Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Noah Lemburis Saputi Mollel (36 total)

MHE. NOAH L. S. MOLLE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri , lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Serikali ina nia njema ya kutoa huduma ya maji, kulikuwa na miradi ya mwaka 2009 miradi ya Likamba, Musa, Nengu, Olotushura na Loskito, je, ni lini sasa Serikali itakamilisha miradi hiyo ya muda mrefu?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Maji katika kukarabati Mradi wa Ilmuro inayohudumia Kata za Oljoro na Laroy. Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha ahadi hiyo ya Mheshimiwa Waziri? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Lemburis Saputu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mradi huu ambao ulianza kutekelezwa mwaka 2009, nipende tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge miradi hii tunakuja kuitekeleza na nimeshafika eneo lake. Nimwahidi namna ambavyo tuliongea pale site tutakuja kufanyia kazi haraka iwezekanavyo na pamoja na hii ahadi ya Mheshimiwa Waziri aliyepita, ukarabati wa Mradi huo wa Ilmuro pia unakuja kufanyiwa kazi hivi karibuni. Fedha tayari zipo na mgao unaofuata na mgao unaofuata na Mheshimiwa Mbunge yupo na atakwenda kutekelezewa mradi huo.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nia ya mfuko huo ni kujaribu kusaidia vijana na akina mama na watu wenye ulemavu katika kukuza ajira, hawaoni sasa ni muda mwafaka wa kuongeza muda kutoka miaka 18 hadi 45 badala ya 18 mpaka 35 ambayo hiyo inawazuia wananchi walio wengi kupata mikopo hiyo na kufanya biashara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la mikopo hii kwa vijana ni kuhakikisha kwamba pia inawawezesha kiuchumi, na hasa vijana wa umri wa miaka 18 hadi 35 kwa maana ya definition ya kijana. Kwa hiyo, wazo lake la kuongeza wigo kutoka miaka 18 hadi 45 linahitaji pia kulifanyia tathmini na kuona kama miaka 45 iko ndani ya umri wa ujana au kama maana yenyewe ya vijana inahitaji kuboreshwa ili kuongeza wigo huo. Kwa hiyo, ni wazo zuri, lengo ni kuboresha na sisi Serikali tunaomba tulichukue hilo tukalitafakari na kuona uwezekano wa kulitekeleza kwa manufaa ya jamii yetu. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, na kutakuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuuliza, kwa kuwa suala la kupanuliwa kwa hospitali hiyo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa muda mrefu; je, hospitali hiyo iko kwenye idadi ya hospitali 21 zitakazokarabatiwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa, hospitali hiyo inatoa huduma kwa akina mama na watoto vijijini ambao hawana uwezo wa kupata huduma za afya kwenye hospitali binafsi ambazo ni gharama kubwa, je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka wa kuiweka hospitali hiyo kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 ili na yenyewe iweze kutoa huduma bora kwa wananchi wetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Noah Mollel Mbunge wa Arumeru Magharibi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie kwamba ahadi zote za viongozi wetu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Nimhakikishie kwamba hospitali hii ya Orturmet ni miongoni mwa hospitali ambazo zimepewa kipaumbele; na nimhakikishie kwamba katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 tumeanza na hospitali 21 awamu ya kwanza; na tutakuwa na awamu ya pili ya hospitali zile nyingine ambazo zinabaki. Nimhakikishie katika awamu hiyo ya pili hospitali hiyo ya Orturmet Arusha ni miongoni mwa hospitali ambazo zitaingizwa ili ziweze kufanyiwa upanuzi na ukarabati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hospitali hii inatoa huduma kwa wananchi vijijini na wengi wao ambao hawana uwezo na ndiyo maana Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba inaingiza kwenye orodha hospitali ambazo zinapewa kipaumbele kwaajili ya ukarabati ili iendelee kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi katika maeneo hayo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Noah kwamba jambo hilo linafanyiwa kazi na mara fedha zikipatikana hospitali hii itakarabatiwa ili iweze kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. NOAH L.S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, kwanza jina langu naitwa Noah Lemburis Sabutu Mollel.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa, namshukuru Naibu Waziri kwa kurekebisha kwamba siyo milioni 314 badala yake ni bilioni 314 ndiyo inayodaiwa na Halmashauri Arusha DC.

SPIKA: Amerekebisha wapi.

MHE. NOAH L.S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, kwenye majibu ya maswali hayo iliandikwa milioni 314 badala ya bilioni 314.

SPIKA: Sasa wewe ndiyo unatutaarifu hilo Mheshimiwa, siyo walitakiwa waseme wao kama hivyo ndivyo? Endelea na swali lako lakini.

MHE. NOAH L.S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa suala hili la ulipaji wa fidia ya umeme lilikuwa liende sambamba na usambazaji wa umeme kwenye Jimbo la Arumeru Magharibi na vijiji vyake hasa ukizingatia kwamba mkandarasi amechimba mashimo ameacha, ameweka nguzo ameacha ajaweka waya, ni lini sasa Serikali itamaliza tatizo hilo?

SPIKA: Tatizo gani?

MHE. NOAH L.S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, la kutokuwepo kwa umeme kwenye jimbo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa sasa hali ni tete kwenye jimbo kuhusu masuala hayo mawili ya fidia na usambazaji wa umeme, Naibu Waziri yupo tayari tuweze kuongozana naye kwenda kuokoa jahazi ambapo hali ni tete kwenye jimbo?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye swali la msingi naomba niliweke vizuri hoja ya Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine ambao wanapitiwa na mradi wa kilovolt 400 wa kwenda Namanga. Ni kweli Serikali imetoa shilingi bilioni 52.67 katika maeneo yote ambako laini inapita. Lakini kila eneo ilipewa fidia yake kulingana na idadi ya watu waliofanyiwa tathmini kwa hiyo pesa hiyo inagawanywa katika maeneo yote ambako line imepita.

Mheshimiwa Spika, juzi nilikuwa Arusha na kati ya changamoto ambazo nilikutana nazo ni pamoja na hii, akiwepo na Mheshimiwa wa Longido, nilitoa maelekezo ya jumla kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wananchi ambao hawajalipwa fidia kwa sasa ambao pesa zao zimeshapelekwa tayari kwa Wakurugenzi wao walipwe fidia hizo mara moja toka juzi. Ni kweli zinaweza zikawa zinatofautiana kiwango kwa kiwango kila wilaya lakini ya jumla ya fedha zake ni hizi. Lakini majibu ya jumla nishatoa juzi, kwa Mheshimiwa Mbunge wa Longido na wananchi walilidhika na Wakurugenzi walikubali na Wakuu wa Wilaya kuanza kulipa fidia hizo mara moja kutoka juzi ndani ya siku 10.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kuhusiana na maeneo ambayo amezungumza ambayo ajapelekewa umeme nimetoa maelekezo na wakandarasi wote wako site na leo tunakutana nao, maeneo yote ambayo awajapatiwa umeme wakandarasi wameanza kazi toka Mwezi Machi na katika wilaya za Arusha wameanza wiki iliyopita na watapelekewa umeme ndani ya miezi 18 kutoka mwezi Machi hadi mwezi Mei. Ahsante sana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri ambayo yanaonesha kwamba kwa kweli Serikali inafanya kazi nzuri sana, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, je, fedha ambazo kiasi kilichotengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo shilingi bilioni 2.5 zinatosha kukamilisha barabara hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Jimbo la Arumeru Magharibi mazingira yake kwa maana ya miundombinu sio mizuri kabisa. Naomba kujua je, tuna barabara mbili, barabara ya Malalua – Nduruma – Bwawani inayounganisha Simanjiro na Arumeru Magharibi na barabara ya TPRA – Likamba inayounganisha na Monduli.

Je, haioni sasa ni busara kwa ajili ya mazingira ya Jimbo hilo magumu barabara hizo mbili kupandishwa hadhi kupelekwa TANROADS? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba fedha iliyotengwa haiwezi ikakamilisha kilometa 18, lakini hii ni fedha ya awali kwa ajili ya kuanza mradi na wakati huo Serikali itaendelea kutafuta fedha ili kukamilisha mradi huu. Mradi huu utaenda kwa awamu, fedha iliyopatikana tutaanza na kazi na kazi itakavyozidi kupatikana basi tutakamilisha huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili nimshauri Mheshimiwa Noah Lemburis, Mbunge wa Arumeru Magharibi kwamba hizo barabara ambazo amezitaja kuna utaratibu maalum ambao kama barabara inatakiwa ipandishwe hadhi zipo taratibu, ziko kanuni ambazo zinapitia kwenye vyombo kuanzia Halmashauri kwenda kwenye DCC, kwenda Mfuko wa Barabara wa Mkoa hadi RCC ambao wanaleta hayo maombi kwenye Wizara yetu na sisi tunafanya tathmini na kuona inakidhi vigezo vya kupandishwa daraja ili barabara hizo ziweze kuhudumiwa na Wakala wa Barabara TANROADS. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Noah uende ukafanya mchakato huo nasi tutafanya tathmini na kama zitakidhi vigezo barabara hizo zitasimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara hii iliahidiwa na Mheshimiwa Rais na umepita muda mrefu sana, na wananchi wamekuwa wakihoji, na katika majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri sijaona commitment. Je, ni lini hasa fedha zitapatikana kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa tunakwenda kuahirisha Bunge keshokutwa na wananchi wamekuwa wakiniuliza kila siku na kila saa kwa sababu hospitali hiyo inatumiwa na wagonjwa wengi sana kwenda kwenye hospitali ya wilaya. Ni nini nitakwenda kuwaambia wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibu nitakaporudi Jimboni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ameuliza tu kwamba lini hasa fedha zitapatikana kwa sababu ahadi hii ni ya muda mrefu, na katika jibu letu la msingi tumeeleza hapa kwamba mara fedha zitakapopatikana basi barabara hii tutaiingiza katika mipango yetu ya kujengewa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa kuwa Serikali ilisikia kelele ama maombi ya Wabunge ambayo waliyatoa katika Bunge lako Tukufu na kusababisha Serikali kutaka kuanzisha chanzo kipya cha fedha ili TARURA iweze kuongezewa, ninaamini tutakavyopata ongezeko la fedha hiyo tutazingatia ombi la Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ameuliza ni nini akawaambie wananchi. Akawaambie tu wananchi kwamba ahadi ambayo viongozi wetu wakubwa waliitoa itatekelezwa mara hapo fedha itakapopatikana. Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kulikuwa na wananchi wa Kata za Oldonyo Sambu, Mlangarini, Bwanani na Nengung’u ambapo Jeshi limechukua maeneo yao na Serikali ikaahidi kwamba ingewafidia.

Je, ni nini sasa kauli ya Serikali kuchukua maeneo ya mashamba haya ya Tanzania Plantation na Nuru Farm ili wale wananchi waweze kufidiwa kama Serikali ilivyowaahidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Shamba la Aghakan lililokuwa chini ya Manyara Estate lilikuwa linaajiri zaidi ya watu 2000 kama ajira; na sasa Aghakan imelichukua shamba hilo tangu mwaka 2006 ikisema itajenga Chuo Kikuu: Sasa ni miaka 16 imepita bila kujenga Chuo Kikuu wala kuajiri wananchi hao.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu shamba hilo kukaa miaka 16 bila kuendelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu maswali mawili ya nyongeza Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na fidia ya Jeshi, ni kwamba nitawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Ulinzi ili waweze kutujulisha vizuri juu yah atua ambazo wameshafikia. Tutakapokuwa tumeshapata taarifa za kina, nitakutana na Mheshimiwa Mbunge ili niweze kumpa mrejesho huo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na shamba la Aghakan; mwaka 2017, Mheshimiwa Rais aliagiza Wizara nne zikutane ikiwemo Wizara ya Mambo ya Nje, Ardhi, Fedha na Elimu kwa lengo la kuzipatia ufumbuzi changamoto hizo za Taasisi. Hivyo inalazimika kusubiria utekelezaji wa mpango wa uendelezaji uliokusudiwa kutokana na mazungumzo yanayoendelea kati ya taasisi hiyo na Serikali, mazungumzo hayo kwa upande mwingine yanaratibiwa na Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakapokuwa tumepata mrejesho au hatua ya mwisho ya mazungumzo hayo, tutamjulisha na hatua stahiki zitafuata. Ahsante. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Namshukuru Mheshimiwa naibu kwa Majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, naomba kutaka kujua, kwa kuwa watu wa Aga Khan kwa maana ya Taasisi ya Aga Khan wanasema kwamba ninyi Wizara ya Ardhi pamoja na Wizara nyingine Tano ikiwemo Mambo ya Nje, Mambo ya Ndani, mnazuia wao wasiendeleze shamba hilo kwa kuwa kuna jambo ambalo hamkulifanya ili waweze kuendeleza shamba hilo. Nini kauli ya Serikali kuhusu taasisi hiyo?

Swali la pili, ni lini utatembelea shamba hilo ili kujua wazi dhahiri shahiri kwamba kuna nini juu ya jambo hilo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO
YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nitoe taarifa kuhusu shamba hili la Aga Khan. Shamba hili wakati linaombwa mwanzo liliombwa kwa ajili ya kilimo, lakini kutokana na maendeleo ya ukuaji wa Mji wa Arumeru Magharibi ikalazimika matumizi ya shamba lile yabadilike na kuwa eneo la kupanga Mji kwa maendeleo ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo kumetokea changamoto baina ya maeneo ambayo yanaendelezwa na hii Taasisi ya Aga Khan na Serikali, hivyo ndivyo mgogoro anaouzungumza Mheshimiwa Mbunge ulipoibuka. Maelekezo ya Serikali ni kwamba, punde tutakapo maliza mazungumzo hayo taratibu nyingine kwa ajili ya uendelezaji zitaendelea.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, swali lake la pili ulikuwa umeshalijibu?

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ombi la kwenda kuona shamba hilo ili kuona maendeleo mengineyo. Natoa ahadi kwamba niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge ili kuona na kufuatilia yanayoendelea katika shamba hilo.

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumwuliza Waziri swali la nyongeza kwamba kulikuwa na watumishi wa Darasa la Saba ambao wamesimamishwa na walikuwa wamefanya kazi kwa muda mrefu na baadaye hawakupewa kiinua mgongo wala chcohote: Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu watumishi hawa ambao kwa kweli wametumikia pia Taifa kwa kipindi kirefu kwa ujuzi huo wa Darasa la Saba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wa darasa la saba walioajiriwa baada ya Mei, 2004 wale Serikali ilikwishatoa tamko na ilimradi wawe walikuwa hawakughushi nyaraka zao walipewa muda mpaka ifikapo Desemba, 2020 wawe wamejiendeleza na kuweza kuendelea na ajira zao na wale ambao hawakujiendeleza, tayari mamlaka ilishatoa tamko kwamba wale washughulikiwe walipwe michango yao ya hifadhi ya jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hadi kufikia Desemba, 2020 jumla ya watumishi 1,191 walikuwa hawakujiendeleza na hivyo wanastahili kulipwa michango yao ya hifadhi ya jamii.
MHE. NOAH L. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itajenga VETA katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha katika Jimbo la Arumeru Magharibi ambayo tayari tumeshawasilisha eneo kwa ajili ya kujenga VETA?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi, wilaya 63 ambazo hazina Vyuo vya VETA tunatarajia kuanza ujenzi mara tu tutakapopata fedha ikiwemo na Wilaya ya Arumeru.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa kuna kundi kubwa la watu ambao sio vijana, wenye umri wa miaka ya 35 hadi 45, wanaachwa sana na ni changamoto kwenye ajira, na bado wapo kwenye kundi la kuajiriwa na Serikali kwa maana hawajafikia ukomo.

Je, ni lini Serikali sasa itarekebisha hiyo sera au itatoa tamko kwamba sasa nao wale watu wapewe mikopo kupitia hiyo asilimia kumi, au kuongeza asilimia 10 ili kupunguza hili wimbi la ukosefu wa ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mikopo hii inatolewa kwa vijana ambao wana umri wa miaka 18 hadi 35 kwa mujibu wa definition ya vijana kwa utaratibu huu wa mikopo ya ten percent. Ni kweli kwamba kuna vijana ambao wana umri wa zaidi ya umri wa miaka 35 ambao pia wangeweza kunufaika na mikopo hii. Kwa hiyo, naomba niichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge tukaifanyie kazi na kuona uwezekano huo na pia kuona kama inaweza ikatekelezwa ama vinginevyo. Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kumuuliza Waziri swali la nyongeza kwamba kumekuwepo na malalamiko kwa wananchi kuhusu ubora wa mbolea zinazoingizwa nchini na makampuni mbalimbali hasa mahindi na mazao ya kunde.

Je, ni nini hasa kauli ya Serikali kuhusu mbegu hizo ambazo zinaingizwa na hazina ubora nchini na wananchi wanaendelea kupata hasara? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Noah kwa ufupi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Mtanzania ambaye amenunua mbegu na ana receipt ya duka lililomuuzia mbegu ile na mbegu ile ikawa ni fake, atoe taarifa Wizara ya Kilimo, kwa sababu tutamchukulia hatua muuzaji kwa maana ya dealer na distributor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo utaratibu wa kisheria ambao unasimamiwa na taasisi yetu ya TOSCI na TOSCI anatoa namba maalum katika kila mbegu inayouzwa mtaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Mtanzania amenunua mbegu na ikawa feki tunamkaribisha afike Wizara ya Kilimo, tutachukulia hatua wote. Tunayo kesi Mkoa wa Ruvuma ambayo mtu aliuza mbegu, alizitia rangi na sasa hivi amepelekwa mahakamani, anachukuliwa hatua kwa sababu huu ni uhujumu uchumi na hatuwezi kuruhusu hili. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha ina Hospitali ya Wilaya ya Oltrument ambayo tangu Serikali ilipoanza kuboresha Hospitali za Wilaya Hospitali hii haijawahi kukumbukwa hata siku moja.

Je, ni lini Serikali itaona sasa umuhimu wa kuongeza majengo haya katika hospitali hiyo ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais tangu mwaka 2012? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Saputu Molllel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Arusha inanendelea na ujenzi na ina upungufu wa majengo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kujenga majengo hayo kwa awamu na Hospitali hii pia itapelekewa fedha ili iweze kukamilisha majengo yote muhimu. Ahsante.
MHE. NOAH L. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kuna mradi wa vijiji tisa vya Oldonyo Sambu, Lengijave na Oldonyo-Wass ambao wanasumbuliwa na maji ya fluoride na imekuwa ikisuasua utekelezaji wake: Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha za kutosha kwa ajili ya kukamilisha mradi huu ambao wananchi wanateseka na maji ya fluoride? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah, Mbunge wa Arumeru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tulipata tatizo na changamoto hii bado ipo, lakini sisi kama Wizara tayari tuna hatua mbalimbali tumeshazichukua na fedha tunatarajia mgao ujao. Mheshimiwa Mbunge nawe katika mradi ule tutapata. Lengo ni kuona tunatekeleza miradi mikubwa ambayo maeneo yake, maji yake chini hayana fluoride ili tuweze kunusuru watoto wanaoweza kuzaliwa na ulemavu na watu wote ambao wanateseka na maji yenye fluoride. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Arumeru Magharibi wananchi wanahitaji umeme kwa asilimia 100. Kuna Mkandarasi ambaye yupo kwenye Jimbo hilo ambaye amekuwa akisuasua kuwapa wananchi umeme, kuna maeneo kuna maeneo amechimba mashimo, hakuna nguzo kwa muda mrefu, kuna maeneo ameweka nguzo hakuna nyaya kwa muda mrefu, maeneo mengine hakuna umeme kabisa....

MWENYEKITI: Sasa uliza swali lako Mheshimiwa.


MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ambao wamesubiri umeme wa REA kwa muda mrefu bila mafanikio?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lemburis Noah Saputi, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ambayo tulichelewa kupata Mkandarasi eneo la Arumeru ni mojawapo, Mkandarasi tayari amepatikana na anaendelea na kazi, katika maeneo ambayo tunaangalia kwa macho ya Karibu Mkoa wa Arusha pia ni mmojawapo. Tunahakikisha kwamba katika muda ambao tumekubaliana nae wa kimkataba kazi yake ya kupeleka umeme kwenye maeneo hayo itakamilika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tunaomba atupe subira kidogo na utatuona sana katika Jimbo lake tukiendelea kuvutana na Mkandarasi kuhakikisha kwamba kazi inakamilika katika muda tuliokubaliana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakwenda kujenga VETA katika Jimbo la Arumeru Magharibi katika Wilaya ya Arumeru?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyozungumza katika majibu ya msingi, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inajenga vyuo vya VETA katika kila Mkoa na Wilaya nchini na tumeweza kufikia Mikoa yote na hivi sasa tunakamilisha Mkoa wa mwisho ule Mkoa wa Songwe. Katika mwaka huu wa fedha tunakwenda kujenga katika Wilaya 63 ambazo zilikuwa hazina vyuo hivi. Iwapo kama Arumeru ni miongoni mwa Wilaya zile 63 bila shaka tutaifikia wilaya hii na kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga katika Wilaya ya Arumeru.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Arumeru hususan Kata 13 ambayo ndio imekubwa na njaa imepakana na Longido, Ngorongoro na Monduli. Katika Wilaya hizo za Ngorongoro, Monduli na Longido chakula kimeuzwa shilingi 700 kwa wananchi, lakini katika upande wa Arumeru Magharibu chakula wananchi wanaambiwa wanauziwa shilingi 885.

Je, ni kwa nini bei katika Wilaya zingine ni shilingi 700 na Arumeru Magharibi ni shilingi 885 na wakati tuko sehemu moja na hali ni hiyo hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa kuna hilo tatizo Waziri haoni haja ya kufika katika Jimbo la Arumeru Magharibi au Wilaya ya Arumeru ili aweze kuona hali halisi ilivyo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo Mheshimiwa Mbunge ameliuliza hapa tulishawasiliana naye na tulitoa ufafanuzi ambao nataka niurudie hapa.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza ya Mheshimiwa Mbunge ni juu ya kituo kuwepo katika eneo ambalo haligusi katika jimbo lake na hivyo wananchi katika eneo lake wanachukua umbali mrefu na bei imekuwa ikiongezeka sana kuweza kupata ile bei ambayo maeneo mengine wanapata.

Mheshimiwa Spika, nilishasema hapa Bungeni ya kwamba katika mazao haya ya mahindi ya bei nafuu, chakula cha bei nafuu kama Mheshimiwa Waziri alivyosema tunapeleke kwenye Halmashauri ya Wilaya na vituo ndiyo vinatengenezwa hapo, lakini ikitokea kwamba katika baadhi ya maeneo kuna umbali mrefu, NFRA tumeshawapa maelekezo ya kusogeza vituo hivyo ili kuweza kuwahudumia watu wote kwa ukaribu zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo katika maelezo ya awali kama katika eneo lake alikuguswa mimi nitatoa maelekezo siku ya leo kuhakikisha kwamba NFRA wanaongeza vituo ili na jimboni kwake pia paweze kuguswa na iweze kupunguza pia hali ya bei kwa sababu moja kati ya changamoto kubwa inayosababisha pia ni kwa sababu ya umbali ambao wamekuwa wakiupiga NFRA.

Kwa hiyo, kwa ujumla wake tumwachie Mheshimiwa Mbunge ya kwamba tutahakikisha pia katika uongezaji wa vituo tutagusa na jimbo lake ili wananchi wake wasiende umbali mrefu na bei pia isiweze kuwa kubwa kama ilivyo hivi sasa. (Makofi)

SPIKA: Ameuliza kuhusu kwenda kujiridhisha.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kuhusu kwenda kujiridhisha hiyo ni kazi yangu mimi kama Naibu Waziri, nilitaka nimhakikishie kwamba nipo tayari baada ya Bunge hili nitakwenda katika eneo hilo kwenda kujiridhisha katika hali ambayo ameisema. (Makofi)
MHE. NOAH L. SAPUTU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza maswali mawili. Kwa kuwa ujenzi wa hospitalli hii na upanuzi wake ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa muda mrefu sasa na haikuweza kutekelezwa.

Je, nini kauli ya Serikali kwa wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ambao wanategemea hospitali hiyo kwa asilimia kubwa na haijajengwa mpaka sasa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kutembelea hospitali hiyo ili ajionee hali halisi ya wagonjwa walivyo wengi na upanuzi wa hospitali hiyo haikuweza kufanyika kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeza sana Mheshimiwa Noah Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi kwa namna ambavyo anawasemea kwa dhati wananchi wa jimbo lake. Nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI itaendelea kushirikiana naye kuhakikisha wananchi wanapata matunda ya Serikali yao sikivu.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ahadi ya Mheshimiwa Rais, ni kwamba ahadi za viongozi wetu wakuu wa nchi ni maelekezo, na ndiyo nimemuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye mwaka ujao wa fedha 2022/2023 tutatafuta fedha ili tuweze kuanza utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais katika ukarabati hii ya Arumeru.

Mheshimiwa Spika, pili, nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge, tutakubaliana hili baada ya Bunge twende tukaitembelee hospitali hiyo.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, kwa kuwa kumekuwepo na changamoto katika Shule za Msingi na Sekondari kwa ajili ya watoto kupata chakula shuleni. Nini kauli ya Serikali kuhusu watoto kupata chakula shuleni kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watoto wanakuwa kwenye ufanisi mzuri kiakili na kimwili?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli suala la chakula shuleni kwa watoto ni jambo ambalo ni muhimu, bado kuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji chakula mashuleni kwa ajili ya watoto wetu. Serikali tulishatoa mwongozo wa namna gani wazazi au walezi wanaweza kushirikiana na Serikali kuhakikisha kwamba watoto wetu wanapata chakula shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mwongozo ule unadadavua na unatoa maelekezo mazuri kabisa kwamba kila upande ni namna gani unaweza kushiriki ili wanafunzi wetu waweze kupata chakula wanapokuwa shuleni. Nakushukuru sana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka au kusambaza umeme kwenye vijiji na vitongoji katika Jimbo la Arumeru Magharibi ambayo imekuwa ni changamoto sana wananchi kupata umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Saputi, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo mradi ambao unaendelea wa upelekaji wa umeme katika vijiji wa REA III Round Two ambao pia unahusika katika kufikisha umeme kwenye vitongji. Lakini muda si mrefu tutaanza Mradi mwingine unaitwa Densification IIC ambao una takribani vitongoji 2,600, nao ni kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji.

Mheshimiwa Spika, lakini kama ambavyo tumekuwa tukisema, tunatafuta pesa kwa ajili ya upelekaji wa umeme katika vitongoji vyote 36,000, takribani trilioni sita na bilioni mia tano ili kumaliza tatizo lolote la umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kwenye vile vijiji vilivyopo kwenye mradi kabla ya Desemba mwaka huu vitaisha na pesa nyingine itatafutwa kufikisha katika maeneo mengine.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mahakama ilishatoa uamuzi kuhusu suala la umri la watoto wadogo kuolewa Tanzania. Serikali haioni kuendelea kukusanya maoni ni kukiuka amri ya Mahakama?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria amesema vizuri kwamba, tulishaleta kwenye Bunge lako hili Tukufu na nimesema kwenye majibu yetu ya msingi, kwamba ni Bunge hili na Kamati hii ilitutaka turudi kwa wananchi ili tupate wigo mpana wa kuwahusisha Watanzania katika hili. Kwa sisi hatuna tatizo na niwakaribishe Waheshimiwa Wabunge kesho wenye nafasi mje tunamaliza hayo majadiliano katika Hoteli ya Morena kesho Saa Saba Mchana, tukishakamilisha tutaleta sheria hii Bungeni. Ilikuwa ni agizo la Bunge siyo la kwetu.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Kwa kuwa, mawakala ambao walitakiwa kutoa mbegu katika Jimbo la Arumeru Magharibi wamekataa kutoa mbegu kwa madai kwamba Serikali haijawalipa fedha zao na kusababishia wakulima kutopata mbolea katika maeneo husika. Je, nini kauli ya Serikali kwa ajili ya kuwasaidia wakulima hawa kwa haraka ili waweze kupata mbolea hasa katika msimu huu wa kilimo?

Swali la pili, kwa kuwa Mawakala hawa wanateuliwa na Wizara moja kwa moja kwenda kwenye Majimbo au Halmashauri.

Je, Serikali haioni sasa ifanye jambo la haraka kuwateua mawakala wa uhakika watakaokwenda kutoa huduma hiyo kwa wananchi hawa ili waendelee kupata huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwamba Mawakala hawajalipwa fedha zao na ndiyo sababu ya kutokupeleka mbolea ya ruzuku kwa wananchi jambo hilo sidhani kama lina ukweli wowote, isipokuwa ni kwamba Serikali inafanya taratibu za kumalizia malipo kwenye baadhi ya Mawakala ambao watalipwa na kazi yao itafanyika, lakini kigezo cha kutokulipwa kwa sababu hiyo ni kigezo ambacho Serikali kupitia Wizara ya Kilimo haioni kama ni njia muafaka wa kuwasaidia wakulima na wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawataka Mawakala wote kutekeleza yale maelekezo ya mikataba ambayo walisaini kati ya Mawakala na Wizara ya Kilimo. Pia kuteua Mawakala wa uhakika jambo hilo tumelipokea na ndiyo maana katika awamu hii iliyofanyika, maana yake imetoa somo kwa Wizara ya Kilimo ambalo katika mwaka unaokuja maana yake itazingatia yale mapungufu yaliyojitokeza mwaka huu ili yasiweze kujitokeza katika msimu ujao wa kilimo. Ahsante. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je ni lini Serikali itajenga Daraja la Unguuni katika Kata ya Nduruma ambayo imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na TARURA na sasa wananchi wanateseka hasa katika kipindi hiki cha mvua na mafuriko yanayowasumbua wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, daraja hili la Kata ya Nduruma tutaangalia kama lipo kwenye bajeti ya mwaka huu ambayo imeshapitishwa lako Tukufu kwa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA). Kama haipo basi tutahakikisha inatengewa fedha katika mwaka wa fedha unaofuata.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Katika Jimbo la Arumeru Magharibi kuna kata kama tano ambazo hazina mawasiliano Kata ya Bwawani yenye vijiji vinne, Olonyowase yenye vijiji vinne, Oljoro yenye vijiji vitatu, Laroi vijiji vitatu na Mwande vijiji vitatu.

Je, ni lini sasa Serikali itapeleka minara na kuhakikisha kwamba wananchi wale ambao wanateseka kupanda juu ya miti na juu ya milima na vigongo kwa ajili ya kupata mawasiliano ya kuwasiliana?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kupokea changamoto ya mawasiliano katika kata ambao Mheshimiwa Mbunge, amezitaja. Tutazifanyia kazi na baadae tutamrejea kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunafikisha huduma ya mawasiliano.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wakati Mheshimiwa Rais alipofanya ziara Arusha, wananchi wa Jimbo la Meru Magharibi katika Kata ya Kisongo Mateves alituahidi soko: -

Je, ni lini sasa Serikali kupitia TAMISEMI itajenga soko la Kisongo Mateves?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa sababu hii kama anavyosema Mheshimiwa Lembris ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, tutakaa na wenzetu wa Halmashauri ya Wilaya kuona kama michoro iko tayari iwasilishwe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuiombea fedha Hazina na kuanza ujenzi wake mara moja.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itaanza kutoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya kati ambao wanapata diploma na vyeti hapa nchini kwetu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Saputu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu ya 2023/2024 jambo hili lilizungumzwa bayana katika Bajeti Kuu ya Serikali. Serikali imetenga fedha kwa ajili ya utoaji mikopo kwa vyuo hivi vya kati na programme hii itaanza mwaka huu wa fedha.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza;

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi waliopisha Barabara ya Mianzini – Sambasha - Kimyaki hadi Ngaramtoni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii ni mpya na imefunguliwa. Tayari tulishandaa taratibu za kuwalipa wananchi ambao tumeifungua ile barabara, na barabara iliyoanza ni mpya wananchi hao watalipwa mara baada ya kukamilisha taratibu zote za fidia, ahsante. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Soko na Stendi ya Kisongo Mateves ambayo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Saputu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba, kwanza Halmashauri zenye miradi hiyo zinaainisha gharama zinazohitajika kwa ajili ya ujenzi wa stendi na masoko hayo. Pia, kutenga fedha kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza utekelezaji. Lakini kama gharama ni kubwa kuliko uwezo wa halmashauri, kuwasilisha Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, tutaenda kulitekeleza hilo, na hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais lazima tutaitekeleza na tutaipa kipaumbele katika miradi yetu ya ujenzi wa masoko na stendi.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, swalil a kwanza; kwa kuwa wananchi katika karne hii ya leo wanateseka kupanda juu ya vichuguu na vilima kutafuta mawasiliano; je, tathimini hii itafanyika ili wananchi hawa wapate huduma? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan aliwapa Wizara hii minara mia saba na hamsini na nane.

Je, sasa Wizara haioni ni wakati muafaka Kata za Oldonyowas, Oldonyosambu, Mwandet, Laroi, Oljoro na Bwawani kupata mgao wa minara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba Watanzania hawapandi kwenye miti, hawapandi kwenye vichuguu ili kupata huduma ya mawasiliano na ndiyo maana Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan inajitahidi sana kutafuta fedha ili kuhakikisha kwamba inatatua changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipengele cha pili cha swali la Mheshimiwa Mbunge, ili kufikia kwenye miradi kutangazwa na zabuni kupatikana hatua ya kwanza tunaanza na kufanya tathmini ili kujiridhisha tatizo likoje, tunafanya feasibility study, baada ya hapo tunafanya detailed design na baada ya hapo tunakuja kutangaza tender, sasa hatua ambayo imefikiwa ambayo Mheshimiwa Mbunge ameiongelea ni hatua ya kusaini Mkataba ambapo tayari pesa zimeshaelekezwa katika maeneo maalum.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge jambo moja kwamba, Serikali tayari imeshapata fedha kwa ajili ya kufanya tathmini katika maeneo yake na tukishakamilisha na fedha zikapatikana, basi tutatangaza tender kwa ajili ya kufikisha huduma ya mawasilino kwa ajili ya wananchi wa Arumeru Magharibi, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Jimbo la Arumeru Magharibi hivi karibuni mvua kubwa zimenyesha na kuharibu miundombinu kweli kweli yakiwemo madaraja, barabara na sasa wananchi hawana mahali ambapo wanapita katika maeneo haya ambapo yalitakiwa kujengwa maradaja mapya.

Ni lini sasa Serikali itapeleka hizo fedha za dharura ambazo tumeziomba kwa ajili ya kuokoa wananchi ambao hawana jinsi ya kwenda shambani, hospitali au popote wanapohitaji kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mollel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa sasa kupitia Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) inaangalia namna ya kupata fedha za ziada za dharura. Bajeti ya TARURA kwa ajili ya dharura kwa mwaka ni shilingi bilioni 11. Kama nilivyosema hapo awali, tayari Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Kairuki, ameshakaa na Waziri wa Fedha kuona ni namna gani TARURA inaweza ikaongezewa fedha za dharura kwenda shilingi bilioni 46 ili barabara hizi zilizoharibika katika kipindi hiki cha mvua ziweze kutengenezwa, zikiwemo hizi za kule Arumeru Magharibi kwa Mheshimiwa Lemburis. Pale ambapo Wizara ya Fedha itaridhia TARURA kuongezewa fedha hii, basi barabara hizi zitaanza kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, nimalizie tu kwa kusema kwamba tunakwenda kuanza kutekeleza mwaka mpya wa fedha mwezi mmoja na siku kadhaa zijazo (mwezi Julai), hivyo basi, wataona barabara hizi zitengenezwe katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa, mnada huo hakuna choo, hakuna maji na wananchi wanapeleka mifugo yao mara kwa mara pale na mnakusanya fedha nyingi pale. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kuchukua hatua ya dharura kujenga choo na kupeleka maji pale ikisubiria mpango mkubwa?

Swali la pili, je, kwa kuwa mnada huo pia Wizara ndiyo inakusanya fedha, kwa nini fedha hizo ambazo mnazikusanya isitumike kwa ajili ya kukarabati mnada huo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, jambo la kwanza tukiri changamoto ambazo Mheshimiwa Mbunge amezieleza na akiwa anahitaji hatua za dharura. Nimuondoe shaka kwamba hizo hatua za dharura kwa mahitaji hayo kama ya vyoo pamoja na maji basi tutawaelekeza wataalamu katika maeneo hayo waweze kuyafanyia kazi haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, pili kuhusu makusanyo ya fedha ambazo zinakusanywa pale kwamba ndiyo zifanye ukarabati, nimwambie tu kwamba mnada ule unahitaji ukarabati mkubwa na ndiyo maana tunataka tufanye tathmini na tuujenge kwa viwango ambavyo vinastahili. Kwa hiyo tutalietekeleza hili kama ambavyo Serikali imepanga katika mipango yake, ahsante. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, je, lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye Kata za Bwawani, Bangata, Kidina, Otoroto na Kimnya kwenye Jimbo la Arumeru Magharibi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu kuweza kuona kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya hivi ndani ya jimbo lake na pale ambapo fedha imetengwa tutahakikisha inaenda mara moja kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo hivi vya kata.

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa, barabara hii inahudumia mikoa mitatu Arusha, Manyara na Dodoma. Je, Serikali haioni sasa ni muhimu kuharakisha barabara hii ili kujenga uchumi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, kwa kuwa barabara hii iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025, Serikali haioni kutoharakisha barabara hii ni kutotekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, ni kweli barabara hii iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini pia ni kweli inaunganisha Mikoa mitatu, kwa maana hiyo ndiyo maana katika jibu langu la msingi hii barabara imetengewa fedha na tumeipitisha inaanza kujengwa kwa EPC+F na kama nilivyosema tutaisaini kuanza ujenzi wa barabara hii kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha kwa mwaka huu, kwa maana ya huu mwezi Juni. Ahsante. (Makofi)

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, eneo linalotumiwa na Kituo Kidogo cha Polisi cha Ngaramtoni linatumiwa tangu mwaka 1984 ambalo liko chini ya Wizara ya Kilimo; je, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, haioni ni vizuri sasa wakaomba eneo hilo ili waweze kurasimishiwa moja kwa moja badala ya kusema hawana eneo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa Jeshi la Polisi ndiyo limepewa mamlaka ya kuangalia raia na mali zao: Je, Serikali inaona ni vizuri Askari kukaa kwenye makuti bila nyumba wala Kituo cha Polisi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA, NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mambo ya Ndani kuzungumzia suala ambalo limetengwa kwa ajili ya shughuli za kilimo na sasa limekosa kibali cha watu wa Polisi kujenga, mazungumzo yanaendelea kati ya Wizara hizi mbili ili kupata kibali cha kuhalalisha hilo eneo ili liweze kujengwa Kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili eneo la usalama wa mali za wananchi, Polisi wanatambua umuhimu mkubwa kabisa wa usalama wa wananchi na mali zao, na hivyo basi ndiyo maana msukumo wa mazungumzo unaendelea kati ya hizi taasisi mbili ili kuweza kuhalalisha hiyo eneo na badae kujenga kwa ajili ya usalama wa wananchi.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nilitaka tu nimshauri Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru wakakae na Halmashauri yao watafute eneo. Eneo la Wizara ya Kilimo linatumika kwa ajili ya wafanyakazi wa utafiti na pale tuliwapa hifadhi ya muda, watafute eneo lingine. Wizara haitatoa kipande cha ardhi cha uzalishaji wa mbegu. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimia Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa mradi huo umechukua muda mrefu na sasa wananchi wanakunywa maji ya floride na wanazaliwa watoto wenye vichwa vikubwa, vibiongo na miguu kupinda. Je, Serikali haioni sasa kufanya haraka kwa ajili ya kukamilisha mradi huo?

Swali la pili, je, Naibu Waziri wa Maji baada ya Bunge hili atakuwa tayari kwenda kukagua mradi huo ili kujionea hali halisi ya wale wananchi wanavyoteseka?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saputu kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mradi tumeweka nguvu kubwa lakini tumekusikia Mheshimiwa Mbunge tutaongeza nguvu.

Swali la pili kukagua mradi mara baada ya Bunge hili Mheshimiwa Mbunge unafahamu nilishakuja Jimboni kwako hivyo sitasita kufika tena kuhakikisha huduma ya maji inapatikana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza; kwa kuwa mnada wa Upili wa Olokii miundombinu yake imeharibika sana, mizani imekufa, hakuna maji na Wizara ndio inakusanya fedha zote katika mnada huo wa Upili.

Ni lini Serikali itakarabati mnada huo ili kuhakikisha kwamba huduma nzuri na bora inapatikana kwenye mnada huo wa Olokii? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, Serikali kwenye bajeti ya mwaka ujao imetenga shilingi bilioni 21.2 kwa ajili ya kukarabati minada yake ya Upili na minada ya mipakani yote, ili kuweza kuwarahisishia wafugaji ambao wanapeleka mifugo yao kwenye minada hiyo. Kwa hiyo, miongoni mwa mnada ambao Mheshimiwa Mbunge anausema utafanyiwa ukarabati kupitia bajeti hii. (Makofi)