Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Dorothy Onesphoro Gwajima (7 total)

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuweza kutoa mchango wangu wa dakika hizi chache kuhusu wasilisho hili wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano ijayo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa shukurani zangu za pekee kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini niendelee kuhudumu kwenye Sekta hii ya Afya.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Afya ni sekta ya huduma za jamii na mpango huu hauwezi ukatekelezeka kwa ufanisi mkubwa kama Taifa hili litakuwa na afya isiyo njema. Kwa hiyo, Sekta ya Afya tunatambua kwamba lazima tujikite kwenye masuala mazima ya kudhibiti magonjwa yasiyoambukizwa na pale inapotokea watu wameumwa, waweze kutibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mjadala huu kwenye Bunge hili ukiangalia umepambwa na imani kubwa kabisa inayotutaka Sekta ya Afya tusimamie Bima ya Afya kwa wote. Natambua kazi kubwa iliyofanywa ya mchakato huu wa kuelekea kwenye Bima ya Afya kwa wote, nami nimeipokea, tuko kwenye hatua za mwisho kabisa za kuleta Muswada wa Sheria. Awali tulidhani ni Septemba, lakini tumeona hapana, hapa tulipo tumeongeza kasi mpaka salamu mle imebadilika. Tukiingia, “Bima ya Afya kwa Wote! Kazi iendelee!” Ndiyo badala ya habari ya asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo ni kwamba, tupate ridhaa ya vyombo vyote vya Serikali kwenye hatua hii iliyofikia ya kuandaa rasimu wa Muswada wa Sheria ili Juni kwenye Bunge lako Tukufu tuje na huo Muswada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepata michango mingine mbalimbali, huu specifically ulikuwa umechangiwa na Mheshimiwa Josephat Kandege, Mbunge. Kwa hiyo, hili ndilo wasilisho letu kwenye hoja hiyo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara, yeye alichangia kusema kwamba katika maendeleo haya, hawa wa Biomedical Engineers wanajifunza kwa vitendo ile internship yao kwa kulipa pesa, hatuwezi kuharakisha maendeleo ya matengenezo ya vitaa tiba vya kisasa tunavyovipata. Akaomba kwamba tuwapunguzie malipo. Nasi sekta yetu imefuta hayo malipo waliyokuwa wanalipa huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia niongelee suala lingine lililochangiwa na Mheshimiwa Kandege kuhusu hatima ya maendeleo ya upatikanaji wa vifaa tiba nchini. Nitambue kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, kwamba mwaka 2018 mpaka 2020, shilingi bilioni 64 zimenunua vifaa tiba mbalimbali katika hospitali za kipigwa na katika Hospitali za Afya ya Msingi na bado zoezi hili linaendelea. Katika ngazi ya hospitali za kipingwa, tumeweza kutumia vifaa hivi vya kisasa kabisa kama LINAC na CT Simulators na vifaa vingine vingi, hadi tukapunguza rufaa za wagonjwa kwenda nje ya nchi kutoka 164 kwa mwaka 2015/ 2016 mpaka wawili mwaka 1920/2020. Kwa hiyo, mwaka huu sasa tutawasilisha bajeti ya shilingi bilioni 229 ili kuendeleza kupata vifaa tiba hivi kuanzia ngazi zote za kibingwa mpaka huko chini. Tunaomba Bunge lako Tukufu lipitishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala la watumishi. Watumishi bado ni changamoto na hapa tutawasilisha bajeti ya shilingi bilioni 144.9 tukiomba Bunge lako lipitishe ili tuweze kusogeza upatikanaji wa watumishi kwenye vituo mbalimbali vikiwepo hivi 487 vilivyojengwa kwenye ngazi ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja iliyochangiwa na Mheshimiwa Fatma Toufiq ya kuhusu namna gani tutaweza kuwafuatilia akina mama wajawazito waweze kujulikana wanapopata huduma ya Afya ya uzazi kuanzia kipindi cha mimba, wakati wa kujifungua na baada.

Mheshimiwa Spika, kwanza tumejenga hivi vituo kama nilivyovitaja hapo ambapo huduma zimesongezwa karibu yao na hospitali 102 za Halmashauri zimejengwa. Hapa tumemsikia Waziri, pacha wangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu Waziri wa nchi, TAMISEMI akisema kwamba amepewa maelekezo na Mheshimiwa Rais kuendelea kujenga hizo hospitali katika Halmashauri zilizobaki ambazo hazikujengewa. Yote hii ni mikakati ya kusogeza huduma za mama mjamzito ili aweze kuwa na ujauzito salama hadi kujifungua.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo tumebuni kitu kingine ambacho ni kanzidata, kwamba anaporipoti tu kliniki, ule wakati aliporipoti anaingizwa kwenye database, anafuatiliwa ili hata kama akipotea, tujue amepotelea wapi? Utekelezaji huu umeshaanza kutekelezwa Arusha, ambapo huko ndiko ameteuliwa Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Sichwale na tunaupeleka nchi nzima. Kwa hiyo, itakuwa ikishaingizwa pale, akipotea tu, mpaka VEO atuambie alipopotelea huyu mama, yuko wapi?

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa michango yote. Naunga mkono hoja, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii nami niweze kutoa mchango wangu kwenye kuelekea kuhitimisha mjadala huu wa hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuonyesha utayari na dhamira yake kubwa katika kuboresha sekta ya afya kwa manufaa ya wananchi.

Katika kipindi kifupi cha uongozi wake kama Rais achilia mbali historia yake ya awali ya kuitendea haki sana sekta hii tayari ameshafanya maamuzi makubwa mazito katika kuimarisha Sekta hii ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Spika, Baadhi tu ya maamuzi aliyoyafanya ni mtaji na msingi muhimu sana katika maendeleo endelevu ya sekta hii, ambapo kwanza amemteua Naibu Waziri mahsusi kwa ajili ya kushughulikia masuala ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamisi jambo ambalo litaimarisha sana uwezo wa sekta hii kuwagusa wananchi wa makundi haya ya jamii yaliyo msingi wa maendeleo ya Taifa (Wanawake, Watoto, Wazee na Vijana na masuala yote ya usawa wa kijinsia).

Mheshimiwa Spika, breaking news nzuri kabisa, Mheshimiwa Rais ameridhia na ametoa bilioni 80 mwaka huu mwezi huu Aprili 2021 ziende kuimarisha eneo la upatikanaji wa dawa, vipimo na vifaa tiba, eneo ambalo limezungumzwa kuwa kero kubwa sana kwa wananchi wetu sasa hivi. Utaratibu wa kununua dawa hizi haraka sana unaendelea ili tuzifikishe mahali sahihi. Hii ni nyongeza ya fedha iliyotolewa kipindi cha Julai mpaka Desemba ya bilioni 43, zikaongezwa nyingine kama 18 jumla bilioni 59 ambazo zilishaenda, ziko huko zinaendelea kufanya kazi yake.

Mheshimiwa Spika, vilevile kama ambavyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI alitoa taarifa Bungeni hapa Mheshimiwa Rais pia ametoa maelekezo kwamba, ujenzi wa hospitali za Halmashauri kwenye maeneo ambayo zilikuwa hazijajengwa uendelee. Kwa hiyo utaona ni namna gani Mheshimiwa Rais amejitoa kuimarisha sekta hii, nasi tunampongeza. Katika kipindi cha muda huu mfupi ambao amekaa inabidi sasa sisi tumuunge mkono na Wizara yangu itashirikiana sana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuhakikisha kwamba hatumwangushi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue sasa fursa hii kumpongeza sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa kuteuliwa kwake kushika nafasi hii nyeti ambayo ni mhimili wa huduma zote nchini ikiwemo huduma za afya, maendeleo ya jamii, jinsia wazee na watoto wanakoishi ambao 70% ya wananchi wote wa Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, nampongeza kwa hotuba yake nzuri ambayo imegusa vizuri sana utashi wa kisera tunazozitoa sisi Wizara ya Afya na miongozo ya kisera katika kuendeleza sekta hii ngazi ya afya ya msingi. Wizara yangu itatoa ushirikiano wa kila namna kuhakikisha kwamba maendeleo ya sekta hii ngazi ya halmashauri yanatimia sambamba na sera inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani kwa Wabunge wote waliochangia mambo mbalimbali ambayo mengine yamekuwa ni michango darasa kwa wataalam wote wa sekta ya afya tulio ngazi zote. Tuwaahidi kwamba tutayafanyia kazi, machache nitayataja hapa kama matano tu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Amandus Julius Chinguile alichangia kwenye masuala ya rasilimali watu yaani kuna upungufu wa rasilimali watu ambapo sasa Wizara imepokea hoja hii na inatambua upungufu mkubwa wa watumishi na imewasilisha maombi ya bajeti kwa mwaka huu 2021/2022 tunaouendea takriban bilioni 144 kwa ajili ya kuwaajiri watumishi wasiopungua 2,775 tunaamini kwamba bajeti hii itapitishwa na sisi pia hatutakuwa wachoyo tutakaa na TAMISEMI kuangalia kwamba tunawatumiaje hawa watumishi hasa waweze kugusa maeneo yale ambayo tumeyapigia kelele kwamba vituo vimejengwa na havifanyi kazi bado.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ajira hizi Wizara imebaini kuwa kuna haja ya kuimarisha uwajibikaji wa watumishi waliopo katika vituo vyetu. Kwanza kuwapangia maeneo kwa tija na kuwapa motisha waweze kufanya kazi kwa moyo Zaidi. Hivyo, tutashirikiana na Wizara zote za kisekta ikiwepo Utumishi na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuja na mpango wa jinsi gani watumishi wetu wanaofanya kazi vizuri watambuliwe kokote waliko, maana suala lingine kuwa na watumishi na suala lingine watumishi wale kuwa productive, efficiency inakaaje.

Mheshimiwa Spika, kuhusu maendeleo ya miundombinu ya afya, Wizara imesikia hitaji la kumalizia ujenzi wa miundombinu na kukarabati ile ya zamani pamoja na kuweka vifaa tiba stahiki, mitambo mbalimbali ya huduma za afya na magari ya wagonjwa (ambulance). Kwa kuwa Wizara yangu inahusika na kutafuta rasilimali toka vyanzo mbalimbali ikiwemo kuwashawishi wadau wa maendeleo waweze kutoa fedha, tutatekeleza jukumu hilo kwa nguvu zote na rasilimali tutakazopata tutazielekeza katika siyo tu hospitali za rufaa za mikoa kanda na Taifa bali tutalenga kuimarisha vituo hivi vya afya vya ngazi ya msingi kwenye halmashauri ili kupunguza rufaa za kwenda kwenye hospitali kubwa za kibingwa.

Mheshimiwa Spika, aidha, tutabuni mbinu nyingine mbalimbali za kuwashirikisha wadau wetu hasa sekta binafsi ili pale tunapokuwa na ufinyu wa bajeti kupitia PPP tuweze kuhakikisha tunakaa vizuri, wananchi wetu hawa tunaowapeleka kwenye bima ya afya kwa wote waweze kunufika na kuona faida ya huduma hizi wakiwa na bima hizo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu dawa na vifaa tiba na vipimo, kama nilivyosema tumepata hizi fedha na Serikali imekuwa ikijitahidi kuwekeza fedha nyingi, lakini sasa Wizara imeenda mbali kufuatilia nini hasa kinajiri eneo hili. Tumebaini changamoto nyingi huku zikiwa zinaweza kuepukika, kuanzia kwenye mfumo wa manunuzi changamoto za watumiaji, ikiwemo namna wanavyosimamia mtaji wa bidhaa za afya na bidhaa zenyewe zinapofika mikononi mwao kule kwenye vile vituo.

Mheshimiwa Spika, changamoto zingine ni namna gani watumishi wetu wamejiandaa kutoa huduma kwa weledi wenye mvuto customer care ili watumiaji wanaofika kwenye vituo vyetu wasiwe tu wale wa msamaha, waje na wale wanaoweza kulipa na wenye bima. Hili eneo tutashirikiana kulifanyia kazi ili hawa wanaoajiriwa wakawe na tija.

Mheshimiwa Spika, hivyo tutatendea haki utafiti huu na yatokanayo yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambapo tumeshabaini maeneo yetu ya kufanyia kazi hususan uwajibikaji dhidi ya vitendo vya ukosefu wa uzalendo, ubadhirifu na ufujaji na kutojali. Kwa kufanya hivyo tutamtendea haki Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kufanya maamuzi magumu aliyoyafanya kuwa licha ya sekta nyingi ambazo zinahitaji fedha hizi ameona kwamba atupe kipaumbele sekta ya afya kwa billioni hizi 80.

Mheshimiwa Spika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri, lakini hujaunga mkono hoja.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nimeunga mkono hoja na bima kwa wote Muswada unakuja Bungeni Juni kabla hatujamaliza Bunge. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kuzungumza na kwa maandishi wakati wa uwasilishaji wa hotuba yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mbunge aliyewasilisha maoni na ushauri wa Kamati kuhusu utekelezaji wa maagizo ya kamati kwa mwaka 2020/2021 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu kwa mwaka 2021/2022 na kuipongeza Wizara yangu, nasi tunamshukuru kwa kututia moyo. Pongezi hizo nimezipokea kwa niaba ya watumishi wetu wote wa sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutoa majibu ya hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge, napenda niwatambue Waheshimiwa Wabunge 34 waliochangia jumla ya hoja 57 katika hotuba yangu ambapo Waheshimiwa Wabunge 29 wamechangia kwa kuzungumza na wengine wameendelea leo ambao tumewarekodi kama sita na Waheshimiwa Wabunge watano wamechangia kwa maandishi. Nina imani kwamba wengine bado wanaendelea na tutuzidi kuzipokea na tutazifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, naomba pia niwashukuru na kuwatambua waliochangia wakati wa hotuba ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Mbunge ambao ni Waheshimiwa Wabunge 26 ambapo pia tumepokea michango yao na tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niwashukuru sana Manaibu Waziri wangu wote wawili kwa michango yao mizuri waliyoitoa kujibu hoja hizi kama utangulizi, kabla sijaendelea sasa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ni nyingi, nzuri zina tija, zina mashiko na zinafaa kufanyiwa kazi; na nyingi zinaweza kufanyiwa kazi vizuri kabisa pasipo hata kuwa na gharama kubwa sana, tukaweza kuleta mabadiliko. Wametufungua mawazo, wametutia moyo, nasi tunaahidi kwamba tumepokea. Mimi mwenyewe nilikaa hapa jana nikaandika sana, nina kila kitu, kama tutaweza kuwasilisha kwa maandishi wataona kwamba kila mmoja tumemtendea haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu michango ni mingi; na kwa sababu yote ni ya muhimu; na kwa sababu muda unaweze usitoshe naomba nijielekeze kwenye maeneo makubwa ambayo wengi sana yamewagusa, naamini hata ambao hawakuchangia kwa kuongea au kwa maandishi, itakuwa hizi zimewagusa.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ni masuala mazima ya dawa.nikimaliza hapo nitakwenda kwenye masuala ya upatikanaji wa watumishi; nikitoka hapo nitagusia masuala ya CAG na MSD kuhusu masuala ya Covid kupitia uzalishaji wa PPE, (Personal Protective Equipment), uliweza ukafanyika na ufafanuzi wake ni upi? Nitagusia kidogo kuhusu miradi ya ujenzi wa hospitali na tunahitaji na hospitali hizi zikamilike ili Muswada wa Sheria ya Bima ukute huduma zinapatikana. Muda ukiniruhusu nitakwenda kwenye maeneo mengine yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la uhaba wa dawa, iliripotiwa kwamba kutoka kwenye hoja za Kamati. Hii imezalishwa na hoja za Kamati, lakini pia Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa mdomo nao wamesema. Kuhusu uhaba wa dawa nchini iliwasilishwa kwamba katika mwaka wa 2021kiasi cha shilingi bilioni 200 kilihidhinishwa na Bunge kwa ajili ya dawa lakini hadi kufikia Machi, 2021 ni asilimia 26 tu ya fedha hizo zilikuwa zimetolewa. Hivyo bajeti inayoidhinishwa na Bunge iwe inatolewa kikamilifu na kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inakiri kwamba mwaka huu 2020/2021 ilitenga hizo shilingi bilioni 200, ambazo ziliidhinishwa na Bunge lako Tukufu kwa ajili ya kugharamia masuala ya dawa na vifaa na vifaa tiba na vitendanishi. Kiasi cha fedha kilichotolewa mathalani sasa kufikia Aprili, 2021 kimeshabadilika, figure sasa inasoma shilingi bilioni 151.38 na kiasi kilichobaki kama cha shilingi bilioni 50 hivi, tayari tumeshaongea na Wizara ya Fedha, tutapatiwa mwishoni mwa mwezi huu Mei ili tukaendelee kununua dawa ambazo zilikuwa zimebakia. Kwa hiyo, Serikali itatimiza lengo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imepokea ushauri na maelekezo ya Kamati katika kuendelea kuimarisha utoaji wa huduma za kinga ambapo pia inahusiana na dawa zitakazohusiana na kudhibiti magonjwa mbalimbali eneo hili. Hata hivyo, hali ya upatikanaji dawa muhimu jana nilisema ilifikia asilimia 75, lakini ukweli ukiangalia, suala la upatikanaji wa bidhaa za afya siyo ajenda ya kuongeza bajeti kama nilivyosema. Kama tusipoangalia mambo mapana sana eneo hili hapa tutakuwa kila siku tukiongeza hii bajeti tunajikuta dawa zimekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya utafiti kwenye Halmashauri zote 184, tumefanya utafiti kwenye hospitali zetu 28 za mikoa, vile vile tumetumia uzoefu ukiwemo wangu mwenyewe nilipokuwa Singida ambapo tulifanya sana mambo haya ya dawa, tumeshirikiana na wadau wetu wote na wataalam wetu wote. Kwa pamoja tumesema lazima tujirekebishe na kujirekebisha huko kuna watu watachukuliwa hatua na wengine wameshachukuliwa, kama MSD, 24 wamefukuzwa kazi na wawili wameshushwa mishahara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwenye Halmashauri, katika Hospitali za Mkoa, taarifa tayari imeshakwenda kwenye vyomba vya sheria kwa ajili ya kuwachukulia hatua. Hii ni kwa sababu kuna uzembe mkubwa sana tena hapa ni wa hatari, nimeuambatisha kwenye kiambatisho changu cha hotuba niliyoiwasilisha jana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tukishamalizana; yaani tunakwenda sambasamba kwamba waliokutwa na hizi hatia za kuwa wamefanya ubadhirifu, wamepoteza, wamedokoa, vyombo vya sheria tumeshawakibidhi taarifa, wanafanya kazi zao. Hawa ni PCCB, watajua wafanye nini. Vile vile mwajiri na waajiri wote wanaohusika, wanachukua hatua zao kwa sababu kuna Sheria za Ajira za Utumishi wa Umma dhidi ya mtu aliyebainika na hayo makosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumechukuwa dimension nyingine ya kwenda kwenye vyombo vya taaluma, yaani Mabaraza na Bodi; lazima tuulizane kwamba hivi unakuwaje mwanataaluma ambaye uzingatii taaluma yako? Wengi wanajitetea kwamba ni uchache wa watumishi, lakini tunakuta matatizo kama haya hata kwenye vituo vikubwa ambavyo watumishi mashallah, wana nafuu, lakini mtu unamwuliza maswali anashindwa kujitetea. Kwa hiyo, tunataka tushughulike na hili suala zima.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, kuna dimension nyingine, lazima tuwekeze mazingira ya uwekezaji wa viwanda kuwa mazuri. Jana nilisema viwanda vimeongezeka nchini, sasa tunaongelea hesabu; vilikuwa tisa, sasa viko 11; 16 viko kwenye hatua ya ujenzi na 15 vinajengwa. Maana yake nini? Bei ya kununua hizi bidhaa za afya nje ya nchi sasa itakuwa ni ndogo kwa sababu tutakuwa tunanunua hapa ndani. Kwa hiyo, tunaweka mazingira rafiki na mwongozo uko tayari na ndiyo umetufikisha hapo ili hawa wanaowekeza wawekeze hapa nchini na hela yetu hii tunayosema ni ndogo tuitumie vizuri tupate mzigo mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaangalia dimension ya ajira kwa watumishi, wataalam wanaohusiana na dawa. Ni kweli utakuta kwenye zahanati au kwenye vituo vya afya watalaam wale ni wauguzi tu, hajasomea dawa. Wakati mwingine unaangalia kumbebesha hili tatizo. Kwa hiyo, kwenye ajira nitakazozisema hapa, tunaangalia Wafamasia pamoja na Wafamasia Wasaidizi tuweze kuwaongeza, tuwapeleke kwenye maeneo yale ambayo yana huduma kubwa zaidi ukilinganisha na yale madogo wataweza kuwafanyia supervision wale wa chini yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dimension ni nyingi, TEHAMA tumeshajitahidi. Tumefunga TEHAMA, nimeeleza kwenye hotuba yangu; tunataka tuziboreshe zaidi kiasi kwamba tukienda kwenye ule mfumo tuione dawa inaishia pale kwa mgonjwa yule. Pia tumeboresha prescriptions za dawa kwamba zinakuwa na leaf tatu; leaf ya kwanza, yaani stakabadhi moja, unapewa wewe mgonjwa uondoke nayo, stakabadhi moja anakaa nayo daktari aliyekuandikia, stakabadhi moja inakaa kwenye dirisha la dawa. Hiyo stakabadhi inakuwa na simu ya yule mgonjwa. Yule daktari tutamwuliza, wewe uliandika panadol ngapi mwezi huu mpaka kitabu hiki kimeisha chenye leaf labda 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tutaona, tutaenda kufanya reconciliation na dirishani, tukitaka tutampigia mpaka mgonjwa tujue. Sasa tutashangaa kama daktari ameandika makopo 20, lakini wagonjwa aliowaona ni wagonjwa wanaoweza wakatumia makopo mawili au kopo moja. Mifumo hii midogo midogo iliachwa, leo hii ukienda pale mtu anapewa dawa tu kama njugu hapewi ile risiti na akipewa haendi nayo nyumbani; lakini benki ukienda unaweka hela zako wewe mwenyewe, unapewa na risiti upeleke nyumbani kwenu ushahidi. Tunataka tuurudishe ule mfumo wa control and cheques ili tuanze kulinda hizi rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dimension nyingine ambayo ningependa kuiongelea hapa, suala la kununua dawa, tunaratibu utekelezaji wa mwongozo wa cost sharing; yaani ni kwamba zamani tulikuwa na mwongozo lakini sasa hivi tumeuboresha. Ni kwamba utakuwa ukinunua hizi dawa, tunawezesha ile revolving yake iweze kuonekana. Zamani tulikuwa tunasema asilimia 67 tunazoweza kuzitumia kwenye eneo la dawa, lakini watu wanakuja wanakwenda chini ya hapo; data zinatuonyesha mtu anatumia asilimia chini ya asilimia 50 (less than 50) hata asilimia 25. Ameletewa bidhaa za dawa, akawapatia wateja, wakachangia pesa, lakini hakurudisha kwenda kununua dawa, definitely mtaji uta- Collapse, kwa sababu inatakiwa iwe revolved.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukajiuliza huwezi ku- revolve dawa peke yake, lazima uende kwenye dimension ya quality care; uboreshe huduma ili wateja wanaokuja pale pia wawe akina sisi ambao tukiugua na kadi zetu za bima, tunaamua kwenda hospitali zile za akina fulani badala ya kwenda zile za kwetu. Kwa sababu ukienda pale unajibiwa vibaya, mazingira mabovu, hupendelei. Kwa hiyo, tunakuwa tunapata watu wa msamaha kama wale niliowasilisha data jana kwamba kwenye Regional Referral Hospital shilingi bilioni nne, kwenye hospitali zetu kubwa za kibingwa, shilingi bilioni 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi ni barriers za management system.zinazosababisha hata huo mtaji wa dawa ukija unaenda kuwapatia watu wasio na bima, kwa sababu wenye bima wameondoka, bima inakuwa inakwenda kwenye vituo vingine na kwenye Serikali hamna kitu; lakini tuna watumishi wetu badala ya kufanya kazi kwenye vituo vyetu na wenyewe wanaondoka, wanakwenda kule private. Kwa hiyo, kuna vurugu nyingi sana hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu, niwape moyo kwamba tumedhamiria kuboresha eneo hili hapa kwa kuangalia determinants zote zinazosababisha mtaji wa dawa uyumbe ili tuondoke kwenye dhana ya kwamba Hazina ziko pesa, tutaongeza, tutaongeza; tuweze kufanya revolving kwa kutumia fursa ambazo wenzetu wa private wanafanya na wanaweza kulipa maji, majengo, mishahara, promotion bila kelele kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote ili yatekelezeke na yasiwe hadithi, tumeamua kufungamanisha kwenye mikataba ya uwajibikaji kwamba sasa tutageuza sasa hizi ziwe Score Card Performance Criteria ili huyu anayepewa kazi hiyo aweze kutekeleza na kupimwa. Hata hivyo tunajiuliza, hizi dawa zinapotelea kule kwenye Halmashauri, determinant gani nyingine tumeiacha? Ni elimu. Tumefurahi sana kuona leo Wabunge wanaongelea habari ya dawa na wanakiri wenyewe kwamba kweli zinaibwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema kule Halmashauri tuna mageti yote ya ulinzi, tuna Kamati ya Huduma za Jamii, tuna Kamati ya Mipango na Fedha ya Baraza la Madiwani, tuna Bodi zetu na tuna Kamati za vituo. Huenda hawaelewi. Ripoti zikiletwa hawawezi kugundua viashiria vya upotevu wa dawa au ubadhirifu. Tutawapa elimu hawa wakiwemo Wabunge ambao pia ni Madiwani, wataweza kuwa na uwezo wa kubaini nini kinaendelea hapa na kuchukuwa hatua kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze kwenye madeni yote ya dawa. Ilitolewa hoja hapa kwamba, kwa nini yasifutwe na Wizara ya Fedha? Serikali imeendelea kulipa madeni kwa kadri yanavyohakikiwa ambapo hadi mwezi Aprili, 2021 imeshalipa jumla ya shilingi bilioni 16.3 na hivyo kubaki kiasi cha shilingi bilioni 260.7. Kati ya deni hilo, shilingi bilioni 31.9 ni deni la vituo vya kutolea huduma za afya na shilingi bilioni 228.7 linatokana na utunzaji na usambazaji wa bidhaa za afya za miradi misonge. Serikali haijafikia utaratibu wa kulifuta hilo deni, lakini imedhamiria kuendelea kulipa deni hilo ili kuiboreshea bohari ya dawa (MSD) iweze kuimarisha mtaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, naomba niseme mbele ya Bunge lako Tufufu kwamba madeni haya yatalipwa na Serikali kupitia Wizara ya Fedha na imeshaanza, lakini tumeweka utaratibu mzuri, vituo vyetu vinadaiwa visinyimwe dawa kule MSD. Kuna makubaliano tu wanawekeana pale, wanakuwa wanazichukuwa zile dawa ili na wenyewe wajenge uwajibikaji wa kwenda kusimamia hiyo rasilimali kama nilivyosema. Usipofanya hivyo, unakuta mtu anakosea fomu ya bima, takribani shilingi bilioni 2.4 hazijalipwa na bima kwa sababu walipohudumia wateja wa bima badala wajaze vizuri ili hizo hela zikalipwe kule, wakakosea halafu hawakuulizana hata kuulizana kwa nini tumekosea, tujirekebishe wapi? Ikawa ni mtindo, ni trend hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunataka na wao tuwafundishe kwamba watakuwa wanalipa kidogo kidogo bila kunyimwa dawa, lakini waende kwenye uwajibikaji uliotukuka kuangalia determinants zote hizi ili kesho tuwe na uongozi wenye ubunifu katika kusimamia rasilimali za Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kiwanda cha Simiyu Medical Product kuna hoja ilitolewa hapa. Hoja hii imeshafanyiwa kazi na tuko kwenye hatua za mwisho za kukamilisha uanzishaji wa kiwanda kitakachozalisha bidhaa zitakazotumika katika vituo vya kutolea huduma za afya zinazotumia malighafi yetu ya Tanzania yaani pamba. Serikali kupitia Hazina inakamilisha taratibu muhimu kabla ya kuanza ujenzi wa kiwanda husika Mkoani Simiyu. Tutalisimamia hili kwa sababu mifuko iliyokuwa inafadhili imekubaliana na imeshawekana sawa, sasa ilikuwa ni utaratibu tu ya kwamba hizo hela zitakapotolewa zitaweza vipi ku-revolve. Hili tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na ushauri kuhusu mifumo ya kieletroniki; nimesema hii tutahakikisha tunaiimarisha sana katika vituo vyetu, hivi sasa ngazi ya Taifa vituo saba vinatumia mifumo ya TEHAMA maana ni vituo vyote; kwa ngazi ya mikoa vituo 14 kati ya 28 vinatumia mifumo ya TEHAMA; katika ngazi ya huduma ya msingi, Halmashauri vituo 971 kati ya 7,279 vinatumia hiyo mifumo. Kwa sababu tumeanza kutengeneza mifumo hii kwa wataalam wetu wa ndani, itakuwa rahisi sana kuipeleka kule kwa kasi kubwa katika kipindi hiki ili tuweze kuboresha ufuatiliaji wa taarifa zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kidogo niongelee kuhusu masuala mazima ya rasilimali watu. Katika upande wa rasilimali watu, kulikuwa na hoja kwamba kuwepo na mkakati wa makusudi wa kuajiri watumishi wa sekta ya afya na Serikali hususani Ofisi ya Rais, Menejementi ya Utumishi wa Umma, ihakikishe inatoa vibali vya ajira kwa watumishi wa afya hasa ikizingatiwa kuwa kuna wataaalam wengi mtaani. Ndiyo kuna wataalam wengi mtaani ambao tumewasomesha wenyewe lakini hatujaweza kuwapatia kazi na ni wa kada mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tumejiongeza. Pamoja na kuajiri watumishi wapya kila mwaka, idadi yao kweli bado haikidhi kama nilivyosema. Kwa hiyo, sasa hivi tuna hivi vituo vyetu ambavyo havifanyi kazi. Tuna wastani wa watumishi 2,800 wanastaafu kila mwaka ambapo tumekuwa hatufanyi replacement kwa kasi. Kama mlivyosikia leo hapa Mheshimiwa Mbunge wetu mmoja alichangia kwamba kumetokea matangazo ya kazi, tuna nafasi takribani 3,337 ukijkumlisha za Wizara ya Afya pamoja na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambapo hizi ni replacement, ndiyo zimetangazwa na ndiyo tunaendelea kuzifanyia kazi ili kusukuma upatikanaji wa watumishi walioajiariwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kibali chetu cha ajira 2021 maombi ya kibali cha ajira mpya ili kuajiri jumla ya watumishi 13.3 pamoja na kibali cha ajira mbadala hiki nilichokisema sasa hivi, kimetolewa ili kuziba nafasi hizo. Tukaona kwamba hapana, tusiendelee tu kwenye kutegemea kuajiri, lazima tujiongeze, tufanyeje ili kuongeza speed ya wenzetu ambao hawana kazi waweze kupata kazi? Tumetayarisha mwongozo, upo kwenye mapitio ya mwisho katika vyombo vyetu Serikali ili tuweze kuwaajiri watumishi wetu kwa mikataba wakati tunasubiri ile ajira kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo ule ukipita, tutaweza kumchukuwa mtumishi tukamwajiri kwa mkataba na anaweza akalipwa nusu ya mshahara wa mtu aliyeajiriwa kama mapendekezo yatapita, kwa hiyo, tutaweza kuwawatia moyo wasikae nyumbani kupoteza ujuzi walionao, wawepo na sisi kadri Serikali inavyopata uwezo, tunazidi kuwachukuwa. Uwezo huo wa kuajiri asilimia 100 lazima tukubaliane tu ni changamoto, siyo tu Tanzania, ni kote kule. Sijui ni wapi walishafika asilimia 100, kwa sababu tunazaliwa kwa asilimia 2.7 kwa mwaka, yaani ni kama vile watu milioni tatu. Unatengeneza hospitali tatu za mikoa, zinazohitaji ikama ya watu 600; sasa, hapa lazima tukubali kuja na huu ubunifu ili tuweze kwenda na mabadiliko ya sayansi na teknolojia katika mustakabali mzima wa kukuza Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumegundua kwamba ukiacha suala la ajira lazima pia hapa tuangalie dimension ya productivity. Unakuta tunao watumishi, ukienda kufuatilia productivity yao ipo chini, au sehemu nyingine wako wengi sana, sehemu nyingine wako wachache sana. Wamekaa kwenye maeneo ya mijini; unakuta wako wengi kwa namba au skills pale ziko nyingi. Tunafanya assessment, tunaitaga WISN, ambayo ni Workload Indicator of Staffing Needs ili tuone wingi wa kazi pale walipo ili tuweze kuwasambaza kwenda kwenye maeneo mengine ambayo yana uhitaji mkubwa kuliko hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii tunaiita redistribution, ilifanyika katika mikoa 11 ambapo ilisaidia kuwapeleka watumishi kwenye ngazi za zahanati na vituo vya afya na maeneo mengine yenye uhitaji. Mikoa iliyotumia mfumo huu ni pamoja na Iringa, Pwani, Tanga, Mwanza, Shinyanga, Dodoma, Morogoro, Ruvuma, Songwe Mara na Lindi; na tunaendelea.

Naomba nigusie hoja ya CAG. Ilitolewa kwamba ripoti ya CAG imebaini kuna changamoto katika ununuzi na uendeshaji wa mtambo wa kuzalisha barakoa MSD na je, Serikali ina maelezo gani kuhusiana na suala hili? Nimefanya ufuatiliaji, tumefanya ufuatuliaji pamoja na wenzangu wote na taarifa ifuatayo naomba kuiwasilisha kwako.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto ya upatikanji wa barakoa nchini na duniani wakati wa janga lilipokuwa kwenye kasi kubwa Covid 19 Serikali kupitia bohari ya dawa (MSD) iliamua kununua kwa dharura mtambo wa kuzalisha barakoa wenye thamani ya dola za Kimarekani 108,700. Mtambo huo ulianza kufanya kazi mwezi Agosti, 2020 ambapo uwezo mtambo huo wakati huo ilikuwa ni kuzalisha barakoa 48,000 kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtambo ulipoanza kufanya kazi ilibainika kuwa compressor yake ilikuwa na uwezo mdogo wa kufanya kazi, hivyo watumishi walipatiwa mafunzo ya kutumia mtambo huo ili kuweza kufanya kazi kwa ufanisi. Hivyo, baadaye, baada ya compressor hiyo kuwa imeshanunuliwa uzalishaji katika miezi mitatu ya mwanzo, Agosti, Septemba, ni kweli ulikuwa mdogo lakini baadaye ulipanda kwa 148,000 kwa siku. Kutokana na uwekezaji wa mahitaji ya barakoa kwa vituo vya kutolea huduma za afya sasa vituo hivi vinapata pale MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu maneno machache kwamba, sisi kama nchi, masuala haya ya barakoa, masuala ya gloves, gowns, protective gear, ni lazima tufike mahali tujihami sisi wenyewe. Hivi ni vitu vya dharura, vinahitajika ICU, vinahitajika kwenye dharura zetu zote zingine zile za majanga, tuna matishio ya Ebola, tuna matishio ya vipindupindu na mambo kama hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ilikuwa ni sawa na tija kufanya haya maamuzi ili ile inunuliwe iweze kufanya kazi pale. Hata huko tunakokwenda, huenda tukanunua hata mitambo mingine ya kufanya ulinzi wa wataalam wetu, maana ukitegemea nje katika nyakati kama hizi ndipo unapouziwa barakoa moja shilingi 100,000 unaanza kutengeneza hoja nyingine tena, ilikuwaje, zile hela zinakuwa hazitoshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba ieleweke tu kwamba taarifa sahihi ni kama nilivyotoa. Huo mtambo capacity yake kwa sasa ni hiyo na ulikuwa ni muhimu na tunahitaji mitambo kama hiyo ili ulinzi wetu katika eneo la afya uwe mzuri zaidi badala ya kutegemea nje ambako zikija tena tunasema hazina viwango.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kidogo kuhusu miradi ya ujenzi. Miradi ya ujenzi tunayo mingi, niliripoti jana miradi 22 kwenye Kiambatisho Na. 14. Hapa ilitolewa hoja kwamba kule Katavi mkandarasi hayuko site licha ya kwamba alitakiwa akabidhi mradi Januari, 2021; kule Hospitali ya Mkoa wa Simiyu nako anasuasua; mradi wa Tumbi nao, EMD nao hauko vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi unatekelezwa na Mkandarasi SUMA – JKT. Baada ya kuufuatilia na kuona changamoto zake ambazo zilifanyiwa kazi ikapelekea mpaka kubadilisha consultant, nimekaa kikao mimi mwenyewe na SUMA – JKT na wale maafande wote tukakubaliana kwamba mradi huo wa Katavi lazima ukamilike kwa wakati. Tunahama kutoka kwenye conventional contracting tunakwenda kwenye force account, maana tumeona kule ndiyo kuna tija tutaweza kusimamia ukilinganisha na utaratibu uliotumika mwanzo ili tuweze kwenda na wakati, ifikapo Desemba au mapema Januari mwakani mradi huu uwe umekamilika uanze kutoa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Tumbi ulikuwa na matatizo, nilitoa maelekezo kwamba ufanyiwe ukaguzi wa kina, kwa sababu ni hatari sana kuja kufikia mahali umemaliza mradi halafu ukakuta kuna tatizo. Taarifa RAS ameifanya, ameikamilisha ataileta na hela zao, bilioni tatu, zipo, tutaziomba zitoke ziende kumalizia kulingana na ile taarifa imesemaje. Hatuwezi kuishia tulipoishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa kifupi miradi yote hii ambayo inaleta changamoto na sisi tumeamua kupambana na hizo changamoto, ikibidi kwa ku-review ile mikataba tuweze kwenda kwenye force account ku- accelerate speed ya kwenda mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na suala kuhusu kumalizia Wodi ya Saratani Bugando. Hii Wodi ya Saratani Bugando ni muhimu sana, tena itapunguza msongamano sana katika Hospitali yetu ya Ocean Road, lakini itawapunguzia wananchi mzigo wa kwenda Ocean Road, kuhama na ndugu zao waje, gharama zinakuwa kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetenga fedha kwenye mwaka huu ambazo ni kama bilioni 1.8, tutazitoa. Tutaangalia kama tutaweza kwenda na kasi ya kumaliza hizo hela kwa wakati ili hela isilale ili tuweze kufanya mpango kupitia Kamati yetu ya Bajeti. Ni suala la kuomba tu kibali kwamba hawa wamekwenda na kasi inayotakiwa tuweze kuona namna gani tutafanya reallocation ndani ya Fungu la Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Afya kuweza kuhakikisha ile wodi inakamilika. Maana vinginevyo, kama hatutafanya hivyo, tunaendelea kuwaumiza hawa wananchi na kuendelea kuiumiza Ocean Road kwa wagonjwa ambao wangeweza wakatibiwa huko waliko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Hospitali yetu ya Kwangwa iliyoko Mara kwamba ikamilishwe mapema, kwani ikikamilika inamuenzi Hayati Mwalimu Nyerere. Ni kweli, Wizara imedhamiria kukamilisha hospitali hii. Inajengwa kwa jengo moja ambalo lina vitalu vitatu; Kitalu A, Kitalu B na Kitalu C. Kwa sasa jengo la Kitalu C limekamilika na huduma za afya ya mama na mtoto zinaendelea kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetenga bilioni 11 katika bajeti ya fedha ya mwaka 2021/2022 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo la Hospitali ya Mkoa wa Mara, Kitalu A na Kitalu B, ujenzi wa jengo la kuhifadhia maiti, jengo la kufulia na kuboresha mazingira yanayozunguka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara, kwa hiyo tuko serious kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona muda wangu umekwisha, nimalizie tu neno moja kuhusu madirisha mangapi ya kutolea huduma kwa wazee. Tuko serious na wazee; kama juzi tulipokuwa na Mheshimiwa Rais niliweza kusema kwamba tumekwenda mbele, tumefanya kikao na mitandao inayoratibu shughuli za wazee ambayo ni taasisi zao mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kwamba madirisha ta wazee yasiwe tatizo. Tumekwenda kuteua watu watatu kila kituo; Muuguzi yupo, Daktari yupo na Nesi yupo, hawa tutawavalisha ma-T-shirt yanaitwa Nakupenda Sana Mzee. Watakuwa wakifika pale hata kama watumishi ni wachache hakuna dirisha maalum, apokelewe kama VIP, apelekwe kwenye chumba ambacho kitamuona huyu mzee. Mwenyekiti wa hii shughuli ni mimi mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tayari wataalam wangu wameshakusanya haya majina na numbers zipo kule, mdogomdogo tumeshaanza. Sisi wenyewe ni wazee watarajiwa, tupende kukutana na mambo ambayo tulijiandalia sisi wenyewe huku wakati tukiwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Wazee tunaifanyia mapitio ili ije kuwa sheria ambayo itatambua haki zao kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha hoja na yote mengine yaliyosemwa sisi tumeyapokea, wanaoniomba niambatane nao kwenye majimbo yao niko tayari, baada ya Idi tunakwenda wote tukayaone yaliyoko huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia machache kuhusu taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo na Huduma za Jamii.

Awali ya yote natoa shukrani sana za pekee kwa Mheshimiwa Dkt. Stanslaus Nyongo pamoja na Wajumbe wa Kamati hii ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa kazi nzuri waliyoifanya. Amewasilisha taarifa hapa na kwa uongozi wake makini mpaka hapa tulipo, Wizara hii imetimiza sasa takribani mwaka mmoja ikiwa na utekelezaji kama uliowasilishwa.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya na uongozi wake kwa kuiunda hii Wizara na kuweza kuipatia fedha katika mtiririko mzuri hadi katika miezi sita ya kwanza karibu asilimia 50 ya fedha zilishapatikana na kazi ikafanyika kama ilivyowasilishwa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maeneo yote ya utekelezaji naipongeza Kamati kwa kuibua changamoto ambazo baadhi wameziripoti hapa na nitazazisemea baadhi ambazo ni za msingi sana katika kuendelea kuifanya Wizara hii kuwa na utekelezaji mzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu upungufu wa watumishi, tutaendelea kuomba nafasi za ajira kwa kadri ya uwezo wa Serikali. Hata hivyo, tutakuja na ushawishi ili sekta zote sasa za binafsi pamoja na za umma zione umuhimu wa kuajiri hizi kada za maendeleo ya jamii. Kwa sababu katika zama za sasa na changamoto tunazokwenda nazo kiuchumi, Maafisa Maendeleo wanahitajika katika kila taasisi, lakini maafisa Ustawi wa Jamii nao wanahitajika kila taasisi. Yaani ukiwa na kundi la watu bila ustawi wa jamii matatizo yake ndiyo kama haya tunayoyaona, kwa sababu wale watu wanakuwa bado hawajaandaliwa kubadilika fikra waende na nyakati za sasa.

Mheshimiwa Spika, tunaandaa pia sheria ya taaluma hizi za maendeleo na ustawi wa jamii ili waweze kusajiliwa kama wanataaluma, waweze pia kupata fursa ya kufungua huduma binafsi kama ilivyo huduma za elimu na afya hivyo kuongeza wigo wa wataalam hawa na upatikanaji wa huduma, wananchi waendelee kunufaika sambamba na ajira za Serikali ili walioko kule sokoni waweze kupata hizi ajira.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ukatili wa kijinsia na kwa watoto. Imeibuka hapa hoja nzuri sana ya masuala ya ukatili hasa kwa Watoto na pia kwa jinsia, imeonekana na wanaume pia ni wahanga.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee kwanza kwa Watoto; kwa upande wa watoto na wanawake tunao mpango wa Serikali tangu mwaka 2017, tulikuwa tunatekeleza, unaitwa Mpango Kazi wa Kutokomeza Ukatili kwa Wanawake na Watoto. Mpango huu umejielekeza kuangalia mambo mtambuka yakiwemo masuala ya kuinua uchumi wa kaya, jambo ambalo Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hasan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imelitilia mkazo sana, kwa sababu wanawake walikuwa wameachwa nyuma sana kama ilivyoelezwa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa.

Mheshimiwa Spika, hatuna maana ya kuwaacha wanaume nyuma, tuna maana ya kupiga mbio ili tuvute kundi la akinamama lisogee na wenyewe juu ili huu ukatili unaopatikana kutokana na uchumi, wenyewe urudi chini. Hata hivyo, tunazo programu zingine mbili ambazo zinawalenga jinsia zote wa kiume na wa kike. Moja inamlea mtoto kuanzia miaka 0-8 na nyingine inachukua kuanzia miaka 10-19, kuwaandaa hawa vijana kuanzia umri wa awali mpaka wawe vijana balehe wavuke salama. Huku tukiangazia kuwafundisha elimu, kuepuka magonjwa, lishe nzuri pamoja na fursa za uchumi. Kwa hiyo akinababa tunaomba mtupe nafasi kwanza tuwasogeze sogeze akinamama, mliwaacha nyuma sana, hatuna maana tutawarudisha nyuma, tutakwenda pamoja kupitia hizi programu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mpango huu wa kutokomeza sasa ukatili mpaka kule vijijini, kuna Kamati za Kutokomeza Ukatili kwa Wanawake na Watoto. Hata hivyo, hawa watoto ni wa kiume pia mle ndani. Sasa suala la akinababa kwamba wanakatiliwa, tunawakaribisha kwenye madawati ya jinsia. Yapo kwenye vituo vyote vya polisi. Ukiona umepigwa na umeonewa karibuni. Sasa hivi tuna mitandao ya akinababa wanaonyanyaswa na wake zao. Tukajiunge huko tupaze sauti, tufanye utafiti vizuri tuje na program baadaye ambayo inasheheni data za kitaalam. Maana hamjitokezi, tunashindwa kujua ukubwa wa tatizo. Kwa hiyo tunawakaribisha kwenye madawati ya kijinsia.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba vita ya kupinga ukatili haitatokea tu kwa mikakati, sera na sheria nzuri, bali kwa mabadiliko ya kifikra, tunaposema tuwe karibu na watoto, tuwe karibu na watoto, tunapoimbaimba don’t touch here and there, sio kwamba tunachekesha chekesha. Tuimbe wote ili watoto waimbe na sisi, waelewe ishara kama unavyomwambia pale pana nyoka haendi, aelewe kwamba hata maeneo haya na haya mtu akikugusa ukatae. Hatuchekeshi tuko serious, kuwa karibu na watoto tuunge mkono. Nawapongeza wotu wanaoimba don’t touch, moto uendelee mpaka watoto tucheze nao, turuke nao sarakasi, ukutiukuti ili akiguswa kama ambavyo akiona nyoka au simba anakueleza. basi pia iwe ni ishara ya yeye kwenye fahamu zake kuona kwamba hili ni hapana nimwambie baba na mama.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, nashukuru sana kwa Kamati, mapambano yanaendelea, ukatili Tanzania haukubaliki, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata fursa hii mbele ya Bunge lako Tukufu kuweza kuhitimisha hoja yangu ambayo imepokelewa na kujadiliwa siku ya leo hapa Bungeni kwenye kipindi hiki cha asubuhi.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kuisimamia Wizara hii na kutupatia miongozo na maelekezo ambayo imetufikisha mpaka hapa ambapo Waheshimiwa Wabunge mmeweza kutoa pongezi zenu, tumezipokea, na kutuasa tuendelee na kazi kadri tunavyozidi kuwezeshwa na jemedari wa kwanza Mheshimiwa Dkt, Samia Suluhu Hassan aliyeiunda hii Wizara ya Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Spika, Shukrani zangu ziende kwa Makamu wa Rais Mheshimiwa Isdor Mpango kwa jinsi anavyotusaidia katika miongozo pamoja na maelekezo na kufuatilia masuala ya usawa wa kijinsia. Kila anapokwenda kwenye shughuli zake za utekelezaji tumekuwa tukimskia akiweka mkazo kwenye masuala ya maadili tuweze kudhibiti mmomonyoko wa maadili katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, vilevile shukrani kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa (Mb), kwa jinsi ambavyo ametoa uongozi kwa mawaziri pamoja na Wizara yetu katika kuendelea kupambana kuboresha huduma za ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Spika, nikushuru wewe mwenyewe kwa jinsi ambavyo umekuwa ukiliongoza Bunge lako pamoja na sisi wenyewe Wizara ya Maendeleo ya Jamii. Kwanza umetuundia Kamati nzuri kabisa ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na kutupatia viongozi mahiri kabisa ambao wameendelea kutupatia uongozi na maelekezo ambayo yametufikisha tulipo. Shukrani kwa Kamati yangu chini ya uongozi wa Mheshimiwa Toufiq (Mb), ambaye ndio mwenyekiti wa Kamati hii pamoja na wajumbe wote wa Kamati kwa jinsi wanvyoendelea kutuongoza.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru Wabunge wote kwa maswali ambayo mmekuwa mkiuliza na michango ambayo mmekuwa mkitupatia. Hoja mbalimbali ambazo mmekuwa mkizilta zimekuwa chachu ya kutufanya sisi tufikiri zaidi jinsi ya kwenda mbele katika hii Wizara kubwa ambayo leo hapa nimeona ikifananishwa unga wa ngano, na kweli kabisa ni sawa, ina mambo mengi sana kwa sababu jamii na ina mambo mengi sana. Hii ni bahari inayounganisha Wizara zote zingine kwenda kufikia jamii.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru Mawaziri wenzangu wote ambao wameendelea kufanya kazi hizi kwa ushirikiano wa kisekta na wameweza kuchangia pakubwa hasa katika suala la ajenda ya jukwaa la usawa wa kijinsia ambayo nimeielezea hapa. Haiwezi kutekelezwa na mtu mmoja, hii inatekelezwa na sekta zote. Ukigusa maji, ukigusa kilimo, ukigusa nishati, sisi wote, biashara tunatekeleza masuala haya ya kwenda kumkomboa mwanamke na kumwezesha kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Naibu Waziri wangu Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamisi kwa kazi nzuri anayofanya na kunipa ushirikiano, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu wangu na watendaji wote, kuanzia ngazi ya makao makuu hadi kwenye mikoa, halmashauri na kata zote. Sifa hizi tunazopata si kwa sababu yangu ni kwa sababu wao wanagusa maisha ya wananchi. Niwashukuru wadau wote niliowataja mpaka dakika hii ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maneno haya ya utangulizi niseme kwamba hoja hii ukiacha hoja za Kamati zilizowasilishwa hapa, nakiri kuzipokea hoja hizi na niliahidi Kamati yangu Tukufu kwamba tutazifanyia kazi na kuwasilisha kwa maandishi masuala yote yaliyozungumzwa mle, kuanzia ukarabati wa miundombinu, upatikanaji wa fedha kwa wakati tufuatilie pamoja na kuwezesha upatikanaji wa watumishi ambao ni wachache hasa kundi hili la Maafisa Ustawi wa Jamii. Tutafanya kazi na Wizara za Kisekta kuweza kuona tunafanyaje ili kuendelea kuwezesha upatikanaji wa huduma za maendeleo na ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Spika, sitaweza kupita kwenye kila hoja ya mchangiaji mmoja mmoja, kwa heshima na taadhima naomba nikuombe niweze kuyaangalia yale masuala machache ambayo yamechangiwa sana na kuweza kuyatolea ufafanuzi kadri muda utakavyo ruhusu. Nikiri hoja zote tumezichukulia kwa uzito stahiki, tutazifanyia kazi na kuziwasilisha kwa utaratibu wa Bunge kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamis, nami naomba nianze kuongeza kwenye eneo hili la mmomonyoko wa maadili. Mmomonyo wa maadili limekuwa ni janga kubwa kwa sababu kwanza linagusa watoto ambao ni Taifa la kesho na watoto hawa wanajifunza kutoka kwetu sisi watu wazima, ambao tumepewa baraka na Mungu tuwalete watoto duniani na tumepewa dhama ya kuwalea na kuwakuza.

Mheshimiwa Spika, tunayo mikakati mingi eneo hili, lakini niseme kwamba tumejiongeza tumekwenda mbele. Ukiacha masuala haya ya kusema kwamba tuwawezeshe kina mama kiuchumi kwa kuunda majukwaa haya ya uwezeshaji wanawake kiuchumi, ambapo Jukwaa Kuu la Taifa tumelizundua jana, tumehakikisha kwamba tutakuwa na kampeni mbalimbali tukishirikiana na haya majukwaa ya kupeleka sauti ya fursa zilizopo kiuchumi maana tuna benki nyingi, tuna wadau wengi na sisi wenyewe Serikali tuna mifuko mingi ya kuwezesha wanawake kiuchumi ili wasiweze kuingia kwenye ukatili lakini taarifa zinakuwa hazifiki kwa wananchi hasa wale wa vijijini.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikizunguka kule, unamuuliza mwananchi unafahamu kama kuna mkopo wa asilimia 10 anakwambia nasikia tu labda hii mikopo ni ya huko kwa wafanyakazi pamoja na watu wa halmashauri. Kwa hiyo tunaona kuna gap kule chini kwenye vijiji na kwenye kata. Kwa hiyo kupitia jukwaa hili na kupitia kampeni zetu hizi tumesema ZIFIUKUKI zijuwe fursa, Imarisha Uchumi, Kata Ukatili Kazi Iendelee. Tutahakikisha tunafikisha sauti ya uwepo wa fursa za uwezeshaji kiuchumi mpaka kwenye kata na mpaka kwenye kijiji. Kila mwanamke mmoja mmoja atajua na atajiunga na jukwaa hili ambalo ndio litakuwa platform ya kuwafundisha, kuwajengea uwezo, wataweza kujifunza kutoka kwa wenzao ili tuwakomboe kama mkakati mmoja wa kutokunyanyaswa.

Mheshimiwa Spika, tuna madawati pia ya jinsia ambayo yapo kwenye Jeshi la Polisi karibu madawati 420, yaani Vituo vyote vya Polisi vina haya madawati na pale tu sio madawati tuna msaada wa kisheria tunaoutoa kupitia Sheria Namba moja, Msaada wa Kisheria ya Mwaka 2017. Wasaidizi wa kisheria wako wengi sana lakini bado wananchi pia hawafahamu. Kwa hiyo, kupitia haya majukwaa pia tutapeleka hii elimu na tutafanya haya matamasha tukiwa tunahusisha na hizo huduma kuzipeleka, sio matamasha tu ya hivi ya kukaa kwenye majumba ni kupeleka zile huduma. Kama ni usaidizi wa kisheria huu hapa, kama ni fursa za kiuchumi hizi hapa.

Mheshimiwa Spika, tumezindua hilo tamasha la kwanza Dar es Salaam, mwishoni mwa Aprili ambapo tulileta taasisi zote zenye fursa za kiuchumi ambapo walihudumiwa wananchi takribani 4,040. Kwa hiyo tunataka tuendelee hivyo kwenye mikoa yote tuifungue nchi, kila mtu ajue uwepo wa hizi fursa isije ikawa wachache tu ndio wanazisikia.

Mheshimiwa Spika, tunakuja na mpango wa pili wa MTAKUWA uliofanyiwa maboresho. MTAKUWA ni Mpango kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili kwa Wanawake na Watoto baada ya ule wa kwanza kuwa umeisha Juni 2022. Mle ndani tumeboresha, masuala ya ukatili wahusike na Wakuu wa Wilaya wahusike na Wakuu wa Mikoa, wanapojadili taarifa zao za Kamati ya Ulinzi na Usalama kwenye halmashauri na mikoa, wakajadili majambazi, wakajadili na hali ya usalama, wajadili na masuala yanayotishia unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto na wanawake.

Mheshimiwa Spika, tunataka kuzijua hizi data zikitokea mikononi kwao, kwa sababu wanafanya hiyo kazi na wana vyombo vyote. Kwa hiyo taarifa zikifika pale na Afisa Ustawi wetu akawasilisha pale, Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa ataweza kuviagiza vyombo vichukue hatua kwa wakati badala ya mama huyu kuwa anahangaika pengine yuko mbali kule kijijini, pengine hana hata usafiri, pengine hata Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa hawajui.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaikaribisha hii mifumo yote ya ulinzi na usalama ili pia iangalie hili suala la watoto pamoja na wanawake wanaonyanyaswa. Tumekuja na kampeni nyingine ya “Taifa letu, Maadili Yetu”, tumeizindua hapa juzi. Nimemsikia Mheshimiwa Mbunge Mwakagenda akisema tupige sana kelele, sasa tutapiga sana kelele kupitia hii kampeni kwa kipindi cha miezi sita inayokuja na ndio maana tumewaunganisha na vilabu vya mipira, tumewaunganisha na wanahabari, tumeunganisha na jamii yenyewe kupitia wenzetu wa SUMAUJATA, FAGDI na tunapata wito na mwitikio mkubwa sana wa wananchi na kila mtu anasema nataka kwenda mstari wa mbele, hasa kupitia hii kampeni. Tutapiga sana kelele ili kufikisha hii sauti kule, sio tu sauti ya kwamba kuna ukatili bali na fursa za kiuchumi kwamba ziko hivi na fursa za kisheria, misaada ya kisheria ili wananchi wajue. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru utoaji taarifa sasa unaongezeka si kwa sababu pengine matukio yanaongezeka sana. Awali kasi ya kutoa taarifa ilikuwa asilimia 12, sasa tunainyanyua kwa sababu wanapata ujasiri na kuona kwamba Dkt. Samia Suluhu Hassan yupo kwa ajili yao, Wizara ipo kwa ajili yao, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya wako kwa ajili yao. Tunaamini hawa watu sasa kama ilivyo kwenye nyumba ya mtu mmoja ameweka askari wa asili ambao tunasema wanalinda ile nyumba, wakibweka, mwizi anakimbia. Lazima hawa wakatili wajue kwamba Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan iko kiganjani kwa huyu wanayetaka kumkatili na ndio maana tunatengeneza namba za mawasiliano 116 na Wizara inazindua dawati lake hivi karibuni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee eneo lingine kuhusu masuala ya NGO hizi ambazo zimekuwa zikihusishwa na masuala haya ya kuchochea mmomonyoko wa maadili. Tulipata hivi karibuni taarifa za wanaharakati ambao pia walikuwa wakishirikiana na Mwakyembe ambaye alikuwa ni Waziri mstaafu kusema kwamba kuna hii hali huko kwenye jamii, baadhi ya mashirika yanahusishwa na kuchochea hivi vitendo.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imechukua hatua ya kuyaita yale mashirika yote yaliyokuwa yametuhumiwa kule, kupitia Sheria ya Msajili wa haya mashirika wakaambiwa watoe maelezo. Baadhi yao wameshawasilisha maelezo na wengine wanayawasilisha. Sasa kwa sababu suala hili ni la kisheria, tukasubiri hayo maelezo yakamilike ili yaweze kuchanganuliwa na Bodi yetu ya Usajili ili wasilishwe kwa mujibu wa sheria. Kama kutakuwa na mtu ambae anaona ameonewa sheria inasema rufaa iende kwa Waziri. Mimi nitapokea, lakini sasa hivi mchakato unaendelea wa uwasilishaji hayo maelezo kujibu zile tuhuma ambazo wamehusishwa nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nisemee kuhusu suala la hela hizi za Machinga ambazo bilioni 22.9 zilipaswa tupewe, lakini hatukuweza kupewa kwa wakati. Kupitia Wizara ya Fedha ambayo tumekuwa tukiwasiliana nayo ilikuwa inafanya uratibu wa Mifuko sio tu huu wa Machinga ili waweze kuweka mifumo vizuri ikiwepo Mfuko wa Maendeleo wa Vijana wa Wanawake, Mfuko wa Taifa wa Watu Wenye Ulemavu na Mfuko huu wa Wamachinga. Sasa taarifa iliyoko ni kwamba hatua zimekamilika na hiyo taarifa itapelekwa kwenye kikao cha kazi cha IMTC kujadiliwa. Baada ya hapo, utolewaji wa hizo fedha utaanza, lakini kupitia kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakapo kuwa analeta hotuba yake atakuwa ameweza kutolea mwongozo sambamba na tathmini hii iliyokuwa inafanywa na ofisi yake.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kwenye suala lingine linalohusu malezi na makuzi, kwa nini tumeweza kufanya mikoa 10 tu, lakini pamoja na WDF huu mkopo tunaoutoa pale Wizarani tumekwenda mikoa minne tu. Hili suala la mikopo hii ya WDF tulipokuwa tumepewa kibali tuendelee kutoa hizi fedha, kulikuwa na maombi tayari yapo pale ofisini ya siku nyingi. Kwa hiyo, ilikuwa mtu aliyeanza kuleta ndio apewe. Tulipoweza kuwachambua wale wapewe ile mikopo ndio ikaangukia hiyo mikoa lakini kwa sababu marejesho yanakwenda vizuri, tumejipanga kuhakikisha kwamba taarifa zinakwenda mikoa yote na halmashauri zote. Hata kama ni milioni ishirini ishirini tunatenga waombaji wajue kuna hilo fungu. Watakaokidhi hivyo vigezo waweze kupatiwa ili hata kama tunampa mmoja mmoja lakini kila mtu aonje uzuri wa hiyo WDF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Serikali ni kwamba, mikopo hii sasa yote tuipeleke benki, kwa sababu wengi wamekuwa katika mikopo kwa mfano ya asilimia 10 hawarejeshi na huu tukaona nao tuupeleke benki. Kwa hiyo utakapokuwa umeshafika pale benki, maana kwa sasa hivi tumesitisha kutoa, watapewa taarifa wote watachukua huko. Sisi tuta-regulate kuhakikisha majukwaa ya uwezeshaji wanawake kichumi yanaleta watu waliokidhi kupata hii mikopo kwenye benki za karibu na maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu masuala ya majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi kwa nini yamepewa mafunzo kwenye mikoa kumi tu. Ndio ilikuwa hivyo kwa sababu mikoa ile ilikuwa imeweza kutekeleza maelekezo mapema ya kwamba yaundwe hayo majukwaa. Kwa hiyo yale yaliyokuwa yameundwa tuliweza kuyapa mafunzo na sasa kwa sababu Jukwaa la Kitaifa limeundwa jana yote hii inakwenda kuingia kwenye kupata mafunzo. Semina kubwa inaandaliwa, wataitwa waweze kupewa ili waweze kuweka mipango ya mikoa yao, kwamba wanataka kuwafikisha wale wanawake katika ngazi ipi ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wajane; wajane ni kundi maalum na nashukuru tunao hapa viongozi wa wajane, tumekuwa tukiwasiliana nao. Tatizo la wajane kweli limekuwa kubwa na mwishoni mwa mwezi huu wa Juni tutakuwa na siku ya wajane, Kitaifa tutaifanyia Mkoa wa Mbeya. Tutakusanyika nao pale na baada ya hapo wale viongozi na wenyewe watapewa mafunzo, kisha wataweka mpango ingawa wao ni sehemu ya wanawake, lakini tutayaangalia mahitaji yao kwa utofauti, kwa jicho la hali ile ya maisha yao yalivyo. Hasa masuala ya kisheria, wananyanyaswa sana, wananyang’anywa mali zao baada ya mwanamume kufariki wanapitia kwenye mateso makali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilishaagiza tupewe list yao wote ambao kesi hazisogei ili tuwaunganishe na watoa huduma za msaada wa kisheria. Kwa hiyo ole wao wale waliobeba mali za wajane, wajue kwamba moto unakuja, tumejipanga, baada ya Siku ya Wajane Mbeya, mkikutwa huko mjue kwamba sheria inakuhusu. Lazima tuwaheshimu kwa sababu ujane ni hali ya kutokujichagulia, bali kudra za Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utitiri wa mikopo umelalamikiwa sana. Nashukuru sasa kwamba jukwaa hili la uwezeshwaji wanawake kiuchumi limeanza. Wanawake wote wanaolia machozi sasa ya mikopo hii isioeleweka wanakwenda kupona. Wanakwenda kuziona fursa zingine tofauti kabisa za mikopo nafuu kupitia haya majukwaa. Sasa na hawa wanaoitwa mikopo ya makomandoo, sijui mikopo ya pasua kichwa, damu na nini, niwaombe huko mliko majukwaa yameanza mtaniona mpaka kwenye ofisi zenu, mniambie mlisajiliwa na nani, mlipewa kibali na nani katika kuwapatia wanawake hawa mikopo ambayo pengine hata haikidhi hadhi ya utoaji mikopo. Waende wakajisajili kwenye utaratibu sahihi, wapewe miongozo ya utowaji mikopo. Kwa hiyo ukombozi wa wanawake umefika kupitia haya majukwaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie eneo moja kuhusu vitambulisho vya Wamachinga. Vitambulisho vya Wamachinga sasa vinavyokuja ni vya kidijitali, vinaweza kuwezesha Mmachinga huyu kutoa fedha na kupokea fedha, lakini vimeunganisha na NIDA pamoja na e-GA pamoja na maeneo yote ambayo Machinga atakuwa anapita kwenye mzunguko wake wa kupata fedha. Akikionyesha kile kitambulisho wanamsoma, mifumo inasomana. Kwa hiyo ni kipindi cha mpito hiki Mwaka huu wa Fedha 2022/2023, kama nilivyosema tayari umekamilika, unafanyiwa majaribio, tutaanza na baadhi ya mikoa, kisha tutaenda nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo suala hili litakuwa limeweza kuwanyanyua Wamachinga kuaminika na kupewa mikopo na taasisi zingine zote, kwa kuwa vitambulisho vyao vitakuwa vimekidhi vigezo vyote vinavyohitajika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu pension ya wazee; niseme kwamba tumepokea wazee ni tunu ya Taifa, wazee tunawapenda na sisi wote tutazeeka. Tunafanya mapitio ya sera ya mwaka 2003 na mwaka jana tulifanikiwa kuunda Baraza la Taifa la Wazee ambapo tuliongea mambo mengi kuhusu mwelekeo wa kuboresha masuala ya wazee. Sera hii tumeshaiwasilisha, hatua nzuri itafanyiwa mapitio. Kwa hiyo humo ndani yake ndio tutakuja mpaka na Sheria ya Wazee, lakini tutakuja mpaka na masuala haya ya pension ya hawa wazee. Kwa hiyo utaratibu unaendelea na tutaendelea kuwasiliana nao kupitia Baraza la Wazee tunalofanya nalo kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa haya machache kwa kibali chako niombe kuwasilisha mengine yote kupitia maandishi, tukizingatia hoja za Wabunge wote ambao wamezitoa hapa siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo niliyoyaeleza, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuhitimisha hoja niliyoiwasilisha mbele ya Bunge lako tukufu siku ya leo tarehe 30 Mei, 2022.

Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla ambao wametoa pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao wamekubali kabisa na kuona Wizara hii ilikuwa imechelewa ilitakiwa ianze siku nyingi sana ili haya yote ambayo yanatukuta hapa leo yangeweza yakawa yamerudishwa nyuma kwa kasi kubwa kwa sababu tungekuwa na mikakati hii tuliyonayo leo mfano ya malezi na makuzi ya watoto tusingekuwa na kizazi ambacho kina ukatili mwingi namna hii hivi leo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo kila jambo linakuja kwa wakati wake, tunashukuru kwa maono yake na tumepokea pongezi hizi, tutazifikisha ili aone kwamba Bunge lako tukufu limeelewa tafsiri ya uamuzi wake mkubwa kwa maslahi ya Taifa letu kwa miaka 50 na miaka 100 mbele.

Mheshimiwa Spika, naishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa ushauri na kuisimamia Wizara yangu kwa umakini mkubwa, ushauri na maelekezo yao yamesaidia katika kuboresha utendaji wa Wizara hii hadi hapa ilipo. Wizara yangu inathamini sana michango yote iliyotolewa naomba nilithibitishie Bunge lako tukufu kuwa tutaifanyia kazi na majibu yote ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge hapa tutaziwasilisha kwenye ofisi yako ili waweze kuzisoma na kuelewa tumezitendeaje haki na kwa sababu hii ni process inaendelea ya Bunge tunaamini kadri tunavyokwenda mbele watakuja kuona kwamba tumezitendea haki.

Mheshimiwa Spika, nachukua tena fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliopata nafasi ya kuchangia hoja yangu niliyoiwasilisha leo Bungeni, michango yao ni mizuri sana ina lengo la kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wizara lakini kuboresha tija na ufanisi wa maisha ya watanzania kwa mingi ya vizazi vijavyo. Jumla ya Waheshimiwa Wabunge nimehesabu hapa 39 wamechangia hoja yangu ambapo kati yao 25 wamechangia kwa kuzungumza na hapo hapo Wabunge 14 wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana pia Mheshimiwa Jafo naye namuongeza anakuwa wa 26 aliyechangia hapa akizungumzia athari nzima ya masuala ya mazingira tunayoishi katika nyanja za makelele na mitetemo jinsi gani inaweza kuathiri afya za Watanzania pamoja na watoto pamoja na wazee na wagonjwa hatimaye tukawa na akili ambazo siyo njema sana tukaanza kusababisha matukio makubwa makubwa na tukakosa tumeyatoa wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika michango iliyotolewa ipo inayotoa ushauri na mengine ni maswali na Waheshimiwa Wabunge waliochangia nimewaorodhesha naomba kwa kibali chako nitakapowasilisha taarifa yangu kwa maandishi niunganishe orodha yao.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nitoe maelezo na ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizoibuliwa na Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja yangu na nikiri kwamba leo Bunge limeweza kuona ukubwa na unyeti wa hii Wizara kiasi kwamba huenda hii siku moja ikawa haitoshi ya kujadili hoja zote hizi maana hapa mambo ni mengi. Lakini nimebaini baadhi ya Wabunge bado hawajaelewa profile ya hii Wizara napenda kusema kwamba ni Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum. Kwenye makundi maalum hapa tunao watoto, tunao wazee, tunao wajane na wamachinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa vijana na walemavu wako kwenye Wizara nyingine iliyo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ingawa sisi kama Serikali mambo yanaingia huku na kule, kijana anaweza akaibuka akawa ni mmachinga, lakini bado kijana anaweza akawa bado kijana akawa tena mjane hivyo. Kwa hiyo, tunafanyakazi kwa pamoja nilikuwa nataka niweke tu sawa hili jambo hapa ili ninapojibu twende pamoja.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba hoja zimetolewa za kutosha nikiangalia katika pillar ya governance nimeona hapa Wabunge wameongelea jinsi gani uendeshaji wa Idara za Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii zilivyo kule kwenye halmashauri. Kwa sababu bila wao kuwa na nguvu kule tunaweza tukasema sisi huku tunaongea sana tunatengeneza miongozo na Sera nyingi lakini kule chini utekelezaji tone yake ikabadilika kutokana na kwamba zile powers hawana ambazo zingekuwa zinaakisi ukubwa wa tatizo ambalo mmelijadili leo hapa.

Mheshimiwa Spika, mmeongelea masuala ya watumishi; upungufu wa watumishi kwa upande wa Ustawi wa Jamii pamoja na Maendeleo ya Jamii kitu ambacho hawa sasa ndiyo engine au hawa sasa ndiyo chachu ya kutengeneza jamii kule ikae sawa hata Wizara ya Elimu ikija, Wizara ya Afya ikija ya Kilimo ikija ya Nishati ikute jamii imeandaliwa kifikra kuweza kupokea haya mambo. Nashukuru kwamba mmelijua hili jambo na nina imani kwamba full council zetu zingekuwa zinajadili kwenye tone hii tungeweza kusukuma zaidi maamuzi na vipaumbele vya halmashauri kiasi kwamba tukapunguza changamoto hizi nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmeona jinsi multi-sectorial approach ilivyo kwenye Wizara yangu kwamba sisi ni coordinator ni kama airport ya Amsterdam tunakaa pale tunapokea kila ndege inatua inaondoka, inaondokaje inategemea na Wizara yangu imewezeshwa vipi kuweza kuzipokea hizi ndege zinazo-take off pamoja na kuondoka, kwa hiyo, tunaamini kwamba imekuwa ni shule pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye masuala ya uwezeshaji wa vitendea kazi kwa hawa maafisa wachache waliopo mmeweza kuona vizuri jinsi ambavyo tunahitaji kufanyakazi kubwa kuwawezesha hilo tumelipokea. Lakini pia mkiangalia sasa hivi kwenye upande wa miundombinu yao ya ufanyaji kazi bado ni changamoto mmechangia vizuri sana mmeweza kwenda kwenye upande wa huduma jinsi gani watatoa huduma kwenye maeneo mbalimbali bado ni changamoto inayotokana pia na wao kutowezeshwa.

Mheshimiwa Spika, mmechambua vizuri kuhusu jamii jinsi ambavyo ina nafasi pia kwenye masuala haya yote, kwa sababu jamii kama jamii ina mambo mengi yanaendelea ndani yake inategemea na utayari wao kuweza kuyatoa na kuyaibua kwenye vikao vyao halali kuanzia kata, kijiji tarafa mpaka Wilaya mpaka mkoa ndivyo hivyo ambavyo tunaweza kama Serikali kuyafanyia kazi kwa urahisi yote hii inaonyesha kwamba tunahitaji dawa ya jamii ambayo ni Afisa Ustawi wa Jamii tunahitaji Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa ridhaa yako naomba nijikite kwenye ukatili. Ukatili imekuwa ni sauti leo imevuma sana humu ndani na imegusa wengi sana, nafurahi kuona kwamba sauti hii imevuma sana kwangu mimi kama Waziri mwenye dhamana na kwa niaba ya Serikali haya ni mafanikio makubwa kwa sababu sasa ule mpango wetu wa MTAKUWWA unaoratibiwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa kutokomeza ukatili kwa wanawake na watoto ndiyo unafanyakazi na umefanikiwa sana. Nasema hivyo kwa sababu zamani matukio haya yalikuwa hayaripotiwi kabisa kila mtu alikuwa anaona aibu anayaficha hayakuwepo. Lakini baada ya MTAKUWWA kuanza mwaka 2017 na 2018 na inaisha Juni, 2022 Kamati zimeundwa mpaka ngazi ya kijiji na kule kwenye mitaa zimeanza sasa kuchukua role yake ya kuelimisha jamii, jamii imepata confidence ya kuanza kuripoti hivi vitu.

Mheshimiwa Spika, topic hii ni kubwa peke yake Mungu anisaidie niimalize ili niende na nyingine, lakini nafikiri ingetosha siku mbili.

Waheshimiwa Wabunge, walio wengi wamezungumzia ukatili dhidi ya wanawake na watoto na kwamba vitendo vya ukatili vinaendelea kushamiri katika jamii na wanaofanya ni ndugu wa karibu. Utafiti wa UNICEF pamoja na Serikali mwaka 2021 Januari - Desemba umeonyesha kwamba 60% ya ukatili huu tunaoongea hapa unafanywa majumbani kwetu wakiwepo wazazi wetu, ndugu, wajomba na watu tunaowaamini huko huko tena usiku mwingi, unaamka mtoto kakatiliwa au mtoto wazazi wameondoka wameenda kwenye shughuli nyingine kakatiliwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna mmomonyoko wa maadili mkubwa sana na kukosa imani ya Kimungu na hofu ya Mungu katika jamii zetu huku ndani. Jambo ambalo ni kichaka cha mtihani mkubwa na hakihitaji sana fedha nyingi kupambana na hiki kitu, kinahitaji mioyo ya uzalendo na watu walioguswa wanaosema hili hapana kila mtu kwa nafasi yake apaze sauti ili masikio ya Watanzania yakisikia na macho ya Watanzania yakiona, asilimia 50 ya tatizo linaondoka kwa sababu wakatili sasa watajiona hawako salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha Waheshimiwa Wabunge wametoa ushauri mbalimbali katika kutatua changamoto hii ya ukatili. Serikali katika kushughulikia changamoto hii naomba niisemee kwamba imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na vitendo hivi ikiwemo kuanzisha Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto kuanzia ngazi ya Taifa, mkoa, halmashauri, kata, kijiji na mtaa. Kamati hizi uzuri wake ukiziangalia zina kila mtu mle ndani kama ni kwenye kijiji kuna kiongozi wa Serikali ya kijiji pale kuna walimu, kuna watu wa afya, kuna ASASI za kiraia pale pale kuna viongozi wa dini, pale pale kuna wanawake, pale pale kuna vijana, pale pale kuna watu maarufu, pale pale kuna polisi jamii na nilishukuru Jeshi la Polisi sana kwa kuzingatia hii ajenda limepeleka vijana wa polisi tena graduates zaidi ya 4500 katika kata zetu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hii inaonesha jinsi gani Serikali inafanya kila jitihada kuweza kuhakikisha kule jamii inaamka kwenye zile kamati kuna Maafisa Maendeleo ya Jamii pamoja na Maafisa Ustawi wa Jamii. Lakini sasa changamoto tuliyonayo katika kupambana na hiki kitu kamati nyingi zimeundwa zinakuwa haziko hai, hata zile zilizojengewa uwezo. Ukienda kwenye full council zetu nyingi unakuta hii taarifa haiko itokanayo na utendaji wa hii kamati.

Kwa hiyo, tunapokwenda kujenga uwezo tunadhani kwamba sasa tutaagiza full council zote na vikao vyote vya halmashauri viagize kuwe na chapter ya taarifa hizi za ukatili ili watu waweze kuwajibika na kuona kwamba ni muhimu hii ajenda iende mbele kama kipaumbele chao.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali haijaishia hapo imeimarisha Madawati ya Jinsia Jeshi la Polisi na hapa mmechangia kwamba tuone namna gani jinsi ya kuyaondoa pale, kwa sababu suala hili ni la Kiserikali tutaenda kujadili chini ya uratibu wa Wizara yangu, lakini kwa ridhaa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu tuone tunafanyaje. Aidha, kuwaelimisha watu wasiogope au kama inabidi hivyo ndivyo hii tathmini inayofanyika ituambie kwamba tuyapeleke eneo gani ili mwitikio uwe mkubwa zaidi.

Lakini pia ukiacha hizi Madawati ya Jinsia Jeshi la Polisi tumeanzisha vituo vya mkono kwa mkono (one stop centre) katika hospitali zetu mbalimbali na zoezi linaendelea na hivi vinakuwa vinatoa huduma jumuishi za kitabibu msaada wa kisheria na ustawi wa jamii kwa manusura wa ukatili na niseme hapa kuna tabia ya jamii kuficha ushahidi; wanakatiliwa, wanaanza kwa kusema huyu ni babu, huyu ni mjomba utapata laana wewe mtoto nyamaza.

Mheshimiwa Spika, kipindi tunapokuja kusikia kinyemela tunakwenda kuwapeleka kwenye haya madawati ushahidi umefutika. Nilitembelea Dawati la Chanika Dar es Salaam, akasema yule Afande yuko pale anaitwa Christina kwamba sisi tumepokea kesi nyingi sana na 99.9% zilizofika kwa wakati zilikwenda mahakamani zikashinda kesi.

Sasa shida inakuwepo imechangiwa hoja hapa kwamba mahakama saa nyingine zinachelewesha kesi nikaenda mpaka kule nikaenda mpaka Polisi nikaambiwa kwamba sasa unapeleka kesi haina ushahidi watu wameamua kupatana zirudi nyumbani wakamalize kindugu. Lakini wengine wamehongana hapo katikati, wengine wamekimbia wametoweka, lakini wale wanaofanikiwa kufika kwenye vituo hivi ushahidi ukachukuliwa asilimia 99.9 kesi zao zimekwenda haraka sana na wameweza kushinda na watu kila siku tunasikia wamefungwa miaka 30, wamefungwa miaka mingapi, hizi ni hatua ambazo Serikali inafanya. Hivyo jamii tunaomba ichukue wajibu wake kutoa msaada kwenye hii mifumo ambayo imeshaanzishwa ili tuweze kwenda sawa katika kufikia ufanisi.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiacha hilo, tunazo nyumba salama, tunao watoto wengi waliofanikiwa kwenda nyumba salama waliweza kuepuka ukatili. Tatizo nyumba salama tunakubali bado ni changamoto na ni zoezi ambalo tumepanga kuendelea kuziongezea sambamba na utoaji elimu katika jamii zetu.

Mheshimiwa Spika, naomba tuseme kwamba kwenye vyuo vikuu nako ni mtandao wa ukatili upo lakini Serikali imefanikiwa kuanzisha madawati ya jinsia kwenye hivi vyuo vikuu pamoja na vyuo vya elimu ya kati. Hatujaishia hapo kwenye shule za msingi pamoja na shule za sekondari kule tunakwenda kuzindua kwenye siku ya Mtoto wa Afrika tarehe 16 Juni, Mabaraza ya Watoto yanakwenda kuzinduliwa pale, lakini Madawati ya Jinsia yanakwenda kuzinduliwa pale, klabu za watoto zitazinduliwa pale. Kwa hiyo, watoto wakikatiliwa nyumbani baba na mama hamna muda wa kusikiliza watakwenda kuyasema shuleni, lakini pale shuleni tunaweka utaratibu Maafisa wa Ustawi wa Jamii hata kama ni wachache tutaomba na wa kujitolea waliostaafu wawe wanakwenda pale kuwaimarisha hawa tupate mpaka ma-matron wanaoweza kuongea na hawa watoto ili waweze kufunguka na kusema mambo ambayo mengine hawawezi kuyasema kule majumbani kwao.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kufanya kampeni ya twende pamoja ya ukatili sasa basi, lakini tumeiboresha hii kampeni tumetangaza na tutatangaza tena kesho fomu maalum ya wazalendo wote wapambanaji popote walipo wakienda kwenye google ukaandika SIMAUJATA. SIMAUJATA ni Shujaa wa Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii Tanzania, tumepata vijana wengi, muitiko ni mkubwa baada ya kutoa hizi elimu za mara kwa mara wanasema tunataka kwenda mstari wa mbele, sisi tumeshachoka kukatiliwa na kuona watu wanakatiliwa, wanajisajili.

Mheshimiwa Spika, itakuwa sasa kila mtaa tunaangalia tumemsajili nani wenzetu wa utalii wametengeneza Jeshi lao la USU na sisi tunatengeneza Jeshi la SIMAUJATA, waende mstari wa mbele, mlango kwa mlango, mkiona wanapita kwa baiskeli wameweka redio kama ndugu zangu wa Kolomije mfungue milango, watakuwa wanasema kile tulichowalisha maneno ili wananchi wasikie waweze kuona hatuwezi ku-afford kuwa na mabilioni ya pesa ya kununua magari kwenda kule, kuna vita vingine ni vya kizalendo tu na moyo katika kulitetea Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hata ninyi Wabunge mlioko hapa wanawake kwa wanaume mnaombwa mjiunge kwenye hiyo kampeni, lakini niseme vita hii inasemwa sana kwenye centre ya uadui tunaona jinsia ya kiume inainuliwa pale. Wale wanaume siyo wote ni wanaume wachache lakini wanaume wengi walio wazuri ni kama vile wamekubali haya mambo yaendelee, hatuoni forum zao tunaona ma-kitchen party ya akinamama, tunaona majukwaa ya akinamama ya VICOBA, tunaona akinamama wanahangaika, tunataka kuona wanaume wanainuka wale waliobarikiwa wenye hekima wanasema kwa wanaume wenzao hapana hii haikubaliki wawakemee tunakimbiza mtu kaiba kuku anakwenda kusitiri njaa tunamshughulikia kweli kweli, lakini tunaacha mbakaji tunamstriri na wababa wapo, matumbo yabebe Watoto, yazae Watoto, wabakwe akinamama, wabakwe watoto wa kiume, wabakwe wa kike hii haikubaliki. Akina baba mko wapi? Wakina baba wazuri mko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dunia sasa inachukua direction ya mkakati wa He for She; He for She maana yake ni kumnyanyua mwanamme atakayekuwa mfano wa nembo ya Taifa ambapo wanaume wengine wakimuangalia wanamuona kwamba sisi mbona kama vile siyo wanaume, tumchoreje mwanamme wetu wa jamii ya Kitanzania ambaye yuko mbali na ukatili, ni baba wa familia, ni mbeba maono ya familia na wengine wote wakimuangalia wanaona aibu, watakimbia wataogopa. Leo wakatli na wabakaji wanabeba nembo ya kiume wanaifanya ndiyo nembo ya sura ya mwanaume wa Tanzania, wanaume naomba muwakatae, amkeni mtualike kwenye vikao vyenu tuje tufungue vikao vya akinababa vinavyosema mwanamme kibaka wewe siyo mwanamme, wanaume wamekuwa na moyo mdogo akiudhiwa na mwanamke anamimina risasi saba kwenye kichwa cha mwanamke, ameuawa kule Shinyanga, ina maana wanaume kama ni viongozi wa familia mioyo imekuwa midogo kiasi hicho hasira kidogo umeua hasira kidogo umekomoa hii siyo sawa bebeni uanaume mseme hapana kwa wenzenu wanaowaharibia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tukisema wanawake wanaweza maswali yanakuwa mengi, sasa imeanza profile kubadilika, wanaume mnakwenda down na mnapelekwa na wenzenu wachache simameni kwenye nafasi zenu Mungu alizowapa, musimamie uanaume wa heri na baraka na furaha na amani kwenye maisha ya watoto hawa wa kike na wa kiume, kwa sababu silaha za kubakia sasa mmepewa nyinyi sisi tutafanyaje wanaume kataeni tuko pamoja na ninyi tupambane na wale wachache. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inaumiza sana na hapa ndiyo sehemu ya kusema ili tubebe spirit ya kitaifa, hili halina hata chama kipi, halina cha imani ipi, halina cha itikadi gani, ni jambo la kitaifa lazima tuende pamoja. (Makofi)

Vilevile Wizara inafanya tathmini ya utekelezaji wa MTAKUWWA kwa kipindi kilichopita kama tulivyosema, tutasubiri hiyo tathmini, lakini aluta continue vita lazima ianze mlango kwa mlango tupeane ushirikiano wakati tunaisubiri tathmini hiyo mbele ya safari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao mashujaa wengine wamejiandikisha na walikuja hapa Bungeni leo watu wanajitokeza kwa wingi, tunao vijana wa Pink Tie ambao wanaongozwa na Pink Tie Foundation hawa ni akina Lilian Mwasha huyu ni mtumishi wa Mungu, akina Salma Dakota, akina Furaha Dominick tunao vijana akina Jacob kutoka Mara wamesajili Safe Network kwa uchungu kutokana na mambo haya haya na wanabeba ajenda kweli siyo suala la mwanamke tu ni suala la mtoto wa kiume pia. (Makofi)

Tunao Wanawake Live akina Joyce Kiria, tunao wengi na wengine siwezi kuwataja hapa, hii inaonesha kwamba sindano imeingia dawa, imeingia sasa ari ya vijana ya kuona kwamba Taifa linatokomea inachemka, utafanyakazi ya kurudisha nyuma na wakatili hawataweka makao makuu ya shetani mwa ukatili Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze sasa tunafanyaje maana yake nyuma ya ukatili pia tuna ajenda ya uchumi huku chini, tuna agenda ya mila ya desturi ambazo ni area pia zimewekwa kwenye MTAKUWWA, lakini tuna masuala ya kisheria niseme kwamba suala hili la hizi programu mbili za kulea watoto wetu malezi na makuzi ya awali ya mtoto tumeisema hapa tumeanza na vituo 20 Dodoma na kumi Dar es Salaam na 15 vimeanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, huu ni mwanzo tu vilikuwa vya majaribio, lengo ni kwenda nchi nzima, hapa nitoe wito kwa akinamama na akinababa ambao wanapenda kuhakikisha watoto wetu sasa wanaanza kukuwa vizuri tujitokeze, tunachangia harusi, tunachangia vitu vingi vituo hivi ni shilingi 10,000,000 hadi 13,000,000 tufanya force account, tuona tunafanyaje viende kwa kasi sana tunao wadau wanatusaidia, lakini na sisi Serikali tunaweka fedha pale, lakini na jamii ya wapenda maendeleo katika spirit ile ile ya kuchangia mambo yaende kwa kasi tujipange ndugu zangu hakuna kuchelewesha mtoto ukimchelewa leo kesho amepotea, vituo hivi vinatakiwa vijengwe nchi nzima na kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa tu wito huu kwa ajili ya kuongezea kasi lakini Serikali mpango wake vishuke ilipo zahanati kama ni kwenye kata kuna hicho kituo ilipo zahanati kwenye kijiji kuna hicho kituo, ilipo shule kuna hicho kituo, walimu watapatikana ndugu zangu kuwalea wale watoto sio kazi kubwa sana hauhitaji ma-degree mengi, hawa hawa tulionao tutaanza nao wakati taaluma hiyo ya saikolojia na vitu vingine vikiendelea kukuwa sambamba na wanaustawi wa jamii wetu wanatengeneza sheria yao kwa hiyo tutakuwa mpaka na kliniki za wana ustawi wa jamii kama tulivyokuwa na kliniki za zahanati au vituo vya afya au za kiuuguzi ili waweze na wenyewe kusajiliwa kama ni private au kama government waweze kuwafikia wananchi popote kule walipo wakati huko tukiendelea kuajiri wa Serikali ili kufikia ile asilimia tunayoihitaji.

Mheshimiwa Spika, usawa wa kijinsia niongelee...

(Hapa kegele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, dakika tatu, malizia; kengele ya pili imeshagonga.

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimia Spika, usawa wa kijinsia tumesemea sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan yeye ni kinara katika haki na usawa wa kiuchumi ambapo jukwaa hilo alilizindua mwaka jana tumesema, andiko linakamilika maana yake ni kwamba ukiacha mikopo ya asilimia 10 mmeisemea sana tunakwenda kuboresha tutaongea na Serikali maana yake ni agenda mtambuka.

Mheshimiwa Spika, tutakuwa na haya Majukwaa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi ambapo fedha zitakuja, wadau wanatuunga mkono, tutakuwa na madirisha ya posta yanaendelea kuwepo, tutakuwa na mikopo mingine ile ya Women Development Fund iliulizwa hoja hapa sio kwamba umefutwa ilitekelezwa kutoka mwaka 1996 hadi 2017, kukatokea changamoto fulani zikahitaji mwongozo utengenezwe, mwongozo unakamilika Serikali itatoa maelekezo jinsi ya kupata fedha na kuendelea kutoa hiyo mikopo kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, masuala ya uwezeshaji kiuchumi katika usawa wa kijinsia yanazingatiwa sana na kufika mwezi wa Julai tutakuwa tumeshaweza kuzindua andiko hili ambazo tumeagizwa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yameulizwa hapa na hapa niseme kwamba wasajili wasaidizi wapo kwenye halmashauri na mikoa yetu walikuwa wanachangamoto ya kukosa fungu la kutekeleza majukumu yao lakini mwongozo wa uratibu wa pamoja na mashirika hayo umeshaandaliwa na umetoa majukumu kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa kuratibu ufuatiliaji wa miradi inayotekelezwa katika mamlaka hiyo. Natoa rai kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kutenga fungu kwa wasajili hawa ili waendelee kutekeleza majukumu yao ya uratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo ni mengi sana lakini kama vita hii tumeikubali ya kuliokoa Taifa letu naomba halmashauri/full council zikae kwenye usukani, taarifa ya kila mwezi inayokuja ikijadiliwa kwa mapana kama ilivyojadiliwa kwenye Bunge lako tukufu, hawa wakatili sio kwamba hawana akili wanajua vizuri wataondoka wenyewe.

Kuhusu suala la ukatili wa mitandaoni tumeshasema tunaandaa sasa kikosi kasi kimeshaandaliwa na sheria itafanyiwa mapitio, sheria zetu huenda ni nzuri sana miaka 30 ni mingi mno lakini saa enforcement yake inategemea mwitikio wa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tathmini ya MTAKUWWA itakapokuja itatuambia kama ni suala la kisheria hatutasita kulileta Bungeni mje mlijadili tuone tunafanyaje, lakini wakati huo jamii yetu twende tukaifungue kwa nguvu zetu zote unatokea ukatili vyumbani kwao sauti zifike hadi vyumbani kwao, mtu afike redio aiweke siting room aseme nimekuja hodi kama ni mtaani watu wasikilize hizi taarifa ili wawe empowered kuweza kuwa na confidence ya kupambana na hayo mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ningetamani kuendelea kusema hadi kesho, lakini naona muda hauniruhusu naomba kuwasilisha na naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye mjadala huu wa Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwanza ninawashukuru Wabunge wote ambao wamechangia katika eneo la maendeleo na ustawi wa jamii wakijielekeza kwenye hoja ya mmomonyoko wa maadili unaoathiri mila na tamaduni zetu nchini Tanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba kusema kwamba mmomonyoko wa maadili ni jukumu au ni kazi ya taasisi ya familia. Taasisi ya familia ambayo ndiyo chimbuko la watoto inatakiwa kurithisha maadili mema kwa watoto wao. Hivi karibuni kama walivyosema Wabunge wengi kuna kuyumba kwa taasisi hii ya familia ambapo sasa watoto wale hakuna anaewatunza katika malezi na makuzi.

Mheshimiwa Spika, imekuwa taasisi ya familia Baba na Mama na walezi ni rahisi kulea na kutunza na kufuatilia maslahi ya gari wanaloendesha, maslahi ya nyumba waliyoijenga, mali walizonazo kama ni mashamba na vitu vingine kuliko kufuatilia malezi na makuzi ya watoto. Kinachoendelea kwenye familia kwenye suala la mmomonyoko wa maadili, linalochangia maovu mengi sana ukianza ulawiti, ubakaji, kuvuta dawa za kulevya, wizi mpaka tunapata panya road.

Mheshimiwa Spika, nikirudi kwenye suala la ulawiti asilimia 60 ya uovu huu unatokea majumbani. Watoto walawiti wanafundishwa na ndugu zao wa karibu halafu ndiyo wanatoka kwenda kuendeleza mtaani, hofu ya Mungu inakuwa haipo, matokeo yake kila anayekuja na mila yake anapita kokote anapandikiza kwenye kichwa cha hawa watoto lolote lile. Hivyo inabidi taasisi ya familia irudi kwenye misingi yake.

Mheshimiwa Spika, naomba kusema Serikali inafanya nini eneo hili. Serikali imefanya mambo mengi sana na mambo haya tumekuwa tukiyatangaza na kuelimisha katika majukwaa mbalimbali na katika vyombo mbalimbali vya Habari. Kitu cha kwanza kikubwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alichokifanya katika kuangalia mstakabali wa hatma ya Taifa hili kwa miaka mingi ni kuiunda hii Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ili iwekeze nguvu zaidi kuhakikisha masuala ya maendeleo na ustawi wa jamii yanakaa sawa.

Mheshimiwa Spika, ninalishukuru Bunge lako Tukufu pia umeunda Kamati ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii ili kuongeza nguvu kushirikiana na Wizara hii na kutoa uongozi katika ajenda zote zilizojadiliwa humu.

Mheshimiwa Spika, naomba pia niseme kwamba Serikali imeendelea na mpango wake wa kutokomeza ukatili kwa wanawake na watoto, ulianza mwaka 2017 umeisha Juni, 2022 sasa tunakwenda kuzindua mwingine wa pili ambako ndani tumeboresha ile mikakati mpaka kwenye Halmashauri zetu kule ajenda hii tumepeleka maelekezo iwe ya kudumu kwenye vikao vyao vyote vya Kijiji, vya Mtaa, vya Kata, kwenye Halmashauri, Kamati zote za Full Council, na Full Council na tutafuatilia kuona utekelezaji wake inajadiliwa vipi.

Mheshimiwa Spika, Sheria Ndogo zitatungwa pamoja na mengine yote taarifa zitawasilishwa sambamba kama tunavyofanya kwenye lishe, tuna mikataba ya utekelezaji masuala ya lishe, hata kwenye masuala ya mmomonyoko wa maadili tutakwenda na sura hiyo ili ku-stimulate haya masuala yaweze kujadiliwa kwa upana wake.

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa gwajima kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Nicodemas Maganga.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa mchangiaji amezungumzia akina Mama na Watoto, hivi wanaume wenyewe huwa hawapati manyanyaso maana wenyewe hajawazungumzia Mheshimiwa Waziri (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri taarifa hiyo kutoka kwa Mheshimiwa Maganga unaipokea?

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ninaipokea naomba kutoa ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, katika suala hili la ukatili wa kijinsia na kwa watoto kwenye jinsia tunamaanisha jinsia ya ‘ME’ na ‘KE’ kwa hiyo hata kwenye madawati yetu ya jinsia, kama baba amekatiliwa akiripoti pale anahudumiwa kama ambavyo mama atahudumiwa lakini wanaume wamekuwa hawaji wanaona aibu, inabidi huu utamaduni tuubadilishe, wakishaona aibu wanakaa nayo moyoni la kwanza, la pili, la tatu wanachukua kisu wanaumiza au wanaua au wanafanya chochote kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nilindie dakika zangu mbili.

SPIKA: Mheshimiwa ukipewa taarifa, ni sehemu ya mchango wako. Kwa hiyo, hapa hulindiwi muda wako. Siyo muda wangu unaotumika, ni wakwako. Ahsante sana.(Makofi)

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSI, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, niendelee?

SPIKA: Dakika moja, malizia mchango wako.

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSI, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, tuna program ya malezi na makuzo kama Serikali ambayo imeanza 2021 mpaka 2025. Inajielekeza kwenye malezi na makuzi ya watoto sambamba na wazazi, watapata semina jinsi ya kulea watoto wao. Tuna program ya kuwekeza kwenye afya na maendeleo ya vijana balehe kuanzia miaka 10 mpaka 19. Hii nayo ni mwendelezo wa Taifa kusuka mifumo ya malezi na makuzi kwa vijana wake. Pia tuna community centered approach ambapo kampeni za jamii zitafanyika huko huko waliko ili kuhamasisha kaya pamoja na familia ziendelee kufuatilia na kuelimika na kujua juu ya masuala haya.

Mheshimiwa Spika, tuna mambo mengi…

SPIKA: Ahsante sana. Sasa hii hoja ni ya Waziri Mkuu. Kwa hiyo, natarajia ulikusudia kuunga mkono hoja? Siyo!

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSI, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, hakika naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)