Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Assa Nelson Makanika (9 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema ambaye kwa kweli amemwezesha kila mmoja wetu kufika mahali hapa. Jambo la pili, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais pamoja naChama changu Cha Mapinduzi ambacho kwa kweli kimeweka imani kubwa kwa sisi vijana, kimetuamini katika umri huu, ni jambo kwa kweli kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais na Chama chetu Cha Mapinduzi. Kwa kweli ni jambo ambalo mimi katika umri huu nisiposhukuru tena mara ya pili nitakuwa sijamfanyia haki Mheshimiwa Rais kwa kusema ahsante sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hotuba zake mbili ambazo alizitoa Mheshimiwa Rais nitajikita kuchangia sanasana katika hotuba yake aliyeitoa Novemba 13 mwaka 2020. Kumekuwa na jambo ambalo ningependa nizungumzie katika hotuba ya Rais na jambo lenyewe ni juu ya kilimo. Jambo la mafuta ya kula limekuwa nicross cutting issue na imekuwa ni current matter ambayo kwa kweli inaendelea kujitokeza mwaka hadi mwaka na mimi leo nitakuwa na mchango kidogo juu ya suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa mafuta ya kula hapa nchini naomba iwe ni ishara ya Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi na chini ya Jemedari Dkt. John Pombe Magufuli kuwa ni ishara ya kutuonyesha kwamba tunahitajika kufunga kamba ndani ya viuno vyetu ili tuweze kufikia azma ya viwanda kikamilifu. Kwa takwimu tu haraka haraka nchi yetu inaonyesha kabisa kwamba inazalisha tani laki mbili za mafuta ya kula, lakini mahitaji yetu ni tani laki tano kwa mwaka, hivyo tunakuwa na upungufu wa tani laki tatu ambazo nchi yetu inaagiza tena hasa katika nchi za bara la Asia san asana Malaysia na nchi ya Indonesia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa tafsiri hiyo inaonyesha kabisa kwamba tunachukua pesa nyingi za kigeni kwa ajili ya kuagiza bidhaa hii ya mafuta ambayo nikisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 15, naona hii ni aibu kubwa kwa nchi kama Tanzania ambayo ina ardhi yenye rutuba kuagiza mafuta nje. Kwa hali halisi ilivyo nakulingana na matamko mengi ambayo Serikali imekuwa ikitoa, naomba nijielekeze kuionesha Serikali kwamba kuna wajibu mkubwa wa kuelekeza katika zao hili la mbegu ambapo mafuta yanatokana na mbegu hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, mwezi Mei, 2017 aliyekuwa Waziri wa viwanda wakati huo Mheshimiwa Mzee wangu Mwijage alinukuliwa akisema: “Takribani asilimia 70 ya mafuta ya kula yanayohitajika kutumiwa hapa nchini huagizwa kutoka nje ya nchi, maana mafuta yanayozalishwa na viwanda vyetu hayatoshelezi kabisa.”

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo, tarehe 4 Septemba2018bado kauli hii imeonyesha kabisa kwamba bado hatujajitosheleza katika kuzalisha mafuta ambayo yanatosha kutumiwa na watu wetu. Hivyo Mheshimiwa Waziri Mkuu alinukuliwa naye pia akisema kauli ambayo inafanana nahiyo nami nitamnukuu kwa kifupi sana, anasema: “Hivi sasa nchi yetu inatumia takribani dola za kimarekani milioni mia mbili tisini na nne kila mwaka kuagiza mafuta nje ya nchi.”

Mheshimiwa Naibu Spika, tafsiri ya hali hii inaonyesha kwamba pamoja na kuwa na janga la corona ambalo limeikumba dunia na limelikukumba dunia na limezikumba baadhi ya nchi bado inaonyesha changamoto hii imekuwa ikijirudia mwaka hadi mwaka, nini kifanyike na ushauri ambao naona nishauri Serikali yangu. Naona kwamba ni vema zaidi ikajielekeza kwenye kilimo cha mazao ya mbegu, kama karanga, zao la chikichi ambalo kwa kweli nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa akionesha jitihada kubwa, amefika Kigoma katika kulishughulikia zao hili la chikichi. Itoshe tu kusema kwamba zao hili la chikichi linaonesha katika takwimu za kidunia kwamba ndilo ambalo limeziwezesha nchi zingine kamaNchi za Malaysia kuweza ku– supplykwetu mafuta haya ya kula na hata kusambaza duniani kote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna faida kadhaa tukijielekeza katika kilimo cha mazao yanayotokana na mbegu. Faida ya kwanza ni jambo la uhakika ambalo soko letu la ndani tutaweza kulihudumia kwa kujitosheleza na hatimaye tutaepuka kuagiza mafuta haya ya mchikichi. La zaidi sana, itakuwa ni ishara tosha ya kwenda kutekeleza ndoto madhubuti ambayo ya kutibu aliyonayo Mheshimiwa Rais ya kuweza kuzalisha ajira milioni nane alizozisema katika Ilani ya Uchaguzi kwenye ukurasa wa tano.

Vile vile tukifanya hivyo kuwekeza katika mazao haya, itakuwa ni ishara tosha kabisa kwamba tutaifanya nchi yetu kuweza ku-export zaidi mafuta na hatimaye kutoka kwenye kundi lakuwa importation country na hiyo hiyo itatuwezesha hata kuimarisha shilingi yetu na hali ya shilingi yetu itakuwa imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie kauli ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika hotuba yake ya Novemba 13, amesema kabisa: “Kwa haya machache ninaona ni vyema zaidi Wizara husika ikachukua hatua madhubuti na kujielekeza katika mazao haya ya mbegu ili tuweze kuepukana na changamoto hii ya mafuta ambayo inajitokeza mwaka hadi mwaka”. Kwa nchi nilizozitaja kama Malaysia na Indonesia lakini nchi kama Malaysia walichukua mbegu kwetu Kigoma katika Kata ya Simbo na wakapeleka kwao kwa ajili ya kuzalisha mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona kengele imelia, nilikuwa na mengi ya kuchangia ila mchango wangu nitauleta kwa maandishi ili Serikali waweze kuona mawazo yangu juu ya hotuba ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana Wizara hii ambayo hakika ni Wizara yenye kuchochea uchumi kwa Taifa lolote lile ambalo lina mpango wa kujiendeleza. Awali ya yote kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pili nimshukuru Mheshimiwa Rais, nimshukuru na Mheshimiwa Waziri kwa jitihada kubwa sana anazozifanya na ndipo niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa umejikita katika maeneo matatu; eneo la kwanza ni miundombinu yenyewe kwa ujumla wake ambao imebeba bandari, miundombinu ya barabara, reli na hatimaye usafiri wa anga. Hivi leo tunajadili Wizara hii na Mheshimiwa Waziri unisikilize vizuri. Wizara yako ndio iliyotufikisha mahali hapa tulipo na kama Wizara yako ingeweza kutazama na kuwa na fungamanisho na Wizara zingine hivi sasa uchumi wetu ungekuwa umekwisha ku-take off kutoka hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni kweli Kigoma na tunaishukuru Wizara yako Mheshimiwa Waziri, Kigoma kwa upande wa barabara tunachokiomba kwenye Wizara yako, ni kutia mkazo na kuharakisha barabara hizi za kuunganisha Mkoa wa Kigoma ziweze kukamilika kwa wakati. Lakini tuna barabara ambayo ni changamoto sana, barabara hii nimekufikisha barabara ya kuanzia Mwandiga inakwenda mpaka Kata ya Kagunga. Barabara hii inapita katika kata tatu ambazo kata hizo zinajumuisha wananchi karibu 70,000 Kata ya Kagunga, Kata ya Ziwani na Kata ya Mwangongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umesikia watu wanaomba barabara kwamba iwekewe lami, pale hatuombi barabara kwamba iwekewe lami tu, ni kwamba hakuna barabara kabisa. Hivi sasa sijui unaweza ukawaambia nini wananchi wa kata hizo, wananchi wa kata hizo wanakwenda kupata matibabu nchi jirani ya Burundi, wananchi wa kata hizo wanakwenda kutafuta huduma zote ambazo ni stahiki katika nchi jirani ya Burundi. Lakini wananchi hao wanatoa kodi katika nchi yetu ya Tanzania, kesh/kesho kutwa utawaambia nini kwamba waone fahari ya wewe kukupa kodi ikiwa kodi wanakupa wewe lakini miundombinu kama hii ya msingi wewe hauwapatii? Upande wa Burundi wameweka mpaka lami, wakitaka kufika sehemu ya Tanzania wanapita nchi ya Burundi ndipo waweze kuingia Tanzania, kwa hili tunahatarisha hali ya usalama wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni ya kiusalama huko tuna Kambi ya Jeshi ukienda Kagunga, lakini hata ukiachilia usalama barabara hii ni barabara ya kiuchumi. Huko tuna Hifadhi ya Gombe, mtalii kufika Gombe ni lazima apite njia ya maji, asipopita njia ya maji hawezi kufika Gombe. Kwa nini tusipeleke miundombinu hii ili iweze kuchochea uchumi wa kitalii? Mheshimiwa Waziri litazame hilo sana ili uweze kuwasaidia wananchi wa Kigoma Kaskazini kwa kata hizo tatu. Lakini kutoka bajeti iliyopita mpaka hii ya sasa tumepoteza zaidi ya wananchi 102 mpaka dakika ya sasa kwa sababu ya kukosekana barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamama wajawazito wanahitaji kujifungua ili wafike Maweni, Kigoma Mjini wanapita njia ya maji wengi wanafia ziwani. Mheshimiwa Waziri uweze kutazama hivi vifo mimi ninaamini Wizara yako haiungi mkono tuweze kupoteza Watanzania wenzetu. Uweze kukaa chini, utazame, ufikirie na hawa ni Watanzania wenzetu, uweze kuokoa maisha yao na wao ili waweze kuona fahari hata hata hao wanaobaki ya kwamba waache kupoteza mama zetu ambao wanaiaga dunia kila kukicha. Natambua ya kwamba kumekuwa na jitihada nyingi sana kuhusu hii barabara naomba sana Mheshimiwa Waziri uweze kuongeza nguvu sana ili hii barabara iweze kutoboka haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni jambo la bandari; bandari ni mojawapo ya kitu ambacho kinaingiza mapato katika nchi hii, lakini katika nchi hii tuna bandari mjumuisho, bandari ambazo zimerasimishwa na ambazo zisizo rasmi zaidi ya 600 na kitu. Lakini ndani ya hizo bandari 600 na kitu bandari mbili tu katika nchi nzima ndizo zinazojiongoza kwa faida. Moja ni bandari ya Dar es Salaam; mbili ni bandari ya Kigoma, bandari zingine zote ambazo mnapeleka miundombinu zinajiongoza kwa hasara. Leo hii shilingi 100 inayozalishwa katika bandari ya Dar es Salaam na shilingi 100 inayozalishwa katika bandari ya Kigoma inaweza ikatumika shilingi 80, shilingi 20 ikaenda kwenye Mfuko wa Hazina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini shilingi 100 inayopatikana katika bandari ya Mwanza inatumika yote na tunakopa shilingi 20 tunakwenda kuwalipa wafanyakazi katika bandari zingine. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumueleza mchangiaji kwamba Mwanza kwa sababu ya kukosa miundombinu ya treni ndio imeonekana haizalishi bandari yake, lakini bandari ya Mwanza ni bandari ya pili kwa ukubwa na ni bandari ya pili kwa uchumi katika nchi hii, asilete hadithi. Ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Assa unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siipokei, nina data kamili hapa ninaweza nikamsaidia kaka yangu hapa aweze kuelewa nina chanzo cha hali ya uchumi wa Taifa mwaka 2020, kimetoa hii takwimu, nitakupa nikusaidie tu kidogo maarifa madogo haya, ya kwamba nchi ya DRC Congo ndio soko ambalo tunaelekea mpaka dakika ya sasa. Asilimia 34 ya mizigo ambayo inaingia katika bandari ya Dar es Salaam inaelekea Congo na ikieelekea Congo maana yake ni Kigoma njia pekee. Asilimia 23 ya mizigo ambayo inapitia bandari ya Dar es Salaam inaelekea Rwanda, asilimia tisa inakwenda Zambia jumla ya asilimia 63 ya mizigo yote inayoingia nchini inaelekea ukanda wa Kigoma haiwezekani Mwanza ikawa ndio bandari ambayo inaingiza uchumi mkubwa, hiyo haiwezekani hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na mchango wangu na itoshe tu kukuambia ya kwamba hali ya takwimu hizi zinazoonesha, hali ya uchumi wenyewe inatuambia miaka mitatu mfuatano inaonesha hali ya uchumi ya kwamba bandari ya Kigoma na ya Dar es Salaam ndizo zinajiongoza kwa faida na sio bandari nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natarajia kwamba Wizara iweze kutazama mambo haya nadhani jambo ambalo linakosa katika uchumi wetu ni linkage pekee, uchumi wetu hauna linkage leo hii tunaweza tukaona the growing market ya bandari ambayo inaelekea mpaka sasa ni Congo, lakini sisi tunaweza tukatoa reli tukapeleka kwingine wakati tunaliacha soko linakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Congo imeingia sasa hivi East Africa, Congo sasa hivi imeingia kwenye soko la East Africa, imekuja kuwa sehemu ya Jumuiya tumejipangaje kuliteka hili soko la Congo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuliteka soko hili ukiitenga Kigoma unaumiza Taifa, ukiitenga Kigoma katika kuteka soko hili unaliumiza Taifa zima, hauiumizi Kigoma pekee. Hivyo mimi ninashangaa reli mpaka dakika ya sasa mara tu baada ya Congo kusema kwamba anaingia kwenye Jumuiya hii tungeelekeza nguvu kubwa kuelekea Kigoma ili tuweze ku-save hii mizigo, asilimia 63 ya mizigo yote tunayotoa na kuingiza inapita hapa. Kwa nini tusielekeze Congo ili tuweze kuteka huu uchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika hivyo hivyo nashangaa sana hata meli, hakuna hata meli moja mpaka sasa hivi ambayo ina-operate katika Lake Tanganyika haipo. Leo hii Kigoma haina hata meli moja, MV Liemba chali haifanyi kazi, Mwongozo chali haifanyi kazi, mnataka uchumi gani wa Congo muuteke? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa tu nilizonazo ambazo ni za uhakika hata meli ambayo imejengwa ya Mwanza haifai na wanasema hakuna bandari ya kuweza kuipokea ile meli ni kubwa, unaelekeza kule kwa nini tusielekee Kigoma. Hii sio kwamba nachukia sehemu zingine, ninajaribu kuonesha ya kwamba soko pekee tupende tusipende kama tunahitaji mapato mengi sharti tuelekee Kigoma. Hivi sasa juzi Mheshimiwa Bashe ametuambia kwamba anakwenda kusaidia hii crisis ya mafuta, I can tell you two years or three years we are going to fail, crisis ya mafuta itarejea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani kote nina mifano ya kutosha na Kigoma msichukulie hata mchikichi, nilitaka nimuambie Mheshimiwa Bashe mchikichi sio long plan ya kufanya sasa hivi, kwa sababu michikichi inalimwa Kigoma miaka na miaka pelekeni teknolojia kuna mafuta mengi yanapotea kule Kigoma. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Assa, muda wako umemalizika.

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nitachangia kwenye Wizara zingine mbele. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Mpango huu wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na kuipongeza sana Wizara kwa kuleta Mpango huu. Nitajikita katika vipaumbele vitano vya mpango huu na nitajikita kwenye kipaumbele namba tatu ambacho kinasema, kukuza biashara na kipengele namba nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nijielekeze kushauri mambo kadhaa kwa ajili ya Mpango huu ambao umekuja mbele yetu. Kwanza, nitazungumzia mpaka wetu wa Kongo na Kigoma. Mpaka huu kihistoria unaonyesha kwamba umekuwa na mchango mkubwa wa kukuza uchumi katika Mkoa wetu wa Kigoma na hata kwa Taifa letu la Tanzania. Hivi karibuni hali ya kibiashara Mkoani Kigoma imedorora na imekuwa ni ya chini sana kwa sababu mpaka ule umekuwa hauthaminiwi. Hii ni kutokana na sera za kiuchumi ambazo kwa kweli Serikali ikizifanyia kazi tunaweza tukatoka mahali hapa tulipo na kuelekea sehemu ambayo tunataka twende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisoma historia ya mpaka ule wa Kongo na Tanzania inaonesha kabisa mwaka 1986 mpaka 1993 kulitokea Mkuu wa Mkoa wa pale kwetu Kigoma, Mkuu wa Mkoa wa kumi kama sijakosea, alikuwa akiitwa Christian Mzindakaya. Mzindakaya alifanya mambo makubwa sana katika uongozi wake ambayo yaliweza kuitoa Kigoma mahali ambapo katika hali ya uchumi ilikuwa ni kwenye shimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye alifanya vitu vichache tu; alichokifanya ni kurekebisha baadhi ya sera za kiuchumi, mfano visa fee ya wa Kongo kuja pale Kigoma aliweza kuishusha, lakini akaondoa na usumbufu wa wageni ambao umekuwepo hivi sasa na unashusha uchumi katika mkoa wetu wa Kigoma. Hivi sasa Mkongo akitoka Kongo kuja Kigoma anasumbuliwa na taasisi nyingi, akiingia tu kidogo TRA atakuwa nyuma, akikaa kidogo hata Polisi atamfuata kwenye hotel. Jambo hilo limekuwa likiwachukiza na hatimaye linaweza kushusha uchumi wetu. Naishauri Serikali kwamba kwa kutumia tu mpaka wa Kongo tunaweza tukapata mapato makubwa sana na tukaweza kusaidia hali ya uchumi katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nizungumzie zao la kahawa. Zao la kahawa linaweweseka sana na nimeweza kushauri hata hapo nyuma nimekaa na Naibu Waziri Kilimo nikamweleza, zao la kahawa linadorora kutokana na vyama vya ushirika tulivyonavyo. Vyama vingi vya ushirika mpaka dakika hii havijawalipa wakulima pesa zao na hawa wakulima wamewakopesha toka mwaka jana na wengine mpaka dakika hii wanawadai. Mfano pale jimboni kwangu kuna Chama cha Kalinzi Mkongoro kina wanachama 273 bado kinadai pesa zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hali inasababisha zao hili la kahawa na tena kahawa inayotoka Kigoma imeonesha inapendwa duniani kote. Kwa namna hii ambavyo tunalimbikiza madeni ya wakulima kwa kweli inashusha hali ya zao hili la kahawa na kusababisha kukosa mapato mengi kwa sababu zao la kahawa ni la tatu kwa kuingiza fedha kigeni hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na muda pia nigusie kipengele cha elimu. Ni kweli tunaandaa vijana wetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia Wizara hii muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuchangia sehemu moja katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani, suala la uraia. Wizara hii ni Wizara muhimu sana katika ujenzi wa uchumi wa nchi yetu, na ni Wizara ambayo hakika ikilegalega kidogo tu inaweza ikatikisa misingi ya uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ina-deal na mambo ya home affairs. Na ukiweza kuangalia raia yeyote yule katika nchi yoyote ili, ili aweze kujenga uchumi wa nchi hiyo, lazima aji-feel proud ya nchi husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwezi Januari, tarehe 26, vyombo vya ulinzi na usalama viliendesha operesheni moja pale maeneo ya Mabwepande. Katika operesheni ile kweli inawezekana kukawa kuna moja wapo ya watu ambao ni wahalifu na watu ambao siyo raia wa nchi yetu ambao wanaweza kuwa waliingia katika nchi yetu kimakosa.

Mheshimiwa Spika, lakini katika operesheni ile namna ilivyoendeshwa, hususan kwa watu wetu wa Kigoma, kwa kweli haikuwa inatuonesha pride kusikia kama na sisi ni sehemu ya nchi hii. Kulikuwa kuna maswali mengi ambayo yalikuwa yakiulizwa, nikiwa mmoja wapo wa mashuhuda. Wananchi wa Mkoa wa Kigoma kutoka sehemu mbalimbali walinipigia simu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilifika pale Dar es Salaam, Oysterbay, nilivyofika pale moja wapo ya maswali yaliyokuwa yakiulizwa yalikuwa yanatwezwa na kuonesha kwamba watu fulani wana haki kamili ya kuwa raia wa nchi hii na wengine ni Daraja B. Jambo ambalo siyo jema katika kujenga uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana – Mheshimiwa Waziri nilikupigia simu na tukazungumza sana, asilimia 80 ya watu waliokamatwa katika operesheni ile walikuwa ni watu wa Kigoma, na sana maswali waliyokuwa wakiulizwa wanatwezwa utu wao, maana utaambiwa sema namba nne, sema namba tano, kana kwamba ni vitu ambavyo mtu anaji-feel inferior sana.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali yangu, niiombe Serikali Sikivu iweze kuangalia historia ya ujirani mwema na nchi hizi husika haiwezi ikaondoa uraia wa watu wa Kigoma. Sisi tumekuwa ni majirani na nchi hizo. Ni vyema zaidi Serikali iangalie approach nyingine ya kuweza kutu-treat sisi watu wa Kigoma ili tuji-feel tuna hatimiliki ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe kitu kimoja, kwa kupitisha tu kidogo katika historia ambayo tunayo na muunganiko wa nchi jirani; sisi tuna historia ambayo inatusema kana kwamba tumekuwa hata katika historia ya kiuongozi. Ukiangalia mwaka 1888 Mjerumani amekuja kutawala hapa kwetu, sisi Kigoma ilikuwa ndiyo makao makuu yake akitawala Rwanda na Burundi, lakini makao makuu ikiwa ni Kigoma. Sasa ukisema historia ituhukumu sisi mtakuwa mnatuonea. Hayo ni masuala ya Mwenyezi Mungu, niombe na sisi tuweze kumiliki haki sawa katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tuna historia ambayo haiwezi kufutika, mfano vijiji vyetu vingi vinafanana. Ukiangalia pale kwetu Kigoma tuna Kijiji kinaitwa Kalinzi, lakini ukienda hata Ngara kuna Kijiji kinaitwa Inkarinzi; ukienda hata Burundi, kuna Kijiji pia kinaitwa Karinzi. Hiyo naonesha ni namna gani historia yetu inavyofanana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hapohapo kwetu Kigoma, mojawapo tuna Vijiji vinaitwa Mnanira, hata ukienda Burundi pia kipo Kijiji cha Mnanira; ukienda Rwanda kipo Kijiji cha Mnanira. Sasa historia hii isije ikawa ni mhukumu kwetu. Hivyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri aweze kuangalia hii Idara ya Uhamiaji iweze kuangalia namna ya kutu-treat sisi watu wa Kigoma ili na sisi tuji-feel kwamba ni sehemu ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nitoe ushauri mdogo sana; ukija ukaangalia suala hili la uraia linaua sana na kudororesha hali ya uchumi katika Mkoa wetu wa Kigoma. Nilikuwa nikiongea na Rafiki yangu mmoja, yeye ni mtu wa Ubelgiji, na nimesoma naye, lakini akawa anashangaa sana, anasema Ubelgiji imejengwa na mali inayotoka katika nchi Jirani ya watu wa Kigoma, Nchi ya Kongo, lakini sisi hiyo mali inapita katika anga la watu wa Kigoma, lakini kulingana na changamoto ya uraia katika Mkoa wetu wa Kigoma…

SPIKA: Mheshimiwa Makanika, kengele imeshalia.

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, lakini niseme tu ya kwamba Serikali iangalie suala hilo kwa umakini, nitaweka mchango wangu kwa njia ya maandishi kumalizia hili. Ahsante.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kufunga dimba la leo. kKabla ya yote nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameweza kutupa salamu za pongezi kwa ushindi tulioupata wa kishindo kwa majimbo mawili ya Mkoani Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunajadili Wizara hii ya Ujenzi ambayo ni Wizara muhimu sana katika nchi yetu ya Tanzania na Wizara hii inamgusa kila Mtanzania na inagusa maisha ya kila masikini wa nchi hii. Miundombinu ndio uti wa mgongo wa nchi hii na ni moyo hasa, kulingana na rejea ya hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Rais wa nchi hii tarehe 22 Aprili, 2021. Lakini ukiangalia bado kuna changamoto nyingi sana, na changamoto hizi zinazopatikana kutokana na Wizara hii, kwa kweli zinaonyesha kabisa kwenye hali ya uchumi wa nchi hii bado kuna shida kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi wa kwanza tarehe 8 Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje bwana Wang’ alitembelea nchi yetu ya Tanzania. Alizungumza kauli moja sana na kauli ile Wachina wengi sana wanaipenda na waliitumia kipindi wako kwenye taratibu za kukomboa nchi yao kiuchumi. Alisema ukitaka kumkomboa mtu mnyonge wa nchi yoyote ile mpelekee muundombinu kwa sababu, mkulima yeyote akilima anataka aweze ku-exchange mazao yake na pesa. Anaweza kufanyaje hivyo ni lazima awe na muundombinu wa kupeleka zao lile alilolima sokoni, atawezaje kama muundombinu hauridhishi au haumfikishi sokoni? Matokeo yake muundombinu ukiwa uko hohehahe hawezi kutoka kwenye hali aliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, niiombe Wizara hii iweze kuweka mpango wake madhubuti. Ukiangalia mfumo wa kibajeti tulionao, ni tofauti kidogo na mifumo ya nchi zingine kama nchi za Marekani. Nchi za Marekani wanatumia federal reserve lakini sisi tunatumia basket fund, ambapo


masikini wa Kigoma analima shamba lake anatoa kodi ambayo kodi hiyo isiporudi kumpelekea muundombinu, inakwenda kujenga muundombinu wa mkoa mwingine. Na hii inatokea endapo tunakuwa hatujaweka mgawanyo sawa wa rasilimali hii ambayo ndio keki ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa Wizara kwa kupitia mfumo huu wa kibajeti tulionao, iweze kuangalia namna ambavyo inagawanya haka ka keki kadogo. Kwa sababu inaweza ikachukua pesa kutoka sehemu nyingine ikaenda kuwahudumia watu wengine. Huenda hata hayo ma-fly over tunayoyasema huenda na kodi pia ya mtu wa Kigoma amejenga yeye kila siku anapitia kwenye matope haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu wa kijijini ameenda kujenga miji yeye bado yuko kwenye hali ya chini, na hii inatokana kulingana na mgawanyo mdogo ambao hauna usawa hata kidogo haumrudii mtu wa kijijini katika kujiletea maendeleo. Nitoe mfano mdogo tu, huku Kigoma kwetu mpaka dakika ya sasa mkoa wetu mnafahamu bado haujaunganishwa na mikoa mingine kwa lami. Sehemu kubwa sana ukiangalia njia ya Kaliua hii mpaka kuja Tabora bado kuna zaidi ya kilometa 90 na kitu hazijaunganishwa kwa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija njia hii ya Kasulu bado haijaunganishwa kwa lami. Pamoja na kwamba tunashukuru ndio mkandarasi yupo, tuombe sana Serikali iendelee kuongeza nguvu sana, ili na mkoa wetu na mikoa jirani hii iweze kuunganishwa kwa lami. Lakini, imekuwa ni jambo la kusikitisha sana juzi nimesikitika sana, Mbunge wa Kakonko anaomba kilometa 3 za lami ndani ya mji tena ndio mjini. Lakini wapo Wabunge ambao wanaomba zaidi ya kilometa 15 tena pembezoni mwa mji, hii sio sawa na Wizara isikie. Hiki tunachokifanya ni kitu ambacho tunafanya tuamshe hisia za watanzania wengine, huku tunakwenda kuwanufaisha watanzania wengine na huku wengine, wataamsha hisia za hasira na tunaweza tukafika mahala ambapo sio pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niiombe Wizara iweze kugawa sungura huyu kwa kuangalia uwiano sahihi kabisa, ili watanzania wote waweze kuona ya kwamba na waji-feel proud ya kwamba ni sehemu ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, itakupa mifano michache tu pale kwetu Kigoma, kuna baadhi ya wananchi mpaka sasa toka tunaupata uhuru hawajawahi kuona gari! Toka uhuru ukienda Kata ya Kagunga, ukienda Kata ya Mwamgongo, ukija na Kata ya Ziwani zaidi ya wananchi 70,000 gari haifiki. Barabara yetu ya kuanzia Mwandiga kupita mpaka Chankere kwenda mpaka Mwamgongo na kufika mpaka bandari ya Kagunga haijawahi toboka mpaka dakika ya sasa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitaka kwenda kuwatembelea wananchi wetu hawa lazima upite nchi jirani ya Burundi. Mheshimiwa Waziri alikuja Kigoma, ameshindwa kufika kuwatembelea wananchi wetu na hiyo yote ni kwa kuwa hakuna barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara iweze kuangalia iwezekanavyo iwapelekee wananchi na hawa wajione ni sehemu ya nchi hii. Waweze kuona ya kwamba na wao wanachangia kuijenga nchi ambayo na wao wanapata haki sawa. Ukiangalia bajeti nilikuwa napitia na nimepitia nikiwa safarini natokea Kigoma, wametengewa ile barabara milioni 200 barabara ambayo inahitaji zaidi ya bilioni 23. Unakwenda kutenga milioni 200 itatoboka lini? Itamalizika lini hii barabara? Na hii barabara iko kwenye Ilani ukurasa wa 74 wa Ilani ya Chama chetu Cha Mapinduzi, umeisema hii barabara kilometa 60 lakini ukiangalia pesa zinazotengwa zinasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, niiombe Wizara nitakuwa na machache sana na msingi wangu ni kwenye hii barabara. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, shida umeiona, utakapokuja ku-wind up hapa uje utuambie ya kwamba ni lini wananchi hawa watakuja kupata uhuru kama wananchi wa sehemu zingine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema machache hayo naomba kuunga hoja mkono, lakini Waziri utuambie ya kwamba barabara hii ya kutokea Mwandiga mpaka kwenda bandari ya Kagunga ambapo Serikali imewekeza mabilioni ya pesa kwenye bandari ile ya Kagunga. Lakini hayana manufaa yoyote, ili yaweze kuwa na manufaa na bandari ile ifanye vizuri lazima tupate muunganiko wa barabara hii ya Kagunga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa kuna barabara ya Mwandiga – Manyovu imeanza ujenzi mwaka 2008. Barabara ile imejengwa lakini kuna wahanga wa barabara ile ambao walibomolewa majumba yao walipoteza na baadhi ya maeneo yao. Hawajalipwa fidia mpaka sasa, nikuombe Waziri ikiwezekana uweze kufika uzungumze nao, imekuwa ni muda mrefu hawajalipwa fidia za nyumba zao zilizobomolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya machache hayo niweze kuunga hoja mkono, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, kwa kunipa nafasi niweze kuchangia wizara hii muhimu sana ambayo hakika ni injini ya uchumi ambao tunatarajia kuuendea kama Taifa, Uchumi wa Viwanda yaani Industry Economy.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naanza kwa kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi kwa ajili ya kuchangia katika wizara hii. Lakini jambo la pili naishukuru Serikali kwa jinsi inavyofanya kazi kwa mambo makuu mawili katika mkoa wetu wa Kigoma. Kigoma ilikuwa ipo gizani lakini mpaka dakika ya sasa Serikali imeweza kuchukua juhudi kubwa sana tunaunganishwa na umeme wa grid ya Taifa na hatua zinaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili kabisa ambalo ninaishukuru Serikali inayoongozwa na Jemedari Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kusaini mkataba wa kufua umeme katika chanzo cha Mto Malagarasi. Sisi Kigoma na location tuliyonayo tunaitegemea hii wizara sana kuliko kitu kingine, kwa sababu ukiangalia katika eneo lile tulilonalo la Kigoma na majirani tulionao bila hii wizara kututazama hatuwezi tukatoka mahala tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia tupo tumepakana na nchi jirani zile nchi zote ku-survive zinaitegemea Kigoma na haziwezi zika-survive bila Kigoma bila kuja kula Kigoma, lakini Kigoma haiwezi ikawalisha wale watu bila hii Wizara muhimu sana wizara ya Nishati. Nakumbuka nimejaribu kupitia sana hapo nyuma Mzee wangu Mwijage aliweza kuwa na wawekezaji kipindi yupo ni Waziri wa Viwanda alipata wawekezaji ambao walipaswa waje kuwekeza katika mkoa wetu wa Kigoma kwa ajili ya kuzalisha sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wale wawekezaji hawakufanikiwa kuzalisha sukari katika mkoa wetu wa Kigoma ukifuatilia vitu ambavyo vilivyo wakwamisha cha kwanza ilikuwa ni ukiritimba wa sheria za uwekezaji. Lakini jambo la pili ilikuwa ni kukosekana kwa nishati ya kuweza kusimika kiwanda cha kuzalisha sukari pale Kigoma, walishindwa lakini mpaka sasa kuna watu wanakuja kuchukua sukari Rwanda wanapeleka mpaka Zambia na wakati ilihali tungezalisha pale Kigoma, lakini hiyo yote ilishindikana ni kwa sababu hatukuwa na nishati ya kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hivyo naomba nielezee hali halisi ya nishati katika mkoa wetu wa Kigoma. Katika mkoa wetu wa Kigoma tunatumia umeme unaotokana na ma-generator tuna vituo vitatu katika Mkoa wetu wa Kigoma, kituo cha kwanza ni Kigoma Mji na kituo cha pili ni Kasulu na kituo cha tatu ni Kibondo. Vituo hivi vyote vitatu vinauwezo wa kuzalisha megawatt 11.25, lakini na sisi mahitaji yetu kama mkoa tunahitaji kuwa na megawatt 10.57, pamoja na hayo yote bado watumiaji wameongezeka kwa kasi sana kutokana na kwamba Serikali imeleta kuwaunganisha wananchi wengi na watumiaji wengi wameongezeka kupitia mfumo huu wa REA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na baada ya kutokana na hiyo ukija ukaangalia hiki kituo cha Kigoma Mji kinahudumia maeneo ya Kigoma Ujiji, kinahudumia na maeneo ya Wilaya ya Uvinza kinakwenda na sehemu ya maeneo ya Wilaya ya Buhigwe, lakini hiki kituo kina uwezo wa kuzalisha megawatt 6.25 tu, ili kiweze kuhudumia hizi wilaya tatu. Pamoja na hayo yote bado kinazidiwa, kinazidiwa kwa sababu hizi wilaya tatu zinazidi hizo megawatt zinazozalishwa na kituo hiki cha Kigoma Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kituo cha Kasulu kina mashine mbili nacho kinalisha Kasulu na kinalisha na sehemu ya Buhigwe, lakini ile mashine moja mpaka sasa haifanyi kazi iseme imekufa. Kwa hiyo, imebidi sasa TANESCO wachukue sehemu ya Buhigwe wairudishe Kigoma Mji mpaka dakika ya sasa wananchi wa Kigoma wananusishwa umeme. Jana umeme umekatika saa kumi na mbili wanarudishiwa asubuhi na imekuwa ni trend ambayo inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hali hii iliyopo kuna minong’ono mingi sana huko kwanini umeme uanze kukatika sasa na kwanini haukuwa una katika hapo nyuma najua mlengo wa Serikali ni kwamba hakuna mgao wa umeme, lakini lazima tuzungumzie uhalisia kabisa ya kwamba upo umeme una katika na wananchi kila siku lazima umeme ukatike na shughuli zinamama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo ningeomba wizara iweze kulichukulia umaanani wake, ukija Kibondo kadhalika hivyo hivyo ina uwezo wa kuzalisha megawatt 2.5 hiki kituo cha Kibondo kinalisha Kankoko, kinalisha na Kibondo, lakini kinahitaji zaidi ya megawatt 3.2 ili kiweze kulisha hizi wilaya mbili nacho kinauwezo wa kulisha hii 2.5.

Mheshimiwa Spika,kwa hiyo, niiombe Serikali najua kuna namna ambavyo inataka kufanya kwa ajili ya kutoa mashine kutoka Loliondo kuja kuisimika pale kituo cha Kasulu, hilo ni zuri kabisa na ningeomba sana wizara iweze kuharakisha kwa sababu sisi Kigoma tumekuwa kwenye hii hali wakati ilihali wenzetu wananufaika na umeme grid sasa ningeomba hii bajeti iweze kuangalia a quick solution ya kuitoa Kigoma mahala ilipo mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuoneshe tu jambo dogo ambalo mpaka sasa ukija ukaangalia Serikali inatumia pesa za watu masikini kutumia kwa ajili ya kutumia haya ma- generator na kama ikiweza kuharakisha kwa mfano; grid ya Taifa wamesema kufikia Kigoma itakuwa imefika mwaka 2023 jambo ambalo ikifika mpaka huo mwaka tutakuwa tumesha hangaika vya kutosha. Ningeiomba Serikali ina uwezo kulingana na hii hatua tuliyonayo iweze ku-speedup huu mradi wa umeme wa grid ya Taifa angalau hata tufike 2022 uwe umeweza kufika ili kuweza kuwa na permanent solution katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka dakika ya sasa katika Mkoa wa Kigoma unit moja ya umeme inazalishwa kwa shilingi za kitanzania 645, lakini unit moja hiyo hiyo ya umeme ukienda Singida inazalishwa kwa shilingi za kitanzania 36 mpaka 50 na Serikali hii hii inaweza kutumia bilioni 1.6 kwa mwezi kwa ajili ya kuzalisha umeme katika Mkoa wetu wa Kigoma hizi ni pesa nyingi sana, kwa nini tusiharakishe sana ili umeme wa grid uweze kufika tuweze kuokoa pesa hizi na hatimaye mwananchi aweze kuona ya kwamba ana unafuu wa kuweza ku-utilize umeme katika mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nishauri mambo machache sana katika wizara hii ili iweze kuyachukulia kwa uharaka sana ambayo moja itakuwa ni permanent Solution, lakini nyingine itakuwa a quick solution kwa ajili ya kuokoa hii hali inayotokana, inayojitokeza kila muda katika mkoa wetu wa Kigoma. Moja kabisa, ni kama nilivyosema ni kuharakisha huu mradi wa umeme wa grid ya Taifa ili uweze kufika kwa haraka sana hiyo ndiyo permanent Solution sisi watu wa Kigoma tutakayoiona ya kwamba mmetutoa kwenye giza, lakini jambo la pili ni kuweza kuharakisha hiyo mashine kutoka Loliondo iweze kufungwa pale katika kituo cha Kasulu ili tuweze kuepukana na hii hali ya umeme kukatika kila iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, na jambo la tatu kabisa na la mwisho, nimuombe Waziri pale kwetu Kigoma kuna muwekezaji ambaye anaitwa the next Solar Wazi Limited amewekeza pale Kigoma anauwezo wa kuzalisha megawatt 4 mpaka 5, lakini anazalisha chini ya megawatt hizo ambapo vilevile tumejaribu kumuona hapo miezi ya nyuma anasema ndio anaweza, lakini Serikali iweze kumpa ushirikiano ili aweze kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa niombe Waziri uweze kuongea na muwekezaji ili aweze kuzalisha zaidi ya hicho kiwango ili tuweze kuepukana na hali ya mgao huu wa umeme katika mkoa wetu wa Kigoma.

SPIKA: Mheshimiwa!

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, kwa machache hayo naona muda umekimbia, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara ya Maji ambayo ni muhimu sana, Wizara ambayo haina mbadala hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimwia Mwenyekiti, pili namshukuru kaka yangu Aweso kwa kazi kubwa sana ambayo anaifanya. Kama Waziri kijana anatufundisha namna ya kutenda na sisi vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha tatu namshukuru Mheshimiwa Rais, ametoa Shilingi bilioni 3.8 kwa ajili ya miradi ya maji jimboni kwetu. Kwa kweli hii ni hatua kubwa sana. Pasi na kuchukua muda sana nitajielekeza kwenye mambo makuu mawili ambayo ndiyo itakuwa msingi kabisa wa hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni namna gani ambavyo nimeona ya kwamba Wizara hii kaka yangu Aweso inatengewa fedha nyingi sana na zinakwenda huko majimboni kwetu, lakini ufanisi wa fedha hizo ni mdogo sana. Nitakupa mfano halisi wa kwa Jimbo letu la Kigoma Kaskazini, tuna miradi zaidi ya tisa, na mwaka huu umeipatia fedha miradi hiyo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, tuna mradi wa Mkigo. Kata ya Mkigo umetupatia Shilingi milioni 986, tunashukuru sana, na Kata ya Nyarubanda na Mradi wa Kalinzi umetupa Shilingi milioni 387. Hizo nazo tunashukuru sana, na hata bajeti iliyopita ulikuwa umeshatupatia fedha. Ukiangalia huu mradi wa Kalinzi umeshapeleka Shilingi milioni 900 na mradi umekwisha, lakini mradi unatoa maji yenye matope. Hakuna ufanisi wa ile fedha ya kwanza ambayo umeipeleka na sasa umeongeza fedha. Tunashukuru, ni kweli tunakwenda kutatua tatizo hili kwa kuweka Solar, lakini nakuomba sana huko chini ushuke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimeona ulichokifanya kimenifurahisha, huku Watendaji wako watasema maji yapo na kwenye makaratasi wanakuonesha ufanisi mkubwa sana, lakini kwa wananchi ukienda hauoni ule ufanisi wa fedha uliyoitoa. Kwa hiyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri uweze kuona, hali ya mradi wa Mkongoroani unafahamu nimefika ofisini kwako mara nyingi, tumesaidiwa na Kampuni ya Enabel na Serikali imeweka nguvu yake humo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi unahudumia Vijiji Saba, kuna Kijiji cha Mkongoro, Kijiji cha Nyabigufa, Bitare, Nyamuhoza, Mkwanga na Kizenga. Mradi huu fedha imeshatolewa asilimia robo tatu yake, lakini ufanisi wake ukienda maji yanatoka mara moja kwa wiki hii haitupi afya sisi! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri uweze kupita, tuna miradi mingi ya Mwandiga, Mungonya, miradi ya Matendosamwa na hii miradi ya Kidahwe. Miradi yote hii unatoa fedha vizuri sana lakini moja ya jambo ambalo ningeomba niishauri Wizara yako, kitu cha kwanza kabisa katika hii miradi, jambo la manunuzi limekuwa ni tatizo kubwa sana huko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano mmoja suala la manunuzi liko kwenye ngazi ya Mkoa lakini ukiangalia mradi wa Mungonya umekwishatoa Shilingi Milioni 412 na zimeshatoka zote. Ukiongea na Meneja wa Wilaya anakuambia changamoto ni viungo vinne kuja kuunganisha kwenye vijiji viwili vipate maji, ameweza kuagiza vile viungo viweze kununuliwa amekwenda Mkoani anasema watu wa manunuzi walichanganya. Mpaka sasa havionekani ni mwaka mzima watu hawapati maji kisa tu viungo viwili vya Shilingi Milioni Mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya manunuzi inaleta shida sana, ningeomba sana nimesikia mnataka kuipeleka kwenye ngazi ya Kikanda itasumbua zaidi. Mimi ninashauri badala ya ngazi ya Mkoa ambayo inaleta changamoto ni vema tungeshusha ngazi ya Wilaya kwenye hali ya manunuzi ili Wilaya ikiona kuna changamoto iweze kuchukua hatua haraka kuliko kusubiri iende ngazi ya Mkoa. Hilo jambo naomba ulitazame sana ili liweze kuleta ufanisi zaidi wa miradi hii ambayo unatoa fedha lakini haiwezi kukamilika kwa wakati na hata ikikamilika hakuna ufanisi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuna hali ambayo umeiona katika Bunge hili, Wabunge wapo walionyanyuka wakapongeza wapo Wabunge wamekupigia makofi kwa sana na Wabunge wengine umeona hapa kama Wabunge wa Mtwara wanalia kwa machozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigoma ni sehemu ya hilo jambo, Kigoma tunashindwa kuelewa kuna changamoto gani, Kigoma na Rukwa, Kigoma na Katavi tunashindwa kuelewa kuna changamoto gani?

Mheshimiwa Waziri wewe ni msomi, unakwenda unachukua maji kutoka Mwanza na Wabunge wa Mwanza wamekupongeza yanafika mpaka Dodoma kilomita 687 lakini pale Kigoma nina Ziwa kilomita tano watu wanalia maji, just five kilometers! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda hata vijiji vingine nusu kilometer hakuna maji, mfano Kijiji cha Kiziba kwa nini isifike hatua kama mnaweza mkapeleka shilingi bilioni 500 kule Arusha, mimi ni mjumbe wa Kamati ya PIC tumekwenda Arusha, tunaona jinsi ambavyo mnaweka miradi mikubwa kwa nini msiifikirie na Kigoma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigoma tuna vyanzo vingi ukiacha Ziwa tu hata hii Mito. Mto Malagarasi una mwinuko mzuri tu, ukichukua Mto Malagarasi sehemu moja unapeleka kabisa kwenda kuhudumia Wilaya ya Kibondo na unahudumia Kasulu ule utakaohudumia Kasulu unashuka mpaka Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana tunaomba sana wazee wa Kigoma inafika mahali wanajiuliza iko shida gani? Sisi tuwe na ziwa hapo mlangoni kwetu, wengine hawana hata ziwa, leo hii wanapongeza na sisi tutapongeza endapo mtaweza kututazama. Lazima Dodoma wapongeze kama mnatoa maji kilometer 687 wanaachaje kupongeza? Sisi Kigoma tunasema nini tuwekeeni mradi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano tu wa hii miradi mnayotupa ni kweli inakuja kutatua matatizo ya maji lakini sio endelevu. Mfano mmoja ni thabiti mwaka 2020 tumekwenda Wilaya ya Kibondo, Waziri Mkuu amekwenda kutembelea mradi mmoja mradi wa Shilingi Bilioni Sita lakini mpaka dakika ya sasa unatoa maji kwa kusuasua, hizo fedha pelekeni kwenye chanzo cha kuaminika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupeni mradi ambao unatoa maji kwenye chanzo cha kuaminika ili nasi Bunge lijalo tuje tupige makofi, tufanane sawa na wa Mwanza, tufanane sawa na wa sehemu zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo machache naomba sana Kaka yangu Mheshimiwa Aweso uweze kukaa chini ujifikirie, ufikirie sana una msemo wako mzuri sana “wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani” lakini Kigoma punje ni mbili kwenye sahani. Sasa hatuuoni huo wali wa kushiba, tunaomba sana na sisi uweze kutujazia wali wa kushiba kwenye sahani ili Kigoma tuone fahari yako wewe kuwa Waziri.(Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii ya Kilimo ambayo ni muhimu sana, Wizara ambayo ina mchango mkubwa sana katika Taifa letu. Asilimia 26.1 ya pato la Taifa linatokana na Wizara hii. Wizara hii ni muhimu sana kwa sababu inatoa ajira ya wastani wa asilimia 65, lakini siyo hivyo, viwanda vyetu na malighafi zake asilimia 65 zinategemea Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru Mheshimiwa Rais, anafanya kazi kubwa sana, lakini nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri Mkuu, anafanya kazi kubwa sana katika Mkoa wetu wa Kigoma na hasa katika zao la chikichi. Mheshimiwa Waziri Mkuu amefanya jambo kubwa sana la chikichi ambapo pamoja na ukuaji mkubwa tunaupigia kelele, lakini jambo la kudhibiti vipimo vya mafuta ya mawese ni jambo kubwa sana katika Mkoa wetu wa Kigoma. Tunatuma salaam hizo za shukrani kwake na kwa Serikali yote na pia kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama, kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya katika Mkoa wetu wa Kigoma. Hivi sasa vipimo vya lita 30 ambavyo vilikuwa vinamnyonya mkulima wa Mawese, vinaonekana kama bangi katika Mkoa wetu wa Kigoma. Hilo tunalishukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ni kijana, kaka yangu Mheshimiwa Bashe, namshukuru sana kwa kazi anayoifanya. Pamoja na mambo mazuri sana aliyoyafanya katika Wizara yake, natambua Benki ya Kilimo (TADB) imetoa mikopo shilingi bilioni 169, lakini shilingi bilioni 108 zimekwenda kama direct landing. Siyo hivyo tu, bado ametoa shilingi bilioni 60 kwa ajili ya kwenda kwa wakulima wadogo wadogo. Kwa hilo tunamshukuru sana na tunaendelea kuipongeza Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. hapa liko jambo moja tu ambalo tunamwomba Mheshimiwa Bashe, sisi kama vijana, naye ni kaka yetu atusikie. Hapa kuna changamoto kubwa sana. Kwenye benki hii ya kilimo, hebu uwape mtaji kaka yangu wafanye kazi.

Mheshimiwa Spika, wakulima wanahitaji mitaji. Benki hizi usipoziwezesha, hawawezi kupata manufaa makubwa na benki hii. Mheshimiwa Bashe nitakupa mfano mmoja. Hivi sasa hii Benki ya TADB inaweza kukopesha wakulima wetu kwa asilimia tisa, lakini wakulima bado wana mizigo mikubwa, ndio maana tunaomba uweze kuiongezea pesa ili angalau asilimia ishuke nane mpaka saba ili mkulima asiwe na mzigo mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini si hivyo Mheshimiwa Bashe, wapo watu ambao wanaingia kama ma-middle men kwenye hii benki ya kilimo, ambao ukiangalia kama Mkoa wa Kigoma, ili hizi AMCOS ziweze kukopesheka lazima kuwe na mtu anaitwa PASS. Huyu PASS ndiye atakuwa mdhamini wa mkulima ili mkulima aaminike, watu hawa jaribu kuwa Cut off. Kwa sababu huyu PASS ana percent yake kwenye mkopo ambao mkulima atachukua. Ukiwaondoa hawa PASS unamuondolea mkulima mzigo mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye kahawa Mheshimiwa Bashe, umefanya jambo kubwa sana katika Mkoa wetu wa Kigoma. Umeweza kufanya jambo la msingi sana mpaka wanunuzi wamekwenda kwa mkulima direct. Wamenunua kahawa na angalau kwa Mkoa wetu wa Kigoma bei si haba, tunakushukuru sana kwa jambo hilo. Lakini mzigo umeutoa ulikokuwa mwanzo umeuhamishia kwenye pembejeo. Hivi sasa lita moja ya dawa ya kutibu kahawa iliyokuwa inanunuliwa kwa shilingi 15,000 hivi sasa ni 50,000. Huo ni mzigo mkubwa sana Kaka yangu Bashe, uweze kuangalia namna gani tuweze kumpunguzia adha mkulima huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, my brother nitazungumzia jambo lingine, jambo la mkulima na pembejeo. Wabunge wengi wamezungumza katika hali hii ya mbolea ya ruzuku na nimekusumbua sana kipindi cha mbolea hii. Mheshimiwa Bashe, nia ni njema ya suala hili na tunaipongeza sisi Wabunge ambao tunatoka kwenye majimbo ya vijijini. Lakini ziko dosari ambazo zimeingia hapa katikati zilitaka kuchafua nia hii, na jambo hili Mheshimiwa Bashe, tutafurahi zaidi ukilifanyia kazi kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano tu mdogo ili niweze kumalizia, naona na muda unakwenda. Mheshimiwa Bashe, kwenye hii program ya mbolea ya ruzuku wapo watu wanne, kuna Serikali, kuna supplier, kuna agency ambaye ni wakala lakini kuna mtu wa mwisho ambae ndiye mkulima.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapata shida kubwa sana ambapo tunaona mkulima anapiga kelele. Mbolea muda mwingine inamfikia kwa bei ya juu sio hiyo ya ruzuku. Wakulima wa Mkabogo kule jimboni kwangu, wakulima wa vijiji vya kule Kalinzi wameweza kufikiwa na mbolea kwa bei ya 120,000 mpaka shambani, wakati ili hali hii mbolea ni shilingi 70,000. Ukiangalia hapa katikati ni kwa sababu hawa mawakala wana sababu kuu mbili.

Mheshimiwa Spika, sababu ya kwanza; wao wanaweza kutoa ile mbolea kwa mkopo. Maana yake ninyi mnamlipa supplier mnamwacha agent, huyu agent hana mtaji mkubwa wa kuweza kupeleka mbolea mpaka kwenye tarafa na vijiji lakini angekuwa na mtaji mkubwa angeweza kufikisha mbolea hii hadi kwenye vijiji.

Mheshimiwa Spika, sasa, changamoto kubwa unakwenda kumlipa supplier cash unamwacha agent huyu aende akazungushe mbolea kwa pesa yake, matokeo yake mbolea haifikishi. Ukiangale pale Kigoma Mjini agent alikuwepo mmoja. Kigoma mjini hakuna mkulima sisi vijijini ndio tunalima lakini hakukuwa na wakala hata mmoja, kitendo ambacho kimeongeza hii nia njema ikaonekana kuwa nia mbaya lakini tunaamini kwa jambo kubwa ambalo unaendelea kufanya, ukaifanye hii kazi kwa ustaarabu mkubwa sana ili wakulima wetu waweze kunufaika na hali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisimalize bila kuunga mkono hoja, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ambayo ni Bajeti Kuu ya mwaka 2022 kuelekea 2023. Mheshimiwa Waziri ametuwasilishia bajeti hii ambayo imekuja na vitabu vinne, nimeipitia na kwa kweli lengo kubwa ni kutafuta, na namna gani tukishatafuta, tuweze kutumia. Nami nimepata jambo la kuweza kusema ili kumshauri Mheshimiwa Waziri aweze kuangalia namna gani anaweza akayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti hii smeelezea vipaumbele ambavyo ndivyo atakavyoviweka mbele na ambavyo vitamwezesha katika kukusanya na wapi atapata mapato hayo. Kipaumbele cha kwanza amesema mwenyewe kwenye bajeti yake page ya 33, amezungumza kwamba atafanya kipaumbele cha kwanza kuwa ni kilimo na atakifanya sana sana kilimo cha Chikichi kuwa Kigoma ndiyo iwe kitovu kikubwa cha kilimo hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, palm economy ndiyo uchumi wenyewe sasa hivi ambao unaweza ukaleta majibu makubwa ya inflation yoyote ambayo inaweza ikapatikana kwenye bei ya cooking oil. Changamoto hii inaweza ikatatuliwa na palm oil peke yake tu. Kabla ya kwenda mbele kabisa nimwoneshe Mheshimiwa Waziri kwamba, sisi wenyewe hata kwenye ripoti yake ya hali ya uchumi amezungumza hili jambo, lakini Waziri mwenye dhamana amezungumza hili jambo kwenye bajeti yake, Bwana Bashe. Nimepitia sana hii bajeti yake page namba 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe anatuonesha kwamba mazao ambayo yanazaa mbegu hizi za mafuta katika namna zilivyozaa kuanzia mwaka 2017 mpaka mwaka 2020, kwenye Jedwali namba 12 ameonesha Waziri mwenye dhamana ya kwamba zao ambalo limeonesha kuzaa kwa negative ndani ya miaka mitano, ni alizeti; na limeshuka kwa asilimia 26.3 kutoka mwaka 2017 mpaka mwaka 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipomfuatilia Waziri, anaonesha kabisa jitihada kubwa bado ameiweka kwenye alizeti. Mheshimiwa Waziri na Mwenyekiti ukija ukatazama Jiografia ambapo alizeti inamea ni semidesert, yaani ni nusu jangwa. Kwa maana hiyo ukienda kuweka matumaini ya Taifa kwamba ulilishe Taifa mafuta ya kula kutoka kwenye alizeti, unaliweka Taifa kwenye hali ya hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Kigoma tuna hali ya Jiografia safi kabisa, mvua hazina changamoto hata kidogo kwetu. Siyo hivyo tu, alizeti ni zao ambalo linaweza likapandwa kwa mwaka na baadaye likishavunwa haliwezi tena kuvunwa mpaka lipandwe tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini chikichi, ukiipanda; sisi tumezaliwa tunakuta michikichi ya miaka 80; mpaka sasa hivi miaka 30 bado ipo. Haja kubwa ipo katika kutazama zao la Chikichi. Jaribu kuangalia, hata juzi tumehudhuria semina hapo, watu wa Benki ya Dunia wameonesha wengi kuwa na statements mbili tofauti, lakini statement moja ambayo hata sisi tunajichanganya, wengi wanasema mfumuko wa bei kwenye mafuta ya kula ni kwa sababu ya vita vya Ukraine; uongo mkubwa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema, mfumuko wa bei kwenye mafuta ya kula unasababishwa na mipango yetu sisi wenyewe kama nchi, wala siyo vita hata kidogo, kwa sababu hivi ni vitu ambavyo tunaweza tukazalisha wenyewe endapo tutaweza kuweka mipango madhubuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jaribu kutazama kwenye jambo hili; ikiwa tunaweza tukakusanya fedha zetu wenyewe, hizi za madafu, tukatenga Shilingi bilioni 480 tukaenda kuagiza mafuta haya kutoka nje, kiasi kikubwa kama hicho, na kule tunapoagiza ndiko kwa watu waliokuja kujifunza hiki kilimo cha Chikichi kwetu; tunatoa fedha zetu tunazipeleka kule kwao, tunakuwa tumepeleka vitu vingi sana, hatujapeleka fedha tu. Tumepeleka fedha za kigeni, tumepeleka ajira za watu wetu, tumewahamishia wale watu waliopata akili mapema wakaweza wakaweka mipango Madhubuti, ndiyo tunakwenda kununua kule. Tunakuwa tumenunua na vingi, tumebadilishana na vingi kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikufahamishe tu jambo usilolijua au mwingine anaweza asilifahamu, mafuta yote tunayokula hapa Tanzania, asilimia 98 yanatokana na Mawese. Ukichukua Korie, ni zao la Mawese. Ni nini kinachofanyika ambacho kinatufanya tuweze kutumia kitu ambacho tunaweza tukazalisha wenyewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo teknolojia mbili tu duniani ambazo Malaysia na Indonesia wanazitumia. Hata sisi wenyewe wafanyabiashara wetu wanakwenda kuchukua kule kutoka kwa hao watu wanakuja huku wanafanya packaging tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mawese wanachokifanya, wanatumia teknolojia ambayo inaitwa deodorization, wanaondoa harufu ya yale mafuta ya mawese. Wakimaliza pale, wanafanya teknolojia ya pili inaitwa colorization, wanaondoa ile rangi ya mawese unayoiona. Ikishatoka pale, ni Korie halisi, tayari kwa packing, inakwenda kutumika kwenye soko letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jambo hili analiweza sana, na kuliweza ni yeye tu, amezungumza kwenye hali ya kubana matumizi, hata hapa mpaka sasa anaweza aka-cutoff kwenye hii bajeti nusu tu, itazaa viwanda vikubwa sana Mkoani Kigoma ili tuweze kuzalisha kwa asilimia kubwa na hatutaagiza mafuta nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu jambo moja ya kwamba kwa kuweza kujibana hata mwaka mmoja katika bajeti zetu, tunaweza tukapunguza lita hizo tunazoagiza nje kwa kiwango kikubwa sana. Ni sisi tu kuamua leo. Mheshimiwa Waziri na Wizara yako, chukueni uamuzi leo mweze kulifanyia kazi hili, tutakuwa tumekwenda kurekebisha katika mfumuko huu na hali ya mafuta ya kula ambayo inasumbua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa gharama hiyo hiyo, hata technical team imefanya research yake, ipo Ofisi ya Waziri Mkuu na ninadhani na Mheshimiwa Waziri utakuwa umeipata. Hii technical team inaongozwa na Mzee mmoja yupo pale Kigoma, wameweza kuangalia namna gani ambavyo kama Kigoma na maeneo mengine ambayo yamezungumzwa kwenye bajeti ikiwemo Mkoa wa Kagera na Mikoa mingine ya jirani katika bonde lile la Mto Tanganyika likitumiwa kwa bajeti hii hii, tunakwenda kuweka mabadiliko makubwa kwenye hali hii ya mafuta ya kula tunayoagiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende hoja ya pili, ni suala la reli. Mheshimiwa Waziri, kwanza tunakushukuru sana na tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa jambo kubwa hili alilolifanya. Sisi tulikuwa na hofu sana. Kwa mchumi yeyote kwa mpango ule wa kwanza uliokuwepo, tulikuwa tuna hofu nchi yetu inakwenda kutengeneza uneconomic hub kwenye nchi jirani. Ila kwa kitendo Mheshimiwa Rais alichokifanya, akaleta ile reli ikaenda kupita pale Uvinza ipande Msongati, iende Gitega, iende Bujumbura na baada ya hapo itokee pale pale Uvinza ifike mpaka Kindu nchini Kongo, ni jambo la kupongezwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunasema Mheshimiwa Rais ameweza kupaona hapo. Wale walikuwa wametutega, kwa sababu tunakwenda kutengeneza hub katika nchi yetu wenyewe. Watu wa Kigoma tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hilo aliloliona, nasi tunasema tutakuwa pamoja naye na tutamuunga mkono. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Assa.

ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)