Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Aloyce John Kamamba (14 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa nafasi, lakini kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge lako Tukufu, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia baraka zake zote na hatimaye kuweza kuchaguliwa, lakini nikishukuru Chama Cha Mapinduzi kwa kuniamini, lakini wananchi wa Wilaya ya Kakonko na Jimbo la Buyungu kwa ujumla kwa kunichagua kwa kura nyingi ikiwa ni pamoja na Rais na Madiwani wote wa Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ya kukiongoza chama chetu, lakini pia katika miradi mbalimbali anasimamia na nchi kwa ujumla. Vilevile niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri ambao wameaminiwa. Wameanza vizuri sisi Wabunge tutaendelea kuwatia shime, ili muweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mbalimbali imeanzishwa katika nchi yetu ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Kakonko. Katika wilaya yetu ipo miradi mbalimbali ya umeme, ipo miradi ya maji, lakini iko hospitali ya wilaya inajengwa, lakini katika uchaguzi uliopita mwaka 2015 Mheshimiwa Rais alitupatia kilometa tatu za Mji wa Kakonko, ujenzi unaendelea. Shida yangu ni ukamilishaji wa miradi inayoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua mfano stendi ya Mji wa Kakonko ambayo iliahidiwa mwaka 2015; ujenzi umeanza kwa kilometa 0.63, lakini ninavyozungumza ule mji wamekwenda wameujaza kifusi, ujenzi haujakamilika na hakuna kinachopendelea, lakini vilevile kuna stendi ambayo nimeitaja bado fedha zake hatujaweza kuzipata. Wazo la jumla ambalo naliomba ni uletaji wa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa miradi hiyo ikiwa ni pamoja na ufuatiliaji na ubora wa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, elimu; nishukuru sana kwamba, Mheshimiwa Rais ameweza kuanzisha program ya mpango wa elimu bila malipo. Hii inawalenga watoto wa Watanzania, lakini ambao wanatoka katika familia maskini. Tumefanikiwa vizuri sana watoto wameandikishwa, lakini imeleta changamoto nyingine ya vyumba vya madarasa na uhitaji wa walimu. Tuna shida kubwa sana ya walimu katika shule zetu za msingi na sekondari. Hasa kwa sekondari walimu wa masomo ya sayansi, lakini kwa shule za msingi walimu katika masomo yote. Niombe tunapotekeleza program hii ya mpango wa elimu bila malipo, chonde chonde, walimu waajiriwe ili waweze kujaza kwenye upungufu ambao tunao.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanafunzi wanaomaliza darasa la saba wapo wanaofanikiwa kwenda kidato cha kwanza, lakini wapo wanaobaki. Tunao wanafunzi wamemaliza kidato cha nne, hawafanikiwi kwenda kidato cha tano au kwenda kwenye kozi yoyote ile, hawa tunawasaidiaje? Ndio hoja inakuja ya kuwa na vyuo vya VETA. Jana katika swali la msingi liliulizwa, lakini ikatajwa kwamba, vinajengwa vyuo vya VETA. Niombe vyuo hivi vijengwe vingi na kwa haraka kwa lengo la kuwasaidia watoto hawa waweze kupokelewa katika vyuo hivyo wapate mafunzo na kozi mbalimbali ambazo zinawasaidia watoto wetu katika masomo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna upangaji wa Walimu. Kuna utaratibu ambao umewekwa, inachukuliwa idadi ya wanafunzi wanagawa kwa idadi ya Walimu, wanafunzi ambao ni 40; utaratibu huo haujibu shida ya Walimu tulionao. Uandaliwe utaratibu maalum tofauti na utaratibu uliopo wa kuangalia jinsi ambavyo walimu wanaweza wakapangwa katika shule zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa kilimo; kilimo ndio uti wa mgongo na wananchi wetu wengi wanategemea kilimo, lakini pembejeo hazifiki kwa wakati. Hiyo inakwenda sambamba na mbolea, lakini Maafisa Ugani. Maafisa Ugani nao hawapo wa kutosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali ichukue hatua za makusudi ili nao waweze kuajiriwa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba, mbolea inapatikana, lakini inapatikana kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna upande wa madini; madini yapo maeneo ambayo yameashabainishwa na uchimbaji unaendelea, lakini kuna maeneo ambayo wachimbaji wadogo wanagundua madini katika maeneo tofauti tofauti katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe nayo Serikali ichukue hatua za makusudi pale ambapo imebainika kwamba, kuna madini yamebainishwa, basi utafiti ufanyike na hatua za ziada zichukuliwe ili uchimbaji uweze kufanyika iwe sambamba na maeneo mengine ambayo uchimbaji unafanyika katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa afya; vituo vya afya havitoshelezi. Nikitoa mfano katika wilaya yangu nina vituo vitatu tu Kituo cha Nyamtukuza, lakini Gwanumpu na Kakonko, havitoshelezi na katika kata kumi vituo hivyo havipo. Naomba sana Serikali iweze kuchukua hatua vituo hivyo viweze kujengwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Maendeleo katika bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya kuchangia yapo mengi katika hotuba iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri lakini nitachangia zaidi tutakapoingia kwenye maeneo ya kisekta, leo nitachangia katika maeneo machache.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisije nikachelewa, nianze kwa kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo nitazungumzia sana maslahi ya watumishi. Nchi hii ina watumishi katika maeneo mbalimbali; wapo wakulima, walimu, madaktari na kadhalika. Hawa wanastahili zao; wanastahili kupandishwa madaraja kwa wakati, wanastahili kwenda likizo, wanastahili kwenda masomoni lakini wapo wengine ambao wanastahili kupata malipo kutokana na kazi wanazofanya kwa muda wa ziada. Kwa bahati mbaya stahili hizi hazipatikani kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi tukasema kwamba bajeti yetu ipo salama bila kuzingatia hilo. Tunapokwenda kukamilisha Mpango huu, wapo watumishi ambao wananung’unika, wapo ambao hawapandishwi madaraja lakini wapo ambao hawalipwi, niombe sana zitengwe fedha maalum kwa ajili ya wale ambao wanastahili kupandishwa madaraja hii ikiwa ni sambamba na kuwapandisha madaraja kwa wakati na walipwe stahili zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nitazungumzia ni miundombinu. Ipo miundombinu ya barabara, reli na kadhalika. Katika hili nitazungumzia miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natoka Mkoa wa Kigoma, lakini katika taarifa iliyotolewa ndiyo mkoa pekee ukiunganishwa na Mkoa wa Katavi haujaunganishwa katika mpango wa barabara kwa maana kwamba kufika kila mkoa. Niombe sana katika bajeti inayokwenda kukamilishwa sasa, mkoa wetu uweze kuunganishwa kwa barabara ambazo zinatosholeza kuweza kufikia kwenye ngazi ya mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo barabara mfano inayotoka Mpanda – Mishamo - Uvinza – Kigoma; Tabora – Kaliua - Uvinza – Kigoma; na Mpanda – Inyonga – Koga - Ipole - Tabora. Niombe sana, barabara hizi zikamilishwe ili wananchi wa maeneo hayo kwa Mikoa ya Tabora, Katavi, Kigoma nao waweze kufurahia uhuru wa nchi yao kwa kupata barabara na kuweza kusafiri bila shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Mkoa wa Kigoma ipo barabara ambayo inatoka Kabingo – Kakonko – Kibondo - - Kasulu - Manyovu – Buhigwe anakotoka Makamu wa Rais. Barabara hii imetengewa fedha sasa huu ni mwaka wa tatu, hawa ambao wanasema ni wajenzi wa barabara kasi yao ni ndogo. Niombe Wizara husika ifanye ufuatiliaji wa jumla ili barabara hii iweze kukamilishwa na wananchi waweze kupata huduma muhimu hasa hiyo ambayo nimeitaja ambayo ni barabara. Niombe sana barabara hiyo ikamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika Wilaya ya Kakonko, tunayo barabara ya Kakonko – Ruhuru - Nyakiyobe - Gwarama - Mpaka wa Mhange. Mpaka huu kuna soko ambalo linaunganisha Mkoa wa Kigoma na Wilaya ya Kakonko na nchi jirani ya Burundi. Pale limejengwa soko kubwa, soko la Kimataifa lakini halina barabara. Niombe barabara hiyo ijengwe kwa maana ya kutuunganisha na wenzetu wa Burundi ili biashara ambayo inastahili kufanyika katika eneo lile ambalo tayari kuna soko iweze kufanyika na iweze kukamilika kwa wakati na kuweza kutusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inakwenda sambamba na barabara ya kutokea Gwarama - Nabibuye inakwenda kuunga kwa jirani yangu Mheshimiwa Ndaisaba Wilaya ya Ngara.

Niombe sana barabara hii nayo iweze kukamilishwa. Barabara hizi zikikamilika wananchi wetu watakuwa na uwezo wa kusafirisha bidhaa kutoka vijijini kwenda mjini na kwenda kule ambako soko linapatikana. Hii ni pamoja na barabara ya kutoka Kibondo kwenda mpaka Mabamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kilimo, wananchi wetu wengi ni wakulima, hili halina ubishi. Shida inayojitokeza katika eneo hilo ni upatikanaji wa pembejeo, mbolea na matrekta tena kwa wakati. Niombe, kwa kuzingatia kwamba kilimo ni uti wa mgongo, wananchi wetu wengi wanategemea kilimo, pembejeo kwa maana ya mbolea, zipelekwe kwa wananchi wetu mapema ili ziwasaidie katika kuandaa kilimo na kulima vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mazao ya kimkakati, mwenzangu kaka yangu Mheshimiwa Vuma asubuhi alizungumzia masuala ya kilimo cha chikichi kwa upande wa Mkoa wa Kigoma. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ametumia muda mwingi sana kuja Kigoma kuhamasisha zao la chikichi. Ametumia muda mwingi na amejaribu kwa nguvu zake zote kuhamasisha jamii ile na wananchi wameamka. Niombe sana katika bajeti hii, nguvu kubwa ipelekekwe katika zao hili na hasa ikizingatiwa kwamba zao hili litaleta jibu sahihi katika tatizo ambalo linalotukabili la upatikanaji wa mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba ipo mikoa mbalimbali ambayo inaweza ikalima zao hili. Mkoa wa Kigoma ukiwa mkoa wa kwanza, lakini zao hili linaweza likalimwa vizuri sana katika Mkoa wa Rukwa, Katavi na Tabora. Niwaombe sana Mawaziri hasa Waziri wa Kilimo, tafiti zifanyike, ufuatiliaji ufanyike, pembejeo zipelekwe, wataalam wapelekwe ili kuhakikisha kwamba zao hili linalimwa kwa wingi katika mikoa yetu na ikiwa katika mazingira hayo nina uhakika itatusaidia kumaliza tatizo linalotukabili la upatikanaji wa mafuta katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la chikichi kama ambavyo nimesema, ndilo jibu la tatizo la mafuta katika nchi yetu. Maeneo mengi katika nchi hii, chikichi inaweza ikalimwa. Ipo Wilaya ya Kyela katika Mkoa wa Mbeya zao hili linaweza likakubali, lakini maeneo mengine hata katika Mkoa wa Kagera, niombe tafiti zifanyike kwa ku-support Mkoa wa Kigoma kilimo hiki cha zao la chikichi kifanyike kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba kinajibu na kinatuletea matunda katika kuhakikisha kwamba shida kubwa ya mafuta inayotukabili inakwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nahitaji kuchngia ni upande wa madini. Yapo maeneo mbalimbali ambayo yamebainishwa kwamba yana madini ikiwemo Mkoa wa Kigoma, maeneo ya Mkoa wa Njombe kama ambavyo umezungumza maeneo ya Mchuchuma. Hata hivyo, yale maeneo mengine ambayo yamebainishwa bado hakuna tafiti za kutosheleza ambazo zimefanywa. Niombe maeneo yale ambayo yamebainishwa kwamba yana dhahabu, almasi na kadhalika tafiti zifanyike kwa kupeleka wataalam wa kutosha na mwisho kabisa uchimbaji uweze kufanyika kwa ajili ya manufaa ya nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Elimu. Kwanza niipongeze Wizara ya Elimu kwa kazi kubwa nzuri sana ya kuratibu na kusimamia elimu nchini, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia hotuba yake ya juzi katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi aliweza kuondoa kwenye asilimia ile inatozwa kwa wafaidika wa mkopo, asilimia sita, tunapongeza sana kwamba hiyo alizingatia na kuiondoa. Vile vile nimpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuratibu mafunzo kwa vijana wetu waliomaliza darasa la saba na kidato cha nne ambayo utekelezaji wake unaendelea sasa.

Mheshimiwa Spika, elimu bora ni ile inayotoa maarifa stadi na ujuzi kwa yule anayejifunza ili yamsaidie kukabili Maisha. Sasa kwa upande wa mtaala wa elimu katika nchi yetu mtaala uko vizuri, upungufu wake ni kumwongea maarifa stadi yule anayemaliza ili aweze kukabili maisha. Wapo vijana wamemaliza darasa la saba, wapo vijana wamemaliza kidato cha nne, wapo waliomaliza kidato cha sita, wapo waliomaliza degree na tunao mfano Walimu wako mitaani, wapo Madaktari wapo mitaani, muda huu wana maarifa ya ziada ya kuweza kuyakabili maisha wanaposubiri kuajiriwa. Kinachotokea hapo ni kwamba hapana, ndicho hicho ambacho sasa tunashauri kwamba Wizara iangalie katika mtaala wake waongeze maarifa hayo yatakayokuja kuwasaidia vijana wetu katika maisha.

Mheshimiwa Spika, nilifanikiwa kuwepo Uganda na Kenya kule kwa upande wa shule ya msingi wana somo linaitwa uchumi. Hilo wanasoma kuanzia Shule ya Msingi lakini kwa wale wanaosoma kwa hatua ya cheti au degree na kadhalika, huyo ambaye anategemea kusoma hawezi akapewa degree yake bila kusoma somo la ujasiriamali au entrepreneurship. Kwa hiyo, kwa maana ile asipopata yale maarifa hawezi akapewa degree yake. Ninachoomba kiongezwe hicho katika mitaala yetu, anapokuwa chuoni anasoma Ualimu au anasoma Udaktari aongezewe maarifa hayo ili yamsaidie, anapokosa kwenye ile kozi iweze kumsaidia kwenye maisha yake.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa wale wanaomaliza kwenye kidato cha nne au kidato cha sita, wengi wamezungumza masuala ya VETA. Niombe sana VETA ziongezwe kila wilaya kwa makusudi ya kwamba yeyote ambaye hakufanikiwa kwenda kidato cha sita, amemaliza kidato cha nne au amemaliza darasa la saba hakufanikiwa kwenda kidato cha kwanza mpaka cha nne, basi aweze kupata maarifa chuoni. Inaweza ikawa kwenye ufundi ujenzi, ufundi mbao au kilimo, hayo yatamsaidia.

Mheshimiwa Spika, katika hilo kuna mkopo unaotolewa kwenye vyuo vikuu, naona haja ya kushauri Serikali iweke mikopo kwa wanafunzi ambao wana soma kwenye vyuo hivi vya kati. Kuna nchi kama Uchina…

SPIKA: Mheshimiwa Kamamba sikukatizi, lakini kwa nini tunajenga hii concept ya kwamba VETA ni kwa wale wasiofanikiwa yaani hiyo inajenga kama kitu fulani inferior hivi. Endelea tu na mchango wako Makamu Mwenyekiti.

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, nazungumza hivi kwa sababu hilo kundi ambalo linakuwa limeachwa, lakini vilevile kwetu kwa sababu mimi ni Mwalimu kutokana na uelekeo wa mwanafunzi, huwa tunawashauri kwamba, kwa uelekeo huu anaweza akaenda akasoma kozi hizo, lakini yule ambaye anafanikiwa kwenda moja kwa moja sawa, lakini kwa yule ambaye anakuwa ameshindwa kupata nafasi ndio nawaangalia zaidi katika hoja yangu ambayo naijenga sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe waweke mkopo nao; kwanza wanatoka katika jamii yetu ni wanafunzi wa kawaidakawaida, lakini anapomaliza masomo yake, tuna hakika anaajiriwa moja kwa moja, anajiajiri, lakini pia huyu anakopesha kwa sababu akimaliza mafunzo yake, atakwenda kujiajiri na kwake anapata nafuu ya kuweza kurejesha mkopo huo kwa wakati, tofauti na huyu ambaye tunampeleka kwenye chuo kikuu, anasoma kwa miaka mitatu ama minne, anarudi mitaani, hana ajira, kwa hiyo si rahisi hata kurudisha ule mkopo anaokuwa amekopeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa hawa ambao wanakwenda kwenye vyuo wanasomea kazi tena kwa muda mfupi na ni wengi na anamaliza moja kwa moja anakwenda kupata kazi yake, ni rahisi kurudisha huo mkopo. Kwa hiyo, niombe katika mikopo ambayo inatolewa kwenye vyuo vikuu vilevile mkopo uweze kupolekwa kwenye vyuo vya kati.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye upande wa ukaguzi au udhibiti ubora wa shule. Wadhibiti Ubora wa shule ndio jicho la Serikali katika kuhakikisha kwamba elimu inatolewa kwa usahihi. Bahati mbaya hawawezeshwi vya kutosha kuweza kusimamia na kuratibu elimu nchini. Niombe wapewe fedha za kutosha waweze kusimamia elimu ya nchi yetu waweze kufanya ufuatiliaji waweze kushauri kwa wakati ili zile changamoto zilizopo katika shule zetu ziweze kurekebishwa, ziweze kusimamiwa na hatimaye elimu iweze kutolewa vizuri kupitia Wadhibiti Ubora. Kwa hiyo, naomba sana Wadhibiti Ubora ambao wapo katika halmashauri zetu zote wawezeshwe ili kuweza kusimamia.

Mheshimiwa Spika, hii inakwenda sambasamba na kuwapa stahili zao. Wadhibiti Ubora wa Wilaya wapo ambao wanasimamia idara. Kuna waraka ulishatolewa wa wao kupewa stahili za Ukuu wa Idara, lakini hawajaweza kupewa stahili hizo. Niombe wapewe hili ziwasaidie katika kusimamia elimu hiyo kupitia ukaguzi ambao wanaufanya.

Mheshimiwa Spika, wapo vijana ambao ni wabunifu, tunawaona kila siku na juzi nimemwona kijana mmoja amebuni mashine ya kukamua muwa kupata juisi. Wapo wengi, niombe Wizara iwachukue hao kwa sababu tayari wameshakuwa wabunifu, lakini wanachoeleza hawana fedha za kuweza kuwasaidia kuendeleza ule ubunifu. Naomba watafutwe, wafuatiliwe wapewe fedha, waendelezwe na hatimaye naamini kwamba wakiendelezwa kwenye ule ubunifu ambao wameshaanzisha, utawasaidia sana kujiongezea kipato lakini itasaidia kuweza kuongeza wabunifu wengi katika nchi hii na kuweza kuboresha miundombinu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kuna mmoja alitengeza mashine ya kutengeneza juisi, lakini yupo mwingine alitengeneza mashine kubwa ya kuchambua nyuzi za katani, niliona Tanga. Kwa kuanzia hawa wafuatiliwe, washauriwe na wawezeshwe ili waweze kuingizwa katika mfumo rasmi na hatimaye waweze kupata fedha za kuweza kusaidia katika kuendeleza ujuzi wao.

Mheshimiwa Spika, kwa leo naomba kuchangia hayo tu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia kwenye Wizara hii ya Uchukuzi. Moja, nikushukuru tena kwa kunipa nafasi, lakini kwa nafasi hii kwanza nikutaarifu kwamba Mkoa wetu wa Kigoma ndiyo pekee katika Mikoa yote 26 ambao haujaunganishwa kwa kiwango cha lami. Nitaarifu kwamba barabara ni uchumi na barabara ni maendeleo. Kutokuwa na barabara maana yake mazao yanayozalishwa katika Mkoa wa Kigoma hayana uwezekano wa kupelekwa kwenye soko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujaunganishwa Tabora kwenda Kigoma, hatujaunganishwa Mpanda kwenda Kigoma, lakini hatujaunganishwa Kagera kwenda Kigoma. Kwa nafasi hii tu nishukuru kwamba kuna makataba umesainiwa wa ujenzi wa barabara ya Kakonko – Kibondo – Kasulu hadi Buhigwe, lakini ujenzi wake unakwenda taratibu sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri hebu fika uangalie ujenzi unavyoendelea sasa. Nimetoka kule kwa shughuli ya kampeni, naona kama vifaa vipo, lakini ujenzi sasa ni mwaka mmoja na nusu, kama unaweza kuhesabu ni kama kilometa 10 tu basi. Sasa naomba atakapokuwa anawasilisha taarifa yake ya mwisho lini barabara hii itakamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo barabara katika Jimbo langu inaanzia Kakonko kwenda Kinonko kwenda Bwarama - Kabale hadi Muhange. Inapofika kwenye mpaka wa Muhange, pale kuna soko kubwa limejengwa zaidi ya shilingi milioni 583 ziko pale, lakini soko lile halifanyi kazi kwa sababu hatuna barabara. Naomba sana na bahati nzuri Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. Magufuli aliahidi ujenzi wa barabara hiyo ambayo ni kilometa 40, ili kuhakikisha kwamba shughuli zinafanyika, naomba atakapokuwa anawasilisha taarifa yake, lini barabara hiyo sasa itajengwa ili iunganishe nguvu ya huku kwenye Makao Makuu ya Wilaya hadi pale kwenye mpaka wa Muhange?

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wananchi ambao barabara hii inapojengwa katika Vijiji vya Kasanda - Kaziramihunda hadi Kabingo, hawa hawajapewa fidia kwa majengo yao. Naomba nayo atakapokuwa analeta taarifa yake ya mwisho tujue wananchi hawa watalipwa fedha zao lini? Zipo fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya kawaida kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara. Ukurasa 321, Mkoa wa Kigoma katika mikoa yote, haijapangiwa kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inakwenda sambamba na ukurasa 335 mpaka 336, fedha za matengenezo ya muda maalum kwa ajili ya barabara, Mkoa wa Kigoma nao kwenye eneo hilo haikupangiwa. Sijajua, kwa nini Mkoa wa Kigoma kama Mikoa mingine ilivyopangiwa haujaweza kupangiwa fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo bandari; pale Bandari ya Kigoma ya Kigoma kuna Meli ya Liemba, ina zaidi ya miaka 100. Wakati Mikoa mingine au kwenye bandari nyingine wananunua meli mpya. Kigoma wanasema kwamba wanakarabati ile ya zaidi ya miaka 100, kwa nini tusinunuliwe na sisi meli mpya, kama wanavyofanya kwenye bandari nyingine? Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iliangalie hili na sisi katika bandari ya Kigoma tuweze kupata meli mpya kama inavyofanyika kwenye Ziwa Victora kama inavyofanyika kwenye ziwa Nyasa na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upo uwanja wa ndege. Kigoma ipo jirani na Kongo, Kigoma ipo jirani na Rwanda, Kigoma ipo jirani na Burundi, lakini kupitia Ziwa Tanganyika kuna muunganisho kwenda Zambia. Naomba uwanja uweze kujengwa, uimarishwe kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wetu wa Mkoa wa Kigoma wanapata usafiri wa ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ambayo ndiyo inachukua moyo wa nchi kwa maana ya usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameweza kutujaalia wote angalau kufikia siku ya leo na kuweza kushiriki kwenye mjadala huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu nimpongeze Mheshimiwa Waziri, unaweza ukamuona yuko kimya, lakini anapeleka mambo yake vizuri. Mheshimiwa Waziri hongera sana kwa kazi kubwa unayoifanya. Lakini kupitia Wizara hii Serikali yetu inafanya kazi kubwa ambayo inahakikisha kwamba mipaka iko salama na sisi tuko salama na wananchi wanafanya shughuli zao. Mheshimiwa Waziri na Serikali yote hongereni sana kwa kuhakikisha kwamba mipaka yetu iko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watendaji hawa wanafanyakazi kubwa na nikichukua mfano Mkoa wa Kigoma, unapakana na nchi nyingi ikiwemo Kongo, Burundi, Rwanda, Na kadhalika, mpaka ni mkubwa na kwa maana ile inahitajika kuwe na doria ya hapa na pale. Lakini watu hawa maafisa hawa maaskari wetu hawana vitendea kazi hasa magari. Niombe wapatiwe magari kwa sababu kutokana na kwamba mfano kwa mpaka wetu wa Kigoma maana yake kuna muingiliano wa watu wa kutoka nchi mbalimbali kuna wanaoingia wanaotoka maana yake inahitajika ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha kwamba mpaka uko salama, lakini hawana vyombo hawana magari niombe sana katika bajeti hii Mheshimiwa Waziri uhakikishe kwamba hawa watendaji, hawa maaskari wanapata magari kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanafanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vipo vikosi mbalimbali ambavyo vimeteuliwa na Jeshi letu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mipaka iko salama katika Wilaya yetu ya Kakonko uko mpaka katika Kijiji cha Rumashi, upo mpaka katika Kijiji cha Nyakayenzi, kipo kikosi katika Kijiji cha Kabingo, kipo kikosi katika Kijiji cha Nyagwijima na kipo kikosi katika Kijiji cha Kakonko. Kote huko kama ambavyo wenzangu wamezungumza maaskari hawa hawana majengo, hawana nyumba za kuishi badala yake wanaishi kwenye nyumba za kupanga. Si rahisi sana kutimiza wajibu wao vizuri kwasababu wamechangamana na jamii niombe wajengewe nyumba zao maalum kama walinzi wetu ili ziwasaidie kuishi salama na waweze kutimiza wajibu wao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya yetu ya Kakonko inavyo vikosi ambavyo nimevitaja, lakini ukichukua kutoka Biharamulo ambako kuna kambi maalum ya ulinzi katika mpaka wa Mkoa wa Kagera na mkoa wetu, kikosi kingine kipo Kigoma, kwa hiyo, hapa katikati hakuna kikosi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba ulinzi upo. Niombe sana kianzishwe kikosi katika Wilaya ya Kakonko ambacho kazi yake itakuwa ni kuhakikisha kwamba mpaka umelindwa na wananchi wetu wanaendelea kuishi vizuri na kwa usahihi wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo nikushukuru na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Wizara hii ya Fedha; na kwanza kabisa naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya ya kutuongoza Watanzania, na kwa uchapaji kazi wake; na kwa hakika anavyochukua hatua kwa haraka sana katika masuala ya Kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze Mheshimiwa Waziri, rafiki yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, na Naibu wake, rafiki yangu Mheshimiwa Eng. Masauni. Kwa kweli mnachapa kazi vizuri, mnasikiliza, mnafuatilia na mwisho mmekuja kutoka na bajeti ambayo ni shirikishi. Mmewakiliza Wabunge wote mkafuatilia changamoto zinazowakabili katika maeneo yao na mwisho bajeti hii ambayo mmeitoa ni bajeti shirikishi inayojibu matatizo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya kuchangia ni mengi lakini nitachangia katika maeneo machache na yale ambayo yametolewa na wenzangu kuhusu vyanzo vya kodi na taratibu zake, ulipaji wa madeni ya posho kwa Madiwani, na yote ambayo yamechangiwa na wenzangu, naomba sana myazingatie na myafanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia maeneo machache na moja nitachangia sana katika eneo la ukamilishaji wa miradi. Ipo miradi mbalimbali, miradi ya kimkakati. Wakati nachangia mara yangu ya kwanza kabisa Bungeni, hoja yangu ya kwanza ilikuwa ni ukamilishaji wa miradi ambayo imeanzishwa. Ipo miradi kama reli ya kisasa (SGR), ununuzi wa ndege, ufufuaji wa viwanda, miradi ya umeme hasa Mradi wa Mwalimu Nyerere na ukamilishaji wa shughuli mbalimbali hasa katika jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo langu tuliahidiwa kama ambavyo wenzangu wamezungumza, lami ya kilometa tatu na pale tayari kuna milioni 75 pale kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Fedha zipo pale, lakini katika ujenzi ule imepelekea mradi ule kifusi kijazwe katika barabara na kwa maana ile hakuna shughuli za biashara zinazofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mazingira yale hata Serikali sasa inakosa kodi, biashara haifanyiki na kwa kuwa haifanyiki wananchi wale hawawezi kulipa kodi kama inavyostahili. Niombe sana Mheshimiwa Waziri apeleke fedha za kukamilisha mradi ule ili wananchi wafanye biashara na sisi kama Serikali tuweze kupata kodi. Hii inakwenda sambamba na umaliziaji wa barabara kama ambavyo nimezungumza ni umaliziaji wa miradi. Kuna barabara inayotoka Kankoko kwenda Kinonko kwenda Nyakiyobe kwenda Ngwarama, kwenda Kabare na kufika kwenye mpaka wa Muhange. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo limejengwa soko kubwa, kuna milioni 585, majengo yamekamilika, lakini hatuyafaidi vizuri kwa kuwa hakuna barabara inayokwenda pale. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii kwa kuwa ndio anamalizia malizia atenge fedha za kumalizia barabara ile ili soko liweze kufanya kazi na sisi ile biashara ya mpakani tuweze kupata kodi. Kwa hiyo ni kuweka fedha, lakini wakati huo huo Serikali nayo itapata fedha kupitia mpaka ule kupitia kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo; katika nchi yetu kilimo kinatoa ajira katika eneo kubwa sana, lakini yapo mambo ya kufanya. Moja; ni kuajiri watenda kazi, hatuna Maafisa Kilimo kwenye vijiji. Naomba sana katika bajeti hii Mheshimiwa Waziri anapohitimisha aangalie makandokando, vifedha vichache vinavyobaki, basi aweze kupeleka fedha kwa ajili ya ajira ya watumishi katika Sekta ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inakwenda sambamba na watalaam kupima udongo. Kwenye kilimo ni sehemu ambayo ajira inafanyika kwa ukubwa sana, lakini wananchi wetu ili mradi anaona ardhi hajui ardhi ile inafaa kwa zao gani, analima tu. Niombe taratibu zifanyike, ardhi ipimwe, ionekane inafaa kwa zao gani, ndipo wananchi waweze kulima pale. Hii iende sambamba na uongezaji wa thamani ya mazao kwa maana ya kupeleka mashine za kuchakata mazao mbalimbali kama muhogo, mahindi na kadhalika ili mazao yetu yaweze kuongezewa thamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pembejeo ni muhimu sana kwenye kilimo, lakini hazipelekwi kwa wananchi kama inavyostahili. Hii inakwenda sambamba na mbolea, lakini kuna suala la dawa, wananchi wanaanza kilimo bila mbolea, inafika muda ambao mbolea ingeweza kutumika kwa ajili ya kumfanya mwananchi alime vizuri hawezi kulima vizuri kwa sababu hana mbolea. Kwa hiyo mbolea ipelekwe, lakini dawa vilevile ziweze kupelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wilaya ambayo natoka Wilaya ya Kankoko ili kumbukumbu ziwepo, ni katika wilaya ambayo tunalima sana zao la alizeti. Kwa hiyo wakati inaandaliwa mipango mbalimbali kwa ajili ya kilimo cha alizeti, basi Wilaya ya Kankoko nayo iangaliwe na iwekwe kwenye mikakati. Hii inakwenda sambamba na Mkoa mzima wa Kigoma ambao zao letu ni chikichi, tuongezewe nguvu ya kutosha ili zao hili la chikichi liweze kulimwa kwa kiwango kikubwa na kujibu changamoto ya mafuta ambayo inakabili nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni pamoja na zao la miwa ambalo kwa kipindi kirefu limezungumzwa katika Mto Malagarasi, eneo lile ni zuri sana na linafaa kwa kilimo cha miwa. Niombe nalo katika mkakati wa jumla kuongeza uchumi wa nchi liweze kuwekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la elimu, tumefanikiwa sana kwenye upande wa elimu, lakini Walimu hawatoshelezi. Kuna idadi ya Walimu imetajwa ya 6,000, hawa hawatoshi. Niombe katika mkakati wa jumla walimu waongezwe ikiwa ni pamoja na kujenga nyumba za Walimu kwa sababu wanakaa mbali ikiwa ni pamoja na kujenga madarasa hasa mwishoni mwa mwaka inafika hatua sasa ni kukimbizana. Inafika hatua Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa hawawezi kwenda likizo kwa sababu wanatakiwa sasa wasimamie ujenzi wa madarasa. Naomba sana madarasa haya yajengwe mapema ili wanafunzi nao wawe wamejiandaa vizuri kwa ajili ya kuanza masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa mabweni kwa ajili ya wasichana; watoto wa kike wana changamoto nyingi pamoja na kwamba na wa kiume nao changamoto nyingi. Sasa niombe Waziri wa Elimu akisaidiana na TAMISEMI na Wizara ya Fedha kama ambao wanashikilia kihenge kikuu, waweke mkakati wa makusudi kujenga mabweni hasa maeneo ya vijijini ili watoto wetu wa kike waweze kupata sehemu ya kuishi vizuri na waweze kusoma, watumie muda mwingi kusoma badala ya kutumia muda mwingi kukimbizana na changamoto ambazo zinawakabili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii iende sambamba na ukamilishaji wa maboma ya maabara, maboma ya madarasa pamoja na maboma ya nyumba za Walimu. Naomba sana Serikali ichukue hatua ya makusudi ili kukabiliana na changamoto hizi na nina hakika watoto wetu watasoma vizuri na wataweza kukabiliana na changamoto ambazo zinawakabili na mwisho elimu itaweza kuwafikia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu nilitaka nichangie hayo, lakini yachukuliwe kwa ujumla wake ili kufanikisha maeneo yote kukamilisha miradi kwa wakati, lakini kuongeza nguvu katika madarasa na nyumba za Walimu ambazo zinajengwa katika shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru wewe mwenyewe kwa kunipatia nafasi kuchangia kwenye Mapendekezo ya Mwongozo wa Bajeti kwa mwaka 2022/2023. Kwa nafasi hii, nampongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kwa fedha nyingi sana ambazo ametuletea sisi Wilaya ya Kakonko kwa ajili ya ujenzi wa madarasa. Tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kakonko kwa fedha ambazo tumepata, zinakwenda kufungua na kujenga barabara maeneo mengine ambayo tangu dunia inaumbwa tulikuwa hatujawahi kupata barabara. Mheshimiwa Rais katupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza pia Waziri wa Fedha kwa Mpango mzuri aliotuletea. Hii inakwenda sambamba na Kamati yenyewe, Kamati ya Bajeti. Nawapongeza sana kwa kazi nzuri ambayo wameifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitachangia katika maeneo machache, moja ni uandaaji na utengaji wa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa miradi ya kimkakati, ipo miradi ya kimkakati kama umeme, mpango wa bwawa la umeme maharufu kwa jina la Mwalimu Nyerere, reli ya kisasa Standard Gauge na miradi mingine kama hiyo. Muda mwingi fedha ambazo zinapangwa katika maeneo hayo zimekuwa ni fedha kidogo naomba sana fedha ziandaliwe za kutosha ili miradi hiyo iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni miradi ambayo ni ahadi ya Viongozi wa Kitaifa, nimekuwa nikifuatilia muda mwingi Waheshimiwa Wabunge wengi wanauliza maswali kufuatia maeneo ambayo viongozi wa kitaifa waliahidi ujenzi wa miradi ya maji, ujenzi wa barabara na kadhalika. Niombe pia fedha ziandaliwe za kutosheleza maeneo hayo ili kuondoa changamoto ambayo inajitokeza muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu, napongeza sana kwamba fedha nyingi zimetolewa na zimepangwa kwa ajili ya ujenzi wa madarasa lakini haijaonyesha kwenye mpango huu fedha kwa ajili ya nyumba za walimu. Kujenga madarasa bila kujenga nyumba za walimu hakutapelekea ukamilifu wake hii ni kwa sababu fedha zimepelekwa kwenye maeneo mfano shule shikizi, ukifuatilia kwa ukaribu shule shikizi zimejengwa katika maeneo mapya, mengi ni maeneo ambayo ni ya wafugaji, mengi ni maeneo ambayo ni ya wakulima kwa hiyo ukijenga madarasa katika maeneo hayo bila kujenga nyumba za walimu katika maeneo hayo kwa ukaribu maana yake wanafunzi watakuwa wanasoma na madarasa yatakuwa yanaachwa wazi, maana yake hayatakuwa na uangalizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba fedha zitengwe kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu na hii itapelekea walimu kukaa karibu na shule lakini hii pia itapelekea shule kuwa na ulinzi kwa maana kwamba walimu watakaa karibu na shule. Vilevile madarasa yale yataweza kutumika vizuri. Kwa hiyo hamuendi kama ambavyo tumeamua kupeleka fedha nyingi upande wa ujenzi wa madarasa basi tupeleke fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la mabweni, mabweni ni muhimu sana kwa ajili ya watoto hasa watoto wa kike kwa upande wa shule za sekondari, kutokuwa na mabweni kunapelekea wanafunzi hawa kusafiri umbali mrefu, kutokuwa na mabweni kunapelekea wanafunzi hawa kukutana na vishawishi njiani. Niombe fedha za kutosho zipelekwe katika maeneo hayo tuwe na mabweni ya kutosheleza wanafunzi waishi maeneo hayo ili kuwa na uhakika kwamba watakuwa na muda mzuri wa kujisomea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajira kwa walimu tumefanikiwa vizuri kwenye mpango wa elimu bila malipo, wanafunzi wapo wengi wa kutosha na muda huu tunapeleka madarasa ya kutosha lakini walimu bado hawajaonekana kwamba kuna mpango maalumu wa kuweza kuajiri. Ninaomba fedha ziandaliwe mpango uandaliwe mzuri ili walimu waajiriwe wa kutosha waweze kusaidia vijana wetu katika maeneo hayo, hii iende sambamba na ujenzi wa maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule zetu za sekondari sawa tunapeleka fedha tunajenga madarasa lakini ukamilishaji wa maabara, ninaomba fedha ziandaliwe za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa maabara. Ujenzi wa maabara unapelekea moja wanafunzi kupata nafasi ya kujifunza kwa vitendo, wakijifunza kwa vitendo inapelekea uelewa mkubwa zaidi niombe hii iende sambamba na ujenzi wa maktaba katika shule zetu za sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ni muhimu sana hasa miundombinu ya barabara, Mkoa wetu wa Kigoma haujaweza kuunganishwa kwenye Mikoa mingine kutoka Tabora kwenda Kigoma, Mpanda kwenda Kigoma, Kagera kwenda Kigoma. Ninaomba fedha ziweze kupelekwa katika maeneo hayo, barabara ziweze kukamilishwa na kuweza kupelekea huduma muhimu sana kwa wananchi wetu hasa kwa Mikoa ile ambayo haijaweza kuunganishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Katika hili nianze tu kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa huduma ambazo amezitoa hasa katika Wilaya yetu ya Kakonko. Mama Wilaya ya Kakonko tumemuona katika madarasa, Mama Wilaya ya Kakonko tumemuona katika hospitali, na kadhalika, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu Kigoma barabara ndiyo siasa, lakini bahati mbaya Mkoa wa Kigoma kwa nchi hii ndiyo Mkoa haujaungwa katika Mikoa mingine, kwa maana ya kuunganishwa na mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujaunganishwa Mkoa wa Kigoma kutoka Katavi, hatujaunganishwa Mkoa wa Kigoma kutoka Tabora, hatujaunganishwa mkoa wa Kigoma kutoka Kagera. Ni aibu kwa Serikali naweza nikasema. Katika hotuba ya mwaka jana Serikali ilisema kwamba, kuna hatua zinafanywa na wataalam wako kule, lakini kazi inayofanyika si njema. Ninaiomba Serikali ichukue hatua ya kusukuma mafundi ili waweze kukamilisha barabara katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimezungumza, ipo barabara ambayo inatuunganisha Wilaya yetu ya Kakonko na nchi ya Burundi ambayo inaanzia Kakonko kwenda Kijiji cha Kinonko kwenda Nyakiyobe kwenda Gwarama kwenda Kabale mpaka Muhangi. Mpaka ule Serikali imejenga soko kubwa sana, lakini soko lile halina huduma, halitoi huduma vizuri kwa sababu hatuna barabara ya kuweza kutuunganisha pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilichangia na nimeomba sana muda mwingi, hebu Serikali chukueni hatua ya kuijenga barabara hii ambayo itaongeza uchumi kwa nchi hii. Pale maji yapo, pale umeme upo, lakini shida ni hiyo barabara. Naiomba sana Serikali itujengee barabara hiyo ambayo ni barabara ya kimkakati, itatusaidia kama nchi kuweza kupata fedha katika mpaka ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo ahadi za Serikali. Mheshimiwa Lusinde amezungumza hapa, kila Mbunge akisimama atasema darasa langu halijakamilishwa, daraja langu halijakamilishwa, alisema Waziri Mkuu, alisema Mheshimiwa Rais. Kwa nini usifanywe utaratibu miradi yote, ahadi zote za Viongozi zikaweza kuorodheshwa na tukaambiwa Wabunge wote kuona kwamba, mimi ahadi yangu ambayo alitoa Rais, mimi ahadi yangu alitoa Waziri Mkuu, mimi ahadi yangu aliyotoa Makamu wa Rais imewekwa kwenye orodha, ili wote tujue kwamba, ahadi ambazo zimetolewa na viongozi zimeorodheshwa na hivi kila Mbunge ataweza kuridhika kwa sababu, atakuwa na uhakika kwamba, ahadi iliyotolewa na kiongozi kwenye eneo lake ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba ikishafanywa hiyo tuanze na ahadi ambayo ilitolewa na marehemu Magufuli katika Mji wa Kakonko. Katika Mji ule tuliahidiwa kilometa tatu ambazo ziko ndani ya Mji wa Kakonko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie kwamba, mpaka muda huu ndani ya miaka Sita tumeweza kujengewa kilometa 0.63. Kwa hiyo, niombe Serikali inapochukua hatua ya kuiorodhesha miradi yote, basi namba moja uwe mradi huo wa ujenzi wa barabara ya lami katika Mji wa Kakonko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo barabara za Mji wa Dodoma. Mji wa Dodoma unakua, hatutegemei kwamba Mji wa Dodoma sasa utakuja urudi kuwa Manispaa au uje kuwa Mji wa kawaida ni Jiji sasa, lakini Serikali hatuoni mbanano wa magari kwenye Mji huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii kutoka Kisasa kuja hapa mpaka Bungeni ni shida kweli. Polisi wakishafunga barabara, labda Waziri Mkuu anakuja au Makamu wa Rais anakuja kwenye shughuli mbalimbali, inakuwa ni mtafutano kwelikweli. Ninaiomba Serikali ichukue hatua ya kujenga barabara ambayo itaruhusu malori badala ya kuingia Mjini katikati Dodoma, basi malori yaweze kupita kule pembeni, nina hakika itasaidia Mji katikati kubaki wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo huduma ambayo inatolewa kwa upande wa miamala ya fedha. kutoa fedha kutoka kwenye account kwenda kwenye mitandao tofauti-tofauti mfano, tiGO Pesa, M-Pesa, na kadhalika ili uweze kupata huduma hiyo lazima uwe na shilingi 1,000. Inaweza ikatokea kwamba, wakati uko kwenye utaratibu wa kutoa huduma hiyo network ikakata, Shilingi 1,000 imeshachukuliwa, utakaporudia usifanikiwe 1,000 imeshachukuliwa, ukirudia na kadhalika utastukia kwamba, Shilingi 5,000 zimekwenda lakini huduma ile haijatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali ifuatilie hilo, kuona uwezekano wa kwamba kama huduma haikuweza kupatikana basi hizo fedha zisiweze kutoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mitandao ya simu Wilaya yangu ina shida sana ya mtandao wa simu, shida ipo kubwa sana katika Kata ya Nyamtukuza, Kata ya Nyabibuye, Kata ya Gwarama, Kata ya Rugenge, Kata ya Mugunzu, Kata ya Katanga, Kata ya Kanyonza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi nikiwa nyumbani siku ukinitafuta usinipate ujue kwamba niko nyumbani mawasiliano hadi nyumbani kwangu hayapo, ninaiomba Serikali ichukue hatua hasa kwenye Mikoa ya pembezoni na Wilaya za pembezoni ziweze kupata huduma ya mitandao ya simu ili tuwe na uhakika kwamba kila Mtanzania anaweza akafurahia mawasiliano ya simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upande wa umeme, bado kuna shida ya umeme katika Mkoa wa Kigoma. Muda huu tunaambiwa kwamba kuna ujenzi wa lane ya umeme kutoka Nyakanazi kwenda Kigoma, hao mafundi hatuwaoni ninaomba Serikali ichukue hatua ya haraka kuona kwamba Kigoma nasi tunapata umeme kwa ajili ya maendeleo ya Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya kwa Taifa letu kwa kutuletea maendeleo ambapo sasa nchi yetu inapiga hatua haraka kutokana na kazi nzuri, tunampongeza sana.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Buyungu ni miongoni mwa majimbo ambayo tumepewa fedha nyingi. Tunashukuru na kupongeza sana.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti hii pamoja na mambo mengine tunaomba kupewa fedha kwa ajili ya ukamilishaji ujenzi wa stendi ya mabasi ya mjini Kakonko unaondelea; fedha kwa ajili nyumba za walimu na madaktari; fedha za ujenzi wa barabara kilometa tatu alizoahidi Rais Magufuli na zitengwe fedha za dharula kwa ajili ya TARURA.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hoja iliyopo mbele yetu, hoja ya Wizara ya Kilimo. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa fedha nyingi ambazo amepeleka katika jimbo letu, lakini kwa bajeti hii ametukumbuka pia, ametupelekea fedha. tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze pia Mheshimiwa Waziri, msaidizi wake Naibu Waziri na watendaji wote kwa kazi kubwa na hasa ikizingatiwa kwamba, Wizara yao ni Wizara ambayo inachangia kutoa huduma kwa zaidi ya asilimia 65. Tunawashukuru na tunawapongeza sana Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja. Naunga mkono hoja kwa sababu tu kwanza niliomba kwenye skimu za umwagiliaji mwaka jana na kweli mwaka huu wameweza kutuingiza kwenye ukarabati wa skimu ambazo zilikuwa na matatizo. Zipo Skimu za Mughwazi, Skimu ya Ruhwiti na Katengela, hizi zimetengewa fedha kwa ajili ya ukarabati, sisi Kakonko tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo pia skimu ambazo ni mpya zinakwenda kuanzwa kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Ipo Skimu ya Ruhuru, Skimu ya Mgunzu, Skimu ya Kanyonza na Skimu ya Churanzi, hizi ni skimu mpya, tunashukuru fedha zimewekwa kwenye bajeti. Sasa niombe fedha zikishapitishwa, nina hakika bajeti ya Waziri itapita, watuletee fedha ili kazi iweze kuanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze vilevile kwa kuzungumzia suala la mbolea. Mbolea ni muhimu sana kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, kilimo kinafanyika, lakini nizungumze kwamba, mbolea na mbegu bora hazipelekwi katika majimbo yetu kwa wakati. Wilaya yetu ya Kakonko tunapata mvua kuanzia mwezi Septemba, lakini mbolea inakuja kufika mwezi Desemba, wakati huo mahindi yanabeba, mbolea ile haiji kutusaidia. Hii inakwenda sambamba na ubora wa mbolea hiyo, katika Wilaya ya Kakonko na mimi mwenyewe ni mkulima, tumepata mbolea lakini ubora wake sio sahihi. Hili nililiwasilisha katika ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, nikatoa taarifa kwamba, mbolea tuliyopata na ambayo nimeitumia hata kwenye shamba langu, shamba halina mabadiliko yoyote.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwamba, Wizara ilituma wataalam, wakaja kuchukua sehemu ya mbolea ile iliyobaki, lakini vilevile wakachukua udongo, sijapata majibu. Kwa hiyo, niombe atakapokuwa anahitimisha tuweze kupata majibu sahihi, kuna Mbunge mwenzangu amechangia hapa suala la ubora wa mbolea tunayoipata haiko sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la bei ya mazao. Wilaya ya Kakonko moja ya zao letu ambalo ni la kimkakati ni alizeti. Alizeti ni zao la mkakati kwa Wilaya ya Kakonko likienda sambamba na zao la chikichi pamoja na muhogo, tatizo hatuna uhakika wa bei. Tuombe Serikali itusaidie kupata bei inayolingana na mazingira yetu, ili wananchi waweze kufaidi vizuri zao hilo la muhogo, ikiwa ni pamoja na zao la alizeti, ikiwa ni pamoja na zao la chikichi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla naomba nitoe sasa ushauri ufuatao: -

Mheshimiwa Spika, nina hakika Wabunge wametoa ushauri, wametoa maoni mbalimbali, haya yote hayawezi kufanyika bila kuwa na wataalam. Kwa hiyo, moja niombe Serikali iajiri watumishi na watumishi hao wapelekwe katika vijiji vyetu, wapelekwe katika mashamba yetu na wasimamiwe, ili waweze kufanya kazi ya kuwafikia wananchi, kutoa ushauri wa kitaalam. Nina hakika baada ya muda si mrefu Serikali yetu, nchi yetu inaweza ikapata chakula cha kutosha na kupata akiba kwa ajili ya matumizi mengineyo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu pia ni kuhakikisha kwamba mashamba yale ambayo yamepelekwa kwa ajili ya vijana maarufu kwa jina la BBT, hebu yapelekwe kwenye Mikoa ile ambayo ina mvua za kutosha. Asubuhi wamechangia kwamba imeletwa Dodoma, kwetu Kigoma limechukuliwa eneo dogo sana, ninaomba maeneo yale ambayo yana mvua za kutosha kama Mikoa ya Kigoma, Rukwa, Katavi, Ruvuma, Mbeya na Njombe, tupeleke huko,nina hakika mvua zipo za kutosha, ardhi ya kutosha na hivyo haitakuwa shida, vijana wetu wataweza kupata huduma hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ni kuhakikisha kwamba mbolea mbegu pamoja na viuatilifu vinapelekwa kwenye Majimbo yetu na kwenye Mikoa yetu kwa wakati, isiwe tunahitaji mbolea ya kupandia inakuja tunamalizia palizi. Tunahitaji mbolea ya kukuzia inakuja mahindi karibu yanaiva. Niombe sana pembejeo zipelekwe mapema katika Mikoa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia yapo mazao ya kimkakati ya chikichi na alizeti tuhakikishe kwamba nayo yanapewa bei ya kutosheleza kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, ninashauri kwamba Serikali ihakikishe kwamba inalinda bei ya mazao mbalimbali ambayo yanalimwa katika nchi yetu. Hii ni pamoja na kuhakikisha kwamba mazao yanahifadhiwa ikiwa ni pamoja na kujenga maghala ambayo yatasaidia wananchi wetu kuweza kuhifadhi mazao na kuyauza kwa wakati ambao utakuwa unastahili na ambapo wataweza kuongeza bei yao.

Mheshimiwa Spika, nishukuru tena kwa nafasi ambayo umenipa, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Bila kusahau kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutuletea fedha kwenye miradi mingi, ametufikia Kakonko, ametufikia Buyungu, tunamshukuu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Wakuu lakini bila kusahau watendaji kwa kazi nzuri, hongereni tunawapongeza sana. Lakini nipongeze Wizara kwa hatua nzuri ambayo mmefikia katika kuratibu mpango wa kurekebisha Sera ya elimu na mtaala, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, niipongeze Serikali kwa kupanua wigo wa kutoa huduma ya fedha kwa watoto wa kidato cha tano na sita ambapo takribani bilioni 10.3 zimetengwa kwa ajili ya watoto hawa tunaipongeza sana Serikali. Hii inakwenda sambamba na fedha za wanafunzi kwa ajili ya chakula, tumetoka shilingi 8,500 kwenda shilingi 10,000 si haba ni hatua nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze Serikali imeweza kupeleka miundombinu na imeweza kufanikisjha kwenye uandikishaji awali, Msingi na Sekondari. Lakini hali hii imepelekea upungufu mkubwa sana wa walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipitia kwenye takwimu yetu ambayo imetolewa na BEST (Basic Education Statistics in Tanzania) ya mwaka 2021, kwa upande wa elimu ya awali, walimu waliokuwa wanahitajika ni mwalimu mmoja kwa 40 lakini hali ilivyokuwa ni mwalimu mmoja kwa 75. Kwa upande wa elimu ya Msingi waliohitajika ni mwalimu mmoja kwa wanafunzi 45 lakini hali ilivyo ni mwalimu mmoja kwa wanafunzi 74. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi ambazo Serikali imeziweka kuajiri walimu 13,130, bado nisisitize Serikali kuhakikisha kwamba inaajiri walimu kwa ajili ya kukidhi mahitaji hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wilaya yangu ya Kakonko, kwa elimu ya awali walimu wnaohitajika ni 224 lakini wako walimu 14 tu upungufu ni walimu 210 upungufu ni sawa na asilimia 93.75 lakini kwa elimu ya Msingi mahitaji ya walimu ni 1189 wako 509 na upungufu ni walimu 680 upungufu sawa na asilimia 57. Nini unategemea katika maeneo kama hayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe ufahamu tu kwamba, athari ya mapungufu ya walimu ni tofauti na mapungufu ya Daktari. Daktari asipopatikna leo Vifo vitatokea leo hii lakini athari ya kutokuwepo kwa walimu athari yake ni ya muda mrefu. Niombe sana Serikali ihakikishe kwamba ina ajiri walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nishukuru tumeweza kupangiwa majengo katika maeneo tofauti. Tumetengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa katika shule mpya za Kazilamihunda na Nyamtukuza, lakini tumeletewa madarasa katika shule za Msingi, Bukiriilo, Gwarama, Kavungwe, Kigarama na Nyamwilonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu ya awali, tumeletewa fedha kwa ajili ya Shule ya Msingi Gwarama. Pia tumeletewa fedha kwa ajili ya Shule ya Msingi Bukirilo, Gwarama, Kavungwe, Kigarama na Nyamwilonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeletewa fedha kwa ajili ya nyumba Shule ya Msingi Nyakaviro, hii ni pamoja na VETA. Sisi tunaendelea kushukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo nichangie kwa upande wa wanafunzi wanaopata elimu hasa watoto wa kike baada ya kupata ujauzito.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tungehitaji kujua baada ya kuweka utaratibu huu, ni wanafunzi wangapi sasa wa kike wameweza kupata elimu baada ya Mheshimiwa Rais kutoa nafasi katika eneo hili? Baada ya hapo ni vema tukafahamu je, changamoto zilizosababisha hawa watoto kuweza kupata elimu mpaka wameweza kupata ujauzito na baadae wameweza sasa kurudishwa je, changamoto hizo tumezifanyia kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu Dada alikuwa yuko peke yake, sasa ana mtoto na anahitaji chakula kwa ajili ya mtoto huyu na anahitaji chakula kwa ajili ya mtoto huyu tunamsaidiaje sasa ili aweze kukidhi masomo yake? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye Sera ya elimu, mwanafunzi akiwa nje ya shule awe wa kike au wa kiume kwa siku 90 mfululizo anaondolewa shule. Tunaangalia sasa mwanafunzi huyu wa kike amepata ujauzito ni zaidi ya siku
270 anarudi shule, hapa panahitaji mjadala wa kutosha. Tunamsaidiaje sasa huyu mtoto wa kiume kijana, kwa mujibu wa Sheria hayuko shuleni kwa siku 90 ameondolewa. Kwa Sheria ile maana yake akiondoka ni moja kwa moja, tunamsaidiaje huyu mtoto wa kiume?

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria hiyo haitoi haki sawa, niombe Wizara ya Elimu iliangalie upya suala hili ili liweze kutoa nafasi sawa kwa watoto wa kike lakini vilevile kwa watoto wa kiume. Hawa Watoto wa kike tumeona changamoto ambayo inawapelekea mpaka wanapata ujauzito lakini mtoto wa kiume nae anakuwa na changamoto mbalimbali katika Maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wanaotoka wanakwenda kwenye boda boda, wapo wengine wankwenda kufanya biashara hali inayopelekea sasa aondolewe nje ya mfumo. Tungetamani nae kwa kuwa mtoto wa kike ameweza kupewa nafasi baada ya kupata ujauzito na huyu mtoto wa kiume pamoja na kwamba kwa mujibu wa Sheria siku 90 zimekwisha na yeye atafutiwe utaratibu ambao utamsaidia kupata elimu baada ya kuwa nje ya mfumo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango mwingine wa kwangu niupeleke kwa wadhibiti ubora. Mdhibiti ubora ndiye jicho la Serikali kwenye upande wa elimu lakini hawajaangaliwa ipaswavyo. Hawajaweza kupewa vitendea kazi vya kutosha ikiwa ni pamoja na fedha za kuweza kufanyia kazi na kuweza kufanya ufuatiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo takwimu ambazo zinaonesha kwamba ukaguzi wa shule haufanyiki kwa zaidi ya asilimia 30. Kwa hiyo, asilimia 70 ukaguzi wa shule zetu haufanyiki. Niombe sana Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba ukaguzi wa shule unafanyika ipasavyo na hasa ikizingatiwa kwamba ndilo jicho linaloisaidia Serikali kujua changamoto mbalimbali katika shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ulitolewa waraka ambapo wadhibiti ubora wakuu wa shule wa wilaya walistahili kupewa fedha za madaraka sawa na wakuu wengine katika halmashauri. Nikwambie kwamba waraka huo haujatekelezwa. Kwa nini hawajapea stahili zao hizo? Niombe sana Serikali iangalie uwezekano wa wadhibiti ubora wa shule kuweza kupewa stahili zao sawa na wakuu wengine wa idara katika halimashauri. Nina uhakika wakiwezeshwa wataweza kufanya zaidi.

NAIBU SPIKA: Ahsante kengele ya pili.

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa niombe UNESCO kama ambavyo tumeshauri kwenye Kamati liweze kuzingatiwa. Ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu. Kwanza nimpongeze na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea miradi mingi katika maeneo mengi sisi wananchi wa Wilaya ya Kakonko, tunamshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nipongeze Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri. Nipongeze kwa bajeti nzuri ambayo inakwenda kuwagusa wananchi wetu wa kawaida hasa kwa kuweza kutoa mkopo kwa wanafunzi katika vyuo mbalimbali hasa vyuo vya kati. Tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jicho sasa linapaswa lipelekwe kwenye vyuo vya kati hasa wale wanaosomea elimu amali ambao wanaweza wakawa ni wale wanaosomea useremala, wanaosomea ushoni, wanaosoma uuguzi na kadhalika; hawa wanasomea kazi. Tunategemea kwamba ndani ya muda mfupi wakikopeshwa watamaliza masomo yao na wataweza kujiajiri na hivi ni rahisi kwao kurudisha fedha ambazo Serikali imewakopesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi katika eneo la kuchangia kwenye bajeti. Ili bajeti iwe endelevu lazima kuwe na vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kui-support bajeti hii, na maeneo ambayo yanapaswa kusupotiwa (to be supported) ni pamoja na kuongeza vipato ambavyo vinatokana na wananchi wanaoingia na kutoka kwenye mipaka ya nchi yetu. Upo mpaka kama wa Mlongo katika Wilaya ya Kyerwa, upo mpaka wa Mabamba katika Wilaya ya Kibondo, upo mpaka wa Mnanila katika Wilaya ya Buhigwe lakini kwa Wilaya ya Kakonko tunao mpaka wa Mhange. Mpaka ule nilisha mwambia hata Mheshimiwa Waziri kwamba hebu tuwekeze katika mpaka wa Mhange, tupeleke wataalam tuweke forodha pale. Nina uhakika kupitia mpaka ule Serikali itaweza kupata fedha.

MHE. CONDESTER M. SCHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Aloyce Kamamba, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Condester Sichwale.

TAARIFA

MHE. CONDESTER M. SCHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nataka kumuongezea taarifa mzungumzaji anayeongea kwamba ni kweli mipaka mingi ambayo tumeona kuna mageti ya forodha ndiyo imekuwa ni chanzo kikubwa sana cha mapato. Mfano Boda ya Tunduma, Namanga, Holili, sehemu zote hizi na nchi yetu imebahatika kuwa na mipaka mingi sana, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge anachokiongea ni sahihi kama eneo lake kuna mpaka akiongezewa geti la forodha kitakuwa ni chanzo kingine kizuri sana cha mapato kwenye nchi yetu.

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Aloyce taarifa unaipokea?

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ninaipokea na ninaomba basi Mheshimiwa Waziri aweze kutuboreshea mpaka wetu wa Mhange kwa kupeleka wataalam, kwa kupeleka majengo pale na tupelekewe fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Kakonko kwenda Kinonko, kwenda Gwarama mpaka mpaka wa Mhange. Nina uhakika natumia maneno mengi kumwomba Mheshimiwa Waziri lakini akichukua ushauri huu iko siku atatumia muda mwingi kushukuru ushauri huu. Naomba sana ushauri huu uchukuliwe, waboreshe mipaka yetu nina hakika kwamba matunda yanaweza yakapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo ahadi za viongozi wetu, zikiwepo ahadi za Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Waheshimiwa Wabunge wengi wamekuwa wakiuliza katika maswali ya msingi lakini muda mwingine katika kuchangia kwao. Ahadi ni deni. Zipo ahadi ambazo Serikali imeweka kwa wananchi wetu katika maeneo mbalimbali ikiwemo Wilaya ya Kakonko. Katika mji wa Kakonko tuliahidiwa kilometa tatu na Hayati Rais Magufuli, tumejengewa kilometa 0.63, tuombe kilometa zilizobaki, kilometa mbili na ushee hivi zikamilishwe ili mji wetu wa Kakonko nao uweze kuwa na hali nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ambayo imewekwa mwaka huu kuna ujenzi wa Hospitali ya Kanda katika Mkoa wa Kigoma na vile vile kuna ujenzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Muhimbili. Nina uhakika fedha zikipelekwa na ujenzi ukafanyika, wananchi wa nchi jirani za Burundi, Congo, Zambia wataweza kupata matibabu katika hospitali hizo. Kwa hiyo pamoja na kwamba tutakuwa tunatoa huduma ya matibabu lakini itakuwa ni chanzo cha fedha kwa nchi yetu. Niombe sana fedha zitengwe, ardhi Kigoma tunayo ili ujenzi huo wa hospiatli ya rufaa pamoja na Chuo Kikuu Kishiriki cha Muhimbili, ujenzi uweze kuanza katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigoma tuna Ziwa Tanganyika lakini katika ziwa letu ukiangalia maziwa mengine kuanzia Bahari ya Hindi meli zipo, Ziwa Victoria meli zipo, Ziwa Nyasa meli zipo lakini Ziwa Tanganyika ni tatizo. Usafiri katika Ziwa Tanganyika ni tatizo, meli hatuna. Tuna miaka mitatu fedha zinatengwa lakini fedha haziendi. Tuombe katika bajeti ya mwaka huu kama ni kuteseka Mkoa wa Rukwa, kama ni kuteseka Mkoa wa Katavi, tumeteseka kwa muda mrefu sana. Tuombe kwenye bajeti hii fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa mikoa hiyo mitatu katika ziwa Tanganyika, tuletewe fedha meli ambazo ni za kukarabatiwa zikarabatiwe lakini na meli mpya ziweze kupelekwa katika maeneo hayo ili miji yetu ichangamke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia panapaswa kuwa na boti za kusafirisha abiria kutoka mji wa Kigoma kwenda Katavi huku chini, kutoka Kigoma kwenda katika miji ya Congo, kutoka Kigoma kwenda Burundi. Tukiwa na mchanganyiko wa wananchi wanaotoka na kwenda jirani, wanaotoka jirani kuja katika miji yetu nina uhakika biashara itakuwepo na uchumi wa wananchi wetu utaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo barabara ambazo ni za kuunganisha Mkoa wa Kigoma na mikoa mingine. Tunashukuru Serikali inaendelea kulifanyia kazi hilo; lakini bado kuna shida ya umaliziaji wa barabara inayounga Kigoma na Katavi pamoja na Kigoma na Rukwa. Kipo pia kipande ambacho kiko katikati ya Kibondo na Kasulu, pale bado pana tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi uliona kwamba kulikuwa na picha inazunguka kwenye mitandao, lakini ule sio udongo wa Kigoma na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa amekwishazungumzia hilo. Yote hiyo inatokana na changamoto ambayo tunaipata kwenye barabara. Tuombe, zile fedha ambazo zinapungua na hazijapelekwa kwenye maeneo hayo, zipelekwe na ujenzi uweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigoma inatengenezwa kuwa ni eneo la uwekezaji katika Kanda ya Magharibi, lakini hatuna uwanja wa ndege ambao unaweza ukaruhusu ndege kuingia na kutoka muda wote. Tuombe Uwanja wetu wa Ndege wa Kigoma upelekewe fedha za kutosha, thamani ambayo inahitajika ikamilishwe ili ujenzi unapokamilika nina hakika tutakuwa na uwezo wa kuwapokea wasafiri kutoka Nchi jirani za Burundi, Congo, Zambia kwa sababu ni rahisi kutokea upande ule wa maeneo yale. Hivyo, Kigoma kama Mkoa utakuwa na nafasi ya kufanya biashara nzuri zaidi na hivyo kuongeza mapato ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru tena kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia na kuwa mtu wa kwanza kwa muda huu wa jioni. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa, nzuri sana ambayo ameifanya hasa katika kupeleka fedha nyingi katika ujenzi wa madarasa, hospitali na barabara. Yapo maeneo mengine ambayo tangu dunia inaumbwa hayajawahi kupata barabara lakini kupitia Mheshimiwa Rais maeneo hayo sasa yamepata barabara, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwa kugusa eneo la kilimo na nianze kupongeza Serikali kwamba kupitia bajeti yake ya mwaka huu, Serikali imeweza kuongeza fedha nyingi kutoka Bilioni 200 kwenda Bilioni 900 tunapongeza sana Serikali kwa fedha hizo ambazo zimepelekwa. Lengo la Serikali nafahamu kwamba ni kuongeza chakula lakini vilevile kujibu changamoto inayokabili Serikali hasa ya mafuta ya kula.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao mojawapo ambalo Serikali imeweza kuliona na kuliweka ni zao la Chikichi. Kwetu Kigoma zao hili linakubali. Kwa hiyo niombe sana Serikali iongeze nguvu ya kutosha kwa kupeleka wataalamu wa kutosha wa mbegu ikiwa ni pamoja na mbegu ya chikichi katika eneo hili. Hii iende sambamba na kupeleka mbegu za kutosheleza kuweza kukidhi mahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi Kigoma ipo, ardhi siyo changamoto, lakini vile vile Kigoma mvua si tatizo, kwa hiyo eneo hilo linaruhusu moja kwa moja zao hilo kuweza kukubali, kwa hiyo naomba sana Serikali iangalie eneo hilo. Vilevile nasisitiza zao la chikichi kwa sababu zao la chikichi kupitia chikichi tunapata mafuta, kupitia chikichi tunapata sabuni, kupitia chikichi tunapata chakula cha mifugo na mazao mengine yote. Kwa hiyo, ili tuweze kufanikiwa naomba sana Serikali iongeze nguvu zaidi katika zao hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kukidhi zao hilo ambalo linaongeza mafuta lipo zao la alizeti. Kakonko tunalima zao hili vizuri sana, lakini changamoto ni upatikanaji wa mbegu, upatikanaji wa mbolea, niombe sana Serikali iandae mbegu mapema, iandae mbolea mapema, iweze kupeleka katika maeneo haya ili Kakonko na Mkoa mzima wa Kigoma tuweze kupata mafuta ya kutosha kupitia alizeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo miundombinu hasa ya barabara, barabara ni uchumi, lakini barabara ndiyo mishipa ya kuongeza uchumi katika nchi. Mkoa wetu wa Kigoma ikiwa sambamba na Mikoa mingine ipo mikoa ambayo haijaweza kuunganishwa kwa njia ya barabara hasa barabara ya lami. Kigoma haijaunganishwa na Tabora, Kigoma haijaunganishwa na Katavi, Kigoma haijaunganishwa na Mikoa ya Mwanza na Kagera. Niombe sana fedha zipelekwe haraka ili ujenzi uweze kukamilika na hatimae Kigoma kama Mkoa nao uwe umeweza kuunganishwa katika maeneo hayo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ipo reli ya kisasa ya Standard Gauge. Nashukuru sana kwamba Serikali imeweza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kutoka Uvinza kwenda mpaka Burudi katika Mji wa Itega na kwenda sambamba mpaka Congo. Najua kwamba Serikali imeweka katika mpango niombe sana Serikali iweze kuongeza fedha za haraka na ujenzi uweze kuanza mara moja kwa sababu barabara hiyo reli hiyo inahitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, elimu bila malipo. Serikali imeweza kupeleka fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba elimu kuanzia Msingi hadi Kidato cha Sita inatolewa bure kwa maana gharama zote zinakwenda upande wa Serikali. Vipo vyuo vya elimu ya kati wapo wanamaliza Kidato cha Nne wanakwenda kusomea ualimu, wapo wamemaliza kidato cha nne wanakwenda kusomea ufundi, wapo wamemaliza kidato cha nne wanakwenda kusomea udaktari na kadhalika. Hawa Serikali inawaangalia kwa kiasi gani? Maana tunaona kwamba Serikali imechukua eneo la huku chini shule ya Msingi na Sekondari Kidato cha Tano na Sita, imekwenda mpaka Chuo Kikuu lakini hapa katikati ambapo pana watoto wa Watanzania wengi Serikali haijaweza kupaona. Naomba Serikali iangalie eneo hilo wapo Watanzania wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, watoto hawa ambao wanakwenda kwenye vyuo elimu ya kati hawana tofauti na hawa ambao wanakwenda Kidato cha Tano na Sita na kwa taarifa vijana wengi sasa badala ya kwenda hata kwenda kwenye vyuo na kadhalika wanatamani sasa kwenda Kidato cha Tano na Sita kwa kuwa Serikali imeamua kwamba iwe elimu bure. Kwa hiyo, niombe kwa kuwa hawa vijana wanakwenda kusomea taaluma wanasomea ufundi, wanasomea u-nurse, wanasomea udaktari ambao wanatoka moja kwa moja na kuweza kujiajiri, naomba Serikali iweze kupeleka fedha katika maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ajira ya watumishi. Ni ukweli kwamba Serikali imejenga madarasa mengi safi, lakini imejenga vituo vya afya safi, imejenga hospitali nyingi safi, imejenga zahanati safi, lakini ni sawa na chakula kizuri ambacho hakina chumvi. Watumishi wanahitajika, Waalimu wanahitajika, Madaktari wanahitajika, sasa sijaona vizuri ni kwa kiasi gani Serikali inapeleka nguvu kubwa zaidi katika kuajiri hawa watumishi ili waweze kufanyakazi kwenye shule zetu za msingi, kwenye hospitali zetu, kwenye zahanati zetu na kadhalika.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala la barabara ambayo inatuunganisha Tanzania na Burundi. Taarifa zilizopo ni kwamba nchi ya Burundi imehamisha Makao Makuu kutoka Bujumbura kuja Mji wa Kitega na Mji wa Kitega uko kilomita kama 150 kutoka mpaka wa Muhange, lakini hatuna barabara sasa ambayo inatuunganisha Tanzania kwa barabara ya lami kutuunga na nchi ya Burundi hasa kwa kwenda Makao Makuu ya nchi ambayo ni Kitega. Barabara ambayo inastahili kutuunganisha ni barabara ya kutoka Kakonko kwenda mpaka kwenye mpaka wa Muhange. Niiombe Serikali ilifanyie kazi hili kwa kupeleka fedha za kutosha, barabara hiyo ijengwe na niombe sana Waziri wa Fedha upeleke wataalam kwenye mpaka huo wa Muhange ambao wanajua kwamba barabara ikishajengwa na wataalam hao wakipatikana watakusanya fedha, kwa hiyo hiyo fedha ambayo utakuwa umeitumia kujenga barabara nina hakika fedha hizo zitarudi bila kuchelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo barabara za Mji wa Dodoma. Dodoma ni Makao Makuu ya nchi, ni Jiji sasa, hatutegemei kwamba Dodoma itarudi iwe Manispaa au iwe Mji Mdogo lakini barabara zake ni tatizo. Ukiangalia sasa hivi Kiongozi yeyote wa Kitaifa awe Spika, awe Naibu Spika awe Waziri Mkuu awe Rais anapita Mji wa Dodoma unakuwa ni tatizo sehemu ya kupita. Sasa ni juu ya Serikali kuamua kulidhibiti tatizo hili mapema, isije ikawa kwamba baada ya muda ni mrefu sasa ndiyo tunaanza kufikiri kujenga barabara za kupitisha labda upande mmoja barabara tatu au nne upande mwingine barabara tatu au nne ni vema zikaanza kujengwa sasa ili kudhibiti tatizo la jam kwa maana ya wingi wa magari katika Mji wetu wa Dodoma. Kwa hiyo, napendekeza ijengwe barabara mapema ya kuweza kupitisha malori, badala ya malori kupita katika Mji wa Dodoma katikati basi malori hayo yaweze kupita pembeni kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa niendelee kupongeza Wizara ya Fedha kwa bajeti nzuri sana, ambayo imeiweka ina vipaumbele vyote muhimu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Serikali yetu inafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja nashukuru sana ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu lakini zaidi nawapongeza sana Wenyeviti wa Kamati kwa uwasilishaji mzuri wa taarifa pamoja na Kamati zote kwa kazi nzuri ambayo wameifanya, wametuwakilisha vema wanakamti kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais sisi Buyungu ametusikia, sisi Buyungu tumemwelewa, sisi Buyungu tunamshukuru sana. Mwaka kesho 2025 kazi yetu itakuwa ni moja tu kwenda kumpigia kura za ndiyo ili aweze kuendelea kutuongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ujenzi wa shule za sekondari na msingi. Katika maeneo ambayo Serikali imefanya kazi vizuri sana ni kwenye upande wa elimu ya msingi na sekondari. Yamejengwa madarasa mengi, vimejengwa vyoo, zimejengwa nyumba za walimu lakini idadi ya wanafunzi vilevile imeongezeka sana. Tunapongeza sana Serikali kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ongezeko la wanafunzi halikwenda sambamba na ongezeko la kuajiri walimu. Nikikupa takwimu kwa upande wa elimu ya sekondari uhitaji wa walimu kwa asilimia 47, na upande wa shule za msingi uhitaji wa walimu ni asilimia 42. Nikichukua Mkoa wa Kigoma upande wa uhitaji wa walimu sekondari asilimia 33 upande wa shule za msingi asilimia 46. Nikichukua Wilaya yangu ya Kakonko uhitaji wa walimu shule za msingi asilimia 38, upande wa sekondari asilimia 52. Ukiangalia kwa ujumla bado walimu waliopo na wanaohitajika ni nusu kwa nusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshangaa ni kuona kwamba walimu wapo kwa asilimia 47 lakini wanafaulisha kwa asilimi 80. Maana yake ni nini? Walimu wa nchi hii wamefanya kazi ya ziada kuziba pengo la walimu ambao hawapo. Hoja yangu walimu waajiriwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye uhitaji wa walimu na ajira, ajira inakwenda kwamba ikishapita umri wa miaka 45 hawezi kuajiriwa; lakini tunao walimu wana miaka zaidi ya kumi wako mitaani. Tuombe sana ajira ya walimu ifanyike ili walimu waweze kuja kusaidia katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za sekondari zimejengwa kila kata nchini, lakini shule hizi zinapojengwa zilizo nyingi zimejengwa katikati ya kata. Na kutoka Kijiji kimoja kwenda kwenye shule zinapojengwa ni umbali mrefu. Kwa hiyo jua likiwaka ni la wanafunzi hao, mvua ikinyesha ni ya wanafunzi hao. Niombe sana yajengwe mabweni kwenye shule zetu za sekondari. Yakijengwa mabweni tuna uhakika moja, wanafunzi wetu wawe wa kike wawe wa kiume tuna uhakika sehemu ambayo wataishi, lingine, itakuwa ni rahisi kwa walimu hawa kuweza kuwafuatilia. Inapotokea kwamba sasa wanafunzi hawa hawana sehemu maalum ambayo wanaishi ni rahisi kuingia kwenye vishawishi, ni rahisi kuja kukutana na mimba za utotoni. Niombe sana mabweni yajengwe ili yaweze kuhudumia watoto wetu katika shule za sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu ya watu wazima. Ukifuata takwimu ambayo walitupatia Wizara ya Elimu wakati wanawasilisha kwenye Kamati idadi ya ambao hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu inaongezeka kwenye nchi hii. Lakini tunao vijana wanaoanza shule ya msingi wanakosa kuendelea kutokana na sababu mbalimbali. Wapo wengine wanaanza lakiniwanakutana na vishawishi mbalimbali, wengine wanapata ujauzito, wengine wanakwenda kwenye biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mpango wa elimu ya msingi kwa walioikosa (MEMKWA) isimamiwe vizuri ili iweze kukidhi mahitaji ya vijana hao ambao wamekosa nafasi. Lakini wapo wale ambao wanakwenda sekondari, nao wanakutana na changamoto ya kushindwa kuendelea kutokana na mahitaji mbalimbali, mwingine anakwenda kwenye biashara na pia wapo wanaopata ujauzito. Tuombe sana vijana hawa wapewe nafasi ya kurudi shuleni, lakini vilevile walimu waajiriwe maalum kwa ajili ya kuhudumia vijana hawa ambao wanahitaji nao kupata elimu ya sekondari kupitia mpango wa elimu ya sekondari nje ya mfumo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Bodi ya Mikopo. Tunashukuru Serikali imeongeza fedha Bodi ya Mikopo, lakini si vijana wote ambao wanahitaji wanapata mikopo, vilevile wapo ambao wanapata lakini kwa kuchelewa. Tuombe sana Wizara ijipange vijana wetu wapte taarifa mapema wale ambao watapata; lakini iangalie zaidi wapo wanaostahili kupata hawapati, hawapati kwa nini? Tumbe sana Serikali ijipange ili kuhakikisha kwamba vijana wetu wanaohitaji mikopo wanapata na wapate kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mitaala mipya imeanza vizuri na wameipanga vizuri, na inakuja kujibu changamoto zinazokabili wananchi na vijana wa nchi hii. Hata hivyo hapakuwa na maandalizi ya kutosha. Walimu maalum kwa ajili ya kuendesha mtaala mpya hawapo; lakini vilevile vitabu havipo. Isitoshe, wale walimu ambao tunao wanaotekeleza mradi au mtaala huu mpya hawajapewa mafunzo. Niombe vitabu viandaliwe, walimu wapewe semina na walimu wengine waongezwe kwa ajili ya kukidhi huu mtaala mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumza sana kwenye upande wa michezo, lakini mimi kwenye upande wa michezo nitazungumzia suala uboreshaji wa michezo hadi kwenye ngazi ya jamii. Tunaipongeza Wizara, inatumia michezo kwa shule za sekondari (UMISETA) na shule za msingi (UMITASHUMTA) kupata vijana kutoka kule kuja kuwaendeleza. Lakini tunao vijana ambao hawako shule ya msingi lakini hawako shule za sekondari, hawa nao sasa tunawasaidiaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukamkuta haujui kusoma na kuandika lakini ukimpeleka kwenye mpira wa miguu ni mzuri sana. Uwekwe utaratibu maalumu wa kuhakikisha kwamba vijana wote walioko mitaani waandaliwe na wafuatiliwe kule ili kuhakikisha kwamba na wao wanaendelezwa kwenye upande wa michezo na katika hilo iandaliwe shule maalum ambako hawa vijana wanaotoka UMISETA, UMITASHUMTA wapelekwe katika maeneo hayo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako mzuri sana.

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)