Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Assa Nelson Makanika (8 total)

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na niipongeze Serikali kwa hatua ambazo imezichukua juu ya zao hili la michikichi, lakini vile vile nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameonesha jitihada za kipekee sana katika kusaidia zao hili la mchikichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upungufu wa mafuta katika nchi yetu, niipongeze Serikali tu kwamba ni kweli imewekeza jitihada kwenye kuzalisha mbegu lakini napenda kujua Serikali imejiandaaje katika kuokoa mafuta yanayopotea kwenye Mkoa wetu Kigoma katika kuwekeza kwenye teknolojia? Kwa sababu kuna mafuta mengi sana yanapotea, hata hii miche iliyopo inapoteza mafuta mengi sana kabla ya kuwekeza kwenye miche mipya hii ambayo ameisema Naibu Waziri. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Makanika, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Serikali tumeanza maongezi na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, TIRDO na SIDO kwa ajili ya kuja na teknolojia rahisi. Kwa sababu tume-invest katika miche baada ya miaka mitatu itaanza kutoa matokeo. Sasa itakapotoa matokeo tunakuja na mfumo wa ku-develop teknolojia ndogondogo ambazo katika household level, wananchi wataanza kukamua mafuta na kuyafanya kuwa crude ili yaweze kuzalishwa na kupunguza upotevu unaoongelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge amerudia jambo hili mara ya pili, katika Kamati vilevile ali- raise concern hii, nataka nimhakikishie kwamba tunajadiliana na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara ili kuja na teknolojia ya kupunguza hasara na upotevu.

Vilevile kuja na teknolojia rahisi ya ku-process mafuta katika primary level, katika level ya crude, pale ambapo miche hii itakuwa ime-mature na kuwafanya wakulima badala ya kuuza matunda wauze mafuta crude kwa processor wa secondary level.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa umuhimu wa reli hii ya kutokea Tunduma kwenda Kasanga unafanana kabisa na umuhimu wa barabara inayoanzia Mwandiga na kuelekea Chankere na inayopita nyuma ya Hifadhi ya Gombe na mpaka kwenda kwenye Bandari ya Kagunga. Je, Serikali haioni kuna umuhimu sana wa kuikamilisha barabara hii haraka iwezekanavyo kwa sababu, barabara hii ni barabara kwanza ya kiuchumi, lakini barabara hii pia ni barabara ya kiulinzi kwa sababu, ukanda huu hatuwezi kuwafikia wananchi wetu pasipo kupita nchi jirani ya Burundi. Je, Serikali haiwezi kututoa kwenye utumwa huu wa kupitia nchi jirani kwenda kuwahudumia watu wetu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa barabara maana anayoongelea ni Barabara ya Mwandiga – Chankere hadi Kagunga. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kusanifu barabara hiyo kwa sababu, barabara hiyo bado haijafunguliwa na tunajua kwamba, ni barabara muhimu sana kwenda Bandari ya Kasanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hiyo kuwahudumia wananchi wa Kagunga. Mheshimiwa Makanika amekuwa anafuatilia sana hii barabara, nimhakikishie kwamba, Serikali inalifahamu na nadhani pia, ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, hii barabara iweze kufunguliwa. Kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha kuona kwamba, barabara hii inafunguliwa. Ahsante.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa changamoto ambazo zinakabili zao hili la kahawa katika Jimbo la Hai zinafanana pia changamoto ambazo zinakabili wakuliwa katika Jimbo letu la Kigoma Kaskazini. Ukiangalia moja wapo ya changamoto ni soko na mkulima kuwa na uhuru wa zao hili kahawa kuuza anapotaka. Vyama hivi vya Ushirika vinawafunga wakuliwa wetu, hawawezi kuuza kahawa zao endapo mnunuzi huru atafika katika maeneo husika. Je Serikali inaweza kutupa tamko leo juu ya hilo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni vizuri Waheshimiwa Wabunge tukaelewa kwamba kuna miss conception juu dhana ya ushirika. Ushirika haumzuii mnunuzi binafsi kwenda kununua zao la mkulima. Ushirika ni mfumo wa wakulima wanaokusanya zao lao pamoja na wakulima wale wanauza kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, experience imeonesha kwamba pale ambapo kunakuwa hakuna mfumo wa ushirika hasa katika mazao haya kama kahawa, pamba, korosho na mazao mengine yote wakulima wamekuwa wakiuza zao lao bei ndogo sana. Kesi iliyoko Kigoma Kaskazini na Mheshimiwa Mbunge tumeongea naye mimi zaidi ya moja mara mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema kama kuna mnunuzi binafsi anataka kununua zao la mkulima hasa kahawa, hasa Kigoma Kaskazini na wewe mwenyewe nimekwisha kwambia mlete tutamruhusu atakwenda kununua kwenye Chama cha Msingi atuambie bei anayonunulia ni shilingi ngapi na volume anayotaka kununua ni kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka transparent kwenye mfumo huu, hatulazimishi kwenda kwenye Chama Kikuu cha Ushirika. Tunamruhusu kwenda kwenye Chama cha Msingi na yoyote anayetaka aje hata jana nimekaa na wanunuzi wanaotaka kununua kwenye Vyama vya Msingi kwenye Wilaya ya Karagwe, Wilaya ya Kyerwa sasa hivi wanasaini makubaliano na Vyama vya Msingi ili waweze kununua kwa bei inayofanana na soko tusipofanya hivyo tutarudisha mifumo isiyokuwa rasmi na wakulima watanyonywa sana. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nashukuru kwanza kwa majibu ya Serikali juu ya zao letu hili la mchikichi ambalo linazaa mafuta ya mawese. Kwa kweli mchikichi ni zao la kipekee sana Kitaifa na Kimataifa, na sisi pia tunategemea tukiona zao hili likiweza kuwanufaisha wananchi wa Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 19 Desemba, 2020 Mheshimiwa Waziri Mkuu alikaa na wadau wa zao hili pale Kigoma ndani ya Ukumbi wa NSSF. Mojawapo ya mambo watu hawa waliomwambia wanahitaji kuona yakifanyiwa kazi ni Bodi ya Mawese na vifungashio maalum.

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Makanika.

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua sasa ni nini mkakati wa Serikali ulipofikia katika kutekeleza mambo haya ambayo walimwomba Waziri Mkuu yafanyiwe kazi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Assa Nelson Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, moja ya mikakati ambayo tunatekeleza ni kuanza sasa kutatua changamoto hizo, lakini zaidi tumeshaunda timu ya wataalam baada ya maelekezo ya Waziri Mkuu, wakati huo tumeshaunda timu ya wataalam kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara na Kilimo ambao sasa wataandaa guidelines kwa ajili ya vifungashio kwenye mazao haya ya kilimo na bidhaa zake, mazao yote ikiwemo ya mawese.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili la bodi, nadhani hili tunalichukua kama moja ya vitu vya kufanyia kazi kama Serikali ili tuweze kuona kama kuwepo kwa Bodi ya Michikichi ni moja ya suluhisho, basi nalo tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Matatizo yaliyoko katika Jimbo la Mwibara na maeneo mengine ya Tanzania, yanafanana kabisa na matatizo yanayopatikana katika Jimbo la Kigoma Kaskazini. Ndani ya Jimbo la Kigoma Kaskazini tuna mradi wa Mkongoro I, ambao umechukua muda mrefu na huu mradi unakwamisha adhima ya Mheshimiwa Rais ya kumtua ndoo mama kichwani.

Naomba kujua ni lini huu mradi utaukamilisha ili tuweze kuwasaidia mama zetu katika Jimbo la Kigoma Kaskazini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge na nimeshafika katika Jimbo lake kiukweli unafanya kazi kubwa, unafanya kazi nzuri kama kijana. Sisi kama Wizara ya Maji tutaendelea kukupa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wizara yetu ya Maji tumesema miradi ambayo imetumia kwa muda mrefu mkakati wetu ni kuhakikisha tunaikamilisha. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge saa 7.00 tukutane tuone namna gani ya ku-push mradi ule ili tuweze kuukamilisha. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha wa hali ya umeme ya Igunga, Julai 19, Mheshimiwa Waziri akiwa Biharamulo alieleza kwamba mnamo mwezi Septemba umeme wa gridi ya Taifa utakuwa umefika Kigoma. Sasa tupo mwezi Septemba, tunataka kujua hali ya umeme wa gridi ya Taifa: Je, umeshawasili Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Assa Makanika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, umeme wa gridi utafika Mkoani Kigoma mwezi huu Septemba kwa sababu ipo njia ya msongo kV 33 ambayo inakamilishwa mwishoni mwa mwezi huu inayotokea Nyakanazi kupita Kakonko – Kibondo Kwenda mpaka Kasulu. Kwa hiyo, umeme wa gridi kwa kuanzia utaingia mwezi Septemba katika Mkoa wetu wa Kigoma.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tuna Kituo cha Polisi katika Wilaya yetu ya Kigoma DC, Kituo cha Polisi cha Mkuti, ukiangalia matukio mengi sana ya kihalifu yanafanyika katika eneo lile.

Je, ni lini Serikali itaweza kumalizia Kituo kile cha Polisi katika hali iliyopo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Makanika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nipo tayari kufuatana na Mheshimiwa Makanika baada ya Bunge hili ili kuona mahitaji ya kituo hicho kwa maana ya kufanya tathmini, kuona fedha zinazohitajika ziweze kutengwa katika bajeti zetu zinazofuata. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; kumekuwa na malalamiko kwa wananchi kadha wa kadha ambayo bado wanaonesha namna gani ambavyo hawakupata stahiki hizo.

Ninaomba kujua ni lini Mheshimiwa Waziri utatenga muda ukawasikilize wananchi wale ili uweze kupata ufumbuzi wa malalamiko hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Assa Nelson Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nipo tayari kwenda kuwasikiliza wananchi, lakini pia nitaomba tukubaliane naye mara baada ya Bunge hili muda sahihi na maeneo ambayo atataka Mheshimiwa Mbunge twende tukawasilize wananchi hawa ili tuweze kutatua hii changamoto ya fidia ambayo ni ya muda mrefu sana. Ahsante.