Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Janeth Elias Mahawanga (6 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Chama changu ha Mapinduzi, kina mama wa Mkoa wa Dar es Salaam na familia yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Miaka Mitano na Mwaka Mmoja. Katika kuongeza kipato cha Serikali na kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia ile Mifuko 18 ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, napendekeza ishirikiane kwa karibu na Wizara ya TAMISEMI pamoja na Halmashauri zetu. Pia iongeze wigo kwa kuhusisha Madiwani nao kwenye Mpango huu ili itengeneze mfumo mzuri wa ukusanyaji wa hizi pesa pindi wajasiriamali hawa wanapopata hiyo fursa kwani fedha nyingi zinatoka kwenye vikundi lakini pia hazirudi. Kwa hiyo, tatizo kubwa hapa ni mfumo wa ukusanyaji wa hizi hela. Watakapohusishwa pia Madiwani katika utaratibu huu itasaidia kwani vikundi vingi kwenye kata zetu Madiwani ndiyo watu sahihi na wanavijua zaidi vikundi itasaidia ufuatiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika kutoa fursa hizi, Serikali iangalie zaidi kwenye kutoa elimu kwa wajasiriamali hawa kwa sababu fursa zipo, mikopo inatoka lakini wananchi wengi wanakwama kutokana na ukosefu wa elimu. Elimu hizi zikajikite katika kukuza ujuzi wa kuongeza thamani za bidhaa zao, upatikanaji wa mitaji, utafiti wa masoko na kuzitambua fursa zinazowazunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya naomba niongelee usajili wa vikundi. Sheria ya Fedha imetoa mamlaka kwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kukasimu shughuli zote za usajili, usimamizi na ufuatiliaji wa vikundi vya kifedha. Makundi haya ya kifedha yamegawanywa katika sehemu nne, kuna mabenki na microfinance ambazo zinapata miongozo moja kwa moja kutoka BoT, kuna SACCOS ambazo zinapata miongozo katika Vyama Ushirika na kuna vikundi vya kina mama ambavyo ni VICOBA wao wanapata miongozo kutoka TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki Kuu ilitoa muda wa mwaka mmoja vikundi yyote viwe vimesajiliwa kupitia sheria mpya. Ule muda uliisha, akina mama walikuwa wako tayari kusajili lakini miongozo kutoka TAMISEMI ilikuwa haijashuka huku chini. Iliongezwa muda wa miezi sita ambao unaisha mwezi Aprili mwaka huu, lakini mpaka sasa bado akina mama wakienda kwenye Halmashauri wanakuta bado hakuna utaratibu wowote ambao umetoka TAMISEMI unaowataka wao wasajili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imeleta hofu kubwa kwenye vikundi vya kina mama kwani kuna vikundi ambavyo vimesimama kufanya shughuli zake za ujasiriamali na kuna vingine vinafanya kwa uwoga vikiwa vinasubiri kuangalia miongozo hii ya usajili mpya inataka nini na inasemaje. Kwa hiyo, niiombe Wizara ya TAMISEMI, ijitahidi kutoa miongozo hii basi ili kina mama wafanye huo usajili kwa kutumia hii Sheria mpya ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali iangalie baadhi ya kero kuzifanya kama vyanzo vya mapato yaani fursa. Kwa mfano, Mkoa wa Dar es Salaam kuna kero kubwa sana ya takataka, Wizara ya Viwanda na Uwekezaji ni wakati sasa wa kuangalia ni jinsi gani kiwanda cha kuchakata taka kinaweza kupatikana kwani zaidi ya kuongeza kipato kwenye nchi yetu itaongeza ajira pamoja na kumaliza hili tatizo la taka, tutapata mbolea na gesi na Serikali itapata pato lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye ushauri, nashauri Serikali irejeshe mifumo ya kuzisaidia na kuchochea benki nchini yaani credit guarantee schemes ambazo zitasaidia wawekezaji kulipa kodi na Serikali itapata pato pia. Vilevile yafanyike marekebisho ya kodi inayohusu ufutaji wa madeni ambayo hayalipiki yaani bad debts write-off iendane na sera, kanuni na Sheria ya Benki Kuu ili kuweka mazingira ya biashara yanayotabirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali iwe inatoa muda wa kutosha inapofanya marekebisho ya sera zake mbalimbali ili kutoa muda wa wadau kujipanga kutokana na mabadiliko ya sera zinapokuwa zinafanyiwa marekebisho. Pia Serikali iweke mazingira mazuri ya kufanya mabenki binafsi kuachana na sera ya kuanzisha benki ambazo zinakuja kuwa mzigo na hazina tija kwenye Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niombe mamlaka ya kukusanya kodi irekebishe Tax Administration Regulation kwa kuondoa utaratibu wa sasa wa kutumia Urgent Notice kutoka kwenye mabenki moja kwa moja badala yake iweke utaratibu wa kukubaliana na walipa kodi kulipa kodi kwa muda rafiki. Hii itasaidia sana kwani wafanyabiashara wengi wataweza kuweka hela benki, watakuwa na imani na kuondoa ile hofu kwamba benki siyo sehemu salama sasa hivi ya kuweka hela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakiweka taratibu hizi wafanyabiashara, wajasiriamali wengi watakuwa na imani, itaongeza hamasa, watu wataweka fedha benki, ukizingatia hata Mheshimiwa Rais wakati anahutubia Bunge la Kumi na Mbili alisisitiza kuwa watu wahimizwe kuweka hela benki ili kusaidia benki zetu zifanye biashara na mzunguko uwe imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya TAMISEMI. Kwanza niipongeze Wizara kwa wasilisho zuri na vipaumbele vizuri kabisa ambavyo kama vitaenda kutekelezeka nina uhakika tutapata matokeo chanya na changamoto zote kwenye jamii yetu zitakwenda kwisha.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwenye mikopo hii ya asilimia 10 ambayo wanufaika ni akinamama, vijana na walemavu. Lengo la Serikali kwa mikopo hii lilikuwa zuri sana lakini uhitaji ni mkubwa kuliko pesa yenyewe na hii inatokana na baadhi ya pesa inayotoka kuwa hairudi. Je, halmashauri zetu zinafanya tathmini ya kuangalia ni kiasi gani kimetoka na kiasi gani kimerudi na kwa nini hakijarudi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanufaika wa pesa hii kuna kitu wanakikosa ambacho ni muhimu sana, wanakosa elimu. Akina mama wengi ni wajasiriamali ambao wanafanya shughuli za kijasiriamali kama usindikaji wa vyakula, lakini wanafanya kwa elimu yao binafsi, kwa uzoefu wao wa kufundishana wenyewe kwa wenyewe. Ningeziomba halmashauri zishirikiane na taasisi ambazo zinaunga mkono juhudi za kuwainua wananchi kiuchumi, hasa wajasiriamali wa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano unakuta kuna matangazo ya SIDO yanayotoa elimu ya ujasiriamali hasa upande wa usindikaji, akina mama wengi wanatamani kwenda kusoma mafunzo haya lakini wanashindwa kutokana na kukosa ada. Halmashauri kama itaandaa utaratibu mzuri ikapata wadau kutoka SIDO, kutoka kwenye benki wataalam wa mambo ya fedha, wataalam wa masoko, wataalam wa fursa na wataalam wa kuongeza thamani ya bidhaa za wajasiariamali wadogo wakashirikiana na Maafisa Maendeleo na Madiwani wetu kwenye kata wakapita kwenye vikundi vile vya akina mama, vijana wakatoa elimu hii, nina uhakika itasaidia sana. Tunasema tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda, tunatafuta vyanzo vingine vya mapato, lakini nina uhakika kabisa mikopo hii ni chanzo tosha cha mapato kama tutawaongezea thamani ya ujuzi wanufaika hawa wakaweza kuwa wajasiriamali wakubwa wakalipa kodi, tutapata mapato kwenye Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kundi lingine la vijana ambao wanamaliza vyuo vikuu wako mtaani hawana kazi. Halmashauri ina uwezo kabisa wa kuangalia mikopo hii ya asilimia 10 ikachukua kundi fulani la vijana at least kundi moja kama kikundi kutoka kwenye kila halmashauri wakawapeleka kupata elimu. Kuna taasisi tano zimeungana ambazo ni SIDO, VETA, NSSF, Baraza la Uwezeshaji Uchumi Wananchi na Benki ya Azania, hawa wanatoa elimu baadaye wanatoa mikopo kwa ajili ya viwanda vidogo kuanzia milioni 50 mpaka milioni 500. Vijana wanaomaliza chuo wakichukuliwa na halmashauri, wakasimamiwa kupata elimu hii kwa kulipiwa huko SIDO au VETA wakaweza kufungua kiwanda wataweza kuajiri vijana wenzao, watatoka kwenye wimbi la kukosa ajira na mwisho wa siku watakuwa walipa kodi wataongeza mapato kwenye Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe halmashauri zetu zishirikiane na benki. Benki nyingi zina bidhaa nzuri sana kwa ajili ya wajasiriamali wadogo, lakini wajasiriamali wengi wanakosa taarifa. Kama halmashauri wataweza kushirikiana na hizi benki ambazo zinainua wajasiriamali wadogo zikapita kwenye kata zetu akina mama, vijana na walemavu wakapata taarifa sahihi wakatumia kile kidogo walichokipata kutoka kwenye ile asilimia 10 hawa watu wanakwenda kuinuka. Ni aibu kuona kijana anakuwa machinga ndani ya miaka kumi. Kijana huyo alitakiwa awe ameshatoka kutoka kwenye ujasiriamali mdogo wa kupita barabarani akaweza kukaa kivulini akawa mlipa kodi mzuri, Serikali itaongeza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe ushauri kwa Wizara ya TAMISEMI. Kuwe na training pia za ndani kwa viongozi wetu kuanzia ngazi ya mkoa, wilaya, kata mpaka vijiji. Viongozi hawa wote wajione wao ni kitu kimoja na wanatembea kwenye safari moja, wanatakiwa wafanye kazi kama timu. Mkuu wa Mkoa ni mteule wa Rais, Mkuu wa Wilaya ni mteule wa Rais, Mkurugenzi ni mteule wa Rais, sasa kama hawa watu hawatakuwa kitu kimoja wakaanza kusigina wenyewe kwa wenyewe misuguano ile waathirika ni wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwananchi anapokuwa na tatizo lake ambalo linatakiwa kuwa solved kwa Mkuu wa Mkoa au kwa Mkurugenzi, lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Janeth.

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa anazofanya katika kuhakikisha Taifa hili linapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zinazohusiana na masuala ya afya. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, magonjwa yasiyoambukiza yanashika kasi kwa ongezeko na hata idadi ya vifo. Kwa Tanzania magonjwa ya moyo yakiongoza na pili ni magonjwa ya saratani.

Mheshimiwa Spika, ongezeko la ugonjwa wa saratani kwa sasa ni zaidi ya wagonjwa wapya 40,000 kwa mwaka na kusababisha vifo takribani 30,000 kwa mwaka huku tukiwa na wagonjwa zaidi ya 73,000 ambao wapo kwenye matibabu.

Mheshimiwa Spika, wahanga wakubwa wa ugonjwa wa saratani ni wanawake, na kundi hili la wanawake wanaopata ugonjwa huu wa saratani hasa ya shingo ya kizazi na saratani ya matiti wanakumbana na changamoto nyingi sana katika jamii mfano kuathirika kisaikolojia, kuathirika kiuchumi, mahitaji ya kijamii na kimwili na mapokeo kwenye jamii.

Mheshimiwa Spika, changamoto hizi na nyingine nyingi zimekuwa miongoni mwa wanawake wengi wanaopata ugonjwa huu kukata tamaa na hata kutozingatia matibabu ya kitaalam ambapo wapo ambao wameishia kujaribu tiba asili, imani za kishirikina na maombi pekee.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kuhakikisha inaongeza nguvu katika kuhakikisha kunakuwa na nguvu kubwa katika kupambana na changamoto za wanawake wanaoathirika na magonjwa ya saratani.

Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara ije na mpango mkakati kuhakikisha tatizo hili la saratani linapewa kipaumbele ili kujenga uelewa mpana kwa jamii kuhusu haya magonjwa ya saratani kwani huku kwenye jamii hili ni tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia bajeti hii. Kwanza naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa bajeti hii nzuri kwa Serikali ya Awamu ya Sita maana ni bajeti ya kwanza. Vile vile, nampongeza Waziri wa Fedha na Mipango na Naibu wake pamoja na timu nzima kwa bajeti hii nzuri. (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, bajeti hii inatia matumaini na faraja kwa Watanzania kwani ni bajeti ambayo imekidhi changamoto zote za jamii yetu kwa kuweka vipaumbele ambavyo Wabunge wengi walichangia katika Wizara mbalimbali. Vile vile, bajeti hii inakwenda kukamilisha mahitaji yote hususan kwenye masuala ya afya na miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napongeza kuhusiana na kipengele cha kodi ya line za simu. Tija ya kodi hii ni nzuri, kama ambavyo bajeti imeonyesha Shilingi za Kitanzania bilioni 360 zinakwenda kupatikana ambapo zitakwenda kujenga zahanati na mahospitali. Naiomba Serikali, fedha hizi kama zitakwenda kutekeleza haya, basi kiu kubwa na changamato ya masuala ya afya katika jamii yetu itakwenda kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naipongeza bajeti hii kwenye kodi ya shilingi mia katika kila lita ya mafuta. Fedha hii itakapopatikana itapelekwa TARURA kama ambavyo imeonyeshwa, ni kitu kizuri sababu fedha hizi zitakapokwenda kutoa changamoto ya miundombinu, uchumi wetu utakwenda kuimarika hususan kwenye jamii yetu hasa vijijini, kwani uchumi wa nchi unategemea sana suala la miundombinu. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kuliona hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile bajeti hii imekwenda kugusa masuala ya vikundi vya akina mama na vijana, hasa katika kutoa mikopo. Ukiangalia hata Mheshimiwa Rais alipoongea na akina mama ali-insist sana suala la vikundi vya akina mama kujiunga ili wapate mikopo ambayo itasaidia kutoa ajira na kufanya biashara zenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kupitia bajeti hii, wakaangalie katika suala la Sheria ya Fedha Mwaka 2018, kwani limekuwa ni mzigo hasa kwenye vikundi vya akina mama. Naiomba Wizara ikatumie wataalamu wa BoT katika kutoa elimu, maana vikundi vingi vimeshahamasishwa kujiunga, lakini kupitia sheria hii wengine wanafunga, hawaelewi sheria ile inataka nini hususan kwenye kutumia teknolojia ya TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Wizara itumie wataalamu wao wa BoT ambao wanaweza kufafanua sheria hizi wapite kwenye Wilaya wakutane na Madiwani na Bibi Maendeleo, watoe miongozo ya sheria hii hasa katika vikundi vya akina mama na vijana ili nao watakaposhuka chini kwenye makato wakikutana na akina mama waweze kufafanua sheria hizi ili vikundi viende kuwa imara vikatumie fursa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kupitia bajeti hii ikaangalie masuala ya sheria za fedha, lakini zaidi sana ikaangalie kwenye kipengele cha mabenki, kwani mabenki yatakaposhirikiana na Serikali katika kuongeza tija kwenye mikopo ya wafanyabiashara, itasaidia sana, maana mikopo ya asilimia 10 bado haitoshelezi. Kwa mfano, Mkoa wa Dar es Salaam, kazi za usafi wa barabara ambazo zilikuwa zikifanywa na akina mama wengi sasa hivi zile kazi zimeamishwa kwa SUMA JKT. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna kundi kubwa la akina mama ambalo limepoteza ajira na kupitia ajira zile walikuwa wakilea familia, wakisomesha watoto na kujikimu kwa mahitaji yao ya kila siku. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie sana taasisi za kifedha hususan mabenki, kuangalia ni jinsi gani ambavyo mabenki haya yataweza kuongeza mikopo kwa akina mama na vijana lakini mikopo hiyo itoke kwa riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naishauri Serikali iwekeze kwenye mfumo thabiti ulioungana (complete and consolidated system) ambayo watakuwa na utambulisho utakaokuwa na kanzidata ya taarifa za wafanyabiashara. Taarifa hizo zikiwa zinahusisha biashara zao, mali zao anuani za makazi ambazo zitaweza kusaidia mabenki kuwatambua hawa watu na kutoa mikopo kwa gharama nafuu, lakini kwa kutumia mfumo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Serikali iangalie kwa jicho la pili kuwekeza katika mabenki yote kuhakikisha kwamba gharama za uendeshaji wa mabenki, zisizidi asilimia 55 ya mapato. Ni kwamba inasema ikizidi benki hairuhusiwi kupata dividend ambayo ni kutoa faida. Kanuni hii imefanya mazingira ya uwekezaji wa mabenki kuwa ngumu. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie sana katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, kwa kupitia bajeti hii, naiomba Serikali ijikite zaidi katika mapato na mwenendo wa uchumi hususan kwenye ukuaji wa pato la Taifa, kwenye mapato na matumizi ya Serikali, kwenye deni la Taifa, Serikali ijikite sana kuangalia ukopaji na ulipaji wa madeni ili Taifa letu lisije likaingia kwenye adha ya kutokopesheka. Zaidi Serikali iboreshe tena kwenye sekta ya fedha; Serikali irejeshe mifumo iliyokuwa inasaidia benki kutoa mikopo kwa wingi (Guarantee Credit Schemes). Benki hizi zilikua kwa kutumia mifuko hii; mifuko ilikuwa inachochea sana utoaji wa mikopo. Kwa hiyo, Serikali ijitahidi kurudisha hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile uendeshaji wa sekta binafsi. Kama tulivyoona Serikali imeweka mazingira mazuri hususan kwenye Mfumo wa Sera na sheria za kodi ambazo zimekuwa ni kivutio kwa wawekezaji wetu. Mwisho, ijizatiti katika tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naipongeza Serikali kwa bajeti hii nzuri na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara ya TAMISEMI, nami kama walivyotangulia wenzangu ninaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kwenye Taifa hili. Pia naipongeza Wizara ya TAMISEMI kwa kazi nzuri inazofanya, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wake wanafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia mambo mawili lakini nitaanza na hili la mikopo ya asilimia 10. Kwanza ninaipongeza Serikali kwa kusamehe madeni ya vikundi vya mwanzo kabisa ambavyo walikuwa wamenufaika na mikopo hii kwa kushindwa kurejesha yale marejesho. Ni kweli na ni wazi kabisa kwamba mwanzo wa mikopo hii kulikuwa na mapungufu mengi sana vikundi vingi vilikuwa vinapewa mikopo lakini hawakuwa na elimu ya kutosha, walijikuta akinamama, vijana na watu wenye ulemavu wakishapata mikopo hiyo wanagawana mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kulikuwa kuna wanaoweza kufanya vizuri na kurejesha na wengine walikuwa wanashindwa kurejesha mikopo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine iliyopo kwenye suala hili ni kwamba kuna kundi la akina Mama ambao wanashindwa kukopesheka sasa hivi kwa kigezo kwamba wanaambiwa mlishakopa awali, kuna wengine wamerudisha lakini wenzetu hawakurudisha, mkawatafute warudishe fedha zile ili muweze kukopesheka tena. Sasa kama Serikali ilishasamehe basi niziombe Halmashauri zichukulie vikundi hivi kama vipya viweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana hawa watu sasa wamekaa pembeni hawakopesheki tena tunawasaidiaje ni akinamama wengi sana na vijana wanashindwa kukopesheka, lakini pia niiombe Wizara kupitia Halmashauri zetu ziangalie tatizo kubwa linalofanya fedha hizi hazirudi.

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Janeth kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Neema Mwandabila.

T A A R I F A

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumpa taarifa dada yangu Mheshimiwa Janeth.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kumwambia kwamba hoja anayoongelea ya masuala ya mikopo ya wanawake ni hoja ya msingi na nilitaka kumpa taarifa kwamba kwenye taarifa ya Waziri TAMISEMI hakuna sehemu inayotuonesha impact ya assessment ya hiyo mikopo tunayoitoa kwamba iliwavusha watu kutoka eneo gani kwenda eneo gani. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Mahawanga unapokea taarifa.

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante ninaipokea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Wizara kupitia Halmashauri zetu iangalie vikundi hivi sababu kubwa inayofanya fedha hazirudi na mpaka impact ya mikopo hii haionekani. Tuangalie zaidi kwenye kuwasaidia hawa wanaopata hii mikopo wengi wao ni wale ambao wanaanza kujiunga kwenye vikundi, wanakosa fursa ya kupata elimu ya mambo ya fursa, ubunifu, utunzaji wa fedha na nidhamu ya fedha sambamba na kufanya biashara kidigitali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia sasa hivi imebadilika, kuna vikundi ambavyo havitegemei mikopo ya Halmashauri hivi vimekuwa vikifanya vizuri sana sababu vina uwezo wa kugharamia mafunzo tuna taasisi, mashirika, watu binafsi mengi sana wanaotoa mafunzo kwenye vikundi vya akina mama, tumeona vinafanya vizuri sana, na mpaka wanatoka kwenye vikundi wanakwenda kufungua microfinance na wengine wanafungua kampuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie hawa wajasiriamali wadogo akinamama na vijana ambao ndio wanufaika wakubwa wa mikopo ya asilimia 10, wanashindwa kukidhi haja ya kuingia kwenye mafunzo haya sababu ya kukosa fedha ya kulipia mafunzo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu haya mafunzo yanatolewa kwa kulipia ada siyo bure, kwa hiyo Halmashauri zetu ziangalie namna ya kuweza kulipia mafunzo haya kuviwezesha vile vikundi viweze kupata mafunzo ili vikundi viweze kudumu fedha hii iweze kuzunguka irudi iwafikie wengi zaidi lakini fedha hii ionekane, isiendelee kupotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna changamoto nyingine ambayo inawakuta akina mama na vijana waliokwishapata mikopo, hawa waliweza kufungua viwanda na kampuni zao walipata kazi kwenye Halmashauri zetu na taasisi za Serikali lakini kwenye kulipwa imekuwa ni issue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana na akinamama wamefanya kazi kupitia Halmashauri wanatakiwa malipo yao wanazunguka kila siku kwenda kuomba walipwe, hawalipwi! Kwa hiyo kazi zimesimama vikundi havizalishi tena, fedha ile hairudi matokeo yake vikundi vinakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahamasisha vikundi, tunawakopesha, tunawapa kazi tunashindwa kuwalipa fedha inapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili nilikuwa ninataka kuongelea kuhusu mashine za POS ambazo zinatumika na Mamlaka zetu kukusanya mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashine hizi zimekuwa na changamoto na zinasababisha upotevu mkubwa sana wa fedha za Serikali. Changamoto ya kwanza ni watumiaji wa mashine hizi wanapokusanya zile fedha, fedha hizi zinatumika zikiwa mbichi kabla hazijawa banked kwa hiyo hapa ni mwanya mkubwa sana wa upotevu wa hivi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niziombe Halmashauri na Wizara ya TAMISEMI iliangalie hili hasa kwenye kipengele hiki cha kutumika fedha mbichi kabla hazijaenda benki. Hii inasababisha upotevu mkubwa wa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya pili kumekuwa na adjustment ambazo zinafanyika bila utaratibu, hili nalo ni kipengele kingine kinachosababisha fedha hizi kupotea, mapato ya shilingi 1,000,000 yanafanyiwa adjustment yanaonekana kama yalikusanywa kama shilingi 100,000, shilingi 100,000 inaonekana shilingi 10,000; shilingi 50,000 inaonekana shilingi 5,000 hapa pana upotevu wa fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu mashine nyingi za POS zinakuwa offline kwa muda mrefu, sasa tunajiuliza fedha hizi zinakusanywaje au zinakwenda wapi? Halmashauri zetu ziangalie hawa wakusanyaji.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Janeth Elias Mahawanga.

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye Taifa letu. Vilevile naipongeza Wizara ya TAMISEMI, Mheshimiwa Waziri, Manaibu na timu nzima na vipaumbele vyao 19 walivyoviainisha kwenye bajeti hii ya 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye mikopo ya asilimia 10. Ni kweli fedha nyingi zimepotea kwenye mikopo hii na sababu kubwa za msingi zinasababisha kwanza ni wahusika na wasimamizi wa mikopo hii kutokuwa waaminifu, hali iliyopelekea kuwa na utitiri mkubwa sana wa vikundi hewa. Vile vile wanufaika wa mikopo hii, wengi wao hawana elimu ya fedha, hawana elimu ya ujasiliamali, yaani ni watu tu kujikusanya; watu watano kutengeneza kikundi, wanapata fedha. Pia maandiko mengi; wanahamasishwa kuandika maandiko ya viwanda vya ufyatuaji matofali, ununuzi wa magari, kilimo cha mjini (green house), na ufugaji wa ngombe wa kisasa. Sasa hivi vitu vyote siyo kweli kwamba mtu anapewa mikopo wiki hii, wiki ijayo anaweza kufanya haya. Hivi vyote vinahitaji elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuona mikopo hii sasa itoke Halmashauri ipitie kwenye taasisi za Kifedha. Naomba, tumeshaona udhaifu mkubwa kwa vikundi hivi vya watu watano watano, kwa nini mikopo hii sasa wasishirikishwe na vikundi vya huduma ndogo za kifedha, hawa ambao ni VICOBA? Kwa sabbau ni vikundi ambavyo vinazungusha hela zao benki. Wananunua hisa zao, wanakopeshana wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona vikundi vidogo hivi vya watu watano watano wakipata zile fedha, walikuwa wanagawana mtu mmoja mmoja, matokeo yake wanashindwa kurudisha, lakini vikundi vya huduma ndogo za kifedha, wale tayari wana fungu lao ambalo wanakopeshana ndani ya kikundi. Ni vikundi ambavyo vina miaka mitano, miaka kumi na wana uwezo wa kukopeshana Shilingi milioni tano, milioni 10 mpaka milioni 20 kwa mtu mmoja. Kiu yao na malengo makubwa ni kufanya mambo makubwa sasa; kufungua viwanda, kufungua makampuni na biashara kubwa kwa ajili ya vikundi. Sasa kwa nini fedha hizi zinazopotea wasiingize na hawa wakawa wanufaika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa wanapeleka fedha zao benki, marejesho yao yanapitia benki na benki wanaona kabisa cashflow yao inavyokwenda, ni rahisi zaidi hata marejesho kukatwa kule. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, vikundi vya huduma ndogo za kifedha wanatamani nao wakawa wanufaika wa mikopo hii ili wafungue viwanda, akina mama wapeane ajira. Watoe ajira kwa vijana, hata kwa watu wenye ulemevu, wote wapo kwenye vikundi vya VICOBA wanahitaji mikopo hiyo wafanye vitu vikubwa. Lengo lao siyo kukopeshana, wana malengo ya kufanya vitu vikubwa, lakini mikopo hii haiko wazi kuonesha kwamba wao ni wanufaika. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho, tunaomba aliweke hili wazi: Je, vikundi vya huduma ndogo za kifedha ni wanufaika wa hii mikopo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kikubwa tunaiomba Wizara itakapokaa na mabenki kuweka utaratibu, wekeni utaratibu mzuri. Mikopo hii wapate watu sahihi kabla ya kupata mikopo watu waandaliwe kwanza at least hata miezi miwili, mitatu. Siyo kweli, elimu ya wiki moja tu, mtu anapewa fedha, anaweza. Kuna wanufaika ambao ukiwafuata huko mtaani, ukiwauliza kwa nini hamrejeshi? Anashangaa, lini amepata mkopo? Tunaamini kwa kupitia benki haya yote yatakwisha. Kwa hiyo, tukuombe Mheshimiwa Waziri, mikopo hii hata kama itapitia kwenye mabenki, lakini bado Halmashauri ina kazi kubwa ya kufanya. Kuwe na utaratibu wa Halmashauri husika kukaa na vikundi; waliopata mikopo, wasiopata na wanaotarajia kupata. Kuwe na elimu endelevu za hii mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona kabisa VICOBA wanafanya vizuri kuliko hawa; lakini ndio hawa hawa akina mama, ndiyo hao hao vijana na ndio hao hao watu wenye ulemavu. Shida kubwa ni kwamba hawa wanaohamasishwa hivi vikundi vya watu watano kuna kitu hakiko sawa. Unakuta kikundi kimeandikiwa andiko. Ukikaa nao ukiwauliza hili andiko lenu mlikuwa mnataka nini? Hawajui hata wameandikiwa andiko gani? Wanaandikiwa maandiko hawayajui. Wanapewa hela, Halmashauri inajua kabisa tunawapa hii hela hawa, andiko lao linasema hivi, hii hela wana uhakika itakwenda kurudi, lakini hairudi, kwa sababu hata walichoandikiwa hawakijui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuombe suala la elimu na kuandaa watu lizingatiwe sana. Kinyume na hapo, kama mikopo hii itaenda benki, utaratibu usipowekwa vizuri, wanufaika wakawa ndio hawa hawa, na taratibu za benki zikatumika kama zile za kuwakopesha watu wengine, tunaenda kutengeneza janga kubwa kuliko lile la PRIDE. Kwa Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nasisitiza utaratibu, Halmashauri itenge fedha kwa ajili ya kutoa elimu kwa hivi vikundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba Wizara, tuangalie kada ya akina mama wanaofanya biashara ya Mama Lishe. Tunaona majengo ya biashara makubwa yanajengwa, lakini akina mama hawa hawapewi kipaumbele, hawapewi eneo. Akina mama hawa, wateja wao ndio hao wafanyabiashara. Majengo yanajengwa, wanapewa wafanyabiashara tu, wao wanakosa maeneo; na wengi wana mikopo, wanatakiwa warudishe marejesho. Biashara zao wanunuzi ndio hao walioko hapo. Kwa hiyo, tunaomba masoko yaliyojengwa maeneo ya biashara yaliyojengwa litengwe eneo kwa ajili ya akina Mama Lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, nami niungane na wenzangu waliozungumzia na suala la ajira. Mtaani tuna vijana wengi hasa kada ya walimu ambao wanafanya kazi kwa kujitolea. Tunaomba ajira za safari hii zije kitofauti. Hawa wanaojitolea wakapewe kipaumbele; wapate kwanza wao kabla ya wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)