Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Answers from Prime Minister to Hon. Prof. Shukrani Elisha Manya (2 total)

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nadhani kila mtu anajua faida ya mradi wa makaa ya mawe pale Kiwira Coal Mine. Kwanza huu mradi ulikuwa unazalisha ajira zaidi ya 2,500 kabla haujaisha na mara kwa mara suala hili limejadiliwa hapa kwenye Bunge lako tukufu. Mwaka 2006 iliahidiwa na Wizara hii kwamba huu mradi utaanza mara moja, chini ya Naibu Waziri kipindi kile, Mheshimiwa Dkt. Medard Kalemani; mwaka 2018 pia ikajadiliwa hivyo kwamba mradi utaanza mara moja, sasa hivi tunaambiwa tena kwamba wako katika hatua za mwisho.

Je, ni lini ukarabati wa mgodi huu wa mawe utakamilika na tunategemea kuajiri watu wangapi? Kwa sasa hivi katika sehemu hii ndogo tumeajiri watu 28 tu lakini capacity ya kwanza ilikuwa ni watu 2,500.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini Serikali itatoa ahadi ya uhakika kwa sababu 2016 tumeahidiwa, 2018 tumeahidiwa, sasa hivi tunaambiwa tena mradi utaanza; ni lini Serikali itatoa ahadi ya uhakika ambapo sasa tutapata ajira za kutosha kwa wananchi lakini pia tutapata za huduma za kiuchumi kwa Wilaya za Rungwe, Kyela pamoja na Ileje? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoa majibu katika swali la msingi, ni kweli kwamba Shirika liko katika maongezi na TANESCO ili kukamilisha hatua za mwanzo kwa ajili ya uchimbaji kuanza. Napenda Mheshimiwa Mbunge ajue kwamba taratibu za uchimbaji zinahusisha upembuzi yakinifu kwa sababu unapokuja kuwekeza unawekeza fedha nyingi. Kwa hiyo, tunapokuwa tunasema kwamba upembuzi yakinifu unafanyika, lengo ni kwamba tunapoingia katika uchimbaji tuweze kuingia kwa namna ambayo tunajua kile kilichopo, fedha inayoingizwa na hatimaye kupata faida.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tuko katika maongezi na kuhitimisha hatua hizi, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili litafanyika baada ya kuhitimisha hatua hizi za mwanzo. Ajira zinazotarajiwa kupatikana tunaweza tukazipata baadaye baada ya kuwa tumemaliza upembuzi wote yakinifu kwa ajili ya mradi.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa majibu hayo.
MHE. BRYCESON T. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, je, ni lini atakuwa tayari yeye na STAMICO twende kupitia katika maeneo ambayo mimi najua bado kuna tatizo ili tuweze kumaliza matatizo yaliyopo kule?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa STAMICO kazi yake, pamoja na majukumu mengine, ni kuwaendeleza wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo waliopo Busanda wengi wanabahatisha kujua dhahabu iko wapi. Je, ni lini STAMICO itakuwa tayari ama kuwakodisha vyombo au kujitolea ili waweze kutambua mahali wanapochimba kuna madini au hakuna badala ya kubahatisha?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge Tumaini Magessa kutoka Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya kikao hiki nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ipo tayari kutembelea Jimboni kwake na kuona maeneo wanayodhani kama yanahitaji kugawiwa kwa wachimbaji wadogo au la.

Mheshimiwa Spika, lakini pia Mheshimiwa Mbunge ajue kwamba Serikali imeendelea kuyatoa haya maeneo kila inapoona kuwa inafaa. Nadhani hata yeye mwenyewe katika jimbo lake ni shahidi kwamba maeneo mengi yameendelea kutengwa na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imewathamini sana wachimbaji wadogo na ndipo wakati ambapo wachimbaji wadogo nchini wamepewa maeneo mengi sana kwa ajili ya kuchimba.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, sasa hivi Serikali inaendelea kuimarisha Shirika letu la STAMICO na siku za karibuni shirika limeweza kununua mitambo ya drilling ya kwake yenyewe. Kwa jinsi hiyo, tunaamini kwamba jitihada hizi zinazochukuliwa na Serikali za kuimarisha Shirika la STAMICO zitawezesha sasa kuweza kupata namna ya kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa kufanyia utafiti ili sasa tunapoelekea maeneo yanayotengwa yawe ni yale ambayo yamefanyiwa tafiti na hatimaye kuwawezesha kuchimba kwa tija. Ahsante sana.