Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Abdallah Jafari Chaurembo (12 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pili nikishukuru chama changu na wananchi wa Mbagala kwa ujumla. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba nzuri ambayo kwa kweli ukiifuatilia inaenda kujibu kero za wananchi.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikijiuliza sana wakati naisoma hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. Katika kila neno kwenye hotuba hii ni dhahiri linahitaji fedha ili tuweze kuitekeleza hotuba hii sambamba na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, nimekaa nikatafakari sana pamoja na matatizo mengi yaliyokuwepo katika jimbo langu, lakini nimeona mchango wangu nijielekeze sana ni kwa namna gani ambavyo naweza kuishauri Serikali namna ya kupata mapato ambayo mwisho wa siku naamini yanaenda kutekeleza hotuba hii ya Mheshimiwa Rais pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, katika kila eneo nililolisoma nimeona tuna nafasi ya kupata mapato ambayo naona Serikali tulikuwa tunayapoteza. Nianze na suala zima la miundombinu.

Mheshimiwa Spika, hotuba yote imezungumza namna ambavyo tunaenda kutengeneza barabara na miundombinu mingine. Hata hivyo, nikija katika suala la utenengezaji wa miundombinu iliyopita na inayotaka kutengenezwa, ni dhahiri kuna baadhi ya maeneo ambayo miundombinu imepita yamelipwa fidia. Baadhi ya Wabunge hapa tumeona wakisisitiza ulipwaji wa fidia kwa baadhi ya maeneo ambayo yametwaliwa na Serikali. Pia nimemsikia Waziri wa Ardhi akisisitiza suala la ulipaji fidia maeneo ambayo yanatwaliwa na umma.

Mheshimiwa Spika, sasa hapa nikaona kuna fedha za Serikali zinapotea. Tunapolipa fidia hatuangalii yule tunayemlipa fidia, hana deni la land rent au property tax? Kama jukumu la kulipa fidia ile ni la halmashauri basi linaishia kulipa fidia na badaye hamna mtu anayejali madeni haya ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, mimi kabla sijaja hapa nilikuwa Diwani katika Manispaa ya Temeke. Tumelipa fidia ya zaidi ya shilingi bilioni 20 lakini baadaye nikafikiria, je, hawa tuliowalipa fidia hawakuwa na madeni ya property tax au land rent? Nikaja kugundua ni fedha nyingi sana ambazo tumezipoteza kwa kutokulipa hizi property tax na land rent. Kwa hiyo, naishauri Serikali washirikiane kati ya taasisi zinazolipa fidia na Wizara ambazo zina mapato yake katika ulipwaji ule wa fidia.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, ni katika miundombinu ya ujenzi. Hotuba ya Bunge la Kumi na Moja na hili la Kumi na Mbili tumezungumzia sekta ya maji, barabara, lakini miradi hii tunaenda kuwapa wakandarasi mbalimbali. Nikawa najiuliza, je, wakandarasi hawa wanazilipa halmashauri zetu city service levy?

Mheshimiwa Spika, mimi nilijaribu pale Temeke, tulikuwa na mradi ule wa uboreshaji wa Jiji la Dar-Es-Salaam. Makampuni yote tuliowapa tenda za ujenzi zaidi ya shilingi bilioni 600 tulihakikisha zinalipa city service levy. Pato la city service levy ndiyo lilikuja kuleta maajabu ya kuweza kujenga madarasa 120 kwa mapato yetu ya ndani. Naomba niishauri Serikali maeneo yote ambayo kuna wakandarasi wanafanya kazi za ujenzi, basi tuone namna gani halmashauri zetu nazo wanaenda kuchukua city service levy zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikaiangalia Wizara ya Ardhi. Wizara ya Ardhi kuna property tax ambayo inapatikana kutokana na majengo yanayojengwa kwenye ardhi zile lakini pia kuna land rent. Halmashauri na majiji mengi zimepima viwanja lakini vinakaa zaidi ya miaka 10 havijaendelezwa; sheria ipo kwa nini Wizara ya Ardhi viwanja vile wasiwauzie watu wengine ili majengo yale yajengwe na hatimaye tuweze kukusanya property tax katika majengo yale?

SPIKA: Sheikh Abdallah utaua hapo. Wako wengi humu hapo walishaugulia tayari, endelea Mheshimiwa. (KIcheko)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, tukitaka tulete mabadiliko ya kweli basi na sisi tunatakiwa tuwe mfano katika kusababisha hayo mabadiliko.

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye sekta ya afya, tumemsikia Waziri hapa asubuhi akisema kuna zahanati moja ilitumia shilingi milioni 40 kununua dawa na ilivyokuja kutoa huduma ikapata zaidi ya shilingi milioni 100, lakini wakaja kununua dawa za shilingi milioni 20. Ni wajibu wetu sasa Wabunge kwenda kufuatilia vitu kama hivi. Tunapofuatilia maana yake malalamiko madogomadogo yanakuwa yanapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye elimu, Serikali yetu imejitahidi sana kuboresha miundombinu ya elimu, lakini yapo makampuni yanaendeleza maeneo kwa kujenga ma-real estate. Kwa mfano, NSSF pale Tuangoma wamejenga nyumba nyingi na wakatuletea wananchi wengi lakini hatuwaoni NSSF kusema hata tunajenga shule moja tukaiita hii ni NSSF Primary School, hawafanyi hivyo. Pia hata maeneo mengi ambayo wamekuwa wakiyamiliki hawayaendelezi kwa muda mrefu. Tukiwaomba maeneo yale basi mtupe maeneo fulani tujenge shule za msingi, sekondari na vituo vya afya, nayo imekuwa mgogoro.

Mheshimiwa Spika, niombe sana, pamoja na kuichangia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais lakini vilevile tupate nafasi kubwa ya kuona ni sehemu gani mapato ya Serikali yanapotea na tuweze kuyadhibiti ili hotuba hii na utekelezaji wa Ilani uende kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, nimalizie, nimeona halmashauri nyingi zikiandika miradi ya kimkakati lakini leo kwenye hotuba ya Rais nimeona kuna mazao ya kimkakati. Nikajiuliza, je, kwa nini katika ile miradi ya kimkakati halmashauri ambazo zina uwezo wa kulima zisiandike andiko la kuomba fedha ili wakalima mazao ya kimkakati ya kihalmashauri ikawa ni moja ya vyanzo vya mapato?

Mheshimiwa Spika, nitakutolea mfano mdogo tu, Halmashauri ya Lindi. Halmashauri ya Lindi imegawa maeneo kwa ajili ya wananchi kuwekeza. Katika semina ile ilikuwa inaeleza mtu ukiwa na ekari 200 ukaweza kupanda mikorosho baada ya miaka mitatu una uwezo wa kila mwaka kupata shilingi bilioni moja. Je, halmashauri ingefanya yenyewe ikatafuta mashamba yake ikachukua ekari 100, ekari 500, ikaomba fedha serikalini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kuwepo leo nikiwa hai. Pili, nakushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuweza kuongea katika kikao hiki cha leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kwa ufinyu wa muda nianze kwa kuzingatia kanuni ya 175 katika Kanuni zetu za Kudumu. Pili, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri aliyeitoa. Kwa kweli ukiisoma ile hotuba, imelezea mambo mengi yaliyofanyika katika nchi hii na kwa kweli mambo yale yamefanywa na viongozi wetu wakubwa kwa Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba natoe ushauri mdogo sana kwa Serikali, lakini tukiufanyia kazi tutaweza kudhibiti uvujaji wa mapato katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kufuatilia miaka yote sioni forum ya kisheria inayompa nguvu Mkuu wa Wilaya aweze kusimamia mapato yanayopelekwa katika Halmashauri zetu kutoka Serikali Kuu. Serikali Kuu inapeleka kwenye Halmashauri zetu, zaidi ya asilimia 80 ya mapato zinaiendesha Halmashauri zetu. Mapato yale yanapofika kwenye Halmashauri zile basi Mkurugenzi anafanya yale anayoyataka bila kupata concern ya Mkuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri iundwe forum maalum ya kumfanya Mkuu wa Wilaya awe Mwenyekiti; Mkurugenzi awe Katibu; Wabunge wa Majimbo na Viti Maalum wawe Wajumbe wa forum hiyo. Forum hiyo nashauri iitwe Kamati ya Maendeleo, Nidhamu na Utawala. Kamati hiyo itatusaidia sana kudhibiti mapato katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme ya watu wa Jimbo la Mbagala. Sekta ya Afya katika Jimbo letu la Mbagala tunayo ile Hospitali ya Wilaya ya Zakiem. Nadhani ni hospitali pekee katika nchi yetu yenye level ya wilaya isiyokuwa na wodi za kulaza wagonjwa. Naiomba sana, Serikali tuipe hadhi hospitali ili tuweze kupata wodi za kulaza wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, katika Sekta ya Elimu, sote tunafahamu katika Jimbo la Mbagala, ndiyo jimbo lenye shule zenye wanafunzi wengi nchi nzima. Shule ya Maji Matitu ina wanafunzi zaidi ya 9,000. Naiomba sana Serikali ilisaidie Jimbo la Mbagala kulipatia shule za kutosha. Katika hili namwomba dada yangu Mheshimiwa Jenista, ndugu zetu wa NSSF wana maeneo mengi wasiyoyaendeleza. Tunaomba sana mtupe maeneo yale yaliyokuwa Tuangoma twende tukajenge shule.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie katika kuzungumza suala la TARURA. Barabara nyingi katika Jiji letu la Dar es Salaam zimekuwa na matatizo makubwa. Mheshimiwa Rais amesema, Halmashauri zetu huko nyuma zilikuwa zinatenga fedha zaidi ya shilingi bilioni nne kila Halmashauri katika ku-service barabara zile. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri utaratibu ule uendelee kurudiwa ili fedha zile zikiunganishwa na fedha zinazotoka kwenye Road Fund ziweze zikafanye kazi kubwa. Kuna Kata ya kama ya Kiburugwa na Kata ya Mianzini iko hoi katika suala nzima la barabara.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara hii ya Nishati na Madini.

Kwanza kabisa niipongeze sana Serikali yetu hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri wanazoendelea kuzifanya katika miradi mikubwa, miradi ya kitaifa, ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wameizungumza. Kwa kweli na mimi niendelee kuuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake na viongozi wote wa wizara kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya katika kuhakikisha suala hili la Nishati na Madini linakwenda vizuri katika Nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tarehe 25 Februari, 2018 Serikali yetu ilitujengea sub-station kubwa pale Mbagala ambayo imekuwa na uwezo wa kuzalisha Megawatts 42 za umeme ambazo zimekwenda sana kunufaisha katika Jimbo la Mbagala. Katika kipindi hiki ambacho tumeanza kutumia sub-station hiyo kwa kweli wananchi wa Jimbo langu la Mbagala walikuwa hawana tatizo lolote la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya kufika mwaka 2020 mahitaji ya Jimbo letu la Mbagala ni Megawatts 32; 2020 ilipofika kwa kuwa Ndugu zetu wa Mkuranga Mkoani Pwani wao hawana sub-station ya umeme, umeme ule ambao unatoka kwenye sub-station ya Mbagala umepelekwa Mkuranga pamoja Lindi. Kitu kilichosababisha Jimbo la Mbagala libaki na Megawatts 8 tu, kitu ambacho kimesababisha sasa tatizo kubwa la umeme katika Jimbo la Mbagala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachofanyika hivi sasa tumekuwa tukipewa umeme kutoka Ilala, Kinyerezi na umeme mwingine ukitoka pale Kurasini. Kwa kuwa umeme huu umekuwa ukitoka sehemu tofauti tofauti; umekuwa na shida kubwa sana ya ukatikaji wa mara kwa mara. Kwa wastani siku moja nilimuonesha Naibu Waziri, kwa siku umeme umekatika zaidi ya mara 45. Sasa tunajiuliza sisi wananchi wa Mbagala tuna tatizo gani? Kama sub-station Serikali yetu imetujengea yenye uwezo wa kuzalisha megawatts 42 uwezo wetu wa kutumia ni Megawatts 32; kwa nini umeme ambao unatokana na sub-station ya Mbagala unapelekwa Mkuranga? Huku ukituacha watu Mbagala tukiwa na masikitiko na malalamiko makubwa ya ukatikaji wa umeme mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliuliza swali la msingi hapa katika Bunge lako hili Tukufu, Mheshimiwa Waziri alinijibu kwamba sub-station ile inakwenda kufungwa transformer ya MVA 50; lakini nimepitia bajeti ya wizara sijaona mahali ambapo imetengwa fedha kwa ajili ya mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe Jimbo la Mbagala ndio jimbo lenye watu wengi katika Nchi hii, na ndio jimbo lilitoa kura nyingi kwa Chama Cha Mapinduzi, sasa niwaombe sana, niwaombe sana, tafuteni utaratibu mwingine wa kuwapa umeme watu wa Mkuranga. Watu wa Jimbo la Mbagala tuendelee kunufaika na sub-station ambayo imejengwa katika Jimbo letu la Mbagala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni mzalendo wa Nchi kwa ujumla, naamini kwamba Mkuranga nao wanahitaji sana suala zima la umeme. Hebu tuangalie namna ya kujenga sub-station Mkuranga ili waweze kujitegemea na sisi Mbagala tuendelee ku-enjoy na matunda ya sub-station ile ambayo imejengwa Mbagala.

Mheshimiwa Spika, wateja wa umeme walioko katika Jimbo la Mbagala ni wateja 75,563. Naamini idadi hii ni kubwa kulinganisha na mikoa mingine ya ki-Tanesco katika Nchi yetu. Idadi ya maunganisho mapya kwa mwezi tuna wastani wa maunganisho 400 kwa kila mwezi. Sasa sielewi kwa nini Tanesco na wizara hii tunashindwa kufanya Mbagala ikawa mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa Mbagala kuwa mkoa, tunakwenda kuondokana na matatizo mengi ukiangalia mita, nguzo na vifaa vingine lazima twende tukapate main store ambayo iko mkoani. Na kulingana na ukubwa wa Mbagala na maunganisho haya mapya ya kila mwezi yanapelekea kunakuwa na ucheleweshaji mkubwa wa kupata huduma hiyo. Wakati nauliza swali Mheshimiwa Waziri alinijibu tuandike maombi; sidhani kama ipo haja ya kuandika maombi. Ninyi wenyewe Tanesco mnaona, ninyi wenyewe wizara mnaona umuhimu wa eneo, hebu niwaombe sana muangalie Wilaya hii ya Mbagala iweze kupata hadhi ya kuwa mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo miradi mbalimbali inaendelea katika jimbo langu la Mbagala. Upo ule mradi wa Malela kule Tuangoma, Yamoto Band kule Mbande, Machimbo pale Azam, Mponda, Yatima n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi hii imekuwa na changamoto kubwa baadhi ya maeneo zinaletwa nguzo kulingana na idadi ya mradi lakini ukifika pale baadhi ya wananchi kwa kutaka umeme walikuwa wameshajiungia umeme kwa kulipa TANESCO na wakaletewa nguzo. Zile nguzo zinazobaki kwenye mradi zinarudi kwanini zirudi wakati bado upo uhitaji wa umeme katika maeneo yale? Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri kama wananchi wamejitahidi kuvuta umeme na mradi umekuja katika eneo lile; basi nguzo zinazobaki ziendelee kufanya extension katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Nimekuwa nikipata changamoto sana katika maeneo ya Kata ya Chamazi, Charambe, Mianzini, Kirungule, Kiburugwa, Mbagala, Mbagala Kuu, Tuangoma, Kijichi, pamoja na kata ya Kibondemaji. Niwaombe sana wizara, niwaombe sana, nguzo zile zinazobaki ziendelee kuhudumia maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lipo tatizo la zile zilizokuwa mita za zamani, wananchi wetu wengi wa Mbagala mnafaham vipato vyao ni vya chini, wengine wameuza majumba yao Kariakoo wamekuja kuhamia Mbagala, nyumba walioyoikuta wameikuta ina mita ya zamani ina deni mpaka milioni 8; leo hii unamtaka mwananchi akinunua umeme wa shilingi 1,000 akatwe nusu ya fedha ile illipe deni la nyuma. Kwa kweli tutakuwa hatuwatendei haki wakazi wetu wa Mbagala. Niiombe sana wizara, iangalie namna bora ya kuweza kumaliza haya madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie, Mbagala bado wanakaa watu wa vipato vya chini Mheshimiwa Waziri; hebu tuangalie namna ambayo watu wa Mbagala si kupata huduma ya umeme wa REA bali wafanye maunganisho kama wanavyounganishwa katika watu wanaopata huduma ya REA. Kwa sababu miundombinu ipo, isipokuwa uwezo wao ni mdogo wa kulipia. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, nafahamu sana utendaji wako wa kazi na kwa sababu lengo letu ni kuongeza mapato katika Shirika letu hili la Umeme la TANESCO basi tutoe namna wananchi wale wanapoweza kuunganishwa umeme kwa kutumia gharama za REA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Nikushukuru sana na niunge mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara yetu hii. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama yetu kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya toka achukue madaraka haya ya Urais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejadili na kupitisha bajeti mbalimbali za Wizara hapa na michango mbalimbali tumechangia. Ni dhahiri bajeti hii ambayo tunataka tuipitishe hapa imetokana na Wabunge wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa maana yale yote ambayo tumeyajadili ndiyo yamekuja kujumuishwa katika bajeti ya Wizara hii ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulizungumza sana suala zima la TARURA iongezewe fedha. Tumeona katika Bajeti ya Wizara ya Fedha kila Jimbo limepewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kwenda kukarabati miundombinu ya barabara. Tumechangia kuhusiana na namna gani ambavyo tunaweza tukaongeza fedha kwa ajili ya kuzipeleka TARURA. Tumetoa michango mbalimbali, wapo waliogusia kuhusiana na ongezeko la fedha katika mafuta, wapo waliochangia katika miundombinu ya mawasiliano na bajeti iliyosomwa na Waziri wa Fedha, vyote hivyo vimejumuishwa. Tafsiri yangu ni kwamba bajeti hii iliyoletwa hapa imezingatia michango ya Waheshimiwa Wabunge wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maneno mengine bajeti hii ni bajeti yetu, ninachotaka kusema tunazo kazi za kufanya, zipo kazi kwanza kwa sisi Wabunge, kwa sababu yaliyoletwa ndiyo tuliyoyataka, kazi yetu ya kwanza kama Wabunge tunatakiwa twende tukawaelimishe wananchi wetu, twende tukawaelimishe wananchi wetu ili bajeti hii iweze kutekelezeka. Ipo sheria ile ya property tax, ambayo ni wajibu wa kila mwenye jengo kuilipia kodi ya majengo, tumekuwa zamani huko tukikusanya kwa kupitia halmashauri zetu, tukaenda TRA, lakini ufanisi ukawa mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tumekuja na mbinu mbadala ya kukusanya kupitia mita za LUKU. Tutakapoenda kuwaelimisha wananchi wetu, nini kinachoenda kutendeka hatutapata tabu kwenye ukusanyaji wa hizi fedha za property tax. Madhalani mwenye nyumba anayepangisha nyumba kwa mwezi shilingi 300,000/= tukiweka utaratibu mwananchi akajua kwamba kwenye 300,000/= hii kwa kila mwezi 1,000 ni kodi ya majengo, kwa hiyo, ni rahisi unaenda kulipa 299,000/= (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, ni kama vile kwenye majumba haya yaliyopangishwa yapo mashimo ambayo yanabeba maji taka, maji taka yale ni jukumu la mwenye nyumba kuyanyonya pale yanapojaa. Sasa kwenye mikataba ni namna ya kukubaliana tu. Aidha, kwenye kodi yangu utakata kiasi kadhaa ili shimo likijaa uwezekunyonya au nipe kodi yangu shimo likijaa nitakuja kunyonya, kwa hiyo, kubwa hapa kinachoitajika ni elimu kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa bajeti hii sisi ndiyo tumechangia kwa kiasi kikubwa mpaka hapa tulipofikia, ninaamini bajeti hii pia ni yawananchi, kwa sababu Wabunge tuliochangia hapa tumewawakilisha wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije sasa upande wa pili kwa Mawaziri, tunaenda kuwahamasisha wananchi wetu ili waweze kulipa kodi, boda boda wapunguze makosa na mambo mengine, lakini pale fedha zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo tuwaombe sasa na ninyi Mawaziri mchukue wajibu wenu kupeleka fedha hizi katika hii miradi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ile miradi michango yetu na elimu yetu tunayoenda kuitoa kwa wananchi tutawaambia, gharama hizi za simu zinaenda kupelekea tupate fedha kwa ajili ya kukarabati barabara, kwa ajili ya kumalizia miradi mikubwa ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninyi mawaziri msipopeleka fedha katika hiyo miradi maana yake sasa pamoja na elimu tuliyoitoa kwa wananchi mnaenda kutupalia makaa kwa wananchi wale, kwa hiyo upande wa mawaziri kwa maana ya Serikali na ninyi tunawaomba mtimize wajibu wenu kuhakikisha miradi ile yote iliyotengewa fedha inaenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe ushauri mambo machache katika masuala mazima ya barabara hasa barabara zile zinazomilikiwa na TARURA. Huko nyuma halmshauri nyingi hasa zile za Dar es Salaam zilikua zinatenga fedha kwa ajili ya barabara zaidi ya bilioni 4 nakumbuka halmashauri ya jiji la Ilala na Temeke zilishawahi kutenga katika miaka mbalimbali. Hebu sasa tuangalie Serikali kama halmashauri hizi huko nyuma zilikuwa zinauweozo wa kutenga hizo fedha hebu angalieni Serikali namna ya kuzikopesha halmashauri hizi fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano; halmashauri ya Temeke Ilala na hizi nyinginezo zikakopeshwa labda bilioni 20 kila moja kwa ajili ya kwenda kukarabati barabara, halafu kila mwaka mkawahambia muwe mnalipa labda bilioni tatu tatu, naamini baada ya miaka mitano barabara zitakuwa zimetengenezwa na fedha zitakuwa zimerudi katika mfuko mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ulizungumza katika hotuba yako kwamba majadiliano yanaendelea kuhusiana na mradi huu wa DNDP, kwa Dar es Salaam mradi wa DMDP ni muhimu kweli kweli. Tunaomba sana muharakishe mazungumzo katika mradi huo wa DMDP. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho posho la wenyeviti wa Mitaa na madiwani, Mheshimiwa Waziri umezungumza halmashauri zile 16 zitaendelea kulipa kwa mapato yake ya ndani. Sisi tuwaombe sana Dar es Salaam tuna mizigo mikubwa sana na sisi Dar es Salaam mchukue gharama hizi Serikali Kuu muweze kulipa ili fedha hizi sasa ambazo wamekua wakilipwa sasa hivi madiwani ziende zikalipe wenyeviti wetu wa Serikali za Mitaa ambao kiukweli wamekuwa na hali mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kumpongeza Waziri wetu wa TAMISEMI, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu ameonyesha kwa kiasi kikubwa ushirikiano mkubwa na Waheshimiwa Wabunge. Kila Mbunge hapa ameandikiwa barua na Mheshimiwa barua na Mheshimiwa Waziri aeleze vipaumbele vyake katika ujenzi wa shule za Sekondari, Wabunge wote tumeandika na zimemfikia waziri naamini ile migongano ya kugombania Sekondari ikajengwe wapi itakuwa imekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe na mawaziri mwingine wote tuunge sasa juhudi alizozifanya Waziri wetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu na sisi kwa kufanya hivyo naamini mambo mbalimbali yataenda kubadilika katika halmashauri zetu, barabara zitajengwa, mashule yatajengwa, zahanati zitajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii tena ili kuweza kujumuisha yale yote ambayo yamechangiwa na Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kamati yetu tumepata wachangiaji 13. Kwa haraka haraka naomba niwataje, Mheshimiwa Londo, Mheshimiwa Shangazi, Mheshimiwa Sanga, Mheshimiwa Migilla, Mheshimiwa Jacqueline, Mheshimiwa Mwakamo, Mheshimiwa Tunza, Mheshimiwa Saasisha, Mheshimiwa Mwanaisha Ulenge, Mheshimiwa Kanyasu, Mheshimiwa Dkt. Alice na Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Wabunge wote waliochangia katika Kamati hii, michango yao inaendelea kutuimarisha sisi kama Kamati ili kuweza kuisimamia na kuishauri Serikali katika mambo kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika michango yote yapo mambo muhimu ambayo Waheshimiwa Wabunge waliyagusia na walitoa msisitizo na sisi kama Kamati tunaendelea kutoa msisitizo kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zile za asilimia 10 endapo Serikali itazisimamia vizuri zitaweza kuondoa umaskini katika nchi yetu. Ukifuatilia takwimu, zaidi ya bilioni 70 zinatolewa kila mwaka kwa kuwakopesha vijana, kina mama na watu wenye ulemavu. Fedha hizi zikitungiwa sheria na kanuni madhubuti pamoja na mifumo thabiti ya kudhibiti vikundi visiweze kukopa kiholela, vikundi viweze kurudisha, nina hakika fedha hizi zitamkomboa Mtanzania kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge pia walizungumzia sana kuhusu fedha za maendeleo. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri wangu hapa, ameelezea namna ambavyo atatuletea kwenye Kamati. Kiukweli kama Kamati tumeona ipo haja ya fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ziende zikatekeleze miradi ya maendeleo. Takwimu zinaonesha kwamba bado kuna upungufu mkubwa wa madarasa kwa wanafunzi ambao watamaliza darasa la saba mwaka huu. Sasa fedha zile tutakapoamua kuzibadilishia matumizi, tukazipeleka kwenye matumizi mengine ambayo si ya miundombinu ya elimu na wala si ya miundombinu ya afya; tatizo hili tutaendelea kuwa nalo. Hivyo basi, kama Kamati tunaendelea kusisitiza kwamba, fedha hizi ziendelee kutumika katika miradi ya maendeleo hasa miundombinu ya elimu na miundombinu ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamezungumzia sana suala la Walimu wastaafu, Walimu waliofariki na kada nyingine mbalimbali zilizostaafu na kufariki. Kamati tutaendelea kusisitiza, nafasi hizi za watu ambao wamestaafu na kufariki ziweze kujazwa mara moja. Kwa maana nafasi hizi zikijazwa tunaendelea kuondoa upungufu mkubwa wa Walimu na kada mbalimbali ambazo zinatokana na mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa sana suala la majanga ya moto. Tumeona, majanga ya moto yamekuwa kizungumkuti sana nchini kwetu, hasa katika maeneo ya masoko. Kamati itaendelea kusimamia na kuishauri Serikali namna bora ya kufanya ili majanga haya ya moto yasiendelee kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifuatilia majanga haya ya moto utaona kila mahali ambapo moto umetokea tunaambiwa chanzo ni umeme. Tunajiuliza, je umeme huu unatoa hitilafu usiku tu na mchana unakuwa haupo? Sasa, ni moja ya majukumu ya Kamati hii kuona ni namna gani tutaendelea kufuatilia na kuikomesha hali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la mifumo mbalimbali, hivyo basi Mamlaka yetu ya Serikali Mtandao (eGA) tutaendelea kuisimamia na kuhakikisha maeneo yote ambayo mitandao ya kielektroniki inatakiwa iwekwe, basi eGA ishiriki katika kuweka mitandao hiyo ili kuepusha mitandao isiendelee kutosomana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yangu ina mambo mengi na kwa sababu ya muda, naomba sasa Bunge lako lipokee taarifa hii na mapendekezo yote yaliyotolewa na Kamati hii ili iweze kutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia, lakini leo mchango wangu utaongozwa sana na maneno ya dini. Mtume wetu Muhammad Swalallahu Allah Wasalaam amesema; “Lamiyashukurillaha Mallam yashukurunasi” hatopatikana mtu atakayemshukuru Mungu wakati hataki kuwashukuru watu. Lakini vilevile, kwenye Zaburi 138:1 inasema; “Nitashukuru kwa moyo wangu wote na mbele ya Mungu nitakuimbia Zaburi”. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeanza na maneno haya ya dini kwa maana, ni vyema tumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya. Mwaka jana wakati kama huu nilizungumza sana kuhusiana na vilio mbalimbali katika sekta ya elimu, afya na barabara katika Jimbo langu la Mbagala. Lakini hapa ninapozungumza matatizo mengi yameenda kutatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano katika elimu msingi, shule tatu mpya zimejengwa katika Jimbo la Mbagala, yYamejengwa madarasa katika shule zilizopo zaidi ya madarasa 50, kwenye sekondari fedha za UVIKO nimepata madarasa 87, lakini mapato ya ndani tumejenga shule mpya mbili za sekondari na vilevile fedha zilizoletwa katika shule maalum nimeletewa fedha kwa ajili ya kujenga shule katika kata zisizokuwa na sekodnari. Sasa naogopa nisije nikaendelea kumshukuru Mungu bila kuwashukuru watu hawa ambao wamewezesha mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye afya; sasa hivi hapa ninapozungumza kule Mbagala umeme ukikatika ukirudi tunasema huooo, sasa hivi kule Mbagala kila dakika tunasema hizooo fedha za Rais. Sasa hivi hapa wananchi wangu wananiambia hizooo shilingi bilioni mbili za kujenga Hospitali ya Wilaya zimeingia jana. Wananchi wa Mbagala wana kila namna ya kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa maana jana peke yake tumepata shilingi bilioni mbili za kujenga Hospitali ya Wilaya pale Mbagala Zakhiem ambayo ilikuwa ina msongamano mkubwa sana na mwaka jana nililizungumza hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vituo vya afya; ndani ya Jimbo langu kwa mwaka huu mmoja vituo vitatu vya afya vinajengwa ambavyo vina thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1.5; zahanati kila kata sasa hivi tunakwenda kuwa na zahanati ambayo tunakoelekea sasa, tunaelekea kwa kila Mtaa nina kila sababu ya kuendelea kumshukuru Rais wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Nabu Spika, kuhusu barabara za TARURA tumepata fedha nyingi za kutengeneza barabara zetu za TARURA. Lakini ombi ambalo limebaki kwa wananchi wa Jimbo la Mbagala upande wa TARURA na Serikali kwa ujumla, tunao ule mradi wa uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam awamu ya pili. Tunaiomba sana Serikali kilio chetu kikubwa sasa hivi Dar es Salaam hasa Temeke na Jimbo langu la Mbagala katika Kata za Chamazi, Charambe, Mianzini, Kiburugwa, Kibondemaji, Kilungule, Mbagala Kuu, Kijichi, Mbagala pamoja na Toangoma tatizo letu kubwa sasa hivi ni barabara. (Makofi)

Kwa hiyo, niombe sana ule mradi unaotokana na uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam awamu ya pili, uharakishwe ili matatizo ya watu wa Mbagala yaende kuwa historia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie utekelezaji wa miradi hii yote ambayo Mheshimiwa Rais ameileta. Niwashukuru sana kuanzia Wenyeviti wa Mitaa, Waheshimiwa Madiwani, Watendaji wa Halmashauri, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa. Kazi nzuri wameifanya katika kusimamia miradi hii na ndio maana leo hii tunasimama kifua mbele kusifia miradi imefanyika vizuri.

Sasa hapa ombi langu Wenyeviti wa Mitaa wanafanya kazi kubwa na nzuri sana, sasa hivi kila jambo unalolitaka, lazima upige simu kwa Diwani au Mwenyekiti wa Mtaa akuelezee uhalisia wa maeneo hayo. Nitakupa mfano wakati tunapata fedha za kujenga vituo vya afya kwa haraka haraka ilionekana maeneo ya kujenga hakuna, lakini tulipowapigia simu Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa wametuonesha maeneo mengi ambayo yametengwa na Serikali kwa ajili ya huduma za jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuone tayari ni namna gani watu hawa walivyokuwa muhimu, lakini tuangalie na maslahi ambayo wanayapata. Nikuombe sana Wenyeviti hawa wa Serikali za Mitaa tutengeneze mazingira mazuri ya kuweza kupata maslahi yao hasa posho. Ninaamini Mheshimiwa Waziri hapa anasikia na anaweza akatoa maelekezo huko baadaye, kuhakikisha Wenyeviti hawa wa Mitaa walau tunawaongezea morale ya kufanya kazi. Anuani za makazi hizi tunazozishughulikia sasa hivi ambao wako mstari wa mbele ni Wenyeviti wa Mitaa pamoja na Madiwani. Sasa niombe sana Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vijiji nao waone namna ambayo tunaweza tukawaongeza maslahi yao ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa Madiwani; mimi nilikuwa Diwani, ili tuwe na Madiwani wazuri ni lazima pia tuangalie maslahi yao. Tumeanza Udiwani tukiwa tunalipwa shilingi 120,000 lakini sasa hivi imefika shilingi 350,000; ndugu zangu kutokana na hali halisi ya maisha ya sasa hivi bado ni fedha ndogo sana. Tuwaombee Madiwani hawa waongezewe fedha ili nao waweze kusimamia vizuri miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa NaibU Spika, nimalizie, tuna suala zima la kujifunza Madiwani, tuombe TAMISEMI ielekeze Mikoa, Madiwani pale ambapo Halmashauri zao zina fursa za kutosha wapewe nafasi ya kwenda kujifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi hapa Dodoma inatengenezwa open market kwa ajili ya wamachinga. Kule Dar es Salaam tuna tatizo kubwa sana la wamachinga, ni wakati muafaka sasa Madiwani wa maeneo tofauti tofauti, wakaenda maeneo mbalimbali kujifunza ili mradi waone namna wenzao wanavyofanikisha mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini hili Mheshimiwa Waziri atalitolea maelezo ili mradi tu kama fedha wametenga kwenye bajeti zao na fedha wanazo, sioni kwa nini wawe na vikwazo vya kupewa ruhusa ya kwenda kujifunza katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kwa kunipa nafasi ya kuchangia taarifa za Kamati hizi mbili. Mimi nitajikita zaidi katika Kamati hii ya Miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nizipongeze Kamati zote hizi mbili kwa sababu mwaka huu wametuletea kwa namna gani kwenye Kamati zao yale maazimio ya Bunge yaliyopitishwa wakati kama huu yametekelezwa. Kwa hiyo, niwapongeze sana Kamati zote mbili na naamini kamati nyingine zote zitakuja na utaratibu huu.

Mheshimiwa Spika, tukianza na mapendekezo ya Kamati ya Miundombinu kwenye ukurasa ule wa 25 kwenye maoni yao ya jumla wamezungumzia sana katika suala zima la ulipaji wa fidia. Ni dhahiri tumeona hapa bajeti zinapitishwa za ujenzi wa barabara mbalimbali, lakini bila kuangalia kwamba barabara hizo zinahitaji kulipiwa fidia bila kujengwa. Matokeo yake ni nini? Matokeo yake utekelezaji wa mradi ule, Mheshimiwa Mbunge anatoka hapa anakwenda kueleza kwenye jimbo lake kwamba barabara fulani itajengwa katika bajeti ya mwaka huu, lakini kumbe ili barabara ile ijengwe ni lazima ilipiwe fidia.

Kwa hiyo niwapongeze sana Kamati hii ya Miundombinu kwa kuona suala la ulipaji wa fidia kwa wananchi lipewe nafasi kubwa na Serikali itenge fedha ili sasa miradi yetu ambayo tutaisimamia bajeti iweze kuwekwa iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, zipo barabara kadhaa ambazo zimeathirika katika kutokulipiwa fidia, lakini fedha za ujenzi wa barabara zimewekwa. Ile barabara ya Mbagala Rangi Tatu mpaka Mwandege inahusika na tatizo hili na wananchi wamekuwa wakisota sana kuhakikisha wanalipwa fidia ili kupisha ujenzi wa barabara. Kwa hiyo, niendelee niiombe Serikali wazingatie mapendekezo ya Kamati hii ya Miundombinu katika suala zima la ulipaji wa fidia.

Mheshimiwa Spika, katika taarifa ya Kamati wameelezea namna ambavyo mradi wa mwendokasi umeweza kufanya kazi pale katika Jiji la Dar es Salaam. Katika taarifa wamesema ukurasa wa 10, Serikali ione namna ya kutatua changamoto za mradi huu. Mradi huu wa mwendokasi pale Dar es Salaam umekuwa na changamoto kubwa, ukisoma ndani ya taarifa unaona changamoto ambazo zipo katika mradi ule.

Mheshimiwa Spika, moja ya changamoto, baada ya miundombinu ya mradi ule kujengwa hasa katika eneo la Mbagala limeenda kuzua taharuki kubwa sana kwa wananchi. Mimi ushauri wangu pamoja na ushauri huu wa Kamati, niiombe Serikali inapoanzisha miradi hii mikubwa iwasiliane na mamlaka zote mbili zinazohusiana na ujenzi wa barabara. Kwa mfano TANROADS wanapojenga barabara kubwa, wakijenga na mifereji maeneo ya kuelekezea maji ya katika mifereji wanawategemea TARURA waweze kuyafikisha katika maeneo maji yanapotaka kufika.

Mheshimiwa Spika, lakini utakuta TANROADS wanafanya kivingine na TARURA nao wanafanaya kivingine, mwisho kinachotokea sasa TANROADS wanafanya kazi nzuri ya kujenga barabara, lakini mwisho wa siku sasa uwezo wa TARURA wa kuweza kuyachukua yale maji ambayo yamekusanywa na TANROADS unakuwa ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwaombe sana Serikali wakati wa kujenga barabara hizi kwenye majiji yetu basi wawasiliane na hizi mamlaka mbili zinazohusiana na ujenzi wa barabara. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, la mwisho, naona kengele inagonga na muda unaisha niiombe sasa Serikali maazimio yote yaliyotelewa katika Kamati hii ni maazimio ya msingi sana. Niombe iende ikayatekeleze ili sasa tija kwa wananchi iweze kuwa na umuhimu mkubwa sana, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuhitimisha hoja hii.

Mheshimiwa Spika, pili, nitoe shukurani za dhati kwa Wabunge wote ambao wamechangia katika taarifa yetu hii ya Kamati, tumepata michango ya zaidi ya Wabunge 13 na Mawaziri Watatu ambao kiukweli katika michango yote wameelezea na wameunga mkono mapendekezo yaliyotolewa na Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika michango iliyotolewa na Wabunge hawa, ambao walimekuwa makini katika michango yao, hoja nyingi zinaenda kumgusa mwananchi wa kawaida ambaye yeye ndiye mwananchi namba moja katika nchi hii. Hoja nyingi zimezungumzwa hapa lakini zipo hoja mahsusi tatu ambazo zimezungumzwa na Wabunge walio wengi.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza ilitokana na TARURA kuhusiana na fedha za dharura na ujenzi wa barabara. Tunapozungumza fedha za dharura maana yake tunajiandaa endapo tatizo litatokea tuweze kutatua tatizo hilo. Tumefuatilia fedha hizi zinazoombwa za dharura zinaenda kutengeneza barabara ambazo zimekuwa zikitengewa fedha kila mwaka na TARURA.

Mheshimiwa Spika, sasa tunatakiwa tujiulize hapa, TARURA kila mwaka tunatenga fedha lakini barabara hizo zikijengwa baada ya muda fulani zinaharibika. Yawezekana katika ujenzi wa barabara hizo vipo vitu vya kitaalam vinakuwa havikidhi vigezo. Moja ya jambo ambalo limeonekana sana, huwezi kujenga barabara usipoweka mifereji. Kwa sababu barabara nyingi zinajengwa bila ya mifereji matokeo yake inapofika wakati wa mvua barabara zile zinaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa napitisha dodoso kwa baadhi ya Wabunge kuwaambia wanitajie barabara moja ambayo ndani ya miaka mitano imetengewa fedha kiasi gani za spot improvement, periodic maintenance na matengenezo mengine. Nilivyojumlisha katika zile barabara nimeona kama fedha zile zote zingejumlishwa kwa pamoja basi barabara ile kwa mwaka mmoja ingejengwa kwa kiwango kikubwa na hatimae tungeondokana na hii kadhia ya kuomba fedha za dharura kwa ajili ya matengenezo ya barabara.

Mheshimiwa Spika, suala la barabara limechukua mjadala mpana sana katika Bunge letu leo kwa maana kila Mbunge aliyezungumza na wengine waliochangia kwa maandishi wamekuwa na kero kubwa ya barabara. Kutokana na hayo, nimepokea nyongeza ya maazimio katika suala hili la TARURA, kwa sababu ulitoa maelekezo toka jana, naomba kwa idhini yako sasa nilisome. Azimio hilo linasema kama ifuatavyo: -

Kwa kuwa, Serikali imetoa mwongozo kwa Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 za fedha za mapato ya ndani katika ujenzi wa miundombinu ya barabara;

Na kwa kuwa, Halmashauri nyingi hazitekelezi mwongozo huo,

Hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kuandaa sheria ya utengaji wa asilimia 10 ya mapato ya ndani katika ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Spika, tunakumbuka huko nyuma Serikali ilitoa mwongozo wa utengaji wa asilimia 10 lakini kwa sababu ulikuwa siyo wa kisheria basi watu walikuwa wanafanya kadiri watakavyo na baada ya kuufanya wa kisheria, Halmashauri nyingi zimekuwa zikitekeleza. Kwa hiyo naomba na hili nalo liwe katika sehemu ya azimio.

Mheshimiwa Spika, nasema hili sababu ukichukua baadhi ya Halmashauri hasa za Dar es Salaam, kwa mfano Halmashauri ya Ilala kwa mwaka inatenga Shilingi Bilioni 6.2 kwa ajili ya matengenezo ya barabara kwa ajili ya zile asilimia 10. Sasa fedha hizi zikitumika vizuri kila mwaka tunazungumzia kilometa takribani 10 za lami nyepesi. Kwa maana hiyo, ndani ya miaka mitano tutakuwa tumetengeneza takriban kilometa 50 za lami nyepesi.

Mheshimiwa Spika, suala jingine ambalo limechukua nafasi kubwa katika mjadala wetu ni mgogoro wa ardhi katika Jiji la Dodoma. Ni wakati sasa Serikali ilichukulie jambo hili very serious. Wananchi wengi katika Jiji la Dodoma na Halmashauri nyingine nchini wamekuwa wakilalamikia masuala haya ardhi. Ukienda pale Kawe, kule Nyakasangwe, sijui wapi, kuna migogoro mikubwa ya ardhi. Kwa hiyo, Serikali sasa tutayarishe mpango maalum wa kwenda kutatua hii migogoro ya ardhi. Migogoro hii mara nyingi inawahusu wananchi wanyonge. Kwa hiyo tunapowaonea wananchi wanyonge tafsiri yake wananchi walio wengi wanaenda kupata uonevu mkubwa katika maeneo yetu. Kwa hiyo ninaomba na kusisitiza sana, migogoro ya ardhi ichukuliwe hatua stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala jingine ambalo limechukua nafasi kubwa ni miradi ya TACTIC, kuna mradi mwingine wa RISE na mradi wa uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam yaani DMDP. Ninaiomba sana Serikali miradi hii Wabunge wengi wanaitegemea, tuangalie uwezekano mkubwa wa kila maeneo yenye mahitaji basi miradi hii ifanyike na hatimae sasa tuweze kuondoa tatizo kubwa la miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, suala zima la TAKUKURU rafiki. Tunazungumzia habari za fedha nyingi za maendeleo katika maeneo yetu lakini Wabunge tusipopata uelewa mzuri wa TAKUKURU rafiki, fedha hizi zinaenda kupotea. TAKUKURU rafiki inamuhusisha moja kwa moja mwananchi wa kawaida wa pale kijijini kwenda kujua fedha zilizoletwa na namna gani atakayezisimamia zile fedha ili ziweze kutekeleza ule mradi kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni rai yangu, Serikali sasa ione namna bora ya Wabunge hawa kuwapa uelewa mkubwa wa dhana nzima ya TAKUKURU rafiki ili na wao waende kutoa maelezo hayo kwa wananchi hawa. Ukisoma ile sheria ya 288 ya uanzishwaji wa Serikali za Mitaa utaona kazi ya Mtendaji wa Kata ni kumsaidia Mkurugenzi katika utekelezaji wa majukumu yake. TAKUKURU rafiki wakielekezwa hawa Watendaji wa Kata na Mitaa wataenda kuisaidia halmashauri, wataenda kuisaidia mapato ya Serikali kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezeka.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo sasa naomba kutoa hoja kwamba mapendekezo yote ya Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa yakubaliwe na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SEBASTIAN H. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya TAMISEMI, lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Wasaidizi wake, Naibu Mawaziri Waziri wawili pamoja na wetendaji katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi alizozileta katika jimbo la Mbagala. Elimu msingi tuna bilioni nne, tumejenga madarasa 142 na shule mpya za msingi nne. Elimu Sekondari tumejenga Shule mpya tatu, tumejenga madarasa 165 na jumla ya fedha zilizo letwa katika elimu sekondari ni bilioni 5.6. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya tumeletewa bilioni mbili kwa ajili ya kujenga hospitali ya Wilaya pale ya Zakem ambayo nimeipigia kelele muda mrefu sana. Tumepewa vituo vitatu vya afya na zahanati mbalimbali zimejengwa katika Jimbo langu la Mbagala. Kwa dhati yangu ya moyo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri na fedha alizozileta katika jimbo la Mbagala. Niwashukuru pia Mawaziri ambao wamesimamia na kutekeleza pamoja na viongozi wangu wa ngazi ya Wilaya, Mkurugenzi pamoja na Mkuu Wa Wilaya na Madiwani kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Sekta ya barabara tumeletewa bilioni 24, imetekeleza barabara mbalimbali katika jimbo langu la Mbagala. Ni jimbo ambalo lilikuwa halina miundombinu kabisa ya barabara; tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo mchango wangu nataka nijikite katika suala zima la barabara. Serikali inatuletea mradi wa uboreshaji wa barabara katika jiji la Dar es Salaam, awamu ile ya pili na ya tatu. Mheshimiwa Waziri ametuahidi mpaka mwezi wa nane mradi huo utaanza, lakini sisi watu wa pwani tunasema dalili ya mvua ni mawingu. Tunatarajia mvua itanyesha kwa maana ya ujenzi uanze mwezi wa nane lakini mawingu hatuyaoni. Barabara hizi sehemu zote zinapokwenda kupita zinahitaji zilipiwe fidia. Hatujaona mpango wowote kwenye bajate iliyotengwa wala kutoka Serikali Kuu, kwa maana ya Wizara ya Fedha, kwa ajili ya kulipia fidia katika maeneo yatakayo pisha ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti,tumuombe Mheshimiwa Waziri akija hapa atupe ufafanuzi, kama fidia hizi zitalipwa na halmashauri basi ni vyema halmashauri zikaambiwa mapema ili na tuweze kujipanga ni namna gani ambavyo tutalipa fidia; kuliko fedha zimekuja mradi unatakiwa uanze lakini fedha za kulipa fidia zinakuwa vikwazo vya utekelezaji wa miradi ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, miundombinu ya barabara katika Mkoa mzima wa Dar es Salaam ni tatizo; na hasa katika jimbo langu la Mbagala. Pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Mheshimiwa Rais ya kutuletea fedha za kujenga barabara lakini ni lazima sasa tuone Wizara kupitia TARURA wanatutengea fedha za kutosha kujengea barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupunguza msongamano katika Jimbo la Mbagala ni lazima barabara za kuunganisha kati ya Wilaya na Wilaya zijengwe; ni lazima barabara za kuunganisha kati ya jimbo na jimbo zijengwe; ni lazima barabara za kuunganisha kati ya kata na kata zijengwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaotokea kusini wanajua pale kuanzia Kokoto mpaka Kongowe kunakua na foleni, ni kilometa mbili, lakini kama Madaraja yanayounganisha Mkuranga na Mbagala yakijengwa msongamano ule unaenda kuwa historia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kuna lile Daraja la Kidete ambalo liko katika Mtaa wa Bamia litaunganisha eneo la Kidete-Mkuranga pamoja na eneo la Mbagala. Kuna lile Daraja la Mbanga Kwalu ambalo liko katika mtaa wa Bamia, likijengwa linaenda kuunganisha Mbanga Kwalu, Mkuranga pamoja na Jimbo la Mbagala. Pia tunalo lile daraja la Churwi ambalo liko Kata ya Mianzini na Kata ya Chamanzi likijengwa linaenda kuunganisha jimbo la Mbagala pamoja na Mkuranga. Kwa kufanya hivi tunaenda kuondoa msongamano wa barabara ile ya Kilwa road.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunataka tujenge barababara ni lazima tuzingatie barabara zipi zinaenda kuondoa msongamano wa foleni katika barabara zetu. Tunazo barabara ambazo zinaunganisha kata kwa kata. Kwa mfano barabara ya Habari Zako hii inaunganisha kata ya Chamazi pamoja na kata ya Mianzini. Tunazo Barabara za Mabwawa ya Samaki, Kona Tope, Maandazi Road, Stanley, kwa Ndunguru na Kwamakuka. Majina haya yanatokana na asili ya Kizaramo ambao ndio wanaishi sana maeneo yale; na ndiyo maana wananchi wa Mbagala miaka hii mitano wamenikabidhi mimi mtoto wao kwa kuwa wanajua nazifahamu kwa majina barabara hizi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti,nakushukuru sana naunga mkono hoja.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nikipongeze Chama changu cha Mapinduzi ambacho kwa kweli wametuandalia Ilani hii ya Uchaguzi ambayo ukiisoma inaenda kuondoa kero kubwa za wananchi wetu. Kwangu mimi Ilani hii ni mkataba kati ya Chama cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Mbagala. Ndiyo maana wakati wa uchaguzi wananchi wa Jimbo la Mbagala walikipa kura nyingi Chama cha Mapinduzi kwa maana waliisoma Ilani hii na wakailewa vizuri. Kwa hiyo, niwashukuru wale wote walioandaa Ilani hii ya Uchaguzi wakiongozwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wetu Dkt. Bashiru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiisoma hii Ilani ya Uchaguzi kwenye ukurasa wa 78 kipengele cha (e) wamezungumzia kuhusu kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam. Vipo vitu vingi vimeorodheshwa huku ambavyo vinaelekea kupunguza msongamano katika Jiji la Dar es Salaam, lakini katika jimbo langu la Mbagala, ukienda katika kipengele cha tatu kimezungumzia upanuzi wa barabara wa Mbagala - Kongowe - Mwandege, kilometa nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanini Chama cha Mapinduzi wameleta Ilani na ameelezea barabara hii? Barabara hii ni kiungo muhimu. Ukiangalia watu wanaotoka Kigamboni, Tuangoma ni lazima wapite katika kipande hiki cha barabara. Pia watu wote wanaotoka kusini, ukianzia Lindi, Mtwara, Songea, Mkuranga na Rufiji, wakitaka kuingia Dar es Salaam, lango lao la kuingilia ni kipande hiki cha barabara kilichozungumzwa. Kwa hiyo, Chama cha Mapinduzi kimeweka hili wakijua wanaenda kuokoa na kupunguza msongamano katika Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ukishafika pale Rangitatu, kwa wale wanaotakiwa kwenda Mbande mpaka Airport wanafika. Kwa hiyo, kipande hiki kidogo cha barabara kikijengwa, kinaenda kupunguza msongamano wa magari katika ya Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote mtakuwa mashahidi, kaeneo hako ka kilometa nne kanasababisha msongamano wa magari, kukapita hako ni zaidi ya masaa matatu ili lipitike eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, namshukuru Rais wangu pamoja na Serikali yake, wameliona hili na wamezingatia Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi. Ukienda katika hotuba ya Waziri, ukifungua randama katika ukurasa wa 134 kiambatanisho cha tatu wamezungumzia pale kuhusu upanuzi wa barabara Rangitatu - Kongowe mpaka Mwandege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile barabara hii kama nilivyosema huko mwanzo, ukurasa huo huo wamesema upanuzi wa Barabara ya Chanika mpaka Mbande. Vile vile ukurasa huo wamezungumzia upgrading ya barabara ya Mbagala Mission - Kijichi na Zakhem. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme nini Rais wetu, Mama Samia amezingatia Ilani ya uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi na ameitafsiri kwa vitendo kwa kutuletea bajeti hii hapa. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi iliyobaki sasa ni kwa Watendaji wa Wizara na Mawaziri. Sasa kama kweli tuna nia ya dhati ya kumsaidia Rais; ambaye ametokana na Chama cha Mapinduzi, ambapo kwenye Ilani yake wameelezea; Rais ametuletea bajeti na ameiweka katika randama ya Mheshimiwa Waziri. Sasa watendaji kazi yenu kubwa iliyobaki sasa ni kwenda kutekeleza kwa vitendo barabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hizi ili zitekelezwe inahitajika ifanyike fidia kipande cha kutoka Kokoto - Kongowe mpaka Mwandege. Wananchi wale zaidi ya 3,000 wamekuwa wakisubiria fidia zaidi ya miaka mitatu sasa na kila nikiuliza swali hapa Bungeni Waziri anajibu, barabara itajengwa baada ya fidia kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu, leo tunapitisha bajeti, Chama cha Mapinduzi wameandika kwenye Ilani kupunguza msongamano. Rais, mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametuwekea kwenye bajeti tunapitisha, bado hatujaona fedha za kufanya fidia za hizo barabara. Sasa nataka nimwone Waziri hapa anatuletea majibu, wananchi hawa ambao wameteseka kwa zaidi ya mitatu kusubiri fidia, ni lini wanafidiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kipande cha barabara sasa kutoka Mbande mpaka Msongola kipande kile kimebaki kilometa nne tu. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, watumalizie kile kipande, ndiyo tunaenda kuondoa ile dhana ya msongamano katikati ya Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna kipande cha barabara ambacho huku mmekiandika kutoka Kijichi - Mission mpaka kuja Zakhem. Mheshimiwa Waziri kipande hiki mmeandika, lakini tunataka tujue hapa mkituletea taarifa mwisho wakati mnajumuisha, pale chini kuna bomba la TAZAMA. Lile bomba la TAZAMA tunatatuaje ile changamoto ili tuweze kujenga ile barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na mradi wa mabasi yaendayo kazi Dar es Salaam (DART). Mheshimiwa Waziri atakuwa shahidi, alifanya ziara katika jimbo langu, wananchi wa Mbagala katika eneo ambalo limepita mradi, barabara imejengwa na maji yote sasa yanaeleke kwa wananchi. namwomba sana Mheshimiwa Waziri atuletee majibu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kutoa mchango wangu katika Bajeti kuu ya Serikali ya mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, kwa niaba ya wapiga kura wangu wa Jimbo la Mbagala, naomba sana nikishukuru chama changu cha Mapinduzi kwa kuandaa ilani ya uchaguzi ambayo inaenda kutatua shida za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi kwa maana kwa asilimia kubwa yale yote ambayo yameahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi tumeona yameletwa kwenye bajeti zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa zimefanyika katika majimbo yetu. Tumeona mambo ya elimu, afya, barabara, maji na umeme. Kila Mbunge hapa ameona vitu vilivyofanywa. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuendelea kumshukuru kwa kazi hiyo aliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukushukuru wewe, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote mliotuongoza katika Bunge hili. Kwa maana mlitupa nafasi za kutosha katika Wizara mbalimbali tumechangia, tumeonesha mbwembwe za hali ya juu katika kudai miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nawashukuru Mawaziri wote, yale ambayo tulikuwa tukiyaomba mmeendelea kuyaweka katika ilani, na katika bajeti kuu za Serikali. Kwa maana hiyo tunatarajia mambo tuliyoyaomba yanaenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi iliyobaki sasa ni kwetu sisi Wabunge kuona namna ambavyo tutaisaidia Serikali namna bora ya kuweza kukusanya fedha ili fedha zile sasa ziende kutekeleza miradi ambayo tumeiomba hapa kwenye Bunge letu. Miradi mingi imeandikwa katika vitabu, lakini ili itekelezwe lazima zipatikane fedha za kwenda kuitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mchango wangu nataka niutoe katika Wizara ya Ardhi na namna gani Wizara ya Ardhi itaenda kuongeza pato katika Serikali. Ukisoma kitabu cha bajeti cha Waziri wa Ardhi ukurasa wa nane, kimeelezea, kulikuwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni 221 lakini makusanyo yalikuwa shilingi bilioni 115 sawa na asilimia 52. Na ukikisoma kitabu hiki, kimesema sababu ya kutokufikia hayo malengo ni taasisi na mashirika 114 yana deni la zaidi ya shilingi bilioni 78.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wakati muafaka sasa wa kuhakikisha hizi wizara na taasisi zinalipa madeni haya, lakini vilevile wamesema wananchi wamekuwa hawalipi pango la ardhi kwa wakati. Mawaziri wetu sasa wa Ardhi na wa TAMISEMI ni wakati wa kushirikiana kwa pamoja kuona namna gani wananchi hawa wanaenda kulipa pango la ardhi. Utaona katika halmashauri karibu zote wanapitisha magari ya matangazo, wanatangaza na kuwahamasisha wananchi waende kulipa leseni za biashara zinazotozwa na halmashauri. Kuna shida gani katika gari lile linalotangaza, wakatangaza na wakahamasisha wananchi kwenda kulipa kodi ya pango la ardhi. Kwa kufanya hivyo, na hakika wananchi wataamasika na pango la ardhi litalipwa na hatimaya tutafikia malengo ya wizara yetu hii ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kufanya transfer katika miliki zetu ambazo tunanunua kutoka kwa watu mbalimbali. Tulio wengi humu tuna zile sales agreement kwenye kufanya transfer tunakuwa hatufanyi na sababu kubwa aidha uhamasishaji unakuwa mdogo au mtu akishakuwa na ile sales agreements inamwezesha kufanya mambo mengine ambayo kama yangezuiliwa, tafsiri yake ingemlazimu kila mtu kwenda kufanya transfer ya ile hati aliyokuwa nayo. Hapa tunapoteza sana mapato kwa maana katika kufanya transfer kuna asilimia kumi ya thamani ya lile jengo zinakwenda TRA na tulio wengi kwa sababu hatufanyi transfer, basi mapato haya tumekuwa tukiyapoteza katika miaka yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala zima la mabadiliko ya matumizi ya ardhi. Ukisoma sheria zilizokuwepo za mabadiliko ya matumizi ya ardhi, ni elfu 30 tu ambayo inatakiwa iende wizarani, lakini ukiangalia taratibu zenyewe za kubadilisha matumizi ya ardhi, ni taratibu ndefu ambazo Serikali inatumia gharama kubwa kufanya hayo mabadiliko ya matumizi ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu na ushauri wangu, tuangalie namna ya kubadilisha hizi sheria angalau katika mabadiliko ya ardhi yaendane na thamani ya ardhi yenyewe. Leo mtu anabadilisha ardhi kutoka matumizi ya kawaida kuwa matumizi ya ujenzi wa petrol station lakini gharama ya kisheria anatakiwa alipe Sh.30,000 ebu tuangalie uhalisia, naamini haya yote tukiyafanyia kazi, basi katika sekta ya ardhi tutapata mapato ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la viwanja vilivyopimwa na vikamilikishwa. Kwa mujibu wa sheria zetu ndani ya miezi 36 huyu mtu anatakiwa akiendeleza kile kiwanja, lakini utakuta viwanja vingi havijaendelezwa. Kwa kufanya hivyo, tunakosa zile kodi za majengo. Niombe sana mamlaka husika, zizingatie hii sheria ya kuhakikisha wale wote waliopewa ardhi wanaziendeleza ardhi zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ulikuwa ndio mchango wangu katika kuhakikisha Serikali inaendelea kupata mapato ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kengele ya kwanza hiyo?

MWENYEKITI: Ndiyo, endelea.

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumzie juu ya Mradi wa Uendeshaji wa Jiji la Dar es Salaam. Tumekuwa tukipata maelezo hapa ambayo yamekuwa hayana mwelekeo miaka yote. Tunaambiwa uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam awamu ya pili upo katika michakato mbalimbali, tuwaombe sana hasa Waziri wa Fedha tumalize mazungumzo haya na kama hizi fedha zikipatikana zitaenda kutatua suala zima la miundombinu ya barabara katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwenye Jimbo langu la Mbagala ukiangalia kata zangu zote kumi, Kata ya Chamazi Kiburugwa, Mianzini, Charambe, Kilungule, Mbagala, Mbagala Kuu, Kijichi, Tuangoma na Kata ya Kibangulile. Kata hizi zinasubiri kwa hamu Mradi huo wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam. Kwa hiyo tumwombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, mradi huu aendelee kuusimamia hili uende kutekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam tumefanyiwa mambo ya kutosha mambo ambayo bado hayajakaa sawa, sasa hivi ni suala zima la miundombinu ya barabara. Tuwaombe sana mawaziri wetu wote wanahusika watilie mkazo suala la uboreshaji wa miundombinu ya barabara katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo yaliyo mengi na machache, naomba kuunga mkono Bajeti Kuu ya Serikali. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu hotuba hii ya bajeti imekidhi mambo mengi ambayo tumekuwa tukiyatarajia Wabunge katika majimbo yetu, lakini imeonesha namna gani ya mambo yaliyotekelezwa katika sekta ya afya, elimu, barabara, maji na umeme, kwa hiyo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kuweza kuyafanya yote haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote hayo yapo mambo machache ambayo yanahitaji marekebisho ya haraka ili tuweze kusonga mbele. Mara kadhaa toka tuanze Bunge hili nimekuwa nikipigia kelele suala la wananchi wa Rangitatu mpaka Kongowe kulipwa fidia zao, ni mwaka wa saba sasa wananchi wale wametathminiwa. Kama unavyojua sisi wananchi wa Dar es Salaam nyumba zetu ndiyo biashara zetu, ndiyo sehemu zinazotupatia riziki. Kwa hiyo nyumba sasa zimekuwa hazipangishiki na haziuziki, tumeendelea kupata ugumu wa maisha kutokana na kutokulipwa fidia zaidi ya miaka saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile sehemu inayotaka kulipwa fidia ni kwa ajili ya kujengwa barabara ile ambayo inatoka Rangitatu kwenda Kongowe. Wote mtakuwa mashahidi bahati nzuri Waziri Mkuu naye ndiyo njia yake ya kuingilia Dar es Salaam, barabara ile imekuwa na msongamano mkubwa kila mwaka tunaizungumzia. Nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri leo amenijibu kwamba barabara imepata kibali cha kutangazwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hoja yangu ya msingi tunatangaza barabara kujengwa, je, hawa watu ambao tumewaweka muda mrefu bila ya kulipwa fidia tunawafanyaje. Naomba sana Serikali itupe majibu lini watu hawa watalipwa fidia na lini barabara hii itaanza kujengwa ili tuondoe sintofahamu ambazo zimekuwa zikijitokeza mara kwa mara katika barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo nataka kuliongelea ni suala zima la alama za X nyekundu zinazowekwa katika maeneo mbalimbali katika Mkoa wa Dar es Salaam. Katika Jimbo langu Barabara yote inayotoka Rangitatu - Charambe kwenda mpaka Maji Matitu – Chamanzi mpaka Msongola kupitia Mbande pande zote mbili imewekewa X, sasa tunajiuliza hawa wenzetu wa TANROADS wanaweka X kwa sababu gani. Bahati nzuri sisi wengine tumezaliwa Dar es Salaam, maeneo tunayokaa ndiyo tuliyozaliwa. Tunafahamu historia ya maeneo yale, maeneo yale yalikuwa ni Vijiji vya Ujamaa ambapo wazawa wa pale walitoa ardhi zile kwa ajili ya kuwapa makazi ndugu zao waliokuja katika maeneo yale lakini kwa masharti watakapokata mti basi mti ule ulipwe fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kijiji kile kukua Serikali tunaishukuru iliamua kututengenezea barabara na mwaka 1994 Serikali kupitia Kampuni ya ADUCO iliamua kuboresha barabara ile, barabara ile ilijengwa kwa upana wa mita saba na nusu kwa pande zote mbili kwa maana ya mita 15. Wakati inajengwa miti ya wazee wetu ililipwa fidia na ikapisha ujenzi wa barabara ile mpaka sasa tunapita kwa amani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2007 Sheria ya Barabara Namba 13 ilitungwa. Katika sheria ile inaelezea barabara itakuwa na mita 27.5 pande zote za barabara kutoka katikati ya barabara, hoja yetu tunayojiuliza, unatuwekea X je, barabara ile ilipandishwa hadhi mwaka gani na ilipandishwa hadhi kwa GN namba ngapi? Ili tuone kama kweli X zile zinazowekwa zinaendana na ile sheria ya mwaka 2007 iliyotungwa Sheria Namba 13.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sheria ile wakati inatungwa hakuna aliyelipwa fidia na kama wapo waliolipwa fidia basi tuwaombe wenzetu wa TANROADS watuletee orodha ya watu waliolipwa fidia ili tupishe eneo lile kwa amani. Tumekuwa tukiwaomba mara kwa mara, lakini wameshindwa kufanya hivyo hatimaye Serikali kupitia Mkuu wa Mkoa imesitisha zoezi lile la kubomoa, zoezi lile tunasema limesitishwa kwa mdomo, tunaomba tupewe maandishi kwamba zoezi hili limesitishwa kwa sababu moja, mbili na tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi tunayo maswali ya kujiuliza, moja, tunataka tujue GN namba ngapi na ya mwaka gani iliipandisha hadhi barabara ile ili tuweze kujua sasa kama sisi tuliokuwepo tulikuwepo kimakosa au tuko sawasawa. Jambo la pili ni wananchi wangapi walilipwa fidia baada ya GN ile kutoka, lakini jambo la tatu kwa nini Wizara ya Ardhi imetoa hati miliki katika maeneo yale pande zote mbili za barabara? Wananchi siyo tu wanamiliki leseni za makazi wanamiliki kwa hati miliki, tunaomba tupewe majibu hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tunataka tujue ni vigezo gani ambavyo TANROADS walitumia kulipa fidia watu waliokuwa barabarani wakati wanajenga stendi ya mwendokasi na hawa waliopo sasa hivi watakiwe kubomolewa bila kulipwa fidia. Mambo haya yameleta taharuki kubwa sana kwa wananchi kwa sababu ni zaidi ya kaya 100,000 zinaenda kuathirika katika barabara ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunajua Jimbo la Mbagala na Jimbo la ndugu yangu Jerry ndiyo yanaongoza kwa population kubwa hapa nchini, kwa hiyo mjue kitendo kilichofanywa na TANROADS kimeenda ku-disturb siasa za Dar es Salaam. Naomba sasa Serikali ije na kauli ambayo itawatoa hofu wananchi wa Mbagala Rangitatu, Charambe, Chamazi na Msongola.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nizungumzie suala la miundombinu ya barabara. Tunafahamu mvua zimenyesha na barabara zimeharibika kwa kweli katika Jimbo zima la Mbagala kama siyo Mkoa wote wa Dar es Salaam barabara zimeharibika sana, tunawaomba sana TANROADS na TARURA waje warekebishe barabara zile ili ziweze kupitika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho tunazo mamlaka au taasisi mbili zinazojenga barabara hapa nchini. Tunao TANROADS na TARURA, ushirikiano wao hauko sawasawa kwa sababu wakati fulani TANROADS wanajenga barabara na wanaweka mifereji lakini maji wanaelekeza katika makazi ya watu na wanasema wananchi suala la maji yale kuyapeleka mtoni ni suala la TARURA, je wali-check bajeti za TARURA wakalinganisha na bajeti zao ili kuona barabara ile itajengwa na TARURA watapokea yale maji kuyapeleka mtoni?

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba sana watendaji wetu wa Serikali pale wanapotaka kufanya maamuzi ambayo yatawagusa wananchi moja kwa moja hasa suala la bomoa bomoa waangalie historia ya maeneo yale, sisi tunawafahamu, ukiangalia TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam wote wanaofanya kazi sasa hivi ni watu ambao wamekuja miaka ya 2000, wangeuliza historia kwa wenzao waliokuwepo nyuma wangepata hadhi ya barabara ile ilikuwaje ili sasa wakurupuke na mipango yao ya kuweka X.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)