Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Aloyce Andrew Kwezi (14 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi naomba nianze kwa kuwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Kaliua lakini pili naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na Chama changu Chama cha Mapinduzi na tatu nishukuru familia yangu kwa kusimama na mimi katika kipindi chote cha uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa ili niweze kuishukuru sana Serikali kwa michango mizuri ambayo imeweza kutusaidia. Suala la kwanza ni kama alivyotoka kuliongelea Mbunge mwenzangu hususani maji. Tabora tumepata Mradi wa Ziwa Victoria wa shilingi bilioni 617 na tunaamini kabisa kuanzia mwezi wa Tano tunatarajia kabisa maji yale yataelekea katika jimbo la Kaliua, Sikonge na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa fadhila hizo tunaishukuru sana Serikali kwa upendo wa wananchi hususani kuwatua akinamama ndoo kichwani, naomba nichukue nafasi hii kushukuru kwamba Hospitali ya Wilaya ya Kaliua kwetu tulikuwa hatujakamilika, lakini hivi karibuni tumepokea zaidi ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya kukamilisha Hospitali ya Wilaya ya Kaliua. Lakini tumepokea fedha za madarasa tumepokea, fedha za maabara na tumepokea fedha za ukumbi kwa Mkurugenzi, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, na nishukuru watendaji wote wa upendo kwa niaba ya wananchi wote ambao tunaendelea kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ningependa kuboresha sehemu ambayo Wabunge wenzangu wamechangia wengi wamechangia hususani suala nzima la barabara. Barabara naona changamoto kubwa kwanza ni kubadilisha ceiling ya TARURA lazima fedha ziongezwe TARURA ili wananchi waweze kunufaika na barabara za vijijini. Hivi tunavyoongea, zipo kata mpaka sasa hivi hazifikiki kata kama Usinge kwenye jimbo langu barabara imekatika, kata kama Useni kilometa 60 barabara imekatika kwa kweli hiki kitu kinatuumiza sana na mimi nilikuwa najiuliza kwa sababu nilikuwa Mtendaji kipindi cha nyuma, hivi zile fedha za emergence ziko wapi siku hizi? Mimi ninajua ni Mfuko wa Dharura inapotokea dharula basi una-take cover muda ule ule, barabara inakatika kata zaidi ya watu 60,000 inaachwa Mfuko wa Dharura tunakwenda kwa stahili gani hii.

Mheshimiwa Spika, emergence fund iwe kwenye level ya mkoa ili taarifa zinapofika ndani ya wiki moja basi tunapotoa taarifa kwamba kuna barabara imekatika kule wananchi wasibaki kisiwani, kwa hiyo nilikuwa nashauri hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lapilli ningelipenda kushauri ni suala nzima la afya. Sisi wote tuko hapa kwa sababu mama zetu walijifungua vizuri ndiyo maana tumefikia level hii na ninaipongeza kwa kuanza vituo vya afya vile 487 ambavyo tumeanza navyo. Mimi nina uzoefu kidogo kwenye sekta hii, operation kwenye kituo cha afya kimoja natoa mfano wa Kilolo kilikuwa kinaitwa Kidabaga, ndani ya miezi mitatu mama zangu waliokuwa wanajifungua walifanyiwa operation akinamama 158; sasa nilikuwa najiuliza hivi kwa kweli tunashindwa kwenda kama tumeweza kwenye kata, kama tumeweza kujenga shule za kata, ni kwa nini tusiongeze nguvu zaidi kwenye vituo vya afya ili kila kata iwe na kituo cha afya? Kwa sababu ajali nyingi za bodaboda zinatokea, operation zingeweza kutusaidia x-ray zinakuwepo pale kwenye kituo cha afya, lakini akinamama wanaojifungua ndiyo naona ni shida kubwa sana kutoka Makao Makuu ya Wilaya mpaka ukafike kijiji cha mwisho kilometa 250 kituo hakipo. Ni lazima tuangalie hiki kitu na tukipe kipaumbele cha pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la tatu ambalo mimi ningeweza kushauri Serikali nilikuwa naishauri Serikali kuhusiana na suala zima la hifadhi, nakushukuru sana Waziri Mkuu Mungu akubariki sana ulipotoa ufafanuzi kuhusiana na mipaka ni kweli kabisa ni changamoto na ningeshauri pamoja na Waziri wa Maliasili, lakini ashirikishwe Waziri wa Ardhi kwa sababu unaweza ukakuta unasema mpaka huu hapa, wananchi wanasema mpaka wetu unahishia hapa siku zote, professionally watu wa ardhi watuambie kwamba huu mpaka unapita eneo fulani kwa kweli kumekuwa na changamoto sana hususani Kaliua kwenye suala nzima la hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme naunga mkono hoja nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Waziri kwa uteuzi, Naibu Waziri nakupongeza watumishi wote wa Wizara hiyo ya Menejiment ya Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kwa kuangalia wananchi na watumishi walioko katika jimbo langu, Jimbo la Kaliua, pale tuna watumishi karibu 2,800; wamenituma watumishi hawa, natambua pamoja na watumishi wengine kwenye utumishi wetu kwenye nchi hii ya Tanzania wanaitaji kulipwa fedha zao kwa maana ya madai, madai haya mara ya mwisho imelipwa mwaka 2016; mwaka 2017 uhakiki umefanyika wa madai ya likizo, madai ya matibabu, madai ya uhamisho, madai ya mafunzo watumishi hawa hawajawahi kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumefanya uhakiki nchi nzima, lakini kulipa hatujawahi kuwalipa. Ninamuomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe watumishi hawa tuwarudishie morali yao ya kufanya kazi kwa kuhakikisha wamelipwa maslahi yao. (Makofi)

Niomba niongelee malimbikizo ya mishahara, hapa napo kuna changamoto kubwa sana, mtu amepanda daraja mwaka 2012, mwaka 2014 mchahara ukabadilika anadai malimbikizo, sasa miaka hii yote malimbikizo bado hajalipwa, shida ni nini? Watumishi hawa tunawavunja mioyo, watumishi wamefanya kazi kubwa sana za kubadilisha maendeleo makubwa sana kwenye nchi yetu, hata kwenye jimbo langu bado wanaendelea kujenga hospitali, madarasa wanasimamia wanafundisha watoto wetu, lakini kwa kweli morali ya watumishi inashuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia watumishi hawa hata increment mara ya mwisho ni mwaka 2014 kupata increment, walikuwa wanapata kila Julai wanapata increment kwenye mshahara kunaongezeka fedha kidogo, wanaweza kukopa, sasa matokeo yake kule kwenye utumishi sasa hivi mimi naona kama hadhi ya watumishi wa umma imeshuka kidogo. Imeshuka kwa sababu watumishi wanakopa kuliko kiwango, napengine tumewadhibiti kupitia mfumo wa Lawson wa utumishi ambao upo kwamba wanakopa one third, lakini wanakwenda kukopa kwenye wakopeshaji bubu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanakabidhi saa nyingine mpaka kadi zao benki, sasa tunakwendaje? Mimi nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri waangalie sekta ya utumishi waiboreshi ipasavyo, na pengine kwa wale wastaafu sasa, hapa napo kuna shida, mstaafu anastaafu anadai malimbikizo hajalipwa, lakini kinachoumiza sana wastaafu unapostaafu unafatilia michango yako unakuta Wizara ya Fedha namuomba sana kaka yangu Mheshimiwa Mwingulu Nchemba watumishi unakuta hatukuchangia ipasavyo na ninyi pale mnachelewesha pelekeni zile fedha za wastaafu kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, wastaafu hao waweze kulipwa fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe umestaafu umefikisha miaka 60, umefikisha miaka 55 unakuta kuna gap kubwa sana huku nyuma, una miaka miwili kwamba hukuchangia, fedha yako haijaenda, anaanza kuzunguka huyu mzee, utumishi wa umma anatakiwa aone furaha ya kulitendea kazi Taifa lake, lakini hapa bado lipo shida. Niombe nashukuru sana wakati wanawasilisha TAMISEMI hapa wakaongea kwamba tunaenda kuziangalia RS zile Sekretari za Mikoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi namshauri Waziri wa Utumishi, shida iko hivi pale kwenye RS ili twende na utendaji mzuri watumishi wengine wa RS wamekuwa ni ma-junior hawajafikia kwenye senior post, hawajafikia kuwa waandamizi. Sasa mtu ajafikia kuwa mwandamizi kwenye Halmashauri kuna watu wana miaka zaidi ya kumi na tano, Maafisa Mipango, Maafisa Utumishi, Wakuu wa Idara, wenye sifa za kutosha kupanda kwenda RS, tumewaacha wale pemeni, tunaangalia RS mtumishi ana miaka miwili, anakuja kuongoza, ana mwongoza Afisa Mipango mwenye miaka 15. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yaani kuna muda tulikuwa tunaona vichekesho kwa sababu wewe inabidi kumshauri sasa kwamba ndugu yangu hiki hapa kipo moja, mbili, tatu. Sasa ni nini hiyo succession plan iko wapi, maana yake mfumo wa kurithishana madaraka wale ambao wako competent kwenye level ya Halmashauri wapande kwenda Mikoani wale ma-senior. Sasa sisi tunaacha huku tunampa mtu wa miaka miwili anamwongoza mwenye miaka 20 yule kule ana Ph.D ana Masters, anafanya kazi vizuri, kwa nini tusichukuane yule tukapandisha wale ambao wanaanza at least ajifunze? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hili linafanana, shida ambayo ilitukuta kwa Hayati ndio succession plan yenyewe hiyo, mama yupo competent kachukua nafasi pale, shida iko wapi? Kwa nini huku bado kuna gap? Kwa hiyo, nilikuwa nashauri tuangalie vizuri eneo hilo ili tuweze kwenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine kikubwa zaidi ni kuboresha vitendea kazi, tunawasaidia Waratibu wa Elimu wa Kata pikipiki, tunasahau Watendaji wa Kata, Maafisa Tarafa. Sasa kwenye kata mkubwa wa kata ni Afisa Mtendaji wa Kata, sasa Afisa Mtendaji wa Kata pembeni hakuna ka- incentive kokote kwake, tumeangalia yaani chini yake kule kuna mtu anapata posho ya madaraka, sasa kwa nini na wenyewe tusiwaangalie ili twende vizuri?

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu kwenye sekta ya utumishi, nataka nichangie sehemu moja mahususi kweli kweli. Maana ukiangali Maafisa Kilimo wachache, hata kwenye jimbo langu ni hivyo hivyo, ukiangalia manesi wachache, ukiangalia sijui nini wachache. Lakini hebu twende kwenye human resource allocation tupange watumishi wetu vizuri, centers zina watumishi wamezidi. Centers kubwa zinawatumishi wamezidi, miji zimezidi, manispaa zimezidi, sijui wapi imezidii, kule unakuta mwalimu wawili, watatu. Ukiangalia sehemu fulani hakuna uwiano wako 40/50 sasa tunasaidia Taifa au tunakwendaje kwenye mfumo huo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nafikiria tuwapange kwanza vizuri hao, lakini tuajiri watumishi wa kutosha kwenye sekta zetu. Afisa Ugani mmoja ana control kata mbili tunategemea kweli kilimo kiinuke hapa? Bado itakuwa ni changamoto. Utumishi niwashauri kingine, ikama zinaidhinishwa kila mwaka za kuajiri, tuna miaka hatujaajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami naomba niwe ni miongoni mwa wale watu ambao wanatoa pongezi kwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Jenista Mhagama, nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri Ndugu yangu Deo na nisisahau timu nzima inayoongozwa na Katibu Mkuu wa Utumishi Dkt. Ndumbaro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kuchangia lakini nianze kuwasilisha kero ambazo wananchi na watumishi wa Jimbo la Kaliua wamenituma. Awali ya yote wamenituma nianze kwa kuwashukuru sana Wizara hii ya Utumishi kwa kuanza kulipa malimbikizo ya mishahara kwa kiwango kikubwa sana. Tunawashukuru sana kwa kweli kwa mwezi Februari peke yake watumishi wa Jimbo la Kaliua mmelipa milioni 400. Pia mmelipa baadhi ya fedha ya uhamisho, nilikuwa napenda nikumbushe hapo Serikali yangu sikivu kwamba Halmashauri ya Kaliua pesa ambazo tunadai arrears pamoja na madai mengine ya utumishi yanafika shilingi bilioni 1.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba tuangalie jinsi gani tunavyokwenda tulipe awamu kwa awamu ili wale watumishi wawe na mazingira mazuri sana ya kufanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nakuja na ushauri na ushauri wangu nataka kidogo tuelewane sehemu moja na kwenda ku-challenge sehemu ya harmony. Ninawashauri wa- harmonize scheme kwa maana ya kwamba tofauti ya mishahara kati ya Serikali Kuu, Serikali za Mitaa pamoja na Taasisi za Serikali. Mishahara ya Taasisi imekuwa ni mikubwa sana tofauti kabisa na mishahara ya watumishi wa Serikali Kuu au watumishi wa Serikali za Mitaa, sasa Wizara ambayo inaandaa hii Scheme of Service ni hii moja, hivi inakuwaje Afisa Utumishi au Mchumi aliyeko kwenye Halmashauri wanahudumia karibu watumishi 3000, 4,000 na huku wamesoma pengine miaka mitatu Degree yao, wanafanya kazi vizuri, inakuwaje mtu wa kwenye taasisi ambaye anasimamia watumishi 100 hawa wa Serikali Kuu na Halmashauri wanalipwa mshahara wanaanzia kima cha chini cha 750,000 wale graduate, lakini wale wa taasisi kule wanakwenda kuanzia 2,000,000 na kidogo huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri hapa hebu fanyeni job evaluation, ukubwa wa majukumu, yaani mimi niongoze watumishi 100, nilipwe mshahara mara mbili ya huyu ambaye anaanza, tulisoma UDSM pamoja au Mzumbe au whatever na ninafanyakazi vizuri na pengine mimi niko kwenye mazingira magumu zaidi. Hiki kitu nawashauri mkiangalie kwa kina kwa sababu madhara yake ni makubwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wengi kutoka Local Government Halmashauri zetu wanakimbia kwenda kwenye Taasisi wakifuata keki nzuri. Hili jambo lazima tuwaambie vizuri kwa sababu tusipowashauri sisi tunakosea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kasinge alichangia vizuri pale nimemwelewa sana, alikuwa anagomba hii miundo kwa sababu huyo ni Afisa Utumishi zaidi ya miaka kumi, sasa haya tunayowaambia ndiyo ambayo tunayaona tunayaishi. Kwa hiyo, tunaomba mliangalie jambo hili hii tofauti ya mishahara imekuwa ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nilikuwa najiuliza hivi sasa hivi tunapoajiri tumeacha kufuata muundo wa utumishi wa umma? Kama tunafuata muundo wa utumishi wa umma nilikuwa najiuliza juzi juzi, mimi najua mtendaji wa kata kwa mfano anapoajiriwa utakuta pengine awe na Diploma au Shahada ya Maendeleo ya Jamii ya Fedha, Usimamizi wa Fedha, Utumishi, Mipango na mambo mengine. Lakini sasa hivi hapa katikati unachukua mtu ambaye kamaliza Education unamuweka Mtendaji wa Kata, Sekondari zetu huku ziko wazi hivi huu muundo! Nawaambia hili la wazi ndugu zangu sitaki kuwaficha, muundo tunaosimamia hapa nadhani mmeuboresha ni wa 2002 maboresho yakafanyika 2013 kwa wale WEOs hawa Watendaji wa Kata na Vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nilikuwa nashauri hivi tutawapandishaje vyeo hawa maana yake akitoka WEO II anategemea kwenda WEO I, au kwenda Senior or whatever huko mbele, sasa anapokwenda lazima kuna sifa zinakuwepo pale, hiki kitu ni nini? Nadhani hatu-utilize resources vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri muangalie mapema ili huko mbele tusije tukawekeana kelele zisizokuwa na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nalishauri linahusiana na uhamisho. Utumishi wanapozunguka kwenye maeneo ya kwetu wanatuambia kwamba Mkurugenzi, Afisa Utumishi sijui taasisi gani, pitisha ila shauri kwamba lina upungufu wa hivi na hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta watumishi wanapoleta zile barua Mkurugenzi anapitisha anashauri kwamba nashauri hapa watumishi ni wachache, wakifika huku mna-authorize wanaondoka, sasa wanaondoka kwa wimbi kubwa matokeo yake Mjini ni wengi, Halmashauri zetu ziko hoi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaambia hili jambo ni la kweli. Muundo kwa mfano, Maendeleo ya Jamii kwenye Wilaya Ikama inataka pale Makao Makuu wawepo angalau wanne au watano. Jimbo la Kaliua Kata hata moja sina Maendeleo ya Jamii hata Mmoja, hawa wananchi wanaelimishwaje hebu niambieni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kaliua ina Kata 28, hakuna Afisa Maendeleo ya Jamii kwenye Kata hata mmoja! Hii mikopo tunawafanyaje? Ni nani anahamasisha shughuli za maendeleo? Waje kwenye kamati hizi huku za LAAC sijui USEMI sijui wapi tunawabana, ooh! sijui nini, lakini Ikama huku kwa nini hatuifuati vizuri, kwa nini hatujaajiri vizuri huko?

Mheshimiwa Naibu Spika, ajira nyingi Mheshimiwa Waziri zimekuwa zinakuja sasa hivi ni karibu mimi nasema ni ajira mbadala (replacement), ndiyo zimetoka nyingi lakini zile ajira zenyewe kwa mujibu wa Ikama mimi nina watumishi labda 2,000 lakini mahitaji yangu ni watumishi 4,000, hawa watumishi fuateni kutoka kwenye source kule, sisi ndiyo tunapata shida kule kwamba ukizunguka hapa Mganga Mkuu yuko wapi, ukizunguka hapa Mhudumu hamna, ukizunguka zahanati fulani ameenda kujifungua, miezi mitatu wananchi wa Kaliua wanahudumiwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kulishauri na naliona ni la msingi sana mimi nilikuwa naomba mafunzo, hebu tufanye mafunzo kwa watumishi hasa wale waajiriwa wa mara ya kwanza. Nafasi zenu zile za uteuzi unamteua Mkurugenzi hajui hata mail box hajui kwamba inatakiwa itoke siku hiyo, anaanza kujifunza folio ni nini, anaanza kufanya hivi…

(Hapa Mhe. Aloyce A. Kwelizi alionesha mfano)

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ni vitu gani? Hebu tuweke watu ambao ama wapelekeni mafunzo jamani kama zamani, wiki mbili, wiki tatu, akitoka kule anajua kwamba huyu Mkuu wa Wiaya ni mkubwa kwangu, huyu ni mdogo wangu, chain of command ikoje, haya ya shuleni ya moja kwa moja, haya yanakuja kufanya huku anaonekana anapwaya sasa, kwa sababu wale Wakuu wa Idara walioko pale wako imara kuliko Mkurugenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mmoja nawapa mfano wa kweli mimi sitaki kuwadanganya, kuna mmoja alipoambiwa yeye Mkurugenzi ni mamlaka ya uteuzi alichokifanya, kwanza akawaandikia Wakuu wa Idara wote anawatengua Vyeo! si mamlaka ya uteuzi? Kumbe amesahau mamlaka ya uteuzi lazima a-consider Madiwani huko, alipopiga simu nikamwambia futa hizo barua haraka Mzee unatuaibisha, sijui mnanielewa? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hayo mambo mngekuwa mnawapa kozi haya yangetokea haya? Wanaingia mle wanafikiri wenyewe pengine ni wakubwa hata kuliko Mwenyekiti wa Halmashauri, wakubwa kuliko DC lakini hawajui kwamba hii ni chain leo wa juu anaongea na wa chini vizuri, wa chini anaongea na hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kulishauri jambo moja kubwa sana, pale kwenye ule mlundikano wa vyeo, sasa hivi wanafurahi Watumishi wamepanda vyeo sana ni kweli, lakini ule mlundikano ambao umetokea sasa iko hivi, yaani Mtumishi ambaye alikuwa amepanda mara ya mwisho 2013 anakuja kupanda 2017 au 2018 anakutana na yule junior ambaye amekuja amemfundisha kazi kakaa naye na nini, sasa hivi wote wako kwenye class moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashauri muangalie kama possible mnaweza mkarudi kwenye ule mfumo wa zamani kurekebisha hili tatizo kwa kutumia accelerated promotion kwamba, wewe hapa kwa kweli hata unajua na ingine ni aibu.

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi njema anayoifanya katika nchi yetu ya kutuletea maendeleo ya kweli. Nitakuwa sijatenda haki endapo sitampongeza Mheshimwa Waziri Mkuu kwa ripoti yake nzuri sana, ripoti ya Waziri Mkuu na bajeti yake hapa kwa kweli ni ripoti ambayo imekwenda shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kuchangia katika sekta ya Maliasili. Jimbo la Kaliua limepakana na Hifadhi ya Ugalla, Hifadhi ya Kigosi ambazo zote hizi ni National Parks, pia Jimbo linalo ofisi za TAWA na TFS. Nimesimama ili tuweze kujenga hoja na kushauriana mambo mbalimbali kwa ajili ya kuwashauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Baraza la Mawaziri lilifanya maamuzi katika vijiji 975 katika Jimbo la Kaliua na katika Wilaya ya Kaliua liliachia vijiji na kuvitambua vijiji 29, walipokuja timu ya Mawaziri Nane, mimi ni miongoni mwa mashuhuda ambao nilishiriki mchakato mzima katika Jimbo la Kaliua, Mkuu wangu wa Mkoa Dkt. Batilda Buriani ameshiriki mwanzo mwisho, Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa naye alishiriki mwanzo mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ambayo ninaijenga inahusiana na Kata inaitwa Ukumbisiganga. Katika Kata ya Ukumbisiganga kuna vijiji viwili, Kijiji kimoja kinaitwa Kumbikakoko na Kijiji cha pili kinaitwa Usinga, Vijiji hivi kwa sasa kumeibuka mgogoro mkubwa sana lakini mgogoro huu umetokana na tathmini iliyofanywa na wataalam. Baraza la Mheshimiwa Rais ameruhusu na kuvitambua vile vijiji ambavyo vipo pale toka mwaka 1974, walikuja wakatangaza wananchi kaeni, tulieni, Mheshimiwa Rais amesikia kilio chenu lakini bado amewaonea huruma na mimi nikashukuru kama Mbunge wao, bado chama kikashukuru kwa mapenzi mema ya Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho kimekuja kutokea hivi sasa ni ile timu ya tathmini imekuja na mapendekezo ambayo ninaweza nikasema kwamba yale mapendekezo sijawahi kuona na nimeona ni kama vile hizi shule kwa kweli saa nyingine hazitusaidii. Hizi shule hazitusaidii kwa sababu gani? Agizo limesema wananchi wakae, wamegewe maeneo lakini badala ya kumegewa maeneo nini kimekuja kufanyika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wananchi kaya 318 kwenye Kijiji cha kwanza kinachoitwa Ukumbikakoko zimependekezwa zitoke Ukumbikakoko ambapo almost ni Kijiji kizima hicho, maana yake ni tofauti ninaona kama vile kijiji kinafutwa sasa, ziondolewe Ukumbikakoko ambayo ndiyo mwisho jirani na Mpanda, kwa hiyo mtu anatoka Makao Makuu, kutoka Makao Makuu ya Kata mpaka ukafike Ukumbikakoko ni kilometa 38. Sasa mapendekezo badala wamegewe yale maeneo ambayo yalikuwa yamependekezwa na hakuna mgogoro wowote, wanasema kaya 318 zitoke pale Ukumbikakoko zivuke Kijiji cha Usinga, zivuke Makao Makuu ya Kata, zivuke Kijiji cha Lumbeyi ziende kuingia kwenye Kata nyingine inaitwa Zuginole kilomita 58 kutoka Kijiji kilipo, halafu zile kaya zinazohamishwa hizo 318 kila kaya iende ikapewe heka tano tano, nilicheka nikasema hii ndiyo shule haijasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kwenye vijiji tujiulize Waheshimiwa Wabunge wote tunatoka kwenye vijiji, mimi ukiniuliza katika Kijiji ambacho natoka kwenye eneo la Baba yangu ni zaidi ya heka 1,000 familia nzima tunalima pale, kwa hiyo kaya moja na kaya za kule ninavyowaambia Kaliua kwa Sensa iliyofanyika ina watu 668,000, badala tufikirie kwamba tutawasaidia hawa sasa hii ni allocation mbovu. Eneo lipo pale wazi badala waongeze lile eneo ambalo lipo jirani pale wanakwenda sasa wanavuka vijiji vinne mpaka wanakwenda kuwa-dump kwenye Kata nyingine, sasa unajiuliza kwa kweli hapa si ndiyo tunafuta, sasa kuna Kijiji pale? Hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha pili kinaitwa Usinga. Kile Kijiji cha Usinga kina kaya 937 zilizopendekezwa kuondolewa kwenye kile Kijiji, hebu pigeni mahesabu ndugu zangu kaya 937 zitoke kwenye eneo lake sasa zinakwenda wapi? Zenyewe zinakwenda kilometa 42 kutoka zilipo, hizi kaya 937 ambazo Rais huku amesema ameona huruma kwa wananchi, wakalishwa na kiapo, Mbunge wao pia nikabebwa na Mawaziri kama Nane walikuwepo pale wakati wanatoa kila kitu, mwaka mmoja umeisha ni mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie Serikali na kuwashauri, kwanza watambue yale maeneo tumeyatunza, mimi nimezaliwa Ukumbikakoko iko pale, Usinga ipo pale, lakini Mheshimiwa Rais kwa sababu anatupenda tunavyoongea kuna miradi ya maendeleo inaendelea pale. Upo mradi wa maji milioni 440 unaendelea, Stesheni ipo pale, pia jirani zetu wa Mpanda ninavyoongea almost ni mita 500 naianza Mpanda kuna kijiji pale, lakini unakuja kuona maelekezo ndiyo maana nikasema utaalam mwingine! Kwa kweli nimeshamuelewa sasa hivi Dkt. Musukuma namuita Daktari kabisa, kwa sababu sasa ile informal education ndiyo naiona umuhimu wake, mmenielewa ndugu zangu? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama mtu umeenda shule unasema kwamba haya vijiji vyote vinaondoka, huku miradi Rais analeta pale inaendelea, zahanati zipo, shule zipo, stesheni zipo na sasa mmeanza kukarabati reli ya kutoka Kaliua kwenda Mpanda tayari wanajenga tena kulekule sasa hii ni nini? The same Government huku tuna-argue hiki hapa, huku mna-argue kitu kingine hiki hapa! Kiongozi mmoja naye anakuja anatamka kwamba msipeleke miradi ya maendeleo huku Rais ana miradi pale inaendelea, madarasa yanaendelea pale hivi ni kitu gani hiki? Miezi michache tu nyuma wametoka pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema kwa kweli kwenye suala la Ukumbikakoko na Usinga ni suala ambalo mimi binafsi limeniuma sana, kwa sababu sikutarajia! Huku tamko ni hili hapa, agizo ni hili hapa lakini kinachokuja kutekelezwa ni tofauti kabisa na kile ambacho kiliamuliwa huko. Sasa maana yake nini? Tena wakanitania Viongozi wangu kule kwamba sasa nenda kawahamasishe kule nikawaambia siwezi kwenda kula matapishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waliniambia pale Mheshimiwa Mbunge kazi imefanyika wakanipamba kweli kweli nikabebwa juu, sasa agizo bado lipo pale hiki kilichotokea ni kitu gani cha kubadilisha? Shida ni nini? Kama maendeleo yote haya yapo. Hivi kuna kaya ambayo hamuifahamu kabisa kwenye Kijiji kuna kaya ambayo ina heka 300, heka
400 mpaka unafikia eti heka tano tano au ndiyo zile Mheshimiwa Mbunge mmoja alisema humu kwamba tunapokuwa na zile garden zetu tunafikiri ni mashamba, tunawa- frustrate watu, umefanya maamuzi “A” leo unakuja kuyakataa maamuzi yako au unashauri vinginevyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ipitie upya ile timu ya tathmini kama walikwenda pale tena na wahusika wakubwa ni TFS wa kule fuatilieni mtusaidie kufanya maamuzi sahihi, na hili nakuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu ulikuwa pale, hivi vijiji navitaja ulikuwa kwetu unatutumikia Baba tena mtiifu, mwadilifu naendeleza kazi yako, hebu tuoneeni huruma vijiji vya Kumbikakoko unavijua, mpaka sasa hivi tunavyoongea ndicho kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hilo lifanyiwe kazi tena haraka ili kuondoa frustration kwa sababu wengine wanaanza kusema usipeleke hela, usipeleke hela kwa kigezo gani? Huku miradi ya umeme inaendelea kule maana yake nini? Tunashindwa kuwa na kauli moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya ambayo yalikuwa yanagusa vijiji viwili ningependa nichangie jambo jingine. Kule kuna kuna barabara inapita ya kutokea Mpanda – Kaliua – Uliankuru - Ushetu mpaka Kahama iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na tayari wemeshafanya detail design kule na kwenye bajeti wamependekeza kujenga daraja la Ugalla, sasa mnajenga kwa ajili ya nani? Hizo Stesheni ambazo mnaboresha kwa ajili ya nani? Kama mnapendekeza wananchi huku kwamba kuna moja, mbili, tatu hakuna madhara tumetunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo hifadhi mnaziona tumetunza, tumehangaika sisi na ndiyo maana maeneo yote tunapokaa hatuna hata mgogoro na mtu lakini kwa vijiji hivi nimeona kama maamuzi yanayofanywa, maamuzi yalifanywa sahihi na Rais wetu anayetupenda na timu yake yote ya Mawaziri huko chini huku kuna shida kinachotokea ni kingine, halafu agizo liko hivi kwamba Wilaya na Mikoa ishughulikie kuhamisha, wanahamisha wanawalipa nini? Hizo nyumba zao? Nikasema sasa hiki, yaani mimi nilichanganyikiwa! Kwa hiyo naomba tufikirie maamuzi sahihi kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Kaliua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchabgia pia kwenye mradi mwingine, mimi nachangia kwenye barabara. Tunae Mkandarasi anaendelea kutoka Kazilambwa kwenda Chaya kilometa 36 ameshapita Usinge ile bypass ya Usinge shida bado nini, kwa sababu tayari mainjinia wetu wa Mkoa kila kitu wameshawasilisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini bypass ya Usinge ile kilometa Saba mliyoahidi Waziri wa Ujenzi kwa nini hamuanzi kuijenga mpaka muda mkandarasi uishe tuingie kwenye gharama na hoja zisizokuwa na msingi tuanze kuleta wakandarasi wengine, mobilization ya material na mambo mengine yaendelee. Mradi wa ufadhili hela ipo shida nini? Mimi kwa kweli napata wakati mgumu tunakuwa na kigugumizi kufanya maamuzi kwa sababu gani? Mkandarasi yupo na mambo yanaenda kwa nini tunakwama? Kwa hiyo, naomba ile bypass ya Usinge barabara ya kilometa saba ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ningependa kulichangia. Tabora ni wakulima wa tumbaku na tumbaku inayozalishwa karibu Tanzania ni kilo milioni 44, kilo milioni 22 inatoka katika Wilaya ya Kaliua, kuanzia tarehe 20 tunakwenda kwenye masoko, sasa kule kwenye masoko nawaomba wale Wateuzi wa Serikali huwa wanafanya tathmini wakishatoka bei inayokuja wananchi wanakuja kupunjwa, haifuatwi ile bei ya wateuzi wa Serikali iliyofanyiwa tathmini, kwa hiyo masoko tarehe 20 niombe tuende vizuri, wananchi wauze tumbaku yao vizuri na mtuongeze mteuzi, mteuzi ni mmoja tu kwa Majimbo yote siyo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kuyasema haya ninaomba Serikali iyafanyie kazi kwa umakini ili tuondoe taharuki ambayo inajitokeza kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja naunga mkono Bajeti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nichukue nafasi hii na mimi kuwa miongoni mwa wachangiaji wako wa leo.

Kwanza niseme kabisa bajeti hii naiunga mkono, mbili niwapongeze sana Waziri na Naibu Waziri pamoja na Mtendaji Mkuu na timu yake yote kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika Utumishi wetu wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo ambayo ninapenda kuyazungumzia lakini nisipogusa maslahi ya watumishi katika Jimbo la Kaliua na nchi nzima nitakuwa sijatenda haki kwa wananchi, nitakuwa sijatenda haki kwa watumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo Wilaya, zipo Halmashauri, zipo RAS, zipo Wizara, mpaka sasa bado zinadai malimbikizo. Kwa hiyo, naomba ndugu zangu hawa wahakikishe kwanza malimbikizo ya mishahara yanalipwa kwa wakati, mbili wahakikishe yale madeni yote wanayodaiwa kwa mfano Kaliua kuna madeni mpaka sasa watumishi bado wanadai, madai ya uhamisho, madai ya likizo, madai ya matibabu Milioni karibu 170, wawape wale watumishi wanafanya kazi nzuri sana ya kuijenga Kaliua.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la msingi ambalo ningependa kulichangia kwanza niombe Wizara hii, ninapata kigugumizi ninapokuwa kwenyeJimbo langu. TAKUKURU
hawana Ofisi ya Wilaya, TAKUKURU wamepanga kwenye nyumba za watumishi, hivi huyu mtumishi anapo - misbehave TAKUKURU anamchukuliaje hatua wakati yeye ni mpangaji wake? Badala yake utamchukulia hatua leo, keshokutwa na yeye anakupandishia kodi unakuwa unahama hama. Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Wakili Msomi, tena mko wawili wote hapo watani zangu. Niwaombe sana kwenye bajeti hii tafadhali sana Kaliua tunahitaji Ofisi ya TAKUKURU.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU wa Kaliua wakiongozwa na Ndugu Abdallah kazi wanafanya nzuri sana. Kwa hiyo, kama wanafanya kazi kwenye mazingira magumu hebu tupeni ofisi ili wafanye kazi kwa uzalendo wao kuokoa fedha za umma na mambo mengine mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia kushauri kwenye suala la wastaafu, wastaafu wetu jamani maisha asilimia 90 ya watumishi wa umma walioajiriwa yanaishia kazini. Unaingia kazini una miaka 18 pengine mpaka miaka 60 hii ni asilimia 90 ya maisha yake, sasa wanapostaafu nini kinatokea? Nje ya usumbufu wa mafao yao yote, usumbufu mkubwa wanaokuja kuupata mimi nasema ni kwenye pension, sijaona utumishi wamekaa chini wanasema, umestaafu ile pension wanakupa mshahara wako wa mwisho. Hivi kwa maisha yanavyozidi kubadilika mtu umestaafu ukabahatika kuishi miaka mia moja na, kama wazazi wangu wako Kaliua pale wana miaka mpaka mia moja, bado ile ile hela waliostaafu nayo ya pension haiongezeki.

Mheshimiwa Naibu Spika, challenge ya maisha haya tunakwenda hivi mpaka lini? Kwa hiyo, ni lazima tuangalie hawa wastaafu wetu angalau kwenye kile cheo alichostaafu nacho si kuna watumishi wanaendelea nacho? Kwa mfano, Wakurugenzi wana SSE kwa hiyo wale ambao wana hiyo na walistaafu kwenye level ile basi tutegemee watakapobadilika wa sasa na wale wastaafu pension zao ziweze kubadilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la msingi jingine niliseme la team work, naomba mje mjifunze Kaliua. Kwa kweli kuna teamwork nzuri sana kuanzia Mkuu wangu wa Wilaya Rashid Chuachua, yuko vizuri. Niko Jimboni lakini kule akizunguka atamsema Mama Samia miradi mizuri sana, atamsema Mbunge Kwezi miradi mizuri sana, atawasema Madiwani tena wa Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu nataka niwaambie hawa viongozi nimefurahishwa sana na Utumishi kitendo mlichokifanya juzi cha induction course kwa Wakuu wa Wilaya, wafundisheni kwa sababu mtu anatoka sehemu hajui majukumu ya Mkuu wa Wilaya, hajui majukumu hata ya wale anaofanya nao kazi ana-share vipi, team work inakuwaje hapo? kwenye Sheria Namba 8 ya 2002, Kanuni za Septemba 2003 mmeongelea Kifungu cha 65 teamwork. Sasa Public Servant maeneo mengi unakuta wengine wanafeli kwa sababu utakuta Mkuu wa Wilaya fulani amekuwa kibaraka wa mgombea fulani, Mkurugenzi fulani anafeli sehemu fulani, sasa haya yanatuangusha, lakini mkishawaeleza kama mlivyowaelimisha juzi kwa kweli kile kitendo kinaendelea kutuimarisha. Nilitaka niwathibitishie Utawala Bora pale tupo vizuri, tunahitaji tu kwenye TAKUKURU mtupatie hiyo ofisi, tunahitaji na gari ya TAKUKURU ili wakina Abdallah na team yake waendele kufanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo ningeweza kulisema Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana hivi karibuni ya kuhakikisha mishahara inaongezeka. Mishahara imeongezeka kwenye mazingira ambayo vitu vingine vyote kulikuwa na mfumuko wa bei, watumishi hawajaona impact kubwa. Nataka niwashauri, mwaka huu mpaka sasa tunaongea ni mwezi Aprili hakuna promotion iliyofanyika mwaka huu. Sasa tunamaliza mwaka bajeti ilishatengwa kwamba ile mishahara yao ya promotion ilitengwa kuanzia Tarehe 01 Julai, sasa tunakwenda mpaka Tarehe 30 Juni, hapa katikakati imebaki miezi minne, mnapokuja kutoa mnatoa with effect kwenye Tarehe ambayo mmetoa barua zenu za promotion, bila ku-consider kwamba hii bajeti ilikuwepo toka Tarehe 01 Mwezi Julai, naomba mlizingatie hili ili watumishi wa umma waneemeke na maslahi mbalimbali ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nichangie pia kwenye eneo moja kubwa sana la allocation ya human resource na maadili, hapa ndiko kuna shida. Hivi vetting mnazifanyaje ndugu zangu? Yaani unafanya vetting leo mtumishi anateuliwa kesho, mambo hayakwenda vizuri, mwezi mmoja mnatengua. Hawa ina maana hamjafanya vizuri vetting si ndiyo hivyo? Sasa mimi nilitaka nishauri kwamba chunguzeni kwa kiasi cha kutosha na mtoe majibu kwa wakati. Mnaziumiza Halmashauri na vetting hizo, kuna Idara mtu anakaimu na kukaimu na kukaimu kibaya zaidi hamuwaambii kwa wakati kwamba huyu hafai, unakuja kukuta alishakaimu hata miaka miwili, miaka mitatu halafu unamletea mtu mwingine, matokeo yake kunakuwa na conflict of interest. Mtu alishajenga matumaini, alijenga na mambo mbalimbali haya hatuyafanyi, niwaombe sana Mawakili Wasomi zingatieni hizo sheria kwa kuhakikisha wananchi wetu wananufaika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwataja hawa wanaokaimu mimi nataka niongelee crisis kwenye suala la ajira. Ajira tumefanya vizuri na jana tumeshauri vizuri kweli, lakini hizi ajira mimi nataka muangalie na kwenye private sector. Private sector kuna miradi mikubwa inaendelea, pale Kaliua kumeanza mradi wa kukarabati ile reli ya kutoka Kaliua kwenda Mpanda na sasa kuna lot ya Tabora - Kaliua mpaka Kigoma. Watu ambao wanakuja mimi nilitegemea wananchi wa Kaliua, wananchi wa Urambo wananchi wa Ulyankhulu mule ambako mradi unapita, sasa wananchokifanya sasa hivi wanahama na watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watumishi ametoka nao hapo Makutupora watani zangu Wagogo wame-enjoy wamenufaika tena tumewafundisha ujanja Wanyamwezi wakifika kule wanahama nao sasa wanaleta rundo kule. Wale Wanyamwezi wangu wanabaki benchi maana yake nini? Hivyo, katika kwenye hii miradi mfuatilie siwaambii huu ni utani, hata sasa hivi mkitaka m - prove nendeni pale kwa sababu wamesimika pale Zugimlole kuna stesheni pale, utakuta wamehama na watu zaidi ya 20 nikawa nauliza hawa? Eti hawa ni mafundi. Mafundi 30 halafu fundi mwenyewe kazi yake ni kubeba tofali wananchi wa Kinyamwezi kule hawana nguvu hizo? Wafipa hawana nguvu hizo? Waha hawana nguvu hizo? Siyo kweli. Kwa hiyo nataka niwaambie haya tukiyafanya tutajenga heshima ya Mama vizuri sana, tutaondoa malalamiko ambayo hayana tija vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sahani hii nilitaka niwashauri kitu kingine kuhusu uboreshaji wa miundo hii. Miundo inakaa kwa muda mrefu sana, mabadiliko yanaenda na sayansi na teknolojia, ninyi bado mnashangaa huku, shida ni nini kwanza? Kwa nini hamjiimarishi? Kibaya zaidi hapa kwenye uimarishaji wa Ikama nilitaka niseme hapa, Halmashauri kule tunawaomba kwamba mwaka huu Kaliua tunataka tuajiri watu 205 tukileta huku ninyi mnakuja kutupa chukua watu 15 hivi kweli tatizo litaisha. Ninachowaambia kwa mfano, mimi Kata zote za Jimbo la Kaliua hakuna Afisa Maendeleo ya Jamii kwenye Kata. Hayo maendeleo wananchi wanahamasihwaje? wamelima tumbaku vizuri sana, wangetegemea Afisa Maendeleo wa Jamii atapita kuwaelimisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaambia jamani Kata zetu ziko 13 zinahitaji hiki na hiki, bado mnatakiwa mchukue ushauri wangu. Baada ya kuyasema haya siwezi kuzuia bajeti yao hawa, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini mbili nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutupa heshima kubwa sana ya kutuletea tunu ya Waziri mchapakazi, Waziri mwadilifu, Waziri mbunifu Bwana Bashe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Wizara hii, lakini nisije nikasahau naanza kujenga hoja yangu moja kwa kuhakikisha nasema naunga mkono hoja kwenye Wizara hii asilimia 100. Na pengine niwaombe Wabunge wenzangu dada yangu Mheshimiwa Esther alikwa hapa ametoka kidogo lakini Wabunge wenzangu ambao walikuwa wanawazia hata kuweka shilingi wasiweke mabadiliko ni makubwa sana. Mheshimiwa Waziri ahsante sana, tunakupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo masuala machache tu ambayo yamenifanya nipongeze, kwanza nimeanza kwa kumpongeza, kwa sababu zao la tumbaku katika Mkoa wetu wa Tabora ndiyo siri kubwa ya uchumi. Zao la tumbaku katika nchi yetu ndiyo zao la pili ambalo linachangia fedha za kigeni baada ya kahawa na nina uhakika kuanzia mwaka huu kwa mauzo yanayondelea na baada ya Mheshimiwa Bashe kuondoa ukomo wa wakulima kuwapangia azalishe kiasi gani cha tumbaku, sasa nina uhakika tumbaku inakwenda kupikwa hata kahawa saa nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mchango wa tumbaku kwenye fedha za kigeni unakwenda kuwa mkubwa sana zaidi hata ya hizi dola ambazo tumeona hapa milioni 154. Kwenye tumbaku nilikuwa na ushauri makampuni mengi yamejitokeza kununua tumbaku na kwa mara ya kwanza nasema kabisa tumbaku kuna soko linaendelea katika Kata ya Kazarole Wi lakini tumbaku tunaongea mpaka inafika dola tatu na kampuni ambazo zimefanya vizuri lazima nizitaje hapa kwa sababu nitakuwa kama Mbunge sijawatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni imefanya vizuri ni Kampuni ya Mkwawa, Kampuni wa Wodika ya Zimbabwe ile na kampuni ya tatu ni Kampuni ya GTI. Hawa wamejitahidi kwakweli sijaona tumbaku mpaka sasa hivi ambayo kwa kampuni hizi zinanunuliwa chini ya dola moja lakini bado kuna makampuni yananunua hata chini ya dola moja. Nilikuwa ninaomba yajitafakari kwa sababu mambo ni mazuri kwa kampuni nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri, Kaliua pale ndiyo Wilaya inayoongoza sasa hivi kwa kuzalisha tumbaku kwa wingi, kwa sababu Mkoa wa Tabora ndiyo unao zalisha nusu ya tumbaku nchi nzima, lakini katika Mkoa wa Tabora Kaliua ndiyo inayozalisha nusu ya tumbaku katika Mkoa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna vitu ambavyo nilikuwa najiuliza na ningependa nimshauri hivi ni kwanini tunashindwa kujenga viwanda vya kuchakata eneo kama Kaliua? Nina wazee wangu nilikaa nao siku moja wakanishauri, Mzee Kisamfu lazima nifikishe salamu zake hapa. Mzee Kisamfu akaniambia mwanangu Kwezi unashindwaje kumshauri Waziri? Unashindwaje kuishauri Serikali? Sasa hawa wazee wote, nimekutana na Kachala, nimekutana na mzee Mwaisame, nimekutana na nani? Wanataka kiwanda angalau cha kuchakata kijengwe Kaliua pale ni junction tuna miundombinu, reli ziko safi kwa maana ya kwenda Mpanda, kwenda Kigoma na kuja huku Dar es salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kila siku tukaweka center moja tu ya Morogoro. Kwa hiyo, nilikuwa naomba uongee na wawekezaji hawa ili waone namna ya kuanza kujenga huko na nimesikitika nikaona Mkwawa ameisha karabati kule, kukarabati ya nini si angekuja tu Kaliua pale maji Mama analeta, umeme unajengwa hivi shida ni nini? Kwa hiyo, nilikuwa nakushawishi hivyo hili malighafi zinatoka pale Kaliua vijana wanahitaji ajira. Wakipata ajira wananchi wa Kaliua nao ni sehemu ya Tanzania lazima tujenge tuepuke zile zana za kusafirishwa mara gari imepata ajali tumbaku imekuaje hayo yote hayatakiwi sisi utatoa pale sokoni unakwenda hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jambo la pili ambalo ningeliongelea ni mbolea, nikushauri kwa Mwaka huu ile mbole ya kupandia huwa inawahi sana mwezi wa nane imeishafika ni kwanini mbolea ile ya mazao mengine isifike mwezi wa nane huo huo? Kwa sababu hakuna tunacho chelewa na tuna muda wa kujipanda nikuombe ujipange kwa mwaka huu tusipate ile adha ya kuchelewa mbolea na uangalie vile vituo pia vya wale mawakala wakave zile kata zote. Kata zetu ziko scattered kutoka Jimbo la Ulyankulu kule mpakani mwa Ushetu kwa Mheshimiwa Cherehani mpaka ukafika Ukumbi Kabuko ni kilometa 271 wilaya moja sasa unaweza ukangalia ukiweka hivyo kuna sehemu zina tuathiri. Kwa hiyo, nilikuwa naomba la mbolea kwanza, zije kwa wakati alafu zije kwa maana ya kutosheleza vituo vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ningependa kushauri na hili nimefurahi ni kweli kabisa kuiweza Wizara hii ni kwa sababu wewe wamekwambia Mnyamwezi na Mgogo mtani wetu huyo anakusaidia na ni mzuri kweli kweli. Kwa hiyo, sina wasiwasi mnatosha kwa sababu mngekuwa hamtoshi kwa kweli leo ningeweza kushika shilingi lakini nashawishika kuwashawishi hata Wabunge wengine ondoeni shilingi twende kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jambo la umwagiliaji ndiyo nilitaka nishauri kwenye hotuba yako nimeona umeandika Uyui alafu ukaandika Igwisi lile Bwawa la Igwisi liko Kaliua. Kwa hiyo, nilikuwa naomba mrekebishe hapo, alafu tulikuwa na maombi maeneo matatu kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji sisi kule mvua ni ya msimu mmoja tunataka angalau kipindi cha kiangazi yale maji tuvune kwa maana ya Zugi Mlole nilikuomba tuwe na bwawa pale pamoja na mradi wa umwagiliaji mzuri lakini nikakuomba Igwisi, nikakuomba Ugunga. Igwisi nimeiona imengia sasa haya maeneo mawili ndiyo nilikuwa naomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, nilikuwa naomba haya maghala sasa. Kwenye maghala ningeomba muwaishe mchakato kwa sababu tenda ilishatangazwa waanze kujenga yaani nimeona ghala zuri sana kwa ndugu yangu na Mwenyekiti wangu Bwana Sillo yuko hapo. Nikajiuliza kiwanda gani? kumbe ni ghala na sisi kwetu maghala yako sehemu tatu nilikuwa naomba na ile wilaya unafahamu ndiyo wilaya inayozalisha mazao kwa wingi katika Mkoa wetu wa Tabora. Ndiyo maana unaona hata own source yetu sisi inategemea mapato ya ndani yote yanategemea mazao. Kwa hiyo, nikuombe mchakato ule wa ujenzi uende kwa kasi ili tuweze kuhakikisha wananchi wa Kiliua wananufaika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa ambalo ningeweza kulisema niseme kwamba wakulima hawa, wakulima mwaka huu wamefurahi. Kwa hiyo, kwa logic ya kuwa na fedha wanajitosheleza kwa mwaka huu wanategemea mengi ila sehemu ya magunia ni shida, wanapokopeshwa magunia yanapokuja kurejeshwa yale magunia, umekopa mia yanarudi 30 sasa mnajikuta kuna mzigo unakuwa unaendelea waangalie wale watu wa bodi na wengine ili kuhakikisha tatizo hilo kwa wakulima linakwisha ili mkulima afaidi matunda mazuri sana ya Rais, matunda mazuri ya wewe Waziri wetu mchapakazi tunae kutegemea na timu nzima kwa ajili ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ningependa kuchangia ni hili la mbegu za alizeti na michikichi, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. Kigoma jiografia yake inafanana na Kaliua ndiyo maana umeona kwanza tulipokea mbegu za michikichi, tulipokea mbegu za alizeti nikuombe sasa mwaka huu zije mapema. Sisi kazi yetu ni kulima na kazi yetu ni kuhamasisha lakini ombi moja tuendelee kuwaelimisha wananchi, kwa sababu sehemu kubwa ya Kaliua na maeneo ya Mkoa wa Tabora wamelima sana tumbaku ili kuhifadhi mazao ya chakula maana yake wanawezakana wakapendezwa na hela wasihifadhi tukarudi kwenye njaa au tukawa na dalili ya kukusumbua hilo ndiyo ningependa kuliomba tulifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii wakulima ambao wamekuwa ni mifano leo wamepiga simu wakanipa ushauri wakasema mfikishie salama Mheshimiwa Bashe, nisipowataja hapa nitakuwa sijatenda haki, Mzee Magola, Juma Issa, Mheshimiwa Behewa, Ndezilio, Juma Haji, Kayungilo, Moshi, Sengirunva na Samweli Nyawita hawa wameniambia fikisha salama. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umeisha.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima zote naunga mkono hoja niwaombe Wabunge wenzangu tuiunge hii Wizara msiweke shilingi toeni shilingi zenu. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba nichukue nafasi hii nikushukuru kunipatia nafasi kwa ajili ya uchangiaji; lakini nianze kwa kuwapongeza sana Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi, hususan Mheshimiwa Waziri, watendaji wake wote akiwemo Katibu Mkuu bila ya kuwasahau watendaji waliopo chini yake kwa maana ya wale Wakurugenzi wa Mashirika yetu ya Reli, TBA na mambo ya anga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimesimama hapa kutoa pongezi na shukrani; hivi juzi tu mliweza kuona Mheshimiwa Rais akiwa katika Mkoa wetu wa Tabora na mambo aliyoyafanya katika Mkoa wa Tabora ni mambo makubwa sana, ndiyo maana nimewiwa nakuona kwamba ni vizuri nikisimama na kutoa pongezi kwenye Wizara hii ambayo inafanya mambo mazuri na mambo ya kufurahisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa napenda nikumbushe Wizara kwenye barabara baadhi ambazo zinapita katika mikoa minne. Katika Jimbo la Kaliua, tuna barabara ambayo inatokea Mpanda; barabara hii inaingia Wilaya yetu ya Kaliua, inapita Jimbo la Ulyankulu, Ushetu inaingia Kahama, inapita Msalala mpaka Geita. Barabara hii kwetu sisi ni barabara ya kiuchumi. Barabara ya Mpanda – Kaliua - Kahama mpaka Geita ni barabara ya kiuchumi kwa sababu kwanza mazao mengi sana yanategemewa kiuchumi yanatokea Mpanda na Kaliua. Lakini gari nyingi sana kwa mfano Kaliua tu kwa siku tunalaza mabasi karibu 28 ambayo yanakwenda Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, lakini tunazo hifadhi zetu kule Katavi, tunahifadhi ya Ugala, lakini bado tuna hifadhi ya Kigosi zote hizi ni National Parks. Uwepo wa barabara hii kiuchumi kwetu sisi bado itatusaidia kuinua uchumi wetu na mpaka sasa ninavyokwambia kwa mfano, Wilaya ya Kaliua ni Wilaya ambayo inafanya vizuri sana kwenye mapato ya ndani. sisi mpaka Disemba tumekusanya kwa asilimia 91; sasa haya mazao yote ambayo tumekusanya tulitegemea kabisa tungekuwa na usafiri bora na imara ingetusaidia sisi kuendelea kuinua uchumi wa wananchi wa Kaliua, Mpanda, Kahama na Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, mwaka jana katika bajeti wakiangalia pale waliweka ujenzi wa daraja la Ugala shilingi bilioni 3.5 na mimi kama Mbunge nikasimama nikasema bajeti imepitishwa na Bunge kuna shilingi bilioni 3.5 ya kujenga daraja la Ugala. Lakini mwaka huu wakasema, sasa tulifanya upembuzi wa awali, sasa tunakwenda kwenye upembuzi wa kina, sasa huku mliweka bajeti ya kujenga daraja leo mnatuambia mmekwenda kwenye upembuzi wa kina inamaana hili daraja mlikuwa mmeliweka kwenye bajeti na mkaweka ile fedha bila kuangalia hayo yote? Lakini hiyo fedha imekwenda wapi hiyo shilingi bilioni 3.5?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba tushauriane kiuchumi na tushauriane ili kujenga nchi yetu hii, tunaposhauri barabara ambayo ina cut across mikoa minne ni barabara ya kiuchumi, ni barabara ya msingi sana. lakini kule sisi tumepakana na nchi mbalimbali kama Burundi Rwanda, Congo tumepakana nazo kule, sasa huoni kama hii ni corridor nzuri sana na ukuangalia ndiyo maana Mheshimiwa Rais amefanya jambo la maana, unasikia kuna lot inakwenda kujengwa reli ile ya kutokea Tabora kwenda Kigoma lakini njia panda ni Kaliua. Kuna reli nyingine inatoka Kaliua inakwenda Mpanda kwa maana joint ya Kalema kule ili tuweze kusafirisha mizigo kwenda Congo. Kwa hiyo, mimi nilikuwa naomba ushauri wa kiuchumi, ushauri wa kitaalam huu ndiyo ushauri ambao tunatakiwa kuuzingatia kwa faida ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi ninalo jambo pia ningependa kushauri. Jambo hili linahusiana sana na barabara ambayo inajengwa, nawashukuru sana kwenye barabara ambayo inajengwa ya kwenda Kigoma. Barabara hiyo kile kipande cha Kazilambwa alikuja Naibu Waziri pale na nadhani ni kilometa 36 ambayo ni karibu shilingi bilioni 38 tunawashukuru sana. Lakini kwenye ile barabara tulikuwa tunaushauri, kuna kijiji kinaitwa Ugansa ambako inajengwa hapo kuingia katika mji mkubwa sana wa Usinge, ile Usinge peke yake ni kata ina watu karibu 80,000 na nina Imani kwa sensa ambayo tunakwenda kuitekeleza sasa hivi sisi kule tunajua kuzaa, idadi ni kubwa sana ya watu kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale tumeweka kilometa tisa ambazo zinaingia mpaka katika Kituo cha Afya, lakini sasa nilikuwa nawashauri, hebu fanyeni ushirikiano kati yenu na watoto ambao ni TARURA, barabara ile ni ya TARURA msipowashirikisha TARURA mkija kuondoka ulinzi na uhifadhi wa ile barabara utakuwa kwa nani. Kwa hiyo, ninaloliomba jambo kubwa sana hapa ni ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nawaomba TANROADS, TARURA hajasimama kama alivyo TANROADS. Nilikuwa nawaomba pale Kaliua kuna majengo mlipomaliza barabara ya kilometa 28 kutoka Urambo – Kaliua, yale majengo yote yaliyobaki Kaliua Mkurugenzi wangu Bwana Jerry Mwaga aliwaandikia barua akawaomba yale majengo yasiendelee kuchakaa Halmashauri tuyatumie, lakini mpaka sasa barua hiyo haijajibiwa. Amekuja Mkuu wangu wa Wilaya mpya Bwana Chacha Matiko, akakumbushia kwa barua. Sasa tulikuwa tunaomba majengo yale yamekaa kwetu, sisi tuna shida mbalimbali, tunahitaji vyuo, vituo vya afya, tunahitaji mambo mbalimbali, lakini majengo yamekaa pale jengo lisipokaliwa nadhani mnaelewa linashuka thamani. Sasa pale majengo yanaharibika kwa nini msitupatie, shinda ni nini mpaka msitupatie. Lakini hapo hapo kuna vifaa ambavyo vimeachwa na nyie TANROADS, mkandarasi amemaliza kazi yake, anapomaliza awa TARURA hawana uwezo wa vifaa kwa maana ya kupima barabara zetu, maabara hawana. Vile vifaa mngekuwa mnawakabidhi watu wa TARURA ili na wenyewe zile barabara zao waweze kufanya, kinyume cha kukaa wanamkodi mkandarasi, wanamkodi Mchina kwa ajili ya kuja kurekebisha barabara zetu; ule ubora wa barabara za TARURA unashuka kwa sababu ninyi hamjawaachia vifaa hivi ambavyo vinabaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo ningependa kushauri, na hili napenda nilishauri vizuri sana kwenye barabara zetu hizi; naomba nawaomba tuangalie kusisitiza uzito wa magari, maana yake kuna barabara zinaanza siku mbili unaiona kabisa hii sijui inazidiwa, sijui ni chini ya kiwango mimi sijaelewa hapo. Kwa hiyo, nilipenda mlifanyie utafiti muangalie tutasimamaje sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ushauri mwingine unakwenda kwenye Shirika la Reli sasa. Nafahamu Mheshimiwa Rais ana dhamira njema sana ya zile reli zile lots mbili ambazo zitakuja Ukanda wetu, lakini kwenye reli sasa hivi reli sisi inatumika Tabora – Kigoma treni inakwenda, lakini Tabora – Mpanda treni inakwenda.

Sasa treni inayokwenda Mpanda mmetuma mabehewa mawili tu, watu wanajaa kuliko kiwango mle. Lakini jambo lingine na Mtendaji Mkuu nikuombe kaka yangu Kadogosa pale engineer, yaani pale kuna wizi umeibuka sijui ni mfumuko wa bei hata sielewi shida ni nini? Yaani hizo hizo behewa mbili mnao polisi ambao wanatembea na zile behewa, lakini wananchi wangu wa Kaliua wanaibiwa kuliko kiwango.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba wale polisi ambao wanafanya kazi pale wahakikishe wanalinda mali za wale wananchi ambao wanasafiri kwa kutumia treni. Lakini kwenye reli hiyo hiyo kwenye vituo, angalieni vile vituo ambavyo vina idadi kubwa ya watu ili mtupe muda mwingi wa kutosha kwa ajili ya kusimam,a kinyume cha kuwa inafika dakika moja tu paaa imeshaondoka mnaleta ajali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ikisimama kwa muda tayari mnatuinulia uchumi wetu sisi kwa sababu zipo bidhaa wajasiriamali wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba walichukue hili la kuimarisha reli yetu na kuimarisha usalama wa abiria ambao wanasafiri. Kwanza idadi ya mabehewa iongezwe kwa maana ya Tabora – Kigoma lakini Tabora – Mpanda ambayo ni mawili tulikuwa tunashauri hata mkitupa manne shida iko wapi, kinyume cha behewa moja linakweta unakuta hadi watu 300, siyo sawa. Kwa hiyo, mimi ushauri wangu mkubwa nilikuwa naomba niishauri Serikali kwenye jambo hilo mtupe kipaumbele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilikuwa na ombi, juzi mlivyokuja mmeona Meneja wetu wa Mkoa wa Tabora anafanyakazi vizuri sana. Kijana anayejituma kabisa anakwenda na kazi yenu, lakini ninachokiona pale sisi kikao cha mwisho cha Road Board, yule bwana anajitambulisha bado ana kaimu tu, sasa nikawa napiga mahesabu yule marehemu ambaye ametufanyia kazi nzuri Mzee Ndabalinze amekuja kijana mwenye kasi tena hajathibitishwa kazini, hebu naomba mumthibitishe ninyi wenyewe mmefungua barabara nzuri mnaona. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza Wizara hii ya Ujenzi kwa kazi nzuri ambazo wanalifanyia Taifa letu na hususani Mkoa wa Tabora ambao kwa kweli sehemu kubwa tunakwenda vizuri. Nisisite kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu wake pamoja na Meneja wetu wa Mkoa wa Tabora. Meneja yule kwa kweli ningeomba Wizara pengine hata mmuandikie barua ya pongezi kwa kazi nzuri ambazo anaziendeleza katika Mkoa wetu wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi yangu maombi tu, pale Kaliua barabara ya kutoka Urambo imepita Kaliua na sasa ipo mpaka karibia na Usinge, lakini bypass ya kwetu pale ni kilometa 5.5. Kwa sababu barabara imepita kulia, imeacha Kata za Ushokola, Kaliua Mjini pamoja na Kasungu, maeneo haya yote naomba hii barabara ambayo inapita katikati ya Mji na Stendi na wafanyabiashara wakubwa wa Kaliua pale tuwasaidie tuweze kujenga ile bypass ili waone faida nzuri ya utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo naomba ni kuanzia Usinge, wanapojenga ile barabara ya Kazilambwa – Chagu, kutoka pale ni kilometa 4 kuingia Usinge Mjini. Naomba na penyewe wasije wakasahau kuhakikisha kwamba hata kama siyo mwaka huu, wakianza mwaka huu Kaliua hizo kilometa 5.5 basi kwa Usinge mwakani wanaweza wakaweka kuingia mjini kwa sababu Usinge ni sehemu kubwa na ina kata karibu tatu na karibia asilimia 23 ya wakazi wa Kaliua wanapatikana Usinge pamoja na Kata ya Usenye. Kwa hiyo, tunaomba hizo lami kilometa 5 waweze kutusaidia pale Kaliua Mjini na kule kilometa nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, naendelea kuwashukuru, kuna barabara nimeona kubwa kweli ya kutokea Kahama – Ushetu – Igwisi – Kazaroho – Kaliua – Zugimlole kilometa 60 mpaka Mpanda, tumeona pale mmetuwekea daraja. Kwa awamu hii mimi naunga mkono kwa kweli tujengeeni kwanza daraja, mmetuandikia hapa mnatutafutia fedha, hizo fedha mhakikishe mnazipata ili barabara hii ya kiuchumi ya kutokea Mpanda kupita Kaliua mpaka Kahama iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho, pale Kaliua ni junction abiria wanaotumia treni kutoka Kigoma wakifika Kaliua wakishuka wanatumia treni inayokwenda Mpanda; eneo lile naomba waongeze muda wa treni kwa sababu muda wa kusimama treni Kaliua ni mchache, ni dakika kumi na ile ni junction ina abiria wengi sana. Kwa hiyo, naomba waboreshe pale kwa kuongeza muda ili uwe wa kutosha. Jambo la pili pale pale ni tiketi, Kaliua tiketi hazitoshi, naomba watupe tiketi za kutosha sisi bado tunatumia sana usafiri wa treni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la tatu hapo hapo, ni usimamizi kwenye vile vituo vidogo, kituo kama kilometa 34, kilometa 48 mpaka Mpanda. Naomba maeneo hayo toeni muda wa kutosha kwa sababu treni inasimama dakika moja unaona imeondoka, mnasababisha ajali. Kwa hiyo, naomba wananchi wa maeneo hayo waweze kuongezewa tiketi na muda wa kutosha kwa ajili ya kuhakikisha wanasafiri vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri pia Wizara pamoja na kazi nzuri walizofanya, ile reli ya kutoka Kaliua kwenda Mpanda ni mbovu mno, wanatumia saa kumi. Sasa saa 10 kwa kilometa chache hizo karibu kilometa 180, naomba waiboreshe wakati tunasubiri hiyo Standard Gauge ambayo inakuja, waikarabati reli hiyo vizuri tupunguze hata muda wa kusafirisha mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nirudie kuipongeza sana Wizara hii kwa kazi nzuri wanazozifanya lakini nawaomba wasisahau kurekebisha zile kilometa 5 za Kaliua mjini pamoja na taa za barabarani, maana wale wananchi wakifika tu Urambo, wanaona Urambo bypass yao ipo safi na taa za barabarani wanauliza Mbunge yupo wapi nami napenda nirudi awamu ijayo. Ndugu zangu chondechonde nawaomba kabisa kwenye bajeti hii muendelee kuwa wasikivu na kunihakikishia mmeniwekea hizo kilometa 5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nawashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Binafsi nakushukuru wewe kwa hekima na busara zako za kuongoza Bunge letu. Pia nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya watendaji kwenye Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa kwa niaba ya wananchi wa Wilaya ya Kaliua hususani Mkoa wetu mzima wa Tabora kuhusiana na zao la tumbaku. Naomba Wizara hii itusaidie, kwanza kabisa kwenye zao la tumbaku kumejitokeza changamoto kwenye soko. Bei elekezi ya zao la tumbaku Serikali imetoa ni dola 1.61 lakini pia gharama ya mkulima kuzalisha anatumia dola 1.4, wanunuzi walipokuja wamenunua chini hata ya gharama ya wakulima; wamenunua chini ya dola 1.2. Haya yametokea siyo kwenye Jimbo la Kaliua peke yake pia yametokea kwenye maeneo ya Usimba, Kasungu, Kaliua Rural, Kamsekwa, Igwisi na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao hili la tumbaku limekuwa na changamoto, ambaye ananunua vizuri kabisa ni kampuni ya GTI, lakini kampuni ya Alliance One wamenunua tofauti kabisa wakati wale ma-valuer wa Serikali wamefika wakatathmini bei ikaonekana ni nzuri walipofika GTI wakanunua kwa bei nzuri lakini walipokuja kununua hawa Alliance One wamenunua kwa bei ya chini sana ambayo inaumiza wakulima. Naomba Wizara iingilie kati kuhakikisha masoko ambayo yamefanyika katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita bei ya wakulima iweze kupanda kama tathmini ya Serikali ilivyokuwa imesema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee CSR kwenye kampuni hizi, kampuni ya GTI hii imetusaidia sana inatoa CSR, tunajua madhara pia ya tumbaku, wanatu-support madarasa, zahanati, vituo vya afya, hata mimi kwangu Usinge wameleta milioni 500. Huyu Allowance One ambaye ananunua sana tumbaku kule hata CSR kwa maana ya huduma za jamii ha-support. Sasa kwa nini yeye anakuwa tofauti na wanunuzi wengine? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kampuni ya Grand Tobacco Limited pamoja na Majestic, wamenunua tumbaku msimu wa 2019/2020 mpaka sasa hawajalipa wakulima wa tumbaku. Pale kwangu kuna chama kinaitwa Mwamko kinadai shilingi milioni mia moja na moja mpaka sasa hawajawalipa. Kibaya zaidi wamerudi kwenda kufunga mkataba yaani unamdai, hajalipa, halafu umefunga mikataba na vyama vya msingi. Naibu Waziri alikuja akatuahidi kulishughulikia lakini muafaka bado, naomba Bunge litusaidie kwenye zao hili la tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye zao hili hili la tumbaku nashangaa sana tumewekewa ukomo wa kulima yaani wewe unaambiwa zalisha kilo mia mbili wakati wewe una uwezo wa kuzalisha zaidi ya kilo mia mbili, hii limit kwa nini wanaiweka? Ni kwa nini Wizara isiingilie kati na kuhakikisha tunapata masoko? Lazima tusimame pamoja kupata masoko ya kutosha. Naomba hii limit iondolewe kwa wakulima wazalishe kadri ya pembejeo wanazopata na uwezo walionao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia Wizara itusaidie kuhusiana na kilimo cha alizeti katika Mkoa wa Tabora. Tabora alizeti inakubali, Singida na Tabora unaitofautishaje, hali ya hewa ya Kaliua, Urambo, Igalula, Nzega na Igunga inafanana na alizeti tunalima. Hizi mbegu ambazo zimesambaza kwenye mikoa mitano kama alivyokuwa analia wa Kilimanjaro tunaomba zifike Tabora. Kwa heshima zote nawaomba waingilie kati watusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niwapongeze kwa jambo kubwa sana, jiografia ya Kigoma inafanana na ya Tabora, mmetusaidia kwenye Jimbo la Kaliua mmetuletea michikichi miche karibu laki moja na nusu. Naomba sambazeni miche ile katika mkoa wote wa Tabora kwa sababu haya mazao yanakubali kwenye Mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la pembejeo na nina ushauri; CRDB Bank na mabenki mengine yanatusaidia lakini Benki yetu ya Kilimo kwa nini isitusaidie kwa sababu riba ya pembejeo ikitoka kwenye TADB itakuwa ni ya chini kuliko ambavyo ipo kwenye mabenki mengine. Asilimia nane ni kubwa, naamini hata kule wanako-support kama TADB akisimama vizuri tutakuwa na mchango mzuri sana na wananchi watanufaika sana kwa sababu asilimia 80 ni wakulima na sisi tumesimama hapa leo tumesomeshwa na wakulima, kama siyo alizeti basi ni kahawa, kama siyo tumbaku basi ni zao lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa mwisho uende kwenye kilimo cha umwagiliaji. Yapo maeneo tunapoteza maji, mafuriko yanatokea hivi tumeshindwa ku-design mabwawa ya kutosha ili kila kiangazi tuzalishe nyanya, vitunguu na mazao mengine ya umwagaliaji. Hatuna sababu ya kudharau kilimo cha umwagiliaji. Nawaomba Kata ya Zugimlole tuwekeeni bwawa pale, Igwisi tumesha design bwawa tunaomba mtuletee fedha, lakini Igagala Namba Tano tume-design bwawa, tunaomba mtuletee fedha hizo ili ziweze kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuwapongeza Wizara hii kwa umakini, unapowapa taarifa wanakuja haraka na wanatusaidia kutatua migogoro mbalimbali. Kwa hiyo, mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri Profesa wangu na Naibu wako makini kabisa Mheshimiwa Bashe, msilale, hiki kilimo ndiyo kinatufanya sisi tuonekane tumetekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa siyo kwa umuhimu CSR nyingi sisi tunazipata kupitia mazao ambayo yanapatikana kwetu na hususani tumbaku. Halmashauri zetu mapato ya ndani zinategemea kwenye tumbaku, naomba hawa watu muwabane walipe, wanapolipa Halmashauri zikapata mapato ndiyo tunaweza kusaidia Serikali Kuu kwenye ujenzi wa vituo vya afya, barabara, kununua mitambo ya barabara na mambo mengine ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, nashukuru kwa hekima na upendeleo ambao umenipatia mimi. Nakushukuru sana, Mungu akubariki, naunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii ya kuweza kuchangia, lakini kwa nafasi ya pekee naomba tu nianze kwa kuwapongeza sana Wizara ya Fedha kwa maana ya uratibu mzuri wa bajeti kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa nafasi ya pekee mama huyu kwa kweli ni msikivu sana na usikivu huo utauona kabisa, kwa mfano mimi katika bajeti iliyopita nilichangia sana kwenye masuala ya Utumishi nikaongelea stahili za Watendaji wa Kata pamoja na Wabunge wenzangu, tukaongelea stahili za Maafisa Tarafa na tukaongelea masuala ya promotion kwa watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyokwambia karibu halmashauri zote wapo busy kuendelea na upandishaji wa vyeo kwa watumishi. Sio hilo peke yake utekelezaji tumeuona kwa ile laki moja moja ambayo inakwenda sasa kwa Maafisa Tarafa na pia kwa Watendaji wa Kata. Siyo hilo peke yake bado kwa wale wastaafu tulilalamika hapa, tumeona mkakati ambao amekuja nao, Mheshimiwa Waziri na usikivu wa Serikali unaonekana moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nisimame nitembee kifua mbele na niwaombe wenzangu tutembee kifua mbele kwa kuamini kwamba, ushauri tunaoutoa ni shauri ambao unasikilizwa na unatekelezwa. Maana yake hakuna kitu kizuri unaposhauri halafu kikafanyiwa kazi na ndiyo maana ya Ubunge, tungekuwa tunashauri halafu msifanyie kazi, kwa kweli tungekuwa tunasema mbona ili tulilisema hakuna ambacho kimefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwaweli nimejisikia faraja sana, ndiyo maana narudia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa usikivu wake. Kwa namna hii naamini kabisa Watanzania wengi hata ukipita vijiweni wanajisikia furaha na amani kwa Serikali ya Awamu ya Sita imekuwa ni Serikali sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze kwa miradi ambayo inaendelea, ukifuatilia bajeti kuu miradi mikubwa yote ya kimkakati bado inaendelea na mama mpaka tunavyoongea yuko Mwanza ametoka kuzindua reli, lakini jana nimeona anazindua masoko ya dhahabu. Pakubwa zaidi ambapo amepalenga na ambapo ndiyo kilikuwa kilio kikubwa cha Wabunge ni suala kubwa la TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba sitaki nimpongeze kwa namna ya kuuma ulimi, nampongeza hapa akiwa ananiangalia kwamba kazi aliyoifanya na ushauri aliofikisha Mwenyezi Mungu ambariki sana, kwa sababu kwenye TARURA mazao ya wananchi wote wanafahamu yanauzwa bei ya chini kutokana na barabara. Mwananchi anatoka na mzigo wake kule wa mahindi, vitunguu, nyanya na alizeti, anakutana na barabara hakuna daraja, hakuna karavati na maji yapo kiunoni. Kwa hiyo matokeo yake yananunuliwa mazao yao kwa bei ya chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa alternative hii ambayo waekuja nayo, naomba niwapongeze sana na wasimamie hilo. Wasimamie hilo ili waturahisishie sisi kujibu maswali, maana yake tukimaliza Bunge hapa tutakuwa kwenye majimbo yetu, tutakuwa kwenye mikoa yetu, kwa hiyo itakuwa ni fursa nzuri ya kuwaambia nini ambacho tumekisema na nini ambacho Serikali sikivu imetekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa lingine ambalo nimeliona hapa na ni lazima niliseme kwenye Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Pale kwenye utalii nimefurahishwa sana kwasababu tulikuwa tunapata wasiwasi kwenye Kamati kwamba utalii ni sekta ambayo inatuingizia fedha za kigeni, lakini baada ya kuondoa yale mapato yanaenda moja kwa moja kwenye Mfuko Mkuu ule, tukawa na wasiwasi watatuzoroteshea maendeleo ya utalii. Sasa niwaombe kwasababu wanatoa in advance labda miezi miwili, wamefanya akili ya ziada sana, kwa hilo nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado nawaomba jambo kubwa kwenye mapato yetu ya ndani, ni lazima zaidi ya hapa tuimarishe sehemu gani kwenye utalii. Kwenye utalii, katika hifadhi zetu kuna maeneo au hifadhi wakati wa masika hazifikiki kabisa. Sasa tunahamasisha Watanzania waende kwenye maeneo ya hifadhi, naomba nitoe mfano wa Kitulo National Park, tulitaka kwenda pale Kitulo tukaambiwa kwa muda huu wa mvua, Kitulo barabara haifikiki. Pia tukataka kwenda kuna Ziwa moja linaitwa Ngosi ikashindikana, sasa hizo ni sample mbili, lakini nilikanyaga Biharamulo kuingia kule Burigi ikawa na yenyewe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba hapa tushauriane vizuri, tunahitaji fedha kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu na kwa ajili ya miradi, nashauri tu-inject fedha nyingi kwenye kuboresha miundombinu ile ya kwenye hifadhi zetu ili hata kama ni masika watu wanataka kwenda Christmas kupumzika mwezi wa Tatu wanataka kwenda mle, pamoja na sikukuu zetu hizi za kuchinja, wawe na uwezo wa kwenda kule kula vitu vyao vizuri wakati wa masika na wakati wa kiangazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningeweza kuwashauri, kwenye sekta ya afya nafahamu kabisa ziko kata hatujakamilisha shule na zipo tarafa ambazo hatuna vituo vya afya, hebu tujaribu kwenye hizi fedha ambazo wameangalia, nafikiria tuwabane kidogo, unajua unapoenda kutoa fedha kwenye M-pesa, kwenye Halopesa, kwenye Tigo pesa na kwenye Airtel Money, kama unatoa milioni moja au unatuma milioni moja unakatwa labda 3,500 au 4,000. Unapokwenda kutoa unakatwa tena 8,000/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomb tujaribu kuangalia hapo je, hatuwezi kuongea na makampuni yetu, yalipe kodi kama kawaida maana yake tusichezee kodi, lakini bado tuangalie ile fedha ambayo ilikuwa inapotea pale kwenye zile transactions, naona ile fedha ni kubwa. Yaani muamala nimekutumia hapo Mheshimiwa unaupokea, mimi niliyetuma nakatwa, wewe ukinyanyuka kwenda kutoa unakatwa karibu 8,000 mpaka elfu 10,000 na zaidi. Sasa ile fedha ni nyingi, kwa nini tusiongee, kwa sababu ni suala la uzalendo na wana- exist nchini kwetu na tunafanya nao kazi, tuwashawishi kwamba if possible, basi angalau na wenyewe wajaribu kuachia shilingi elfu moja moja ziende kwenye TARURA, kwa sababu barabara za vijijini ndiyo mishipa ya uchumi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitaka tuyapunguze maneno mengi ni hapo ambapo tumelenga kwenye TARURA, afya, elimu na maji. Haya maeneo tukibana vizuri, naamini kabisa mwelekeo wetu utaendelea kuwa vizuri na kama nchi tutaendelea kutembea kifua mbele kwa kuhakikisha tunawasaidia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kubwa naendelea kupongeza ni la Madiwani wetu, nawaambia kabisa by professional mimi ni Afisa Utumishi, kwa hiyo nimekaa halmashauri karibia miaka 15 ninachokiona…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo ya kwanza?

NAIBU SPIKA: Malizia sentensi yako unachokiona…

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokiona ambacho ningekishauri, inawezekana kuna halmashauri ambazo wakawa na wasiwasi kuwalipa moja kwa moja, naomba kupitia ule Mfuko Mkuu wajaribu kuziangalia zenye uwezo mkubwa sana, ndiyo iwe hivyo kwa maana yale majiji makubwa yenye fedha, lakini hizi halmashauri zingine zote zinasuasua, wahakikishe wanawalipa kupitia hii Serikali Kuu moja kwa moja, kusiwepo kwamba hiki na hiki, zile za daraja A, zile halmashauri kama Kinondoni hapo sawa.

NAIBU SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikupongeze sana na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nianze tu kwa kuunga mkono hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Ezra.

Mheshimiwa Spika, naomba tu niwasilishe kwamba, kwa kweli katika huu muda wa wiki mbili kelele zimekuwa ni nyingi sana kwa wanafunzi ambao wamekosa mikopo na kwa wanafunzi ambao wamepata kiwango cha chini kabisa cha mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu nilikuwa najiuliza maswali mepesi tu kwamba, Serikali imefanya vizuri sana kwenye kujenga sekondari, tena nyingi karibu kila kata na pengine kata zingine zina sekondari mpaka tatu. Pia Serikali imefanya vizuri sana kwenye vyuo, kwa maana ya ujenzi na kila kitu, lakini ongezeko la wanafunzi ambao wanasoma limekuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa haya yote, nimeona kuna gap ambalo Serikali haijafanya vizuri. Serikali haijafanya vizuri kwenye eneo hili kwamba huku kote wametoka vizuri. Tumekuja vizuri, lakini shida kubwa imekuja kutokea volume ya wanafunzi ambao wanaingia vyuo vikuu ni kubwa sana, ni lazima tuongeze Bajeti. Kwa hiyo la kwanza, naishauri Serikali ije na mkakati hapa Bungeni wa kuhakikisha ina-cover wale wanafunzi wote wanaofaulu vizuri, wasibaki nyumbani.

Mheshimiwa Spika, hapa tunatengeneza bomu. Huwa najiuliza hata vigezo eti wanasema kwamba huyu alisoma shule ya private, labda alikuwa analipiwa milioni mbili, milioni mbili na kadhaa. Sasa nikawa najiuliza wazazi hatuelewi kama kuna wengine wanafilisika, hatuelewi kama kuna wazazi wengine wanastaafu, kama tunaelewa kwamba wapo wazazi ambao uwezo wao unapungua ni kwa nini tunawawekea masharti magumu kiasi hiki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababau mimi leo inawezekana nina uwezo, kesho kutwa nisiwe na uwezo wa kifedha, kwa hiyo mtoto wangu abaki nyumbani? Kwa mfano, ongezeko tu la takwimu za jana, Tabora tumekwenda kwenye milioni 3.3, kitu ambacho lazima tubadilishe, lazima tu allocate hizi resource vizuri.

Mheshimiwa Spika, nashauri hapa kwenye jambo lingine kubwa tu. Bodi ya Mikopo ni lazima watoke kwenye boksi walilojifungia, lazima wawe na uwezo wa kukaribisha private sectors kwenye uwekezaji wa mikopo kama mabenki. Ni kwa nini tusiwape mabenki angalau ideas na vigezo ili wawe na uwezo wa kutusaidia? Ni kwa nini tujifungie kwamba ni Serikali tu, wakati tunaelewa kabisa nchi zinazoendelea zinakwenda zaidi ya hiki ambacho tunachokifanya.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwamba wote humu tumepewa utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Ndiyo maana kuna mwingine alijaribu kuitoa, tulipopewa ile Ilani ya Chama Cha Mapinduzi hatuwezi kukubali wananchi wetu, wanafunzi ambao wapo kwenye majimbo yetu waendelee kuteseka kwa kukosa mikopo, sasa mwisho wa yote tutaulizwa haya, Ilani ilitekelezwaje hapa utasemaje? Nilijenga tu madarasa halafu nikaacha watoto maelfu wamekaa nyumbani. Wamekaa huku bila kuwasaidia haiwezekani!

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naiomba Serikali itoke kwenye boksi ije na kuhakikisha wanafunzi wote ambao wamefanya vizuri wanakwenda. Vilevile kigezo kingine ni zile taaluma ambazo wanakwenda, yaani mtu ambaye anakwenda Udaktari unampa asilimia ishirini, sio hali ya kawaida jamani tuelewe kabisa kuna mabadiliko ya tabia ya nchi, leo mkulima analima, kesho inawezekana asipate mazao. Sasa kama asipopata mtoto wake ameshayumba ulimpa asimilia ishirini. Tunajenga mazingira gani kwa hawa watoto?

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, kwanza nirejee kusema tu, kama Serikali mkakati tunauhitaji na mkakati huo ujadiliwe kwa kina, lakini kama tulivyofanya kwenye sekta nyingine. Tumefanya vizuri tulipoyumba kidogo kwenye mafuta kukawa na mambo mazuri yakaja, tukafanya na maeneo mangine ambayo wameshauri Waheshimiwa Wabunge wengine. Hivyo, nashauri hili kwetu ni dharura kwa sababu simu tunazopokea hapa nina message ya bwana mmoja anaitwa bwana Bada katoka kutuma message hapa, Mheshimiwa Mbunge unatusaidiaje na kadhalika. Sasa ni maelfu ya watu.

Mheshimiwa Spika, kelele zinakuwa nyingi. Ukikuta Jimbo lina watu karibu laki tano, wazazi na sisi kule ni mafundi wa kuzaa, haya niambieni hizo kelele zinakuwaje? Haiwezekani hivi, ni lazima tuwasaidie watu na ndiyo kutekeleza kwenyewe Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Kwa hiyo suala la ilani tuliyopewa kuinada lazima itekelezwe ili huko baadaye pia mambo yaweze kukaa vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kwa kusema kwamba ni vizuri hawa watu wa Bodi ya Mikopo wakubali mabadiliko, kuna malalamiko bado yanakuja tu, yaani malalamiko wasijione Miungu watu, wanatakiwa kuwa na changes. Utumishi wa sasa hivi ni utumishi wa service delivery, kauli nzuri na mambo mengine, unapigiwa simu na mtu amekwama badala umfafanulie vizuri unamwambia kamalize huko huko tumeshawapa maelekezo mpaka vijijini, Mtendaji wa Kijiji anajua taratibu za mikopo kwa undani? Wewe kama umepata fursa ya kutumikia watu watumikie. Kwa hiyo nataka wajirekebishe kwenye masuala yao ya maadili, huko nako wanalalamikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nimesimama mbele ya Bunge lako kwa heshima kubwa. Awali ya yote nianze kuwapongeza sana Ofisi Rais TAMISEMI, Mheshimiwa Waziri hongera sana Manaibu wako wote wawili ni watu ambao wanatupa ushirikiano wa kutosha tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, pia nisisahau kumpongeza mshauri Mtendaji Mkuu wa Wizara Profesa Shemdoe pamoja na timu yake yote, nisiwasahau Ndugu Seif pamoja na DID Ndugu Moga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu kwanza nimeanza kwa kuwapongeza kwa sababu ninakiri kwamba kazi iliyofanyika na TAMISEMI ni kazi kubwa sana, kazi hii imefanyika kwenye Majimbo mbalimbali katika nchi yetu ya Tanzania. Mfano, kwangu Kaliua wamenisaidia mpaka sasa tunapoongea tumemaliza hospitali ya Wilaya karibu Bilioni 2.2, tunaendelea na ujenzi wa vituo vya afya viwili Shilingi Bilioni Moja, lakini tunaendelea na zahanati nane za ujenzi, ndiyo maana nasimama na kusema siyo hiyo tu hata barabara kazi iliyofanyika ni kubwa sana na nilikuwa najiuliza hawa mabwana hii teamwork wanaitoa wapi. Nikagundua inawezekana hawa ni mashabiki wa ile timu ya nguvu moja ile, ndiyo maana mambo yanazidi kuwa mazuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Wabunge wenzangu kuweka msimamo mkubwa sana kwa Waheshimiwa Madiwani. Waheshimiwa Madiwani wanaishi mazingira magumu sana, wapo Madiwani kutoka Kijiji mpaka Kijiji ni kilomita 60. Kwa mfano, kwangu kuna Kata inaitwa Ukumbisiganga kutoka Ukumbisiganga mpaka Usinga kilomita 48, Diwani anatakiwa ahudumie wananchi kule. Anahudumia vipi hana pikipiki, posho 350,000 kwa kweli mfumuko wa bei upo, hii hali kwa nini tuiangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawiwa kuishauri Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, nawaomba kwa heshima zote tuhakikishe Madiwani tunawapandishia posho zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nina ushauri mkubwa sana sehemu ya Kamati zile za kwetu kule Halmashauri, Kamati ya Elimu, Afya na Maji na Kamati ya Uchumi, Ujenzi na Mazingira. Kamati hizi hazikagui miradi kwa sasa, kwa nini Kamati ya elimu, afya na maji haikagui miradi yake ya elimu, miradi yake ya elimu na miradi yake afya. Kwa nini Kamati za uchumi hazikagui miradi ya kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo mliyoutoa TAMISEMI hapo nataka niwashauri mlielekeza Kamati ya fedha ndiyo ikague, hizi Kamati zingine wanapokutana kwenye vikao tumewanyima ownership, wanatakiwa wafahamu nini kinaendelea kwenye maeneo mengine. Kwa hiyo, nashauri mtoe mwongozo angalau mara mbili kila mwaka hizi Kamati za Elimu, Afya na Maji na Kamati za Uchumi, Ujenzi na Mazingira zikague mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri jambo lingine kwenye upande wa TARURA, bararaba mtandao wa barabara kwangu ulikuwa kilomita 1,370 sasa vijiji 26 Mheshimiwa Rais kaviachia, sasa mtandao umeongezeka tuna kilomita 2,370 naomba tuangalie zile bajeti zetu za maintenance pamoja na mambo mengine ili kuhakikisha tunaisaidia TARURA vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizugumzie suala la Watumishi, nimeongea mazuri yaliyofanyika lakini haya mapya yote yaliyofanyika zikiwemo shule shikizi zinahitaji watumishi, zinahitaji walimu, zinahitaji watumishi wa Idara ya Afya, zinahitaji Maendeleo ya Jamii. Naomba kwa hekima zote, niwaombe Serikali yangu Sikivu ya CCM tuhakikishe tunawapata watumishi hawa ili kuhakikisha tunakuwa na kauli moja ya kusaidia nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nimalizie kwa kuomba jambo moja, TARURA hawana vifaa vya maabara hebu TAMISEMI wazungumze na watu wa ujenzi. Miradi inapokamilika yale majengo yaachwe kwenye Halmashauri husika, kinyume cha kuyaacha hayafanyi chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kwangu Mkurugenzi alishaomba TARURA wakitumia yale kama Ofisi na vile vifaa vya maabara Mratibu wa Mkoa wa TARURA hana vile vifaa. Barabara zetu tunazipimaje? Ni kwa nini tusiweke uratibu mzuri wa vifaa ili barabara zetu zipimwe vizuri na tuweze kujua na kuzijenga kwa ubora unaotakiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nakushuru, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nichukue nafasi hii nikushukuru sana wewe kunipa nafasi nzuri ya kuchangia lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dokta Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri na kuhakikisha nchi yetu iko salama, miradi inakwenda na hakuna mradi uliosimama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nimpongeze Waziri pamoja na Naibu Mawaziri wake wote, pia niwapongeze watendaji wote, nisimsahau Mtendaji Mkuu wa TANROADS pamoja na Meneja wa Mkoa wa Tabora. Meneja wa Mkoa wa Tabora anafanya vizuri sana na sisi Wanatabora, Wanakaliua tunamshukuru sana kwa kazi nzuri anayoifanya katika Mkoa wetu wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mazuri nimeanza kupongeza kwa sababu kazi zinazofanyika Kaliua ni kazi ambazo hazijawahi kufanyika kwa miaka yote iliyopita. Kaliua kwanza tumenufaika kuna barabara inatokea Kaliua kwa maana ya Chagu - Kazilambwa ya kilometa 36. Mheshimiwa Rais wetu ameleta shilingi bilioni 38 na barabara sasa hivi iko zaidi ya asilimia
90. Kwenye miradi ya reli SGR, ule Mkataba wa Tabora – Kigoma unapita Kaliua lakini ukarabati wa reli ya Kaliua – Mpanda unakwenda vizuri. Hii ndiyo sababu ya mimi kuanza kupongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi chini Mwenyekiti wake, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Waziri mambo machache, jambo la kwanza kabisa pamoja na kumshukuru ninavyomwambia kwa sasa tunaendelea na kufunga taa pale Kaliua Mjini, lami sehemu kubwa imekamilika na wanaendelea na ufungaji wa taa kutoka relini Kaliua mpaka Kasungu na kwenda kwenye T. Zoezi hilo linatekelezwa na Mkandarasi mzalendo SAMOTA na nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkandarasi yule kwenye Mkoa wa Tabora amefanya kazi kubwa sana, ukiangalia barabara ya kutoka Urambo kwenda Kaliua ni Mkandarasi huyo aliyeweza kuijenga. Wakandarasi hawa hebu muwa-empower mhakikishe kama wana madeni wanalipwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kubwa kwa Mheshimiwa Waziri, pale Kaliua ile barabara yetu ya mchepuko kutoka Ushokola relini pale kwenda mpaka njiapanda ya kuunga Urambo zimebaki kilometa 2.3, nimeona kwenye bajeti inayoanza mwezi wa Julai mmeweka kilometa moja, Mheshimiwa Waziri nikikuangalia hivi najua ni material ya Kinyamwezi kabisa, kwa heshima zote nakuomba mwezi Julai tunapoanza ile kilometa moja hebu ongezeni ziwe kilometa mbili zikamilike ili mimi nitakaposimama mwakani tunasogea sogea kwenye mambo ya uchaguzi tuendelee kuimba CCM hoye, iyena iyena au siyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ombi langu la kwanza linagusa Ushokola na ni hilo kubwa sana, Mtendaji wako ana taarifa zote na Meneja wako wa Mkoa wa Tabora anafahamu hili. Kwa hiyo, ombi langu la kwanza ni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili kubwa Mheshimiwa Waziri linagusa barabara ya kiuchumi, barabara ya kutoka Mpanda – Kaliua – Kahama. Mheshimiwa Waziri barabara hii imewekwa kwenye Ilani zaidi ya mara tatu na mimi sitegemei nimebakiza miaka miwili kwenye kipindi hiki niendelee kuona maneno. Mimi ni muumini wa utekelezaji naamini na wewe ndivyo ulivyo. Nikuombe kwenye bajeti ya Katavi mmeweka ujenzi wa daraja, ninaomba daraja hilo lianze mara moja isiishie kwenye kuandika bila utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge wa Katavi nimeona anaongelea jambo hilo na mimi naungana naye, tuko pamoja tunategemea mazao ya tumbaku kutoka Mpanda kuja Kaliua kwenda Tabora na maeneo mengine yawe safari nzuri kabisa bila wasiwasi wowote. Pia mazao ya asali tunayategemea sana lakini mazao mengine ni mahindi pamoja na mchele. Niwaombe sana mhakikishe barabara hii inakamilika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri juzi tulikaa na wewe hapa wiki iliyopita, ile barabara ya kwenda Kigoma zile kilometa 36 nilizozieleza, ule mchepuo wa kwenda Ugansa – Usinge ndiyo kilio kikubwa cha Wanakaliua. Mchepuo ule barabara iko chini ya ufadhili wa OPEC kama sikosei. Ulimpigia simu Mtendaji Mkuu na Mtendaji Mkuu akasema hana shida, leo mpo watatu hapa pamoja na Meneja wangu hebu malizeni jambo hili. Fedha ipo kwa nini wasianze? Wazee wa Usinge wanapiga simu kila siku hata hapa nikwambie tu nimepokea simu nyingi sana na nitawataja hawa wazee ili furaha yao ikamilike kwamba Mbunge wao Kwezi nimetamka kwako kwamba ile barabara ya mchepuo ya kilometa Saba inakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wazee hawa walionituma ni George Kamsini, Mzee wa pili aliyenituma ni Juma Kitakala, Mzee wa tatu ni Malabe, Mzee wa nne ni Mademo, kijana Kakobe, Mama yangu Mama Mau na Rehema Hamisi wamepiga simu leo, wanataka lami Usinge. Mheshimiwa Waziri kilometa saba kitu gani na fedha ipo? Mtendaji Mkuu tena nimpongeze Mtendaji Mkuu ni msikivu sana, hata usiku ukituma message anajibu. Mtendaji Mkuu nakwambia Meneja wa Mkoa wa Tabora yuko hapa, mkitoka hapo nje anzeni na Kaliua tafadhali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwathibitishie sisi Kaliua tuko na nyie, wilaya iko makini, iko salama chini ya Mkuu wa Wilaya yetu Rashid Chuachua anasimama vizuri, hakikisheni jambo hili limekwisha, mnampa kero. Mnanipa kero, mnampa kero Mwenyekiti wangu wa Mkoa wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuongelea ni suala zima la reli. Jamani, Kaliua pale ni njiapanda kama ilivyo njia panda Tabora na kwenye upande wa reli ni vivyo hivyo. Niwaombe sana hizi ajira zinazojitokeza hakikisheni wenyeji wamepata ajira hizi, vijana wa Kaliua wapo wa kutosha, vijana wa Mpanda wapo wa kutosha, vijana wa Kigoma wako wa kutosha kwa sababu hizo reli zinatunufaisha wote. Wasihame na watu kutoka mbali sana kuhakikisha wanapata pale. Hata ule ukarabati fuatilieni ule ukarabati wa Kaliua – Mpanda tunahitaji wenyeji wapate. Zipo kazi ambazo hazihitaji shule, zinahitaji nguvu. Si mnasemaga mizigo mizito wape Wanyamwezi? Sasa mnakwepaje mnahama na watu? Niombe mlifuatilie hilo Mheshimiwa Waziri, tufanye kazi kwa pamoja tuhakikishe tunafaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa kwenye reli ambalo ni la mwisho kwangu nilikuwa naomba kuna vituo kabla ya stesheni na stesheni pale kati kati wanatozwa faini wananchi wanapovuka kutoka vijiji ‘A’ kwenda vijiji ‘B’ naomba ufuatilie jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, Mheshimiwa Waziri nakutegemea sana, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba nichukue nafasi hii kwanza kukushukuru kunipatia nafasi ili niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara yetu ya Maliasili na Utalii. Lakini awali ya yote nianze kwa kuwapongeza sana Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea nayo. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wakurugenzi wote wa taasisi zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naanza kwa kuwashukuru kwa sababu Kaliua ni miongoni mwa maeneo ambayo yamepakana na Hifadhi kubwa mbili, kwanza tuna Ugara National Park, lakini pia tunayo Kigosi, lakini tuna TFS na tuna TAWA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ile timu ya Mawaziri nane ilipita katika Wilaya yetu ya Kaliua na tumenufaika kwa sababu sehemu kubwa ya changamoto imeweza kutupunguzia. Wilaya yetu takribani vijiji 26 vilikuwa kwenye hifadhi, lakini kwa kazi nzuri iliyofanywa na timu hiyo, sasa wananchi wale wako huru na tunajipanga kwenda kwenye matumizi bora ya ardhi katika vijiji vyetu. (Makofi)

Mimi nina machache ambayo ningeweza kuyashauri, kwanza kwenye Hifadhi ya Ugara; Hifadhi ya Ugara ni Hifadhi mpya, lakini hifadhi hiyo mpya mimi nimekwenda kutembea na timu mbalimbali ya uongozi wetu wote wa wilaya tumekuta hifadhi ile ni nzuri sana na inavivutio vizuri sana. Mimi nilikuwa napenda niishauri Wizara kuwekeza nguvu nyingi kwenye ukarabati wa miundombinu na miundombinu ambayo tunaomba kwa Hifadhi ya Ugara ni barabara nzuri ifike Ugara National Park, lakini miundombinu ya mawasiliano, miundombinu ya internet na miundombinu ya hoteli na camps mbalimbali. Nalisema hili sio kwa maana ya Ugara peke yake, lakini ukienda Kigosi miundombinu ya kuingia Kigosi ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado ukienda Katavi miundombinu ya kuingia Katavi ni shida, ukienda Biharamulo pale Burigi Chato hiyo yote miundombinu ni shida. Lakini ukiangalia ukanda wote ambao nimeutaja unaweza ukafanya vizuri kama inavyofanya vizuri ukanda wa Kaskazini, lakini tunaendelea kuangalia tukiwekeza fedha nyingi ukanda ule wote umepakana na nchi mbalimbali, Uganda jirani zetu, Congo jirani zetu, Burundi jirani zetu. Sasa nchi hizi zote zingeweza kutuletea tija kwa sababu vivutio tulivyonavyo huko ni vizuri na tukivihamasisha vizuri tukavitangaza vizuri nina uhakika ule ukanda wote utafunguka vizuri sana. Kwa sababu unakuta kutoka Burundi mpaka unaingia Hifadhi kilometa 30, sasa kwa nini hatujatangaza kwa kiwango ambacho ni kizuri na kiwango kikubwa zaidi? Nilikuwa nashauri miundombinu ile kwenye hifadhi zote ambazo nimetaja iboreshwe na twende kwa kasi zaidi kama Mheshimiwa Rais anavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine nilikuwa naliomba ni kwenye marekebisho ya mipaka, ni kweli tumepita, vijiji viko huru, lakini baadhi ya maeneo bado urekebishaji wa mipaka bado migogoro haijaisha. Kwa mfano, Igagala Namba Nne hicho ni kijiji, Ugansa bado, Usinge bado, Luganjo Mtoni bado, Kombe bado; nilikuwa naomba maeneo haya wayape kipaumbele, ili kuhakikisha sasa wananchi tunaishi kwa furaha kwa amani tukiendelea kulinda hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tabora ni miongoni mwa mikoa ambayo inazalisha asali na uzalishaji mkubwa umepakana na hizo hifadhi. Sasa nilikuwa nawashauri kwanza naomba tupewe muda kwa sababu kuna eneo ambalo limeongezeka la TFS likaenda Ugara sisi kule kuna mizinga. Tunaomba tupatiwe angalau miezi miwili wale wananchi wavune na waweze kutoa mizinga yao, hilo ndilo ombi ambalo ningependa mliangalie kwa ukanda mzima wa Urambo, ukanda mzima wa Kaliua na ukanda mzima wa kuelekea njia ya Ushetu pote humo ni wafugaji wa nyuki. (Makofi)

Ushauri wangu mwingine ni kuhusiana na utalii wa ndani; Mheshimiwa Rais ametusaidia kwenye Royal Tour kwa maana ya kutusaidia kufungua huko, lakini tunapopata janga sisi wa ndani tunakwama kwa sababu miradi mikubwa inategemea wafadhili. Ni kwa nini sisi tusijenge utamaduni wa kuhamasisha utalii wa ndani tukajengeka kifikra kuwa tayari kutembelea hifadhi zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri utalii wa ndani tuupe hamasa kubwa sana na mimi niwaombe Wizara watoe nguvu pale Kaliua ile hifadhi ukifika kule kwa kweli, kuna kivutio kikubwa, nilimuona Mr. Shelutete alikuja kama mara mbili, lakini nilipokuja kuangalia sikuamini, ile ni Kaliua kweli? Kwa sababu, ilikuwa ni vivutio vizuri kweli kweli, sasa sasahivi wananchi wamehamasika, lakini miundombinu bado nis shida. Niombe zaidi tuweke hiyo miundombinu ili tuweze kufikika kwa hali ambayo ni nzuri na hali ambayo itatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nashauri pia kuhusiana na askari wa maliasili. Natambua kabisa na wenyewe wanapata changamoto wapo askari wanauawa kabisa, lakini nilichokuwa nashauri mimi hebu tuwape mafunzo askari wetu namna gani bora ya kukabiliana na wale ambao hasa zile vurugu za kawaida za mipakani kwa sababu nguvu ikitumika kubwa malalamiko yanakuwa ni makubwa sana. Nashauri tuboreshe mahusiano zaidi kwa maana ya kuwapa mafunzo ambayo sio lazima watumie silaha peke yake, lakini hata kuelimisha kwa maana ya kutujengea mahusiano mazuri na hifadhi zetu zitakuwa ni endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja, nimalizie; Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja Kaliua, Kaliua tulikamata magogo pale tukauza shilingi bilioni moja na nusu, Waziri Mkuu aliahidi kile kijiji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30, malizia sentensi.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, Kijiji cha Wachawaseme wapewe zahanati yao. Mkurugenzi wangu ameshaleta ile bill ya zahanati pale, mpaka leo tumepata shilingi bilioni moja na nusu, zahanati karibu shilingi milioni 70 bado hamjatuletea.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)