisi ambao tunatoka majimbo ya vijijini sijui changamoto ni nini, lazima tukubali kwamba kule kama wanataka kuwarudisha watu vijijini, lazima Serikali itengeneze mazingira mazuri, huo ndiyo ukweli. Ukienda vijijini tunajenga sasa hivi madarasa, lakini hakuna mpango wowote wa namna gani sasa hata hayo madawati yanaweza kuwa yanatengenezwa baadaye. Sasa hivi tunajenga darasa tunaweka na madawati, lakini nataka niwaambie ukienda shule zote za Chemba 112, upungufu wa madawati ni asilimia 70, wazazi hawana uwezo wa ku-cover hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka tunaweza kuwa tunatengeneza asilimia 10, lakini ni makakati upi wa Serikali kwa nchi nzima sasa wa kuhakikisha wanaenda kutatua hiyo kero. Tunajenga madarasa ya aluminum, yana tiles, lakini watoto wataendelea kukaa chini, kwa sababu tumeweka vipaumbele sehemu nyingine, sehemu nyingine tumeacha. Nimwombe Waziri wa Fedha lakini pia nimwombe Mheshimiwa Profesa Kitila, rafiki yangu tunafahamiana sana tangu tukiwa Pugu Secondary, anajua na nilikuwa mshabiki wake alikuwa akigombea u-head prefect, natafuta kura zake. Nimwombe sana atafute namna ambayo tunaweza kutatua changamoto zilizoko, lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme maneno mawili ya mwisho. Kuna tatizo kubwa sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia muda wako. Kengele ya pili imeshalia.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kuwapa pole sana wananchi wangu wa Kijiji cha Handa, ambao wamechomewa nyumba na mahindi kuanzia jana na juzi operation ya kuchoma nyumba na watu wa TFS, inaendelea. Amesema Mheshimiwa Deus Sangu, hapa tulitamani tuijadili ili tueleze hali halisi, jana watu kadhaa wamechomewa nyumba zao, mahindi yao yamechomwa halafu watu walioenda kuchoma pale ni watu wa TFS na magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yawezekana kabisa wananchi wangu wamevunja Sheria. Sasa unawezaje mtu mwenye akili za kawaida unaenda unachoma nyumba ya mtu, labda kweli ipo kwenye msitu wa hifadhi, unachoma nyumba ina magunia 60 unachoma, unaenda nyumba ya pili ina magunia 30 unachoma, ndiyo nini sasa?

MWENYEKITI: Mheshimiwa, ahsante kwa mchango wako kwenye matayarisho ya mipango.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu ambazo zimetolewa na Wizara ya Maji zinaonyesha asilimia 72 ya watu waishio vijijini sasa wanapata maji, lakini kwenye wilaya yangu sidhani kama asilimia 42 inafika. Nilikuwa nategemea sana mradi mkubwa wa Bwawa la Farkwa na kwenye mradi huo tayari Serikali ilitoa zaidi ya shilingi bilioni 7.8 kuwahamisha watu, lakini cha ajabu zaidi, haukutengewa hata shilingi moja kwenye bajeti hii. Wasiwasi wangu mkubwa ni kwamba sasa wale watu wanaenda kurudi pale na hakuna namna tena ya kuja kuwaondoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo mengi, kulikuwa na migogoro mingi sana kwa ajili ya kuhakikisha watu wale wanahama pale. Sasa hili jambo limenishtua sana. Nilitamani wakati Waziri anakuja ku-wind-up aniambie kwanini hawakutenga fedha angalau kidogo kwa ajili ya bwawa lile? Ninaamini, ili tuweze kutatua changamoto ya maji kwenye Makao Makuu ya nchi, ilikuwa ni lazima tuanze haraka sana utekelezaji wa mradi ule kwa sababu mradi ule ni katika miradi ya maji ya kimakakati tuliyonayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Wizara, Wilaya yangu ya Chemba ni katika Wilaya ambazo ni kame kweli kweli na ndiyo maana tumejaribu kufanya miradi mingi ya maji na miradi mingine inashindikana hasa ile ya kuchimba visima. Nasi tunaamini, namna peke yake ya kutatua changamoto za maji kwenye wilaya ile ni kujenga bwawa hili kwa haraka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kusema pia, kuna changamoto nyingine ambazo zinashangaza sana. Tuna visima ambavyo vilichimbwa mwaka 2014. Katika visima vile, wakati huo Halmsahauri siyo RUWASA; walitangaza tenda kwa ajili ya usambazaji. Mkandarasi akapatikana, lakini mpaka leo hii hawajasaini mkataba wa yale maji wasambaze. Mpaka leo, kuanzia mwaka 2014! Vile vile maji yale yamechimbwa kilometa sita kutoka vijiji vilipo. Kwa hiyo, haina faida yoyote kwa sababu lazima watu waweke punda kwenda kuchota maji kilometa sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami naiomba Wizara ya Maji ikashughulikie visima vile vitatu ambavyo ni Chandama, Mapango na Machiga. Watu wengi ambao hawajasoma kule kijijini wanashindwa sana kuelewa, inawezekanaje mkachimbe maji, mtangaze tenda, mkandarasi apatikane, halafu msisaini afanye kazi? Wanashindwa kuelewa, nini kinaendelea pale? Naomba Waziri wa Maji atakapokuja ku- wind-up hotuba yake ya mwisho, aseme chochote ili watu wa kule watuelewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, nimeona mmenipa visima kadhaa vya maji; mmeonyesha kwenye jedwali kwamba tutapata visima 13 kwenye bajeti hii, lakini mmetenga shilingi milioni 180. Ni ukweli usiopingika kwamba kwa namna ambavyo Wilaya ya Chemba ilivyo dry milioni 180 haziwezi kuchimba visima 13. Sana sana zitachimba visima vinne. Sasa takwimu hizi ni za kwenda kumgombanisha Mbunge na watu wake, kwamba tumetajiwa vijiji ambavyo vinaenda kupata maji, lakini kiuhalisia ni kwamba maji kwa bajeti hii haiwezekani. Namwomba Mheshimiwa Waziri, anapotenga fedha angalie na Wilaya zenyewe na namna gani unaweza kupata maji kwenye mazingira haya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto nyingine hii inaitwa ya manunuzi. Tulipata mradi pale Chemba Mjini na tuliambiwa mradi ule una shilingi milioni 250, lakini mpaka leo umeshindwa kutekelezwa. Ukimwuliza Meneja wa RUWASA, tangu mwezi wa 11 anasema watu wa manunuzi hawajaleta vifaa mpaka leo, miezi sita. Nami nikisimama jukwaani nawaambia ndugu zangu tumepata fedha milioni 250 tunaweka sawa mambo ya maji hapa. Jambo dogo kama hilo, tunatumia miezi sita kununua vifaa vya maji, sijui mabomba, mnatuweka kwenye wakati mgumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana, juzi baada ya Waziri wa TAMISEMI kuja pale, mmetupa shilingi milioni 150. Siku mbili tu kaja, ametoa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kuhakikisha maji yanapatikana pale hospitali. Nawashukuru sana, lakini nawaomba msisubiri mpaka Mheshimiwa Waziri aje, tukiwaambia sisi, ndio tumewaambia mahitaji ya watu waliopo kule.


Mheshimiwa Naibu Spika, hilo pia nilitaka niseme, tuachane na utaratibu kwamba manunuzi lazima yafanyike HQ, kila mtu ukimuuliza yanafanyika HQ, sisi tuko Dodoma HQ Dar es Salaam tunahitaji vifaa vya milioni 20 tunasubiri mpaka watu wa Dar es Salaam waje wanunue, hii haiwezi kuwa sawa hata kidogo. Nimwombe Waziri abadili utaratibu au aweke utaratibu ambao ni rafiki ili tunapopitisha bajeti vifaa vile vipatikane kwa haraka zaidi.

Mheshimwa Naibu Spika, nataka pia niongelee juu ya uchakavu wa miundombinu ya maji iliyopo katika wilaya yangu. Tuna miradi mizuri kabisa ambayo imekuwepo kwa muda mrefu, changamoto kubwa tuliyonayo sasa maji hayapatikani. Shida ni ndogo tu, wakati mwingine unaona


mradi unahitaji milioni 30 tu, lakini kata nzima inashindwa kupata maji kwa sababu tu eti fedha za kukarabati miundombinu milioni thelathini mpaka uende kuomba Wizarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana nilikuwa nimefanya ziara kwenye Kata moja ya Nahoda, tenki limepasuka, tenki lenyewe kulinunua ni milioni moja, watu zaidi ya vijiji sita zaidi ya miezi mitatu hawapi maji. Nimwombe sana Waziri lazima tuwe na utaratibu rafiki ambao unawezesha pale matatizo yanapotokea, pale changamoto za maji zinapotokea waweze kuzitatua kwa urahisi na kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi walau nami nichangie kidogo kwenye mwongozo huu wa Mpango. Kwanza kabisa nichukue fursa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema ambaye amekuwa akitujalia afya njema na uhai na tumekuwa tukikutana hapa mara zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Nina hakika kwamba Watanzania wote sasa wana matumaini makubwa, kazi inaendela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwongozo wa Mpango huu nataka nichangie katika sehemu mbili muhimu; sehemu ya kwanza ni kilimo na pia sehemu ya pili ni barabara. Kabla sijachangia nichukue fursa hii pia kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi kubwa ambayo ameifanya. Mwongozo wa Mpango unatupa sisi fursa ya kuwaeleza nini kiwepo kwenye Mpango unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto kubwa kwenye kilimo ni utekelezaji wa mipango ambayo ipo.

Nimejaribu kusoma Mpango wa mwaka 2019/2020 mambo mengi yameandikwa, lakini sisi wakulima kiukweli kabisa Serikali haijawekeza vya kutosha. Maneno haya yamesemwa na kila Mbunge, lakini mimi najaribu kuangalia tu kwa takwimu. Kwa mfano, ukiangalia kwenye zana za kilimo, mpaka sasa hivi sisi tuna asilimia 20. Hiyo asilimia 20 yenyewe ni kwenye maandalizi tu, yaani ile hatua ya kwanza kabisa ya kuchambua ardhi ndiyo tunatumia labda matrekta na zana nyingine, lakini kwa mantiki kamili ya kutumia zana za kilimo bado tupo chini ya asilimia nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mazingira hayo, hakuna namna ambayo tunaweza tukaisaidia nchi hii ambayo asilimia kubwa ya Watanzania wapo kwenye sekta hii ya kilimo. Ni changamoto kubwa kweli kweli. Sasa hivi tunapoongea, ukifanya ziara kwenye maeneo yote ya Tanzania au hasa Majimboni, mbegu zenyewe hazijafika. Sasa unaanza kujiuliza maswali mengi sana, kwamba kwenye Mpango tumeweka tayari, maana yake hata tukija kusema sasa tuwekeze shilingi trilioni moja, bado changamoto hii itakuwepo pale pale. Kwa maana tumeweka kwenye Mpango, tumepitisha kwenye bajeti, lakini mbegu hiyo bado mpaka sasa hivi haijafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa ambalo naliona, ni lazima tuhakikishe tumewekeza vya kutosha kwenye kilimo. Kama hatutafanya hivyo hakuna namna ambavyo tutakwepa watu wengi kuhamia mjini. Ukiangalia population kubwa ya Dar es Salaam ya vijana wengi wanaoitwa Wamachinga ni kwa sababu hakuna kazi kwenye kilimo hicho. Hatujawekeza vya kutosha kwenye kilimo. Tukiwekeza vya kutosha tutapunguza gharama hizo ambazo zimewekezwa kwa ajili ya Wamachinga; majengo yanayojengwa, fedha zile tungewekeza kwenye kilimo, vijana wale wasingekuwa na sababu ya kukimbilia mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu mimi naiona katika mwono huo. Mimi pia nalima, lakini najaribu kuangalia mazingira ya kilimo kile, anaweza akaja kijana akalima mwaka mmoja akaamua bora aende mjini akauze bidhaa mkononi kwa sababu ya mazingira yenyewe yalivyotengenezwa. Nataka niwaombe sana Wizara ya Fedha iangalie namna ambayo itatenga fedha za kutosha waingize kwenye kilimo. Tutaweka Mpango leo, lakini kama fedha hazitaenda huko nina hakika kabisa vijana wengi watakimbilia mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka pia niongelee kuhusu barabara. Tuna barabara yetu; halafu unaweza kujiuliza maswali mengi sana, kwamba tuna barabara ambayo inaunganisha mikoa minne. Mwenzangu Mheshimiwa Mtaturu alikuwa ameiongolea pale kwamba barabara inaunganisha mikoa minne, eti imetengewa kilometa 20 kati ya kilometa 420 na kitu. Sasa sijui wataalamu huwa wanachambua kwa kuangalia vigezo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia barabara hii, ndiyo barabara kubwa iliyobaki, lakini barabara hii ukiangalia faida, niliwahi kumwambia Waziri; hivi nyie mnavyoweka mipango na kujenga hizi barabara mnatumia vigezo gani? Unawezaje kuacha barabara inayounganisha mikoa minne, unaenda kujenga barabara ya kuunganisha wilaya na wilaya halafu umetenga kilometa 70?

Mimi nafikiri kama walivyoshauri Kamati ya Bajeti, wameandika maneno mazuri sana pale, kwamba tukajenge kwanza barabara zile ambazo tayari zipo kwenye mpango zimalizike then ndiyo tuingie kwenye barabara nyingine. Pengine hii itaweza kutibu lile tatizo ambalo wewe unaliona, kwamba wanakuja na Mpango, Wabunge wanasema, lakini mwisho wa siku hakuna ambacho kinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kusikitisha sana kwamba una barabara muhimu kuliko zote halafu hiyo ndiyo inatengewa fedha kidogo sana. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kama yupo hapa, Waziri wa Ujenzi wakati ujao, sisi tupo Wabunge wanane ambao tunaguswa na barabara hiyo; nataka nimwambie, ukileta tena kilometa 20 sisi hatutakuwepo tena hapa Bungeni. Kwa sababu ni barabara ambayo ukiangalia faida zake ni kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunaenda kupanua Bandari ya Tanga, mizigo yote ambayo inatakiwa kwenda Rwanda na Burundi, lazima ipite kwenye barabara hiyo. Ni kwa namna gani unaenda kujenga barabara nyingine huko kilometa 70, kilometa 80 ya kiwango cha lami…

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa nimekuona.

T A A R I F A

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wasiofahamu, barabara inayozungumziwa hapa ni ya Handeni – Kibilashi – Kiteto – Kondoa – Singida kilometa 460. (Makofi)

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nimeipokea taarifa bila wewe kuniuliza, lakini ni ukweli, najaribu kueleza namna ambavyo barabara ile inaweza kusaidia. Najaribu kuangalia, hivi barabara zinajengwa kama unaongeaongea Bungeni au ni Serikali? Ina maana kama haitakuwa Mbunge, barabara hiyo haitajengwa? Kuna vitu vingi vinachanganya sana, kwa namna ambavyo umuhimu wa hii barabara ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana kwamba nimesoma vizuri ushauri ambao umetolewa na Kamati ya Bajeti na ninaomba wauzingatie, wasituweke kwenye mtihani wa kuja kupambana na mipango yao waliyotupangia. Nashauri kama walivyoshauri Kamati ya Bajeti kwamba barabara zile ambazo zipo kwenye Mpango, ambazo zimepangwa muda mrefu sana, zijengwe zimalizwe ndiyo mlete tena mipango mingine ya kujenga barabara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja hii ya Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Waziri na watalaam wake wote kwa namna ambavyo wamewasilisha hoja hii. Naomba na mimi niseme tu kwamba napongeza kama wenzangu wote walivyopongeza na pongezi zote zilizotolewa ni za kweli na ni sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwanza nataka kuongelea juu ya upungufu wa vyumba vya madarasa lakini lazima ni declare interest kwamba mimi jimbo langu nila vijijini yaani hata pale Makao Makuu ya Chemba bado panaitwa kijijini. Sasa labda nitoe takwimu kidogo mahitaji ya vyumba vya madarasa kwenye jimbo langu kwa ujumla ni vyumba 1,562 lakini vilivyopo ni vyumba 700 tu maana yake ni nini? Kuna upungufu wa zaidi ya asilimia 50 na ukweli ni kwamba watu wa vijijini tunafahamiana kwamba ni watu maskini, uwezekano wa kujenga vyumba hivi vingi vyote hivi haiwezekani, kama tulivyofanya kwenye sekondari lazima tuje na mkakati wa makusudi wa kuangalia namna gani tunaweza kwenda kuongeza vyumba hivi vya madarasa hivi shule za msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi binafsi nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi ambao aliufanya wa kuidhinisha zile fedha za UVIKO zitumike katika kujenga madarasa ya sekondari. Kwa hoja ile ile mimi nawashauri Wizara ya TAMISEMI lazima waje na mpango mwingine muhimu ili walau kupunguza kwa kiwango fulani upungufu mkubwa wa madarasa kwenye shule hizi za msingi. Hoja hiyo pia iendane pia na upungufu wa walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna upungufu mkubwa sana wa walimu lakini kuna jambo huwa najiuliza sana kwamba unaona kabisa takwimu zinaonesha labda Wilaya ya Chemba ina upungufu mkubwa zaidi kuliko wilaya nyingine, lakini wanavyokuja kuletwa walimu unaona wamegawiwa kwenye yale maeneo ambayo kuna walimu wengi zaidi. Sasa hili jambo hili nililisema mwaka jana, lakini naomba safari hii lizingatiwe kwamba ndiyo tunaenda kuajiri walimu lakini kwa nini tusiajiri walimu tukawapeleka kule ambapo kuna upungufu mkubwa zaidi. Changamoto hii inaweza ikaendelea kwamba kila siku tunaendelea kuongelea habari ya upungufu wa walimu. Mwaka huu tunaongelea upungufu walimu, walimu wanaajiriwa lakini hatuzingatii ni wapi kuna upungufu mkubwa ili walau tukapunguze gape kule kuliko kupeleka kule ambapo kuna walimu wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo shule zangu za msingi zinawalimu wanne na wanafunzi 500 ninamna gani katika mazingira haya walimu hawa wanaweza kufundisha kule kijijini na ni ukweli usiopingika kwamba kuna Mbunge mmoja alitoa hoja ya msingi sana kwamba kuna umuhimu wa kuwaajiri wale walimu ambao wapo tayari kukaa kule porini. Kuna walimu wanajitolea, zilipotolewa ajira wao wakanyimwa wameendelea kujitolea na tunalazimika sisi Halmashauri au vijiji kuchanga fedha kuwalipa wale walimu kufuatana na mazingira yetu, lakini wale wanaojitolea wapo pale hawaajiriwi.

Mimi nafikiri safari hii kuwe na mkakati wa makusudi wa kuangalia kwamba huyu yupo hapa miaka mitatu anajitolea, ajira zimekuja hakuajiriwa, kijiji kinaendelea kuchanga fedha kwa ajili ya kumlipa walau kwa kumuajiri tutakuwa tumepunguza mzigo kwa wale wanakijiji waliopo pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili; nilitaka niongelee kidogo kuhusu na mimi naamini Mawaziri hawa vijana wanaenda kutatua changamoto hii. Kuna changamoto kubwa sana kwenye malipo ya Madiwani hasa zile stahiki ndogo ndogo kama posho, hii ni changamoto kwa Tanzania nzima. Mimi ni mjumbe wa LAAC nimejaribu kupita kwenye hizo Halmashauri unaona hapa wanalipwa vingine, hapa wanalipwa vingine. Sasa ni lazima tuje na mwongozo mmoja kwa sababu asilipwe kama hisani hali iliyopo sasa hivi malipo ya Madiwani yale ya posho yanazingatia tu namna gani yule Mkurugenzi anajisikia wakikutana na Mkurugenzi mwenye roho mbaya ni mgogoro kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nini nataka kusema lazima TAMISEMI wenyewe waje na mwongozo mmoja kwa Halmashauri zote ili kila Mheshimiwa Diwani ajue kabisa yeye anapoenda kwenye kikao stahiki zake ni zipi mgogoro huu wa malipo umeharibu sana mahusiano kati ya Mkurugenzi na Madiwani na kazi zinakwama .

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe vijana mliopo hapa ambao sisi tunawaamini sana kwamba nendeni sasa kuanzia bajeti hii andikeni waraka mmoja na futeni nyaraka nane, tisa zilizopo ambazo hazieleweki na ni kweli ukianza wewe kama Mbunge mara nyingi unajaribu kurekebisha ugomvi kati ya Wakurugenzi na Madiwani, lakini unaona kabisa Madiwani wana hoja wana waraka, Mkurugenzi naye ana waraka sasa sijui inakuwaje! Kwa hiyo, unaanza unakaa unashindwa uchukue waraka wa Mkurugenzi aliokuja nao au waraka wa madiwani waliokuja nao.

Mimi niiombe wizara kwenye bajeti hii njooni na waraka mmoja na futeni nyaraka zingine vyovyote vile ambavyo mtaona itafaa itasaidia kutuliza hali ya migogoro iliyopo kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimwia Naibu Spika, jambo lingine ni usimamizi wa fedha; usimamizi wa fedha kwenye miradi yetu nimesema mimi ni mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali kuna changamoto kubwa sana kwenye fedha hizi zinazopelekwa kwenye miradi, lakini pia na shida hii naiona huku TAMISEMI kwanini labda nitolee mfano mmoja tumeenda kwenye Halmashauri ya Magu kuna jengo limeanza kujengwa mwaka 2011 mpaka leo halijamalizika, lakini pia ukimuuliza Mkurugenzi anasema apewe fedha zilezile ambazo ziliandikiwa proposal mwaka huo zitamaliza kujenga jengo lile. Mimi nikamwambia hiki kitu hakiwezekani yaani wakati mfuko unauzwa shilingi 11,000 ndiyo ujenzi ulianza, leo mfuko mara mbili ya bei ile bado anasema fedha ile ikija atamaliza lile jengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nafikiri hapa kuna shida, lakini shida nyingine kubwa pale kuna mtu anaitwa Mkaguzi wa Fedha za Ndani, Mkaguzi yule yupo chini ya Mkurugenzi, ni namna gani anaweza kuandika taarifa wakati mtu anayemlipa ni Mkurugenzi? Ni lazima hivi vitu viangaliwe upya kwamba kile kitengo ni cha muhimu sana kwa sababu fedha nyingi ambazo tunapeleka pale, lakini mtu ambaye anaweza kuandika ripoti ya kweli analipwa posho na Mkurugenzi ni kwa namna gani sasa ni vipi ambavyo yeye anaweza akasimama akaandika ripoti ya aina yoyote ya kuhusu Mkurugenzi ambaye yeye ndiye anayemlipa posho anakaa kwenye dawati pale kuandika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka pia nilisemee hilo, lakini la mwisho pengine Mheshimiwa Waziri kwenye jimbo langu alipokuwa Waziri Ummy alikuja na akaahidi kutengeneza barabara ya kilometa 18 kwa kiwango cha changarawe, barabara ile ndiyo inayotumika kila siku, sasa baada ya kuwa ni ahadi ya Waziri sisi hatukuitengea fedha tulizopewa, sasa watu wakipita pale wananitukana mimi, lakini unaona wewe shida imeanza kwenu msingetuahidi mnatujengea barabara ile maana yake nini maana yake ni kwamba sisi tungetenga fedha zile ambazo mmetupa kujenga barabara ile…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaj)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja hii muhimu ya Waziri wa Utumishi. Kwanza kabisa nachukua fursa hii kumpongeza Waziri mwenyewe, lakini pia kumpongeza Naibu Waziri, Katibu Mkuu na wataalam wote. Kipekee kabisa niwapongeze watumishi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama umewahi kuwa mtumishi kidogo tu unafahamu hali halisi iliyopo huko. Watumishi wa Tanzania wanafanya kazi kwenye mazingira magumu, nami nafahamu watu wengi wamejaribu kuchangia hata chanzo cha kuhama, mimi Jimbo langu ni la vijijini, unaweza ukaenda kwenye zahanati ambayo iko kijijini kabisa lakini unakuta mtoto wa kike ana miaka 23 anafanya kazi huko na yupo huko anafanya kazi vizuri. Kwa hiyo kipekee kabisa niwapongeze watumishi wa Tanzania wanajitolea na wanafahamu hali halisi ya nchi yetu, niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu hapa ni moja tu. Naomba niendelee kuongelea kuhusu changamoto ya upungufu wa watumishi tulionayo. Hili tatizo ni la Kitaifa, lakini naomba nitoe mfano kwa Wilaya ya Chemba na hasa kwa watumishi wa afya. Nilimsikia Daktari Chaya, jirani yangu Manyoni yeye ameongeza watumishi wa afya, angalau yeye anafika asilimia 50. Mimi kwenye Kada ya Afya nina asilimia 27 tu. Mahitaji ya watumishi kwa ujumla ya Kada ya Afya ni 838, lakini tulionao ni 173, sawasawa na asilimia 22 tu. Mnaweza mkafikiria ni kwa namna gani sasa unaweza kuhudumia hawa watu wetu walioko huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme maneno kadhaa, sisi tuna vituo vya Afya vinne, tuna kituo cha Afya kipya sasa hivi ambacho tumejengewa na KOICA kipya kabisa ambacho kimejengwa kama Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo, hivi tunavyoongea hakina mtumishi hata mmoja na hatuwezi kukifungua kwa sababu hakuna watumishi, lakini tumejengewa na wafadhili. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kituo hicho kipo kule Soya na katika maeneo ambayo tulifanya vibaya kwenye kura ilikuwa ni kwa sababu hiyo. Tukaenda kutafuta Mfadhili huko akatoa bilioni 1.2 amejenga Kituo cha Afya. Kituo cha Afya kipo tayari na wamenunua kila kitu na vifaa, lakini hakuna watumishi, hakuna namna ambavyo tunaweza kukiendesha kile Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri wa Utumishi lakini pia nimwombe Waziri rafiki yangu Mheshimiwa Bashungwa pale aangalie kwenye watumishi hawa wanaoajiriwa, watupelekee kule. Hospitali ya Wilaya ipo tayari, lakini nataka niwaambieni Wilaya ya Chemba hakuna Daktari wa Meno hata mmoja, yaani wilaya nzima pamoja na kuwa tuna Vituo vya Afya vinne, tuna Hospitali ya Wilaya, tuna Vituo vya Afya viwili ambavyo viko tayari havina Madaktari, lakini Wilaya nzima ukitaka kwenda kutibiwa meno lazima uende Kondoa au lazima uje Dodoma. Niwaombe sana, niwaombeni sana hawa wanaowaajiri angalieni sana Wilaya ya Chemba. Ni kweli Wilaya ya Chemba ilikuwa sehemu ya Kondoa, sasa kila kitu kipo lakini watumishi hatuna. Nataka niombe hili lizingatiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili na la muhimu sana, tuangalie juu ya ikama ya uwiano, yaani unaweza ukashangaa sana kwamba hizi Wilaya zingine sijui ziko wapi. Utakuta wakati Wilaya ya Chemba ina asilimia 22 ya Watumishi wa Kada ya Afya, zipo Wilaya zina asilimia 88, sasa hii haiwezi kuwa sawa hii, yaani Tanzania hii Wilaya moja ina asilimia 22, Wilaya nyingine ina asilimia 87 na watumishi hao hao wanaajiriwa na Serikali, hii haiwezi kuwa sawa. Ni lazima tuangalie njia nzuri ambayo walau tutagawana watumishi hawa pamoja na kuwa kuna upungufu kila mmoja apate walau kwa kiwango kile ambacho kinastahili. Hilo lilikuwa la muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, sina mambo mengi, nafahamu kuna shida kwenye Kada ya Elimu lakini angalau kwenye Kada ya Elimu tuko asilimia 49, upungufu uliyopo ni kama asilimia kama 51, hivyo tuangalieni huku ambako Wilaya zetu zimeanzishwa juzi juzi na Wilaya za vijijini na ni ukweli kwamba wakati mwingine unaweza ukashangaa sana wanasoma taarifa za namna gani kwenye Afya Wilaya fulani imefanya, halafu unalinganisha Wilaya ambayo ina asilimia 22 ya watumishi unailinganisha na Wilaya ambayo ina asilimia…

MWENYEKITI: Weka mic yako vizuri Mheshimiwa Mbunge.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasema kwamba, unataka kulinganisha wilaya hiyo na wilaya ambayo kimsingi haina watumishi wa afya wala watumishi wa elimu. Niwaombe sana sana, nimesimama hapa kwa ajili ya ombi hilo maalum Kituo cha Afya Soya ambacho tayari kimekamilika, kimejengwa na wafadhili wa KOICA, watuletee watumishi wa afya ili hospitali ile ifunguliwe na tulishamwomba na Waziri Mkuu aje aifungue. Sasa anafunguaje wakati hakuna hata Daktari mmoja. Pia tumeshawatumia database kule TAMISEMI wanafahamu kwamba kuna idara ambazo kabisa hatuna Madaktari kama nilivyosema Idara ya Meno. Niwaombe sana, waliangalie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi naomba nichukue fursa hii kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama yetu Samia kwa namna ambavyo ametoa fedha nyingi kama tulivyoomba kwenye bajeti iliyopita. Ninaamini kama wenzangu walivyosema sidhani kama wakati wowote imetokea kuomba fedha 100% na zikatoka 100% nampongeza sana.

Mheshimiwa Spika, pili, nachukua fursa hii kuwapongeza kwanza Waziri mwenyewe Mheshimiwa Jumaa Aweso, Naibu Waziri na pia nampongeza Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na wataalam wote. Ninafahamu kwamba kweli kwa sasa tunaona mwelekeo wa Wizara. Vile vile tunaona mwelekeo kwamba changamoto za maji zinapungua. Nami namwomba Mheshimiwa Rais awabakize bakize maana ukiwa na midfield wazuri ukaingiza mwingine unaweza ukapoteza, ili angalau baada ya miaka kadhaa tunaweza tukaona tumepata mwelekeo mzuri.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme machache kwanza, kuhusu jimboni kwangu. Ni ukweli usiopingika, nanyi wataalam mnajua kwamba Jimbo la Chemba pengine ndiyo lina upungufu zaidi wa maji. Pengine ni kwa sababu ya eneo lenyewe lilivyo, maana nafahamu kwamba mmekuwa mkifanya jitihada za kuja kuchimba visima lakini maji hayapatikani. Takwimu zinaonesha kwamba kwa sasa vijijini wanapata maji kwa asilimia 87, lakini kwangu ni asilimia 28.1 mpaka leo. Sasa unaweza ukaona kama hii takwimu ya asilimia 87 imeshushwa na asilimia 28.1 maana yake changamoto ni kubwa sana. Kwa nini? Kwa sababu wakichimba maji wanakosa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sana mwaka 2021 kwenye bajeti iliyopita mlikuja na jambo zuri sana kwamba sasa tunakwenda kuchimba mabwawa mawili ya kawaida pale Chemba. Namwomba sana Katibu Mkuu, kwa sababu fedha mmepewa asilimia 95 na sasa kuna fedha zinaendelea. Maana yake hizo fedha mlizopewa na za kwangu za yale mabwawa mawili zipo, lakini mpaka leo naona kuna shida kidogo, hatujayaona hayo mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini moja ya kunusuru hali iliyopo, ni hizi rasilimali tugawane sawa. Kuna jambo moja kidogo linaumiza kichwa. Unaona Wilaya fulani upatikanaji wa maji ni asilimia 90, lakini miradi mikubwa ndiyo inapelekwa huko. Nawaomba sana wataalam waliopo huko, ni vizuri sasa tukawekeza kwenye maeneo ambayo upatikanaji wa maji au asilimia ya maji ni chache, ili twende wote kwa pamoja. Naamini kwamba wana kikosi kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nawashukuru maana Mheshimiwa Waziri anasema, asiyeweza kumshukuru mwanadamu mwenzake, hata Mungu hawezi kumshukuru. Kwa hatua za makusudi mwaka 2021 mmenichimbia visima kama 15, lakini bahati nzuri nafikiri target ilikuwa ni kuchimba visima 18 lakini bahati mbaya maeneo mengi yakawa yanachimbwa, maji hayapatikani. Naamini asilimia zinazokuja sasa hivi, zitakuwa pengine zimepandisha upatikanaji wa maji kutoka asilimia 28 point ngapi, angalau zifike 40.

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho ninasisistiza; nasisitiza tena na tena, nawaomba yale mabwawa tuliyoandika kwenye bajeti ile angalau mkachimbe pale ili tuweze kuwa na uhakika wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi mnafahamu mwaka 2021 niliongea sana juu ya Bwawa la Farkwa. Kipekee kabisa naishukuru Serikali. Pia nakushukuru wewe Waziri mwenyewe, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Naibu Waziri, nimekuwa mara kadhaa nikikutana nao kokote; kwenye korido au sehemu yoyote na lazima niulize hili jambo limekaaje? Kwa hiyo, nawashukuru sana. Sasa kuna mwelekeo bwawa lile linaenda kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wasiwasi wangu mkubwa, andiko la mradi ule mimi nimepitia. Andiko lile linasema, tunaenda kujenga Bwawa la Farkwa kwa ajili ya kuleta maji Makao Makuu Dodoma. Nanyi mnafahamu kule Chemba maji ni changamoto, ukichimba hayapatikani.

Mheshimiwa Spika, nawaomba twende kuweka mradi ule lakini ni lazima maji yale yaanze kutumika Chemba kabla hamjaleta Makao Makuu. Haiwezekani sisi tuwe na ng’ombe tukamue maziwa, tuyalete Dodoma, ndiyo tufungiwe kwenye packet tuletewe Chemba. Haiwezekani. Nawaomba sana mwangalie adjustment ya aina yoyote, phase ya kwanza, sisi watu wenye mradi tupate maji halafu phase ya pili ndiyo tulete huku Makao Makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika, mimi nakaa Dodoma mara nyingi zaidi, angalau maji yanapatikana kidogo. Kule Chemba maji hakuna. Tuna vijiji 114. Vijiji ambavyo angalau maji yanapatikana kidogo ni vijiji 57. Vvijiji 57 vingine hakuna maji kabisa. Mnaweza mkaona hali ilivyo ngumu. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, nakuamini sana, naamini kikosi kilichopo, na naamini jambo hili linaweza kwenda kumalizika.

Mheshimiwa Spika, la pili, nawashukuru pia kwa mradi huu ambao ndugu yangu Mwana FA anaongelea. Mradi huu wa miji 28 tumeuongelea sana Bungeni na kwenye maeneo mengine. Nawashukuru sana kwa sababu mradi huu angalau pia unakwenda kupandisha takwimu za upatikanaji wa maji kwenye Wilaya yetu ya Chemba. Nami naomba kama walivyoomba wenzangu kwamba uwahishwe basi ili uanze mapema.

Mheshimiwa Spika, moja ya changamoto nyingine ambayo naiona, ni kwamba ule mradi unaenda ku-cover maeneo ya mjini Chemba na pale mjini kidogo sasa hivi tuna mradi unaendelea. Sasa sijui ni nini. Nafikiri ni lazima tushauriane; yaani lazima niwepo pia kushauri wapi tunahitaji maji zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea kushukuru, niwashukuru sana na Counsenuth, hawa wenye shirika hili kwa kweli wametusaidia sana na wana teknolojia ya kisasa. Nawashauri watu wa Wizara, hebu jaribuni kuongea na wale watu. Wale watu wakipima pale ambapo sisi tumekosa, wao wanapata. Wana mpango wa kuchimba visima tisa, lakini visima sita sasa hivi vina maji. Nao wanaenda sehemu ambayo sisi tumetoa shilingi 45,000,000 tukakosa maji, wao wakienda wanapata. Sasa hii challenge naomba niwaambie, hebu tuangalie, au kama ikiwezekana yule mtu ambaye anafanya geographical survey pale, mumtumie. Kwa sababu kuna hoja ambayo mimi siielewi sana. Nimewapeleka sehemu ambapo sisi tumechimba tukashindwa, wao wakichimba wanapata maji; na wananihakikishia kwamba hapa sisi tunapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa nafasi hii naomba niwashukuru sana Counsenuth, kwa hakika mnafanya kazi ya kitume, mmetusaidia sana watu wa Chemba na asiyeweza kumshukuru mwanadamu mwenzake, hawezi kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, naona unashika mic. Baada ya kusema haya, naambiwa muda wangu umekwisha, naomba kuunga hoja mkono.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi nianze kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mambo makubwa kabisa ambayo anaifanyia nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru pia kwa hotuba nzuri ya Waziri Mkuu kila mtu humu ndani anafahamu namna ambavyo Waziri Mkuu ni mwema, muungwana ambaye ni rahisi kabisa kufikika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nichangie kwenye maeneo mawili muhimu, Eneo la kwanza ni eneo la maji, moja ya maeneo ambayo yamekuwa na shida kubwa ya maji kwenye nchi yetu hii ni Wilaya ya Chemba ni kwa sababu ya hali ya kijiografia ni maeneo machache sana ambayo ukichimba maji unapata.

Mheshimiwa Spika, nataka nimshukuru Waziri wa Maji baada ya kuelewa changamoto hizi yapo mambo makubwa sasa Chemba yanafanyika naomba nitaje miradi michache tu ambayo sasa inaendelea. Ninafahamu watanzania wote wanafahamu moja ya changamoto kubwa ya wananchi ni maji. Na hasa maeneo ya vijijni kama kwetu, kwenye eneo langu la chemba kuna miradi mingi inaendelea moja ya miradi hiyo ambayo kwa dhati kabisa namshukuru Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa Kelema ambao una milioni 500, Mradi wa Babayo ambao unaendelea una milioni 500, Mradi wa Kubungo unaendelea unazaidi ya milioni 335, Mradi wa Chandama milioni 550, mradi wa machija una milioni 700 na mradi wa visima 11 vya awali milioni 550. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya yanaenda kupunguza kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa maji. Naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais lakini pia namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji. Mara kadhaa kule ambako nimeenda kutoa ushauri ni namna gani tutatue chamgamoto ya Chemba kwa sababu ni maalum ameweza kunielewa na kunisikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika. Pamoja na miradi hiyo lakini pia tuna miradi mikubwa ya mabwawa nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu jana katika hotuba yake alielea kwa kina namna gani wanaenda kutekeleza mradi wa Bwawa la Farukwa. Kwenye bajeti iliyopita tulitengewa milioni 283 nishukuru watu wako site na kazi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, kwenye mradi huo kuna jambo la kufanya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ukisoma vizuri andiko la mradi ule linaeleza linaenda kuhudumia watu milioni 2.5 wa Dodoma mjini haliongelei kokote Habari ya Chemba. Mheshimiwa Waziri Mkuu tumefika kwenye eneo la mradi ukatuahidi na sisi tutapata maji naomba wataalamu wetu waanze kufikiria ni namna gani na sisi tuaenda kupata maji kwenye mradi ule.

Mheshimiwa Spika, nishukuru sana namna ambavyo Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Waziri wa Maji ambaye mara kadhaa umefika kwenye mradi huo. Lakini pia niwashukuru kumekuwa na miradi ya mabwawa midogomidogo. Tumechimba mabwawa manne kwenye mwaka huu wa fedha lakini pia tuna mradi mkubwa wa bwawa la bilioni tatu pale Chidoka. Kandarasi ilitangazwa tukaenda kumtambulisha mkandarasi lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu mpaka leo yule mkandarasi hajawahi kufika sijui nini kinaendelea.

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana hebu yule mkandarasi afike kwa sababu tulimchezea ngoma siku ile tunafungua ule mradi sasa akipotea moja kwa moja nauliza sasa zile ngoma tulicheza mbona sasa hivi hayumo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana kwa kweli Wizara ya Maji lakini pamoja na shukrani hizo yapo maeneo naomba wanisaidie tumefanya survey wenyewe kwenye vijiji tisa kwa ajili ya kupata maji. Na nafahamu kuna hizi mashine za Uviko zimekuja Dodoma kwa sababu tume survey wenyewe kwa gharama zetu kwenye vijiji vya Chang,ombe, Magandi Jinjo, Jangalo, Songoro, Piho, Tandala, Dinai, Takwa tunaomba zile mashine zikaanzie eneo la Chemba kwa sababu ndio eneo ambalo lina asilimia ndogo zaidi ya upatikanaji wa maji kwa Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya miaka miwili hii ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tumepunguza upungufu wa maji kwa asilimia kubwa sana watu ambao wanafikafika Chemba wanafahamu kwamba miaka miwili iliyopita upatikanaji wa maji ulikuwa ni asilimia 23 sasa hivi tume jump mpaka asilimia 36, haya ni mageuzi makubwa sana lakini miradi hii ikikamilika, miradi hii ambayo sasa hivi inaendela tunaenda kupanda mpaka kwenye asilimia 54. Kwa hiyo, nisipomshukuru Mheshimiwa Rais kwa fedha nyingi ambazo zinapatikana nitakuwa siyo muungwana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba nitoe shukrani kwenye eneo la barabara miaka miwili iliyopita bajeti ya barabara ya Chemba ilikuwa ni milioni 700 tu lakini mtandao mzima wa barabara ulikuwa ni kilomita 736 unaweza ukafikiria ni namna gani unaweza kutengeneza unamtandao kilometa 700 halafu unapata bajeti ya milioni 700. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sasa tumeongezewa zaidi tunapata bilioni 2.3 angalau maeneo mengi ya vijijini yanaweza kupitika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaombi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. kwa barabara ambayo inatoka Kontoro, Sanzawa, hadi Ntendo lakini pia inavuka eneo la Mto Bibu kwa hiyo bajeti ya bilioni 2.3 hakuna namna ambavyo tunaweza kujenga imeshafanyiwa kila kitu na inahitaji zaidi ya bilioni tatu yenyewe peke yake. Wakati Mheshimiwa Rais amekuja Chemba Dkt. Samia Suluhu Hassan nililisema hilo na tukaahidiwa sasa tuwasiliane na Wizara husika ili kazi ile ikafanyike nikuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu hebu tusaidie katika hilo maana fedha zinazokuja kwa ajili ya barabara hatuna uwezo wa kutumia maana tulitumia fedha hizo bilioni 2.3 maana yake sasa tutumie fedha zote kwenye barabara moja wakati barabara nyingine zitakuwa zina hali mbaya.

Mheshimiwa Spika, tuna barabara kubwa ambayo imetangazwa kandarasi, barabara ya kutoka Kibarashi, Handeni hadi Singida. Barabara hii zaidi ya kilomita 100 ipo kwenye jimbo langu na ambaye nina uhakika barabara hii ikijengwa Maisha ya watu wa Chemba itakuwa rahisi sana. Lakini barabara hiyo ina viunganishi vya barabara ambavyo kujenga peke yake itakuwa changamoto nyingine.

Mheshimiwa Spika, ninomba kuna kiunganishi cha kutoka Goima Mondo hadi Bichwa kuunganisha na barabara kuu ya Arusha chenye kilomita kati ya 24 na 28 nacho naomba kiangaliwe namna ya kujengwa lakini si hiyo tu kuna barabara ya kutoka Malamaya kiunganishwe na hiyo barabara eneo la Donsee kilometa kati ya 28 na 26 nazo hizo barabara zinatakiwa zitafutiwe fedha ili ziweze kujengwa kwa hiyo kufanya hivyo tutakuwa tumepata package nzima ya barabara yote ambayo hii sasa tunaongelea ya kutoka Kibarashi hadi Singida kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba pia kuishukuru Serikali kwa sababu yapo mambo mengi yamefanywa kwenye Afya. Miaka miwili iliyopita Chemba haikuwa na Hospitali ya Wilaya kulikuwa na ujenzi umeanza lakini tumepata fedha zote na hospitali imekamilika zipo changamoto za Watumishi, sasa hivi pale, ipo changamoto ya Gari ya Ambulance. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ikikupendeza kwa sasa hivi hospitali inahudumia watu wengi sana inahudumia watu zaidi ya laki tatu. Kama kuna uwezekano wa kupata gari sehemu yoyote kwa sababu kwa saizi hali iliyopo inabidi tukachukue gari la Kituo cha Afya Mbijo ili lije lifanye kazi kwenye Hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, tatizo hilo limekuwa ni tatizo la muda mrefu na nimewahi kuliuliza kwenye swali la nyongeza lakini nikaahidiwa mpaka sasa hivi hatujapata gari hilo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya nakushukuru sana, kwa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Kwanza kabisa ninachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, ambae ametujalia afya njema na amekuwa akitujalia uhai. Naomba nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hakika asilimia 96 ya fedha zilizotoka ni kubwa sana. Wabunge wa muda mrefu wataona ni muujiza kidogo kwamba siyo rahisi fedha nyingi kiasi hicho zitoke kwa pamoja kwa ajili ya miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninamshukuru Mheshimiwa Waziri. Ndugu yangu, Mheshimiwa Aweso, amekuwa akifanya kazi kubwa na Naibu Waziri wake, lakini pamoja na kazi kubwa leo itabidi niseme maneno machache kidogo. Nashukuru kwa mradi wa Farkwa, mradi mkubwa kabisa ambao naamini unaweza kutosheleza maji Dodoma. Changamoto ni moja tu katika mradi ule, andiko la mradi ule linaonesha maji yale yanakuja Dodoma maana yake sisi Chemba hatuna tunachopata katika mradi mkubwa ule. Sasa sijui hao walioandika wanawaza nini, yaani sisi tuna ng’ombe tunamlisha, tunakamua maziwa, tunapeleka watu wakanywe sisi tusipate, hii haiwezekani!

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishasema mara kadhaa, nimesema kwenye vikao vya ndani, lakini bado kila kikao mnaeleza maji haya ni kwa ajili ya Dodoma. Sasa sisi wananchi wa Chemba kwa nini tuwe na lile bwawa, la nini, linatusaidia nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri alisema ndugu yangu pale kwamba na yeye kwenye bwawa lake maelekezo ni hayo hayo, kwamba maji yanapatikana kwenye Jimbo lake lakini eti maji hayo yakatumike sehemu nyingine, hii haikubaliki. Ninataka niwahakikishie Mheshimiwa Waziri, mkiweka mabomba pale tutaenda na vijana wetu kwenda kuyakata, kwanza tuanze kutumia sisi halafu ndiyo watu wengine waende kutumia. Mheshimiwa Waziri, naomba ninukuliwe hivyo na hivyo ndivyo ninavyoamini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nina jambo la pili, umekuwa ukitupa miradi mingi sana ya maji na Chemba ni moja ya maeneo ambayo yanapata miradi mingi ya maji,
2021/2022 tulipata visima 11 lakini mpaka leo kwenye visima hivyo vilivyochimbwa ni vitatu. Tume-carry mwaka huu tulikuwa na visima vitano, hakuna kilichochimbwa mpaka leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa nini tuje hapa kwenye bajeti tujadiliane kwamba bwana tumekupa visima hivi, mimi niende vijijini nikaseme halafu fedha hizo, yaani visima hivyo havipo, hii haiwezi kuwa sawa. Mimi nafahamu namna ambavyo ninyi ni wachapakazi na mnafahamu nimetembea kila mahali kuhakikisha – na mimi naambiwa fedha zimetoka asilimia 96, ukiwauliza Wakandarasi kwangu wanasema hawajapata fedha ndiyo maana hawatekelezi miradi, hili jambo linaumiza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninafahamu kwamba mkiniambia kuna maji naenda kule kuwaambia ndugu zangu hapa kwenye Kijiji X maji yanakuja. Sasa nabaki naonekana mimi Mbunge mwongo wakati fedha tumepitisha hapa lakini kule hazifiki. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, ninafahamu namna ambavyo unafanya kazi vizuri, katika hili kidogo tunaweza kupishana kwa nia njema zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna miradi miwili ya siku nyingi sana,Mradi wa Machije ambao una milioni 700 na mradi wa Chandama ambao una milioni 500. Mradi huu ulikuwa ni kabla RUWASA haijaanzishwa, mpaka leo mkandarasi kaweka bango hakuna kinachoendelea na kila siku tunau-carry over kwenye bajeti nyingine. Maana yake ni nini? uki-carry over unanipunguzia mimi ceiling ya kuendeleza miradi mingine. Wakati mwingine ukisema sana unaonekana kama unaleta vurugu. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri, mimi ni katika watu wanaokupenda sana na kukuamini, unafanya kazi kubwa, lakini wakandarasi wa namna hii wa nini? Na kwa nini iwe Chemba tu, kwa nini kwamba Chemba ndiyo miradi haiwezi kukamilika? Nataka nikuombe sana uingilie. Nikuombe baada ya kumaliza bajeti yako hii, najua tutakupitishia vizuri, twende kule ukamalizie na wewe hii miradi ambayo inakera zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la muhimu sana na hili ni la nchi nzima kwamba ni lazima tuweke sera ya uhakika. Amesema Mheshimiwa Taletale kwamba pale kwake upatikanaji wa maji ni asilimia 31, yapo maeneo upatikanaji wa maji ni asilimia 92, nchi hii moja haikubaliki. Wewe mwenyewe mara kadhaa umesema kupata maji ni haki ya mwananchi yeyote yule, haikubaliki! Kwangu pia ni asilimia 36, ukienda Jimbo la jirani ni asilimia 72.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima hao wanaopanga bajeti waangalie namna gani wanaweza walau ku-balance ili maeneo yote haya tuwe na uwiano unaofanana, walau unaokaribiana, hii haikubaliki. Kwamba una asilimia 36, mlipakodi huyohuyo kuna mlipakodi mwingine ambaye ana asilimia 92 na huyo mwenye asilimia 92 ndiye anayepewa miradi mikubwa mingi zaidi ya maji, haya mambo lazima tuyaweke sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima kuwe na mpangilio na uwiano wa namna gani tunaweza kugawana hizi rasilimali za nchi yetu haiko sawa kabisa, niliomba kulisema hilo ili wakati mwingine muangalie namna ambavyo tunaweza kwenda mbele kwa uelewano mzuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye miradi ya UVIKO walinunua magari na Mheshimiwa Waziri tulikubaliana, tuliongea vizuri, kwamba kwa sababu Chemba kuna changamoto kubwa ya maji kuliko eneo lolote la Dodoma magari yale yakaanzie Chemba. Ninataka wakati unajumuisha ujibu maswali mawili maana kuna changamoto kidogo, utaniambia tangu yamekuja yamechimba visima vingapi. Maana lile gari tukimpa raia mwingine atachimba visima 100 kwa mwaka, lakini likiwa Serikalini linachimba visima 10 kwa mwaka mzima, haiwezi kuwa sawa na tija yake itakuwa ni ndogo sana, lazima tufike mahali tuangalie namna sahihi na bora ya kuyatumia hayo magari.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe mara kadhaa nimekusikia ukisema kwamba yako maeneo ambayo ukichimba maji ni ngumu kuyapata na moja ya maeneo hayo ni la Chemba. Tuna mradi wa Chemchemi ya Ntomoko kule, kuna eneo la pale Igunga, kidogo kilometa kama tano, sita hivi. Tumechimba mara nne hatujapata maji lakini tunaweza kuyaleta pale kwa gharama ndogo kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana, unajua namna ambavyo nakuheshimu, najua wewe ni mdogo wangu, lakini naomba katika hili tuweze kusaidiana. Hatuwezi kuendelea kila mwaka kuja hapa Bungeni mimi nisimame niseme upatikanaji wa maji ni asilimia 32 na mwakani uwe asilimia 32, hii haiwezi kukubalika kabisa na uwezekano wa kupanda unakuwa ni mdogo kwa sababu tunapitisha miradi ambayo haitekelezwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya naomba nitumie nafasi hii kukushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi walau nichangie kidogo katika Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia afya sote na tuko hapa. Nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anaendelea kulihudumia Taifa hili kwa namna ambavyo anatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hakika anafanya kazi kubwa sana. Mimi nafahamu kila Mbunge hapa kwa wakati moja au mwingine ameshawahi kwenda kuomba jambo. Mnafahamu namna ambavyo yuko rahisi na anafikika. Pia nimshukuru Naibu Waziri ni rafiki mzuri wa ndugu zangu wote mlioko hapa na mimi ninaamini wale ambao tunatoka kwenye Majimbo yenye shida nyingi, Majimbo ya Vijijini ambao watu hawana uwezo wa kutibiwa, mara moja au mara mbili tumeenda kwake na ametusaidia. Nichukue nafasi hii pia kumshukuru Katibu Mkuu na Watendaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimshukuru Mtendaji Mkuu wa MSD. Tumekuwa na changamoto ya muda mrefu sana huko nyuma. Ninyi ni mashahidi huko vijijini dawa zilikuwa hazifiki lakini kwa sasa kuna flow nzuri ya dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri utakuwa ni shahidi Bunge lililopita moja ya ajenda kubwa iliyokuwa hapa ni MSD, ndiyo maana kila anayechangia leo, maneno yamekuwa machache kwa sababu dawa zinafika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo la muhimu hapa la kuongea, kwamba kazi ya MSD imebaki kupelekewa fedha, kwenda kununua dawa na wale waliopeleka fedha kwenda kuchukua. Sasa hili jambo haliko sawa. Hatuna option nyingine, ni lazima MSD wapewe fedha. Kama tuna dhamira ya dhati ya kuhakikisha afya za Watanzania zinakuwa imara na kupunguza gharama za Serikali za kununua dawa, ni lazima fedha iliyoombwa na MSD wapewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto, wakati mwingine unaweza kujiuliza maswali, kwamba mbona MSD kila mwaka wanapewa fedha, lakini hawana capital ya kuagiza dawa wenyewe? Nimejaribu kufuatilia hili jambo nikaona ni kweli kwamba Wabunge wengi wanaweza wakafikiria hilo kwamba wale MSD pengine kuna fedha ambayo wanabaki nayo. Ukweli ni kwamba fedha wanayopelekewa ndiyo wanayotumia kwenda kununua dawa, na kafaida kale kadogo pengine ndiyo anakatumia kuendesha ofisi. Sasa ni lazima sasa tuangalie namna bora ya kutoka hapo walipo. Namna bora ni kuhakikisha Wizara ya Fedha imewapa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui kama tumewahi kufikiria, ni lazima tuamini kwamba katika kitu cha thamani kubwa hapa duniani ni uhai. Ni ukweli kwamba afya ndiyo uhai. Hapa nyuma kumetokea ugonjwa wa Uviko. Ilikuwa ni changamoto kubwa kwa sababu dawa zote tunaagiza huko nje, na viwanda vyetu vilikuwa vimefungwa. Kwa nini hilo halionekani? Maana yake kuna siku tutakosa dawa moja kwa moja, kwa sababu tumeshindwa ku-empower MSD. Bawaomba sana Wizara ya Fedha, waangalie kwa upana mkubwa changamoto hii kwa namna ambavyo ilivyo kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri tuna mtendaji mzuri wa MSD sasa hivi, tunaweza tukamwamini, tukampa fedha, tukaangalia baada ya miaka mitatu, nini kinaendelea? Ila tukiendelea kuwapa fedha ili waagize dawa, wataagiza dawa, watapeleka huko kwenye hospitali, nao hawana kitu, na hawana Development Plan ya aina yoyote, maana yake maisha yetu yatakuwa ni hayo. Nawaomba Wizara ya Fedha katika hilo la msingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hangamoto kubwa sana na ya kupindukia ya watumishi wa afya. Jimboni kwangu mwaka 2022 tumefungua zahanati nane kwa pamoja, lakini hizo zahanati hazina wahudumu. Mheshimiwa Rais ametoa fedha nyingi zinakuja vijijini, nikutolee mfano kwenye hospitali yetu ya wilaya, mmetuletea fedha, tumefunga X-Ray mpya, Ultra-Sound mpya, mashine ya macho mpya, ya meno mpya, lakini hakuna mtumishi hata mmoja. Maana yake zinachakaa. Mmetuletea mpya, zinachakaa, hakuna chochote kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana, mwenzangu mmoja alisema tunavyoendelea kuweka hii miundombinu ya afya ni lazima tufikirie pia ni namna gani tutapata watumishi wa kwenda kusaidia kwenye vifaa hivi. Haina tija yoyote. Watu wangu pale Chemba wakiona kuna X-Ray mpya kweli, kuna Ultra-Sound, lakini hakuna chochote kinachoendelea. Mtu akitaka kufanyiwa Ultra-Sound, ni lazima aje Dodoma General. Namwomba Mheshimiwa Waziri sana katika hilo hebu tusaidie. Naamini sasa kwenye watumishi hawa, ajira mpya zilizotangazwa mtatufikiria zaidi katika Wilaya yetu ya Chemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kada zote za afya, sisi tuna asilimia ishirini na kitu ya watumishi. Kwa hiyo, unaweza ukaona changamoto kwa ukubwa wake ilivyo kubwa. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuwaombeni sana, sana, sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la muhimu, miradi ya afya ambayo inatekelezwa, hii miradi ya World Bank,na Global Funds, kuna changamoto kidogo ipo. Kwa mfano, kuna jengo la Kata ya Msaada limeanza kujengwa mwaka 2007. Mwaka 2007 hapa wengine walikuwa bado wadogo, mpaka leo halijakamilika na limeishia njiani na watu wanaliona. Kila Mbunge akija, anaambiwa kama unataka tukupe kura, hebu malizia hilo jengo. Sasa kwa nini tunakuwa na mipango ambayo haikamiliki?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna Kituo cha Afya Makorongo. Sasa hivi kinatumika na kilifunguliwa na Mheshimiwa Rais wakati huo Jakaya Mrisho Kikwete, hakina theater, hakina maabara, hakina mochwari. Kwa nini kiwe nusu? Nawaombeni sana, nimeandika barua mara kadhaa. Nilimwomba Mkurugenzi akaandika, tukaambiwa tulete BOQ lakini mpaka leo bado hakijakamilika, wala hakuna fedha yoyote ambayo imekuja kwa ajili ya umaliziaji wa majengo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niishukuru tena Wizara, niwashukuru watendaji, na Waheshimiwa Mawaziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara muhimu sana ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia afya njema na ametujalia uhai tupo hapa leo. Jambo la pili namshukuru Mheshimiwa Rais kwa hakika anayo dhamira njema, ana nia njema. Sisi ambao tunatoka maeneo ambayo yana migogoro wanafahamu kwamba iliteuliwa Kamati ambayo ina Mawaziri Nane ambao wanashuhulikia huu mgogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kidogo sana kuhusu mgogoro na watu Chemba nisiposimama kuongea kwenye Wizara hii watanishangaa sana na inawezekana nikapoteza kabisa asilimia 40 ya kura zote. Kwangu kuna changamoto moja ndogo sana lakini shida kubwa ya changamoto hii ni utashi wa Viongozi tuliyonao. Hii naomba niseme wazi kama kumsema hivyo nakosea potelea mbali lakini nataka niseme ukweli. Tuna mgogoro ambao umeanza mwaka 2014, mgogoro huu umeacha wakulima wananchi wangu 1,168 bila mashamba. Ni jambo la ajabu sana kwamba unakuta watu wana mashamba alafu unawaondoa tangu mwaka 2014 mpaka leo wanaendelea kuzurura haujui wanaishi vipi? Ni jambo la ajabu na haliwezi kutokea sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo cha mgogoro huu ndiyo maana nasema shida ni viongozi. Chanzo cha mgogoro huu ilikuwa ni ku–review mipaka, wakati wana – review mpaka kati ya Chemba na Kiteto maeneo ambayo yalikuwa ya Kiteto yalirudi 197 Kondoa wakati huo, sasa hivi ni Chemba. Baada ya kurudi Kondoa ambaye ni Chemba mashamba yao yakabaki Kiteto maana yake ni nini? maana yake kiijiji baada ya kuweka mipaka mipya wananchi wangu wamebaki na kijiji lakini mashamba yao yamebaki Kiteto na sisi wote tunafahamu, kwamba mipaka ya utawala haikufanyi upoteze haki yako ya shamba lako. Hii inafahamika lakini cha ajabu wananchi wale walilazimishwa na kunyang’anywa mashamba yao kwa sababu tu sasa mipaka ya kiutawala wamerudi huku Chemba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la ajabu sana. Ninayo hukumu ya Mahakama hapa, wameenda Mahamani wameshinda, tena Mahakama ya Wilaya ya Kiteto kule kule lakini mpaka leo bado watu wamebaki hawana mashamba. Sasa mimi namuomba Waziri kama kuliko nibaki na watu ambao hawana mashamba naombeni kile Kijiji cha Oruboroti kichukeni kiwe Kiteto ili mashamba yao wabaki nayo, kuliko kubaki na watu 1,168 hawana mashamba maana yake wamekuwa tegemezi kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nimekuwa nikipata ushirikiano sana wa Viongozi wa kutoka Kiteto wenyewe, ninayo barua ya Waziri wa TAMISEMI wakati huo, ambayo inamuelekeza Mkuu wa Mkoa wa Manyara na Dodoma kwamba kwa sababu ya ku– review mipaka hiyo isiwe sababu ya wananchi wa Oruboroti kupokonywa mashamba yao, mipaka hiyo ni ya kiutawala tu. Barua hiyo haijawahi kufanyiwa kazi ninayo hapa Mheshimiwa Waziri, matokeo yake watu wangu wakienda kulima wanashikwa, wengine wanapelekwa, imagine mtu anachukuliwa Kiteto anapelekwa kufunguliwa kesi Arusha badala ya Manyara, huko anabambikiwa kesi ya nyara za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuombe sana mimi nina uhakika yeye anaweza kutusadia, jambo hili limekuwa linaumiza sana hasa kwa watu wa Chemba. Siyo hivyo tu, nataka nikuonyeshe jambo la ajabu sana, baada ya hukumu ya Mahakama kutoka Mkuu wa Wilaya ya Kiteto ninayo barua hapa, alimwandikia Afisa Tarafa wa Makame ambapo ndiyo mashamba yapo. Kwa sababu wananchi hao wameshinda kwenye kesi yao Mahakamani, warudishiwe mashamba hayo ndani ya wiki saba. Mkuu wa Wilaya anamwagiza Afisa Tarafa wake na hakuwahi kutekeleza mpaka leo, sasa hii ndiyo nchi ya namna gani? Hii ndiyo nchi ya namna gani? wakati alikuwa ana uwezo tu wa kumpigia simu tekeleza hilo mara moja, tafsiri yake ni kwamba, yawezekana haya maandishi lakini utashi wao wa kutatua changamoto hii haipo, kwa hiyo nikuombe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana pia tulikuwa na Mkuu wa Mkoa, Mbunge mwenzetu hapa anaitwa Mnyeti na wakati huo Mkuu wa Wilaya pia alikuwa Mbunge hapa, nakumbuka majibu waliomjibu maana Mnyeti alimwambia kwa nini unachukua mashamba ya watu wa Chemba? Mkuu wake wa Wilaya ambaye ni Mbunge sasa hivi ananisikiliza kasema hao watu ni wa Chemba lakini, akamwambia Chemba ni Rwanda? Wewe una akili gani? Nakumbuka nilikuwepo, nakushukuru sana Mheshimiwa Mnyeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo unaweza ukaona sababu ya migogoro hii ni sisi viongozi wenyewe. Mimi nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, juzi kama siku tatu, nne zilizopita wameenda tena kubandika maeneo ya Chemba. Kuna changamoto nyingine ni ya ajabu sana, vipo vijiji ambavyo viko Wilaya ya Chemba lakini vinaitika Kiteto kwa sababu tu wao ni Wamasai kwamba wako tayari kwenda kwa Wamasai wenzao. Kitongoji kipo Chemba lakini wao michango yote kila kitu wanafanya kwenye Wilaya ya Kiteto na ukienda kuwagusa shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi niombe sana, kwa sababu kama ni suala la ku– review mipaka na beacon tayari limefanyika, sasa sijui tutumie maarifa gani? mimi nikuombe sana Mheshimiwa Waziri hebu upate fursa na wewe ukatembee, safari hii Mheshimiwa Waziri eneo lile watu wamekufa mara kadhaa, naiona hali, naliona joto lilivyo, ninaona kabisa hali ilivyo kwamba mvua zikinyesha mwaka huu hali itakuwa tete sana. Sasa niwaombe sana, niwaombe sana hebu ifikie mwisho wa mgogoro huu kwa sababu kama ni Mahakamani tumeenda tumeshinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo limekuja pale Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri kuna watu wanaitwa WMA, WMA wamekuja wamekuta watu wana mashamba, wameongea na kijiji, kijiji hakikuwahi kulipa fidia wala hiyo WMA hawajawahi kulipwa fidia wanawaondoa wananchi wangu na sasa hivi wameendelea kujitanua kwenye maeneo mengine kumekuwa na mgogoro mkubwa sana. Migogoro hii ya ardhi inamaliza ndugu zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi wiki mbili zilizopita amekufa Mwenyekiti wangu wa kitongoji, kwa sababu ya mgogoro wa ardhi, wamemuua kuna mgogoro wa ardhi pale wameenda wakamuua na sasa hivi kesi inaendelea Mahakamani. Kwa hiyo unaweza ukaona namna ambavyo kuna changamoto kubwa hii. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri nimesimama hapa kwa ajili ya kuongea hili tu, na nimesema kwamba kama kuna sababu yoyote au kama ni lazima wale wananchi wa kijiji cha Oruboroti kurudi Kiteto ili mashamba yao yabaki naomba wawachukue, ili mradi warekebishe beacon kuliko kukaa na watu ambao hawana mashamba na kila siku wanatuletea shida. Mimi nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, mimi mchango wangu leo ulikuwa huo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo wanashukuruni sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa mwisho.

Kwanza kabisa na mimi nichukue fursa hii ya kuwapongeza Waziri na wenzake kwa hotuba nzuri sana. Kiukweli katika hotuba za safari hii zilizokuja vizuri kama ikitekelezwa inaweza kutusogeza sana. Hotuba hii inajibu maswali mengi, changamoto nyingi za kisera na mimi naamini watu waliopo kwenye Wizara hii wanatosha kutekeleza mambo waliyoandika wenyewe, kwa sababu hizo, mimi naomba nieleze zaidi mambo ya Chemba. Naomba nieleze changamoto tulizonazo hasa za umeme kwenye Jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza, wenzangu wameongea juu ya Wakandarasi, sisi kwenye awamu hii REA round ya tatu awamu ya pili ina-cover vijiji 50, sasa hivi Mkandarasi yuko site mwaka mzima lakini kwenye vijiji hivi 50 amewasha kijiji kimoja tu ndani ya mwaka mmoja, tafsiri yake kumaliza atatumia miaka 50 vijiji vingine vilivyopo. Wenzangu wameiongelea changamoto hii sasa mimi sipati majawabu kwa nini changamoto hii ipo hivyo. Nafahamu kabla ya kuomba kazi walifanya survey walitafuta majawabu namna gani watapita kuweka kazi hii, lakini hiyo changamoto imeonekana kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri katika hili, zipo Wilaya au Majimbo jiografia yake ni ngumu sana kumpa mwaka mmoja, mwaka mmoja na nusu au miaka miwili kumaliza vijiji vyote 50, mimi hapa maeneo yangu kutoka kijiji kimoja hadi kijiji kingine ni kilomita 50 mpaka 70, unaweza ukaona kabisa jinsi gani kazi hii ilivyokuwa ngumu. Mimi ninawashauri kama wanataka kazi hii itekelezwe kwa wakati, zipo Wilaya ambazo ni lazima waweke Wakandarasi wawili otherwise tutaendelea kugombana leo kwenye mkutano, unaeleza ndugu zangu Serikali hii tiifu imeleta fedha kwa ajili ya vijiji vyote na ndani ya miaka miwili vijiji vyote vitakuwa na umeme lakini inachukua miaka minne. Mimi nimuombe Waziri muangalie uwezekano kwenye Wilaya ambayo jiografia zimekaa vibaya, tuangalie kama tunaweza kuongeza Wakandarasi ili kazi hii ifanyike kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia zipo changamoto nafikiri changamoto zingine ni za kiutawala huko huko. Kwa mfano, mimi ninavyo vijiji ambavyo miundombinu yote imemalizika tangu miezi sita iliyopita lakini hawajawasha umeme. Kila ukienda ukiuliza vipi unaambiwa tunakuja kesho kuwasha, sasa changamoto hii nafikiri ni ya kiutawala zaidi, mimi niwaombe watu wanaohusika hebu tusaidieni yale maeneo ambayo tayari miundombinu ya umeme iko tayari wawashe. Wamesema wenzangu umeme huu una fursa nyingi kwamba tukiwasha umeme, zipo faida za kiuchumi zinapatikana kule sasa kwa nini tunawachelewesha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilipata simu ya mteja mmoja ana kiwanda kidogo cha kukamua alizeti, yeye anakimbizana na alizeti inayotoka shambani sasa hivi, amekamilisha lakini amefika pale wanamuambia kesho, kesho kutwa, kesho kutwa sasa hii ni changamoto kubwa sana. Mimi niwaombeni sana umeme huu unafaida kwetu sisi kule Chemba kwa sababu vijana wengi sasa watapata ajira huko. Niombe sasa hawa watu wanaohusika hebu mjitahidi, pale ambapo maeneo yale miundombinu imekamilika waende kuwasha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia vipo vijiji kama Magandi, Machiga tangu mwaka jana miundombinu iko tayari, mpaka imefika mahali wanagombana na Meneja wa TANESCO kwa sababu wanamuambia kesho, kesho kutwa mtu anafika mahali anachoka. Mimi niwaombeni sana kwamba tunawajibu wa msingi sasa wa kuhakikisha hili zoezi la kuwasha umeme, miundombinu ikikamilika mfanye kwa haraka ili watu hawa wanufaike na huo umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni muhimu sana na wenzangu wameliongelea, Wilaya yangu tunaposema Chemba ni Wilaya mpya hakuna mjini kote ni vijijini, sasa tunashindwa kutafsiri ni nani anapaswa kulipa shilingi 300,000 ni nani anapaswa kulipa shilingi 27,000? Ninaiomba Wizara hebu waje na mfumo sahihi ambao sasa utatofautisha kwa sababu nyie wenyewe mnapita Chemba ni barabarani hapo, Chemba ni kijijini bado na nina uhakika watu wenye uwezo wa kulipa hiyo shilingi 300,000 ni wachache sana, hebu tuangalie namna bora ambayo tunaweza kuwasaidia hao watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, kuna jambo ambalo halijafanyika, tunafahamu umeme utasaidia sana kupunguza shida za maji huko vijijini. Sasa hizi projects za umeme hazikuweka bajeti ya kuweka umeme maeneo yenye taasisi, kama shule za msingi ukiona shule ya msingi ina umeme labda imejengwa kijijini pale pale, lakini ni ukweli usiopingika visima vingi vya maji viko pembezoni kidogo ya kijiji, sasa nafikiri tuangalie upya namna gani ambavyo tunaweza tukasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maeneo yangu mimi, yapo maeneo ambayo maji yanauzwa shilingi 400, shilingi 300 kwa dumu, kwa sababu tu wanatumia dizeli ku-pump zile mashine ili maji yapatikane. Mimi niwaombe sana ndugu zangu nami nakuamini sana Waziri, namuamini sana Naibu Waziri na Viongozi wote mlioko huko jambo hili liko ndani ya uwezo. Nawaombeni mtusaidie, naombeni muangalie namna bora umeme ambao unaweza ukafika kwenye visima hivyo vya maji shule za msingi na zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema siku moja hapa kwamba nina Kituo cha Afya cha Makorongo, ninakumbuka siku Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete alivyokuja kukifungua aliwaambia leteni umeme nikasema mpaka leo umeme haujafika. Sasa unaanza kujiuliza alikuja Waziri, alikuja Mkuu wa Mkoa akasema maneno hayo, alikuja Waziri Kalemani akasema maneno kesho kutwa umeme uwe umefika hapa, sasa wewe ndugu yangu haujafika pale, najua wewe ukifika mambo yatakuwa sawa, ndugu zangu nawaombeni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)