Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Abubakar Damian Asenga (21 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nami namshukuru Mwenyezi Mungu, Mheshimiwa Rais, Chama changu cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Kilombero kwa kunipa imani ya mimi mtoto wa fundi charahani mwenye nywele za kipilipili leo kusimama hapa kuwawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu ya dhati kaka yangu Mheshimiwa Polepole atanisaidia kufikisha shukrani zangu zote kwa chama kwamba sisi vijana tunawashukuru sana. Sisi vijana wadogo ambao tumepata nafasi ya kuingia katika Bunge hili tuna imani kubwa na ma- senior mliokuwepo humu mtatusaidia sana kutufundisha na kutuelekeza bila kutuacha tuharibikiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Wabunge wenzangu wengine wamechangia, nami nitumie fursa hii kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Kwanza, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani yake kwa vijana na katika maendeleo ya nchi yetu. Nitachangia katika sekta mbili au tatu, ya kwanza miundombinu ambayo ameizungumzia katika ukurasa wa 26.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 mimi nilikuwa mgombea wa Ubunge wa Chama cha Mapinduzi japokuwa sikutangazwa, Mheshimiwa Rais alifika jimboni kwetu, tulimuomba ujenzi wa barabara ya lami ya Ifakara – Kidatu kwa kiwango cha lami. Barabara hii haikuwapo kwenye Ilani lakini kwa mapenzi yake Mheshimiwa Rais aliahidi ataijenga na akaleta mkandarasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba wasaidizi wa Mheshimiwa Rais kuifuatilia barabara hii kwa ukaribu. Namshukuru sana Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Eng. Chamuriho alifika ameona changamoto za Mhandisi Mshauri (consultant) ambaye amekuwa aki-delay katika mambo ya GN na designing ili ahadi hii ya Mheshimiwa Rais iweze kutimilika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jambo hilohilo kwa kuongezea kidogo ni kwamba katika swali langu la msingi Mheshimiwa Waziri amejibu hapa kwamba barabara hii itakamilika Oktoba 2021. Sisi ambao tuko site kule ukitazama unaona muda huu ni mfupi sana. Kwa hiyo, naomba Wizara ifuatilie kwa makini barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni katika elimu. Mheshimiwa Rais akituhutubia hapa Bungeni aliahidi jambo la msingi kwa dada zetu, wasichana wa nchi hii kwamba atajenga sekondari za watoto wa kike kila mkoa. Naomba Wizara husika iliharakishe jambo hili lifanyike kwa wakati. Mkoa wetu wa Morogoro, Jimbo la Kilombero liko katikati ya Mkoa mzima. Pendekezo langu Wizara itakapojenga shule hizi ijenge katikati ya Mkoa ili kutoa nafasi kwa majimbo na wilaya zote kupeleka watoto pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili katika elimu, mjadala umekuwa mwingi sana hapa kuhusu suala la elimu ya chuo kikuu. Mheshimiwa Rais amesema katika hotuba yake ukurasa wa 33 mabilioni ambayo Serikali inatoa kwa mikopo ya elimu ya chuo kikuu. Pendekezo langu ni kwamba vile vyuo vya umma, mathalani University of Dar-Es-Salaam, Chuo Kikuu cha Dodoma, Serikali inalipa mfagizi, dereva mpaka anaepeleka karatasi pale, kwa nini tusifikie hatua ya kusema kwamba vyuo vya umma wanafunzi wasilipe ada kwa sababu Serikali inapeleka pale kila kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na mjadala huu wa mikopo, Bodi ya Mikopo, asilimia za kukatwa kuja kulipa ni kubwa, anapata huyu huyu hapati, lakini kwa sababu Serikali inapeleka huduma zote katika vyuo vya umma kwa kuanzia nilikuwa nashauri tuanze kulifikiria hilo. Mheshimiwa Rais amefanya vizuri sana katika elimu bure lakini tunakokwenda tufikirie vyuo vya umma ambavyo Serikali inahudumia kila kitu kwa nini mtoto wa Kitanzania asiende kusikiliza lecture akapata ufahamu? Kuwe na mjadala baadaye ama anatokea nyumbani ama anatokea wapi lakini afike apate nafasi ya kusoma chuo kikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na mjadala hapa kuhusu kazi nzuri ambazo Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli amefanya. Mimi kubwa kuliko yote ni suala la kunifanya nijiamini kama Mtanzania. Mimi kama kijana wa Chama cha Mapinduzi nimezunguka katika nchi za Afrika na tulikuwa na mafunzo ya vijana wa Afrika, hasa Afrika ya Mashariki, kuna nchi hapa walikuwa wanajisifia na Marais wao, leo sisi tukienda tunaheshimika kwa Rais wetu, ndiyo salamu yetu ya kwanza. Kubwa kuliko yote ni hilo Rais amenifanya mimi najiamini kila sehemu na kila wakati amekuwa akirudia kusema Watanzania tuwe makini tunaweza, Tanzania ni tajiri, ile imani inatufanya tunashinda vita. Hilo ni kubwa kuliko yote na ndiyo maana linakuza mjadala hapa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani kwa kukumbukwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Ummy na Manaibu Mawaziri wake wote kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya na tunaendelea kuwashukuru sana kwa mchango wao kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe taarifa kuhusiana na wananchi wangu wa Jimbo la Kilombero ambapo jana kuna mvua zilinyesha na Mto wetu Lumemo ulijaa maji na maji mengine yakamwagwa kwenda kwa wananchi. Namshukuru Mheshimiwa Jenista kwa ushauri na msaada anaoendelea kutupatia kukabiliana na hali hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, michango mingi tumetoa hapa na michango mingi tunayotoa katika Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, inataka kutumia tu pesa. Nina maoni kwa Mheshimiwa Waziri na Wizara waangalie vipaumbele vya kuwekeza kwenye miradi mikakati ya kuzalisha mapato ya halmashauri. Watafute fedha katika bajeti yao wawekeze katika halmashauri ambazo zimeandika maandiko, zime-qualify, zina Hati Safi; kama Halmashauri ya Mji wa Ifakara wanasema tukiwekeza bilioni tano katika soko baada ya miaka miwili, mitatu zile fedha zitarudishwa kwa sababu Mji wa Ifaraka una biashara kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba tunazungumzia mahitaji lakini wazo langu la kwanza la msingi nataka kuwaomba muwekeze. Kwa mfano, sisi tuna andiko letu kuhusu soko la Ifakara. Soko la Ifakara pale mjini mvua ikinyesha ni balaa tupu na linakusanya millions of money kwa siku. Kwa hiyo, pamoja na kwamba tunataka zahanati, hospitali na kadhalika lakini pia wanaweza kuweka vipaumbele katika kuchangia miradi mikakati kama vile stendi, soko na kadha wa kadha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, Mji wetu wa Ifakara una mitaa 33, nimeona kwenye hotuba Mheshimiwa Waziri ameitaja ni zaidi ya mwaka mmoja mpaka sasa hivi hakuna Mtendaji wa Mtaa hata mmoja. Nimekaa na Wenyeviti wa Mitaa, barua imeandikwa na mimi nimekumbushia. Sasa Mheshimiwa Waziri kwa kweli mitaa 33 hauna Mtendaji wa Mtaa hata mmoja zaidi ya mwaka mmoja, Wenyeviti wanafanya kazi wenyewe, kwa kweli ni jambo ambalo linakarahisha. Tunaomba utusaidie na ile barua nitakuletea nakala unisaidie pamoja hizo posho za Wenyeviti wa Mitaa nazo wanalalamika sana kwamba zinachelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali kwa kubadilisha kanuni ya mikopo hii ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Sasa tumeambiwa watu watano, mwenye ulemavu mmoja anaweza kukopeshwa, hii ilikuwa changamoto kubwa sana kwa upende wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nalotaka kuchangia ni kuhusu TARURA. Kwa mfano, Jimbo langu la Kilombero ni wakulima wa mpunga na miwa, barabara zetu zote ili tuzimalize lazima tuchonge, tuweke kifusi, tushindilie. Zamani halmashauri yetu ilikuwa na vifaa vya kufanyia kazi hizo, kwa sababu watu wa TARURA ni ma-engineer, kwa nini Wizara msione uwezekano wa kununua vifaa vinne tu wanaseme ma-engineer, wakivipata katika halmashauri na wilayani hata dharura za ukarabati wa barabara zikitokea watafanya. Kwa mfano, Jimbo la Kilombero tuna milima ina vifusi kibao mpaka wilaya nyingine zinakuja kuchukua vifusi kutoka kwetu. Tupate grader, shindilia (roller), excavator, tipper; vifaa vinne tukipata kama halmashauri mwaka mzima tutaweza kutengeneza barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba TARURA, najua imepata bajeti ndogo sana, kwa mfano kwetu sisi kuna shilingi milioni 454 haiwezi kufanya kazi ya jimbo zima. Pamoja na kuongezewa bajeti lakini tungewekeza hizo fedha, kwa mfano, tukitengewa one billion tukapewa grader na excavator tutatafuta hata tipper zitachukua kifusi zitakwenda kumwagia kwenye barabara za wananchi mwaka mzima tunafanya hiyo kazi, Mbunge unapewa fedha za Jimbo unaweza kununua mafuta ukaweka kwenye grader ukaenda ukachonga, ukaweka kwenye tipper ukaenda kumwaga kifusi wananchi wakaendelea kupata huduma za barabara. (Makofi)

Mji wa Ifaraka unakua kwa kasi sana kiasi kwamba Jumamosi na Jumapili benki hazifungwi. Tunaomba hawa TARURA watuwekee taa za barabarani, zile lami za Ifakara Mjini zina mashimo, tuongezewe lami kwa mfano barabara za Posta kwenda Hospitali ya St. Francis, CCM zamani kwenda kwa Salewa, naomba tuweze kuwekewa lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo kwenye TARURA, tunaishukuru Serikali tunajengewa na TANROADS barabara ya Kidatu kwenda Ifakara. Katikati ya barabara hizi kuna Stendi Kuu kwa mfano Mwaya, Kidatu na Ifaraka Mjini, barabara zile za kuunganisha kutoka barabara kubwa kwenda kwenye stendi zile au masoko ni za TARURA. Kwa hiyo, kwa sababu kuna mradi mkubwa lami wa kilometa 66.9 ambao utatuunganisha na Mkoa wa Morogoro, TARURA waunganishe stendi na hiyo barabara kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme jambo moja kubwa sana tunaomba Waziri atusaidie na hapa kweli nitamshika kidogo ushungi, ni kuhusu mgawanyo wa mali katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara na Halmashauri ya Mji wa Mlimba. Sisi ni Wilaya ya Kilombero, tuna Jimbo la Mlimba na Jimbo la Kilombero. Jimbo la Kilombero lina Halmashauri ya Mji wa Ifakara na Jimbo la Mlimba lina Halmshauri ya Mji wa Mlimba.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali paligawanywa mali Kata 9 za Mji wa Ifakara na Kata 26 za Jimbo la Kilombero. Baadaye Mheshimiwa Rais akatengua mgawanyo huo akaiongezea Halmashauri ya Mji wa Ifakara Kata 10 na Mlimba akaipunguzia ikabaki na Kata 16. Sasa mgawanyo ulifanyika wakati Halmashauri ya Mji wa Ifakara ina Kata 9, Makao Makuu ya Wilaya yote yale ya Halmashauri ya Ifakara ndiyo yalikuwa Makao Makuu ya Wilaya yana nyumba za Serikali, nyumba za taasisi, nyumba ya Mkuu wa Wilaya na ofisi zote za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimelisema mara kadhaa hili tunaomba zile nyumba za Serikali ambazo ziko Ifakara zitumiwe na Halmashauri ya Mji wa Ifakara kwa sababu Halmashauri ya Mlimba ni mpya imeanza kujenga kila kitu na juzi Serikali imepeleka one billion kujenga makao makuu ya halmashauri mpya. Sasa hapa Halmashauri ya Mji wa Ifakara inabidi tuanze kuomba upya fedha Serikalini tujenge tena nyumba za Serikali na za Wakuu wa Idara. Hivi Mheshimiwa Waziri navyozungumza TAKUKURU wamepangishiwa nyumba halmashauri, Mbunge nimetafuta ofisi ya vyumba viwili naambiwa nyumba zote zinamilikiwa na Halmashauri ya Mlimba wakati zipo Halmashauri ya Ifakara, imebidi nimuombe Mkuu wa Wilaya kanimegea kichumba ndiyo ofisi ya Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nachokiomba chonde chonde kwa sababu mnapeleka fedha Mlimba, basi hii Halmashauri ya Mji wa Ifakara iweze kutazamwa vizuri na ipate hizi nyumba zote, zibadilishwe au zifanyiwe hata tathmini ikipatikana kama ni shilingi bilioni 2, 3, Halmashauri ya Mlimba wapewe fedha hizo sisi tupewe zile nyumba ziendelee kutumika kwa sababu sasa hivi zina popo na zimekuwa mapori wakati huo Mkurugenzi wa Ifaraka hana nyumba; nyumba kagaiwa Halmashauri ya Mlimba ambayo ni kilometa 20 kutoka Ifakara. Hii ni Serikali moja lazima kwa kweli tujipange pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la msingi ambalo naomba kuchangia ni michango ya elimu ya madawati na viti. Kule tunagombana na wananchi kwa sababu ukienda wana-play video ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli amemwita Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Elimu kawafokea Ikulu hataki michango ya shule. Tena ana-play kabisa anasema Mbunge wewe wa CCM umekuja, angalia Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli huyu, apumzike tu kwa amani, wanalalamika wanachangishwa wapeleke viti na meza wakati wamemsikia Mheshimiwa Rais anasema hataki michango na mwenye mchango apeleke kwa Mkurugenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wangu pamoja na kwamba hawana sekondari na wanataka sekondari, wanasema walau hii michango ingekuja wakati tunavuna mpunga sio Januari na Februari tunaenda kulima tunachangishwa tunaambiwa Sh.50,000, Sh.60,000 na lazima uje na kiti na meza. Mheshimiwa Waziri amesema atanunua madawati, atatusaidia madarasa, katika uongozi wake akiweza kutatua changamoto hii ya michango atakuwa ametusaidia kiasi kikubwa sana. Naomba utoke ufafanuzi wananchi wanaruhusiwa kuchangia namna gani? Kama Serikali inasimamia ile elimu bila malipo tuambiwe wazi kwa sababu kuna mkanganyiko. Maelekezo ya Serikali yanatoka kwamba Februari ikifika wanafunzi wote waingine form one, Mkuu wa Wilaya hana bajeti, Mkuu wa Mkoa hana bajeti, anarudi kwa Wenyeviti wa Vijiji anaenda kuomba michango ambapo mwanakijiji mmoja akitoa anataka na wenzake wote watoe hata kama ana uwezo ama hana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo kuhusu afya. Sisi Ifakara tuna hospitali ya St. Francis, ni hospitali ya Mission, Serikali itatuchukua muda mrefu sana hata kama tunajenga hospitali yetu kuifikia hospitali hii. Hospitali hii ina gharama kubwa, inahudumia Jimbo la Mlimba, Ulanga, Malinyi, Kilombero na wakati mwingine mpaka Mikumi, zamani walikuwa wanapewa OC shilingi milioni 4 au 5, lakini sasa hivi imeshuka mpaka Sh.100,000. Umeme wanatumia shilingi milioni 10 kwa mwezi hawajapunguziwa. Tunaomba Serikali muiangalie hospitali ya St. Francis ili iweze kupunguza gharama wakati tunajenga hospitali yetu ya Jimbo. Jimbo letu lina Kata 19, tuna vituo vitatu vya afya, hivi navyozungumza Kituo cha Mang’ula wodi ya kina mama bado ina changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu spika, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ili na mimi nichangie bajeti yetu. Nami kama walivyosema Wabunge wenzangu mara kadhaa, napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na wasaidizi wake wote kwa kutuletea bajeti ya namna yake ambavyo kama Waheshimiwa Wabunge wameshasema mara kadhaa hapa mazuri ya bajeti hiyo nami nirudie yale ambayo wana Kilombero na wananchi wa Morogoro wanayashukuru na kuyapongeza. Mathalani suala la fedha za TARURA, milioni 500 kila Jimbo, Bima ya Afya kwa wote, mazingira mazuri ya biashara na kuwekeza katika kukuza thamani ya mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli ni bajeti ya namna yake na Mheshimiwa Waziri kaka yetu Mwigulu anathibitisha ubora wa watu ambao wanapenda timu ya yanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Pamoja na pongezi hizo nina mambo kama mawili ama matatu ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala zuri sana linalohusu posho kwa Waheshimiwa Madiwani tunalishukuru na tunalipongeza jambo hili. Lakini kama sisi tumesema Waheshimiwa Madiwani ni Wabunge wenzetu kule kwenye halmashauri, naishauri na kuiomba Serikali huko mbele tunakokwenda kuwe na utaratibu maalum wa vyombo vya usafiri kwa madiwani. Vyombo vya usafiri ambavyo vitawekewa utaratibu kama tulivyowekewa Wabunge mkopo wa magari tunaweza kufikiria pia Waheshimiwa Madiwani wakawekewa mkopo kama wa lazima hivi usiokuwa na riba kubwa wa kupata walau pikipiki nzuri za kisasa za kuwasaidia Waheshimiwa Madiwani kufanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa kuwa Halmashauri imeondolewa mzigo wa posho sasa hivi mambo ya simu na nini kule kwenye halmashauri wanaweza wakayaangalia. Lakini pendekezo langu; Mheshimiwa Waziri ukweli ni kwamba kutokana na changamoto za baadhi ya majimbo Madiwani wakati mwingine wanateseka sana kwenye usafiri. Wasipopanda gari la Mbunge watadoea doea gari za halmashauri, lakini wakiwa na pikipiki zao zitawasaidia kufika kwenye vikao kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili mimi nina jambo mahsusi kwa Mheshimiwa Waziri, hasa la barabara yangu ya Ifakara Kidatu, na hapa nataka niseme kidogo, naona ukishika kalamu Mheshimiwa Waziri, mimi nafarijika sana. Sisi tunajenga barabara kilometa 66.9 ya lami, mwaka wa nne tunajenga. Yaani kila siku nikisimama hapa nasema mpaka nimeenda nimekaa chini kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina changamoto nyingi, na hasa inauma kwa sababu unakuta wataalamu wa ujenzi wa barabara hii wanalalamika lakini wanakwambia Mbunge hii naongea mimi na wewe. Sasa barabara yetu Mheshimiwa Waziri imesainiwa na Wizara yako, na juzi tulikuwa na kikao na Wizara ya Fedha pale. Nataka kushukuru kwa dhati Katibu Mkuu wa Ujenzi na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha kaka Emmanuel Tutuba kwa kweli ni msikivu, na kikao cha juzi kimeanza kuleta matumaini kwamba kuna changamoto kwa kweli watazitatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kikao chetu cha mkoa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa Waheshimiwa Wabunge wote wa Mkoa wa Morogoro katika mambo ambayo tuliambiwa tunatakiwa kupata elimu ya kuyasemea mojawapo ni barabara hii; na kwenye kikao kile wataalamu wa ujenzi bila kutaka kuwataja hapa walisema changamoto; kuwa ni mvutano wa Mhandisi mjenzi na mshauri. Na wakasema kwamba mhandisi mshauri akimaliza muda wake aende, kwa sababu barabara ina fadhiliwa na European Union mkandarasi mshauri ameshachukua bilioni tisa mpaka sasa tunajenga kilometa 66.9 ameshachukua bilioni tisa mpaka sasa hivi barabara inasuasua. Mheshimiwa Waziri jambo hili liko kwako mkataba wa barabara ile ya ujenzi ya Ifakara Kidatu umesainiwa na Wizara ya Fedha. Sasa nimejaribu kumuelewesha Mheshimiwa Katibu Mkuu na nimeona respond yake kwamba atafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza na wewe European Union wameshaanza kusita kutoa fedha za mshauri, Serikali yako kwenye bajeti hii inatakiwa imlipe 1.4 Euro milioni karibu bilioni 4.6 za kumuongezea mkataba mkandarasi ambaye anamaliza mkataba wake Juni. Hii bilioni 4.6 wataalamu wale ambao wanatuambia Mheshimiwa Mbunge tuongee pembeni wanasema pesa hizi ni nyingi na huyu mshauri analipwa hela nyingi kuliko wakandarasi wote nchi hii kwanini? Kuna jambo gani nyuma ya pazia? Na hao wa ujenzi wanasema nusu ya fedha hizo aidha TANROAD inaweza kusimamia hiyo barabara au wakandarasi washauri wengine. Tuna miradi mikubwa hapa inataka akili nyingi kuliko kilometa 66 za barabara, kwa nini mkandarasi mshauri hapa alipwe fedha nyingi zaidi?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa tuliambiwa hawa watu waligombana huko nje ya nchi kwenye mradi, ugomvi wao na mvutano wao kugombana wanauleta hapa, mpaka mambo mengine yanataka kwenda kwenye mahakama za kimataifa, mara huyu kamkataa huyu mara huyu kamkataa huyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamuomba Mheshimiwa Waziri, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameingilia jambo hili, Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi alienda na ametoa maelekezo kwamba ili barabara ile ikamilike ambayo iko chini ya Waziri wa Fedha inatakiwa Mhandisi mshauri, Juni hii analize aondoke ili TANROAD wapewe nguvu wasimamie barabara hii na wakandarasi washauri wanaoona wanafaa ili tuweze kusongambele. Kwa hiyo Mheshimiwa nakuomba chonde chonde, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesha intervene na wewe uki-intervene hapo tutamaliza jambo hili vizuri na barabara yetu itaenda mbele. Ni aibu sana, kilometa 66.9 ambazo fedha zipo kwenye Wizara yako mfadhili kalipa lakini mpaka leo tunasuasua. Mfadhili ameshaonesha hataki kumlipa mkandarasi mshauri pesa tena kwa sababu amefika maximum ya malipo yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa sababu wataalamu wetu wa ujenzi wanatuambia mambo haya tuyaseme na sisi wanasiasa hasa vijana kama Mungu akipenda as a factor remain constant ceteris paribus we have nothing to lose because age is on our side, Mungu akipenda. Kwa hiyo kutetea nchi hii tutaendelea kusema ukweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye kilimo; mimi la kwangu nataka kuungana na Mbunge wa Hai, kuhusu ushirika. Ushirika ni matatizo, matatizo kweli kweli. Na kama kweli tunataka kukuza kilimo chetu, na mimi nina interest na kilimo cha miwa kule, ni vizuri Wizara ya Kilimo ikatoa elimu ya kutosha kwa watu wa ushirika; hasa zile Bodi ili ziweze kuendeleza mazao ya ushirika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakwambia hapa mfano wa jambo moja ambalo limefanywa na viongozi wangu wa ushirika kule, na migogoro hii Mheshimiwa Waziri anahangaika nayo kuitatua kila siku. Wanabandika taratibu za kutafuta zabuni zinafatua wanakuja wanatengua, mgogoro! Mgogoro! Mgogoro! Mgororo. Kama alivyosema Saashisha, kwamba Bodi hizi za ushirika lazima ziangaliwe vizuri. Kama zimebandika taratibu wanataka wazabuni wenye sifa hizi wamepatikana wasitengue zile barua zao, kwa sababu wanavyotengua barua wanampa leo huyu inaleta mgogoro mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nataka kutumia nafasi hii kuwasihi sana wakulima wangu wa miwa hasa wa Sanje ambao wananipigia simu kila wakati wanataka Mkutano Mkuu ili waamue jambo hili liishe; na naomba sana wavute Subira na Mungu atatusaidia tutamaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kusisitiza kwamba namuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama kweli wanataka kupandisha thamani ya mazao yetu kama walivyoahidi katika bajeti basi wasimamie vizuri ushirika, na nimemuomba Mheshimiwa Waziri awaruhusu hawa wakulima wa miwa wafanye mkutano wao mkuu waamue juu ya jambo hili. Ninamshukuru Dkt. Ndiyege ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Ushirika, amelifanyia kazi jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokwenda sasa, kama kweli tunataka Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia iendelee kufanya vizuri sisi pamoja na wote wanaomshauri ni vizuri tukasisitiza kuhusu mambo ambayo Mheshimiwa Rais aliyafanya akiwa Makamu wa Rais na Hayati Dkt John Pombe Magufuli yakaendelezwa na yakasimamiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokwenda sasa, kama kweli tunataka Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia iendelee kufanya vizuri sisi pamoja na wote wanaomshauri ni vizuri tukasisitiza kuhusu mambo ambayo Mheshimiwa Rais aliyafanya akiwa Makamu wa Rais na Hayati Dkt John Pombe Magufuli yakaendelezwa na yakasimamiwa, kwa sababu Watanzania wanaona na wanasikia. Ni hatari sana sasa hivi ukisikia kwamba kuna mkulima wa gunia moja analazimishwa kutozwa ushuru, maana yake Serikali iliyopita ilikuwa inasisitizwa ukiwa na chini ya tani moja vusha vusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimekwenda kule Morogoro, nimekuta wakulima wanalalamika wanasema mbona sasa hivi tunatozwa na tulikuwa hatutozwi. Kwa hiyo, mtu yoyote anataka kukwamisha Serikali hii ni yule anayetaka kutengua mazuri ambayo Mheshimiwa Samia aliyafanya akiwa na hayati Dkt. Magufuli ambayo sasa hivi anayaendeleza na kurekebisha upungufu au kuuondoa, mathalani hiyo ya Machinga kuguswaguswa, mazao chini ya tani moja watu kuanza kutozwa ushuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kwamba, Serikali yetu kurudi katika mikopo, lazima tuombe Mungu kwamba mikopo hii ambayo nchi yetu itachukua, iwe ni mikopo mizuri, yenye masharti mazuri. Hayati Dkt. Magufuli alisikika mara kadhaa akisema, tahadhari za nchi ya Afrika kuhusu mikopo hii. Kwa hiyo, mambo haya yote yakisimamiwa vizuri itaonekana kwa kweli tunasonga mbele na tunaenda mbele pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudi kwenye miradi ya maji na Wizara ya Maji. Ni wazi kuwa kuna Wabunge tulikutana hapa kama 28, tukakutana na Waziri wa Maji ambaye anafanya kazi nzuri, tukazungumzia Miradi ya Miji 28 na kwamba miradi ile ni muhimu na kwa sababu ilikuwa ni mkopo kutoka Exim Bank ya India process zilikuwa zinaendelea. Sasa kaka yetu mara nyingi anafuatilia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia hoja iliyopo mezani ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nami kama walivyosema wenzangu kwa kanuni ile ya kibinadamu, usipomshukuru mtu basi hata Mwenyezi Mungu huwezi kumshukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali ya Awamu ya Sita na Viongozi wote wa Serikali kwa miradi mbalimbali ambayo wananchi wa Jimbo la Kilombero, Mkoa wa Morogoro wameendelea kuipata. Tunamshukuru Mkuu wetu wa Mkoa Mheshimiwa Martin Shigela na viongozi wake wote na Wakuu wa Wilaya kwa usimamizi mzuri unaoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vitu unatakiwa kuviomba katika mjadala huu wa kupanda bei ambao unaendelea katika Bunge lako ni kuiomba Serikali na kumuomba Mwenyezi Mungu kwamba, miradi ya Serikali na mipango na mikakati yote ambayo imesomwa kwenye hotuba ya Waziri Mkuu isije ikakwama, kwa sababu Serikali ilishajipanga kutuletea maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo tulipambana katika corona baadhi ya miradi haikukwama, tumuombe sana Mwenyezi Mungu miradi yetu isikwame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasi kama Wabunge tunatoa mawazo yetu hapa, lakini kama walivyosema baadhi ya Wabunge tusisahau kumtanguliza pia Mwenyezi Mungu mbele, tumuombe Mwenyezi Mungu atusaidie janga hili tuvuke salama. Semeni Amina. (Makofi)

WABUNGE: Amina. (Makofi)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mwenyezi Mungu awajalie viongozi wetu busara na hekima tushikamane wakati huu Watanzania, semeni amina!

WABUNGE: Amina. (Makofi)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ukurasa wa 29. Ni imani yangu kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu atanisikiliza, ukurasa wa 29 ametoa taarifa ambazo napenda Waziri wa Kilimo azisikilize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na tatizo hili la kupanda bei lakini kama wananchi wetu wanaendelea kuzalisha halafu katika kuzalisha huko wanakutana na vikwazo, tunazidi kuongeza uchungu mara mbili. Mheshimkiwa Waziri Mkuu katika ukurasa wa 29 anasema, katika vyama vya ushirika 6,013 vilivyokaguliwa vyama vyote hati mbaya, hati chafu, kasoro vyama 300 tu vya ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka kusema hapa vizuri kabisa, kama Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake ameona katika vyama 6,013 vya ushirika vilivyokaguliwa na CAG, vyama 2,674 Hati yenye Shaka, vyama 1,253 Hati Isiyoridhisha, vyama 1,729 Hati Mbaya kasoro vyama 300 tu. Mpaka tunavyozungumza hivi huko kuna wakulima wanauza mazao yao kupitia ushirika, Warajisi wa Ushirika wapo maofisini wanaendelea kula bata, biashara kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo nina imani naye ananisikiliza kwamba, tunaomba mabadiliko. Kwa mfano, Mkoa wa Morogoro tumeshalalamika sana kuhusu Mrajisi wa Mkoa. Tumeshalalamika sana kumhusu Mrajisi wa Kanda na nimesikiliza baadhi ya Mikoa hapa wamelalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ni moja. Mimi nilikuwa DAS Rombo na wewe ulikuwa DAS Arusha unakumbuka, tumeondoka Kilimanjaro tuna malalamiko ya Mrajisi wa Mkoa. Tumefika hapa aliyekuwa Waziri wa Kilimo wakati ule akatumia siku tatu kufanya mabadiliko ya Warajisi wa Mkoa. Kwa nini Kilombero hawafanyi mabadiliko na Mkoa wa Morogoro haufanyiki mabadiliko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaeleza sababu na Mheshimiwa Waziri nimemtumia mpaka video na sauti kwamba, kuna watu kule wanasema mua na sukari ni dhahabu nyeupe, wanafanya wanavyotaka. Sasa mwananchi akizingatia huku kuna bei zinapanda, huku ana mua wake kiwandani, hapewi nafasi ya kwenda kuuza hasira inapanda mara mbili. Tunaomba Waziri wa Kilimo mmezindua kilimo vizuri sana vijana wameanza kupenda kilimo, lakini ushirika utawavuta nyuma na ushirika unaweza ukawa kama dude ambalo limewashinda Mawaziri wengine huko nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fanyeni mabadiliko Kilombero na katika Mkoa wote wa Morogoro. Kwa nini Mrajisi huyu haondolewi malalamiko yote tumeyasema? Kwa nini huyu Mrajisi wa Kanda sijui anaitwa Ndugu Mshumba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nitakuomba nita-play sauti ya mwananchi mmoja kati ya wananchi 20 walionipigia simu kumlalamikia huyu mtu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanapandikiza Wakandarasi, wanafanya mambo yao, wanavuruga kilimo na kilimo cha mua ni muhimu katika nchi yetu. Kilimo cha mua ni muhimu kwa wananchi wa Kilombero. Kilimo cha mua kinatusaidia kujitegemea katika sukari, lakini Warajisi wanafanya madudu wanavyotaka wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaenda kwenye Mkutano Mkuu wanavunja Bodi wao wanalazimisha kuleta watu wa bodi wanaowataka wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sishangai Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kusema vyama vyote vya ushirika vilivyokaguliwa ni hovyo, wala sishangai kwa sababu ya Warajisi hawa ambao tunawalea. Nimemuona Mbunge wa Katavi hapa Kaka yangu Kakoso analalamikia mambo ya ushirika, kwa hiyo naomba ichukuliwe hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako naomba ni-play sauti mojawapo ya mwananchi ukiniruhusu, tusikilize hapa mwananchi analalamika kuhusu mambo ya ushirika ili Mheshimiwa Waziri aweze kuchukua hatua.

MWENYEKITI: Hapana Mheshimiwa, haujaruhusiwa kufanya hilo jambo.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Asenga unatakiwa uombe na Kiti kikikuruhusu ndiyo uendelee. Endelea kuchangia.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-play sauti ya mwananchi akitoa malalamiko yake kuhusu…

MWENYEKITI: Table Mezani halafu itapokelewa.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa. Naomba kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza suala la ushirika nataka kuzungumzia kidogo kwenye suala la ujenzi. Ni imani yetu hapa kwamba, Mawaziri watakapokuja watatusaidia kujibu baadhi ya changamoto. Nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu amejaribu kuzungumza baadhi ya miundombinu inayojengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Kilombero tuna changamoto moja kubwa ya barabara ya Ifakara – Kidatu. Sasa hivi tumekuwa wataratibu na wapole kwa sababu, tunaona dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Katibu Mkuu wa Wizara Injinia Aisha Amour na Meneja Mkuu wa TANROADS Injinia Mativila. Tuna imani kwamba, Waziri atakapokuja hapa atatuambia ule mkwanziko wa settlement na Mkandarasi kikao kitafanyika lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba ukija hapa Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi atatusaidia kujua ahadi ya Mheshimiwa Rais katika eneo la Mang’ula Kona aliyotupatia itaisha lini? Fidia za wananchi waliotoa kuhusu ile barabara zitaisha lini? Na kwa nini Kilombero ilirukwa katika taa za barabarani? Nafikiri tutapata majibu hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema katika ujenzi nataka kuzungumza katika Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kidogo, nina imani Mawaziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa watakuja hapa. Sisi kama wananchi wa Kilombero katika Bunge hili la Bajeti tunatarajia tulitoa wazo kwamba, kama ilivyofanyika katika Wizara ya Maji, Mheshimiwa Rais amenunua miundovifaa vya kupima maji na kuchimba maji, tulitoa wazo TARURA ni vizuri Serikali ikanunua vifaa kama ma-grader, excavator, kwa baadhi ya Wilaya ikazipatia vifaa hivi ili kupunguza gharama kubwa za ujenzi wa barabara ambazo sasa hivi hali yake ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamesema hapa upande wa Wizara ya Afya nami nataka kuchangia kidogo. Wakati nimesimama hapa nazungumza nilimpa Naibu Waziri wa afya juzi ki-memo changu kumwambia hospitali yetu, kituo chetu cha Kibaoni-Ifakaraka ambacho tunakitumia sasahivi kama hospitali ya Wilaya hakina dawa kiasi kwamba, wamama wajawazito wanarudishwa nyumbani bila dawa. Sasa Wabunge wengi wamesema hapa kuhusu mambo ya MSD na mimi naomba Serikali na Mheshimiwa Waziri Ummy wachukue hatua za haraka iwezekanavyo kuhakikisha wanakabiliana na suala la dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji. Tuna imani Waziri wa Maji atakapokuja hapa tunataka kusikia habari ya Miji 28. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia ametaja miradi ya Miji 28 na Ifakara, Kiburubutu, ipo ndani ya miradi ya Miji 28. Imani yetu ni kwamba Waziri wa Maji atakapokuja hapa atatupa picha na muda gani mradi wetu ule unaenda kutolewa majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sitaki useme. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Bajeti kwa Wizara ya Kilimo ya Kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe na Mheshimwia Anthony Mavunde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia namfahamu Mheshimiwa Hussein Bashe tangu mwaka 2008 akigombea Uenyekiti wa Umoja wa Vijana na baadaye Umakamu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana kama Katibu Mkuu wetu Isack alivyosema. Sifa pekee ambayo naweza kuisema ni kwamba ni mtu ambaye ni mgumu kubanduka katika jambo la ukweli analoliamini. Wakulima wa nchi hii wana imani kubwa kwamba kwa sifa hiyo, basi kilimo kimepata tiba ya kweli kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba Mwenyezi Mungu aijalie nchi yetu iepukane na majanga na Mheshimiwa Rais akusanye mapato ya kutosha ili bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ameiomba aipate. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, napenda kushukuru kwamba juzi nilisimama hapa katika Wizara ya Maji kuzungumzia mambo ya wakulima wangu wa Muwa. Napenda kutumia nafasi hii kushukuru Waziri Mheshimiwa Bashe na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, kaka yangu Martine Shigela kwa kutatua changamoto ile. Sasa hivi wananchi wangu wa Kata ya Sanje huko ni shamrashamra kwamba jambo lao limesikika na utatuzi umepatikana, wanaendelea na uvunaji wa miwa na tarehe 19 wanaanza kuingiza miwa katika kiwanda cha Ilovo kwa ajili ya uzalishaji wa sukari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitagusia kama mambo manne ama matatu kutokana na muda. Mkoa wetu wa Morogoro ni ghala la Taifa. Kwa hiyo, tunamwomba Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Bashe atusaidie sana tafsiri ya ghala la Taifa, kwa kuwa Mkoa wa Morogoro ni Mkoa mzuri sana una ardhi nzuri sana inayofaa kwa kilimo cha kawaida na inafaa kwa kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa yetu ya mkoa, juzi tuliambiwa tuna hekta karibu laki 300 zinazofaa kwa umwagiliaji, lakini nasikitika kidogo kuna miradi imeanzishwa na Serikali na inakwama Morogoro haiendelei, hasa ya umwagiliaji. Nitakutajia baadhi hapa ili Mheshimiwa Waziri unisaidie kuinukuu na wale wanaopulizapuliza usije Kilombero, washindwe, walegee, uje uione hii miradi na uone jinsi fedha za Serikali zimewekwa na miradi haijakamilishwa, wananchi wanapata adha kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Skimu ya Mang’ula Youth, fedha za Serikali zimeenda pale, mradi haujakamilika. Tuna Mark Magombela, tuna mradi wa Kisawasawa, Serikali ilipeleka fedha lakini haijapeleka fedha za kumalizia. Wakulima hawana pa kuhifadhi mazao yao kama Msalise na Mkula. Maeneo mengine wameomba Shilingi milioni 280 kumalizia na maeneo mengine wameomba Shilingi milioni 150 kumalizia, lakini fedha hazijaenda. Kwa mfano, Mkula wawekezaji wamejenga maghala makubwa kabisa, na mwekezaji kafunga hajamaliziwa fedha yake na wakulima wanashindwa kuhifadhi mpunga wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama tunasema Mkoa wa Morogoro ni ghala la Taifa na tunaweza kuzalisha; unajua karibu 50% ya hitaji la mchele tu la ndani ya nchi yetu, Mkoa wa Morogoro peke yake unaweza. Sasa kama miradi hii haitafanyiwa kazi, kwa vyovyote vile ni wazi kwamba hatutaweza kuwa ghala la Taifa kikwelikweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kibaoni pale karibu na Ifakara Mjini kuna hekta karibu 10,000 Lungongole ambazo zinafaa kwa kilimo, lakini bado upembuzi yakinifu unasuasua kutokana na ufinyu wa fedha. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri utusaidie ili tuweze kutafsirika kama Mkoa wa Morogoro ni ghala la Taifa. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Mheshimiwa Waziri pamoja na sifa tunazosema kwako na msimamo wako, katika muda atakaokujalia Mwenyezi Mungu kuongoza Wizara ya Kilimo, itakuwa ni aibu kubwa sana ukiacha nchi hii inaagiza sukari kutoka nje. Itakuwa aibu kubwa kweli kweli! Sisi Morogoro hasa Kilombero kama wakulima wa muwa, nami nimekuwa nikipiga kelele kila siku kuhusu wakulima wa muwa na mambo ya ushirika; nitasema baadaye kuhusu ushirika. Sukari, sukari, sukari, ni aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kuzungumza habari ya importation of sugar, najua ni vita kubwa hii ya uingizaji wa sukari. Kwa msimamo wako tunajua uta-control, isiue kilimo chetu cha ndani cha miwa. Maana yake sisi tulienda Kilombero na Waziri aliyepita akaona miwa karibu 200,000 inabaki. Yaani nchi hii tunaingiza sukari na juzi nimemwona Rais Museven anazindua Kiwanda cha Sukari kitakachozalisha tani 5,000 kwa siku, yaani cha kawaida tu. Sisi tuna-import sugar wakati tuna ardhi ya kutosha, tuna kila kitu cha kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, achana na ardhi, miwa imeshalimwa tani 200,000 kiwanda hakina uwezo. Waziri akaenda akatoa statement pale wawekezaji wa Ilovo wakakubali kufanya expansion ya kiwanda. Mpaka sasa hivi imeishia kwenye ku-clean layer tu, wanasema tunaogopa. Importation of sugar; kwamba kuna mashaka kwamba sukari itaingizwa bila utaratibu. Tutawekezaje hapo 500 billion? Mheshimiwa Waziri tuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kile na upanuzi huo usipofanyika, na hata nimemwona Balozi Mpungu amezungumza kwenye vyombo vya habari akielezea mashaka yake katika uwekezaji ule. Miwa tani 200,000 itaendelea kubaki; na mpaka Magereza walikuwa wanaendelea kulima miwa, na matokeo yake ni kwamba wananchi malalamiko yao yataendelea, na nchi yetu itazidi kuingiza sukari kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua uingizaji wa sukari na vibali hivi vina faida yake, lakini ni wazi kwamba nchi hii hatutakiwi kuingiza sukari kutoka nje. Sisi tunatakiwa kuzalisha sukari kuuza nje. Nimeona hata wawekezaji wa Kagera wale, wakina Nasoro wa Kagera wanahangaika na maeneo tu, wapewe maeneo waweze kulima miwa wazalishe sukari. Wapeni maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wilaya ya Kilombero upande wa Mlimba kule Mofu kuna hekta 10,000 za Bodi ya Sukari zinamilikiwa. Unatafuta mwekezaji mdogo azalishe sukari. Kwa hiyo, katika uongozi wako legacy mojawapo ni kuhakikisha utamu wa nchi hii kwa wananchi katika chai unazalishwa na unatosheleza wenyewe humu humu ndani na unakuwa wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu; ukiwa Naibu Waziri wakulima wangu wameshasafiri na mabasi hapa mara tatu au mara nne ukawapokea wakilalamikia makato ya kodi ya 2% na ulitoa statement kwamba hela yenu mtarudishiwa. Mpaka sasa hivi hawajarudishiwa. Wakulima wa Kilombero wanauza sukari, hawauzi miwa. Ndiyo mkataba wa kiwanda na wakulima. Wakulima, unalima muwa wako, kiwanda kinavuna, kinaenda kinachakata, kinauza, kikishauza, kikishatoa gharama zote, ndiyo mkulima analipwa na kodi imekatwa. Mkaja kuanzisha 2% ya kwenye mazao, wamekatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alitoa statement kwamba ile pesa itarudishwa, haijarudishwa. Sasa huko mbele tukiwa na nia ya kushika Shilingi tutakuwa tunakukosea adabu, lakini ukweli ni kwamba unajua mwenyewe wanakaa mwezi, wanapanda basi, wanakuja kufuatilia two percent yao. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa ahadi zenu hizo mhakikishe kwamba fedha zao mnazirudisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Doctor hapa mtaalamu wa ushirika, fanya mabadiliko katika ushirika; na hii hafumbifumbi macho, mimi mwaka 2021 nimefuatilia matatizo ya ushirika. Nimeenda pale kusaini kitabu kwa Mrajisi Taifa hapa mara 11, watu wanaingilia hapa wanatokea hapa. Fanya mabadiliko katika ushirika, lete modal. Yupo Mheshimiwa Dkt. Cherehani hapa, ukikaa naye, unajua ana utalaamu wa ushirika, anaweza kukusaidia mawazo. Watu wanalalamika sana kwenye ushirika, na taarifa ya Waziri Mkuu hapa Bungeni inatosha kukupa picha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mkuu anasema vyama 6,013 vilivyokaguliwa, vyama 357 pekee ndiyo hati zake zinaridhisha. Kuna watu wa Ushirika tuna Mrajisi tuna nani, na Morogoro wana matatizo makubwa, mimi siumi maneno na mwaka jana iliundwa tume mpaka leo taarifa inafichwafichwa, siumi maneno kama Mkoa wa Morogoro Ghala la Taifa Ushirika hawajatimiza wajibu wao na vyama hivyo katika vyama 6,013 na sisi tumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawahami, watu hawarekebishwi, watu hawabadilishwi kama mikoa mingine tunavyoona. Ukisema wanasema Mbunge una ajenda binafsi, haiwezekani Waziri ukaja hapa ukatuambia Waziri Mkuu katoa taarifa kasema vyama 6,013 Waziri Mkuu wa nchi hii, vyama 357 pekee ndiyo vina hati ya kurizisha, Waziri ukileta statement yako hapa lazima utujibu taarifa hiyo wa Waziri Mkuu wewe unaishughulikia kwa namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kengele imepigwa, nakushukuru naomba kusisitiza kuunga mkono bajeti lakini kusisitiza kwenye ruzuku ya mbolea, chonde chonde wakulima wangu wa mpunga, wakulima wangu wa miwa wanataka ruzuku katika mbolea. Mwaka huu jasho limewatoka kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa nafasi ya kuchangia hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwa kuanza na mimi nimpongeze Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mambo makubwa anayoyafanya katika nchi yetu. Uongozi wake unalifanya Taifa letu limeendelea kuwa tulivu sana, na hata pale tunapopata changamoto kubwa hizi za mijadala ya kisiasa bado nchi yetu imetulia sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhusu Hassan kwa miradi mikubwa ambayo amatuletea katika Jimbo la Kilimbero; na hasa hasa ametuletea viongozi makini wa Mkoa wa Morogoro. Ametuletea Mkuu wetu wa Mkoa Mama Fatma Mwasa na Mkuu wa Wilaya mpya Wakili Dunstan Kiobya; kwa kweli wanafanya kazi kubwa nzuri. Tunawaombea afya ili waendelee kumsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni Bunge la Bajeti tunajadili mambo ya bajeti, na katika bajeti ni mipango na matumizi. Kama nilivyosema awali, ni kwamba kuna aina nyingi za bajeti lakini katika nchi yetu tuna bajeti ambayo tunapanga matumizi mengi halafu baadaye tunatafuta vyanzo vya fedha. Sasa katika Hotuba ya Mheshimiwa Rais juzi akipokea taarifa ya CAG ametuonesha njia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwambakuna sehemu tukiwekeza, tukiacha uoga tutapata takriban 50% ya bajeti ya nchi yetu. Mheshimiwa Rais anasema tuache uoga katika uwekezaji wa bandari; 50% anayosema Mheshimiwa Rais tuna bajeti takriban ya trilioni 40 hapo. Mheshimiwa Rais anazungumzia trilioni 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi kama Wabunge katika vitu ambavyo tulitakiwa tuvikimbize ni kuhakikisha hii trilioni 20 ya bandari tunaipata kwa wakati. Kwa sababu mambo mengi tunayozungumza hapa, tunaomba na mimi nitasema mengine ya kuomba hapa. Kwa hiyo naishauri Serikali, namshauri Mheshimiwa Waziri Mkuu, leteni marekebisho kama ya Sheria ya Ununuzi ya kukaribisha hawa wawekezaji wanaotakiwa. Wabunge tumetembea hapa tumeona nchi za wenzetu wanavyowekeza katika bandari na matrilioni ya fedha wanazopata. Sasa kama una gari sasa hivi pale inatupa trilioni moja, kuna mtu anaweza akaja akatupa trilioni 10 ama 20 ni kitu cha kufanya haraka; trilioni si fedha ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda India; pale Mundra miaka 20 iliyopita ilikuwa pori, sasa hivi wana port ambayo inaongoza kwa mapato India na Asia. Sisi tuna Bagamoyo pale tunajadiliana tu, waoga, bandari isibinafsishwe. Mheshimiwa Rais amefafanua vizuri sana; tuache uoga, tuwekeze, tuwape watu wenye mifano ya kuendesha bandari duniani tupate pesa. Wabunge tunalalamika hapa kituo cha afya, mama ana-click tu unapata kituo cha afya. Mimi namshukuru sana Mheshimiwa Rais pale sasa hivi ameteua wakurugenzi wa bandari ile vijana wadogo kama mimi hivi lakini ukiwasiiliza unajua hawa ni watu wa biashara na hawataki mchezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri Mkuu ninaomba sana. Kabla sijalalamika mambo mengine huko na kuomba fedha anzeni mambo pale, sheria zije hapa kama za ununuzi zina mchakato mrefu zibadilishwe ili uwekezaji ufanyike tupate fedha; hilo la kwanza la mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nilitaka kuzungumza kuhusu maadili kama wenzangu walivyosema hapa. Kuhusu hili jambo la maadili nafikiri sidhani kama sisi Wabunge tunapata muda wa kuzungukazunguka Dar es Salaam tu peke yake. Mimi nilikuwepo wakati ule Makonda anaanza kufanya yale mambo ya kupambana na hawa watu na jambo hili. Najiuliza kwa nini Tanzania sisi hatunyooshewi vidole na nchi hizi ambazo zina-support ushoga duniani. Kuna sehemu hatujafanya vizuri, ni kama jambo hili linachekewachekewa. Mimi nina watoto wawili wa kiume nikiwaangalia watoto wangu nikisoma vyombo vya habari, ni jambo la hatari; na viongozi wetu muwe makini sana kwenye harusi mnazokwenda. Mnaenda kwenye harusi mnasherekea harusi, mnacheza pale unashangaa wale watu wanakuzunguka pale picha inarekodiwa zinasambazwa huku mnaonekana na ninyi viongozi mna-support jambo hilo. Jambo la hovyo la mambo mabovu ya maadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, katika East Africa tukigawanyika katika kutetea jambo hili tumeumia. Tazameni Uganda kinatokea nini kwa Museveni. Museveni alivyoanza ku-fight jambo hili nini kinampata? East Africa sisi tumekaa tunaziangalia namna gani. sasa kuna mwanasheria mmoja ametushauri Wabunge, ameandika hapa amesema sheria yetu peke yake itakuwa ngumu sana ku-fight mambo haya ya ushoga na mambo ya jinsia moja. Akasema kifungu 154 cha sheria kinazuia kuingilia kinyume cha maumbile, hakizuii ushoga mwandishi kafafanua kwa ufupi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja nisome. Anasema kifungu cha 154 cha Kanuni za Adhabu kinazuia mwanaume kumwingilia mwanamke kinyume cha maumbile na mwanamume kumwingilia mwanamke kinyume cha maumbile. Adhabu ya kosa hili ni kifungu cha miaka 30 yamkini kifungu hiki hakiwezi kuzuia ushoga kwa sababu ili mtu apatikane na hatia ni hadi athibitishe kuingilia, anus penetration. Sasa nani atathibitisha kuingilia kati ya aliyeingiliwa na aliyeingilia wakati wote wanafanya kwa hiari. Kifungo hicho kinashindwa kuanzia hapo, hii maana yake hata ukiwaona wanafanya bado unashindwa kuthibitisha kuingilia hata hivyo utawaona wapi wakifanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uganda adhabu ya kuingilia ni hadi miaka 10 wakati kwetu ni maisha ama miaka 30. Hata hivyo Uganda wanafanikiwa kuzuia matendo haya kwa sababu sheria yao haijaishia kwenye kuingilia watu wao wanashughulikia matendo ya ushoga na usagaji kwa ujumla wake wakati huku tunashughulikia kuingilia ni maelekezo mawili tofauti. Mwanasheria anasema; na ndio hii sababu unaona sisi tuna adhabu kubwa lakini hatupingwi, hatupigiwi kelele za kimataifa na wanaotetea ushoga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anaendelea kusema ni kwa sababu wanajua kuwa sheria ya Uganda inaweza kufuta janga hili wakati ya kwetu haiwezi. Uganda kuingilia kinyume cha maumbile ni kosa, kuonesha ama kuvaa au kufanya kiashiria chochote cha ushoga na usagaji ni kosa, kujitangaza kuwa ni shoga ama msagaji ni kosa. Mwenye nyumba, mwenye hoteli, lodge, gesti kumpangisha shoga na msagaji ni kosa. Kuvaa mavazi yanayoashiria mwanamme kuwa shoga au mwanamke kuwa msagaji ni kosa, kaka zetu wanabinukabinuka huko mtaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chombo chochote cha habari ama mtandao wa kijamii kumtangaza katika namna yoyote kukubali vitendo hivyo ni kosa na mengine mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uganda ushahidi wa kimazingira unaweza kukuwajibisha kuwa ni shoga. Hatuwezi kuishia kuzungumza kuwa hata wanyama hawafanyi hivyo halafu ushoga ukaisha, tunahitaji hatua za kisheria za kushughulika na watu hawa. Wako huko kwenye maharusi, wako huko mjini watoto wa kiume wanavaa blauzi, wanabinuka binuka, wawakamate, watengeneze jopo la Madaktari, wathibitishe, wawafunge. Waziri Mkuu ni Muislamu, Rais Muislamu, Dkt. Mpango Mkristo, Mwenyezi Mungu, atawauliza wakati wamepewa madaraka ya kuongoza nchi hii walichukua hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata semina moja ya Mzee Kinana anasema kuna namna nyingi, ninyi ambao mna machine tools za ku–deal na mambo hayo wanaweza wakafanya wakapotea watoto wa kiume wanaovaa magauni na kubinuka mjini. Waende kwenye maduka Sinza watazame watoto wa kiume wanabinuka binuka hovyo, wanavaa vibatiki, sidiria, watoto wa kiume! Sasa sheria zetu haziwezi kufanya hivyo, tunapiga piga mark time hapa, walete sheria kwamba uki–post unakamatwa, tabia zako hazieleweki unakamatwa, jopo la Madaktari wanakaa wanathibitisha. Watazame sheria ya juzi Mahakamani pale, yale mambo ya Zanzibar anasemaje yule mtalam pale, anasema: “Ninachoweza kuthibitisha ni kwamba tundu la huyu mtu unaweza kuingiza vidole viwili.” kaishia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu wanavaa blauzi, kwani sisi tunakereka na ushoga kwa taarifa ya Mwakyembe na zile taasisi kwa sababu gani? Kwa sababu watu wanaonekana, sikilizeni taarifa ya Mwakyembe, sikilizeni yule dada na yule aje afanye presentation hapa mwone. Usiku kuna mzungu Masaki huko anakusanya mashoga wanafanya party. Sasa hili ni jambo ambalo kama tunakereka nalo, Serikali wana machines, watumie kwa hawa, wawapakie kwenye malori, wawapeleke kwenye magereza, sisi Idete kule, Kilombero kule magereza yetu ndiyo magereza yanayoongoza kutokuwa na watu wa kutosha, wawalete kule wawafunge na mashamba ya kulima yapo, unalima na jembe futi moja hivi, waje kule walime. Watu wanachezacheza hapa ushoga, ushoga, tunalalamika tu, wawakamate hao watu wawatie ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwa sababu ya muda, nataka kumshukuru Mheshimiwa Rais, kwa miradi mikubwa ambayo ametuletea lakini hasa hasa niseme kuhusu Barabara yetu ya Ifakara – Kidatu, kweli Mheshimiwa Rais ametusaidia. Utakumbuka nilitaka kukaa chini kwenye kapeti hapa kuhusu Barabara yangu ya Ifakara – Kidatu, lakini tangu Mheshimiwa Rais Samia ameingia miaka miwili hii tayari nina kilomita 42 katika kilomita 66 za lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wakati huu tayari tumeshapata bilioni 42 za Mradi wa Maji wa Kiburubutu. Nimejulishwa hapa tayari tuna pesa ya VETA iliyoenda kujenga Chuo cha VETA pale Ifakara ambapo advanced milioni 45 imeenda kwa ajili ya ku–clear eneo na tumepata Mahakama mpya. Namshukuru sana Waziri wa Mambo ya Ndani alikuja Kilombero na ni imani yangu atatusaidia kupata Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali katika mikakati yake ya Kilimo, Waziri Bashe, ametuambia kwa mara ya kwanza Serikali itaanza kununua mpunga kwa bei nzuri, tunaomba mbolea iwahi, tunaomba suala la wakulima wa miwa lifanyiwe kazi, tunashukuru kwa kiwanda cha sukari kipya kinaendelea, tunaomba kikamilike kwa wakati, tunashukuru Mheshimiwa Rais, kwa sekondari nane mpya tumejenga. Tumejenga zahanati nne, tumejenga vituo vya afya viwili, juzi ametuingizia milioni 300 Ifakara za sekondari, ametupa milioni 470 za sekondari advanced, ametupa milioni 500 juzi la Jengo la Mama na Mtoto katika halmashauri yetu na ametupa bilioni 13 za Mradi wa Substations ya kukuza umeme Ifakara, ametupatia lami kilomita mbili Ifakara, ametupatia lami Mwaya na mambo mengi Mheshimiwa Rais, ametusaidia kufanya. Tangu dunia iumbwe Halmashauri ya Ifakara na Wilaya ya Kilombero haijawahi kupata fedha nyingi kiasi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya alikuja Ifakara, akatembelea St. Francis Hospitali, ni Hospitali ya Rufaa, hospitali ambayo inasaidia halmashauri tano na wilaya tatu, Baba Askofu pale anaomba msaada kwa sababu tunashirikiana na Serikali CT–Scan, MNRI na Ultrasound za kisasa, naomba Waziri awasaidie, kama alivyofika pale ametembelea, ameona hali halisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba viwanda, tuna majengo tayari ya viwanda. Kutokana na kwisha kwa muda naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi. Nami kama walivyosema wenzangu, kwanza natoa shukurani za dhati kwa Rais wetu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa moyo wake mkubwa wa kuendelea kufanya kazi katika nchi yetu. Anasema, hakuna kilichosimama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikuwa Ikulu tunazindua jengo, kuna watu walifikiri litasimama, halijasimama; mradi mkubwa wa Maji wa Bwawa la Nyerere, haujasimama unaendelea; Daraja la Busisi halijasimama, linaendelea. Sana sana vile vilivyosimama, sasa hivi vinaendelea. Mfano ni barabara yetu ya Ifakara – Kidatu ilikuwa imesimama huko nyuma na sasa inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno mazuri haya yanathibishwa na kauli ya kaka yangu Mheshimiwa Freeman Mbowe, anasema mama anaupiga mwingi sana na mama anafanya kazi kubwa. Mheshimiwa Mbowe ameanza kumwelewa mama sasa hivi, hawaongei tupu tupu, wanaanza hata kufanya fanya miradi ya maji, nimeona huko, na wakichangisha pesa wanazibakiza kwenye vijiji, hawaondoki nazo zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii yote ni uthibisho wa uongozi mzuri wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kujenga umoja wa nchi yetu na tunamuunga mkono tunampongeza sana. Mheshimiwa Waziri wewe na watumishi wako wote katika Wizara hiyo, tunawashukuru sana na tunawapongeza sana kwa kazi mnayofanya. Wenzangu wametangulia kusema Wizara hili ni kubwa na kazi ni kubwa kweli kweli na maneno ni mengi, lakini wote ambao Mheshimiwa Rais amewaamini, endeleeni kumsaidia, onyesheni uwezo wenu katika kufanya kazi kubwa na wasaidizi wako wengine kama ma DG Bandari na akina Kadogosa huko ni vijana wadogo, wameanika sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaambia sisi tunajua ipi ni ipi, na ipi siyo ipi? Kama kuna maneno mengine ya kuupuza, wayapuuze waendelee kufanya kazi. Watu wanataka kutoka Dodoma kwenda Dar es Salaam kwa reli. Walale Dar es Salaam waje wafanye kazi Dodoma warudi Dar es Salaam kula bata, Mji wa kibiashara, mama kashasema na kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri amekuja hapa leo anaomba 3.5 trillion katika bajeti yake na nina imani Bunge litampitishia bajeti yake. Tunamwomba sana na tunaiomba Serikali hasa Waziri wa Fedha ahakikishe fedha hizi zinakuja kwa wakati ili miradi hii itimie. Kwa mfano, Serikali kufikia mwaka Februari, 2023 katika sekta ya ujenzi imetoa fedha za kutosha karibu 85 percent, lakini ukienda kwenye uchukuzi kule kweli fedha ni chache ni asilimia 59 tu peke yake. Kwa hiyo, tunaweza tukapitisha hapa bajeti lakini utoaji wa fedha ukichelewa, automatically miradi itapungua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya ujenzi, Wizara ya Ujenzi ni mambo ya fedha tu. Sasa ni muhimu sana kama kuna maeneo Mheshimiwa Waziri mnaweza kufanya uwekezaji, ambavyo Mheshimiwa Rais amesema na Wabunge wenzangu wengine wamechangia, yatakayozalisha fedha za kutosha msiyacheleweshe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza hapa, na hii ni mara ya pili nazungumza. Rais wa nchi, kiongozi wa nchi Dkt. Samia Suluhu Hassan anasema tukiwekeza katika bandari tunaweza kupata nusu ya bajeti ya nchi yetu. Hili siyo jambo dogo, ni jambo kubwa sana kusema nusu ya bajeti ya nchi yetu. Sasa hapa tunazungumza, Wabunge wote tunadai fedha. Tunadai fedha, lakini hili jambo kwanini mnalichelewesha? Kwanini mnasema mnachelewesha uwekezaji katika bandari? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Rais, alienda Dubai mwaka 2021 katika Dubai Expo, tukamwona Waziri wa Kilimo na Waziri wa Viwanda. Mheshimiwa Waziri ulikuwepo pale, watu wa bandari walikuwepo pale. Mkaonesha fursa siku nzima pale za nchi yetu, mkapata wawekezaji, mkaanza kuzungumza katika mikata ya nchi na nchi kushirikiana. Jambo mojawapo likiwepo ni bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Dubai na Dubai Port, wameonesha nia nzuri ya kutusaidia katika Bandari yetu, DP World. Agreement imeingiwa pale, mchakato hatuoni unaendelea. Tumekwama wapi? Wekeni jambo hili wazi, muungeni mkono Mheshimiwa Rais tupate fedha hizi. Hii bandari imebinafsishwa huko nyuma, imeshabinafsishwa sana, wanasema ooh, usiogope, usiseme, ukisema watu wakubwa; huko nyuma ilikuwepo tangu enzi ya Mkapa mmeweka wapi? Sasa leo Dubai inafanya vizuri duniani, watu wanakimbilia Dubai, Serikali ya Dubai, DP World wanataka kuja kuwekeza katika bandari yetu. Cha msingi, mtuweke wazi, mnawekeza nini? Ajira za Watanzania zitakuwa ngapi? Tunapata Shilingi ngapi? Sasa hivi tulikuwa tunapata Shilingi ngapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato, thirty five percent ya TRA ni karibu Shilingi trilioni saba wanachukua bandarini. Akija mwekezaji tunapata Shilingi ngapi? Wafafanulieni Watanzania, wata-support uwekezaji huu na bandari haiuzwi, haibinafsishwi tunaingia mashirikiano ya uendeshaji. Hawa DP World wanaendesha nchi saba Afrika ya Bandari. Duniani wana bandari 70. Hapa tunafanya siasa, siasa nusu ya bajeti ya fedha tunaikosa. Ukienda huyu wanamkuta huyu; mfanyabiashara anataka kwenda bandarini anachafua wengine, vurugu. Muungeni mkono Mheshimiwa Rais, agreement hiyo imeshaingiwa, imeshasainiwa kule Dubai, mchakato wa pili ufuate na mchakato wa tatu ufuate tuweze kunufaika kama wenzetu wa Senegal, Algeria, na Egypt ambapo DP World wako kule na wanawekeza kitu kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumalizia kwa kusema kwamba, kwa upande wangu wa Jimbo, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, umekuja Kilombero mara mbili. Katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 nilijua ajenda ya Barabara ya Kidatu – Ifakara ni kubwa. Pale Jimboni Kilombero hujakamilisha barabara hii, miaka yako mitano unasepa. Kwa hiyo, nikakaa na wazee wakaniambia, tumezunguka kwenye kampeni tumesema barabara ile isipojengwa hatugombei tena. Ndiyo maana unaona tumelala kwenye matope, tumekaa kwenye kapeti Bungeni, kilomita 66.6. Mheshimiwa Waziri leo karibu kilomita 50 mmeweka. Hiyo ni kasoro kama 15 au 16 hivi ambazo mimi naomba Mungu ngoma hii imalizike hiyo, iishe. Sasa Mheshimiwa Waziri unanijengea barabara mpaka roundabout ya Ifakara pale kibaoni, ni kama kilomita tano za mjini unaziacha, ile kilomita tano ya lami ya zamani ni ndogo sana…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Abubakari kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Taletale.

TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa ndugu yangu Mheshimiwa Asenga, naona anachangia kwa furaha sana, nami natamani furaha yake ihamie kwetu jibu la Kisaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa. Ndiyo ukae vizuri na Profesa Mbarawa, na muda wangu ananiishia.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Asenga, taarifa unaipokea?

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea. Akae karibu vizuri na Waziri hapa apate matunda mazuri. Profesa Mbarawa ni msikivu, Engineer Isack ni msikivu, Engineer Mativila ni msikivu, watamsadia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema Waziri anatujengea barabara mpaka roundabout ya Kibaoni. Barabara hii ikikamilika keshokutwa, mabasi yatapita mjini kwenda Ulanga, kwenda Malinyi, kwenda Mlimba, Ifakara Mjini hapatoshi. Tunaomba ile barabara ya kilometa 10 ya mchepuko ya Mbasa – Katindyuka ijengwe kwa lami watu walipwe fidia. Ndiyo matunda ya barabara ya Ifakara – Kidatu yatatokea. Maana vinginevyo tunaenda kupeleka msongamano Ifakara Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelekeza barabara kubwa hizi zinazopita kwenye vijiji, mweke taa za barabarani. Kidatu – Sanje – Mkuwe – Mang’ula A – Mang’ula B – Mwaya – Kiberege – Kisawasawa, wekeni taa kwenye vijiji barabarani. Watu wanauza maembe, wanauza ndizi jioni kwenye vituo vya daladala. Waziri Mkuu kaelekeza, nataka kujua kama mnatuletea taa za barabarani ama hamtuletei?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemwona Naibu Waziri wa Uchukuzi. Ifakara ina kituo kikubwa sana cha TAZARA, Ifakara tuna Uwanja wa Ndege sasa hivi kutokana na Mradi wa Kupambana na Malaria wa Ifakara Health ambao Mheshimiwa Rais alienda Marekani. Wanafugwa mbu Ifakara pale, ndege zinatua miruko mpaka 50 kwa mwezi. Kila siku karibu inatua ndege ndogo, uwanja wetu haufai. Waziri wa Uchukuzi tunakuomba, kwa sababu barabara hii ya Ifakara – Kidatu sasa hivi inaishia kilomita moja kwenda Airport, kwenda TAZARA tuunganishie hizo kilomita moja ama mbili tuunganishe na hii barabara kubwa na Airport, barabara kubwa na TAZARA. Ni jambo ambalo linaweza kusaidia Kata yetu ya Kibaoni ikachangamka kwa sababu ni Makao Makuu ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa taa za Ifakara Mjini na TANROADS barabara ile lakini ni kilomita mbili tu umefunga taa katika kilomita tano nilizokuomba. Tuletee hizo taa zilizobaki Mji wetu uendelee kuchangamka na sisi ni wauzaji wazuri wa mchele mzuri, unaonukia. Wanakuja Watanzania wengi sana kununua mchele kule, Wazanzibari wako wengi pale Ifakara. Taa zile zitasaidia mji wetu utapendeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti la mwisho. Juzi tumekutwa na mafuriko. Nimeenda na Meneja wako wa TANROADS Mkoa Eng. Razak, mtu mzuri. Baada ya mafuriko tu amekuja, ametazama makalavati yale na changamoto zake. Ameona, amesema yuko tayari kutusaidia endapo Waziri utamsaidia. Msaidie Engineer atusaidie jambo hilo la makalavati, atusaidie ahadi ya Mang’ula Kona. Mheshimiwa Waziri, umefika Mang’ula Kona, umeona pressure ya watu, ahadi ya chama ya Mang’ula Kona. Nimeambiwa karibu shilingi milioni 300 zinatakiwa kukata ule mlima wa hifadhi ambao Rais ametupatia kwa nia njema ya kuondoa kero ya wananchi. Mheshimiwa Waziri tusaidie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii na mimi kuchangia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Hapa leo nachangia, pamoja na ushauri mwingine, lakini jambo langu kubwa ni moja tu la mgogoro wangu wa ardhi kule Ifakara, Kata ya Mlabani ambao unahusisha eneo la Baba Askofu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kabla ya kwenda huko, naomba nikishukuru Chama cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sera nzuri tunazoendelea nazo kuhusu ardhi. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri waendelee kusimamia sera hizi kwa sababu tunavyotembea katika nchi jirani tunaona huko mabalaa, kwamba ardhi huko katika nchi za jirani ni ardhi za watu, lakini sisi Tanzania ardhi bado ni mali ya umma na ni mali ya Serikali. Hili ni jambo la kijamaa kabisa na kwa sisi wajamaa tunataka liendelee kuwa hivyo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa Rombo kule kama DAS, nilikuwa navuka jirani pale Kenya, unaona kwamba mwenye kipande cha ardhi anakuwa kama Mungumtu, kwa hiyo sisi Tanzania ni muhimu sana tukaendelea nalo hili kuliweka katika misingi kabisa kwamba litakuwepo miaka dumu daima dumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwa Jimbo la Kilombero, Wilaya ya Kilombero, Halmashauri ya Mji wa Ifakara, kwa mkakati wa Serikali wa hatimiliki. Katika jimbo langu sehemu kubwa sana za vijijini wamepewa hatimiliki na baada ya kupewa tu zile hatimiliki za kimila, ardhi imepanda thamani sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ambayo tunayo ni kwamba wananchi hawakupewa elimu ya kutosha kwamba wanavyouziana zile ardhi kuna utaratibu wa kisheria wa kufuata ili umiliki utoke katika kaya au mila kwenda kwa mtu mwingine. Kwa hiyo ombi langu kubwa kwenye jambo hili ni kwamba, lazima elimu ya kutosha itolewe kuhakikisha kwamba wanaambiwa maana ya hati ya kimila ni nini na wanavyotaka kuuziana wanauziana kwa namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunakushukuru Mheshimiwa Waziri, tunaishukuru Wizara kwa mikopo ya Halmashauri. Halmashauri ya Mji wa Ifakara ilipata fedha milioni 250 ambazo kwa kweli tunashukuru sana Wizara yako kutupatia fedha hizi angalau mmethubutu na mmeanza kuonesha. Changamoto kubwa katika jambo hili ni kwamba upimaji wa viwanja katika Halmashauri zetu malengo yake ni nini, pamoja na kupanga Miji lakini kitu kingine ni kwamba inasaidia watu wasio na uwezo vijana kupata viwanja vya kujenga. Sasa lazima Halmashauri ifikie kuongeza mapato lakini inaongeza mapato kwa kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona wananachi wangu hasa vijana wakilalamika fedha gharama ya mauzo ya viwanja ni kubwa, nimekusikia kwenye speech yako Mheshimiwa umezungumza umesema hapa gharama hizi ni kubwa. Vijana wetu wadogo, vijana wetu ambao wanafanya biashara kama watoto wa fundi cherehani, nywele zao za kipilipili, kiwanja cha milioni tatu atanunua wapi? Kiwanja cha milioni mbili atanunua wapi? kwa hiyo lazima kuna maeneo na kule kwetu kuna mashamba makubwa ya bei rahisi vipimwe viwanja vya laki tano, milioni na muda wa kulipa uwe mrefu hata kama ni mwaka miezi sita. Mtu anapewa siku 90 alipe milioni mbili, milioni mbili na nusu watu hawawezi wanaacha viwanja na viwanja vinabaki kwa akina Asenga tuna watu wengine. Wale vijana wadogo kwa mfano Hansi wa Kidatu, Maisha wa Lumemeo, Sande, Mijije, wakina Kalyoma, wakina Mido hawa ni vijana wadogo sample ya Jimbo la Kilombero vijana maarufu ambao wanajulikana hawawezi hata siku moja kumiliki maeneo hayo kutokana na bei hiyo kuwa milioni tatu ama milioni nne.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusisitiza pia kwamba wekeni wazi, nimeona maoni ya watu hapa, ninachofahamu Mheshimiwa Waziri ni kwamba Tume hii haina mamlaka ya kupima, mamlaka ya kupima yapo kwenye Halmashauri zetu, kwa hiyo ufafanuzi huo uwekwe wazi ili muweze kuziwezesha Halmashauri kama Wabunge wengine walivyoshauri hapa. Halmashauri ndiyo ziwezeshwe zipime na ziangalie level na maeneo na watu wenye uwezo kama nilivyosema awali vipatikane viwanja, nchi hii viwanja vya laki tano vinaweza vikapatikana vijijini. Ifakara kule pimeni viwanja vya laki tano, tano, milioni, vijana na wakulima wale waweze kumiliki viwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anapata gunia zake tano akiuza alipe kiwanja, sasa mtu anauza gunia kumi bado haitoshi kulipa kiwanja, gunia kumi za mpunga. Sasa hii kwa kweli inakuwa ngumu matokeo yake wageni wanamiliki ardhi na wananchi wetu wa kawaida wanakosa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili ni kubwa Mheshimiwa Waziri, kuna mgogoro pale ambao mimi niliusikia tangu 2015, Kanisa la Roma chini ya Baba Askofu Libena, Baba Askofu Salutaris Libena tunavyozungumza hivi yuko Roma anapiga goti kuombea nchi yetu, anaombea Jimbo letu wako Roma huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgogoro tangu 2015 Rais alipokuja pale wakati ule aliambiwa mbele ya umati, kuna eneo kubwa la kanisa liko Ifakara Mjini karibu heka 1,000, kuna hekari kama 200 sikumbuki vizuri zimevamiwa na wananchi wamejenga, hawa ni wananchi wetu. Mwanzoni kanisa lilikuwa na msimamo wa kutaka watu wale wahamishwe, lakini mimi mwenyewe nimeenda kuzungumza na Baba Askofu. Baba Askofu Libena amekubali wananchi wale wapimiwe wamilikishwe apewe ardhi mbadala, ni jambo kubwa na ni jambo zuri na nimeenda Kata ya Mnadani nimekaa na wananchi wako tayari kupimiwa kulipa hati zao ile fedha ikatafutie Baba Askofu ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri fedha za kupima tu zinakosekanaje, sasa wewe ni Mama yangu, wewe msikivu, mimi hapa kweli nilete ukorofi wa kushika shilingi kwenye jambo hili, hata wananchi wangu watasema tena kwa Mama Mabula kweli mbona umekosa adabu. Nisaidie Kamishna Frank ni mtu mzuri, Kamishina wetu wa Ardhi Mkoa wa Morogoro mtu mzuri, ukimsaidia kwenye barua yake na barua yake nimekuletea mezani hapo ili Baba Askofu akirudi huko aliombee Taifa.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Asenga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ndulane.

TAARIFA

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huo anaozungumza Mheshimiwa Abubakari Asenga ni wa kweli kabisa na ulianza wakati nilipokuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Ifakara. Just imagine, Kata Tano ya Mji wa Ifakara ziko ndani ya eneo la Kanisa Katoliki Jimbo la Ifakara, kwa hiyo ni mpango muhimu naomba asaidiwe.(Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga taarifa unaipokea.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kabisa Kaka Ndulane nakushukuru sana Mkurugenzi wangu na ikimpendeza Mungu urudi tena pale kwa mara nyingine kuwa Mkurugenzi! Hiyo nimechomekea tu. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana kwa kweli alikuwa Mkurugenzi wetu wa Halmashauri yetu ya Mji wa Ifakara, yeye na Mbunge wa Mikumi Mheshimiwa Dennis Londo naye alikuwa Mkurugenzi pale wanajua mgogoro huu, nasi Wakurugenzi wetu wana bahati ya kuwa Wabunge. Kwa hiyo hawa wawili walikuwa Wakurugenzi na sasa hivi ni Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka kusema ukweli kwamba hili jambo ni very serious kabisa na tunashukuru Baba Askofu asije akabadilika kama amekubali kutoa ardhi hii kwa wananchi wale waliovamia na ameweka mpaka kabisa hawaruhusiwi kuendelea kuvamia tena maana pale kuna hospitali kubwa ya kansa amejenga, Good Samaritan, kuna hospitali ya St. Francis katika hilo eneo ya Rufaa ya Kanda, sasa wananchi wale hawawezi kuendeleza, hawawezi kupata mikopo, kwa sababu ardhi ile siyo ya kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo Mbunge mwenyewe nimetafuta hela nimepeleka katika Kata ya Mnadani fedha za zahanati, hatuna eneo la kujenga zahanati Baba Askofu anasema mpaka mmalize mgogoro wangu ndiyo nitawakatia eneo la kujenga zahanati. Kwa hiyo, maendeleo katika Kata ya Mnadani na Ifakara kwa ujumla yanakwama kutokana na mgogoro huu, viwanja hivi ni takribani elfu kumi tu, wananchi wale wapimiwe wapate hati zao waweze kwenda kukopa huko waweze kufanya maisha yao vizuri, tupate baraka za Baba Askofu, maana Baba Askofu unajua akishavaa madude yake yale anatisha Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, tunakuomba sana utusaidie jambo hili liishe na mimi sitaki kukukera hapa wala kuongea sana muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimechangia ardhi kwa sababu ya agenda hiyo moja kubwa na Baba Askofu aliniambia sijui kama mlisoma wote anakufahamu vizuri, sasa mimi napata mashaka wewe Waziri huwezi kumsaidia Baba Askofu kwenye jambo la haki kama hili, mimi nataka kusikiliza majibu hapa leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, namimi nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia bajeti yetu ya Wizara ya Fedha na kama walivyosema wenzangu na mimi nianze kwa kutoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani zangu za dhati kwa Katibu Mkuu wetu wa Chama cha Mapinduzi, chama tawala na wazi kabisa ziara zake zinaonesha utofauti mkubwa sana wa chama tawala kilicho madarakani na vyama vya upinzani kwamba anakofika maeneo kuna kero ya maji basi anawaita Mawaziri na viongozi wanatatua kero hizo hilo ni jambo jema na jambo zuri la kuungwa mkono, tunaomba sana viongozo wote na watumishi wote wa Serikali kuhakikisha wanaenda sambamba na maelekezo ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo namshukuru Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Dkt. Natu Mwamba amenisaidia na anaendelea kunisaidia kuhusu barabara yetu ya lami ya Ifakara – Kidatu. Barabara ile iko chini ya Wizara Fedha, amendelea kusaidia kutatua changamoto na mambo yanaenda vizuri na Mheshimiwa Waziri uliniahidi kwamba utatembelea barabara ile ya lami ili ukaone ule mkeka unavyopendeza pendeza sasa hivi maana yake wanachora ile mistari ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo niseme kabisa Mheshimiwa Mwigulu wewe katika kuwasilisha bajeti hatuna mashaka na wewe na ni wazi tu kwamba watozwa ushuru duniani hawajawahi kupendwa, kwa hiyo, kuna watu wengi wanaweza wasipende lakini kazi yako yenyewe hiyo ya kukusanya mapato kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu ni kazi ambayo kwa vyovyote vile huweza kupendwa na watu wote. Mtu akitaka kukupima tu kwa kigezo rahisi ni kwamba tulikuwa na malengo ya kukusanya shilingi trilioni 41.4; ukikusanya shilingi trilioni 41.4 ni sawa sawa na 100% na mpaka unawasilisha bajeti yako ya Wizara yako hii kwa taarifa za Aprili, 2023 umekusanya shilingi trilioni 32.4 ukifanya multiplication equation hapo tu utapata ni karibu 78% mmeweza kukusanya mapato yetu, ina maana na bajeti utekelezaji wake ni kama 78%, nawapongeza sana, tunawashukuru sana lakini lazima tuongeze nguvu ya kukusanya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano TRA walipanga kukusanya shilingi trilioni 23 lakini mpaka wanawasilisha walikusanya shilingi trilioni 18.8. Kwa hiyo ni imani yangu kwamba uwekezaji mkubwa unaendelea kufanyika utaongeza mapato katika Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti yako nimejaribu kuipitia pitia ina mambo mengi mazuri na kwa haraka haraka labda niseme kwamba suala la kufanya inflation libaki katika single digit ni jambo zuri, suala la VAT kuanza kufikiria kadirio la VAT litaanza kuanzia milioni 200 mpaka milioni 500 ni jambo zuri sana, kuweka kodi na kuongeza kodi katika mashine za kamari ni jambo zuri, lakini haitoshi, ongezeni kodi katika mashine za kamari ili ku-discourage vijana wetu kushinda katika mambo haya ya kamari na Serikali itaendelea kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umezungumza katika bajeti yako kuna suala la kuboresha adhabu za TRA zisiende moja kwa moja katika mazingira ya kutengeneza rushwa, ni jambo zuri. Tunaomba kuwe na mifumo imara ambayo itawezeshesha kupunguza mianya ya rushwa.
Mheshimiwa Spika, naunga mkono taarifa ya Mheshimiwa Waziri aliyoandika kwenye bajeti yake kuhusu kuwezesha Ofisi ya CAG iende zaidi kwenye kuzuia taratibu kuvunjwa, kuliko kwenye kuona makosa na kuyaandika makosa ya Serikali. Tunapongeza kuhusu kupunguza riba kutoka 16.5% to 15%. Tunaendelea kupongeza kama alivyosema Mbunge aliyetangulia kuhusu hiyo bilioni moja ya vifaa vya walemavu ni jambo zuri sana na Mwalimu Nyerere alishawahi kusema katika Taifa hili makundi ya watu yanayopaswa kutegemea watu wengine ni wazee sana, watoto na walemavu. Kwa hiyo, jambo hili ni zuri sana kwa walemavu wetu na nchi yetu itapata baraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amezungumza mchakato wa mikopo ya 10% ya Halmashauri. Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo ya kusimamisha mchakato ulivyokuwa awali, swali letu la msingi ukija kujumuisha hapa Mheshimiwa Waziri tusaidie, vijana, akinamama huko majimboni na kwenye halmashauri wanasubiri mchakato mpya wa Mheshimiwa Rais alioelekeza kuhusu mikopo ya 10% ya halmashauri utakuja kwa utaratibu gani, na utakuja lini? Kwa sababu sasa hivi wamekaa dilemma na wanasubiri na nimeona kwenye hotuba yako umesema kwanza jambo hilo litatolewa majibu, ni vizuri mkaanzisha mapema kwa mfano Ifakara tulishaanzisha kukopesha watu pikipiki, tumesimamisha zoezi hilo linaleta manung’uniko sana.

Mheshimiwa Spika, kilimo; mwaka jana tuliongeza bajeti ya kilimo kwa shilingi bilioni 954; mwaka huu naona Waziri Bashe umempa shilingi bilioni 970; ni mapato makubwa, lakini ushauri katika suala la kilimo na tunashauri safari hii Waziri Bashe watuwahishie mbolea sisi wakulima, mwaka jana nia ilikuwa njema, lakini kwa kweli mbolea ilichelewa kidogo kuna baadhi ya maeneo ikaleta manung’uniko. Tunaomba Wizara ya kilimo itazame Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Morogoro ni ghala la Taifa, Mkoa wa Morogoro hata ukipeleka mradi wa umwagiliaji hauna haja ya kuchimba kisima, vyanzo vya maji vipo.

Kwa hiyo, tunamuomba Waziri wa Kilimo atusaidie kuangalia Mkoa wa Morogoro ni ghala la Taifa na sisi tunaongoza nchi nzima katilka kilimo cha mpunga na miwa ya sukari. Tunamshukuru Waziri Bashe ametutengenezea kitalu pale Illovo cha mbegu za miwa, nafikiri mbegu hizo zitaenda kwa wananchi na wakulima wa muwa watapata mbegu nzuri kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamuomba Waziri wa Kilimo, Waziri Bashe mpunga safari hii hautakauka kwa sababu hakuna jua la kutosha. Teknolojia ya kulima kwa mpunga kuanika kwenye majamvi ilishapitwa na wakati, Waziri wa Fedha tusaidie kuingiza mashine hizi kwa rahisi zikakaushe mpunga. Mpunga safari hii hautakauka, Ifakara kuna shida ya jua, tunaomba mashine hizi ziende kwa wakati.

Namshukuru sana Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Bashe alinipelekea timu ya watu kuanza mchakatio wa uaratibu wa kununua mpunga kwa Ifakara pale utakaosababisha wakulima kuuza mpunga kwa Serikali kwa bei nzuri kabla ya walanguzi hawajafika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo kubwa kwenye kilimo na ushuru hapa nataka kusema vizuri. Serikali ya Awamu ya Tano ilikuwa ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi na hapa nasisitiza vizuri sana naomba Mheshimiwa Spika na Mawaziri wawili wa Kilimo na wa Fedha wanisaidie.

Mheshimiwa Spika, kuna kero kubwa sana sasa katika Wilaya za Ulanga, Malinyi na Kilombero kwa maana ya Jimbo la Mlimba, Ifakara, Malinyi na Ulanga kuhusu tozo ya chini ya tani moja. Serikali ya Awamu ya Tano na Mheshimiwa Rais Samia akiwa Makamu wa Rais alizunguka kwenye kampeni akasisitiza tumeondoa tozo ya chini ya tani moja kwa wananchi. Katibu Mkuu wa CCM Comrade Chongolo amepita juzi ameulizwa na wananchi Ifakara akasema katazo hilo halijaondolewa, lakini wananchi wanatozwa geti la Idete, wanatozwa geti la Ulanga na mpaka mkaa wanapimiwa kilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waziri semeni jambo hili, mwakani tuna uchaguzi wa Serikali za Mitaa, hili jmbo linatia hasira wananchi message zao wanazotuma huku ni hatari kabisa, naomba sana mlisemee jambo hili je, limefutwa na kama limefutwa toeni tamko tumefuta, chini ya tani moja watu wanatozwa. Zamani wakati wa Serikali ya Awamu ya Tano hakukuwa kuna mambo ya barua na urasimu, kwa nini sasa hivi unarudishwa urasimu mwananchi aje na barua, sijui aje na nini, mbona huko nyuma haikuwepo? Hili jambo linamchafua Mheshimiwa Rais na hapa nimelisema kwa kifupi linachafua kweli kweli, wachukue hatua waseme wamerudisha au wamefuta? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nataka kusema kuhusu TASAF. TASAF mmekuja na mradi mzuri sana wa wazee wetu kujishughulisha kwenye barabara za mitaro. Kila siku Mbunge ukiamka unakutana na suala la TASAF, TASAF fedha zao pelekeni. Mtu akichimba mtaro anapata shilingi 3,000 kwa siku mtu, amefanya mitaro miezi mitatu fedha hazijaenda, watu wanalaumu, watu wanalalamika naomba sana Mheshimiwa Waziri tusaidie kupata majibu haya ili nia yako njema ya kuendelea kupunguza kero na tozo kero kwa wananchi iendelee kuwa nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho ni kusisitiza kuhusu madeni, mimi nipo kwenye Kamati ya Miundombinu, Mheshimiwa Waziri tunakuomba bajeti yako tutaipitisha hapa vizuri kabisa, tunaomba wakandarasi katika Kamati ya Miundombinu tunaona kuna wakandarasi wa ndani na wa nje wanadai na madeni yenye riba, tunaomba sana myalipe. Kuna kampuni tumekutana nayo Dar es Salaam ya Mtanzania ESTEN inajenga barabara pale akina Mzee Giri, ni Tanzania hajalipwa, kuna kampuni tulikutana nayo ya CHICO lipeni makampuni haya ili yaweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nataka kusema kuhusu ukurasa wa 42 alichosema Waziri. Jambo la msingi sana Mheshimiwa Waziri amesema anaomba viongoizi wote katika nchi hii kuchukua hatua za haraka kuhusu uzembe wa miradi inayoiua fedha, watu wasisubiri taarifa ya CAG, wasisubiri mwenge, wala wasisubiri viongozi wakuu. Hili jambo tunataka tuliunge mkono. Kama tutakuwa tunapeleka fedha na Mheshimiwa Rais anatafuta fedha zinaenda kwenye halmashauri hakuna usimamizi wa kutosha, tunacheka na watu itakuwa hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la kwanza Serikali iendelee kuboresha maslahi ya watumishi, wakuu wa idara na wote wanaodai madeni, iboreshe maslahi ya Madiwani iwape vyanzo vya kutembelea Madiwani wakakague miradi, tuwasikilize Madiwani wetu wanasemaje. Nasema katika Halmashauri ya Ifakara mmeleta pesa kibao pale lakini miradi hohe hahe, anasema RC, anasema DC, hatuna hata engineer wa ujenzi, mama kaleta shilingi bilioni moja hospitali ya Halmashauri, kuna shilingi milioni 500 za Kituo cha Afya Mbasa, kuna shilingi milioni 500 za Kituo cha Afya Msolla Station, madarasa 120. Sisi na wenzetu waliopewa pesa hapaeleweki. Kwa hiyo, tutaendelea kusisitiza, atakayekasirika akasirike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2022/2023. Nami kama walivyosema Wabunge wenzangu hapa, napenda kuendelea kuwapongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha bajeti hii vizuri kabisa na kuwasilisha kazi inayoendelea ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Nawashukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, kaka yetu Emmanuel Tutuba ambaye kwa kweli ni Katibu Mkuu msikivu sana na usikivu wake sisi tumeuona katika ufuatiliaji wa Barabara yetu ya Ifakara – Kidatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema kwenye bajeti hii kuna mazuri mengi sana, nikisema tutumie muda hapa wa kuyasema hayo mazuri tutamaliza dakika zetu, lakini tunaenda kutaja mazuri huku tukichangia.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, mimi kama Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuna mambo ambayo tunataka tuyapongeze na tuiombe Wizara ihakikishe kwamba, bajeti hii inafanikiwa na mambo haya yanafanyika, ili Serikali zetu za mitaa ziweze kufanya vizuri zaidi. Jambo la kwanza, nimemsikia Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti yake na nimesoma, anasema kuhusu uboreshaji wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani hasa katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, sisi katika Kamati ya LAAC maeneo mengi tumepita tumekuta kwamba, kitengo hiki ni kama kimekufa. Ni kwamba, ni kitengo tegemezi kwa Mkurugenzi ambaye wanamkagua na kumshauri. Sasa kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni wazi kwamba, kinaenda kuboreshwa Kitengo hiki cha Ukaguzi wa Ndani na kitakuwa indicator kubwa kwa CAG anavyoenda kukagua katika halmashauri zetu. Hilo ni jambo la msingi sana na tunamwomba Mheshimiwa Waziri kwa kweli kiboreshwe kama alivyosema, watafute fedha katika bajeti hii wahakikishe wanamwezesha CAG, kama walivyosema wamempa asilimia mia ya bajeti yake, basi na Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kwa Taifa na katika halmashauri kiende vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukomo wa bei. Sisi katika hesabu za Serikali za Mitaa huko, tenda na mambo mbalimbali, tumeona kwa kweli kama kuna sehemu hela zinapigwa basi ni katika tenda mbalimbali hizi za halmashauri zetu. Tumemsikia Mheshimiwa Waziri kasema kwamba, utaratibu wa ununuzi utakuwa na ukomo wa bei usiotofautiana sana na soko; basi tunashukuru na tunapongeza hatua hii itaokoa sana fedha za Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, mengine wamesema katika TEHAMA, mimi bado nasema TEHAMA ni muhimu sana katika dunia ya sasa ya sisi vijana. Hatuwezi kwa kweli, kuendelea kuogopa TEHAMA, tufanye mikutano, Mabaraza ya Madiwani, imeshindikana Waheshimiwa Wabunge kushiriki vikao vyote vya Mabaraza ya Madiwani. Pamoja na maelekezo mbalimbali ya Serikali kwamba, lazima tushiriki kama Wabunge katika vikao hivyo, lakini imeshindikana kwa sababu lazima vitaingiliana na ratiba za halmashauri, vitaingilina na ratiba za Bunge. Kwa hiyo, kwa kutumia hiyo TEHAMA itatusaidia sisi kushiriki, kwa hiyo, mimi naunga mkono jambo hilo lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa tuliona matatizo makubwa ya kurejeshwa fedha katika miradi. Ikishafika 30 Juni, Wakurugenzi wa Halmashauri wanakuwa wanahangaika, wanahaha kuhakikisha kwamba, wanawahi hata saa nyingine kulipa bila utaratibu kwa sababu, fedha zitarudi kwenye mfumo. Tumemsikia Mheshimiwa Waziri anasema hilo halitakuwepo kwa sababu, hilo ni kuwaadhibu wananchi ambao hawana hatia.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine zuri ni Usajili wa Wakuu wa Taasisi kwa ushindani, kuwapa malengo ya taasisi na malengo yanayopimika, ni jambo zuri, kufuta ada ni jambo zuri, kuongeza bajeti ya kilimo kutoka bilioni 294 mpaka 954, ni jambo zuri. Hapa kwa kweli, nitapasemea huku mbele kwa sababu, naona hili ni jambo kubwa sana ambalo ningekuwa na uwezo ningemwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha, basi tarehe Mosi, Julai au tarehe 2 Julai, ampatie Waziri wa Kilimo hizi fedha zote ili akatekeleze bajeti ya kilimo kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mazuri ni mengi sana, lakini napenda kusema wazi kwamba, mimi kama kijana siwezi kuunga mkono suala la kuondoa 5% katika 10% ya mikopo ya vijana katika halmashauri. Kama walivyosema Wabunge wengine hapa haiwezekani, kwanza haieleweki. Mimi nina Ilani ya Uchaguzi nimesema hapa nimeisoma hii Ilani inaahidi kuhusu hiyo 10% na sisi tunatekeleza hii ilani sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Godfrey Chongolo, amezunguka hata juzi anasema kuhusu hiyo 10%. Sasa wale waliofanya ubadhirifu kukopa fedha hizi bila utaratibu wasisababishe fedha hizi zikaondolewa kwa vijana, Serikali iwawajibishe tena hata kule Kilombero, Morogoro tunao. Wawajibike waende Mahakamani wachukuliwe hatua wawajibike. Machinga ni watu wazuri sana, lakini tutafute vyanzo vingine mbadala vya kuendeleza masoko ya Machinga.

Mheshimiwa Spika, halmashauri ambayo ina mapato ya bilioni moja ukitoa 10% milioni 100, ukitoa 5% ni milioni 50, itajenga soko gani na 50 zinazobaki zitasaidia vijana wangapi? Kwa hiyo, nafikiri Mheshimiwa Waziri arekebishe katika paper yake hapo tuachane na jambo hili tuendelee kutekeleza ilani kuhakikisha kwamba, tuna 10% ile ya 4:4:2 kama ilivyo kawaida.

Mheshimiwa Spika, ziko falsafa zinatufundisha, pamoja na utekelezaji wa bajeti ya Mheshimiwa Waziri, kufikiri nje ya box zaidi na kutazama bajeti zetu nyuma. Sidhani kama kuna bajeti ilishawahi kuja hapa Bungeni haikuwa na shamrashamra? Bajeti zote zina shamrashamra, bajeti zote zinapendeza, bajeti zote tunasema ni sawa, tunazisema vizuri, lakini tunafanya tathmini ya miaka mitano nyuma mathalani. Tunaweza tukasema korona hii ya juzi, vita ya Ukraine, lakini miaka mitano nyuma utekelezaji wetu wa bajeti ni asilimia ngapi? Ni vitu gani vinatukwamisha katika kuhakikisha hatufikishi asilimia 80 ya utekelezaji wa bajeti? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa si lazima Mheshimiwa Waziri, sijui kama hii 41 trillion ambayo tunaitafuta sasa hivi tutaipata na tutatekeleza kwa 100% ama asilimia 80 ama asilimia 90 sina uhakika, lakini kufikiri nje ya box ama falsafa ya kusema jikadirie kihalali, kama anavyosema Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson; lazima tujikadirie kwa kujiuliza miaka 10 nyuma je, tunajitazama kweli sisi kama Watanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu, hatuwezi kutaja bajeti zinazoongezeka tu tuonekane nchi yetu inaendelea, lakini utekelezaji haufiki 80%, lazima tujikadirie kihalali na ni lazima tufikirie nje ya box. Tazama 2016/2017 ilikuwa trilioni 25; mwaka unaofuata 2017/2018 ikawa trilioni 26; mwaka 2018/2019 ikawa trilioni 28; mwaka 2019/2020 ikawa trilioni 29; mwaka 2020/2021 ikawa 32; mwaka 2021/2022 ikawa 39; mwaka 2022/2023 tuna trilioni 41. Inaongezeka ndio, ni vizuri, lakini hata katika economics ya form five na six katika economics ya diploma, yuko baba yangu Mkenda atasema, walitufundisha aina tatu za bajeti na ziko nchi zinatumia aina nyingine za bajeti. Sasa kama nchi yetu tangu ipate uhuru inatumia aina moja ya bajeti, deficit budget kwamba, matumizi tunapanga mengi kuliko mapato, tuachane nayo na kwa ushahidi kwamba, hatufikishi asilimia 80. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wametufundisha kuna balanced budget kwamba, zipo nchi zinapanga matumizi sawa na mapato yao na kwa sababu, zina mipango ya maendeleo ikitokea fedha za IMF, World Bank na misaada mingine wanachukua, wana-click katika ile check list kitu gani tulipanga kufuata tukifanye tuingize pale na Watanzania ni waelewa, hiyo ni balanced budget kwamba, tunapanga matumizi sawa na mapato yetu.

Mheshimiwa Spika, tumefundishwa kuna surplus budget. kwamba, unaweza ukapata mapato mengi ukapanga matumizi kidogo, lakini ya mwisho hii deficit ambayo tunaing’ang’ania ya matumizi mengi kuliko mapato, ufanisi wake miaka mitano nyuma unaonekana haufiki 80%. Kwa hiyo, nasema kufikiri nje ya box, kujikadiria sijui hii 41 trillion iko wapi kwa sababu, tunakopa tena five trillion hapa tunaongezea kwenye hii bajeti. Hatuna uhakika kwa sababu, majanga yamekuwa majanga, Covid-19 itakuja Covid-42 itakuja ngapi, sisi tunaamini hizo nchi zitatupa hizo fedha tuongezee kwenye bajeti utekelezaji ukija hapa asilimia 60, asilimia 70 au asilimia 80. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania ni waelewa. Mathalan tunapata shilingi trilioni mbili kwa mwezi kutoka TRA. Kwa mwaka ni shilingi trilioni 24, mapato yasiyo na kodi shilingi trilioni sita, una shilingi trilioni 30. Mheshimiwa Waziri panga mipango yako katika shilingi trilioni 30 tuletee hapa tutoe vipaumbele vya kutekeleza asilimia 100. Peleka kwenye hizo Wizara kama tano za mfano, tutekeleze asilimia 100, tusonge mbele, watu wataelewa. Halafu on the way tukipata fedha za World Bank, UVIKO na kadhalika, tunakaa kama Bunge tunaeleweshwa, tunaendelea na mpango wetu wa Serikali wa miaka mitano. Hilo Watanzania watalielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mathalan tunahitaji shilingi bilioni 954 hii ya kilimo, hata Mheshimiwa Waziri Bashe apewe kesho. Ila kwa mfumo wa Wizara zote kupewa pewa fedha hivi, hakuna Wizara itatekeleza kwa hundred percent. Vipaumbele vya Taifa letu ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nasisitiza, katika kilimo hapa ni pazuri sana na vipaumbele vya Taifa vichache vya kutekeleza kwa asilimia 100 kwa kutegemea mapato yetu tuliyokuwa nayo ni ya uhakika, kuliko kwenda mwakani kwa sababu tuna fourty one, lazima tujikadirie kihalali. Tuna fourty one leo, mwakani tunataka tuwe na fourty five billion, how tunaipata na uchumi wa dunia unarudi chini?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri siyo lazima kufikiria zaidi ndani ya box tangu uhuru mpaka sasa hivi, ndani ya box tu, kwamba sisi surplus bajeti mwaka 2021 ilikuwa fourty one, tukiongeza fourty five ndiyo tutaonekana tunaendelea, no! Tuna uhakika gani na mapato ya nchi yetu ya uhakika ya TRA na mapato yasiyokuwa na kodi tukijumlisha tupange mipango hiyo, Watanzania watatuelewa.

Mheshimiwa Spika, uzuri wake, Mheshimiwa Rais Samia sasa hivi amesema vizuri sana, amekuwa muwazi na anakuwa kama ana mashaka na mambo ya mikopo. Wakati wa mikopo hii ya one trillion ya COVID amezungumza wazi, tumieni vizuri mikopo hii, Watanzania watalipa. Juzi tulikuwa tuna miradi 28 ya maji, amezungumza hivyo hivyo, amesisitiza kwamba tutunze sana fedha hizi za mikopo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashauri sana kwa kumalizia kuwa Mheshimiwa Waziri mwakani kama hii haitafika eighty percent, basi tufikirie bajeti ya kupanga kutokana na matumizi yetu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, tujikadirie tuje nje ya box. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kupata dakika tano za kuchangia Mpango wetu wa Maendeleo Awamu ya Tatu. Ukiusoma ule mpango na hotuba ya Mheshimiwa Waziri utaona wazi kwamba umejikita katika shabaha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza unasema, kuhakikisha kuwa uchumi wetu unakua kati ya asilimia 6 na asilimia 8. Pili, kuhakikisha kuwa mapato ya Halmashauri zetu yanatoka asilimia 15 mpaka 16.8 ya pato la Taifa. Tatu, ni kulinda mfumuko wa bei (inflation) tubaki katika single digit ya asilimia 3 mpaka asilimia 5. Nne, kuendelea ku-maintain hifadhi ya fedha za kigeni walau kwa miezi minne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Kilombero kazi yangu kubwa ni kuwakilisha mawazo na maoni yao kuhusu Mpango huu. Mathalani, ili kufikia shabaha hii ambayo imeandikwa hapa na Mheshimiwa Waziri katika Mpango wetu wa Halmashauri kujitegemea kwa hadi asilimia 16.8, kama walivyosema Wabunge wenzangu wengine waliotangulia, ni wazi kwamba tukijikita katika kilimo tunaweza kufanikisha jambo hili. Kwa mfano kwenye zao la miwa ya sukari, Mheshimiwa Rais alishaelekeza kwamba nchi yetu ijitegemee kwa sukari na wakulima wetu wamewekeza katika zao hili. Hata hivyo, taarifa za Wizara katika Mpango zinasema tunatupa miwa tani milioni moja kwa mwaka. Uwekezaji wa miwa peke yake katika Jimbo la Kilombero utakuza mapato ya Halmashauri kwa two percent na hapo tayari tutakuwa tumefikia shabaha ya pili ya Mpango wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni miradi mkakati katika Mpango wetu wa Maendeleo. Mathalani, Serikali imesema itaendelea kuwezesha miradi mkakati ili kuziwezesha tena Halmashauri. Jimbo langu la Kilombera na wananchi wetu, tayari wana andiko kuhusu soko na namna gani soko na stendi zitakavyokuza mapato ya Halmashauri kufikia shabaha ya Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne ni kilimo kwa maana ya mpunga. Amezungumza mchangiaji wa kwanza, Mheshimiwa Prof. Muhongo hapa kwamba tuwekeza katika kilimo ili tuweze kuendelea. Amesema pia watu duniani ni karibu bilioni saba na nusu ya watu duniani wanatumia mpunga. Jimbo la Kilombero linazalisha mpunga kwa zaidi ya asilimia 70. Katika Mpango huu endapo tutawekeza katika kilimo cha mpunga kwa kiwango kubwa, tunaweza kufikia shabaha ya Mpango huu ambao ni kukuza mapato ya Halmashauri kutoka asilimia 15 mpaka asilimia 16.8. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengine ni mambo ya miundombinu. Mheshimiwa Waziri kama ulivyozungumza, mara kadhaa tumesema katika kilimo ambacho tunataka kukikuza ili tuweze kufikia maendeleo ya ukuaji wa uchumi kwa asilimia 6 -8 lazima tuwe na miundombinu ya kutosha ya kusafirisha mazao ya wananchi na wakulima wetu vijijini. Ndiyo maana mara nyingi tukisimama hapa tunazungumzia habari ya barabara ambazo zimekuwa historia kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tukajikita pia katika kuboresha miundombinu yetu. Mathalani katika Jimbo la Kilombero, tuna barabara hii tunaizungumzia mara zote ya Ifakara – Kidatu ambayo itaunganisha Wilaya za Ulanga, Malinyi, Mlimba, Kilombero, Mikumi na Mkoa wa Morogoro. Hatimaye itawawezesha wakulima wetu kuuza bidhaa zao vizuri na kuchangia katika pato letu la Taifa na kuchangia katika Mpango wetu wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni fursa mbalimbali ambazo zinatokea katika kilimo kwa kuwakumbuka wananchi hawa. Matahlani, alizungumza mama yangu mmoja Mbunge wa Morogoro hapa kwamba zamani kulikuwa na huduma za matrekta katika vijiji vyetu. Katika Mpango huu wa Maendeleo ambao tumesema asilimia karibu 80 ya wananchi ni wakulima, endapo tutarejesha matrekta katika vijiji vyetu tunaweza kufikia malengo yetu na hasa kwa Mkoa wa Morogoro ambao mimi ni Mbunge katika moja ya majimbo yake na umechaguliwa kuwa ghala la taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, endapo mpango wa maendeleo utakumbuka hii mikoa ambayo ni ghala la taifa, automatically tutakuza kilimo na tutapata maendeleo ya haraka na kufikia shabaha ya Mpango ya uchumi kukua kwa asilimia 6 mpaka 8, mapato ya Halmashauri kutoka asilimia 15 mpaka 16.8 kwa pato la Taifa, tutalinda mfumuko wa bei na tunaweza kuuza mazao yetu nje kupata fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nawasilisha na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii kama ya bahati nasibu kuchangia mpango wetu ambao lengo la mpango huu ni kuwa na uchumi wa viwanda ambao unaenda sambamba na kilimo. Na unavyosema kilimo katika nchi yetu huwezi kuacha mikoa mikubwa ile ambayo inajishughulisha na kilimo na mkoa mmojawapo ni Mkoa wa Morogoro ambao unashikilia takribani asilimia 7.7 ya ardhi ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa sisi kwa kifupi kabisa tunaomba Mheshimiwa Waziri kwamba, katika mkoa tulikaa tuna mpango mkakati wa maendeleo ya kilimo, mifugo na uvuvi Mkoa wa Morogoro. Kitabu hiki kina kila kitu, kimeelezea fursa mbalimbali ambazo zitasaidia sana Mheshimiwa Waziri kufika katika malengo yake ya mpango. Na tumesema fursa zilizopo katika mpango huu tukiunganisha mpango na kitabu ambacho mwaka 2020 tulikiombea kura kwa wananchi, yaani Ilani ya Uchaguzi.

Mheshimiwa Spika, kama kweli tunataka mpango huu ufanikiwe katika kupanga ni kuchagua mara zote nimegusa kwa mfano suala la kilimo cha miwa tu peke yake. Nimesema kuna miwa Kilombero tani takribani 300,000 zinalala zinasalia na ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Baba yangu Profesa Mkenda, tuliendanaye ameona hali halisi. Wawekezaji wale katika Kiwanda cha Ilovu cha Kilombero cha sukari kwa mfano kwa sasahivi wanatafuta takribani bilioni 400 kukuza, kupanua kile kiwanda kiweze kuchukua miwa ile tani 300,000 ambayo miwa hiyo tani 300,000 ikichakatwa itazalisha tani elfu 30 mpaka 35 za sukari.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu leo inaingiza tani 40,000 za sukari, tukiweza kuchakata miwa ile ambayo ipo yani sidhani kama kuna mpango ambao unaweza kwenda kutuelekeza sehemu nyingine kwenda kupanda miwa, kuanzisha mradi mpya, lakini huku kuna watu akina Balozi Mpungu Mwenyekiti wa Bodi wanatafuta bilioni 400, bilioni 500 wapanue kiwanda kitumie miwa ambayo tayari ipo ya wananchi na nchi yetu isiingize tena sukari. Maana hapa keshokutwa tunaenda kwenye uhaba wa sukari watu wataanza kuingiza sukari, tunaingiza tani 40,000 wakati miwa inabaki tani 300,000. Kwa hiyo, nisisitize tu Mkoa wa Morogoro una fursa nyingi. Kwenye kitabu humu tumesema kuna mashamba 12 makubwa. Tunahitaji bilioni 100 tu kwa mwaka huu akitutafutia Mheshimiwa Waziri tuta-push mpango wetu.

Mheshimiwa Spika, tuna hekta zinazofaa kwa kilimo milioni 2.2 tunatumia asilimia 43 tu, 900,000 ndio tunazolima. Tuna hekta zinazofaa kwa umwagiliaji 323,000 zinafaa kwa umwagiliaji tunalima 28,000. Sasa kam kweli tuna mpango tunataka ku-boost uchumi wetu wa nchi yetu na tunasema uchumi wa viwanda tunauunganisha na kilimo basi Mkoa wa Morogoro utazamwe, Wizara na wasimamizi wote wa sera watusaidie kupata fedha kuongezea halmashauri zetu fedha ili tuweze ku-deal na kilimo.

Mheshimiwa Spika, nimesema kwenye miwa, kuna mpunga, amesema hapa brother wangu, pacha wangu Mheshimiwa Kunambi. Upande wake sasa hivi jeshi linatengeneza mradi mkubwa sana wa umwagiliaji. Kwa hiyo, kwa nafasi hii nilikuwa naomba baadaye nitamkabidhi kwa sababu, dakika ni chache, nitamkabidhi Mheshimiwa Waziri kitabu hiki atusaidie.

Mheshimiwa Spika, mwisho kuna miradi mkakati, sisi Halmashauri yetu ya Mji wa Ifakara ime-qualify na tumeomba takribani miaka miwili mitatu iliyopita kwamba, kama malengo mojawapo ni halmashauri zijitegemee, sisi tume- qualify kupata soko pale Mjini Ifaraka ni mji mkubwa sana. Kwamba, soko lile tukipewa zile fedha tulizoomba takribani bilioni tano zitarejeshwa ndani ya miaka mitano na halmashauri yetu itapata mapato makubwa. Tunaomba hilo Mheshimiwa Waziri nalo alifikirie.

Mheshimiwa Spika, la pili. 2018 Mheshimiwa Rais, Hayati, alivyokuja kule kuna kiwanda kikubwa kilikuwa cha chuma, cha vifaa vya reli kina hekta 250-kina majengo, ma- hall kabisa na mashine zipo ndani yake. Tangu kimerudishwa kile kiwanda kipo idle.

SPIKA: Kiwanda cha Mang’ula?

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, cha Mang’ula cha chuma kimekuwa pori. Kuna wawekezaji wamepatikana huko nimemwambia Waziri wangu Mheshimiwa Profesa Mkenda amenisaidia kuna baadhi amewaona, Mheshimiwa Profesa Mkumbo pia, tuwasaidie tuwaruhusu kama wako tayari kuwekeza hata wakiwekeza kiwanda kidogo cha miwa watatumia hiyo miwa tani laki tatu.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ili nichangie katika Wizara ya Ujenzi. Kwa ukweli kabisa kwa dhati ya moyo wangu japokuwa nina mgogoro kidogo na barabara yangu kubwa kule iliyopelekea mpaka nikaa kwenye matope, lakini nimshukuru Mheshimiwa Waziri Injinia Chamuriho, mwezi Januari mapema kabisa alitenga muda wake, akaenda jimboni kwangu kwa dhati ya moyo, namshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Kaka Emmanuel Tutuba kwa kweli kuna vitu ambavyo vilikwama kuhusu barabara yetu ya Ifakara - Kidatu na juzi nilikuwa kule site amezungumza na yule mkandarasi, kwa hiyo naona dalili njema. Kwa kweli kwa dhati nimpongeze sana Katibu Mkuu huyu, nina imani atatusaidia kutatua changamoto za barabara yetu ya msingi sana kutoka Ifakara kwenda Kidatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua mgogoro huu Waziri wangu wa Ujenzi anafahamu fika kwamba barabara hii ni miongoni mwa barabara ambazo zimesainiwa na Wizara ya Fedha. Najua watu wangu wa ujenzi inawezekana kwenye mioyo yao hawajaridhika sana kwamba barabara hii imekuwajekuwaje Wizara ya Fedha wakasaini mikataba na wakati utaalam uko kwenye Wizara ya Ujenzi. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na wataalam wake na watu wa TANROAD wa Mkoa wanafanya kazi nzuri, wanafanya vizuri, watusaidie kuendelea kuifuatilia barabara ya Ifakara - Kidatu kwa sababu ndio barabara ya ajenda yetu kubwa ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikaa chini kwenye matope kwa sababu nilikaa na wananchi kuanzia saa tano usiku barabara ilikuwa haipitiki mpaka saa tano asubuhi. Ukiniuruhusu hata hapa Bungeni nitakaa endapo Waziri kwenye majumuisho yake ataniambia kwamba barabara hii
itakamilika kwa kiwango cha lami kama Naibu Waziri alivyowahi kujibu Bungeni hapa kwamba Oktoba safari hii itakamilika, ijapokuwa ni muda mfupi sana. Kwa hiyo ukiniruhusu nitakaa hata hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusisitiza nikae?

NAIBU SPIKA: Hapana hapana Mheshimiwa.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, huo ni msisitizo kwamba barabara hii tangu 2017 mpaka sasa hivi ni mvutano…

NAIBU SPIKA: Tutaweka utaratibu mzuri, usiwe na wasiwasi wale wanaotaka kumwonyesha Mheshimiwa Waziri kwa vitendo; kuna mzee wa sarakasi, kuna wewe unataka kukaa, kuna Mheshimiwa anataka kugalagala, tutafanya hilo jambo nje pale, tutaweka utaratibu. (Makofi/Kicheko)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika zangu zilindwe, kwa sababu dakika tano ni chache, ili nisishike shilingi na naomba uniweke kwenye orodha ya watu watakaoshika shilingi. Mgogoro huu tumeujadili wilayani, tumeujadili mkoani kwenye kikao mpaka cha RCC na Wabunge wa Mkoa wa Morogoro na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, ikaonekana kwamba mjenzi contractor na consultant wana mvutano mkubwa kuhusu barabara hii na unachangia kuchelewesha barabara hii. Sababu gani? Kuna nje ya nchi huko, walipata tenda pamoja wakagombana na wamekuja site wanagombana. Sasa tukashauriana, mmoja yule hasa consultant anatakiwa aondoke apishe ili kutafuta mtu mwingine wa kusimamia barabara ile ili iweze kwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefuatilia, inaonekana consultant kuna mkubwa huyo anamtetea na sitaki kumtaja jina lake hapa, lakini Mheshimiwa Waziri tumezungumza naye jambo hili na ameniahidi kwamba bado muda mfupi huyo consultant amalize mkataba ili twende vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano, kwa mfano barua ambayo mkandarasi ameandika kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha ambaye ameifanyika kazi kwa kiwango cha asilimia 90. Anasema kuchelewa kwa GN na Exemption ndani ya miezi 40 wamepata GN mara tisa, barabara hii haiwezi kukamilika na barabara hii ina mgogoro mkubwa sana na imeahidiwa na viongozi wa chama akiwepo Spika alipokuja jimboni kwetu kuomba kura. Sasa hili tusishikiane shilingi nataka majibu ya huyu consultant anaondoka lini? (Makofi)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, amefanya kazi miezi mitano. Nilindie dakika zangu.

NAIBU SPIKA: Kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Godwin Kunambi.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika nampa taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na mambo mengine, kilichofanya mradi huu uchelewe kwa muda mrefu ni kitendo cha Wizara ya Fedha kusaini mkataba na ikashindwa kujiombea exemption kitu ambacho kwa mujibu wa sheria hakiwezekani. Ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Abubakari Asenga, unaipokea taarifa hiyo

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa murua, taarifa bora kabisa. Kama nilivyosema nimewaomba watu wa Wizara ya Ujenzi waridhike kwenye mioyo yao japokuwa barabara hii ilisainiwa na Wizara nyingine na nina imani chini ya Katibu Mkuu mambo mengi yataenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine, ndani ya miezi mitano consultant amemwongezea contractor makalavati karibu kumi na tano, anazidi kutengeneza ucheleweshaji. Kwa hiyo namwomba sana Mheshimiwa Injinia Chamuriho, anisaidie, alibebe hili, awashauri watu wa Wizara ya Fedha, awashauri kwa sababu Waziri ni mtaalam, ameingia kwenye mikataba na ujenzi wa reli ya kisasa, viwanja vya ndege, kununua ndege, hii kilometa 66.9 itamshindaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwenye barabara hii, namwomba Mheshimiwa Waziri, angalau kule kijijini kwetu kila tarafa ina vituo vile vikubwa ambavyo vinafanywa kama masoko, watakavyoendelea na dizaini na marekebisho, watusaidie kuweka vile vituo na taa angalau za barabarani ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu wanakuja barabarani kuja kuuza ndizi, kuuza karanga kwa hiyo barabara hiyo ikidizainiwa ikawa na maeneo makubwa ya vituo itatusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii katikati ina kituo kinaitwa Mang’ula Kona. Hii Mang’ula Kona ni kona hatari sana pale ajali zinatokea mara kwa mara. Kwa sababu gani kuna kona? Ni kwa sababu kuna mita 50 kwa 100 za eneo la TANAPA zimeingia barabarani. Nimemwomba Waziri wa Maliasili na Utalii ameniambia anaweza kutusaidia, tunaomba atusaidie Injinia achonge apanyoshe pale ili kuondoka ile kona ambayo imeitwa kona, kona na inasababisha ajali za mara kwa mara. Kwa hiyo naomba sana Mheshimiwa Waziri anisaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kugusia kuhusu Kiwanja cha Ndege cha Ifakara. Kuna Kiwanja cha Ndege, ndege zinatua kwenye kiwanja kile cha vumbi, Mji wa Ifakara una mzunguko mkubwa wa pesa, wafanyabiashara wale wanaambiwa zikija ndege mara kwa mara, kwa mfano laki moja, laki mbili, waende Dar es Salaam watapanda, wataenda na mji wetu utaendelea kuboreka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa kabla sijasahau, niseme naunga mkono hoja za taarifa za Kamati zote tatu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nami napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi ambazo ametuletea katika Halmashauri yetu ya Mji wa Ifakara na Jimbo la Kilombero. Sasa hapa lazima tutofautishe kuletewa fedha na matunda ya zile fedha katika miradi ile.

Mheshimiwa Spika, ukienda huko kwenye kuona miradi kutokana na fedha ambazo Wizara ya TAMISEMI imetuletea na Mheshimiwa Rais ametuletea ni vitu viwili tofauti na ni vitu viwili mbalimbali. Napenda sana kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea Mkuu wa Mkoa wetu, Dkt. Malima na Mkuu wetu wa Wilaya, Dunstan Kiwobya. Waziri wa TAMISEMI na viongozi nataka niwaambie, kama sio huyu DC mpya aliyekuja, Wakili Dunstan Kiwobya, basi miradi yetu ingekuwa mibaya mara tatu. Huyu Mkuu wa Wilaya aliyekuja naye ameshaanza kuletewa chuki na hao ma-tycoon wa Halmashauri kwamba anaingilia mpaka kwenye kusimamia, mpaka kwenye kufunga taa usiku ili miradi iende. Kwa hiyo, pamoja na hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kweli, kwa mabadiliko haya ya kutuletea Mkuu wa Wilaya, yamesababisha angalau kidogo miradi ya Halmashauri tunaanza kuiona.

Mheshimiwa Spika, nitagusia upande wa TAMISEMI. Najua maeneo mengi sana yamesemwa kuhusu wizi na ubadhirifu, lakini nataka kusema kwenye TAMISEMI na Halmashauri kwa sababu nilikuwa Mjumbe kwenye Kamati ya LAAC, na tuliyaona mengi sana na mengine leo yanajirudia yale yale. Tulikuwa na Mwenyekiti wetu, mama pale katika Kamati ya LAAC.

Mheshimiwa Spika, nina imani sana na Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Mchengerwa. Kwa kweli, kwa dhati ya moyo wangu nina imani naye sana kwamba atafanya mabadiliko. Kwa nini nina imani na Mheshimiwa Mchengerwa? Kwa sababu, ameteuliwa tu, ameenda kule Lindi na Mtwara akazitaja Halmashauri ambazo miradi mibovu na miradi haiendi. Hata sijamlalamikia, hata sijamwambia, kataja huko kwenye vyombo vya habari, nikasema eh, Waziri ndio huyu sasa tumempata. Basi hatua zitachukuliwa na tutaona mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule kwangu, Mheshimiwa Waziri Mkuu, wameiba mpaka vile vifaa vya maafa ya mafuriko ulivyonipa. Mimi nimepata mafuriko Ifakara, nimekuja kwa Waziri Mkuu nimelia, naomba magodoro, naomba sufuria, naomba mablanketi. Mheshimiwa Jenista Mhagama akaniambia nakusaidia, Waziri Mkuu kaniambia nikusaidie. Nimeenda bohari, nimepakia vifaa, magodoro, blanketi, sufuria, na kadhalika, nimeendanavyo mpaka Ifakara. Namwambia Mkurugenzi, tugawie watu waliopata mafuriko vifaa hivi. Wameiba katika stoo ya Halmashauri bila kuvunjwa kwa stoo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nimemwambia DC wetu Dunstan Kiwobya akahakikisha, akathibitisha. Watu wameandikiwa barua rudisheni kimya kimya. Vingine Naibu Waziri wa Uchukuzi pale, Rais wa RedCross, Mheshimiwa David Kihenzile, RedCross nao walinipa, wameiba. Vifaa vya maafa wameiba Ifakara.

Mheshimiwa Spika, ukisema, chuki, na Wakurugenzi wengine wanaingia kwenye siasa wanasema huyu tunamsubiria 2025 tutashughulika naye. Wameiba. Hakuna mtu yeyote ameenda Polisi, magodoro yale na mablanketi yale yana ubora wa namna yake, wanaambiwa warudishe yale ya dukani hayaeleweki. Fuatilieni mtaona, hakuna hatua iliyochukuliwa. Kwa hiyo, nasema kwa dhati kwamba, nina imani na Mheshimiwa Mchengerwa kwa sababu bila kukwambia uliitaja Halmashauri yangu kuzembea katika miradi, kukamilika katika miradi nikajua utachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nikwambie, Mheshimiwa Rais na Wizara mmetuletea shilingi milioni 528 za kujenga sekondari. Mmeleta tarehe 25 mwezi wa Sita, juzi ndiyo ujenzi umeanza. Hakuna hata wiki. Ukifuatilia unaambiwa wanabishana wampe mkandarasi huyu, wampe mkandarasi huyu, mradi haujakamilika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nafikiri …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Asenga, ngoja nielewe vizuri hapo. Hizo ni hoja zako ambazo unataka Serikali isikie ama ziko kwenye taarifa ya CAG?

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, zipo kwenye taarifa. Nataka kusema kuhusu ubadhirifu katika Halmashauri ambazo Taarifa ya Kamati ya LAAC imesema hapa kuhusu kuchelewa kwa miradi na ubadhirifu katika Halmashauri. Ndiyo ninachokisema.

SPIKA: Haya.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Kwa hiyo, hiyo ni mifano nimetoa kwenye jimbo langu Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, nimetoa mifano ili kuthibitisha ukweli wa Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, mifano ndiyo hiyo. Miradi inachelewa. Kamati imesema, nami natoa mfano Ifakara mradi hela zimepelekwa tarehe 25 mwezi wa Sita, mradi umekuja kuanza tarehe 15 mwezi wa Kumi ambapo ndiyo tarehe ya mwisho kwa mradi kukamilika. Kwa namna hii hatuwezi kufika, hatuwezi kuendelea.

Mheshimiwa Spika, nataka kusema suala la vikao na sisi kuwa Wajumbe wa Kamati za Fedha na Mabaraza ya Madiwani. Waziri Ummy akiwa Waziri wa TAMISEMI hapa, hii hoja imetolewa hapa, alitoa maelekezo kwamba ni vizuri Wakurugenzi wakaongea na Wabunge wao namna ya kuandaa vikao hivi. Jambo hilo halijafanyika, lakini leo tunaweza tukawajibishwa sisi kwamba ni Wajumbe wa Kamati za Fedha, Wajumbe wa Mabaraza ya Madiwani, lakini wewe unatupangia hapa ziara za Kamati, unatupangia Bunge lako, kwa nini vikao hivi visifanyike hata weekend kwa umuhimu wa sisi kushiriki ili tuseme?

Mheshimiwa Spika, vinginevyo nataka nikwambie, kama hatuingii kwenye Kamati za Fedha hizi, na watu wanapanga ratiba tofauti na Bunge, wana malengo yao. Siyo kwamba watu hawajui kwamba kuna siku moja inaweza ikapatikana Mbunge akapata nafasi akashiriki Kamati ya Fedha, akashiriki Baraza la Madiwani, wanapanga wanajua, Mbunge akiwa hapa hili hatakubali. Hilo la kwanza. (Makofi)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa inatoka wapi? Mheshimiwa Mtaturu.




TAARIFA

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, sehemu pekee ambayo tunashirikishwa Wabunge ni kipindi ambacho Halmashauri zinaitwa kwenye Kamati ya LAAC na PAC. Hapo ndiyo tunashirikishwa vizuri sana na tunaweza kushiriki ili kwenda kuchangia mawazi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Abubakari Asenga, unapokea Taarifa hiyo?

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa mikono miwili. Pia, hata vile vikao kimoja kimoja unachovizia ama Katibu wako anaenda kwenye Baraza la Madiwani, maana Kamati ya Fedha hata Katibu wako haruhusiwi kwenda. Wanasema Mbunge mwenyewe uwepo. Sasa wakichengesha ile tarehe huwezi kushiriki, watu wameshapitisha mambo kule. Unakumbuka Makamu Mwenyekiti wa CCM Taifa, Comred Abdulrahman Kinana, katika semina alituambia, katika mambo muhimu ya Mbunge kufanya ni kutokupoteza hii Kamati ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, haya la pili, makabrasha hayo yanakuja lini? Kabrasha unaletewa kama nyumba hivi, siku moja, labda saa sita, kesho kikao. Utapitia nini, utaacha nini?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunachoomba ni kwamba, wanapoandaa hivi vikao washirikiane nasi, tupate makabrasha kwa wakati, tujue tukienda kwenye Kamati ya Fedha tunapitia nini na tukienda kwenye Baraza tunapitia nini? Wako Madiwani wazuri sana. Sio Madiwani wote wanahusishwa ama wanatuhumiwa na kadhalika, lakini wako Madiwani ambao ni wazuri, wanasimamia, lakini baadaye wanaitwa wanaambiwa mradi wako utahamishwa, sijui nini, wanatishiwa na hatimaye unakuta, ile kauli ya Mheshimiwa Rais kwamba Madiwani chukueni hatua, fanyeni kazi yenu, inakuwa inakwama.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kufunga dimba, nami nichangie katika Wizara yetu ya Maliasili na Utalii.

Kama kawaida, kwa dhati ya moyo kwa kweli napenda kushukuru na kumpongeza shemeji yetu Wana- Kilombero, Waziri wetu Dkt. Ndumbaro kwa maana mama yetu anatoka kule na Naibu Waziri, Mheshimiwa Mary kwa sababu hawa walikuja Jimboni kwetu mapema sana na wakatusaidia kufanya jambo kubwa kabisa kuliko mambo mengine makubwa ya utalii na kulinda rasilimali ambayo haijawahi kufanyika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya kwanza watu waliona askari wakifukuzwa hadharani baada ya kupatikana ushahidi wa kutosha kwamba askari wale walikuwa wanatuhujumu na kunyanyasa wananchi. Kwa hiyo, tunamshukuru sana kwenye jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nashukuru kwa suala la soko. Alijibu hapa juzi Mheshimiwa Waziri kwamba yale maelekezo yake ya kutujengea Soko la Samaki zuri pale kwenye Daraja la Magufuli, yapo kwenye bajeti hii. Nami nawaomba Waheshimiwa Wabunge jamani tuchangie tuboreshe mwisho wa siku tupitishe bajeti hii ili Wana- Kilombero wapate Soko hili la Samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nataka nikuambie, kuna kijana mmoja hapa wa Kilombero, anasoma Chuo Kikuu hapa, ni engineer amechora soko zuri sana kama ishara ya Panton lililowahi kuzama zamani na wananchi na likaua watu. Ametengeneza soko simple la aina ile ambalo litakuwa na eneo la kupigia picha ili kuvutia watu wanaotaka kupiga picha kuonekana kwa daraja lile, lakini kuonekana kwa viboko na kuonekana kwa mamba ambao wanaenda kuota jua katika Mto Kilombero. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na hata Katibu Mkuu wetu, nimeambiwa analifanyia kazi suala lile la ombi letu la kupata eneo la mita 50 katika Tarafa ya Mang’ula Corner. Nimemwomba sana Mheshimiwa Waziri na namwomba tena Katibu Mkuu wa Wizara mfikirie, kwa sababu Mkandarasi yuko site, ameanza kutandika lami. Sasa katikati pale kuna eneo linaitwa Mang’ula Corner, barabara imejikunja sana. Kunyoosha ile barabara Mkandarasi ameshindwa kwa sababu eneo ni la kwenu, anaambiwa zile mita 50 zilizoingia ni za Udzungwa kwa hiyo hawezi kunyoosha barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie, nitafurahi sana akirudi hapa akituambia kwamba tumepatiwa eneo lile na Mkandarasi; na Waziri wa Ujenzi ametuambia wazi kwamba akipata jibu lako anaweza kumwambia Mkandarasi akachonga ile barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, sisi tulipata nafasi, mimi na baadhi ya Wabunge kabla hatujawa Wabunge, Mheshimiwa Dkt. Kiruswa na kaka yangu Mwana-FA tulipanda Mlima Kilimanjaro mwaka 2019; na tulipofika pale juu tulifikisha picha ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kama ishara ya kumuenzi kwa mazuri ambayo alifanya katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kushuka katika Mlima Kilimanjaro tuliandika mawazo na maoni yetu. Maana wageni wengi wanaotoka na tunaokutana nao kule juu; ni safari moja nzuri lakini ni hatari sana na safari ngumu. Wanafika pale juu, wanapopiga picha kwenye ule ubao pale kileleni, tulishauri kuwe na picha ya Baba wa Taifa upande wa kushoto na upande wa kulia wa kile kibao kuwe na picha ya Rais ambaye yuko madarakani. Naomba Wizara wajaribu kulifanyia kazi suala hili. Kufika pale juu, kileleni siyo mchezo. Sasa mtu akifika pale, anakutana tu na maandishi kwamba “Hongera umefika juu ya kilele cha juu zaidi Afrika.” Sasa kungekuwa na zile picha; ya Baba wa Taifa na Rais ambaye yuko madarakani, ingekuwa jambo zuri sana kwa utambulisho wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepanga pia na baadhi ya Wabunge na tutamwomba Mheshimiwa Waziri atusaidie kwamba mwaka huu Mungu akipenda tutapanda tena Mlima Kilimanjaro, tutapandisha picha ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuionyesha Afrika na kuiambia dunia kwamba Tanzania ina thamini akina mama, inapenda wanawake na kwamba wanawake wanaweza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wale Wabunge ambao wameagana na nyonga zao, wako tayari kupanda Mlima Kilimanjaro, wanione, tuliongeze lile group ili tupande pale juu tufikishe picha ya Mheshimiwa Mama Samia pale juu kileleni.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Asenga, mimi mwenyewe nilishapanda huo mlima, wala huna haja ya kuagana na nyonga Waheshimiwa Wabunge. Mjiandae tu, hata ambaye nyonga yake hawajaagana, anao uwezo wa kupanda mlima.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa sawa. Yeyote ambaye yuko tayari, tupande wote Mlima Kilimanjaro na tufikishe picha hiyo ya Mheshimiwa Mama Samia kumuunga mkono kwa mambo mazuri anayofanya katika nchi yetu na hususan mambo yale ambayo yanaongeza sekta ya utalii kwa ujumla na kuondoa zile dhana potofu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimdokeze Mheshimiwa Waziri jambo moja. Nimekuwa nikipata meseji nyingi sana kutoka kwa Kiongozi wa Wavuvi wa Ifakara anaitwa Shaibu Majiji; baadhi ya askari tena wameanza kunyanyasa wavuvi kinyume na maelekezo yako. Ulielekeza wavuvi wale wakienda kuvua, wavue kwa utaratibu kule kwenye maeneo ya hifadhi; wavue kwa nyavu zinazotakiwa, wavue samaki waondoke nao, wasijenge. Walikubali kufanya hivyo na walifurahi ahadi yako ya kujenga soko. Sasa kuna maneno maneno yameanza, kwa hiyo, naomba ulifatilie hilo, uone namna gani hawa askari wetu wazuri wa TAWA ambao wengine uliwapandisha vyeo, wanaoweza kusimamia maelekezo yako vizuri.

Mheshimiwa Waziri, lingine tunaloliomba, sisi ukivuka daraja la Magufuli kuna eneo linaitwa Limaomao, liko karibu zaidi na Mbuga ya Nyerere na zamani Selous, tulikuwa tunaomba Wizara yako ifikirie namna ambavyo mnaweza mkaweka geti pale, kwa sababu ni njia rahisi sana ya game drive ya kuingia Nyerere na kwenda Selous na itakuwa imeongeza mapato yetu. Ni kwamba ukivuka daraja la Magufuli pale kushoto, kuna njia zamani ilikuwa inatumika kwenda Mbuga ya Selous ambayo sasa hivi ni Nyerere. Kama tukipata geti pale, itatusaidia kuchangamsha mji wetu wa Ifakara na Jimbo letu la Kilombero. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, lingine ni tembo. Ukivuka Daraja la Ruaha, unaanza Jimbo la Kilombero kilometa takribani 35 unapakana na Mbuga ya Udzungwa. Mbuga hii ya Udzungwa ina tembo wengi sana na ni hifadhi yetu, nami naelewa concern yenu ya kulinda hifadhi yetu kwa sababu siyo mali yenu ni mali yetu sisi sote wananchi. Kuanzia hizo kilometa 35, tembo wanavuka kutoka Udzungwa wanaiongia chini upande ambao wananchi wanaishi. Changamoto ni kubwa kweli kweli. Naomba mwapatie askari wale zana ili waweze kufika kwa wakati maeneo ya wananchi kuwafukuza tembo wanavyoingia mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kuna issue ya ushoroba na kwamba mmejenga daraja pale kama Serikali la kuhakikisha mnapitisha tembo kwamba wale tembo wanaenda kusalimiana, yaani kuna mashemeji wako Udzungwa, kuna wake sijui wako kule Nyerere, kwa hiyo, wanapita kila mara kwenda kusalimiana huko kama alivyosema Naibu Waziri, mmetengeneza njia maalumu chini ya daraja, mmejenga kwa daraja zuri kwamba wanavuka vizuri; mnawatengenezea fence. Tunaliunga mkono jambo hilo lakini kwa kweli kwa dharura sasa hivi, Askari wetu wale wanatakiwa kupewa magari, kupewa mafuta wafukuze tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimeenda kwenye msiba, tembo ameua mtu pale; na issue sana siyo fidia ndogo au fidia kubwa; ni mbinu gani tunafanya kuhakikisha tembo hawaui watu? Tembo wanapita kwenye njia yao, wakikua banda la mtu la udongo anaishi humo ndani, wanagonga, wanaenda mbele huko kula mpunga. Tembo wanapenda mpunga kweli Mheshimiwa Waziri. Sasa wasije wakatutia njaa kule tunakoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nisiseme mengi, nataka kuwaomba Waheshimwia Wabunge hapa watusaidie tupitishe hii mambo ili tupate lile soko na ile issue ya Mang’ula Corner.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nami kama Mjumbe wa Kamati ya LAAC naunga mkono Taarifa ya Kamati kwa asilimia mia moja. Nasi kama Wabunge wa Bunge hili la kwanza tunaendelea kujifunza kwa Mwenyekiti wetu na Katibu wetu wa Kamati ya LAAC Bwana Bisile, mambo mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama walivyosema wenzangu, nami nakupongeza wewe na Mheshimiwa Naibu Spika kwa kuchaguliwa; na siku ile tumekuchagua tukakutana na Waandishi wa Habari, wakaniuliza kwa mic mdomoni ghafla: “Unafikiri Dkt. Tulia atakuwa Spika wa namna gani?” Basi mimi nikasema atakuwa Spika wa STK; kwa maana ya Sheria, Taratibu na Kanuni. Tumeshaanza kuona humu sasa, sheria, taratibu na kanuni zikishughulikiwa vya kutosha. Uzuri wa hiyo STK ni kwamba inatujali sisi manjuka, haitubani sana. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuendelea kuchangia kama walivyochangia wenzangu kwa haraka nikijumuisha vipengele vinne ama vitano ambavyo Mwenyekiti amevisema katika taarifa yake. Uutagundua kwamba karibu tunazungumzia upotevu au watu kuchezea karibu shilingi bilioni 64.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika taarifa yake, matumizi ya fedha mbichi, anazungumzia shilingi bilioni 18.7; kufutwa kwa miamala ni shilingi bilioni 4.5; kurekebishwa kwa miamala ni shilingi bilioni 4.8; na mawakala fedha ambazo wamezikusanya, hawajazipeleka katika Hazina za Halmashauri ni shilingi bilioni 35. Hii ni karibu shilingi bilioni 64, ukiigawanya shilingi milioni 500 kwa Vituo vya Afya, ni karibu Vituo vya Afya 13.

Mheshimiwa Spika, katika kuzunguka na Kamati ya LAAC kwenye Halmashauri mbalimbali nimejifunza vitu vingi sana. Kutokana na ufinyu wa muda, ukweli ni kwamba kama tunataka maendeleo ya nchi hii, ni lazima kutazama Halmashauri zetu vizuri. Vinginevyo fedha zitakuwa zinatafutwa na Mheshimiwa Rais Samia duniani kote, zinaletwa, tunapeleka Idara za Kilimo, Elimu, lakini watu wanazichezea fedha hizo. Ni jambo la hatari sana. Nasi kama Wabunge siku hizi tunalalamika hapa.

Mheshimiwa Spika, Mwenyekiti amesema, kwa miaka mitatu trends zinaonesha bajeti yako katika Bunge hili haipelekwi karibu kwa fifty percent. Amesema tunaidhinisha shilingi bilioni 977 inapelekwa shilingi bilioni 497 kwa sababu ya fedha hizi kutokukusanywa vizuri na fedha zile ambazo tunatakiwa tupate kama mapato, hazikusanywi. Wabunge wamesema kuhusu POS na kadha wa kadha.

Mheshimiwa Spika, napenda kusisitiza, ni lazima tuishauri Serikali yetu, nami mwisho nitashauri. Nimeona juzi Mheshimiwa Rais Samia amechukua hatua tu, amepeleka fedha za madarasa, watu wamecheza nazo, akaondoka na Wakurugenzi Wanne. Tumeona Mkuu wa Mkoa wa Mara alivyozungumza kuhusu Wakuu wa Idara na changamoto katika Halmashauri. Lile siyo tatizo la Mara peke yake, ni karibu tatizo la nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, ushauri wetu, hivi katika yote haya yanayozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge katika malalamiko, kweli tuko serious katika nchi hii, kuna Halmashauri haina Mkuu wa Idara ya Ununuzi? Kweli kabisa! Yaani, tunazungumza hapa, fedha zinaenda mabilioni na mamilioni ya fedha kwenye Halmashauri; Halmashauri Mweka Hazina anakaimu. Serious! Tunazungumza fedha zinaliwa, unaenda unakutana na Afisa Mipango anakaimu; au unakuta mtu anayelalamikiwa ni Mkuu wa Idara miaka 20, ana malalamiko yake mpaka wananchi wanajua upungufu wake na miradi anayoifanya katika Halmashauri ile, anaachwa.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi hata kidogo kuendelea. Kupanga ni kuchagua. La kwanza, ni muhimu sana kujaza Ikama ya Watumishi muhimu. Tunajua Serikali haiwezi kuajiri watu wote, Serikali ya nchi hii inashindwa kuajiri Wakuu wa Idara wa kila Halmashauri wakapatikana watu smart, wenye sifa walio-perform, wakasimamia fedha zetu katika Idara! Haiwezekani hata kidogo. Tupange, tuchague tuhakikishe tunapata watumishi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuwezesha kitengo cha Ukaguzi wa Ndani. Sisi katika taarifa ya CAG, tunayopata kwenye Kamati, kwenye Halmashauri zote kuna Wakaguzi wa Ndani; na Wakaguzi wa Ndani ni kama indicator kwa Mkurugenzi.

Mheshimiwa Spika, kwa sisi ambao tulikuwa ma-DAS, anamwambia, Mama utaratibu huu wa kufanya manunuzi hapa haujafuatwa; utaratibu upo hivi, na hivi na hivi. Mkurugenzi asiyesikia, unamkuta kwenye taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, hivi huyu Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani katika Halmashauri, gari yake mbovu, anaazima gari kwa Mkurugenzi; akitaka kwenda kwenye ukaguzi wa miradi anachukua mafuta kwa Mkurugenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili suala linasemwa. Nimeangalia video, Youtube ya hotuba za Mabunge ya miaka kumi nyuma, wanalalamikia hili jambo. Hivi mtu unayemkagua na kumshauri halafu unaenda kumwomba mafuta, atazingatia ushauri wako? Akiona unamsumbua, anakukanyagia tu, mafuta hakupi. Ndiyo malalamiko kila sehemu ukienda Wakaguzi wa Ndani wameshindwa kwenda kukagua miradi.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naomba kuwasilisha. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa muda na mimi kuchangia; na ninaanza kwa kuunga mkono hoja kwa sababu mimi nimesimama hapa sina nongwa kubwa na Waziri wetu wa Maji, Naibu wake na Katibu Mkuu. Naibu Waziri alikuja jimboni kwangu akapanda kwenye milima juu kabisa kwenye vyanzo vya maji, ametusaidia sana, Mungu awabariki sana mnafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa mara ya kwanza tunamshukuru Mheshimiwa Rais Samia kwa kutusaidia Mradi wa Miji 28, mradi wa Kiburubutu ambao tangu Mbunge akiwa marehemu Abbas Gulamali ulikuwa haujafanyiwa kazi na haujapatiwa pesa, safari hii umepatiwa pesa kwa hiyo, tunawashukuru sana na tunawapongeza. Naomba tu mtusaidie katika vile visima ambavyo tumechimba sasahivi mpango wa pili ni ma-tank tupate fedha kwa ajili ya ma- tank.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika muda wangu huu ambao nimepewa wa kuchangia sauti yangu inaongea kwa unyonge sana kutokana na masikitiko ya wananchi wangu ambao tunawaboreshea maji; wengi ni wakulima wa mpunga na miwa.

Juzi tarehe 5 mwezi wa tano walikaa katika vyama vyao wakaamua kuhusu maslahi yao ya miwa katika mikutano yao mikuu, lakini jana nimepokea simu zaidi ya hamsini wakiwa wanasikitika kuhusu maamuzi yaliyofanywa na Serikali kuingilia maamuzi yao; kwa kweli imenisikitisha sana. Natumia nafasi hii kusema ili Serikali iliyopo hapa isikie isaidie kufuatilia. Kama tunaboresha maji huku tunaendelea kuharibu na kuingilia shughuli za wananchi za uzalishaji itakuwa hatufanyi kitu chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia muda wangu huu ili Mawaziri na viongozi waliokuwepo hapa wasikie. Kwenye biashara, kwenye kilimo cha muwa kuna shida kubwa sana. Naligusia hapa kwa sababu hakuna maana nyingine yoyote kama tunaboresha mambo ya maji kwa wananchi halafu wakulima kule wananyanyaswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kuna kiongozi wa Serikali ameenda kuzungumza na wananchi, hawajafurahia maamuzi yao Kata ya Sanji. Na kwa bahati nzuri nimeongea na Mheshimiwa RC, Mkuu wa Mkoa Shigela, analifanyia kazi hili. Nimeongea na Waziri Bashe analifuatilia. Jambo hili halijakaa vizuri na Mheshimiwa Waziri Mkuu uko hapa naomba kutumia nafasi hii wananchi wangu wasikie kwamba, nimelisema hapa na tunalifuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tume zimeshaundwa kufuatilia jambo hili, lakini halifanyiwi kazi na tume zinafichwa taarifa, yanazushwa maneno ya uwongo kujenga faida ya watu kunufaika na kilimo cha muwa na sukari. Mambo haya ni kama yale yaliyotokea Kasalali, mambo haya ni kama yanayotokea hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimetumia muda huu wa kuchangia Wizara ya Maji kushukuru kwa miradi waliyotuletea, lakini kwa kweli ni masikitiko makubwa sana na kilichotokea jana; kwa mara ya kwanza kupokea mimi simu karibu hamsini za wananchi wakilalamika wanataka kupanda mabasi kuja Dodoma kwa sababu maamuzi yao yamekiukwa. Ni imani yangu ni kwamba, kuwa Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa watachukua hatua madhubuti za kuwasikiliza wananchi wale upya; kwa sababu Sheria za Ushirika wamefuata na taratibu wamefuata, lakini zemeenda zimetenguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishia hapa. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara yetu ya Maji.

Mheshimiwa Spika, wakati naanza kuchangia na mimi niwapongeze timu ya Wananchi kwa ushindi mkubwa sana na jambo zuri ambalo wamelifanya, hizi ni baraka zinazotokana na Waziri wetu kuhudhuria mechi hii, pamoja na mfadhili wetu GSM, Mwenyezi Mungu awabariki kutupa raha hiyo kiasi hicho. Hapo nje ya Bunge nimekutana na Naibu Waziri wa Michezo, Mheshimiwa Mwana FA, ananiambia amehamia rasmi timu ya Wananchi na ametangaza kwenye page yake kwamba amehamia timu ya Yanga. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naanza kwa kuchangia Wizara yetu ya Maji kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kama mnakumbuka tulikuwa tuna suala la miji 28 na Wabunge wote ambao tunahusika na miradi ya maji katika miji 28 tulikuwa kila mara tukimsumbua Mheshimiwa Waziri kuhusu miradi hii na tulipopata nafasi ya kukaa na Mheshimiwa Rais katika kikao, Waheshimiwa Wabunge walipomuuliza Mheshimiwa Rais alisema subirini tutalifanyia kazi jambo hili na baada ya miezi sita tumeona matokeo yametoea. Nami katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara mradi wangu wa maji wa Kiburubutu Mkandarasi amefika kwa bajeti ya shilingi bilioni 42 na sasa hivi wanapima udongo pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, nawashukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, wote mmefika Jimboni kwangu mmepanda milimani kule mmeona hali halisi, nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watumishi wote wa Wizara hii ya Maji pamoja na Engineer wetu wa RUWASA Wilaya ya Kilombero, Eng. Mlelwa. Kwa kweli mradi ule wa Kiburubutu ni muhimu sana katika Halmashauri ya Mji wa Ifakata ambako utasambaza maji katika Kata Tisa za Tarafa ya Ifakara, ni mradi muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ni aibu sana Mji maarufu kama Ifakara wenye wajanja wengi, unapita barabarani unakutana na mabomba ya mdundiko. Ifakara water base yetu ipo juu ndiyo maana tunapata mafuriko kila mara. Kwa hiyo, mwananchi akichimba tu mita tatu chini anapata maji. Watu wanakunywa maji ambayo hayajapimwa, hayana viwango. Kwa hiyo, huu mradi unasubiriwa kwa kiasi kikubwa sana na kwa hamu kubwa sana ukamilike.

Mheshimiwa Spika, kuna wananchi ambao wanapanda kwenda Kiburubutu kule kuangalia kweli Mkandarasi yupo na kweli jambo hili litatokea? Maana yake ni mradi ambao umetangazwa tangu wakati wa Mwalimu Nyerere. Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan wameleta fedha na kwa mara ya kwanza tunaona Mkandarasi. Wizara na Mheshimiwa Waziri tunakuomba, umefika Ifakara umeona presha ile ya watu ilivyo kubwa wakisubiri mradi huo. Tunakuomba sana utusaidie mradi huu uweze kukimbizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kweli tuna imani na ile Kampuni ya LNT kwa sababu imekuwa ikiwaita viongozi wa Wilaya na viongozi wa wananchi, mimi mwenyewe Mbunge kila mara wanani-update kinachoendelea, kinachofanyika, kwa hiyo na mimi nikipita kwenye mikutano ya wananchi ninasemea. Jimbo letu la Kilombero, Halmashauri yetu ya Mji wa Ifakara unaweza ukafanya mambo yote, lakini kwa kweli Mradi huu wa Kiburubutu ndiyo namba moja kuliko vitu vyote. Kwa hiyo, ukikaa na watumishi wako wa Wizara huko muangalie muwe mnagusia jambo hili, ni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tunaomba wakati tunaendelea na mradi huu wa maji wa Kiburubutu, gari la Wizara lilipita kwenda kuchimba visima Jimbo jirani la Mlimba kwa ndugu yangu Mheshimiwa Kunambi na likapita pale Ifakara, tuliomba kwamba kuna visima ambavyo tulichimba tunaomba tupatiwe pesa ili visima hivi vianze kufanyiwa kazi. Vijiji cha Kanyenja, Mikoreko, Iyanga na Mtaa wa Jangwani pale Ifakara.

Mheshimiwa Spika, kwa vile mradi huu wa Kiburubutu utatumia miaka miwili mpaka mitatu, kwa haraka basi tupatiwe fedha katika maeneo haya yenye visima hivi, miradi ya maji ya matenki iwekwe pale kama ulivyotusaidia Sagamaganga na Ungongole wananchi waendelee kutumia maji haya katika miaka hii miwili au mitatu wakati wakisubiri huu mradi wa miji 28.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, Kata zangu kumi kutokea Zinginari, Kiberege, Kisawasawa, Mwaya, Mang’ula A, Mang’ula B, Sanje, Mkula mpaka Kidatu, wananchi hawa wako kandokando ya Milima ya Udzungwa na Hifadhi ya Udzungwa, Hifadhi ile ya Udzungwa inaporomosha maji kwenda kwenye mashamba ya miwa, huko nyuma wananchi walitengeneza miundombinu yao wenyewe, walichangishana wakapeleka matenki kule juu wakajenga wakatega maji kwenye maporomoko yale ya udongo na maji yakawa yanateremka wanatumia majumbani kwao.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi imekuja system ya mita, hatukatai kwamba lazima tuchangie maji. imefungwa system ya mita kwamba tunatakiwa kuchangia. Wananchi wanauliza swali kwamba miundombinu hii tulijenga sisi, tunaweza kuzungumza na Serikali, na RUWASA tukakubaliana tupate bei hata ya chini sana ya kuchangia bili za maji, kwa sababu wanaenda kutoza sehemu ambako RUWASA haikuweka fedha. RUWASA wanasema kwamba huko mbeleni ikitokea miundombinu imeharibika watakarabati, lakini tayari wanatumia maji miaka yote. Kwa hiyo, tunaomba sana suala la bili kwa wananchi wetu ambayo miundombinu ilikuwa ya kwao, ipitiwe upya, hasa elimu kabla ya kutoza ifanyiwe kazi, vinginevyo hali itakuwa ngumu sana.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni suala la mafuriko. Tumeona Ifakara juzi tumepata mafuriko na kila mwaka karibu tunapata mafuriko. Nami nilisema suala la mafuriko katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara ni suala mtambuka. Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maji na Wizara ya Nishati mnaweza mkakaa mkajadili kuhusu yale mafuriko. Mamilioni ya lita za maji kila mwaka yanapotea kwenda kwenye mashamba ya watu na makazi ya watu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amefika mpaka kwenye kile kichaka cha Mto Kilombero ambacho kilikuwa kimezibwa. Namshukuru sana Engineer Bonde Emmanuel anafanya kazi nzuri, wamefukua pale, maji yanapita. Tuliomba Wizara ya Nishati, tunaomba Wizara ya Kilimo, na ninyi mfukue ule mto. Kwanza utaongeza maji. Fifty percent sasa hivi inachangia kwenye mto Kilombero ambao Mto kilombero, ambao unachangia sixty five percent kwenye Bwawa la Nyerere. Kwa hiyo, tutapelaka maji kujaza Bwawa la Nyerere; pili, kwenye kilimo watapata maji yale ambayo yanapotea kwenye mabwawa ya kilimo; tatu, maji yale yanaweza yakafanyiwa utaratibu mzuri, ninyi Wizara ya Maji mkayatumia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunasisitiza sana Mheshimiwa Waziri, mafuriko ya Ifakara haiwezi kuwa historia ya mazoea. Siyo kweli. Hata wazee wetu zamani walikuwa wanaboresha tuta na mafuriko yanapungua. Sasa msizoee yale mafuriko, naomba mkae kama Wizara tatu kwa pamoja na mkisaidiana katika jambo hilo, mfikirie, na Ifakara inaweza kuondokana na mafuriko.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nawashukuru sana, naishia hapa. Mheshimiwa Wazri nakushukuru sana. Naomba Kiburubutu, naomba suala la bili za maji na mafuriko mnisaidie. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Mapendekezo ya Kurejea Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Afrika ya Mwaka 2009
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mezani. Mimi kama mjumbe wa Kamati ya Miundombinu kwa kweli tulipata nafasi nzuri ya kupitia hoja hii na naunga mkono hoja ili turidhie Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Mwaka 2009 kwa sababu faida ni nyingi kuliko hasara, na nchi yetu si kisiwa useme kwamba kuna baadhi ya vitu tunaweza kujitenga navyo, japokuwa watu wanaweza kuwa waogawaoga na mambo haya ya maridhiano. Mimi nataka kuchangia maeneo kama matatu au manne.

Mheshimiwa Naibu Spika, chini ya Shirika la Usafiri wa Anga ICAO na wa OAU kama Mheshimiwa Waziri na Mwenyekiti wa Kamati walivyowasilisha hapa, Tanzania tuliridhia ile ya mwaka 1969 na kwa mujibu wa Katiba hii mpya ya 2009 ni wazi kwa kile kipengele ambacho kinasema kwamba nchi 15 zikisha saini utekelezaji unaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Tanzania tumeshaanza kusukumwa nje kwa sababu nchi 41 tayari zimeshasaini maridhiano haya na wenzetu wanaanza kunufaika kuliko sisi. Hata huko nyuma tulishawahi kupata hadi fedha za uwekezaji kwenye mambo ya ushirikiano wa usafiri wa anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano mmoja, mimi na baadhi ya Wabunge wenzangu tulisafiri hapa na Timu ya Wananchi tukaenda katika nchi mojawapo. Tukiwa na ile Timu ya Wananchi pamoja na Waheshimiwa na wanashabiki wengine wa hiyo timu katika nchi hiyo, tulivyotua pale airport tulitumia kama masaa matatu hivi, bila ya kujali hawa ni Wabunge ama sio Waheshimiwa Wabunge na viongozi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mlolongo ulikuwa mkubwa sana. Sasa hatukufahamu kitu, baadaye katika upelelezi nitaeleza umuhimu wa maridhiano haya, tukawa tunaangalia wale watu wanaotuhudumia pale kama kuna wengine ni wanachama labda wa timu nyingine pinzani na sisi hata katika nchi yetu ama katika nchi ile nyingine na kujiuliza kwa nini tunapata usumbufu wa namna hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, tukajua, mojawapo ya sababu ni kwamba nchi hiyo tuliokwenda sisi hatukuwepo kwenye maridhiano ya pamoja ya anga. Kama tungekwenda katika nchi nyingine ina maana tungenufaika, tungefika pale wangeambiwa kuna Watanzania 50 wanakuja katika nchi yetu. Tungepokelewa vizuri, tungepita na ule usumbufu ungeondoka pale na ile furaha yetu ya kumtandika mtu katika nchi ile na kushinda ile mechi ingekuwa vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hata wakati wa kurudi usumbufu ulikuwa vile vile. Kwa hiyo, naridhia na nawaomba Waheshimiwa Wabunge turidhie jambo hili kwa sababu faida ni nyingi kuliko hasara. Ukiona uwekezaji mkubwa ambao Serikali ya Chama cha Mapinduzi inawekeza sasa hivi katika kununua ndege na juzi tu tumepata ndege ya kusafirisha mizigo, tukiongeza network ya mashirikiano itatusaidia sana kuhakikisha kwamba ndege yetu inapeleka mazao sehemu nyingi sana na inaongeza wigo ndani ya nchi na katika nchi zingine za Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku moja Mheshimiwa Bashe anaweza akaelekeza ndege ikatua pale Ifakara ikachukua mchele, ikapeleka katika Nchi za Afrika hizo zitakazokuwa zimesaini kama ni 55 ama ni vipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la ajira; kuna watu wamekuja kusaidia Shirika letu la Ndege la Tanzania kutokana na uzoefu wao katika mahusiano ya umoja wa mashirikiano ya anga katika nchi nyingine. Tutamkumbuka vizuri sana marehemu Mheshimiwa Omary Nondo, Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema, alitolewa katika mashirika haya ya kimataifa ya mashirikiano haya yaliyopita na akaja kutoa uzoefu mkubwa sana katika nchi yetu. Pia, tuna mifano mingi ya Nchi nyingine kama vile Misri, wanajiunga na hii Katiba ya Afrika lakini wanajiunga na Umoja wa Nchi za Kiarabu. Yote hii ni kuongeza network ya biashara katika safari ya anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kwa kifupi kwamba, pamoja na mambo yote aliyoyasema ya mafanikio kwa mfano ya kupata miongozo ya ndege ya kutosha. Sisi sasa hivi tunaongeza ndege nne, nafikiri kwenye Kamati yetu tumepewa. Kama tunaongeza ndege nne halafu tunajifungia wenyewe kwenye East Africa na Nchi kama Tanzania, bado hatuna soko kubwa la kujiwekeza vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naijua tahadhali ambayo imesemwa na baadhi ya watu kwamba lazima tuweke kanuni au utaratibu mzuri tusije tukafungua anga tu halafu ikawa kama tunafungua soko la watu wengine. Hata hivyo, katika soko kubwa hilo hilo na sisi tunaweza kufanya vizuri zaidi kwa kuuza ndege zetu, kuuza Kiswahili chetu, kupambania vijana kupata ajira katika shirika hilo na katika nchi nyingine. Pia, sambamba na kupata fedha za uwekezaji ambazo zitatolewa na hiyo AFCAC ili nchi yetu iweze kufanya vizuri katika biashara ya usafiri wa anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumalizia kwa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge turidhie Mkataba huu, turidhie Katiba hii ya 2009 ili iweze kutumika na nchi yetu iingie katika network ya Afrika nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante sana kwa nafasi hii. Nami ninamshukuru Mheshimiwa Rais, Waziri na Watumishi wote wa Wizara ya Mambo ya Ndani, moja kwa kufahamu kwamba katika dunia tunayoenda sasa ya sayansi na teknolojia ni aibu sana kuendelea kutumia Askari barabarani kuongoza magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona katika bajeti ya Waziri kwamba mmeanza kufunga taa katika Majiji makubwa kama Dar es Salaam, Arusha na Mwanza, hii programu ni nzuri sana na ni muhimu ikaendelea katika maeneo mengine kama Morogoro na kwingineko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dunia ya sasa haiwezekani hata kidogo kwa kweli tuna upungufu wa Askari karibu asilimia 40 ya nchi yetu halafu tunaendelea kutumia Polisi kwenda kuongoza magari barabarani. Tunaomba hii teknolojia iendelee mbele watu wakae sehemu wachache wa-control computer watazame magari yanaoenda speed. Mtu anakamatwa hata kama mbele ya kilometa 50 anapewa faini kuliko Askari kukaa kila kichochoro, wakati huo wananchi katika vijiji wananchi katika Kata wanalalamikia wapate Askari wa kuwalinda. Kwa hiyo, hili ni jambo zuri na ni jambo kubwa, mpango huu Mheshimiwa Waziri ni vizuri ukawekewa fedha za kutosha ukaenda katika Majiji yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mimi kushika shilingi ya Kaka yangu Mheshimiwa Masauni nitashika kwa mambo mawili. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wote wamefika Jimboni kwangu. Mheshimiwa Waziri tumeenda nae Jimboni mpaka tumepita vichochoroni mpaka kwenye Magereza ya Idete ameenda mpaka Gereza la Kiberege ameenda kule, tumeingia ndani kona zote. Leo Watanzania wa Kilombero wa Ifakara wanaangalia hivi ninavyochangia, ahadi yao ya Wilaya ya Kilombero kukosa Kituo cha Polisi cha Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ni Wilaya kongwe sana, haina Kituo cha Polisi cha Wilaya, tumeshatafuta eneo tumelipata na mimi Mbunge nimepeleka tofali, anapokaa OCD wetu hapafai, wakati wa mafuriko maji yanaingia. Kwa hiyo, kama ni kushika shilingi Mheshimiwa Waziri mimi nitataka ufafanuzi wa Kituo cha Polisi cha Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni Kituo cha Polisi Tarafa ya Mwaya Kata ya Mwaya. Mheshimiwa Waziri umefika umekuta kituo cha Polisi cha mbao, katika dunia ya sasa hivi Kata ambayo inaongoza kwa watu wengi, mimi nina tofali za kuchangia pale Wizara inanipa nini? Tujenge Kituo cha Polisi ama tukarabati tuondoe zile mbao katika Kata ya Mwaya Askari wetu wapate Kituo cha Polisi chenye sifa ya kukaa vizuri. Kituo cha Polisi cha Mwaya kila mwaka Waandishi wa Habari wanaenda wanakipiga picha wanakisambaza hizo picha. Kwa hiyo, siyo vizuri jambo hili ni baya sana katika Kata yetu ya Mwaya, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana chondechonde haya mambo mawili makubwa unisaidie Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kilombero na Kituo cha Polisi cha Kata ya Mwaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, NIDA imekuwa usumbufu kama baadhi ya Wabunge walivyosema. Wananchi wetu walishakubali kupata Namba za NIDA achana na haya mambo ya kitambulisho. Namba hizi haziji kwa wakati, sasa kama kweli mmeweka bilioni 42.5 Mheshimiwa Waziri tafauteni utaratibu ambao namba hizi watazi-print kwa wakati. Mimi kila siku napokea meseji hapa 10, 15, 20, nimekwama nimekuja Wilayani nimetafuta NIDA nimekosa. Nikatafuta na mimi operesheni nikaongea na Mkurugenzi wa NIDA na mimi nikatafuta chochote kitu, tukawachukuwa watu wa NIDA wakaanza kuzunguka katika Kata kufanya operesheni ya kuandikisha, haijasaidia kitu bado watu wengi hawajaandikishwa na watu wengi hawajapata namba. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba sana jambo hilo utusaidie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, Ifakara inaonekana inaongoza katika utapeli wa kimitandao. Kuna vijana wachache ambao wamekuja kutuharibia Mji wetu wa Ifakara. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana kwa kuniletea OCD mpya na Mkuu wetu wa Wilaya wameanza operesheni maalum ya Kamati ya Ulinzi na Usalama kuhakikisha kwamba Ifakara inasafishika na tunaondoka katika hiyo rank ya kwanza ya utapeli wa kimitandao kama juzi nilivyomuona Afande RPC wa Morogoro anachukua hatua na tunasafisha Mji wetu na Kilombero inakuwa safi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa dakika tano za kuchangia Wizara ya Ujenzi. Nami kwa kifupi nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Mkurugenzi Mkuu wa TANROADS. Kama utakumbuka vizuri nilikuwa na mgogoro mkubwa wa barabara yangu ya Ifakara Kidatu kiasi cha Kwenda, siyo kuruka sarakasi lakini kwenda kukaa kwenye matope. Hivi ninavyozungumza na wewe lile eneo tulilokaa kwenye matope lina kilometa 20 za lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kuwapa taarifa wananchi wangu kwamba, katika kilomita 66.9 zile ambazo tulikuwa na mgogoro mkubwa…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa mnaotoka, Waheshimiwa sitaki kutaja majina ila mtoke kwa nidhamu na staha ya kibunge.

Mheshimiwa Asenga endelea.

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunilindia dakika zangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli bila unafiki na kwa dhati ya moyo, napenda nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Profesa Makame Mbarawa kwa kuja Jimboni kwangu mara mbili kufuatilia barabara hii ya Ifakara - Kidatu ambayo ni barabara muhimu sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Waziri alivyofika Ifakara na Kilombero, ukweli ni kwamba changamoto kubwa ya barabara hii na nimemwomba Katibu Mkuu Engineer Aisha Amour na Engineer Mativila watusaidie kero kubwa ya fidia. Fidia ya barabara hii kwa wananchi wa Mbasa, Katindiuka, Mlabani mpaka kutokea Lipangalala imekuwa ni kero kubwa. Hivi ninavyozungumza wananchi walikuwa wanataka kuja Dodoma kufuatilia fidia yao, kwa sababu takriban miaka minne sasa wamewekewa alama na bila kulipwa fidia yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naona anashika kalamu pale anaandika, namwomba sana atusaidie kero hii kubwa na nimewasiliana na Meneja Razak wa TANROADS Mkoa wa Morogoro, amenijibu majibu mazuri kwamba wanafanya upembuzi upya ili kupata thamani ya sasa ya fidia kwa wananchi hao. Meneja wa TANROADS Mkoa ni bwana mdogo, anafanya kazi nzuri na tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tunapenda kushukuru pia Waziri alipokuja Kilombero ametupatia taa za barabarani katika Mji wa Ifakara. Ifakara Mjini sasa kuna barabara ya TANROADS inayopita pale, ina msongamano mkubwa ndiyo maana tunasisitiza kuhusu barabara ya mchepuko, lakini Mheshimiwa Waziri ametupatia taa za barabarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu la pili, Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri, baada ya ombi la fidia kwa wananchi wetu wa Mbasa, Katindiuka na Mlabani ni ombi la kuchukua barabara ya roundabout ya Kibaoni kuelekea TAZARA kwa kuwa Wizara hii ni ya Uchukuzi pia, TAZARA yetu ya kibaoni ina hali mbaya. Naomba wachukue ile kilomita 2.5 ambayo nimemwomba pia Katibu Mkuu Balozi Engineer Aisha Amour kutoka roundabout ya Kibaoni kuelekea mpaka TAZARA kwa sababu TAZARA ni yao. Ile barabara inapita stendi yetu ya Kata ya Kibaoni, stendi yetu ambayo tunaitumia kama ya wilaya, tunaomba sana watusaidie kuchukua barabara hiyo ili tujenge hata kwa lami nyepesi ili iweze kupitika wakati wote na wananchi wanaokwenda kupanda treni kuelekea TAZARA.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyosema Wabunge wengine wa Mkoa wa Morogoro, naomba kusisitiza, kama tunavyosema Mkoa wa Morogoro katika kilimo ni ghala la Taifa, ni wazi kuwa amesema Mheshimiwa Kunambi hapa pacha wangu wa Jimbo la Mlimba, kwamba sisi ni wakulima wazuri, tunalima mpunga wetu mzuri, ubwabwa wetu mzuri, mama Aleksia amesema hapa. Hata hivyo, bado mkoa wetu na hasa kiungio kama Jimbo la Ifakara, Jimbo la Kilombero, Halmashauri ya Mji wa Ifakara, haujaunganishwa na mikoa mingine. Waziri akimsaidia barabara Mheshimiwa Kunambi akitokea Njombe lazima atapita Ifakara. Akimsaidia barabara Mheshimiwa Antipas wa Malinyi, lazima atapita Ifakara kwenda Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkimsaidia Mheshimiwa Salim wa Ulanga lazima apite Ifakara kwenda Lindi. Kwa hiyo tunasisitiza sana, tunajua kuna upungufu wa bajeti, lakini kwa kweli katika hali ya Chama cha Mapinduzi ya kuhakikisha kwamba tunaunganisha mikoa na mikoa mingine, tunaomba tuwe na mkakati mzuri wa kuhakikisha Mkoa wa Morogoro unaunganishwa na Lindi, Ruvuma na Njombe. Naomba kusisitiza sana hilo, sitaki kusema mambo mengi hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia hapa kwa kumshukuru Waziri kwamba katika kilomita 66 za Ifakara - Kidatu sasa tuna kilomita 21 zinaenda kuwekwa lami. Narudia kusisitiza Mheshimiwa Waziri Profesa Makame Mbarawa suala langu la fidia, ombi langu nasisitiza chonde chonde, fidia kwa wananchi wetu wa Kata za Mbasa, Mlabani, Lipangalala na Katindiuka wamesubiri sana, imeshapita miaka minne, naomba Waziri alichukue na hiyo barabara ya kilomita 2.5 kutoka roundabout ya Kibaoni kuelekea TAZARA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)