Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Kabula Enock Shitobela (11 total)

MHE. ESTER A. BULAYA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalinda Akinamama wanaochenjua dhahabu dhidi ya sumu ya zebaki ambayo ina madhara makubwa kiafya?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Serikali katika kuwakinga akinamama wanaochenjua dhahabu kwa kutumia kemikali ya zebaki ni kuendelea kutoa elimu ya uchimbaji na uchenjuaji salama wa madini pamoja na madhara ya kemikali hiyo kwa wachimbaji wadogo. Elimu hiyo inatolewa na Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mpango huu, Serikali kupitia Wizara ya Madini imejenga Vituo vitatu (3) vya Mfano vya uchenjuaji wa madini ya dhahabu katika maeneo ya Itumbi (Chunya), Lwamgasa (Geita) na Katente (Bukombe) ambayo yameonekana kuwa na wachimbaji wadogo wengi zaidi. Teknolojia ya uchenjuaji inayotumika katika vituo hivyo ni Carbon–in–Pulp (CIP) ambayo ni mbadala wa matumizi ya kemikali ya zebaki.

Mheshimiwa Spika, zipo kampuni tayari za uchimbaji mdogo ambazo zimeanza kuchenjua dhahabu kwa kutumia teknolojia ya shaking table, meza inakuwa itatikiswa kufuatia gravity ambayo haitumi zebaki wala kemikali yoyote. Teknolojia hii Wizara inaendelea kuifanyia majaribio ili kuona tija yake kabla ya kuanza kuitumia kwa wachimbaji wote hasa wale wachimbaji wadogo.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza: -

Je, Serikali imefikia wapi kuhusu kufanya uchunguzi ili kujua chanzo cha ugonjwa wa saratani katika Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa na ina mpango gani wa kudhibiti ongezeko la ugonjwa huo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imeshafanya utafiti wa kina nchi nzima uliosaidia kutambua kuwa Kanda ya Ziwa ni saratani zipi zinaongoza ambazo ni saratani ya kibofu cha mkojo, saratani ya mji wa uzazi wa kinamama, saratani ya damu, macho na figo. Aidha, wataalamu wamekusanya sampuli za damu za watu 7,000 ambao hawana saratani ili kulinganisha na sampuli za damu za wenye saratani. Utafiti huu utasaidia kubaini chanzo cha hizo saratani. Hivyo, kwa sasa bado utafiti unaendelea na visababishi vinavyosemwa bado ni nadharia tu kutokana na shughuli za kijamii katika maeneo husika.

(b) Mheshimiwa Spika, hadi sasa mpango wa kudhibiti ongezeko umejikita katika kutoa elimu ya afya kwa viashiria vinavyodhaniwa pamoja na kuzingatia mkakati wa kitaifa kwenye maeneo saba yaliyoainishwa ili kudhibiti viashiria vya saratani. Ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, ni lini serikali itakamilisha ujenzi wa bandari zilizopo Mkoa wa Mwanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) imekuwa ikiboresha miundombinu ya Bandari za Mwanza Kaskazini na Kusini kwa kutumia bajeti zinazopangwa kila mwaka. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, TPA imekamilisha uboreshaji wa jengo la abiria, awamu ya kwanza na matenki manne ya kuhifadhia mafuta katika Bandari ya Mwanza Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka fedha 2022/2023 Serikali kupitia TPA imepanga kufanya utanuzi wa eneo la maegesho ya meli (berth extension), kuongeza kina cha maji (dredging) barabara ya kuingia Bandarini na kuboresha miundombinu saidizi katika bandari ya Mwanza Kaskazini. Kwa upande wa Bandari ya Mwanza Kusini, TPA imepanga kuongeza eneo la maegesho ya meli (berth extension), barabara ya kuingia Bandarini na uboreshaji wa Miundombinu saidizi. Aidha, uboreshaji huo utaenda sambamba na ununuzi wa mitambo ya kuhudumia mizigo bandarini. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, ni sheria gani inayotumika kwenye tozo za bandari nchini?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tozo za bandari zinatozwa kwa mujibu wa Sheria ya Bandari Namba 17 ya mwaka 2004. Kwa mujibu wa sheria hiyo, kitabu cha viwango vya tozo (tariff book) huidhinishwa na mdhibiti ambaye ni Shirika la Wakala wa Meli Tanzania (TASAC).

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Bandari Namba 17 ya mwaka 2004 imeeleza vyanzo vya mapato vya TPA ambavyo vinajumuisha tozo za bandari (kifungu Na. 67). Aidha, sheria hiyo inaelekeza TPA kuandaa tariff book inayoainisha viwango vya tozo za bandari kwa kila huduma, ahsante.
MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza kabisa tatizo la vifo vya akinamama katika Mkoa wa Mwanza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali ya Mheshimiwa kabula Enock Shitobelo Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeimarisha huduma za akina mama kujifungulia katika vituo vya huduma katika Mkoa wa Mwanza kwa kujenga vituo vya afya 22 vinavyotoa huduma za upasuaji, na inaendelea na ujenzi wa vituo vya afya 15 vitakavyotoa huduma za upasuaji mara vitakapokamilika. Aidha, serikali imeimarisha utoaji wa elimu ya Afya ya uzazi kuhusu viashiria vya hatari kwa akina mama wajawazito na kupitia ajira mpya zilizotangazwa itapeleka wataalamu zaidi ili kuhakikisha akina mama wajawazito wanapata huduma sahihi kutoka kwa wataalamu, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kudhibiti matukio ya ubakaji na ulawiti katika shule za bweni?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sehemu ya kudhibiti matukio ya ubakaji na ulawiti kwa wanafunzi, Serikali imetoa Waraka wa Elimu namba 11 wa mwaka 2002 kuhusu malezi, unasihi na ulinzi wa mtoto ambapo Waraka unaelekeza kila shule na chuo cha ualimu kuanzisha huduma za malezi na ushauri nasaha kwa wanafunzi. Katika utekelezaji wa Waraka huo Serikali imewezesha mafunzo kwa walimu wawili wa ushauri na unasihi kwa kila shule pamoja na kuanzisha dawati la ulinzi na usalama wa mtoto shuleni kwa lengo la kutoa fursa kwa wanafunzi kuzungumza na kuripoti vitendo vya unyanyasaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imetoa Waraka wa Elimu namba mbili wa mwaka 2023 kuhusu utoaji wa huduma ya bweni kwa wanafunzi wa elimu ya awali na msingi ambapo waraka huu unaelekeza kuwa huduma ya bweni itolewe kwa wanafunzi kuanzia darasa la tano na kuendelea. Hatua hii imezingatia ukweli kuwa wanafunzi wa umri huo walau wana upeo wa kutambua baya na zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu kwa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla ni kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa mtoto dhidi ya vitendo vya unyanyasaji wawapo shuleni na majumbani pia.
MHE. FURAHA N. MATONDO K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, lini Serikali itaongeza wauguzi katika Hospitali ya Bugando kwani kwa sasa ina upungufu wa wauguzi 1,200?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Bugando ina watumishi jumla 1,930, wauguzi wakiwa 667. Katika watumishi hawa wote, Serikali inawalipa mishahara watumishi 1,120. Hopsitali ya Bugando kwa mapato yake ya ndani inawalipa watumishi 2,205 mishahara kamili pia inawalipa watumishi 605 nusu mshahara.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza:-

Je, Serikali haina njia mbadala ya matumizi ya matimba kama ngazi ambayo yanamaliza miti na hivyo kuharibu mazingira?
WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa magogo ya miti ni moja ya teknolojia rahisi na muhimu katika ujenzi wa migodi ya chini ya ardhi kwenye shughuli za uchimbaji mdogo wa madini nchini, ambapo miti hiyo hutumika katika ujenzi wa kuta na dari za migodi ili kuweka mazingira salama ya migodi midogo kwa wachimbaji. Wachimbaji wadogo hununua miti hiyo kutoka kwenye hifadhi za misitu na mashamba ya miti kupitia mawakala wa miti kwa kufuata taratibu za uvunaji wa miti. Teknolojia ya matumizi ya magogo ya miti imeenea zaidi kwa wachimbaji wadogo kwa kuwa inasaidia kuimarisha usalama wa migodi na haihitaji uwekezaji mkubwa wakati wa ujenzi wa migodi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia zipo teknolojia nyingine zinazotumika kwenye ujenzi wa migodi ya chini ya ardhi ambazo hutumia zege na vyuma ili kuimarisha kuta na dari za migodi hiyo. Teknolojia ya zege na vyuma hutumiwa zaidi na Wachimbaji wa Kati na Wakubwa kwa sababu ni ghali ukilinganisha na wachimbaji wadogo.
MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza:-

Je, nini mpango wa Serikali wa kuondoa magugu ambayo yanasababisha uchafuzi katika Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali wa Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ili kudhibiti magugu maji yasiendelee kuleta athari katika Ziwa Victoria, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali tangu mwanzoni mwa miaka ya tisini. Hatua hizo ni pamoja na:-

(i) Kutekeleza Mradi wa Hifadhi ya Mazingira katika Ziwa Victoria (Lake Victoria Environmental Management Project) ambao pamoja na mambo mengine ulitekeleza shughuli zilizolenga kudhibiti magugu maji kwa kutumia njia mbalimbali zikiwemo za kibaiolojia;

(ii) Kutoa elimu na kuwajengea uwezo wananchi wanaoishi karibu na Ziwa namna ya kujitolea katika kazi za kutokomeza na kuenea kwa magugu maji kila yanapojitokeza Ziwani; na

(iii) Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imeandaa na inatekeleza Mkakati na Mpango Kazi wa Taifa wa Kukabiliana na Viumbe Vamizi wa mwaka 2019-2029 ambao unatoa mwongozo wa namna ya kuzuia kuingia na kuenea kwa viumbe vamizi na pia una mipango endelevu ya kushughulikia viumbe vamizi waliopo na wale wale wanaoweza kuingia.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea na juhudi hizi za kupambana na magugu maji katika Ziwa Victoria ili kudhibiti uhabirifu wa mazingira na athari zitokanazo na uharibifu huo nchini, nakushukuru.
MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapunguza tozo zinazotozwa na TPA kwani imekuwa ikitoza tozo kubwa kwenye mizigo kuliko Makampuni binafsi?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE FREDY MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha Bandari zote za Tanzania zinatoa huduma bora na kwa gharama nafuu ili kuendana na hali halisi ya ushindani katika bandari za ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika. Katika kufikia azma hiyo, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ipo katika hatua za mwisho za kufanya mapitio ya gharama za huduma za bandari. Hivi sasa, uchambuzi wa maoni yaliyowasilishwa na wadau mbalimbali yanafanyiwa kazi na zoezi hili linatarajiwa kukamilika Julai, 2022.
MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga chumba maalum yaani Incubator kwa ajili ya Mama na Watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya Ukerewe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe inatoa huduma kwa watoto wachanga na wale waliozaliwa kabla ya muda yaani Njiti. Hata hivyo, nafasi inayotumika kutolea huduma hiyo ni ndogo kwa mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya inaendelea na uhakiki yaani assessment kwenye Hospitali zote za Halmashauri nchini ili kuweza kubaini mahitaji ya vyumba vya kuhudumia watoto njiti na kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa majengo hayo, ahsante.