Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Innocent Lugha Bashungwa (41 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nianze kwa kukupa pole sana kwa changamoto ulizokumbana nazo lakini hata mimi nimekuwa na siku ngumu leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwanza kwa kuwashukuru wananchi wangu wa Karagwe kwa kuniamini na kunituma katika nafasi hii ya uwakilishi hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nitumie nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais Magufuli na Serikali yake kwa kuanza kwa jitihada kubwa sana kutekeleza kaulimbiu ya „Hapa Kazi Tu‟.
Watanzania wengi wanamuunga mkono Mheshimiwa Rais na Serikali yake katika jitihada zake za kuhakikisha tunabana matumizi yasiyokuwa ya lazima ili fedha iende kwenye miradi ya maendeleo ya kuwasaidia Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili kuna jambo la ufisadi ambalo linaendeshwa kwa hii style ya operation tumbua majipu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais na kumwombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kuwa na moyo huu kwani kwa kuziba mianya ya upotevu kwa pesa sasa itakwenda kwenye huduma za jamii, wananchi wa Tanzania wapate dawa hospitalini na shule zetu ziwe na elimu bora na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitolea mfano wa Jimbo langu la Karagwe mpaka hivi sasa development grant hatujapata hata shilingi moja. Kwa hiyo, ni matumaini yangu katika jitihada hizi za kubana matumizi na kupambana na ufisadi ili hizi fedha ziende kwenye miradi ya huduma za jamii hata Jimbo langu la Karagwe mtatuangalia kwa jicho la huruma. Kwa sababu tumefikia katikati ya mwaka wa fedha lakini development grant hatujapata hata shilingi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamkumbuka Mheshimiwa Rais, wakati wa kampeni lile tukio la kihistoria la push ups lilitokea Karagwe kwenye viwanja vya Kayanga. Wanakaragwe wanamkumbuka sana na wana imani na Mheshimiwa Rais. Katika kampeni Mheshimiwa Rais aliahidi Wanakaragwe kwamba tutashirikiana kutatua mradi wa maji kwa sababu sehemu nyingi maji ni tabu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa maji wa Lwakajunju, ahadi hii imekuwa ni kiporo cha miaka mingi. Mheshimiwa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete aliahidi kwamba atawasaidia Wanakaragwe kuondokana na adha ya maji kwa kutoa maji Ziwa Lwakajunju lakini kwa miaka yote kumi mradi huu haukutekelezwa. Mheshimiwa Rais Magufuli alivyokuja kwenye kampeni Karagwe aliahidi kwamba akiwa Rais huu mradi wa maji wa Lwakajunju utatekelezwa haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais Magufuli aliahidi kwamba barabara ya Nyakahanga - Chamchuzi itapandishwa kwenye kiwango cha TANROADS na iwekwe kwenye mpango wa kuwekwa lami kwani kule Chamchuzi kuna ziwa ambalo linatutenganisha na Rwanda. Baada ya kuiweka barabara hii kwenye mpango wa TANROADS, Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba tutaweka kivuko ili kuboresha biashara kati ya sisi na wenzetu wa Rwanda.
Pia katika ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa wananchi wa Karagwe ipo Hospitali ya Wilaya. Karagwe hivi sasa ina wananchi shilingi 355,000/= na takwimu zinaonyesha kwa mwaka tunakua kwa wastani wa watu shilingi 10,000/=. Bila Hospitali ya Wilaya na hii idadi ya watu, kwa kweli tunapata adha kubwa sana. Tunaendelea kutegemea hospitali ya Kanisa la Lutheran, tunawashukuru sana lakini na wao wanaelemewa kwa hii idadi ya watu na ambao tunakua kwa wastani wa watu shilingi 10,000/= kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ahadi za Mheshimiwa Rais kuna suala la bei la kahawa. Napenda kuishukuru Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri Mwigulu kwa kukaa na Wabunge wanaotoka kwenye mikoa inayozalisha kahawa ili tuanze mchakato wa kupunguza hizi kodi ambazo ni kero kubwa kwa Watanzania wanaolima kahawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika ahadi za Mheshimiwa Rais lipo suala la kutatua migogoro ya ardhi. Napenda kutumia nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Lukuvi kwa kuanza vizuri kushirikiana na sisi kuhakikisha tunatatua migogoro ya ardhi. Katika hii awamu ya kujitahidi kuwa na uchumi wa viwanda, viwanda hivi havitajengwa kwenye sky, vitajengwa kwenye ardhi na ni vizuri tukatatua migogoro hii ili kuweza kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji wa ndani na nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ina upungufu wa walimu wasiopungua 400 hasa hasa wa shule za misingi. Naamini Waziri wa Elimu yumo humu ndani na kilio cha Wanakaragwe anakisikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kutumia nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kusambaza umeme vijijini. Wilaya ya Karagwe imepata umeme huu wa REA lakini kuna vijiji vingi bado havijapata. Naamini Serikali itajitahidi ili wale wananchi ambao hawajapata umeme katika Wilaya ya Karagwe nao wapate ili ahadi ambazo tumeahidi wakati wa kampeni ziweze kutekelezwa kwa muda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kushauri Serikali, kuna mfuko wa Halmashauri wa kukopesha vijana na akina mama. Kwa ninavyoona, tutafute namna ya kukuza mfuko huu ili uweze kukopesha vijana na akina mama zaidi kwani kama mnavyofahamu tatizo la ajira kwa vijana na akina mama ni la kitaifa na kwa kukuza mfuko huu wa Halmashauri tutakuwa tumewasaidia vijana wengi kujiajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia kero za Karagwe. Sasa niende kwenye machache ya kuishauri Serikali katika jitihada zake za kujenga uchumi wa viwanda. Pamoja na jitihada za kupambana na ufisadi ili kukuza mapato ya ndani ya nchi, hii peke yake haiwezi kutosha hata tukitumbua majipu namna gani. Lazima Serikali ijipange katika kuhakikisha tunajenga miundombinu ambayo itasaidia kukuza sekta binafsi lakini wakati huohuo itasaidia nchi yetu kupata kipato zaidi. Kwa mfano tuna natural harbors, hizi bandari tukiziboresha na zikawa efficient, landlocked countries ambazo zinatuzunguka zitaweza kupitisha cargos zao nyingi na tutaweza kupata mapato kwa njia ya customs. Hiyo itakuwa ni income lakini kwa wakati huohuo itakuwa imejenga miundombinu ya kusaidia sekta yetu binafsi ikue.
Mheshimiwa wenyekiti, pia ipo haja ya kujenga reli nchini na kuunganisha na nchi za jirani ili kukuza biashara na uchumi wetu. Kama takwimu za TRA zinavyoonyesha, mapato makubwa tunayapata kupitia customs. Kwa hiyo, ujenzi wa bandari na reli siwezi kusisitiza vya kutosha namna ambavyo tukizijenga pamoja na kwamba zipo capital intensive, zitatusaidia sana kukuza mapato, kuongeza tax base ili hii flow ya income kupitia customs iweze kukua kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu nia ya Serikali ya kuwa na uchumi wa viwanda. Napenda kutoa angalizo. Ukiangalia takwimu za mwaka jana kwa ukuaji wa sekta, sekta ya mawasiliano ilikua kwa 15.3%, sekta ya ujenzi ikakua kwa 13%, huduma za fedha 9.9%, usafirishaji 8.8%...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge ahsante, muda wako umekwisha.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mnafiki, tena mnafiki sana nisipoanza kwa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais na Baraza lake la Mawaziri kwa kuendelea kuchapa kazi kwa bidii na kwa weledi mkubwa na wananchi wa Tanzania wana matumaini makubwa sana na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimepitia Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa „A‟ mpaka „Z‟, pia nimesoma Hotuba ya Upinzani maoni yao juu ya Mpango huu, kitu cha kusikitisha hotuba ya Mheshimiwa David Silinde rafiki yangu, yeye kama Msemaji Mkuu wa Upinzani, Nasikitika sana hotuba yake imetumia takwimu za kupotosha Bunge lako Tukufu na Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda ukurasa wa tatu wa hotuba ya Kambi ya Upinzani juu ya utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano, kwa kutolea mfano, kuna sentensi inasema takwimu za Wizara ya Fedha zinaonesha kuwa kwa kipindi cha miaka mitano fedha ambazo zimetolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ni wastani wa asilimia 26 tu, hiyo tunazungumzia historia. Watanzania wanataka kujua tunapokwenda mbele tumejipanga vipi? Ukiangalia Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa miaka mitano ijayo tunatoka kwenye hii asilimia 26 kwenda asilimia 40 ya bajeti ya maendeleo imetengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika hotuba hii, kwa mfano, Kambi ya Upinzani wanadai kwamba Mpango wa Maendeleo wa Kwanza na huu wa Pili umeasisiwa na Benki ya Dunia, Shirika la Fedha Duniani na wahisani. Hii siyo kweli, mpango huu uliletwa Februari, 2016 katika Mkutano wa Pili tukaujadili, maoni na mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge yameingizwa katika Mpango huu wa Pili ambao uliwasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha hapa jana. Kwa hiyo, siyo kweli kwamba mpango huu unaasisiwa na Mashirika ya Kimataifa, huo ni upotoshaji kwa Bunge lako Tukufu na Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninashangaa sana ndugu zetu wa Upinzani kule kuna wasomi wengi tu nawajua, lakini nashangaa katika hotuba yao kuna mapendekezo kwamba Mpango huu utengenezewe sheria. Mimi sijawahi kuona Mpango unatengenezewa sheria kwa sababu sheria iko fixed Mpango ni dynamic. Sasa ukitunga sheria kwa Mpango ambao uko dynamic ina maana kila mwaka tutakuwa tunatunga sheria ya kutekeleza Mpango, hiyo inawezekana kweli? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitaalam Mpango unakuwa na monitoring and evaluation framework, kazi yetu kama Bunge ni kuishauri na kuisimamia Serikali, baada ya kuupitisha huu Mpango wa miaka mitano kazi yetu ni kila mwaka tunaletewa taarifa ya utekelezaji, tunapitia na kuangalia kama utekelezaji wa kila mwaka unaendana na Mpango wa miaka mitano, lakini siyo kusema tutunge sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda ukurasa wa nne pia kuna upotoshaji mwingine wa takwimu. Paragraph ya mwisho inasema Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kulithibitishia Bunge hili na wananchi kwa ujumla kama shilingi 4,970.04 kwa siku zinatosha kuhudumia familia nzima. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri haijasema familia nzima, imesema income per capita, wastani wa pato la mwananchi, sasa humu wanatuletea taarifa za eti pato la familia, mmeitoa wapi hii? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa tano, deni la Taifa ukiangalia takwimu toka National Bureau of Statistics na Wizara ya Fedha, Deni la Taifa sasa hivi liko 20.9% na maximum debt sustainability threshold ni asilimia 50 ya GDP. Kwa hiyo, tukisema kwamba Deni la Taifa siyo stahimilivu hizo takwimu tunazitoa wapi na wakati nchi yetu ina takwimu ambazo tunazitumia hizi hapa? (Makofi)
Pia ukiangalia katika debt sustainability threshold pia kuna kuangalia asilimia ya deni as percentage ya total export. Takwimu zinaonesha ni asilimia 104.4 na ukomo ni asilimia 200, sasa hii hatari inatoka wapi Waheshimiwa Wabunge?
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda ukurasa wa nane, kushuka kwa thamani ya shilingi. Mimi nashangaa hapa kuna hoja kwamba kushuka kwa thamani ya shilingi kutaathiri utekelezaji wa maendeleo, sijui ni logic ya wapi.
Ninavyofahamu kama nchi ikikopa kwa ajili ya miradi ya maendeleo tunakopa kwenye dola. Dola ikija hapa nchini inaweka pressure kwenye shilingi, kwa hiyo, shilingi inapanda against dola, sasa ukisema kwamba kushuka kwa shilingi kutaathiri maendeleo pia sioni logic. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilichotegemea katika hotuba hii ya Kambi ya Upinzani ni kuuleta mpango mbadala kwamba Mpango wa Miaka Mitano mliouleta siyo mzuri, mzuri ni huu hapa ndiyo tuuangalie lakini siyo kuleta taarifa ambazo zinapotosha umma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuchangia kuhusu upotoshaji wa takwimu, hii inanikumbusha wakati niko chuo, Profesa wetu wa Statistics...
KUHUSU UTARATIBU
MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu....
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa siikubali kwa sababu tukisema kila mwaka tuwe tunaletewa sheria ambazo tunazipitia kwanza ni utumiaji mbaya wa fedha za umma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya muda sasa naomba niende kwenye ushauri juu ya Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Karagwe ni sehemu ya nchi na pia linastahili kuwekwa katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Karagwe tuna tatizo kubwa la maji na Mheshimiwa Rais Mstaafu, Jakaya kikwete aliahidi mradi wa Lwakajunju, naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano imeniahidi kwamba katika kipindi cha miaka mitano itahakikisha mradi huu unatekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa jiografia ya Karagwe tuna miji mikubwa mitano ya Afrika Mashariki inayotuzunguka, ninaiomba Serikali katika Mpango wa Miaka Mitano watujengee barabara ya kuanzia Nyakasimbi kwenda Nyakakika, Nyabionza, Kibondo, Kiruruma mpaka Rwabwele, kwa sababu barabara hii itafungua fursa za kiuchumi kwa wananchi wa Karagwe na Kyerwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Mpango wa Miaka Mitano napenda kuiomba Serikali iweke mpango wa kujenga hospitali ya Wilaya kwa sababu sasa hivi tunagemea hospitali ya kanisa la ELCT ya Nyakahanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia pia kuhusu umuhimu wa kujenga reli ya Kati ambayo itatuunganisha na nchi za jirani ili tuweze kutumia bandari zetu na reli yetu kupata mapato kupitia customs.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni la muhimu sana na ninawaunga mkono Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kuchangia katika kusisitiza umuhimu wa kujenga reli ya Kati na reli ambayo itatuunganisha na nchi za jirani ili iweze kutusaidia katika kukuza uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili, ili Serikali isiendelee kukopa sana ninaishauri Serikali iangalie mikakati ya kupata wawekezaji kupitia PPP framework na pia kuangalia ni namna gani tunaweza tukakopa kwenye International Capital Markets badala ya kuweka pressure ya kukopa ndani na kukopa kwenye soko la nje ambalo riba zake ni za gharama.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera hatuna Chuo cha VETA napenda kuiomba Serikali katika huu Mpango wa Miaka Mitano pia waweke mpango wa kujenga chuo cha VETA katika Mkoa wa Kagera.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia asilimia kubwa ya Watanzania wako kwenye bottom of pyramid, inabidi mpango wa Serikali wa viwanda uangalie zile sekta ambazo zinaajiri Watanzania wengi kama sekta ya kilimo. Tuwekeze kwenye kujenga value chain katika sekta ya kilimo ili iweze kutengeneza ajira kwa vijana na kukuza uchumi wa nchi.
Pia inatubidi kuwa na SME developments plan sijaona mkakati wake, kwa sababu ukiangalia kampuni za size ya kati tukiweza kuzisaidia zitaajiri watu wengi na itatusaidia kutatua tatizo la ajira kwa vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna haja ya kuunda SACCOS za vijana kwa sababu SACCOS hizi zikiwekewa mitaji zitasaidia kuwakopesha vijana ili waweze kujiajiri na kwa kufanya hivyo tutatatua tatizo la ajira kwa vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii muhimu ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Waziri Jenista na kaka yangu Mavunde kwa kazi nzuri wanayoifanya. Tunawashukuru kwa kutupa ushirikiano mzuri
katika kuwahudumia Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Magufuli, Mheshimiwa Makamu wa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi na dira ya miaka mitano ya maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mawili katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kipengele cha hali ya uchumi nchini ukurasa wa 13 mpaka 40 kuna mambo ambayo hotuba imeyazungumzia ningependa kuchangia mambo mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala; kwenye mjadala sasa hivi kuna mjadala kuhusu size ya Bajeti ya Serikali. Katika Mwaka wa Fedha wa 2016/2017, Serikali ilitenga trilioni 29.5 na katika mwaka ambao unakuja wa Mwaka wa Fedha 2017/2018, bajeti hii itapanda kutoka 29.5
kwenda kwenye trilioni 31.7.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mijadala kuhusu size ya Bajeti ya Serikali naona Serikali kwa sababu dhamira yake na nia yake ni kutatua changamoto za Watanzania kwa kasi, si mbaya kuwa na malengo marefu na kwa vile Serikali ya Awamu ya Tano tunajua ina dhamira ya kuhakikisha inatumia vizuri fedha za umma, nadhani Waheshimiwa Wabunge tujikite kwenye kusimamia kile ambacho Serikali inakikusanya kama kinaenda kwenye kutekeleza miradi ya maendeleo. Sio mbaya kuwa na malengo if you aim higher na ukaweka jitihada ya ufanya kazi ili kwenda kwenye hayo malengo mapana ni jambo la kupongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani TRA ilikuwa inakusanya takriban bilioni 800, lakini Serikali ingependa ikae kwenye kusifiwa kwamba inatimiza malengo ya kila mwezi, basi tungejiwekea target za bilioni 800, tunaendelea kupongezana kila mwezi lakini Serikali ikajipa challenge ikasema tujivute twende kwenye trilioni 1.2. Kwa hiyo, unaona kwamba ni hatua nzuri, unakuwa na malengo marefu, lakini unajitahidi kwenda kwenye hayo malengo marefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo naiona kwenye uandaaji wa bajeti ni kwamba asilimia kubwa ya Watanzania, kikundi cha wananchi ambao wako vijijini, asilimia kubwa ya wale Watanzania ni kwamba uchumi unakua lakini hauwagusi wale asilimia kubwa. Kwa mfano, katika mpango wa maendeleo wa 2017/2018 na katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukiangalia kwa upande wa kilimo kwanza kwenye ukuaji wa Sekta ya Kilimo 1.7% ni kidogo mno. Hatuwezi kuona social economic transformation kwenye Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Sekta hizi ambazo zinaajiri Watanzania walio wengi kama tutaendelea kupata ukuaji wa 1.7%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuiomba Serikali katika Bajeti za Kisekta ambazo zinakuja, tuone bajeti ya kutosha imetengwa kwa ajili ya pembejeo, tuone kuna mpango wa kupata maafisa ugani wa kutosha ili vijiji vyetu vipate maafisa ugani, tuone bajeti ya kutosha kwenye kilimo
cha umwagiliaji. Mwaka wa Bajeti wa 2017 ilitengwa hela kidogo sana kwenye kilimo cha umwagiliaji. Katika Bunge hili baada ya ukame ambao ulitupata kule Karagwe, niliomba Serikali ije kwenye kata kumi ambazo zina vyanzo vya maji tutathmini kuona kama tunaweza kufanya kilimo cha umwagiliaji, lakini mpaka hivi sasa sijapata timu ya wataalam kufanya hii tathmini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ili tuweze kwenda kwenye uchumi wa viwanda na kwenda kwenye middle income country status lazima tufike mahali tuone jitihada za kibajeti zinazolenga kutoa bajeti ya kutosha kwenye Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili Watanzania wengi hawa ambao wanajishughulisha kwenye hii sekta tuweze kuwasaidia kujikwamua kutoka kwenye umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mazao ya biashara, kodi kero 27 kwenye zao la kahawa tumeondoa kodi moja tu ya ada ya leseni ya kusindika kahawa ya dola 250 tu. Tuko kwenye rekodi, kwenye Ilani tumeahidi kwamba tutaondoa hizi kodi kero kwenye zao la kahawa. Mheshimiwa Rais alikuja Kagera akaahidi kwamba kwenye bajeti hii ya 2017/2018 tutaziondoa hizi kodi kero. Mheshimiwa Waziri Mkuu
nakushukuru ulikuja Karagwe tukaahidi lakini sijaona jitihada ya Serikali kuondoa hizi kero kwa sababu kwenye hotuba ya Waziri Mkuu hazitatajwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye kusaidia yale makundi ya wananchi ambao wako vijijini pia kuna haja ya kuangalia wajasiriamali wadogo na wa kati na kuweka mazingira wezeshi ili kuwasaidia kukua. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu inatambua kwamba 56% ya
wananchi ni nguvu kazi ya vijana, lakini kwa sababu tumekuwa na malengo ya kukusanya mapato ya kila mwezi kwa mfano, kumekuwa na aggressive behavior katika kukusanya mapato kiasi kwamba haya makundi ambayo tunategemea kuwasaidia kuwakwamua kutoka kwenye
umaskini tunajikuta zile aggressive behavior za kukusanya kodi kwa mfano upande wa bodaboda, ukija Karagwe, bodaboda awe kwenye gulio, msiba au shambani, pikipiki zinawindwa na askari wa usalama barabarani kwa sababu wana target ya mapato kiasi fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo matokeo yake unakuta badala ya kumsaidia yule kijana ambaye tumeshindwa kumpatia ajira kwa sababu tatizo la ajira ni la nchi nzima na si Tanzania tu ni Afrika na dunia nzima, wale vijana ambao wanajiajiri tunatakiwa kuwawekea mazingira wezeshi ya kukua. Kama amejiajiri kama bodaboda basi tumsaidie ili aweze kukua. Kwa hiyo, matokeo yake, kwa sababu ya target za mapato unakuta tunawaathiri yale makundi maalum ambayo tulitakiwa kuwasaidia kuwawekea mazingira wezeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa, niende kwenye changamoto zlizoko kwenye Jimbo la Karagwe na nimezileta kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ili nimwombe aweze kunisaidia yapate attention inayostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mradi wa maji wa Rwakajunju. Huu mradi ni ahadi ya muda mrefu, Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni tuliwaahidi wana Karagwe katika hii Serikali ya Awamu ya Tano tutatekeleza mradi huu. Serikali ikatenga dola milioni 30 kwenye Mwaka wa Fedha 2016/2017, lakini nashangaa kwenye bajeti ya mwaka huu 2017/2018, fedha hizi sizioni sasa sijui zimeenda wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu nakumbuka ulivyokuja karagwe tuliwaahidi wana Karagwe kwa vile zilikuwa zimeshatengwa kwenye bajeti ya mwaka uliopita, tukawaahidi pale tulikofanya Mkutano pale Kihanga tena ukamwomba Mkurugenzi wa Halmashauri aje kwenye jukwaa awaambie kwamba wananchi wa Kata ile ya Kihanga na wenyewe watapata huduma ile ya maji kutoka
kwenye mradi wa Rwakajunju. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mradi huu usipotekelezwa kwa kweli kuna hali ya hatari huko mbeleni. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu anisaidie katika hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la elimu. Naipongeza Serikali katika elimu ya bila malipo, tunakwenda vizuri na Serikali inaendelea kurekebisha pale ambapo tunakwama lakini ili tuweze kwenda vizuri, naomba Bajeti ya 2017/2018, tutenge fedha za kutosha kwa ajili ya kuajiri walimu. Wilaya ya Karagwe peke yake tuna deficit ya walimu 840 wa shule za msingi, tuna deficit ya walimu wa sayansi 96.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la afya. Katika malengo ya Serikali ya kuwa na kituo cha afya kila kata nadhani ni malengo mazuri lakini hatuwezi kuyatimiza kwa muda mfupi. Nipende kuishauri Serikali angalau tulenge kuwa na kituo cha afya kwa kila tarafa ili katika kipindi cha miaka mitano tuweze kuonesha kwamba tuna malengo ya muda mrefu lakini katika kipindi cha miaka mitano tumeweza kuwa na kituo cha afya cha kila tarafa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na migogoro ya ardhi. Pale Kihanga tulipofanya mkutano, zile hekta 2000 ambazo Mheshimiwa Waziri Mkuu alielekeza Serikali irudishe kwa wananchi mpaka hivi sasa bado. Walienda pale wakasema tunawapa hekta 2000 lakini zimelenga sehemu
ambapo wananchi tayari wanakaa, hazijatolewa kutoka kwenye ranch ya Kitengule na wenye ma-block, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu asiingilie katika hili suala ili tuweze kurudisha hekta 2000 kwa wananchi kama tulivyowaahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipo concerned sana na dhamira ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda kutokana na uzito mdogo unaopewa sekta zinazohusisha Watanzania wengi takriban asilimia 70 au zaidi. Kiasi kidogo sana cha fedha zilikuwa zikitengwa miaka ya nyuma, lakini hata hivyo zilizotolewa ni takriban asilimia 50 au chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 0.92 ndiyo imetengwa kwa ajili ya sekta ya kilimo kwa bajeti ya 2016/2017. Azimio la Maputo la kutenga asilimia 10 ya bajeti kwa ajili ya kilimo tutafika kweli kwa utaratibu huu? Ili uchumi wa viwanda tuweze kuwa nao, kama kweli hiyo ndiyo dhamira ya Serikali ni lazima tuoneshe kwa vitendo kwa kutenga bajeti ambayo itawagusa kiuchumi wananchi waliopo kwenye bottom of pyramid ya rasilimali watu na hawa ni wakulima, wafugaji na wavuvi kwa pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya kwanza na kwa kutumia bajeti ya kilimo kama kielelezo, naona malengo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano tumeanza vibaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, bilioni 100 kila mwaka kwenda TADB lazima zitengwe na zielekezwe kwenye kukopesha SME’s na ikiwezekana kwenye uwekezaji mnaongeza mnyororo wa thamani. Ila katika hili sijaona mpango mkakati wa SME development strategy inayolenga kukuza SME’s zinazojikita kwenye kilimo na mifugo – value chain. Ni lazima Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano unyambulishwe kwenye annual spectral budgets kama nilivyoeleza hapo juu, lakini kwenye hili mpango unaenda Kaskazini na bajeti ya sekta kipaumbele inaenda Kusini. Hatutafika kwa style hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa hotuba yake nzuri na iliyosheheni mipango mizuri ya uchumi wa viwanda hapa nchini. Katika hii ninapenda kusisitiza Serikali ihakikishe uchumi wa Viwanda unajielekeza kwenye kuongeza mnyororo wa thamani (value chain) kwenye shughuli za asilimia 70 ya Watanzania ambazo ni kilimo, mifugo, uvuvi na Biashara ndogo na kati (SMEs) The focus should be at the bottom of the population pyramid ndipo kuna asilimia 70 ya wananchi au zaidi. Kwa kufanya hivi uchumi wa wananchi hawa ambao karibu wote ni maskini utakuwa na malengo ya nchi yetu wa kufikia uchumi wa kati (MIC) ifikapo 2025 yatafanikiwa. Aidha, tutakuwa tumepata uchumi wa viwanda wenye tija na weledi kwa Watanzania walio wengi. Ninaomba sana Serikali izingatie ushauri huu. Ninashukuru Mheshimiwa Waziri Mwijage kwa kutambua hili katika hotuba yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Karagwe ni moja ya Wilaya nchini ambazo zinazalisha mazao mengi na kusaidia kulisha Watanzania hasa wanaoishi Mjini. Pamoja na mchango huu mkubwa wa kuzalisha kwa wingi mazao mengi hasa maharage na kahawa, sijaona Serikali ikileta wataalamu kuwapa mafunzo wakulima kuhusu namna ya kulima kwa tija na kuwasaidia mikakati ya kuwaunganisha na masoko. Kushindwa kufanya hivi kwa Serikali kumesababisha mazao kuharibika mashambani, (Post harvest loss) kwa miaka mingi kwenye Wilaya ya Karagwe na kwingineko Nchini. Je, kwa nini Serikali haijatenga bajeti ya kuwasaidia wakulima wa Karagwe na mafunzo ya kufanya kilimo cha biashara na kuwapa mikakati ya kuwaunganisha na masoko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli aliahidi wananchi wa Kagera kwamba Mkoa utajengwa uwanja wa Kimataifa kwenye eneo la Omukajunguti lakini katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mwijage sijaona wala kusikia fedha zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza ahadi hii ya Serikali ya Awamu ya Tano.
Aidha, sambamba na hii ahadi ya Mheshimiwa Rais, pia wananchi wa Kagera waliahidiwa na Mheshimiwa Rais Special Economic Zone (SEZ) sambamba na mipango ya uwanja wa ndege wa Kimataifa. Mkoa wa Kagera kijiografia umezungukwa na Miji mikubwa ya Afrika Mashariki ambayo kuwepo kwa SEZ na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa utakuza biashara za Mkoa wa Kagera na kusaidia kukuza uchumi wa Nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mheshimiwa Waziri atakapo simama kujibu hoja za Wabunge name nijibiwe katika SEZ na uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Omukajunguti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imewaahidi wananchi wa Kagera Kiwanda cha kusindika nyama kwa miaka mingi sana. Kuna eneo kubwa lililotolewa kwenye Ranch ya RAHCO ya kitengule takribani hekta 36,000 kwa mwekezaji huyu ila hakuna uwekezaji wa kiwanda cha nyama mpaka hivi sasa. Hii haikubaliki na ni mfano mzuri wa matumizi mabaya ya ardhi. Je, kwanini Serikali inatoa maeneo kwa wawekezaji ambao ni waongopaji na wakati kuna Watanzania wanakosa maeneo ya kufanya uwekezaji katika sekta ya mifugo? Naomba tamko la Serikali juu ya uwekezaji wa Kiwanda hiki cha kusindika nyama kwenye Ranch ya Kitengule. Aidha, Mkoa wa Kagera tuna maziwa mengi sana. Tunaiomba Serikali ituletee Wawekezaji wa kujenga kiwanda cha kusindika maziwa. Jirani zetu wa Rwanda wana ardhi na hali aya hewa inayofanana na Kagera.
Rwanda inasindika Maziwa yanaitwa Nyamo UHT na yanauzwa Afrika Mashariki nzima, Iweje Kagera ambayo ina ardhi kubwa kuliko Nchi ya Rwanda na tuna rasilimali ya ardhi na hali ya hewa ya kuwezesha uzalishaji wa maziwa mkubwa tusipate wawekezaji wa kusindika maziwa? Tunaiomba Serikali iweke diary zone Mkoa wa Kagera na miundombinu stahiki iwekwe ili kuvutia uwekezaji huo. Ninaomba tamko la Serikali kuhusu hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama ya saruji Mkoa wa Kagera ni mara mbili ya gharama ya saruji Mkoa wa Dar es Salaam. Je, Serikali ina mpango gani wa kuvutia uwekezaji wa saruji kwenye Kanda ya Ziwa ili wananchi wa Mikoa ya ukanda huu wapate saruji ya bei nafuu kama wenzao wa Kanda ya Pwani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii muhimu ya sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa dhati kabisa kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Serikali kwa kazi nzuri wanayoifanya hususani katika sekta hii ya elimu. Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 tuliahidi kutekeleza elimu bila malipo na tumeona tangu Serikali ya Awamu ya Tano imeaingia madarakani Serikali inafanyakazi nzuri katika ahadi hii ikiwemo ruzuku ya kusaidia elimu bila malipo imetoka bilioni 19 hivi sasa imefikia bilioni 23, kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Profesa Ndalichako kwa hotuba nzuri na pia niwapongeze Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ikiongozwa na Mheshimiwa Peter Serukamba na Wajumbe wote kwa taarifa nzuri ya Kamati na ni matumaini yangu kwamba Mheshimiwa Waziri pamoja na Mheshimiwa kaka yangu Naibu Waziri Olenasha kazi nzuri mnayoifanya mkiweka taarifa nzuri ya Kamati na michango ya Wabunge nina imani kabisa tutaleta maboresho makubwa katika sekta ya elimu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, mimi nina mambo kama manne na muda ukiruhusu basi nitazungumzia mambo matano:

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianzie na suala la maslahi ya walimu nchini. Hapa Bungeni toka nimekuwa Mbunge tunakwenda mwaka wa tatu, katika kipindi cha maswali na majibu katika bajeti zilizopita tumezungumzia sana juu ya kero zilizopo kwenye maslahi ya walimu nchini, tumeona speed ya kutatua kero hizi haiendei katika speed ambayo inaridhisha. Moja ya changamoto ya speed ndogo katika kutatua kero za walimu nchini ni tatizo la muundo wa kitaasisi. Kuna mambo mengine ukiyafuatilia unaambiwa hili suala liko chini ya Afisa Utumishi wa Wilaya, ukitoka kwa Afisa Utumishi wa Wilaya wanasema hili liko Wizara ya Utumishi, ukienda Utumishi wanasema hili liko Wizara ya Afya. Niishauri Serikali, sina shida na structure ilivyo ya kitaasisi, lakini Serikali mtambue kwamba lazima muwe coordinated vizuri katika kuhakikisha mnatatua changamoto za sekta ya elimu nchini kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kuna walimu Karagwe na nchini toka mwaka 2012 mpaka hivi sasa hawajapandishwa madaraja, kuna walimu nchini ikiwemo Karagwe walimu waliopandishwa madaraja toka mwaka 2012 mpaka hivi sasa mishahara yao haijarekebishwa ku- reflect daraja walilopandishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna walimu ambao waliondolewa madaraja lakini mpaka hivi sasa wako kwenye daraja hilo hilo, hawajui kama watakaa kwenye daraja hilo mpaka wanastaafu; kuna walimu ambao Serikali iliwahamisha kutoka shule za sekondari kwenye shule za msingi lakini mpaka hivi sasa hawajapata stahiki zao. Kule Karagwe Serikali imetoa shilingi milioni 50 lakini mahitaji halisi ni zaidi ya shilingi milioni 400, wakati Mheshimiwa Waziri ana- wind up nitake kusikia kutoka TAMISEMI na Wizara ya Utumishi na kwa sababu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Ndalichako ndiye una dhamana ya kusimamia sera ya elimu nchini tunaomba tusikie majibu ya Serikali mmeji-coordinate vipi kuhakikisha mnatatua kero za walimu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuzungumzia ni uwekezaji katika sekta ya elimu. Wawekezaji katika sekta ya elimu ni wabia wa Serikali na ni wasaidizi wa Serikali katika kutoa huduma ya elimu nchini. Kwa hiyo, Serikali mnatakiwa muwaangalie hawa kama partners, Serikali mnatakiwa mtambue kwamba uwekezaji katika elimu is social investment siyo business as usual. Kwa hiyo kwa kutambua hilo, Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imezungumzia vizuri changamoto hii. Nipende kuomba Mheshimiwa Waziri hii perception iliyopo kwamba kuna tag of war kati ya Serikali na sekta binafsi naomba katika winding up yako uwahakikishie wawekezaji katika sekta ya elimu na Watanzania kwamba Serikali na hawa wawekezaji mko pamoja na wote ni partner katika kutoa elimu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tax payments na non- tax payments katika sekta ya elimu ambazo wote tukitambua kwamba elimu ni social investment lazima mziondoe kwa sababu hii ni social investment siyo business as usual. Kwa mfano…

T A A R I F A . . .

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimwa Mwenyekiti, taarifa ya ndugu yangu Mwambe siipokei kwa sababu Roma haikujengwa siku moja. Kama nilivyosema kwenye utangulizi wangu toka Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani tumeona jitihada nzuri zikienda kwenye kuboresha sekta ya elimu na ndiyo maana nimesema kupitia Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na Wabunge Serikali ichukue ushauri huu ili tuzidi kuboresha sekta ya elimu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye point yangu ya tatu na jambo hili nimelisikia hata kwenye taarifa ya Kamati na mdogo wangu Mlinga amelizungumza, zuio la Serikali la wanafunzi wetu kukaririshwa mimi sijaelewa mantiki yake labda Mheshimiwa Waziri wakati una-wind up nisikie rationale ya kuzuia wanafunzi wasikaririshwe ni nini, kwa sababu ukiangalia takwimu katika ufaulu zina-alarm sana, ukiangalia division zero na four asilimia isiyopungua 60 hawaendi form five na vyuo vikuu kwa sababu wanapata division zero na four kwa vile kujifunza ni building blocks na kuna baadhi ya syllabus usipozielewa syllabus zinazofuata hutazielewa vizuri. Ukizuia wanafunzi wasikariri ili waweze kujenga maarifa na weledi mzuri kabla hawajapanda darasa lingine pia ndivyo unazidi kuchangia katika kufeli kwa wanafunzi kupata division zero na four.

Kwa hiyo, ushauri wangu Serikali mkae na wadau wa elimu muangalie jinsi ya kuliweka hili vizuri kwa sababu inabidi tuhakikishe watoto wetu tunawaandaa kufaulu lakini kuwa tayari kwa ajili ya soko la ajira pale wanapohitimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili, hii asilimia 60 au zaidi ambayo inaishia form four kwa kupata division zero na division four niishauri Serikali kuwa na mkakati maalum wa Vocational Training Institutions ziweze ku-absorb vijana wetu hawa as many as possible kwa sababu tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda, tunahitaji skill set siyo mpaka mtu awe na degree, anaweza akawa ana certificate ya ushonaji, anaweza akawa na certificate ya kutengeneza grill lakini tunawaangaliaje na tuna mkakati gani ndani ya sekta ya elimu kama Waziri mwenye sera na una-coordinate vipi na Wizara nyingine kuhakikisha kuna mkakati mahsusi ndani ya Serikali wa kuhakikisha wanafunzi wetu hawa wanaopata division zero na four wanakwenda kwenye Vocational Training Institutions na pale wanapomaliza tunahakikisha tunawapa mikopo ya bei nafuu ili na wenyewe waweze kuanza maisha na kupunguza tatizo la ajira nchini na kama mnavyofahamu vijana hawa tusipokuwa na mkakati mahsusi ndipo utakuta hata uhalifu nchini unaongezeka. Kwa hiyo, nipende kuiomba Serikali, pamoja na hili suala la zuio la kukaririsha
mliangalie vizuri. Pia muangalie hawa ambao wanaishia form four tuna mkakati gani kuhakikisha wanaenda kwenye short courses, wanapata certificate na wakishapata hizo skills tunawasaidiaje kupata mikopo ya bei nafuu ili waweze kujikimu na maisha. (Makofi)

Jambo la nne sasa niende Jimboni kwangu Karagwe. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana nilivyokuja kwako nilikwambia kwamba Karagwe wakati naingia kama Mbunge tulikuwa hatuna hata A-Level moja, ulinisaidia sasa hivi tumejenga mabweni mawili pale Bugene Sekondari, A- Level imeanza, sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri jiografia ya Karagwe ilivyo nimeshakuomba kwamba tusaidie tupate A-Level tatu, Nyabihonza Sekondari imezungukwa na Kata Nane ambazo hazina A-Level kuna mrundikano mkubwa sana wa wanafunzi sasa hivi Bugene Sekondari kwa sababu kwanza miundombinu bado ni michache lakini Wilaya yangu nina wananchi zaidi ya 360,000 na asilimia kubwa ya Taifa hili ni vijana.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba Bugene sekondari tusaidie ikamilike iwe full-fledged A-Level lakini wakati unafanya hivyo pia nisaidie Nyabihonza Sekondari, Nyakasimbi Sekondari na Kitundu Sekondari na zenyewe zikamilike ili ziweze kusaidia na Wilaya ya kaka yangu Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Wilaya ya Kyerwa, Wilaya ya Ngara tuwe tuna A-Level ambazo zitakuwa zinasaidia hii elimu bila malipo ambayo Serikali imeanzisha, wale watoto wakienda sekondari tuwe tuna A-Level ndani ya Mkoa ambazo zitasaidia kuandaa Taifa la kesho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, point ya mwisho ni Sheria ya Elimu Namba 25…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mapendekezo ya bajeti mwaka wa fedha wa 2018/2019. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na Serikali kwa ujumla, tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais katika Wilaya ya Karagwe, tunashukuru sana kwa bilioni 70 ambazo Serikali ime-commit katika bajeti hii ya 2018/2019 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa Rwakajunju, mradi ambao wananchi wa Karagwe wameusubiri miaka mingi sana, kwa hiyo tunamshukuru sana Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishukuru Serikali kwa kutusaidia kupata Kituo cha Afya cha kisasa pale Kayanga na nashukuru Serikali kwa commitment ya kujenga kituo cha afya kingine katika Kata ya Nyaishozi, Kituo cha Afya cha Nyakayanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na Watalaam wa Wizara kwa kutuletea mapendekezo ya bajeti ambayo kusema ukweli ni improvement ya bajeti zilizopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zipo na ndio maana tumekaa kama Bunge kuchambua mapendekezo haya na kuboresha na ni matumaini yangu kwamba, Mheshimiwa Waziri Mpango kwa kuanza mapendekezo ya Kamati ya Bajeti ni mazuri sana tunawapongeza sana Kamati ya Bajeti kwa mapendekezo mazuri. Kwa hiyo, naamini sana Mheshimiwa Dkt. Mpango akichukulia mapendekezo ya Kamati ya Bajeti kama msingi akaongezea na haya ambayo tunashauri, naamini kabisa tutapitisha bajeti ambayo ina weledi mkubwa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimimwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nina machache ya kuchangia. Nianze kwa kusisitiza sana Serikali, hii ni bajeti ya fiscal year ya nne tangu Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani. Tumekuwa tukilia sana kuhusu suala la stahiki za Walimu. Kuna Walimu wamemaliza toka mwaka 2015 mpaka sasa hivi hawajapata ajira na hawajapata ajira si kwamba shule zetu hayahitaji Walimu, kuna upungufu mkubwa wa Walimu katika mashule yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha akae na wenzake katika Serikali waliangalie hili kwa umuhimu wake na kwa manufaa ya watoto wetu ambao ni kizazi cha ni Taifa la kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Walimu ambao walipandishwa madaraja toka mwaka 2012, lakini mpaka sasa hivi mishahara yao haijarekebishwa ku-reflect yale madaraja ambayo wamepanda. Kwa hiyo, kiujumla changamoto ya upungufu wa watumishi ipo hata upungufu wa Wauguzi katika vituo vyetu vya tiba. Serikali wanafanya kazi nzuri ya kuweka miundombinu ya vituo vya afya, hospitali na zahanati, lakini itakuwa haina maana kama tunakuwa tuna majengo mazuri lakini hayana Wauguzi kwa ajili ya kuhudumia Watanzania. Kwa hiyo, hili naomba pia naomba waliweke katika vipaumbele vya mwaka huu wa bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia ni hili suala zima la takwimu ambazo Mheshimiwa Waziri kila mwaka wa fedha akisoma wastani wa kipato cha Mtanzania na uhalisia wa mtaani unaona kuna ukakasi. Sishangai na nitasema kwa nini. Ukiangalia mapendekezo ya bajeti hii ya 2018/2019, Serikali imefanya kazi nzuri katika kuhakikisha upande wa yule mpokea malighafi kwa maana ya msindikaji au manufacturing wameweka unafuu mkubwa sana na ndio maana tunapendekeza bajeti hii ni mwanzo mzuri wa kusaidia nchi kwenda kipato cha kati kupitia uchumi wa viwanda, kwa hiyo ni hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwaombe Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu yao, waangalie hii 67% ya Watanzania ambao ni wakulima, wafugaji, wavuvi na hawa Machinga na Mamalishe hiyo ndio component kubwa. Kwa hiyo, unafuu wakiukita kwenye hiyo asilimia 67 ya Watanzania ile tunayoita source economic transformation tutaiona kwa haraka sana, lakini tukiendelea hivi hii asilimia
33 ambayo sana sana ambayo ni trade sector, manufacturing na service sector, sawa na yenyewe ni component muhimu, lakini, component hizi mbili kwa upande mmoja mkulima, mfugaji, mvuvi na mfanyabiashara mdogo mdogo machinga, mamalishe tukiweza kuwa-align vizuri na ile component ya ambayo ina receive kile kinachotengeneza yaani malighafi kwenda kwenye manufacturing sector tutakuwa tumefanikiwa kama nchi na tutainua Watanzania kutoka kwenye umasikini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza kwa sababu wameshaandaa kama ilivyo sasa hivi na improvement itakuwa ni incremental, sasa nishauri angalau mwaka huu wa fedha waangalie yale mazao matano tuliyoyafanya kipaumbele, waangalie namna gani tutamsaidia mkulima wa haya mazao matano angalau hii disposable income yaani kuanzia tarehe Mosi Julai, mwezi unaokuja tutakapoanza kutekeleza hii bajeti aanze kuona impact ya moja kwa moja kwenye kipato chake cha mfukoni. Tukifanya hivyo wakati Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anasoma bajeti ijayo wastani wa kipato cha kila Mtanzania hatapata ukakasi ambao anaupata sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie informal sector, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wamekuwa wakiizungumzia sana, lakini naona bado iko changamoto ya namna gani tunafanya kui-tap ili iweze kuwa sehemu ya formal sector. Sasa nimezungumzia changamoto za Machinga, Mamalishe, Wafanyabiashara wadogo wadogo hawa wote wapo kwenye hii informal sector. Hii ni potential ya kuongeza kwenye tax base ambayo bado iko null. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia jinsi Tanzania bado tuko chini ya viwango vya kimataifa, ukichukua ratio ya tax collection as percentage ya GDP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili tuweze ku- broaden tax lazima tufike mahali hii informal sector ikiwezekana ndani ya Serikali kuwe na chombo maalum cha kuihudumia ikiwezekana hata Wizara, kwa nini, kwa maana hii ni asilimia kubwa ya Watanzania. Ukienda kwenye miji, ukienda kwenye mitaa kule vijijini akimama wanafanya kazi kwenye jua kali, wana familia zao kupitia kwenye vipato hivi vidogo wanasomesha watoto, wanatibu familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini kama Serikali tusifike mahali angalau kila halmashauri kunakuwa na mkakati maalum wa kuhakikisha hawa akinamama wanaofanya biashara ndogo ndogo barabarani tunawawekea miundombinu na kupitia miundombinu hiyo sasa tunawaingiza kwenye formal sector hata Serikali itapata mapato lakini wanyonge hawa nao wataweza kujikwamua kutoka kwenye umaskini. Kwa hiyo, ifike mahali Serikali iangalie hii informal sector ikiwezekana kuundwe chombo maalum ikiwezekana hata Wizara kwa ajili ya kushughulika na changamoto zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie changamoto ambayo ipo kwenye zao la kahawa. Natoka Mkoa wa Kagera, tunazalisha kahawa kwa wingi na tunachangia asilimia kubwa sana katika uzalishaji wa kahawa hapa nchini. Tumesema hapa Bungeni kwamba, stakabadhi ghalani kuna potential kubwa ya kumsaidia mkulima wa kahawa kutoka kwenye umaskini, lakini matayarisho bado kuna walakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, hivi sasa kule Kagera na maeneo mengine nchini msimu wa kahawa umeshaanza, lakini sasa hivi mwananchi akipeleka kahawa kwenye Vyama vya Msingi, kwenye risiti anaandikiwa kilo lakini haandikiwi bei ambayo ameuzia. Kwa hiyo, napenda kuomba Serikali huu mfumo wa stakabidhi ghalani walichukulie kama yai kwa sababu usipokwenda vizuri huko mbeleni kuna hatari kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wananchi wakulima wa Tanzania wanategemea mazao haya ya biashara katika kujikwamua katika umasikini. Kwa hiyo, zao la kahawa naomba waliangalie kwa umakini mno, waende vijijini waangalie changamoto za wakulima wa kahawa na Serikali waweze ku- intervene ili stakabadhi ghalani iweze kumsaidia mkulima wa kahawa kweli. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nikushukuru wewe Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa nafasi, ili niweze kuchangia hoja zilizoko mbele yetu. Kwanza nianze kwa kupongeza, niungane na waliokwishazungumza kupongeza Wenyeviti wa Kamati zote mbili kwa taarifa nzuri. Nawapongeza Wenyeviti hawa pamoja na Waheshimiwa Wabunge wa Kamati hizi kwa maoni na ushauri waliotupa na tunawaahidi tutaufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali anayoiongoza pamoja na Watanzania tunafanya kazi usiku na mchana kujenga uchumi wa viwanda. Na ukiangalia takwimu tunaenda vizuri, lakini wapo wachache wanazungumza kwa ujumla na statement zao zinapotisha dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mchango wa Mheshimiwa Lema; pamoja na mchango wake maana ameuzungumza kwa ujumla kwamba, utawala bora na sekta ya viwanda na biashara viko-linked na hajatumia takwimu katika kueleza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia nianze na takwimu ya Rand Merchant Bank ya Afrika Kusini kwenye ripoti ya mwaka jana mwaka 2019, Ripoti ya Where to Invest in Africa, Tanzania tumechukua nafasi ya saba kati ya nchi 54 Afrika ikiwa ni nchi yenye, best nation ya investiment, Tanzania tumechukua nafasi ya saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msisitizo nisome kipengele ambacho kinaisema hii Tanzania, kinasema hivi kwenye hii ripoti, “in the ranking Tanzania maintains the 7th position as the most attractive country to invest in the continent with a score of 5.57 in 2018 against a score of 5.59 in 2017.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiangalia FDI nchini zinaongezeka, lakini ukiangalia takwimu pia za UNCTAD FDI flows mwaka 2018 hapa Tanzania zilikuwa ni US Dollar milioni 938 na mwaka jana ikapanda kwenda bilioni 1.1 sawa na ongezeko la asilimia 17.3. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Lema anavyosema kwamba, wawekezaji hawaji nchini kwa kweli, ni jambo la kupotosha. Niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge statement tunazozitoa kama hazina takwimu ambazo ni official tunajiharibia sisi wenyewe kwa sababu, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli na Watanzania tunafanya kazi kwa bidii sana kujenga uchumi wa viwanda kwa hiyo, ni wajibu wetu sote kuhakikisha tunasemea mazuri na jitihada nzuri ambazo Serikali inazifanya, ili kuendelea kuvutia uwekezaji, lakini tunaenda vizuri Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ningependa kutaja takwimu chache tu zinazoonesha namna tunavyoenda kwenye sekta ya ujenzi wa uchumi wa viwanda. Mchango wa Sekta ya Viwanda kwa ajira nchini, mwaka 2015 mchango wa sekta ya viwanda ilikuwa ni 8%, lakini hivi sasa imepanda kuwa 12.5 na malengo ya Serikali ni kufika mwaka 2025 mchango wa sekta ya viwanda kwa ajira uwe ni 20%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ukiangalia mchango wa manufacturing sector mwaka 2015 ilikuwa ni 5.5%, lakini hivi sasa imepanda ni 8.3%, lakini ukiangalia mchango wa ujenzi wa uchumi wa viwanda kwa ujumla wake, yaani in aggregate terms, mwaka 2015 mchango wa sekta ya viwanda ilikuwa ni 21.1% na hivi sasa ni 23.7% na ukiangalia mikakati ya kujenga miradi ya vielelezo hasahasa kwenye uwekezaji mkubwa ambao nchi yetu inafanya kwenye sekta ya miundombinu takwimu hizi zitaongezeka kwa sababu, miradi hii itachochea ukuaji wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaenda vizuri kwenye ujenzi wa sekta ya viwanda na tuendelee kushirikiana kusemea mazuri haya, ili kuendelea kuvutia uwekezaji na kuwapa moyo wale wawekezaji ambao tayari wako hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Development Budget. Bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara ni bajeti ya Serikali nzima, yaani trilioni 33.1 tulizopitisha kwenye mwaka huu zote zinaenda kwenye kujenga uchumi wa viwanda.

Kwa hiyo, tunakosea pale tunapoangalia ile Development Budget ambayo iko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, yani kama sekta kwamba, ndio Development Budget kwa sababu, ili uweze kujenga uchumi wa viwanda sekta zote, zile sekta ambazo ni za huduma za jamii, zile sekta ambazo ni za uzalishaji, zote kwa pamoja zinaungana kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara yangu pamoja na kwamba, bajeti ya maendeleo bado tunaendelea kupokea kwa mwaka wa fedha huu tunaotekeleza, lakini hata zile trilioni 4.9 ambazo ziko kwenye Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano zile na zenyewe ni sehemu ya mchango wa sekta ya viwanda kwa hiyo, tunaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni kwenye Maoni na Mapendekezo ya Kamati wamesisitiza sana kulinda viwanda vya ndani. Serikali tunafanya jitihada kupitia kuongeza import duties, kutoa huduma za biashara mipakani, kudhibiti bidhaa fake kwenye njia za panya, lakini pia hata sisi Watanzania tuna jukumu la kuhakikisha tunalinda viwanda vya ndani na bidhaa wanazozizalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia majirani zetu wananchi wamepata elimu ya kupenda bidhaa zao za ndani na kwa kufanya hivyo, yaani ule uzalendo wa kusema kwamba, tukipenda bidhaa tunazozalisha wenyewe tutatengeneza ajira za vijana na akinamama ndugu zetu, yaani unakuta tunakuwa tumeshapunguza ule mzigo wa Serikali kufanya kila kitu kudhibiti, lakini sisi wenyewe kama raia tukihamasika tukatumia bidhaa zetu hiyo na yenyewe ni kuchochea sbhughuli za viwanda vyetu hapa nchini na kuhakikisha viwanda hivi vinazalisha, ili vizidi kutengeneza ajira hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nipende kuwaomba Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuwaelimisha wananchi kupenda bidhaa ambazo zinazalishwa hapa nchini, lakini kwa upande wa Serikali tunaendelea kufanya jitihada kwa kufanya tafiti. Na zile bidhaa ambazo tunazalisha hapa nchini tutaendelea kuongeza kodi pale inapowezekana, ili kuendelea kulinda viwanda hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia na jambo hili alizungumzia Mheshimiwa Mwakajoka kwamba kero kwa wafanyabiashara Serikali hatujafanya vizuri, ningependa nitofautiane naye kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwenye World Bank cost of doing business Tanzania tume-improve kutoka nafasi ya 144 kuja nafasi ya 141. Kwa hiyo tume-improve kwa nafasi tatu. Mikakati niliyoielezea na nitakayoitaja hapa kwa mfano blueprint, tayari ni document ambayo Serikali imesha-commit kwa Watanzania na wawekezaji kwamba tutatekeleza blueprint hii ambayo imesheheni changamoto ambazo wafanyabiashara na wawekezaji wamekuwa wakiilalamikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Serikali imewasikiliza, tumeandaa blueprint, huu mwaka wa fedha tunaotekeleza kuna kero 54 zimeshafanyiwa kazi na hivi sasa kabla ya Bunge la Kumi na Moja kwisha, mkakati wa Serikali ni kuleta Muswada wa Uwezeshaji Biashara. Muswada huu ndiyo umebeba changamoto zote ambazo ziko kwenye blueprint ili tuweze kuhakikisha zinasimamiwa na legal force, yaani kwa maana tuwe tuna sheria inayosimamia utekelezaji wa blueprint.

Kwa hiyo, baada ya kufanya hivyo, tutazidi kuondoa keroambazo zinawakumba wafanyabiashara wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeendelea kuboresha taasisi ambazo ziko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara. Tunajua BRELA, TBS na TANTRADE ni taasisi ambazo zinatoa huduma kwa Watanzania kila siku. Kwa hiyo, mkakati wa Serikali na ninyi ni mashahidi, sasa hivi hizi taasisi tunaziboresha kwa kasi kubwa sana.

Mheshimjiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye hizi taasisi, kipindi cha nyuma kulikuwa hakuna Idara za customer care, kulikuwa hakuna hotline, ukienda kwenye huduma za biashara mipakani kulikuwa hakuna namba za Maafisa wanaohudumia ili kama hujaridhika na huduma zao upige simu Wizarani na kumlalakimia Afisa fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Mikakati yote tunayo kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge tuendelee kusaidiana muendelee kutupa ushirikiano ili tutekeleze mikakati hii tuzidi kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bajeti inayokuja, tumepanga kuweka maafisa yaani commercial attache kwenye nchi ambazo tunafanya biashara nazo sana ili commercial attache hao washirikiane na TANTRADE kuhakikisha tunawasaidia wafanyabiashara wetu waweze kufanya biashara na mauzo ya nje ya wafanyabiashara wetu yaweze kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba na hilo, naomba nizungumzie mikataba iliyozungumzwa humu Bungeni kwenye maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. Mkataba wa Ursus hata sisi Serikali hatujaridhika nao, tayari tumeshapendekeza kuunda government negotiating team kwa ajili ya kupitia mkataba huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge hili tayari tumeshalifanyia kazi, bado hii GNT ianze na mkataba huu utaboreshwa kwa manufaa ya nchi yetu. Pia tumeenda mbali, hata Mkataba wa TANCOL hatujaridhishwa nao. Tumefanya uchambuzi tumekuta Mkataba wa TANCOL hauna maslahi kwa nchi yetu na tayari tumeshaanza mchakato wa kuunda GNT ili tuweze kupitia Mkataba wa TANCOL kama tulivyofanya kwenye Barrick na kama tulivyofanya kwenye AIRTEL. Tutaenda na wembe huo huo kwenye Mkataba wa TANCOL. Pia hata Mufindi Paper Mill baada ya kutembelea Kiwanda kile tumegundua uhasi ambao unaukuta kwenye TANCOL na Mikataba mingine upo pia kwenye Kiwanda cha Mufindi Paper Mill. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, Serikali tutaendelea kupitia vile viwanda ambavyo vilibinafsishwa baada ya kuchambua na kujiridhisha kwamba kuna maeneo hasi, hatutasita kuchukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na Taarifa za Kamati wamelalamikia urasimu katika utoaji vibali, wamelalamikia masuala ya electronic stamps (ETS), wamelalamikia VAT ambazo kwa miaka mingi zimekuwa hazilipi kwa wafanyabiashara na wenye viwanda na vile vile wamelalamikia urasimu na mkanganyiko ambao upo ndani ya TASAC na kero za bandarini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, mimi kama Waziri wa Viwanda na Biashara sekta ambayo ndiyo driving force ya kujenga uchumi wa viwanda, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango tuko naye hapa, Waheshimiwa Mawaziri wa upande wa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi wapo; baada ya kikao hiki tutakaa tuangalie namna tunavyoweza kushirikiana kama Serikali kuhakikisha tunatatua changamoto hizi ili jitihada nzuri na maoni yenu ya ushauri mliotushauri, tutakaporudi mwakani changamoto ambazo mmezitaja tuwe tumezitekeleza kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, lakini nawashukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti Suleiman Saddiq, Makamu Mwenyekiti pamoja na Waheshimiwa Wabunge wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa ushirikiano ambao mnaendelea kuipa Wizara yangu. Nawashukuru sana, tuendelee kushirikiana na maoni na ushauri ambao mmetupa tutaufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia hoja ya Waziri wangu wa Kilimo. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema nikaweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia hoja hii. Pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Rais wa Watanzania, kwa kuniteua, kuniamini na namhakikishia kwamba nitaendelea kumsaidia kwa kushirikiana na Mheshimiwa Waziri wangu na Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu katika kutimiza majukumu ambayo Mheshimiwa Waziri wetu Japhet Hasunga, anatuongoza katika kuyatimiza. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, namwombea kwa Mwenyezi Mungu amjalie afya njema ili azidi kusukuma gurudumu la Watanzania la maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru sana Waziri wangu Mheshimiwa Japhet Hasunga kwa hotuba nzuri iliyosheheni mikakati ambayo tunakuahidi pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaisimamia katika kuhakikisha inatimiza yale malengo ambayo tumewaahidi. Vile vile nitumie nafasi hii tumshukuru sana Naibu Waziri mwenzangu, pacha wangu, Mheshimiwa Omary Mgumba, kwa ushirikiano anaonipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu pamoja na Watumishi wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya katika kutimiza majukumu ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuishukuru sana familia yangu, mke wangu Jennifa Bash, a.k.a mama Araska, pamoja na watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru sana vilevile michango ya Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji, tunashukuru sana kwa michango yenu mizuri, ushauri na kwa namna ambavyo wanaendelea kutoa ushirikiano kwa Wizara yetu na tunaahidi tutazidi kuwapa ushirikiano kwani Kamati ni extension ya Bunge na Kamati ndiyo think tank inayoshauri Wizara. Kwa hiyo, tunawashukuruni sana kwa michango na ushauri wenu.
(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kuwashukuru sana Kambi Rasmi ya Upinzani, tumesikia ushauri na maoni yao na naamini watatuunga mkono katika kupitisha hii hoja ili tuweze kwenda kufanyia kazi ule ushauri ambao wameipatia Serikali. Vile vile nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Wabunge wote ambao wamechangia hoja yetu ya Wizara, Waheshimiwa Mawaziri, tunawashukuru sana kwa michango na ushauri wetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho katika shukurani, nitumie nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Karagwe kwa namna wanavyoendelea kuniamini na kunipa ushirikiano nami naendelea kuwaahidi kwamba sitawaangusha katika jukumu langu la kuwawakilisha hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo, sasa niende kuchangia kwenye maeneo ambayo yalikuwa cross cutting na nianze na suala la bei za mazao. Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia mazao mbalimbali lakini kwenye suala la bei kuwa chini. Nipende kuwakumbusha tu kwamba suala la bei tunaangalia matokeo, lakini pia lazima tuangalie mchakato unaotupeleka kwenye bei, ni mchakato gani ambao tunatakiwa kushirikiana kuufanyia kazi, ili bei za mazao ya wakulima wetu ziweze kupanda.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia suala la bei, ni suala la factors kadhaa, kuna suala la kodi na tozo, Serikali sikivu ya Awamu ya Tano, katika Bunge hili la Kumi na Moja tayari tumeshatoa tozo na kodi kero nyingi katika mazao. Kwa vile kodi na tozo siyo factor peke yake ambayo inasaidia bei kupanda, Serikali tunaendelea kufanya jitihada kuhakikisha, kupita ushirika, tunazingatia kanuni za ubora wa mazao, tunawapa elimu wakulima ili kupitia ushirika tuweze kusimamia suala la ubora kwa sababu bei, ukiondoa kodi kero na tozo, lakini suala la ubora ni suala muhimu sana katika kuhakikisha mazao yetu yanapata bei nzuri na namna pekee ya kusimamia suala la ubora ni kupitia ushirika.

Mheshimiwa Spika, kuna takwimu zinaonesha kwamba hata kwenye upande wa pamba, upande wa kahawa, upande wa chai, ushirika ume-prove kwamba ndiyo namna bora ambayo tunaweza tukasaidia kuwaelimisha wakulima wetu wazingatie ubora ili mazao haya tunapoyapeleka kwenye masoko, suala la ubora au quality liweze kuwa zuri na kuweza ku-attract bei ya mazao yetu. Kwa hiyo, ushirika katika models ambazo zipo za kusaidia wakulima wadogowadogo katika peasant setting, ushirika ndiyo ume-prove kuwa mfumo mzuri ambao tunaweza tukautumia kuwasaidia wakulima wakazingatia suala la ubora.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge concern yao kubwa ni kukosa uadilifu na utawala bora katika mfumo wa ushirika na sisi Wizara tuwahakikishie, hili ni jukumu ambalo wametupa, tutaendelea kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha tunapata viongozi wazuri katia AMCOS zetu, tunapata viongozi katika Unions zetu ili viongozi hawa tuweze kuwasimamia na kupita huu mfumo wa ushirika, tuweze kuzingatia ubora wa mazao ili mazao haya yanapokwenda sokoni yaweze kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, katika bei pia kuna suala la supply and demand, yaani unapopeleka zao sokoni, inategemeana na wingi wa mazao uliyokuta katika soko ukoje. Hilo suala liko nje ya mkakati kwa sababu ni exogenous factor lakini tunaendelea kujitahidi kupitia kuzingatia ubora na katika ushirika, tunataka kuhakikisha tunasheheni mambo mengi, si tu katika kuzingatia ubora, lakini ushirika utatusaidia kupata takwimu, kwa sababu wakulima wanakuwa organized katika mfumo AMCOS, ni rahisi sana kujua AMCOS x katika wilaya fulani ina wakulima wangapi. Kwa hiyo, kama ni suala la pembejeo, kama ni suala la mafunzo ya uzingatiaje wa kilimo bora, kupita ushirika, kwa sababu tunaweza tukapata takwimu kirahisi, itatusaidia sana kwenye mambo ya kutoa extension services kwa ajili ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii ni sababu nyingine ambayo inaonyesha kwa nini ushirika ni mfumo mzuri, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tuwaombe waendelee kutupa ushirikiano katika suala zima la kuboresha ushirika kwa sababu kuna faida nyingi ambazo tunaweza tukazipata katika kuhakikisha tunalinda na kuboresha maisha ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, pia katika ushirika, mikakati ambayo hotuba ya Mheshimiwa Waziri imesheheni likiwemo suala la bima za mazao, ni rahisi sana kutoa huduma hii katika mfumo wa ushirika ambao umekuwa organized vizuri. Pia hata suala la mambo ya kangomba, butula, baada ya kuwa na ushirika imara, ni rahisi ndani ya AMCOS au Union, kukawa kuna Mfuko au SACCOS, ambayo itasaidia kutoa advance kwa wakulima wetu wakati wa kulima ili mkulima huyu asiingie katika majaribu ya kukutana na mtu ambaye anataka amnyonye kwa sababu ya shida.

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, hata rafiki zangu akina Mwambe ambao wanasema tuhalalishe suala la mfumo wa kangomba, tunaweza tusihalalishe mfumo wa kangomba, lakini katika kuimarisha ushirika, tukaweka mfumo wa SACCOS ndani ya AMCOS, kutoa advance kwa wakulima ili waweze kuondokana na zile changamoto na shida ambazo zinawapeleka kwenye kangomba, butula, na mambo ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ningependa kulichangia, limejitokeza sana katika michango ya Waheshimiwa Wabunge ni suala zima la uzalishaji na usambazaji wa mbegu. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri kama mlivyoona, sisi Serikali tumejipanga kuhakikisha tunakuwa tuna mkakati ambao pia tunausimamia kuutekeleza na mkakati huu ni kuhakikisha, sasa hivi tatizo lililopo ni kwamba, mzalisha mbegu na mkulima wanategemea mvua wote kwa wakati mmoja. Mkakati wa Serikali, ni kwamba, huyu anayezalisha mbegu ASA, TARI, wakati wa kiangazi, tutatenga fedha kwa ajili ya kumwezesha TARI na ASA waweze kuzalisha mbegu wakati wa kiangazi ili mbegu hizi ziwepo, ziwe tayari wakati wa msimu mkulima anapozihitaji.

Mheshimiwa Spika, tukifanya hivyo, tutaondokana na hii changamoto ambayo Waheshimiwa Wabunge walio wengi wameichangia kwamba mbegu hazipatikani, zilizo bora, zinazostahimili ukame, zinazostahimili magonjwa, lakini tuna Taasisi ya ASA na TARI ambazo Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha wakati wa kiangazi wanatumia pivot irrigation badala ya kusubiri mvua ili mbegu ziwe tayari mkulima wetu mvua inapoanza basi aweze kupata hizi mbegu. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge waunge mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wetu kwa sababu mambo haya yote baada ya kupitisha tutakwenda kwenye utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo napenda kulizungumzia ni suala la masoko kwa sababu ni mtambuka, linahusu mazao yote ya kimkakati na mazao mchanganyiko. Tayari, chini ya uongozi wa Waziri wetu Mheshimiwa Japhet Hasunga, tumeshakaa na wenzetu upande wa Wizara ya Viwanda, ku-link kilimo na viwanda. Tumekaa na breweries, kwa sababu breweries nyingi zinatumia ngano, zinatumia mahindi, zinatumia mtama na zinatumia zabibu. Tumekaa nao na hivi ninavyozungumza tunakaribia kusaini partnership ambayo mahitaji yao wameshayabainisha na tumewaomba wa-project kwa miaka mitano, kama ni zabibu watahitaji kiasi gani, kama ni mtama watahitaji kiasi gani, kama ni mahindi watahitaji kiasi gani ili tuweze kwenda kwa wakulima sasa katika wilaya na mikoa ambayo inalima haya mazao kwa wingi na kuhamasisha kwamba, limeni kwa sababu soko lipo na ni la kiasi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, breweries tumeshakaa nazo, na tumeshakaa hata na viwanda ambavyo vinatengeneza soft drinks. Ukiangalia maembe, machungwa, wana import concentrate kutoka nchi za jirani na wakati wakulima wetu ukienda kule Tanga, wakati wa msimu machungwa yanaoza. Kwa hiyo, tumeshakaa na hizi soft drinks, viwanda vinavyotengeneza soda hizi na sasa hivi kwa sababu ya watu kuzingatia afya, viwanda hivi vinaanza kutengeneza juice sambamba na distribution ya soda. Sasa zile juices ambazo wanatengeneza zenye flavor ya pineapple, zenye flavor ya mango, zenye flavor ya orange, wanaagiza concentrate. Sasa sisi tunataka kwa sababu tumeshakaa nao, tujue mahitaji yao, twende tukahamasishe kilimo cha maembe, kilimo cha machungwa, kilimo cha nanasi ili badala ya ku-import concentrate, viwanda hivi viwe vinanunua malighafi hii ya wakulima hapa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo, tayari Wizara yetu tumeshakaa na hawa International off-takers, ninyi mashahidi, tulikaa na WFP, (Word Food Program), tumeingia nao mkataba wa muda mrefu kupita NFRA watakuwa wanakusanya mahindi na sasa hivi si mahindi tu, ukienda South Sudan wanahitaji mtama.

Kwa hiyo pia kupitia NFRA tutakuwa tunawahamasisha wakulima walime mtama halafu NFRA au aggregate, lakini WFP anakuwa anachukua hapa Tanzania kupita NFRA na wanunuzi binafsi, kupeleka kwenye nchi ambazo hazina ardhi yenye rutuba, hazina amani kama Tanzania. Kwa hiyo, sasa ni muda sahihi wa kuhakikisha wanaunga mkono bajeti ya Kilimo ili tuweze kuipeleka kwenye utekelezaji na kuchukulia hii geographical comparative advantage tuliyonayo katika nchi za Afrika Mashariki na SADC kwa sababu tunaweza tukazalisha kwa kiasi kikubwa na tukaweza kuondokana na hii changamoto ya wakulima wetu kulima, lakini masoko yakawa yanakosa.

Mheshimiwa Spika, tunawahakikishia Waheshimiwa Wabunge wakiunga mkono bajeti hii haya mambo yote tunayowaambia tutaweza kupeleka kwenye utekelezaji na matokeo makubwa watayaona kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala ambalo Mheshimiwa pacha wangu Mheshimiwa Omary Mgumba amelizungumzia, tukizungumzia mambo ya umwagiliaji mara nyingi tunafikiria ujenzi wa mabwawa makubwa, fedha nyingi, lakini niwaombe Waheshimiwa Wabunge, kama alivyosema Mheshimiwa Mgumba, kupitia halamshauri zetu…

SPIKA: Dakika moja umalizie.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Spika, nashukuru. Suala la mabwawa kwa mfano kwenye mpunga, hauhitaji skimu kubwa, tunaweza tukaangalia jinsi ya ku-rain harvest, yaani kwa uchimbaji mdogo tu unakinga unapata maji kwa ajili ya kilimo cha mpunga na mazao ya bustani badala ya kusubiri kwamba mpaka mradi mkubwa uje uletwe na Tume wa Umwagiliaji kwenye wilaya husika, sasa sisi ndani ya Serikali tutakaa na halmashauri, Wakuu wa Mikoa, kuhakikisha suala la rain harvest linakuwa sambamba na uchimbaji wa mabwawa tunayozungumzia.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora). Nianze kwa kuendelea kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Magufuli, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Makamu wa Rais na Baraza la Mawaziri kwa kuendelea kufanya kazi nzuri ya kuwaletea matumaini Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia kwangu bajeti ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), ningependa kuchangia katika sehemu mbili; sehemu ya kwanza, ni changamoto za wananchi wangu wa Jimbo la Karagwe na sehemu ya pili ni ushauri kwa Serikali. Kwa sababu changamoto kwenye Jimbo langu la Karagwe ni nyingi, naomba kwanza nijikite kwenye hizi changamoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene kwa kazi nzuri na kuwa msikivu pale tunapomfuata kuwasilisha changamoto za wananchi wetu. Namshukuru Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa kuwa msikivu na kwa kutupa ushirikiano mzuri katika kusikiliza changamoto za wananchi wetu na kaka yangu Naibu Waziri, Mheshimiwa Jafo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Karagwe ina changamoto nyingi, lakini kwanza nianze kwa kuwashukuru wananchi wa Karagwe kwa kuendelea kuniamini na kunituma hapa kuwa Mbunge wao. Wiki mbili zilizopita Karagwe tulipata janga kubwa, tumepata janga la moto pale Kayanga, maduka zaidi ya 117 yaliungua.
Mhesimiwa Mwenyekiti, kwa kweli, naomba nitumie nafasi hii kuwapa Wahanga wa moto, wananchi wa Karagwe pole sana na nitumie nafasi hii kwanza, nimshukuru Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Simbachawene kwa kuwapa pole Wana-Karagwe na kwa kuniahidi kwamba Serikali itaangalia namna ya kuwasaidia hawa wahanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, juzi kulitokea tukio la ujambazi stesheni ya Nyakaiga, majambazi wakaua mwananchi mmoja pale na mwingine wakamjeruhi sana. Pale Nyakaiga ni stesheni kubwa, ina wananchi wengi lakini hatuna huduma ya kituo cha polisi. Napenda kuiomba Serikali itusaidie, pale Mji umekua, Serikali itusaidie kujenga kituo cha polisi ili wananchi waweze kuishi kwa amani na usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, kuna changamoto nyingi Jimbo la Karagwe, lakini nitaje chache. Nianze na madeni viporo. Pamoja na jitihada ya Serikali kupeleka fedha za maendeleo, bado kuna changamoto ya kuchelewesha hizi fedha.
Katika Halmashauri ya Karagwe, bado tuna madeni makubwa ya wakandarasi, watumishi na wazabuni. Napenda kuiomba Serikali katika kipindi cha mwaka huu wa fedha wa 2015/2016 kabla hatujaenda mwaka wa fedha mpya, Serikali ijitahidi ituletee fedha ambazo tulitakiwa kupata katika kipindi cha mwaka wa fedha ili tuweze kupunguza haya madeni na fedha ambayo imetengwa kwa mwaka wa fedha unaokuja 2016/2017 iweze kwenda kufanya kazi za maendeleo ambazo tumezitarajia katika mwaka wa fedha unaofuata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna tatizo kubwa la upungufu wa watumishi katika Jimbo la Karagwe. Kwa upande wa walimu, sekta ya elimu kwa shule za msingi tu, tuna upungufu wa walimu 832. Kwa upande wa shule za sekondari tuna upungufu wa walimu 92.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya kwa upande wa upungufu wa watumishi tuna upungufu wa wauguzi 40 na madaktari watano na kwa upande wa kilimo Afisa Ugani tuna upungufu wa watumishi 15 na upande kwa maendeleo ya jamii tuna upungufu wa wataalam 27.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama takwimu zinavyoonesha, Halmashauri yangu ina upungufu mkubwa sana wa watumishi. Napenda kutumia nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri Angellah Kairuki, aione Karagwe. Tunakutegemea sana na tunaamini utatusaidia katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala la madeni ya Halmashauri, napenda kuishauri Serikali, kama fedha kutoka Hazina imekuwa ikichelewa kutolewa kwa miaka mingi, basi tuangalie ule utaratibu wa asilimia 70 ambazo zinatoka Halmashauri kwenda Hazina, tuigeuze ile; zile asilimia 70 zibaki kwenye Halmashauri halafu asilimia 30 ndiyo iende Hazina ili fedha za maendeleo siziwe zinachelewa kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu wa vitendea kazi hasa kwenye sekta ya afya kwenye Jimbo la Karagwe. Karagwe ina watu wasiopungua 350,000 na sisi tumezaa Jimbo jipya la Kyerwa ambalo bado tunaendelea kulihudumia katika huduma za afya kama Wilaya mama ya Karagwe ambayo imezaa Jimbo la Kyerwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua Kyerwa na Karagwe, tuna jumla ya watu wasiopungua 800,000, lakini bado tuna ambulance moja tu ambayo inahudumia vituo vya afya 35 na jiografia ya Karagwe imesambaa sana. Kwa hiyo, naiomba TAMISEMI itusaidie angalau tupate ambulance mbili ili wananchi wa Karagwe wapate huduma ya ambulance pale tunapohitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika upande wa afya, tuna hospitali ya Nyakahanga lakini imeelemewa. Kama nilivyosema, Kyerwa bado haijawa na Hospitali ya Wilaya, Karagwe Wilaya mama pia haina hospitali ya Wilaya. Tunategemea hiyo hospitali ya ELCT. Natumia nafasi hii kulishukuru kanisa la ELCT kwa kuendelea kusaidia wananchi wa Karagwe na hospitali ya Nyakahanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Karagwe tunakua kwa watu wasiopungua 10,000 kwa mwaka; hospitali imekuwepo miaka mingi sana, imefika mahali imeelemewa na inasaidiwa na kituo cha afya cha Kayanga ambacho hivi sasa hakina wodi ya akina mama na watoto. Kina wodi ya wanaume; na kituo hiki hakina wodi ya kulaza wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji. Kwa hiyo, napenda kumwomba kaka yangu, Mheshimiwa Simbachawene na Naibu Waziri Mheshimiwa Jafo, mtuangalie katika hili pia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna changamoto za barabara ambazo ziko chini ya TAMISEMI. Kuna barabara ya kuanzia Nyakasimbi kwenda Nyakakika, Kibondo, Nyabiyonza, Kiruruma mpaka kwenda kwenye Wilaya ya Kyerwa kupitia Rwabwere, hii ni barabara ambayo inaunganisha Wilaya mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Serikali hii barabara ipandishwe kwenye kiwango wa TANROAD kwa sababu kwa kufanya hivi tutakuwa tumeondoa mzigo kwa Halmashauri, itatengenezwa katika kiwango kizuri na itasaidia kuinua uchumi wa wananchi wa Karagwe na Kyerwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais Magufuli wakati alipokuja Karagwe kuomba wananchi ridhaa ya kuwa Rais wa Tanzania alituahidi barabara ya Nyakahanga kwenda Chamchuzi tuipandishe TANROAD na ijengwe kwa kiwango cha lami na tuweke kivuko pale Chamchuzi ili kusaidia kuimarisha biashara kati ya Karagwe na jirani zetu wa Rwanda. Kwa hiyo, napenda kuiomba Serikali itusaidie hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimefuatilia Wizara ya Ujenzi wakanielekeza kuwa kuna utaratibu wa kuingiza ahadi za Mheshimiwa Rais kwenye kitabu cha ahadi za Mheshimiwa Rais, lakini mimi ni mwakilishi wa wananchi wa Karagwe, Mheshimiwa Rais alitamka mwenyewe, Mheshimiwa Rais hawezi kusema uongo, na mimi hapa mwakilishi wa wananchi wa Karagwe siwezi kusema uongo. Napenda kuiomba Serikali itumie taarifa hii kama ni rasmi kwamba hili kweli lilitamkwa na watusaidie tupate hii barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia nguvu ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kuhitimisha hoja ya Wizara yangu. (Makofi)

Pia nitumie nafasi hii kukushukuru wewe, Naibu Spika wetu na Mbunge wa Mbeya Mjini, juzi nilikuwa Mbeya kwa kweli nilifurahi kuona kauli chanya za Wana Mbeya Mjini wengi kukupongeza kwa kazi nzuri unayofanya. Hongera sana Mheshimiwa Naibu Spika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitumie nafasi hii kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, mama mahiri, mchapakazi tunampongeza kwa kazi nzuri anayoifanya kuiongoza nchi yetu. (Makofi)

Nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango kwa kazi nzuri anayoifanya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutimiza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa kwa miongozo na maelekezo anayotupatia Mawaziri katika kutimiza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kauli, kwa maandishi na kwa support kwa ujumla Bunge zima toka asubuhi kwa kweli imekuwa ni furaha tupu. Waheshimiwa Wabunge tunawapongeza kwa ku-support michezo, sanaa, utamaduni na habari toka asubuhi yaani muda ungekuwa unatosha kwa kweli michango tungepata mingi sana kwahiyo tunawashukuru wale 29 ambao mmechangia hoja yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwashukuru Kamati inayoongozwa na Mheshimiwa Nyongo na Makamu Mheshimiwa Kamamba na Waheshimiwa Wajumbe wote kwa maoni na ushauri ambao mmekuwa mkitupatia. Na niwaahidi Wizara yangu kwa maoni na ushauri ambao mmetupatia tutauekeleza kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijibu hoja zilizotolewa kutoka kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge na nianze kwa kumshukuru Naibu Waziri Mhehimiwa Pauline Gekul kwa ufafanuzi mzuri wa hoja za Wabunge. Na nianze kwenye Tasnia ya Habari; kumekuwa na hoja kwamba Serikali tusaidie wanahabari kwenye stahiki zao na hoja hii ilichangiwa na Wabunge kadhaa, Mheshimiwa Bulaya pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine ningependa kuwaondolea wasiwasi Waheshimiwa Wabunge, Serikali ndio maana kwenye Sheria Na. 12 ya mwaka 2016 ukiangalia moja ya malengo ya sheria ile ni kuhakikisha stahiki na maslahi ya wanahabari yanazingaitiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachoweza kuwahakikishia pamoja na Wabunge sheria ile imeelekeza kuanzisha Bodi ya Ithibati, Baraza Huru la Wanahabari na vyombo hivi viwili moja ya majukumu ni kuhakikisha vinasimamia maslahi ya wanahabari. Na sisi Serikali kwa vile tunajali maslahi na stahiki za wanahabari tutahakikisha tunatumia sheria hii kuhakikisha mambo mazuri kwa mfano, bima kwa wanahabari, mambo ya pensheni na mazingira bora ya kazi yanazingatiwa kwa wamiliki wa vyombo vya habari kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, ningependa kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge pamoja na wanahabari kote nchini Serikali tupo pamoja nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja pia kwamba Serikali hufungia vyombo vya habari ambavyo vinafanya kazi za kiuchunguzi. Sheria Na. 12 ya mwaka 2016 kifungu 52(2) kinasema kwamba si kosa kuikosoa Serikali. Kwa hiyo, Serikali haijawai kufungia chombo chochote cha habari eti kwa vile kinafanya kazi za kiunchunguzi. Kwa vile magazeti ambayo yalifungiwa yalikuwa ni mambo ya kimaadili na uvunjifu wa Sheria ya Habari, lakini sio kwamba wanafanya kazi ya kiuchunguzi, hiyo si kweli.

Kwa hiyo, pamoja na Waheshimiwa Wabunge nitoe wito kwa wanahabari na wadau wote wa tasnia ya habari waendelee kufuata Sheria na Maadili ya Habari na Utangazaji. Nia ya Serikali ni kuweka mazingira wezeshi ili kazi zao ziweze kufanyika vizuri, lakini lengo la Serikali siyo kufungia vyombo vya habari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye upande wa michezo; na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge kuipongeza Azam kwa mkataba ambao walisaini na TFF kwa kweli mkataba huu utaleta mchango na mageuzi makubwa katika maendeleo ya sekta ya soka nchini. Lakini Azam tumewaona wakisaidia pia tasnia ya ngumi kwa hiyo nitoe wito kwa wadau wengine wafanye kama Azam ili tushirikiane pamoja na Serikali kuhakikisha tunaendeleza michezo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna suala la utawala bora katika michezo na Waheshimiwa Wabunge sana sana wamejikita katika kuelezea changamoto zilizopo za utawala bora upande wa soka hasa hasa TFF.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kwamba kwa utaratibu wa FIFA, Serikali inatakiwa iwe eyes on, hands off katika masuala ya michezo. Lakini pia Serikali tunatambua kwamba hata FIFA inashirikiana na Serikali kote inakofanya kazi katika kusimamia masuala ya michezo.

Kwa hiyo, kwenye suala la utawala bora Serikali tuko serious, zipo sheria za nchi ambazo zinasimamia masuala ya utawala bora na katika hili Waheshimiwa Wabunge, Wizara imepokea malalamiko, kwa hiyo, nikiri kwamba malalamiko haya na sisi tumeyapokea na tayari nimeelekeza Baraza la Michezo Tanzania kufanyia chambuzi malalamiko haya ili tuweze kuyafanyia kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwenye suala la utawala bora Serikali tuko serious, tutahakikisha sheria na taratibu za nchi zinasimamiwa. Kwa hiyo, ningependa kutoa wito na nilishatoa wito huu kwa TFF waendelee kuzingatia misingi ya utawala bora hapa nchini katika suala zima la maendeleo ya soka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa kuna suala la rushwa. Kwamba, TAKUKURU ilikuwa inachunguza jambo ambalo limechukua muda mrefu. Nimefuatilia jambo hili na kwa vile bado liko kwenye uchunguzi basi niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kuwa TAKUKURU italitolea ufafanuzi wake pale uchunguzi utakapokuwa umekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na Waheshimiwa Wabunge ningependa kuzungumzia changamoto ambazo zimetajwa kwenye maendeleo ya michezo nchini kwa kutumia mfano wa pyramid. Pyramid ukiiangalia upande wa chini inakuwa ni pana halafu kadri unavyopanda inakuwa ni nyembamba. Sasa kwenye maendeleo ya michezo nchini kwenye hotuba yangu nimesema kuna mpango mkakati wa maendeleo ya michezo ambao tunauzindua Julai, 2021 yaani mwezi wa saba na katika mkakati huu Waheshimiwa Wabunge, kwenye hotuba yangu nimesema sports for all, kwamba lazima tuhakikishe shule za misingi na sekondari watoto wote wawe kwenye shule za msingi za umma au binafsi, shule za msingi na sekondari wanapata fursa ya kucheza michezo shuleni kama wanavyopata fursa ya kusoma masomo mengine. Jambo hili tayari tumeshashirikiana na Wizara ya Elimu, namshukuru Mheshimiwa Profesa Ndalichako pamoja na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Jafo kipindi kile, lakini hata Mheshimiwa Ummy tumeendelea kushirikiana katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeunda utatu wa kushirikiana kuhakikisha masuala ya UMITASHUMTA na UMISETA tunajipanga upya kuanzia mwaka huu na ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge mtaangalia mkakati wa UMITASHUMTA na UMISETA wa mwaka huu uko tofauti na miaka iliyopita. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, tarehe 8 Juni ataenda kutufungulia mashindano kule Mtwara. Lakini kuanzia mwaka huu kwenda miaka inayokuja Waheshimiwa Wabunge mtaona tofauti kubwa. Tumejipanga kuhakikisha kupitia UMITASHUMTA na UMISETA watoto wetu wanapewa mazingira mazuri ya kufanya michezo lakini pia tunashirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha watoto wanaofanya vizuri kupitia michezo hii basi tunawaendeleza badala ya kuacha UMITASHUMTA na UMISETA imeisha basi wanapotea mpaka mwaka unaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia miaka ya nyuma watoto walikuwa wanacheza unakuta wiki moja kabla ya UMITASHUMTA na UMISETA ndipo wanaandaliwa kwenda kushiriki kwenye michezo. Safari hii kupitia TAMISEMI tayari maelekezo yameshatolewa kwenye shule za msingi na sekondari kote kwamba somo la michezo ni somo muhimu kama masomo mengine. Kwa hiyo, tutaendelea kusimamia hili ili kuendelea kutengeneza vipaji kwa watoto wetu kuanzia shule za msingi na sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, sambamba na hili tuanshirikiana na TAMISEMI kubainisha shule ambazo zitakuwa ni shule maalum za michezo kwenye shule za msingi kila mkoa na sekondari. Zoezi hili tumekubaliana likamilike kufika mwezi huu mwishoni ili kwenye mipango ya Serikali ya miaka ya fedha inayokuja, basi fedha iwe inatengwa tunahakikisha shule hizi maalum zinapata vile vifaa vya lazima ili watoto wanaofanya vizuri wenye vipaji wanaenda kwenye kwenye hizi shule maalum sambamba na combination ambazo zitakuwa zinatolewa form five na six ili kuandaa walimu wa michezo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa kutumia hii pyramid approach vipaji tutakavyoinua kupitia shule za msingi na sekondari katikati ya pyramid kuna upande wa sekta binafsi pia kushiriki kwa kujenga academies na tumeona academies mbalimbali hapa nchini. Tunaipongeza Serikali na kuwaunga mkono wawekezaji hawa na tutaendelea kushirikiana nao kuhakikisha suala la kuibua vipaji kutoka kwenye shule za msingi na sekondari basi hapa tunakuwa tuna sports academies nyingi na sisi Serikali ili kuonesha mfano tumetenga shilingi bilioni 1.3 kwenda kwenye Chuo cha Malya ili kuwe kuna sports academy, wale wanachuo wanaojifunza michezo wajifunze kwa vitendo huku wakifundisha kwenye shule hii ambayo itakuwa inaendeshwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo kwenye pyramid mwisho inakuwa nalo hapo ndiyo unakuta vilabu kama Simba, Yanga, Namungo, Ihefu na vilabu vingine. Lakini hapo ndipo tunaenda kwenye professional sports yaani wachezaji wa ndani kwenye vilabu, lakini na wachezaji wa nje. Tukitumia approach hiyo mimi sina shaka kwa namna Serikali ambavyo tumejipanga tutafanya vizuri na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu mizuri ambayo itatupa muelekeo na kusaidia kuboresha haya niliyoyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yapo mapitio ya sera, sheria na kanuni ili kuhakikisha mkakati huu tunaenda vizuri na unakuwa na matokeo ambayo mmetushauri. Katika hili mimi namshukuru Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, ametuelekeza kwamba pamoja na mikakati yote hii angependa kuona wanawake katika michezo nao wanafanya vizuri. Haiwezekani tukawa tuna mama mahiri, shupavu Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, nina Naibu Waziri mwanamke, halafu timu za wanawake zinafanya vibaya. (Makofi)

Kwa hiyo, nawahakikishia kwenye hili tutahakikisha michezo inaenda sawia wanaume na wanawake na timu za wanawake zinafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, hoja ya viwanja vya CCM ni kwamba Wizara yangu imeratibu jambo hili; Azam, TFF na Chama cha Mapinduzi wako katika maongezi ya kuangalia namna ya kushirikiana ili kuendesha viwanja vya Chama cha Mapinduzi nchini. Katika hili niwaelekeze TFF, sauti ya Wabunge ni sauti ya wengi, katika fedha ambazo wanazipata kutoka FIFA pamoja na vyanzo vingine hebu tuanze kuangalia na kuweka nyasi bandia kwenye viwanja ambavyo viko kwenye mikoa mbalimbali. (Makofi)

Kwa hiyo, TFF kwenye hili najua mnajenga uwanja wa kisasa pale Kigamboni na Tanga lakini kwenye vipaumbele kuanzia mwaka huu ambao na mimi naomba nipitishiwe fungu basi TFF tuanze kushirikiana kuhakikisha nyasi bandia kwenye viwanja mbalimbali mikoani basi tunashirikiana katika kuvijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni suala la wachezaji wa kigeni vs local content kwa maana ya kukuza vipaji ndani ya nchi ni suala ambalo lina mjadala na lina pande mbili. Ningependa kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge, mwaka jana mlituelekeza tushirikishe wadau ili tuweze kulipatia mwelekeo. Baada ya kuwashirikisha wadau, mwongozo unasema maximum ya wachezaji wa ndani kwenye klabu ni wachezaji wasiozidi kumi.

Kwa hiyo, kama kutakuwa na ushauri na maboresho katika hili sisi tuko tayari kupokea ushauri wenu ili tuone namna ya kulipeleka lakini nia hapa ni ku-balance import substitution ni jambo zuri ili tuweze kutengeneza vipaji vya hapa ndani. Lakini hiyo isiweze kuathiri malengo ya vilabu katika kutafuta wachezaji wazuri. Katika hili nipende kusisitiza na kuelekeza wale wanaoleta wachezaji kutoka nje basi leteni wachezaji ambao wana-profile ambazo zinaeleweka na zitaleta mageuzi katika kufundisha vijana wetu ambao wanacheza hapa ndani. Ipo kasumba unakuta mchezaji ametoka nje lakini akija anacheza, anazidiwa na wachezaji wa ndani. Sasa hiyo inakuwa na maana gani? (Makofi)

Kwa hiyo, ningependa kuwasisitiza vilabu pamoja na wadau wa mchezo wa soka tuangalie profile za wachezaji tunaowaleta ili watakapokuja kweli waweze kutoa chachu kwa wachezaji wetu wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa kuna hoja ya uwanja wa michezo hapa Dodoma ambao uliahidiwa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliuliza Mheshimiwa Mavunde. Ningependa kumhakikishia kwenye hili tuko katika hatua nzuri. Eneo la kujenga tumeshalibainisha na Serikali kupitia Wizara ya Fedha maana mkakati wa Serikali ni kupitia mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere kwenye corporate social responsibility hapo ndipo tutapata fedha za kujenga uwanje huu. Kwa hiyo, commitment ya Serikali iko pale pale na jambo hili tutalisimamia katika utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa kuna suala la Muungano. Ningependa kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge michezo inatuunganisha, ni sehemu ya fursa ya kujenga Muungano wetu. Kwa hiyo, changamoto zilizopo TFF na ZFF tutawaelekeza na kuwasihi waendelee kushirikiana kwa sababu michezo na sanaa ni maeneo ambayo yanatuunganisha vizuri sana katika Muungano. Kwa hiyo, mimi kama Waziri mwenye dhamana nitaendelea kuhakikisha kupitia michezo ZFF na TFF wanashirikiana katika kuleta mageuzi ya maendeleo na michezo Bara na Visiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa Sanaa niungane na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza mdogo wangu Naseeb Abdul a.k.a Diamond. Nami niendelee kutoa wito kwa Watanzania, katika hili tumuunge asilimia 100 ili kijana wetu ashinde. Hii ni heshima kwa nchi yetu, lakini katika hili pia niwapongeze vijana wetu waliopata tuzo za AFRIMMA ya mwaka 2021 alikuwepo Diamond, Nandy na Zuchu, na wenyewe tunawapongeza. (Makofi)

Katika hili niendelee kusisitiza iwe kwenye michezo, sanaa, timu au mtu anapoliwakilisha Taifa letu hebu turudi kuwa wamoja kama Watanzania tuweke ushabiki wetu pembeni. Kwa hiyo, hata hili la Diamond, najua kwenye muziki pia kuna ushabiki, kuna timu fulani na timu fulani. Ningependa kutoa wito kwa wadau na Watanzania kwenye hili tuungane na tumuunge mkono kijana huyu akifanikiwa kupata award ya BET inaleta inspiration na hamasa kubwa kwa vijana wengine wanaochipukia katika sanaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la sports and arts arena; Serikali inachukua jambo hili kwa uzito sana Waheshimiwa Wabunge. Ningependa kuwatoa wasiwasi. Sasa hivi kwenye bajeti tumetenga shilingi milioni 20.9 yaani milioni 20 na laki tisa kwa ajili ya kumlipa mtaalam elekezi aweze ku-design mchoro na kusanifu ili tuweze kujua gharama halisi ya kujenga hii sports and arts arena. Kwa hiyo, kwenye bajeti inayokuja ya mwaka unaokuja tutakuwa tumeshajua gharama halisi ni nini ili tuweze kuziombea fedha kwenye bajeti inayokuja. Kwa hiyo, kwenye mwaka huu tumetenga hela ya kumlipa consultant afanye usanifu halafu mwaka unaokuja tutaweza kujua gharama halisi ni kiasi fulani ili tuweze kuiombea fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna suala la BASATA. Waheshimiwa Wabunge, kwenye hili Wizara tuko na ninyi. Tunatambua hata kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi fursa ziko kubwa sana katika tasnia ya sanaa kutengeneza ajira kwa vijana wetu. Lakini sambamba na hili, tutafanya kila linalowezekana kuweka mazingira wezeshe. Ndiyo maana nilielekeza kanuni ya 25 tu-withdraw, tushirikishe wadau tuweze kufanyia maboresho, kwa sababu lengo la Serikali ni ku-promote sector itengeneze ajira na kuchangia Pato la Taifa, lakini tusifanye hilo kwa cost ya kudidimiza maadili. Kwa hiyo, hata kanuni tunayoiandaa tunatafuta balance ya ku-promote sector kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyoelekeza, lakini sambamba na hilo, maadili lazima tuyalinde. Katika hili tumeenda mbali, tupo tunaandaa mwongozo ambao tutashirikisha ma-producer na Idara za Muziki kwenye redio na tv ili kila mmoja katika eneo lake ajue kwamba jambo hili tumekubaliana ni katazo kwa hiyo hata mimi ninawajibika kulisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, ninaamini tukifanya hivyo tutaondoa urasimu unaolalamikiwa lakini tutasaidiana katika kuhakikisha maadili hatuyadidimizi kwa gharama ya kuangalia tu ku-promote sector. Hakuna Taifa ambalo halina maadili, Taifa lolote linajivunia na utambulisho wake ni mila na desturi zake. Kwa hiyo, ningependa kutoa wito kwa wasanii wetu waendelee kuipa ushirikiano Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na tuangalie na tusaidiane kuhakikisha mwongozo tutakaoutoa wote tunashirikiana katika kuusimamia pamoja na Kanuni mpya ambayo niwahakikishie hatutachukua muda mrefu kuikamilisha ili iweze kuingia katika utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kulikuwa kuna hoja pia kuhusu COSOTA, suala ya mirahaba. Nilivyoangalia kiasi ambacho COSOTA imekusanya nikaona ni kidogo sana, lakini pia nikaangalia potential ya kukusanya mirahaba kupitia COSOTA nikaona ni kubwa sana. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tulichokifanya katika hili TCRA kwa teknolojia iliyopo muziki ukipigwa kwenye redio au tv, hata ukipigwa kwa sekunde 15 tunajua redio fulani imepiga muziki wa msanii fulani. Kwa hiyo, TCRA inashirikiana na COSOTA kutengeneza mfumo ambao tutautumia kuboresha mfumo wa ukusanyaji mirahaba kwa wasanii wetu. Mimi ningependa siku tunawaita wasanii, tunagawa bilioni kadhaa sio milioni 199 ambayo iko hivi sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo ningependa kuwaomba mtupe muda mpaka mwisho wa mwaka ili jitihada hizi nilizozitaja tuziweke katika utekelezaji angalau tutakapoandaa tukio la kutoa mirahaba kwa wasanii, hata ukimkaribisha Mheshimiwa Rais au Makamu wa Rais au Waziri Mkuu aje kuzindua hilo tukio liwe linaendana na hadhi yake. Lakini huwezi ukamkaribisha Mheshimiwa Rais au Makamu wa Rais au Waziri Mkuu aje kugawa mrahaba wa milioni 190. Kwa kweli mimi kwa ninavyotazama fursa ya kukusanya mirabaha hii, najua mpaka kufika mwisho wa mwaka tutakuwa tumepiga hatua nzuri. (Makofi)

Kwa hiyo, ningependa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge mtuamini katika hili na wasanii tutafanya vizuri. Tumejipanga vizuri kuhakikisha tunatumia mifumo na teknolojia katika kuwasaidia wasanii kupata mirahaba na haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili ni suala la aggregate ambalo limetajwa; tunafanya mawasiliano na tunajadiliana na wasanii, Mheshimiwa Babu Tale, Mheshimiwa Mwana FA mmekuwa washauri wazuri katika hili. Tutaangalia namna bora ya kulipeleka hili ili liweze kuwasaidia wasanii wasinyonywe kama ilivyo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa kuna michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge, lakini mimi kama nilivyosema hapo mwanzo, nikiri kwamba tumepokea na hoja zote tutaziwasilisha kwa maandishi na niwashukuru sana, hii Wizara ni Wizara ambayo kazi kubwa ni kuratibu. Kwa vile tunawasikia na mnatupa ushauri mzuri mimi niwahakikishie nitaendelea kushirikiana na Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yangu ya Wizara ili kuratibu mawazo na ushauri mzuri ambao Bunge hili tukufu mnatupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, natoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YANJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Profesa Muhongo pamoja na Naibu Waziri kwa hotuba na kazi nzuri wanayoendelea kufanya. Kwa bahati mbaya sitapata nafasi ya kuchangia, yangu ni machache.
Mheshimiwa Naibu Spika, Karagwe Vijijini ina vijiji 110 na kila kimoja bado kinahitaji huduma ya REA III. Orodha ya vijiji tayari tumeshawasilisha Wizarani, naomba sana Karagwe ipate REA III kuanzia Julai, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Upinzani wamekuwa objective na ushauri wao naomba tuuzingatie hasa:-
(a) Mapitio ya mikataba ya umeme wa emergency;
(b) Energy Mix Policy or National Energy Policy isisahau hydro-power bado ni potential na environmentally friendly tuipe weighting ya kutosha;
(c) Hoja za wachimbaji wadogo zina mashiko;
(d) Dira ya STAMICO tuiangalie na tuizingatie whether kupewa tail- end production segment ni economical kwa STAMICO;
(e) Mfuko wa abandonment cost and environmental rehabilitation haupo wazi, ni vema Serikali ikatoa maelezo ya uendeshaji wake; na
(f) Sheria ya Watumishi iweke katazo kwa Watumishi wanapostaafu kujiunga na kampuni za nishati na madini kwani kwa hali ilivyo sasa ina-attract rent seeking behavior.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana kwa kazi nzuri za kuwahudumia wananchi na kwa ushirikiano mnaonipa kuwahudumia wananchi wa Karagwe. Naomba nichangie yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru barabara ya Nyakahanga-Nyabiyenza-Nyakakika imekasimishwa TANROADS na kutengewa shilingi milioni 150 kwa mwaka wa fedha 2017/2018, pamoja na shukrani nawaomba tena nipo chini ya miguu yenu barabara hii mniwekee nguvu
ipande officially kwenda TANROADS. Bahati nzuri wote wawili mmeshatembelea Karagwe na nimewalilia sana kwa kuonesha umuhimu wa hii barabara kwenye kukuza uchumi wa Wilaya na nchi yetu kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inahudumia kambi za JWTZ, barabara hii inatuunganisha na nchi ya Rwanda. Mheshimiwa Rais aliahidi kilometa tano za lami, nimeshakaa na Madiwani na kupitia Baraza la Madiwani tumeridhia kwamba kilometa hizi za lami ziende kwenye barabara tajwa Nyakahanga-Nyabiyenza-Nyakakika eneo korofi sana la Kajura Nkeito. Nawaomba sana fedha hizi zitengwe na kuletwa ili tuweze kudhibiti eneo hili korofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kivuko Single Custom ili kuimarisha biashara kati ya Wilaya ya Karagwe na nchi ya Rwanda kwenye eneo la Chamhuzi Kata ya Bweranyange ambalo lipo kwenye barabara tajwa kwenye aya ya kwanza na ya pili hapo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine nawapongeza na kuwashukuru kwa ushirikiano mnaonipa kuwahudumia wananchi wa Wilaya ya Karagwe. Nitashukuru iwapo nitapata reaction yenu wakati wa majumuisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, thanks and God bless.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Afya, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watumishi wote, nianze kwa kuwapongeza kwa kazi nzuri ya kuwahudumia Watanzania. Binafsi ninawashukuru sana Waziri na Naibu Waziri kwa ushirikiano mnaonipa kuwahudumia wananchi wa Jimbo la Karagwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maombi mawili ambayo ni kwanza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Hatua za awali kwenye Halmashauri na RCC zimekamilika tunakwamishwa na urasimu, ipo kwenye mchakato kwa upande wa Serikali Kuu. Wizara ya Ujenzi tayari imeridhia majengo ya TANROADS yaliyopo karibu na Makao Makuu ya Wilaya eneo la Kihanga yatumiwe kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya. Tunaishukuru sana Wizara ya Ujenzi.

Naiomba Wizara ya Afya uwapanguse machozi wananchi wa Karagwe kwa kushirikiana na TAMISEMI ili kiasi cha fedha kitengwe kwenye bajeti mwaka 2017/2018 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali, hata kama ni kiasi kidogo cha fedha. Nitashika shilingi ya Waziri iwapo sitapata maelezo ya kuridhisha juu ya jambo hili. TANROADS itachukua majengo yake iwapo ujenzi wa hospitali hautaanza mwaka 2017/2018 kama tulivyoahidiwa kwenye maombi yetu na ombi namba mbili, please refer to request number one.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ya kuongoza Wizara hii muhimu. Aidha, nampongeza Katibu Mkuu na watumishi wa Wizara kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Idara ya Malikale ishirikiane na Halmshauri ya Karagwe na Ofisi ya Mbunge kuendeleza maeneo ya Malikale ikiwemo yaliyokuwa Makao ya Chifu Rumanyika. Mara nyingi nimekuja kuwaona Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri juu ya jambo hili, naomba msaada kwa niaba ya wananchi wa Karagwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iweke utaratibu wa ujirani mwema na vijiji vinavyopakana na Pori la Akiba la Kimisi kwenye Kata za Rugu, Nyakasimbi, Nyakakika, Nyakabanga na Bweranyange kwa kusaidia kuboresha sekta ya elimu hasa kusaidia ujenzi wa madarasa ya shule za msingi, nyumba za walimu, matundu ya vyoo na kuchimba visima vya maji. Msaada huu ni wa muhimu sana na utasaidia kujenga royalty and sense of community ownership kwa maliasili za umma zilizo kwenye Pori la Akiba la Kimisi badala ya kulitazama with contempt.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri arejee memo yangu niliyomwandikia tarehe 19/05/2017 humu Bungeni juu ya ombi la kuleta wataalam toka Idara ya Utalii kuangalia border belt ya Wilaya za Ngara, Karagwe na Kyerwa ili kufanya ukanda huu ukuze utalii kwa kutumia vivutio vya Malikale, Maporomoko ya Rusumo, Mto Kagera, Ziwa Lwakajunju, Game Hunting kwenye Bonde la Kimisi, Ibanda na Rumanyika Game Reserves na vivutio vingine tulivyojaliwa na Mwenyezi Mungu kwenye border belt hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti,majirani zetu Rwanda on the other side of the border wanajipatia fedha nyingi za kigeni, kwani wametumia fursa asili nilizozitaja kukuza utalii Rwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti,naomba nijibiwe maombi haya kwa maandishi. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kufikia hatua hii ya kuhitimisha hoja ya bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika dunia hii nina madeni makubwa kwa watu sita. Kwanza ni Mwenyezi Mungu, ninamshukuru sana kwa wema wake ninamshukuru sana kwa kutujalia uzima tukaweza kufika mahali hapa jioni hii kwa ajili ya kuhitimisha hoja ambayo umenipa nafasi ya kutoa ufafanuzi kwa michango ya Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuniamini lakini pia kwa niaba yake nipokee pongezi nyingi sana ambazo Waheshimiwa Wabunge kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI mmezielekeza kwa Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa nzuri ya kuliongoza Taifa letu ambayo anaifanya na ninyi ni mashuhuda kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Rais wetu ameupiga mwingi sana kwenye mitaa na vijiji, vijijini na mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nitumie nafasi hii kulishukuru Bunge lako Tukufu kwa namna ambavyo mnaisaidia Serikali katika kutimiza wajibu wake, binafsi nikushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Spika pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa kweli deni ambalo ninalo kwenu pamoja na Mheshimiwa Rais na Watanzania ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mijadala hii mmenikumbusha kwamba imani hii ambayo mnayo kwangu, Waheshimiwa Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na Wataalam wote ambao wako chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kweli kwa niaba yao niwaahidi hatutawaangusha. Tutalinda imani hii kwa kufanya kazi kwa bidii na weledi mkubwa ili tusimuangushe Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, tusiliangushe Bunge lako Tukufu pamoja na Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika shukrani zangu niwashukuru sana wananchi wangu, mabosi wangu, wananchi wa Karagwe kwa kuendelea kuniamini katika majukumu yangu ya kuwawakilisha hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika shukrani zangu pia niishukuru familia yangu kwa kuendelea kuniombea na kuniunga mkono katika majukumu yangu ya kulisaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee ninakupongeza wewe binafsi pamoja na Mheshimiwa Spika, Wenyeviti, Wabunge kwa uongozi wenu mahiri uliouwezesha Bunge lako Tukufu kujadili bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa weledi mkubwa. Ninawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii na wale ambao hawakupata fursa ya kuchangia kutokana na sababu mbalimbali likiwemo suala la muda. Maoni na ushauri uliotolelewa na Waheshimiwa Wabunge umesaidia kutoa mwelekeo wa kuboresha mpango wa bajeti ili kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa nimpongeze tena Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kuwezesha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, taasisi zilizo chini yake, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kutekeleza majukumu yake katika kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipoishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa inayoongozwa na Mheshimiwa Abdallah Chaurembo, Mbunge wa Jimbo la Mbagala, Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi, Wajumbe wa Kamati na Sekretarieti kwa uchambuzi makini wa Mafungu 28 ya bajeti yanayosimamiwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kimsingi pongezi nyingi ambazo Ofisi ya Rais, TAMISEMI imepata katika utendaji wake zinatokana na ushirikiano mkubwa wa Kamati ya USEMI na Kamati ya LAAC chini ya Mheshimiwa Grace Tendega Mwenyekiti na Mheshimiwa Selemani Zedi Makamu Mwenyekiti, tunawashukuru sana kwa namna ambavyo mnatusimamia katika kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutambua mchango mkubwa wa viongozi wenzangu katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kipekee nawashukuru sana Naibu Mawaziri Mheshimwia Dkt. Festo Dugange, Mbunge wa Jimbo la Wanging’ombe na Mheshimiwa David Silinde, Mbunge wa Jimbo la Tunduma na Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa Tanzania Bara kwa msaada wanaonipa katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Profesa Shemdoe na Manaibu Makatibu Wakuu kwa mchango wao katika kufanikisha maandalizi ya mpango wa bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, bosi wangu, nakushukuru sana kwa namna unavyotuongoza. Ninakushukuru sana kwa maelekezo ambayo unaipatia Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuwahudumia Watanzania. Kwa hiyo pongezi hizi ambazo tumezipata na Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Waziri Mkuu pia zije kwako unatusimamia vizuri, wewe ni Kiongozi mahiri, tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo hoja mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezizungumza. Ninawashukuru Manaibu Mawaziri kwa ufafanuzi mzuri na mimi naomba kwa muda ambao umenipa nitoe ufafanuzi kwa hoja mbalimbali na nianze na hoja ambayo pamoja na kwamba haikutokea kwenye Bunge hili lakini mitandaoni kulikuwa na sintofahamu. Suala la ununuzi wa pikipiki 68 za Maafisa Ustawi wa Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge tarehe 14 mwezi Aprili, 2022 niliwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023. Katika eneo la utekelezaji wa bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022, sehemu ya huduma ya Ustawi wa Jamii nilisoma kwamba, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imefanya ununuzi wa pikipiki 68 aina ya boxer zenye thamani ya Shilingi Milioni 789.9 kwa ajili ya Maafisa Ustawi wa Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge ninaomba kutoa taarifa kwamba idadi ya pikipiki 68 iliyotajwa kwenye Hotuba yangu siyo sahihi na hii imetokana na makosa ya kiuandishi. Usahihi ni kwamba pikipiki 68 zimenunuliwa na wadau kwa gharama ya Shilingi Milioni 227.5 ambao walikuwa wanatekeleza miradi ya USAID Kizazi Kipya, katika baadhi ya Halmashauri katika Mikoa 21 ambazo zilinunuliwa na kusambazwa mwezi Septemba mwaka jana, 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa lengo la kutosheleza mahitaji ya pikipiki kwa Maafisa Ustawi wa Jamii, Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliona inunue pikipiki 200 aina ya boxer, kwa sasa ziko katika hatua ya mwisho ya manunuzi. Pikipiki hizi zinanunuliwa kupitia fedha za mpango wa maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO-19 kwa gharama ya Shilingi Milioni 562.4. Pikipiki hizo zitasambazwa kwenye maeneo ambayo hayakupata kwenye mgao wa pikipiki 68. Hivyo jumla ya pikipiki zitakuwa 268.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kwamba ofisi ya Rais, TAMISEMI imenunua pikipiki moja kwa Shilingi Milioni 11 siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la miundombinu ya wafanyabiashara wadogo yaani machinga. Waheshimiwa Wabunge hapa Dodoma tunayo tuiite modal ya soko la machinga ambalo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge, Kamati ya USEMI mlipata fursa ya kutembelea soko hili na ninaamini hata Waheshimiwa Wabunge katika zunguka zunguka yenu mmeshapata fursa ya kuangalia soko hili ambalo linajengwa nasi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa niaba ya Serikali na kwa ushauri wa Bunge kupitia Kamati ya USEMI tumeona ni vyema soko lile ambalo wote tumependezwa nalo tutafute master plan na tutengeneze standard ambayo kwenye Majiji na Manispaa tutakuwa tunajenga masoko ya wazi ya machinga kama hili ya Dodoma ili wafanyabiashara wadogo wamachinga waweze kuwa na maeneo rafiki ya kufanyia biashara zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha miundombinu ya kufanyia biashara kwa wafanyabiashara wadogo - machinga, Serikali imechukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha shughuli zao zinafanyika kwa tija. Hatua ambazo zimechukuliwa ni pamoja na kuwapanga machinga kwenye maeneo rasmi kwa utulivu pasipo kutumia nguvu katika Halmashauri zote zilizokuwa na machinga wengi kupitia Ofisi za Wakuu wa Mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine iliyochukuliwa ni Serikali kutoa Shilingi Bilioni Tano kwa ajili ya kuboresha maeneo ya kufanyia biashara machinga katika Halmashauri 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine inayoendelea ni kuwepo kwa majadiliano na Wizara ya Fedha na Mipango ili kufanya marekebisho ya Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura Na. 290 ili kuruhusu sehemu ya fedha za mikopo ya asilimia 10 kutumika katika kuboresha miundombinu ya machinga. Marekebisho ya sheria hii yamependekezwa kufanyika kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2022. Majadiliano hayo yakikamilika, tunatarajia kiasi cha Shilingi Bilioni 38 zitapatikana kupitia mlango huo kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya wafanyabiashara wadogo yaani machinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo kingine cha mapato kinachotarajiwa ni kupitia asilimia 10 ya fedha zilizotengwa kwenye miradi ya maendeleo ya mapato ya ndani ya Halmashauri. Kupitia chanzo hiki kiasi cha Shilingi Bilioni 36.82 kinakadiriwa kupatikana. Mapendekezo ya kutumia asilimia 10 ya fedha za miradi ya maendeleo zinalenga kuhusisha Halmashauri zenye mapato yanayozidi shilingi bilioni tano pamoja na Halmashauri nyingine ambazo zimejumuishwa kwenye mpango wa kuboresha maeneo ya machinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia vyanzo hivyo, Halmashauri zitakusanya jumla ya shilingi bilioni 74.83 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya machinga. Jumla ya fedha itakayotumika katika kuboresha miundombinu hiyo itakuwa shilingi bilioni 79.83 ikijumuisha shilingi bilioni tano ambazo zimekwishatolewa na Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kama seed capital.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge katika hii seed capital ambayo Mheshimiwa Rais ametupatia shilingi bilioni tano ndipo tumekaa na Wizara ya Fedha na Mipango kuangalia vyanzo vingine ambavyo vitadunduliza kwenye hii Bilioni Tano ili tuweze kujenga miundombinu ya masoko ya wazi ya wamachinga kwenye Majiji, Manispaa na hata baadhi ya Halmashauri za Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua mchango mkubwa wa kundi hili katika kukuza uchumi, hivyo ninapenda nitumie fursa hii kuwaelekeza viongozi wote wa Mikoa, Wilaya na Halmashauri kuhakikisha vitendo vya kuwanyanyasa machinga na kutumia nguvu katika kuwaondoa na kuwapanga ikiwemo kuharibu bidhaa zao kama ilivyotokea kwa Jiji la Mwanza vinakomeshwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu tangazo la ajira. Naomba nitumie fursa hii kwanza kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa idhini ya ajira za watumishi wa sekta ya elimu na afya 17,412 ambapo nafasi 9,800 ni za Walimu na 7,612 ni Kada za Afya ambao watatarajiwa katika Mwaka huu wa Fedha 2021/2022, wataajiriwa Mwaka huu wa Fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa taarifa rasmi kuwa watanzania wenye sifa wanaelekezwa kuanza kuomba kuanzia leo. Napenda kuwaelekeza kuwa maombi ya ajira hizi ni bure na yanafanyika kupitia mfumo wa kieletroniki ambao maelekezo yake yatakuwa katika tangazo la ajira. Asilimia tatu ya ajira hizo ni kuajiri ndugu zetu wenye ulemavu kulingana na sheria inavyotutaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaelekeza Wakurugenzi wote wa Halmashauri kuhakikisha wanawanunulia ndugu zetu watu wenye ulemavu mafuta kwa ajili ya sun screen. Jambo hili Mheshimiwa dada yangu Mheshimiwa Stella Ikupa alichangia kwa hisia na uchungu mkubwa. Tumekusikia Dada yangu kwa niaba ya ndugu zetu hawa wenye uhitaji huu, sasa nitumie nafasi hii kuwaelekeza Halmashauri zote kuhakikisha mafuta haya yanapatikana kwa ndugu zetu hawa wenye uhitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu TARURA. Nitumie fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa pongezi walizozitoa kufuatia utekelezaji wa agizo la TARURA kuanza mapema ununuzi wa mikataba ya utekelezaji wa miradi ya barabara. Katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 ununuzi wa kazi utaanza mwanzoni mwa mwezi Mei. Waheshimiwa Wabunge katika hili yani nikimaliza kusoma bajeti na mkatupitishia, TARURA wanaanza maandalizi ya manunuzi, tofauti na zamani bajeti inapitishwa, Mwaka wa Fedha unaanza, mikataba inachelewa kusainiwa na mahali pengine wakandarasi wanaenda mvua zimeanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo Waheshimiwa Wabunge baada ya kuja kwenye Wizara hii tulivyofanya study tukakuta TANROADS wao wamekuwa wakitumia utaratibu huu kwa miaka mingi sana. Kwa hiyo, tukaona hata TARURA, bajeti tuu inapopitishwa na Waheshimiwa Wabunge niwaombe sana mtusaidie mtupitishie bajeti hii ili kesho TARURA waanze kujipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha ugawaji wa rasilimalifedha za TARURA, inafanya mapitio ya formula itakayotumika katika kugawa rasilimali fedha za ujenzi wa matengenezo ya miundombinu ya barabara kulingana na hali ya maeneo husika. Jambo hili Waheshimiwa Wabunge mmetueleza sana kwa hiyo naomba muendelee kutupa ushirikiano tutalifanya kwa tathmini ya kina ili kuwe kuna formular kulingana na jiografia na ukubwa wa uhitaji katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuleta weledi na usimamizi makini tutapima utendaji kazi za Mameneja wa TARURA ngazi za Mikoa na Wilaya na nimeagiza kila quota niwe napata taarifa ya utekelezaji wa miradi ya barabara kwenye Wilaya zetu. Kutokana na taarifa hiyo tutaweza kuchukua hatua kwa wale Regional Managers na District Managers ambao watakuwa hawatoshi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niwashukuru sana kwa namna ambavyo mnaendelea kushirikiana na sisi, mnapoona kuna kasoro kwenye maeneo yetu tupeni taarifa ili tuweze kuchukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana Mheshimiwa Zeeland baada ya kufanya ziara kule Mvomero, nilitoa maagizo Machi 10, jana katika mchango wake akanitaarifu kwamba yale maagizo ambayo nilikuwa nimeyatoa kule Mvomero hayajafanyiwa kazi, leo mmeona hatua ambazo nimechukua. Kwa hiyo niendelee kuwaelekeza Wakurugenzi wawe makini tumewaamini katika kusimamia Halmashauri hizi, Mheshimiwa Rais wetu, mpambanaji wetu, mnaona ninyi ni mashahidi Waheshimiwa Wabunge miradi inatiririka kwenye Majimbo yetu haijapata kutokea. Kwa hiyo, lazima tushirikiane Waheshimiwa Wabunge katika kuhakikisha fedha hizi zinapoenda zinasimamiwa kikamilifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami kwa ushirikiano wenu ninawaahidi wale Wakurugenzi ambao watakuwa wanatimiza wajibu wao, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutakuwa wabunifu katika kuwa-recognize kwa kazi nzuri ambayo wanafanya, wale ambao watakuwa ni wazembe tutaendelea kuchukua hatua kama mlivyoona leo kule Mvomero. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ufuatiliaji na tathmini, uratibu katika ngazi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mikoa na Halmashauri. Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuimarisha ufuatiliaji na tathmini katika ngazi za Makao Makuu, Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuimarisha usimamizi kwenye Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Rais amemteua Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Sekta za Uchumi na Uzalishaji kama ilivyo Sekta ya Elimu na Afya. Waheshimiwa Wabunge kama mnavyofahamu pale TAMISEMI tunae Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya Elimu, tunaye Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya Afya na Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo mmetueleza kwamba Wizara hii inamgusa kila mwananchi ilimpendeza akatuongezea Naibu Katibu Mkuu ambae anashughulikia masuala ya Utawala yaani ya TAMISEMI. Sambamba na hilo kama mlivyochangia productive sectors, sectors ambazo zinazalisha na kwa sababu TAMISEMI ndiye mratibu mkuu wa miradi ya kisekta, Naibu Katibu Mkuu huyu pia anajukumu hilo, kwa hiyo ningependa kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ambazo zinazalisha Mheshimiwa Bashe, Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Ndaki, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa shemeji yangu Dokta Kijaji, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, tunaendelea kushirikiana ili hizi productive sectors sisi TAMISEMI kwa sababu utekelezaji wote unafanyika ngazi za Halmashauri, tuji- coordinate vizuri ili kuhakikisha vipaumbele vyao na bajeti zao ambazo wanazitenga kupitia Idara hii ambayo inasimamiwa na Naibu Katibu Mkuu huyu ambaye Mheshimiwa Rais ametupatia tuweze kuwasaidia wenzetu ambao wanasimamia sekta za uzalishaji kuhakikisha vipaumbele vyetu na vya kwao vinasomana ili kupeleka huduma bora kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge kwenye hili tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutuwezesha kupata hii additional manpower na nimpongeze Dokta Sweetbert Mukama anafanya kazi nzuri kwa kushirikiana na Naibu Makatibu Wakuu na Katibu Mkuu. Kwa hiyo, tutaendelea kupitia Idara hiyo kuweza kutoa huduma hata kwenye productive sectors. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa Fedha 2022/2023 Serikali imeongeza bajeti ya matumizi mengineyo katika Ofisi za Wakuu wa Mikoa kutoka Bilioni 57.44 hadi Shilingi Bilioni 79.09 ili kuwezesha utekelezaji wa majukumu ya ofisi hizo ikiwemo ufuatiliaji na usimamizi wa shughuli za Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya hivyo na tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutuwezesha. Ofisi ya Rais, TAMISEMI hatuwezi kwenda na manual system, yaani Waziri likitokea jambo Katavi kule toka Dodoma unakimbia na wakati kuna RC ngazi ya Mikoa kwa maana ya Tawala za Mikoa lakini ngazi ya Serikali za Mitaa yuko Mkuu wa Wilaya, kwa hiyo mkakati ambao tunao na tumeanza kuufanyia kazi ni kuhakikisha tuna-strengthen Regional Secretariat pia hata Halmashauri zetu CMT ili kuweza kusimamia miradi kwa kufuata mtiririko huo wa mifumo na changamoto ambazo ziko kwenye mifumo tunazirekebisha. Hii in the long term itasaidia sana kuwa kuna mifumo na structure ya Serikali ambayo badala ya ku-divert yaani Wizara inafanya kila kitu kwenye vijiji, mitaa, tuna-strengthen Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ili sasa structure ya utumishi iweze kufanyakazi kwa weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hii pia ndiyo imepelekea kwanza tuwawezeshe Sekretarieti za Mikoa, sasa tuwadai kazi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala kazi kwenu. Waheshimiwa Wabunge wakitupitishia bajeti hapa tumewaongezea bajeti, matararajio yangu ni kwamba hamtakuwa mnafanya basic work mtakuwa mnaenda kwenye Halmashauri na kusimamia miradi ku-monitor na ku-evaluate na kutoa taarifa ili wale wanaofanya vizuri tuwape promotion tuwape recognition na wanaofanya vibaya tuweze kuchukua hatua stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeimarisha mfumo wa kupima utendaji wa Wakurugenzi na Wakuu wa Idara kwa kutumia viashiria muhimu yani KPI’s ukusanyaji wa mapato ya ndani ni moja ya kigezo, upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo ni kipimo kingine, matumizi sahihi ya fedha hizo ni kipimo kingine, usimamizi wa mikopo ya asilimia 10 ikiwa ni pamoja na marejesho ni sehemu ya kipimo, usimamizi wa miradi ya maendeleo na uzuiaji na utekelezaji wa hoja za CAG ni moja ya vipimo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye quarterly report ambazo nitakuwa nasoma za mapato tunabadilisha mfumo kidogo tutakuwa tunatoa grade, zipo Halmashauri zitapata A, zipo zitakazopata B, C sasa watakaopata mswaki ndiyo kama yaleyale ya hati chafu, ni kuwachukulia hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia KPI’s hizi hata Mkurugenzi anaweza akajipima kabla hajachukuliwa hatua yuko wapi katika kusimamia miradi na vigezo hivi ambavyo tumeviweka. Ofisi ya Rais, TAMISEMI nimezungumzia hizo KPI’S na matokeo ya upimaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na Mamlaka za Serikali Mitandao yani e-GA tumeanza kuboresha mfumo huu ili kuwezesha kutumika kwa urahisi kwa vituo vyote 5934 vya Serikali hususani hivi vilivyopo vijijjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwezo wa kuunganika na kusomana na mifumo ya Kitaifa ili tuweze kupata taarifa na takwimu ngazi ya Taifa na kuhakikisha usalama wake wa mifumo hii na database. Lengo la Ofisi ya Rais -TAMISEMI ni kuweka mfumo huu kwenye vituo vyote ifikapo mwaka 2024/ 2025 kazi hii itafanywa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo na kusimamiwa na Ofisi za Wakuu wa Mikoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hatua za kinidhani kwa watumishi. Ofisi ya Rais - TAMISEMI katika kusimamia masuala ya nidhamu na maadili ya kazi katika Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa, imekuwa ikichukuwa hatua za kinidhamu kwa watumishi wanaokiuka sheria na taratibu za kazi ikiwemo ubadhilifu, uzembe, ukiukwaji wa maadali ya kazi na taaluma zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Ofisi ya Rais -TAMISEMI imewasimamisha kazi Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Wanne, imewashusha vyeo Waganga Wakuu wa Mikoa wawili, Waganga wa Wakuu wa Halmashauri - 14, Afisa Elimu Mkoa - Mmoja, Maafisa Elimu ngazi ya Wilaya - Tisa na Wakuu wa Vitengo vya Manunuzi ngazi ya Halmashauri - 24.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa wito kwa watumishi wote wa umma kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za utumishi wa umma, ninazielekeza Mamlaka za Nidhamu kuhakikisha zinachukuwa hatua stahiki kwa wale ambao wamebainika kukiuka taratibu. Serikali itaendelea kuwachukulia hatua kali wale wote watakaobainika kukiuka taratibu za maadali ya kazi na taaluma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ujenzi wa Vituo vya Afya vya Tarafa na Kata za Kimkakati. Ofisi ya Rais – TAMISEMI inatambua umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika uendelezaji wa miundombinu sambamba na kuiwezesha kutoa huduma za afya kwa kuwa na vifaatiba na watumishi. Katika kutekeleza hilo Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeweza kufanya tathmini ya uhitaji wa vituo vya afya 428 ambapo vitajengwa kwa kipindi cha miaka mitatu ijayo kuanzia mwaka wa fedha 2022/2023 ambavyo vitajengwa katika Tarafa zisizokuwa na Vituo vya Afya na Kata za kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge kwenye hili Ofisi ya Rais -TAMISEMI tulileta fomu mkajaza zile Tarafa ambazo hazijapata vituo vya afya lakini zile Tarafa ambazo zimeshapata vituo vya afya maeneo ambayo ni kimkakati yanahitaji kupewa vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuahidi pamoja na Bunge lako Tukufu, kipaumbele ambacho tumejiwekea, mwaka huu na niwashukuru sana mmeunga mkono jambo hili tukamilishe maboma lakini kuanzia Mwaka wa Fedha 2023/2024 tuende sasa kwenye zile fomu ambazo mlijaza maeneo ambayo yanahitaji vituo vya afya tuendelee na utaratibu huo wa kujenga kuhakikisha vinapokamilika vinapata vitendea kazi na masuala ya Wauguzi. Hivyo, Waheshimiwa Wabunge niwashukuru kwa kuunga mkono mkakati wetu wa kwamba mwaka huu kipaumbele kikubwa kiwe kwenye kukamilisha maboma.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Rais ameshatupatia fedha tuko hatua za uzabuni wa kununua vifaatiba kama hivi mnaona tumeajiri na tutaendelea kuajiri kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ukarabati wa Shule, Vituo vya Afya na Zahanati Kongwe. Kwa Mwaka wa Fedha 2015/2016 mpaka 2021/2022, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeweza kufanya ukarabati wa Shule Kongwe za Sekondari 89 kati ya shule 92. Kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 Ofisi ya Rais- TAMISEMI imepanga kufanya kukarabati wa Shule za Msingi Kongwe jumla ya Shule zilizoanza kabla ya mwaka 1961 ni shule 2,147. Shule hizi zitakarabatiwa kwa awamu baada ya kukamilisha tathmini ya gharama za ukarabati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukarabati huu ni endelevu katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 jumla ya vyumba vya madarasa 1,700 vya shule za msingi kongwe ambavyo vimetengewa jumla ya shilingi bilioni 34 vitakarabatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa afya ya msingi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imepanga kufanya ukarabati wa Hospitali za Halmashauri Kongwe 19 kati ya hospitali 77, ambapo jumla ya Shilingi Bilioni 16.55 zimetengwa. Ofisi ya Rais - TAMISEMI itafanya zoezi la kutambua vituo vya afya na zahanati zilizojengwa kati ya mwaka 1961 hadi 1970 ili kuweka mkakati wa kuvikarabati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge haya ni maelekezo yenu tumewasikia tunaenda kufanya tathmini ili kuweka kwenye vipaumbele kwenye mwaka wa fedha unaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ukamilishaji wa miradi iliyoanzishwa na kutokamilika. Ofisi ya Rais-TAMISEMI inakubaliana na hoja za Waheshimiwa Wabunge za kuwepo kwa miradi iliyoanzishwa miaka ya nyuma na bado haijakamilika ninapenda kuwaelekeza Wakuu wa Mikoa wote Tanzania Bara kuhakikisha wanawasilisha taarifa ya kina kuhusu miradi na gharama zake za ukamilishaji ili Ofisi ya Rais- TAMISEMI iweze kuitambua miradi hiyo na kuweka mikakati ya ukamilishaji wake, taarifa hiyo iwasilishwe kabla au ifikapo tarehe 30 Juni mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakubaliana na hoja za Waheshimiwa Wabunge kuhusu ukosefu wa vifaa na vifaatiba katika vituo vya afya vilivyokamilika kujengwa. Kuanzia Mwaka wa Fedha 2018/2019 hadi Mwaka wa Fedha 2021/ 2022 Serikali imetoa kiasi cha Shilingi Bilioni 82.9 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na vifaatiba katika ngazi ya Afya na Msingi ambapo Shilingi Bilioni 15 zimetumika kununua vifaa na vifaatiba na kuvisambaza katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, vifaa vingine manunuzi yake yanaendelea, vifaa hivi vinajumuisha vifaa na vifaatiba kwa ajili ya utoaji wa huduma za upasuaji na huduma za mionzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 imetenga Shilingi Billion 47. 7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwenye vituo vya afya 159, Ofisi ya Rais - TAMISEMI inafuatilia vifaa na vifaatiba ambavyo tayari vimeshalipiwa fedha kutoka Bohari Kuu ya MSD ili kuondoa changamoto ya vituo vya afya vilivyokamilika na kukosa huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuimarisha makusanyo ya mapato ya ndani ya Halmashauri. Ofisi ya Rais - TAMISEMI itaendela kuzisimamia halmashauri ili ziongeze wigo wa ukusanyaji wa mapato ya ndani. Mikakati iliyowekwa ni pamoja na kuwajengea uwezo Maafisa wanaokusanya mapato, kuboresha mfumo mapato na utambuzi wa fursa na ujibuji wa vyanzo vipya vya mapato. Aidha utendaji wa Halmashauri utapimwa kuzingatia upelekeji wa asilimia 40 kwa 60 na 70 kwa Halmashauri hizi chache zenye makusanyo makubwa zinazotokana na makusanyo ya mapato ya ndani yasiyolindwa katika miradi ya maendeleo, utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi vya wanawake, viijana na watu wenye ulemavu na ulejeshaji wa mikopo na ujibuji wa hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa wakati na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha za umma ili kuleta tija na kuimarisha utoaji huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Halmashauri ziliidhinishwa kukusanya shilingi bilioni 863.85 kutoka katika vyanzo vya mapato ya ndani. Hadi Februari 2022 zimekusanya shilingi bilioni 586.07 sawa na asilimia 68. Fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ni shilingi bilioni 331.08 hadi Februari 2022, shilingi bilioni 216.11 sawa na asilimia 65.27. Ofisi ya Rais - TAMISEMI itaendelea kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha fedha zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo zinapelekwa kwa wakati katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais -TAMISEMI katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 imepanga kuongeza mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za Mitaa kufikia shilingi trilioni 1.1 sawa na ongezo la asilimia 17.18. Mafanikio haya yatafikiwa kwa kila mmoja kutekeleza majukumu yake, kufanya ufuatiliaji mara kwa mara, fedha zote zinakusanywa

kuingizwa benki kabla ya matumizi, vyanzo vyote kuwa na POS katika kukusanya mapato, kufanya tathmini ya wadaiwa na kuweka mikakati ya kukusanya madeni hayo na matumizi sahihi ya mifumo ya kieletroniki ikiwemo mfumo wa TAUSI, GoTHoMIS katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, matumizi sahihi ya mashine za kukusanyia mapato (POS) ni muhimu hivyo ninaelekeza kila Mkoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kufanya yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhakikisha POS zote hasa zile za zamani kabla ya mwaka 2019 zinawekewa toleo jipya la APK Toleo la 499649 ili kuondoa mianya ya kupoteza mapato.

Mbili; kufanyika kwa ukaguzi wa POS kila mwezi ili kubaini POS zipo ngapi, zipo wapi, ngapi zipo online, ni nani wanaozitumia.

Tatu; Kuhakikisha POS zote ambazo haziko hewani ziko offline kutokana na ubovu au kutojulikana zilipo zinafifishwa kwenye mfumo yani zinakuwa di-activated.

Nne; kufanya job rotation kuzungusha wanaosimamia ecosystem nzima ya ukusanyaji wa mapato Wahasibu na wengine.

Tano; kuhakikisha mapungufu ya POS kwenye maeneo ya ukusanyaji yanabainika na mkakati wa kununua POS unawekwa kukidhi mapungufu hayo ili kuongeza mapato.

Sita; Kuhakikisha register zote za POS zinahuishwa kuendana na taarifa za mfumo kwa usahihi kutoa hamasa ya kudai risiti kwa kila huduma kutoka kwa mkusanya mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais -TAMISEMI inahuisha mfumo wa ukusanyaji mapato wa TAUSI ambao utafanya yafuatayo: -

i. Usimamizi wa POS, maboresho ya POS na changamoto zake sasa mfumo huu wa tausi unaenda kutibu yale mapungufu ambayo tumeya-experience kwenye mfumo wa POS.

ii. Usimamizi wa float ili kuondoa matumizi ya fedha mbichi na kuondoa madeni ya float management.

iii. Kuhamasisha malipo ya kodi, tozo na ushuru, kwa kielektroniki bila kufika ofisi za Mamlaka za Serikali za Mitaa yani online payment kwa maana ya caShless system.

iv. Kujifanyia tathmini ya kiasi mlipaji anachopaswa kulipa (online assessment)

v. Kutoa leseni na vibali vya kieletroniki digital license na permit.

vi. Kuunganisha mfumo na mifumo ya TRA kupata mapato ghafi ya wafanyabiashara kwa ajili ya kupata kodi halisi ya huduma (service levy).

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na Mamlaka za Serikali za Mitaa Mtandao inaendelea kuboresha mfumo wa GoTHOMIS ili uweze kutumika na vituo vyote vya kutoa huduma za afya vya ngazi ya msingi, hasa maeneo ya vijijini, maboresho yatazingatia maelekezo yaliyotolewa na Mheshimiwa Rais kuhusu kuimarisha mifumo ili izungumze. Mfumo huu unasaidia kusimamia na kudhibiti madawa na vifaatiba, kutoa taarifa ya magonjwa na ugonjwa na kusimamia mapato yatokanayo na uchangiaji wa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo kwa sasa upo kwenye vituo 1,161 na utawekwa kwenye vituo vyote vya afya ifikapo Mwaka wa Fedha 2015/2016. Kuhusu Serikali itoe waraka mpya wa posho za Madiwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri mwenye dhamana za Serikali za Mitaa alishatoa waraka wenye kumbukumbu ya tarehe 23 mwezi wa 12 mwaka 2014 juu ya posho za mwezi za Madiwani. Aidha posho za vikao za Waheshimiwa Madiwani zimeelekezwa katika waraka uliotolewa mwaka 2007 na kusitishwa katika waraka wa tarehe 16 Agosti, 2012 ambapo ni Shilingi 40,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo posho za Waheshimiwa Madiwani ni hisani ya Mkurugenzi wa Halmashauri. Kwa sasa tunaandaa miongozo Waheshimiwa Wabunge ili kuhakikisha posho za vikao za Waheshimiwa Madiwani mwongozo huu tutafanya tathmini ili kuhakikisha angalau kunakuwa kuna mfanano nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiti chako kilishatoa mwongozo kuhusu masuala yanayohusu stahiki za Waheshimiwa Madiwani kupitia Kamati ya Bajeti yataendelea kujadiliwa ili kuweza kuhakikisha tunajenga mustakabali mzuri Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Madiwani katika kuhakikisha tunatekeleza ilani ya Chama chetu vema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Kamati ya Fedha peke yake kukagua miradi katika Halmashauri zetu. Kamati za Kudumu za Halmashauri zinaweza kutembelea miradi ya maendeleo au shughuli yeyote inayotekelezwa kwa niaba ya Halmashauri na ambayo inahusu Kamati husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri nyingi Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango ndiyo imebeba jukumu hilo peke yake kitu ambacho ni kinyume na Kanuni za Kudumu za Halmashauri. Waheshimiwa Wabunge jambo hili mmelizungumza tutakaa tulitathmini ili tuweze kulitolea mwongozo mzuri, kwa sababu kamati zote ziliundwa kwa kuleta weledi katika kusimamia miradi, kwa hiyo tungependa kuona kamati zote zinatimiza wajibu wake kulingana na mgawanyiko wa majukumu katika halmashauri zetu, kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge ili tumelichukuwa tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoanza nashukuru sana, nikushukuru wewe nimshukuru Mheshimiwa Spika, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu mizuri, tumewasikia hoja zote ambazo mmechangia tumezichukua na kwa ushirikiano ambao mmeendelea kutupatia niwahakikishie mimi pamoja na Waheshimiwa Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na timu nzima ya Watumishi wa Ofisi ya Rais - TAMISEMI tutaendelea kuwapa ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha yale ambayo mmetuelekeza, mmetushauri tunayaweka katika utekelezaji wa Serikali na kuhakikisha mwaka wa fedha utakaokuja zile hoja ambazo mmezieleza hapa na tumezichukua tunazitekeleza kwa weledi mkubwa ili tutakaporudi hapa tusiwe tuna maswali mengi ya viporo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitumie nafasi hii na Waheshimiwa Wabunge kuwashukuru sana na mimi nawaahidi ushirikiano uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na afya, pili ninakushukuru sana kwa namna ambavyo unaendesha vikao nakupongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na mdogo wangu Mheshimiwa Deo Ndejembi, kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kuongoza Wizara ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, tunawapongeza sana kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuliongoza Taifa letu, pia nitumie nafasi hii kuwashukuru tena Waheshimiwa Wabunge kwa kutuwezesha kupitisha bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, bajeti ambayo tunaenda kuitekeleza kwa nguvu na jitihada kubwa tukishirikiana na nyinyi. Bajeti ya Utumishi ni bajeti ambayo inasomana kwa karibu sana na bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa hiyo nashukuru kupata fursa hii ili niweze ku-clarify baadhi ya mambo ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeyajadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la ajira. Katika hili ninamshukuru sana Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutupa kibali cha kuajiri Walimu 9,800, kwenye upande wa afya kuajiri Wauguzi 7,612. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kutupa kibali hiki, tunaenda sasa kuajiri vijana wetu ambao wamekuwa wakisubiri ajira kwa muda mrefu. Kwa hiyo, watapata fursa lakini pia tunaenda kupunguza uhitaji wa mahitaji ya Walimu na Wauguzi katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili Waheshimiwa Wabunge ningependa niwaondoe wasiwasi, mfumo wa kuomba ajira wa online kwa siku ya mwanzo kwa sababu wanaoomba ni wengi, kumekuwa kuna changamoto ya mambo ya mtandao lakini timu yangu inafanyakazi kwa jitihada kubwa kuhakikisha wanoomba huduma ya kuomba kupitia mtandao inaenda vizuri, nami baada ya kutoka hapa naenda kwenye eneo ambalo wanafanyia kazi kujiridhisha marekebisho haya yafanyike ili wale wanaoomba hizi ajira waweze kuomba kwa urahisi sana kupitia mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa ajira Waheshimiwa Wabunge utaratibu uliopo na application ya mtandaoni imezingatia uhitaji wa ajira kwenye maeneo. Kama ni upande wa Wauguzi, kama ni upande wa Walimu imeangalia mahitaji ya nchi nzima, kwa hiyo wanapoomba inapeleka pale ambapo pana uhitaji mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ningependa mtuamini kwamba utaratibu uliopo unaenda kukidhi maeneo ambayo yana mahitaji critical, lakini hoja ambayo tumeipata hapa ya kwamba ajira izingatie maeneo kwa maana ya Wilaya, Majimbo ni wazo lakini naomba mtupe nafasi upande wa Serikali tulichukue tukaliangalie, tuangalie namna ambavyo linaweza likatekelezeka au kama utaratibu uliopo unaweza ukaboreshwa ili kuweza kuzingatia hilo, hilo pia tutaliangalia Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa machinga ningependa nitumie nafasi hii kutoa maelezo kwa ufupi sana, nimpongeze Mheshimiwa Kaka yangu Mheshimiwa Gwajima amelielezea vizuri, Mheshimiwa Rais wetu maelekezo aliyoyatoa kwa wamachinga ni kuwawekea mazingira rafiki ya kufanyia kazi na kuwapanga kwa utaratibu ambao hatutumii msuli, kwa utaratibu ambao hatuchukui mali zao na kuzihodhi, kwa utaratibu ambao unajenga ustawi wa machinga huyu kuweza kufanya kazi kujipatia riziki, ku-support familia zao na kwa pamoja kama machinga waweze kusaidia katika kujenga uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni kundi ambalo tunalitambua na kulithamini kama Serikali. Serikali ya Awamu ya Sita kama nilivyoeleza kwenye bajeti yangu, pamoja na Bilioni Tano ambazo Mheshimiwa Rais ametupatia kwenda kujenga miundombinu hii rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Dodoma kama nilivyoeleza tunajenga Machinga Open Complex, Waheshimiwa Wabunge baadhi yenu mmetembelea eneo hili, kwa dhamira njema ya Mheshimiwa Rais wetu bilioni tano ambazo alizitoa tumekuja kujenga soko hili kama mfano lakini tunataka tuende kwenye Majiji, Manispaa na baadae hata kwenye Halmashauri za Mji ambazo zina Machinga wengi ili tuweze kujenga masoko ambayo ni rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningependa kutumia nafasi hii kutoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa, maelekezo haya yazingatiwe na nimeshaelekeza Wakuu wa Mikoa kwenye masuala ambayo yanahisia kama machinga, bodaboda, mama lishe, tufanye consultations kati ya Mikoa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili operation ambazo zitakuwa zinafanyika tuwe tunauelewa wa pamoja ili kuhakikisha usimamizi wake wa operation hizi uweze kuwa ni rafiki na kwa matarajio ambayo Serikali inataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali dhamira yake ni kuhakikisha tunaweka mazingira mazuri ya vijana wetu machinga akina Mama na Vijana ambao wanategemea sekta hii na tutaendelea kufanya sekta hii izidi kuwa Rafiki, izidi kuwa na matumaini kwa watu ambao wanaitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tunaendelea kufanya kila aina ya jitihada kujenga nyumba za watumishi, kwenye bajeti mmeona kwa mara ya kwanza bajeti ambayo tumeitenga kwa ajili ya kujenga nyumba za Walimu hasa hasa Walimu ambao wanaishi maeneo ya mbali. Jambo hili tumelizingatia kwenye bajeti na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kila mwaka wa fedha tutakuwa tunatenga fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za watumishi ili kupunguza uhitaji mkubwa wa nyumba za watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kengele ya kwanza muda bado ninao basi. Kuhusu upungufu wa watumishi nimeshasema Mheshimiwa Rais tunamshukuru ametupatia kibali kwa ajili ya kuajiri Walimu na Wauguzi

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upandishaji madaraja, katika hoja ambazo zimetoka kwa Waheshimiwa Wabunge tutaleta majibu kwa kila hoja, kwa kila Mbunge aliyechangia ikiwemo takwimu, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, kwa kipindi ambacho amekaa madarakani mwaka mmoja amepandisha madaraja kwenye Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa, pia kwenye arrears tumekuwa tukishirikiana vizuri na Ofisi ya Rais, Utumishi kukusanya arrears na kuwapelekea Hazina ili kuhakikisha malimbikizo ya mishahara kwa watumishi wetu yanalipwa. Kwa hiyo, jambo hili tutaendelea kushirikiana ili tuweze kuhakikisha wenye haki ya kupandishwa madaraja lakini pia wenye haki ya kulipwa malimbikizo wanapata haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeshakubaliana na Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama, baada ya kuhitimisha hotuba yake na nitumie nafasi hii kuwaomba sana Waheshimiwa Wabunge tumpitishie bajeti ili akaweze kutekeleza haya mengi mazuri ambayo yamesheheni katika bajeti yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekubaliana baada ya leo Wizara mbili zitakaa, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utumishi tujipange vizuri kwa mambo ambayo mmetuelekeza humu.

Tujipange vizuri katika kutekeleza bajeti zetu mbili kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge pamoja na kuchangia maeneo ambayo yamehusu Ofisi ya Rais, TAMISEMI niwahakikishie Mheshimiwa Dada Jenista ni role model wa Wabunge wengi sana humu na tunajivunia yuko hapo. Kwa hiyo, kwenye mambo ambayo mmezungumza hapa nasi kwa vile mlituunga mkono, mkapitisha bajeti yetu kwa kishindo, muamini Wizara hizi mbili kwa kweli tuna ushirikiano wa karibu, changamoto ambazo mmezitaja tutashirikiana katika kuhakikisha zinatekelezwa kwa manufaa ya wananchi wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na suala la posho za Watendaji wa Kata. Nitumie nafasi hii kuwaelekeza Wakurugenzi wote nchini

MWENYEKITI: Hilo nakuongezea dakika moja liongee vizuri hilo la Watendaji wa Kata.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Serikali ilitoa posho ya madaraka kwa Watendaji wa Kata 100,000 kwa mwezi na tukaelekeza Wakurugenzi kuhakikisha kila mwezi Mtendaji wa Kata anapata hii 100,000 iweze kumsaidia katika majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Halmashauri, Watendaji wa Kata wamekuwa wakifuatilia kana kwamba hii ni hisani. Kwa hiyo nitumie nafasi hii kuwaelekeza Wakurugenzi kote nchini kuhakikisha kila mwisho wa mwezi Mtendaji wa Kata anapata hii 100,000 akiwa kwenye Kata yake, kuondokana na adha ya kutoka kwenye Kata kwenda kwenye Halmashauri kudai hii posho kana kwamba ni hisani. Hii siyo hisani ni haki ya Watendaji wetu kwa hiyo, Wakurugenzi zingatieni hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili kwenye bajeti ijayo tunatambua kazi nzuri ambayo Watendaji wa Kata wanafanya, tutatenga bajeti kwa ajili ya kuwapa usafiri, katika hili nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan tunaona hata Wizara za kisekta Mheshimiwa Rais ametoa vibali kwa ajili ya kuhakikisha Maafisa Kilimo kwa upande wa kilimo wanapata usafiri, Maafisa Ugani na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwenye bajeti itakayokuja ya 2023/2024 tutahakikisha Watendaji wa Kata na wenyewe tunawapa kipaumbele katika kuhakikisha wanapata usafiri ili waendelee kufanya kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kuisimamia Serikali ngazi za Kata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyoko mezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri Lukuvi na Naibu Waziri Angeline Mabula kwa kazi nzuri wanayoifanya kuisimamia Wizara hii nyeti kwa Watanzania. Pia niendelee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuleta mabadiliko kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la migogoro ya ardhi katika Jimbo langu la Karagwe. Katika hili niishukuru Serikali kwa kuwa wasikivu kwani tayari Jimbo la Karagwe tumeshatembelewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kutatua migogoro ya ardhi na changamoto nyingine za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu alitutembelea, Mheshimiwa Profesa Muhongo, Mheshimiwa Mwijage, Manaibu watatu, kaka yangu Mheshimiwa Injinia Ramo, kaka yangu Mheshimiwa Masauni na Mheshimiwa Dkt. Kalemani. Hii ni kuonesha jinsi gani Serikali ya Awamu ya Tano inavyochapa kazi, tunawaunga mkono na kabla ya yote, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo matatu ya kuchangia na nianze na suala la land bank yaani benki ya ardhi. Upungufu wa viwanja vilivyopimwa ni changamoto ambayo iko nchi nzima na Serikali ya Awamu ya Tano kama wananchi wote wanavyofahamu ni Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda. Huu uchumi wa viwanda hatutaujenga mbinguni bali ni kwenye ardhi, kwa hiyo ni muhimu sana tukatatua migogoro ya ardhi kote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Mkoa wa Kagera, ukipata mwekezaji mkubwa bado tuna changamoto kubwa ya ardhi. Maeneo yanaonekana yapo, lakini ukienda kila sehemu wanakwambia eneo lina mtu, hatujatenga maeneo maalum kwa ajili ya kuvutia uwekezaji na kwa ajili ya kujenga makazi ambayo yana mipango mizuri. Ili sasa tuweze kuzuia ujenzi holela na migogoro ya ardhi, lazima tujipange tuhakikishe tuna benki ya ardhi kote nchini ikiwemo Mkoa wa Kagera. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa katika benki ya ardhi, naishauri Serikali tusiziachie tu Halmashauri zetu, iwe ni Sera ya Kitaifa ambayo inaratibiwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kushirikiana na Mikoa yetu na Halmashauri. Katika hili, ningetamani kuona Aprili mwakani tunapokuja Bungeni kama Mheshimiwa Waziri walivyofanya kazi nzuri ya kuorodhesha migogoro yote ya ardhi nchini, basi tuwe tuna mpango mkakati wa namna gani tutajipanga kuwa na benki ya ardhi kote nchini kwa kila Wilaya na Mkoa tuvione na kila Wizara isifanye kazi kwenye silos. Kama ni Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, vikae chini tuwe tuna-coherent plan kwa ajili ya land bank. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia ni National Housing. Kwanza nawapongeza sana National Housing kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwa kweli mkakati wao unaonesha kwamba hata Tanzania shirika letu hili linafanya kazi katika karne ya 21 kwa weledi mkubwa sana. Katika hili hazikosi changamoto, nionavyo National Housing imejikita vizuri sana katika kusaidia kujenga nyumba kwa ajili ya watu wenye kipato cha kati na cha juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili si jambo baya, lakini nipende kuipa changamoto National Housing pia waangalie ni namna gani kibiashara yaani rate of return iwepo, lakini tujikite kusaidia asilimia kubwa ya Watanzania ambao wako kwenye bottom ya population pyramid ili waweze kupata nyumba za bei nafuu. Katika hili lazima kuangalia watumishi na wafanyabiashara wadogo namna wanavyoweza ku-afford hizi nyumba za bei ya chini na zijengwe kote nchini ili kuondoa tatizo la ukosefu wa nyumba na ambazo ziko katika mipango miji mizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichangie katika suala la urasimishaji ardhi. MKURABITA imejitahidi lakini bado kuna changamoto kubwa kwani ukiangalia katika nchi nzima na kama hotuba ya Mheshimiwa Waziri inavyoonesha ni vijiji 11,778 tu ambavyo vimepata hati miliki. Tanzania sasa hivi tuna takribani watu milioni 50, hizi ni hati kidogo sana. Kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali tujikite kuhakikisha tunapima vijiji vingi kadri inavyowezekana kwani katika Serikali ya viwanda, wananchi wakishapata hizi hati wanaweza wakazitumia kama dhamana kukopa katika mabenki. Hivi tunavyojipanga kuanzisha benki mbalimbali kwa ajili ya kusaidia wananchi walio wengi ambao hawajiwezi basi kwa kuwa na hizi hati miliki tutakuwa tumewasaidia kupata dhamana ya kwenda kukopa kwenye mabenki ambayo yatakuwa na mikopo ya bei nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, MKURABITA kwa ushauri wangu napendekeza iwe chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa sababu ya uratibu. MKURABITA kama ikipata fedha za kutosha, sababu moja ya changamoto kwa mfano ni kufidia wananchi. Kuna ule mpango wa Land Tenure Support Program, inasikitisha kwamba kama wafadhili hawatupi hela basi hela inakuwa haipo ya kuendesha huu mpango. Kwa hiyo, niiombe Serikali mipango kama hii ambayo inapelekea wananchi wengi wa Tanzania kupata hati miliki waweze kuzitumia kama dhamana, tutafute kila mbinu kuhakikisha inapata fedha za kutosha na ardhi nchini zinapimwa kadri inavyowezekana ili tuweze kuwa na matumizi bora ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi ni hayo tu lakini sina shaka mipango ya Wizara yetu hii ni mizuri na naamini kabisa kama watafuata ushauri, basi mpango kazi wa mwaka 2016/2017 ukitekelezwa tutasonga kwa kasi kutatua changamoto za ardhi nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuhitimisha hotuba yangu. Kabla sijaendelea nianze kwa kukushukuru wewe kwa kuliongoza Bunge letu kwa weledi mkubwa. Nafahamu umekuwa kiongozi bora wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa vile pia kule Mbeya Mjini wananchi wanakupa ushirikiano. Natumia nafasi hii kuwashukuru Wanambeya Mjini na kuendelea kuwaomba waendelee kukupa ushirikiano, Taifa linakutegemea. Kwa kweli tunakushukuru sana kwa uongozi wako mahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naishukuru sana Kamati ya NUU inayoongozwa na Mheshimiwa Vita Kawawa, Makamu Mwenyekiti Vincent Mbogo pamoja na Wanakamati. Tunawashukuru sana kwa namna ambavyo mnaendelea kutuelekeza na kutushauri ili Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iendelee kuwa ni Wizara ambayo inamsaidia vyema Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao mmechangia katika kikao hiki. Tunawashukuru sana kwa ushauri wenu ulikuwa very constructive. Tunawashukuru kwa madini ambayo mmetupatia, yanaenda kutuimarisha kama Wizara ili tukajipange vizuri kuendelea kuhakikisha tunamsaidia Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, kuendelea kuyasaidia majeshi yetu, kuendelea kujenga ustawi na kujiimarisha.

Mheshimiwa Spika, kama Dada yangu Mheshimiwa Jesca alivyosema, pia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ni sehemu ya kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kama alivyoinukuu. Kwa hiyo, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa ushauri na maoni ambao ametupa. Nawashukuru hata wale ambao hawajapata nafasi ya kuchangia kwa sababu ushiriki wao na support yao kama tulivyo hapa ni sehemu ya mchango. Kwa hiyo, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, mpendwa wetu, Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kweli anafanya kila aina ya jitihada kuhakikisha majeshi yetu na vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kutimiza wajibu wake. Yapo mambo makubwa ambayo Mheshimiwa Rais anawezesha vyombo vya ulinzi na usalama, lakini kama mnavyojua, yapo ambayo tunaweza tukayaweka wazi na yapo ambayo yanaendelea kuwa classified, lakini Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu anafanya kazi kubwa sana ya kuviwezesha vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. Tunamshukuru.

Mheshimiwa Spika, vile vile tunamshukuru Mheshimiwa Rais, kwenye dira yake ya kuwezesha kukua kwa diplomasia ya kiuchumi. Kama mnavyofahamu, Diplomasia ya Kiuchumi inapofanikiwa hata Diplomasia ya Ulinzi inafanikiwa. Kwa hiyo, nasi upande wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa tunaendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais kupitia Diplomasia ya Kiuchumi pia ametusaidia kuimarisha Diplomasia ya Ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati nchi yetu ina amani ambayo tunaipata kwa gharama kubwa ya wanajeshi na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kuendelea kushirikiana wakiwezeshwa na Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, wakati wa amani ndiyo wakati wa kujenga uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo, tuendelee kumpa ushirikiano Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Waheshimiwa Wabunge wenzangu pamoja na Watanzania ambao mnanisikiliza. Mheshimiwa Rais ametengeneza mazingira wezeshi ya kuzalisha, kuendesha shughuli za kiuchumi, sasa tushikamane naye bega kwa bega kuhakikisha tunaendelea kujenga nchi yetu, kujenga uchumi na kuhakikisha kwa kweli Mheshimiwa Rais tuna kila sababu ya kumuunga mkono kwa asilimia mia moja ili azidi kutenda maajabu.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, mnaona kwa namna ambavyo tunapata miradi ya maendeleo kwenye majimbo yetu. Tutembee kifua mbele tuwe na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, tumpe moyo, tushikamane naye bega kwa bega. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa niende kwenye kujibu hoja ambazo zimejitokeza kwenye mijadala, na kwa sababu ya muda sitaenda hoja baada ya hoja, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kila hoja tumeichukua, tunaenda kuifanyia kazi. Kamati ya NUU ni Kamati ambayo iko makini sana. Wana mfumo wa monitoring and evaluation. Hoja ambazo zilijadiliwa hata kwenye miaka ya fedha iliyopita, wana utaratibu wa kusema hii bado, hii tayari, hii hebu tueleze. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati ya NUU tutaendelea kufanyia kazi haya ambayo mmechangia na kutuelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la ajira JKT. Huku jeshini tunakuita kujiandikisha, siyo ajira, lakini kwa sababu ya kuelezea tulichukulie hivyo hivyo “ajira”, lakini huku tunajiandikisha kwa sababu mwanajeshi anajiandikisha kwa sababu ya kuwa tayari kutumikia Taifa lake na mahali popote na kwa gharama yoyote ikiwemo maisha yake. Kwa hiyo, tunaendelea kuwashukuru sana askari wetu pamoja na maafisa kwa kujitoa kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ajira za JKT nimefanya uchambuzi, 45% ya vijana ambao wanajiunga na JKT ndio wanapata fursa ya kuajiriwa na vyombo vya ulinzi na usalama. 55% kwa sababu vyombo vya ulinzi na usalama nafasi ni chache, ndiyo hiyo JKT inawafundisha ujuzi wa ufundi stadi ili warudi wakajiajiri au kupitia mifumo mingine ya Serikali waweze kusaidiwa kujiajiri.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba Waheshimiwa Wabunge kama walivyochangia, tunalo jukumu la kushirikiana kuhakikisha hii 55% ambayo inarudi mtaani, kwa kadiri inavyowezekana tunashirikiana kuipunguza. Hapa mmetupa mawazo tufanye nini ili kuweza kupunguza hii 55% ya vijana ambao wanahitimu kwa kujitolea JKT lakini wanarudi mtaani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na mawazo ya Bunge kwamba, kama nilivyosema kwenye hotuba yangu, sisi kupitia JKT tayari tumekaa na Wizara ya Kilimo, tayari tumekaa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Waheshimiwa Marais wetu; Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mheshimiwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Hussein Ally Mwinyi, kwenye mkakati wa kuhakikisha Uchumi wa Bluu unakuwa ni sehemu ya kuzalisha ajira na kujenga uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumekaa na tunaendelea kuchambua namna ambavyo tunaweza kushirikiana kama ile MoU ambayo tumeisaini na Wizara ya Kilimo vile vile tulisaini MoU na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili kutekeleza haya ambayo mmetushauri. Hivyo hivyo, hata kwenye Sekta ya Viwanda tutafanya hivyo. Pia mmetuboreshea zaidi kwamba tunahitaji kukaa hata na Ofisi ya Waziri Mkuu, Vijana tujadili na tuwe tuna mkakati wa pamoja ambao ikiwezekana tuulete mbele ya Kamati ambazo zinasimamia watupe ushauri halafu uwe ni mkakati wa pamoja wa kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuzalisha ajira za vijana wengi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, hili tumelichukua ngoja tukalifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la exemption, hili naizungumzia pamoja na bonded warehouse. Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha yupo, tutakaa tuangalie namna bora ya kuweza kulifanyia kazi jambo hili. Ni jambo ambalo linahitaji uchambuzi na kuangalia fiscal implications na nini zikoje, hata Kamati imeshauri hivyo hivyo kwa sababu ni jambo zito. Nikiri hata kwenye upande wa majeshi yetu, tukiweza kulitekeleza bila kuathiri fiscal projection za Serikali, litaleta weledi na ufanisi mkubwa kwenye majeshi yetu. Kwa hiyo, hili tumelichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwathibitishie na kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, jukumu kubwa na la msingi la majeshi yetu ni kulinda Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hata kwenye masuala ya ajira, formula ya 21 kwa 79 inazingatiwa kwa 100%. Kwa hiyo, ningependa kumtoa wasiwasi kaka yangu Mheshimiwa Ussi Pondeza, labda ni kwa sababu za kimawasiliano tu lakini majeshi yetu yanaheshimu Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tutakaa pamoja na ndugu zetu upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhakikisha kwamba hili jambo hata kama kuna miscommunication, linakaa sawa. Ila niwathibitishie kwamba tunaheshimu na kusimamia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lilijitokeza suala la Shirika la Nyumbu, mmeelezea vizuri kwamba mashirika haya ukiangalia sababu za kuasisiwa kwake bado ni mashirika muhimu. Tumshukuru Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu alituelekeza na tukaandaa mpango kazi wa miaka 10 ya Shirika la Nyumbu, lakini baada ya kufanya mapitio, tumeona tunaweza tukafanya vizuri zaidi. Kwa hiyo, tunafanya mapitio ya mkakati huu wa mpango wa miaka 10 ili Shirika la Nyumbu liweze kujikita kwenye mambo ambayo yataleta tija kama tulivyo-discuss hapa.

Mheshimiwa Spika, sambamba na mkakati huo, tayari Shirika la Nyumbu liko kwenye mjadala wa kutengeneza magari ya Zimamoto zaidi kusaidia Wizara ya Mambo ya Ndani. Tumetengeneza magari ya Zimamoto matatu, tuliyafanyia testing, yanafanya kazi nzuri. Hata Shirika la SCANIA lilipokuja Shirika la Nyumbu, kwa sababu tunatumia engine za SCANIA, ilibidi waje wafanye accreditation, engine isiingie kwenye body ambayo inaenda kufanya vitu ambavyo ni substandard. SCANIA walipofika Shirika la Nyumbu walishangaa, wakasema kama Shirika la Nyumbu linaweza likatengeneza magari ya Zimamoto yenye ubora wa kimataifa namna hii, kwa nini mnaendelea ku-import? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jambo hili hata Kamati ya NUU wameliona, tunaendelea kushirikiana kuangalia namna bora tutakavyoshirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani kufanya import substitution ya magari ya Zimamoto taratibu kwa kadiri ya uwezo wa uzalishaji ndani ya Shirika la Nyumbu utakavyoruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile hata Shirika la Mzinga tunasema mazao ya msingi, lakini tukija huku kwenye Kamati wanaelewa mazao ya msingi ni yapi? Tunaendelea kuangalia mashirika mengine kwenye nchi rafiki ambazo tunashirikiana nazo kwenye masuala ya kiulinzi kuliwezesha Shirika la Mzinga kuweza kuzalisha mazao ya msingi zaidi yanayozalishwa hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, vile vile, tunaandaa sheria ambayo tutaileta Bungeni hapa ya Defense Industry. Sheria ambayo itakuwa facilitative kwa mashirika yetu ya kiulinzi, sambamba na kuyajengea ustawi wa kufanya vizuri zaidi na kwa kuingia partnership na mashirika mengine ya kiulinzi kwenye nchi ambazo ni rafiki, tunashirikiana nazo kiulinzi. Pia sheria hii itaangalia namna ya ku-facilitate uwekezaji wa sekta binafsi katika sekta ya ulinzi. Ndiyo maana kwenye hotuba yangu nilisema, Wizara pamoja na kuandaa sheria hii, pia tumeanza kubainisha maeneo ambayo tutaweka exclusive zone kwa ajili ya uwekezaji wa sekta ya ulinzi sambamba na hii sheria ambayo tutaileta mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Sera ya Ulinzi, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, kwenye hili naomba mtupe muda ili tulifanyie uchambuzi zaidi. Ukiangalia historia ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, wakati nchi yetu inapata uhuru, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ilikuwa ni Wizara moja pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje. Walikuwa wanatumia sera moja na kulikuwa kuna sababu za msingi. Kwa hiyo, ni vizuri tukafanya uchambuzi, tukashirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje kuangalia wazee hawa walipokaa na kutengeneza hii sera ambayo ni pacha, inatoa guidance kwenye masuala ya kiulinzi kwa sababu tunapolinda mipaka ya nchi ni mipaka ya nchi yetu dhidi ya nchi jirani. Kwa hiyo, suala hili ni lazima liwe na mtazamo wa ndani kulinda mipaka, lakini pia liwe na sura ya mambo ya nje.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, jambo hili kwa msukumo wa Bunge hili kupitia Kamati ya NUU, ilitufanya twende deep zaidi kuangalia na tukagundua kwamba hili jambo inabidi twende taratibu tufanye uchambuzi na tushirikiane kwa kina na Wizara ya Mambo ya Nje ili tuweze kuwa na sera ambayo itaweza kukidhi yale ambayo tunatarajia sera iweze kusaidia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, suala la ajira upande wa JKT nimeshalisema na kama tukifanya kama mlivyotushauri, itakuwa ni sehemu ya mkakati wa kutengeneza ajira milioni nane ambazo tumeziahidi kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika michango ya Waheshimiwa Wabunge, mlisema nitakaposimama hapa nielezee tutajenga makambi mangapi ili kuwezesha vijana wanaomaliza Form Six kwa mujibu wa sheria kuweza kwenda JKT wote, lakini vile vile hata vijana ambao wanajitolea kuweza kupeleka idadi kubwa zaidi kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, takwimu za JKT zinaonesha miundombinu ambayo tunayo kwa ajili ya kupokea vijana wanaomaliza Form Six bado tunapokea wachache kuliko miundombinu inavyoweza ku-support. Kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha vijana ambao wanatakiwa kwenda JKT wanapomaliza Form Six kwa mujibu wa sheria watii matakwa ya kisheria hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha tunapokea takribani 22,000 na wakati tuna uwezo wa kupokea 26,000. Kwa hiyo, kuna gap ya 4,000 lakini mtaani mtazamo ni tofauti. Upande wa vijana ambao ni kwa mujibu wa sheria, utakuta wanasema walitaka kwenda, lakini miundombinu haitoshi. Hii changamoto ya kutotosha kwa miundombinu ni kwa upande wa vijana ambao wanajitolea. Hilo nikiri changamoto ipo na tutakaa na Wizara ya Fedha na Mipango kuangalia namna ambavyo tunaweza tukasaidiwa ili kuweza kuongeza miundombinu kuweza ku-accommodate vijana wengi zaidi ambao wanajitolea waweze kupata fursa ya kupata mafunzo ya JKT. Kwa hiyo, hili tunalichukua ili tukalifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, mawazo yalikuwa ni constructive. Waheshimiwa Wabunge mmetupa ushauri mzuri, tumechukua yote na itoshe kusema kwamba tutaenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Naibu Mawaziri kwa ushirikiano ambao wamenipa katika kuwasilisha hotuba hii. Vile vile nimhakikishie Mheshimiwa Mathayo, mtani wangu, tutaenda Musoma tuangalie maeneo haya ambayo ameyataja na tushirikiane kama nilivyosema, lazima tuangalie pande zote mbili. Majeshi yetu yanahitaji maeneo ya kufanyia mazoezi na kujiandaa kivita. Kwa mtazamo wa macho ya kiraia, unaweza ukaona eneo la jeshi ni kubwa, lakini kwa mtazamo wa kitaaluma ya kijeshi ni eneo dogo na majeshi yetu hayawezi kwenda nchi ya nje eti waazime eneo kwa ajili ya kufanya mazoezi. Hiyo itakuwa siyo jeshi. Kwa hiyo, mazoezi lazima wafanyie humu humu ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tuendelee kushirikiana, tutatue migogoro ya ardhi baina ya wananchi wetu na majeshi, lakini pia mtusaidie kutoa elimu kwa wananchi wetu, tuheshimu maeneo ya jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimalizie. Kulikuwa na maombi maalum ya Waheshimiwa Wabunge wawili; Mheshimiwa Mathayo kwamba twende site, nitakuja.

Pia kaka yangu Mheshimiwa Rashid Abdalla Rashid, nitakuja Pemba tukaangalie maeneo ambayo umeyataja tutembelee ile skuli ambayo umesema tuitembelee. Nitumie nafasi hii kuwapongeza vijana kwa kazi nzuri wanayoifanya ya ku-perform vizuri na kupata heshima ya performance nzuri ya skuli hii. Basi nitakapokuja tutaangalia hizo changamoto za migogoro uliyoitaja ili tutafute namna bora ya kutatua changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru tena kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA K.n.y. WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kukushukuru tena kwa kunipa nafasi ya kufanya majumuisho ya mjadala kuhusu Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, kwanza, nashukuru sana michango ya Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia kwa kuzungumza na kwa maandishi. Nitoe shukrani kwa Mheshimiwa David Kihenzile, Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mheshimiwa Geoffrey Mwambe, Haji Mlenge, Mheshimiwa Ramadhan Suleiman Ramadhan, Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla, Mheshimiwa Abbas Tarimba na Naibu Waziri Mheshimiwa Exaud Kigahe kwa michango yao mizuri.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa namna ambavyo wameshiriki mjadala huu.

Mheshimiwa Spika, Wizara tumepokea maoni mazuri ambayo yanalenga kuboresha Muswada huu.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kama mnavyofahamu, suala la kutunga sheria ni jambo endelevu, ndiyo maana kila mwaka Serikali inakuja na Miswada mbalimbali kwa lengo la kuboresha masharti ya sheria zetu na kuzifanya ziendane na wakati.

Mheshimiwa Spika, naishukuru tena Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa ushirikiano. Serikali imezingatia maoni yaliyotolewa na Kamati kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie kwa kutoa maelezo kwa baadhi ya hoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mjadala wa Muswada huu kulikuwa na hitaji la kuzungumza kama Muswada huu umezingatia utekelezaji wa blueprint. Ukiangalia maudhui katika blueprint malengo ya Serikali ni kuondoa urasimu, lakini vile vile kufanya maboresho ya sheria mbalimbali ili kuweza kuvutia uwekezaji na biashara na kulinda biashara ambazo tayari tunazo ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia maudhui ya Muswada huu yamelenga kulinda na kuvutia uwekezaji, kwa mantiki hiyo, Muswada huu ni sehemu ya kutekeleza blueprint. Kwa hiyo ningependa niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba blueprint ni comprehensive na Serikali inaendelea kufanya kila jitihada za kisera, kisheria na kikanuni kuhakikisha tunaendelea kutekeleza blueprint. Kwa hiyo huu ni mwendelezo na Muswada huu unaenda kutekeleza hilo.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna concern ya jina, kwamba jina likiwa linavutia (jina by itself) linaweza likawavutia wawekezaji. Hata hivyo, napenda kuwaondoa wasiwasi pia kwenye suala la jina. Ukiangalia kwenye literature wawekezaji kwenye nchi yoyote wanaangalia nini, sio jina as such kama jina la kituo, kwa mfano Tanzania Investment Centre bali wawekezaji kabla hawajaenda kuwekeza kwenye nchi yoyote wanaangalia masuala mbalimbali. Kwanza, uwepo wa amani katika hiyo nchi na Tanzania tunajivunia kuwa ni kisima cha amani. Hivyo, hiyo nayo ni factor ya kuvutia uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wawekezaji vile vile huwa wanaangallia uwepo wa rasilimali watu (work force) je, ni competitive, ukiangalia unit labour cost ya kutengeneza bidhaa fulani ukilinganisha na nchi nyingine, je, nchi yako ina- compete katika hilo. Kwa hiyo ndio maana tunaendelea kuwekeza katika elimu, katika Vyuo vya Ufundi Stadi ili kuwaandaa watu wetu kuwa competitive ili iwe ni sehemu ya kuvutia wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, lingine, wawekezaji huwa wanaangalia predictability yaani sera zako zinatabirika kiasi gani, sheria na hata siasa. Nchi ambazo zina machafuko au amani haina uhakika yaani haitabiriki, nchi hiyo haiwezi kuvutia uwekezaji. Yote haya tunaona ni namna gani nchi yetu tuko competitive, kwa sababu haya yote ninayoyataja nchi yetu tuna kila sababu ya kujivunia na kuwa na confidence kwamba tunaweza kuvutia uwekezaji. Hata hivyo, inabidi tujikite kwenye suala ambalo hata kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge na hili jambo nadhani linahitaji muda wa kutosha kutoa elimu kwa jamii, suala la mindset. Hatuwezi kufanya na kutegemea kwamba tutatunga sheria ambayo itakuwa ni silver bullet ya kila kitu, kama ni urasimu ipo sehemu sheria inaweza ikapunguza, lakini ipo asilimia kubwa ya kupunguza urasimu kwa kubadilisha fikra za sisi wenyewe kama Watanzania.

Mheshimiwa Spika pamoja na Wabunge wenzangu kwenye suala la mindset changes, sisi wote kama viongozi tuna jukumu la kuisaidia jamii yetu kuwa na mindset ambayo ni facilitative badala ya kuwa frustrating hata kwenye utumishi wa umma, vile vile kuvutia uwekezaji, kuvutia biashara, mindset ya kudhibiti (regulatory) ni mindset ambayo inatuchelewesha. Kwa hiyo kwenye hili tuendelee kushirikiana ili tuweze kuwa na fikra chanya ya sisi viongozi, utumishi wa umma na kuendelea kuelimisha ili kuwa na mikakati ya kuhakikisha tunakuwa na mindset sahihi ya kuvutia uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, wawekezaji huwa pia wanaangalia fiscal structure au fiscal regime ya nchi ikoje kwenye upande wa kodi kwa maana ya tax payments, regime ikoje na hata non-tax payment upande wa halmashauri zetu, zile tozo na non-tax charges ambazo halmashauri zetu zinatoza. Wawekezaji huwa wanaangalia vitu vya namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika kujibu masuala ambayo yamejitokeza, ningependa kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba tumeleta Muswada huu unaolenga kuwa sheria bora zaidi kuliko ile ya mwaka 1997. Suala la jina, kwa mfano kuna Mheshimiwa Mbunge alisema kwamba, wawekezaji wanapenda nini. Napenda niwakumbushe kwamba Mwaka 1990 tulikuwa na Sheria inaitwa The National Investment (Promotion and Protection Act, 1990) unaona ni jina lefu, lakini malengo yalilenga kutibu kile ambacho pia tumekichangia hapa kwamba tuweke protection kwenye jina lakini pia tuweke promotion. Hata hivyo, mwaka 1997, tulifanya marekebisho ya sheria hii ambayo leo hii pia tumeiboresha na sheria hiyo imebadilishwa mara nyingi ili kuifanyia maboresho. Kwa hiyo ningependa kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba, kikubwa ni maudhui yaliyopo kwenye sheria na sio jina limebeba uvutiaji kiasi gani.

Mheshimiwa Spika, vile vile Muswada huu utakuwa sheria bora kwa kuwa umebeba matarajio ya wananchi wetu. Muswada huu pia unalenga kuwa sheria itakayoboresha mifumo ya kitaasisi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kwamba kwa nini sheria hii haijainclude sekta za madini, gesi asili na extractive industry kwa ujumla wake. Ukiangalia nchi zote rich countries huwa zinakuwa na tax regime inayojitegemea kwenye usimamizi wa extractive industries. Sisi Tanzania sio kwamba tuko peke yetu bench mark nchi zote ambazo zina utajiri wa gesi ya asili huwa zina a different tax regime kwa ajili ya kusimamia sekta hizi, lakini sheria hii haizui Kituo kuwa facilitative hata kwenye uwekezaji ambao uko kwenye hizo sekta. Kwa hiyo hilo nalo ningependa kuwaondolea wasiwasi Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine kwamba, kwa nini sekta binafsi kusiwe na mjumbe? Ukiangalia muundo wa Serikali, muda wote huwa inashirikiana na Tanzania Private Sectors Foundation ipo Tanzania National Business Council na Tanzania Chamber of Commerce Industry Association. Kwa hiyo pamoja na maboresho ya sheria hii bado Serikali itakuwa inawajibika na kulazimika kushirikiana na taasisi hizi za sekta binafsi ili kuhakikisha tunashirikiana ili kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ningependa kuwahakikishia wewe
pamoja na Bunge lako Tukufu kwenye upande wa kanuni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa, dakika mbili malizia.

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA (K.n.y. WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA): Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa kanuni, sheria yenyewe inalenga kuwa facilitative. Nitashangaa sana kwamba sisi ambao tumeleta Sheria hii iwe facilitative kwenye uwekezaji na ufanyaji biashara wenyewe tukatengeneze kanuni ambazo zitatufunga. Kwa hiyo napenda kuwatoa wasiwasi kwamba Kanuni ambazo tutazitunga ni kwa ajili ya kusaidia na kuipa nguvu sheria hii iweze kufacilitate uwekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile nimalizie na suala la mtaji (threshold) Serikali imezingatia kuwawezesha Watanzania wenzetu kuwa sehemu ya kunufaika na hivi vivutio na ndio maana masharti yametoka hitaji la dola laki moja kuwa dola elfu hamsini. Hii haimaanishi kwamba kila atakayetaka kufanya biashara anazuiwa kufanya biashara. Sheria hii imelenga wale ambao wamekuwa wakihitaji incentives za Kituo basi waweze kunufaika na ndio sababu Serikali imeona ni vyema kushusha kutoka dola laki moja kwenda dola elfu hamsini. Hata hivyo, zipo sheria mbalimbali ambazo zitaendelea kusaidia wafanyabiashara wadogo sana na wakubwa ili waendelee kufanya biashara zao na kuweka mazingira ya kuwasaidia wakue. Watakapofika kwenye uhitaji wa kwenda TIC basi sheria hii itakuwepo na ndio maana imezingatia suala la Watanzania ambao kipindi cha nyuma ya mwaka 1997 ilikuwa mpaka uwe na dola laki moja lakini sasa imeshusha kuwa dola elfu hamsini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.
Ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hoja hii nyeti na muhimu sana kwa mustakabali wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Profesa Maghembe na Naibu Waziri, Mheshimiwa Injinia Ramo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuiongoza Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mdau mkubwa na naamini kwamba maendeleo ya watu na utunzaji wa mazingira ni vitu viwili ambavyo vinaendana (environmental conservation can co-exist with social economic development). Kwa hali inayoendelea katika Pori la Hifadhi la Kimisi nimeanza kuwa na mashaka kwamba tusipojipanga vizuri kama nchi itafika mahali nchi yetu itageuka kuwa jangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nikiwa mtoto Pori la Akiba la Kimisi tulikuwa tuna wanyamapori wengi, kulikuwa kuna twiga, zebra, tembo na wanyama wengi lakini sasa hivi limejaa ng‟ombe kutoka nchi za jirani. Nimeangalia kwenye sheria za nchi yetu, nimeangalia kwenye Mpango wa Taifa wa Ardhi wa 2013 - 2033 sijaona sehemu yoyote inayosema kwamba mapori ya akiba yatumiwe na ndugu zetu wa nchi za jirani kufuga ng‟ombe wao na wakati wananchi wetu wana shida ya malisho bora na maeneo ya kulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa upande wa Karagwe, Kata ya Rugu, Nyakasimbi, Nyakakika, Nyakabanga na Bweranyange wananchi wangu wana shida sana na maeneo ya malisho bora na maeneo ya kulima lakini wanapakana na Pori la Akiba la Kimisi ambalo inasemekana kuna ng‟ombe wengi sana kutoka nchi za jirani. Naiomba Serikali iliangalie suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama kiongozi siwezi kuingia mle kwenye pori hata wananchi wangu wanashindwa kuingia na kwa kuwa wananchi wanafahamu kwamba haya mapori matumizi yake hayafuati sheria za nchi za mapori ya akiba, wengine wanashawishika kuingia mle kwa sababu hawako tayari kuona ng‟ombe wao wanakufa kwa kukosa malisho na wakati kuna wafugaji kutoka nchi jirani wapo kwenye lile pori. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali iandae Tume iende mle ichunguze status ya Kimisi irudi kwenye Pori la Akiba. Mimi na Madiwani wangu tutafuata utaratibu pale itakapobidi kama ni kuomba Serikali itenge maeneo kwa ajili ya wakulima na wafugaji basi tufuate utaratibu wa bottom up kwa mujibu wa sheria za nchi yetu. Watu wanatoka nchi jirani wanakuja kufugia kwenye mapori ya akiba na hiki ndiyo chanzo cha migogoro. Nazungumzia kwa Kimisi, lakini naamini pengine picha ya Kimisi inafanana na mapori ya akiba mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali baada ya ku-clear Kimisi ikawa katika hali ambayo inafuata utawala wa sheria, turudi kule zamani ambapo lile pori la akiba lilikuwa ni pori ambalo tunaweza tukafanya utalii. Wenzetu nchi ya jirani ya Rwanda wana ardhi chache lakini wanaitumia vizuri. Kwa mfano, pale Kimisi natamani sana Serikali ituletee twiga, zebra na tembo pawe conserved tuweze kufanya utalili kama majirani zetu Rwanda wanavyofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili niombe Serikali kwa sababu wakati wa kutenga Kimisi Serikali haikuhusisha vijiji vya jirani kunyoosha mipaka iende pale Kimisi katika hizi kata ambazo nimezitaja tuangalie upya ile mipaka na tuweke mipaka ya kudumu. Mimi kama Mbunge wa Karagwe naamini kabisa kwamba wananchi wa Karagwe tunaweza tukawa tuna conservation ya pori ambalo linatuletea mapato ya kitalii na wakati huo huo tukapata malisho bora na sehemu za kulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuiomba Serikali, sasa haya ni mambo ya Kitaifa kidogo, kuna asilimia 25 ya mapato kutoka mapori ya akiba yanatakiwa kwenda kwenye Halmashauri kusaidia vijiji ambavyo vipo jirani na mapori ya akiba, lakini kwenye Halmashauri ya Karagwe hii hela hatujawahi kuiona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri Mheshimiwa Profesa Maghembe atakaposimama kujibu hoja nisikie msimamo wa Serikali kwenye Kimisi na pia nisikie msimamo wa Serikali kuhusu asilimia 25 ambayo inatakiwa kuja kwenye Halmashauri ya Karagwe kutoka kwenye mapato ambayo yamepatikana kutoka kwenye mapori ya akiba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la utalii kwenye nchi yetu umekuwa ni wimbo sasa tunasema nchi yetu ina-potential ya utalii inaweza ikatuingizia fedha za kigeni zaidi lakini sioni mikakati ambayo inanipa matumaini kwamba sasa sekta ya utalii itakua na kuweza kuchangia pato la Taifa. Napenda kuishauri Serikali, Wizara ya Maliasili na Utalii wasifanye kazi kwenye silos, washirikiane na Wizara nyingine kwa mfano kama kuna maeneo ambayo ni ya kipaumbele kwenye uwekezaji wa utalii, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ishirikiane na Wizara ya Maliasili kuhakikisha hayo maeneo yanapata miundombinu ili tuweze kuvutia uwekezaji kwenye maeneo hayo ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania kwenye ranking imekuwa nchi ya 130 na wakati kwenye vivutio duniani ni ya pili. Hii inaonesha kwamba hatujajipanga na tukijipanga sekta ya utalii inaweza ikatusaidia kukuza uchumi wa nchi na kutengeneza ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la mambo ya kale na hii ni sehemu ambayo tukijipanga vizuri inaweza ikatusaidia kuongeza pato na ajira kwa wananchi wetu. Karagwe kwenye historia na sisi tumo. Kama mnakumbuka Speke na Grant walipita Karagwe wakati wanaangalia jinsi ya kwenda Uganda. Kwa mfano sehemu ambapo Chifu Rumanyika alipokuwa anakaa tunaiomba Wizara ya Maliasili na Utalii itusaidie. Nimeshaongea na wana diaspora kutoka Karagwe wapo tayari kushirikiana lakini tunahitaji msaada wa Serikali kutuwekea miundombinu ya pale na tukae tuangalie ni namna gani tunaweza tukasaidia kuhifadhi malikale kwa Karagwe na sehemu nyingine za nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto kidogo kwenye Kata ya Bweranyange, hizi ni Wilaya ambazo ziko mipakani na nchi za jirani na ni vizuri tukahakikisha tunatunza ulinzi na usalama wa mipaka yetu. Kule kwenye Kata ya Bweranyange kuna kambi ndogo ya jeshi wananchi wangu wananipigia simu wanalalamika kwamba wamefika mahali wanaogopa kuoa wanawake wazuri kwa sababu wanahofia eti watanyang‟anywa na wanajeshi. Mimi siamini kwamba hali iko hivi lakini…
MWENYEKITI: Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Bajeti ya Serikali. Nianze kwa kukupongeza Mheshimiwa Naibu Spika kwa kazi nzuri unayoifanya ya kuendelea kuliongoza Bunge letu Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango na Naibu Waziri kwa maandalizi mazuri ya bajeti na Serikali kwa ujumla. Pamoja na maandalizi haya mazuri, mapungufu hayakosi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nianze na bajeti ya sekta ya kilimo iliyotengwa, asilimia nne nukta tisa ambayo ni takribani shilingi trilioni moja nukta tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninatamani sana malengo yetu ya Serikali na nchi yetu ya kuwa nchi yenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 tuyafikie na natamani sana malengo ya nchi yetu ya kuwa na uchumi wa viwanda ifikapo mwaka 2020 tuyafikie. Lakini ili tuweze kuyafikia, lazima tutende kwa vitendo, asilimia 4.9 ya bajeti ya sekta ya kilimo ni ndogo sana. Kwa sababu ukiangalia Watanzania walio wengi takribani zaidi ya asilimia 75 wamejikita kwenye shughuli za kilimo na hili tuweze kuwa na social economic transformation ya kuweza kutupatia uchumi wa viwanda, inatubidi kuhakikisha shughuli zao ambazo wanazifanya ndipo tuelekeze hizi sera za uchumi wa viwanda. Sasa shilingi trilioni 1.5 ni ndogo sana kama kweli tuna dhamira ya kujenga uchumi wa viwanda ambao unawagusa asilimia zaidi ya 75 ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango anaweza akasema kwamba tukisaidia kujenga miundombinu in one way or another tutakuwa tumesaidia sekta ya kilimo. Ni sahihi, miundombinu ni catalyst ya maendeleo, lakini ifike mahali turudi kwenye kutimiza lengo tulilosaini la Maazimio ya Maputo kwamba asilimia kumi ya bajeti iende kwenye sekta ya kilimo, bado tuko mbali sana. Nipende kuiomba Serikali jambo hili ilitilie maanani sana kwa sababu uchumi wa viwanda utakaowagusa Watanzania wengi, lazima tuhakikishe sekta ya kilimo tunajikita huko kuchakata kwa mazao ya wakulima na wafugaji ndio iwe focus ya mwelekeo wa Serikali ya viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili naomba nizungumzie bei ya kahawa. Waheshimiwa Wabunge wanaotoka kwenye Majimbo yanayolima Kahawa wameizungumza sana, viongozi kabla ya uchaguzi wamewaahidi wakulima wa kahawa kwamba zile kodi kero 26 zitaondolewa baada ya hii Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani.
Sasa nipende kumuomba Waziri wa Fedha atakaposimama kufanya wrap-up atuambie hizi kodi zinakatwa lini. Sasa hivi wakulima wa kahawa wako wanavuna kahawa, walitegemea bei ya msimu huu ihusishe makato haya ili wapate faida zaidi hata kama soko la bei ya kahawa la dunia liko chini, tukiondoa hizi kodi itasaidia wakulima wetu wapate bei nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, naomba nizungumzie Taasisi ya TSC (Teachers Service Commission). Niishukuru Serikali kwa kuanzisha hiki chombo ambacho kimelenga kutetea maslahi ya walimu nchini, lakini toka mwaka jana baada ya kuunda sheria sijaoana mchakato ambao unaonesha kwamba kweli hiki chombo kimejipanga kutatua kero za walimu nchini. Sijasikia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ikizungumzia wamejipanga vipi katika rasilimali watu na fedha kuhakikisha TSC ina take off, na ukiangalia changamoto za walimu bado zipo, arrears za walimu bado hazijalipwa asilimia 100. Na nikizungumzia Karagwe naamini changamoto hii pia ipo katika nchi nzima, suala la kupandishwa madaraja walimu lakini effect ya payment inachelewa. Sasa TSC ingekuwa imeshaanza naamini sasa hivi wangekuwa wako katika kutatua hizi changamoto, kwa hiyo nipende kuiomba Serikali, TSC ni chombo muhimu cha kutetea maslahi ya walimu nchini, kipeni rasilimali watu na fedha ili kiweze kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la wigo wa kodi. Ukiangalia historia ya uandaaji wa bajeti za Serikali, kwa kweli bado tuna narrow tax base, ifike mahali Wizara ya Fedha na Mipango na Serikali kwa ujumla muangalie avenues nyingine za kodi ili tuweze ku-broaden tax base. Wale existing tax payer’s itafika mahali watakuwa wanakuwa disincentivized kuendelea kulipa kodi kwa sababu kila mwaka tunaongeza increments kwenye tax items hizohizo, tunashindwa kuwa wabunifu wa vyanzo vipya vya mapato ili tax base ipande, mapato yakue bila kuweka burden kubwa kwa wale honest tax payers na katika hili niiombe Serikali muandae mkakati wa kuleta informal sector kwenye formal sector ili huu mkakati wa ku-broaden tax base uendane na kuingiza informal sector kwenye formal sector ili tuweze kukuza mapato nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie suala la Dar es Salaam Stock Exchange. Serikali yetu kwa muda mrefu imekuwa ikijitahidi kuweka sera za kukuza Dar es Salaam Stock Exchange, lakini nimeshangaa katika bajeti hii ambayo imewasilishwa tunapiga hatua tatu mbele, halafu tunakwenda hatua nne nyuma. Capital gains tax on sales of shares, kwa kweli Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, nikuombe sana, kwa kufanya hivi tutakuwa tunaua Dar es Salaam Stock Exchange isiweze kushindana na stock exchange nyingine ambazo ziko Afrika Mashariki, na ni mkakati mmoja wapo wa kuisaidia nchi yetu tuweze kupata mitaji ya kuwekeza kwenye uchumi wetu wa viwanda kupitia kwenye Dar es Salaam Stock Exchange. Na hii ni dalili ya kuwa na narrow tax base ambayo inaangalia low hanging fruits, twende kwenye high hanging fruits, najua ni kazi lakini naamini kwa uwezo wako mahiri na Wizara yako kwa kushirikiana na Wizara nyingine mnaweza, hii kodi ya capital gain tax on sales of shares naomba muiondoe Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la mwsiho. Karagwe, NSSF ilikuwa na lengo zuri la kushirikiana na Vyama vya Ushirika kutoa mikopo ya bei nafuu kwa wananchi lakini ule mchakato ulikwenda ndivyo sivyo. Kuna wananchi wengi Jimbo la Karagwe walitozwa hela, wengine mpaka kufikia shilingi 280,000 kwamba watapata mkopo wa bei nafuu na baadaye wataingizwa kwenye Bima ya Taifa. Huu ni mpango mzuri, niombe Serikali i-review huu mkakati lakini pia izungumze hizi fedha ambazo wananchi wangu walitoa kwa ajili ya kupata mikopo ya bei nafuu na Bima ya Taifa wanarudishiwa lini na kama hawarudishiwi basi turudi kwenye huu mpango, uwe reformed uweze kuwasaidia wananchi wa Karagwe na nchi nzima kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha vizuri, vilevile nitakuwa mkosa fadhila nikianza kuchangia Mpango bila kwanza kuishukuru Serikali kwa jitihada wanazoendelea kuzifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. John Magufuli; Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu; Waziri Mkuu wetu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa; na Baraza la Mawaziri lote kwa jitihada wanazoendelea kuzifanya kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Kagera na janga la tetemeko la ardhi lililotupata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wabunge wote kwa kuguswa na kwa mchango wenu mlioutoa katika kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Kagera. Pia niishukuru Serikali kwa jitihada za kidharura ambazo wanaendelea kuzifanya kuwasaidia wananchi wa Wilaya ya Karagwe kwa janga la njaa lililotupata lililosababishwa na ukame wa muda mrefu ambao haujawahi kutokea katika historia ya Karagwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada za Serikali, nipende kuiomba Serikali ili kuwaondoa wananchi wa Karagwe kutoka kwenye utegemezi wa kuomba chakula Serikalini, Serikali ishirikiane na mimi na Waheshimiwa Madiwani kuhakikisha tunajenga mpango mkakati wa kati na wa muda mrefu wa kuwasaidia wananchi wa Karagwe kutoka kwenye utegemezi wa kuomba chakula, kwenda kwenye kujitegemea kama tulivyokuwa kabla ya kupata janga la njaa ambalo limesababishwa na ukame na ukame umesababishwa na mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Serikali ituletee chakula chenye bei ya ruzuku haraka iwezekanavyo ili wananchi wengi wa Karagwe waweze kupata chakula, hasa maharage na mahindi, Serikali ituletee mbegu za mazao yanayostahimili ukame, taarifa tumeshaiwasilisha kwenye Kamati ya Maafa ya Taifa. Naiomba Serikali iifanyie kazi haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itusaidie kutatua migogoro ya ardhi, hasa migogoro mikubwa. Kuna mgogoro wa Kihanga ambapo Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja alipokelewa na halaiki kubwa ya wananchi wa Karagwe na akaiagiza Serikali ifanye haraka iwezekanavyo kuhakikisha zile hekta 2,000 ambazo wananchi wa Kihanga waliahidiwa toka NARCO ziende kwa wanakijiji, lakini mpaka hivi sasa maelekezo haya hayajafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali itusaidie, pori la akiba la Kimisi usimamizi wa kisheria umekuwa siyo usimamizi wa kisheria, umekuwa ni double standard, kuna mifugo mingi inatoka sehemu mbalimbali za nchi, kuna mifugo kutoka nchi za jirani iko Kimisi, lakini mimi na Waheshimiwa Madiwani tumekuwa tukiwaambia wananchi wetu wa Karagwe kwamba lazima watii utawala wa kisheria na ng‟ombe wao wasiingie mle Kimisi, sasa kinachoendelea ni double standards.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, kama lile pori la akiba la Kimisi wameshindwa kulitumia kwa tija na kwa kufuata misingi ya sheria, basi lirudishwe kwa wananchi kupitia Halmashauri ili katika Baraza la Madiwani tukae na kupanga matumizi bora ya kutumia hili eneo kwa kuzingatia sasa hivi Karagwe tuna tatizo la ukame, tunahitaji ardhi ya ziada kwa ajili ya kulima na kufuga. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, tengeni eneo la pori la akiba la Kimisi angalau wananchi wangu wa Karagwe wapate eneo la kulima na kufugia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niiombe Serikali itusaidie, tuna Kata sita ambazo zina maji ya kutosha, tuwasaidie wananchi wa Karagwe waende kwenye kilimo cha kujitegemea. Serikali ilete wataalam waangalie ni namna gani tunaweza tukafanya kilimo cha umwagiliaji katika Kata ya Bugene, Kanoni, Kamagambo, Boranyange, Nyakakika na Lugu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie mapendekezo ya Mpango. Hapa kikubwa sana, hasa ni kuangalia katika vile vipaumbele vinne. Napenda kuishauri Serikali mwisho wa siku tutapimwa ni namna gani maendeleo ya uchumi na maendeleo ya watu vimefungamana. Sasa, katika hili bahati mbaya sana tumekuwa tukitumia GDP kama kigezo cha kuangalia uchumi wa nchi unakuaje, siyo Tanzania tu ni dunia nzima. Bahati mbaya sana, kupima GDP kama kigezo cha maendeleo siyo kipimo kizuri kwa sababu ukiangalia ukuaji wa uchumi kwa takwimu tu hali yake haifanani na hali ya mtaani. Matokeo yake, taarifa zinakuwa zina takwimu nzuri lakini hali ya maisha ya wananchi haibadiliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishauri Serikali katika Mpango wa kuwa na uchumi wa kati ifikapo 2025, katika malengo ya kuwa na uchumi wa viwanda, nirudie kwa mara nyingine; tujikite kwenye shughuli ambazo zinawahusisha Watanzania wengi na si shughuli nyingine bali ni Sekta ya Kilimo na Mifugo, ujasiriamali mdogo na wa kati, pamoja na mnyororo wa mazao yaani value chain ya mazao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo Serikali itajikita katika maeneo haya matatu, kilimo na mifugo, biashara ndogo na kati na value chain ya mazao, tutakuwa tumewagusa Watanzania wengi zaidi ya asilimia 70 na tutakuwa tunakwenda kwenye mwelekeo mzuri wa kufikia uchumi wenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025, lakini tukiendelea kusaidia zile sekta ambazo multiply effect yake ni ndogo, kusema ukweli inaweza kufika 2025 bado tukawa tunaulizana maswali magumu humu Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusisitiza sana, kwenye upande wa value chain ya mazao lazima tuangalie ni namna gani tunawasaidia wananchi wa Tanzania kutoka pale walipo hata kama ni hatua ndogondogo lakini ni hatua ambazo zinamsaidia kila Mtanzania kukuza kipato chake popote alipo katika shughuli hizi ambazo anajishughulisha nazo. Baada ya ku-focus katika hivi vipaumbele vitahakikisha maendeleo ya uchumi na maendeleo ya watu vinafungamana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika hili lazima tuweke mazingira wezeshi, mikopo ya bei nafuu katika hizi sekta ambazo nimezitaja. Kwa mfano; tuna Benki ya Maendeleo ya Kilimo; mpaka hivi sasa ina bilioni 60 tu. Ukiangalia kwa vitendo kama kweli tunataka kusaidia kilimo na mifugo kwa kuwapatia wananchi wetu mikopo ya bei nafuu, lazima tuiwezeshe Benki ya Maendeleo ya Kilimo ipate mtaji wa kutosha iwasaidie wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna VICOBA Vijijini na Mjini kuna SACCOS, tuzisaidie zipate mitaji ya bei nafuu ili ziweze kukopesha vijana na akinamama vijijini na mjini ili waweze kutumia mitaji hii kufanya shughuli ambazo wanajishughulisha hata kama ni kidogo lakini multiply effect yake ni kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hatuwezi kupata maendeleo endelevu katika mpango wetu wa kuwa na uchumi wa kati kama hatuwekezi kwenye rasilimali watu. Niipongeze Wizara kwa kuliona hili katika mapendekezo ya mpango, lakini hii haitoshi. Kwa mfano, hivi sasa kuna wanafunzi wengi sana Vyuo Vikuu wanasubiri kupewa mikopo Serikalini, sasa tukifanya kwa vitendo kuonesha namna gani tunawekeza katika rasilimali watu tunatakiwa tuhakikishe katika Taasisi zetu za Vyuo Vikuu ili Taifa na work force ambayo tunaiandaa tunaiwezesha kupata mikopo ili waweze kusoma na tuweze kutumia hii work force kusaidia uchumi wetu na kusaidia kwenda kwenye malengo ya uchumi wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma taarifa ya ndugu zetu wa Upinzani. Niwapongeze, wana mapendekezo mazuri, lakini katika taarifa yao wamesahau ku-acknowledge kwamba Serikali yoyote makini kuna transition period. Toka Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ikijipanga kuhakikisha inatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kama tulivyowaahidi wananchi na Watanzania wana imani sana na Serikali ya Awamu ya Tano, watupe muda tunajipanga, Serikali ni sikivu na naamini kabisa tutawavusha Watanzania kama tulivyoahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia taarifa ya Kamati ya Bajeti.
Mheshimwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuishukuru Kamati ya Bajeti kwa kutuletea taarifa nzuri ambayo imefanya uchambuzi mzuri juu ya hali ya utekelezaji wa bajeti ya Serikali.
Mheshimwa Mwenyekiti, naomba kwanza kuipongeza Serikali kwa malengo mazuri ya mwaka huu wa fedha wa 2016/2017 Serikali ilitenga asilimia 40 ya bajeti iweze kwenda kwenye miradi ya maendeleo. Mipango hii ni mizuri na imelenga kuwasaidia Watanzania waweze kupata maendeleo ambayo tuliwaahidi katika utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, zipo changamoto na ndiyo maana nimeishukuru Kamati ya Bajeti kwamba wamejitahidi sana kutathmini changamoto hizi na sisi tuna wajibu wa kuzijadili na kuishauri Serikali, bahati nzuri tupo kwenye midterm review ya bajeti. Kwa hiyo, nina imani kwamba Serikali ni sikivu na mapendekezo haya ambayo Kamati imetoa na Waheshimiwa Wabunge watatoa yatafanyiwa kazi ili tunavyokwenda kwenye second half ya utekelezaji wa bajeti ya Serikali hizi changamoto zifanyiwe kazi na baadhi ya changamoto ziwe carried over kwenye bajeti inayofuata.
Mheshimwa Mwenyekiti, naomba nianze na Deni la Taifa, nianze kwenye ukurasa wa tatu wa taarifa ya Kamati ya Bajeti, ninukuu kuhusu mwenendo wa miradi ya maendeleo hasa hasa michango ya washirika wa maendeleo. Kwenye ukurasa wa tatu mwisho kabisa; “mwenendo wa utoaji wa fedha za washirika wa maendeleo unaonesha ni upungufu kwa asilimia 26 ya fedha yote iliyotarajiwa kutolewa. Kamati haikupata majibu ya kuridhisha kuhusu sababu za washirika wa maendeleo kutotimiza ahadi zao kwa asilimia mia moja.”
Mheshimwa Mwenyekiti, kusema ukweli na mimi nipo concerned sana; tumeweka malengo mazuri, tume-target asilimia 40 ya bajeti iende kwenye fedha za maendeleo na hivi sasa tumefika kwenye nusu ya mwaka wa bajeti kwa asilimia kubwa fedha za maendeleo tulitegemea hao wahisani watakapotoa fedha ndizo tutumie kwenye kufadhili miradi ya maendeleo. Ukiangalia ukusanyaji wa TRA, ukichukua ile trilioni takribani 1.2 kila mwezi ya TRA inayokusanya ukalipa mishahara ya watumishi (wage bill), ukalipa madeni ya Taifa, chenji inayobaki ni kidogo mno. Tulitegemea wahisani wakitoa fedha za maendeleo ule mchango wao tutaunganisha na ile chenji inayobaki kwenda kufanya kazi za maendeleo. Wahisani kwa vile hawatoi hizi fedha kwa kweli mimi naona tupo kwenye state of emergency, its very alarming kwamba tupo kwenye midterm review lakini hatujapata fedha ambayo tulitarajia wahisani watupatie ili tuweze kutekeleza miradi ya maendeleo.
Mheshimwa Mwenyekiti, nini kifanyike? Ukiangalia madeni ya Taifa hayaepukiki ni lazima yalipwe. Ukilipa Deni la Taifa kwa sababu asilimia kubwa tunalipa nje hii fedha tunayolipa inaenda kusaidia ku-stimulate uchumi wa kule. Kwa hiyo, ukienda mtaani ndiyo maana unakuta wananchi wanasema hali ya uchumi ni ngumu ni kwa sababu fedha nyingi tunazokusanya zinaenda kulipa madeni ya nje na ina-stimulate uchumi wa kule na siyo uchumi wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, hii ni changamoto kubwa, nipende kushauri Wizara ya Fedha labda sijui tufanye road show kwenda kuongea na taasisi za fedha za Kimataifa. Tuangalie ni namna gani tunaweza tukapata fedha za maendeleo kwa sababu local revenue collection ya TRA tayari ina commitment ya wage bill na madeni ya Taifa, sasa tunafanyaje ili kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa.
Mheshimwa Mwenyekiti, siyo mbaya Wizara ya Fedha ikakaa ikaangalia realistically kulingana na picha iliyopo hivi sasa na bajeti ambayo tulipitisha tunafanyaje ku-adjust ili utekelezaji wa hii bajeti uwe realistic na hali ilivyo ukizingatia wahisani wamekuwa wagumu katika kuchangia asilimia zao ambazo tunatakiwa kupata.
Mheshimwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya hitimisho tungependa kujua kwa upande wa Wizara ya Fedha tupate maelezo wanafanya nini ili kukabiliana na hii hali.
Mheshimwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la makadirio ya Pato la Taifa. Ukiangalia drivers za mapato na changamoto za maafa ambazo zimetupata, kwa mfano, kwa Halmashauri ambazo zilitegemea kukusanya mapato kwenye kilimo, hivi sasa kwa sababu ya ukame mapato yatapungua. Kwahiyo, hii pia inaendelea kuweka presha kwenye ukusanyaji wa mapato ya ndani ambayo tulikadiria kwamba yakipatikana ndiyo yasaidie katika kutekeleza bajeti. Kwa hiyo, unaona kwamba issue inazidi kuwa serious, yale mapato ya ndani kuna changamoto zake na mapato ambayo tulitegemea kutoka nje wahisani hawatoi, kwa hiyo hii changamoto is a serious case.(Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, niende kwenye sekta ya kilimo; wote tunakubaliana kwamba sekta ya kilimo ndio uti wa mgongo wa uchumi wetu hasa hasa kwa upande wa Watanzania wengi wanajishughulisha kwenye hii sekta. Kwenye mpango wa maendeleo wa miaka mitano tulichangia, Waheshimiwa Wabunge tukatoa mapendekezo yetu, lakini ikija kwenye utekelezaji bado naona kuna changamoto. Kwa sababu ukiangalia hata fedha ambazo zimeenda kwenye bajeti ya sekta ya kilimo ni kidogo. Ukiangalia ukuaji wa sekta ya kilimo mwaka wa fedha wa 2014/2015 sekta ya kilimo ilikua kwa asilimia 3.4; mwaka 2015/2016 asilimia tatu.
Sasa hivi changamoto ambazo tumezipata za ukame na mabadiliko ya tabianchi sitashangaa tukipata takwimu za mwaka wa fedha 2016/2017 sekta ya kilimo itakuwa imeshuka zaidi. Sasa kwa sababu tuna malengo ya kuwapeleka watanzania kwenye middle income country status, kuna kila haja katika midterm review ya bajeti hivi sasa kuangalia ni namna gani tunakwenda mbele. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, asilimia 70 ya Watanzania wanategemea sekta ya kilimo; nilitegemea kwenye mpango wa Serikali tuangalie ni namna gani tunamsaidia mkulima. Kwenye upande wa pembejeo; pembejeo ambazo tumezipata katika Wilaya zetu ni kidogo mno. Ukiangalia maafisa ugani tuna shortage kubwa kwa kila kijiji, kila Wilaya Maafisa Ugani wa Kilimo ni wachache mno na Maafisa Ugani wa Mifugo ni wachache mno. Hizo ndiyo indicators ambazo tuki-focus nazo na tukazifanyia kazi sekta ya kilimo ikakua tutakuwa tumesaidia kuwainua asilimia kubwa ya Watanzania kwenda kwenye uchumi wa kati. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, kwenye upande wa masoko; lazima ile value chain ya kilimo tuisaidie. Tumepata tatizo la ukame, nilitegemea kuona mipango ya Serikali ya ujengaji wa warehousing, kila Wilaya iwe na maghala ya kuhifadhi vyakula, wakati wa harvest vile vyakula ambavyo vinakuwa ni surplus tunakuwa tuna maghala vinahifadhiwa vizuri, demand na supply vinakuwa-balanced kulingana na serving za mazao kwa kila Wilaya.
Mheshimwa Mwenyekiti, bila hizi warehousing kila Wilaya unakuta wananchi wanalazimika kutumia kile wanachokipata kabla hakijaharibika kwa sababu preservation method za warehousing hatunazo katika Wilaya zetu. Sekta ya kilimo ni nyeti sana na nipende kuishauri Serikali hii midterm review tunayoifanya wajikite sana kwa kuangalia tunawasaidiaje Watanzania kuboresha sekta ya kilimo ambayo inaajiri asilimia kubwa ya Watanzania. Nakushukuru!
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jitihada zenu za kuboresha sekta ya elimu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi, nilishauri na Baraza la Madiwani likapitisha hoja yangu ya kuwa na malengo ya na A-level kila tarafa. Karagwe tuna tarafa tano lakini ipo A- level moja tu. Ninaomba Wizara itusaidie kwenye vipaumbele vya kukamilisha malengo ya A-level mbili kama ifuatavyo:-

Nyaboyonza sekondari bwalo moja, jiko moja, bweni moja na vitanda; Kituntu sekondari bweni la wavulana; Bisheshe sekondari si A-level ila sekondari hii tunaomba msaada ikamilike haraka kusaidia watoto wanaotembea umbali mrefu kupata elimu ya sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupanda madaraja imekuwa tatizo kwa Karagwe, mapunjo ya mishahara, walimu wengi Karagwe kuanzia mwaka 2013 hadi sasa hawajalipwa hiyo fedha na madeni tayari yamehakikiwa na orodha ya walimu wanaodai CWT walipewa orodha hiyo mpaka sasa walimu hawajui muafaka ni lini wanalipwa.

Aidha, kwa walimu Karagwe kuna usugu wa kutopandishwa madaraja kwa zaidi ya 13. Utakapokuja kuhitimisha naomba uniambie tatizo hili linasababishwa na nini? Kwa nini mshahara unachelewa kurekebishwa ili uendane na tarehe ya kupandishwa daraja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, madeni yanayodaiwa na walimu yanakuwa na makato, na hii si haki kwa walimu. Serikali iweke utaratibu wa kulipa riba kwa madeni ya walimu ili walimu hawa wapate time value of money pamoja na consideration ya inflation (mfumuko wa bei).

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejitahidi sana kupitia Mfuko wa Jimbo na michango yangu binafsi kusukuma kazi za uboreshaji wa elimu ya msingi Karagwe. Naomba Wizara iingilie kati kwenye shule ya msingi Ahakanya na shule ya msingi Rwentuhe ambapo walimu na wanafunzi wanasomea kwenye miti. Tayari nilishampa picha za shule hizi Mheshimiwa Waziri Profesa Joyce Ndalichako. Pia shule ya msingi Rweizinga kwenye kijiji cha Mgurika, kata ya Bweranyange kuna baadhi ya wanafunzi wanasomea kwenye darasa la udongo lililoezekwa na majani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni mbili za kupanua Chuo cha VETA cha KDVTC hazijafika kwenye chuo, ninaomba Wizara itusaidie kupata fedha hizi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ya kutekeleza adhma ya Serikali ya viwanda. Ombi, Mkoa wa Kagera tunasahaulika kwenye vipaumbele vya flagship projects hususan uanzishwaji wa viwanda vinavyoendana na comperative advantage za mkoa husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri, wakati ana-wind up atueleze Wanakagera ni lini Serikali itasukuma uwekezaji wa kiwanda cha kusindika nyama ili kusaidia kutunza uchumi wa mkoa kwa kuwa unaongoza kwa wingi na ufugaji ng’ombe nchini. Kufanya hivi kutasaidia kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji inayosababishwa na ng‘ombe wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara itusaidie vijana wa Kagera hususani Wilaya ya Karagwe waweze kuwafikiria na SIDO‘s SME guarantee scheme.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kufanya kazi kwa weledi mkubwa na kwa kuwa wasikivu kwa sisi Wabunge. Pongezi pia zimwendee Katibu Mkuu na watumishi wa Wizara kwa mipango yenye kuleta matumaini ya kumtua mama pamoja na watoto wetu ndoo vichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kutenga $ 30m kwa ajili ya mradi wa Lwakajunju (Kayanga), Ukurasa wa 85 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Naomba Wizara ifanye hima mradi huu uende kwenye utekelezaji, kwani kiasi hicho hicho kilitengwa Financial Year 2016/2017, lakini hakukuwa na disbursement, same amount ime-carry forward Financial Year 2017/2018. Sasa naomba this time twende kwenye utekelezaji kwani mradi huu ndio uhai wa kura za Mheshimiwa Rais, Mbunge na CCM kwani ndiyo ilitusababishia ushindi 2015. Mradi huu naomba usifanye kosa la kushindwa kuacha huduma ya maji kwa vijiji vyenye chanzo (Lake Lwakajunju) yaani Kafunjo, Nyakashenyi, Kijumbura, Bweranyange, Kijumbura, kutasaidia ulinzi shirikishi kwa additional benefits.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iliiomba Halmashauri ya Karagwe kuleta taarifa ya maeneo yenye uhaba mkubwa wa vyanzo vya maji. Rejea barua yenye Kumb Na. DE 208/ 287/OIN/96 ya tarehe 15/04/2016 na majibu ya hiyo barua Kumb Na. KGR/HWK/T.6/9.Vol.1/02 ya tarehe 22/04/2016. Vijiji hivi ni Nyakahita, Kigarama, Kashanda, Chonyonyo, Chabuhora na Kishoju. Naomba sana Wizara itusaidie kwenye utekelezaji wa bajeti iliyowasilishwa na Wizara. Aidha, naomba niongeze Kijiji cha Rwenkorongo nacho kina shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nawapongeza tena kwa kazi nzuri na Mwenyezi Mungu awajalie afya njema. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti hii muhimu sana ambayo inabeba asilimia 65 ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Tizeba na Naibu Waziri, Mheshimiwa Olenasha kwa kazi nzuri wanayoifanya kusimamia hizi Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Pia nichukue nafasi hii kupongeza Kamati ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, kwa kweli wamefanya kazi nzuri ya uchambuzi wa sekta hizi muhimu kwa Watanzania na nina imani kwamba Serikali itazingatia yale mapendekezo mazuri ambayo Kamati imetoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina machache ya kuchangia katika bajeti hii, naomba nianze na suala la kodi kero 17 ambazo zimeondolewa. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kutimiza ahadi ambayo aliahidi wakati wa uchaguzi na kodi kero hizi ziko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Mheshimiwa Rais tunakupongeza sana na tunakuombea ili uendelee kuchapa kazi tutimize zile ahadi ambazo tuliwaahidi Watanzania katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi nzuri, changamoto bado zipo, kwa sababu nia ya Serikali katika kuondoa kero hizi 17 kwenye kahawa ili kumsaidia mkulima wa kahawa bei ya kahawa iweze kupanda. Kuondoa kodi ni hatua muhimu katika kupandisha bei, lakini bei ni factor ya zaidi ya kodi, kuna thamani ya bidhaa yenyewe. Sasa ili zao la kahawa liweze kupanda bei sambamba na upunguzwaji wa hizi kodi kero, Wizara inawajibika kuwasaidia wakulima wa kahawa kuongeza thamani kwenye ile bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna Mfuko wa Kahawa ambao baadhi ya kodi zilikuwa zinaenda kwenye ule Mfuko ili uweze kumsaidia mkulima wa kahawa aweze kulima kahawa ambayo ina thamani. Mfuko huu sijui unasimamiwaje, umekaa kimya, nimefuatilia naambiwa Mfuko hauna hata shilingi moja. Naomba Wizara irudi kuhakikisha Mfuko huu wa Kahawa zile kodi zilizotakiwa ziingie katika Mfuko huu ili uweze kumsaidia mkulima wa kahawa, basi tumsaidie mkulima wa kahawa ili kahawa anayolima iwe na ubora. Kwa vile Serikali imeshaondoa kodi kero hizi 17, basi kahawa ikiwa na ubora ukaongeza hizi kodi ambazo zimetolewa, zitamsaidia mkulima wa kahawa kupata bei nzuri katika kahawa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kodi hizi ambazo zimeondolewa nyingi zimelenga kwenye zile kampuni ambazo zinasindika, sasa trickle down effect ya kodi lazima Serikali isimamie kuhakikisha hii reduction ya kodi ambayo imetolewa inaenda kwa mkulima kwa sababu ndiyo nia ya Serikali kumsaidia mkulima wa kahawa. Kwa hiyo, kupitia Bodi ya Kahawa, kupitia Vyama vya Ushirika Serikali iendelee kufanya hizi reforms ili tuone mwisho wa siku mkulima wa kahawa ndiye anayenufaika along the value chain.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika hili, napenda kuiomba sana Wizara, mara nyingi tunaziachia Halmashauri ndizo zihangaike na kumsaidia mkulima wa kahawa, lakini suala la miche, kama nilivyosema ule Mfuko wa Kahawa, wekeni fedha za kutosha ili tuwasaidie wakulima wapande kahawa kwa wingi na kwa sababu sasa hivi tumeshawaondolea kodi kero ili uzalishaji upande.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Serikali sasa hivi hizi kodi kero ambazo zimeondolewa, ina maana imekosa mapato kwa upande mmoja, lakini tukimsaidia mkulima wa kahawa akapandisha uzalishaji kilimo cha kahawa Serikali itapata mapato kupitia Kodi ya Mapato na halmashauri pia kupitia zile tozo ambazo wanatoza na wenyewe mapato yatapanda. Kwa hiyo Serikali itakuwa imepoteza kwa upande mmoja lakini ime-gain kwa upande mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika mchango wa kilimo kwenye Pato la Taifa. Naomba nitaje takwimu chache ili kuonesha picha ya hali ya Sekta ya Kilimo katika kuchangia Pato la Taifa. Nakumbuka sekta hii ndiyo inayogusa asilimia 65 ya Watanzania, kwa hiyo ni muhimu sana hizi takwimu zikai-alarm Serikali kwamba tujitahidi tufanye reform ambayo itapelekea jitihada nzuri ya Serikali ya kuweka miundombinu ili kutupeleka kwenye uchumi wa kati, jitihada nzuri za Serikali kuhakikisha tunakuwa na uchumi wa viwanda. Ili tuweze kuwa na hiyo socio-economic transformation ya kubeba asilimia kubwa ya Watanzania lazima takwimu hizi tusifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo kwa miaka sasa imegota kwenye asilimia 28 mpaka 29 kama mchango kwenye pato la Taifa. Hii inatuambia kwamba tukiweza ku- double ukuaji wa sekta ya kilimo kwenye pato la Taifa tutakuwa tumewasaidia Watanzania asilimia 65. Kwa hiyo, tuna kila haja ya kuhakikisha tunaisaidia hii Wizara ipate fedha za kutosha kufanya miradi ya maendeleo ili iweze kuinua asilimia kubwa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sekta hii inakua kwa asilimia 1.7 takwimu za 2016, mwaka 2005 sekta hii ilikuwa inakua kwa asilimia 5.2, unaona trend inarudi chini, ni lazima Serikali ifanye kila jitihada ili tuweze kurudisha hii trend ianze kupanda, kwa sababu kukua kwa sekta hii ndiko kunamsaidia Mtanzania ajikwamue kutoka kwenye umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni sehemu ya Azimio la Maputo, hata Kamati ya Kilimo na Mifugo wamelitaja hili. Mwaka 2016 bajeti ya Serikali asilimia 4.9 tu ndiyo ilienda kwenye Sekta ya Kilimo; mwaka 2010 ilikuwa ni 7.8, kwa hiyo unaona trend nayo inashuka. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Kamati ya Bajeti, kaeni tuangalie hizi takwimu zinatupeleka wapi, lazima tuzi-reverse hizi trends tuanze kuelekea kwenye kuhakikisha asilimia 10 ya bajeti ya nchi inaenda kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia disbursement ambayo inaenda kwenye sekta ya kilimo, haiendi yote. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri na Kamati, kilimo peke yake disbursement ilikuwa ni asilimia 3.3, hii ni kidogo mno. Naiomba Serikali kabla ya mwezi Juni kwisha jitahidini angalau tuende kwenye asilimia 50 mwezi ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwenye mifugo kiasi kilichoenda ni asilimia nane tu, hizi takwimu ni alarm, inabidi tufanye u-turn ili tuweze kwenda kwenye trend nzuri ambayo itawainua asilimia kubwa ya Watanzania. Kwa kufanya hivyo, tutahakikisha miundombinu ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inaijenga kukuza uchumi inasaidia Watanzania walio wengi. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kutengeneza malighafi ambazo zitaenda kwenye viwanda hivi ambavyo tunataka kuvitengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hoja hiyo ya mchango wa kilimo kwenye Pato la Taifa, sasa niende kuipongeza Serikali kwa kuleta utaratibu wa Fertilizer Bulk Procurement. Utaratibu huu ni mzuri sana, naipongeza Serikali kwa sababu inaonesha dhamira yake kutaka kumsaidia mkulima aweze kupata mbolea. Katika hili, pamoja na hii jitihada nzuri, Serikali zote duniani huwa kwenye planning na coordination kwa sababu Serikali ni kubwa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii muhimu ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Magufuli na Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuendelea kuchapa kazi ya kuwahudumia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, msingi wa kujenga uchumi wa viwanda unaendana sambamba na kuboresha huduma za jamii ikiwemo kuhakikisha tunapata maji safi na salama kwa kila Mtanzania. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri na hizi jitihada.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu Waziri, wanafanya kazi nzuri, ni wasikivu na kwa kweli nawapongeza kwa kuleta mpango mzuri wa bajeti kwa ajili ya mwaka 2017/2018. Niwape moyo kwa sababu katika bajeti iliyopita hata wenzetu wa Upinzani walikuwa wanasema tuwe tuna realistic budget. Sasa Wizara imeleta bajeti ambayo inatekelezeka na badala yake wenzetu wanasema kwamba iongezwe na wakati hao hao mwaka 2016 walikuwa wanasema tunaleta bajeti ambazo ziko ambitious, tuzi- reduce ziwe realistic. Sasa bajeti imekuja realistic lakini bado unaona wanapinga. Kwa hiyo, mpinzani ni mpinzani. Kwa hiyo, niwape moyo, Serikali chapeni kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeze Kamati ya Maji ya Bunge kwa kuleta hoja ya kuongeza tozo kwenye Mfuko wa Maji. Nawapongeza sana kwa sababu ni muda muafaka kuleta hiyo hoja ili tuweze kuiunga mkono. Nashukuru Waheshimiwa Wabunge wengi wameunga mkono hoja, kwa sababu ukiangalia fedha kutoka kwa wahisani zinazidi kupungua, kwa hiyo, lazima kama nchi tuhakikishe tunaweka utaratibu wa kutoa huduma muhimu kama huduma ya maji kwa Watanzania kwa kutegemea fedha za ndani. Kwa hiyo, naishukuru sana Kamati ya Maji ya Bunge kwa kuleta hii hoja, naomba tuiunge mkono na naamini Serikali ni sikivu, itaichukua na kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hoja hii inatekelezeka kwa sababu tayari tuna uzoefu kwa upande REA. REA tulivyoitengea mfuko, unaona sasa hivi yale matumaini ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma ya umeme, yanatekelezeka. Kwa hiyo, tukifanya hivyo kwenye upande wa maji, naamini kabisa tutafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa niende Jimboni. Naishukuru sana Serikali; namshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Serikali nzima kwa Mradi wa maji wa Rwakajunju kwa kutenga Dola milioni 30 kwa ajili ya kutekeleza mradi huu ambao tumeusubiri sana Karagwe. Naishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha Dola milioni 30, lakini naomba sana sasa twende kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka wa fedha 2016/2017 fedha hii pia ilikuwa imewekwa lakini mchakato ulichukua muda. Kwa hiyo, naiomba Serikali tuweke jitihada ili wana Karagwe tuwatue akina mama ndoo vichwani na watoto wetu ili tuweze kutumia muda huu kufanya kazi za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huu wa Rwakajunju napenda kuiomba sana Wizara izingatie vile vijiji ambavyo vinatoa haya maji vinavyopakana na Ziwa Rwakajunju. Kuna kijiji cha Kafunjo,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi kwa Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazofanya kusimamia Wizara ambayo ndiyo heart beat ya uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inabidi tutumie catch-up economic growth approach as opposed to endogenous technology – driven economic growth approach ambayo wenzetu nchi zilizoendelea zinatumia kwa kutumia industrial revolution ambayo diffusion yake ilianzia England na kusambaa West. Tanzania inabidi catch-up approach tuielekeze kwenye kilimo, ufugaji, uvuvi na ujasiriamali mdogo mdogo ili (taken together) tuweze kutoka kwenye umaskini ambao ni asilimia 65 ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iangalie na kuzipa uwezo TIB na TADB ili ziweze kuwa mstari wa mbele na engine ya kusukuma catch up economic growth ninayozungumzia. Kwa hali ilivyo sasa, kwa kweli bado we are not walking the talk. Nashauri mkae na TIB na TADB muangalie synergies na nani atafanya nini na kwa nini lakini kwa kushirikiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza Sera ya Bima inayoandaliwa 2017/2018. Nashauri NIC ajikite kwenye kusaidia majukumu ya kibima kwenye catch-up economic growth hapo juu. It has to be integrated badala ya kuendelea na business as usual ambayo quite frankly naona tija na weledi wa NIC in its current practice haupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 50 kwa kila kijiji ni vema zikachelewa lakini tukajipanga, tukalenga kwenye kutekeleza catch–up economic growth as argued above. Nashauri mkae na UTT na TADB na kutumia uzoefu wao, washauri model ya kutumia milioni 50 kwa kila kijiji katika namna iliyo endelevu na inayolenga ku-achieve niliyoeleza hapo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Mpango wa Bajeti ya Maendeleo wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2018/2019. Nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa wasilisho zuri la Mapendekezo ya Mpango huu na nimtie moyo kwa sababu ameleta Mpango huu ili tuweze kumpa ushauri na naamini kabisa mna muda wa kutosha kuweza kufanya
review kwa ku-take into account ushauri ambao tunawapa sisi Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze pia kwa kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna ya kipekee walivyoweza kusaidia kutoa commitment ambayo iko serious kwa Mradi wa Maji wa Rwakajunju kwa Wanakaragwe, nawashukuru sana Serikali. Pia nawashukuru kwa commitment ya kuweka lami barabara ya Bugene kwenda Benako ambayo itafungua fursa kubwa sana katika Wilaya yetu na Ngara pamoja na nchi za jirani za Rwanda. Nawashukuru pia kwa commitment ya kuweka lami barabara ya Mgakorongo kwenda Morongwa itatufungulia fursa na ndugu zetu wa Uganda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo pia nitumie nafasi hii kuzungumzia suala la uwanja wa Chato. Mimi nadhani wenzetu upande ule wamekosa, hoja kwa sababu huwezi ukatumia muda mahsusi wa kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Taifa unazungumzia taa kufungwa kwenye uwanja wa Chato. Taa za shilingi milioni tano unasimama Bungeni unasema Serikali imetumia shilingi milioni tano, yaani ni kukosa hoja kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia jiografia ya nchi yetu na nchi za jirani East African Communities na nchi za Great Lakes ni sahihi kabisa kuweka uwanja pale Chato kwa sababu lazima tuangalie future, tusiangalie leo. Chato ina access ya Ziwa Victoria pale, kwa hiyo, ukiweka uwekezaji wa reli ambao utaenda mpaka Rwanda, ukaweka dry port ya Isaka (bandari kavu), ukaweka potential ya kutumia usafirishaji wa maboti ya mizigo kwenda Kenya na Uganda, Chato iko strategically located kwa ajili ya kuhudumia mikoa ya kule upande wa Kagera, Geita hata Kigoma, DRC, Burundi na Rwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye siasa tufanye lakini si kwenye mambo ya maendeleo ambayo yako serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi katika mpango wa maendeleo ulioko mbele yetu nipende kushauri Wizara ya Fedha, kwamba mfanye re adjustment approach. Serikali na nchi yetu, vision ya kuwa na uchumi wa viwanda by 2025 uko clear kwa wananchi wetu, kwa wadau wa maendeleo na kwa private sector na dunia nzima. Kwa hiyo jambo hilo ni muhimu sana kwa sababu tuna vision ambayo tunataka tuhakikishe mpango mkakati unatupeleka kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninachokiona ambacho ni changamoto na muda wa kubadilisha mkakati upo Serikali ime front load sana uwekezaji kwenye sekta ya viwanda na biashara moja kwa moja badala ya kuweka effort kubwa ya ku-facilitate sekta binafsi iwekeze katika viwanda halafu nguvu ya Serikali m-front load bajeti kubwa iende kwenye sekta ambazo zinawahusu Watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mpango wewe ni mchumi, ukiichukua ile Douglas Production Function kwa uchumi wa Tanzania ambao hauko complicated mambo ya financial market, financial derivatives sisi Tanzania we have to do the best with what we have. Tuna ardhi ambayo ni arable tunaweza tukafanya kilimo, tuna labor force ya kutosha, asilimia 67 ya Watanzania wako kwenye sekta ya kilimo.

Kwa hiyo, tunachohitaji pale ni kuwa karibu na hawa wakulima, wafugaji, wavuvi na kuangalia katika maisha yao ya kila siku zile shughuli ambazo wanazojishughulisha nazo, tTukiwasaidia wakapiga hatua mbili, ile asilimia 67 ya Watanzania ambao wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: ... itasaidia kukuza uchumi na kupunguza umaskini.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na Wizara nzima kwa kazi nzuri ya kusaidia kuweka miundombinu wezeshi ya kukuza uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Wilaya ya Karagwe barabara ya Nyakahanga – Nyakakika (kilometa 96) imekasimishwa TANROADS (2017/2018) na ilitengewa shilingi milioni 150. Fedha hizi ni kidogo mno ukilinganisha na ukorofi wa barabara. Financial year 2018/2019 imetengwa hiyo hiyo shilingi milioni 150, ninasikitika hii fedha haitaweza kutosha maeneo yote korofi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi, barabara hii ni korofi sana naomba iongezewe fedha; ahadi ya kilometa tano za lami kwenda eneo korofi zaidi la Kajura Nkeito naomba itimizwe, eneo hili lipo barabara hii tajwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Bugene – Benako ni financial year ya pili bajeti zinatenga hewa kwa ajili ya kujenga kwa kiwango cha lami, kwa nini? Je, wananchi wa hii barabara watalipwa lini fidia zao? Detailed design imekamilika.


Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mugakorongo – Marongo kwa nini detailed design yake inachukua muda mrefu na wakati barabara hii ikiunganishwa na ile ya Bugene – Benako zinaunganisha Afrika Mashariki na kukamilika kwake kutachochea uchumi wa Kagera na nchi yetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Wizara iongeze bajeti ya TARURA kwani hizi feeder roads za vijiji ndizo tunazitegemea kusafirisha mazao ya wakulima, wafugaji na wafanyabiashara wadogo kwenye kuzalisha uchumi wa kaya na nchi. Ratio ya mgao iwe angalau 40/60 minimum. Ideally ration iwe 45/55.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee namshukuru sana Meneja wangu wa TANROADS Mkoa, Engineer Kasamwa kwa kazi nzuri ya kusimamia kazi za mkoa na kwa ushirikiano anaonipa. Ni matumaini yangu maombi yangu yatakubaliwa. Nawatakia majukumu mema. Ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema nikaweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kutoa mchango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la REA, na katika hili suala la REA nianze kwa kuipongeza Serikali. Kupitia REA Serikali inafanya kazi nzuri ya kuwapelekea vijijini huduma hii muhimu katika maendeleo ya Watanzania. Pamoja na jitihada nzuri za kupeleka umeme vijijini kupitia REA, changamoto za REA ukiziangalia kwa kwa undani zinasababishwa na mambo makubwa mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, mimi nipo kwenye Kamati ya Nishati na Madini, tumekuwa tukiishauri Serikali zile tozo za kutoka kwenye mafuta kwenda kwenye mfuko wa REA zimekuwa ring-fenced lakini kumekuwa kuna mkwamo, ile hela haiendi moja kwa moja kwenye mfuko ili iweze kwenda kwenye REA kuhudumia usambazaji wa umeme vijijini.

Kwa hiyo, nipende kuiomba Serikali wakati wanafanya wind up tusikie upande wa Serikali ni lini hii automation ya transfer ya hela, kwa sababu mwananchi akienda kununua mafuta kwenye sheli (Shell/Petrol Station) ile tozo inatozwa pale pale analipa cash, sasa kwanini kunakuwa kuna mkwamo? Kwa nini hii hela isiende moja kwa moja kwenye mfuko wa REA ili wakala wa REA waweze kusambaza umeme vijijini bila kusuasua? Pia kwenye REA hapo hapo kwa upande wa TANESCO ukiangalia TANESCO na REA wanavyofanya kazi ni sawa na treni ambayo ina mabehewa mengi lakini ina kichwa cha treni ambacho uwezo wa engine yake ni mdogo sana.

Mheshimiwa MNaibu Spika, kichwa cha engine ni upande wa TANESCO; TANESCO ina madeni makubwa imefika kwenye point ambapo inaweza ika-collapse kwa sababu inadaiwa na inashindwa kutoa huduma ya umeme nchini kwa sababu ya madeni makubwa zile cost za maintenance zimekuwa accumulative. Kwa hiyo, ile speed ya REA kusambaza umeme vijijini inakwamishwa na TANESCO kushindwa kufanya majukumu yake kwa sababu haina pesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipendekeze Serikali ifike mahali idara zile za REA ambazo zinahusika na kusambaza umeme vijijini tuvi-merge na REA ili ule ufanisi wa REA zile idara ambazo zipo upande wa TANESCO ambazo zinahusika na huduma za umeme vijijini viwe-merged kwenye REA ili REA iendelee kufanya kazi vizuri kama inavyofanya; halafu TANESCO inayobaki iendelee kutoa huduma ya umeme maeneo ya mjini. Tukifanya hivyo wananchi wetu vijijini watapata umeme vizuri bila kusua sua na upande wa mijini TANESCO itajikita kutoa umeme mjini. Hii itatupeleka kwenye dhamira ya kwenda kwenye uchumi wa viwanda na kwenda kwenye uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ningependa kulizungumza ni miradi mikubwa ambayo Watanzania wanaisubiri kwa hamu kubwa sana ya kutufikisha kwenye uchumi wa viwanda. Miradi hii ni pamoja na Mradi wa Stigler’s Gauge ambao ni mradi mkubwa sana. Ninamshukuru Rais Magufuli na Serikali ya Awamu ya Tano kwa kulisimamia hili. Mradi wa Standard Gauge Railway ni mradi mkubwa sana, Tanzania itakuwa kama Ulaya miradi hii ikitekelezwa. Hata hivyo sisi Bunge tunatakiwa tuwe sehemu ya kui-facilitate Serikali iweze kutekeleza miradi hii kwa kasi ya haraka sana kwa sababu Watanzania wanasubiri miradi hii kwa hamu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nipende kupendekeza kwa mikopo ya nje ambayo inaweza ikawezesha Serikali kutekeleza miradi hii. Ifike mahali tuangalie mechanism ya Bunge ya kuwa na oversight kwa Serikali lakini bila kuikwamisha Serikali katika kuwa na wigo wa kwenda kukopa mikopo ya bei nafuu. Wakati tunajadili Kamati ya bajeti hapa kulikuwa kuna hoja kwamba kwa nini Serikali imekopa additional ya shilingi bilioni 1.46 kabla ya kuja Bungeni.

Sasa nipende kupendekeza kwamba Serikali mje na mechanism ambayo itatufanya sisi ile checks and balance yakuisimamia Serikali inakuwepo. Lakini Serikali bado mnakuwa na freedom pale fursa inapojitokeza ya kukaa na hizi Development Financial Institutions, kukaa na wale wanaoweza kutupa mikopo ya bei nafuu kwa ajili ya miradi ya bei nafuu kama Stigler’s Gauge na SGR muweze kufanya hivyo kwa sababu hakuna Serikali ambayo inadhamira ya njema na Watanzania kama Serikali ya Awamu ya Tano. Sasa kwanini tuwe sehemu ya kikwazo badala ya kui-facilitate ili iweze kutoa maendeleo ambayo tumewaahidi Watanzania kwa kasi ambayo Serikali inataka twende. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kuhusu upande wa sekta ya madini hasa hasa wachimbaji wa kati na wadogo. Kwa miaka mingi tumeona watu wanaochukua hizi Special Mining Licenses, tumehangaika nao, lakini kwa sababu ya uchanga wa sekta na taasisi zetu kuendelea kuzijengea uwezo tumekuwa na changamoto kubwa sana ya kupata fair share ya tax collection.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nipende kupendekeza kwamba Serikali ifike mahali jitihada zote tuzipeleke kwenye hawa wachimbaji wa kati ambao tukiweza kuwa-facilitate wataweza kutengeneza ajira humu humu nchini na pia yale mapato ambayo wanayapata yatawekezwa hapa hapa Tanzania, badala ya kuendelea kuangaika na ku-facilitate wawekezaji wakubwa wa Kimataifa ambao wanafanya tax planning, madini yetu yanaenda kodi hatuzioni, wanatuachia mapango tu kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Serikali kwa sababu ipo katika ku-reform ili kuhakikisha resources za nchi zinawanufaisha Watanzania jambo hili nadhani limefika mahali pake. Tumetembea kwenye mikoa ambayo inachimba dhahabu wachimbaji wa kati wana uwezo mkubwa sana. Teknolojia za dunia sasa hivi zinaweza zikawa adopted na hawa wachimbaji wa kati wakaweza kuisimamima migodi vizuri lakini pia wakaajiri Watanzania na mapato wanayopata yanabaki hapa hapa nchini.

Kaka yangu Mheshimiwa Lubeleje ameniomba dakika chache nimuachie kwa hiyo naomba niishie hapo ili Mheshimiwa Lubeleje kaka yangu uweze kutumia hizo dakika. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nianze kwa kuendelea kuwapa pole wananchi wangu wa Karagwe kwa pengo kubwa tulioachiwa na ajali ya City Boys, Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu waliofariki mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda mimi nina mambo mawili; nianze na suala la kahawa na katika hili niipongeze Serikali kwa kuja na mfumo wa stakabadhi ghalani, lengo la kuleta mfumo wa stakabadhi ghalani ni kumsaidia mkulima wa kahawa ili aweze kunufaika na zao la kahawa na zao hili limsaidie kumtoa kwenye umaskini. Sasa ili tuweze kutimiza hii dhamira nzuri ya Serikali mimi Serikali naishauri mambo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwenye suala la butura; namna pekee ya kupambana na changamoto ya butura ni Serikali chini ya Vyama vya Msingi kuanzisha SACCOS ambazo zitakuwa zinakopesha wakulima wakati kahawa iko mashambani inasubiri kukomaa kuiva basi Serikali chini ya Vyama vya Msingi ianzishwe SACCOS itoe mikopo ya bei nafuu ili mkulima aweze kukopa na pale vyama vya ushirika vitakapouza kahawa yake aweze kukatwa mikopo hii ya bei nafuu. Kwa hiyo, hiyo ndio namna ambayo itatusaidia kuondokana na changamoto ya Butura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili pamoja na nia njema ya Serikali huu mfumo wa stakabadhi ghalani ili iweze kuleta weledi na uweze kumsaidia mkulima wa kahawa inabidi tujipange. Sasa bahati mbaya mfumo huu umeletwa wakati tunaingia kwenye msimu wa kahawa mwaka huu. Ushauri wangu kwa Serikali ili tuweze kujipanga vizuri maana kahawa lazima tuhakikishe iwe na ubora na ubora huu ndio itausaidia kupata bei nzuri sokoni. Serikali itumie mwaka huu kujipanga ili msimu wa mwaka unaokuja ndipo twende kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani, tutumie mwaka huu kuhakikisha kahawa inapotoka mashambani kwenda kwenye mnada ubora unazingatiwa kuanzia shambani kuna mambo ya miundombinu ya maghala, vyama vya ushirika vina madeni sasa hatujui Serikali imejipangaje kukaa na hivi vyama vya ushirika kuhakikisha haya madeni hayahamii kwa mkulima wa kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mambo haya yanatakiwa atupate muda wa kujipanga ili tutakapohamia kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani basi mfumo umsaidie kweli kweli mkulima wa kahawa kumkwamua kutoka kwenye umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuzungumzia ni mfuko wa uwezeshaji wananchi chini ya ofisi ya Waziri Mkuu. Mfuko huu ni wa muhimu sana hasa hasa kipindi cha sasa hivi cha Serikali ya Awamu ya Tano ambapo tunalenga kwenda kwenye uchumi wa kipato cha kati kupitia uchumi wa viwanda na tumekuwa tukisisitiza kwamba Serikali ijikite kwenye kusaidia Watanzania wengi katika shughuli ambazo Watanzania wengi wanajishughulisha nazo kilimo, mifugo na biashara ndogondogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfuko huu na sisi Wabunge wote humu ndani kwenye Wilaya zetu tumehamasisha watanzania Serikali hawezi kumsaidia Mtanzania mmoja mmoja tumehamasisha Watanzania wajiunge katika vikundi vya akina mama na vijana ili kupitia mfuko wa uwezeshaji wananchi kiuchumi ofisi ya Waziri Mkuu Serikali iwapatie mikopo ya bei nafuu. Sasa mfuko huu una bilioni 1.6 peke yake na toka mwaka 2013 mfuko huu haujawahi kupewa hata shilingi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali hii Mwananchi Empowerment Fund ipeni hela ya kutosha iweze kuwasaidia wananchi kupitia vikundi vya wakina mama na vijana hasa vijijini ambapo tayari tumeshahamasisha na programu ya shilingi milioni 50 najua Serikali huko miaka ya mbeleni itaileta lakini tukitumia mfuko huu utawasaidia wakinamama na vijana Tanzania kuendelea na biashara ili zile shilingi milioni 50 zitapokuja baadae ziwakute wako katika kuzalisha shughuli za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nipende sana kuomba Serikali ilichukue hili Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi upewe hela ya kutosha; shilingi bilioni 1.6 ni hela ndogo...

(Hapa Kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa watumishi wa Wizara kwa kazi nzuri. Changamoto zinazozungumzwa na Wabunge mkizifanyia kazi zikaungana na yale mazuri mnayofanya, hakika tutapiga hatua katika sekta hii kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara izingatie na kusimamia matumizi bora ya ardhi katika kutatua migogoro ya wakulima, wafugaji na wawekezaji kwenye Ranchi za Kitengule, Kikurula na Mwisa. Nashauri yafuatayo yafanyike:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ikae na wawekezaji wa Kitengule na Kikurula Ranch akiwemo Super Doll na kuhakikisha mpango kazi wa matumizi ya ranchi yanaheshimiwa. Maelfu ya hekta zimetolewa Kitengule ila matumizi bora ya ardhi (ranchi ) hayazingatiwi.

Mheshimiwa Spika, interest yangu Mbunge na Wana Karagwe ni kuona wawekezaji kwenye Ranchi za Kitengule na Kikurula wanasaidia kutengeneza ajira kupitia matumizi bora ya ardhi (uwekezaji), wanachangia kipato cha Taifa (kodi na CSR) kwa kata zinazozunguka ranchi.

Mheshimiwa Spika, vikundi 25 vya Karagwe vya SACCOS za wafugaji, naomba sana vipate vitalu Mwisa II kuondoa migogoro ya ardhi kati yao na wakulima na wawekezaji niliowataja hapo juu.

Mheshimiwa Spika, Chuo cha Ufugaji cha Kikurula kimesahaulika, naomba Serikali ikisaidie ili kipate kipaumbele kwenye bajeti ya maendeleo na kiwe center of excellency kwa Kanda ya Ziwa. Ahsante sana.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watumishi wa Wizara kwa jitihada nzuri za kusimamia sekta ya utalii na shughuli zote za Wizara.

Mheshimiwa Spika, ushauri, takwimu za mchango wa sekta kwenye pato la Taifa (17%) na rate ya ukuaji ya number of arrivals kwa mwaka (3.3%) haziridhishi. Tanzania ina unique comparative advantage za kijiografia ambazo bado lazima ziwe optimized ipasavyo. Vikwazo ninaviona ni viwili.

Mheshimiwa Spika, kwanza Benchmark Tax Region ya sekta ya utalii against nchi washindani wetu. Findings za benchmarking zisaidie Wizara kukaa na Wizara nyingine zinazohusika (mfano Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji na Ofisi ya Makamu wa Rais) na kujadili kwa pamoja ulazima wa kuboresha tax region ya sekta kuongezeka competitiveness.

Mheshimiwa Spika, strategy, Wizara iache mazoea ya kutegemea TTB pekee kufanya promotion marketing. Angalia nchi nyingine zilizofanikiwa wametumia modality zipi kufanya promotion and marketing.

Mheshimiwa Spika, naomba vigingi vilivyowekwa kwenye vijiji vya Mgoruka, Rweizinga zoezi lirudiwe upya na kushirikisha wananchi pamoja na mimi Mbunge ili kuleta ustawi mzuri na ujirani mwema kati ya wananchi wangu na mapori akiba ya Kimisi na Burigi.

Mheshimiwa Spika, kaeni na Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji muangalie namna ya kushirikiana ili kutumia teknolojia ya majiko jadidifu kama mbadala wa utumiaji wa mkaa. Kutumia mabavu kukataza utumiaji mkaa si sustainable na ni ishara ya kukosa innovation na mikakati ndani ya Serikali.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukupongeza wewe kwa kutuongozea kikao vyema, lakini pia niungane na waliyochangia kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati zote mbili pamoja na Wajumbe wa Kamati hizi kwa kazi nzuri ambayo mnafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawapongeza Wenyeviti kwa Mawasilisho mazuri, lakini kipekee nitumie nafasi hii kuishukuru sana Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mwenyekiti, Mheshimiwa Vita Kawawa, Makamu Mwenyekiti Vincent Mbogo pamoja na Wajumbe wote wa Kamati kwa ushirikiano mzuri na maoni, ushauri na maelekezo ambayo mnatupatia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, tunawashukuru sana kwa ushirikiano huu. Pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango na yale ambayo Bunge litaazimia lakini pia maoni na ushauri ambao wametupatia tunaenda kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza mpendwa wetu Mheshimiwa Rais na Amir Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan. Katika michango ya leo na katika Bunge hili Mheshimiwa Rais, Waheshimiwa Wabunge wamempongeza kwa kazi nzuri ya kuimarisha diplomasia ya uchumi na diplomasia ya uchumi pamoja na diplomasia ya ulinzi ni vitu pacha. Kwa hiyo Mheshimiwa Rais, kazi nzuri ambayo ameifanya ya kuhimarisha diplomasia ya uchumi, kazi hiyo hiyo nzuri imetuimarisha katika suala la diplomasia ya ulinzi. Kwa hiyo na hilo tunamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri wenzangu, kama wanavyofahamu majeshi yetu yanayo mahitaji makubwa, yapo mahitaji ya kisekta na katika hili niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri. Ukienda kwenye Vikosi na maeneo ya Majeshi yetu utakuta wanahitaji huduma ya maji, kwa hiyo itabidi tukae na Wizara ya Maji; Barabara wakati mwingine kwa shemeji yangu Angellah Kairuki upande wa TARURA; Mheshimiwa Profesa Mbarawa upande wa TANROADS na Sekta nyingi. Kwa hiyo niendelee kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa ushirikiano wanaotupatia katika kuhudumia majeshi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye hoja. Moja ya michango ya Waheshimiwa Wabunge, ilikuwa ni ni kuhusu ajira kwa vijana wetu kupitia JKT. Ningependa kuwakumbusha kwamba, jukumu la kwanza na kubwa la JKT toka suala la kujiunga na JKT kwa mujibu wa sheria liliporudi mwaka 2013, yamekuwa masuala ya kuwajenga vijana kimaadili na kiuzalendo. Hata hivyo, kutokana na changamoto ya ajira nchini, Serikali imefanya kila aina ya jitihada hata kupitia JKT, wale vijana ambao wanaenda kwenye mafunzo ama kwa mujibu wa sheria ama kwa kujitolea, jitihada za Serikali zinaendelea kufanyika kuhakikisha kwa kadri inavyowezekana vijana hawa wanapata ajira kupitia kwenye Vyombo vya Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Takwimu za 2018, 2019 na 2020, vijana ambao wameenda JKT asilimia 45 wamepata ajira kwenye Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama. Serikali tunaendelea kuwa wabunifu hasahasa kwenye masuala ya mawanda upande Sekta za Uzalishaji ili kuhakikisha hata hii asilimia ambayo hawapati fursa kwenye Vyombo vya Ulinzi na Usalama, wanapata fursa kwenye maeneo mengine likiwemo suala ambalo Mheshimiwa Hussein Bashe, amelitaja Memorandum of Understanding kati ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Wizara ya Kilimo. Sasa hivi iko tayari na panapo majaliwa wiki ijayo tutaisaini ili kujikita zaidi kwenye program za Wizara za Kilimo, kwa mfano, kuna Skimu ya Umwagiliaji kule Chita. Kupitia skimu hii kwa Takwimu ambazo Mheshimiwa Waziri Bashe, amezisema kwa mfano uzalishaji wa mbegu za alizeti tani 500 zimefanyika kupitia program hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeendelea kushirikiana na Wizara ya Kilimo kuzalisha mbegu za mazao mbalimbali kwa mfano upande wa MAhindi tumezalisha tani 300 kupitia JKT, upande wa mpunga tumezalisha tani 468, upande wa mazao ya mafuta tumezalisha mbegu tani 206, lakini hata kwenye mazao ya chakula mahindi tumezalisha tani 3,876, Mpunga tani 1,276, hizi ni takwimu za mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, kila sekta kuwa wabunifu katika kuhakikisha tunazalisha ajira milioni nane kama tulivyoahidi kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 – 2025, tutaendelea kushirikiana na Wizara za Kisekta kubuni mawanda ambayo yatasaidia vijana wengi kupata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunaliangalia ili kusaidia vijana kupata ajira ni kuangalia mitaala ambayo inafundishwa kwenye upande wa ufundi stadi na JKT. Kuangalia namna ya kupata accreditation ili vijana wanaopata ufundi stadi upande wa JKT iwe ni sawa na yule ambaye amehitimu VETA na Taasisi nyingine ambazo zinatoa Vocational Training.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie pia hivyo hivyo, kulikuwa na hoja ya uhitaji wa kuweka alama za mipaka pamoja na barabara za ulinzi; Waheshimiwa Mawaziri, Dada yangu Mheshimiwa Angeline Mabula, Waziri wa Ardhi; Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Waziri wa Ujenzi; pamoja na Mheshimiwa Mwigulu, Waziri wa Fedha, tumevichukua hivi, tutaendelea kushirikiana nao ili tuweze kuvitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii na naunga mkono hoja.(Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya pamoja ya ziada ya Nagoya – Kuala Lumpur kuhusu Uwajibikaji Kisheria na Fidia kwa Madhara yanayoweza kutokea kutokana na matumizi ya Bioteknolojia ya Kisasa katika Kutekeleza Itifaki ya Cartagena (Nagoya – Kuala Lumpur Supplementary Protocol on Liability and Redress on Cartagena Protocol on Biosafety) pamoja na Azimio la Kuridhia Itifaki ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika kuhusu Kulinda Haki Miliki za Wagunduzi wa aina mpya za Mbegu za Mimea. (Protocal for Protection of New Varieties of Plants (Plant Breeder’s Rights) in The Southern African Development Community – SADC) pamoja na Azimio la Kuridhia Mkataba wa Marrakesh wa mwaka 2013 unaowezesha upatikanaji wa kazi zilizochapishwa kwa watu wasioona, wenye uoni hafifu au ulemavu unaomfanya mtu kushindwa kusoma (The Marrakesh Treaty to Facilitate Access to Published Work For Persons Who Are Blind, Visually Impaired or Otherwise Print Disabled)
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuhitimisha hoja ya Mkataba wa Marrakesh. Pia naishukuru sana Kamati ya Viwanda na Mazingira kwa ushirikiano walioipa Wizara yangu katika mchakato mzima wa kuandaa azimio hili mpaka kufikia Bungeni leo hii. Nawashukuru sana Mheshimiwa Suleiman Saddiq Murad, Col. Masoud pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ya Viwanda Biashara na Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Naibu Waziri Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya, Katibu Mkuu, Mkurugenzi wa COSOTA na wataalam wote kwa kazi nzuri walioifanya katika maandalizi ya azimio hili la Mkataba wa Marrakesh.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawashukuru sana Chama cha Wasioona wakiongozwa na Mwenyekiti Lucy Benito pamoja na Emmanue Simon, Katibu; nawashukuru sana kwa kufika kwenye Bunge letu Tukufu kushuhudia azimio letu hili muhimu sana kwa walengwa wetu, ndugu zetu, watu wenye ulemavu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Naibu Waziri, dada yangu Mheshimiwa Stella Ikupa, Mheshimiwa Balozi Venance Mwamoto, Mheshimiwa Dada Amina Mollel na Mheshimiwa Kaka Ally Saleh, wametoa mchango mkubwa sana katika kusukuma azimio hili liweze kufikia hatua muhimu ya leo. Nawashukuru sana Waheshimiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia, waliotoa ushauri na wale ambao hamjachangia, wote najua mnaunga mkono hoja hii. Tunawashukuru sana kwa niaba ya ndugu zetu watu wenye ulemavu, nawashukuru sana kwa kuunga mkono hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi nimekuja kushukuru kwa sababu hoja hii haijapingwa na Mbunge hata mmoja zaidi ya kutoa maoni ushauri na tumeelekezwa na Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira pamoja na michango ya Waheshimiwa Wabunge kwamba mara tu baada ya kuridhia Itifaki, basi tujitahidi sana marekebisho ya Sheria ya COSOTA yafanyike haraka iwezekanavyo ili ndugu zetu walengwa waweze kunufaika na itifaki hii, nasi kama Serikali, ushauri huu tumeuchukuwa tutasukuma kwa nguvu ili mapitio ya sheria hizi yaweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na concern ya copyright kwa mwandishi wa awali, pale ambapo maandishi yake yanahamishwa kwenye muundo wa nukta nundu, kwamba copyright yake, intellectual propaties, atapoteza ile haki, lakini napenda kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge, kuhama kwa machapisho kunahama pia kwa copyright ya author. Kwa hiyo, jambo hili nilitaka kuwaondoa wasiwasi, copyright inahama pamoja na muundo wa machapisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Ally Saleh kama alivyopendekeza, tuna fursa ya kujifunza kutoka kwenye nchi ambazo tayari zimesharidhia. Kwa hiyo, tutaangalia best practice kwenye hili pamoja na mengine ili kuhakikisha mapitio na ya sera na sheria yanakidhi kiu na nia ya kuhakikisha mkataba huu unawasaidia ndugu zetu wasioona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulitolea maelezo ni suala la ushirikishwaji wa wadau. Mchakato mzima umeshirikisha wadau kikamilifu; na kwa mara nyingine niwashukuru sana ndugu zetu upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wadau wote kupitia COSOZA wametupa maoni mazuri sana ambayo yamepelekea kukamilika kwa mchakato wa kushirikisha wadau na kuleta azimio hili hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutahakikisha maudhui ya itifaki yanatafsiriwa katika Kiswahili ili yaweze kupatikana kote nchini kwa walengwa wetu pamoja na suala zima la kanzidata kama ilivyoshauriwa. Kuwa na kanzidata ni muhimu sana kwa sababu itatusaidia kuwahudumia walengwa wetu vizuri. Kwa hiyo, jambo hili nalo tumelichukuwa tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa kunipa nafasi hii tena na ninaomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii adimu ili niweze kuchangia bajeti kuu ya Serikali. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kama Waziri wa Viwanda na Biashara naomba uniongezee dakika moja ya kushukuru. Nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kuamini vijana kwamba tunaweza kuweka mchango mkubwa katika Taifa hili. Mheshimiwa Rais Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru Makamu wa Rais, Waziri Mkuu pamoja na wewe, pamoja na Bunge kwa support ambayo mnaendelea kunipa katika kutumika wananchi na kutumia Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kushukuru sana kwa michango ambayo Waheshimiwa Wabunge wametoa katika kuchangia hii bajeti kuu ya Serikali. Michango mikubwa ambayo inahusu Wizara yangu imejikita zaidi kwenye masoko ya uhakika kwa mazao ya wakulima wetu na nitatumia muda mwingi kuzungumzia hili kwa sababu ya umuhimu wake. Mheshimiwa Rais wetu amekuwa akizungumzia nia ya kuunganisha kilimo na viwanda kwa sababu tukifanya hivyo tutawainua wakulima wengi nchini kwenda kwenye uchumi wa kati, kwa hiyo hoja yangu imejikita zaidi kwenye industrialization agriculture.

Mheshimiwa Spika, nikianza na mazao ya kimkakati, hata leo imetolewa mwongozo kuhusu zao la pamba. Pamoja na jitihada nzuri za Serikali kusaidia Ginners nchini, lakini wakulima wetu wamehamasika kwenye upande wa zao la pamba, uzalishaji umetoka tani 222,000, msimu huu tunategemea kuvuna tani zisizopungua 400,000.

Kwa hiyo kuendelea kutegemea Ginners peke yao kama soko la wakulima wa pamba hatutaweza kutoka kwenye mkwamo wa bei kushindwa kupanda. Kwa hiyo katika hili Serikali tumeazimia kuhakikisha textiles ambazo zilibinafsishwa lakini hazifanyi kazi, baada ya Bunge hili naanza nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Textiles nchini zilikuwa 32, sasa hivi zimebakia tano ambazo zinafanya kazi, wengi wamekiuka mikataba ile ambayo walisaini kwa mujibu wa ubinafsishaji. Sasa Serikali tunataka kuhakikisha textiles hizi zinafanya kazi ili wakulima wa pamba wanapolima, tusitegemee tu kwamba Ginners liwe soko peke yake. Ile sera ya C to C (Cotton to Cloth) sasa tunaanza kwenda kwa vitendo kuhakikisha mkulima anapovuna shamba, soko lingine linaenda kwa Ginners lakini soko lingine linaenda kwenye textiles ili ziweze kutengeneza garments, ziweze kutengeneza pamba nyuzi na wakulima wetu wapate soko la uhakika.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hili, nitumie nafasi hii kutoa clarification kuhusu zao la korosho. Kumekuwa kuna upotoshaji mkubwa sana na upotoshaji huu umepelekea dunia kuamini kwamba korosho yetu imeoza kumbe siyo kweli. Baada ya kuapishwa nimetumia wiki nzima nikienda ghala kwa ghala kwenye mikoa inayolima korosho, korosho yetu iko katika hali nzuri.

Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge niwaombe tuweke utaifa mbele na uzalendo mbele, hakuna korosho ambayo iko reject hata moja, korosho yote ni grade I na grade II. Sasa tunapowasiliana na wanunuzi duniani kuna watu bado wanaendelea kupotosha kwamba msinunue korosho ya Tanzania siyo safi.

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge hili kuwaambia wananchi, Serikali is open for business, korosho yetu ina ubora, Waheshimiwa Wabunge wanaotoka kule wanajua. Tuwe wamoja, tushirikiane Taifa moja kuhakikisha tunawasaidia wakulima wa korosho, tutoe hii korosho lakini msimu unaokuja tukijipanga vizuri hata zao la korosho bado lina potential kubwa ya kuwasaidia wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa sababu ya muda niseme kwamba kuhakikisha viwanda vilivyobinafsishwa vinaanza kufanya kazi, lakini pia tunafungua fursa za masoko za kimataifa kwa kushiriki katika forum za kimataifa kama World Economic Forum, kuhakikisha tunashirikiana na Balozi zetu, kuwa na mkakati mzuri wa kutafuta masoko ya uhakika. TANTRADE tunai-reform upya ili iweze kujikita katika kuhakikisha inakuwa interface ya nchi na dunia kutafuta masoko ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Mpina, Waziri wa Mifugo na Uvuvi pamoja na Mheshimiwa Japhet Asunga, Waziri wa Kilimo tumejipanga katika kuhakikisha tumejipanga katika kuhakikisha tunafungamanisha hizi sekta na kuhakikisha tunaongoza Serikali na Watanzania kwenda kwenye uchumi wa viwanda kupitia value adding. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, kwa sababu ya muda kutotosha nimalizie na suala la blueprint.

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mbilinyi.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri mpya wa Viwanda na Biashara anayechangia kwamba hivyo viwanda vilivyobinafsishwa anavyozungumzia kwamba baada ya Bunge atarudi kuanza navyo ili avirudishe kazini, nataka nimpe taarifa kwamba vingi hata ile mitambo hakuna ilishang’olewa. Kwa hiyo anaona kiwanda ni kama godown tu lakini ndani mitambo hakuna tena, kwa hiyo kama kilikuwa kiwanda cha textile ndani ya hicho kiwanda hatakuta mitambo kwenye maeneo mengi sana. Naomba alijue hilo.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, taarifa ya ndugu yangu Mheshimiwa Sugu siipokei kwa sababu sisi viwanda vilivyobinafsishwa hata infrastructure bado ni value na tunataka tukae na wawekezaji wale ambao wako serious tukae nao tuingie joint venture, waingie kwenye mpango kazi wa kusaidia kuhakikisha tunachakata mazao ya wakulima kwa ajili ya soko la ndani. Tanzania ni member wa East Africa tunalipa fees kila mwaka kushiriki katika hiyo membership, ni member wa SADC, hayo yote ni masoko ambayo tungependa nchi yetu iwe ni production hub kwa ajili ya hayo masoko pamoja na maeneo mengine ya dunia. Kwa hiyo, katika hili niwape tu confidence kwamba Serikali tukihakikisha vile viwanda vilivyobinafsishwa vinafanya kazi wakulima wetu hawawezi kupata shida katika masoko ya mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka kumalizia na suala la blueprint, Serikali tumeanza katika bajeti hii kodi kero 54 zimeondolewa na tayari tuna action plan. Kwa hiyo ni kukuomba wewe pamoja na Wabunge tushirikiane katika kuhakikisha tunaondoa unnecessary red tapes ambazo zimekuwa zikiwakumba wafanyabiashara nchini. Serikali katika hili nia yetu na tumejipanga vizuri katika kuhakikisha tunafanikisha katika hilo. Kikubwa ni change of mindset yaani Watanzania tuichukulie biashara kama ni fursa ya kutengeneza ajira kwa vijana na akina mama nchini lakini Private Sector Development ndiyo injini ya kusaidia uchumi wetu ukue katika namna ambayo ni sustainable.

Kwa hiyo Watanzania ile mindset ya ku-frustrate biashara tutoke huko tu-facilitate kila mmoja katika nafasi yetu ili private sector iweze kukua na kutengeneza ajira kwa vijana na akinamama. Tutafanikiwa katika hili kama tutashirikiana kuhakikisha blueprint na action plan yake wote tunashirikiana kwa pamoja kuhakikisha inatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu tutahakikisha sera za viwanda ambazo ni za mwaka 2003 nilizozikuta, tunafumua zote na ku-update kwa sababu ukitegemea kwenda kwenye uchumi wa viwanda kwa kuwa na injini ya Vits inayovuta Semi-trailer hatuwezi kufika. Kwa hiyo pa kuanzia ni kuhakikisha sera hizi za zamani za 2003 tunazi-overhaul ili ziweze ku-reflect priority ya nchi ya kwenda kwenye uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali. Naomba nianze kwa kuunga mkono hoja asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuleta muswada wa muhimu katika kujenga mustakabali wa nchi yetu hasa hasa kwenye maeneo ya usimamizi wa fedha za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria na Katiba pamoja na Wajumbe wa Kamati kwa maoni na ushauri wao ambao wameutoa katika kuboresha muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nijikite kwenye kipengele cha mikopo, msaada na dhamana, hasa kwa upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Taasisi za Umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu sasa hivi kuna ushindani mkubwa katika International Capital Markets. Muswada huu umelenga kuzisaidia Serikali zote mbili, kwa maana ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili ziweze kushirikiana katika kuhakikisha ukienda kukopa kwenye Masoko ya Kimataifa ya Mikopo basi sheria zetu zinatusaidia kupata mikopo hii kwa masharti nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye International Capital Markets bila sheria za namna hii tunaweza tukawa tuna mipango mizuri, tukapitisha bajeti zenye mipango mizuri ya maendeleo lakini sheria zikatukwamisha. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kuangalia hili, kwa sababu maboresho ya muswada yanalenga kusaidia Serikali zetu ziweze kupata mikopo ya bei nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuwasihi Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa jicho la tofauti kwamba pengine muswada huu unalenga kukandamiza maslahi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Mimi siioni hivyo, kwa sababu ukikopa katika utaratibu wa pamoja tunapata riba nafuu. Sasa muswada huu umelenga kutusaidia hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kama ninavyofahamu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni sovereign country na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, muswada huu umelenga kusaidia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iweze kukopa kwenye International Capital Markets kupitia Muungano wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishukuru kwenye muswada katika kuhakikisha tunasimamia vizuri fedha za umma kuna checks and balances. Hii Kamati ya Kitaifa ya Kusimamia Madeni ya Taifa, mapendekezo yake yanalenga kumsimamia Waziri wa Fedha asiwe na mamlaka ya peke yake kujiamlia mikopo mikubwa ambayo tunakopa katika International Capital Markets bila kuwa na chombo ambacho kitamsimamia na kumshauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la kuwa na hii The National Debt Management Committee ni mpango mzuri na utasaidia dhamira ya Serikali kuhakikisha fedha za umma zinasimamiwa ipasavyo ili Watanzania waweze kupata maendeleo ambayo tumewaahidi katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia muswada umelenga kumsaidia Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweze kuwa na msingi wa sheria wa kukasimisha madaraka kwa Gavana wa Benki Kuu kwa sababu sheria zilizokuwepo hazikuwa na kifungu ambacho kinaruhusu mamlaka ya kumkasimisha Gavana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia muswada umetoa msingi wa kisheria ambao utamruhusu Waziri wa Fedha kuweza kukasimisha madaraka kwa Gavana ili aweze kutoa dhamana za Serikali kwa mujibu wa sheria. Kabla ya hapo kulikuwa hamna kifungu ambacho kinampa madaraka hayo Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Kwa hiyo, hili ni eneo lingine ambalo linaonesha muswada huu umelenga kuboresha usimamizi wa fedha za umma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. Muswada umeweka mapendekezo mazuri, umepanua wigo ili hata wale wanafunzi ambao wapo kwenye elimu ya juu ambao wanachukua diploma waweze kupata fursa ya kupata mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika hili nipende kushauri, kwa sababu tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, uchumi wa kati (middle income country) pia tuangalie hata hizi Vocational institutions hasa taasisi kama Dar es salaam Technical Institute, Arusha Tech., hivi vyuo vya ufundi tusiviache pembeni katika mpango mzima wa kuboresha na kupanua wigo kwa ajili ya vijana wetu wanaosoma masomo ya elimu ya juu. Tuangalie hata Vocational Training Institutions kwa sababu tunalenga kuwa na uchumi wa viwanda, hivyo tukiwasaidia vijana ambao wanaenda kujifunza ufundi stadi, wakapata mikopo, tutakuwa tunawasaidia kupata ujuzi ambao watatusaidia kupunguza tatizo la ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pamoja na maboresho mazuri kwenye upande wa kuwezesha vijana ambao wanaenda kwenye vyuo vya ufundi stadi muswada haujawatendea haki vijana hawa. Nipende kuomba marekebisho haya yafanyike ili tupanue wigo vijana wengi wa Tanzania waweze kupata mikopo ya elimu ya juu zikiwepo Vocational Technical Institutions.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maboresho ya sheria pia kuna Sheria ya Kodi ya Mapato. Najua sasa hivi Tanzania Revenue Authority chini ya Wizara ya Fedha wanajitahidi sana kukusanya mapato ili tuweze kupata fedha za kuweza kutekeleza miradi ya maendeleo. Hata hivyo katika udhibiti wa utumiaji wa msamaha wa kodi Taasisi za Dini zimejikuta katika wakati mgumu sana. Nipende kuiomba Serikali si kwamba taasisi zote zilitumia vibaya misamaha ya kodi, taasisi nyingi za Dini zinatumia hii misamaha ya kodi vizuri. Sasa Serikali iweke utaratibu mzuri ili wale ambao ni waaminifu katika Taasisi za Dini waweze kupata misamaha ya kodi kwasababu misamaha hii inawasaidia Watanzania wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato pia kuwekwe utaratibu mzuri ambao utazisaidia Taasisi za Dini ziweze kuendelea kuwasaidia Watanzania walio wengi kupitia hizi taasisi, ziendelee kusaidiwa katika misamaha ya kodi ambayo ilikuwepo kipindi cha nyuma lakini ikafanyiwa marekebisho ili kudhibiti matumizi mabaya ya msamaha wa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina mengi ila nilipenda kusisitiza jinsi gani wenzetu wachache ambao wanapinga huu muswada. Sisi tumekuja hapa Bungeni kutunga sheria, kuishauri na kuisimamia Serikali. Sasa ukiangalia muswada huu una nia njema kabisa ya kusaidia Serikali ili iweze kusimamia vizuri fedha za umma, iweze kusaidia Serikali zetu mbili - Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna wengine wanasema vitu ambavyo vimelenga kupotosha. Si kwamba muswada una nia yeyote mbaya ya kuweza kukandamiza Serikali yoyote. Muswada umelenga kusaidia Serikali zetu ziweze kujipanga na kupata fedha katika nyanja mbalimbali ikiwemo kwenye International Capital Markets ili tuweze kutekeleza yale ambayo tumewaahidi Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kwa mara nyingine. Ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2019
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hii hoja. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa AG, Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Kamati kwa kuleta Muswada mzuri ambao unalenga kuboresha utendaji wa Serikali katika maeneo ambayo hoja hii ya kubadilisha sheria imegusa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni-acknowledge, kwa upande wa Kambi ya Upinzani Mheshimiwa Ally Saleh alipongeza eneo la Miswada hii la takwimu kwamba Serikali imesikia na imefanya maboresho mazuri. Kwahiyo si kwamba Serikali haijasikia kuna maeneo ambayo wamesema na Serikali imerekebisha kwa hiyo tuna-acknowledge hizo pongezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuchangia maeneo matatu. Nianze na suala la marekebisho ya Sheria ya Makampuni. Waheshimiwa Wabunge ukiangalia Sheria iliyokuwa ya zamani ilikuwa imechanganya majukumu ya kibiashara na majukumu ya NGOs. Sasa sheria hii inafanya Wizara ya Viwanda na Biashara ijikite kwenye majukumu ya kibiashara naya viwanda, lakini jukumu la NGO liende kwenye eneo ambalo litashughulikiwa vizuri na kusaidia NGO kufanya majukumu yao.

Mheshimiwa Naibu Spika,kwa hiyo jambo hili nashangaa kwa nini wale ambao wanapinga hawalielewi, sisi Wizara ya Viwanda na Biashara kazi yetu ni kusimamia Sera na Sheria na Kanuni za biashara na viwanda. Sasa mambo ya NGO kuwepo kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara ilikuwa ni kukosea tu-beginwith. Ssa sheria hii inafanya marekebisho ili NGO iende kwenye eneo ambalo tutasimamia NGOkwa mujibu wa sheria na katiba za nchi, kwahiyo hili jambo nadhani kuna watu watakuwa wamefanya lobbying kutaka kuleta sintofahamu,kwahiyo ningependa Waheshimiwa Wabunge muelewe kwamba nia ya Serikali ni njema, sisi majukumu ya viwanda na biashara ambayo mmetupa tuyasimamie na mambo ya NGO yaende mahali ambapo panahusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, ukiangalia kwa hali ilivyokuwa NGO zikiwa kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara kulikuwa kuna usumbufu sasa sheria hii inaleta ufanisi, sheria ya NGO ya kutaka NGO ziwe na compliance certificate ilikuwa ni duplication ya efforts, lakini marekebisho ya sheria yatasaidia NGO zisiwe na huu usumbufu ambao ulikuwepo wa kuandikisha BRELA, lakini sambamba na hilo kutakiwa kuwa na certificate of compliance. Kwahiyo, ningependa kuwatoa hofu NGO nchini, kaeni tayari ile miezi miwili ambayo mmepewa, baada ya Mheshimiwa Rais kusaini hii sharia, basi ndani ya miezi miwili wahakikishe wana-migrate kwenda kwenye sheria mpya na kama Serikali tulivyosema nia yetu ni kuratibu mambo ya kibiashara yawe ya kibiashara na mambo yaki-NGO yawe yaki-NGO.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia,ni bidhaa zilizopandishwa ushuru. Serikali imekuwa sikivu Waheshimiwa Wabunge ukiangalia kwenye Budget Act ya 2018/2019 na Budget Act ambayo tumeipitisha leo hii, kuna maeneo mengi ambayo tumepandisha ushuru kulinda Kampuni za ndani, lakini wajibu na haki ni two size of the same coin, tume-protect viwanda, lakini viwanda hivi lazima sasa tufike mahali tuwe na performance agreement kwamba tume-protect tumepandisha ushuru, lakini sasa wewe wajibika katika kuhakikisha unatimiza yale malengo ambayo umeahidi baada ya sisi kutoa hiyo protection.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, nitaje tu maeneo machache. Tumepandisha ushuru wa forodha wa asilimia 10 badala ya asilimia sifuri kwenye gypsum powder; kwenye mafuta ghafi ya kula ya mawese yaani crudepalm oil,kwenye mafuta ghafi ya kula ya alizeti, kwenye mafuta ya kula ya mawese, bidhaa za chuma na misumari, viberiti, viazi, fresh of chilledandother seeds na maeneo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo baada ya Bunge hili, mimi kama Waziri wa Viwanda na Biashara nitakaa na Kampuni ambazo zimejikita kwenye hizi bidhaa ambazo tumezipa protectionkwa kuongeza ushuru wa forodha ili tuangalie mpango wao wa kazi na kuhakikisha protection inakuja na responsibilityna accountability.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, ile blue print na action plan ambayo tumeileta kwenu na mmeipitisha inalenga kuleta ufanisi, hata kuhamisha NGOni kuleta ufanisi, yaani sisi Viwanda na Biashara tujikite kwenye kusaidia biashara na viwanda nchini. Utaratibu huu wa kuwa na performance agreement ya bidhaa ambazo tumezi- protect na kuhakikisha kampuni ambazo zinahusika katika haya maeneo, tunataka tujenge uchumi wa viwanda. Sambamba na hilo kampuni hizi zisilale tu kwasababu tumewapa-protection wananchi wanategemea bidhaa ambazo zitakuwa ni bora lakini za bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuki-protect bila kuhakikisha tunakuwa na performance na agreement ya hizi kampuni ambazo zinatengeneza hizi bidhaa, matokeo yake bei itapanda, halafu bidhaa itakuwa haitoshi na itakuwa kinyume na matarajio ambayo Serikali inapenda kwamba tutoe protection, lakini responsibility na accountability ziwepo kwa kampuni ambazo tunazi-protectziweze kuzalisha bidhaa ambazo zitakuwa zinatosha na ni nafuu kwa wananchi wetu.Kwa hiyo nilipenda niliweke hilo kwamba ufanisi huu ambao tunaufanya kupitia hizi sheria utatusaidia Wizara ya Viwanda na Biashara kujikita kwenye maeneo ambayo wametuelekeza kupitia blue print tuweze kuyatekeleza

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ambalo limechangiwa kuhusu BRELA ni changamoto za urasimu, lakini pale BRELA tayari tuna infrastructure ya wananchi ku-registeron line, lakini kuna technicalities ambazo tutahakikisha tunazirekebisha ili mwananchi popote anapokuwa aweze ku-registeronline na tayari tumeruhusu ukishakuwa na kitambulisho cha NIDA unaweza ukafanya registration bila kuwa na kadi. Hizo ni moja ya hatua ambazo tumezifanya ili kuhakikisha kupitia BRELA tunakuwa tunamfumo ambao uko onlinena wananchi wanaweza wakatumia onlineregistration kusajili kampuni mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunapanga kuwa nabusiness clinics ili kuwafuata wananchi kwenye mikoa kuondoa usumbufu wa kuja kwenye Makao Makuu ya BRELA kwa ajili ya kufanya registration.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, nampongeza Mheshimiwa AG, Waziri wa Katiba na Wabunge kwa kuunga mkono hii hoja ya marekebisho ya sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hojana nashukuru sana. (Makofi)