Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Prof. Shukrani Elisha Manya (14 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kujibu baadhi ya hoja ambazo zimechangiwa na Waheshimiwa Wabunge. Pia, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliotoa mchango wao.

Mheshimiwa Spika, utaona kwamba, wengi wa Waheshimiwa Wabunge wametoa michango ya kujaribu kuboresha na kuendeleza sekta yetu ya madini, wakitambua kwamba ni moja ya sekta ambazo kama ikisimamiwa vizuri ni kweli kwamba itachangia pato la Taifa kwa kadiri ya malengo yaliyo katika sera. Pia ni sekta ambayo katika nyakati ambazo hazitabiriki inaweza ikawa ndiyo sekta mkombozi kwa ajili ya kuchangia uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nitaanza na hoja ya Mgodi wa WDL ambao ni kweli kwamba umeacha uzalishaji kwa muda. Pia ni kweli kwamba kuacha uzalishaji kwa Mgodi huu wa WDL ambao Serikali ina hisa, inatokana na sababu ambazo ziko nje ya uwezo wetu. Kwa sababu, janga la Covid 19 ndilo ambalo lilisababisha kuanguka kwa soko la almasi kwa sababu walaji wengi wa madini haya ya almasi walikuwa wako katika lock down na kwa jinsi hiyo wakawa wameshindwa kununua almasi na soko la almasi likaanguka. Hata hivi tunavyoongea, ni kweli kwamba soko hili halijatengemaa sana na hivyo linakuwa ni sababu ambazo ziko nje ya uwezo wetu.

Mheshimiwa Spika, napenda kupokea maoni ya Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ya Madini itakuwa bega kwa bega na kusaidia kuwezesha WDL ili kuweza kupata fedha katika benki zetu.

Mheshimiwa Spika, tukupe tu taarifa kwamba katika siku za karibuni benki zetu za ndani zimepata mwamko mkubwa sana wa kuona kwamba, biashara ya madini ni biashara inayolipa nao wameanza kuwekeza fedha katika sekta ya madini. Hili jambo halikuwa huko nyuma na tukubali kwamba, maisha ni dynamic, maisha yanakwenda, hatimaye benki zetu zimeelewa kwamba wanaweza wakakopesha wachimbaji nao pia wakapata faida na Wizara ya Madini iko nyuma ya Mgodi wa WDL na tunaamini kwamba wataweza kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuongea pia hoja ya Geological Survey ambayo imechangiwa na Wabunge wengi pia, kwamba Geological Survey ndiyo taasisi ya Serikali ambayo inaweza ikafanya utafiti na hatimaye kutoa takwimu na ramani za kuonesha wapi madini yalipo.

Mheshimiwa Spika, napenda kusema tu kwamba pia Serikali imeendelea kutambua umuhimu wa GST. Katika mwaka wa 2020/2021 GST ilipewa fedha maalum kiasi cha shilingi bilioni 3.3 na fedha hizi zilielekezwa katika kuboresha miundombinu ya maabara, vifaa vya ugani, ilipewa magari sita na pia vifaa vya kuratibu matetemeko ya ardhi na vifaa vya jiofizikia. Kwa mtindo huo basi, GST imeendelea kujizatiti kuona kwamba itaendelea kufanya utafiti na kutoa taarifa za awali na kutoa ramani ambazo kimsingi zinapatikana pale GST.

Mheshimiwa Spika, wawekezaji wakubwa wale ambao sasa wanaweza wakaja kuleta taarifa zinazotaka feasibility study wanaweza wakatumia taarifa hizo za awali na wana ramani na hatimaye kuwapa wawekezaji wakubwa ili tuendelee kupata madini mengine yaliyotafitiwa vizuri kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge wa Ngara amesema kwa ajili ya Tin, Tungsten, Iron pamoja na madini mengine.

Mheshimiwa Spika, pia katika habari ya utafiti wa GST ni kweli kwamba utafiti katika hifadhi zetu umeshafanyika mahali mahali na hivi tunajua kabisa mahali ambapo kuna madini katika hifadhi za Selous, Rungwa, Moyowosi, Lukwati, Kigosi. Hivyo, Wizara itawasiliana na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuweka utaratibu bora wa kuendelea kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais ili tuweze kufanya uchimbaji katika maeneo haya ya hifadhi huku tukizingatia usalama wa mazingira ya hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende pia kusema kwamba tayari GST imeona umuhimu wa changamoto za wachimbaji wadogo kwama sio wote wanaoweza kufika Dodoma na kuleta sample zao kwa ajili ya kufanya analysis katika maabara. Kutokana na hali hiyo, tayari GST imeanza kupeleka huduma za maabara na jiolojia katika maeneo ya Geita na Chunya kwa kuanzisha ofisi za muda, na zoezi hili litakuwa endelevu ili kuendelea kupeleka huduma katika maeneo ya uchimbaji.

Mheshimiwa Spika, napenda pia niongee hoja iliyoletwa na Mbunge inayohusu helium gas; ni kweli kwamba katika Ziwa Rukwa tunao wingi wa gesi ya helium na wakati mwingine tujue tu kwamba ipo katika hatua ya utafiti wa kina, maana utafiti hadi kufikia uzalishaji lazima upitie hatua. Kwa hiyo tunapoongelea geli ya helium ni kweli kwamba mwekezaji yupo, Kampuni ya Helium One ipo na walishafanya utafiti ule ya preliminary na sasa wapo katika infill drilling. Infill drilling ni kuonyesha kwamba baada ya kuona kwamba mashapo yapo, sasa wanakwenda katika hatua ya kuthibitisha. Sasa wakimaliza hapo ndipo wanapoweza wakaja na feasibility study ambayo sasa ndio itatuonesha jinsi uzalishaji utakavyofanyika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni kweli kwamba helium gas ipo, uzalishaji haujaanza na kabla ya uzalishaji kuanza ni kweli kwamba Wizara itatoa semina elekezi kwa watu wanaozunguka maeneo ya uzalishaji ili kwamba waweze kunufaika na gesi hii ya helium.

Mheshimiwa Spika, pia Wabunge wameongelea juu ya kwamba hatujaanzisha migodi mipya siku za karibuni, ni kweli na kwamba pia tumekuwa na utegemezi sana juu ya madini ya dhahabu; naomba nitoe mfano kidogo ambao unaweza ukaleta perspective katika eneo hili. Tuna Madini ya aina nyingi, makaa ya mawe tani moja ni Dola 45, kilo moja ya dhahabu ni Sh.140,000,000, kwa vyovyote vile wawekezaji watapeleka fedha zao katika madini yanayolipa. Kwa hiyo, kwa msingi huo ndio maana dhahabu imeendelea ku-attract investment kwa sababu ni madini yatakayolipa na kurudisha fedha haraka. Kutokana na hilo ndio maana yameendelea kuchangia kwa wingi katika pato letu linalotokana na madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuamini kwamba kwa kuingia ubia na Tembo Nickel tukaiingiza aina mpya ya madini katika uzalishaji wa nchi yetu, lakini pia napenda kuamini kwamba Serikali inafanyia kazi utoaji wa leseni mpya mbili siku za karibuni, ambazo ni Mradi ya Nyanzaga uliopo Sengerema kwa Mheshimiwa Tabasam lakini pia na Mradi wa Rare Earth uliopo Songwe. Kwa kuingiza miradi hii pia tutaanza kuingiza maingizo mapya ya uchimbaji na uzalishaji katika nchi yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Profesa.

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga hoja mkono. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi hii kukupongeza kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi kushika wadhifa huo na nikutakie kila la kheri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji napenda kujikita katika hoja ambayo inazungumzia dhana ya muunganiko pamoja na mwendelezo katika utoaji huduma ili kukuza uchumi. Lugha rahisi ni connectivity and linkages.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika sekta ndogo hiyo ya kilimo ya mazao ya bustani, maua, mbogamboga pamoja na matunda; kwanza ni sekta ambayo inakua kwa kasi, imeonekana ikikua kwa asilimia saba kulinganisha na kilimo chote kwa ujumla kikikua kwa asilimia nne, pia kinachotoa ajira nyingi kwa Watanzania na sasa inakadiriwa kwamba at least Watanzania milioni 6.5 katika mnyororo mzima wanashughulika na sekta hiyo ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuweka mkazo kwamba sekta hii ndogo ya maua, mbogamboga pamoja na matunda ni sekta ambayo ni logistic sensitive. Ninasema hivi kwa sababu tunahitaji usafirishaji kutoka kwa wazalishaji lakini je, ni wote katika mnyororo ule wanajua kwamba tuna- deal na perishable goods? Je, askari wetu barabarani wanajua kwamba hili ni kontena la maparachichi ambayo yanapaswa yafikie soko mapema? Je, tunapofika kwenye ports kuna handling facilities ambazo zitasaidia kutooza mapema kwa ajili ya bidhaa hizi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unagundua kwamba kama hii ni emerging market kwa sasa, lakini je, watu wote katika mnyororo mzima unaotaka tutoe kutoka uzalishaji kufikisha bidhaa yetu sokoni ikiwa katika hali njema wana ufahamu huo? Je, pale Mamlaka ya Bandari tutachukua siku chache kuliko msafirishaji wa copper kwa sababu hizi ni perishable goods? Je, ufahamu huo upo? Je, kuna facilities za ku-handle kwa sababu hiki ni kitu ambacho kinahitaji uharaka?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tunahitaji kuwa na connectivity katika sekta hii kwa sababu tusipofanya hivyo tutagundua kwamba tija yake inaweza isionekane mapema na ndiyo maana huenda hata takwimu za nini tunapeleka nje ya nchi kutoka kwenye hii sekta ndogo imesababishwa na kutokuwa na facilities, lakini wakati mwingine pia kutokuwa na wadau wote kuhusishwa ili tuweze kufikia malengo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa msingi huo ninapenda kuiomba Serikali pamoja na Wizara husika kwamba tunapokuwa na kitu ambacho ni emerging market kama hii hapa ili tuweze kupata tija maana yake ni kwamba lazima tuwahusishe wadau wote wanaohusika, kwanza kuwapa elimu hiyo, lakini pia kuwapa tahadhari kwamba hebu tusifanye yale mazoea, maana yake ni kwamba tusije tukawa tunachelewesha bidhaa zetu hatimaye zikaoza au zikaharibika ubora kwa sababu tu watu fulani anadhani kwamba anapaswa kwenda kama ambavyo nafanya bidhaa nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii mara nyinge imetokea katika bandari zetu, lakini pia katika airports zetu japo ni kweli kwamba kuna improvement sana kuwepo na standard cold rooms katika airport zetu kwa ajili hiyo, nadhani kwamba bado kunahitaji kuwa na sensitivity juu ya jambo hili ili tuweze kupata tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu naelewa dakika zangu siyo nyingi niliamua niongelee jambo hili tu kwamba hebu sasa Serikali kwa maana ya Wizara ya Kilimo ijue kwamba wateja wake ni wengi sana, iwape elimu, iwape msukumo ili kwa pamoja kusiwe na vikwazo katika kufikia soko ambalo tunalihitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuliweka mkazo juu ya yale mashamba ya Arusha ambayo hayafanyi kazi kwa sasa, Serikali ifikie kuleta suluhisho la jambo hilo ili tuweze kupata tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia taarifa yetu ya mwaka ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Nianze kusema kwamba naunga mkono hoja mapendekezo yote ambayo yamependekezwa kwa Serikali kwa ajili ya kuboresha Sekta zetu za ushalishaji.

Mheshimiwa Spika, nitaongelea mambo mawili au matatu kutegemeana na muda. Nianze kwa kusema kwamba athari za mabadiliko ya tabia nchi ni dhahiri sana kwa maana ya kwamba tumeshuhudia ukame mkubwa, vifo vya mifugo na wanyama na pia mvua kidogo, na hata zinaponyesha siyo kwa wakati na wakati mwingine zikinyesha, zinaleta mafuriko yote ambayo yameleta upungufu wa maji. Kwa jinsi hiyo, katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi, Serikali ikajielekeza katika ujenzi wa mabwawa ili kuhakikisha kwamba tunapata maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, maji kwa ajili ya umwagiliaji na maji kwa ajili ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, sasa hoja yangu iko katika utekelezaji wa jambo hili. Tunachokiona ni kwamba kwa sababu ya msukumo, kila Wizara sasa inakwenda na kujenga bwawa. Ukifika Chamakweza utakuta Bwawa la Mheshimiwa Ndaki, ukienda upande huu unakuta Bwawa la Mheshimiwa Aweso, ukienda upande huu unakuta Bwawa la Mheshimiwa Bashe, yaani Wizara tatu au nne zote zinaenda kujenga mabwawa ambayo design ni tofauti. Life time, yaani bwawa litakaa muda gani, wakati mwingine haijulikani. Standard ni tofauti, fedha inayotumika na viwango ukiyalinganisha pia ni tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuishauri Serikali kwamba ili tuweze kupata tija katika msukumo wa jambo hili, Wizara zote ambazo zinadhani kwamba zinapaswa kuwa na mabwawa kwa ajili ya kukabili athari za mabadiliko ya tabia nchi ziwe coordinated ili tupate sehemu moja ambapo tunapata design, itakayotusaidia kuelewa kwamba bwawa letu litadumu kwa wakati gani?

Mheshimiwa Spika, kuna mabwawa ambayo tumeyatembelea, yamejengwa mwaka 2022 lakini mwaka huu 2023 ng’ombe wameshapasua uzio na wanaingia ndani ya bwawa. Hiyo haiwezi kuleta tija. Kwa hiyo haya mambo yaweze kuratibiwa mahali pamoja ili tuweze kupata tija inayotokana na ujenzi wa mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine; katika ujenzi wa miradi mikubwa ya kimkakati ambayo tumeishuhudia Serikali yetu ikiyatekeleza, mingi sana ya miradi hii ni kwamba inajengwa na Wakandarasi wa nje. Utakuta mjenzi ni Kandarasi wa nje lakini hata mshauri wa mradi ni kandarasi wa nje. Hali hii inawanyima wakandarasi wetu wa ndani uwezo na ujuzi ambao ni muhimu sana kwa wakati ujao. Kwa sababu hata sisi tunatamani hapo baadaye kampuni zetu, za Watanzania ziweze kuwa na uwezo wa kufanya hii miradi mikubwa na ikiwezekana na sisi tuweze kupata kandarasi katika nchi za nje. Sasa hili halitawezekana iwapo kandarasi zote wanachukua wale wa nje na hakuna sheria inayombana yule kandarasi wa nje kumtumia mtu wa hapa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, fedha nyingi tunayoipata kwa njia ya mikopo na fedha ya kodi za Watanzania utakuta zote zinatumika kwenda nje ya nchi na hapa ndani tunabakia na fedha za vibarua. Sasa hili jambo tunadhani ni kwamba Sera ya Uwezeshaji ya Kitaifa ipo ya local content, kinachoonekana ni kwamba haisimamiwi vizuri au haitumiki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuiombe Serikali, tunaisihi sana Serikali katika hili iweze kuhimiza habari ya local content katika miradi mikubwa inayofanyika hapa nchini. Tungejikuta kwamba baada ya kumaliza ujenzi wote wa miradi hii kuna baadhi ya kampuni za Watanzania ambazo zimeshajijengea uwezo hata nao kuanza kuwa kampuni za Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hoja yangu hapa ni kwamba local content, Sera yetu ya Taifa iliyopo iweze kusimamiwa vizuri. Kwa sababu kwa jinsi ilivyo sasa hivi, haisimamiwi vizuri hata kidogo au haitumiki kabisa. Kwa hiyo, Watanzania na kampuni zao wanaendelea kuwa na kazi zile ndogo ndogo wakati zile zenye tija na faida kubwa zinaendelea kuwa ni zile za kandarasi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, tumeongea juu ya upungufu wa samaki Ziwa Victoria, na sababu zinaeleweka. Kuna uvuvi haramu wa kutumia matimba na wanaotumia matimba; matimba ni kitu kikubwa, siyo kitu ambacho kinafanyika kwa kificho. Pia, kwa sababu ya upungufu wa samaki ambao inasemekana Ziwa Victoria sasa samaki wazazi ni pungufu ya asilimia 0.4. Mazalia ya samaki kule ziwani yanajulikana yalipo, lakini yameshambuliwa, sasa haya yanafanya vile viwanda vya samaki pale katika Mwambao wa Ziwa Victoria yanakosa malighafi na kwa hiyo, hata ajira zinapotea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, itafikia wakati tulipokwa ni kinara wa kusafirisha minofu ya samaki nje ya nchi, hatimaye tutashindwa. Ninaloliona hapa ni kwamba kuna mambo mengine ambayo kunakosekana alertness (nakosa neno zuri la Kiswahili) upande wa Serikali. Kwa sababu kuna mambo ambayo huhitaji kujadili, unahitaji kuchukua hatua za haraka ili tuweze kuponyesha hali ya maziwa yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba alertness upande wa Serikali ichukue hatua za haraka na maamuzi ya haraka wakati mwingine ili tuweze kuokoa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, naona kengele yangu imegonga. Nakushukuru, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia katika Hotuba ya Bateji ya Wizara ya Maji ambayo kwa Mwaka huu wa Fedha inakwenda kutumia bilioni 709.36.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nipende kupongeza na kutambua jitihada za Serikali kupitia Wizara ya Maji, na hasa dhamira njema na utashi kwa Mheshimiwa Rais wa kuwapatia wananchi wake maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani pamoja na matumizi mengineyo. Ni jitihada hizi za Serikali ambazo sasa tunaona dhamira njema ya Mheshimiwa Rais. Tunaongelea Mradi Mkubwa unaotoa maji kutoka Ziwa Victoria kuleta katika Makao Makuu ya nchi hapa Dodoma. Hili linatambua neema ambayo Mwenyezi Mungu ametupatia, ukiiangalia Jiografia ya Afrika utagundua kwamba sisi ni moja ya nchi ambayo tumebarikiwa sana kuzungukwa na Maziwa Makuu matatu tena mojawapo ni Ziwa Tanganyika likiwa ni moja ya Ziwa lenye kina kirefu katika Maziwa ya hapa Duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pamoja na kwamba hesabu si nyepesi kihivyo lakini kutoka Ziwa Victoria kuja Dodoma ni kilomita 700. Ukichukua umbali huo huo kutoka Ziwa Tanganyika au kutoka Ziwa Nyasa utagundua kwamba kama tukivitumia vyanzo vikuu hivi vitatu nusu ya nchi ya Tanzania inapaswa kuwa supplied na maji bila kutafuta vyanzo vidogo vidogo vinavyokauka. Kwa hiyo, mimi nilikuwa napendekeza sana kwamba kwa dhamira njema ya Mheshimiwa Rais na utashi wa Serikali kama tumethubutu kubuni Mradi unaotoka Ziwa Victoria hadi Dodoma, utashi huo huo uelekezwe katika vyanzo vikuu vingine vya Ziwa Tanganyika ambalo ni Ziwa lenye kina kirefu, maji ambayo hayatakauka na Ziwa Nyasa na tuone kwamba vyanzo hivi vingine vidogo vidogo ndivyo vihudumie sehemu nyingine ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika maeneo matatu. Jambo la kwanza ni mfumo wa uondoaji maji taka pamoja na usafi wa miji. Hadi sasa kwa kadri ya ripoti ya Mheshimiwa Waziri ni kwamba tumefanikiwa kuwa na mifumo hiyo kwa asilimia 15 na kwamba lengo letu ni kwenda asilimia 30 ifikapo mwaka 2025. Na utangundua kwamba tuna miaka mitatu ambayo imebaki na sisi ndiyo tuko nusu ya mwendo. Sasa nipende pia kutambua kwamba kama hatuwezi kuwa na uondoshaji na mifumo mizuri ya kuondoa maji taka katika miji yetu, miji yetu inakuwa siyo misafi na ndiyo maana utakuta mito inayotiririka katika miji yetu siyo misafi. Lakini katika nchi za wenzetu maeneo ambapo unakuwa na baraka ya mto kupita katikati ya Mji ndiyo maeneo ambayo yamefanywa kuwa ya vivutio, sehemu za utalii na mito inajengwa kiasi kwamba hata boti zinapita, watu wanafanya sherehe mle. Lakini sisi kwa sababu ya kutokuwa na mifumo mizuri mito yetu inakuwa inatiririsha maji taka. Na hilo Mheshimiwa Waziri nilizani kwamba Serikali iweze kutoa msukumo mkubwa ili kwamba Miji yetu iweze kuwa misafi. Kwa hiyo, Wizara ya Ardhi hapa pamoja Mipango Miji watusaidie, wananchi wasitutangulie ili kwamba tunapopanga makazi basi na mifumo ile ya kuondoa maji taka iweze kupangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu mabwawa ya Kimkakati ya Farkwa pamoja na Kidunda; yameongelewa na Wabunge wenhgi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati miradi hii inaibuliwa ni kweli kwamba idadi ya watu katika miji husika ilikuwa ni ndogo. Sasa kama tunaiita kwamba ni miradi ya kimkakati maana yake ni kwamba hata tengeo lake la fedha linapaswa kuwa la kimkakati. Haliwezi kusubiri bajeti ya kila mwaka kwa sababu la sivyo idadi ya watu itazidi kuongezeka katika miji, watu watakosa maji na tutajikuta kwamba tunashindwa kuwa na miji ambayo ni salama ni misafi na pia miji inakuwa hailingani na maendeleo tunayoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili Mheshimiwa Waziri nilidhani kwamba hebu tuendelee kulipanga kimkakati, na hasa haya mawili; kwa sababu Farkwa inapaswa ihudumie hapa Makao Makuu ya Nchi, lakini pia Dar es Salaam tunaona kwamba idadi ya watu inazidi kuongezeka. Kama wewe mwenyewe ulivyosema chanzo cha Ruvu kilionesha kukauka mwaka uliopita. Kwa hiyo, hili lazima lipangwe kimkakati ili tuweze kuwasaidia wananchi wa maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda kuongelea ni ujenzi wa mabwawa wa ukubwa na malambo madogo. Tumeendelea kushuhudia kwamba utekelezaji wa miradi hii mingine inafanikiwa lakini mingine haifanikiwi; na ni kwa sababu miradi inakamilika halafu kiongozi wa kitaifa anakwenda kukagua anakuja kupewa taarifa ya kwamba mradi huu siyo thamani ya fedha. Sasa hapa nadhani tunapaswa Serikali ifanye mkakati kwamba tunapeleka fedha nyingi sana katika kujenga haya malambo. Sasa mimi pendekezo langu, ili isitokee Kiongozi wa Kitaifa anakwenda kwenye mradi halafu anakuta mradi umetengenezwa vibaya tuwe na kamati za continues monitoring and evaluation zinazohusisha viongozo wa Tamisemi; ili Waziri wa Maji anapokwenda au Waziri Mkuu anapokwenda kukagua mwisho wa wakati basi hata Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya pamoja na timu yote ya Tamisemi wanaweza kuwajibika kwamba tuliukagua kila wakati na hivyo tutaondokana na dhana ya fedha kutolewa lakini mradi unakuja kukataliwa kwa sababu fedha zimetumika vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama, Kamati hizi za Continues Monitoring and Evaluation zitakuwa zinagharimu fedha kidogo; tuzitumie ili kuepuka miradi kuja kukataliwa kwa sababu imekuwa inatumika vibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja na ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi njiweze kuchangia katika Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema tu kwamba sisi ni sehemu ya Umoja wa Nchi za Afrika ambao katika makubaliano ya Azimio la Malabo tulikubali kwamba, asilimia 10 ya bajeti iweze kutengwa kwa ajili ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kutenga bilioni 751.12 niongezeko la asilimia 255 ikilinganishwa na bajeti iliyopita. Ongezeko la asilimia 255 ni kweli kwamba ni la kupongezwa, linaonesha utashi na azma ya Mheshimiwa Rais ya kuboresha kilimo. Na tunatamani kwamba sisi kama signatories wa Malabo Declaration tufikishe asilimia 10, kwa sababu hii bilioni 751 ni asilimia 1.83 ya bajeti, ni kama tumeanza sasa kuipukuchua. Kwa hiyo tuombe sana kwamba, hebu matokeo yatakayotokana na ongezeko kubwa hili yasababishe Serikali kuona kwamba inafikia kiwango ambacho sisi tumekuwa tukikubaliana na wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi katika Kamati ya Kilimo tunaamini kwamba, kama kilimo kikipewa msukumo mkubwa kama ambavyo tumekubaliana, tunaamini kwanza nchi itajitosheleza kwa chakula na kubakiza ziada kubwa kwa ajili ya kuuzwa nchi za nje. Yaani watu wataamini kwamba, kama kuna dhiki na dhahama mahali fulani basi Tanzania ni mahali pa kukimbilia. Lakini pia uchumi wa wananchi mmoja mmoja na uchumi wa Taifa utakua kwa kiasi kubwa sana na nchi itakuwa inatatua tatizo la ajira kwa vijana. Na inawezekana hata tatizo la machinga ambalo limekuwa ni gumzo katika nchi likaondoka kwa sababu ya kuweka msukumo mkubwa katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna jambo tumejifunza sana kutokana na crisis ya Ukraine na Urusi ni kwamba kama nchi tunapaswa kujitegemea kujitosheleza kwa mazao ya chakula yale ya msingi lakini na mafuta ya kula. Hilo nadhani lisiondoke katika vichwa vyetu, tumejifunza kwamba wakati wa crisis ni muhimu sana uwe unajitosheleza kwa mahitaji yale ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo napenda kutambua na kupongeza jitihada za Serikali na azma ya Mheshimiwa Rais kupitia Wizara ya Kilimo kwamba imeamua kwa dhati kuimarisha utafiti, lakini pia kupima afya ya udongo. Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja na uongozi wote wa Wizara niwapongeze sana kwa msisitizo wa kusema kwamba watatoa ruzuku katika mbegu bora na kutoa ruzuku katika mbolea. Haya mambo yalipaswa kufanywa zamani, lakini kwa sababu tumekuwa na mwanzo basi tuendelee hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina hoja fulani ninayotaka kuiweka hapa, kwamba historia inakupa namna ya kujifunza kwa ajili ya leo, lakini pia na kwa ajili ya kesho na kwa sababu hii ni historia ya nchi yetu ukiangalia katika kilimo kumekuwa na cycle fulani ambayo nataka kuiweka hapa kama hoja yangu ya msingi. Hoja hiyo ni kwamba, nchi inaanzisha zao fulani inaliita zao la kimkakati na Serikali inatia nguvu, watu wanalima kwa nguvu zote lakini baada ya muda unashaanga tu kwamba zao lililokuwa la mkakati zao hilo linakufa. Halafu Serikali inakuja kulifufua tena na mfano ni zao la mkonge na zao la ngano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwamba baada ya mageuzi haya ambayo tumeyaanzisha sasa, hii cycle ikome, ifikie mahali tunaposema kwamba tunazalisha parachichi, tunazalisha ngano, tunazalisha zao Fulani, basi sisi tuwe kinara ili wakati wa crisis watu wajue kwamba tukienda Tanzania tunapata haya mazao. Kwa hiyo hiyo cycle ya kuanzisha, kufa, kufufua, kuanzisha, haitufanyi tukawa na maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni block farms. Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwamba katika hili natambua kabisa kwamba ni jambo la msingi, lakini hebu tuone kwamba vijana tena vijana halisi wanaoonekana ndiyo, waingie hapa pamoja na umuhimu wa kuwepo wawekezaji wakubwa lakini vijana tunajua kwamba watakuwa hawana mitaji, lakini Serikali inapaswa iwape upendeleo ili vijana hawa ndiyo waingie katika block farms kwa kufanya hivyo tutakuwa tumeondokana na tatizo la ajira za vijana ambao wanamaliza level mbalimbali za elimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kwa sababu ya muda ni kwamba kilimo ni ushindani na nchi jirani sisi tunapopanga hapa kwamba tuimarishe kilimo chetu na nchi jirani wanafanya hivyo hivyo na masoko yetu ni hayo hayo. Napendekeza hiki kitengo kisiwe ni Kitengo cha Utafiti lakini Wizara iwe na Kitengo cha Intelijensia kuangalia mwenendo wa masoko ili kwamba kama kunatokea tafrani mahali fulani basi kitengo hiki kinaweza kikatoa information ya namna ya kwenda. Kwa hiyo hiki tuweze kukifanya na tukifanya hivyo naamini kwamba nasi tutaendelea kuwa washindani katika soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hivyo, naomba kuunga hoja mkono ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hoja ya hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nipende kuipongeza Serikali kwa jinsi ilivyoandaa bajeti nzuri ambayo kweli kama itakavyokwenda kutekeleza kwa jinsi ilivyoandaliwa basi inakwenda kuleta tija na maendeleo makubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nitaongelea hoja tatu kama muda wangu utaniruhusu. Hoja ya kwanza ambayo napenda kuiongea katika Bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni kupongeza jitihada za Serikali katika kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili. Katika ukurasa wa 90 wa hotuba hii inasema kwamba; “Kiswahili kimetafsiriwa katika lugha rahisi katika vyombo vinavyo toa haki kwa maana ya Sheria ya nchi lakini pia Kiswahili kimeendela kufundishwa katika vyuo vikuu vya nje ya nchi.”

Mheshimiwa Spika, hili si jambo jepesi; na wote tunakumbuka kwamba Kiswahili kimeendelea kuwa nembo ya umoja wetu kama Watanzania lakini pia kimekuwa ndio msingi wa ustawi wetu kwa sababu sisi ni watu ambao tumetawayika sana kwa makabila na lugha zetu, lakini Kiswahili kimeweza kutuleta pamoja.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizi kubwa za Serikali mimi ninavyoangalia ni kama vile umahiri katika lugha yetu ya Kiswahili na hasa katika lugha andishi unazidi kushuka; na hii ni kwa sababu utagundua kwamba matumizi ya nahau, semi, misemo, methali katika watumiaji wa Kiswahili yanazidi kushuka.

Mheshimiwa Spika, niruhusu nitoe mfano mwepesi; ukiwaita vijana wa darasa la nne ambao tunaamini kwamba ndio wameweza kujua kusoma na kuandika halafu uwaambie hivi; ninaomba muniandikie jina la Mwenyezi Mungu Subhanahu Wa Ta’ala baadhi yao wataliandika hilo jina kwa herufi kubwa, lakini wengine wataliandika jina hilo hilo lakini kwa herufi ndogo, na sisi wote tunajua kwamba jina ambalo ni kuu kiasi hicho linapaswa kuandikwa kwa herufi kubwa na ni makosa sana katika vitabu vya dini kulishusha hadhi ukaliandika kwa herufi ndogo.

Mheshimiwa Spika, lakini msingi wa hoja yangu ni nini? Ni kwa sababu hawakujengwa kuelewa tofauti baina ya mambo haya; na sasa sisi tunataka kukipeleka Kiswahili chetu kama bidhaa kwa watu wa nje, sasa tunapelekaje Kiswahili kama bidhaa kwa watu wa nje kama sisi msingi wetu hapa ndani si mzuri?

Mheshimiwa Spika,kule kwetu Ukerewe iwapo unachochea viazi; maana viazi ni chakula kikuu kule kwetu; ukianza na moto mdogo mdogo baadae vile viazi hata ukichochea sana havitaiva kabisa. Maana yangu ni kwamba, kama msingi wa lugha ya Kiswahili utajengwa vibaya hapa chini katika shule za awali, maana yake tusitegemee maajabu huku juu.

Mheshimiwa Spika, na Waingereza walifanikiwa sana kukifanya kingereza kikawa ndiyo lugha takriban ya ulimwengu mzima. Sisi pia tunayo nafasi sasa. Yawezekana hii ndiyo nafasi yetu kama Watanzania kuifanya lugha yetu iweze kuwa ni lugha ya bara zima lakini pia iweze kuwa ni lugha ya mataifa mengine. Sisi ndio chimbuko, sisi ndio chanzo cha lugha hii ya Kiswahili. Kwa nini wenzetu majirani wafanye jitihada hatimae watupite?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi nataka kusema, kwamba tunahitaji kujenga msingi imara wa matumizi ya lugha ya Kiswahili katika ngazi zote kuanzia zile za awali; na ikiwezekana, na ikiwezekana tutumie nguvu kubwa kuwaomba wafundishaji wa Kiswahili wapigwe msasa ili watujengee watoto ambao wanaweza wakaongea kwa umahiri na wanaweza wakaandika kwa umahiri.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu huu usichukuliwe kama mjadala wa nini lugha ya kufundisha hasa katika Vyuo Vikuu, hapana. Mimi huwa si muumini wa mjadala huu, mimi ni muumuni wa kwamba kama mazingira yanaturuhusu tuwe mahiri katika lugha ya Kiswahili ambayo ni lugha yetu ya Taifa; lakini pia tuwe mahiri katika lugha ya kingereza ambayo ni lugha ya biashara.

Mheshimiwa Spika, na unapokuwa mahiri katika matumizi ya lugha unakuwa na ujasiri. Yaani huwezi kwenda mahali umeitwa ukaongee ukatoe muhadhara, ujasiri utakuja kwa sababu ya huo umahiri. Kwa hiyo hoja yangu hapa ni kwamba, tunayo nafasi kama taifa la kubidhaisha Kiswahili chetu na kwa jinsi hiyo tuichukue kwa jitihada unganishi. Kama ni vyuo, kama ni watunga Sera, kama ni wafundishaji basi tulishughulikie jambo hili ili hatimaye na sisi tuweze kupenyeza lugha yetu kuwa lugha ya kimataifa lakini iliyojengewa msingi imara.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia ni katika ukurasa wa 29 wa Bajeti ya Waziri Mkuu. Katika ukurasa huo tunapongeza jitihada za Serikali ambazo zimeelekezwa katika kuongeza bajeti ya kilimo, kupanua eneo la umwagiliaji na kuweka ruzuku katika mbolea na upatikanaji wa mbegu bora kama mahitaji muhimu ya kufanya kilimo chetu kiweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kuna jambo hapa ambalo huwa linasahauliwa na jambo hili ambalo linasahauliwa ni la mkulima yule mdogo mdogo. Hapa ndani ya Bunge utakuta kuna Wizara yenyewe inajinasibu na ni jambo zuri kwamba tunataka tumtue mama ndoo kichwani, jambo ambalo linapongezwa sana kwa sababu ni kweli Wizara ya Maji wamefanya jambo kubwa sana, lakini huyu mkulima mdogo nilitamani hata kama sio katika bajeti hii, tuje na slogan, tuje na usemi wa kwamba ni lini tutamtua mkulima mdogo wa nchi hii jembe la mkono?

Mheshimiwa Spika, lile jembe linafanya tu mikono inakuwa sugu, halina tija, yaani mtu analima hekari nyingi sana, anatumia muda mrefu sana na kula yake inakuwa ni ngumu na hawezi kupata maendeleo kupitia jembe hili la mkono. Kwa hiyo, mchango wangu ni kwamba kama haiwezekani katika bajeti hii, lakini tuje na Mkakati ambao utamtua mkulima mdogo wa nchi hii jembe la mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya tatu, naamini muda wangu unaruhusu ni matumizi ya mifumo ya TEHAMA. Serikali imefanikiwa sana na hasa ilipoanzisha mfumo ule wa GEPG katika makusanyo ya fedha za Serikali. Pia lengo lingine la kuwa na mifumo hii pamoja na kurahisisha kutoa huduma, lilipaswa kuwa ni kupunguza ubadhirifu kupitia mifumo hii. Sasa katika Ukurasa wa 70 katika hotuba ya Bajeti ya Waziri Mkuu wanasema kuhusu habari za rushwa, kesi za rushwa zilizoendeshwa mwaka 2022 ni 696 na 248 ziliamuliwa na 142 walikutwa na hatia”.

Mheshimiwa Spika, sasa katika utendaji wa Serikali Afisa Masuuli yeye check yake ni yule Mkaguzi wa Ndani, lakini pia Afisa Masuuli hawezi kuamua kutoa fedha katika akaunti ya benki bila kuwa na Mhasibu. Hivi kwa nini rushwa inaendelea kutawala? Kwa nini ubadhirifu unaendelea kuwepo? Je, ni kwa sababu hatua zinazochukuliwa ni kidogo? Je, hawa watu wanatoa wapi ujasiri? Kwa nini hawana hofu? Je, hatua zinapochukuliwa zinahusisha watu watatu au idara tatu ya Afisa Masuuli mwenyewe, ya yule Mkaguzi wa Ndani na yule Mhasibu wake wote wanashirikiana katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, tungetamani kuiomba Serikali, mifumo ya TEHAMA inayoanzishwa iweze kuwa na lengo la makusudi la kuhakikisha kwamba kila mtu anapata mrejesho ili kudhibiti ubadhirifu wa mali ya umma.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwamba, wakati mwingine mifumo hii ya TEHAMA inakuwa ndio sababu ya hasara kwa wananchi. Mfano mdogo kabisa, mfumo unakuwa uko down pale Bandari, kwa mfano, mtu anayetoa gari, halafu siku zikipita hasara inakuja kwa mwananchi wakati mfumo ulikuwa ni hasara ya Serikali. Hebu watusaidie mifumo iweze kuwa sababu ya kurahisisha, lakini pia kutoa huduma ambayo ni njema ambayo haimpi hasara yule ambaye ni mwananchi wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hivyo, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Makamo wa Rais Mazingira na Muungano. Mimi nitajikita katika sehemu ile ya Mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika,ni kweli kwamba suala la mazingira ni mtambuka, na kama walivyotangulia wenzangu lina gusa Wizara na taasisi mbalimbali za Serikali pamoja na Sekta binafsi; na kwa jinsi hiyo tungetamani hata kwa namna ambavyo suala la mazingira linashughulikiwa ndani ya Serikali liweze kuwa na mfumo ambao pia ni jumuishi; la sivyo likiachiwa Wizara moja kama Wizara moja tutaona kwamba athari zake zinaweza zisishughulikwe ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katika kuchangia hoja hii na mimi ningependa kuendelea kuweka msukumo zaidi, kwamba bajeti inayotengwa kutoka fedha za ndani kwa miradi ya maendeleo bilioni 1.6 dhidi ya bilioni 15 za wahisani nadhani hatujitendei haki. Tunapaswa tukubali kwamba wakati mwingine changamoto zinazotokana na athari za mazingira ni changamoto ambazo ni zetu binafsi kuliko hata zile ambazo zinatoka kwa fedha za wahisani na kwa hiyo tuombe Serikali; kwa mwaka huu kama ilivyopendekezwa sawa; lakini kwa miaka ijayo tuendelee kuweka msukumo wa kuongeza bajeti ili itusaidie kuweza kushughulikia hoja za mazingira ndani ya nchi yetu wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nipende kuwapongeza Serikali kwa jinsi ambavyo wamekuja na kampeni ya upandaji miti kote nchini. Lakini kampeni hii ingefanikiwa sana iwapo kungekuwa na mwongozo wa aina gani ya miti ipandwe kulingana na hali halisi ya maeneo husika. Kuna hatari ya kupanda miti katika vyanzo vya maji, na tunajua kuna miti ya mikaratusi, ukiipanda kwenye chanzo cha maji itanyonya maji yote na chanzo hicho kitakauka. Sasa tumeanzisha kampeni nchi nzima lakini mwongozo unachelewa. Tuwaombe Wizara waharakishe mwongozo kwa kuangalia ikolojia ya mahali husika ili wapande miti kulingana na mahitaji ya eneo husika, hilo litaweza kuwa na tija zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nilikuwa nikiwaza kidogo, kwamba kama tungekuwa tunafanya maamuzi haya ya kujumuisha pamoja; muda mfupi uliopita Serikali imejenga majengo mengi sana ya taasisi za Serikali kwa maana ya shule na hospitali; laiti tungeliongeza fedha kidogo halafu tukaweka mifumo ya ukasanyaji maji katika taasisi hizi maana yake ni kwamba tungekuwa na maji ya kutosha kwa ajili hasa ya kumwagilia miti hii ambayo tunataka ipandwe nchi nzima. Kwa hiyo wakati mwingine tunapokuwa tunakuja na hoja ambazo ni jumuishi tuone kwamba tunaweza tukalisaidia. Leo kama kila shule iliyojengwa ingekuwa na mfumo wa ukusanyaji maji au kila hospitali iliyojengwa ingekuwa na mfumo wa ukusanyaji maji tungeona kwamba maji yangekuwepo yakutosha. Hata kumwagilia miti itakayopandwa na hata ukame utakapokuja bado miti inaweza ikakua vile vile.

Mheshimiwa Naibu Spika, muda uliobaki naomba nichangie kuhusu uchafuzi wa mazingira katika maeneo ya makazi; na haya yanasimamiwa vizuri tu kwa bajeti iliyopo, kwa hiyo tunachosisitiza hapa na kuomba ni usimamizi wa taasisi husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni kelele na mitetemo katika makazi ya watu. Bado tunashuhudia katika nchi ambayo tuko katika uchumi wa kati, nchi ya wastaarabu baada ya saa nne usiku tunashuhudia kelele kutoka katika vilabu, kutoka katika nyumba za ibada. Sijui kuna shida gani katika hili, lakini sio sawa, kwamba katika nchi ya wastaarabu bado tuendelee kusikia mziki anao upenda DJ wa klabu husika wakati mimi siupendi mziki kwa wakati huo na ninahitaji kulala; na mara nyingi imetusumbua tunakwenda mahali kufanya kazi katika mji husika lakini unalazimika kusikiliza mziki uliochaguliwa na klabu hadi saa nane usiku, hili jambo halipendezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba tena kwa mara nyingine, NEMC wanaweza, mahali kwingine walikwenda na wakapiga stop na haikuendelea tena; lakini mahali kwingine wanatoa faini tu na bado watu wanaendelea kupigia watu kelele usiku. Tunadhani kwamba sisi ni nchi ya wastaarabu ambayo inapofika saa nne usiku hatuhitaji kuendelea kupigiwa kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, na hili nalo linahitaji usimamizi wa kawaida tu. Mfumo wa ukusanyaji wa taka ngumu. Nilikuwa nataka nipendekeze kwa Wizara na taassisi husika. Kwamba, mbona sisi katika nchi yetu leo bado tunachanganya maganda ya ndizi na ya viazi pamoja na chupa ya coca cola na heineken iliyoisha halafu wote unakuwa ni uchafu mmoja upelekwe dampo, kwa nini? Yani tumeshindwa kama nchi kutoa elimu ya kwamba taka zinazotoka jikoni zitengwe mahali fulani, chupa zitengwe mahali fulani hata basi ziende zikatumike tena. Ninadhani tutatenda haki sana iwapo tutawaambia wananchi wetu waweze kutenganisha aina ya taka za nyumbani ili kwamba ziweze kutumika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu viwanda. Viwanda vingi sana vimejengwa katika maeneo ya makazi, na wakati mwingine viwanda hivyo vinatoa moshi mzito na kutiririsha maji machafu katika maeneo ya makazi. Kwa mfano ni wakazi wa Kibangu Makuburi. Viwanda vile vilivyoko pale EPZA vinaendelea kutoa moshi mzito pamoja na kutiririsha maji machafu. Hili hebu NEMC walisimamie vizuri. Kupiga faini peke yake hakutoshi, unapiga faini leo lakini tatizo bado lipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, sijui kama ni mimi binafsi lakini nadhani kwamba Watanzania wote tunaona. Sasa hivi maeneo ya mjini, hasa katika Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani utagundua kuna vituo vya mafuta vinajengwa katika makazi ya watu kila baada ya mita 100, na wakati mwingine vituo hivi vya mafuta viko upande wa kushoto na kulia mwa barabara ya lami. Sasa unajaribu kujiuliza, kwa nini hali hii iko hivyo? Hivi hatuoni hatari ya kwamba vituo vya mafuta viko katika makazi ya watu na wakati mwingine havina hata uzio? Hivi ikitokea ajali ya moto tutasemaje? Kwamba ni kwa sababu hatuwezi kusimamia? Au ni kwa sababu tumeona hii hali ya kujenga holela ya vituo vya mafuta iendelee katika makazi ya watu? Sidhani kama hili ni jema kwa usalama wa Raia wa nchi yetu. Tunaomba sana Wizara husika iweze kulishughulikia kwa ufasaha. Utitiri wa vituo vya mafuta katika makazi ya watu katika jiji la Dar es Salaam si afya na wala si jambo la usalama kwa usalama wa raia.

Mheshimiwa Naibu Spika,baada ya kusema hayo najua muda wangu unakwisha, naomba niunge mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia hoja ya Waziri wa Madini ambayo inatamani tupitishe Bajeti ya shilingi 89.3 kwa ajili pia ya malengo makubwa ya kukusanya maduhuli yanayofikia Trilioni
1.006 na nitangulie kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kwamba kesho yetu ya madini kama sekta ni kesho njema na hivyo tuunge hoja mkono kwa kupitisha Bajeti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ambazo tumeshuhudia ukuaji wake mwaka hadi mwaka ni sekta ya madini na ni kweli kwamba kwa mwendo ambao tunakwenda nao ile asilimia 10 ya kuchangia Pato la Taifa kufikia Dira yetu ya Taifa ya mwaka 2025 itaweza kufikiwa bila shida. Hii inatokana na maono makubwa ya Wakuu wetu wa Nchi lakini pia na uongozi mzuri wa Wizara na Taasisi zilizo chini yao, pia na uelewa mkubwa wa wadau kwa maana ya wachimbaji wakubwa na wadogo pamoja na watu wote ambao wanajihusisha na sekta ya madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu nitoe pongezi za dhati na za pekee sana kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa diplomasia yake ya hali ya juu. Hii ni kwa sababu katika ile ziara ya Makamu wa Rais wa Marekani tulisikia ahadi ya kujengewa kiwanda kinachotengeneza betri kwa kutumia madini yetu ya nickel. Huu ni ukombozi mkubwa na lazima tumpongeze sana Rais jinsi ambavyo anajua kutumia diplomasia yake katika kuvutia uwekezaji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachochagiza ukuaji huu wa sekta pamoja na mambo mazuri ambayo tunayashuhudia ni pamoja na yale mabadiliko ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017. Ni kweli kwamba hatua kubwa imepigwa na hasa katika kuwawezesha Watanzania kushiriki kutoa huduma katika migodi lakini pia na kuwahudumia wachimbaji wadogo, kama kuna Wizara inatamani kujua namna local content inavyotekelezwa waende Wizara ya Madini. Kwa hiyo, hilo ni jambo la kujivunia na tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo katika miaka hii Sita ya kuwepo kwa Sheria ya Madini ni muhimu pia tukafanya tathmini kuona kama zile fikra tulizokuwa nazo mwaka 2017 zinatekelezeka zingine au zingine hazitekelezeki na kwa jinsi hiyo kuna mambo ambayo kama Wizara wanaona kwamba hayakuwa sawa na matarajio basi yanaweza yakaletwa ili kwamba yaweze kurekebishwa na moja ya mambo kama hayo ni leseni hodhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leseni hodhi zimerudishwa Serikalini kwa njia ya sheria lakini wawekezaji nao bado ni kama hawana ridhaa nalo, lakini pia wachimbaji wadogo wanaziangalia na kuzichokonoa fulani kwa hiyo unakuta kwamba siyo sisi wala Serikali wala wawekezaji wanaonufaika nadhani hili Mheshimiwa Waziri anaweza akaona kama ndani ya muda huu linamletea shida, basi anaweza likafanyiwa marejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wakati Tume ya Madini inaanzishwa ilileta pamoja watumishi ambao walikuwa na viwango tofauti vya mshahara, na ilitegemewa katika kuleta upatanifu na ulinganifu, wale wadogo wasogezwe katika wale waliokuwa na mshahara mkubwa, lakini jambo hili halikufanyika hivyo badala yake wale wakashushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linapunguza morale na wakati ambapo ndio watu unaowategemea waweze kukusanya maduhuli ya trilioni moja. Sasa hawa ni watumishi, walikuwa juu halafu wakashushwa na ukiangalia hiyo payroll kama mtu alikuwa ana commitments zake huko nyuma, wengine walipata mshahara negative (hasi), anaendaje kukusanya maduhuli huku hana fedha? Kwa hiyo, hili nadhani liko kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Simbachawene Wizara ya Utumishi hebu vuta mafaili ungalie hawa watu, kwa sababu pia wakati mwingine Serikali tujifunze kulipa ujira sawasawa na kazi ya mtu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anakwenda Mererani kilomita mbili anakwenda kuchukua Tanzanite ya bilioni tatu halafu anapoileta juu badala ya kuthaminisha mshahara wake unahesabika maelfu kadhaa. Nadhani tujifunze kulipa kwa kadri ya ujira wa mtu. Siyo sawa mtu aliyezama kilomita Mbili analeta madini ya thamani ya bilioni tatu mshahara wake mwisho wa mwezi unahesabika. Yeye si naye ana roho, nyama na damu jamani au? Kwa hiyo, hilo nadhani Mheshimiwa Simbachawene unaweza ukaliangalia hebu livute katika mafaili yako wasaidie hawa watumishi wa Tume ya Madini ili morale yao ipande ili waweze kukusanya maduhuli ya Trilioni 1.006. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije sasa kwenye hoja yangu ambayo nataka kuichangia asubuhi hii ya leo. Siasa za Kimataifa zina makundi ya wenye uchumi Nchi Saba tunawaita G7, pia siku za karibuni kuna kundi la watu wanaitwa BRICS hawa ni Brazil, Urusi, India pamoja na China na Afrika Kusini. Hawa watu katika kujaribu kuondoa matumizi ya dola kwa sababu ni kama ni makundi yanayoshindana wameamua kwamba wao watakalolifanya kubwa ni kununua dhahabu kwa wingi, kuweka akiba katika nchi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naleta siasa hizi za Kimataifa katika mjadala wangu asubuhi ya leo? Hoja hapa ni kwamba kama hawa ambao wanajaribu kuona kwamba ili uchumi wao uweze kutengemaa wanaiona dhahabu kuweka akiba kama njia ya kuimarisha uchumi kwa maana ya kwamba wakati ujao yawezekana nani ajuaye dola yawezekana isiwe na nguvu katika kufanya biashara ya Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni kwamba na kwa sababu pia sheria yetu inaturuhusu Kifungu cha 88 cha Sheria ya Madini, Kifungu Kidogo cha Pili kinasema mrabaha hapo mbele uweze kukusanywa kwa thamani ya madini yaliyosafishwa (refined gold) ili itusaidie na sisi kama nchi tuweze kuwa na akiba ya dhahabu, ili tuweze kulinda na kutegemeza uchumi wetu ambao unaendelea kukua siku kwa siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni kwamba dhahabu tunayo, refinaries, tunazo hebu sasa tufikirie yaani ifikie mahali tunapopanga mipango yetu ya uchumi na kuukuza basi tununue dhahabu na kuiingiza katika benki yetu ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu nyingine niongee habari ya Liganga na Mchuchuma kidogo, pamoja na kwamba inapenda kuongelewa katika Wizara ya Viwanda lakini bado ni madini na wala siyo bidhaa hadi pale yalipo kwa hiyo ni sawa tu kuiongelea katika muktadha wa madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Liganga kuna chuma, vanadium na titanium. Madini yote ambayo yana thamani kubwa sana, lakini pia Mchuchuma kuna makaa ya mawe mazuri kabisa na kimsingi ndio huwa kuelelezo cha makaa ya mawe katika mfuatano wa madini Tanzania. Sasa hawa watu walipewa leseni kwenye kampuni ya ubia mwaka 2014 na sheria zetu za madini zinawaruhusu angalau miezi 18 wawe wameanza uchimbaji hawajaanza.

MWENYEKITI: Malizia mchango wako Mheshimiwa muda wako umeisha.

MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninakushukuru kwa hayo, wakati mwingine Mungu akijaalia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Waziri wa Maji, ambayo anataka Bunge limuidhinishie bilioni 756.21 kwa ajili ya kuendelea kuwapelekea huduma ya maji watanzania. Nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, moja ya sekta ambazo zimeiheshimisha Serikali ya Awamu ya Sita ni sekta ya maji. Hii ni kwa sababu ya miradi mingi ambayo imekwenda moja kwa moja kwa wananchi na haya hayawezekani isipokuwa kwa utendaji mzuri wa watendaji wa Wizara, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote. Kwa msingi huo kwa kweli pongezi wanzozipokea wanastahili. Kwa mtindo wanaokwenda wanaitekeleza kabisa azma ya Mheshimiwa Rais, kuwatua wanawake ndoo kichwani na tunawaombea baraka zote za Mwenyezi Mungu juu ya hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitangulie kuunga hoja mkono kwamba Wabunge wote tuweze kukubali bajeti hii ya bilioni 756.21 iweze kwenda kuwasaidia wizara kutekeleza majukumu yao katika mwaka fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, ninazo hoja tatu za kuchangia katika hotuba ya Waziri asubuhi ya leo.

Mheshimiwa Spika, moja ni ambayo imezoeleka kwa lugha rahisi ya local content lakini kiswahili chake ni uwezeshaji watanzania kushiriki ujenzi wa miradi mikubwa ya maji. Katika hoja hii mara nyingi sana tunazo hoja mbili muhimu kwa nini watanzania au kampuni za kitanzania huwa hazipewi kandarasi katika ujenzi wa miradi mikubwa ya maji.

Mheshimiwa Spika, moja ni uwezo wa kitaalamu; pili, ni mtaji. Lakini kama nitakavyoongea haya mambo mawili yametuchelewesha na kwa misingi hiyo fedha nyngi imeendelea kupelekwa kwa kampuni za nje kumbe tunaweza. Kwa sababu gani ninasema hivi? Ukweli si kwmba hawana uwezo. Je, wamepewa nafasi kuonesha uwezo wao? Kamati yetu ya Maji na Mazingira ilitembelea mradi wa Dareda – Sigino – Singu – Bagala ambao pia unaleta maji katika Mji wa Babati. Tulichokiona Mradi huu ulisanifiwa na wazawa, wale wa BAWASA, wataalam wazawa lakini mradi huu pia umejengwa na wazawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu pia ukaokoa bilioni 15 ukatumia bilioni 12.7 badala ya bilioni 27 na unatekelezeka kwa ubora uleule. Hoja hapa ni kwamba kumbe wataalam wetu wanaweza. Tujifunze kupenda cha kwetu, kwa sababu mara nyingi sana tukikaa hapa tuna dhana ya kwamba watanzania hawawezi kumbe watanzania wanaweza kama watapewa nafasi, kama watawezeshwa hilo limedhihirika wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nampongeza Mheshimiwa Waziri, pomoja na menejimenti yake kwa kuwaamini watalamu hawa ambao wameweza kutekeleza mradi kwa uwezo mkubwa sawasawa na miradi mingine ambayo tumeitembelea. Na kwa jinsi hiyo liwe ni funzo ndani ya Serikali yetu, kwamba wazawa wapewe nafasi na pia wapewe mitaji. Na wakati mwingine, kama tumeona uwezo wao ni mzuri wahamasishwe kufungua kampuni zao ili waweze kuchukua kandarasi kubwa badala ya kusubiri mtu astaafu miaka sitini halafu ndipo atumie utaalamu wake kwa kufungua kampuni. Wahamasishwe kufanya hivyo ili huko mbele katika miradi mikubwa hii inayoendelea kujengwa hapa nchini tupate kampuni za Kitanzania ambazo zitashindana ndani pamoja na nje ya nchi. Kwa hiyo hilo ni jambo zuri la kujifunza kutoka Ofisi ya Babati jinsi ambavyo wanatekeleza mradi wao wenyewe.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu nyingine inatokana na ziara hiyohiyo ya Kamati tulipotembelea katika maeneo ya Nzega. Kumekuwa na uzoefu wa wananchi ambao wanaamua kuanzisha makazi mbali kidogo na wenzano; wanakaa kwenye mashamba huenda ya babu zao. Sasa mradi unatekelezwa halafu wao wako mbali kidogo, kwa hiyo Serikali inatumia gharama kubwa kuwapelekea watu wachache mradi wakati ni kwa sababu wao waliamua kujitenga; na nadhani hili pia ndio limeleteleza hizi shule shikizi kwa sababu watu wachache wapo mahali walikoamua kwenda lakini Serikali inalazimika kuwapelekea huduma.

Mheshimiwa Spika, hoja hapa ni kwamba nadhani kuna sababu ya sisi kupanga makazi na namna ya kurahisisha Serikali kutotumia gharama kubwa kwa ajili ya kuwapelekea watu huduma, la sivyo watu wata detach, wataenda mbali halafu wanahitaji huduma. Hivyo nilitamani kwamba Serikali iangalie, kwamba tuweze kupanga makazi kwa ajili ya kurahisisha kuwapelekea watu huduma bila kutumia gharama kubwa.

Mheshimiwa Spika, hoja ambayo pia Wabunge wengine wameiongelea, mafanikio haya tunayoyashuhudia katika Sekta ya Maji yametokana mara nyingi kwa kutumia vyanzo ambavyo ukiacha mradi wa Ziwa Victoria yanayoweza kuathirika na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi na katika ukurasa wa 81 wa hotuba ya Waziri amedokeza juu ya mpango kabambe wa kitaifa wa uendelezaji wa maji ameuita National Water Master Plan upo katika mpangokazi wake wa kutekeleza katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anayo bajeti moja tu ya mwakani kuelekea 2025. Ningemsihi Mheshimiwa Waziri, katika mpango wake huu hebu ile tunayoiongelea kama gridi ya taifa ya maji hebu iweke, itakupa mileage, itakupa cha kuzungumza baada ya wewe kumaliza uwaziri wako.

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu gani nasema hivi, hii itatusaidia pia kuanza kutumia maji kutoka katika vyanzo ambavyo havikauki. Yaani Misri wanatumia maji ya chanzo kikubwa kutoka Ziwa Victoria, wanakunywa wanamwagilia wanapata faida lakini sisi tunavyanzo vikubwa vya maji lakini hatuja vitumia vizuri. Kwa hiyo katika ule mpango kabambe wake ninamsihi sana Mheshimiwa Waziri; kwamba haina maana watu kama wa Kisiwa cha Ukerewe ambao wao wanazungukwa na maji lakini leo hii bado upatikanaji wa maji ni asilimia 57, siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri watu wa Katavi, Rukwa watu wa Mbeya watu wa Kigoma wanazungukwa na ziwa ambalo lina kina kirefu sana lakini bado hawatumii maji ya kutosha. Mheshimiwa Waziri mcheza kwao hutunzwa, kwenye National Water Master Plan wayaingize haya na atakwa amefanya vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana nakuksukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ambae anataka Bunge lako liweze kumpitishia bajeti ya bilioni 74.2 ili aweze kutekeleza majukumu yake. Pia, mimi nitangulie kuunga hoja mkono kwamba Waziri tutakupitishia bajeti hiyo ili uweze kwenda kushughulikia ustawi wa jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitangulie kumpongeza waziri pamoja na naibu wake na watendaji wake kwamba, wizara yao ndani ya muda mfupi tangu imeundwa wameweza kutengeneza miongozo na kuanzisha madawati ambayo watatathimini utendaji kazi wao ili mwishowe tuweze kuona kwamba wanafikia ule ufanisi ambao unatarajiwa baada ya kuandaa hiyo miongozo pamoja na madawati waliyoanzisha mahali pote yalipo aanzishwa. Lengo ni jamii yetu iendelee kupata ustawi na maadili yaweze kupatikana lakini pia kushughulikia changamoto ambazo zinaikabili jamii yetu.

Mheshimiwa Spika, asubuhi ya leo ningependa kutoa mchango wangu kuhusu sehemu moja ya kwanza inayohusiana na elimu ya makuzi pamoja na malezi ya mtoto.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa tabia ya mtu inafanyika katika miaka saba ya awali. Katika miaka saba hii ya awali ndipo mtoto katika akili yake changa anaweza kuelekezwa mambo yaliyo mema na akili yake changa iko tayari kupokea kutoka kwa wazazi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunaambiwa kwamba katika miaka hiyo saba ile mitatu ya awali ndiyo ya msingi kabisa maana ndipo tunapojenga msingi wa kupokea maadili, msingi wa kuchambua yaliyo mema na ndio maana napenda nitumie mitahli moja inayotoka katika kitabu cha Mithali 22:6 inasema “Umlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mzee”.

MBUNGE FULANI: Haleluya.

MHE. PROF. SHUKRAN E. MANYA: Mheshimiwa Spika, sasa, kama hilo ndilo hoja ya kwamba malezi ya mtoto angali mtoto mdogo akilelewa vizuri hataweza kuiacha njia hii hata uzee wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yangu ni nini? Katika kipindi hiki cha miaka ya awali na ndio mana tunapendekeza miaka hii ya awali, mtoto aweze kukaa na wazazi wake. Wazazi wake wapate namna ya kumuingizia maadili wanayoyataka wao. Kwa hiyo, ndio muda wa kumlinda mtoto yaani first line of defense (hatua ya kwanza ya ulinzi wa maadili ya mtoto ni akiwa nyumbani kwao) ndipo ambapo anawekewa misingi ambayo ataweza kuiishi hata huko baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, anapokuwa amelindwa ndio muda wa kumweleza mtoto kwamba wewe ni wa jinsia ya kike, wewe ni wa jinsia ya kiume na wala hakuna trans gender wakati huo akiwa mdogo. Yaani asifike mahali eti akishakuwa mtu mzima anakutana na mafundisho ya kwamba eti kuna jinsia ya katikati hapa, hapana. Akiwa mtoto mdogo ndio wakati wa kumweleza, ndio wakati wa kumweleza mtoto, wewe unapaswa kujitambua kwamba ukiwa wa jinsia ya kiume au ya kike hakuna kuguswa na mtu yeyote yule sehemu zako za siri. Huu ndio wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ndio wakati wa kumuonesha mtoto upendo, ndio wakati wa kumuonesha mtoto imani, kujenga naye imani na ujasiri wa kwamba iwapo mtu awae yote si mjomba, si baba mdogo, si shangazi, mtu awae yote atakapo kutendea jambo lolote ambalo si jema baada ya kumfundisha jema, apate imani na ujasiri wa kuja kumwambia baba yake au mama yake kwamba fulani amaenitendea hivi, huu ndio wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, kwa jinsi hiyo kama hivyo ndivyo, huu wajibu unawaangukia wazazi na hasa akinamama. Na ni wajibu ambao haupaswi kuahirishwa wala haupaswi kupokezana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa jinsi hiyo niombe sana, yawezekana kweli jamii yetu inahangaika kutafuta mali, yawezekana kweli tunajaribu kutengeneza namna ya kujenga chumi zetu za familia, ni kweli.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni wajibu ambao hauhamishiki, kwa sababu ni wajibu ambao hauwezi kuahirishwa, wazazi tusiseme huu usemi ambao tunapenda kusema kila wakati “sina muda” hapana. Wazazi tutenge muda hata kama majukumu yetu ni makubwa kiasi gani yanatutaka, ni lazima kila siku inayopita tutenge muda wa kukaa na watoto wetu na usemi wetu wa kusema sina muda hiyo sio usemi unaopaswa kusemwa na mtu aliye na mtoto mdogo ambae ni mzazi anaetambua kwamba huu ndio wakati wa kujenga maadili ya mtoto wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbona hata kama tunakuwa busy mbona tunakuwa na muda wa whatsApp, twitter na facebook katika simu? Si ni bora tuache hiyo Facebook, tuache hiyo twitter lakini tupate muda wa kujenga maadili ya Taifa lijalo. Tukifanya hivyo, mafundisho yote yanayokuja yale ambayo ni potofu hata haya ya kumwandaa mtu katika kumuingiza mtindo wa ushoga, kama ameandaliwa vizuri mtoto atakuwa anajitambua na mtoto atakataa kushawishiwa katika maadili potofu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wazazi lazima turudi tuchukue sehemu yetu, tukae kama wazazi, tufanye wajibu unaotuangukia na wala tusisingizie shughuli za kuingiza mali au shughuli za uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa namchukua huyu mtoto kwamba pale nyumbani ameandaliwa vizuri, baadae anatamani kwenda kwenye jamii, yawezekana ni shule au yawezekana kupata masomo ya dini huko. Lazima tuweke mifumo thabiti na salama inayomhakikishia huyu mtoto ulinzi wake.

Mheshimiwa Spika, ninaposema hivi ni kweli kwamba Mheshimiwa Waziri, atasema ameanzisha madawati lakini ni lazima tuweke mifumo rahisi na myepesi ya kushughulikia iwapo hawa ambao wamepewa dhamana ya kumlinda na kumtunza wanakwenda njia ambayo sio. Maana kama walivyosema wenzangu, watu wengine ambao wameaminiwa ni shule, viongozi wa shule, wameficha maovu haya wakitamani kuyamaliza kwa njia nyepesi, hapana. Kwa hiyo, Serikali iweze kuweka mfumo ambao ni rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kama muda wangu umekwisha.

SPIKA: Dakika moja.

MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, niongelee hoja ya mtoto yatima. Mtoto yatima akiwa private school (shule ya binafsi) inakuwa vigumu kurudishwa katika mfumo wa shule za Serikali. Kwa hiyo, katika dawati lake inapotokea mtoto yatima wazazi wake wamefariki, Serikali iweze kurahisisha namna ambayo huyu mtoto anaweza akasaidiwa kutoka shule ya binafsi kurudishwa katika shule ya Serikali ili wazazi wasiweze kupata shida sana katika kumhudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ili niweze kuchangia Bajeti ya Serikali ya mwaka 2023/2024. Kwanza kabisa, nichukue nafasi ya kuipongeza Serikali kwa kuchukua hoja nyingi sana za Wabunge katika kupanga Bajeti yake. Pia jioni ya leo nitaongelea maeneo mawili ambayo ndio hasa napenda kuyaongelea yaliyochukuliwa katika bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kabisa ni ile ambapo Serikali imedhamiria kuanzisha akiba ya dhahabu kupitia Benki Kuu. Katika ukurasa wa 18, hotuba ya Waziri inasema, naomba ninukuu: “Serikali imekamilisha taratibu za kununua dhahabu kupitia Benki Kuu ya Tanzania kwa ajili ya kuanzisha akiba ya dhahabu ya Taifa.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hii ni njema kwa sababu kwanza itaimarisha sarafu yetu ya Tanzania, lakini pia ni akiba kwa vizazi vijavyo, yaani hata kama migodi ya dhabu itaisha, lakini tutawapeleka watoto wetu na vizazi vijavyo kwenye vault na kuwaonesha kwamba hebu angalieni urithi wenu. Kwa hiyo, hilo ni jambo la kupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natamani Mheshimiwa Waziri afanye mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa kule Benki Kuu ya Tanzania kuna kilo 418 ambazo zimekuwa zikitaifishwa kwa sababu ya makosa ya utoroshaji na kwa sababu sheria inasema kwamba, ukipatikana umetorosha hiyo itataifishwa. Sasa hizi kilo 418 zina thamani ya bilioni 53.2. Pendekezo langu achukue hizi kilo 418 apeleke zikasafishwe (refinery) ili iwe kianzio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ili pendekezo la Mheshimiwa Waziri liweze kuthibitika, yaani maneno yake yathibitike kwamba Serikali inaanza, kwa nini asitaje kwamba mwaka huu anaanza na kilo ngapi katika kuanzisha akiba ya dhahabu ya Taifa? Nadhani hapo atakuwa ametenda haki kuliko yaendelee kubaki kama maneno kwenye makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, niongelee uanzishwaji wa Tume ya Mipango. Hili pia ni jambo ambalo limeongelewa sana na Wabunge wengi na tumeona Serikali imelichukua na hatimaye kuliweka katika utekelezaji na katika hili tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna matarajio ya wananchi katika uanzishwaji wa Tume ya Mipango. Moja kabisa, tunataka kuona kwamba Tume yetu inaondoa duplication of efforts (kurudiwa rudiwa jambo kufanywa na Wizara zaidi ya moja lakini jambo ni lile lile). Wakati fulani nilikwishasema hapa kwamba, Wizara ya Maji imekuwa ikijenga mabwawa, Wizara ya Mifugo nayo imekuwa ikijenga mabwawa, lakini Wizara ya Kilimo, kazi hiyo hiyo. Hebu tuombe sasa kwa sababu ya kuwepo kwa Tume ya Mipango hii duplication iweze kuondolewa na tuweze kupata tija kuliko mradi unaofanana ukafanywa na Wizara zaidi ya moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba tunategemea Tume yetu ya Mipango iweze kuiangalia nchi na Jiografia yake na idadi ya watu waliopo na maendeleo yaliyokwishafanyika katika eneo lile na maendeleo yanayohitajika. Mifano ambayo ni halisi, Jimbo moja unaweza ukakuta lina kata nne lakini Jimbo lingine lina kata 45, lakini wote wanasema wanapewa kilometa moja ya lami, kwa nini? Yaani kata nne, kata 45 kilometa moja ya lami? Hapana. Au VETA moja, hii inawezekanaje? Tunategemea Tume yetu ya Mipango iweze kuondoa kutokuwa na usawa katika maeneo kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta hapa nchini kuna wilaya moja ina kilometa saba tu za lami tangu iwepo, nyingine ina kilometa 200, lakini zote ziko katika nchi moja. Tunategemea Tume yetu ya Mipango iweze kuangalia mahali ambapo pako disadvantaged ili waweze kushiriki keki ya Taifa sawasawana hili linajenga umoja wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine, wakati mwingine utakuta mikoa mingine inazungukwa na Maziwa makubwa lakini huduma ya maji ni hafifu katika maeneo hayo. Tunategemea Tume yetu ya Taifa iliangalie hili ili kuweka msawazo sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, wakati mwingine zao moja linapokuwa linapata bei nzuri katika soko, utashangaa mikoa yote ya Tanzania wanataka wawe wakulima wa zao hilo hilo. Hii haiwezekani lazima kuwe na kanda za ikolojia na mazao yanayostawi katika eneo husika ndiyo yalimwe. Sio kwamba Tanzania nzima baadaye tunakuja tunakuta kwamba kuna mikorosho kila mahali, hapana hii haiwezekani. Kwa hiyo, tunategemea Tume yetu ya Mipango iangalie hali ya hewa, wingi wa mvua, joto, halafu iseme jamani hapa sio pa korosho, hapa ni pamba ni hivyo na si vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika matarajio ya Tume ya Mipango, katika mipango yake ya kitaifa, napenda sana Tume ya Mipango izingatie cultural integration, nilikuwa natafuta neno zuri hapa mwingine akanishauri kwa kuniambia ni mwingiliano wa kiutamaduni. Hili naomba nilisema hivi, tulipo hapa wote, Taifa hili lina makabila 120 lakini limeweza kulinda umoja wake kama tulivyo kwa sababu ya mwingiliano ambao tumekutana JKT, vyuoni na wengine tumeoana na kuoa kwa kuingiliana hivyo na tukalinda umoja wetu wa kitaifa na ndio maana hapa hakuna mgogoro ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kuna shule za Kata. Kwa hiyo mtu atasoma primary pale pale, secondary pale pale, halafu utakuta watu wanasema naomba mkoani kwangu peleka chuo kikuu. Kwa hiyo, mtu atakuwa m-local akiwa m-local utashangaa tunajenga ukabila na ukanda. Kwa hiyo, lazima katika mipango ya kitaifa kuwe na vyuo ambavyo vitabaki katika Kanda moja ili watu tuendelee kuingiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la sivyo, kinyume chake utakapotengeneza Taifa la wa–local wenye ukanda mmoja, wa kabila moja kwa sababu tangu primary mpaka chuo kikuu kama ni Kagera yaani ni hao wenzako tu hao hao, hapana. Lazima tuangalie cultural integration kiasi kwamba tuendelee kuingiliana. Kwa hiyo, katika mipango yao lazima waangalie kwamba inapofikia level fulani tuwaruhusu watu waende sehemu nyingine ili tuendelee kuingiliana ili tuweze kuendelea kujenga umoja wa kitaifa, tuondoe ukanda, tuondoe ukabila. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndiyo matarajio yetu katika utendaji kazi wa Tume ya Mipango ambayo tunaamini itapewa meno na kuweza kufanya kazi yake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia katika hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, na cha kwanza kabisa niweze kumpogeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo aliona vema kuweza kuunda tena Wizara hii kwa sababu Wizara hii inashughulikia mambo mtambuka, lakini ni kweli kwamba inashughulikia ustawi wa jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ustawi wa jamii yetu una uhusiano mkubwa sana na ustawi wa mama na mtoto; na mimi asubuhi ya leo ningependa kukita mchango wangu juu ya lengo la Wizara ambalo linasema kuendelea kuimarisha huduma za ustawi wa jamii na haki kwa familia na watoto, ikiwemo malezi ya kambo na kuasili, watu, walezi wa kuaminika, malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto, ulinzi na usalama kwa watoto dhidi ya vitendo vya ukatili pamoja na huduma za utengamao katika familia.

Mheshimiwa Spika, na ni kwa nini niulete mchango wangu kuhusiana na hili lengo?

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kuamini kwamba changamoto katika jamii tunaweza tukawa tunaangalia ukatili unaokuja kutokea baadae, lakini chanzo cha mambo yote haya tungetambua kwamba yanaanza katika familia. Na kwa jinsi hiyo malezi ya mtoto, elimu ya malezi ya mtoto inapaswa kutolewa katika jamii yetu tangu wazo la kutaka kuwa na mtoto linapotungwa katika mawazo ya wenzi wanaotarajiwa; na ni kwa sababu mapungufu ya elimu hii ndio chanzo cha kupata hata watoto ambao baadae tunakuja kuwaita watoto wanaokaa katika mazingira magumu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wizara inapotengeneza sera kwa sababu najua ni Wizara mpya, lazima ione umuhimu wa kufikisha elimu hii kwa jamii nzima ili kwamba jamii sasa iweze kujua kwamba, tunapokuwa tunatarajia kupata watoto maana yake tunaambatana na wajibu. Na jamii ifikie mahali itambua kwamba wajibu wa malezi ya watoto ni wajibu usiohamishika na hasa watoto wanapokuwa miaka zero mpaka miaka 11, ni wajibu usiohamishika. Maana mara nyingi pia unakuta katika jamii yetu tunapenda kuamini kwamba mtoto atazaliwa, atapelekwa kwa ndugu yake fulani, hapana, this is non transferable responsibility. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kama ni non-transferable, elimu hii inapaswa kuwaendea watu wote wanaotarajia kuwa na watoto hapo mbeleni, maana yake baba na mama; na wajibu huu, mimi ningependekeza hata mimba inapokuwa imetungwa na kama binti anapaswa kwenda kliniki basi na yule baba naye aende kliniki akapate elimu hii asisingizie kwamba, ni majukumu, hapana. Kama anafanya kazi mahali pa kazi, waajiri watoe ruhusa baba waende kliniki wakapate elimu ya malezi ya watoto. Na kwa sababu gani nasema hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine kama Taifa tumeongelea hali ya udumavu. Hali ya udumavu inatokana na kutokuwa na lishe bora wakati wa mimba. Sasa unakuja baadae kuhangaika, elimu ya msingi, elimu ya awali, sijui tuition, tuition itafanya nini kama mtoto alidumaa wakati wa mimba? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, habari ya lishe bora lazima iwe ni elimu ambayo itapelekwa kwa watu wote wahusika. Na mimi kwa kuongelea habari ya non transferable kama jukumu la malezi, hata inapofikia kuongea habari ya elimu tunayoitoa, hivi kuna sababu ya mtoto wa miaka sita kwenda boarding? Akalelewe na nani? Na matron na hao.

Mheshimiwa Spika, sasa tunakuta kwamba tunshindwa kujenga bond kati ya baba na mama mhusika anakwenda kujenga bond na matron, anakwenda kujenga bond na mtu ambaye hamfahamu. Kwa hiyo, unakuta hata mtoto anapokua hana bond na wazazi wake, lakini tuko hapa kwenye mitaala yetu ya elimu tunapendekeza shule za boarding za watoto wadogo, si sawa, si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunapokuwa tunajadili msingi wa ustawi wa jamii mimi napendekeza ndani ya Bunge lako tukufu, nimesema sentensi ambayo nitairudia tena; wajibu wa malezi yam toto mchanga kwa wazazi wake is non transferable, na kama ni non transferable maana yake si matron wa chekechea au wa shule ya awali ambaye ana jukumu la kulea mtoto wako. Na kwa msingi huo tujadili kama kweli ni sahihi kuwa na shule za kulea watoto katika umri ule mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, elimu hii ikifikishwa napendekeza ifikishwe kwa namna zote, sasa hivi njia za kidijitali yawezekana ni za msingi sana kupeleka elimu hii. Kwa hiyo, Wizara iweke sera itakayohakikisha kwamba elimu hii inawafikia Watanzania wote ili tuweze kuwa na jamii ambayo ina ustawi.

Mheshimiwa Spika, ninaelewa muda wangu si mrefu sana niongelee jambo la mwisho katika ustawi wa jamii yetu. Ni kweli kwamba tunapenda burudani, sasa ninamfikiria mtoto mdogo aliyezaliwa yuko mahali fulani nyumbani, halafu katika jamii hiyo kuna club kubwa inayopiga muziki mdundo wake mpaka saa nane usiku na kuna mtoto mdogo hapa ambaye ngoma zake za masikio sidhani kama zinaweza kuhimili huo muziki. Lakini watoto wako majumbani, kuna wazee wenye pressure majumbani, kuna wazee ambao wanatamani utulivu lakini ngoma inadunda mpaka saa nane usiku, inasambaa kilometa tano kutoka ukumbi wa mahali ilipo, si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikutolee tu mfano unatoka hapa Dodoma unakwenda Mbeya unakwenda kwa ajili ya kuhudumia wananchi wako, halafu usiku huo unaofika umefika saa nne usiku unatamani uwe na masaa manane ya kulala, halafu ngoma inarindima usiku mzima, kesho utakuwa tayari kwa ajili ya kazi, hapana. (Makofi)

Kwa hiyo, ili tuweze kuwa na ustawi wa jamii teknolojia ya kuzuia muziki ipo, burudani tunaipenda ni kweli, lakini ikomee masaa ambayo jamii inapohitaji ustawi wa afya ya akili kama balozi anavyosema watu wapumzike ili tuweze kuwa kesho yake kutayarishwa kwa ajili ya kufanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo napendekeza tunapoongelea ustawi wa jamii yetu pia hebu watoa burudani watuburudishe tunapenda, lakini watuachie muda tupumzike sisi, wazee, wenye pressure na watoto wetu wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami ya kuchangia katika Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutambua jitihada za Serikali katika kuongeza bajeti katika sekta za uzalishaji. Jambo ambalo Wabunge wote tumelifurahia, kwamba kuongeza bajeti katika sekta za uzalishaji kwa maana ya kilimo, mifugo na uvuvi, tunakwenda kufanya uzalishaji mkubwa. Na kama tija ambayo tumeiongea sana katika Bunge hili itatokea, basi tunakwenda kujikwamua mahali pakubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipende kupongeza jitihada na hatua ya Serikali ambayo imetambua kwamba kuna sababu kubwa na ya msingi ya kuziba mianya ya upotevu wa fedha katika matumizi ya Serikali. Jambo la kwanza, Mheshimiwa Waziri wa Fedha alipendekeza juu ya hasara inayopatikana kutokana na watumishi waliopumzishwa majukumu yao. Wabunge wengi wameongelea, na nipende kukumbuka kwamba Mheshimiwa Janejelly alisema kwamba kama Kanuni zetu zinaruhusu basi kweli huo mpango wako uendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi ninapenda kusema kwamba, ili Serikali isipate hasara juu ya watumishi hawa ambao wanapumzishwa majukumu yao, basi muda mchache uwekwe baina ya wao kupumzishwa na kurudishwa katika majukumu yao. Serikali ijipe timeline ni wiki mbili au mwezi mmoja, mtumishi awe amerudi kufanya majukumu yake, lakini anapokaa mwaka mzima, mtumishi huyu kwanza anakuwa demoralized halafu anajisikia ni reject. Sasa Serikali inapata hasara hapa, mtumishi yuko demoralized hapa kwa sababu hajarejeshwa katika kazi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili tufunge loop. Wakati Serikali haitaki kupata hasara tufunge loop upande wa pili mtumishi arudi mapema katika majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika kupunguza matumizi ya Serikali ni kuhusu matumizi ya magari. Nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri juu ya hili; lakini napenda huku nako tufunge loop, kuna loose loops hapa mahali pia. Yaani tumeona hasara inayopatikana kwasababu ya wingi wa magari, lakini Mheshimiwa Waziri wa Fedha wale wakala wa kutengeneza haya magari hebu jiulize unao watumishi wa kutosha kule ndani? Kama hawa watumishi hawatoshi wanaotengeneza wanatoka upande gani? Na kwanini usilipe zaidi ya ambavyo unapaswa kulipa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo si ajabu ukakuta; nitoe mfano ambao ni rahisi sana; wote hapa tunajua kuwa wind screen ya gari 250,000 lakini inapotoka voucher TEMESA unakuta imekuja mara tatu au mara nne zaidi ya hiyo, wind screen. Huu nimeutoa mfano ambao ni halisi nimekutana nao. Wote tunajua kwamba wind screen ni 250,000 au 300,000 ya Prado au Landcruiser lakini angalia katika voucher zako za matengenezo ya magari yako hutakuta hiyo bei. Mara nyingi utaambiwa 750,000 au 1,000,000. Hapo napo, kwa zile gari ambazo utaamua zibaki kwa wale watendaji wakuu wa Wizara basi hebu funga loop upande wa TEMESA uone kwamba bei unazoletewa za vipuri vya magari ndizo bei halisi za soko kama ambavyo unatamani pia kupunguza upande wa umma procurement. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine; Ofisi ya CAG imependekezwa kuongezewa watumishi na pia kufanya technical pamoja na financial audit. Hata hivyo hiyo bado ni audit. Mimi ninapendekeza, kwasababu kazi yao ni ku-audit na una audit na una audit kazi iliyokwishafanyika sasa tija itatoka wapi? Mimi nadhani kama tuna mpango wa kunusuru nidhamu ya matumizi bora ya fedha za Serikali basi hawa watu katika hii Ofisi ya CAG wapewe pia jukumu la monitoring and evaluation pamoja na kufanya audit. Wakiendelea kufanya audit bado watamkuta mtu ambaye amekwisha kutumia vibaya fedha za Serikali halafu anakuja kuwajibishwa. Sasa, tunapaswa tuzuie matumizi hayo, ambapo ni pamoja na kufanya monitoring and evaluation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niongelee kuhusu Wizara ya Maliasili na Utalii, na nitambue mchango mzuri kabisa na maono ya Mheshimiwa Rais ambaye kwakweli amekwenda kutanzua kitendawili ambacho mataifa ya nje; watu wengi wanadhani kwamba mataifa ya nje wao ni werevu, lakini kama wangekuwa ni werevu na atlas wanazo kwanini kila wakati walipokuwa wanauliza Mlima Kilimajaro upo wapi wanasema huu upo nchi nyingine. Kwa hiyo, si kwamba lazima wawe werevu, walikuwa ni wajinga. Sasa Mheshimiwa Rais ametusaidia kuwaondolea ujinga waliokuwa nao wa kujua vivutio vipi vipo upande gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kupata tija katika hilo our hospitality na tour guides wetu wanapaswa kuongezewa uwezo wapenzi. Bado hospitality yetu kama nchi haipo top watch. Kwa hiyo hili wizara husika na Serikali ikae pamoja ione kwamba tunahitaji ku-improve sana upande wa hospitality yetu pamoja na tour guides; hilo litatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za karibuni tumeona wachezaji wakubwa wa vilabu vikubwa vya Ulaya wakija, na wanakuja Serengeti; lakini hawa pia tunawaona wakati wa mapumziko yao ya wakati wa kiangazi wakienda kupata mapumziko katika fukwe na hasa za Bahari ya Mediterranean Barbados pamoja na Dubai. Kwanini sisi, yaani tunajua wanalolitaka tuna joto lote na jua lote na mchanga wote wanaoutaka, kinapungua nini Tanzania? Hatujaweza kuimarisha beach sports, maana ndicho wanachokitafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na pale Pwani ya Dar es Salaam kuna visiwa vizuri; kwanini Serikali isione kwamba kuna sababu ya ku-improve mazingira ya uwepo wa visiwa katika ufukwe wa Dar es Salaam halafu ikaingia pamoja na sekta binafsi ku-improve beach sports ili tuwateke waje Serengeti wakimaliza wapumzike pale kwenye beach zetu? Kwa hiyo kuna sababu ya kuanzisha kile wanachokitapata katika Bahari ya Mediterranean visiwa vya Ibiza, Barbados na Dubai tukilete pale Dar es Salaam ili waweze kukaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika ku-improve habari ya utalii; watu wengi sana tunapokwenda katika miji unasema kwamba nita spend siku moja ya ziada au ya pili kwa ajili ya shopping au kwa ajili ya kuangalia mji, lakini miji yetu haijatoa hayo mazingira. Kwa hiyo, watalii wanakuja wanaishia Serengeti wanapanda ndege na kuondoka; na sababu kubwa ni kwasababu hatuna museums zinazovutia. Yaani tuna museum lakini yawezekana vilivyomo ndani ya museum haviwavutii kusema kwamba nita spend siku moja Arusha, nita spend siku moja Dar es Salaam kwa ajili ya kuangalia, what’s is there to see hatujaweza kuwapa hicho watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa napendekeza kwamba, mbona Tanzania tunavyo vitu vya kuwapa? Kwa mfano; tumekuwa tukiongea katika hili Bunge juu ya mjusi yule wa Tendaguru aliyoko Ujerumani. Kwani Tendaguru siniyakwetu? na Tendaguru ambayo hamuijui vizuri kijiolojia ni mahali ambapo katika Bara la Afrika ndipo panapoongoza kuwa na masalia ya wale mijusi na viumbe wale wa zamani. Kwa hiyo, haya mabaki yalichimbwa mwaka 1905. Hivi Serikali ilishawahi kuwekeza kiasi kwamba tuone kama tunaweza tukachimba na sasa tukapata mjusi wetu wa kuchimba sisi wenyewe? Maana yule alichimbwa na Wajerumani karne imepita sasa. Kwa hiyo, mimi ninapendekeza Serikali iweke fedha katika utafiti pale Tendaguru ili ikiwezekana watu wetu wa archeology waende pale wajaribu kuchimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa kwamba kazi ya kumuunganisha ni kazi kubwa sana lakini tupate na sisi mifupa baadhi baadhi tuiweke katika museum yetu. Lakini pia jambo ambalo tunalo la kuvutia zaidi … (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. PROF. SHUKRANI E. MANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia Muswada ulioko mbele yetu, Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji ya Mwaka 2022. Pia kama sehemu ya Wajumbe wa Kamati tunaunga mkono mapendekezo ya Serikali yaliyoletwa na tungetamani kuona kwamba yale ambayo wanayapendekeza katika Muswada huu, waende kuyasimamia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani tunaunga mkono mapendekezo ya Serikali na pia nitumie nafasi hii kuliomba Bunge lako Tukufu yaani Wabunge waweze kuunga mkono hoja iliyoletwa na Waziri, ni kwa sababu moja mapendekezo haya yanabeba maudhui ya kulinda vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo la msingi sana kama tusipolinda vyanzo vya maji vya asili vilivyopo gharama za kupata maji kwa ajili ya domestic use, lakini pia tunakwenda kupanua mahitaji ya maji katika nchi hii katika kilimo na umwagiliaji, itakuwa shida sana kama vyanzo vya maji havitalindwa. Kwa hiyo ni hoja ya kwanza kwa nini tunaunga hoja mkono, kwa sababu inaenda kuimarisha udhibiti na usimamizi wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, Wizara iendelee kuongeza jitihada za kuwafikishia maji Watanzania, wakishakuwa wamepata maji kwa ajili ya matumizi, maana yake kuvilinda vyanzo vya maji inakuwa ni rahisi, lakini kama mtu hana maji ya kutumia kwa vyovyote atayatafuta kwa njia anayoiona. Kwa hiyo kuwafikishia wananchi maji ili wapate maji ya kutumia itakuwa pia ni ulinzi kwa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa nini tuunge hoja mkono? Hoja hii imebeba maudhui ambayo pia wadau wametia maoni yao kwa maana kwamba wadau muhimu katika sekta ya maji pia wamekubaliana na mapendekezo haya na kuweka maboresho yao ambayo Serikali imeyapokea. Vile vile kwa nini tuunge hoja mkono? Ni kwa sababu inapendekeza adhabu na faini kwa mtu au taasisi ambayo itajihusisha na uharibu wa vyanzo vya maji pamoja na kuharibu mfumo wote wa udhibiti wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika Kamati msisitizo wetu ulikuwa kuwa, elimu na ushirikishwaji wa wananchi katika ulinzi na usimamizi ndiyo iwe nyenzo kubwa ya ulinzi. Kwa sababu gani tunasema hivi? Kama unapendekeza adhabu na faini lakini mtu hajui kwamba hata anakosa, siyo sawa. Kwa hiyo Serikali yaani Wizara itumie muda wa kutosha kwa vyombo vya habari kwa namna yoyote inayoweza kupeleka elimu na kuwashirikisha wananchi. Huo ndiyo utakuwa ni ulinzi unaojitosheleza, lakini ukienda na nguvu ya adhabu na faini zilizopendekezwa, watu watatoa faini lakini hutakuwa umelinda vyanzo vya maji, kwa hiyo ndiyo maana tukasema kwamba Wizara itoe elimu na iwashirikishe sana wananchi ili wao wenyewe baada ya kupata elimu waweze kuwa ni walinzi wazuri wa vyanzo vya maji na usimamizi utakuwa ni bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, watu wengi sana nchini Tanzania tumechimba visima vya maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, lakini hatukujua kwamba tunahitaji vibali na kwamba kuna faini katika hilo. Ni ukweli usiopingika kwamba katika sasa sijui Kiswahili cha aquifer ni nini, lakini katika aquifer moja ukitoboa mashimo mengi sana ya visima, utaharibu kabisa mfumo wa maji, lakini hatujui. Sasa ndiyo maana kwamba lazima hiyo elimu wananchi waipate, kwamba jamani nyinyi katika mkondo huu hapa mko katika aquifer moja, geological formation ya aquifer moja hatuhitaji visima 20 hapa, la sivyo tutaharibu, elimu hiyo hatuijui, ni lazima tuipate ili tuweze kulinda hivyo vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine watu huchimba visima akipata maji katika yale maji ya juu juu ambayo siyo aquifer anaamini amepata maji, baadaye kisima kinakauka elimu hiyo hatuijui. Kwa hiyo ndiyo maana Wizara hii inahitaji kufanya sana uhamasishaji na ushirikishwaji ili hata visima vilivyochimbwa vionekane kwamba vina ubora wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu pia wamekuwa wakitumia chemchem yao siku zote, Waziri hajawapelekea maji ya bomba, wanaitumia kwa jinsi wanavyoweza, wakati mwingine anamwagilia ili apate kabichi ya kula. Mheshimiwa Waziri asiende akampiga faini mtu yule amweleweshe kwanza na amsaidie namna ya ambavyo atapata maji kwa ajili ya kukidhi mahitaji yake, kwa sababu maji ni hitaji la msingi. Sasa Waziri akifika akampiga faini kwa sababu anatumia maji ya chemchem hajampa maji, nadhani Waziri anaelewa kabisa kwamba maji ni haki ya msingi, anayahitaji kwa matumizi, kwa hiyo tusitangulize faini kabla ya kutoa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ibara ya 13 inapendekezwa Waziri aweze kuanzisha maabara kwa ajili ya ubora wa maji. Hili jambo ni la kupongezwa na Mheshimiwa Waziri atafute vyanzo vya fedha kokote anakoweza kupata aanzishe maabara za kupima ubora wa maji. Kwa nini nadhani kwamba hili ni jambo la msingi? Watanzania wanaotoka baadhi ya maeneo sasa siyo kwamba na-abuse lakini tunaona kwamba wana meno ambayo yana rangi ya kahawia kwa sababu ya fluorine. Mara nyingi tunadhani kwamba hiyo ndiyo athari peke yake ya fluorine nyingi katika maji, lakini florine ikizidi inaleteleza hadi osteoporosis, ugonjwa wa kukonda mifupa inakwenda mpaka kukuharibu joints, inazi-damage fluorine nyingi, lakini watu wengi katika maeneo ambayo tunatoka wanatumia maji, tunaona tu meno yao yamekuwa kahawia tunasema anatoka Singida, huyu anatoka Moshi huyu. Kwa hiyo lazima Waziri aweke maabara ili zipime ubora wa maji kabla ya kutumiwa kwa sababu athari za elements nyingi katika maji ni kubwa zaidi ya zinazoonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa uchafuzi wa maji ambao ni mbaya zaidi na huwa hatuiongelei ni nitrate. Nitrate inaingia katika maji kutoka kwenye vyoo na maji ya viwandani mara nyingi visima vile vilivyochimbwa vifupi wanatumia yale maji kukiwa na nitrate nyingi sana. Sasa unashangaa kwa nini tuna saratani nyingi na kuna birth defects yaani kizazi kinaharibika kwa sababu ya too much nitrate katika maji. Kwa hiyo water quality laboratories ni za msingi sana ili Watanzania watumie maji ambayo yako quality, tutamsaidia sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu kutojadili kwamba vyanzo vya kansa vinatoka wapi kumbe vingine ni kwa sababu ya too much nitrate. Kwa hiyo Water Quality Laboratories ni za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, sera tunajadili Sera ya mwaka 2002 ambapo population ya Watanzania ilikuwa ni 34,000,000 sensa itatwambia lakini tuko almost doubled, sasa una sera ya population ya watu ambao wame-double, yawezekana ikawa haikidhi mahitaji ya sasa. Kwa hiyo tunaomba Wizara iharakishe mchakato wa kuwa na sera mpya ambayo ita- take on both, Dira ya Maendeleo ya miaka 25 mingine, lakini pia kuangalia maendeleo ya kisasa, miji yetu imekua na kila maendeleo mengi yamefanyika Tanzania baada ya miaka hii 20, tupate Sera mpya ya Maji ambayo itakuwa inakidhi mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mchango huo, naunga mkono hoja na tumwombe sana Waziri akayasimamie haya na atafanikiwa sana katika Wizara ambayo amepewa dhamana kuisimamia. Ahsante sana.