Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Kabula Enock Shitobela (4 total)

MHE. ESTER A. BULAYA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalinda Akinamama wanaochenjua dhahabu dhidi ya sumu ya zebaki ambayo ina madhara makubwa kiafya?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Serikali katika kuwakinga akinamama wanaochenjua dhahabu kwa kutumia kemikali ya zebaki ni kuendelea kutoa elimu ya uchimbaji na uchenjuaji salama wa madini pamoja na madhara ya kemikali hiyo kwa wachimbaji wadogo. Elimu hiyo inatolewa na Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mpango huu, Serikali kupitia Wizara ya Madini imejenga Vituo vitatu (3) vya Mfano vya uchenjuaji wa madini ya dhahabu katika maeneo ya Itumbi (Chunya), Lwamgasa (Geita) na Katente (Bukombe) ambayo yameonekana kuwa na wachimbaji wadogo wengi zaidi. Teknolojia ya uchenjuaji inayotumika katika vituo hivyo ni Carbon–in–Pulp (CIP) ambayo ni mbadala wa matumizi ya kemikali ya zebaki.

Mheshimiwa Spika, zipo kampuni tayari za uchimbaji mdogo ambazo zimeanza kuchenjua dhahabu kwa kutumia teknolojia ya shaking table, meza inakuwa itatikiswa kufuatia gravity ambayo haitumi zebaki wala kemikali yoyote. Teknolojia hii Wizara inaendelea kuifanyia majaribio ili kuona tija yake kabla ya kuanza kuitumia kwa wachimbaji wote hasa wale wachimbaji wadogo.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza: -

Je, Serikali imefikia wapi kuhusu kufanya uchunguzi ili kujua chanzo cha ugonjwa wa saratani katika Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa na ina mpango gani wa kudhibiti ongezeko la ugonjwa huo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imeshafanya utafiti wa kina nchi nzima uliosaidia kutambua kuwa Kanda ya Ziwa ni saratani zipi zinaongoza ambazo ni saratani ya kibofu cha mkojo, saratani ya mji wa uzazi wa kinamama, saratani ya damu, macho na figo. Aidha, wataalamu wamekusanya sampuli za damu za watu 7,000 ambao hawana saratani ili kulinganisha na sampuli za damu za wenye saratani. Utafiti huu utasaidia kubaini chanzo cha hizo saratani. Hivyo, kwa sasa bado utafiti unaendelea na visababishi vinavyosemwa bado ni nadharia tu kutokana na shughuli za kijamii katika maeneo husika.

(b) Mheshimiwa Spika, hadi sasa mpango wa kudhibiti ongezeko umejikita katika kutoa elimu ya afya kwa viashiria vinavyodhaniwa pamoja na kuzingatia mkakati wa kitaifa kwenye maeneo saba yaliyoainishwa ili kudhibiti viashiria vya saratani. Ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, ni lini serikali itakamilisha ujenzi wa bandari zilizopo Mkoa wa Mwanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) imekuwa ikiboresha miundombinu ya Bandari za Mwanza Kaskazini na Kusini kwa kutumia bajeti zinazopangwa kila mwaka. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, TPA imekamilisha uboreshaji wa jengo la abiria, awamu ya kwanza na matenki manne ya kuhifadhia mafuta katika Bandari ya Mwanza Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka fedha 2022/2023 Serikali kupitia TPA imepanga kufanya utanuzi wa eneo la maegesho ya meli (berth extension), kuongeza kina cha maji (dredging) barabara ya kuingia Bandarini na kuboresha miundombinu saidizi katika bandari ya Mwanza Kaskazini. Kwa upande wa Bandari ya Mwanza Kusini, TPA imepanga kuongeza eneo la maegesho ya meli (berth extension), barabara ya kuingia Bandarini na uboreshaji wa Miundombinu saidizi. Aidha, uboreshaji huo utaenda sambamba na ununuzi wa mitambo ya kuhudumia mizigo bandarini. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELO aliuliza: -

Je, ni sheria gani inayotumika kwenye tozo za bandari nchini?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tozo za bandari zinatozwa kwa mujibu wa Sheria ya Bandari Namba 17 ya mwaka 2004. Kwa mujibu wa sheria hiyo, kitabu cha viwango vya tozo (tariff book) huidhinishwa na mdhibiti ambaye ni Shirika la Wakala wa Meli Tanzania (TASAC).

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Bandari Namba 17 ya mwaka 2004 imeeleza vyanzo vya mapato vya TPA ambavyo vinajumuisha tozo za bandari (kifungu Na. 67). Aidha, sheria hiyo inaelekeza TPA kuandaa tariff book inayoainisha viwango vya tozo za bandari kwa kila huduma, ahsante.