Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Questions to the Prime Minister from Hon. Edward Olelekaita Kisau (1 total)

MHE. EDWARD K. OLELEKAITA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nishukuru kwa majibu mazuri sana ya Serikali na yenye kutia moyo.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kama tuna majengo ambayo yana hadhi yuko tayari kununua vifaa, je, atakuwa tayari hata ndani ya Bunge hili wakati linaendelea, kutembelea Kiteto ukiongozana na mimi kukagua baadhi ya majengo tuliyonayo ili tuweze kuangalia kama hilo linawezekana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Vyuo vya VETA ni muhimu sana kwa taifa letu na hususan kwa vijana; na kwa kuwa Wilaya ya Kiteto ni wilaya kongwe sana nchini, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuwahakikishia wananchi wa Kiteto kwamba Wilaya ya Kiteto VETA iko kwenye priority list na Chuo cha VETA kitajengwa kwa manufaa ya Taifa letu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Olelekaita, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la kutembelea Kiteto liko wazi, nitamuomba Mheshimiwa Mbunge baada tu ya kikao hiki tuweze kuonana ili kuiweka ratiba yetu vizuri ya kwenda kuona huko Kiteto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili alilolizungumza ni dhahiri, nilibainishie tu Bunge lako Tukufu kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi kwamba Serikali ina azma thabiti ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga vyuo vya VETA katika kila wilaya na mkoa nchini.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, vijana wetu hawa pamoja na kupata taaluma katika vyuo hivi vya VETA, tuna vyuo vyetu vilevile vya FDC. Mfano, hukohuko Kiteto Chuo cha Wananchi cha Tango kinafanyiwa ukarabati mkubwa na kitaanza kutoa fani za mifugo, kilimo, umeme, ushonaji na uwashi. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge vijana wetu sasa wanaweza kwenda kujipatia taaluma zao pale, lakini tuna vyuo vingine vya VETA vilivyoko katika Mkoa wa Manyara ambapo napo vilevile wanaweza kwenda kupata mafunzo hayo. Hata hivyo, suala la mpango wa Serikali wa kujenga vyuo vya VETA katika kipindi kijacho tutakapopata fedha tutahakikisha tunapeleka chuo katika Wilaya ya Kiteto. Ahsante.