Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers from Prime Minister to Hon. Prof. Shukrani Elisha Manya (2 total)

MHE. ANTON A. MWANTONA Aliuliza:-

Je, ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2019 ya kufufua mradi wa uzalishaji wa makaa ya mawe Kiwira itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nami kwa vile nasimama kwa mara ya kwanza mbele ya Bunge lako Tukufu, nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia Mheshimiwa Rais kwa imani aliyonipatia kutumika katika utumishi huu mtukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira ulikabidhiwa Serikalini kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) mwaka 2013 kwa lengo la kuuendeleza. Katika jitihada za kuuendeleza mgodi huo ambao ni wa chini ya ardhi, STAMICO, kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wanaendelea na mpango wa pamoja wa muda mrefu wa kuzalisha umeme zaidi ya MW 200 kutoka katika mgodi huo. Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) yako hatua za mwisho kukamilika kabla ya kuwasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa mapitio.

Mheshimiwa Spika, tayari timu ya wataalamu wa STAMICO na TANESCO wametembelea eneo la mradi kwa lengo la kutambua mahitaji halisi ya uendelezaji wa mradi huo. Aidha, maandalizi ya kuhuisha taarifa ya upembuzi yakinifu ya mradi ya mwaka 2007 yanaendelea. Katika taarifa hiyo, tathmini ya awali inaonesha kwamba jumla ya mashapo yanayokadiriwa tani milioni 93 yapo katika eneo hilo na gharama zinakadiriwa ni jumla ya Dola za Kimarekani milioni 480 ambazo zitahusisha kuchimba makaa ya mawe, kujenga mtambo wa kuzalisha umeme na kujenga njia ya kusafirisha umeme kutoka eneo la mradi yenye urefu wa kilometa 100.

Mheshimiwa Spika, malengo ya muda mfupi ni kuendelea na uchimbaji wa makaa ya mawe kwa matumizi ya viwanda vya ndani na nje ya nchi. Kwa sasa uchimbaji huo unaofanywa na STAMICO unaendelea katika eneo la Kabulo ambapo tangu mwaka 2017 uchimbaji ulipoanza hadi kufikia Desemba, 2020 Shirika limezalisha tani 50,949 za makaa ya mawe na kuuza tani 29,686.56 zenye thamani ya shilingi 2,264,472,998.70. Baadhi ya makaa hayo yameuzwa kwenye viwanda vya simenti nchini vikiwemo viwanda vya Mbeya Cement, Lake Cement pamoja na kampuni ya Sanflag ya Jijini Arusha.

Mheshimiwa Spika, Shirika limefanya tathmini ya ukarabati wa miundombinu ya mgodi wa chini wa Kiwira kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa makaa ya mawe ili kuendelea kuvipatia viwanda malighafi hiyo, lakini pia ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzalishaji mkubwa kwa ajili ya mitambo ya kuzalisha umeme pindi makabuliano na TANESCO yatakapokamilika. Aidha, shirika liko katika maandalizi ya mwisho ya kuanza ukarabati wa miundombinu hiyo. Ahsante.
MHE. BRYCESON T. MAGESSA Aliuliza:-

STAMICO inamiliki maeneo yenye dhahabu lakini haiyatumii huku wachimbaji wadogo wakiwa hawana maeneo ya kuchimba.

Je, kwa nini Serikali isiwapatie wachimbaji wadogo maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Tumaini Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa majukumu ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ni kuwaendeleza wachimbaji wadogo nchini. Katika kufanya hivyo Shirika limekuwa likifanya kazi kwa karibu sana na wachimbaji hao katika kuhakikisha kwamba wanaongeza uzalishaji katika maeneo wanayochimba. Kupitia mkakati huo, Shirika pia limekuwa likitoa maeneo yake kuwapatia wachimbaji wadogo kwa lengo la kuwaendeleza.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018, Shirika lilitoa maeneo ya uchimbaji kwa vikundi 15 vya wachimbaji wadogo vilivyoundwa katika eneo la Lwamgasa (Geita) kwa usimamizi wa viongozi wa Kijiji na Afisa Ushirika yenye ukubwa wa kilomita za mraba 0.08. Vilevile, mwaka 2019, Shirika liligawa pia eneo la leseni ya Buhemba kwa vikundi vya wachimbaji wadogo waliopo Ilasaniro Mkoani Mara lenye ukubwa wa kilomita za mraba 1.2 na jumla ya leseni ndogo za uchimbaji 15 ziligawiwa. Aidha, kwa kushirikiana na mbia Shirika lilitoa leseni tatu katika eneo lake la mradi wa Buckreef (Geita) kwa wachimbaji wadogo wa maeneo hayo yenye jumla ya kilomita za mraba 7.2.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo kwa sasa hakuna maeneo ambayo yanamilikiwa na STAMICO bila kuendelezwa. Shirika linaendelea kuendeleza maeneo yake kwa kufanya utafiti ili kujua kiwango cha mbale kilichopo kabla ya kuanza uchimbaji. Pia Shirika limeanza kuendeleza leseni yake ya dhahabu ya Buhemba kwa kushirikiana na mbia na uzalishaji unatarajiwa kuanza Septemba mwaka huu 2021. Ahsante.