Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Ally Mohamed Kassinge (4 total)

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata fursa hii ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mradi wa kuchakata gesi unaofanywa katika eneo la Likong’o, Mkoani Lindi ni miongoni mwa miradi ya kimkakati ambayo imekusudia kuinua fursa za kiuchumi katika ukanda wa Kusini na Tanzania kwa ujumla. Nini maelezo ya Serikali kuhusiana na hatua iliyofikiwa ya mradi huu mpaka hivi sasa na Watanzania watarajie nini kutokana na mradi huu. Ahsante sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna mradi huu mkubwa wa kimkakati wa LNG ambao uko Mkoani Lindi na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Kassinge anauliza swali na anayejibu ni mnufaika nambari moja. Mradi huu hatua tuliyofikia sasa ni nzuri, kwa sababu tayari TPDC wameshiriki kikamilifu kwenye hatua zote za awali ikiwemo na kulipa fidia wananchi wote waliokuwa kwenye eneo lile, wote wameshaondoka. Eneo lile sasa linaandaliwa kulima barabara mbalimbali huko ili kuligawa kwenye plots zile ambazo huduma mbalimbali zitatolewa makazi, sehemu ya kuweka mitambo na maeneo ya utoaji wa huduma nyingine.

Mheshimiwa Spika, hatua nyingine muhimu zaidi ni ya majadiliano ambayo Wizara ya Nishati kupitia Waziri aliyepo sasa ameshaanzisha hiyo timu na wako Arusha kwa sasa wanaendelea ku-negotiate, kufanya majadiliano na yale makampuni. Makampuni yenyewe yako kama manne ambayo yameonesha nia ya kwenda kuwekeza pale eneo la Likong’o pale Mkoani Lindi kwa ajili ya kuchakata gesi.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ambao pia utaleta faida kwa Watanzania wote, tumeenda kuwahamasisha, nilikuwa ziarani Mkoani Lindi wiki mbili, tatu zilizopita. Nimetembelea eneo lile la huu mradi, nimekutana na wananchi na nimewaambia wananchi wajipange sasa kunufaika na huo mradi. Kutakuwa na mambo mengi, watakuja watu wengi, kutakuwa na shughuli nyingi, watu wajikite kwenye kilimo, walime mazao yatakayoweza kuuza, watu wafuge watauza, lakini na huduma nyingine hoteli na nyumba za kulala wageni, ziandaliwe. Hizo ndiyo fursa ambazo tunazipata kwa kuwa na miradi mikubwa ya kimkakati kama wa LNG.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Watanzania wategemee mafanikio makubwa kwa mradi huu ambao tayari mchakato wake unaenda katika hatua nzuri ya kwenda kuanza uchimbaji, uanzaji wa kuchimba na kuwekeza kwenye mradi huo. Kwa hiyo kwa ujumla wake miongoni mwa miradi mikubwa nchini ambayo pia ni ya kimkakati umo na mradi huu ambao utatengeneza fursa nyingi ikiwemo na ajira kwa Watanzania wote, kwa Watanzania wale ambao watapata nafasi ya kuajiriwa kwenye eneo lile. Hizo ndiyo fursa ambazo zinatarajiwa na Watanzania kupatikana kupitia mradi huo. Ahsante sana.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Swali litajikita katika eneo la zoezi la utambuzi wa mifugo kwa kutumia hereni za kielektroniki.

Mheshimiwa Spika, ninafahamu kwamba Serikali ilipoanzisha zoezi hili ilikuwa na nia njema kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameieleza lakini sisi wananchi pamoja na hayo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameyaeleza tunatambua pia kwamba zoezi hili lingepunguza kwa kiwango kikubwa migogoro ya wafugaji dhidi ya watumiaji wengine wa ardhi, kwa sababu mifugo ingekuwa imetambuliwa.

Mheshimiwa Spika, sasa wakati Serikali imesitisha zoezi hili ili iweze kufanya tathmini kwa miezi mitatu; nini mkakati wa Serikali wa muda mfupi na wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba uingizaji holela wa mifugo hautoendelea na hautoweza kuathiri na kuleta migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba yako matatizo kwenye sekta ya ufugaji ambapo kwa sasa tunaona kuzagaa holela kwa mifugo yetu, lakini pia mifugo mingi kuingizwa kwenye vyanzo vilivyohifadhiwa kisheria na kusababisha madhara mengine kama ambavyo sasa tumeona vyanzo vingi vinakauka.

Mheshimiwa Spika, kusitisha kwa miezi mitatu kutaiwezesha Wizara sasa kuweka mkakati thabiti kwanza kuhakikisha kwamba wanakutana na wadau na kuelimisha namna nzuri ya ufugaji kisasa kama alivyotamka kwenye taarifa; na pili, kushirikisha mamlaka za Serikali za Mitaa kwa maana ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kutambua maeneo yote yenye mifugo na mipaka yao ili sasa lengo la kuweka hereni ambapo moja kati ya malengo ya kuweka hereni yaliyokusudiwa ni kuhakikisha kwamba tunapunguza kuhamahama kwa mifugo hii kiholela kutoka eneo moja mpaka eneo lingine, kwa sababu hereni inatambulisha mahali mfugo ulipo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa utaratibu huu tutakuja kujipanga vizuri na kesho kutwa tuna kikao cha Mawaziri wote wenye sekta zinazohusu mifugo, maji, mazingira pamoja na ardhi, pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa hapa Dodoma kuweka mkakati wa kudhibiti hali hiyo. Hiyo ndiyo moja kati ya njia ambayo tumeamua ili tuweze kufikia hatua nzuri ya kuelimisha pia na wafugaji umuhimu wa kufuga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo mnakumbuka wakati tunaendesha zoezi la wanaohama kwa hiari Ngorongoro, na watu wa Loliondo kupisha lile eneo na kuwaweka mahali pazuri na upimaji wa vijiji vyao, tuliiagiza Wizara itumie vizuri eneo la Msomera kuwa ni eneo la ufugaji kisasa la kimkakati kama pilot area ili wafugaji wengine wapate kujifunza kutoka Msomera.

Mheshimiwa Spika, wakati Wizara inaendelea na zoezi hilo la kuratibu vizuri pale Msomera, tunataka sasa mfumo huo uhamie kwenye Halmashauri nyingine zote nchini ili ufugaji sasa uwe na tija, wafugaji watambulike, mifugo tuitambue, tuwasaidie kutohama kwa umbali mrefu unaosababisha mifugo kupata shida, kutafuta malisho na huku Serikali ikijipanga kujenga maeneo ya kunyweshea na majosho. Huo ndiyo mkakati wa Serikali.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kutokana na taarifa iliyowasilishwa. Kwa mujibu wa waraka ambao unaelekeza adhabu za viboko kwa wanafunzi wenye utovu wa nidhamu, viboko visizidi vinne na ameidhinishwa Mwalimu Mkuu au Mkuu wa Shule au atakayeidhinishwa na wakuu hao kutoa adhabu hiyo. Kutokana na usimamizi au udhibiti ambao hauko sawa, imebainika taharuki kama ambavyo imejiri hivi karibuni.

Je, kwanini Serikali isirekebishe waraka huu na kuongeza kwamba wakati aliyeidhinishwa kama ni Mkuu wa Shule au mwingine aliyeidhinishwa anatoa adhabu kukawa na Kamati maalum ya usimamizi na kubariki adhabu hiyo ili kuondokana na taharuki kama hizi? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli waraka wetu wa elimu umetoa maelezo thabiti ya namna ya utoaji wa adhabu shuleni, kama nilivyosema kwenye maelezo yangu, adhabu ya viboko ni moja kati ya adhabu zinazotumika katika kumjenga mtoto na kumfanya aweze kutii sheria za shuleni na viboko visizidi vinne. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa uundwaji wa Kamati Shule zote za Msingi zina Kamati ya Shule, na Shule zote za Sekondari zina Bodi ya Shule. Pale ambako mwanafunzi hufanya kosa kubwa kuliko haya makosa madogo madogo basi mtoto huyo, kwanza hatua inayochukuliwa mzazi kuitwa kujulishwa tabia na mwenendo wa mtoto huyo ili sasa kumshirikisha mzazi katika kumjenga mtoto kinidhamu. Mbili, pale ambako adhabu hiyo inahitaji kumfukuza shule unashirikisha sasa Kamati ya Shule. Kwa hiyo, utaratibu wa utoaji adhabu umewekwa vizuri kabisa na ndiyo ambao unafuatwa mashuleni. Hili ambalo limejitokeza hivi karibuni ni tatizo la mmoja kati ya watumishi wengi kutenda bila kufuata utaratibu lakini siyo utaratibu ambao umewekwa na siyo ambao unatumika kwenye maeneo mengi. Ahsante sana.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu Serikali imekuwa ikitekeleza sera yake ya elimu bila malipo au maarufu kama elimu bure kwa misingi ya kuwapunguzia gharama wazazi au walezi wa vijana ambao wanasoma katika shule zetu za sekondari hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado kumekuwa na michango kadhaa katika shule zetu za umma, ikiwemo michango ya ulinzi, shajara pamoja na chakula;

Je, Serikali haioni umuhimu wa kupitia upya sera hii ili hii michango ambayo nimeainisha ambayo kimsingi inabebwa na wazazi au walezi iwe ni jukumu la Serikali kwa dhana ile ile ya kuwapunguzia gharama wazazi au walezi wa vijana wetu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini na mkuu wa wilaya mstaafu kama ifuatavyo: - (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza Sera ya Elimu bila Bila Ada kwa lengo la kuwaondolea adha wazazi ya kuwa na michango mingi na ile michango holela, michango holela. Kila mwezi Serikali yetu inapeleka fedha kwenye halmashauri kwa ajili ya kuwezesha shule zetu za Sekondari, wale wakuu wa shule na uongozi wa shule kuweza kutumia kwenye maeneo ambayo walikuwa wanatarajia sana kupata michango kutoka kwa wazazi ili wazazi wasichangie maeneo hayo na badala yake wazazi waendelee kusimamia maboresho ya mtoto mwenyewe kwenda shule kwa kumnunulia sare, viatu na vitu vingine.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba si maeneo yote yameweza kupata fedha hii hasa eneo la chakula na ulinzi, kama ulivyoeleza. Maeneo haya ambayo tumetolea fedha ni yale maeneo ambayo yanafanya ukarabati mdogo mdogo wa majengo yanayoharibika, vifaa vya kufundishia na kujifunzia, vitabu, chaki na vitu vingine ili kuondoa adha ya waalimu kuwachangisha wazazi fedha.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo sasa tunaendelea kushughulika nalo ni maboresho sasa. Tunazo shule nyingi za sekondari ambazo wanafunzi wanaenda asubuhi na kurudi jioni na wanapokuwa shule hawapati chakula. Nikiri kwamba eneo hili Serikali bado tunaendelea kuchakata ili tuone namna nzuri ya kutoa huduma ya chakula shuleni; ingawa tumeona sekta binafsi zinashiriki, wakati mwingine wazazi wenyewe wanaweka mpango wao.

Mheshimiwa Spika, sasa, niliposema michango holela; Tunayo ile michango holela ambayo labda waalimu wanasema njoo kesho na shilingi mia mbili, elfu moja, mia tano, ambazo zinakera kwa wazazi. Hiyo tumeidhibiti na tumepiga marufuku na haipo kabisa na kama ipo, tumeshatoa maelekezo na hapa pia nitatoa maelekezo. Sisi tunaruhusu michango rasmi inayokwenda kufanya shughuli za maendeleo. Shule za msingi, shule za sekondari hizi ni shule za wananchi. Kila kijiji kina shule ya msingi na kinasimamiwa na kijiji chenyewe, na tumeunda kamati ya shule kwa shule za msingi. Sekondari ziko kwenye kata, tumeunda bodi ya shule na inamilikiwa na kata kwenye vijiji vitatu, vinne au vitano, wanasimamia na Mtendaji wa Kata ndio kiongozi wetu anayesimamia maendeleo ya shule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inapotokea labda choo kimebomoka hatuzuii wazazi kukaa na kukijenga kwa kuchangia na kujenga hiyo ni michango ya maendeleo. Ingawa michango hii pia tumeiwekea masharti kidogo kwamba anayetakiwa kusimamia michango hii ni mkuu wa wilaya pekee au yeyote ambaye mkuu wa wilaya amemchagua kusimamia. Tunaogopa sasa watu kuchangisha kule holela na ndiyo kwa sababu nilisema michango holela. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi Serikali inaendelea kufanya mapitio ya sera hii ili kuwezesha mzazi kupata unafuu zaidi wa kutoa michango kwa ajili ya maboresho ya shule zetu. Lakini pia bado hatuondoi nafasi ya uwajibikaji wa wananchi kwenye shule zao katika kufanya maboresho. Na niliposema mkuu wa wilaya mstaafu najua hili umelisimamia vizuri sana ulipokuwa mkuu wa wilaya kabla hujawa Mbunge na kwa hiyo Serikali tunaendelea kusimamia haya.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa wakuu wa wilaya wote nchini, kwenye halmashauri zao kusimamia kutokuwepo kwa michango holela inayokera wananchi na kushindwa kufanya shughuli nyingine na badala yake kuwa wanasababisha wanafunzi wanaondolewa shuleni; hiyo tulishapiga marufuku kabisa. Lakini pia Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kwamba wanatuhudumia hizi shule lakini na kuweka mpango mzuri kwenye maeneo ambayo yanahitaji pia Halmasjhauri isimamie kupitia bajeti zao, kama ni lazima kuzungumza na wazazi lakini wazazi wenyewe kupitia kamati zao wafanye maamuzi haya ndiyo ambayo kwa sasa tunayasimamia. Lakini niwahakikishie tu kwamba ombi la Mheshimiwa Mbunge la kufanya maboresho ya sera yetu hayo tumepokea na tunayafanyia kazi, ahsante sana. (Makofi)