Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Dorothy Onesphoro Gwajima (12 total)

MHE. SALMA R. KIKWETE Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Wazazi na Walezi wanatoa ushirikiano katika kuwatetea na kuwalinda watoto dhidi ya vitendo vya ubakaji, ulawiti na unyanyasaji unaoendelea kwa sasa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete Mbunge wa Mchinga kama kwamba je Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wazazi na na walezi wanatoa ushirikiano katika kuwatetea na kuwalinda watoto dhidi ya ubakaji, ulawiti na unyanyasaji unaoendelea kwa sasa?

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali hili kama ifuatavyo; katika kukabiliana na tatizo la Ubakaji, Ulawiti na Unyanyasaji wa watoto, Serikali imechukua hatua zifuatazo: Kuandaa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA wa mwaka 2017/2018-2021/2022) ambapo kupitia Mpango huu Serikali imekuwa ikitekeleza afua zinazolenga Kutoa Elimu ya Malezi ya watoto kwa wazazi/walezi; Kutoa msaada wa Kifamilia na Mahusiano; na Kusambaza Agenda ya Taifa ya Wajibu wa Wazazi/Walezi katika malezi chanya ya familia.

Mheshimiwa Spika, mikakati mingine ni pamoja na; Kuandaa programu ya Taifa ya Malezi Makuzi na Maendeleo ya awali ya mtoto, kupitia program hii vituo vya majaribio 30 vya kijamii vya malezi, makuzi, na maendeleo ya awali ya mtoto vimejengwa katika mikoa miwili ya Dar es Salaam ambapo ni vituo 10 na Mkoa wa Dodoma vituo 20 na Serikali inaendelea kuhamasisha ujenzi wa vituo vingine katika mikoa iliyobaki.
MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza:-

Je, lini Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe itakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Mkoa wa Songwe?
WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe kwa kujenga majengo mawili ikiwa ni Jengo la Huduma za Uchunguzi wa Maabara ambalo limefikia asilimia 98 na Jengo la Huduma za Wagonjwa wa Nje (OPD) ambalo ujenzi umefikia asilimia 96. Majengo haya mawili yanatarajiwa kuanza kutoa huduma ifikapo mwezi Julai, 2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza ujenzi wa Jengo la Huduma za Afya ya Uzazi pale pale ambao utakamilika mwezi Februari, 2022 na kiasi cha shilingi bilioni tano kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi huo.
MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza:-

Je, lini Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe itakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Mkoa wa Songwe?
WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe kwa kujenga majengo mawili ikiwa ni Jengo la Huduma za Uchunguzi wa Maabara ambalo limefikia asilimia 98 na Jengo la Huduma za Wagonjwa wa Nje (OPD) ambalo ujenzi umefikia asilimia 96. Majengo haya mawili yanatarajiwa kuanza kutoa huduma ifikapo mwezi Julai, 2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza ujenzi wa Jengo la Huduma za Afya ya Uzazi pale pale ambao utakamilika mwezi Februari, 2022 na kiasi cha shilingi bilioni tano kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi huo.
MHE. SHALLY J. RAYMOND K.n.y. MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza:-

Je, uwepo wa Kiwanda cha kuua mazalia ya Mbu (Tanzania Biotech Product Limited) umesaidia vipi mapambano dhidi ya Malaria nchini?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hawapo, inakuwa shida sana kuwaona mpaka uvae miwani ya x-ray. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lilikuwa linauliza je, uwepo wa kiwanda cha kuua mazalia ya mbu kimesaidia vipi mapambano dhidi ya malaria nchini? Tangu Kiwanda cha Tanzania Biotech Product Limited kuanza uzalishaji mnamo mwaka 2016, jumla ya lita 340,520 za viuadudu zimenunuliwa na Serikali kwa gharama ya shilingi bilioni 4.5 ambazo ni wastani wa shilingi 13,200/= kwa lita. Lita hizi za viuadudu zilisambazwa katika Mikoa 28 na kuzifikia Halmashauri zote 185 nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi hizi ziliungana pamoja na utekelezaji wa afua zingine za udhibiti wa malaria zikiwemo matumizi ya vyandarua, kupulizia viatilifu - ukoko ndani ya nyumba hasa kwenye maeneo yenye kiasi kikubwa cha maambukizi ya malaria na uwepo wa vipimo na dawa zenye ubora kwenye kutibu wagonjwa watakaothibitika kuwa na malaria. Hivyo, matokeo ya juhudi hizi ni kuwa, zimefanikisha kupungua kwa idadi ya Mikoa yenye hatari kubwa ya maambukizi ya malaria kutoka Mikoa 11 mwaka 2017 hadi Mikoa Saba mwaka 2020. Aidha visa vipya vya malaria vimepungua kwa asilimia 35 kutoka wagonjwa 162 kwa kila watu 1000 mwaka 2015 hadi wagonjwa 106 kwa watu 1000 mwaka 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kutumia bidhaa za Kiwanda chetu cha Kibaha kwa ajili ya kuchangia jitihada za Serikali kufikia kumaliza Malaria (elimination) ambapo tumedhamiria kuwa ifikapo 2025 kiwango cha malaria kiwe kimepungua hadi kufikia asilimia 3.5 kutoka asilimia 7.5 ya mwaka 2017. Aidha, Serikali itahakikisha kila Halmashauri inaendelea kuwajibika kwenye kuhakikisha kuwa inatenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya utekelezaji na hapa wanafanya vizuri. Mwaka huu wa fedha tunaoenda kuuanza mpya wametenga bilioni 2.7 lakini ilikuwa milioni 600 mwaka 2020/2021. Kwa hiyo tunaenda vizuri. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mashine za incubator za kutosha nchini ili kuzuia vifo vya watoto?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru kwa kuwa na utashi wa kuangalia afya za watoto wachanga katika Taifa letu kama sehemu ya changamoto tuliyonayo sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali lake kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kifaa cha incubator hutumika kuwasaidia watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati au wenye uzito pungufu ili kuwapatia joto na kuzuia wasipoteze maisha. Hadi sasa tuna incubators 214 nchi nzima kwenye hospitali mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo tafiti zimeonesha kuna changamoto nyingi sana za kutumia incubators kuliko faida zenyewe. Incubators zimesababisha kusambaa kwa magonjwa kutoka mtoto mmoja kwenda kwa mwingine atakayefuatia kulazwa hapo. Aidha, hakuna ukaribu wa mama aliyejifungua na mtoto aliyewekwa kwenye incubator.

Mheshimiwa Spika, matumizi ya incubator katika mazingira ambayo umeme siyo wa uhakika nayo inakuwa changamoto. Hivyo, katika mazingira hayo, incubator inaweza kuwa chanzo cha uambukizo na vifo badala ya kusaidia. Hata hivyo incubators chache zilizopo zinatumika kwa ajili ya watoto waliozaliwa na uzito pungufu sana (extreme low birth weight) kwa kuzingatia kanuni za usafi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, hivyo, Wizara inasisitiza kuwa kila hospitali ianzishe vyumba maalum kwa ajili ya matibabu ya watoto wachanga ili kuendana na mwongozo wa Kitaifa wa Matibabu ya Watoto Wachanga. Vyumba hivyo ni chumba cha huduma ya Mama Kangaroo, yaani mtoto anakaa na mama kifuani kwake muda mwingi kwa watoto waliozaliwa na uzito pungufu, lakini pia na chumba cha matibabu ya mtoto mchanga mgonjwa. Kufikia Julai, 2021, jumla ya hospitali 159 zilishaanzisha vyumba hivyo na kazi inaendelea kwenye hospitali nyingine. Ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani suala la kuwapatia wazee wasiojiweza vitambulisho kwa ajili ya kupata matibabu bure limetekelezwa kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge, kwa swali lake zuri na kwa mapenzi yake kwa wazee wetu ambapo nasi ni wazee watarajiwa; kwamba wanaendeleaje hawa wazee wasiojiweza kupata vitambulisho vya kupata matibabu bure, limetekelezwaje.

Mheshimiwa Spika, naomba kulijibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, zoezi la kuwatambua wazee na kuwapatia vitambulisho linaendeshwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa zote hapa nchini. Hadi kufikia Desemba, 2020 jumla ya wazee 2,344,747 wametambuliwa sawa na asilimia 87 ya makadirio ya wazee wote nchini. Kati yao wanaume ni 1,092,310 na wanawake ni 1,252,437. Aidha, wazee wasio na uwezo 1,087,008 wamepatiwa vitambulisho vya matibabu bure na wazee 856,052 wamepatiwa kadi za matibabu za Mfuko wa Afya ya Jamii iliyoboreshwa (iCHF).

Mheshimiwa Spika, vilevile, katika kuhakikisha kuwa makundi yote ikiwemo wazee wanapata huduma bila kuwa na kikwazo cha ugharamiaji, Serikali ipo kwenye hatua ya kuandaa Muswada wa Bima kwa wote utakaowasilishwa kwenye Bunge lako Tukufu ili kuundiwa sheria. Tunatarajia kwa hapa tulipofikia ni Novemba. Ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA Aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kuja na mpango mkakati wa kuwezesha NGOs kupata rasilimali fedha kupitia njia mbalimbali ikiwemo ruzuku katika maeneo mahsusi kama ambavyo inafanyika kwa Vyama vya Siasa, hasa baada ya uamuzi wa Serikali kuanzisha Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ambayo inahusisha Asasi za Kiraia katika malengo yake?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM Alijibu: -

Mheshimwa Mwenyekiti, ahsante sana. awali ya yote kwa ridhaa yako naomba niseme maneno machache tu kwa sababu hii ni Wizara mpya.

Mheshimwa Mwenyekiti, kwanza, naomba kutoa shukrani zangu za pekee kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa maono yake makubwa ya kuunda Wizara hii mpya itakayoshughulikia masuala ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalum.

Mheshimwa Mwenyekiti, hakika maono yake yamekuja kwa wakati ambapo kwa sasa kasi ya maendeleo kupitia msukumo wa teknolojia ni kubwa na changamoto za nchi yetu ni nyingi katika makundi mbalimbali ya jamii zetu, jambo ambalo linahitaji chombo mahususi cha kuangalia kwa kina zaidi changamoto hizi na fursa zilizopo ili kuweza kuiendeleza jamii yetu.

Mheshimwa Mwenyekiti, aidha, namshukuru kwa imani yake kwangu kuendelea kuniamini na kuniteua niweze kuisimamia Wizara hii. Mimi na timu yangu yote ambayo ametuamini tunaahidi hatutamuangusha. Tutaungana na jamii na wadau wote kuhakikisha tunaleta msukumo wenye tija kuendeleza maono aliyonayo na jamii yetu kuweza kuendelea na kuwa na ustawi.

Mheshimwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naomba nijielekeze kwenye swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum. Majibu ya swali hili ni kwamba: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa sasa haijatenga fungu maalum kwa ajili ya ruzuku kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Hata hivyo, Serikali kwa kutambua umuhimu wa mashirika hayo kuwa uendelevu, tarehe 30 Septemba, 2021 Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliagiza Wizara kwa kushirikiana na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na wadau mbalimbali kuandaa Mpango Mkakati wa kuwezesha mashirika haya kupunguza utegemezi. Rasimu ya andiko la awali la Mpango huu imeandaliwa ambayo imeainisha njia mbalimbali za kuwezesha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuweza kupata rasilimali za kutekeleza shughuli zao. Ahsante.
MHE. AMINA DAUDI HASSAN aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kutoa elimu kwa Wanawake kuepuka ndoa za siri ambazo zina changamoto ya malezi ya familia?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Daudi Hassan, Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa ndoa ni Taasisi muhimu katika kuimarisha haki na ustawi wa familia. Hivyo, Serikali kupitia utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wa mwaka 2017/2018 hadi 2021/2022 eneo namba nne linalohusu malezi na mahusiano ya familia imeendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu malezi chanya na mahusiano ndani ya familia ili kuwa na familia inayozingatia maadili mema.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia ipo kwenye hatua za mwisho za kukamilisha Mwongozo wa Taifa wa Uendeshaji, Usimamizi na Uratibu wa Mabaraza ya Usuluhishi wa Ndoa na Familia ambao utasaidia kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuzingatia taratibu za ufungaji wa ndoa pamoja na kuyajengea mabaraza ya usuluhishi wa migogoro ya ndoa na familia uwezo ili kuendelea kutoa elimu katika jamii.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI K.n.y. MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza: -

Je, Serikali ipo tayari kuanzisha shule maalum kikanda ili kusaidia watoto walioathirika na ukatili wa kijinsia?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathan Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwasaidia Watoto manusura wa ukatili, ambapo imeweka mifumo mbalimbali ikiwemo; Kamati za Jamii za Ulinzi wa Wanawake na Watoto; Madawati ya Jinsia kwenye Vituo vya Jeshi la Polisi na Magereza; Vituo vya Mkono kwa Mkono kwenye Hospitali; Madawati ya Jinsia Vyuo Vikuu na Kati; Madawati ya Ulinzi wa Watoto Shule za Msingi na Sekondari; pia Nyumba Salama kwa ajili ya Manusura kupata huduma jumuishi.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza: -

Je, lini Serikali itawahamisha wataalam wa maendeleo ya jamii kuwa chini ya Wizara?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali inatekeleza Tamko la Sera ya Ugatuaji wa Madaraka kutoka Serikali Kuu kwenda kwa wananchi kwa kushusha madaraka kutoka Serikali Kuu kwenda Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kusogeza huduma na utalaam karibu na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kufuatia kuundwa kwa Wizara hii ya Maendeleleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ambapo kada za msingi za kitaalam ni Maafisa Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii, Serikali inaendelea na hatua za kuimarisha mifumo ya uratibu ngazi ya Sekratarieti ya Mikoa na Halmashauri ili kujibu mahitaji ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara hii mpya.
MHE. MARTHA N. GWAU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili ikizingatiwa kuwa ukatili kwa watoto na wanawake umeongezeka?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Nehemia Gwau, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mpango wa kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili (kujenga nyumba za kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili), Serikali imeandaa Mwongozo wa Uanzishaji na Uendeshaji wa Nyumba Salama wa Mwaka 2019, kwa ajili ya manusura wa vitendo vya ukatili pamoja na wahanga wa biashara haramu wa usafirishaji wa binadamu. Lengo ni kuweka mazingira wezeshi kwa uanzishaji huduma ya nyumba salama kwa manusura wa ukatili wa kijinsia na kwa watoto hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hadi kufikia June 2023 jumla ya nyumba salama 12 zimeanzishwa na kusajiliwa katika Mikoa ya Arusha, Kigoma, Kilimanjaro, Dar es Salaam na Mwanza. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta binafsi kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma hii kwa mujibu wa Mwongozo wa mwaka 2019.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kufuatilia mila potofu za kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama hasa Manyara na Arusha?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi kuhusu mpango gani Serikali tunao kufuatilia mila potofu za kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama hasa mikoa ya Manyara na Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kuwa kuna mila zenye faida ambazo zinapaswa kuendelezwa na mila zenye kuleta madhara ambazo Mheshimiwa Mbunge ameziita “Mila potofu” ikiwemo mila ya kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama. Mila hii ina madhara kwa kuwa inachochea ukatili wa kihisia, ndoa za utotoni na ina mnyima mhusika haki yake ya msingi ya kumchagua mwenza wa kuishi naye umri utakapofika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutokomeza mila za aina hiyo, Serikali imeandaa utaratibu wa kufanya majadiliano kuhusu masuala ya kimila na majadiliano haya yanahitaji umakini mkubwa katika kuyajadili. Hivyo basi, Wizara imeandaa mwongozo wa Taifa wa uendeshaji majadiliano kuhusiana na mila na desturi zenye madhara kwa jamii wa mwaka 2022. Majadiliano hayo yanakuwa ni jumuishi yanayohusisha viongozi wa mila, viongozi wa dini, wazee maarufu na wataalam waliopo katika ngazi ya jamii ili kuja na ujumbe mahsusi wenye lengo la kutokomeza mila zenye madhara ikiwa ni pamoja na kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa Wataalam wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii waliopo ngazi za Jamii kuandaa majukwaa ya kuongoza majadiliano haya kuhusu mila hiyo yenye madhara na kuja na ujumbe mahsusi utakaotumika kutoa elimu ikiwa ni kwenye nyumba za ibada pia na kwenye redio mbalimbali. Ahsante.