Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Asia Abdulkarim Halamga (1 total)

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ya Tanzania imeweza kusaidia baadhi ya nchi za Afrika kujikomboa katika uhuru wa nchi zao. Moja ya nchi hizo ikiwa ni Afrika ya Kusini, Angola, Zimbabwe, Msumbiji na maeneo mengine. Katika nchi yetu ya Tanzania, maeneo ambayo yalishiriki katika mkakati huo wa kuzisaidia nchi hizo ni pamoja na Kongwa, Mazimbu Morogoro, Nachingwea na maeneo mengine. Nini kauli ya Serikali kwa Mataifa haya kuhusu kuchangia maendeleo katika maeneo haya ambayo nimeyataja nchini kwetu.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Halamga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, najua swali hili una maslahi nalo kwa sababu Kongwa ni moja kati ya maeneo ambayo wanaharakati hawa wa kupata uhuru kwenye nchi zao waliishi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali na Taifa letu la Tanzania limefanya kazi kubwa sana kuhakikisha kuwa nchi zetu za Bara la Afrika zinapata ukombozi kwa kukaribisha hapa wanaharakati wao kuja kuweka mikakati ya kwenda kukomboa nchi zao na nchi nyingi zimefanikiwa. Mkakati huu ulisimamiwa sana na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye pia alikuwa na ndoto ya kuona Afrika imejitawala na tunaiona imefikiwa, Bara la Afrika kwa kweli sasa hivi kila nchi imejitawala yenyewe na inaendelea na shughuli zake.

Mheshimiwa Spika, sasa maeneo yaliyotumiwa na hawa wapigania uhuru kwenye nchi yetu ikiwemo na Kongwa kama alivyosema lakini pia Dakawa, Wilaya ya Kilosa, pale Mazimbu Morogoro hata kule Nachingwea Mkoani Lindi yametoa mchango mkubwa sana ya ukombozi wa maeneo ambayo wapigania uhuru walikuja hapa. Maeneo haya namna ambavyo yanaendelezwa hayana mchango mkubwa sana kutoka kwao lakini tunaendelea kufanya mawasiliano nao kwa utaratibu ule wa kujenga mahusiano na nchi hizi.

Mheshimiwa Spika, bado tuna mahusiano na nchi zote ambazo zimepata uhuru kwa kuwa na wapigania uhuru wao hapa nchini na wao wanatambua mchango huu ingawa mchango wa kuboresha maeneo haya si mkubwa sana kwa sababu ya kubadilika kwa vizazi kwenye nchi zao na kutambua umuhimu wa Tanzania kwenye ushiriki wa ukombozi wa nchi zao. Hata hivyo, tumeimarisha sana kwenye sekta ya kiuchumi, kisiasa lakini pia kijamii pale ambapo tumefungua Balozi kwenye nchi zao, tunayo mawasiliano na nchi nyingi zipo kwenye Jumuiya ya SADC ambayo pia tunakutana mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya viongozi wa nchi hizo wanapokuja Tanzania wanapata hamu ya kwenda kutembelea maeneo haya. Wote mnakumbuka mwaka 2020 kulikuwa na Mkutano wa SADC hapa na Mheshimiwa Rais Ramaphosa miongoni mwa Marais waliokuja, alipata nafasi ya kwenda Mazimbu na mimi niliandamana naye kwenda kuona eneo lile na akaambiwa changamoto zilizopo pale na ahadi ambazo amezitoa. Tunaamini viongozi hawa ambao bado wana kumbukumbu sahihi na kuona uthamani wa Tanzania kwenye uhuru wao wataendelea kuutambua mchango wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini na sisi tunayo namna ya kuwakumbusha, tunapokuwa na matukio tunawakumbusha na wao wakiwa na matukio yao ya uhuru wanakumbuka nchi yetu Tanzania. Ni vile utofauti sasa wa yule aliyeshiriki kwenye ukombozi namna alivyokuwa anathamini nchi yetu; wote mnakumbuka Mheshimiwa Mandela alipotoka gerezani nchi ya kwanza kuitembelea ilikuwa Tanzania, hii ni kwa sababu alikuwa anajua umuhimu wa Tanzania na uhuru uliopo sasa Afrika Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatarajia pia na Marais wengine kupitia taratibu zetu za Kidiplomasia wataendelea kuitambua nchi yetu na maeneo ambayo wamepatia uhuru kwa kuungana na maeneo hayo kuyaboresha na kuweza kuyafanya kuwa endelevu kama maeneo ya kumbukumbu kwao na sisi pia. Kwa hiyo, tunaendelea kushirikiana na nchi hizo ili kujenga mahusiano ya karibu zaidi kwa Bara la Afrika. Ahsante sana. (Makofi)