Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Sagini Jumanne Abdallah (19 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nianze kwakumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa na kwangu mimi ni mara ya kwanza kuzungumza katika Bunge lako Tukufu. Niwashukuru pia wana CCM na hasa Wajumbe wa Butiama kwa kuniwezesha kupita kwenye kura za maoni na baadaye vikao vya chama vikaleta jina na baadaye nikapita bila kupingwa. Watu wa Butiama nawaahidi mtumishi bora uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishukuru familia yangu kwa kunipa moyo wakati wote wa harakati na wanaponipa moyo ninapohudumia wananchi wa Butiama kupitia Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hotuba za Mheshimiwa Rais zote mbili, napenda nianze kusema naunga mkono hoja hiyo, lakini nianze kwa kusema moja kwa moja zinapaswa kuwa rejea kwetu sote hususani wasaidizi wa karibu sana wa Mheshimiwa Rais kwa maana ya Mawaziri wetu na watendaji wote wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hotuba hizi hakuna jambo aliloliacha kwenye sekta ya kilimo, kwa mfano imezungumzwa kwa kirefu kuanzia ukurasa wa 13 mpaka wa 15 lakini imekwenda kutaja mifugo mpaka ukurasa wa 17 ambapo Mheshimiwa Rais amesisitiza umuhimu wa kuongeza tija katika mazao ya ukulima, ufugaji na uvuvi. Sasa ushauri wangu kwenye hili baada ya Rais kulizungumza kitaifa,ni jambo jema sasa wasaidizi wake warudi kwenye ngazi za utekelezaji ili kweli kilimo hiki kiweze kuleta tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya Wabunge wamezungumza hapa kiwango cha chini cha uzalishaji kwa heka, nimehudumu pale Simiyu, wastani kwa hekari moja ya pamba wananchi wa kawaida wanapata kilo mia sabini, lakini pale pale Simiyu Wilaya ya Maswa wapo wakulima bora wanaweza kupata kilo 1,200 kwa hekari moja. Sasa kumbe upo uwekezano wa kuongeza productivitykwa heka badala ya kufikiria kuongeza ukubwa wa mashamba ni muhimu wataalamu wetu wajikite kuwaelekeza wananchi hasa wakulima namna ya kuongeza uzalishaji kwa hekari moja, mbili kuliko kuongeza ukubwa wa mashamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye mifugo, nilikuwa naongea na wananchi wajimbo langu nilifanya ziara baada ya vikao vilivyopita, unakuta ukubwa wa ng’ombe kwa maana ya uzito ng’ombe anaweza akawa na kilo 90, tukawa tunatania baadhi ya wananchi wanakilo 150, 120 kwa uzito, ina maana mtu anamzidi ng’ombe uzito, jambo ambalo halikubaliki. Sasa Wizara ya Mifugo na Wizara ya Kilimo tunaona wameanza vizuri na kasi nzuri, nampongeza Waziri na Wasaidizi wake, lakini zaidi na Katibu Mkuu kwa kazi ambayo wameanza kwa kasi kwenye sekta ya kilimo, ambapo wameshakutana na wataamu lakini wamesogeza huduma za ugani karibu na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Simiyu kwenye viwanja vya 88 Nyakabindi utaalam wote wa sekta ya mazaoupo pale, kwa hiyo wananchi wetu wa mikoa ya jirani wamekuwa wakienda pale kupata elimu ya namna ya kuongeza tija kwenye mazao yao. Vile vile nimeona kwenye sekta ya mifugo Waziri na wataalam wanajitahidi kuhamilisha mifugo (artificial insemination)ili tuweze kupata koo bora na hivyo tuweze kupata uzalishaji wa mifugo iliyokuwa bora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amezungumzia miundombinu na mimi kwenye hili namuunga mkono sana na naomba Watanzania wengine tuendelee kumuunga mkono kwenye hili. Nakumbuka kabla ya Rais wetu hajaingia kwenye sekta ya ujenzi watu wa Kanda ya Ziwa wakitaka kwenda Dar es Salaam ilikuwa inalazimika wapite Bukoba, waende Kampala, waende Nairobi ndiyo wafike Dar es Salaam, unaenda kwenye nchi yako unapita kwenye nchi nyingine mbili, lakini leo mtu anatoka Bukoba anaingia sehemu yoyote ya Tanzania kwa lami, hivi ni vitu vya kumpongeza Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Jiji la Dar es Salaam tafiti za World Bank, nakumbuka niliwahi kutoa taarifa iliyokuwa inaonesha kwambakwa ile foleni tuliyokuwa nayo, tulikuwa tunapata hasara, tunapoteza karibu shilingi bilioni 40 kwa siku kwa ile foleni tu, leo Rais amesaidia kufungua hizo barabara, kuweka hizo flyover, kupanua ukubwa wa barabara,efficient ya usafiri umeanza kuiona, frustration ambazo wananchi walikuwa nazo, wawe wanafunzi kuchelewa shule, wawe wagonjwa wanaopelekwa hospitali, wawe wasafiri wanaoenda airport walikuwa wanakumbwa na msongo wa mawazo kwenye foleni za barabarani, lakini leo tunaona Dar es Salaam inavyopitika, tunataka mikoa yote iwe hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba Rais wetu aendelee, nina imani hata nchi jirani wanatuonea gere kwa namna tulivyopambana kuboresha miundombinu yetu. Ushauri wangu kwenye sekta hii ya usafiri na usafirishaji ni kushuka kule chini, Waheshimiwa Wabunge wamesema karibu wote kwamba kiwango cha fedha wanazopewa TARURA hakitoshelezi sekta ya TARURA kuboresha barabara za halmashauri na za vijijini. Nafahamu sababu, wakati wanaweka hivi viwango vya asilimia 30 kwa 70 kiwango cha barabara za halmashauri kilikuwa ni kilometa 58, leo tunazungumza zaidi ya kilometa 120,000 za barabara za vijijini, sasa kuendelea kuwapa kiwango cha asilimia 30 kwa kweli ni kuwatweza wataalam wetu wa TARURA na kufanya walaumiwe pasipo na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunazungumzia hizi barabara kuu, naomba pia barabara za wilaya zetu zizingatiwe. Nafahamu tunayo barabara kutoka Ziroziro kwenda Bukabwa, Bwiregi, Nyamimange, Silolisimba hadi Serengeti, ushauri wetu hizo barabara zisaidiwe. Naona sekta ya ujenzi wanajenga kilomita mbili mbili kila mwaka,kwa kasi hii itachukuwa miaka makumi kabla hatujafika mwisho. Piai ipo barabara ya kutoka Mazami kupitia Butiama kwenda Nata, hii nayo ikamilike, maana ni ya muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta ya nishati…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA:Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JUMANNE A. SAGINI:Mheshimiwa Naibu Spika, basi nashukuruna naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru wewe kwa kuendesha vizuri sana kipindi hiki cha hoja yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia afya na kutuwezesha kukutana hapa leo ili kujadili hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Ninamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini kama Msaidizi wake kwenye nafasi ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ninamshukuru Makamu wa Rais, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Waziri Mkuu, Waziri wangu Mheshimiwa Injinia Masauni kwa miongozo bora kabisa wanayonipa katika utekelezaji wa majukumu yangu. Pia ninawashukuru Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakuu wa Vyombo na Wasaidizi wao kwa msaada ambao wamekuwa wakinipa katika utekelezaji wa majukumu ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishukuru familia yangu kwa msaada na watoto kuvumilia wakati mwingine nakuwa nao mbali. Zaidi niwape shukrani za pekee wananchi wa Butiama kwa kuendelea kunivumilia ninapokuwa natekeleza majukumu haya, wakati mwingine nakuwa nao mbali na hasa siku ya leo wanapomhifadhi katika nyumba yake ya milele aliyekuwa Mbunge wa eneo hilo niliyepokea nafasi yake, Mheshimiwa Nimrod Mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mengi hapa, lakini mtoa hoja atakuja ayaguse mengi. Mimi mdogo wake niguse yale machache ambayo yametajwa na Waheshimiwa Wabunge. Moja ni kuhusu miundombinu ya majengo ya ofisi, makazi ya Askari wa vyeo tofauti kwa vyombo vyote vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge watakumbuka na katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wangu imesemwa bayana kabisa namna ambavyo dhamira ya Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan alivyoamua kushughulikia changamoto zinazokabili vyombo vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kwa uchache tu nikiwarejesha Waheshimiwa Wabunge katika ukurasa wa 50 wa Kitabu cha Bajeti mpaka 65, imeelezwa kwa kirefu namna ambavyo Jeshi la Polisi kwenye miradi yake ya maendeleo imegusia ukarabati wa ofisi, makazi pamoja na kujenga vituo vipya vya polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nyumba, mtakumbuka mwaka uliopita, Mheshimiwa Waziri wangu alizindua mkakati wa ujenzi wa nyumba 1,760 kama sehemu ya utekelezaji wa mpango wa maendeleo wa Sekta ya Usalama wa Raia na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa majengo, imetajwa hapa na Waheshimiwa tofauti tofauti kuhusu Magereza na Polisi. Nilitaka niwatajie maeneo machache ambayo tumefanya kazi kubwa. Kwenye upande wa Magereza imeelezwa vizuri sana kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wangu kwamba yako maeneo yanayomilikiwa na Jeshi la Magereza yalikuwa hayajamilikiwa rasmi kwa maana ya kuwa na hati lakini katika bajeti hii, zaidi ya shilingi bilioni 1.778 zimetengwa kwa ajili ya kulipa fidia, kulipia upimaji wa viwanja na kukabidhi hati kwa ajili ya vyombo vyetu hivi hasa Magereza. Ukurasa wa 19 mpaka 21, aya ya 31 mpaka 34 kwenye bajeti yetu imeeleza bayana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya maeneo hayo kwa mfano, nitaje Chuo cha Kiwira kitanufaika, Chalinze, Namtumbo, Nanyumbu, Hanang’, Muleba, Liwale, Kalambo, Mlele, Ikungi, Bahi, Wazo Hill, Kimbiji, Namvuti, Chamwino na Kaliua. Kote huko maeneo yameshalipiwa, kinachofuata ni ujenzi na hati tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa Jeshi la Zimamoto na Uokozi, zaidi ya shilingi milioni 210 zimetengwa kwa ajili ya kulipa fidia ili hatimaye jeshi hili limiliki maeneo hayo ili fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi ziweze kujengwa na kuepusha migogoro iliyopo kati ya wananchi na vyombo vyetu. Uhamiaji kadhalika wametengewa zaidi ya shilingi milioni 120 kwa ajili ya kulipa fidia. Polisi wametengewa zaidi ya shilingi milioni 554.8 kwa ajili ya kulipia fidia maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeelezwa juu ya uimarishaji wa Magereza, Magereza chakavu na mengine yanahitaji kujengwa upya. Niwakumbushe kwamba imeelezwa katika hotuba ya Waziri wangu kwamba mwaka huu unaokuja, Magereza 12 yafuatayo yatajengwa na kukamilishwa yale yanayoendelea kujengwa; Gereza la Msalato, Kaliua, Kakonko, Karatu, Kilosa, Kyabakari, Gairo, Kingurungundwa, Mpimbe na Sengerema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya ujenzi maeneo ya Zimamoto na Uokozi imeelezwa kwa ufasaha na Mheshimiwa Kichiki Neema Lugangira. Tumesema katika eneo hilo zaidi ya shilingi bilioni 2.3 zimepokelewa ili kuendeleza ujenzi eneo la Songwe, eneo la Simiyu, Manyara, Kagera, Katavi, Geita na Njombe na ujenzi unaendelea kutekelezwa na kwa mwaka ujao zimetengwa zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa majengo ya mikoa hiyo saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vitendea kazi kwenye upande wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, zaidi ya shilingi bilioni tatu zimetengwa kwa ajili hiyo na kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri mmesikia majadiliano yanayoendelea na moja ya nchi wahisani ili kupata zaidi ya shilingi bilioni 100 kwa madhumuni tu ya kuimarisha vitendea kazi kwa ajili ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji hususan magari na vifaa vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameeleza Mheshimiwa Mbunge kutoka Manyoni juu ya nini tufanye? Nimhakikishie Mheshimiwa, katika Wilaya yake ya Manyoni tumetenga gari. Atapewa gari la lita 1,000 kwa ajili ya ku-support shughuli za Zimamoto na Uokozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la Uhamiaji, mwaka 2022/2023 wamepata zaidi ya shilingi bilioni 5.6 kwa ajili ya kununua magari 30 kuwezesha utekelezaji wa majukumu yao. Mwaka ujao tumetenga shilingi bilioni 3.8 kununua magari 23 kusaidia utendaji hasa misako na doria ambayo imelalamikiwa kwa kiwango kikubwa hapa na baadhi ya Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu usalama barabarani. Imetolewa hoja hapa na Mheshimiwa Shabiby kuhusu umuhimu wa kuzingatia ratiba za magari yale badala ya kutegemea tu speed governor na vitu kama hivyo. Pamoja na kutumia hizo teknolojia, ushauri wake tunauchukua na tunaanza kuufanyia kazi. Baraza la Taifa la Usalama Barabarani eneo hilo ni eneo linalosisitizwa sana ili ratiba inayotolewa na LATRA izingatiwe na mabasi yote na basi litakalo-overspeed kwa maana ni mwendo hatarishi hata kwa usalama wa abiria na wenye mali, wadhibitiwe ili waende kama ratiba zao zinavyoonyeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa hapa kwamba baadhi ya Askari wetu wa Usalama Barabarani wanapungukiwa maadili na kufanya vitendo vinavyokiuka nidhamu na maadili ipasavyo. Niweze kusema IGP kupitia Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani, kwa kweli amekuwa madhubuti sana kusimamia nidhamu ya Askari wa Usalama Barabarani. Mtakumbuka IGP alivunja ile Kamati inayohusika na utoaji wa leseni za udereva na kuiunda upya baada ya kuonekana wanakiuka maadili. Nikwambieni, IGP amewaondoa baadhi ya Askari wasio na maadili kwenye kikosi hiki na kupeleka wengine ili kuhakikisha kwamba nidhamu inakuwa nyenzo namba moja katika utendaji wa jeshi letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge mmoja amezungumzia juu ya uhakiki wa leseni. Mheshimiwa nimekuona. Leseni zile zinahakikiwa kwa sababu uvunjwaji wa kile Kikosi cha Leseni cha Jeshi la Polisi ni baada ya kubaini kwamba zipo leseni zilizokuwa zinatolewa kinyume cha taratibu na wengine walizipata bila hata ya kufanya mafunzo.

Mheshimiwa Mewnyekiti, nikwambie, katika leseni zaidi ya 29,000 zilizohakikiwa katika muda huu mfupi, tumebaini uwepo wa leseni zaidi ya 2,000 ambazo hata wenye nazo walikiri kwamba hawakuzipata kwa utaratibu unaokubalika. Sasa ukishakuwa na watu wanaendesha vyombo vya moto, wanabeba abiria, hawakuhudhuria mafunzo yoyote na ukabaini, lazima uchukue hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo tuvumiliane. Hatuna dhamira ya kumnyang’anya mtu leseni aliyeipata kwa njia za halali na ni mtu ambaye anajua hiyo kazi ya uendeshaji wa magari. Kwa hiyo, nikuondoeni shaka kwamba, wale ambao watakuwa na leseni zao, hawatanyang’anywa kama wamepitia mafunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda wa dakika tano, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye kuchangia. Mpango ulioandaliwa na Serikali kwa ujumla wake ni mzuri hasa huu wa miaka mitano. Kwanza niwapongeze Wizara ya Fedha kwa namna walivyochambua zile changamoto, maana yake wameainisha ni vitu gani vilisababisha Mipango miwili iliyopita na hususan Mpango wa Pili kushindwa kutekelezeka kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ninayoiona tu ni ile mikakati inayowekwa ya kushughulikia hizo changamoto ili mpango wa III uweze kutekelezwa kwa ufanisi. Ushauri kwenye eneo hilo waichambue vizuri ile mikakati ya utekelezaji katika ku-deal na zile changamoto kwa kuwa kuainisha nani anafanya nini, wakati gani, kinahitaji rasilimali kiasi gani ili changamoto kama hizo zisije zikajitokeza kwenye utekelezaji wa Mpango wa Tatu, kinyume chake tunaweza tukaingiza statement tutafanya hivi ukajikuta hizo statement hazijachambuliwa vizuri, changamoto hizo zikaendelea kuathiri utekelezaji wa Mpango unaofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuzungumza ni juu ya ile mikakati ya utekelezaji wa Mpango. Changamoto kubwa ninayoiona hapa ni kuainisha Mipango ya Wizara, Idara Zinazojitegemea, Taasisi na Serikali za Mitaa, Mikoa na kadhalika. Serikali ni pana kweli, ukizungumza kwa ujumla tu kuainisha mipango ya MDAs na Mpango Mkuu wa Serikali, kumbukumbu zangu wakati niko Serikalini kuna tendency ya ku-cut na paste, mtu atakwambia Mpango huu umezingatia MKUKUTA, Vision 2020 – 2025, sijui SP ya Wizara, lakini ukienda kuangalia mambo yaliyozungumzwa huoni moja kwa moja kama yana-linkage zozote na hiyo mikakati mikubwa ya kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ushauri wangu kwamba Wizara ya yenye dhamana na fedha ifanye kama ilivyowahi kufanya huko nyuma, kutaka hizi MDAs zichambue unaposema umezingatia MKUKUTA, Vision 2020 – 2025, Mpango wa Miaka Mitano, awamu ya tatu, aoneshe kindakindaki nini kiko wapi na eneo gani. Kwa kufanya hivyo Mpango unaweza ukajikuta unatekelezwa, lakini vinginevyo inaweza kuwa ni wishful statements ambazo utekelezaji wake unaweza kuwa na changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuimarisha mifumo ya upatikanaji wa takwimu; imetajwa kama ilikuwa changamoto. Ningetamani waainishe sababu zilizosababisha kuwe na changamoto ya upatikanaji wa hizi takwimu na sasa tumejipangaje hizi takwimu ziweze kupatikana hasa kutoka kwenye private sector. Kama pamekuwa na changamoto na hatujaijua itakuwa ngumu awamu ijayo pia kuzipata hizo takwimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye muundo wa utekelezaji ambapo Wizara, Tawala za Mikoa na Halmashauri na private sector zinaingizwa, tuonyeshe details kama nilivyosema mwanzo kwani wakati mwingine unaweza kukuta hakuna link kati ya vinavyotokea kwenye Serikali za Mitaa na hivi vinavyokuja kuzungumzwa ngazi ya Serikali Kuu. Ili mpango uwe jumuishi ni vizuri hizo linkage zionekane bayana, badala ya kuwa na jedwali tunaloonesha local government lakini huioni vizuri kama ina match na yale matakwa ya kisekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Sekta ya Kilimo, nataka nishauri jambo; kwenye vijiji, kwenye kata ndiko shughuli za kilimo zinakofanyika, lakini Maafisa Ugani, wataalam wa kilimo kule ni wachache sana. Kuna kata moja Mheshimiwa mmoja alizungumza hapa ina barabara ya umbali zaidi ya kilomita 250, kata moja ina vijiji 16, hivi kweli kama una Afisa Ugani mmoja anawezaje kuwa effective kutekeleza shughuli za ugani kwenye kata kubwa kama hii? Ni ushauri wetu kweli kama tunataka kilimo kilete tija tuwe na vijana wanaojua eneo lao la kilimo, lakini tuwapeleke kule kilimo kinakotekelezwa hasa vijijini vinginevyo tutakuwa bado tuna changamoto tukidhani tutaongeza tija kwenye kilimo, lakini kisifanye hivyo kwa sababu ya uhaba wa wataalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ugharamiaji wa Mpango, nadhani wadau wanaotajwa na Serikali ni wengi sana, lakini utaona kuna future tutafanya hivi, litatokea hivi, nilidhani kwa vile Mpango unaanza 2021/2022 mpaka 2025/ 2026 hizi engagement zote zimeshafika, vinginevyo itafika Julai tutatumia muda mrefu sana ku-engage hawa wadau wote, halafu utekelezaji sijui utakuja kuanza lini. Kwa vile kuna dalili za kuchelewa, ni ushauri kwamba sasa Serikali ifanye haraka ku-engage na hizi Taasisi za Serikali, Taasisi Zisizo za Kiserikali, Wadau wa Maendeleo na kadhalika na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwenye kuianisha mifumo ya Serikali na ya sekta binafsi; unajua kwenye Serikali kuna urasimu, kuna junior officer anaandaa dokezo senior officer analipokea, Mkurugenzi Msaidizi anaweka comments, Mkurugenzi halafu liende kwa Katibu Mkuu, wakati mwingine inaweza ikachukua hata mwezi kufikia uamuzi, lakini kwenye sekta binafsi vitu vinaenda haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni maoni yangu kwamba pengine katika usimamizi wa Mpango huu kuwe na mfumo wa tofauti, tukifuata huu mfumo wa Serikali wa madokezo kupita kwa watu saba kabla ya uamuzi, tunaweza tukajikuta tumechelewa kutekeleza Mpango wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante, kengele imeshagonga.

MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, dada yangu Ummy na wadogo zangu Manaibu Waziri, nawafahamu ni wachapakazi kweli kweli, tuna imani na ninyi, mtafanya mambo makubwa. Imempendekeza Rais aweke Waziri na Manaibu wawili; ameweka Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu wawili. Nadhani nia ni kuhakikisha kwamba TAMISEMI inachemka kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi nawashukuru kabla sijaanza kuchangia moja kwa moja kwa namna mlivyo wasikivu na wasaidizi; miezi miwili iliyopita shule zangu mbili kule Butiama ziliungua moto; Shule ya Chief Ihunyo na Shule ya Bumangi Sekondari zote za A’ level, kwa kweli wepesi wenu wa kutatua tatizo lile umewatia moyo sana wananchi wa Butiama, walimu na wanafunzi wa shule zile. Endeleeni kufanya hivyo kwa Watanzania wengine. Mbali tu na kutimiza wajibu wenu, pia mnapata baraka za Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukisoma hotuba hii ya TAMISEMI, jukumu lao la kwanza walilolitaja ukurasa wa tisa inaendelea mpaka ukurasa wa 10, ni kusimamia utekelezaji wa Sera ya Ugatuwaji wa Madaraka D by D kutoka Serikali Kuu kwenda Serikali za Mitaa. Sera hii D by D wakati mwingine inazungumzwa, pengine nifafanue kidogo. Bahati nzuri ni- declare interest kwamba nimekaa kwenye sekta hiyo kwa miaka kadhaa, D by D inayotajwa inaweza ikatafsiriwa kama Decentralization by Delegation, Decentralization by Deconcentration and Decentralization by Devolution.

Mheshimiwa Spika, Tanzania tuliamua kuchukua mwelekeo wa Decentralization by Devolution ambapo unapeleka madaraka kikamilifu kwenye ngazi za chini kwa maana ya watumishi, fedha, ujenzi wa uwezo, lakini na kurekebisha mahusiano kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Hizo nyingine tulizijaribu Tanzania kwa nyakati tofauti na hazikufanya vizuri sana, ndiyo maana Serikali ikaamua kwenda kwenye D by D ya devolution. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye usimamizi wa rasilimali watu, inatakiwa tupeleke wa kutosha na wenye weledi. Ukiziangalia Halmshauri zetu, karibu kila Mbunge aliyezungumza ameongea kuhusu changamoto ya upungufu wa watumishi. Ukienda kwangu Butiama, nilishaieleza pale TAMISEMI; Idara ya Mipango, Idara ya Utumishi, Maendeleo ya Jamii, Ujenzi, Usafi wa Mazingira, vitengo vya ukaguzi wa ndani, TEHAMA, Ugavi, Uchaguzi, Sheria na Nyuki vyote vina makaimu; na bahati mbaya wengine wanaokaimu hawana hata sifa za kuja kudhibitishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali iko hivyo kwenye upande wa Utumishi. watumishi wanatakiwa wawe wanne, yuko mmoja; Katibu Muhtasi wanatakiwa sita, yuko mmoja Halmashauri nzima; Idara ya Fedha wanatakiwa 11, wapo sita na kadhalika. Unaweza ukatoa mifano mingi, ukishuka kutoka Makao Makuu ya Halmashauri ukaenda ngazi ya chini. Sasa kama kweli tunataka Local Government ziweze kutoa huduma stahiki kwa wananchi, ukishakuwa na upungufu wa rasilimali watu wa kiasi hiki, itaathiri tu. Ndiyo maana sikushangaa Butiama kupata hati yenye shaka, kwa sababu ina watumishi wachache sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka juzi, 2018 TAMISEMI na Serikali kwa ujumla ilikubali walimu wapandishwe madaraja. Kwa sababu ya kuwa na Afisa Utumishi mmoja tu na mdogo, hana hata uzoefu, hakuna kilichofanyika. Walipandishwa watumishi 50, watumishi zaidi ya 348 walibaki bila kupandishwa madaraja. Hii yote ni udhaifu unaotokana na upungufu mkubwa wa rasilimali watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala la fedha. Ukiangalia duniani kote, property tax ni jukumu la msingi la local authorities, yaani wanakusanya mapato yale na wanatumia huko huko. Sisi hapa tumebadilisha equation, mapato ambayo ni ya msingi duniani kote ya local authorities yamepelekwa Serikali kuu halafu TAMISEMI na Local Government wanaanza tena kuomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia Idara ya Bajeti inajadili labda one third irudi, wakishakusanya irejeshwe. But what is justification? Hawa ndio wanaohudumia hiyo mitaa, ndio wanasafisha mazingira yale, lakini fedha zile za property zinakwenda juu halafu kurudi kwake ndiyo kama hivyo mnavyosema kwamba hazienei. Hatueleweki kwa wananchi. Nadhani ifike hatua tusaidie TAMISEMI ipate fedha stahiki iweze kutimiza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia bajeti ya Serikali, vis-à-vis bajeti ya TAMISEMI. Bajeti Kuu ya Serikali ni shilingi trilioni 36.258 na bajeti ya TAMISEMI ni shilingi trilioni 7.683. Maana yake shilingi trilioni 28.575 inabaki Serikali Kuu wakati TAMISEMI inahangaika na mikoa 26, Local Government 185. Hivi katika mazingira haya TAMISEMI inawezaje ikatoa huduma fanisi kwa wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninajua tuna deni la Taifa ambalo ni shilingi trilioni 10.663 ukizitoa pale, bado Serikali Kuu inabaki na shilingi trilioni 17.912. Hawa ni Wizara ambao ni occasionally kugusa wananchi ni kwa nadra, labda miradi mikubwa ya Kitaifa. Wanaohangaika na mazingira ya wananchi, usalama wao, barabara zao, maji yao ni local authorities, lakini bajeti walionayo inahuzunisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, athari zake ni nini? Ndiyo hapo tunajadili TARURA kupata kupata fedha kidogo, barabara hawezi kuzitengeneza. Ukirejea kwa mfano kule Butiama, ukienda Kata ya Buswahili, barabara ya Kiagata – Wegero - Kongoto, ukienda Bwiregi – Masuhura - Lyamisanga mpaka Kirumi kupitia Mang’ora, ukienda Kukirango – Kyabakari - Kamgegi mpaka Mugango, ukienda Butiama – Muriaza – Kibubwa - Mwikoko - Masurura ni maeneo yasiyopitika kabisa. Sasa watawezaje hao TARURA kufanya kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati inaanzishwa hii Taasisi ya Road Board, kilometa za barabara zilikuwa 58,000, leo wana zaidi ya 100,000 lakini equation ya location ya resource ya Road Board Fund ni thirt by seventy, justification iko wapi? Tutamlaumu TARURA, tutamgawana, lakini kwa uwezo alionao hawezi akarekebisha hizi barabara zetu, labda kutokee miujiza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaona kuna maboma mengi ya madarasa, zahanati, ofisi kutokamilishwa, ni kwa sababu ya under financing. Ukienda head quarter za local authorities, kwa mfano Butiama, Makao Makuu hayajakamilika, certificate wanaleta, inachukua muda kuleta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Makao Makuu. Nyumba za viongozi angalau ya DC imekamilika pale Butiama, lakini hana ofisi, Halmashauri jengo halijakamilika na viongozi hawana hata nyumba na ni wilaya mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malalamiko ya posho za Madiwani ni rampant every where, posho zenyewe ni kidogo. Tungekuwa tunajenga hoja kwenye posho za Madiwani, Wenyeviti vya Vijiji, Wenyeviti wa Vitongoji zifikiriwe kuwekwa. Kwa kiwango hiki, ni shida kabisa! Ushauri wangu kwenye hili, Serikali iangalie vigezo vya kugawa financial resources kwa ngazi zake zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni yale mahusiano kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Naomba kushauri, TAMISEMI ikubali kujenga uwezo wa Wizara nyingine wajue dhana ya D by D ili waweze kuwa-support kwenye utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Niungane na wasemaji waliopita, kuwapongeza viongozi wa Wizara hii, Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara kwa mabadiliko yaliyo bora kwenye sekta hii ya madini. Tunachoomba ni kuboresha zaidi ili tuweze kunufaika kwa upana zaidi.

Mheshimiwa Spika, wapo baadhi ya hawa mineral explorers wanachukua leseni, wanashikilia maeneo kwa muda mrefu sana wakionyesha kufanya utafiti, lakini wananchi hawa wachimbaji wadogo wadogo wanakuwa wanafahamu kwamba maeneo hayo kuna madini. Matokeo yake inaanza kuingia migogoro baina ya hao wenye leseni na wale wachimbaji wadogo wadogo. Ushauri wangu, haya nimeyaona kwenye Jimbo la Butiama yakijitokeza. Kwa mfano, ipo leseni ya muda mrefu eneo linaitwa Rwamkoma, wana zaidi ya miaka sita wana leseni ile ya utafutaji madini. Pia lipo eneo lingine Katario, huyu mwekezaji wa kati ana leseni zaidi ya miaka nane lakini hajafanya chochote.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba, Wizara ikubali wawekezaji wa namna hii, haya maeneo wayaache kwa ajili ya wachimbaji wadogo waanze kuchimba madini, wafanye shughuli zao za kiuchumi badala ya kuendelea kuyaweka na wakati mwingine kukimbizana wakionekana ni vibaka wanaingia kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hili litafanyika kwa mfano kwenye Wilaya ya Butiama, Vijiji vya Nyakiswa, Kiawazaru, Katario, Kiabakari, Nyamisisi, Singu, Nyakiswa, watanufaika sana na wataweza kutoa CSR kwenye halmashauri na hivyo kuboresha huduma za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna eneo lingine ambalo tunadhani Serikali itusaidie, nimewatembelea wananchi kabla ya kuja huku Bungeni, wanasema, wamejifunza Mererani na Wizara ikawa-encourage kujenga fence kuzunguka kwenye mgodi wao unaitwa Irasanilo Mine kule Buhemba. Wamejenga ukuta ule zaidi ya milioni 200 wameshawekeza pale wale wachimbaji wadogo. Ushauri wetu kwamba Wizara isaidie kukamilisha fence ile ili wao waendelee kuwekeza kwenye uchimbaji, badala ya kuwaachia wananchi peke yao wale wachimbaji wadogo wakijenga fence kuzunguka eneo lote la mgodi. Hilo likifanyika litakuwa kwa kweli limewatendea haki sana watu wa Buhemba na Irasanilo Gold Mine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile, nafahamu kwamba, Wizara imeipa nafasi STAMICO kuanza kuchimba madini na eneo hili la Buhemba ni eneo lililochaguliwa na STAMICO. Sasa inavyoonekana kama Waziri ataiachia STAMICO ichimbe pale, wale wachimbaji wadogo wataathirika sana. Sasa, najua kuna maeneo mengi, lakini ikiwapendeza, Wizara ione uwezekano wa eneo la Kilamongo kuliacha kwa ajili ya wachimbaji wadogo badala ya eneo lote kuiachia STAMICO. Kwa sababu, STAMICO ni wachimbaji wa kiwango cha kati, itakuwa ngumu sana kwa wananchi hawa ambao walikuwa wanachimba pale itaonekana kama tumewatelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako malalamiko ya baadhi ya wawekezaji kwenye sekta hii hususan kwenye eneo la makinikia. Sasa, liko eneo ambalo lina dhahabu kule Butiama, eneo la Nyasirori, kuna wawekezaji wa Kichina pale, lakini tunamuuliza kwa nini hachangii maendeleo ya halmashauri, anasema zaidi ya miaka minne hajaweza kufanya chochote kwa sababu, so far nchini hapa hatuna teknolojia ya ku-process makinikia, bado yanatakiwa yasafirishwe nje, lakini anasema pana vibali ambavyo kwa muda wote huu havijaweza kutolewa na kwa hiyo, muwekezaji huyu yupo tu lakini hakuna chochote kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, ni ushauri wangu kama Serikali inatambua kwamba, hatujawa na technology ya ku-deal na haya makinikia, basi hizo taratibu za kuwezesha hawa wawekezaji kusafirisha makinikia huko nje ziendelee. Bahati nzuri katika ripoti ya Mheshimiwa Osoro ilionekana wazi kwamba, wanaweza kufanya tathmini ya kujua kwenye makinikia kuna dhahabu kiasi gani. Sasa kama uwezo huo wanao, wafanye assessment kwa yale makinikia, huyu mwekezaji aruhusiwe kuyasafirisha, kodi za Serikali zilipwe ili halmashauri na wananchi wanufaike.

Mheshimiwa Spika, najua kwamba iwapo mgodi ule utaruhusiwa kuendelea, zaidi ya ajira 500 zitapatikana. Kwa hiyo, Serikali pia itapata kupitia pay as you earn. Kwa hiyo, nashauri haya yakifanyika yatakuwa yametusaidia sana kule Nyasirori ili Butiama nayo ianze kuchangamka kwenye sekta ya madini kama maeneo mengine yalivyochangamka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa hatua mbalimbali zilizochukuliwa ili kuboresha maendeleo na usimamizi wa ardhi hapa nchini likiwemo suala la usimamizi wa wataalam wa sekta ya ardhi. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Waziri, Naibu Waziri na wataalam wakiongozwa na Katibu Mkuu, naomba kushauri kuhusu maeneo yanayohitajika kufanyiwa kazi zaidi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, mamlaka ya upangaji ni Mamlaka za Serikali za Mitaa lakini ushirikiano wao na wataalam wa Wizara kwenye baadhi ya maeneo si wa kuridhisha. Bahati mbaya wataalam wa ardhi kwa baadhi ya maeneo hawana ushirikiano miongoni mwao. Surveyors wanafanya kazi bila kushirikiana na wataalam wengine. Hali hii inadhoofisha uendelezaji bora wa ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ili kuondoa kuendelea kuwepo kwa makazi holela yasiyopangwa, nashauri kuwepo maamuzi ya kisera na kuandaliwe miongozo ya upangaji wa vijiji na miji midogo ambayo haijapangwa. Viongozi wa ngazi za kata na vijiji wapewe mafunzo ya namna wanavyoweza kupanga vijiji vyao na kusimamia mipango hiyo. Ikiwa wakati wa operation vijiji, vijiji vingi vilipangwa vizuri, hatuna sababu kuwa na vijiji visivyopangwa leo wakati wasomi wameongezeka, na vitendea kazi vimeongezeka. Vijiji hivi vinapozidi kukua vinasababisha kuwa na miji isiyopangiliwa yenye makazi holela, miji isiyokuwa na maeneo ya masoko, vituo vya mabasi, viwanja vya michezo, shule, vituo vya afya na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi inaongozwa na mtaalam kijana msomi, Profesa Magigi, lakini tume hii haijawezeshwa vya kutosha kifedha ili iweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Tume hii inapaswa kuzisaidia mamlaka zote za upangaji ambazo ni Halmashauri 184. Lakini kwa bajeti iliyopo na kwa kutegemea uhisani wa World Bank itakuwa vigumu kuzifikia Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ufanisi. Ushauri wangu hapa ni kwamba Tume hii itengewe fedha za ndani za kutosha ili ifanye kazi muda wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia kwenye sekta ya elimu. Nami niungane na Wabunge waliozungumza tangu jana kupongeza juhudi za Wizara ya Elimu katika kuimarisha na kuboresha elimu kwa ajili ya vijana wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze ushirikiano unaoimarishwa kati yao na TAMISEMI maana Wizara ya Elimu imebaki na sera, TAMISEMI imebaki na utekelezaji lakini tunaona jinsi wanavyoendelea kushirikiana. Wizara inatafuta resources inazipeleka TAMISEMI na TAMISEMI wanatekeleza miradi. Wizara inabuni maandiko yanakwenda kutelezwa na TAMISEMI kwa maslahi ya maendeleo ya nchi yetu. Hata huu Mpango wa Elimu bila Malipo najua uliandaliwa na Wizara ya Elimu na ikatoa miongozo na TAMISEMI ikaingia kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda nitajikita kwenye maeneo machache. Bahati nzuri mimi ni mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii lakini ukiisikiliza jamii yote imekuwa ikizungumza juu ya kutoridhishwa na mwenendo wa elimu kwa ajili ya maendeleo ya vijana wetu. Wakati mwingine tusipokuwa waangalifu tunaweza tukajikuta lawama hizi zinaelekezwa kwa Waziri na Waziri na wataalam wake wakaona kama ni watuhumiwa wa kushusha elimu yetu. Mimi naomba niwashauri kwamba viongozi wa Wizara na wataalam walioko Wizarani ni wawakilishi wetu tu katika kusimamia sekta ya elimu. Hivyo, ni vema watusikilize sisi wawakilishi wa wananchi na wadau wengine wanapozungumza mambo haya then wapange mikakati ya utekelezaji na uboreshaji kwa kuwahusisha wadau hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, naungana na wasemaje wote waliopita wanaosema elimu yetu ina changamoto. Sote tuna watoto na tunaona wakitoka vyuoni au shuleni hali zao huwaje. Wakati fulani nikiwa mmoja wa watendaji wa Serikali wataalam wanapoandika hata ile ku-draft barua Mtendaji Mkuu unakuwa na kazi ya ziada kurekebisha barua ile. Hii zote ni indicators kwamba uwezo wa vijana wetu ni changamoto kubwa. Kwa hiyo, ni vizuri tukishauriwa kwamba pana changamoto tuisikie na tuone namna ya kui-address. Kama mtu anamaliza chuo kikuu hawezi kuandika barua nzuri ya kuomba kazi inayoshawishi lazima tujue kwamba kwenye elimu yetu lipo tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, naomba nijikite kwenye Jimbo la Butiama, nimkumbushe Waziri, najua nililisema hili kwenye Kamati na nikajibiwa lakini nina maoni kwamba ni vizuri tukasikiliza na tuone namna ya kutanzua. Katika dhamira ya kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa letu, Serikali ilikubali kuanzisha Chuo cha Kilimo na Teknolojia cha Mwalimu (Mwalimu Julius Nyerere University of Agriculture and Technology) ni zaidi ya miaka kumi sasa hakijaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuo hiki kipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi yam waka 2010-2015 lakini kiko kwenye Five Years Development Plan I ya mwaka 2010/2011 - 2015/2016 lakini pia kiko kwenye Five Years Development Plan II ya mwaka 2016/2017 - 2021/2022. Kwa kuanzia Mkoa wa Mara na Wilaya ya Butiama walifanya mambo mengi; moja ni kukubali ku-sacrifices iliyokuwa Shule ya Sekondari O-Level na A- Level iitwayo Oswald Mang’ombe High School yenye ekari 86 yawe majengo ya kuanzia chuo kikuu hiki, lakini Butiama ilitoa ekari 573 kama eneo la kujenga campus kuu na eneo la Baiki. Pia tulikubaliana kwamba viwepo vitivo kwenye Wilaya zote za Mkoa wa Mara na kule Rorya Kinesi walioa jumla ya ekari 75; Serengeti eneo la Kisangula walitoa ekari 136 na maeneo yote yalipewa hati miliki kwa jina la chuo hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa upande wake ilitekeleza wajibu wake ambapo ni pamoja na kukubali kuanzisha mitaala 35; 26 ya shahada na 9 stashahada, miongozo na sera mbalimbali zaidi ya 25 ilitayarishwa na kuidhinishwa na mamlaka husika kwa maana Ofisi ya Rais, Utumishi na Msajili wa Hazina. Wizara pia ilitoa wataalam 79; academic staff 42 lakini watumishi mwega ambao ni administrative staff 37.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachohuzunisha tangu watumishi hawa wapelekwe zaidi ya miaka saba iliyopita chuo hakijaanza lakini wanalipwa mishahara. Kinachotuuma zaidi ni kwamba shule ile ilijengwa ili itumike lakini sasa haitumiki kwa ajili ya wanafunzi wa sekondari pia haitumiki kama chuo. Sasa watu wa Butiama na Mkoa wa Mara wanauliza chuo hiki kitaanza lini? Anayetakiwa kusajili chuo hiki ni TCU ambayo iko chini ya Wizara. Wizara chini ya Mheshimiwa Prof. Ndalichako ilikubali chuo kianze na wakapeleka wataalam including Deputy Vice Chancellors lakini hadi leo hakuna kinachoendelea. Wananchi wanauliza hivi lengo la Serikali lilikuwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi wananchi wa Butiama wanataka chuo kianze kama ilivyodhamiriwa awali. Wamechoka kusubiri, wanaomba majibu ya Serikali. Kwa kweli katika mazingira haya majibu yasipokuwa ya kuridhisha najiuliza hivi nitaachaje kuing’ang’ania shilingi ya Mheshimiwa Waziri wangu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imegonga.

MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja lakini naomba swali langu hili lijibiwe vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi hii ambayo kwa kweli ni kama ya nyota ya jaha baada ya wale wawili uliowataja kutoonekana hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kuungana na Wabunge waliopita kuipongeza Wizara ya Maji na Serikali kwa ujumla kwa namna wanavyofanya kazi. Mheshimiwa Aweso na Naibu wako mnaitendea haki Wizara hii. Nami niwaombee kwa Mungu muendelee kuwa na afya njema mchape kazi ili hatimaye malengo ya upatikanaji wa maji wa asilimia 90 mjini na asilimia 80 vijijini yaweze kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja hii ya Wizara ya Maji, nami niungane na wajumbe waliokwishachangia Wizara hii inahitaji fedha za kutosha. Nimekaa TAMISEMI tulikuwa na uhusiano wa karibu na Wizara ya Maji, wakati mwingine twaweza kuwalaumu lakini wanajitahidi kufanya kazi, maana wao lazima wapate consultant awaonyeshe kwamba hapa pana maji halafu wapate contractor achimbe, changamoto huja pale ambapo consultant ameonyesha pana maji hapa halafu contractor anakuja kaambiwa chimba mita 90, anachimba mita 90 hapati maji. Nadhani ndiyo maana Wabunge wanalalamika kwamba yanakuwa ni mashimo wananchi hawapati maji na imekuwa ni vilio vya muda mrefu tangu kwenye vile visima kumi vilivyofadhiliwa na World Bank miaka kadhaa iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni kubwa ni utaalamu na wataalamu wa sekta hii ya maji. Mimi nataka niamini kwamba wataalamu wale hawatoshi na Serikali ifanye uamuzi wa makusudi hasa kwenye kipindi hiki ambacho wanatumia mfumo wa force account kuwa na wataalamu wa kutosha kutimiza majukumu ya Wizara hii, vinginevyo itakuwa ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona pale Butiama sina hakika kama wataalamu wanazidi wawili wale ambao ni water engineers (wahandisi wa maji), lakini wana wale mafundi michundo (technicians), ambao ndiyo wengi lakini hawana uwezo wa kutelekeza miradi hii kwa utaratibu wa force account kwa sababu panahitajika na uzoefu wa namna fulani. Kwa hiyo, wakati tunazungumzia utekelekezaji huu bila kumwezesha nguvu kazi ya wataalamu itakuwa ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la ujumla ambalo nataka niliseme ni mfumo tu wa kuwaunganishia wananchi maji. Mimi hapa naomba nikiri kwamba Engineer Cyprian Luhemeja wa Dar es Salaam amefanya ubunifu mzuri sana ndiyo maana Dar es Salaam inafanya vizuri. Niliwahi kumuuliza kwa nini kasi ya upelekekaji wa maji kwa wananchi imekuwa kubwa, anasema yeye anatumia mapato yake ya ndani kununua vitendea kazi na kusambaza maji mpaka kwa walaji. Kwa hiyo, gharama zile zinakuja kufidiwa baadaye kwenye bill za watumiaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini huku wilayani wananchi wanatakiwa walipie vifaa, vifaa vyenyewe mara nyingi vinakuwa vya bei kubwa, wale wataalamu ndiyo wakanunue zaidi ya laki tatu, nne, tano, mwananchi wa kawaida kijijini kuzipata kwa mara moja inaweza ikawa ni changamoto. Kwa hiyo, tunapofika kwenye usambazaji Waziri atusaidie wajenge uwezo wa taasisi zao ziweze kugharamia vifaa hivi halafu wananchi wakatwe kidogo kidogo wanapolipia bill hizi za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye Mkoa wa Mara. Mkoa huu una wilaya zake kama nne zinazungukwa na Ziwa Victoria; Wilaya za Bunda, Musoma, Rorya na kwa kiasi fulani Butiama. Hata hivyo, ukiondoa Musoma Manispaa wilaya nyingine zote zilizobaki zina changamoto kubwa ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Butiama pale kwa Baba wa Taifa, Ikulu pale hawana maji ya uhakika. Ni bahati mbaya wakati fulani viongozi wa Wizara walikwenda hadi wakafanya sherehe ya kusaini mikataba ya utekelezaji wa mradi wa maji ya Mgango, Kyabakari, Butiama na vijiji vile zaidi ya 19 vitakavyonufaika lakini haukutekelezwa wananchi walibaki kushangaa. Namshukuru Mungu mwaka huu kwa kasi ya aina yake wame-sign na mkandarasi na vifaa tumeanza kuviona site, kwenye hili tunawapongeza sana Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu sisi watu wa Butiama ni vizuri mradi huu utekelezwe kwa kasi ya aina yako Mheshimiwa Waziri. Mimi naomba baada au kabla Bunge halijaisha twende tuone ile kasi kama inalingana na mpango kazi wa utekelezaji wa mradi ule kwa sababu bado wananchi wana mashaka, je, itakuwa kweli? Sasa kweli tupite kule yale mambo unayofanya maeneo mengine Mheshimiwa ufike pale ukohoe ili watu tuwe na imani kwamba kweli mradi ule utatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunaomba mradi ule utekeleze kwa kasi kuna kata zinazoambaa na Mto Mara na Ziwa Victoria hasa pale Nyabange hawana maji ya uhakika. Ukienda Butiama hawana maji wakati wanaulinda Mto Mara. Mmesea vizuri kwenye hotuba yako Mheshimiwa Waziri kwamba kila mwaka tunaadhimisha Mto Mara na sherehe hizo hufanyika Butiama lakini vijiji hivi vinavyokulindia Bonde la Mto Mara havina maji. Hizi kata zote nne za Bwiregi, Namimange, Buswahili, Silolisimba, zinapakana na Mto Mara lakini hawana maji kabisa, haieleweki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunafarijika kama Taifa kwamba maji ya Ziwa Victoria sasa yanaelekea kuja Dodoma maana tayari yapo Igunga na Tabora Mjini wanasema pameshapata ni zaidi ya kilometa 500 lakini wale wanaopakana na Ziwa Victoria zero kilometa hawana maji. Hatuna roho mbaya, lakini haipendezi kwa watu wanaokulindia chanzo hiki kukosa maji kwa muda wote huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi mingine ikiwemo mikubwa hii ya kitaifa na hata ile ya visima, ni ushauri wetu taasisi zenye watu wengi kama shule tuhakikishe angalau tunapoweka miradi hii iwe karibu na hizi shule. Haipendezi shule ina watoto 1,000 au 2000 hawana chanzo cha maji kwenye maeneo ya shule na wakati huo tunaambiwa kuna magonjwa mengi yanayosababishwa na utumiaji wa maji yasiyofaa. Tuna shule nyingi za sekondari, shule za msingi wilaya ya Butiama na wilaya zingine lakini hazina maji. Ni ombi langu wakati tunatekeleza miradi hii ambayo tunashukuru Mkoa wa Mara na Wilaya ya Butiama imepata vijiji kadhaa tukumbuke kuliko na taasisi za elimu hizi ziweze kupata maji mfano vituo vya afya, zahanati na hospitali ziweze kupata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneo hayo, naomba niunge mkono hoja na niwatakie utekelezaji mwema wa bajeti hii. Ahsante sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia kwenye sekta hii ya afya ambayo ni muhimili wa amani na utulivu na maendeleo watu wenye afya watafanya vizuri kwenye shughuli za kilimo shughuli za elimu shughuli za ujasilliamali na nyinginezo. Na mimi kwa kuanza niungane na Wabunge wote waliopongeza juhudi za Serikali na Wizara ya Afya mahususi katika kuimarisha sekta hii ya afya kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, karibu kila Mbunge yeyote aliyeko hapa na asiyekuwepo anapotoka kuna athari ya jambo jema lililofanywa na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na sekta ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natoka Mkoa wa Mara, kule kuna Ushahidi wa jambo kubwa ambalo Awamu ya Tano na ya Sita watakumbukwa na wananchi wa mara hususani juu ya hiyo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa. Hospitali ile ina historia ndefu ujenzi wake kwanza waliweka jiwe la msingi mwaka 1975, ujenzi ukaendelea mpaka mwaka 1987 ukasimama lakini kwa maamuzi yenye tija ya mpendwa wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli mwenyezi mungu amweke roho yake mahala pema peponi 2018/2019 waliweza kufanya uhamuzi wa kutoa zaidi ya bilioni 15 kwa ajili ya kuhakikisha hospitali ile inakamilishwa. Na sote sasa tunaona hospitali ile inapendeza bahati nzuri imejengwa kwenye mwinuko wa Mlima Mkendo ina vutia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa, Serikali ikamilishe majengo machache yaliyobaki ili huduma muhimu za rufaa ngazi ya mkoa ziweze kuanza kutolewa kwa ukamilifu. Lakini hilo la muhimu kwa majengo yaliyokamilika ambayo yanaweza kuanza kutoa huduma za rufaa ngazi ya mkoa, ni vizuri tupate vifaa tiba majengo yale ukifika utakuta maeneo mengi yanayotakiwa kuwepo vifaa tiba hakuna vifaa tiba ndio maana hadi sasa huduma zinaendelea kutolewa kwenye hospitali iliyokuwa inatumika kimsingi ni hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni watumishi Wabunge wengi waliozungumza wameonyesha upungufu wa watumishi maeneo yote sasa na huku ambako tumejenga hospitali hizi mpya, ni vizuri kuwe na mkakati maalum kama wa ajira kwa ajili ya watumishi wa kada zote za sekta za afya zinazohitajika. Wakiwemo madaktari, madaktari bingwa, wauguzi wafamasia wataalam wa usingizi nakadhalikadhalika. Kwa hospitali hii ya rufaa ya Mkoa wa Mara ina upungufu mkubwa sana, niombe wizara kwa jambo jema mlilolifanya likamilishwe kutuletea wataalam wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ninalotaka kuzungumza kwenye sekta ya afya ni mafunzo ya watalaam wa afya hususani madaktari bingwa, uzoefu unaonyesha kuwa hospitali kubwa za mijini hasa majiji makubwa ya Dar es salaam, Arusha, Mbeya, Mwanza, Tanga nakadhalika, wanaomadaktari na madaktari bingwa wakutosha, kuliko mikoa inayoonekana ni ya pembezoni, kiasi kama mkoa wangu wa mara. Nakumbuka miaka michache iliyopita wizara ilifanya uhamuzi wa kufanya rationalization ya kuhamisha bahadhi ya madaktari bingwa kutoka jijini Dar es salaam, na kuhamishia mikoa ya kusini na mikoa yetu kama kule Simuyu nakadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilivyoonekana wataalam bingwa waliokwisha zoea Dar es Salaam si rahisi sana kukubali kwenda kufanya kazi kwenye mikoa hii ya pembezoni. Taarifa nilizonazo wengi wa madaktari wale waliamua ku-resign waliamua kuacha kazi na kurudi Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri sasa kwenye hilo tufanyaje, ninadhani wakati umefika sasa tuzisaidie hizi Hospitali za Rufaa za mikoa huko zilizo wawe na utaratibu wakuwaendeleza watumishi wao mabingwa, kama mtu ameshazoea kuwa Musoma kule ukienda ukampeleka ni rahisi kurudi lakini aliyezoewa Dar es Salaam ukwamwambia nenda Musoma anaona kama vile katupwa hivi na wengi wanasema nimetupwa Mara nimetupwa Mtwara, nimetupwa Katavi wakati kule kuna watanzania wanaohitaji huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwenye hili naomba niwapongeze of course Katibu Tawala wetu wa Mkoa wa Mara pamoja na medical officer incharge huyu Dr. Johakimu Eiyembe na RMO wake kwa uhamuzi wakutraini maafisa wataalam wao wanne. Lakini kwa uamuzi ule wa kutumia mapato yao ya ndani wizara ikaamua kuwasaidia kuwasomesha mmoja vitu vya aina hii vikiendelea vitatupunguzia mahitaji makubwa ya madaktari bingwa kwenye hizo hospitali za pembezoni. Kwa hiyo, hili niwasifu Wizara kwa kulifanya kwa ajili ya wataalam wetu kutoka kule Mkoa wa Mara, lakini liendelee kufanyika mara kwa mara ili kujenga uwezo wa hospitali hizi za pembezoni pia kupata wataalam wanahitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni makusanyo ya mapato ya ndani, ukipitia taarifa ya wizara ya utekelezaji utaona kwamba kwa sehemu kubwa, taasisi za Wizara hazikusanyi vya kutosha mapato yao ya ndani. Na nimeona zipo taasisi chache kwa idhini yako nizitaje zimefanya vizuri sana. Hospitali ya Mloganzira kwa mfano imekusanya zaidi ya asilimia 99 ya malengo yake lakini ipo Hospitali ya Benjamin Mkapa hii imevuka malengo kwa asilimia 118 ambako imekusanya zaidi ya shilingi bilioni 13, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imekusanya zaidi ya asilimia 74 sawa na bilioni 45, taasisi ya chakula na lishe asilimia 73 lakini taasisi nyingine zinazobaki zinasuasua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili pia lipo kwenye hospitali za Rufaa za Mkoa, pia kuna mapungufu ya ukusanyaji, ushauri wangu kwenye hili wizara iweke utaratibu wa watu kwenda kujifunza kwenye hizo hospitali zilizofanya vizuri ili uzoefu huu usaidie kuimarisha mapato ya ndani kwenye hospitali zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkona hoja nawatakia heri katika utekezaji wa majukumu yao. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa maandishi ni kama ifuatavyo:-

Kwanza, Serikali iongeze miradi ya umwagiliaji hasa kwenye Wilaya na Mikoa inayopakana na maziwa na mito ikiwemo Ziwa Victoria, Tanganyika, Nyasa, Manyara, Eyasi na Rukwa. Hii itasaidia kupunguza utegemezi wa mvua hasa kipindi hiki chenye changamoto ya mabadiliko ya tabianchi.

Pili, Serikali ifanye uamuzi wa makusudi wa kuajiri Maafisa Ugani wa kutosha kwenye Mikoa na Halmashauri ambazo kilimo cha mazao ndiyo shughuli yao kuu ya kiuchumi. Kwa kufanya hivyo, tutasaidia kuongeza kwa kasi tija katika kilimo cha mazao.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia kwenye sekta hii ya nishati. Nami niungane na wote waliompongeza Waziri, Naibu na timu yake kwa juhudi na kazi nzuri wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nitaomba kwa kweli niache yale ya kitaifa niende kwenye Jimbo la Butiama. Butiama ndiko alikozaliwa Baba wa Taifa na tunasema tunamuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kazi nzuri aliyowafanyia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sisi tunaishukuru Serikali hususan Serikali ya Awamu ya Tano na Sita kwa kujitahidi kuona kwamba vijiji vyote vinafikiwa na umeme. Ninavyo vijiji 59 na kwa kweli vyote kwa tafsiri ya access, kufikiwa vimefikiwa. Changamoto tuliyonayo ni huko kufikiwa walikokuona wananchi na wote wanatamani wapate umeme. Wakati fulani mtani wangu mmoja aliwahi kuongea hapa kadri tunavyopanua huduma ndivyo watu wanavyotamani na ni kweli kwamba kila mtu sasa anataka apate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, pale Butiama pamoja na kuwa na vijiji 59, vyenye vitongoji 370 ni vitongoji 147 vilivyofikiwa sawa na asilimia 40; vitongoji 223 havijafikiwa sawa na asilimia 60. Hata kwenye hivyo vijiji na vitongoji vyake unakuta wamegusa center tu. Kwa mfano, ninayo Kata moja maarufu ya Nyamimange, Tarafa ya Kiagata kuna vitongoji 10 lakini vitongoji vyenye umeme ni vitatu tu; Kiagata Madukani, Kewancha na Serengeti ndiyo vyenye umeme lakini vitongoji saba vifuatavyo Isangura, Kebwasi, Nyamihuru, Sania, Mtakuja, Masongo, Mamititu havina umeme na hali iko hivyo karibu kwenye vijiji vingine vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hali kama hii haiwaridhishi wananchi wanaona kama wameachwa lakini hali inakuwa mbaya zaidi pale taasisi za umma zinazohudumiwa wananchi wengi hazifikishiwi umeme kama hospitali, vituo vya afya, zahanati na shule. Ni vizuri tukatambua tunapokwenda kwenye REA III round II wajue kwamba bado wana kazi kubwa sana huko Butiama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru juzi tumepewa orodha ya majina ya wakandarasi watakaohudumia majimbo na wilaya zetu. Kwa Butiama sijui ni bahati mbaya au nini tumepewa mkandarasi anaitwa Giza Cable Industries. Sasa nimemtafuta tangu juzi simu yake inasema haipatikani jina lenyewe walilochagua wala halitii matumaini. Bora angeita Nuru au Mwanga yeye kaita Giza na hapatikani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, wananchi wengine wanalipia umeme lakini hawaunganishiwi, hili nalo ni tatizo mwenzangu amelisema asubuhi. Ninaye mwananchi hapa Mama Omari wa Kitongoji cha Kohoko kule Nyamikoma amelipia nguzo mbili Sh.551,147.32 tangu tarehe 10/04 lakini hawajasogeza nguzo wala hawajachimba mashimo na hakuna kinachoendelea wakiulizwa wanasema tatizo ni mita. Sasa kama tatizo ni mita walikuwa na sababu gani ya kumtaka mwananchi huyu alipie.

Mheshimiwa Spika, lipo hili tatizo la kukatikakatika umeme hili limesemwa na Wabunge wengi. Kule majimboni wameweka ma-group ya WhatsApp haya watu wanazungumza umeme unavyokatika mpaka wanatumia maneno yanayofedhehesha Shirika letu. Nakumbuka wakati fulani nikiwa pale Simiyu na hata Butiama naona yanaendelea mambo ya kukatika kwa umeme, wanasema umeme wa TANESCO unavyokatika utafikiri mwanamuziki Fally Ipupa.

Sasa nikajiuliza Fally Ipupa ni nani nilikuwa sijamjua, kwamba umeme unavyokatikakatika ni kama Fally Ipupa au wengine wana-comment yamekata umeme yaani badala ya wamekata wanasema yamekata umeme, yamerudisha, yamekata tena yaani namna umeme unavyokatika unakera wananchi mpaka wanasema utafiriki kuna mtoto anajifunza namna ya kuwasha na kuzima. Mheshimiwa Kalemani tunajua unafanya kazi kubwa sana lakini tuombe wataalamu walioko mikoani na kwenye wilaya pengine hawatusaidii vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona nimepigiwa kengele basi mimi nishukuru kwa nafasi hii, naunga mkono hoja nikiamini kwamba haya niliyoyasea yatafanyiwa kazi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nikupongeze, umeenea vizuri. Nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza mchana huu kwenye sekta ya maliasili. Naomba nianze kwa kuungana na waliozungumza asubuhi kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wataalamu wote wa sekta ya utalii kwa kazi nzuri wanazofanya kuinua na kuendeleza Sekta ya Utalii pamoja na changamoto mbalimbali zikiwepo Covid 19 zilizoikabili Taifa letu mwaka jana 2020 na sehemu ya mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze zaidi na ninaona hili analifanya sana Naibu Waziri la kuhamasisha utalii wa ndani. Tukiweza kwa kweli kuwafanya Watanzania wengi kufanya utalii kwenye hifadhi zetu, tutakuwa tumechangia kwa kiwango kikubwa sana uchumi wa nchi na vile vile tutakuwa tumewafanya wananchi wafaidi rasilimali zao. Haipaswi watu tulio na rasilimali nyingi namna hii tuendelee kuzitazama kupitia runinga, kwenye picha na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo nami niwashajiishe Wabunge wenzangu, kinachofanywa na TANAPA pale nje tukitekeleze. Wanatuomba tukashiriki Ngorongoro. Mimi nipo tayari, nadhani na Wabunge wengi watakuwa tayari kwenda Ngorongoro, kama njia ya kuimarisha utalii wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza kwa kuanzisha TFS kama taasisi ya kusimamia eneo la misitu. Yako maeneo ya kuzungumza kwa ajili ya kuboresha, lakini kwa ujumla taasisi hii inatimiza wajibu wake vizuri maeneo yaliyo mengi ukiacha changamoto za hapa na pale, hasa nguvu inapotumika kupita kiasi. Ushauri wangu kwenye maeneo haya hasa TFS na maeneo mengine, kuendelea kutoa elimu. Tusichoke kutoa elimu kwa wananchi wetu na Umma kwa ujumla ili kuimarisha uvunaji wa miti au misitu endelevu na kuendelea kupanda miti mingine ili kuhakikisha kwamba nchi yetu inabaki kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitegemea sera za mabavu hazitatufikisha mbali sana, utaendelea kutengeneza uhasama kati ya wananchi na Serikali yao. Jambo ambalo kwenye eneo hili linanipa shida kidogo ni pale ambapo mtu ameotesha miti yake mwenyewe, wala TFS hawakuja kumsaidia, akitaka kuvuna mti mmoja au miwili, anawekewa conditions nyingi bila sababu za msingi. Nilidhani hapa tungewatambua watu ambao wamejitokeza kuotesha misitu na wanapotaka kuvuna kwa kweli wasiandamane na masharti. Haya iwakute wale ambao wanakwenda kuvuna bila kuchangia kuotesha miti hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kuzungumza ni juu ya utalii kwa ujumla kitaifa na ninataka niangalie kanda zetu. Naipongeza nchi yetu kuwa na rasilimali za utalii karibu kila kona ya Tanzania; Kusini mpaka Kaskazini, Magharibi hadi Mashariki, kote kuna vivutio vya ama hifadhi au mapori tengefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani utakubaliana nami kwamba set up ya utalii wa nchi yetu, pamoja na kwamba maliasili zimetawanyika nchi nzima, ziko circuit zaidi towards the North, wakati vivutio vingine viko towards the west, towards the South, na East na kadhalika. Nataka niwaombe wakati ambako Kaskazini wamefanya vizuri sana, nataka niwapongeze kwa kweli, wapo wajasiriamali, wasafirishaji, watu wa kupokea watalii, hoteli nzuri, barabara nzuri na kadhalika; na hata customer care ipo vizuri, ni jambo jema sana. Ila najiuliza, hivi ilitokea kwa dharura tu hawa wakawa wazuri hivyo, kanda nyingine wakawa washamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake najiuliza, iweze kwa mfano umbali wa kufika Serengeti kutokea Mwanza haizidi kilometa 140, lakini kwa nini tumlazimishe mtu anayetaka kutembelea Serengeti ashuke KIA aanze kutembea kilometa zote hizo, kwenye risks zote za barabarani, mpaka aje kuifikia Serengeti, apite Ngorongoro, apite Manyara, is too much! Wakati bahati nzuri wenzetu wa Uchukuzi wamefanya kazi kubwa kuimarisha uwanja wa ndege wa Mwanza, sasa unaitwa Uwanja wa Kimataifa, sasa tunatamani kuona watalii wa Kimataifa wanaolenga kwenda Serengeti washuke Mwanza. Wakifika kule, watapata fursa ya kutembelea hiyo west circuit yote; wataona Rubondo, Saanane, Ibanda Kyerwa, Ibanda Rumanyika, Burigi Chato, Gombe, Fukwe za Ziwa Victoria and so forth and so forth. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili nawaomba Wizara, mje na mpango na mkakati madhubuti wa kufanya ukanda wa Magharibi nao pia uwe busy kwenye maeneo ya Kitalii kama ilivyo ukanda wa Kaskazini. Kinachoshangaza, unapita pale Serengeti Ndabaka Gate wala huoni pilikapilika za watalii wakiingia, lakini ukienda upande mwingine kwa kweli shughuli zipo nyingi za kutosha. Kwa hiyo, ni ushauri wangu kwamba hilo tuliangalie kama kweli tunataka kuimarisha maeneo yote ya nchi yetu yanufaike na hizi rasilimali tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuzungumzia ushirikiano wa Wizara zinazogusa utalii kwa njia moja au nyingine. Nilikuwa naziangalia hapa karibu Wizara nyingi tu, karibu zote, labda nusu; Wizara ya Maliasili yenyewe, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Wizara ya Nishati, Wizara ya Mawasiliano, mention Wizara zote; Wizara inayoratibu watu wa dini, kuna makongamano ya Kitaifa na ya Kimataifa ya Dini, tukiweza hawa wote kuwahamasisha wakaja kwenye dini zao, lakini wakaenda kwenye utalii, tutakuwa tumechangia kupata rasilimali nyingi za fedha za kigeni. Tuna taasisi nyingine hata za ndani, Scouts wanaweza wakahamishiwa wakaenda huko kufanya mikutano yao, lakini wakaenda kwenye utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza ya Kitaifa naomba niguse Butiama. Hapa nina jambo moja, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize. Pale Butiama kuna hifadhi inaitwa Hifadhi ya Taifa ya Msitu wa Kyanyari, lakini kwa kweli ukiangalia vile vilima vya Kyanyari hakuna msitu, ni mlima tu umenyanyuka wenyewe hivi labda na majani mafupi, hakuna mti hata mmoja, lakini mmeita hifadhi na ika-cost watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamekuwa pale tangu mwaka 1974, mmeenda kuweka beacons mwaka 2013 na mkaondoa kaya 220 kwenye hekta zao walizokuwa wanazimiliki na kufanya shughuli za kiuchumi 1,500. Sisi tunasema, lingefanyika sawa, lakini liwe shirikishi. Wananchi hawakushirikishwa, vijana wanakuja TFS kutoka Musoma, wakabandika ile, wakaondoka. Linalowakera wananchi wa pale, wakati mnasema hii ni hifadhi, ameibuka huko mwekezaji wa madini, amepewa vibali vya kuwa na vitalu kumi kwenye eneo lile lile. Sasa tunajiuliza hapa, kama unawaondoa hawa kwa ajili ya hifidhi, iweje leo ukaribishe mwingine aendelee na shughuli za uchimbaji na utafutaji wa madini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho naomba niseme moja hili la utalii Butiama. Butiama ni kwa Baba wa Taifa. Watu wanakwenda pale mara nyingi, lakini naona wanaishia kufanya ibada kwenye kaburi la Baba wa Taifa na kuondoka au kupita kwenye ile makumbusho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Butiama ni eneo ambalo lina vitu ambavyo wangeweza kujifunza vya kitamaduni. Mfano, tuna makabila yasiyopungua 10; kuna Wairegi, Wakenye, Wakirobha, Wakabwa, Wazanaki, Waluo, Wajita, Waruri, Wakwaya, Wasimbiti, Wasukuma na kadhalika. Haya makabila, ni faida, kuna tamaduni pale. Vyakula vyao ni tofauti; kwa hiyo, nilidhani mje mtusaidie...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Haya, ahsante.

MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia mchana huu, juu ya hii bajeti ya Serikali. Nami niungane na wasemaji waliokwisha tangulia kuanza kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuweka dira iliyotafsiriwa vizuri sana na Waziri wa Fedha na Mipango, siyo kutafsiri tu na hata kuiwasilisha kwa ufundi kweli kweli. Mheshimiwa Mwigulu Nchemba umejieleza vizuri na tumekuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nimpongeze Waziri na timu yake akiwemo Naibu Waziri Mheshimiwa Masauni, Katibu Mkuu Tutuba, Naibu Makatibu wote watatu, Ndugu Amina Shaaban, Ndugu Adolf Ndunguru na Dkt. Khatibu Kazungu na Makamishna wote wa Wizara ya Fedha. Kwa kweli mimi naomba Waheshimiwa Wabunge wote tuiunge mkono bajeti hii kwa sababu ninaiona ni bajeti iliyoandaliwa kwa usikivu wa kiwango cha juu sana. Naomba kwa muda niliopangiwa nirejee maeneo machache, yanayoonesha kwamba tunastahili kuiunga mkono bajeti hii kwa asilimi 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza usikivu wa hii tozo ya shilingi mia kwa lita ya diesel au petrol ili kuhudumia barabara zilizo chini ya TARURA. Wabunge wote tumeonge kuhusu hali mbaya ya barabara zetu na kwa uamuzi huu, kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri mwenyewe, tutapata zaidi ya shilingi bilioni 322. Fedha hizi zikiongezwa kwenye fedha iliopo ya sasa kwa mchanganuo wa asilimia 30 kwa 40 zinazokwenda TARURA, ambazo ni bilioni 272.5 kutakuwa na jumla ya shilingi bilioni 594.7 kwa ajili ya kuhudumia barabara za Halmashauri na za jamii. Haya ni mapinduzi makubwa kufanywa, mwaka wa kwanza wakati Serikali ya Awamu ya Sita inaingia madarakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini fedha hizi zikitumika vizuri, zitasaidia sana kupunguza mfumko wa bei kwa sababu wataalamu wa uchumi wanatuambia mfumko wa bei unasababiswa na kupanda kwa gharama za chakula, imekuwa ni ada chakula Mpanda kule kiko chini sana maeneo mengine kipo juu kwa sababu hatuwezi kufika kutokana na miundombinu ni mibovu. Kwa hali hii bei ya chakula kitaifa kila mtu ataweza kuimudu na itakuwa ya chini vilevile hata maisha ya jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge aliongea kwa uchungu hapa hali ya barabara ilivyo mbaya, wagonjwa kufia njiani, madaraja yaliyokatika hayawezi kuhudumiwa, lakini kwa fedha hii nina imani hali inaweza ikawa nzuri kwenye barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu ambalo naomba nikumbushe hapa, ni iwapo fedha hizi zitatumbukizwa kwenye mfuko wa barabara zigawanywe na Road Funds Board, au kutakuwa na sheria maalum iliyotengwa kwa ajili ya hizi fedha. Kwa sababu kama zitaingia mfuko wa barabara basi kuna umuhimu wa ile sheria ya mfuko wa barabara irekebishwe kuondoa ile uiano wa asilimia 30 to 70, na kama itakuwa na sheria yake mahsusi, zikaenda TARURA bila ya vikwazo itakuwa vizuri. Kwa hiyo naomba hilo Mheshimiwa Waziri alifikirie lisije likaturudisha kwamba sheria haijabadilishwa tutaenda kwa mgao ule wa 30 kwa 70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ambalo naliona ni mapinduzi makubwa, Waheshimiwa Wabunge wote tumelizingumza ni malipo kwa Madiwani, maeneo mengi ilikuwa ni changamoto, mbaya kabisa ilikuwa inafedhehesha. Madiwani ndiyo watunga sera kwenye vyombo vyetu vya Serikali za Mitaa, ndiyo wafanya maamuzi, ndiyo waajiri, lakini kwa kweli Halmashauri nyingi zipo chini kimapato walikuwa wanafedheheka sana na waligeuka kuwa wanyonge, wengine Mkurugenzi anaweza kuamua akasema sina hela hawalipi kwa hiyo anaweza kuwakopa ili waendelee kuwa wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uamuzi wa Serikali wa kuwalipa moja kwa moja hili nalo linamapinduzi sana, Madiwani wetu watakuwa na uwezo sasa hivi wa kusimamia Halmashauri zetu bila ya kushawishiwa kwa kupewa fedha. Jambo ambalo naishauri TAMISEMI yale malipo mengine ya vikao, tumeondoa kwenye posho zao za kila mwezi Serikali kuu inatoa, sasa tena tusisikie na siyo jambo jema kusikia Wakurugenzi hawawalipi hata posho zao zile za vikao, hili ni la TAMISEMI najuwa Waziri yuko makini na wasaidizi wake litatatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze kwa uamuzi wa kuwapa hawa Maofisa wa ngazi za Tarafa, na Kata posho ya kuwawezesha kusafiri kwenda kuhudumia wananchi, nilitaka niseme kitu lakini sasa ndiyo kimetoka hicho cha shilingi laki moja. Kule kwenye ngazi ya jamii ukienda kwenye Kata kuna Maafisa Elimu Kata, zamani tukiwaita waratibu wa elimu Kata, wao wanapata posho ya shilingi laki mbili kwa mwezi, na wanapewa vyombo vya usafiri pikipiki ili waweze kuzitembelea Kata zao. Sasa Afisa mwenye Tarafa nzima anapewa shilingi laki moja, lakini siyo jambo baya maana ndiyo tumeanza, tuone umuhimu wa kuiboresha kwa miaka ijayo ili kuwawezesha hawa watu kufanya majukumu yao vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni suala la ulipaji wa kodi ya majengo kupitia umeme. Ninajua yapo maamuzi ya kisera yalishafanywa na Serikali zetu ziliyopita na hii ya sasa, kwamba kuna watu walishasamehewa hata kulipa kodi za majengo wakiwemo watu wazima, wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa utaratibu huu unless Wizara ije na utaratibu, sheria au kanuni zake zikae vizuri. Je, watu wenye umri mkuwa ni namna gani watakaokuwa exempted, vinginevyo kwa vile wana nyumba za kutumia umeme ikiwa generalized ina maana hata hawa ambao tuliowasamehe, watalazimika kulipia kodi za majengo kupitia umeme. Kwa hiyo hili nalo tumuombe Waziri kwenye sheria au kanuni ile aliweke vizuri sana, kwa sababu wananchi wameshtuka wanadhani watabanwa kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ambalo nataka kulisema kama ushauri kwa Serikali, ili uchumi ukue kwa kiwango tunachotaka Serikali ikubali kuajiri watumishi hasa wa kada muhimu. Muda wangu mwingi nimefanya kwenye utumishi nimeufanyia kwenye sekta za Serikali za Mitaa. Ninafahamu kuna kada muhimu sana kule ambazo zinaupungufu mkubwa wa watumishi. Moja ni Internal Auditors, maeneo mengi Internal Auditors hawapo na hawa ndiyo wanafanya ile preliminary audit kabla CAG hajaingia. Hasa kama hawa hawapo na ndiyo wadhibiti wa mwanzo itakuwa ni changamoto, kwenye Local Government hakuna Wahandisi, Quantity Surveyors hawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilidhani Serikali ifanye kazi ya kuchambua zile kada muhimu ambazo zikiwepo zitasaidia kusimamia uchumi tunaotaka ukue, pia tutaimarisha utoaji wa huduma bora kwenye mamlaka zetu. Kwa maoni yangu nilidhani kada hizi tatu nilizozitaja tungezipa kipaumbele cha ajira ili waweze kusaidia kusukuma mbele Serikali zetu za Mitaa na Serikali Kuu kwa wale ambao hawana ajira hizi, vinginevyo naunga mkono hoja hii na tumuunge mkono Mheshimiwa Waziri akafanye kazi yake kwa mwaka ujao. Ahsanteni sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja ya Itifaki iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri wangu Engineer Masauni mchana huu, lakini nianze pia kwa kuwashukuru katika vitu ambavyo vimetupa unafuu sana leo tunapojadili Itifaki hii karibu wasemaji wote wamekuwa-positive wameunga mkono hoja nasi kwa kweli tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi tunaridhika na yote yaliyotolewa kwa maana ya kuunga mkono hoja yetu, zaidi na ushauri mbalimbali uliotolewa. Kuna maangalizo kadhaa yametolewa ningetamani kugusia machache kadri ya muda ulionipangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wengi wamerejea manufaa, ambapo wazungumzaji karibu wote wamerejea manufaa kama yalivyoainishwa na mtoa hoja kwenye ukurasa wa 10, ukurasa wa Nane aya ya 10 ambapo amechambua hoja karibu 11 zinazosema manufaa ya kuunga mkono ama kuridhia Itifaki hii. Kwa hivyo, tunashukuru nimeona Mwenyekiti wa Kamati pia amerejea manufaa haya, kwa hiyo manufaa kwa kweli ni makubwa kwa sababu, tayari kama nchi tunayo Sheria ya Kuzuia Ugaidi lakini tulikuwa tumesimama nchi kama nchi, lakini kama wasemaji wengi walivyozungumza masuala ya ugaidi huvuka nchi moja kwenda nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania watakuwa wanakumbuka na Waheshimiwa Wabunge mtakuwa mnakumbuka kwamba, hivi karibuni kumekuwa na matukio yametokea karibu na mpaka wetu na nchi ya jirani kule Mozambique. Kwa hiyo, utaona uhalifu unafanyika Tanzania wanakimbilia kule, kwa sababu bila ushirikiano wahalifu wanaokimbia nchi jirani utawafanyaje? Kwa hiyo, ni lazima kuwa na Itifaki ya namna hii inasaidia fursa kama hizo za ushirikiano baina yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Wabunge wametukumbusha na mimi nalipokea, lakini tuwape tu assurance ni kwamba nchi yetu ipo makini, hatuwezi kwa sababu nchi moja au mtu mmoja kasema huyu hana sifa hizi mumuondoe Tanzania na sisi tukafuata na ndiyo maana kwa kulizingatia hilo tumechukua muda kujiridhisha na hadi tunapoleta Itifaki hii Bungeni tumejiridhisha kwamba tunachokwenda kufanya ni cha uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka Waheshimiwa Wabunge miaka kadhaa iliyopita ziko nchi zilikumbana na changamoto za vikundi na kutaka ku- blacklist vikiwemo zile zinavyotoa huduma kwenye nchi yetu, lakini Serikali ya Tanzania haikukurupuka kufunga huduma zile tu kwa sababu nchi Fulani ilisema shule fulani, zahanati fulani kwa sababu ipo hivi ifungwe! Ni kwa sababu tulifanya uchunguzi wa kujiridhisha hakuna dalili zozote za kuonesha vitendo vya ugaidi kwenye eneo hili, kwa hilo nalo litaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo nchi zilikumbana na changamoto za vikundi na kutaka ku-blacklist vikiwemo vile vinavyotoa huduma kwenye nchi yetu, lakini Serikali ya Tanzania haikukurupuka kufunga huduma zile kwa sababu tu nchi fulani ilisema shule fulani, zahanati fulani kwa sababu iko hivi ifungwe. Ni kwa sababu tulifanya uchunguzi tukajiridhisha hakuna dalili zozote za kuonesha vitendo vya ugaidi kwenye eneo hili. Kwa hiyo hilo nalo litaendelea na polisi wetu watajiepusha, kwa sababu hata Waziri alivyokuwa anaisoma alisema tutazingatia matakwa ya katiba, kuzingatia haki za binadamu ikiwemo kuepuka kubambikia watu wasiohusiana na makosa hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hiyo inatukumbusha, mara kadhaa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan, amevikumbusha vyombo vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kutokubambikia watu kesi. Kwa hiyo hayo yanakwenda hadi hayo yatakayozungumzia masuala ya ugaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia naomba na mimi niunge mkono hoja hii, kwamba Bunge kwa pamoja turidhie Itifaki hii ili tuweze kuungana na nchi nyingine 21 ambazo zimeweza kuridhia kwenye nchi zao ili tunufaike na uwepo wa Itifaki hii pamoja na wanachama wenzetu wa OAU.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu asubuhi hii.

Kwanza niungane na Waheshimiwa Wabunge wote ambao tumeona walio wengi kwa kweli wamechangia very positively kuhusu kazi nzuri ya ulinzi wa Taifa letu unaofanya na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na kwa kweli, hii kama alivyomaliza mzungumzaji wa mwisho, ni kazi nzuri na miongozo mizuri inayofanywa na Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Waziri wangu wa Ulinzi Dkt. Tax, lakini Katibu Mkuu, Wakurugenzi, Wakuu wa Majeshi na wasaidizi wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingi zimezungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge, katika kuchangia naomba na mimi niseme machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, moja kuhusu umuhimu wa barabara za mpakani; hili kweli Serikali inajua umuhimu wake. Wizara ya Ulinzi na JKT itawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa madhumuni ya kuimarisha barabara hizi za mpakani. Hoja imezungumzwa ya kuweka lami, lakini nadhani jambo la msingi hizi barabara zote zianze kupitika halafu ziimarishwe kuwa barabara za lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja iliyoibuliwa na Mheshimiwa Ng’enda, tunashukuru moja umeisema, lakini nilitaka nichangie hii ya doria katika Ziwa Tanganyika, lakini pia tuseme na maziwa mengine hata na bahari yetu.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili jeshi letu liko imara, lakini litaimarisha ushirikiano na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ikiwemo polisi na vyombo vingine, ili kuimarisha doria kwenye maeneo hayo. Tusingependa kuona wananchi wetu wanadhalilishwa na wahalifu au kama alivyowaita majambazi au maharamia kutoka nchi za jirani, lakini pia nikiri wapo hata miongoni mwa wananchi wa Tanzania wanaofanya vitendo hivi vya uhalifu, wote hawa wanahitajika kudhibitiwa.

Mheshimiwa Spika, hili la nyimbo za kizalendo majeshini; tunaimarisha hilo sana. Zinaimbwa nyingi ila nyingine akiziona ni za hamasa tu. Na tunashukuru umetusaidia kwamba kuna mazingira fulani fulani ili waweze kufanya mazoezi hayo kwa ufanisi wanahitaji nyimbo zinazogusa hisia kama hizo ambazo Mheshimiwa Ng’enda alitaka kama vile kuzinyanyapaa.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni hili la ajira; naomba nichangie kwenye hili la ajira; imeelezwa hapa, lakini nataka niseme kwa kweli, ajira si kwamba iko restricted kwa Jeshi la Wananchi tu, wale wanaopitia JKT. Hiki ni kigezo muhimu kwa sababu, tunazungumzia uzalendo, utayari, uchapakazi na JKT ndio hutoa mafunzo ya namna hiyo. Kwa hiyo, sio Jeshi la Wananchi tu wanaolazimisha waajiriwa wao wapite huko, bali hata Polisi mmeona tumesema juzi hapa, Magereza pia, Uhamiaji, wote wanakuwa wamepitia huko, lakini hata taasisi za kiraia pia wanapitia huko.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo sasa naomba niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia hizi hoja za Kamati tatu zilizoko mbele yetu. Nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa kuiwezesha vizuri sana sekta yetu inayosimamia usalama wa raia. Ni matarajio yetu kwamba kwa uimarishaji huu basi vyombo vyetu pia vitimize wajibu wao kwa kuzingatia matarajio ya Watanzania kama yalivyoelezwa na Waheshimiwa Wabunge wengi waliochangia hoja hizi. Nikushukuru wewe binafsi kwa namna unavyoongoza mjadala huu na uvyotu-guide vizuri ili tuweze kuwawakilisha vizuri wananchi waliotuleta hapa. Mwisho nizishukuru Kamati zote tatu kwa michango mizuri zilizotoa kwenye sekta tunayoisimamia, na zaidi Wabunge waliochangia kwa kiango kikubwa kwenye maeneo ya uhamiaji na eneo la Polisi, hasa eneo la tozo lililotolewa azimio na Kamati yetu ya PAC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu haya yaliyojitokeza Uhamiaji, hizo concerns za Kamati, za CAG na za Wabunge ni very valid, ni za msingi kabisa. Hakuna mtu ambaye anatarajia chombo kilichoaminiwa kije kifanye mambo ambayo yanakiuka kabisa maadili. Na kwa kweli hata Mheshimiwa Rais mwenyewe wakati akifunga mafunzo ya askari wetu wanaoingia Immigration alisema bayana kwamba yapo mambo ambayo lazima Wizara na Immigration tuyafanyie kazi, hasa yale yanayohusika na ubadhirifu kwenye sekta hiyo ya visa na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi kama Wizara tunaungana na wote kusisitiza haja ya uadilifu, uaminifu, uzingatiaji wa sheria, uepukaji wa wizi na ubadhirifu kwenye maeneo yote yaliyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, Wizara (Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Idara ya Uhamiaji) tunazingatia ipasavyo maelekezo ambayo mara kwa mara yamekuwa yakitolewa na CAG wakati wa ukaguzi na Kamati zetu hizi ambazo zinatusimamia. Mimi niwahakikishie kwamba wakati wote Wizara itashirikiana na CAG na Kamati za Bunge na Wabunge kuchukua hatua stahiki pale ambapo haja ya kufanya hivyo ipo.

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya maelezo haya, naomba nigusie maeneo yaliyojitokeza kwa hisia kali miongoni mwa wasemaji na kwenye Ripoti ya Kamati. Nikumbushe tu kwamba hii ni Ripoti ya 2020/2021, kwa hiyo tunayoyaongea hapa sisi kwenye sekta huku kuna hatua zimeshachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, moja ambalo nimeliona likijitokeza hasa kwenye michango ya Wabunge, inakuwa kama vile pengine kuna kutilia shaka uwezo wa Wizara na pengine taasisi yetu ya Immigration kuchukua hatua. Niwaondoe shaka Waheshimiwa Wabunge, wote tuko pamoja.

Mheshimiwa Spika, jambo moja juu ya hii habari ya visa zilizotakatishwa hizi. Baada ya uchunguzi ule Serikali ilichukua hatua, kwa sababu kulikuwa kunaonekana kuna jinai, DCI alilichunguza jambo lile kwa undani sana. Lakini uchunguzi ule haukumuwezesha kuwa na ushahidi ambao ukipelekwa mahakamani wale watuhumiwa wangeweza kutiwa hatiani.

Mheshimiwa Spika, kama alivyoshauri CAG kwenye ripoti yake, DCI pia alishauri kwamba mamlaka husika za kinidhamu zichukue hatua. Naomba nilitaarifu Bunge lako kwamba Immigration imechukua hatua dhidi ya watumishi wote 32 waliotuhumiwa kuhusika na matendo yale na hatua za kinidhamu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa, wale waliokuwa na uongozi wametolewa na wengine tumewapa siyo chini ya miaka miwili hawawezi kufikiriwa kwa uongozi wowote ule. Tumewaweka kwenye matazamio wasifanye matendo kama hayo. Hata hivyo, Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu ili yeyote atakayejitokeza kufanya mambo hayo yenye mwelekeo wa kijinai wanapelekwa mahakamani.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la tuzo na tozo, tumesikiliza maoni ya Wajumbe na maoni ya Kamati. Ushauri wote uliotolewa tunaukubali na maazimio yale hatuna shida nayo kabisa. Isipokuwa nina mambo machache ambayo nadhani tuyatolee ufafanuzi ambayo baadhi ya Wabunge walisema kama vile sasa ule mfuko hauna usimamizi kabisa. Nilimuona Mheshimiwa Sangu akiongea kwa uchungu sana juu ya jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, niwaeleze kwa kifupi. Mfuko huu upo kwa mujibu wa Kifungu cha 66 cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi Nchini, Sura ya 322. Sheria ile imebainisha vyanzo vya mapato, lakini hata kwenye PGO Na. 135 aya ya pili na PGO 135 aya ya 2(b) yameainishwa mule maeneo gani yanaweza yakawa vyanzo vya mapato na mamlaka ya matumizi.

Mheshimiwa Spika, na vyanzo vya mapato kama vinavyofahamika kwa mujibu wa sheria ni adhabu za makato ya mishahara kwa watumishi wanaofanya makosa ya kinidhamu, asilimia 50 ya mauzo ya mali za kuokotwa zinazokuwa polisi, makusanyo kutoka benki, taasisi, viwanda na migodi inayopata huduma za ulinzi toka Jeshi la Polisi. Na kwa sasa tuna jumla ya vyanzo 55.

Mheshimiwa Spika, akaunti hii iko BOT, maana yake Benki Kuu, na utaratibu wa matumizi umeainishwa vizuri sana. IGP kabla ya kuanza kutumia, huandaa mpango unaouwasilisha kwa Katibu Mkuu wa Wizara, naye ana- share na Waziri. Tukishajiridhisha ngazi ya Wizara, ndiyo anapelekewa Paymaster General kwa ajili ya kuruhusu fedha zitoke zikagharamie mpango ule ambao uliridhiwa kabla. Haamki tu akapanga hizi ziende zikatumike huku. Fedha hizi zinapofika kwa matumizi, huhamishiwa kwenye akaunti ya Miscellaneous Deposit Account iliyoko chini ya Wizara ya Fedha, akaunti ambayo huwa inakaguliwa.

Mheshimiwa Spika, tunakiri kwamba kutokuwepo kwa kanuni ni udhaifu ambao tumeanza kuufanyia kazi kama Wizara na kabla ya audit ijayo tutakuwa tayari tunazo kanuni za kusimamia mfuko huu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naona muda wangu umeisha, lakini nimalizie tu kwa kusema, kulikuwa na hoja ya kutumia fedha hizi kama msingi wa kujenga kwa haraka vituo na nyumba za wafanyakazi. Hilo tumeanza kulifanyia kazi kwa kuwasiliana na Banks ili tuweze kupata fedha nyingi zaidi halafu mfuko ule utumike kurejesha.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, nashukuru kwa hayo, lakini tuko pamoja na haya yaliyoshauriwa nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kiafya kuwepo hapa mchana huu kujadili wasilisho la Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Pia nimshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na wasaidizi wake Makamu wa Rais, Waziri Mkuu kwa imani yao na hata wakaona nastahili kuteuliwa kuwa Naibu Waziri, kusaidia kwenye Wizara hii. Ahadi yangu ni kwamba nitamsaidia ipasavyo Waziri wangu kutekeleza majukumu kwa bidii uaminifu na uadilifu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, shukrani kwa wananchi wa Butiama na Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Butiama kwa imani yao kwangu na leo ipo Kamati ya Siasa hapa, nawaahidi tu sitawaangusha. Maendeleo ya Butiama yanabaki kuwa kipaumbele changu cha juu katika utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Spika, naungana na Wabunge wote waliozungumza, kwa kutambua mchango wa kazi nzuri inayofanywa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tunawashukuru sana na tutaendelea kuthamini mchango na mawazo yao ili kuboresha zaidi utendaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umetolewa ushauri na Kamati na wasemaji mbalimbali walipata nafasi ya kuzungumza. Kwa uchache wa muda sitawataja, lakini itoshe tu kwamba majibu yetu bila shaka tutayaandaa kwa maandishi na kuwatambua wote waliochangia. Kamati imezungumza na nitajikita kwenye maeneo mawili ya NIDA pamoja na Uhamiaji. Imetajwa kwamba Wizara na Serikali ifanye juhudi za kupata shilingi bilioni 5.3 ambazo hazijatolewa ili NIDA itekeleze majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, naomba nikueleze pamoja na Bunge lako Tukufu kwamba, baada ya ushauri huo katika robo ya tatu zaidi ya Sh.2,382,000,000 zimetolewa na kupelekwa NIDA ili kutekeleza majukumu yao na Wizara imewasilisha maombi Hazina ili Sh.2,712,000,000 zilizobaki pia ziweze kutolewa katika robo ya nne kuwezesha NIDA kutekeleza mpango wao wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuwafikia wananchi wenye vigezo vya kutambuliwa na kusajiliwa ili wapewe vitambulisho vya Taifa, hili linaendelea kufanyika. Tunafahamu NIDA imeanza kwenye Wilaya zote 139 za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Wilaya za Zanzibar. Hata hivyo juhudi za kuboresha zile ofisi zinaendelea na kama tulivyosema katika bajeti ya mwaka ujao, uboreshaji wa bajeti umekuwa mkubwa kabisa, zaidi ya Shilingi Bilioni 56.4 zimetengwa kwa ajili ya shughuli za NIDA na humo ndani kuna zaidi ya Sh.42,000,000,000 zinazokusudiwa kwenye vitambulisho vya uraia, matarajio yetu ni kwamba fedha hizi zitatoka hasa baada ya changamoto ya kimkataba iliyokuwepo kati ya NIDA pamoja na Mzabuni shughuli hizo sasa zinaweza zikaendelea kutekelezwa ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo vipo vitambulisho zaidi ya 750,000 na Waziri amesema hapa asubuhi kuwahimiza wananchi ambao hawajachukua vitambulisho hivyo wakavichukue, ni matarajio yetu kwamba vitambulisho hivi vinatolewa kwa sababu vinahitajika hakuna sababu yoyote vitambulisho kubaki kwenye ofisi zetu za Wilaya.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wahamiaji haramu imezungumzwa hapa kwa uchungu sana na sisi linatugusa, lakini wakati mwingine nchi inabanwa na Sheria za Kimataifa na mikataba ambayo nchi imeingia duniani huko, kwamba ukishamkamata huwezi ukawezesha kama Mheshimiwa Muharami ameshauri pale. Hata hivyo, tunatafakari hayo, kama nchi nyingine zinawasafirisha, zinawapitisha, kwa nini sisi ndio tuchukue mzigo wa kuwachukua na kuwahifadhi kwenye majela yetu, tuwalishe halafu kuondoka bado tuwagharamie.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, sasa hivi hawa wafungwa wa Kiethiopia zaidi ya 4,025 waliopo kwa usafiri wa anga ndio unasema kwenye hii mikataba wanastahili kulipiwa nauli shilingi Bilioni 6.35 na tukiwapeleka kwa barabara si chini ya Shilingi Bilioni 3.2 sasa zote hizi zingeweza kufanya mambo mengine kwa ajili ya Watanzania. Hata hivyo tunaendelea kuwasiliana na Serikali ya Ethiopia ili waje wachukue raia wao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu vitendea kazi kwenye Uhamiaji tunaendelea kuboresha mambo haya, mwaka huu pekee magari sita yamenunuliwa na mwaka ujao tumepanga kununua magari 30 na ujenzi wa makazi na Ofisi za Uhamiaji ngazi wa Wilaya na Mikoa kama tulivyosema kwenye bajeti yetu vitaendelea.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)
Hoja ya Kuazimia Kuwahamisha Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kwanza niseme kwamba nimetumika kwenye sekta ya TAMISEMI miaka 12 nimetumika Serikali Kuu miaka 18 na kote tuliona changamoto. Wakati niko miaka 18 kwenye Wizara ya Elimu tulibaini kwamba elimu inaweza ikasimamiwa kwa ufanisi kama kila kitu kitafanyika makao makuu lakini ilikuja kuthibitika vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadae tulifanya utafiti mdogo wakati ule Wizara ya Utumishi. Tulikuta mwalimu ameacha kazi miezi sita au zaidi Wizara haina habari inamlipa mshahara kwa sababu usimamizi wake ulikuwa unafanywa na Katibu Mkuu wa Wizara wakati ule Dar es Salaam kwa shule zilizotapakaa nchi nzima lakini achia mbali utoro na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, haya maamuzi ya D by D nadhani Tanzania hayajaeleweka vizuri. Kama itakupendeza najitolea kuwa mwalimu katika kipindi kimoja tujielimishe D by D kule kulikofanikiwa walinya nini. Kwetu hapa tutazilaumu sana halmashauri lakini ule uwezeshaji haujafanyika ipasavyo. Nitoe elimu kidogo kwenye nchi zilizofanya vizuri sana kwenye ugatuaji wa madaraka kuna principle moja wanayoi-apply inasema “The principle of subsidiarity” maana yake pale ambapo shughuli zinafanyika…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa inatokea wapi?

MJUMBE FULANI: Kwa Sophia.

SPIKA: Mheshimiwa Jumanne Sagini kuna taarifa kutoka kwa Sophia Hebron Mwakagenda.

TAARIFA

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwanza amesema kwamba amefanya kazi miaka 12 ya uzoefu na 18 ya uzoefu. Bado ni Waziri wa Serikali hii, kwa nini hajafanya hili suala? Kwa sababu mtoa hoja baada ya kuleta hiyo hoja yake ni baada ya mambo kutokwenda sawa. Kwa hiyo, nampa taarifa ni vema wakatengeneza kutumia uzoefu alionao na vitu ambavyo amevifanya ni labda itasaidia Taifa hili, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Jumanne Sagini unaipokea taarifa hiyo?

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa sababu tu hana ufahamu na nilichofanya, nimefanya mengi sana kwenye sekta hii. Hata ukatibu mkuu pale miaka saba, minne ya unaibu na mitatu ya Ukatibu Mkuu nilifanya haya. Sasa nasema hivi principle ile inasema hivi, unaposimamia jambo ambalo linafanyika pale ulipo, ufanisi wake unakuwa mkubwa zaidi kuliko ukisimamiwa kutoka mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa tabia ya ubinadamu naomba niseme kwa Kingereza kwa sababu nimeitoa huko normally people do what you inspect not what you expect. Ukiwa makao makuu ya Wizara ukamsimamia mwananchi aliye kwenye kijiji ufanisi wake uko ndugu wapi ndugu zangu. (Makofi)

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kilichokosekana kwenye mfumo wetu wa ugatuaji…

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …kilichopungua kwenye mfumo wetu wa ugatuaji ni nafasi…

SPIKA: Mheshimiwa Sagini kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kunti.

TAARIFA

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, leo maafisa ushirika na maafisa ugani wako TAMISEMI na wako hapo kwenye miguu na ndiyo wanafanya vibaya kuliko kitu kingine chochote.

SPIKA: Mheshimiwa Sagini unaipokea taarifa hiyo?

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naipokea anakosa Subira tu, nilikuwa nataka nimwambie ni kwa nini tunaona huo udhaifu. Moja, baada ya uamuzi huu wa kupeleka madaraka karibu na wananchi, wizara za sekta na watendaji kwenye local government walipaswa wafanye realignment moja kwenye attitude na perception kwa sababu wizara hizi zilizoea kutekeleza. Leo ukiwaambia washiriki kwenye sera wafanye M and E, mentoring and evaluation wafanye capacity development ya watu kule hayo hayafanyiki. Peleka resources, peleka vifaa… (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, kengele imeshagongwa Mheshimiwa Sagini ahsante sana. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuzungumza kwa ufupi kuhusu Muswada wa Sheria ya Fedha na mapendekezo yaliyoletwa na Serikali ili kuridhiwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, niishukuru Serikali na hapa nadhani Wabunge tukubaliane kwamba katika Muswada huu kwa sehemu kubwa sana Serikali wamekuwa wasikivu. Ukiangalia kwa makini mambo mengi ambayo yamelalamikiwa sana katika Bunge lililopita na hata mwanzo mwa Bunge hili, yamefanyiwa kazi kubwa sana kwenye hotuba ya bajeti na yanaonekana kuwa reflected vizuri sana kwenye mapendekezo haya ya Muswada wa Sheria ya Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo mengine pengine ni sintofahamu ya baadhi tu ya watu, hata niliona mijadala mingine jana na pengine juzi, ni sintofahamu inayotokana na uelewa tu ambao nadhani ukifafanuliwa vizuri tunaweza tukakubaliana kwamba hatua hizo bado ni njema.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano, marekebisho yaliyofanyika yaliyo mengi yanalenga kuboresha maeneo ambayo Wabunge tumelalamikia. Mtaona hata hii PAYE imeshushwa kutoka asilimia tisa kwenda asilimia nane, lilikuwa ni jambo la muda mrefu. Iliwahi kuwa double digits, tangu Serikali ya Awamu ya Nne, ikashushwa kidogo, ikashushwa tena Awamu ya Tano ikaenda kwenye single digit, naona Awamu ya Sita pia imeendelea kushuka single digit kwenda asilimia nane.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo ni kuwapunguzia makali wafanyakazi, maana yake inavyoonekana wafanyakazi ndio ambao wamekuwa wakibeba mzigo wa kuendesha nchi yetu kupitia kodi kuliko maeneo mengine. Sasa angalau hii ya kupunguza inawapa nafuu wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika usikivu huo huo tuliona kuna lengo la kutoza asilimia 3 ya mapato kwa wachimbaji wadogo, lakini sema hawa ni wachimbaji wadogo hawaja-graduate wala mapato yao hayajajulikana vizuri unakwendaje kuwakata kodi asilimia tatu, lakini nalo naona Serikali imesikia imeliondoa, jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jingine ambalo ni usikivu ule ule ambao Wabunge wengi tulichangia ni kwenye kodi za majengo. Tuliona huko nyuma imekusanywa na TRA changamoto zikaonekana, lakini sisi ambao tumefanya Sekta ya TAMISEMI tunapenda kuamini kwamba kodi za majengo ukisoma mapato ya asili ya Local Government Authorities huwa ni property tax.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hapa miaka kadhaa iliyopita kodi hizi zilikuwa zinakusanya asilimia moja pamoja na Serikali Kuu, kwa usikivu ule ule tunaona imeamuliwa sasa fedha zitakusanywa kupitia TANESCO, lakini Serikali inazungumzia kuweka utaratibu wa kurejesha asilimia 15 kwenye Serikali za Mitaa ili waweze kuzitumia kuboresha mazingira yalipo majengo hayo, jambo jema hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa ungeniuliza hapa ningemshauri Mheshimiwa Dkt. Mwigulu hii ingeenda juu zaidi kwa sababu unapokusanya kodi ya majengo watu wanataka kuona kwenye mazingira yale ya majengo kwa kiasi gani yamekuwa bora, usafishaji, uzoaji wa taka mijini, usafishaji wa mitaro na kuiboresha pale inapokuwa imeharibika, mapato haya ndiyo ambayo kwa hiyo hata mwenye nyumba angeona analipa na thamani anaiona pale mbele ya nyumba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunasema ni mwanzo mzuri wa kurejesha kiwango hiki, lakini matarajio yangu ni kwamba kiwango hiki kingepanda juu kingewasaidia sana Local Government kuwa na mapato ya uhakika zaidi. Lakini nafarijika alivyofafanua kwamba kwa wale ambao hawana mita za LUKU mfumo uliopo utaendelea kwa maana Local Government zijidhatiti kwa ajili ya kukusanya property tax kwenye majengo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni hili ambalo kidogo limeibua hisia la transfer pricing mimi nadhani kama hatua ambazo zinasemwa zilikuwa zinafanyika za kufilisi kabisa biashara, nadhani haikuwa na tija sana. Sasa hii inayopendekezwa si kuto adhibu badala yake ni kurekebisha adhabu ile kwa asilimia Fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa mawazo wangu na ningeomba Wabunge tuliunge hili mkono, kwamba madamu hatuende kumsamehe, lakini anakwenda kupewa adhabu isiyohusisha kufilisi kabisa, nadhani ni muelekeo mzuri zaidi kuliko kuzungumzia kwamba ulenge kufilisi halafu unafunga biashara hata wale watu waliokuwa wanalipa kutokana na biashara ile hawatalipa fedha hiyo wala hutaipata, mapato wala hutayapata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ambacho ningeomba Serikali ifanye ni kujenga uwezo wa watalaam wetu kubaini michezo ya transfer pricing kwa sababu ninavyojua hatuna watu wenye weledi huo, kwa hiyo, Serikali ingejizatiti kujenga uwezo wa watu wetu kwenye sekta hasa ya TRA na sekta yenyewe ya fedha ili kubaini vitu hivi kwa mapema zaidi kuliko…

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jumanne Sagini kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Constantine Kanyasu.

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninampongeza mchangiaji Mheshimiwa Sagini, lakini dawa pekee ya transfer pricing ni kwa Serikali kusimamia vizuri sheria ya Local Content ambayo imeeleza vizuri kwamba katika mazingira ambapo supplier au mali inayotakiwa haipo Tanzania na supplier anatoka nje basi lazima huyo aingie ubia na mtanzania ili kuweza kuficha ile kitu, lakini kwa bahati mbaya imekuwa haisimamiwi. Nakushukuru sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jumanne Sagini unaipokea taarifa hiyo.

MHE: JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea, lakini haiondoi bado umuhimu wa kuendelea kujielimisha zaidi namna ya kubaini ujanja unaotumiwa na hawa wenzetu ili vijana wetu waweze kuyabaini mambo haya mapema na kuyadhibiti yanavyotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)