Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Alice Karungi Kaijage (19 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa name ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kufika kwenye Bunge hili leo. Pia naomba nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi, Jumuiya ya Wanawake pamoja na wanake wema sana wa Mkoa wa Pwani ambao waliridhia kunisindikiza na kunifanya niweze kuwa Mbunge wao kuwawakilisha. Navishukuru Vyama vya Wafanyakazi; pia nashukuru familia yangu, Mama yangu, ndugu, jamaa na marafiki kwa ujumla wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijielekeza kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, nimesoma hotuba zote za 2015 na 2020; Mheshimiwa Rais ameonyesha nia njema na dira katika kuiendeleza Tanzania, lakini ameonyesha dhamira ya wazi kwenye kulinda amani yetu na pia kuudumisha Muungano wetu. Nina sababu zote za kushukuru Vyombo vya Usalama na Ulinzi ambavyo kwa pamoja na wananchi wenye nia njema wameweza kushirikiana kuendelea kulinda amani ya nchi yetu. Wanastahili pongezi kubwa sana vyombo vya Ulinzi na Usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, tumeona suala nzima la huduma za jamii katika ujumla wake, wenzangu wamezungumzia, lakini naomba nijikite kwenye suala la afya. Ukiangalia kwenye Ilani na hotuba yake, Mheshimiwa Rais ameeleza nia njema kabisa ya kuboresha huduma za kibigwa na pia kuongeza miundombinu pamoja na vifaa vya kutosha vya kisasa. Siyo suala la kupinga kabisa lipo wazi kwa jinsi ambavyo huduma za kibigwa zimeimarika. Ukiangalia taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, halina ubishi wote tunafahamu. Muhimbili hiyo hiyo mpaka sasa wanapandikiza figo, wanaweka masikio, cochlear implant, wanafungua kichwa ubongo bila kufungua fuvu. Kwa hiyo, huduma nyingi zimeimarishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema hayo kwa sababu nina jambo moja la kulisema. Katika suala nzima la magonjwa la kiharusi (stroke) imekuwa ni tatizo ambalo ni kubwa sana kwa siku admission au wanalazwa wagonjwa watano mpaka sita Muhimbili, acha Mlonganzila au hospitali zingine za rufaa. Kwa hiyo nina wazo moja, tunaomba taaisisi ya Stroke ianzishwe; wagonjwa wale wanakaa muda mrefu, wanachangwanywa na wagonjwa wengine, immunity yao ni ndogo. Kwa hiyo kuna uwezekano kama wakianzisha stroke center kama wenzetu South Africa na Egypt wanafanya pawe na stroke nurse, pawe na wataalam, kwa hiyo itakuwa ni kitengo kinachojitegemea, kitafanya outreach, elimu kwa jamii pamoja na kuwa na Manesi katika hospitali zingine ambazo ni kubwa ili kupunguza tatizo la stroke ambayo sisi wote ni wahanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye Hospitali yetu ya Mirembe. Hii ni hospitali ya muda mrefu, ina miaka 93, imeanzishwa mwaka 1927. Hii hospitali inachukua Watanzania wa kawaida na sisi ni wahanga hatuwezi kukwepa kuingia pale siku moja. Hii hospitali ni ya muda mrefu ina miundombinu chakavu, mikongwe, lakini inasababisha kupata taswira nzima ya huduma njema inayotolewa pale. Pili ipo katika Makao Makuu ya Nchi. Mazingira mazuri yanawatia moyo wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii na Watanzania wale ingawa afya yao ina matatizo lakini wanastahili kukaa kwenye mazingira mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, bed state kwa siku wagonjwa hawapungui mia tano, kuna Isanga, kuna Mirembe Proper na vituo vingine vya kutolea dawa za kulevya, vyote hivyo viko chini ya Mirembe. Naomba sasa ufike wakati bajeti yao iongezwe, ikiwezekana sasa iwe taasisi, kwa mwezi wanatumia zaidi ya milioni 280, kwa maana ya huduma za kila siku kwenye taasisi ile. Naomba iangaliwe taasisi ya Mirembe kwa sababu sisi sote ni wahanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia mchango wa maandishi katika Wizara ya Afya na nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii, pia nakupongeza Mheshimiwa Spika, Naibu Spika pamoja na uongozi wote wa Bunge kwa kazi nzuri mnazoendelea kuzifanya.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia kwa umahiri suala zima la afya, nampongeza pia Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, pia naipongeza Wizara ya Afya kwa kumshauri vyema Rais katika kusimamia suala zima la upatikanaji wa dawa nchini. Nampongeza Mama Samia Suluhu kwa ziara yake ya Uganda ambayo imeleta unafuu kwa waathirika wa virusi vya UKIMWI kupata dawa za kupunguza makali ya virusi vya UKIMWI hapa nchi jirani ya Uganda katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, ni jambo kubwa na zuri limefanyika hivyo tunaipongeza Wizara na wataalamu wake wote kumshauri vyema Rais.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi za Serikali za kuhakikisha upatikanaji wa dawa, bado tunaendelea kuishauri Serikali kama nilivyochangia katika bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba Serikali ione sasa namna bora ya kuongeza uwezo wa upatikanaji wa dawa kwa kuingia ubia kwa kufufua kilichokuwa kiwanda chetu cha dawa cha Mkoani Arusha (Tanzania Pharmaceutical Industry- TPI) hivyo Serikali kupitia MSD itachukua 60% ya hisa za uwekezaji wa kiwanda kile ambazo zilikuwa ni za mwekezaji binafsi na hisa 40% zitabakia kwa Msajili wa Hazina kama ilivyokuwa toka mwanzo. Kwa hiyo Serikali itakuwa na 100% ya hisa ili kufufua kiwanda chetu cha Arusha. Tunaamini kwa usimamizi mzuri wa MSD tutakuwa na uwezo mzuri wa kuzalisha dawa za kutosha kwa ajili ya wananchi wetu na pia tunaweza kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia kwa dhati na kwa moyo wa kizalendo na kwa kujitoa muhanga katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda ikiwa ni pamoja na viwanda vya kutengeneza dawa ili kuelekea katika kutimiza malengo endelevu ya milenia.

Mheshimiwa Spika, nikiwa kama mwakilishi wa wafanyakazi wa Tanzania Bara Bungeni, napongeza kitendo cha Mheshimiwa Rais na Serikali yake kuendelea kuboresha maslahi ya watumishi na kuongeza mshahara kwa asilimia 23.3 jambo ambalo halijawahi kutokea katika Serikali yetu na suala la ongezeko la mshahara limekuwa ni kilio cha wafanyakazi kwa miaka isiyopungua sita.

Mheshimiwa Spika, ninaendelea kuliomba Bunge kuazimia kumshukuru na kumpongeza Rais na Serikali yake kwa niaba ya wafanyakazi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuandika hayo naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza, naomba nianze kupongeza Serikali kwa kuleta Mpango huu mzuri, pamoja na mipango mingine yote iliyotangulia tuliona kwamba ina nia ya kuhakikisha tunafikia Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025 sanjari na kukuza malengo endelevu ya SDGs. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu umekuwa na nguzo muhimu tatu, ikiwa ni utawala bora, maendeleo ya watu pamoja na kukuza uchumi. Kukuza uchumi ni kuwekeza katika sekta za kiuchumi na kiuzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa muda mrefu imeendelea kuingia katika mikataba na makubaliano mbalimbali aidha kupitia wahisani, mikopo, uwekezaji ambalo ni jambo jema sana, lakini tumeona mara nyingi Mheshimiwa Rais amekuwa akihoji, ndugu zangu hivi kweli huu uwekezaji una tija? Hivi hii miradi ina tija? Tija ni nini basi? Tija ni uwiano kati ya kitu unachowekeza na kile kinachopatikana, lakini kikionyesha mabadliko chanya katika mtu mmoja mmoja, katika taasisi na nchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tija ni nini ili kama mwekezaji anaweka mradi wake au analeta msaada wake au anaweka kampuni yake, mwisho wa siku anapoondoka aache ajira endelevu, aache ujuzi, akuze ujuzi kwa wale ambao wanahusika na pia kubwa kabisa waache teknolojia pamoja na ubunifu. Yaani mradi unapokwisha asiondoke yeye na vitu vyake akaacha vitu vitupu. Kwa mfano katika kuwekeza 100% kwa maana ya consultancy anaanzisha mradi yeye 100% mgeni anakuwepo pale pengine engineer wetu au mtaalam wetu anashuhudia tu msumari unavyopondwa pondwa kwenye shirika hilo au kwenye kampuni au mradi au mashine inavyofungwa, lakini ule ujuzi hashiriki moja kwa moja, anapoondoka anaondoka na ujuzi wake mwekezaji. Kwa hiyo ifikie sehemu, nashauri Serikali hii miradi safari hii, tunaona watu wengi wanalalamikia miradi ya maji, miradi mbalimbali ambayo tumeingia lakini kama nilivyofafanua nini maana ya tija. Je miradi hii inaacha tija kweli? Kwa nini? Sasa ifikie sehemu tutumie chombo kile kinaitwa chombo cha kukuza tija na ubunifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani liliitwa Shirika la Tija la Taifa, chombo hiki kipo na kipo vizuri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu chombo hiki sasa kipewe meno kipewe uwezo ili kuondoa haya malalamiko yote ambayo yako kwenye miradi ambayo ina mambo mengi ambayo ni baadhi lakini kwa kweli ni mingi, miradi ambayo imekuwa ina-fail. Chombo hiki kabla miradi au mikataba haijaanza kutekelezwa, chombo kikaangalie kikapime hii miradi itakuwa na tija kama nilivyoeleza maana ya tija ili baadaye kusiwepo na malalamiko. Huu ni wakati wa kukipa chombo hiki meno na uwezo maana tunacho, tunacho kwenye Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia viwanda tulivyopata ni vingi sana kwenye nchi sasa hivi. Kweli ni vingi na ni vizuri, ni jambo jema, lakini chombo hiki bado kina uwezo wa kwenda kutathmini vile viwanda, kufanya analysis na kutoa ushauri ili mwisho wa siku viwanda visiwe vya kupotea, viwe vina-sustain vinakaa muda mrefu yaani vinaendeleza kuwa na tija, maana yake havikufanyiwa huu upekuzi mwanzo ndiyo maana tunaona kuna malalamiko mengi, kwenye viwanda hatujui itakuwaje baadaye na miradi imeshaonyesha jinsi ilivyokuwa kwenye Mipango iliyopita. Kwa hiyo, nashauri chombo hiki kitumike ili kilete tija katika miradi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitoe mfano, wenzetu China wakati wanaandaa Olympic 2008 walikuwa wametoa nafasi kwa wawekezaji, lile ni jambo kubwa lilihitaji watu wawekeze kwa wingi, lakini walikuwa wakali, wakasema unakuja kuwekeza ndiyo, lakini kuanzia mwanzo wa mchakato wa kutaka kuwekeza, kama ni kujenga uwanja wewe mwekezaji utafanya kazi kwa asilimia 70 na sisi wazawa consultancy mzawa atafanya 70 ili pale wanapomaliza watapata faida ya 70% yes lakini 30% kutoka anapowekeza anajenga kiwanda au anajenga uwanja ile pesa inabaki ndani inazunguka kwa sababu yule mwekezaji wa ndani (consultancy) alikuwepo toka mwanzoni. Kwa hiyo inabidi kuangalia mfano wa wenzetu, wameendelea lakini wako makini sana na mali yao na mzunguko wa pesa yao ndani mwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwenye suala la afya, na-declare interest, suala zima la kada ya physiotherapy. Naipongeza Serikali sana imefanya bidii nyingi lakini taaluma hii ambayo ni matibabu kwa njia mbalimbali ikiwemo mazoezi tiba, wataalam ni wachache, wenye shahada hawazidi 100 kwenye nchi nzima, lakini pia chuo ambacho kinatoa shahada hii ya physiotherapy Kiswahili chake matibabu ya njia mbalimbali ambayo pia ni mazoezi tiba, ni KCMC peke yake. Niipongeze Wizara ya Afya sasa ina mpango wa kuanzisha hii kozi kwenye Chuo cha Muhimbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado haitoshi, naomba niishauri Serikali ifanye uanzishaji wa kozi hii kwenye Chuo cha UDOM na Bugando. Hawa watu wanahitajika sana kwa sababu tunafungua hospitali nyingi za mikoa kwa bidii na pia hospitali za wilaya, pamoja na vituo vya afya. Pia nashauri kwa sasa kwenye vituo vya afya na hospitali za wilaya, hivi vitengo viwekwe, havipo, tufikirie viwekwe na wataalam waongezeke, wapelekwe kule kwa sababu ni idara muhimu sana, lakini ina watu wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia pawepo na wazo la kuongeza Shahada ya Uzamili na Uzamivu ikiwezekana ya kada hii ya physiotherapy hatuna kwenye nchi yetu. Ili upate Shahada ya Uzamivu lazima uende nje ya nchi. Kwa hiyo nilikuwa nashauri hili jambo litekelezwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongea hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema kuweza kusimama na kuchangia. Pia naungana na wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali yake kwa jinsi ambavyo anafanya kazi kwa umahiri mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakushukuru wewe kwa kuniruhusu kuchangia mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi wa mpango huu na bajeti hii ya mpango wa maendeleo wa mwaka huu 2022/2023 ambao ni mpango wa pili katika Mpango wa miaka mitano wa 2021 mpaka 2026.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nina sababu zote za kumpongeza pia Waziri wetu wa Mpango na Fedha na timu yake yote; na vile vile nampongeza Mwenyekiti wa Kamati kwa kazi nzuri waliyoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye mapendekezo ya Mpango, eneo la vipaumbele vya Mpango. Kwenye eneo hili kuna mambo mengi sana, lakini mimi naomba nichangie kipengele cha kuchochea uchumi shindani na shirikishi. Hapa yapo mambo mengi yamezungumzwa, mazuri sana. Kuna suala zima la mapinduzi ya TEHAMA, tunawapongeza Serikali imewezesha kabisa kuanzisha mfumo wa Taifa wa anuani za makazi, pilot study ikiwa Mwanza, lakini mimi nitajikita kwenye suala zima la kuimarisha miundombinu na mifumo ya kitaasisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna suala zima la kuboresha mifumo ya kiutawala na Menejiment ya Utumishi wa Umma na Mifumo ya Utoaji wa huduma za Serikali kwa wananchi. Ukiangalia kwenye mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi, inaonekana kwamba kipaumbele cha kugharamiwa itakuwa ni masuala mazima ya miradi ya maendeleo, sensa ya watu, mishahara, deni la Serikali na huduma za jamii, yaani maji afya na elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, kwa sababu Serikali sasa imekuja na jambo zuri sana, imekuja na suala zima la mfumo wa kuwezesha mifumo kuweza kubadilishana taarifa. Hili ni jambo kubwa limeanzishwa, labda kama watu wengine hawafahamu. Huu mfumo utawezesha mifumo yote kuingiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa Serikali ishafanya pilot study na mifumo mengine, kama mifumo mbalimbali ya taasisi mbalimbali kama NIDA, BRELA, NHIF, TAMISEMI yenyewe, Ofisi ya Ajira, Hazina kwenye payroll, kote sasa hivi imefanya pilot study.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nazungumzia hilo? Kuna suala zima la kuhusisha mifumo hii ili kusaidia utumishi na wananchi. Kwa nini nasema hivyo? Serikali sasa hivi imeanzisha mfumo wake wenyewe wa taarifa za utumishi na mishahara. Zamani tulikuwa tunatumia Lawson ya wageni, sasa hivi tuna mfumo unaitwa Human Capital Management Information System. Kwa hiyo, Serikali ina mfumo wake wenyewe. Kupitia huu mfumo, kuna taarifa zote za watumishi. Kwa hiyo sasa, mfumo huu unaingiliana na mfumo huu mkubwa ambao umeanzishwa ambao utakuwa unawezesha mifumo yote kubadilishana taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nauzungumzia kwa sababu gani? Ni kwa sababu mfumo huu utasaidia sasa, kwa mfano mtumishi anatarajiwa kustaafu mwakani, kwenye taarifa zake kwenye mfumo zinaonekana. Kwa hiyo, moja kwa moja mfumo utapeleka kwenye mfumo wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambao wameshaunganisha. Kwa hiyo, moja kwa moja mtumishi atakuwa hana shida tena kuanza kutafuta documents.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyowahi kusema, mtu kaajiriwa Kigoma kaja kustaafu Kibaha; kwa hiyo, sasa hivi huu mfumo utakuwa unarahisisha kwani taarifa zote ziko pale. Kwa hiyo, kama anataka information kutoka NIDA, inakuja kwenye ule mfumo ambao unawezesha mifumo ya kuwasiliana; kama inatoka kwenye NHIF, unakuja pale. Kwa hiyo, mtumishi sasa atakuwa hana shida tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiishi hapo tu. Huu mfumo unaendelea, kuna suala zima limeanzishwa linaitwa e- mfejesho. Nazungumzia suala la Serikali kuhudumia wananchi kupitia hii mifumo. Sasa hivi huu mfumo ulioanzishwa na umeanza kufanya kazi, unamwezesha mwananchi wa kawaida kuleta malalamiko yake, mapendekezo, pongezi na ushauri kupitia simu ya kawaida tu, massage au kupitia internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukasema kuna tatizo la TEHAMA, lakini ngoja nikwambie; naipongeza Serikali chini ya Mheshimiwa Mama Samia sina wasiwasi wa speed yao ya kuongeza mifumo ya mawasiliano. Kwa nini nasema hivyo? Mpaka sasa hivi tumeona katika mwaka huu wa Mpango unaoishia, kumeweza kufungwa mkonga wa Taifa wenye kilomita 409, utaunganisha kutoka Msumbiji mpaka Mtwara; na pia mkongo mwingine ambao umekamilishwa ni wa kutoka Namanga mpaka Arusha. Hii inaonyesha jinsi Serikali ina dhamira kabisa ya kuhakikisha mawasiliano yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la mwananchi wa kawaida kuwasiliana na Serikali au kupitia internet, baada ya muda kwa speed ninayoiona kwa ufanyakazi wa Mheshimiwa Mama Samia na Serikali yake, tutakuwa hatuna shaka. Kwa nini nazungumzia suala hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Serikali au bajeti inayokuja iseme suala la kuwezesha huu mfumo. Ni mfumo muhimu sana ambao utaleta harmony kule chini kwa watumishi wetu. Kwa sababu kama mfumo utaweza kuwasiliana na mifumo ya hifadhi ya jamii; sasa hivi naishukuru Serikali kusema kweli, wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Serikali sasa hivi imeweza kulipa mafao shilingi trilioni 1.5, imelipa pension shilingi bilioni 449 mpaka sasa; na mpaka sasa hivi Serikali imeanza mchakato wa kuhakikisha kwamba unalipa Hati Fungani maalum zisizo taslimu kiasi cha shilingi trilion 2.1. Hata kama haijalipa zote, lakini unaona nia njema ya kuendelea kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa mama Jenista hapa anapambana kila siku ya vikao vya wafanyakazi pamoja na taasisi tusimvunje moyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba, nia ya Serikali ni njema...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Alice pokea taarifa.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja iliyozungumzwa hapa mapema ambayo inajibiwa, iliyozungumzwa Mheshimiwa Bulaya, inayojibiwa na mtu ambaye hatakiwi kujibu, ni hivi, kwa mujibu wa hesabu jumuifu za Taifa, kama ambavyo imekuwa reported na CAG kwenye report iliyotolewa Machi mwaka huu, madeni ya mifuko kiujumla wake, kama inavyokuwa reported 2017/2018 ni shilingi trilion 19. Kwa hiyo, hoja hapa ni kwamba, kama umechukua fedha za mifuko shilingi trilioni 19, unakuja kwenye Mpango unatuambia shilingi trilioni mbili, tena inahusu pre- 1999 ambapo kwenye pre-1999 mlikuwa mnadaiwa shilingi trilioni saba. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, kwa mambo haya, tusifanyie mzaha. Imefika kipindi sasa mifuko inabidi makusanyo yao kwa mwezi ndiyo wanalazimika kulipa pension na hayatoshi, inabidi wakatafute kwingine. Kwa hiyo, hakuna mtu mwenye nia mbaya, hakuna mtu ambaye hatambui, kwa sababu tunasema tunatambua hicho kidogo kilichofanyika, lakini kuna mzigo nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampa taarifa Mheshimiwa Mbunge ili aweze kuipokea tu kiroho safi. Hapa hatutafurani mchawi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Taarifa hiyo Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage unaipokea?

DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii siipokei kwa sababu mimi nipo katika ku-support na kuona nguvu ya Serikali inayofanyika kutatua whether ni shilingi trilioni 20 au shilingi trilioni 30, lakini nia thabiti ya Serikali tunaiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa anayezungumza, kwanza hakuna nia njema yoyote ya Serikali hapa. Hiyo shilingi trilioni mbili ya non cash bond kwenye shilingi trilioni saba, huu ni mwaka wa 22, tangu mwaka 1999. Hakuna nia nzuri ya Serikali. Serikali yenyewe haijapeleka michango, inadaiwa deni sugu shilingi bilioni 171. (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage unaipokea?

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei. Naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali inapokuja na Mpango huu ioneshe nia thabiti na kwa mapema sana kuhakikisha kwamba ina-support mfumo huu... (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Alice Kaijage pokea taarifa kutoka kwa Waziri wa Nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuungana na Mheshimiwa Mbunge anayechangia kwamba nia njema ya Serikali inaonekana kwa sababu, kama nia njema ya Serikali haingekuwepo, hatungefanya utathmini wa hiyo mifuko kuangalia sustainability yake; lakini kama nia njema ya Serikali ingekuwa haionekani, hatungehimiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu kwa mujibu wa Sheria ya Hifadhi ya Jamii, kazi ya mifuko hiyo kwa mujibu wa sheria ni kuandikisha wananchama, kukusanya michango, kufanya uwekezaji na kulipa mafao ya wananchama. Kwa hiyo, ili haya mambo yote yatimie, ndiyo maana Serikali kila jambo linalotokea ambalo ni hatarishi, linaloweza kuizamisha sekta, Serikali imekuwa ikisimama imara kufanya marekebisho na kuhakikisha kwamba sekta inaendelea kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampa taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba ni kweli nia ya Serikali ipo. Kila tatizo ni lazima tupambane nalo ili kuweka ustawi wa sekta kwa ujumla wake. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt Alice Kaijage, unapokea hiyo taarifa.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili taarifa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niseme kwamba Mpango utakapofika, bajeti ioneshe nia njema na kwa haraka ku-support mfumo huu ambao utawezesha mifumo yote kuwasiliana. Utarahisisha wafanyakazi kuhudumiwa na Watanzania kwa ujumla. Tumeona Mheshimiwa Mheshimiwa Waziri wa Utumishi ameanzisha ile “Sema na Waziri wa Utumishi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe nimeshawasiliana kwa simu, inawezekana. Kwa hiyo, Watanzania wataweza kuwasiliana na matatizo yao yatakuwa solved haraka na pia ina uwezo wa ku-counter check kwamba aliyeomba swali lake au hoja yake imejibiwa, anaona. Kwa hiyo, huyo ambaye hajajibu kama ni mtumishi mtendaji anawajibishwa. Kwa hiyo, ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba bajeti itakapokuja ihakikishe kwamba imechangia au imewezesha mfumo huu mkubwa ambao utawezesha mifumo yote kubadilishana taarifa, uko vizuri na umeimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuchangia katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Namshukuru Mwenyezi Mungu pia kunipa nafasi ya kusimama. Naendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa usimamizi mzuri wa Serikali yake yote mpaka tunaona jinsi ambavyo Wizara hii inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Jenista Mhagama pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Deo kwa kazi nzuri sana wakishirikiana na watendaji wote wa Wizara husika katika kufanikisha malengo ya kuboresha utumishi huu wa umma.

Mheshimiwa Spika, jukumu kubwa ambalo ofisi hii inalo ni kuhakikisha kwamba Utumishi wa Umma unaendelea kuzingatia suala zima la misingi ya utawala bora. Misingi ya utawala bora ni kufanya kazi kuzingatia sheria, sera na taratibu mbalimbali walizojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitatofautiana na wenzangu wengi walionitangulia; Serikali Awamu ya Sita katika mwaka huu tunaomaliza imeonyesha dhamira ya dhati kabisa ya kuboresha maslahi ya Watanzania ambao ni Watumishi wa Umma. Naepuka kurudia vyote walivyosema wenzangu kwa habari ya mishahara, upandishaji madaraja kufuta kodi ya Bodi ya Elimu ya Juu kwenye mishahara yetu, kupunguza kodi ya mshahara mpaka 8%, na mambo kadha wa kadha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala zima la upandishaji wa madaraja, wamevunja rekodi kwa maana ya mambo yote ambayo ameahidi Mheshimiwa Rais kwenye mwaka uliopita kupitia bajeti yake, kwa asilimia kubwa sana yametekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo yote mazuri yaliyotekelezeka, tunaendelea kutambua hali tete ya uchumi duniani unavyokwenda pamoja na adha mbalimbali za kivita. Pia tunatambua anguko la kiuchumi katika sehemu mbalimbali duniani, lakini pamoja na yote hayo, watumishi wa nchi yetu bado wanaendelea kuomba suala zima la upandishwaji wa mshahara kulingana na pato letu, basi liendelee kuzingatiwa pale itakapowezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mishahara hii tunashauri itakapopandishwa pale itakapowezekana, basi iwe kama zamani, izingatie suala zima la living wage, yaani mtu mshahara wake umsaidie kupanga mwezi mzima kula tarehe moja mpaka tarehe 30. Kwa nini? Sasa hivi mtumishi wa kawaida anapata mshahara mpaka tarehe 10, 15 umekwisha. Hii inapelekea kumpa msongo wa mawazo na inasababisha magonjwa mbalimbali hasa yasiyoambukiza ambayo pia ni mtihani mkubwa kuyagharamia. Hata hivyo naipongeza Serikali kwa kujiandaa kuja na Mfuko wa Bima ya Afya kwa Wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika utawala bora ni kusimamia suala zima la sheria, sera na taratibu walizojiwekea waajiri na watumishi. Hii pia inajielekeza katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba Serikali na Chama cha Mapinduzi inatumbua umuhimu wa vyama vya wafanyakazi ili kuleta mahojiano kati ya waajiri pamoja na waajiriwa kuboresha utumishi mahala pa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, tunashauri Wizara hii iendelee kusimamia kwa ukaribu utawala bora katika sehemu mbalimbali kati ya waajiri ili wafanyakazi wawe na uhuru wa kujiunga na vyama vyao bila vizuizi. Pia maslahi yao mbalimbali yaweze kuzingatiwa na kusimamiwa kupitia vyama vyao, kwani mtu mmoja mmoja sio rahisi kuhudumiwa. Kwa hiyo, naomba Wizara izingatie kwamba mahali pa kazi pote, watumishi wawe na uhuru wa kujiunga na vyama vya wafanyakazi na Mabaraza yawe huru ili wafanyakazi waweze kufumuka na kueleza changamoto zao.

Mheshimiwa Spika, hakuna sheria inamruhusu mfanyakazi mmoja atoke na kuleta changamoto yake. Hii inapelekea migomo ambayo siyo halali. Kwa sababu vyama vya wafanyakazi ndiyo pekee vinaruhusiwa kuendesha mgomo. Sasa kama wafanyakazi hawapati nafasi ya kueleza mambo yao kwenye Vyama vya Wafanyakazi wataeleza wapi? Vyama vya Wafanyakazi vikipata tatizo vinapeleka kwenye Tume ya Usuluhishi na ikishindikana, kwenye Mahakama Kuu, kwenye Kitengo cha Kazi. Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi inaweza kusema sasa nendeni kwenye mgomo.

Mheshimiwa Spika, natoa mfano wa madereva Tanzania. Madereva wana changamoto zao mbalimbali. Hivi ninavyozungumza na wewe kuna hatari ya mgomo, lakini ni kwa sababu waajiri wengi wamekuwa hawawapi uhuru wafanyakazi kujadili mambo yao kwa utaratibu. Hii inapelekea watu wachache kuanzisha migomo kinyume na utaratibu. Kwa hiyo, ofisi hii naishauri kupitia suala zima la utawala bora, basi isimamie masuala mazima ya wafanyakazi katika vyama vyao mahali pa kazi ili kuepusha misuguano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali, awamu iliyopita imetoa ajira za kutosha na sasa ziko ajira karibia 30,000. Kwa upande wa Idara ya Afya, mgawanyo wa ajira umekwisha. Mimi ninayo document, ajira zimeshagawiwa zote katika Wizara ya Afya, ila nina jambo moja nilisemee ambalo huwa nina interest nalo na nitakuwa sijawatendea haki nisiposema huku ndani.

Mheshimiwa Spika, nimezungumzia sana suala la Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili ya Milembe. Nimesemea sana hili suala mbali ya upungufu wa watumishi, vifaa na kadhalika. Tunaishukuru Serikali sasa imepanua hospitali katika suala zima la magonjwa mahututi pamoja na Emergence Department. Pamoja na upanuzi huo, lakini katika mgawanyo huu ile Hospitali ya Milembe haijapewa mtumishi hata mmoja. Ninashauri katika mgawanyo wa watumishi wa afya, hebu warudie tena, kwa sababu wako wanaojitolea katika hospitali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii huduma ni nyeti, watu wengi wakienda kwenye ajira, ikifika wakati wa kusoma, wanaondoka, wanasoma kozi nyingine. Hawa-specialize kwenye suala zima la afya ya akili, lakini watu wanaojitolea wapo pale, sasa ajira zimetoka wameona pia Milembe haijawa located. Kwa hiyo, nawashauri kama wenzangu kwamba suala zima la ajira tuliangalie kutokana na umuhimu wa sehemu husika.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia kabisa ni suala zima la ajira Wahadhiri wa Vyuo Vikuu. Nashauri kama inawezekana, Sekretarieti ya Ajira kama iwe kama zamani, iachie sasa vyuo viajiri especially watu ambao ni academic staff. Wanaweza wakaajiri technical staff lakini academic staff wawaachie kwa sababu TCU inashauri, angalau mtu mwenye GPA 3.5 aajiriwe, lakini Sekretarieti ya Ajira inasema
3.8. Kwa hiyo, unakuta Vyuo vya Umma vinakosa watu ambao wamewa-train wenyewe na wanawafahamu. Pamoja na kwamba wana GPA hiyo, lakini wanawafahamu kwamba uwezo wao ukoje. Angalau academic staff kama itawezekana Sekretarieti ya Ajira iwaachie basi vyuo waajiri wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ikiwezekana, maprofesa wetu muda wao wa kustaafu uwe angalau miaka 60 ili wapewe mikataba baadaye ya kuendelea. Watu hawa ni watu wazima lakini wana experience kubwa na wameona mengi, siyo rahisi kukosea. Tunawahitaji kwenye vyuo katika uboreshaji wa kupata Watanzania ambao wana ujuzi wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema machache hayo...

SPIKA: Mheshimiwa Kaijage, naona Mheshimiwa Dkt. Paulina Nahato amesimama. Ni taarifa, utaratibu ama nini? Washa kisemeo.

T A A R I F A

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba academic staff ambao wanafundisha, umri wao wa kustaafu ni miaka 65 na sio 60. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kaijage, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, siipokei. Nilikuwa nilikuwa nashauri kama itawezekana, waweze kustaafu at age ya 60, halafu waanze kupewa mikataba kuanzia 60 kwenda juu mpaka watakapochoka wenyewe, kwa sababu ni watu muhimu sana na wana uzoefu na uelewa mkubwa. (Makofi)

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Kaijage ngoja tuliweke vizuri. Kwanza walikuwa wanastaafu miaka 60, Serikali ikapandisha mpaka miaka 65. Sasa kwa mchango wako, unataka Serikali irejeshe 60 halafu iwaachie mpaka huko mbele au ianzie hiyo 65 isogeze mbele?

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ianzie 60 halafu waendelee mpaka watakapo choka wenyewe, kwa mikataba lakini ndio wazo langu.

SPIKA: Ni sawa. Nilitaka tu niliweke sawa ili uwe umemwelewa huyo aliyekuwa anatoa taarifa. Kwa hiyo, endelea na mchango wako.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nianze kwa kumpongeza Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wote ambao Wizara zao ziko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Watendaji na Wajumbe wa Kamati wote wanaohusika na Wizara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri ambayo imekuwa ikifanywa na Serikali, kwa maana ya kupambana na masuala ya HIV/AIDS mahali pa kazi, pia kuna mipango mingi sana ambayo imeendelea kutekelezwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ili kuendelea kupambana na masuala haya sehemu za kazi. Kuna mpango unaoitwa Mpango wa Utatu unaoshughulikia masuala ya HIV/ AIDS mahali pa kazi. Mpango huu umekuwepo toka mwaka 2008. Kwa hiyo, nashauri kama inawezekana, mpango huu ufanyiwe tathmini kwa jinsi ambavyo umefanya kazi kwa nia njema tu ya kuuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna suala zima la zile Kamati za UKIMWI mahali pa kazi pamoja na elimisharika. Naishauri Serikali ifanye usimamizi mzuri, Kamati ziwe active mahali pa kazi. Zitasaidia wale waathirika watoe hali zao za afya yao kwa waajiri wao wawe wawazi wapate huduma, lishe, wapunguziwe majukumu ya kiutendaji mahali pa kazi kama ambavyo Mwongozo wa Utumishi wa Umma Namba 2 wa 2006 unavyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ila suala la saratani ya mlango wa uzazi, linahusiana sana na suala la HIV/AIDS kwa akina mama. Kwa sababu, ugonjwa huu asilimia 70 unasababishwa na mdudu anaitwa Papillomavirus 15 and 16. Pia sababu kubwa sana ya ugonjwa huu au virus hao kuambukiza ni kwa kujamiiana kwa njia ambayo siyo salama kama ambavyo UKIMWI kwa asilimia kubwa unaambukiza. Tumeona katika kituo cha huduma kule Tunduma, wanawake wamefanyiwa vipimo hivi 2900, kati yao 70 wamekutwa na viashiria vya saratani ya mlango wa uzazi na kati yao 43 wamepelekwa kabisa kwa maana ya rufaa kupimwa.

Mheshimiwa Spika, pia pale Mbeya kati ya wagonjwa nane waliopimwa saratani ya mlango wa uzazi ambao ni waathirika na wasio waathirika, sita wamekutwa ni wale waathirika, kabisa wana saratani ya malngo wa uzazi, wawili ndio sio waathirika. Kwa hiyo, unaona jinsi ambavyo hivi vitu vinaoana. Tunashauri Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, hivi vituo vyetu vinavyohusika na masuala ya HIV/AIDS waongezewe sehemu ya kufanyia upembuzi wa saratani. Najua Serikali inafanya sehemu nyingine, lakini pia huku tunawapata wagonjwa mapema. Hawa wamama wakipatikana mapema, tiba yao ikiwa mapema wanapona kabisa.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu Tume ya Udhibiti wa Biashara na Matumizi ya Dawa za Kulevya. Chombo hiki kimeendelea kutoa elimu ya biashara ya dawa za kulevya kama ambavyo inaonekana katika sheria yake Na. 5 ya Mwaka 2015. Naungana na wenzangu wengi ambao wamesema jamani chombo hiki kitengewe fungu la maendeleo. Kwa nini? Kitengo hiki, mbali ya uraibu, hawa sasa hivi wana changamoto kubwa sana ya kupata magonjwa ya afya ya akili yanayotokana na matumizi ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, tumeona pale Gereza la Ruanga, Mbeya, wametenga wodi moja kabisa kwa ajili ya wafungwa na mahabusu ambao wamepata magonjwa ya afya ya akili kutokana na matumizi ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, ninasema waongezewe fungu la maendeleo Na. 2 kwa sababu gani? Wanakuwa na wigo mdogo sana kwa ajili ya huduma ya utengamano wa tiba kwa hawa waraibu. Hii inaathiri sana kasi yao ya matibabu. Pia, nasema watengewe kwa sababu kiliniki za urahibu ambazo ziko mpaka sasa hivi ni chache kutokana na fungu dogo kwenye chombo hiki cha kudhibiti UKIMWI, lakini imeonesha matokeo chanya sana. Kwa sababu hawa waraibu wameimarika, wamekuwa na afya bora na pia wanapata huduma ya magonjwa ambatana, kama vile magonjwa ya UKIMWI, magonjwa mbalimbali ya zinaa na TB. Hawa waraibu ambao wana-attend kliniki ambazo ni chache, haya matatizo yamepungua miongoni mwao.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakushukuru.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage. Kabla hujakaa, Mheshimiwa unajua Kiswahili kigumu; waraibu ni watu gani?

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, waraibu ni wale ambao wameathirika na madawa ya kulevya ambao wako kwenye matibabu ya Methadone. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nami kupata nafasi ya kuchangia Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kwanza kabisa, naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuaminiwa na kupewa dhamana hii kubwa pamoja na Naibu Mawaziri wa Wizara hiyo, watendaji bila kusahau Kamati ya Bunge iliyohusika na Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali bado imeendelea kuwa na vipaumbele vyake katika kuwahudumia Watanzania. Moja ya kipaumbele cha Serikali katika kuwahudumia Watanzania ni kuhakikisha Watanzania wote ikiwezekana wanapata matibabu kwa kutumia mifuko ya bima ya afya hasa wale ambao wako katika sekta ambazo siyo rasmi, kwa maana ya wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara, wajasiriamali wadogo wadogo, bodaboda, mama ntilie na kadhalika, watu hawa ndiyo wako wengi kwenye jamii yetu, makundi haya ni zaidi ya asilimia 85 ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali ikaja na wazo zuri sana katika kuboresha maisha ya Watanzania kwa kuanzisha huu Mfuko wa Bima ya Afya ya Jamii ulioboreshwa. Mfuko huu umekuja kwa nia njema sana, una muundo mzuri, una watendaji na wasimamizi kuanzia ngazi ya mkoa mpaka ngazi ya kijiji na mtaa. Nia ya mfuko huu ilikuwa kuhakikisha wanachama wote hawa wanapatiwa huduma za msingi za jamii kwa maana ya kupata ushauri wa daktari, kupima vipimo maabara, kupata dawa zile za msingi kwenye ngazi husika kama ni zahanati, kituo cha afya, hospitali ya wilaya na mkoa tunaita essential drugs katika kituo husika, pia huduma ya mama na mtoto. Pia kutokana na kituo cha huduma ya afya kwa mfano kwenye zahanati atapata mapumziko, kwenye kituo cha afya atalazwa na upasuaji mdogo, kwenye hospitali ya wilaya atapata upasuaji mkubwa na mdogo pia ila kwenye hospitali ya mkoa atapata vyote pamoja na huduma zote za rufaa ambazo zimethibitishwa katika huduma za mfuko huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto katika kupita kwetu, watanisaidia Waheshimiwa Wabunge; kwenye kampeni zetu kule vijijini akitokea mtu kuchangia suala la afya, kama hajachangia changamoto za mfuko huu; na akichangia changamoto za mfuko huu anapokewa na wanachama wote au Wajumbe wote kwenye Mkutano husika, kuona jinsi ambavyo changamoto ni kubwa. Wanasema, Mheshimiwa uliyesimama hapo tunakuheshimu, kama wanakuheshimu watakwambia hivyo. Mimi nakwenda hospitali nakosa hata Paracetamol japo ya kunishusha homa nikajipange kutafuta fedha kununua hiyo dawa ambayo haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, changamoto ni kwamba wale wale wanachama wetu wa mfuko huu ndio wamekuwa wahamasishaji wakubwa wa kuwatangazia wenzao wasijiunge na mfuko huu, lakini siyo kosa lao ni kwa sababu ya upungufu uliopo kwenye huduma zinazopatikana kwenye mfuko huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine, unapokwenda kwenye kituo cha afya, unajaziwa Form C2, inaitwa kwenda kutafuta dawa kwenye pharmacy nyingine, pale imekosekana. Kuna tatizo; ukiangalia ile form yao, ile dawa inaweza ikawa labda ni ya shilingi 5,000, lakini ukienda kwenye pharmacy nyingine ambayo zimesajiliwa anakujazia form, lakini ile dawa anaandika shilingi 15,000.

Kwa hiyo, mfuko utaendelea kupwaya kwa sababu utawanufaidisha watu wengine. Kwa hiyo, iundwe mamlaka ya kudhibiti na kusimamia suala la madawa kwenye mfuko huu, tunapigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine, uhamasishaji wa wananchi kujiunga na mfuko huu, sasa uendane na upatikanaji wa huduma ambazo nimezitaja, kwa sababu hatuwezi kupata nguvu sisi wanasiasa na vyombo husika kwenye ngazi husika kuwashauri watu wajiunge, wakati tukisema kiukweli, hizi huduma hazipatikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tunajua Serikali inaendelea kuchangia sawa sawa na wanachama wanaochangia pamoja na wadau, wanaita tele kwa tele. Kwa hiyo, ina maana fedha ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niieleze Serikali, katika muundo uliowekwa ambao ni mzuri tu, kutoka ngazi ya mkoa mpaka Kijiji, wajiwekee malengo angalu ya miezi miezi mitatu mitatu tu, halafu wajifanyie tathmini. Hii itaongeza uwajibikaji na commitment. Kwa hiyo, huu mfuko badala ya kuwa wa hasara na watu kuvunjika moyo, utawasaidia kama ilivyokuwa lengo la kwanza la Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushauri hivyo, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Naomba nianze kwa kuunga mkono hoja. Pia namshukuru sana Mwenyezi Mungu kupata nafasi ya kuchangia bajeti hii muhimu sana katika uongozi huu wa Awamu ya Sita na pia katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ikiwa ni bajeti ya kwanza ya miaka mitano 2021/2022 na 2025/ 2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kumpongeza mama yetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu. Tunamwangalia kiongozi siyo katika maono tu na katika level ya usikivu, huyu mama ni msikivu pamoja na Serikali yake yote wamekuja na bajeti ambayo imejibu matamanio mengi makubwa ya Watanzania, pia imejibu hoja mbalimbali ambazo kwa umoja wetu Wabunge tumekuwa tukichangia na tukiishauri Serikali katika Wizara zote ambazo tumechangia, imejibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuipongeza pia Wizara yote, Waziri wetu, Naibu Waziri, Kamati pamoja na Watendaji wa Wizara hii kwa umakini mkubwa kutetea bajeti hii njema. Napongeza vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo vimetufanya kuendelea kuwa na amani mpaka tumefanya mambo yote haya kwa utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali yetu kuendelea kutambua na kuthamini mchango muhimu sana wa watumishi katika kuchangia pato la Taifa. Tumeona jinsi ambavyo Serikali imejibu kwa ujumla wake, kwa mwavuli wake kuhusu maslahi ya wafanyakazi. Sitachambua moja moja, yapo dhahiri kwenye bajeti na wenzangu wameyachangia, lakini kuna suala zima la utengaji wa karibu shilingi bilioni 449 kwa ajili ya upandashaji wa madaraja. Ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali, katika upandishaji wa madaraja haya; natoa mfano, unakuta kuna kada moja ya taaluma na level sawa ya elimu, lakini unakuta mmoja ameajiriwa mwaka 2014 mwingine 2020 lakini wamekuja kupandishwa daraja pamoja 2020, wanakuwa level moja ya daraja. Hii inavunja morali kwa kwa yule aliyetangulia. Kwa hiyo, naomba nishauri, mnapopandisha madaraja kwa hizi bilioni zilizotengwa, karibia watumishi 92,000 wameshahakikiwa, lakini suala la seniority tulizingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo Halmashauri zisizopungua 184 na tafiti zinaonesha karibia asilimia 80, Halmashauri zetu tunategemea ruzuku ya Serikali Kuu. Hata hivyo, naomba niipongeze Wizara ya Fedha na Mipango, mwaka 2018 mlikuja na miongozo ya uandaaji wa miradi ya kimkakati katika Halmashauri zetu ili kujijenga kimapato na baada ya kujijenga kimapato Halmashauri zetu ziweze kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi wetu kule kwenye grassroot. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa napongeza kwamba katika miradi ya kimkakati yote iliyowekwa, miradi sita imekamilika, miradi 32 bado ipo kwenye hatua ya ukamilishaji. Hata hivyo, tafiti zinaonesha miradi hii ya kimkakati ina changamoto nyingi sana. Mojawapo ni changamoto za kiutendaji ambayo ni pamoja na ukosefu wa wataalam wa kuandika yale maandiko. Ukosefu wa hatimiliki za ardhi na changamoto za kimuundo nyingine na kitaaluma na taasisi, ni ukosefu wa watalaam husika wa kusimamia miradi ile kwa maana ya ma-engineer na wazabuni na vitu vya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwamba imeendelea kuajiri walimu na watumishi wa afya, tunashukuru sana. Naomba nishauri, kada nyingine nazo mziajiri kwa sababu nia njema ya dhima ya bajeti hii ya kujenga uchumi na viwanda kwa maendeleo ya watu, ni kule kwenye watu chini kwenye Halmashauri. Nia yenu njema ya kuja na mikakati hiyo ya kuboresha na kujenga kimapato Halmashauri zetu, changamoto hizi tuziangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri wadau wanaohusika na utekelezaji wa miradi hii ya kimkakati mkiwemo ninyi Wizara ya Fedha na Mipango, ikiwepo TAMISEMI, Sekretariati za Mikoa na Halmashauri, mkae kwa Pamoja. Kuna vigezo vimewekwa ambavyo siyo rafiki na siyo halisia na uwezo wa baadhi ya Halmashauri. Nia ni njema, lakini nashauri mkae mziangalie tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza Serikali imekuja na mpango mzuri sana wa afya kwa wote, nia na makusudi ni kwamba kaya zisizopungua 12,000 zipate bima ya afya, lakini pia katika hizo kaya 12,000 asilimia 20 ndiyo kaya za watu ambao hawana uwezo kabisa na Serikali inasema kila mwaka itakuwa inatakiwa ipate zaidi ya shilingi bilioni 140 na kila mwaka ili angalau katika miaka hii ambayo lengo lake ni katika 2034/2035 kila Mtanzania awe amefikiwa na Mfuko wa Bima ya Afya, yaani kila mwaka iwe inapata zaidi ya shilingi bilioni 149. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna changamoto ya mfuko huu, lazima uwe unapata michango kutoka sekta binafsi, sekta zisizo rasmi na sekta rasmi, najua changamoto ipo kwenye sekta ambazo siyo rasmi. Kwa hiyo, naishauri Serikali itafute mbinu nzuri sana za kuhakikisha kwamba sekta zisizo rasmi zinashiriki kikamilifu katika kuchangia mfuko huu ambao una nia njema sana ya kwamba kila Mtanzania apate bima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie. Nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kuendeleza mapambano dhidi ya matatizo haya makubwa na ambayo ni mtambuka, masuala ya UKIMWI, kifua kikuu, dawa za kulevya na magonjwa yasiyoambukizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba magonjwa yasiyo ya kuambukiza ni magonjwa yale ambayo tunasema hayana vimelea vinavyosambazwa. Hata hivyo, tafiti zinaonesha kabisa kwamba magonjwa yasiyo ya kuambizwa limekuwa ni tatizo kubwa sana na bahati mbaya niseme kwamba the latest study ni ya mwaka 2016 ambayo imekuwa-reported na Shirika la Afya Duniani (WHO), inasema katika vifo 43 vya mwaka 2016 asilimia 71 vilikuwa ni vya magonjwa yasiyo ya kuambukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna study nyingine zinazoendelea duniani, zinasema kufikia mwaka 2050 kutakuwa kuna ongezeko kubwa sana la wazee, wanamaanisha kuanzia miaka 65 kwenye study yao. Wanasema asilimia 68 ya wazee hao itakuwa Afrika, Tanzania ikiwa mojawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni suala lisilopingika kwamba magonjwa yasiyoambukiza kweli sasa hivi yanayakuta makundi yote, lakini asilimia kubwa ni wazee na ni magonjwa yanayochukua muda mrefu na tiba yake takriban ni ya kila siku, ni magonjwa ya kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hili ili kuonesha ukubwa wa tatizo. Kwa hivyo naungana na wenzangu waliotangulia, lakini labda niwe specific zaidi. Niseme, Wizara ya Afya inafanya kazi nzuri sana katika kupambana na janga hili, lakini ifikie mahali sasa, kwa sababu magonjwa haya kwa asilimia zote ni magonjwa yanayozuilika, ni kwamba watu tu hawana uelewa. Hata tunapokaa sisi hutakiwi kukaa zaidi ya saa moja, lazima uinuke utembee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna alimu kubwa ambayo jamii haiifahamu. Kwa hiyo utaona msingi wa matatizo haya ni sehemu ya kuzuia (prevention). Tungeiachia Wizara ifanye suala la tiba, lakini suala la prevention, kama tulivyoshauriana liwekwe chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na liundiwe tume. Kwanza tukishazuia pia tutapunguza burden kwa Serikali na kwa Wizara. Kwa hiyo tume hii ikiundwa, au chombo hiki kikiundwa, kwanza hawa watu watakuwa dedicated na watakuwa answerable na wataweza kusimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo sheria nyingi sana, tumezipata humu humu ndani, sheria zisizopungua 60 ambazo zinasaidia kuzuia magonjwa ya kuambukiza. Hata hivyo, sheria zile ni nani anazisimamia? Wizara imeelemewa. Kuna miongozo imewekwa, hata hivi siku za karibuni umetoka mwongozo, umeshaenda kwenye halmashauri zetu zote, lakini, ni nani anazisimamia? Wizara imeelemewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, suala la prevention ya magonjwa yasiyoambukiza na ambayo ndio msingi wa kuzuia magonjwa haya, hebu tuangalie namna ya kulifanya. Wawe watu ambao watakuwa very dedicated, watakuwa na mipango na watatupa taarifa.

Nashauri hivyo, kwamba sasa ifikie mahali tutambue ukubwa tatizo hili, tuishauri Serikali iangalie utaratibu wa kupambana, kwa maana ya kuzuia. Kwa sababu tukizuia, ukitoa elimu, kwa sababu ukishaunda chombo cha kuzuia kitatoa elimu kwa wakati, kitakuwa kina bajeti na kitafanya mambo yote. Ukishazuia na ukishatoa elimu ina maana hakuna matokeo ya ugonjwa kwa ukubwa wake.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja.

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa, hitimisha kwa dakika moja.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba pia nishauri kuhusu kuongeza bajeti kwa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya. Huku tunaona operations zao ni nyeti, wanahitaji vyombo muhimu vya maabara, watu wanao-graduate kwenye methadone wanahitaji pia wapate study za kazi; mambo ni mengi sana kwenye mamlaka hii.

Kwa hiyo nazidi kushauri, kama nilivyoshauri mara ya kwanza, hebu tuanglie bajeti ya hawa watu ili kuwawezesha waweze kufanya kazi kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Namshukuru Mwenyezi Mungu na naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuipongeza Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri; na Mheshimiwa Deo Ndejembi, Naibu Waziri, kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kushughulikia masuala yote ya maslahi kwa ujumla ya wafanyakazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi hiki cha mwaka mmoja na miezi kadhaa tumeona kuna changamoto kubwa ya wafanyakazi na ajira, lakini tumeona takribani watumishi 180,000 wamepandishwa vyeo na kubadilishwa kada, lakini suala zima la madai pamoja na malimbikizo ya mishahara pia Serikali imeendelea kuhakiki pamoja na kulipa. So far mpaka sasa hivi watumishi takribani 37,000 wamelipwa madai yao na malimbikizo jumla ya shilingi trilioni 65 zimetumika, kwa hiyo tumeona nia thabiti ya Serikali kuendelea kushughulikia maslahi ya wafanyakazi, tunawapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala zima la uhuishaji wa miundo ya maendeleo ya utumishi wa wafanyakazi. Hili suala nimekuwa nikilisema sana kwenye michango yangu, lakini sasa hivi kumekuwa na uhuishwaji wa miundo ya watumishi takribani 22 kwenye Wizara na 47 kwenye Wakala wa Serikali na Mashirika ya Umma. Kwa hiyo, tunaipongeza Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala zima la kutoa vibali. So far wametoa vibali karibu mia tisa kwa ajili ya kutoa ajira kwa nafasi zilizokuwa wazi, pia wametoa vibali karibu mia tano kwa ajili ya nafasi za uongozi, pia wametoa vibali 550 kwa ajili ya ajira ambazo sio za mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wameshughulikia miundo mbalimbali, kwenye utumishi wa umma kuna miundo mingi, lakini sasa hivi kuna muundo mpya umetoka unasimamia utendaji wa kazi na upimaji wa Mtumishi.

Muundo huu utakuwa na tija sana kwa sababu mtumishi atapimwa, atajiandalia kazi zake na mwisho atapimwa kutokana na kazi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundo iko mingi lakini kuna suala zima pamoja na pongezi nilizozitoa kuna suala ambalo limekuwa kero ambalo wenzangu pia wamelisemea ni kukaimu kwa muda mrefu. Watumishi wanakaimu kwa muda mrefu, naishauri Serikali sasa inaweza kuandaa kanzidata ili kupata uelewa wa watumishi ambao wana mwelekeo wa uwezo wa kupata hizi nafasi. Kwa hiyo, kuwe na mkakati maalum wa kuandaa hili jambo, limekuwa ni kero kubwa kwa watumishi. Watumishi wamefanya kazi kwa bidii wana uwezo, sasa ifikie sehemu wapate kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la watumishi Serikali imejitahidi kuajiri sasa, lakini bado kuna changamoto. Naishauri Serikali kama inawezekana kuanzia halmashauri zenye uwezo basi itoe vibali waajiri angalau kwa muda kwenye shule zetu na zahanati zetu, lakini zinapotoka ajira rasmi wale watu walioajiriwa kwa vibali hivi vya muda wapewe kipaumbele ya kuajiriwa kwenye ajira zitakazotoka. Hii itasaidia kuleta huduma njema ambayo sasa hivi inakosekana, japo tumepata hospitali na madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi ya kuchangia katika hotuba hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa kibali pia cha kusimama, nampongeza sana Mama Samia Suluhu Hassan na Serikali yake yote kwa jinsi ambavyo wanaendelea kufanya kazi kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, magonjwa yasiyoambukiza ni magonjwa mengi na mengi yao yanazuilika, machache ni ya kurithi lakini ndiyo maana tumeendelea kuishauri Serikali katika Sheria zisizopungua 62 ambazo zimepitishwa na Bunge hili, nyingi sana kwa njia moja au nyingine zinahusika katika masuala mazima ya kuzuia magonjwa haya yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, tunaomba Serikali izipitie na kuziboresha sheria hizi ili ziendane na mapambano dhidi ya kuzuia magonjwa ya kuambukiza ambayo hakika mengi yanazuilika. Sheria hizi ni kama moja apo Sheria ya Tumbaku, Sheria ya Bima ya Vyombo vya Moto vya Barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ajali za barabarani zinatokana na vyombo vya moto ni mojawapo ya magonjwa yasiyoambukiza, tatizo hili limekuwa tatizo kubwa sana. Nimeona nizungumzie hili kwa sababu lina kuja kwa kasi kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri kwamba Serikali ije na mpango wa uhakika sana wa kuhakikisha inapunguza madhara inayotokana na vyombo vya ajali barabarani. Kama inawezekana Serikali iunde Mfuko wa Ajali za Barabarani tunaita (Road Accident Fund) huu mfuko utasaidia kwanza kupunguza gharama kuwagharamia wale watu wanaopata madhara ya hizi ajali za barabarani ambao ni mojawapo wa ugonjwa usioambukiza, lakini pia mfuko huu utasaidia vituo vyetu vya afya viwahudumie hawa waathirika au waliopata madhara ya ajali kwa haraka kwa upesi bila kujali kabisa rasilimali fedha, yaani huu mfuko utasaida akipata ajali tu paa! akienda kituo cha afya atahudumiwa bila kungoja kwanza malipo ya rasilimali fedha. Kwa hiyo, mfuko huu utasaidia sana kuokoa maisha ya ndugu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninashauri uboreshwe kwamba wahanga wanaotokana na ajali hizi wawe wanalipwa kutokana na bima ya chombo kile kilichosababisha ajali. Kwa sababu sasa hivi ni mpaka dereva ashitakiwe ahukumiwe aonekane anahatia ndiyo yule muhanga wa ajali alipwe fidia au wale wafiwa walipwe fidia.

Mimi nashauri iboreshwe hii bima kuna Sheria ya Bima ya Vyombo vya Moto iboreshwe kwamba, wahanga walipwe siyo kwa kuzingatia mashtaka au ya dereva kuhukumiwa hapana! As long as chombo kimethibitika ndiyo kilisababisha ile ajali au kile kifo basi sheria iboreshwe kwamba wawe wanalipwa kutokana na ile bima ya kile chombo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hii sheria iboreshwe kwa sababu ni sheria mojawapo ambayo inahusika na magonjwa yasiyoambukiza ambayo ni ajali imezidi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni masuala ya magonjwa yanayohusika na masuala ya UKIMWI. Ni suala lisilopingika kwamba asilimia 90 ya mapambano au madawa Afua zote za kupambana na UKIMWI tunategemea wafadhili, ni suala lisilopingika kwamba viwanda katika nchi au maboresho ya viwanda katika nchi ni mojawapo ya mustakabali wa kuboresha maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivyo? Kulikuwa na kiwanda Arusha cha kutengeneza dawa za kuzuia makali ya virus vya UKIMWI mwilini, kiwanda hicho kilikuwa kimepewa ufadhili mkubwa wa European Union wakatengeneza mitambo ya kisasa kweli kweli, lakini kiwanda hiki kimekufa. Ninaishauri Serikali kupitia MSD wakifufue kile kiwanda, Msajili wa Hazina na asilimia 40 wale Wawekezaji walikuwa na asilimia 60 sasa MSD kwa maana ya Serikali ilinunua asilimia 60 ya kiwanda kile. Kwa nini nasema hivyo? Dawa, matibabu kwa mwananchi ni suala la usalama. Hatuwezi kutegemea kila siku matibabu ya mwananchi wako yatoke nje ya nchi. Huwezi kujua mtu anawaza nini, kuna vita kuna kila kitu!

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi leo kuna vita mtu atakazana kutengeneza dawa akuletee wewe, aache kupambana na vita yake? Kwa nini tusiwekeze kwenye viwanda vyetu hapa nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tusiwekeze kwenye viwanda vyetu hapa nchini? MSD kwa miaka miwili sasa hivi kwenye ile Keko Pharmaceutical Industries walianza kutengeneza dawa moja tu ya paracetamol, na sasa hivi wana products kumi, vilevile wale wale wametengeneza barakoa. Mwananchi wa kawaida alikuwa hawezi kununua barakoa, lakini sasa hivi tumetengeneza barakoa pale Dar es Salaam, tuna kiwanda. MSD pia imetengeneza kiwanda cha gloves kule Mufindi kwenye baridi, maana ndiyo mazingira yanayotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo bado tuna uwezo wa kufanya vitu vyetu. Suala la dawa ni usalama, usalama kabisa kwa wananchi ambao unawaongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la dawa za kulevya. Haya ni mapambano ambayo ni nyeti sana. Wenzetu wanatumia vyombo vya kisasa ambavyo ni sophisticated kama vile boti na mitambo mbalimblai. Sasa nishauri tena kwa mara ya tatu, hii mamlaka itengewe fungu la maendeleo ili waweze kununua vifaa vya kisasa, pamoja na kujenga vituo ambavyo waraibu wakishahitimu wanaenda kufundishwa stadi kazi ili wasirudi tena kwenye dawa za kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii mamlaka sitoiongelea sana; kila siku naongea, kwamba waongezewe fungu la maendeleo, waongezewe fungu la pesa kwa kuwa kazi yao ni ngumu na ni ya kishawishi sana. Sijasema waongezewe mafao binafsi, waongezewe mazingira ya kufanya kazi, waongezewe wafanyakazi, kwa sababu wana upungufu wa wafanyakazi zaidi ya 189. Kazi yao ni ngumu. MACH clinic zao ziko chake. Kwa mfano Kanda ya Ziwa yote ina MACH clinic moja tu ambayo iko Mwanza. Ile dawa wanakunywa kila siku, hivyo haiwezekani utoke Ukerewe uje Mwanza leo asubuhi halafu kesho urudi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo nashauri tena kwa mara ya tatu katika michango yangu. Mamlaka ya Kudhibiti Dawa za Kulevya itengewe fungu, iongezewe fedha kwa kuwa kazi yake ni nyeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu Workers Compensation Fund. Nimeiona imeelezwa vizuri; lakini nilikuwa nashauri, lengo lisiwe tu kutoa fidia au ufanisi uwe tu kwa sababu umetoa fidia, hapana. Lengo liwe ni kuwekeza maeneo ambayo yatasaidia kupunguza ajali maeneo ya kazi; siyo mafanikio ni kufidia, hapana. Lakini pia nilikuwa nashauri, ikiwezekana mitaala ya medical schools zote iwe inajumuisha masuala ya ulemavu utokanao na ajali na magonjwa mahala pa kazi. Mitaala ya medical schools ihusishe masuala yote ya tathmini ya ulemavu unaotokana na ajala na magonjwa mahala pa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho kabisa ni suala la wenzetu OSHA. Nipongeze kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya ya kuhakikisha usalama wa nguvukazi mahala pa kazi. Hata hivyo, nilikuwa naishauri Serikali, kwamba, ije na sheria, kama ikiwezekana, ambayo itawezesha kuajiri either part-time or fulltime watu wote wanaohusika na masuala ya OSHA mahala pa kazi ili kuhakikisha usalama wa nguvukaziwatu mahala pa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache naunga mkono hoja, ahsante.(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahante sana, na mimi namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya, lakini pia naungana na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ya kulitumikia Taifa letu la Tanzania. Pia nampongeza Waziri Mkuu pamoja na timu ya mawaziri katika Sekta ile pamoja na watendaji kwa kazi nzuri wanayofanya kwa Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachangia fungu 65, ilani ya Chama Cha Mapinduzi Ibara ya 168 imeendelea kutambua mchango muhimu sana wa wafanya kazi na vyama vya wafanyakazi na waajiri kwenye uchumi wa nchi yetu. Si hivyo tu, hata kwenye hotuba ya Waziri Mkuu ukurasa wa 65 pia imeeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hayo, haina ubishi kabisa kwamba vyama vya wafanyakazi ndivyo vinavyohusika kuwaunganisha na kuleta harmony kati ya waajiri na wafanya kazi. Kupitia mabaraza yao wanajadili mambo mbalimbali ambayo yanawagusa na ambayo yanawasumbua sana wafanyakazi; lakini pia ndiyo forum sahihi. Hatutegemei wafanyakazi wakose vikao waende kwenye waandishi wa habari na kwenye platforms za siasa zinaendelea sasa hivi kueleza mambo yao; wana mabaraza yao kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nazungumzia hayo? Fungu 65 ndipo mahala sahihi kuhusiana na mambo ya vyama vya wafanyakazi na wafanyakazi. Nashauri, watakapokuja watueleze, kwenye Fungu 65 mpaka sasa, kitengo cha wafanyakazi na vyama vya wafanyakazi kumefanyika nini na bajeti ijayo wanampango gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema kwa sababu idara ina Idara ya Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi ambaye ndiye anayehusika kwenda kufuatilia masuala mbalimbali na utendaji wa vyama vya wafanyakazi kule pembezoni mikoani ambako kuna matawi ya wafanyakazi. Kwamba wanaendeshaje mambo yao kutokana na utaratibu na kanuni walizojiwekea. Kama Idara hii ya Msajiri wa Vyama vya Wafanyakazi itakuwa haina baketi itakwendaje kufanya shughuli hizo? Lazima tusikilize matataizo yao na tumuwezeshe Msajiri aende akafuatilie kwenye mikoa na pembezoni, kule ambako kuna matawi ya vyama vya wafanyakazi, akaangalie wanavyofanya kazi zao kulingana na taratibu walizojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la wakala wa huduma za ajira nchini (TaESA). Hili baraza linahusika na kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri. Nipongeze sana Serikali, sasa hivi kupitia ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora imeshirikiana sasa hivi na Ofisi ya Waziri Mkuu kuanzisha Mfumo wa Taifa wa Kusimamia Ajira. Hii itasaidia kwa sababu mfumo huu utakuwa na taarifa za nafasi za kazi zote nchini na utakuwa na takwimu kamili za soko la ajira nchini. Kwa hivyo nipongeze Serikali kujua kwamba kuna umuhimu wa wao kuungana na Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi. Katika muunganiko huo TaESA inahusika na suala la usimamizi wa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ukoje hapo? Kwamba hii TaESA ijulikane, TaESA iongezewe nguvu. Kama alivyosema mjumbe mwenzangu, kwenye Skill Development Leavy kwenye SDL iongezewe bajeti. Hii TaESA inahusika kutafuta ajira, inahusika kuwapeleka vijana kwenye mazoezi ya vitendo, lakini bajeti yake ni ndogo na pia haijulikani na haitoki. Watoto hawaifahamu na hata wazazi hawaifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nipongeze kwamba sasa kuna ushirikiano kati ya ofisi ya utumishi na ajira lakini sasa TaESA Ifanye kazi iende ikatafute hizi nafasi, iende mikoani,
kwenye viwanda ikae na waajiri, itapata hizi nafasi kwa hiyo itasaidia kupata nafasi kwa ajili ya wananchi wetu.

Kuna Baraza la Uchumi, na hili baraza liko kwa mujibu wa Sheria. Tunabaraza lingine kwenye hii ofisi linaitwa LESCO, hili linaitwa Baraza la Uchumi na Jamii. Baraza hili linaishauri Serikali kupitia Ofisi ya Waziri wa Kazi, inamshauri Waziri wa Kazi juu ya mambo mablimbali ikiwepo Sera ya Taifa ya Soko la Ajira, njia tofauti mbalimbali za kupunguza ukosefu wa ajira pamoja na pia kutoa takwimu za usimamizi wa sheria ya ajira nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabaraza yote yapo kwenye ofisi, hatusikii kazi zake hatuoni ripoti yake tunakazana kutafuta ajira za vijana. Kama kuna mabaraza yapo kwa mujibu wa sheria yawezeshwe; kama ni bajeti ya ESDL iongezwe ili haya mabaraza kwa kusaidiana na juhudi mbalimbali za Rais mpaka analeta mashamba vijana walime basi hayo mabaraza yawe active, yaongezewe bajeti yatoke yajulikane yafanye kazi inayotakiwa kufanywa. Wanapokuja watuambie hayo mabaraza yamefanya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nipongeze Serikali kwa kuja na ongezeko la Mshahara wa kima cha chini hasa kwa sekta binafsi. Sensa ya mwaka jana imeonesha kabisa kuwa sekta binafsi ndiyo inayoongeza kuwa na watumishi wengi sana. Sheria ya Kazi inaonesha kwamba Bodi ya Ajira Sekta Binafsi inatakiwa iongezewe bajeti ili tunapopandisha safari hii iwe ndio mwanzo wa mchakato kwa sababu upandishaji wa kima cha chini umechelewa sana. Iwezeshwe, ianze mchakato mapema kwa sababu maisha kila mwaka yanabadilika, kwa hiyo ni lazima kima cha chini kipande kila mwaka. Kwa hiyo Bodi hii iwezeshwe, iongezewe bajeti ili ianze mapema mchakato wa kufatilia kima cha chini hasa cha watu wa sekta binafsi ndio wengi katika utumishi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada hayo nasema naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu. Pia, naendelea kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kujali huu utumishi wa Umma, maana mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Tumeona jinsi ambavyo Serikali imeendelea – japo kuwa ana keki ndogo – lakini imeendelea kujali utumishi wa Umma ukilinganisha na ambavyo ilikuwa hapo nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze pia Mawaziri wetu, Mheshimiwa Simbachawene, pamoja na Mheshimiwa Ridhiwani. Nampongeza pia Mheshimiwa Jenista Mhagama, wakati tunajadili bajeti yetu hiii tulishirikiana naye vizuri kwa sababu wakati huo yeye ndio alikuwa Waziri wa Wizara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Wizara imeendelea kufanya kazi zake ambazo ni za msingi kwa maana ya kusimamia utumishi wa Umma, utendaji kazi bora, pia kuhakikisha stahiki za wafanyakazi zinasimamiwa sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hii ni Wizara ambayo ina- deal na rasilimali watu, rasilimali watu ukiisimamia vizuri ndiyo inaweza kusimamia rasilimali nyingine; rasilimali ardhi, madini, maji n.k. Na haya malalamiko yote ambayo tunayaona, kama kuna usimamizi mzuri wa rasilimali watu hatutakuja kuyaona. Ubadhirifu hatutakuja kuuona. Kwa hiyo, ni muhimu sana kusimamia rasilimali watu, kwa hiyo Wizara hii inafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivyo; nikienda kwenye Fungu 32. Fungu hili limekuja na mifumo mingi, mifumo hii ndiyo kwanza inaanza, kuna mfumo ambao tunauita wa Utendaji Kazi katika Utumishi wa Umma. Mfumo huu ni kama ule ambao ulikuwa OPRAS siku za nyuma. Ule ulikuwa unaamua, mnakaa watumishi mnajikusanya mnajijazia. Na mwajiri anakuwa anakutazama unafananaje anakujazia. Lakini sasa hivi kuna mfumo huu umekuja unasimamia utendaji kazi wa utumishi wa Umma na mwingine unasimamia utendaji kazi wa taasisi za Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu mpaka sasa hivi umefanya majaribio kwenye taasisi 11 za Umma na umefanya kazi nzuri sana. Na sasa hivi mfumo huu utakuwa unaangalia ubora na wingi (workload). Kwa hiyo, automatically inakwenda kwenye mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakati unamjazia mtumishi utapunguza upendeleo na unyanyasaji, whether unampenda au humpendi lakini zile grades zimekuja kwenye mfumo. Kwa hiyo, hii itatoa moyo kwa watumishi sasa hivi, watakuwa na ari. Kwa hiyo, itakuwa na usimamizi mzuri na wafanyakazi watafanya kazi kwa moyo na hakutakuwa na uonevu kama ambavyo nimesema.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri mifumo hii ndiyo kwanza inaanza, ina nia njema, naomba mamlaka mtandao iongezewe bajeti kuwe na fedha za kutosha kuhakikisha usimamizi wa mfumo huu. Ni mwema, lakini kama hautasimamiwa vizuri, hautakuwa na ulinzi, ina maana ile tija haitaonekana; ndiyo ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mfumo mwingine unaitwa wa Taarifa za Utumishi na Mishahara. Mfumo huu ni mzuri sana kwa sababu tunakumbuka zamani, mchakato wa mshahara ulikuwa unachukua hata siku 14, lakini sasa hivi mchakato wa mshahara siku moja tu umesambaa kote, umefika kwa siku moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unaweza kuona mifumo hii ina nia njema ya kuboresha maslahi ya watumishi ili wafanye kazi kwa bidi ili kulinda utumishi katika sehemu nyingine mbalimbali, kutoa tija. Ukimpa mtumishi mshahara wake kwa wakati unamtia morali, unamtia moyo, anafanya kazi kwa ufanisi. Kwa hiyo, mifumo hii tusiidharau. Nimeijadili kwa sababu imeanza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mfumo mpaka sasa hivi umeshaunganishwa kwenye taasisi 433 kati ya taasisi 522 tulizonazo kwenye utumishi wa Umma. Kwa hiyo, unaweza ukaona jinsi ambavyo Serikali inakazana. Nashauri kwamba mifumo hii isimamiwe kwa udhibiti mkubwa sana na pesa ziongezwe, iimarishwe, isambazwe kote. Huu mfumo pia, kwa mfano…

TAARIFA

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa anayechangia. Hapo awali tulishauri Bunge hili kwa habari ya kuondokana na Mfumo wa OPRAS, na Serikali sikivu ya Awamu ya Sita ilisikia, ikaenda kwenye mifumo hii mipya, PEPMIS na iLMIS ambayo kimsingi imeanza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kumuunga mkono mzungumzaji, anazungumza jambo jema sana kwa Taifa letu. Ninashauri ni muhimu sasa Wizara ya Utumishi ianzishe kitengo maalum kitakachoratibu uendeshaji wa mifumo hii nchi nzima. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kaijage, taarifa.

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kueleza jinsi ambavyo Mfumo huu wa Taarifa za Utumishi na Mishahara unavyofanya kazi vizuri. Sasa hivi ulivyoanza kufanya kazi kwenye taasisi hizi ambazo zimeshaunganishwa ukifika umri wako wa kustaafu automatically mfumo huu unatoa jina lako kwenye mshahara, unalihamishia kwenye mifuko ya pensheni. Kwa hiyo, itapunguza zile taratibu za mtu kuendelea kulipwa mshahara wakati alishatoka kwenye umri wa kustahili mshahara, na itapunguza udanganyaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu umeunganishwa na taasisi mbalimbali; NIDA, RITA na mifuko mingine ya hifadhi ya jamii. Kwa hiyo, umeanza sasa hivi, tutaona baadaye effect yake. Sasa hivi ukifika muda wako wa kustaafu, umri wa kustaafu, kwa sababu RITA imeunganishwa na mfumo huu, automatically jina lako linahama, hupati tena mshahara, linahamia kwenye pensheni kwa hiyo, nipongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuomba kwamba mifumo hii iwezeshwe ili iweze kufanya kazi kwa tija na izalishe vizuri na watu waweze kuona umuhimu wake na hivyo, watumishi wakifanya kazi wawe wanajua kwamba mwisho wa siku watakuwa na utulivu na watakuwa hawana wasiwasi juu ya mafao yao na stahiki zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mfumo mwingine unaoitwa wa Tathmini ya Mahitaji ya Watumishi wa Umma. Sasa huu ni mfumo muhimu sana kwa sababu ndiyo ambao utakuwa unaonesha watumishi wako wangapi, wako sehemu gani, kuna upungufu wa watumishi kiasi gani, kuna wingi wa watumishi kiasi gani. Kwa hiyo, utakuwa unarahisisha Serikali kufahamu kwamba yamkini vituo viko sawa, vina level sawa, kwa mfano labda vya hospitali, kituo fulani kinahitaji watumishi 500, kingine watumishi 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukija kuangalia kwenye workload na idadi ya mtu ambaye ameona mgonjwa unagundua kwamba katika kituo fulani, japo kinafanana na kingine, lakini wana madaktari 50, wengine wana 100 lakini hawa wana wagonjwa wachache, kwa hiyo, kutakuwa kuna urahisi wa kuhamisha watumishi kutoka sehemu fulani kwenda sehemu nyingine kulingana na jinsi ambavyo mfumo unaonesha idadi, uwezo na ubora na workload anayotumia yule mtu kutibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mfumo huu utapunguza malalamiko mengi ambayo Wabunge wengi wamechangia. Unakuta sehemu fulani kuna watumishi wengi, sehemu nyingine kuna watumishi wachache lakini vituo vinafanana. Lakini ukiangalia katika uhaliasia workload aliyonayo mtumishi mmoja na yule mwingine ni tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mfumo huu ni mzuri sana, utabaini idadi ya uhalisia wa uhitaji wa wafanyakazi, utakuwa bayana. Nimeona niseme hivi vitu; nimeshazungumzia mambo mengi kuhusu wafanyakazi na kuwatetea, lakini naomba niwaoneshe, kwa sababu niko kwenye Kamati hii, mambo yanayokuja mbeleni yatakuwa mazuri. Ila tunachokiomba; Serikali iongeze bajeti ya e- Government ili mifumo hii isimamiwe vizuri iweze kuwa na tija baadaye. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nampongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kuendelea kujali kabisa tasnia hii ya Afya, lakini nimpongeze Mheshimiwa Waziri Ummy pamoja na Naibu Waziri Mollel pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kazi nzuri njema wanayoendelea kufanya. Kwa kipekee sana niwapongeze watoa huduma wote wa afya Tanzania kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nianze kwa kuunga mkono hoja asilimia 100. Mnamo Tarehe 05 Februari, 2021 nilisimama katika Bunge lako Tukufu kuzungumzia suala zima la Hospitali ya Mirembe. Nikaelezea ukongwe wake ilikuwa ni mwaka 1993 by then, nikaelezea miundo duni dhaifu na mikongwe, miundo duni ya watumishi kufanya kazi iliyo dhaifu, nikazungumzia uzito wa kazi wa eneo lile walikuwa wana-bed state kama wagonjwa 500 kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia walikuwa wanatumia shilingi milioni 280 kwa mwezi. Nikashauri miundombinu irekebishwe japo wana tatizo la akili lakini wanahitaji kuhudumiwa katika sehemu nzuri, nikashauri pia ikiwezekana iwe Hospitali ya Taifa ya Magonjwa ya Akili iwe Taasisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kuipongeza Serikali sikivu ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan chini ya Waziri Ummy Mwalimu jinsi ambavyo jambo hili limetekelezwa kwa umakini mkubwa sana. Pia ninashauri suala hili pia liendelee kuzingatiwa na kufikiriwa kwa Hospitali yetu ya Kibong’oto kuwa taasisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo Tarehe 11 Februari, 2021 nilisimama humu ndani pia kuzungumzia suala zima la matibabu mbalimbali ya aina mbalimbali ikiwepo na mazoezi tiba, kwamba wataalam hawa wako wachache na pia Tanzania nzima Shahada inapatikana Chuo cha KCMC tu. Nikashauri ikiwezekana vyuo vingine kama Muhimbili, Bugando, UDOM hii taaluma ianzishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali sikivu sana ya Mama Samia Suluhu Hassan imekuja na shahada hii ya mazoezi tiba na vitendo mbalimbali vya matibabu katika Chuo cha Muhimbili. Ninaipongeza Serikali ya Mama Samia kuwa sikivu chini ya uongozi wa Waziri wetu Ummy Mwalimu na Watendaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Serikali imekuwa sikivu sana, leo mimi nakuja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ina Upanga na Mloganzila. Kwa siku wagonjwa wa nje tu kwenye hospitali hii ni 2,500. Muhimbili wanaona wagonjwa 2,000 kwa siku, Mloganzila 500 na nusu ya wagonjwa hao ni wa msamaha yaani hawana uwezo wa kulipia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sivyo tu, katika wagonjwa wa msamaha tuna wagonjwa ambao ni wafungwa. Hospitali ya Muhimbili peke yake inatumia shilingi milioni 72 kwa mwezi kuhudumia wafungwa, kwa maana ya kumuona Daktari, vipimo na dawa bure. Hospitali ya Muhimbili inatumia shilingi milioni 300 kwa wagonjwa wafungwa waliolazwa. Chai ya asubuhi, chakula cha mchana na jioni kwa mwezi shilingi milioni 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, Hospitali ya Muhimbili kwa mwezi kwa umeme na maji shilingi milioni 450 inalipa. Siyo hivyo tu, kuna magonjwa mengi yasiyoambukiza lakini niende kwa matatizo ya figo. Wanaofanya dialysis kusafisha damu kwa Muhimbili kwa siku wanafanya dialysis kwa wagonjwa 110, Mloganzila 30 na nusu ya hao ni hawana uwezo wa msamaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Muhimbili kwa mwezi inasamehe wagonjwa kwa gharama ya shilingi bilion 1.8 mpaka shilingi bilioni mbili msamaha. Nataka kusema nini? Hii Muhimbili magari yake yakiharibika, yakipata ajali, wakienda TEMESA wanatozwa fedha nyingi sana walipe. Wakienda ku- clear mizigo yao GPSA vitendeakazi mbalimbali vitendanishi wanalipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwa wafungwa, kwa nini basi Wizara ya Mambo ya Ndani kama inawezekana hiyo bajeti ya kuwatibia wafungwa iletwe Wizara ya Afya au la, watibiwe lakini bili ile ipelekwe Mambo ya Ndani walipe. Hospitali kama Muhimbili ina uwezo gani kwa gharama zote hizo? Bajeti yake haizidi shilingi milioni 400 kwa mwezi kutoka Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna shida bajeti ni ndogo, keki ni ndogo, basi pamoja na hayo yote bajeti inatengwa mwezi Julai tunaipitisha lakini inafika Muhimbili Septemba. Wagonjwa hawangoji kuugua Septemba, wagonjwa wanaumwa kila siku na tukumbuke Muhimbili ni Hospitali ambayo wagonjwa hawapelekwi ambaye ameugua siku mbili labda ana malaria au UTI, infection ya mkojo ni wagonjwa ambao wameshatibiwa huko wanakuja gharama yao ni ya juu sana. Kwa hiyo, ninasimama hapa kusema leo kwa sababu Serikali imekuwa sikivu sana. Imekuwa sikivu kwa Mirembe na mambo mengine niliyozungumza, leo Muhimbili naomba bajeti itakapopita iende haraka sana na pia iangaliwe kwa jicho la tofauti sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina hayo machache naomba Serikali sikivu ya Mama Samia Suluhu Hassan chini ya Waziri mahiri Ummy Mwalimu waangalie Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa jicho la tofauti sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru Profesa Janabi kwa kazi kubwa anayoifanya pale Muhimbili, imebadilika sana. Nilizungumza siku moja humu ndani pawe na stock center, naona Mloganzila wametenga, ka hiyo ina maana itakuwa kama Jakaya Kikwete, itakuwa wanapata huduma stahiki, hivyo tuwawezeshe tuwatie moyo, mazingira yawe safi pia wapate vitendeakazi kwa wakati, bajeti ije kwa wakati, wagonjwa hawasubiri muda, wagonjwa wapo kila siku tena wanaumwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo naomba kuunga hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia mapendekezo ya Serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2023/2024 kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kutujaalia uhai na afya njema, namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anawezesha vyema utekelezwaji wa bajeti ya Serikali. Nakupongeza Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, Katibu wa Bunge na watumishi wote wa Ofisi ya Bunge kwa kuendelea kufanya kazi kwa weledi mkubwa. Nampongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Naibu Waziri Mheshimiwa Hamad Chande na Mawaziri wote na watendaji wote wa Wizara za Serikali kwa kazi kubwa wanazozifanya katika kufanikisha malengo ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshmiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inayokwenda kuwagusa wananchi moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kuendelea kuimarisha utendaji kazi katika utumishi wa umma ambapo imeanzisha mifumo miwili, ambapo mfumo wa kwanza ni wa usimamizi wa utendaji kazi wa utumishi wa umma (PEPMIS), na mfumo wa pili ni wa usimamizi wa utendaji kazi kwa taasisi za umma (PIPMIS), pia imeanzisha mfumo wa taarifa za kiutumishi na mishahara (HCMIS). Mfumo huu umeunganishwa na mifumo mbalimbali ili kuhakikisha kwamba taasisi mbalimbali zinaweza kubadilishana taarifa kwa mfano imeunganishwa na PSSF, HESLB, Sekretarieti ya Ajira, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Mfumo wa Malipo ya Serikali (MUCE), mfumo wa mahudhurio, mifumo ya kibenki mbalimbali ili kufuatilia mikopo ya watumishi, PEPMIS na HCMIS lengo ni kurahisisha huduma za watumishi na pia mifumo yote inafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuja na mkakati wa kulinda majanga ya kimtandao mwaka 2022, pia imekuja na mwongozo wa matumizi bora, sahihi na salama ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), naipongeza sana Serikali kwa juhudi kubwa sana inazozifanya na pia kati ya taasisi 522 za umma, taasisi 433 zimeweza kuunganishwa na mfumo wa kiutumishi na mishahara.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa taasisi 134 tu za umma ndiyo zimeweza kuhifadhi mifumo ya taarifa kwenye vituo vikuu vya kuhifadhi taarifa na mifumo ya Serikali (Government Data Centers) vyenye usalama na uhakika kwa upatikanaji wa taarifa za Serikali, hivyo tunaishauri Serikali katika bajeti ijayo ya mwaka 2023/2024 iwezeshe Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora kutenga fedha za kutosha kuwezesha taasisi zingine kuhifadhi taarifa zao kwa ajili ya usalama wa taarifa za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha uliopita yaani 2022/2023 naipongeza Serikali imeweza kulipa malimbikizo ya mishahara ya watumishi 116,792 yenye thamani ya zaidi ya bilioni 199, imetoa vibali vya ajira mpya 7,499 na ajira mbadala 6656. Pia zaidi ya taasisi 62 zimeweza kuandaa na kuhuisha miundo na mgawanyo wa majukumu na imeidhinishwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, pia miundo 63 ya maendeleo ya utumishi na mishahara ya taasisi za umma imehuishwa na kuidhinishwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali imebuni Daftari la Huduma za Serikali Tanzania (GST) ambao mpaka sasa hatua za usanifu wa mfumo zimefanyika na taarifa kutoka kwenye taasisi 51 zimekusanywa. Naishauri Serikali katika bajeti ijayo iwezeshe Wizara hii kukamilisha huduma hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika nia yake ya kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, imeanzisha vituo viwili vya huduma katika majengo ya Ofisi za Posta katika mikoa ya Dodoma na Dar es Salaam, mwananchi akifika katika vituo hivyo anaweza kupata huduma katika taasisi za NIDA, RITA, Uhamiaji, NHIF, BRELA, Polisi, NSSF na PSSF. Jambo hili limekuwa na matokeo chanya sana kwa wananchi, naishauri Serikali katika bajeti ijayo yam waka 2023/2024 iongezewe pesa ili vituo zaidi viweze kuongezwa katika mikoa mbalimbali ili kusogeza huduma kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, katika huduma za jamii, nimekuwa nikichangia mara nyingi eneo la afya, lakini nakumbusha tena bajeti inapotengwa katika Wizara yoyote hususani ya afya tunaomba pesa ifikishwe kwa wakati kwani maradhi huwa hayasubiri, mfano bajeti inapitishwa mwezi Julai, 2023 lakini inafika kwenye hospitali husika mwezi Septemba, hii haileti tija kwa kuwa ugonjwa hausubiri. Hivyo ninashauri bajeti inapotengwa, iwe inafika kwa wakati ili iweze kuleta tija.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kujali suala zima la elimu ya Mtanzania kwa ujumla, kuongeza mikopo na kuendelea kugharamikia mpango wa elimu bila malipo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuchangia hayo naunga mkono hoja mapendekezo ya Serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2023/2024.
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuchangia pia ninakuombea kila la kheri katika kupambana kupata nafasi ya Urais wa Bunge la Dunia, Mwenyezi Mungu akutangulie.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuja na Muswada huu muhimu sana wa Sheria ya Tume ya Mipango kwa mwaka 2023.

Mheshimiwa Spika, Sheria hii inaenda kuanzisha Tume ya Mpango ambayo Tume hii itakuwa na mamlaka kubwa ya kusimamia masuala yote yanayohusu Mipango ya Maendeleo ya Taifa letu. Lakini nchi nyingine zote duniani zimekuwa na mifumo mbalimbali ya kisheria, ya kitaasisi ya kusimamia mambo haya ya Mpango wa Maendeleo. Nchi nyingi duniani Amerika ni mojawapo na nyingine nyingi. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge jambo hili ni muhimu sana na siyo geni.

Mheshimiwa Spika, Katiba yatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 Ibara ya 63, imetoa maelekezo, imeainisha kwamba kuna nia na makusudi ya kuandaa mpango au kuandaa Tume ya kuandaa Mpango wa Maendeleo. Si hivyo tu hata Sheria ya Bajeti Sura namba 439 imeweka mfumo wa kisheria na kitaasisi wa usimamizi na upangaji wa utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo. Kwa hiyo jambo hili lina baraka zote.

Mheshimiwa Spika, tunajua kabla na baada ya Uhuru kumekuwa kuna chombo cha namna hii cha kusimamia mambo ya Mipango ya Maendeleo. Toka tulipopata Uhuru mwaka 1961 mpaka mwaka huu kumekuwa kumeundwa na vyombo mbalimbali vyenye majina mbalimbali vyombo 11. Vyombo vitano vyote vilivyoundwa toka kupatikana kwa Uhuru vilikuwa chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alikuwa ni Mwenyekiti. Kati ya vyombo 15 ambavyo yamesimamia Mipango ya Maendeleo kwa Taifa letu toka tupate Uhuru vitano vyote vilikuwa chini ya usimamizi Rais kama mwenyekiti na kiongozi, vitano vingine vilikuwa chini ya Waziri kwa maana wizara husika ni kimoja tu kilikuwa chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais. Kwa hiyo, vyombo 11 vimekuwepo toka tupate Uhuru vikisimamia suala zima la kusimamia Mipango ya Maendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, chombo cha sasa hivi ambacho sasa hivi inaendakuundwa Tume hii. Tume ya Mpango inaenda kuundwa kisheria tofauti ni tofauti kabisa inaenda kuundwa kisheria japo taasisi zilizopita zilikuwa zina faida kama zilizopita zimetiletea tumekuwa kundi lenye hadhi ya uchumi wa kipato cha kati, cha chini mwaka 2020, kwa hiyo zimekuwepo zikifanya kazi nzuri ila sema zimeelemewa. Kwa hiyo, umuhimu wa kuanzisha Tume kisheria inayofanya kazi peke yake ni muhimu sana si kama zingekuwa hazifanyi kazi ila zimeelemewa kwa hiyo utendaji unakuwa siyo wenye tija sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tume hii inayoenda kuanzishwa au tume pendekezwa inaweza kwenda kutokana na Sheria ya Tume ya Mipango ya 2020/2023 inaenda kuandaa, kusimamia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa. Lakini si hivyo tu iko thabiti ina Idara mbalimbali ambazo zitakuwa chini ya Manaibu Katibu Wakuu Watendaji kama ambavyo imeainishwa kwenye Sheria. Kutakuwa na Idara ya Sekta Binafsi ambayo mwanzo haikuwepo, tulikuwa hatuhusishi Sekta Binafsi katika kuandaa mpango.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe credit kubwa, lakini si hivyo tu kutakuwa kuna Idara mahususi kwa ajili ya kusimamia masuala yote ya ubunifu na utafiti kabla ya kupanga mipango. Hii nayo itakuwa chini ya Naibu Katibu Mkuu anayejitegemea. Lakini si hivyo tu kutakuwa na Idara ya ufuatiliaji na tathmini ya utendaji ili kuona mpango una tija? Nilikuwa nauliza wenzangu lazima kuwe kuna Idara mahususi ya ufuatiliaji na tathmini ya je, mipango tunayoifanya inaleta tija? Sasa itakuwepo chini ya Naibu Katibu Mkuu wa Idara hii. Lakini si hivyo tu kutakuwa kuna Idara ya kusimamia maeneo ya vipaumbele.

Mheshimiwa Spika, tukirudi kwenye Muswada, Muswada pendekezwa huu wa Tume ya Mipango kwenye Ibara ya 4 sehemu ambayo inaonyesha kuanzishwa kwa Tume Ibara ndogo ya pili ina sema hivi “Tume itakuwa ni Idara inayojitegemea chini ya Ofisi ya Rais” imeeleza bayana.

Mheshimiwa Spika, si hivyo tu kama Kamati katika Muswada huu tulishauri mabadiliko kadha wa kadha mabadiliko katika Ibara ya 3, Ibara ya 5, Ibara ya 7, Ibara ya 8, Ibara ya 11, Ibara ya 12, Ibara ya 14, na Ibara ya 21. Kwa kweli Serikali imetupa ushirikiano imeenda kurekebisha imekuja kwenye jedwali la marekebisho ambalo imelisoma pamoja na Muswada kwa mara ya pili. marekebisho yote yamewekwa, imetupa ushirikiano mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitasoma marekebisho moja tu ambalo sisi tumeona ni muhimu na hakika hili tumepata kama Kamati ni kwamba katika Ibara ya 6 sehemu ya pili ya Muswada huu ambayo inaeleza majukumu ya Tume ambayo ni around19 lakini likuwa na Ibara ndogo tatu tu sisi tukapendekeza kama Kamati kuwe na Ibara ya 4 ambayo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, kwa ridhaa yako naomba nisome katika Muswada. Ibara ya 7(4) inasema “mpango wowote wa muda mfupi au wa muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa Sheria hii au Sheria nyingine iliyotungwa na Bunge au kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara ya Katiba hautabadilishwa au kuacha kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge”. Tunaipongeza Serikali imekuja na badiliko hilo imeridhia na imeingia kwenye Muswada wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashauri Bunge na Wabunge wenzangu Muswada huu ni mzuri sana, ni Muswada wenye faida wenye vision ya Taifa kama walivyotangulia kusema wenzangu. Kwa hivyo kwa Sheria hii mahsusi inayoanzisha Chombo cha Kitaifa cha kusimamia kuratibu uaandaaji, kutekeleza mipango ya Taifa ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nashauri pia Wabunge wenzangu waunge mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuchangia pia ninakuombea kila la kheri katika kupambana kupata nafasi ya Urais wa Bunge la Dunia, Mwenyezi Mungu akutangulie.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuja na Muswada huu muhimu sana wa Sheria ya Tume ya Mipango kwa mwaka 2023.

Mheshimiwa Spika, Sheria hii inaenda kuanzisha Tume ya Mpango ambayo Tume hii itakuwa na mamlaka kubwa ya kusimamia masuala yote yanayohusu Mipango ya Maendeleo ya Taifa letu. Lakini nchi nyingine zote duniani zimekuwa na mifumo mbalimbali ya kisheria, ya kitaasisi ya kusimamia mambo haya ya Mpango wa Maendeleo. Nchi nyingi duniani Amerika ni mojawapo na nyingine nyingi. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge jambo hili ni muhimu sana na siyo geni.

Mheshimiwa Spika, Katiba yatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 Ibara ya 63, imetoa maelekezo, imeainisha kwamba kuna nia na makusudi ya kuandaa mpango au kuandaa Tume ya kuandaa Mpango wa Maendeleo. Si hivyo tu hata Sheria ya Bajeti Sura namba 439 imeweka mfumo wa kisheria na kitaasisi wa usimamizi na upangaji wa utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo. Kwa hiyo jambo hili lina baraka zote.

Mheshimiwa Spika, tunajua kabla na baada ya Uhuru kumekuwa kuna chombo cha namna hii cha kusimamia mambo ya Mipango ya Maendeleo. Toka tulipopata Uhuru mwaka 1961 mpaka mwaka huu kumekuwa kumeundwa na vyombo mbalimbali vyenye majina mbalimbali vyombo 11. Vyombo vitano vyote vilivyoundwa toka kupatikana kwa Uhuru vilikuwa chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alikuwa ni Mwenyekiti. Kati ya vyombo 15 ambavyo yamesimamia Mipango ya Maendeleo kwa Taifa letu toka tupate Uhuru vitano vyote vilikuwa chini ya usimamizi Rais kama mwenyekiti na kiongozi, vitano vingine vilikuwa chini ya Waziri kwa maana wizara husika ni kimoja tu kilikuwa chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais. Kwa hiyo, vyombo 11 vimekuwepo toka tupate Uhuru vikisimamia suala zima la kusimamia Mipango ya Maendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, chombo cha sasa hivi ambacho sasa hivi inaendakuundwa Tume hii. Tume ya Mpango inaenda kuundwa kisheria tofauti ni tofauti kabisa inaenda kuundwa kisheria japo taasisi zilizopita zilikuwa zina faida kama zilizopita zimetiletea tumekuwa kundi lenye hadhi ya uchumi wa kipato cha kati, cha chini mwaka 2020, kwa hiyo zimekuwepo zikifanya kazi nzuri ila sema zimeelemewa. Kwa hiyo, umuhimu wa kuanzisha Tume kisheria inayofanya kazi peke yake ni muhimu sana si kama zingekuwa hazifanyi kazi ila zimeelemewa kwa hiyo utendaji unakuwa siyo wenye tija sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tume hii inayoenda kuanzishwa au tume pendekezwa inaweza kwenda kutokana na Sheria ya Tume ya Mipango ya 2020/2023 inaenda kuandaa, kusimamia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa. Lakini si hivyo tu iko thabiti ina Idara mbalimbali ambazo zitakuwa chini ya Manaibu Katibu Wakuu Watendaji kama ambavyo imeainishwa kwenye Sheria. Kutakuwa na Idara ya Sekta Binafsi ambayo mwanzo haikuwepo, tulikuwa hatuhusishi Sekta Binafsi katika kuandaa mpango.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe credit kubwa, lakini si hivyo tu kutakuwa kuna Idara mahususi kwa ajili ya kusimamia masuala yote ya ubunifu na utafiti kabla ya kupanga mipango. Hii nayo itakuwa chini ya Naibu Katibu Mkuu anayejitegemea. Lakini si hivyo tu kutakuwa na Idara ya ufuatiliaji na tathmini ya utendaji ili kuona mpango una tija? Nilikuwa nauliza wenzangu lazima kuwe kuna Idara mahususi ya ufuatiliaji na tathmini ya je, mipango tunayoifanya inaleta tija? Sasa itakuwepo chini ya Naibu Katibu Mkuu wa Idara hii. Lakini si hivyo tu kutakuwa kuna Idara ya kusimamia maeneo ya vipaumbele.

Mheshimiwa Spika, tukirudi kwenye Muswada, Muswada pendekezwa huu wa Tume ya Mipango kwenye Ibara ya 4 sehemu ambayo inaonyesha kuanzishwa kwa Tume Ibara ndogo ya pili ina sema hivi “Tume itakuwa ni Idara inayojitegemea chini ya Ofisi ya Rais” imeeleza bayana.

Mheshimiwa Spika, si hivyo tu kama Kamati katika Muswada huu tulishauri mabadiliko kadha wa kadha mabadiliko katika Ibara ya 3, Ibara ya 5, Ibara ya 7, Ibara ya 8, Ibara ya 11, Ibara ya 12, Ibara ya 14, na Ibara ya 21. Kwa kweli Serikali imetupa ushirikiano imeenda kurekebisha imekuja kwenye jedwali la marekebisho ambalo imelisoma pamoja na Muswada kwa mara ya pili. marekebisho yote yamewekwa, imetupa ushirikiano mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitasoma marekebisho moja tu ambalo sisi tumeona ni muhimu na hakika hili tumepata kama Kamati ni kwamba katika Ibara ya 6 sehemu ya pili ya Muswada huu ambayo inaeleza majukumu ya Tume ambayo ni around19 lakini likuwa na Ibara ndogo tatu tu sisi tukapendekeza kama Kamati kuwe na Ibara ya 4 ambayo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, kwa ridhaa yako naomba nisome katika Muswada. Ibara ya 7(4) inasema “mpango wowote wa muda mfupi au wa muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa Sheria hii au Sheria nyingine iliyotungwa na Bunge au kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara ya Katiba hautabadilishwa au kuacha kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge”. Tunaipongeza Serikali imekuja na badiliko hilo imeridhia na imeingia kwenye Muswada wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashauri Bunge na Wabunge wenzangu Muswada huu ni mzuri sana, ni Muswada wenye faida wenye vision ya Taifa kama walivyotangulia kusema wenzangu. Kwa hivyo kwa Sheria hii mahsusi inayoanzisha Chombo cha Kitaifa cha kusimamia kuratibu uaandaaji, kutekeleza mipango ya Taifa ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nashauri pia Wabunge wenzangu waunge mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Sekta ya Sheria wa Mwaka 2023
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Muswada wa Sheria wa Marekebisho ya Sheria katika sekta ya sheria. Naomba nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mawaziri wote wa sekta hii ya sheria, Mwanasheria Mkuu, pamoja na Watendaji wote wa sekta hii kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi iliyotukuka.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kujielekeza kwenye Sehemu ya Tano ya sheria hii ya Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Sekta ya Sheria ya mwaka 2020/2023. Naomba nijielekeze kwenye Sehemu ya Tano ya Muswada huu ambayo inarekebisha Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe Taasisi hii ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ni taasisi muhimu sana kwenye nchi yetu na ni kati ya taasisi chache sana ambazo zimetokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 katika ile Ibara ya 129.

Mheshimiwa Spika, katika Ibara ya 15 ya Muswada huu ulioletwa, inapendekezwa kuwekwa kwa nafasi ya Naibu Makatibu Wakuu wawili wa Tume. Pia, ukiangalia katika Sheria Mama katika kifungu cha 3 cha Sheria Mama ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, sheria hii imetamka kwamba itumike Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, Kamati tuliomba sheria hii itaje kwamba hawa Manaibu Makatibu wa Tume, mmoja atokane na Tanzania Zanzibar na mmoja Tanzania Bara, sheria itamke hivyo. Si hivyo tu, sheria hii katika Sheria Mama ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora katika kifungu cha 11(3), utaona sheria imebainisha wazi kabisa majukumu ya Kamishna Mkuu wa Tume.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo huo tumeshauri sheria hii itamke wazi majukumu ya hawa Naibu Makatibu Wakuu wawili, majukumu ya Naibu Mkuu wa Tume kutoka Tanzania Zanzibar na majukumu ya Naibu Katibu wa Tume kutoka Tanzania Bara yawe yametamkwa kabisa kwenye sheria.
Mheshimiwa Spika, naomba pia nijielekeze katika Sehemu ya Kumi na Tatu ya Muswada huu ambayo inafanya marekebisho katika Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Sura 171. Katika hii Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Muswada huu unapendekeza katika Ibara ya 48, kuwepo na takwa la lazima kwa Wizara zote, vitengo vyote, wakala wote pamoja na taasisi mbalimbali za Serikali inapoleta marekebisho madogo ya sheria au inapoleta sheria mpya lazima ipitie kwenye tume ili kupata utafiti ndipo ipite Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, ni jambo jema sana. Tukumbuke wakati tunapitisha bajeti ya taasisi hii muhimu ya mwaka 2023/2024, kama kuna changamoto kubwa tulikutana nayo ni changamoto kubwa ya ufinyu wa bajeti ya taasisi hii, lakini pia upungufu wa watumishi. Sasa tulipitishia bajeti ya shilingi bilioni 5.19, lakini pia taaasisi hii haina fungu la maendeleo. Kwa hiyo, tukiangalia mabadiliko haya yanayopendekezwa kwenye sheria hii ambayo anakusudia kuifanya sheria hii kuwe na takwa la kilazima kwamba Wizara zote, Taasisi zote za Kiserikali, Wakala na vitengo vyote kabla havijapeleka sheria kwenye Baraza la Mawaziri vipite kwenye tume hii ifanyiwe utafiti.

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo jema, lakini kwa concern tuliyoona kwenye changamoto inayokumba taasisi hii, bajeti ndogo, upungufu wa wataalam, tunajua sheria zinakuja kutoka kwenye taasisi mbalimbali, watakuja Madaktari, Wanasheria wenyewe, watu wa kilimo hata watu wa atomic. Sasa hawa wote taasisi haina hao wataalam.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeshauri ili kuepukana na ucheleweshaji wa utungwaji wa sheria maana zitaenda kurundikana kwenye tume kwa upungufu wa bajeti na watumishi, basi Serikali wakati inajiandaa kuipa majukumu hii taasisi iongezee bajeti na wataalam ili mwisho wa siku wanapokuja na sheria ili taasisi hii ishughulikie kila sheria na kila marekebisho ya sheria, basi iwe imeshawezeshwa vizuri ili iweze kuwa uwezo wa kufanya hayo maamuzi ili isije ikachelewesha sheria na hivyo kuchelewesha utaratibu mzima wa nchi kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo katika Sheria Mama ya Tume hii ya Kurekebisha Sheria, Kifungu cha 4(2)(e), jukumu hili limewekwa bayana katika Sheria Mama, lipo katika kifungu hiki, sema halikuwekwa takwa la ulazima. Kwa hiyo, sisi kama Kamati tulishauri kama inawezekana kifungu cha 4 kwenye Sheria Mama kiendelee kufanya kazi hiyo wakati wanaboresha uwezo wa taasisi hii nyeti.

Mheshimiwa Spika, pia Ibara ya 48 ya Muswada huu iondolewe. Kwa kweli niseme kwamba, Serikali kupitia Wizara ya Sheria wamekuwa ni watu ambao ni wasikivu sana, wanaonesha ushirikiano mkubwa na Kamati, wamepokea maoni yetu yote na wamekuja nayo kwenye jedwali la marekebisho. Nawapongeza sana na nawatakia kazi njema.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 4) wa Mwaka 2023
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Muswada wa Sheria wa Marekebisho ya Sheria katika sekta ya sheria. Naomba nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mawaziri wote wa sekta hii ya sheria, Mwanasheria Mkuu, pamoja na Watendaji wote wa sekta hii kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi iliyotukuka.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kujielekeza kwenye Sehemu ya Tano ya sheria hii ya Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Sekta ya Sheria ya mwaka 2020/2023. Naomba nijielekeze kwenye Sehemu ya Tano ya Muswada huu ambayo inarekebisha Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe Taasisi hii ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ni taasisi muhimu sana kwenye nchi yetu na ni kati ya taasisi chache sana ambazo zimetokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 katika ile Ibara ya 129.

Mheshimiwa Spika, katika Ibara ya 15 ya Muswada huu ulioletwa, inapendekezwa kuwekwa kwa nafasi ya Naibu Makatibu Wakuu wawili wa Tume. Pia, ukiangalia katika Sheria Mama katika kifungu cha 3 cha Sheria Mama ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, sheria hii imetamka kwamba itumike Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, Kamati tuliomba sheria hii itaje kwamba hawa Manaibu Makatibu wa Tume, mmoja atokane na Tanzania Zanzibar na mmoja Tanzania Bara, sheria itamke hivyo. Si hivyo tu, sheria hii katika Sheria Mama ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora katika kifungu cha 11(3), utaona sheria imebainisha wazi kabisa majukumu ya Kamishna Mkuu wa Tume.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo huo tumeshauri sheria hii itamke wazi majukumu ya hawa Naibu Makatibu Wakuu wawili, majukumu ya Naibu Mkuu wa Tume kutoka Tanzania Zanzibar na majukumu ya Naibu Katibu wa Tume kutoka Tanzania Bara yawe yametamkwa kabisa kwenye sheria.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nijielekeze katika Sehemu ya Kumi na Tatu ya Muswada huu ambayo inafanya marekebisho katika Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Sura 171. Katika hii Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Muswada huu unapendekeza katika Ibara ya 48, kuwepo na takwa la lazima kwa Wizara zote, vitengo vyote, wakala wote pamoja na taasisi mbalimbali za Serikali inapoleta marekebisho madogo ya sheria au inapoleta sheria mpya lazima ipitie kwenye tume ili kupata utafiti ndipo ipite Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, ni jambo jema sana. Tukumbuke wakati tunapitisha bajeti ya taasisi hii muhimu ya mwaka 2023/2024, kama kuna changamoto kubwa tulikutana nayo ni changamoto kubwa ya ufinyu wa bajeti ya taasisi hii, lakini pia upungufu wa watumishi. Sasa tulipitishia bajeti ya shilingi bilioni 5.19, lakini pia taaasisi hii haina fungu la maendeleo. Kwa hiyo, tukiangalia mabadiliko haya yanayopendekezwa kwenye sheria hii ambayo anakusudia kuifanya sheria hii kuwe na takwa la kilazima kwamba Wizara zote, Taasisi zote za Kiserikali, Wakala na vitengo vyote kabla havijapeleka sheria kwenye Baraza la Mawaziri vipite kwenye tume hii ifanyiwe utafiti.

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo jema, lakini kwa concern tuliyoona kwenye changamoto inayokumba taasisi hii, bajeti ndogo, upungufu wa wataalam, tunajua sheria zinakuja kutoka kwenye taasisi mbalimbali, watakuja Madaktari, Wanasheria wenyewe, watu wa kilimo hata watu wa atomic. Sasa hawa wote taasisi haina hao wataalam.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeshauri ili kuepukana na ucheleweshaji wa utungwaji wa sheria maana zitaenda kurundikana kwenye tume kwa upungufu wa bajeti na watumishi, basi Serikali wakati inajiandaa kuipa majukumu hii taasisi iongezee bajeti na wataalam ili mwisho wa siku wanapokuja na sheria ili taasisi hii ishughulikie kila sheria na kila marekebisho ya sheria, basi iwe imeshawezeshwa vizuri ili iweze kuwa uwezo wa kufanya hayo maamuzi ili isije ikachelewesha sheria na hivyo kuchelewesha utaratibu mzima wa nchi kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo katika Sheria Mama ya Tume hii ya Kurekebisha Sheria, Kifungu cha 4(2)(e), jukumu hili limewekwa bayana katika Sheria Mama, lipo katika kifungu hiki, sema halikuwekwa takwa la ulazima. Kwa hiyo, sisi kama Kamati tulishauri kama inawezekana kifungu cha 4 kwenye Sheria Mama kiendelee kufanya kazi hiyo wakati wanaboresha uwezo wa taasisi hii nyeti.

Mheshimiwa Spika, pia Ibara ya 48 ya Muswada huu iondolewe. Kwa kweli niseme kwamba, Serikali kupitia Wizara ya Sheria wamekuwa ni watu ambao ni wasikivu sana, wanaonesha ushirikiano mkubwa na Kamati, wamepokea maoni yetu yote na wamekuja nayo kwenye jedwali la marekebisho. Nawapongeza sana na nawatakia kazi njema.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)