Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Amina Ali Mzee (5 total)

MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, hatua zipi zinachukuliwa na Serikali kuwawezesha vijana wanaofanya biashara mtandao ili kuwezesha mapato ya Taifa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu na mikopo ili kuwezesha upatikanaji wa ajira ya ndani na nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Serikali kazi yake ni kuhakikisha kwamba inaweka mazingira wezeshi kwa vijana ili waweze kufanya biashara hiyo. Sambamba na hilo kupitia biashara zozote za kimtandao Serikali imeweza kurasimisha shughuli hizo kwa kuanzisha sheria ya makosa ya kimtandao maana yake kwamba kijana ili aweze kujua mipaka ya namna gani biashara yake akaifanye.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna Sheria ya Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta ya Mwaka 2010, hii yote inatoa guidelines za namna gani kijana anaweza kuingia katika biashara hiyo.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kwa sababu unapofanya biashara lazima kuna transactions zitakuwa zinafanyika, ili sasa kumlinda katika zile transactions Serikali pia ilichukua jukumu la kuanzisha Sheria ya Miamala ya Kieletroniki ambayo sasa transaction yoyote inakuwa inatambulika, anapokuwa anafanya hizi biashara.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kupitia Wizara yetu kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia vijana hawa, Serikali ina mpango mzuri wa kutoa elimu ambapo vijana watakuwa wanajua namna gani na sehemu zipi wanaweza kuwa wanapata mikopo kwa ajili ya kujiongezea kipato na hatimaye tunaongeza pato la Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali moja la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natambua wanufaika wakubwa ni vijana Watanzania: Je, Serikali ina mpango gani wa kupanga fedha kwa ajili ya kukiendeleza chuo hiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBAS P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshakuwa na mpango wa kujenga jengo hilo litakalokuwa na urefu wa ghorofa sita na tayari fedha zimeshatengwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Amina kwa kuwa mfatiliaji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tuna habari nyingine njema ambayo Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan ameshatoa zaidi ya shilingi bilioni 54 kwa ajili ya kuwasaidia vijana zaidi ya 150,000 ambao wataenda kupata mafunzo mbalimbali katika vitengo hivyo ikiwemo uchumi wa bahari. Ahsante. (Makofi)
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Usalama wa vyombo vya majini ni lazima kwa maisha ya watu na mali zao. Je, Serikali inafanyaje kila baada ya muda kuvifanyia ukarabati kisheria?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba usalama ni jambo la msingi na ni lazima lifanyike. Kwa sheria yetu tunafanya ukaguzi kila mwaka kwa vyombo vyote vya majini na kwenye maziwa makuu, na huwa tunatoa cheti kinachoitwa seaworthiness certificate. Hata hivyo, hatulazimiki tu kwa mwaka, tunaweza tukafanya pia kwa wakati wowote inapobidi shirika lijiridhishe na vyombo hivyo. Ahsante.
MHE. AMINA ALLY MZEE: Mheshimiwa Spika, asante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Je, Serikali haioni sasa iko haja ya kuharakisha juu ya mradi wa ujenzi wa Mkongo wa Taifa uenee nchi nzima?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge wa Viti Maalum - Zanzibar kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nilishukuru Bunge lako tukufu kwa kutupitishia bajeti ambayo inaenda kuhakikisha kwamba ujenzi wa Mkongo wa Taifa unakamilika. Lakini kama nilivyosema katika jibu la msingi ni kwamba tayari tuna Wilaya 43 ambazo zimeshakamilika lakini katika bajeti ya mwaka jana Wilaya 23 tena zinaenda kukamilishwa. Lakini katika bajeti ambayo imepitishwa Ijumaa Wilaya 15 zingine zinaenda kukamilika kufikisha jumla ya Wilaya 81. Hivyo tunaomba kabisa kwamba kufikia mwaka 2025 wilaya zote nchini zitakuwa zimepata huduma ya mkongo wa mawasiliano wa Taifa. Nakushukuru.
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kuharakisha utungaji wa sheria hiyo, Ili shirika liweze kujiendesha kibiashara?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Serikali haioni haja ya kuhakikisha inalipatia magari shirika liweze kujiendesha na liweze kujitegemea ili liendane na soko nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza la Mheshimiwa Amina, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa Shirika la Utangazaji (TBC) ambalo linaongozwa kwa notice ya Serikali 186 ya mwaka 2007 kutokana na Sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 2002. Serikali ipo katika mchakato huo wa kuhakikisha kwamba utungaji wa sheria ya mwaka 2003 unafanyika kwa haraka. Sasa tayari tupo katika hatua ya pili ya uchambuzi, baada ya kuwa tumepata maoni mahususi kutoka Wizara ya Fedha. Hivyo, utungaji wa sheria huu upo katika hatua nzuri na baada ya hapo tutafikisha katika Bunge lako tukufu kwa ajili ya utaratibu unaotakiwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tayari Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuboresha vitendea kazi. Vitendea kazi ni pamoja na magari, ni kweli kabisa tunahitaji kuwa na OB Van za kutosha katika kanda zetu, lakini katika mikoa kulingana na ukubwa wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, tayari ametoa fedha kwa ajili ya kuboresha studio zetu za TBC kwa kiwango ambacho kinaendana na teknolojia ya sasa. Tayari ametoa Shilingi bilioni 3.235 kwa ajili ya studio iliyopo Barabara ya Nyerere, kwa ajili ya TBC Taifa na TBC FM. Vile vile alitoa Shilingi milioni 601.8 kwa ajili ya kuboresha studio yetu ya hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais, kwa kazi kubwa anayoifanya, kwa sababu hiki ni chombo cha umma ambacho kipo kwa ajili ya kuelimisha, kuburudisha na kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kukushukuru sana.