Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ndaisaba George Ruhoro (13 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Nami nianze kuwashukuru wananchi waJimbo la Ngara kwa kunichagua kwa kishindo kikubwa na siku ya leo nipo hapa Bungeni kama Mbunge miongoni mwa Wabunge wa Bunge la Kumi na Mbili. Vilevile naomba nishukuru Chama changu Cha Mapinduzikwa kuniteua, bila Chama Cha Mapinduzi kuniteua leo hii nisingekuwepo hapa.

Nimesoma sana kwa umakini mkubwa hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukiondoa vitabu vya dini kwa maana ya Biblia, hii hotuba ya Mheshimiwa Rais ni Biblia yangu ya pili. Ukiangalia namna hotuba hii ilivyopangiliwa maudhui yaliyomo utagundua kabisa ndiyo maana Taifa letu linasonga mbele kwa sababu Jemedari wetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yuko vizuri na mipango ipo vizuri.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie hotuba ya Rais kwenye maeneo matatu: Eneo la kwanza ni kuwezesha wananchi kiuchumi; eneo la pili, ni ufugaji; na eneo la tatu, ni upande wa sekta za maji, umeme pamoja na barabara.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na sehemu ya kwanza ya uwezeshaji wananchi kiuchumi. Ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa11 imeelezea kwamba kuna mifuko ya kukopesha wananchi zaidi ya 18 na mifuko hiyo inaonekana haileti tija kwa sababu ya gharama za kuendesha mifuko hiyo, suala la uratibu, lakini ukiangalia na namna ya kupima matokeo inaleta changamoto kunapokuwepo na mifuko mingi.

Mheshimiwa Spika, ukisoma hotuba hiyo ukurasa huo wa11 utaona kuna ombi ambalo linamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kuangalia uwezekano wa kuunganisha mifuko hii ili iweze kuleta tija kwa Watanzania. Mimi mwenyewe nilisikia baadhi ya mifuko kwa mara ya kwanza alipokuwa anaisoma Mheshimiwa Rais. Nataka nikueleze Watanzania hawajui hii mifuko tena ukiangalia, Mheshimiwa Rais amesema kwenye hotuba yake hapa kwamba mikopo hii ni ile isiyokuwa na riba na ile yenye riba nafuu.

Mheshimiwa Spika, hata sisi Wabunge tungependa kwenda kukopa kwenye mifuko hii tukaachana na kukopa hadi kwenye gratuity za kwetu, naomba niiombe Serikali hasa Ofisi ya Waziri Mkuu iweke utaratibu mzuri kwanza wa utoaji taarifa kwa Watanzania juu yahii mifuko. Vile vile iweke utaratibu mzuri hii mifuko iweze kusaidia wananchi na wananchi wote nchi nzima waweze kupata taarifa sahihi za mifuko hii na utaratibu wa kuweza kupata fedha kutoka kwenye mifuko hii ya kuwezesha wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye upande wa ufugaji na hapa najikita kwenye kitu kinaitwa uhimilishaji, huduma ya uhimilishaji ni huduma inayomfanya mfugaji ahamuwe muda na siku ambapo na siku ambapo mfuko wake utapata mimba, huduma ya uhimilishaji inamwezesha mwananchi kupanga akitaka ng’ombe wake apate mimba kesho yake anamwita Daktari wa Mifugo, anaweka homoni pale anaweka mbegu na ng’ombe wake anapata mimba.

Mheshimiwa Spika, huduma hii inaweza kumfanya mfugaji kuamua idadi ya mifugo anayoitaka kila mwaka na hivyo tunaweza kuzalisha mifugo mingi na hivyo kukuza uchumi wa kaya moja moja na Taifa kwa ujumla. Naiomba Serikali kwenye eneo hili la uhimilishaji iweze kutenga fedha za kutosha kununua zana za uhimilishaji na kupeleka Madaktari wa Mifugo kwenye chuo kilichopo Arusha kinachofundisha masuala ya uhimilishaji ili kuweza kuleta tija kwenye eneo hili la ufugaji.

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye upande wa miundombinu hasa specifically kwenye sekta za maji, umeme pamoja na barabara. Jimboni kwangu na maeneo mengine nimesikia Watanzania wengi sana wanalalamika hasa vibarua pamoja na kampuni za Kitanzania zinazofanya kandarasi kama sub-contractors na makampuni ya nje. Mimi mwenyewe nimewahi kuwa sub kwenye tenda ambayo walipewa Wajerumani. Nataka nieleze wazi kwamba tunapigwa sana kwenye eneo hili, mzungu anasaini mkataba wa dola milioni tatu anakupatia kazi kama sub tunafanya kazi yote asilimia 98, inapokuja kwenye malipo kipindi kingine anatuzungusha, kipindi kingine bargaining power inakuwa ni ndogo na hata kipindi kingine Watanzania tunadhulumiwa.

Mheshimiwa Spika, achilia mbali sisi ambao niConsultants, njoo upande wa vibarua takribani maeneo mengi sana nchi nzima, wananchi vibarua wanalia. Hapa ninaombi kwa Serikali hasa kwenye idara zote hizi upande wa sekta ya maji, umeme na barabara, naomba Wizara ziweke utaratibu mzuri wa wananchi hawa wa Tanzania kulipwa moja kwa moja kutoka kwenye Wizara husika. Tukifanya hivyo, Watanzania watalipwa moja kwa moja na ile dhuluma ambayo tunadhulumiwa haitakuwepo, ni suala la Serikali kuweka utaratibu mzuri, mkandarasi mkubwa anatoa taarifa kwa aliyetoa kazi za vibarua ama aliyefanya naye sub-contractors, then Serikali inalipa moja kwa moja, tunadhulumiwa sana kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa,naomba nieleze changamoto iliyopo kwenye upande wa barabara. Barabara nyingi hasa za mjini ni chafu kwa maana ya kwamba zimejaa mchanga. Utaratibu uliopo wa kusafisha barabara nimeshindwa kuelewa vizuri, nilikuwa najiuliza, barabara inajengwa nzuri ya lami lakini baada ya muda mfupi unakuta michanga imejaa na kaeneo ka kupita ni kadogo katikati ya barabara na ile michanga inamomonyoa barabara. Naomba Serikali iangalie utaratibu mzuri iuandae wa kusafisha hizo barabara kutoa michanga kwenye lami. Najiuliza jukumu la kusafisha barabara wakipewa TAMISEMI, akapewa Mheshimiwa Jafo, mtaa husika ukahusika kusafisha zile barabara ile michanga itaondoka maeneo yale na barabara zitakuwa safi.

Mheshimiwa Spika, zile barabara za mijini zilizotengenezwa kwa gharama kubwa hata ukipita wewe jaribu kuchungulia kwenye kioo cha gari yako utakuta michanga imesogea kabisa mpaka inataka kumaliza barabara.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.(Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Naomba nianze kwa pongezi. Wapo Mawaziri wanne ambao wamegusa maisha ya wananchi wa Jimbo la Ngara na ninapenda nitumie nafasi hii kuweza kuwapongeza. Naomba kumpongeza Mheshimiwa Prof. Adolf Mkenda na Mheshimiwa Hussein Bashe kwa kugusa maisha ya wananchi wa Jimbo la Ngara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipomwomba Mheshimiwa Prof. Mkenda miche ya michikichi ndani ya siku saba, alituma watu wa TARI, walifika Ngara na kuotesha vitalu vya miche ya mchikichi. Ahsante sana. Nilipoomba miche ya kahawa, Mheshimiwa Hussein Bashe ndani ya mwezi mmoja amenipatia miche 300,000 na wananchi wangu wa Jimbo la Ngara wameshaipanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, speed hii ya Wizara ya Kilimo ni speed ya dream-liner naomba muweze kuindeleza. Vile vile, naomba nimpongeze Mheshimiwa Dorothy Gwajima pamoja na Mheshimiwa Godwin Mollel kwa kuendelea kuimarisha huduma za afya na hasa kwa kufika kwenye jimbo langu la Ngara na kuhakikisha kwamba changamoto zile za ukosefu wa madawa wamezifanyia kazi na sasa zile simu nilikuwa ninapigiwa kwamba hakuna madawa kabisa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, zimepungua. Ahsanteni sana kwa kuja Ngara, naomba kazi mnayoifanya ya kuboresha huduma za afya muweze kuendelea nayo na mtu yeyote asiwakatishe tamaa, mimi na wananchi wa Jimbo la Ngara nipo pamoja nanyi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kumpongeza Mheshimiwa Maryprisca na Mheshimiwa Aweso kwa kuja Ngara pia kugusa maisha ya wananchi wa Jimbo la Ngara. Walikuja Ngara na wakati Mheshimiwa Maryprisca anafika pale, alikuja na barua mkononi ambayo ilikuwa na taarifa za kupewa kibali cha kuruhusiwa kujenga mradi wa maji mpya ambao unaenda kutatua matatizo ya maji kwenye Mji wa Ngara Mjini pamoja na viunga vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri hao waliogusa maisha ya wananchi wa Jimbo la Ngara, naomba niseme kwamba Wizara yote itakayotugusa kabla sijaendelea na mchango, nitakuwa nawapongeza hapa hivyo, nikija kuwaomba msaada kutokea Ngara Waheshimiwa Mawaziri, basi ujue kabisa kwamba ukinisikiliza haraka haraka utakula pongezi ndani ya hili Bunge. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende moja kwa moja kwenye eneo la kilimo na ninaomba nichangie kwenye upande wa kilimo cha zao la alizeti. Mahitaji ya mafuta ya kula Tanzania kwa mwaka mmoja tunaitaji metric tani 400,000 mpaka 500,000 za mafuta ya kula. Uwezo wa kuzalisha mafuta ya kula kama Taifa ukijumlisha michikichi, alizeti na kadhalika, tunazaliza metric tani 200,000 mpaka 250,000 kwa mwaka. Hii inafanya tuweze kuagiza mafuta nje ya nchi kwa kutumia fedha za Kitanzania zenye dhamani ya Dola za Kimarekani milioni 80. Tunatumia fedha hii wakati Watanzania wapo na wana uwezo wa kulima alizeti na hayo mazao mengine tukazalisha mafuta ya kula hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania tuko tayari kuzalisha mafuta ya kutosheleza mahitaji ya Taifa. Wapo wakulima wa kutosha, wako wasindikaji wa mafuta ambao kwa Mkoa wa Manyara peke yake, nikitolea mfano, kuna viwanda vya kukamua na kusindika mafuta ya alizeti 234; na kwenye Jimbo la Ngara kipo kiwanda kimoja ambacho ni changu mwenyewe na chenyewe kina uwezo wa kuzalisha mafuta ya kula ya alizeti yanayotosheleza wakazi wa Jimbo la Ngara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, changamoto kubwa inayofanya tushindwe kuzalisha mafuta ya kula ya kutosha, ipo kwenye upatikanaji wa mbegu bora ya kisasa. Taasisi za utafiti za Tanzania tulizonazo hazijawahi na sijui kama wana mpango wa kuanza uzalishaji wa mbegu bora ya alizeti aina ya high breed. Teknolojia wanayoitumia kwa sasa kuzalisha mbegu ya alizeti inaitwa Open Pollinated Varieties (OPV), maana yake wanazalisha mbegu yenye daraja la kati ambayo haiwezi kuzalisha mafuta ya kutosha kutosheleza mahitaji ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mantiki hiyo, naomba nitumie nafasi hii kuweza kumwomba Waziri wa Fedha kufanya mambo yafuatayo; kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu, mwana wa Nchemba, naomba utusaidie mambo yafuatayo: moja, Wizara yako isaidie kulinda viwanda vya ndani hususani vile vinavyomilikiwa na wasindikaji wadogo, viwanda vya kati na vile vidogo hususani kwa kuzielekeza mamlaka, hasa TRA kujitafakari inapokwenda kwenye viwanda hivi na kuviathiri kupitia makusanyo ya kodi kwenye usajili, lakini pia na kodi za ukaguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia zipo mamlaka nyingine zinazoathiri viwanda hivi vidogo vidogo. NEMC, hitaji la kufanya Environment Impact Assessment ambalo linataka ukiwa na kiwanda uweze kutoa shilingi milioni 10, hiyo una- depots benki, umekopa huku kuanzisha kiwanda; hii nayo inatuathiri kwenye viwanda vidogo vidogo. Hivi vitu Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango viangaliwe ili athari inayopatikana kutokana na vitu hivyo ipunguzwe ili viwanda hivi viweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ni muhimu, ninaomba Vituo vya Utafiti vya Serikali vya Mbegu viwezeshwe ili vianze kuzalisha mbegu bora za kisasa. Narudia tena kwa msisitizo na herufi kubwa, VITUO VYA UTAFITI VYA SERIKALI VIWEZESHWE KUZALISHA MBEGU BORA ZA ZAO LA ALIZETI ZA KISASA MBEGU ZA HIGH BREED.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye soko, mbegu la zao la alizeti inanunuliwa shilingi 35,000/=. ukienda Mbeya Vijijini, ni mwananchi gani ana uwezo wa kumudu gharama hii ya mbegu shilingi 35,000/= kwa kilo moja? Hayupo! Ndiyo maana mimi kule kwenye Jimbo langu la Ngara nimenunua mbegu na nikatoa mikopo nikawagawia wakulima. Ninaomba watu wa kilimo waje wajifunze, tume-pilot na inaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ni muhimu sana ninaiomba Wizara ya Fedha iweze kusaidia Pamoja na Wizara ya Kilimo ni utolewaji wa mikopo ya mbegu kwa wakulima. Wakulima wawezeshwe kununua mbegu ili waweze kupanda zao la alizeti kwenye mashamba yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya kawaida, mwananchi ana shamba lake amelilima, mbegu sokoni inauzwa shilingi 35,000/=, hata kama tukiwezesha kwenye Taasisi zetu za Utafiti, sidhani kama itashuka shilingi 10,000/=. Bila kumwezesha mkulima huyu kwa kumpatia mkopo aweze kununua ile mbegu na kupata nguvu ya kupalilia shamba zima na baadaye kuvuna, hawezi kulima mashamba makubwa kibishara. Hivyo wakulima wawezeshwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hayo mambo matatu tutakuwa tumepata faida zifuatazo: moja, tutawezesha Watanzania kupata mbegu za kutosha tena mbegu bora za zao la alizeti, ambapo endapo tutawezesha Taasisi zetu za Utafiti kuzalisha; na hii haina chenga chenga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hatuwezi kutenga fedha za kuwezesha taasisi zetu zizalishe mbegu ya kisasa na badala yake tukawa tunasubiria Mataifa ya nje ambayo yana kampuni zao zinazozalisha mbegu za kisasa, wao ndio waje watuuzie, tena wanatupiga kweli kweli, kilo moja shilingi 35,000/=; bila hivyo tutakuwa hatujawatendea haki wananchi wangu wa Jimbo la Ngara, Shubi pamoja na Wahangaza na Wasukuma wa Nyamagoma pamoja na Wahaya wa Benagu. Tutakuwa hatujawatendea haki wananchi wa Dodoma wanaolima alizeti, Wagogo pamoja na wengine wa Singida, Wanyiramba na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo, tutapunguza gharama ya kununua mbegu ya zao la alizeti sokoni iliyopo kwa sasa. Kama tutawekeza kwenye viwanda vyetu vya kuzalisha mbegu, tutawezesha upatikanaji wa chakula cha mifugo cha kutosha. Yale mashudu yanatumika kwa ajili ya kulishia mifugo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia.

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia kabisa sekunde tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwekeza hivi kwa kuwezesha taasisi zetu tunaenda kuondoa tatizo la mafuta kwenye nchi yetu ndani ya kipindi cha miaka miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara ninakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji. Kwa namna ya kipekee kabisa ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji, kaka yangu Juma Aweso; napenda kumpongeza Naibu Waziri, Mheshimiwa Maryprisca; napenda kumpongeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Eng. Sanga kwa utendaji wao mkuu uliotukuka wa Wizara ya Maji. Kwa kweli tunawashukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa, napenda kuwashukuru viongozi hawa kwa kuridhia kuidhinisha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Mradi wa Maji wa Ngara Mjini ambao pia utafikisha maji kwenye Kijiji cha Mkididili, Buhororo, Kumuyange, pamoja na Nyamiaga. Ninawashukuru sana kwa kuidhinisha hiyo fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa, napenda kuwashukuru Serikali ya Uingereza, Balozi wa Uingereza pamoja na mtu anaitwa Eng. Lukas Kwezi, kwanza kwa kubuni mradi wa nyumba ni choo, lakini kwa kubuni mradi wa RBF (Result-Based Financing). Kwa Jimbo la Ngara peke yake kupitia ubunifu wa hii miradi na ruzuku walizotupatia kama Taifa, tumepata takribani shilingi milioni 604 kwenye awamu iliyopita ya mgawanyo wa fedha za RBF.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwomba ndugu yangu Eng. Lukas Kwezi aendelee kuwa na ubunifu huu na kwa vile mradi huu unakaribia kufika mwisho, basi aweze kubuni mradi mwingine wa miaka mitano ili katika kipindi changu cha miaka mitano cha kuongoza Jimbo la Ngara niendelee kupata mgao kama huu kila mwaka ili niweze kuondokana na changamoto za maji zilizoko kwenye Jimbo la Ngara. Napenda pia kushukuru, nimeona ukurasa wa 154 orodha ya miradi iliyotengewa fedha na Wizara ya Maji kwa ajili ya Jimbo la Ngara, kwa kweli ninashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nielekeze mchango wangu kwenye upande wa usimamizi endelevu wa rasilimali za maji. Waheshimiwa Wabunge waliotangulia hapo nyuma kabla yangu, wameeleza changamoto nyingi zilizopo kwenye usimamizi wa miradi ya maji. Nami naomba hapa Wizara ya Maji mnisikilize vizuri, nina uzoefu kwenye kutengeneza hizo CBUWSO ambazo ndiyo Kamati za Maji na kuzisimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimuundo wa hizi CBWSO kuna tatizo la social setup. Maeneo mengine ni ngumu kutenganisha uongozi wa Kamati ya Maji pamoja na Uongozi wa Serikali ya Kijiji. Maeneo mengine utakuta Mwenyekiti, Katibu na Mweka Hazina wa Kamati ya Maji wana undugu na Serikali ya Kijiji. Hivyo, hata kwenye uwajibikaji wao inakuwa ni ngumu. Hata mimi Mbunge siwezi kukubali Kamati ya Maji iwajibishwe wakati Kamati hiyo hiyo ukitaka kuiwajibisha ni kama vile unawajibisha wapigakura wangu walionichagua kwenye kile kijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwaomba Wizara ya Maji waje na model nyingine ya kusimamia miradi ya maji vijijini inayoitwa Franchise Model. Sina Kiswahili cha jina hilo, lakini Franchise Model ni utaratibu wa kusimamia miradi ya maji kwa kuwapa mikataba watu binafsi au kampuni ziweze kuendesha ile miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hii nchi kuna double standard kama mjini kuna Watanzania na vijijini kuna Watanzania, halafu mjini zimepewa kusimamia maji kama DUWASA na DAWASA, halafu vijijini tumeachiwa sisi wananchi wenyewe tusimamie miradi yetu ya maji. Haya mambo hayakubaliki kwa sababu kama wanatuachia sisi wananchi hatuna mafunzo, hatuna wataalam, tunawezaje kusimamia miradi hii ya maji ambayo ni uwekezaji mkubwa, fedha ya Serikali inaingia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara ya Maji waruhusu RUWASA iweze kuwapa mikataba makampuni binafsi ama watu binafsi wenye uwezo wa kuendesha hii miradi ya maji. Ni rahisi kumwajibisha mtu binafsi, pump ikikataa kufanya kazi, bomba likikatika ama tape ikavunjika ni rahisi kwenda kumwajibisha mtu binafsi ama kampuni binafsi kuliko kuwawajibisha wananchi ambao ndio wasimamizi wa hiyo miradi ya maji. Hilo naomba lieleweke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nielekeze mchango wangu pia kwenye kitu kinaitwa Mfuko wa Maji wa Taifa yaani National Water Fund. Maji unayoyaona tunayoyatumia yana sehemu mbili, ukishachukuwa maji ukayatumia, asilimia kubwa ya maji yanayotumika yanageuka kuwa maji taka yaani waste water. Maji taka haya ni yale tunayotumia vyooni, ni yale tunayotumia bafuni na asilimia 80 ya maji yote unayopeleka nyumbani yanabadilika na kuwa maji taka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Taifa wa maji una jina ambalo haliakisi mnyororo mzima wa maji. Jina lake ni National Water Fund, nawaomba sana Wizara Maji mwende mkabadilishe hili jina kutoka National Water Fund kwenda kuwa National Water Fund and Sanitation yaani Mfuko wa Maji wa Taifa na Usafi wa Mazingira. Hapo tutakuwa tumeakisi ile sehemu ya pili ya matumizi ya maji ambayo maji mengi yanaenda kubalika na kuwa maji taka.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji taka uwa tunayahifadhi vyooni hasa yale tunayoyatumia vyooni na tunayahifadhi kwenye septic tank, maji mengine ambayo ni maji taka ni yale yanayotoka jikoni. Tunavyoyahifadhi haya maji kwenye septic tank zile septic tank zina tumika na baadaye zinajaa. Ukienda ukachukua sampuli ya maji taka kwenye septic tank vyooni ukiyapima unakutana na virusi zaidi ya laki moja, unakutana na protozoa zaidi ya elfu 10, unakutana na virus protozoa pamoja na bakteria, wadudu wengi wako kwenye yale maji taka, ndio maana kuna umuhimu wa kuwekeza fedha kwenye usimamizi endelevu wa maji taka ili…(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashusha nondo na najua watanitafuta ili niwaongezee nondo. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kupiga makofi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee, yale maji taka yale kwenye maeneo ya mijini ambako kuna mifumo ya sewerage yaani ya sewer system, vyoo vile vinaunganishwa kwenye ile mifumo na yale maji yanaenda kutibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo ya miji inayokuwa hasa kwenye Jimbo langu la Ngara, Mji wa Rulenge na Mji wa Ngara Mjini hata hapa Dodoma, maji haya yapo kwenye septic tank yanahitaji kuchukuliwa na magari yanayokwenda kufyonza yale maji na kwenda kuyapeleka kwenye mifumo ya kuyatakasa ili maji hayo yanapotolewa kwenye ile mifumo yawe pathogens free yaani yasiwe na hao wadudu niliowataja na maji hayo hata tukuyaruhusu yakarudi ardhini yanakuwa hayawezi kuchafua maji yaliyoko chini ya ardhi yaani underground water. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana naishauri Wizara ya Maji kubadilisha jina la Mfuko kutoka kuwa kwenye Mfuko wa Maji wa Taifa kuwa kwenye Mfuko wa Maji na Usafi wa Mazingira wa Taifa na matumizi ya fedha iliyoko kwenye huo Mfuko yaweze kuwekezwa kwenye kusimamia hayo maji taka ili tuweze kuondoa magonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisikia milipuko mjini ujue ni hayo maji taka yaliyosambaa. Ukisikia magonjwa kama kipindupindu na mengine ya kuhara ujue ni haya maji yameachiliwa, yametapakaa mijini yanaleta magonjwa kwa wananchi. Ndio maana siku ya leo nachukua fursa hii kuwaomba Wizara ya Maji na kuwashauri kabisa kwa namna ya kipekee, mgawanyo wa fedha za Mfuko wa Maji na Usafi wa Mazingira, nimeshaanza kuuita hivyo, ziende kwenye maji safi na ziende kwenye kusimamia maji taka.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba Wizara ya Maji iwekeze kwenye mifumo ya kisasa ya kutibu maji taka inaitwa Faecal Sludge Treatment System, haina Kiswahili sijawahi kukisikia, lakini kuna mfumo mwingine unaitwa Decentralized Waste Water Treatment System (DEWATS). Hii nayo

NAIBU SPIKA: Hiyo Mheshimiwa…

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, hii nayo haina Kiswahili chake.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndaisaba hiyo ungekuwa umemwona Mheshimiwa Maige kabla angekupa tafsiri hiyo. (Makofi)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia na kwenye kamusi sijaona, naomba unisamehe.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kuchangia kwamba, Wizara ya Maji iwekeze kwenye kujenga hiyo mifumo ili katika sehemu nyingi katika nchi hii ambapo septic tank zinajaa, wananchi waweze kwenda kunyonya vyoo vyao na wapeleke maji taka hayo yaende kutibiwa kwenye hiyo mifumo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba Wizara itakapoanza kutekeleza haya mawazo yangu, Jimbo langu la Ngara liwe la kwanza kupewa allocation kwa sababu hizi nondo nimezileta mimi na Wizara itakapoanza kufanyia kazi mchango wangu sisi jimbo la Ngara tuweze kupewa kipaumbele. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ruhoro kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Agnes Hokororo.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka kumpa taarifa mzungumzaji hilo neno alilosema tiritimenti, kwa lugha ile ya kwetu ni treatment. Ahsante. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, malizia sekunde thelathini.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli mchango wake, sijui nini hiyo aliyoitoa nimeikataa, kwa sababu mimi ningemuambia ataje Faecal Sludge Treatment System asingeliweza kutaja, kwa hiyo naikataa. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa, naomba mawazo yangu mawili hayo Wizara ya Maji iweze kuyachukua na iende ikayafanyie kazi hasa hili la kubadilisha jina la Mfuko wa Maji wa Taifa

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: lakini vilevile na kwenye mifumo ya usimamizi endelevu wa miradi ya maji yaani Kamati za Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya bajeti, awali ya yote napenda kuanza kumshukuru na kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi mzuri ambao ameuonesha tokea awe Rais wetu na kwa kazi nzuri sana ambayo anaendelea kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya muda mfupi Mama Samia ameonyesha uongozi mzuri uliotukuka na jamii ya Kimataifa imetambua kwamba Tanzania tuna Rais kweli kweli Rais Mama. Vilevile, napenda niweze kuwapongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu Waziri wake na viongozi wengine wote wa Wizara, kwa kuweza kutuletea bajeti ya kisayansi kwenye Bunge letu hili. Bajeti ambao kwa kweli imegusa maeneo mbalimbali ya vipaumbele ya nchi, imegusa makundi mbalimbali kwa kweli mimi nina washukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili bajeti hii iweze kutekelezeka, ni wazi kwamba lazima tupanue wigo wa kodi na ni lazima maeneo yote nyeti ya makusanyo ya fedha yaweze kuboreshwa ili kodi iweze kukusanywa. Kwa minajili hiyo Jimbo la Ngara ni miongoni mwa Majimbo ambayo yamekaa kimkakati, Jimbo la Ngara linapakana na nchi mbili za Rwanda na Burundi na kutoka Ngara kwenda Goma - DRC ni kilomita 355 na kutoka Ngara kwenda Juba ni kilomita 1,094. Hivyo, tunao mwingiliano mkubwa wa maeneo yote haya na biashara ya mpakani kwenye Jimbo la Ngara imeshamiri kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya forodha vinavyotakiwa kufanya kazi kwenye Jimbo la Ngara ni vituo vinne lakini mpaka sasa ni viwili tu vianavyofanya kazi yaani kile cha Kabanga na kile cha Rusumo. Kulikuwa na kituo cha forodha cha Mgoma ambacho kilianza kufanya kazi miaka ya nyuma lakini baadae kituo hiki kilifungwa na TRA upande wa Tanzania waliondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wenzetu wa upande wa Burudni wamejenga jengo kubwa sana la kisasa, wameweka taasisi zao za mamlaka wa mapato pamoja na Uhamiaji kwa upande wa Burundi. Upande wa Tanzania, kuna mtaalamu alitoka TRA Makao Makuu wamekuwa wakienda pale Mgoma, kwenda kutembea, kwenda kufanya assessment na ripoti wanazoaifanyia assessment hazijawahi kutoka na kinachoendelea hatujui ni kitu gani. Nimuombe Mheshimiwa Waziri atoe maelekezo TRA, taarfia iliyoenda kuchukuwa pale itoke na kituo hiki kiweze kunya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kamati ya kushughulikia masuala ya magendo ya Mkoa inaitwa ‘fast’, kazi yake ni kwenda kukamata wafanya biashara ambao kwa kweli ule mpaka ni lazima wafanyabiashara wautumie kwa magendo, kwa maana ni ngumu mfanya biashara kusafiri zaidi ya kilomita 50, kwenda kutafuta huduma za forodha, wakati anaweza kupitisha kwenye njia za panya mzigo wake wa kilo 10 kilo 20 na akaweza kuupitisha. Hivyo badala ya kuhangaisha hawa wafanyabiashara, ninaomba sana Wizara ya Fedha na Mipango, iweze kutoa maelekezo kama zamani huduma ya forodha ilikuwepo, na kulikuwa na majengo ya kawaida yanayotumika na upande wa pili wa Burundi wapo tayari kwa ajili ya biashara mapakani sisi tunakwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri atakapokuwa ana-conclude, kwa kweli tunaomba uwatendee haki wananchi wa Ngara na wafanyabiashara wote kwa kuruhusu kituo hiki cha forodha cha Mgoma, kiweze kuanza kutoa huduma za forodha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwengine, tuna kituo kingine cha forodha cha Murusagamba, kilijengwa mwaka 1990, baadae kikaungua, mwaka 2016 kikajengwa upya baada ya kuwa kimeungua, baada ya hapo TRA Mkoa na TRA Ngara wakaomba kupewa namba maalum ya utambulisho wa kituo hicho yaani Identification Code Number. Tokea mwaka 2016 Mheshimiwa Waziri hiyo namba hatujapewa kwenye kituo chetu cha forodha cha Murusagamba. Kamishna wa TRA ameishikilia hiyo namba, nakuomba Mheshimiwa Waziri hiyo identification number ya kituo chetu cha forodha cha Murusagamba iweze kuletwa ili kituo chetu kianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na modem, ile modem ilichukuliwa kutoka kituo chetu cha forodha cha Murusagamba ikapelekwa Kerwa, ikatumika Kerwa na baadae ikachukuliwa ikapotelea hewani, mpaka sasa hivi modem yetu Mheshimiwa Waziri ya kituo cha forodha cha Murusagamba hatujui imepotelea wapi. Nakuomba Mheshimiwa Waziri, modem yetu irejeshwe kwenye kituo chetu cha forodha cha Murusagamba ili kituo hiki kiweze kuwa automated, kianze kusoma na wafanyabiashara waache kupata taabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfanyabiashara anapokwenda na gari lake la mzigo anafika Murusagamba analipaki pale, inabidi asafiri umbali wa kilomita 123 one way, kwenda kupeleka nyaraka zake zipigwe muhuri kwenye kituo cha forodha cha Kabanga na baadae arudi tena asafiri kilomita 123 jumla kilomita 246 kutafuta huduma ya forodha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwamishwa na vitu viwili ambavyo ni identification number na hiyo modem, naomba utoe maelekezo hivi vitu viletwe ili kituo chetu cha Murusagamba kiweze kutoa huduma kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Ngara, kwa ajili ya wafanyabiashara na wakati huo huo kiweze kusaidia kukusanya mapato ya Serikali ambayo yanahitajika ili bajeti hii ulioileta Mheshimiwa Waziri iweze kutekelezeka katika kipindi chote hichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee eneo la urasimu lililokuwa likiwakumba wadau wa maendeleo hasa NGO. Kwenye ukurasa wa 29 wa hotuba ya bajeti Mheshimiwa Waziri ameonyesha bayana kwamba kumekuwa na ukiritimba kwa wadau wa maendeleo wanapokuwa wanaleta fedha zao kwaajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo wanakutana na figisu figisu kule Wizara ya Fedha na kulikuwa na sheria ambako inataka msaada unapokuja ndani ya nchi on entry ule msaada uweze kukatwa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka dunia ilikuwa inatucheka, kuna haja gani ya kukata kodi kwenye msaada unapoingia moja kwa moja pale BOT wakati msaada huo huo unaendelea kuukata kodi nyingine kama vile PAYE withholding tax na kodi nyengine baada ya msaada ule unapoingia kwenye matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulimwengu mzima ulikuwa unatushangaa Tanzania, yupo mfadhili mmoja kwenye bajeti yake anatenga zaidi ya dola milioni 500 kuzisaidia nchi zinazoendela kama Tanzania, sisi na figisu figisu zetu tunaendelea nazo Kenya mpaka wakaongezewa fedha zetu zaidi ya dola milioni 200 wakapelekewa sisi tunaendeleza figisu figisu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba yako Mheshimiwa Waziri umeweka vizuri sana tunaomba futilia mbali hiyo sheria ambayo inasema tutoze kodi moja kwa moja on entry wakati fedha hizo zinaongeza wigo wa kodi kwenye Taifa letu. Nakuomba Mheshimiwa Waziri wala usipate kigugumizi, futilia mbali hizi sheria, watu wanatushangaa ule ni msaada! Mataifa ya nje yanatenga fedha zao kuja kutusaidi nchi zinazoendelea, tunakwenda kukata kodi ya moja kwa moja, wakati tunao uwezo wa kukata kodi hivyo hivyo tukaipata baada ya fedha hiyo kuingia kwenye matumizi. Kwa kweli hapa umeitendea haki nchi na Mheshimiwa Rais tunampongeza kwenye eneo hili, nenda futilia mbali hiyo sheria inayotaka tukate kodi kwa sababu imekimbiza wadau wetu wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalonapenda kuliongelea, ni mradi wa kielelezo wa Kabanga nikel ambao umeoneshwa ukurasa wa 16 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Baba yangu alipozaliwa alikuta kuna kitu kinaitwa mradi wa Kabanga Nikel, akakua akamuoa Mama yangu wakanizaa na mimi, nami nimezaliwa nimekuta kuna mradi wa huu wa Kabanga nikel, mimi pia nimekua nimeoa na nimepata mtoto wa kwanza anaitwa Ndairagije nae amekuta kuna mradi wa Kabanga Nikel. Nimekaa nimepata mtoto mwingine anaitwa Irakoze naye amekuta kuna mradi wa Kabanga Nikel. Kwa upande wa Marais, amekuja Rais wa kwanza, wa Pili, wa Tatu, wa Nne, wa Tano na sasa hivi tunae Rais wa Sita naye amekuta mradi huu wa Kabanga Nikel mchakato unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa kweli Kabanga Nikel wawezeshwe umeme upelekwe, leseni ya kuchimba haya madini itoke ili uwekezaji huu sasa Mama Samia anyanyue ngoma. Hii ngoma inanyanyuka na Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu umeisha lakini ninaomba sana mradi huu hawa watu wapewe leseni ili uwekezaji uweze kuanza. Ahsanteni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea na mchango wangu mahususi nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kutoa maelekezo na wananchi 1,142 wa Jimbo la Ngara waliokuwa wanadai fidia muda mrefu baada ya mashamba yao kuvamiwa na maji wakapata hasara kubwa, kulipwa Shilingi Bilioni Tatu na Milioni Mia Tisa. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara ninamshukuru Rais wetu kwa upendo mkubwa alionao kwa Watanzania na kwa fedha hizi ambazo amezituma Ngara ni ushahidi na ushuhuda kwamba Rais wetu anawapenda na kuwajali Watanzania, ndiyo maana sisi wananchi wa Jimbo la Ngara tunatambua jambo la Mama na tuko nae hadi 2030.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipotoa maelekezo kuna watumishi mbalimbali wa Serikali walishiriki kwenye mchakato wa kuhakikisha wananchi wangu wanapata fidia hiyo. Mathalani Waziri wa Nishati Mheshimiwa Januari Makamba amefanya kazi kubwa sana kuhakikisha wananchi wa Jimbo la Ngara wanapata fedha yao.

Vilevile Mkuu wa Wilaya ya Ngara Mheshimiwa Kanali Mathias Kahabi nae amefanya kazi kubwa sana kuhakikisha tunachakata hizi fedha na wananchi 1,142 wanapata shilingi bilioni tatu na milioni mia tisa. Kwa upendo mkubwa tunamshukuru Mheshimiwa Rais, tunamshukuru Mheshimiwa Makamba pamoja na Mkuu wetu wa Wilaya kwa kazi nzuri waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nielekeze mchango wangu kwenye ile sheria kandamizi ambayo inawalipa wananchi kiduchu pale ambapo mashamba yao yanakuwa yamevamiwa na kuliwa na wanyama wakali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi kwamba dunia nzima mabadiliko ya tabianchi (climate change) yanafahamika. Mabadiliko haya yanasababisha kuongezeka kwa joto duniani ambalo linaathiri uoto wa ardhi uliopo, uoto wa asili pamoja na kuleta mvua za rasharasha, matokeo yake huko porini majani hupungua na wanyama kuanza kuhangaika kutafuta mahali pa kupata malisho. Hii ni miongoni mwa sababu kubwa zinazofanya tembo wasiweze kukaa porini na badala yake wanahainga kwenda kutafuta chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa tembo wanapotoka huko porini pamoja na simba wanafanya uharibifu mkubwa mbali na kuharibu mazao, wanajeruhi wananchi, wanasababisha mauaji ya watu pamoja na mifugo yao. Mathalani wananchi wangu wa Jimbo la Ngara wanaokaa kwenye vijiji vya Ngoma, Wakalemela, Kamuli pamoja na Mrusagamba wameathiriwa sana na wanyama tembo kwa kushindwa kukaa kwenye hifadhi na kwenda kwenye maeneo ya wananchi na kusababisha uharibifu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo Kanuni inaitwa The Wildlife Conservation Dangerous Animals Consolation, Regulation of 2011. Hii ni kanuni ambayo inawaumiza Watanzania, kama ambavyo wachangiaji wa kamati hii wameshaeleza tokea asubuhi, ukienda kwenye regulation 4(1) utakuta kwamba sheria hii imeeleza kwamba kama mwananchi analo shamba lenye ukubwa zaidi ya heka tano na shamba lile tembo wakalivamia na wakala lote wakalimaliza, sheria hii inasema kwamba mwananchi yule atalipwa tu hekari tano pekee hata kama alikuwa amelima hekari 12.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni uwekezaji kama uwekezaji mwingine. Kilimo ni biashara kama biashara nyingine, mbali zaidi kanuni hii imesema mwananchi huyu atalipwa Shilingi Laki Moja kwa hekari moja. Naomba Waheshimiwa Wabunge mfikirie, mwananchi wamekopa pesa ameandaa shamba, amenunua mbegu, amepanda, hajavuna tembo wanakuja wanaharibu shamba lake, halafu sisi tunaoona wanyamapori ni bora kuliko Watanzania, tunasema kwamba acha mashamba yaharibike sisi tembo waweze kuishi kwa kula mashamba ya watu halafu tunafidia Shilingi Laki Moja Moja kwa heka moja, siyo sawa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna jambo tunatakiwa kulifanya kama Bunge ni kuhakikisha hii kanuni tunaiitisha inafanyiwa marekebisho na badala ya kutoa kitu kinaitwa kifuta jasho na kifuta machozi, sheria hii iende ikatoe full compensation kwa sababu wananchi hawa wanakuwa wamewekeza kwenye mashamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiendelea eneo hili sheria hii inasema kama wanyama hawa hasa tembo wametoka porini wamekuja kwenye shamba lako wakafanya uharibifu kwenye robo ya shamba ama nusu ya shamba, sheria inasema wewe mwananchi hutakiwi kufidiwa kitu chochote. Sasa wananchi wa kawaida wanajiuliza ina maana tembo akishafika kwenye shamba la migomba wakila nusu kile kilicholiwa inakuwa siyo migomba tena inakuwa ni mitipori au ni nini? Tunajiuliza hivi basis ya hii sheria wakati inatengenezwa ilikuwa na maana gani? Tunawatesa Watanzania (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtanzania ameweka fedha yake pale tembo wakila sisi tunafurahi kwa sababu kule porini kuna njaa basi tembo amekuja amekula migomba ya mtu anarudi akiwa ameshiba, wewe unaleta mtalii unakusanya fedha lakini mkulima anaendelea kuumia! Jambo hili siyo sawa. Ninaomba Bunge hili miongoni mwa maazimio ambayo Bunge linatakiwa lichukue iwe ni kwenda kubadilisha hii kanuni badala ya kutoa kifuta jasho pamoja na kifuta machozi iweze kutoa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa maazimio ambayo Bunge linatakiwa lichukue iwe ni kwenda kubadilisha hii kanuni badala ya kutoa kifuta jasho pamoja na kifuta machozi iweze kutoa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nafuatilia muda wangu bado kabisa; ukiangalia kwa mfano pale ambapo wanyama wamesababisha madhara makubwa hasa kuuwa, wenzangu waliyotangulia kuchangia wameshasema kwamba ikitokea mwanadamu ameuliwa na mnyama mkali, fidia iliyowekwa na kanuni hii ni shilingi milioni moja. Sasa mimi najiuliza assume sisi wote hapa tulipo ni Wabunge, umefanikiwa umemuoa mke wako mzuri, umezaa naye watoto wawili au watatu, mtoto wako anatoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine katikati anakutana na tembo ama anakutana na simba, yule mtoto analiwa halafu unakuja kukutana na Serikali wanakuambia pole sana kwa kupotelewa na mtoto wako, tena mtoto wa kwanza au wa pili ila tutakuja kukupa kifuta machozi shilingi milioni moja, haingii akilini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kuwafuta machozi wananchi wetu tunawatia hasira, twende mbele ukiachana na hapo anapokuwa amekufa mwanadamu, anapopata ulemavu wa kudumu hebu fikilia kwanza kwa mfano ukipoteza reception na ulikuwa hujaolewa na hutopata mchumba tena, sheria inasema upewe shilingi laki tano. (Makofi)

Sasa mimi najiuliza hivi hizi sheria wakati zinatengenezwa mwaka 2011 factors ambazo tunaziona sasa hivi zilikuwa ni zile zile au zimebadilika? Na ndiyo maana napenda kushawishi Bunge hili hizi kanuni ziende zikafanyiwe marekebisho ili ziende zikatende haki kwa Watanzania, wananchi wetu waweze kupata compensation inayolingana na madhara wanayokuwa wameyapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo linachekesha kwenye kanuni hii, inapotokea labda ametoka simba porini, halafu yule simba ameingia kwenye zizi la mifugo na ndani ya lile zizi la mifugo kuna mbuzi, kondoo halafu yule simba akaenda akawala wale mbuzi na kondoo sheria yetu inasema yule mwananchi kwa upande wa mbuzi atatakiwa kufidiwa shilingi 25,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi 25,000 ni fedha sawa ya kununua jogoo tena kipindi kingine ukikutana na jogoo lilotulia shilingi 25,000 haitoshi. Sasa unajiuliza mwananchi amepata hasara. amepoteza kondoo, amepoteza mbuzi, Serikali inakwenda kumlipa shillingi 25,00 kwa kila mfugo uliyopotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yanawaumiza Watanzania na kipindi kingine Watanzania hawana pa kulalamikia ndiyo maana wanatutuma sisi tuje hapa tuwasemee na ndiyo maana ukienda kwa upande wa ng’ombe, thamani ya ng’ombe mmoja ni kuanzia shilingi 700,000 mpaka shilingi milioni tatu. Sheria inasema inapotokea mifugo ya mwananchi imeliwa na wanyamapori hasa simba, sheria inataka mwananchi yule apewe shilingi 50,000 kwa kila mfugo uliopotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wangu wa Ngara wa maeneo niliyoyataja mwanzoni walishasema ng’ombe wakiliwa hii fedha haiwasaidii chochote badala yake inawapa fedheha, mwananchi anapoteza mifugo miwili, mifugo tatu halafu Serikali inakuja kulipa fidia ya shilingi 50,000 kwa kila mfugo, wananchi tunawaumiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana kwa unyenyekevu mkubwa Bunge lako tukufu liazimie twende tukafanye mabadiliko ya hizi sheria pamoja na hii kanuni, tuwafute Watanzania machozi kweli, tusiende kuwadanganya huku moyoni tunafurahia kwamba sisi tumeshaona kwamba Mifugo na yale mashamba ni vyanzo vya chakula kwa wanyama wetu waliopo porini, pengine tunawaza hivyo, lakini kama hivyo ndivyo sivyo ninaomba Bunge liazimie sheria hizo ziende zikafanyiwe marekebisho na wananchi wetu waweze kupata compensation ambayo kwa kweli ni nzuri na iliyotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mchango wangu unaishia hapo. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami ya kuchangia kwenye Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye vitu vitatu na vyote viko kwenye eneo la kilimo. Nitatumia lugha mchanganyiko. Eneo la kwanza ni effective utilization of labour force, post-harvest loss na productivity kwenye agriculture.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye effective utilization of labor force; ukiangalia Tanzania majority age group ni vijana ambao ndiyo tunawategemea waweze kuzalisha. Hawa vijana kama ambavyo nimechangia mchana wakati mzungumzaji alipokuwa anachangia pale walio wengi ni wale waliomaliza kidato cha nne, wengine darasa la saba na wengine wametoka vyuo vikuu. Hawa vijana kama nilivyokuwa nimegusia mwanzoni wanaposikia shughuli za kilimo, ufugaji, iwe ni kulima ni kama vile hiyo kazi ni ya watu fulani ambao sio wao wenyewe. Kwanza wanaumia, hawako tayari kwenda kufanya hizo kazi, kwa hiyo kama Taifa hatuja-harness vizuri ile nguvu ya wale vijana katika kuzalisha mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia China, Wachina wanafanya kazi kama nyuki, angalia Vietnam, Vietnam wanafanya kazi kama nyuki, njoo Tanzania. Saa tatu kamili za asubuhi, mtu ameshatoka shambani yuko nyumbani amekula kishoka. Saa nne kamili za asubuhi tayari ameshakunywa aina ya maji, ameshaanza kuchangamka mpaka saa sita anazungumza Kiingereza. Matokeo yake kama Taifa hatujanufaika vizuri na matumizi ya nguvu za vijana katika kuzalisha ili tuweze kupata mafanikio tunayoyataka kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya haya, vision na mission tuliyonayo kama Taifa huko tunakoelekea kwa spidi, sisi tunaelekea huku, wananchi ambao ni wazalishaji tumewaacha huku. Hivyo kama Taifa nina ushauri sasa, kwenye eneo hili la matumizi sahihi ya nguvu kazi za vijana kwenye kujenga Taifa nashauri mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la kwanza, vileo vipigwe marufuku kuuzwa na kunywewa mida ya kazi. Ni rahisi sana, kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alisimama akakataza viroba na vikapotea, vivyo hivyo katazo linaweza likatolewa wananchi wakabaki wanakunywa muda wa weekend.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la pili, nashauri turejeshe mfumo wa kufundisha vijana wetu uzalishaji wakiwa shuleni, nenda sekondari, ukienda sekondari mwanafunzi anasoma kuanzia form one hadi kidato cha sita hajawahi ku-practise ufugaji wala kilimo. Naishauri Serikali kwenye Mpango huu unaokuja wa miaka mitano turejeshe haya mashamba darasa kwenye shule zetu. Hawa ambao wameshamaliza muda wao umepita tuwaache, lakini hawa ambao wako kwenye shule zetu tuwafundishe kulima na tuwafundishe ufugaji. Wale watakaobahatika kuendelea na Vyuo Vikuu, wataendelea. Wale ambao hawatabahatika waweze kuona hizi shughuli za kilimo kama sehemu ya ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihamie upande wa kuongeza uzalishaji (increasing productivity). Tanzania tumebahatika kuwa na mito, mabonde na ardhi nzuri yenye rutuba. Eneo linalolimwa ni dogo, mkuu wa kaya ambaye mara nyingi ni baba, unakuta kwenye kaya zetu ukienda vijijini hata hapa Dodoma mtu amelima nusu eka, amelima eka moja, ana vimbuzi viwili nyumbani, akiongeza na ng’ombe watatu amemaliza, watu wameridhika. Hii kasi tuliyonayo sisi kama Serikali kwamba watu tufanye kazi people are relaxing, hawana haraka, ameridhika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali, kupitia mifumo iliyopo ya kuhudumia na kusimamia maendeleo tutoe maelekezo. Tutoe target kwa kila mkoa, wilaya na kijiji, ili familia zote za vijijini ziweze kuzalisha. Badala ya kulima eka moja au mbili ziweze kuwa eka nyingi ili nguvu ya Serikali inayoenda kuwekezwa kwenye kilimo iweze kuonekana ndani ya kipindi cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la post harvest loss sijaweza kulizungumzia, ila niseme tu kwamba naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara napenda kuanza kuwashukuru viongozi wa TAMISEMI kwa kuweza kuidhinisha mafungu mbalimbali ya fedha ambayo tayari yameshafika kwenye Jimbo langu la Ngara. Mathalani naomba niwashukuru Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Mheshimiwa David Silinde, Mheshimiwa Dugange na Dkt. Riziki Shemdoe.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miezi michache iliyopita, Jimbo langu la Ngara limepokea mafungu mbalimbali ya fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya aina mbalimbali kwenye vituo vya afya, shule za sekondari, na kwenye shule za misingi. Nawashukuru sana kwa kuweza kutupatia fedha sisi wananchi wa Jimbo la Ngara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utajikita kwa watumishi. Watumishi hasa Walimu pamoja na wale wa kada ya afya wana changamoto nyingi sana mtambuka ambazo wamekuwa wakiishi nazo kwa muda mrefu. Kuna malipo call allowance wanayotakiwa kulipwa watumishi wa kada ya afya, kwenye Jimbo langu la Ngara, kuna watumishi wana miaka nane mpaka kumi na zaidi hawajalipwa hii fedha inayoitwa call allowance, wanaishi kwenye mazingira magumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Walimu, kama ambavyo wenzangu wamechangia, kwenye Jimbo langu la Ngara, Walimu wana changamoto nyingi sana, Walimu wanadai kupandishwa madaraja, wanadai malimbikizo ya uhamisho pamoja na allowances za matibabu, hawajalipwa kwa muda mrefu. Kama kuna watu wako hoi, basi ni hawa watumishi na uhoi wenyewe unatofautiana. Kuna mtu yuko hoi anaumwa anameza Panadol, mwingine ni hoi yuko ICU na mwingine yuko kabisa kwenye vitu vingine. Hawa wako hoi, naombeni sana TAMISEMI wa-coordinate na watu wa utumishi ili Ngara tupate kibali cha kupandisha vyeo. Toka mwaka 2008 hatujapata kibali ambacho tumeshakiomba mpaka sasa. Kwa hiyo hawajapandishwa madaraja toka mwaka 2008, 2009, 2020 na sasa ni 2021. Napenda kuiomba TAMISEMI wa-coordinate na watu wa utumishi ili tuweze kupata vibali angalau kwa kuanzia kibali cha mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kitu kinaitwa Bodi ya Walimu kama kuna kitu kinaenda kutuvuruga Tanzania ni hii inaitwa Bodi ya Walimu. Walimu wana makato ya aina mbalimbali mpaka sasa kwenye mishahara yao. Sasa tupo hapa kuna kitu kinaendelea huko TAMISEMI, wanatengeneza Bodi ya Walimu na inakuja na sheria inayotaka walimu wawe wanakatwa fedha kila mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna jambo walimu hawataki kulisikia ni hili hapa la kuja na sheria inayotaka walimu wakatwe fedha na kila mwezi hela yao iondolewe. Kwanza mishahara yenyewe ni midogo, halafu tunataka tena kuwakata hela. Hilo jambo litaleta vurugu, halikubaliki walimu kwenye jimbo langu wamesema hawataki kusikia kitu kingine kipya kitakachokuwa na madhara ya kukata fedha zao kwenye mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu, hasa ya shule za sekondari na msingi; Jimbo langu la Ngara lina changamoto kubwa hasa katika upande wa matundu ya vyoo. Mathalani, shule za sekondari zina upungufu wa matundu 132, ukiangalia hapa maana yake wanafunzi 2,640 hawana mahali pakujisaidia. Ninaomba sana TAMISEMI watakapokuja wana-consolidate michango yetu basi Ngara watuongezee matundu ya vyoo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa nyumba za walimu, tuna upungufu wa nyumba za walimu 344. Maana yake ni kwamba walimu wenye familia ya watu watano, zaidi ya watu 1,720 wanaishi katika mazingira yasiyoeleweka eleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa upungufu wa walimu, tuna upungufu wa walimu 197; maana yake ni kwamba inapotokea fursa ya kuajiri walimu wapya kwa upande wa Jimbo la Ngara, wachukue walimu wawaambie waingie kwenye vyumba vya madarasa. Vyumba vya madarasa viwili vikijaa wafunge mlango halafu hao wote watuletee kwenye Jimbo la Ngara.

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa walimu 197 ni sawasawa na madarasa mawili yaliyojaa wlaimu. Ninaomba sana, ninawaomba TAMISEMI itakapotokea fursa ya kuajiri walimu wapya basi Ngara watuletee idadi ya walimu wanaolingana na madarasa mawili yaliyojaa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa afya sera ya afya inasema kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya. Nina upungufu wa vituo vya afya 17, nina upungufu wa zahanati 29; maana yake ni kwamba upungufu wa zahanati 29 unasababisha watu 72,000 wakose mahali pakwenda kupata huduma za afya. Ninaomba sana TAMISEMI watakapokuja ku-consolidate angalau Ngara waniongezee vituo vitatu vipya vya afya. Hizo ni zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa vituo vya afya, ninaomba sana kwasababu tuna upungufu wa vituo vya afya 17 ambapo watu 340,000 hawana mahali pauhakika pakwenda kupata huduma za afya kutokana na ukosefu wa vituo vya afya. Ninaomba angalau TAMISEMI watuongezee vituo vya afya angalau vitatu katika mwaka huu wa fedha ili kuweza kuondokana na changamoto za eneo hili la miundombinu ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa TARURA; kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kwenye michango ya nyuma, TARURA inahitaji ongezeko la bajeti, hili halina mjadala. Kwa upande wa Jimbo langu la Ngara, TARURA wamekuwa wakipewa ukomo wa bajeti unaolingana kwa miaka yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba kwa Jimbo langu la Ngara tuna madaraja, tuna makalavati 652 na fedha tunayopewa ni ya kutengeneza kalavati 15 kwa mwaka; maana yake ni kwamba tunahitaji miaka 43 kuweza kujenga makalavati ya Jimbo la Ngara, a good 43 years! Ina maana kwamba hili jambo halikubaliki, ninawaomba sana waweze kutu-consider. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara, napenda kukushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ngara ni miongoni mwa majimbo yaliyojaliwa na Mwenyezi Mungu kuwa na madini ya aina mbalimbali. Tuna madini ya manganese ambayo concentration yake kwenye jiwe ni asilimia 30 hadi asilimia 55. Tuna madini ya tin, concentration yake kwenye sampuli ya jiwe ni asilimia 50 mpaka asilimia 68. Tuna madini ya tungsten, concentration yake ni asilimia 65 kwenye jiwe. Tuna madini ya chuma, concentration yake kwenye sampuli ya jiwe ni asilimia 75. Mbali na madini hayo, Ngara tumejaliwa kuwa madani ya nickel, cobalt, palladium na platinum.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kujaliwa huko kuna tatizo kubwa sana la ukosefu wa takwimu za wingi wa madini hasa madini ya manganese, tin, tungsten pamoja na chuma. Tunakosa takwimu ambazo zinaweza kuwafanya wawekezaji kuja kuwekeza kwenye jimbo la Ngara ili tuweze kuchimba madini hayo na wananchi walionichagua waweze kupata ajira kutokana na madini haya. Wananchi wa Jimbo la Ngara tumechoka kuendelea kukalia madini, kijiji kiko juu ya mwamba ambao umejaa madini. Wakati madini hayo yanaweza kuchimbwa yakatoa ajira na nchi ikakusanya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kuishauri Wizara ya Madini kupitia Geological Survey of Tanzania waweze kufika kwenye Jimbo la Ngara waje kufanya utafiti kwenye maeneo yote haya niliyotaja yenye madini haya; waweze kwenda Bugarama, Kihinga, Mgaza na Ntanga wakafanye utafiti na watuletee takwimu za wingi wa madini haya kwa maana ya mtandao mzima wa mwamba wenye madini haya. Tukiweza kupata takwimu hizo, tuweze kupata wawekezaji waje kuwekeza kwenye Jimbo la Ngara na hatimaye wananchi waweze kupata ajira na madini hayo yaweze kutumika kuchangia kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, naomba pia niongelee suala local content pamoja na CSR. Kwa vile Jimbo la Ngara kuna mgodi mkubwa sana wa Kabanga Nickel ambao unakwenda kuanza hivi karibuni na kwa kuwa kwenye Jimbo letu la Ngara huu ni mgodi wetu wa kwanza mkubwa unaoenda kuanza, na kwa vile Halmashauri ya Wilaya ya Ngara haiungi mkono wale wanaosema fedha ibakie kwa Mzungu, sisi tunataka fedha tuletewe kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ngara, miradi yetu ya maendeleo tusimamie wenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwenye michango ya hapo leo asubuhi, nimesikia baadhi ya Waheshimiwa wanalalamika kwamba kipindi kingine unaweza ukaambiwa na Mzungu unataka nini, unataja shule mbili, anakujengea shule mbili kwa shilingi milioni mia kwa shule moja wakati zingejengwa kwa shilingi milioni 50, matokeo yake unakuta kwamba mpaka chenji yenu imebakia kwa Mzungu. Kusema kwamba hizi fedha zibakie kwa hao wawekezaji ni kuendeleza mawazo ya kikoloni na kuonesha kwamba sisi kama Taifa hatuwezi…

SPIKA: Mheshimiwa Ndaisaba hebu rudia hiyo pointi yako, Waheshimiwa Wabunge muwe mnawasikiliza Wabunge wanachoongea, hebu irudie vizuri Mheshimiwa. (Makofi/Kicheko)

MHE NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nasema hivi, suala la kusema kwamba fedha ibakie kwa Mzungu ni kuendeleza mawazo ya kikoloni kuonesha kwamba sisi hatuna uwezo wa kusimamia rasilimalia zetu, mipango yetu na kwamba ili tuweze kufanya maendeleo inabidi watu wengine waweze kutufanyia maendeleo jambo ambalo halikubaliki. Kwa minajili hiyo Mgodi wa Tembo Nickel utakapoanza kwenye Jimbo la Ngara naomba sana Wizara ya Madini ije itupatie mafunzo Halmashuari ya Wilaya ya Ngara hasa Madiwani na wananchi ili tuweze kusimamia fedha zetu sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunasema kwamba fedha ibakie kwa Mzungu, tunasema kwamba hata fedha tunayoletewa na Serikali Kuu kwenye halmashauri zetu hatuwezi kuzisimamia. Fedha inayotoka kwa Mzungu kama CSR na ile inayotoka Serikali Kuu haina utofauti, fedha ni fedha.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mmeona jinsi nilivyoshangaa, nani yuko right kati ya makofi yenu na maelezo haya? Mimi niko na Mheshimiwa Ndaisaba, malizia Mheshimiwa. (Makofi/Kicheko)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ngara tumejiandaa kunufaika na Mgodi wa Kabanga Nickel almaarufu kama Tembo Nickel. Wananchi na makundi mbalimbali ya wafanyabiashara tumejiandaa kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali kwenye mgodi huu. Huduma hizo ni pamoja na usafiri, ulinzi, kuuza bidhaa mbalimbali hasa mbogamboga, matunda na vyakula vya aina mbalimbali ambavyo vinahitajika mgodini.

Mheshimiwa Spika, kama Wizara ya Madini haiwezi kuja kuandaa wananchi ni ngumu sana kama mgodi unaanza mwaka huu kupanda parachichi likaota na tukaweza kuuza pale mgodini. Naomba Wizara ya Madini ije kwenye Jimbo la Ngara iandae wananchi ili tuweze kunufaika na Mgodi huu wa Kabanga Nickel ambao unakwenda kuanza hivi karibuni.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema mwanzoni, kwenye Jimbo la Ngara tuna madini mapya na mwenyewe nimeenda maabara kuhakikisha kwamba kweli haya mawe yana madini. Tuna madini ya tin, tungsten na manganese.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara ije Ngara kuwawezesha wachimbaji wadogo wadogo tuanze kuchimba madini hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, awali ya yote nianze kwa kukushukuru kwa kunichagua nikawa Mjumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo ambapo mwanzoni nilipoona jina langu lipo kule nilikuwa nina wasiwasi, lakini nilipofika kule kwenye Sheria Ndogo nikagundua kwamba kule ndiko ambako sheria zinazoongoza nchi kwenye grassroot/ kwenye Halmashauri zipo pale na mambo mengi yanayogusa wananchi yapo kule kwenye Sheria Ndogo, kwa unyenyekevu mkubwa sana nakushukuru sana kwa kunichagua nikawa Mjumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Spika, naomba mchango wangu niulekeze kwenye Kanuni za Sheria za Filamu na Michezo ya Kuigiza, naanziaa hapo. Taasisi ambazo zimekasimishwa madaraka ya kutunga sheria ndogo ndogo tunatarajia zifanye kazi hii kwa weledi mkubwa, lakini zifanye kazi hii katika namna ambayo hizi sheria ndogo zinazotungwa haziji kuharibu mambo na badala yake zinakuja kujenga.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kanuni hii ya Sheria za Filamu na Michezo ya Kuigiza imeweka masharti kwa taasisi ya Serikali ikiwemo Bunge, kuomba kibali cha kutaka kutengeneza filamu pale ambapo taasisi hiyo inahitaji kutengeneza filamu. Taasisi kama TANAPA, Taasisi za Elimu zinahitaji kutengeneza filamu kwa ajili ya shughuli mbalimbali kwa mfano Taasisi za Elimu zinahitaji kutengeneza filamu kwa ajili ya kufundishia; taasisi kama TANAPA wanahitaji kutengeneza filamu kwa ajili ya kuvutia watalii ili tuweze kuongeza vivutio vyetu NA tuweze kuvitangaza kupitia filamu.

Mheshimiwa Spika, lakini kanuni hii inataka taasisi za Serikali kuomba vibali kabla ya kutengeneza filamu, mbaya zaidi kanuni iliyotengenezwa inakinzana na sheria mama yenyewe ambayo sheria mama iliondoa hitaji hilo la kuomba vibali kwa taasisi za Serikali zinapotaka kutengeneza filamu. Niombe kanuni hii iweze kuondolewa/sharti hili liweze kuondolewa kwenye hii Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza.

Mheshimiwa Spika, kanuni ya 16 ya sheria hii imeorodhesha vitu ambavyo ni maudhui yanayokatazwa na sheria hii, matarajio yetu sisi nikiwemo na mimi mwenyewe ni kwamba muigizaji anapotaka kuigiza kwa mfano muigizaji anataka kuelezea madhara ya dawa za kulevya ni matarajio yangu kwamba tunamuona mtu yule anaishi maisha yake halisi kwenye jamii, baadaye tutamuona anaanza kutumia dawa za kulevya na baada ya hapo tutaona madhara ya dawa za kulevya; lakini sheria hii maudhui yaliyooneshwa inakataza yule mhusika wa filamu kuigiza kile kipengele cha kutumia dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, sasa kama inakataza kile kipengele muhimu katika uigizaji maana yake ni kwamba inauwa kabisa tasnia ya uigizaji na filamu nchini. Sio hapo tu imeenda hadi kwenye mavazi, hadi kwenye umalaya na kadhalika sisi tunatarajia mtu akiwa malaya tumuone anavyokuwa malaya, baadaye tumuone anavyopata magonjwa ikiwepo hayo ya zinaa, tuone madhara yake ili watu watakaokuwa wanatazama ile filamu yale maudhui waone lile jambo ni baya na baada ya hapo waweze kuliacha kwenye jamii, lakini kwenye kanuni ya 16 imekataza mambo yote hayo naomba kwa kweli hii kanuni na yenyewe ifanyiwe marekebisho.

Mheshimiwa Spika, lakini kanuni hii ya sheria za filamu na michezo ya kuigiza imeweka maombi ya vibali bila ya kutumia njia za kisasa za mtandao; fikiria muigizaji yuko Jimbo la Ngara aje kuomba kibali cha kutaka kutengeneza filamu yake hapa Dodoma ama Dar es Salaam; fikiria mtu ambaye yuko Sumbawanga kwa kweli jambo hili na lenyewe halipendezi kwa sababu katika karne hii ya kutumia mtandao tunatarajia kwamba maombi haya yarahisishwe na yafanyike kwa njia kielektroniki.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tunaomba eneo hilo na lenyewe liweze kuboreshwa lakini niende kwenye kanuni ya Bodi ya Kitaaluma ya Walimu yaani Tanzania Teachers Professional Board. Kama alivyosema Mwenyekiti wetu wa Kamati wakati anawasilisha, ni kweli kwamba wakati tunachambua sheria hizi walikuja wadau mbalimbali wakiwa wanalalamika kwamba hawakushirikishwa wakati wa kutengeneza kanuni hizi.

Mheshimiwa Spika, ili sheria iende kwa walaji na waweze kuikubali ni muhimu sana sheria hiyo iweze kuwashirikisha hivyo sheria hii ni kama vile inakosa uhalali kwa sababu walaji walilalamika kwamba hawajashirikishwa. Lakini ukifuatilia kwa mfano kanuni ya 8(6)cha Kanuni ya Bodi ya Kitaalama ya Walimu, imemtaja Mwenyekiti miongoni mwa watu wanaotakiwa kuweka sahihi kwenye kile cheti kinachomruhusu mwalimu aweze kufanya kazi ya ualimu.

Mheshimiwa Spika, huyu Mwenyekiti hajasemwa ni Mwenyekiti wa Kijiji, Kata, wa kitu gani kwa hiyo ukiangalia kwa ujumla sheria hii ina mapungufu makubwa ambayo yanahitaji kuboreshwa. Kanuni ya 8(2) ya sheria hii imetaja cheti kinachoitwa Ordinary Certificate of Secondary Education wakati cheti kama hiki ndani ya nchi hii hakipo cheti kilichopo ni Certificate of Secondary Education, sasa tunajiuliza hawa watu tuliowakasimisha madaraka ya kutunga sheria hawaangalii vitu vilivyopo?

Mheshimiwa Spika, hivyo hii kanuni ya walimu hii imelalamikiwa sana tunaomba ifanyiwe marekebisho, vitu vilivyokatazwa tunaona vinarudi.

Mheshimiwa Spika, naomba dakika mbili kuna mtu hakuwepo…

SPIKA: Haya malizia.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kuna kurejea kwa tozo za kero hapo nyuma Serikali iliyokuwepo ilikuwa imeshaanza kufuta tozo zote ambazo ni za kero, hebu fikiria Watanzania wanapokuwa wametoka kwenye kazi ngumu, wananchi wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanatakiwa waende wakapumzike, wengine wanakwenda kwenye kumbi za starehe wengine wanakwenda kwenye kumbi za sinema.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna hii kanuni za ada na tozo mbalimbali za Halmashauri zimeanza kuweka tozo kubwa kwenye maeneo haya ya starehe. Sisi tunapokuwa majumbani kwetu tunaangalia tv zilizoko majumbani kwetu lakini tukumbuke kuna watanzania wengi hawana tv eneo lao la kwenda kujidai mida ya jioni ni kwenye hizi kumbi za starehe pamoja na sinema. Ninaomba hili jambo liangaliwe ili tuache Watanzania wafurahie maisha hasa wanapokuwa wametoka kwenye kazi ngumu.

Mheshimiwa Spika, kuna tozo hizi zimesemwa bajaji shilingi 1,500 basi la abiria ambao lina siti 20 shilingi 1,500 hii ni Jiji la Mbeya wanataka kutoza vitu vya namna hii, wakati mwingine bajaji anaongea na mteja shilingi 1,000/buku tu anampeleka mteja kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. Hivyo vitu hivi visipoangaliwa vitaanza tena kurudisha zile kero ambazo kwa kweli tulishatoka huko na sasa hivi wananchi wanaishi maisha mazuri, hivyo hizi sheria ndogo ndogo zote ambazo zinaleta kero tusiweze kuzipitisha.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa unyenyekevu mkubwa kwanza kwa kuniongezea dakika Mwenyezi Mungu akubariki ninaunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Nitumie sekunde chache sana kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Kwa kuridhia na kutoa leseni ya kuchimba madini ya Nickel yaliyoko kwenye Jimbo la Ngara. Wananchi wa Ngara wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Rais, wanampenda; na siku akitua Ngara tutayabeba yale magari ya msafara anayokuja nayo Rais. Kwa kweli tunamshukuru sana Rais kwa kuweza kutoa leseni hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze kwenye mchango wangu na niende moja kwa moja kwenye mgongano wa masilahi. Wakati tunafanya uchambuzi, tuliletewa sheria kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) na kwenye sheria ile Kifungu cha 32(2) kinaruhusu Maafisa wa Serikali na wale waliopo kwenye ofisi hiyo ya Makamu wa Rais, (Mazingira) kuweza kushiriki kwenye zabuni za kufanya tathmini ya masuala ya mazingira (environmental impact assessment) pamoja na audit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutafakari na kuichambua kwa umakini ile sheria tuliyoletewa, tuligundua kwamba Mkurugenzi wa Taasisi ya Serikali ambaye ameajiriwa kama mtaalam wa kutoa huduma za mazingira, ana uwezo wa kushiriki kwenye zabuni, na kitakachotokea ni mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mkurugenzi wa Kampuni hiyo hiyo ama Taasisi ya Serikali imetangaza zabuni, halafu naye akaomba tender, halafu Mwenyekiti wa Kamati ya Manunuzi akamnyima tender bosi wake, kitakachotokea pale ni kwamba yule mtu atapangiwa kazi ya kufagia, consequence ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kama huyu mtumishi wa Serikali ameshiriki naye kuomba tender ambayo imetangazwa na Serikali, kitakachotokea pale, quality ya ile kazi inaweza kuwa jeopardized. Kwa sababu, kwa mujibu wa Sheria ile ya Mazingira, wataalam hawa wa Serikali wanaofanya EIA, wanatakiwa kwenda kuhakiki taarifa iliyoandikwa na mtu aliyepewa kazi ya kwenda kufanya EIA. Sasa kama tuna sheria inawaruhusu nao kwenda ku-compete na kuomba kazi hizo, hawawezi kusimamia vizuri kule wakati nao wanatakiwa kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitafakari sana eneo hili tukagundua kwamba wataalam hawa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira walioweka Kanuni hii, waliongozwa na uroho na ndiyo maana wakaweka Kanuni inayowa-favour wao wenyewe ili waweze kuomba kazi wanazozitangaza wao wenyewe na waweze kuzifanya wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba wewe na Serikali, kazi hizi tuwaachie private sector na twende tukafanye marekebisho ya kipengele hiki kuhakikisha kwamba tunaondoa kabisa mgongano wa masilahi kwenye shughuli zote zinazohusiana na masuala ya environmental impact assessment pamoja na environmental audit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunafanya uchambuzi, Mezani kwetu ilitua Sheria Ndogo kutoka Halmashauri ya Bumbuli. Sheria hii inahusu ada na ushuru mbalimbali wa mazao kwenye Halmashauri ya Bumbuli. Kanuni ya 9(8) inasema mtu yeyote haruhusiwi kubeba ama kununua mazao kama hana kibali na risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliitafakari sana hii sheria, tukagundua kwamba sisi Watanzania muda wote hatuna mahitaji ya kutosha. Ukiamua kununua kilo mbili za karanga, unakwenda dukani unachukua karanga zako unarudi nyumbani. Sasa Maafisa wa Serikali hasa wa Halmashauri wana uwezo wa kutumia vibaya vifungu hivi vya sheria na kuanza kuumiza wananchi. Katika hali ya kawaida, hakuna mwananchi anayeweza kupata kibali kwenda kununua mazao gunia moja, debe mbili au debe tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba kwa unyenyekevu mkubwa, Kanuni hii ifutwe kabisa, isipite kwa sababu Kanuni hizi tunapozipitisha ndizo zinakwenda kuleta kero kwa wananchi na matokeo yake wananchi wanaichukia Serikali yao, wanachukia viongozi wao kwa sababu ya hizi sheria tunazozipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye Sheria ya Kudhibiti Ombaomba ambayo wenzangu wameshaisema kidogo. Nami nijielekeze kwenye concept inaitwa anthropology. Huu ni utaratibu wa kusaidiana kama binadamu. Dunia nzima ombaomba wapo, sema wenzetu wame-advance na kuita Homeless, American Beggars, Tanzanian beggars, all are beggars. Halmashauri ya Wilaya ya Chunya wametengeneza Sheria ya Kudhibiti Ombaomba kabisa. Tena wameenda mbali, Mkurugenzi amkamate ombaomba ampeleke kwa RAS. Sasa tukajiuliza RAS ana utaratibu wa kupokea ombaomba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli hawa watu ni ombaomba au ni watu wenye uhitaji? Ifike mahali kama nchi tubadilishe baadhi ya terminology ambazo ndani yake zinaleta ambiguity. Kunaweza kukawa na tafsiri hasi kwenye baadhi ya maneno tunayoyatumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuomba Wizara husika ikiwezekana wapige marufuku kabisa hili neno ombaomba na badala yake tubadilishe tuseme ni watu wenye uhitaji. Kwa sababu watu hawa badala ya kusaidiwa, sisi tunaona ni ombaomba, sasa tunatunga sheria tuwakamate tuwarudishe walikotoka. Sheria hii ni ya kibaguzi na tunaomba isipite kabisa kwa sababu madhara yake ni kufanya wananchi waichukie Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wameshazungumza mambo mengi tuliyokutana nayo wakati tunachambua hizi sheria ndogo ndogo. Nikuhakikishie kwamba sheria inapotua kwenye Kamati yetu, tunaichambua neno kwa neno, mstari kwa mstari na tunakwenda mbali kuchambua maana halisi iliyopo kwenye vifungu vile tulivyoletewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria nyingi tulizozipokea kama ambavyo nimekuonyesha hapo, zina vipengele vya ovyo ovyo ambavyo vinaweza kutuchonganisha na wananchi na kufanya wananchi waweze kuichukia Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabisa Bunge lako Tukufu lisipitishe maeneo yote tuliyokwishaonesha kwamba vifungu hivi havifai, vitafanya wananchi waichukie Serikali. Lengo la sheria hizi ni kuchochea maendeleo na siyo kukusanya ushuru tu hata kama wananchi wana hali mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka mara ya mwisho kuchangia kwenye Bunge hili ilikuwa ni siku mbili kabla wewe Mwenyewe Mheshimiwa Naibu Spika hujagombea na tukakuchagua kuwa Naibu Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo nimeona ni budi niweze kusimama hapa nikupongeze wewe mwenyewe kwa ushindi mzito ulioupata pamoja na Spika wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hongera sana kwa ushindi mnono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na pongezi hizo, naomba pia niweze kuchukua fursa hii kwenye dakika zangu za kuchangia kuweza kumpongeza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutenga muda na kufika Mkoa wa Kagera siku chache zilizopita ambapo alitoa maelekezo mahususi yenye lengo la kuwasaidia wakulima wa kahawa kwenye Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa ambayo wakulima wamekuwa wakidhulumiwa sana hasa wakulima wa kahawa. Kulikuwa na utitiri wa tozo mbalimbali ambapo mkulima wa kahawa anatozwa tozo 47; na matokeo ya tozo hizi ni kwamba mkulima alikuwa hanufaiki kabisa na zao lake la kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika Kagera kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, akafuta tozo 42 kati ya 47 na kubakisha tozo tano tu. Hongereni sana Waziri Mkuu na Mheshimiwa Mama Samia. Wakulima wa Kahawa Mkoa wa Kagera na Tanzania kwa ujumla tunaahidi kuiunga mkono Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia, tunaipenda na tunaomba iendelee kutuhudumia wakulima wa kahawa na kuhakikisha kwamba wakulima tunaendelea kunufaika na zao letu la kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na kuondoa tozo 42 kati ya 47, Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelekezo mahsusi kwa Vyama vya Ushirika kuacha kwenda kuchukua mikopo ambapo mikopo ile mwisho wa siku inakwenda kulipwa na mkulima mwenyewe. Wakulima wa kahawa wanachokita, wanapoandaa mashamba yao, wanapopanda kahawa, zinakuja kutoa matunda baada ya miaka mitatu. Wakulima wanakuwa wamehenya kweli kweli, wanakuwa wameumia kweli kweli. Mkulima anachokitaka, anapovuna kahawa yake, aende kuiuza kwa bei nzuri. Naendelea kuipongeza Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia, imetujali sisi wakulima kwa kuondoa tozo hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na kuondoa tozo hizi ambazo zilikuwa zinawakandamiza wakulima, Serikali imeelekeza Vyama vya Ushirika viache kwenda kuchukua mikopo kwa lengo la kwamba mikopo hiyo ilipwe na mkulima ambaye anapolima kahawa yake wala hajui kwamba kuna mtu atakwenda kuchukua mkopo ili kahawa yake ndiyo ilipe ule mkopo. Maelekezo haya yametolewa, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu iendelee kusimama maelekezo haya kuhakikisha kwamba wakulima wetu hawarudi kule walikotoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwamba Vyama vya Msingi ndivyo viweze kusimamia uuzaji wa kahawa; na vyama vyote vya Ushirika…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba Serikali hii ni ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa nimeipokea na ndiyo maana nimeendelea kumpongeza Mama yetu tokea nianze kuchangia. Nakushukuru sana kwa taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nielekeze mchango wangu kwenye Fungu Na. 65 ambalo linahusu Mfuko wa kuwezesha vijana na hasa kwenye mchakato mzima wa kuwezesha vijana kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii kwa mwaka, vijana wanaohitimu Vyuo Vikuu…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa tuwe na utulivu kidogo ndani.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Najua ni kengele ya kwanza.

NAIBU SPIKA: Wewe endelea tu.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Vijana wanaohitimu Vyuo Vikuu kwa mwaka wengine wamesema ni 90,000 lakini wale wanaomaliza Degree peke yake ni 48,000 na matokeo yake ni kwamba namba yote hii inapomaliza Vyuo Vikuu inarudi mtaani bila ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona juhudi nzuri za Ofisi ya Waziri Mkuu za kuhakikisha kwamba vijana hawa wanapotoka Vyuo Vikuu wanapatiwa ajira. Nimeomna ushirikiano baina ya Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Vyuo Vikuu ambapo tumesomewa kwamba wahitimu zaidi ya 2,000 wameweza kupatiwa mafunzo mbalimbali ya ujasiliamali na hivyo kuwawezesha kuanzisha miradi mbalimbali ya kujiajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu ni pamoja na kutambua Makampuni ya Vijana na kushirikiana na PPRA na kusaidia makampuni haya kuyaunganisha na wazabuni wakubwa ili tender zinapokuwa zinatolewa vijana hawa na wenyewe waweze kunufaika na tender za nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Manunuzi ya Mwaka 2011 imeelekeza kwamba makundi maalum wakiwepo vijana, wanufaike na asilimia 30 ya fedha zote za zabuni, lakini katika uhalisia wake ni kwamba vijana wanaojua mambo haya au waliofahamishwa juu ya fursa hizi ni wachache sana na matokeo yake vijana wengi hawana ajira, tender za nchi hii zinaendelea kutolewa kwenye makampuni ya nje na mengine ya ndani makubwa, vijana wengi wameachwa pembeni kwenye utaratibu huu na kwenye mfumo huu wa zabuni za nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mfumo ukiwekwa vizuri na sheria hii ikasimamamiwa, tutawasaidia vijana wengi sana waweze kujiajiri kwenye mfumo wa tender, yaani zabuni na wengine wataweza kufanya shughuli za kandarasi. Sasa hivi tumewaachia vijana wako mtaani, wanashinda club house, wanaikosoa Serikali na kukosoa chama chetu na kusema maneno yanayohusiana na mambo ya kupingapinga, lakini zipo fursa za ku-drain vijana wengi tukawaingiza kwenye zabuni baada ya kuwatoa mitaani na tukawawezesha vijana wetu kujiajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa iliyopo ni utekelezaji wa sheria ya kutoa fursa kwenye makundi maalum nchi hii. Naomba kuishauri Serikali na hususan Ofisi ya Waziri Mkuu, iweke utaratibu mzuri wa kwenda kusimamia sheria zinazolinda maslahi ya makundi maalum ili kila tender inayotolewa nchi hii, kuwe na utaratibu wa tenderer kutoa taarifa ni kikundi gani amekihusisha kwenye zabuni yake na amekilipaje? Hii itahakikisha vijana wetu nchi hii wananufaika na zabuni zote zinatolewa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu iweke utaratibu maalum wa kukusanya taarifa na makampuni yote ya vijana kuhakikisha kwamba kila kampuni ya kijana iliyopo nchini hii inapata fursa hizi. Haya mambo hayafahamiki, vijana wetu hawanufaiki na hizi fursa, wapo kimya utadhani fursa hazipo, lakini zipo hazitangazwi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuwa mchangiaji wa kwanza kuanzisha shughuli hii asubuhi hii, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambae ameendelea kuonesha mapenzi makubwa kwa Watanzania kupitia kuachilia fedha ziende zikatekeleze miradi ya maendeleo. Wabunge watakubalina nami kwamba wao ni mashuhuda wa upendo mkubwa wa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan ambae anasukuma fedha nyingi kwenye Majimbo kwa ajiali ya kutatua changamoto nyingi za Watanzania. Nami na wananchi wangu wa Jimbo la Ngara tunamshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, juzi ameidhinisha 2,700,000,000 kwa ajili ya kwenda kujenga Chuo cha Ufundi - Ngara. Tunamshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hasssan na tunaendelea kumuunga mkono.

Mhehsimiwa Mwenyekiti, vilevile nimshukuru Waziri Mkuu, kwa kazi kubwa anayoifanya pia na kuwasilisha hotuba nzuri sana hapa Bungeni ambayo imejaa matumaini kwa Watanzania, kwa kweli ukisoma hotuba ile ya Waziri Mkuu inatuonesha inatupeleka kwenye Tanzania tunayoitaka. Ninamshukuru tena Waziri Mkuu na Waziri wa Kilimo kwa jambo lile la Kahawa, wananchi na wakulima wa Kagera na wale wa Wilaya ya Ngara kwa miaka zaidi ya 50 iliyopita tulikuwa hatujawahi kupata bei ya nzuri ya Kahawa. Katika msimu iliopita kwa mara ya kwanza tumeuza kilo moja shilingi 3,700 mpaka shilingi 2,000. Ni matarajio yetu kwamba msimu unaokuja Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa Kilimo wataendeleza hatua ambazo zilichukuliwa kwenye msimu uliopita ili wananchi wa Jimbo la Ngara na wale wa Mkoa wa Kagera tuendelee kufurahia matunda mazuri ya Serikali yetu kwa kuendelea kuuza Kahawa kwa bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielekeze sasa mchango wangu kwenye eneo la sekta ya madini. Katika hotuba ya Waziri Mkuu alielezea malengo na dira na mwelekeo wa sekta ya madini hapa nchini. Alielezea kwamba kwa upande wa makusanyo ambayo Wizara ya Madini ilikuwa imelenga kwenye mwaka wa fedha uliopita, walikuwa wamepanga kukusanya bilioni 479.51 na wakafanikiwa kukusanya bilioni 409.66 ambayo ni sawa na asilimia 85 ya target yote ambayo Wizara ilikuwa imejiwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumweleza Waziri Mkuu na Mawaziri wengine hasa Waziri wa Madini kwamba kuna mambo kadha wa kadha kwenye sekta ya madini ambayo yanakwamisha juhudi za Serikali ili kuweza kufikia makusanyo ambayo yanatarajiwa, yamkini pengine makusanyo yangefika mpaka trillioni moja endapo vitu ninavyokwenda kuvizungumza vingefanyiwa kazi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ambalo napenda kuchangia na naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu alichukulie kwa umuhimu wa aina yake ni eneo la kodi la mapato asilimia 30. Wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu, leseni wanazopewa ni zile leseni za kuwaruhusu kufanya utafiti na kuchimba madini kwa wakati mmoja, hii ina maana kwamba anachimba shimo hapa anakwenda anachimba shimo pale, fedha anazozipata hapa anazirudisha tena kwenye utafiti, TRA wao wanachokiangalia ni mchimbaji huyu kwenye akaunti yake zimeingia Bilioni ngapi, wanaomba nyaraka za viambatanisho, anapotoa nyaraka ambazo siyo risiti za EFD wanazi-reject na wana–subject kwenye kodi ya mapato ya asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi hiyo haipo, wachimbaji wadogo hawana na hawataipata na sana sana Serikali itakwenda kuwafilisi kupitia TRA, kwa sababu, shughuli zao zile ni za kusaga mawe, kuchimba mashimo, kusogeza vifusi, na kusomba maji. Shughuli zote zinafanywa na Watanzania wa chini ambao hata TIN Number hawana, hata line za simu kwa kuwa hawana vitambulisho vya NIDA wanatumia za ndugu zao. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba, ni watu ambao wako kwenye informal sector kuweza kupata risiti, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali katika eneo hili. TRA waachane na kodi ya asilimia 30 (Corporate Tax), waache kuwalazimisha wachimbaji wadogo kufunga mahesabu kwa sababu, hawawezi kufunga mahesabu kwa nature ya biashara zao. Naomba Serikali baada ya kukata mrahaba asilimia sita, baada ya kukata ada ya ukaguzi asilimia moja, baada ya kukata Service Levy, Serikali ikate asilimia moja kama kodi ya mapato kutoka kwenye mauzo ya dhahabu on point of sale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ni sawasawa na ule mchezo wa Biko au Bingo au ule mchezo wa Tatu Mzuka, kwamba, unapocheza Bahati Nasibu ukawa umeshinda pale, Serikali pale pale inachukua kodi yake.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndaisaba, naomba upokee Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Iddi Kassim.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa tu mchangiaji. Ukiacha Corporate Tax ambayo ni asilimia 30, sasa hivi TRA wanaenda wanazunguka, wanataka kuweka kodi nyingine asilimia mbili kumwongezea mchimbaji mdogo huyu ambaye hajawezeshwa kupewa mitaji na kupewa maeneo yenye utafiti, ahsante.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Ndaisaba unapokea Taarifa?

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea vizuri sana. Nakushukuru.

MWENYEKITI: Kengele yako ya kwanza imeshagongwa.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli muda wangu nimekuomba unilindie. Niongezee hata dakika tano tu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa endelea kuchangia, kengele ya pili itapiga sasa hivi.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Sasa nielekee eneo la pili la VAT. TRA wameendelea kuwabana dealers wote ambao wanafanya biashara ya dhahabu. Wanawataka hawa dealers waweze kulipa VAT kwenye dhahabu wanazonunua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamaanisha kwamba, dealer akiweza kununua dhahabu ya shilingi milioni 100, akishai-subject kwenye VAT anatakiwa kwenda kuuza ile dhahabu shilingi milioni 118. Hii fedha haipo kwa sababu dhahabu, inanunuliwa kwa thamani ya bei ya Soko la Dunia. Hii inamaanisha kwamba, dhahabu inayonunuliwa Tanzania kwa mfumo huo wa VAT, haiuziki mahali popote pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwaambia TRA, hii fedha kwa dealers haipo na wale dealers wanaowasumbua kule Kahama, Tanga na maeneo mengine kwamba walipe VAT asilimia 18, hawataipata na matokeo yake ni kwamba wachimbaji na dealers wote wataendelea kutorosha dhahabu hapa nchini. Kwa sababu ukinunua dhahabu kwa utaratibu ulivyo hapa Tanzania, huwezi kuiuza mahali popote pale duniani. Naomba niishauri Serikali na TRA, waachane na mambo ya VAT kwenye dhahabu. Warudi kwenye utaratibu ule ambao nimesema wa nipe nikupe, ama nilipe nisepe. Tukutane sokoni, wachukue asilimia moja, iwe inawatosha na Serikali wataona mapato yanavyoongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ni eneo la kuchimba madini kwenye hifadhi. Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, alishaeleza kwamba, tembo na wanyama wengine huko porini hawali madini. Ukienda kwa mfano kwenye Game Reserve ya Kigosi, mle utakutana na sungura na nyoka tu, hata swala hakuna, wala simba hakuna, lakini pale kuna madini ya dhahabu. STAMICO wamepewa leseni wanatakiwa wachimbe madini yale, lakini ukienda TANAPA ni wagumu utafikiri ukipeleka grader mle linamaliza miti yote linaifyeka wakati unachimba kwenye kaeneo kadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda muafaka sasa, naishauri Serikali watengeneze mkakati, watengeneze task force, watengeneze Mwongozo ili uweze kuja na mbinu nzuri za kuweza kuchimba madini kwenye hifadhi, hata yale madini ya Emerald kule Mayoka kwenye Hifadhi ya Manyara, madini yale yachimbwe yaweze kufaidisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia kwenye hotuba ya Waziri. Siku ya leo nitazungumzia Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, na nitazungumzia narrative na mkanganyiko uliopo kwenye eneo la maadili, umasikini, uzalendo na utajiri katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikiona mtumishi yeyote wa umma anapotajirika, anapomiliki gari, anapomiliki nyumba, umbea unaanza kwenye maeneo mbalimbali ya kazi. Inafika mahali baadhi ya viongozi, hata Waziri akienda nje ya nchi, akikutana na wawekezaji wakimpenda yule Waziri kwa utaalamu wake na uwezo wake alionao wakataka kuja kuwekeza nchini, hata kama wanataka washirikiane naye, yule Waziri anaruka maili 100. Anaogopa, anajiuliza, hii fedha nikiipata kwa kuwekeza na hawa watu, nitaiweka wapi? Ni kwa sababu kwenye Taifa letu kumekuwa na mkanganyiko kati ya hayo mambo matatu mpaka manne.

Mheshimiwa Spika, wale watu wa Tume ya Maadili ya Utumishi wa Umma, wame-focus mara nyingi kwenye kuangalia properties na kwenye fedha za watu, wakichukulia hicho kama kigezo kikuu cha kujua kwamba huyu ni mzalendo ama sio mzalendo. Sijui hiyo narrative imetengenezwa kuanzia mwaka gani? Inafika mahali mtu kuwa na mali, kuwa na utajiri anakuwa na msongo wa mawazo, anawaza atauweka wapi.

Mheshimiwa Spika, Taifa letu katika mchakato wa maendeleo na makuzi ya Watanzania tunapopeleka watoto shuleni, wanakwenda kusoma kuanzia Chekechea mpaka Vyuo Vikuu. Wanasoma, wanamaliza degree zao, wanakuwa na kipindi kile cha kuhangaika kutafuta ajira. Kipindi kile vijana wengi wanakuwa wametawaliwa na mawazo ya ku- enterprise, wanakuwa na startups nyingi sana. Asilimia 99 ya startups nyingi zinafia pale kwa sababu nyingi zinakosa mitaji ya kuziwezesha ili ziweze kukua. Sasa wale Watanzania wachache wanaobahatika, labda ataajiriwa TANESCO, Wizara ya Madini, au eneo lingine, ile knowledge aliyoipata shuleni inamsaidia kupata ajira kwenye ile taasisi ya umma.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa ameingia kwenye taasisi ya umma, atafanya kazi miaka mitano mpaka 10, na pale ataweza kupata uzoefu wa kutosha. Eneo sahihi ambalo binadamu yeyote anaweza akawekeza ni eneo lile ambalo amelifanya kazi na amelisomea. Sasa Watanzania kwa hizi sheria zetu tulizoziweka za Tume za Maadili ya Viongozi wa Utumishi wa Umma, wanapoanza kuwekeza siku ile ile tu amejenga kakibanda, umbea unaanza. Ataandikwa kila sehemu, atashtakiwa kwa bosi.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri amejitihadi basi kwenye zile fomu zetu tunazozijaza kila mwaka za maadili ya viongozi, awe ameandika nina nyumba mbili, nina viwanja viwili, basi nimenunua na Subaru. Sasa figisu zitakazoanzia hapo, pamoja na ku-disclose ile, pamoja na ku-declare kwamba mimi pamoja na kwamba ni mtumishi wa TANESCO ninamiliki hiki na hiki na hiki kinachofanana na yale ninayoyafanya. Bado figisu ni nyingi, ni nyingi tena huyo ndio asahau kabisa hata kuja kupandishwa cheo. Kwa sababu ataonekana sio mzalendo, ataoneka huyu mtu hana maadili, ni mwizi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine tunataka Taifa letu liendelee, tunataka Watanzania wawekeze, tunataka Watanzania wawe na mali, tunataka makampuni ya Watanzania, tunataka tutoze kodi. Sasa hii confusion mimi huwa najiuliza, ni lazima ifike mahali kama Taifa tuweke mipaka ya definition ya conflict ya interest. Mwisho wa siku
tunajikuta sheria tunazoziweka kama Taifa zinakuja kuwabana Watanzania na watu wanashindwa kuwekeza kwenye Taifa lao.

Mheshimiwa Spika, nimeona hii Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma wamekwenda mashuleni, wanaanzisha club za wanafunzi, wamekwenda huko kwenye sekondari na shule za misingi, sijui wanawafundisha vitu gani kule. Maana unaweza ukakuta confusion ya narrative tuliyoanza nayo kwenye enzi zile pengine ni wakati wa ujamaa bado wanaiendeleza. Mimi ningejua kama wanakwenda kwenye ile shule ambako kuna mwanangu Ndairagije na Irakoze ningewaondoa pale ningewapeleka shule nyingine. Wasiwapelekee confusion hiyo.

Mheshimiwa Spika, matarajio yangu ni kwamba hawa watu wanavyofundisha maadili ya umma, basi wafundishe na Watanzania kujifunza kuwa na kiu ya kuwekeza, kutunza mali, ku-enterprise ili Taifa letu na sisi tuwe na mabilionea ambao ndani ya Afrika watasikika na ndani ya ulimwengu watasikika wanaotoka Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kama kweli tunaenda kuwapitishia bajeti na wameshaanza kazi ya kwenda mashuleni kwenye sekondari na shule za msingi kufundisha watoto wetu, naomba kabisa waende watengeneza mtaala mzuri unaochanganya maadili, uzalendo na utajiri. Isifike mahali kwenye Taifa letu mtu akiwa na hela kidogo anajiuliza Mungu wangu, nitazificha wapi?

Mheshimiwa Spika, hawa watu wanapokuja kwako, siku wakigundua kuna ka-issue ama labda kuna kiwanja kimoja ulikisahau, yaani wanakuja kama Polisi, as if gereza liko mlangoni kwako, kesho wanakufunga. Nilitarajia hawa wenzetu wawe facilitative, yaani wawe engaging, waende kuwa-engage Watanzania, umepataje hii? Okay ulipata vizuri, endelea kuwekeza na vitu vya namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, sasa imefika mahali kwenye Taifa letu kwa kweli Watanzania wengi wanaishi kwa uoga, wale walioko kwenye Ofisi za Serikali ni waoga, hata Mawaziri wenyewe. Mimi nilitarajia kwenye Taifa letu tuwe na Mawaziri wanamiliki hata ndege, sasa sijawahi kusikia hata Waziri mmoja hapa anamiliki ndege. Ni waoga! Nilitarajia kwamba kwenye Taifa letu tuwe na Mawaziri ambao akienda nje kweli ametumwa na Serikali kwenda kufanya kazi hii na hii; pia ni expert kwenye eneo lile, watu wanapenda kufanya nao partnership, joint venture, lakini wote ni waoga. Sasa matokeo yake ni kwamba tunajinyima fursa. Kama mtu anataka kufanya partnership, sheria zetu zinatubana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba hii ofisi ya masuala ya Utumishi na Utawala Bora waende waangalie kwa kina haya masuala ya maadili, uzalendo, umaskini na utajiri. Waangalie confusion inatoka wapi? Watusaidie huko mashuleni wanakokwenda kuwafundisha watoto wetu masuala ya uzalendo, wakajifunze masuala ya kuwekeza, masuala ya kuweka akiba, masuala ya kutunza; yaani wawe na kiu ya kuwa matajiri. Hii narrative ya kuonesha kwamba mtu ukiwa na mali ni fisadi; yule ni fisadi yule, yule ni mwizi, ona sasa ameanza kuwa na kitambi, mwizi yule! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kote Tanzania, vijiweni wapi, mtu yeyote, tena baadaye wanavuka wanasema, aah, yule ni Freemason. Kwa hiyo, tumekuwa na narrative ambayo kwa namna moja inaturudisha nyuma. Kwa unyenyekevu mkubwa, nimalizie kwa kusema kuwa, naomba watu wa Utumishi na Utawala Bora watutengenezee mtaala unaohamasisha utajiri ndani yake.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)