Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile (8 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Mpango wa Serikali. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia na mimi kuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nikishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi ya kuwa mgombea na hatimaye kuchaguliwa na wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwa kura nyingi za kishindo.

Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mwenyekiti wetu wa chama kwa kazi kubwa aliyoifanya akisaidia na Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wamezunguka nchi nzima kunadi Ilani ya CCM wakishirikiana na viongozi wetu waandamizi wa chama na hatimaye Wabunge wengi tukarudi ndani ya Bunge, wengine kwa mara ya kwanza kwa kishindo kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawashukuru sana. Wengi tumeingia ni kwa matumizi hayo, kwa harakati hizo za viongozi wetu wakuu, lakini zaidi ya hayo kutokana na kazi nzuri iliyofanywa ya kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na comrade wetu, jemdari wetu, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Pamoja na kazi hiyo nzuri, pamoja na pongezi hizo ambazo nimempatia Mheshimiwa Rais, sasa nijielekeze kuchangia kwenye Mpango huu wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye halmashauri nyingi ikiwemo ile ambako mimi natokea, uchumi wetu ni kilimo. Pamoja na Serikali imeelekeza hapa maelekezo yake kwamba, itawekeza zaidi na kuimarisha upatikanaji wa pembejeo, bado nishauri kuna migogoro mingi ambayo iko kwenye maeneo mengi na hasa wafugaji na wakulima. Nikitolea mfano kwa Jimbo langu la Nachingwea kuna mwingiliano mkubwa baina ya wafugaji na wakulima. Niishauri Serikali tutenge maeneo maalum yatakayowawezesha wafugaji kwenda kukaa kwenye eneo ambalo sasa litakuwa na miundombinu yote kwa maana ya maji na malisho badala ya kufanya ufugaji wa sasa wa kuhamahama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tunapokuwa tunazungumzia kilimo ni eneo mtambuka, wakulima wetu wengi wanalima kilimo cha kizamani sana, wanatumia jembe la mkono. Kwa kweli katika hili niiombe sana Serikali iwekeze vya kutosha ili wakulima wetu waondokane na kilimo kile cha kizamani, waende sasa kuingia kwenye kilimo cha kisasa. Katika eneo hilo basi tuongeze kwenye rasilimali watu kwa maana ya wale wataalamu wetu wa kilimo waende zaidi kwenye vijiji vyetu, wakatoe elimu zaidi na kuwasaidia wakulima wetu ili waweze kulima kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania yetu ni Tajiri, tuna madini, lakini tuna maliasili ya kila namna, Mwenyezi Mungu ametujalia sana. Katika hili yako maeneo ambayo bado hatujayafanyia kazi kwa upande wa madini. Nikitolea mfano kule kwetu eneo la Nditi, Kiegeyi, bado tumeomba vibali, tumeomba leseni ya uchimbaji kwenye maeneo yale, lakini bado Wizara haijatilia mkazo . Nashukuru Mungu nilizungumza na Mheshimiwa Waziri wa Madini akaniahidi atatembelea kule Nachingwea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii Ofisi ya Rais TAMISEMI. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza pia dada yangu Waziri Mheshimiwa Ummy na Naibu Mawaziri kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuongoza Wizara hizo. Natambua kazi nzuri inayofanywa na Wizara hii ya TAMISEMI kwenye sehemu ya elimu, afya mmefanya kazi kweli kweli tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, lakini hata hivyo, wacha nizungumzie kidogo suala la TARURA. Ukiona mtu mzima analia kwakweli kuna jambo. Kwenye suala la TARURA Waheshimiwa Wabunge wengi kila anayesimama analia kuhusu TARURA, TARURA shida, changamoto.

Katika hili niiombe sana Serikali waone namna watakavyokuja na muarobaini kuhusu TARURA. Lakini TARURA hii nitaizungumzia kwenye maeneo mawili, la kwanza kwenye muundo wenyewe wa TARURA. Yuko mtu anaitwa mratibu anakaa pale Mkoani, yeye ndiyo anafanya kila kitu, tender anatoa yeye na kila kitu. Sasa tumemuacha huyu meneja ambaye yuko Jimboni, wilayani ambaye anajua sasa barabara gani ni kipaumbele, yuko hana shughuli yoyote na hata tukizungumzia kwamba anashauri kule mkoani bado anayeshauriwa ana mambo mawili, kukubali au kukataa huo ushauri. Siku ya siku bado mkoani ndiyo wenye mamlaka ya kuongeza wapi kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ukosefu wa hii bajeti. Kwa kweli mimi niiombe sana Serikali, dada yangu Ummy najua ni mchapakazi sana. Mheshimiwa hebu njoo na muarobaini kuhusu TARURA ni namna gani tunaweza tukaongeza mapato yatakayotuwezesha kufanya kazi kwenye sehemu hii ya TARURA, nikuombe sana na naamini hili kwa uchapakazi wenu kwa uzuri kama mlivyofanya vizuri kwenye maeneo mengine ambayo nimewapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia kuhusu watumishi hasa watumishi wa afya na walimu. Huko nako ni shida, sisi tunaotoka pembezoni mwa nchi, hawa watumishi huwa wanaomba maombi ya moja kwa moja kwenda kwenye maeneo yale kwa ajili ya kupata cheque number tu lakini baada ya hapo wote wanaomba kuondoka kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Wizara, hebu tuwe na mpango maksudi wa kuhakikisha kwamba hao wanaoomba kwenye maeneo yale kwakweli wanakwenda wakiwa na ari ya kufanya kazi na sio tu kwenda kwenye maeneo yale kwa ajili ya kuchukua cheque number. Hapo hapo niendelee pia kushauri Wizara kwamba basi tuwape kipaumbele, wako vijana ambao wametoka na wana-apply kutoka kwenye maeneo yale wameshayazoea. Hebu tuwape kipaumbele, sizungumzii kwamba wale wengine wasipate nafasi, la hasha lakini basi tuone mpango ambao utatuwezesha na sisi tulioko pembezoni mwa nchi kuweza kupata watumishi ambao kwa kweli watakuwa na ari ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine nizungumzie kwenye maboma. Maboma haya yako maboma ya zahanati lakini pia maboma ya shule za msingi na sekondari. Hebu tuuone huu mpango mkakati, kabla ya kuendelea na vipaumbele vipya tuone mpango mahsusi wa kwenda kumalizia haya maboma. Lakini tukifanya hivyo twende sambamba sasa na kuhakikisha vituo vyetu, shule zetu zinakwenda sasa kupata watumishi wa kutosha na hapo niende kule kwangu kwenye jimbo langu la Nachingwea, kuna kituo chetu cha afya Kilimarondo. Mheshimiwa Waziri ikikupendeza, ukipata nafasi twende utembelee eneo lile. Daktari yupo lakini pia na watumishi wengi wapo lakini hawatoshelezi. Eneo lile ni mbali kabisa kutoka Makao Makuu ya wilaya. Tuone namna maeneo yale tunavyoweza kuyapa kipaumbele ili basi waweze kupata watumishi watakaokidhi kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuzungumzia pia suala la Posi, zile mashine za kukusanyia mapato. Huko nako iko shida. Wataalam wetu walio wengi haawana ufahamu wa kutosha na hasa kwenye zile kata. Tujikite kutoa elimu namna gani ya kutumia zile mashine kwa ajili ya kukusanya mapato.

Mheshimiwa Spika, kinachotokea, kwa sababu maeneo mengine wako waliopata shoti kwa namna hii mashine ile hawezi kuitumia vizuri. Badala yake sasa wakati wa kutoa ripoti anakuta anachotakiwa kuwasilisha ni kikubwa kuliko alichonacho. Kinachotokea sasa wanafunika zile posi, anaiweka pembeni anaendelea. Sasa tuwe na mpango huo wa kutoa elimu kwa hawa wataalam wetu kule chini, tunajua wengine hawana taaluma hiyo ya uhasibu. Basi tuwape walau zile kozi ambazo zitawawezesha kupata ujuzi huo. Lakini pia kuhakikisha tunafuatilia kadri inavyowezekana, kadri tunavyopata muda ili mapato yanakusanywa kisawasawa. Kuna mapato mengi yanapotea na nina hakika tukiimarisha kwenye eneo hilo kwa kweli tutafanya vizuri kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako vijana wengi ambao kwa kweli wanalia. Nikionesha hapa message za simu za kila Mbunge hakuna atakayekuwa anasema mimi sina message ya kijana kutoka kwenye Jimbo langu hana ajira. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, tunajua kwamba kipato chetu tunachokusanya ndicho kinachokwenda kuajiri vijana au ajira mpya. Tuone namna ya kuongeza ajira, vijana wetu wako wasomi, wako huko mashambani, vijijini wanao ujuzi wa kutosha. Tuone namna ya kuwatumia hawa kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado niendelee kuzungumzia tena wale walimu au watumishi wanaotoka kutoka maeneo mengine kuhitaji kuhamia maeneo mengine hebu tujaribu namna ya kuyaona hapa. Mheshimiwa Waziri wako watumishi ambao wanataka kutoka Tanga kwenda Nachingwea mahali ambapo tuna shida ya watumishi sasa process zile zinazotumika ili huyu mfanyakazi kurudi kule ambako moyo wake unatamani ni shida.

SPIKA: Ahsante Mheshimia Chinguile.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona na kunipa nafasi na mimi nichangie Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nami niwashukuru sana viongozi wetu wa Wizara, kwa kweli Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri vijana mnatuheshimisha sana kwa sababu mnachapa kazi nzuri. Kwa kweli hii inaonesha kwamba vijana wakipewa nafasi wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo, yako maeneo ambayo na mimi nitayazungumzia kwa jimbo langu; kuna Vijiji vya Namanga, Rweje, Mchangani pamoja na Kiegei, Matekwe na Nakilimalono. Maeneo haya tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika na vibali kwa ajili ya uendeshaji wa miradi ya maji kwenye maeneo haya tayari vilishatoka lakini kwa bahati mbaya sana maeneo haya hayajapelekewa fedha. Naomba sana wakati anahitimisha hotuba yake aseme lolote kwa ajili ya maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, ukitoka Nachingwea Mjini kuelekea Liwale ni kilometa 5 tu, ukipita nyakati za usiku utakuta moto unawaka siyo wachawi, hawa ni kinamama ambao wanahangaika kuhamia maji, inasikitisha! Maeneo hayo sisi tunakua hali iko hivyo mpaka sasa hali iko hivyo.

SPIKA: Kuhamia maji ndio nini?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, wanakwenda kwa ajili ya kusubiria maji kwenye vile visima vidogo vidogo. Sijui Kiswahili chake rahisi niseme nini lakini kwa kweli ni kuhemea lakini kwa kweli wana shida kwenye maeneo haya. Hata ukizungumzia kama kuna mafanikio ya maji yamepatikana maeneo haya ni lazima uangalie kushoto, kulia maana hawatakuelewa. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na juhudi zote ambazo amezifanya maeneo haya kwa kweli yapewe kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo ya Matekwe yana mabwawa ambayo yalichimbwa maalum kabisa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji lakini mpaka leo kazi ile mahsusi iliyokusudiwa kwenye mabwawa haya haijatekelezwa. Niishauri Wizara badala ya kusubiri mradi huu ambao hatujui utaanza lini wafikirie namna ya kutuma wataalam ili waone maji haya yanapoweza kutumika kwa matumizi ya kunywa kwenye maeneo husika. Maeneo haya ni mbali na maeneo ya mjini, kwa kweli sio tu wanakunywa maji machafu lakini wanakunywa maji ambayo mbuzi, ng’ombe, tembo na wanyama wengine wanatumia. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara ipigie mstari wa huruma kabisa kwenye maeneo haya ili wapiga kura wangu wa Jimbo lile la Nachingwea waweze kufaidika pia na miradi hii.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa maji wa kutoka Masasi kuja Nachingwea lakini kupitia kwenye Kata ya Ndomoni, nashukuru Ndomoni maji yamefika. Hata hivyo, kwenye kata hiyo hiyo kuna eneo lingine ambalo lina watu wengi la Ndomondo na Makitikiti. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na mafanikio haya ya mradi huu kuufikisha hapa, aone namna ambavyo atawapelekea maji watu wa maeneo haya ya Ndomondo na Makitikiti. Kwa sasa wanakwenda kilometa nyingi kutafuta maji na hii sasa kwa wale ambao kwa kweli wameoa ni shida. Wapo watu ambao sasa wamekuwa na mapengo baada ya kupewa vipigo na wanaume zao maana anaondoka asubuhi anarudi saa 8 na hii si sawa.

Mheshimiwa Spika, uko mradi wa maji wa Mbwinji umefika Nachingwea, naishukuru sana Serikali lakini tunahitaji huu mradi utanuke kwenye baadhi ya maeneo. Najua Mheshimiwa Waziri anaufahamu vizuri hebu atusaidie ili watu wengi zaidi waweze kupata maji haya safi na salama kutoka kwenye mradi huu wa Mbwinji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, yako maeneo ambayo wenzetu wa TASAF walishachimba visima vya maji sasa yamebaki mashimo. Namwomba sana Waziri akipata muda twende Nachingwea tukaone maeneo haya, vile visima havijawahi kutoa maji hata siku moja. Tulichoshuhudia ni wale wataalam wa maji waliokuja kuchimba vile visima wametuachia mashimo lakini sio hivyo tu, wametuachia na wapwa zetu kule jimboni. Hatukuhitaji wapwa, sisi tumehitaji maji! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya nayazungumza kwa uchungu kwa sababu yako mashimo, unafika kijijini unakuta mashimo manne matano na yote hayajatoa maji. Hii ni hasara kwa Serikali. Waziri naomba twende kwa pamoja tujue ni nini kilichotokea maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, najua huu muda umenipa wa ziada lakini kwa kweli inasikitisha sana ningepata muda mrefu ningezungumza mambo mengi ungejiuliza haya mambo yanafanyika Tanzania au lah! Nimuombe Waziri tukiambatana pamoja na mimi kwa kweli atakwenda kujionea mwenyewe. Haya mambo yapo, pamoja na kuwasifu kwa kweli mnafanya kazi nzuri twende tukakamilishe kazi hii ambayo kwa kweli taifa linatutegemea sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa zawadi ya uhai. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwa namna wanavyonipa ushirikiano tangu wamenichagua kuwa Mbunge wao na nawaahidi sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu kwa Wizara hii ya Afya. Tunayo changamoto ya watumishi wa afya, kwa mfano kwenye Halmashauri yangu ya Jimbo la Nachingwea, mahitaji ni watumishi 1,077 na waliopo ni 305, upungufu ni 772, hatuwezi kufanya kazi kwa namna hii.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hiyo nichukue nafasi hii kuwapongeza sana watumishi wa afya wa Jimbo la Nachingwea kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na upungufu wao huo. Mahitaji ya Hospitali ya Wilaya ya Nachingwea ni watumishi 256. Mpaka sasa wako 169, sasa hawa 136 wanakwenda sasa kugawana kwenye zahanati 35 na vituo vya afya vitatu, haiwezekani! Niiombe sana Wizara kwenye hili waone namna watakavyokuja na mpango wa kutatua changamoto hii ya watumishi wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru sana Wizara walitujengea jengo zuri pale walituletea milioni zaidi ya 400 kwa ajili ya jengo zuri la Mama na Mtoto kwenye Hospitali yetu ya Wilaya ya Nachingwea. Pia walituletea milioni 200 kwa ujenzi wa Kituo cha Afya cha Naipanga, nawashukuru sana. Pamoja na shukrani hizi jengo lile la mama na mtoto ni zuri, lakini mpango wake ni kupatikana kila Idara, Idara ya upasuaji jengo ni tupu halina kifaa hata kimoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Wizara na nimezungumza mara kadhaa na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wameniahidi, lakini basi angalau wakija kuhitimisha waseme lolote ili wananchi wale wa Jimbo la Nachingwea waweze kupata faraja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo changamoto ya ambulance. Ambulance tunayoitegemea sasa ni ya Kituo cha Afya Kilimarondwa ambacho ni kilometa 96 kutoka kwenye Hospitali ya Wilaya. Ile ambulance ya wilaya pale ni mbovu haiwezi tena kuendelea na kazi. Sasa tufikirie kwamba ambulance inatoka kilometa 96 inakuja kutoa huduma katikati ya Wilaya ambapo ni umbali na barabara ni ya vumbi. Kwa kweli Wizara ione namna itakavyotusaidia kwenye Jimbo hili la Nachingwea ili na sisi tupate ambulance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote niendelee kuishauri Wizara, wenzangu wamesema hapa, sasa hivi tunalo ongezeko kubwa sana la magonjwa ya saratani na hasa ya shingo ya kizazi, lakini pia na magonjwa ya ini. Hebu tuone namna ambavyo wataalam wanaweza kufanya utafiti ili kubaini chanzo cha ongezeko la magonjwa haya kwa sasa ni nini, ili basi tuweze kutoa elimu kwa wananchi wetu na kwa hiyo tutapunguza wagonjwa wanaohitaji sasa kupata huduma kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze zaidi kwenye magonjwa ya malaria kipindi kilichopita tuliendelea kutoa elimu kubwa sana kwenye magonjwa haya kupambana na ugonjwa huu wa malaria. Sasa ni kana kwamba tumepunguza speed, niiombe Wizara turudi, kulikuwa na mipango hapa ya kugawa neti na vitu vingine, ile mipango bado iwe endelevu. Yapo maeneo ambayo kama hatutapeleka elimu ya kutosha bado wananchi wetu ni kana kwamba wanasahau.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, pamoja na kazi nzuri inayofanywa na wizara yetu ya Ujenzi, nichangie kwenye eneo la barabara ya Kibiti - Lindi, barabara hii haina muda mrefu lakini kwa sasa ina maeneo korofi kweli kweli niombe wizara ifanye kadri inavyoweza ili yapitie maeneo haya na kuyarekebisha mara moja. Maeneo haya Mbwemkuru, Malendego mpaka Nangulukuru kipande hiki ni kibovu kweli kweli na kinaweza kikasababisha ajali endapo hazijachukuliwa hatua za makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninzungumzie eneo la barabara za kutoka Nangulukuru kwenda Liwale, Liwale – Nachingwea, Nachingwea – Ruangwa, Ruangwa - Nangulukuru. Maeneo haya yamedumaa kwa sababu pamoja na mambo mengine ni hali ya barabara ya maeneo haya, tukijengewa barabara maeneo haya hata kiuchumi yatakwenda kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa masikitiko makubwa niendelee kusema tu kwamba maeneo haya tunazalisha korosho kwa wingi, tunazalisha ufuta kwa wingi, lakini barabara zake ni mahandaki. Niombe sana sana wizara iweke upendeleo maalumu kabisa. Mheshimiwa Mbunge wa Liwale hapa amezungumza, amezungumza jana tena kwa hisia kali kabisa, kwa kweli ipendeze baada ya Bunge hili au wakati Bunge linaendelea Mheshimiwa Waziri aende akatembelee haya maeneo akajionee mwenyewe. tunachokizungumza tunamaanisha watu wetu wanapata shida kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa unyenyekevu mkubwa nizungumzie kipande cha barabara kutoka Masasi kwenda Nachingwea. Wakati tunafunga kampeni za uchaguzi mwaka jana aliyekua Rais wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hayati alizungumza na wapiga kura wa Jimbo langu la Nachingwea kwa njia ya simu na kati ya vitu alivyowaahidi ni barabara hii ya Nachingwea kwenda Masasi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye kumbukumbu ya barabara hii upembuzi yakinifu umeshakamilika miaka mitano iliyopita, lakini mwaka 2016 ilitengewa shilingi bilioni moja kwa maana ya kishika kasima hakuna kilichoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumi na saba kumi na nane ilitengewa bilioni 3.5 hakuna kilichoendelea 2018/2019, 2019/ 2020 ikatengewa bilioni 1.3, 2020/2021 ikatengewa bilioni 1.4 mwaka huu imewekewa bilioni 1.5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Waziri atakapokuja kujibu hapa kwa kweli nitashika shilingi kama huna maelezo yatakayotoa matumaini ya lini barabara hii itajengwa, na kwenye hotuba yako huku nimeona Mheshimiwa Waziri amesema Serikali inaendelea na kutafuta pesa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii ya Masasi – Nachingwea.

Mheshimiwa Naibu Spika, imetafutwa kwa miaka mitano, upembuzi yakinifu na vitu vingine vimeshakamilika hebu tuchukuwe juhudi za makusudi kwa ajili ya watu wetu hawa. Watu hawa wanajuwa kujiletea maendeleo yao wenyewe lakini kama miundombinu ikiwa ni shida kwa kweli hii haikubaliki. Nitaishikilia shilingi hiyo Mheshimiwa Waziri mpaka mwisho ili nione unawatendea haki wananchi wa Jimbo langu la Nachingwea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nizungumzie pia changamoto nyingine ya kipande cha barabara nilichokizungumzia cha kutoka Nachingwea – Ruangwa. Tukumbuke Ruangwa yupo Mheshimiwa Waziri Mkuu anateremka Uwanja wa Ndege wa Nachingwea hii barabara ni mbovu. Naomba tufanye juhudi za makusudi ili kuwezesha hata viongozi wetu wakiwa wanateremka uwanja wa ndege waweze kutembea kwenye barabara ambazo kwa kweli watakuwa na usalama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara ya kutoka Masasi - Lindi ina matuta na mimi nafikiria hawa wakandarasi au wahandisi wetu walifikiria nini maana haya matuta ni makubwa kiasi ukiendesha speed hata kama ni 60 ukipita kwenye hilo tuta utapata ajali tu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsate sana, kengele imegonga.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa. Awali niunge mkono maoni ya Kamati zote mbili kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anafanya bidii ya kuhakikisha maisha bora ya Watanzania yanendelea kupatikana.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na timu yake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Wakati wamekuja mbele ya Kamati tuliendelea kuridhishwa sana na utekelezaji wa maazimio ya Bunge lako. Pia nimpongeze Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI na timu yake kwa kazi kubwa na nzuri, kwakweli kazi zinaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo ninanyongeza ya ushauri kwenye maeneo kadhaa kwa sababu maazimio haya na maoni ya Kamati na mimi ni sehemu yake.

Mheshimiwa Spika,najielekeza kwenye TARURA, tuendelee kuwapongeza, wenzetu TARURA wanafanya kazo kubwa na nzuri kwelikweli katika maeneo ya nchi yetu. Hata hivyo bado niendelee kuomba kwa Serikali waendelee kuwezeshwa kifedha, bajeti yao iongezwe na hasa kwenye eneo la dharula. Inapotokea Msimu wa mvua hali inakuwa ni ngumu na wanakuwa na kazi kubwa kwelikweli. Wakiwezeshwa wataendelea kuimarisha utoaji wa huduma, na kwa kweli miundo mbinu kwenye maeneo yetu itaendelea kuimarika.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hilo hilo la TARURA tuliendelea kushauri na bado naendelea kusisitiza kuishauri Serikali; bado eneo la manunuzi liendelee kusogezwa namna ambavyo itawezekana kufika kwenye eneo la Wilaya. Kwa namna ilivyo sasa hivi manunuzi na tendering hufanyiwa kwenye ngazi ya mkoa. Wale mameneja wa TARURA walioko kule wilayani kwenye halmashauri wanabaki kama PS, hawana mamlaka kwa hawa wakandarasi kwa kuwa tayari wamepewa tender kutoka huko mkoani. Sasa matokeo yake wanakosa namna ya kusimamiwa vizuri kule kwenye halmashauri; na hata sisi tulioko kule tunashindwa namna ya kuwasimamia vizuri. Lakini kazi inayofanyika na TARURA ni nzuri na wanaendelea kufanya kazi kwenye mazingira hayo.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoke hapo nijielekeze kwenye mradi wa ujenzi wa Shule za Sekondari. Niipongeze sana Serikali kwa uamuzi huu; na kweli hizi shule ni nzuri na zinapendeza. Hata ukifika kule kwenye jimbo langu la pembezoni la Nachingwea unakuta shule iliyojengwa kwa mradi huu wa SEQUIP inapendeza kweli kweli, tunaishukuru Serikali.

Mheshimiwa Spika, lakini bado na mimi niendelee kusisitiza kwenye eneo lile la gharama halisi ya hizi shule. Milioni 470 yako maeneo mengine huwezi kumaliza uhitaji wa hiyo shule. Bado tuendelee kuangalia kulingana na eneo. Huwezi kufananisha eneo la Dar Es Salaam na eneo la Nachingwea au kule Tunduru. Niiombe sana Serikali ipitie upya jambo hilo, na kama ni suala ambalo linaweza likarekebishika basi tuweze kupata ufumbuzi wa haraka.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye mchango tena kwenye Kamati ya Huduma. Nimepitia vizuri hapa, lakini yapo mapendekezo kadhaa na maoni ambayo Kamati wametoa. Ni ukweli usiopingika kwamba kwenye ukatili wa kijinsia wako baadhi ya wanaume na wenyewe wanapata kadhia hiyo. Kwa sababu ya kitamaduni ya Kiafrika na Kitanzania hatuna mahala pa kulalamika, yawezekana wengine tuko ndani humu lakikini hakuna anayeweza kutuzungumzia.

Mheshimiwa Spika, kwenye mapendekezo ya Kamati na mimi naomba nipendekeze nyongeza kwenye ukurasa wa 41(i) kuishauri Serikali, kufanya utafiti wa kina kujua nini chanzo cha ongezeko la ukatili wa kijinsia nchini hususani kwa wanawake na watoto. Hapa iongezwe na wanaume, kwa sababu tunachoshauri hapa ni kufanya utafiti. Kama bado wako wanaume ambao nao wanakumbwa na mazira haya tujue.

Mheshimiwa Spika, hii inaweza ikawa ni kichekesho lakini yapo. Wapo wanaopigwa, wapo wanaofungiwa na manyanyaso mengine kadha wa kadha. Lakini ugumu wa kujitokeza na kusema mimi nimefanyiwa haya mazira kwa sababu ya tamaduni zile zile za Kitanzania na Kiafrika tunashindwa kufanya hivyo. Lakini huo ndio uhalisia; na kwa sababu hapa tunachoshauri ni kwenda kufanya utafiti basi na hilo ipendeze liingie kwenye utafiti ili watuletee sasa tafiti zinasema nini. Hilo jambo lipo sawa basi kama halipo tutamshukuru Mungu, tutaendelea na lile lile kwamba wanawake na Watoto.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naendelea kurudia tena yale maoni ya Kamati na mimi ni sehemu yake. Kwa hiyo naunga mkono kwa asilimia mia moja. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai, lakini kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa ajili ya kuboresha maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu Waziri, Mheshimiwa Deo Ndejembi, kwa kweli, wanafanya kazi nzuri. Na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, yako mambo mengi tumewashauri, lakini tumejadiliananao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye upungufu wa watumishi. Kwenye Jimbo langu la Nachingwea kwa mfano, kwenye elimu ya msingi mahitaji ni watumishi 1,319 waliopo ni 788, upungufu ni 531. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu sekondari. Mahitaji ni 786, waliopo ni 412, mapungufu ni 374. Na afya vilevile nae neo la utawala kwa maana ya maafisa watendaji wa kijiji na wa kata. Eneo hili tulitolee macho kwa ukubwa wake na hasa maeneo haya ambayo ni mikoa ya mipakani, Lindi, Mtwara na maeneo mengine. Twendeni tuyape kipaumbele cha makusudi kabisa. Na hapa ndipo tunapokuja sasa kuona namna ambavyo wenzetu wanaoomba kwa mfumo huu wa mtandao akipangiwa kwenda Nachingwea anasema niko tayari, lakini akifika baada ya miezi mitatu, baada ya muda anasema sasa baba ni mzee kwelikweli, amezeeka baada ya mwaka mmoja? Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anachagua kwenda Nachingwea ni kwa sababu, nafasi iko Nachingwea, lakini akishapata check number basi anakumbuka sasa kumbe naweza nikaomba kwa sababu sheria ipo na inamruhusu yeye kuomba uhamisho baada ya muda fulani. Kwenye hili, mimi nishauri Serikali yangu, tuone namna ambavyo tutatoa kipaumbele kwa wale wenye sifa ya kufanya hizi kazi wanaotokea kwenye maeneo haya; na hii itatusaidia, wale vijana wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii imejaliwa wasomi kwelikweli katika kila kata, kila wilaya, wasomi, ma-graduate ni wengi kwelikweli wapo. Ni Serikali tu kuweka utaratibu mzuri wa kuwatumia hawa ma-graduate ili tusipate upungufu huu kwa sababu ya watumishi wengine kuhama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwa wale makaimu. Nilitoa taarifa hapa kwa Mbunge mwenzangu, sasa naona nilielekeze hilo. Kwa mfano, Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nachingwea ziko idara na vitengo vinne kuna makaimu, lakini kibaya zaidi yuko kaimu anakaimu zaidi ya miaka 11, hii haikubaliki. Sasa hapa utamleta sasa mtumishi ambaye wewe umeona ana sifa kutoka eneo lingine, huyu mtu nimesema hapa tunampa ugonjwa wa sonona, tunamsababishia pressure na magonjwa mengine yasiyoambukiza, hii si sawa. Na kama ni vetting tunamuacha miezi sita ya kisheria, anakwenda mwaka, anakwenda miaka miwili… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge ni vizuri hilo jina ulilosema anakaimu miaka 11 ukawapatia pia Mawaziri badae.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inapomletea sasa mkuu wa idara kutoka eneo jingine na yeye awe chini yake kwa kweli, unamuacha kwenye mazingira magumu sana huyu mtumishi. Hii si sawa na haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo yako nimeyapokea nitafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya wastaafu, kuna suala la uhakiki. Hili ni kizungumkuti, kila mwaka wanakwenda kuhakikiwa mkoani; ni jambo jema kuhakiki kama wazima au la, lakini suala la kutoka huko vijijini waliko kwenda mkoani jambo hili ni gumu na hawa wastaafu walio wengi hali zao ni ngumu kwelikweli. Hapa Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema… (Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Kuchauka.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa Taarifa muongeaji, hili suala la kwenda kuhakikiwa mkoani limekuwa ni janga kwelikweli. Mtu anatoka Kijiji kwa mfano Mpigamiti, kilometa zaidi ya 30, aje Liwale Mjini kilometa 50, atoke Liwale Mjini kwenda Lindi ambako ni kilometa 360. Huyo mstaafu huyo ana umri wa miaka 80 au mwingine ana miaka labda 75 hivi, unamtakia kweli maisha mema?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mzigo huu. Kwa hiyo, nampa Taarifa anachikisema ni sahihi kabisa kwamba, huu mzigo tunaubeba sisi Wabunge. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unapokea Taarifa?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii si sawa na bahati nzuri hao wastaafu walio wengi wamechoka sana. Tuone namna ya kuwawekea mazingira rahisi sehemu ambayo ya kuhakiki, wanaweza kufanya kule Halmashauri, lakini pia tunaweza tukaboresha kwa namna nyingine ambayo tunaona inafaa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwenye hizi ajira mpya zinazotolewa, hili nalo ni tatizo lingine. Tatizo sio kupata ajira, tunajua na tunaiheshimu sana mamlaka, na kwakweli kubwa zaidi niipongeze Serikali kwenye eneo hili kwa kutoa hizo ajira. Kazi kubwa hiyo mmefanya tunawashukuru, lakini ni namna gani hawa vijana wanakwenda kupata hizi kazi? Ni kizungumkuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na huu mfumo wa ajira kwa maana ya kuomba kwenye mtandao si Rafiki na hasa kwa wale vijana walioko vijijini. Huu mtandao una changamoto, unaweza ukakaa wiki nzima bado wewe unaendelea kuingia online na mtandao hausomi, badala yake hata muda wa kuomba hizo nafasi umeshapita. Tuone namna tutakavyowasaidia hawa vijana kweli wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako Wabunge hapa wamesema ni vizuri sasa tukaona mgawanyo mzuri kwa kutumia wilaya, majimbo, namna tutakavyoona inafaa ili kila kijana Mtanzania aweze kunufaika na hizi ajira zinazotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho, niwapongeze sana wenzetu wa TASAF na hasa kwenye ile miradi ambayo wameitekeleza, wanafanya kazi nzuri sana. Nimesema mimi ni mjumbe wa kamati na tumeona miradi mingi inapendeza kwelikweli; tumekwenda Zanzibar, kazi nzuri tumeiona. Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako ya TASAF mimi nawapongeza sana. Kazi hii nzuri iendelee, lakini pia sasa mtolee macho na maeneo mengine ambayo hamjafika kwenye miradi ya kimkakati ikiwemo kule Nachingwea, Liwale, Rwangwa na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mambo anayoitendea Tanzania tangu ameingia madarakani ni makubwa, nasi wote ni mashaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI, na kwenye hili nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa kazi nzuri, na speed hii aliyoanza nayo naamini Halmashauri zetu sasa ziko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Naibu Waziri Mheshimiwa Festo Dugange na Mheshimiwa Deo Ndejembi kwa kweli wamekuwa wakizunguka kwenye halmashauri zetu wakikagua utekelezaji wa maono ya Mheshimiwa Rais namna fedha ambavyo amezipeleka. Hawa wanaendelea kufuatilia kwamba zinakwenda kufanya kazi sawa sawa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nimesema ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI. Kwenye ziara yetu tuliona miradi mingine ambayo imechelewa kukamilika na kati ya sababu wanasema ni mvutano wa wapi mradi utekelezwe. Wala haiingii akilini na kwenye jambo hili niiombe sana sana sana TAMISEMI hapa kubwa ni ushirikishwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati miradi inakwenda wenzetu wataalamu kule site hawashirikishi wadau muhimu wanaohusika kwenye ile miradi wakiwemo Waheshimiwa Wabunge. Huku ndani tunafanya kazi ya kusemea Majimbo yetu sasa miradi ikiwa inakwenda ni vizuri tushirikishwe ili kwenda sawa sawa kutokwamisha hii miradi kwa sababu ya kuvutana ni wapi mradi ukajengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Wizara ielekeze wataalam wetu kule watushirikishe, washirikishe Waheshimiwa Wabunge, lakini pia na wadau wengine ili kwenda kutekeleza miradi hii kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge wa Jimbo la Nachingwea na Makao Makuu ya Wilaya ya Nachingwea ni mamlaka ya Mji Mdogo zaidi ya miaka 10 sasa. Tumeshatuma maombi ya kuwa Mji kamili zaidi ya miaka saba iliyopita. Niiombe sana sana Wizara jambo hili ni jema na sisi litakwenda kutuongezea uwezo kama halmashauri. Niwaombe sana muone namna ambavyo mtaharakisha jambo hili jema ili Nachingwea sasa Mamlaka ya Mji Mdogo iwe Mji kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao upungufu kwenye Sekta ya Afya na kwenye Sekta ya Elimu. Kwenye eneo hili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa sasa kibali kwa ajili ya kuajiri watumishi wapya kwenye eneo hili la elimu pamoja na afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu kwa mfano; tukiwa tunazungumzia habari ya kuboresha miundombinu kwa maana ya majengo, yako majengo chungu nzima ambayo bado wananchi walijitolea bado hayajakamilishwa. Tunashukuru kwa namna ambavyo Serikali imetuletea madarasa, imetuletea vituo vya afya ni jambo jema lakini ziko nguvu za wananchi ambazo zimelala na bado hazijulikani hatma yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana sana sana Wizara waende kumalizia yale maboma ambayo wananchi walijitolea na nguvu zao wanaziona. Tuna vituo vya afya, tuna shule lakini pia tunazo zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kidogo kuzungumza kwa habari ya upungufu wa nyumba za waalimu. Mfano mdogo Nachingwea mahitaji nyumba ni 413; zilizoko ni 72. Sasa utaona hiyo walimu wa sekondari mahitaji ni 413, zilizopo ni hizo 72, upungufu ni 341. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa walimu wetu wanafanya kazi nzuri namimi nitumie nafasi hii kuwapongeza watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye elimu, kwenye afya na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu Nachingwea tunajivunia hata kwenye rekodi ya sasa tumekwenda sana na Lindi kiujumla kama Mkoa lakini kwa hali hii tuiombe sana Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu ambazo kwa kweli upungufu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matundu ya choo kwenye shule za sekondari. Mahitaji ni 564, yaliyoko ni 318; upungufu ni 246. Hebu angalia hiyo tofauti bado tuna kazi ya kufanya. Tunatambua na tunashukuru kwa kazi kubwa iliyofanyika lakini bado tunaomba zaidi kuendelea kutusaidia kwenye halmashauri hasa hasa hizi zilizoko vijijini kwa sababu zilisahaulika kwa muda mrefu. Sina mashaka na Mheshimiwa Waziri najua kazi hii utakwenda kuibeba vizuri na kazi hii itakwenda kufanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA. Wenzangu wamesema hapa kazi nzuri inayofanyika na TARURA hakuna asiyeiona. Waheshimiwa Wabunge wenzangu mtakubaliana kwamba TARURA wanafanya kazi nzuri chini ya Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi wetu wa barabara Engineer Komba wanafanya kazi nzuri pamoja na watumishi wote wakiwemo wale wa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nachingwea. Wanafanya kazi nzuri. Basi tuiombe sana Wizara iendelee kuangalia namna ambavyo wataongeza fedha ili hawa watendaji wetu mahiri kabisa watuboreshee miundombinu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kabla Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kuingia; Nachingwea fedha ya matengenezo ya barabara tulikuwa tunapata shilingi bilioni moja. Baada ya kuingia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imebadilika bajeti ya mwaka ni zaidi Shilingi bilioni tatu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jema na sisi kama Wabunge tunapaswa kuungana kwa kauli moja kuendelea kumtia moyo Mheshimiwa Rais, anatuheshimisha. Kazi inayofanyika kwenye Majimbo kwa kweli kila mmoja anajua na tunacho kitu cha kusema 2025 na kule Nachingwea wanasema wao 2025 na Mama Samia wala hawafichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wao wanasema na Mama Samia. Wanajua haya yaliyobaki kama changamoto anakwenda kuyatatua kwa kipindi hiki ambacho kipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo habari ya Shule ya Mchepuo wa Kiingereza, shule za msingi. Kuna utitiri huo wa halmashauri zetu kuanzisha hizo shule za mchepuo wa kiingereza, ni jambo jema lakini jambo hili linakwenda kuweka matabaka tena. Niiombe Wizara twende tukaboreshe shule zetu za msingi zillizoko kwenye vijiji vyetu. Tupeleke waalimu wa kutosha, tupeleke vitendea kazi vya muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja.