Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao (33 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, hotuba hii ya Mheshimiwa Rais ni miongoni mwa hotuba tamu sana katika nchi hii. Hizi hotuba za kishujaa hazitakiwi kuachwa bila kujadiliwa wala kusifiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameonesha ushujaa mkubwa sana ndani ya miaka mitano. Nimeangalia hotuba ya miaka mitano, nikaangalia na hotuba hii aliyoitoa juzi anafungua Bunge la Kumi na Mbili, mimi binafsi naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusiana na suala la mifugo. Katika mifugo Mheshimiwa Rais amesema kwamba wafugaji katika nchi hii sasa wana nafasi kubwa ya kupewa maeneo ya kupata vitalu, lakini waandaliwe sera nzuri kwa ajili ya kuacha kwenda kuchunga mifugo kwa aina ya zamani sana. Leo wafugaji wanatembea kuchunga wakati tunayo ardhi kubwa ya kutosha tungeweza kuzalisha nyasi, tunayo mabua ya mahindi yanapatikana kila mkoa, kwa nini wasitengeneze sera nzuri kwa ajili ya mifugo yetu?

Mheshimiwa Spika, leo wafugaji wanahamishwa kama hawapo kwenye nchi yao. Kila siku kesi zinakuwa nyingi, ukiangalia taarifa ya habari ni migogoro mikubwa ya wafugaji. Katika hili kama utaandaliwa mfumo mzuri sisi pamoja na kuwa nchi ya pili kwa ufugaji katika Afrika, tutakuwa nchi ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwenye hili suala la nyama, wananchi wa Tanzania hawajahamasishwa kula nyama. Mwananchi mmoja anatakiwa kwa kiwango cha chini ale kilo, ana hali mbaya nusu kilo, lakini akila hata robo kilo tu soko la nyama peke yake halitoshi katika nchi hii. Sisi wenyewe tunakuwa ni soko kubwa sana la nyama, kwanza tuanze kula sisi nyama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la maeneo haya ya malisho. Ni kwamba wakikata vitalu na hawa wafugaji wakapewa maeneo ya kwenda kuchunga kwanza ni walipaji wazuri kwa wakati. Leo katika nchi hii mifugo imeenea nchi nzima na miongoni mwa wafugaji ambao wanapata tabu, lazima tuwe wakweli, ni Wasukuma na Wamasai. Tumekuwa tunakwenda kila kona unahamishwa unaondoka, sasa hii imekuwa ni hatari. Kwenye hotuba hii tunakwenda katika uchumi wa kati, nafikiri Waziri wa Mifugo na Waziri wa Sheria waliangalie jambo hili tuwe huru katika nchi yetu katika suala la mifugo.

Mheshimiwa Spika, sasa niende upande wa kilimo cha pamba. Nchi hii pamba inalimwa katika mikoa 11. Katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na Mheshimiwa Rais ametembea nayo katika kampeni, anasema tunahitaji kuzalisha tani milioni moja, tuna uhakika wa kuzalisha zaidi ya tani milioni tatu lakini ni kama pamba itaokolewa na Serikali kwa dhamira ya kweli.

Mheshimiwa Spika, Kwa mfano, kama tumeweza kuokoa Shirika letu la Ndege leo liko hai kwa nini tusiokoe pamba yetu ya Tanzania kwa mambo matatu tu? Jambo la kwanza ni kwamba pamba hii ya nchi yetu itumike kwenye kuzalisha nyuzi na kutengeneza nguo katika nchi hii. Serikali inunue viwanda vya nyuzi na nguo halafu uone kama kilo moja ya pamba haitauzwa Sh.2,000 mpaka Sh.5,000 kwa kilo. Hii nguo niliyovaa mimi leo inauzwa Sh.170,000 au Sh.150,000 ukipata kwa gharama nafuu wakati haina robo kilo ya pamba. Sasa tunaonekana watu wa ajabu, ni lazima tumsaidie Mheshimiwa Rais na tuweke dhamira ya kweli, hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili, ni kupiga marufuku kuuza pamba kwa robota, kwa sababu uuzaji huu wa pamba wa robota unaifanya nchi hii inakuwa mtumwa, wanatuchezea katika maeneo makuu. Wanatuchezea katika mbegu, tunazo nchi zinazolima pamba katika Afrika; Burkina Faso ukiangalia Mali, Sudan, Misri, Zimbabwe na ukiwaona wenzetu Waganda leo wanakwenda kuchukua pamba ya Msumbiji wanasema ni miongoni mwa pamba bora katika Bara la Afrika hii yote ni kutuchezea akili, lakini kama tutakuwa tuna viwanda vyetu hatuwezi kuulizwa hilo jambo kwasababu pamba ni kilimo cha mabepari.

Mheshimiwa Spika, mbegu katika nchi hii hivi viwanda vya pamba vilivyopo huwezi ukailinda mbegu, unaweza ukatoa maelekezo kwamba mbegu ya kupandwa katika nchi hii inalimwa Igunga…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Hii kengele na yenyewe tena, basi bwana.

SPIKA: Ya kwanza hiyo.

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Sawa. Hapa nipo mahali patamu sana basi tu.

Mheshimiwa Spika,suala la mbegu haliwezi kulindwa na wafanyabiashara, suala la mbegu litalindwa na Serikali, lakini suala la pembejeo, mbegu na dawa na pamba ina muda ina timeframe, mwisho wa kupanda mbegu ni tarehe 15 mwezi 12, lakini mbegu inafika Januari, hizi dawa baada ya kupulizia, roho inaniuma muda unakuwa ni mdogo, sijui nifanyeje kuhusiana na suala la pamba. Serikali imerudisha viwanda vyetu vya Nyanza, SHIRECU, halafu tunashindwa kuiokoa pamba, zaidi ya wananchi milioni 16 ndiyo roho yetu.Mheshimiwa Rais tutamsaidiaje katika hili maana yake roho inatuuma, tuokoleeni pamba.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema naomba nichangie Mpango wa Maendeleo uliowasilishwa kwetu leo na Mheshimiwa Mwingulu Nchemba, Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wake aliowasilisha leo sijaona mahali ambapo amezungumzia habari ya zao la pamba. Zao la pamba katika nchi hii linalimwa zaidi ya mikoa 14 na pamba hiyo unayoiona ina uwezo wa kuwa na viwanda vitano. Angalia uchumi mkubwa unaotokana na pamba; pamba ikizalishwa vizuri na ikatafutiwa bei, Serikali ikawekeza katika pamba; na Serikali ilivyojitoa katika kuwekeza katika pamba, wakaachiwa mabepari, zao hili litakuwa limekufa. Kwa nini? Limekufa kwa kupata bei ndogo. Mabepari wameshusha bei. Tusiite wawekezaji, kwa sababu kwenye pamba kule kuna mabepari, zao la pamba likawa limekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaiambia Serikali, katika Mpango wake wa miaka mitano, wanafanyaje kulifufua zao la pamba? Serikali ikiwekeza katika zao hili, tutapata viwanda vya pamba, viwanda vya nyuzi, viwanda vya nguo, viwanda vya vyakula vya kuku na mifugo na tutapata mafuta. Haya mafuta ambayo leo mnayaagiza kutoka Malaysia na kwingineko, mnalazimisha mafuta, mafuta, yako kwenye pamba. Huko kote, hizi ni kodi utapata Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Bahati nzuri wewe unatoka kwenye Jimbo ambalo pamba inalimwa. Hebu waonee huruma wananchi wa Iramba, Sengerema wakiwemo na wananchi wengine Tanzania nzima. Njoo na mpango wa pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika pamba ninachotaka kueleza, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba utapata kodi, leta sheria tu hapa. Badala ya pamba kutozwa ushuru, njooni na Sheria hapa mchukue hata VAT asilimia kumi na pamba muipe bei ya shilingi 2,000/=. Ekari moja ya pamba ina uwezo wa kutoa tani moja ya pamba. Sasa kama kuna mtu anapata shilingi milioni mbili katika pamba na Serikali ikachukua kodi ya asilimia 10, mkachukua shilingi 200,000/= kwa ekari moja, mikoa inayolima 14: Je, utakuwa na shida gani tena ya pesa hapa Mheshimiwa Mwigulu? Hii miradi yako yote itaisha. Treni ya mwendokasi, sijui kuna Bwawa la Nyerere na la wapi, sisi walimaji wa pamba tu tunatosha kutengeneza kodi ya kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili, kuna suala la Ziwa Victoria, kule ukianzia juu; Tarime kule, ukaenda moja kwa moja mpaka kule Misheni mwisho kabisa, Kanyigo, kuna wananchi wanaokaa mwambao wa Ziwa, hawajatumikishwa katika kilimo cha irrigation. Sisi tukimwagilia, sasa hivi umeme upo, tukopesheni mashine za kumwagilia, wananchi wetu wana uwezo wa kuzalisha kiwango kikubwa cha mazao. Mnataka uchumi gani kama huu uchumi tunauachia wazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwa mfano, kwenye Jimbo langu tu la Sengerema pale, kuna mradi wa maji wa shilingi bilioni 23, unadaiwa deni la umeme la shilingi milioni 300. Umeme unakatwa, mradi wa shilingi bilioni 23 unateswa na shilingi milioni 300. Sasa tunashangaa, hawa ndio wawekezaji? Ndio Watanzania wanaotaka uchumi wa bluu? Unaandaa mradi wa shilingi bilioni 23 na una deni la shilingi milioni 300, halafu ule mradi unakaa haufanyi kazi, unadaiwa shilingi milioni 300! Ni maajabu makubwa sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha aliangalie sana hili suala katika miradi kama hii. Huu ni mradi mmoja tu wa Sengerema, sijui miradi mingine inayoteswa na vijipesa vidogo kama hivi kwa uwekezaji mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la uvuvi. Kule katika uvuvi tuna matatizo makubwa. Sheria za Uvuvi zilizoko kule katika Ziwa Victoria na hatujui Maziwa mengine huko; leo kuna samaki ambao ni wadogo hawakui. Kuna furu, kuna vimote na samaki wa aina nyingi; barara, hizi ni lugha za kienyeji kule. Wao wanajua hawa samaki hawakui, lakini wanakamatwa nao wale Samaki, nyavu zinachomwa moto. Mlikuwa na Kiwanda cha Nyavu, fufueni kiwanda hicho halafu mtengeneze nyavu zinazotakiwa na Serikali, lakini mkiwaacha waagizaji wakaleta nyavu, matokeo yake mnakwenda kuzichoma moto, mnatengeneza umasikini katika Ziwa Victoria. Liangalieni sana hili jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyozungumza tunakwenda kufunga mradi. Mgodi wa Buzwagi unafungwa. Sengerema kuna wawekezaji katika Mgodi wa Nyanzaga wameomba kufungua Mgodi wa Nyanzaga; leo ni mwaka wa nne toka mwaka 2017, mnataka wawekezaji gani? Huu mradi unakuja kuzalisha pesa. Uwekezaji wake tu wa kuandaa ule mgodi una shilingi trilioni moja, leo mnataka wawekezaji gani? Kwa sababu tu ule mradi unatakiwa kukua Sengerema watu hawautaki, halafu wanataka kuita wawekezaji. Waje wawekezaji gani wakati wengine mnawakataa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha aangalie katika Mpango wake wa miaka mitano, tunahitaji Mgodi wa Nyanzaga Sengerema ufunguliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kuna suala kubwa sana hapa tunalozungumzia la utengenezaji wa barabara. Hizi barabara unazoziona zinakwenda kwa wananchi, ambazo zinatengenezwa na TARURA, nilifikiria sana kwa nini TARURA isirudi ujenzi? Hata hivyo, naangalia kazi waliyonayo watu wa ujenzi; ukiangalia miradi aliyonayo TANROAD na bado ukamwongezee tena mradi mwingine wa TARURA, sishauri TARURA ihame. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana Mheshimiwa TARURA ibakie mahali pake, lakini kuna pesa ziko hapa. Nilizungumza hapa siku moja nikawaambieni, jamani kuna pesa za TARURA, kuna pesa ziko kwenye ukokotoaji wa mafuta, wanakokotoa watu wa EWURA. Shilingi 90/= kila siku ya Mungu wanakusanya katika huu ukokotoaji, hizi fedha zinakwenda kutumika vibaya. Shilingi 1,080,000,000/=. Ukichukua pesa hizi Mheshimiwa Mwigulu, kwa mwezi ni shilingi 32,400,000,000/=; kwa mwaka kunakuwa na fedha hapa zaidi ya shilingi bilioni karibu 400 ambazo zinakwenda kwenye hizi tozo ndogo ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa walioweka tozo, wote wako kwenye bajeti. Mnakwendaje kuweka kwenye tozo la mafuta? Kule kuna import duty, kuna import levy pale, kuna petrol levy pale; mnakwenda kuweka hivi vitu vingine vya nini? Hii fedha ileteni TARURA tutengeneze barabara zetu. Tunazo Halmashauri za Miji. Halmashauri za Miji tunazo 21, Halmashauri za Wilaya tunazo 137, tunazo Manispaa 20 na Majiji sita, kwa nini TARURA haongezewi fedha hapa za kufanyia kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwa Mheshimiwa Mwigulu juzi nimepita barabara ya Ndago, nimepita Shelui kuzungukia Ndago, hata yeye hana barabara. Nitashangaa sana kama Mheshimiwa Mwigulu hata wewe hutakubali TARURA iongezewe fedha. Hutarudi 2025. Haya maneno nakwambia kabisa, usidhani hatutarudi sisi tu, hata ninyi Mawaziri mtakomea ndani huko huko. Tengenezeni pale TARURA, ipeni pesa za kutosha tutengeneze barabara zetu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wewe hapo hutarudi kama barabara hizi hazitatengenezwa. Msidhani kwamba hili ni suala ni la Tabasam pekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nafikiri message imekwenda. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam huu utabiri wako huu! (Kicheko/Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndiyo. Hili ni hatari! (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, angalia dakika zangu lakini.

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza Mheshimiwa Tabasam, subiri kidogo.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndiyo.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu humu ndani ni Senator na mimi nataka kwanza kumkaribia kidogo, lakini sasa wewe ni mgeni kabisa, ukitutabiria sisi kutokurudi humu ndani, nahisi hali yako wewe ni mbaya zaidi kuliko ya kwetu. (Kicheko/Makofi)

Endelea Mheshimiwa, karibu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kukwambia, TARURA ni janga la Kitaifa. TARURA, yaani kama ingekuwa nchi nyingine tungekuwa tuna mjadala wa Kitaifa tufanyeje kuhusu TARURA?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kuwaambieni jamani, Waheshimiwa Wabunge humu ndani, nimewaelezeni kwamba fedha ziko kwenye mafuta. Nikawaambia kwamba, nilimwambia hapa Mheshimiwa Spika, tukae tujadili hili jambo, kuna fedha kule sisi tuwaonyeshe. Hii Habari ya kuwa tu bei za mafuta zinapanda kila mwezi, bado hatuna manufaa nazo hizi fedha, kodi yetu iko pale pale, hili ni jambo ambalo kwenda kwenye uwekezaji, kama Serikali haiwezi kuagiza mafuta yake, ninachotaka kukuambia Mheshimiwa Mwigulu, utatwanga maji kwenye kinu. Haitawezekana nchi yoyote inayotaka uchumi wake isipoweka fedha kwenye kuagiza mafuta yake. Tegemeeni wafanyabiashara waje wawatengenezee nchi, hili jambo halipo hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo nchi marafiki nyingi, hili suala la mafuta; tunalo eneo letu la TIPER pale. Lile eneo amepewa mwekezaji ambapo hakuna hata faida yoyote. Tungeenda kutengeneza matenki tukawa na reserve kubwa pale ya lita hata bilioni mbili. Leo mafuta yanakuja kupanda bei katika Soko la Dunia, sisi tunaweza tuka-stabilize pale tukabakia salama. Endeleeni kuudharau huu ushauri ninaowapeni, kwa sababu unatolewa na mtu wa Darasa la Saba katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana. Mimi nimewasilisha. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia Mpango huu wa Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia suala la elimu; Elimu ya Msingi na Sekondari pamoja na Vyuo. Mwaka 2016 Serikali ilianza Mpango wa kusomesha watoto bure katika shule za msingi na sekondari kidato cha kwanza mpaka cha nne (O- Level). Mpango huu wa Serikali uliungwa mkono sana na ukafurahiwa na wananchi kila kona ya nchi hii. Watoto waliokuwa wanakwenda kuchunga ndege katika mashamba ya mpunga, wanachunga ng’ombe, wote walipelekwa madarasani. Sasa hivi ni mwaka 2021 watoto hawa ambao walianza kusoma elimu bure wanakadiriwa kufikia milioni mbili na mwaka kesho watafanya mtihani wa darasa la saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, amesema Serikali ina mpango wa kujenga shule 1,000 mpya za sekondari. Upungufu ninaouona kwa idadi hii kubwa ya wanafunzi takriban milioni mbili, hata kama wanafunzi hawa watafaulu kwa asilimia 80, inaonekana mpango huu wa Mheshimiwa Waziri Mkuu wa madarasa kujenga shule 1,000 bado ni mdogo sana. Mimi napiga hizi hesabu naona hapa kuna upungufu wa karibu madarasa 103,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna madarasa 103,000, mnakuja na mpango wa kujenga shule 1,000 mpya, hawa watoto watasomea chini ya mti? Bahati mbaya sana watoto hawa ni wajukuu wa Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu ndio aliyeleta Mpango huu wa kusoma bure; na watoto wameupokea wakaenda darasani na sasa hivi wanasoma siyo mchezo. Baadaye tutatengeneza tension kubwa sana ya nchi hapa. Mheshimiwa Waziri Mkuu ataanza kuzuia watu wasiende likizo na wapi, sasa hii ni hatari. Hili jambo inaonekana kama anaachiwa Waziri Mkuu peke yake, wakati hili ni janga la nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana mpango huu wa bajeti kwa haya madarasa 1,000 Wabunge muyakatae. Ninyi Wabunge shauri yenu mwaka kesho watoto watakuja kwenye majumba yenu, hakuna Mbunge atakayekuwa salama, hizi shule ni chache. Mheshimiwa Waziri wa Serikali za Mitaa na Manaibu tafadhalini sana rudini mkaandae mpango mwingine mpya mjenao hapa vinginevyo hali itakuwa tete hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna kitu kibaya kama Waziri Mkuu bajeti yake watu wakang’ang’ania shilingi, hii itakuwa ni hatari sana katika nchi. Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakuheshimu sana katika jambo hili, lakini wasaidizi wako ulionao naona wanataka kukutengezezea bomu haya madarasa ni madogo. Mimi kwangu tu kwenye Jimbo la Sengerema nahitaji shule mpya 30 na nchi hii ina majimbo karibu 200, itakuwaje? Hii ni hatari Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la walimu; walimu wa shule za msingi na sekondari katika nchi hii wako laki mbili na sitini na moja kama na mia mbili hamsini na tatu. Walimu wa shule za msingi wako laki moja na sabini na tano na amia nane, walimu wa sekondari wako elfu themanini na tano. Upungufu walimu elfu arobaini. Kwenye mpango ajira zinazoonekana hapa ni chache. Hawa wanafunzi 40,000 Serikali iliwekeza, imewasomesha hawa wanafunzi kwa pesa za mikopo, leo hawa walimu wako mitaani halafu ninyi mna upungufu wa walimu 40,000, hamtoi ajira. Mwaka kesho ni janga la kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jamani bajeti yetu hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu, msimfedheheshe Waziri Mkuu. Waziri wa Fedha, Waziri wa Kazi, Waziri wa Elimu liangalieni hili suala kwa sababu huko shuleni sisi ndio tunajua shule moja unakuta ina walimu 16 wanafunzi elfu moja na zaidi. Kwa mfano, kwangu Shule moja ya Msingi Mnadani wanafunzi wa darasa la sita ni 500, sasa kwa shule nilizonazo mimi tu peke yake kwa Sengerema Mjini wanafunzi watakaofanya mtihani ni zaidi ya wanafunzi 7,000 sasa hii si ni hatari, tutawapeleka wapi hawa wanafunzi?

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui bwana mwaka kesho itakuwaje. Kila atakayekuwa anaingia humu atakuwa anameza dawa za ugonjwa wa moyo, hatari itakuwepo kubwa sana mwaka kesho. Tunaiomba Serikali katika jambo hili ilitilie mkazo wa hali ya juu sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam, hilo la ugonjwa wa moyo kila anayeingia humu ndani ni unabii au ni kitu gani?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, hali itakavyokuwa kwa sababu, nachotaka kukwambia sasa hivi bado tuna maboma kule. Kwa mfano, mimi nina ujenzi wa sekondari 15 ambazo hazijakamilika jana nilikuwa naangalia hii hesabu mimi mwenyewe nikawa naogopa, hawa nilionao sasa hivi elfu saba sijamaliza kuwapeleka sekondari, mwaka kesho kuna bomu lingine linakuja na mwaka huu bado wanakuja hawa watu, sasa najiuliza…

NAIBU SPIKA: Sawa, sasa kuhusu ugonjwa wa Wabunge, hilo hata wewe fanya mazoezi usijenao humu ndani. Wabunge hawa wa Mheshimiwa Spika Ndugai watarudi wazima kabisa humu ndani. (Makofi/Kicheko)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nachotaka kukwambia mimi niko serious katika jambo hili. Mimi nafikiri huu mtaala wa ualimu muufute katika vyuo vikuu kwa sababu mnawapeleka watu wanakwenda kusomea ualimu, una upungufu wa walimu hamtaki kuajiri wako mtaani, inakuwaje? Mnafikiri hawa wazazi ambao watoto wao wamekwenda kusomea ualimu na wako nyumbani mnategemea nini? Hawa vijana wetu itakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu tunao, lakini katika huo upungufu tulionao wa walimu hamtaki kuajiri, mnakuja na ajira 6,000. Mimi nashindwa kuelewa jambo hili. Jamani twendeni mbele ya safari, lakini mjue kwamba tunakwenda kufanya kampeni 2025 na kampeni tuanze sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe kama hunisikilizi ananisikiliza Mheshimiwa Samia. Mheshimiwa Samia ndiyo atajua hawa 40,000 upungufu utakuwaje. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam, hebu tuelewane kidogo, hebu kaa kidogo nikueleweshe.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii inakuwa hatari.

NAIBU SPIKA: Wewe changia hoja, hakuna mtu anayehitaji kutishwa, hayupo. Mara useme watu hawatarudi, mara watu watarudi na pressure, aah aah, wewe changia tu hoja yako umalize.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika zangu umezilinda hizo maana tayari umeshanipotezea moja hiyo. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam inabidi nikupeleke darasani. Usiwe unabishana na Kiti. (Kicheko)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, sibishani.

NAIBU SPIKA: Eeh, usibishane. Na mimi pia sipangiwi muda wa kuzungumza humu ndani unayepangiwa ni wewe, malizia mchango wako.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu wa walimu elfu arobaini. Mheshimiwa Waziri Mkuu utaangalia katika bajeti yako uone namna gani tutafanya ili tuondoe hili tatizo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni maboma. Yako maboma yaliyojengwa kwa ajili ya madarasa, yako maboma yaliyojengwa kwa ajili ya nyumba za walimu, lakini yako maboma yaliyojengwa kwa ajili ya zahanati na yako maboma yaliyojengwa kwa ajili ya vituo vya afya. Ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba uunde kikosi kazi kipite nchi nzima, kitakuletea taarifa iliyo sahihi kwa sababu, kuna taarifa nyingine zinafichwa kwa ajili ya usalama wa hawa wakuu wetu walioko kule. Wanaogopa kusema maboma yaliyopo kwa sababu wanaonekana tayari pesa zinazokusanywa katika halmashauri zetu zinatumika vibaya. Maelekezo yako uliyokuwa unayatoa kwa ajili ya hizi Halmashauri zetu kutenga fedha, hazina mapato ya kutenga fedha kumaliza maboma haya ni lazima Serikali isaidie mpango huu wa haya maboma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine tulilonalo sisi kule ni la vyuo hivi vya VETA pamoja na maendeleo ya jamii. Hivi vyuo naombeni vitumike vizuri kwa sababu uwekezaji uliotumika hapa; kwa hii miaka sita tumewekeza shilingi trilioni moja na milioni mia sita na hamsini, kila mwezi tunawekeza katika elimu shilingi bilioni 23. Sasa hizi shilingi bilioni 23 kwa miaka yote hii mpaka sasa hivi leo ni miezi 72 sawa na shilingi trilioni moja na milioni mia sita, halafu baadaye hawa wanafunzi wakishindwa kufaulu wanarudi nyumbani. Ushauri wangu, darasa la saba wakishindwa kufaulu wapelekwe moja kwa moja kwenda kwenye hivi Vyuo vya Maendeleo ya jamii pamoja na vyuo vya VETA.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema. Naomba kuchangia mchango wangu katika bajeti ya Viwanda na Biashara kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu nazungumzia suala la viwanda vya kuchakata pamba katika nchi hii. Mikoa inayolima pamba katika nchi hii ni mikoa 17, lakini Wilaya 54 zinalima zao la pamba kwa ukubwa kabisa. Katika Ilani yetu ya uchaguzi tumeainisha kwamba tutatengeneza tani milioni moja katika nchi hii ndani ya miaka mitano kuanzia mwaka 2021 na kuendelea mpaka mwaka 2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kufikisha tani milioni moja kama hujajiandaa kuwa na viwanda. Ushauri yangu kwa Serikali katika Wizara ya Viwanda na Biashara; Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo ni miongoni mwa wasomi wakubwa wenye heshima katika nchi hii, mimi binafsi nakukubali na ninashangaa maono haya Mheshimiwa Rais aliyapataje ya kukufikiria kwamba Profesa Mkumbo anaweza akawa sababu ya kubadilisha maisha ya Watanzania, akakuweka katika hii Wizara. Sasa itendee haki hii Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, Mheshimiwa Profesa Mkumbo, Waziri wa Viwanda na Biashara, andaa andiko, mimi najua wewe ni mwandishi mkubwa katika nchi hii, andaa andiko kwa ajili ya kuweka mashine za kuchakata pamba. Hizi mashine zilizopo katika vyama vyetu vya ushirika vya Nyanza, Shirecu, Musoma, Kagera kule Biharamulo, Tabora na Singida; hivi viwanda haviwezi sasa hivi kuchakata pamba kwa sababu mashine hizi zilikuwa za kizamani. Hizi mashine zimetoka India, kuna mashine zimefungwa kule Nyakalilo mwaka 1959, mashine zimefungwa pale katika ginnery ya kwetu Nyamililo, hizi ni mashine zimewekwa pale mwaka 1967.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashine zimekuja kufungwa Buyagu Ginnery, hizi ni mashine za mwaka 1972. Lakini kuna mashine mpya ambayo imefungwa pale Manawa Ginnery katika Wilaya ya Misungwi, hii ndiyo mashine mpya peke yake katika Mkoa wa Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashine zilizoko Nasa Ginnery, ukienda Nyambichi Ginnery Kwimba; hizi mashine zimechoka. Nenda Bariadi, hizi mashine zilizoko kule zimechoka; nenda Maswa, kiwanda kilichoko Maswa sasa hivi ni gofu. Majengo yapo na haya majengo ni imara; andaa andiko la kuweka mashine za kisasa ambazo gharama zake ni ndogo, ni dola 50,000 mpaka dola 70,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashine hizi zikishachakata pamba andika andiko Mheshimiwa Profesa Mkumbo, kila Halmashauri ambako pamba inalimwa wawe na viwanda vya nyuzi. Lazima utenganishe kiwanda cha kuchakata pamba na kiwanda cha nyuzi. Hizi viwanda vya nyuzi vikiwa katika Halmashauri husika, huko hawa Wakuu wetu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na sisi Wabunge, tutahakikisha hili zao la pamba linatoa ajira kubwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya hapo nyuzi zitauzwa katika viwanda vikubwa. Tutakuwa tuna viwanda vikubwa katika makao makuu ya mikoa ambako pamba inazalishwa. Kule watatengeneza majora halafu yale majora yatashuka chini tena kwa ajili ya hao washonaji watakaokuwa wanashona nguo hizi. Kwa hiyo, watashona nguo na tutazalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa Mkumbo aende akajifunze Thailand. Thailand hawalimi pamba kama Tanzania, lakini leo ndiyo nchi ya kwanza duniani kwa kuzalisha nguo za watoto na nguo za akina mama. Pamba inatoka Tanzania, hatuwezi kukubali katika jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa Mkumbo kaa ufikiri uwasaidie Watanzania na utapata heshima kubwa; ukibadilisha mapinduzi ya zao la kilimo na viwanda katika nchi hii utapata heshima kubwa sana. Na kule unakokwenda kutengeneza walipakodi, utakwenda kuwatengenezea kule katika kilimo. Mazao ya kilimo yakipata uchakataji mzuri katika nchi hii tutaiokoa nchi hii na ajira itapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema tunatengeneza ajira milioni nane; nini milioni nane, tutatengeneza ajira milioni 17. Kwa sababu tukiwa na viwanda sisi nchini, tujiondoe kuuza robota. Na usifikiri kutengeneza viwanda vikubwa, kuna viwanda vinakuja katika kontena la 20 feets au 40 feets, kontena dogo tu, kontena lile dogo linakaa hata makao makuu ya kata. Watalima pamba na watachakata robota. Uwe na viwanda vya kuchakata robota 35 mpaka 100, basi inatosha. Utaibadilisha nchi hii kuhusiana na suala la pamba. Kila Mbunge anayesimama hapa anazungumzia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, kuna jambo ambalo linaonekana katika nchi hii halileti afya, suala la biashara ya Zanzibar na Tanzania. Hili jambo lazima liangaliwe kwa nguvu kubwa. Haiwezekani nchi inaitwa Tanzania Bara, Tanzania Visiwani tunaunda Tanzania, leo mzigo ukija ukaupitishia Zanzibar unaonekana umefanya jambo haramu katika nchi hii, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tengenezeni sera nzuri ya biashara katika nchi hii. Wazanzibari waone wana haki ya Muungano kuuza vitu hapa na sisi Watanzania tuone tuna haki ya kuuza bidhaa zetu Zanzibar. Haiwezekani kitu kama hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Wazanzibari hawatufurahii sisi kwa sababu tumefunga mpaka, yaani inaonekana kama mzigo unatoka Zambia au Uganda, haiwezekani kitu kama hiki. Kwa hiyo tengenezeni sera nzuri ya biashara, kwamba mzigo utakaoshuka Zanzibar kuja Tanzania Bara ni asilimia tano au kumi ulipiwe ushuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo biashara zetu za mipakani za sheria za Afrika Mashariki, hizi biashara zilizoko tumetengeneza majengo. Ukienda katika mpaka wa Burundi na Tanzania kule Kobelo, leo tunagongwa Kobelo, unagonga Kabanga, ukienda Rusumo, hali kadhalika. Ukienda katika mpaka wa Tanzania kule Misenyi, Mtukula, ukienda mpaka wetu sisi wa Sirari leo ule mlango wa Sirari unaonekana ukipitia Sirari unakuja wewe unakuwa kama unafanya biashara haramu, haiwezekani kitu kama hiki katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalieni hii biashara ya mipakani, Tanzania imeshuka katika biashara ya kuagiza mizigo nje ya nchi. Wekeni hizi kodi kwa sababu wewe ndiyo una haki ya kutengeneza walipa kodi wapya na wewe ndiyo una haki ya kulinda walipa kodi na wafanyabiashara katika nchi hii. Hii dhamana umeichukua wewe umepewa na Mheshimiwa Samia Suluhu kuhakikisha wafanyabiashara wanakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nchi, Rais akija wa aina hii biashara inakufa, akija Rais wa aina nyingine biashara inapanda, haiwezekani katika nchi hii. Tengenezeni sera ya biashara wafanyabiashara tufanye biashara kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na-declare mimi ni mfanyabiashara, lakini biashara nyingine tumeziacha katika nchi hii. Leo kuna biashara mfano kama sasa hivi nilitoa ushauri mimi, kuna biashara ya mifugo, hii biashara ya mifugo ni kubwa sana katika nchi hii. Leo mifugo wetu, ng’ombe wananunuliwa na watu wa Comoro, wanakuja kununua ng’ombe Kahama, Sengerema na Kwimba. Wale ng’ombe wanapelekwa Comoro wanalishwa miezi miwili wanakwenda kuuzwa Ufaransa, haya ni mambo ya ajabu sana. Kwa nini sisi tusitafute soko la ng’ombe Ufaransa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna soko kubwa kule Ghuba, wenzetu wanakwenda katika ibada ya Hijja sasa hivi. Hii ibada ya Hijja Mheshimiwa Profesa Mkumbo, ni kwamba mnatakiwa mkatafute soko hili la mbuzi na ng’ombe haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mbuzi anauzwa mpaka dola 200, 300 Saudi Arabia, wakati huyu mbuzi anauzwa kwenye masoko Kongwa, Sengerema na sehemu nyingine kwa shilingi 50,000, shilingi 70,000, anauzwa Saudi Arabia dola 300; sasa haya ni maajabu makubwa sana. Ng’ombe anauzwa shilingi 700,000, anakwenda kuuzwa dola 2,000 au 1,500 Jiddah. Sasa hili ni jambo ambalo hii ni kazi yako Mheshimiwa Profesa Mkumbo; hakikisha hii minada kwenye haya masoko yetu tuuze sisi wenyewe katika hizi nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala la kuweka viwanda vya nyama. Viwanda vya nyama katika nchi hii ni vichache kulinganisha na idadi ya ng’ombe tulionao. Tanzania leo ni nchi ya pili kwa mifugo ikitoka Botswana…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tabasam kwa mchango wako mzuri, muda wako umemalizika.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Lakini kama umenikatia kidogo hivi maana yake bado nilikuwa naendelea kuserereka, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa niaba ya jina la Jimbo la Sengerema naomba kuchangia mchango wangu katika bajeti hii ya nishati.

Mheshimiwa Spika, kazi ya uspika ni kazi ya ngumu sana, nilikuwa sijui wakati huo sijawa Mbunge lakini nimeona kwamba una kazi ngumu kiasi gani cha kwanza ni kwamba kuhakikisha Wabunge wako wote wana uwezo wa kufanya kazi katika maeneo gani katika hizi kamati. Mimi tu Mwenyezi Mungu alikuonesha maono kwamba mpeleke MheshimiwaTabasamu katika Kamati ya Nishati na Madini hongera sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza lazima nikusifie wewe mwenyewe binafsi kuona Mheshimiwa Tabasamu ninafiti pale lakini ninachotaka kukuambia kitu kingine cha msingi sana kilichopo ni Mwenyekiti wa Kamati hii ni mzalendo wa kwelikweli. Yaani haya yote unayoona Waziri anafanikiwa ni kutokana na kamati hii ikiwa na mwenyekiti na msaidizi wake Naibu Mwenyekiti na sisi wajumbe kuwa wazalendo katika kamati hii. Tumezunguka katika kamati kuangalia hii miradi yote ya kimkakati miradi ya umeme mikubwa iliyopo na bado ndo tukaja na maono kuja kukusaidia kwamba tuangalie katika vina saba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sheria ya mafuta na gesi ya mwaka 2015 nyinyi mmepitisha Bungeni hapa mnajua inazungumzia nini kuhusiana na suala la usalama wa mafuta kama ni usalama wa nchi, usalama wa Taifa. Lilikuwa ni kosa sana kuachiwa mtu binafsi aendeshe muhimili mkubwa kama huu kwa kuweka vina saba hili lilikuwa ni kosa tusilirudie tena katika nchi hii naomba Hansard iweke hiyo na ukiona mtu anakuja kuzungumza hapa kwamba GFI basi ujuwe kabisa halitakii mema Taifa hili tunahitaji uzalendo wa kweli kutoka moyoni katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kampuni ya wajanja wawili watatu wanaondoka na milioni 168 kwa siku kwa miaka 6 poleni sana watanzania katika jambo hili inaumiza sana raia yoyote wa Tanzania ambaye ana machungu kwa ajili ya uzalendo wa nchi hii mkaja hapa mnakuja kuzungumza GFI kwanza hatujui amelika kodi kiasi gani kwa sababu ameanza kufanya kazi hii mwaka 2015 anachukuwa bilioni tano kila mwezi kwa mwaka ni bilioni 60 bajeti karibu ya wizara tatu kosa kubwa sana katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, huyu mtu kachukuwa bilioni 60 mpaka 72 kwa miaka 6 karibu bilioni 450 hatakiwa kumzungumza mtu huyu kweli tunakuja Wabunge tunakuja kuzungumzia habari ya GFI sasa hivi badala ya kuja kujipa pole kwa kazi hii vina saba ni nini? Vina saba ni mafuta hayahaya petroli hii, diseli hii, mafuta ya taa kinachowekwa ni chemical tu kidogo wajanja fulani bei ya dola moja anauza huyu SWISCAP wamekuja wawili kama partner mmoja SWISCAP anauza vina saba GFI anaweka vina saba halafu EWURA anakuja kukugua hivi vina saba kwa miaka sita.

Mheshimiwa Spika, leo tunaleta mawazo ya kizalendo kwamba TBS anatosha kuja kufanya kazi hii tuweze kupata pesa kuokoa hizi pesa ambazo walikuwa wanachukuwa wajanja wawili watatu kuna watu wanataka kuja kusema GFI aendelee kuweka haya mafuta jamani tunaitakia mema nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kukuambia hapa kinachobakia ni uzalendo wa Waziri husika uzalendo wa kwako wewe kama Spika uzalendo wa sisi kama kamati tukushauri vizuri juu ya jambo hili huyu mtu sijui katika hii bilioni 60 alilipa kodi alilipa payee hatujui ulipaji wake wa kodi tunamuomba Waziri wa Fedha kwanza afuatilie watu waende wakaangalie GFI alilipa kodi kiasi gani na hili jambo lije lielezwe bunge haiwezekani huyu mtu tena aje arudi hapa mkataba wake umeisha mwezi wa tisa akaongezea kwa cotetion kazi ya bilioni 60 inaweza ikaongezwa kwa cotetion akaongezewa miezi mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwezi wa Kumi na Mbili, mkataba umeisha wa miezi mitatu akaongozewa miezi mitatu, tarehe 28 mwezi wa pili kaongezewa miezi mitatu inaumiza sana katika roho leo tunasema aweke TBS watu wanakuja kusema hapa sheria kwamba TBS hana sheria maana yake ni nini kuitwa TBS tunaomba tafsiri ya neno TBS ni nini?

Mheshimiwa Spika, hili shirika la viwango la Taifa viwango vya aina yoyote iwe gesi iwe mafuta kila kitu iwe dawa ndio kazi ya TBS. Sheria gani ije iundwe tena kwa ajili ya TBS na TBS huyu naomba kwa manufaa ya nchi niongezewe dakika kidogo naomba nakwenda kwa sababu nakwenda mbele huko kuna jambo kubwa nakuomba sana maana yake nasikia kengele inalia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyozungumza huyu TBS sasa hivi akiwezeshwa, akiwezeshwa wafanyakazi, miundombinu, akanunua hizi machine zinauzwa Finland zinauzwa Uturuki, machine zinauzwa China na hivi vinasaba ni vitu vinatengenezwa maabara tukatengeneza wataalam wetu wakaja wakafanya hii kazi kwa ajili ya uzalendo hili ni suala la usalama wa nchi hatakiwi kuachiwa mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza hatujui huyu GFI hii vina saba alivyokuwa anaviweka yeye katika hizi kampuni za mafuta katika nchi hii depo 22 amewauzia kiasi gani, ya kuwapa kwa sababu hana haki mali ni ya kwake…

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa unapewa na Mheshimiwa Shabiby.

T A A R I F A

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Spika nataka nimpe taarifa Mheshimiwa mzugumzaji kwamba hata kama TBS itafanya kwa bei kubwa bado ile pesa itaingia kwenye taasisi ya Serikali. Kuliko kufanya mtu binafsi nataka nimpe taarifa kwa sababu pesa itaingia kwake.

SPIKA: Unaipokea taarifa hiyo Mheshimiwa Tabasamu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika kwa mikono sabini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni kwamba hivi vina saba SWISSCAM alikuwa anamuuzia GFI kwa dola saba kwa cubic 5 lakini sasa hivi baada ya kuonekana GFI kakosa kazi SWISSCAM anamuuzia vina saba TBS kwa dola 3.5 na mimi kwa ajili ya uzalendo nimekwenda kumfuata Mkurugenzi wa TBS DG nikamwambia hata hiyo bei bado umewapa kubwa agiza wewe mwenyewe Finland Uturuki utapata kwa 0.8. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya maneno ya wizi ukome katika nchi hii ninachotaka kuwaambieni kama Mheshimiwa Tabasamu nimetishiwa kuuwawa kwa ajili ya hawa watu wa GFI, kuleta habari hizi tu hapa Bungeni nikatishiwa kuuwawa nimemwambia Mheshimiwa Spika na kesi hii iko hapo kwa RPC Dodoma, na hatujapata majibu walionipigia simu na namba zao ziko pale kwa ajili ya kunitisha kazi hiyo umefanyiwa wapi.

Mheshimiwa Spika, naomba na hili unisaidie kunilinda kwa ajili ya uzalendo nimeleta jambo hili kwa sababu tunatafuta pesa za barabara za TARURA, hivi ninavyozungumza na wewe ukiondoa kodi iliyopo hapa kwenye mafuta kwa mfano kwa mwezi huu mambo haya ni madogo sana kwa mwezi huu tu peke yake kodi ya petrol ilikuwa ni shilingi 792, kodi ya diesel ilikuwa ni shilingi 600 kama sikosei hapa kwa lita 666, kodi ya mafuta taa ilikuwa ni shilingi 615 lakini tozo zilizoko hapa nitakuprintia karatasi kesho nikuletee vikampuni vidogo vidogo ambavyo viko kwenye idara zetu mpaka zimefika pamoja na huyu GFI alivyokuwepo tumefikisha shilingi 92 tozo peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukichukuwa kodi ya shilingi 790 Mheshimiwa Waziri wa Fedha nisikilize upo hapa hii ndio inayoingia hazina na katika hiyo shilingi 790 kuna shilingi 100 kwa ajili ya petrol fee hii ni kwa ajili ya utafiti wa petrol na mambo mengine. Pesa inayobakia 690 ndio kodi. Hii shilingi 92 hii inaenda tena kama tozo kwa sababu tunakuja kwenye bajeti kuu ntakuja kukukaba huko hawa kwa nini wanaleta tozo kodi nyingine hii tozo ikatwe kule iende TARURA habari ya kutuambia kwamba TARURA imepewa bilioni 150 kwamba kila halmashauri imepewa milioni 500 ni kuja kutufunga mdomo hili tusisema hili jambo haiwezekani Wabunge katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika jambo hili hii shilingi 92 chukueni calculator zenu shilingi 92 hizi ambazo zinapotea hapa wanachukuwa huko zinakwenda kwenye tozo kutumika vibaya hizi zikipigiwa hesabu kwa siku tunauza petrol peke yake. Lita 5,600,000. Diesel tunauza lita 6,200,000, mafuta ya taa kama lita 100,000 kwa siku ukichukua hapa hizi shilingi mabilioni ya shilingi kwa kila siku hizi zinatosha kwenda TARURA, jamani inakuwaje haya maneno leo mimi nakuja kutishiwa kuuwawa kwa sababu nimeleta jambo hili heri nife kwa ajili ya Tanzania Spika utanilinda. (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa kwa mzungumzaji Mheshimiwa Tabasamu kwamba kwa ukubwa wa hoja ambayo anaizungumza inayohusu uzalendo wa nchi nimemwomba Mheshimiwa Tabasam nimpe taarifa kwamba ni vizuri Waziri wa Nishati atakapokuja ku-wind up atoe commitment ya kumpa ulinzi kwa ajili ya usalama wake pia.

SPIKA: Bahati mbaya hahusiki sana na masuala ya usalama; endelea kuchangia Mheshimiwa Tabasam, Serikali imesikia.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naendelea kukushukuru. Ninachotaka kukwambia ni kwamba hapa tuna mambo mengi sana kuhusiana na hili suala la vinasaba. Hivi vinasaba inaweza ikaandaliwa bajeti tu ya kununua vinasaba vya mwaka mzima ambavyo haviwezi kuzidi bilioni 10 au 15, huyu TBS akaendelea kuweka na ile hela ambayo ilikuwa inakwenda TBS au GFI yote iletwe TARURA. Haya maneno gani haya? Kwa sababu lile ni shirika la Umma linawajibika kufanya kazi ya Umma. Hizi pesa tuziokoe ziende huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza na wewe naomba tu nitoe ushauri wangu mdogo sana kuhusiana na hili suala la umeme. Hili suala la umeme kwa mfano sasa hivi tunapata shida sisi ya kusambaza umeme vijijini, nguzo zipo. Haya, utengenezaji wa nguzo TANESCO sasa ifikie mahali inunue mashine yake ya kokoto, inunue mashine ya kutengeneza nguzo, iwe na mashine yake itengeneze nguzo migogoro hii iishe.

Mheshimiwa Spika, lakini suala hili la kufanya kazi hizi kwa kutumia wakandarasi, tunashukuru Mungu tunakwenda kwa kasi, vifaa vingine vinatakiwa viwe vyetu. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa uzalendo wako, endelea kuwa mzalendo hivyo hivyo; Naibu Waziri, endelea kuwa mzalengo; Katibu Mkuu, endelea kuwa mzalendo. Simamieni hii hali ya mafuta.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunakuomba utuuonge mkono katika hili suala sisi Kamati ya Nishati na Madini kwa kazi nzuri tuliyoifanya kuishauri Serikali kuwaondoa GFI. Tupigiwe makofi ndani ya hili Bunge. Lakini habari hii hapana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia taarifa ya CAG. Ni kwamba Wabunge wengi wamezungumza hapa kwa hisia kali, na wanaonesha wanavyoguswa namna upotevu wa fedha za Serikali. Hata hivyo kitu kinachonishangaza ni kwamba; mimi nilikuwa naangalia pamoja na ugeni katika Bunge hili kwa miaka miwili. Taarifa hizi zinazosomwa hapa za CAG ni hadi tarehe 28 mwezi wa pili mwaka huu. Sasa, kutokea mwezi wa pili mwaka huu tunakuja kusoma taarifa hizi kuja kuanza kuzichambua, ni mwezi wa kumi na moja, tofauti yake ikiwa takribani miezi kumi au tisa ipo pale.

Mheshimiwa Spika, sasa hapa kunakuwa na ombwe kubwa sana hapa katikati; mambo mengi yanakuwa yamekwishakuharibika au yanakuja kurekebishwa wakati taarifa hii inaonekana kama inakuwa imepitwa na wakati. Kwa sababu kuna jambo linakuja kuzungumzwa hapa sasa hivi, limeshafanyiwa kazi. Sasa tunauliza, kwa nini hili jambo tusianze tu baada ya taarifa ya CAG kuletwa na kupelekwa kwa Mheshimiwa Rais ikapokelewa. Pale pale, Kamati yako ya PIC ianze kazi hapo hapo, halafu na Bunge hili la Mwezi wa Tatu, tuanze kujadili kwa siku nyingi siyo hizi siku tisa; twende kwa siku 30 ili tuweze kuwaadabisha hawa watu.

Mheshimiwa Spika, fedha zinazopotea ni nyingi sana. Leo mimi nimekuja na vitabu hapa, yote nimeyasoma, nilikuwa naangalia. Hiki ni kitabu tu kwa ajili ya Sengerema peke yake, Jimbo langu, ninapotoka mimi. Hii ni kwa ajili ya Serikali za Mitaa, taarifa hii ni kwa ajili ya mashirika ya umma. Sasa ukichukua hizi taarifa na hii nyingine niliyonayo hapa, yakikaguliwa haya yote, hata yakisomwa haya, bado hatuwezi, sisi Wabunge, kwa nafasi yetu finyu na ratiba zetu za Bunge hatuwezi kwenda sawa kuzichokoa zote hizi tukaziweka zote hapa kwako. Kamati yako hii ya PIC pamoja na kazi nyingi ulizokuwa umeipa. Wanazunguka sana na hao wanaokwenda kuwaita kwenda kwenye hao mashirika ya umma au taasisi za Serikali wanaonesha wana kiburi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa hili Bunge lako tunataka kujiuliza, je, tulichokosea hapa ni wapi? Ni mfumo wetu wa Bunge? Tuangalie Mabunge ya wenzetu kule Jumuiya ya Madola yanashiriki vipi katika shughuli hizi zinazoletwa na taarifa ya CAG kuzifanyia kazi. Tukijifunza kwa wenzetu tukaona wanadhiti namna gani hili jambo, halitajirudia. Hapa kuna taarifa za tangu mwaka 2011. Kwa hiyo, wameshaona taarifa hizi zinazoletwa hapa labda zinaletwa kama taarifa za mapato ya harusi au zinaletwa hapa za michango ya kanisani, kwamba labda hii michango haitakaguliwa au michango ya msikitini.

Mheshimiwa Spika, lakini hizi ni fedha za kodi za wananchi, tukiwemo sisi Wabunge, tunakatwa kodi, na wewe unakatwa kodi kwa sababu na wewe ni Mbunge. Sasa, ifikie mahali tuje na maamuzi makali, kwa sababu sasa hivi naangalia hiki kitabu kimoja, kinazungumzia taarifa zilivyo pamoja na vielelezo. Sasa najiuliza tuje na sheria, tukuombe hapa umwambie Mwanasheria Mkuu wa Serikali aje na sheria ya kuiongezea meno kumuongezea meno CAG. Kwa sababu akimaliza kukagua anawaomba wale watu walete vithibitisho; taarifa zinazokosa vithibitisho ndizo zinaletwa hapa kama zimeiva vilivyo; kwamba hizi ni sahihi; kwa nini asiwapeleke Mahakamani moja kwa moja, huyo huyo CAG, kwa sababu yeye ndiye mwenye ushahidi na watoa ushahidi anao yeye? Hao watu baada ya hapo wanapelekwa TAKUKURU, hili jambo linakwenda kufia kule na hawa watu unawaona wanaendelea kupata vitambi, wanapiga miluzi barabarani na mwaka kesho, tunakuja kujadili taarifa nyingine tena ya CAG.

Mheshimiwa Spika, mimi napata kigugumizi sana. Mama yetu Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu kama sasa hivi tunavyomuona anavyosafiri, leo yuko China, sijui kesho kutwa ratiba yake inasemaje hayo ni mambo ya kiitifaki. Lakini anapokwenda huko anakwenda kutafuta hizi fedha, na bahati mbaya fedha hizi zingine zinazoletwa ni madeni. Sasa zikija hizi fedha hapa zinakuja kuibiwa, na tunakuja tena na taarifa nyingine mwezi wa pili tena, mwaka kesho tutapokea vitabu vingine kama hivi; hivi havijafanyiwa kazi anachukuwa vitabu vingine. Sasa mama anahitaji usaidizi wa hatua akali kabisa, zibadilishwe hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa sababu sehemu ya Mawaziri na Manaibu wanatoka kwetu sisi kama Wabunge, na sisi ni wenzetu wale, lakini kule wanakokwenda kufanya nao kazi ni watendaji na wataalamu wa Serikali. La sivyo, taarifa zitakuwa zinakuja tunaondoka na Mawaziri, kesho tena tunaweka Wabunge wengine, tuanondoka nao. Sasa inaonekana tunajipiga sisi kwa sisi. Sasa jamani Wabunge ninachotaka kuwaambieni humu ndani, tukiwa pamoja lazima tuombe sheria kali kwa hawa watu; na anayetajwa na taarifa ya CAG kwanza hawa watu wangekuwa wako nje na wanaripoti polisi kila siku, mpaka kazi zao ziishe na mishahara ikatwe. Tuunde sheria kama hiyo, watu wataacha kucheza na hizi fedha (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilichonisikitisha zaidi kumbe mpaka sasa na Ubalozini fedha zinaibiwa, tena Ubalozi wa heshimia kama Marekani. Naangalia hapa mimi fedha za visa tu ambazo zimeibiwa ni takriban milioni 670. Kule kule Marekani tumenunua jengo dola milioni 25 na lile jengo lilikuwa na sehemu za kukodisha lina floor sita na katika lile jengo floor mbili zinafanya kazi. Floor nne hazifanyi kazi na wateja waliokuwa katika zile floor nyingine nne wamehama kwa sababu ya kushindwa kukarabatiwa lile jengo. Tumepata hasara shilingi bilioni 27 sawa sawa na vituo vya afya zaidi ya 70.

Mheshimiwa Spika, sasa huyu mama sijui tutamsaidiaje? Sisi Wabunge ndio tunatakiwa tumsaidie. Kama na mabalozi na wenyewe tena, ndio watu wa heshima, anaondoka anakwenda kule, balozi tena anakuwa naye ni sehemu ya upigaji, hii nchi sasa ni hatari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naangalia hapa Ubalozi, sijui wa Uholanzi, Addis -Ababa, Kampala, Berlin; yaani hakuna balozi hapa ambaye yuko salama. Sasa kama tuna mabalozi 43 tunaibiwa fedha kiasi hiki, hata fedha za visa, wageni ambapo wanapita, yaani watu hawaogopi. Kwa sababu mgeni anayepita, atapitia mipakani uwanja wa ndege, taarifa ziko kote, halafu na hizo na zenyewe zinaibiwa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuja kwenye suala la Msajili wa Hazina. Hii KADCO ni sehemu tu ya kampuni ambazo ninyi mnaziona ambazo Msajili wa Hazina anazo ambapo kule Msajili wa Hazina ninyi mnaona hiyo ni sehemu ndogo tu, kuna TIPER kule. Pale TIPER kuna tatizo kubwa. Tuna wanahisa wenzetu pale. Msajili wa Hazina ni sehemu ya mtu ambaye anatakiwa kuitwa aje aoneshe mashirika yote ambayo sisi tuna hisa, tunayoyamiliki na watu wengine tofauti, yaje yakaguliwe na Kamati hii ya PIC.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hali hiyo, bado kuna PUMA. Kule PUMA, kumenza kuuzwa kwa sababu kuliuzwa Sheli, Sheli wakauza kwa BP na BP wakaenda kumuuzia PUMA. Sasa hivi PUMA sijui wanaenda kumuuzia nani tena! Kwa hiyo, kote kule Msajili wa Hazina na kwenyewe kule tuna mali zetu, siyo sehemu hiyo tu. Kwa hiyo, yaletwe mashirika yote halafu Msajili wa Hazina atakuwa anasema hapa hakuna fedha, hapa fedha ziko hivi.

Mheshimiwa Spika, pia tuna uwanja nyuma ya Chuo cha Mwalimu Nyerere pale Kigamboni na lile eneo linalozunguka katika hayo maeneo. Huu uwanja uko wazi, zaidi ya ekari 60 au 100 ziko pale, lakini ICD ziko Dar es Salaam sasa hivi kila kona, watu wanavunja nyumba wanaanza kuhifadhi makontena. Barabara ya kupeleka haya makontena kule kwenye huo uwanja ambao uko bandarini pale pale ng’ambo ya bandari, tungeweza kuweka makontena, haya makasha yote. Kasha moja linaanzia Dola 250 na kuendelea. Tungehifadhi makasha pale, hizi tozo zisingekuwepo. Inaonekana usaidizi kwa Mheshimiwa Rais bado hajapata watu sahihi wa kumsaidia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pamoja na mambo mengine, hivi viwanja ambavyo majengo yanavunjwa; anaonesha hapa CAG. Viwanja vinavunjwa na vile viwanja vinakaa wazi. Si tungekuwa tunaweka haya makasha matupu na yenyewe yakawa ni sehemu tu ya ICD kule, mpaka siku watakapokuja kujenga hayo majengo, tuanze kupata hizo fedha za kontena. Kwa hiyo, mahali pa kupata fedha papo na CAG hapa anatuonesha.

Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha, CAG hapa amenishangaza mimi anasema, zaidi ya mashirika 60 ya Serikali hayana Bodi za Wakurugenzi. Sasa ni maajabu. Bado
anasema CAG ameshindwa kwenda kukagua… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Malizia sentensi, dakika moja.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, CAG ameshindwa kwenda kukagua hizi Bodi za Wakurugenzi kwa sababu sheria inamruhusu Katibu Mkuu wa Wizara husika kusimamia tu kwa muda wa miezi 12. Baada ya miezi 12, CAG hawezi kwenda pale wala Katibu Mkuu hawezi tena kwenda katika lile shirika. Kwa hiyo, wale Wakurugenzi (directors) waliobakia kule walewe wanaendesha yale mashirika kama mali zao binafsi. Imenitia hofu sana.

Mheshimiwa Spika, pia pale pale kuna bodi ambazo ni za muhimu sana katika nchi hii. Kama Bodi ya Pamba; unakuta Bodi ya Pamba na ya Mbolea; leo tunatoa ruzuku ya mbolea, hakuna Bodi ya Wakurugenzi kule.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Sengerema naomba ushauri wangu kwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mpango. Nimeangalia Mpango wake nimeusoma vizuri uliowakilishwa hapa na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa niaba yake, lakini kuna maeneo ambayo nataka nipite katika kuishauri Serikali katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kelele nyingi zimepigwa na Waheshimiwa Wabunge hapa kuhusiana na TARURA, wamezungumza sana kwamba TARURA iongezewe pesa na wengine wamekwenda mbali zaidi wakitaka pesa za kuongeza TARURA zitoke katika mafuta. Sishauri mafuta yaongezwe bei kwa sababu anayeumia ni mwananchi wa chini, mwananchi maskini na mfumuko wa bei utakuwa ni mkubwa sana na sisi tunajitahidi kupunguza mfumuko wa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kuhusu TARURA; kwa Waziri wa Serikali za Mitaa ni kwamba TARURA wabadilishe mfumo wao kwa hiki kidogo kilichopo. Hawa ma engineer wa TARURA waliopo katika miji, manispaa, majiji na halmashauri zetu wapewe mikataba performance watakayoifanya katika maeneo yao ndiyo itakayowapa nafasi ya kurudi. TANROADS wametoa mikataba kwa ma- engineer wao wa Mikoa na wamefaulu kwa mfumo huo. Haiwezekani meneja wa TARURA anaharibu, anahamishiwa sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ushauri wangu pia kwa Waziri Mpango katika Mpango huu aliyenao na kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, hawa TARURA sasa hivi waruhusiwe kufanya kazi za force account, tutaona matokeo yake. Kwa mfano, katika wilaya yangu, halmashauri moja tu, Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, tuna kilometa 1,730, bajeti milioni 607, haiwezekani! Ukichukua kwa bei za TANROADS ambazo zipo za mikoa, kilomita moja inaanzia milioni 15 mpaka milioni 20. Kwa hiyo, milioni 600 inatengeneza kilometa thelathini na una kilometa 1,700, kwa hiyo nahitaji miaka 50, wakati huo nitakuwa nimeshindwa uchaguzi na nimezeeka na nimestaafu. Wabunge wote hakuna atakayerudi kwa mfumo huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, TARURA waruhusiwe kununua mitambo na mitambo yenyewe watakayoruhusiwa kununua ni mitambo mitatu tu motor grader moja, roller compactor na roller excavator, vingine vinaweza vikakodiwa. Kwa hiyo, TARURA watatengeneza barabara kwa uzuri, pesa za TARURA zitatoka wapi? Hapa ndipo pazuri, ni kwamba uwagizaji wa mafuta katika nchi hii hapa kuna tatizo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wanapeleka Muswada huu wa kuagiza mafuta kuagiza mafuta kwa pamoja 2014; Muswada huu uliletwa hapa Bungeni kwa zimamoto, mbio mbio, sasa hapa ndiyo kuna tatizo. Kwa mfano, bei ya mafuta ya Januari, bei yake ilikuwa karibu shilingi 230 au 300 kwa lita, lakini bei ambayo imeonekana ipo kwenye kukokotoa kwa EWURA, bei ya mafuta imefika shilingi 708. Katika shilingi 708 ya petrol kuna nauli iko pale shilingi arobaini na tisa na senti. Mafuta yale ya petrol yamefika hapa shilingi 757 wakati bei halisi kwa wakati huo, mwezi Januari wakati yanaagizwa, hayakuzidi shilingi 300. Sasa kama nchi inataka kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi, hatukwepi sasa hivi nchi kuagiza mafuta yetu kama nchi, tuna matenki tipper yana mamilioni ya hifadhi, kwa nini tusinunue mafuta kwa shilingi 300. Katika nchi ambazo zinazouza mafuta nchi za OPEC wananauza mafuta haya kwa discount.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo bei ya mafuta ni dolla 160 kwa tani ambayo ni sawasawa na Sh.370 kwa lita. Kama huyo mwagizaji anayepewa tenda anayafikisha mafuta hapa kwa Sh.708, kuna gape pale karibu ya Sh.300. Hii ni hatari sana kwa uchumi wa nchi, sisi tunalalamika hatuna pesa, halafu tunawachia watu wanaagiza mafuta. Naomba ushauri wangu uzingatiwe katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Fedha, Mipango na Bajeti na Kamati ya Nishati na Madini, kwa ruhusa yako pamoja na Waziri wa Uwekezaji, tukutane kwa dharura, mimi naomba, tukajadili hili kwa manufaa ya nchi. Pamoja na tozo hizi, kuna pesa ambayo ni excise duty shilingi mia tatu na kitu, kuna pesa ambazo ni levy shilingi mia tatu na sabini karibu, kuna fedha ya petrol fees shilingi mia moja. Hizi ndiyo pesa zinazokwenda Hazina, zaidi ya shilingi mia saba, lakini kuna tozo, hapa ndiyo roho yangu inaniuma, kuna tozo ya shilingi 80 ya hizi mamlaka, zimeweka hapa pesa zao shilingi 85. Tukizichambua pesa hizi zitakazobakia halisia ni karibu shilingi 60, zitolewe kwa sababu hizi mamlaka ziko chini ya Wizara ambazo zinaleta hapa bajeti zao, tunawapitishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wapeleke kule wakapewe hela Hazina. Shililingi 60 itakayobakia hapa katika hiyo 85, ninachotaka kuomba, pesa hizo ziende TARURA, zinatosha kugharamikia barabara zetu. Haiwezekani tukaliacha hili jambo likapita na tukikutana leo kwa dharura, kesho tunakuletea majibu hapa na tunaondoa hili jambo. Tuishauri Serikali, tumshauri Mheshimiwa Mpango atengeneze bajeti, lakini kuna pesa kwenye mafuta huku zinapigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna GFI, hawa GFI hawa ni watu wanaweka marking katika mafuta wanachukua shilingi 14 kwa lita. Mauzo yetu ya mafuta ni karibu ni lita milioni sita mpaka 12 kwa siku. Huyu mtu anayechukua shilingi kumi na nne anaondoka na pesa zaidi ya milioni 90, kila siku ya Mungu huyu mtu anachukuwa milioni karibu kumi na mbili kwa mwezi, kwa mwaka na gharama za marking kuweka ile dawa ya marking utaona Finland na wapi, nchi zote zinazouza zinauza gharama ndogo sana. Mtu huyu ana wafanyakazi wawili wawili kila depot katika nchi hii ambao hawazidi wafanyakazi sabini, anachukua shilingi 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna EWURA sijui anachukua shilingi ngapi, kuna watu wa mizani wanachukua pesa pale, kuna watu wa survey kuangalia tu mafuta yamepita kwenye bomba hii shilingi 85, mambo mengine naogopa hata kuyasema hapa kwa ajili ya usalama wa nchi, haiwezekani! Naomba turudi mezani tufukue hii kitu Waziri wa Nishati hiki kitu wakati kinapitishwa hakuwepo, Waziri wa Fedha hakuwepo, Waziri wa Uwekezaji hakuwepo. Naomba kutumia Bunge hili kwa hizi kamati tulizopo, iwe ni msaada katika nchi, turudi mezani kwa amri yako, halafu kesho tuje na majibu. Hawa watu wote ambao wanaingiza tozo zao hapa uagize waje hapa Bungeni haraka leo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Aaaaaa.

Ndiyo ninachotaka kukwambia.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tabasam, dakika kumi zimeisha.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kukwambia pamoja na hali hii, naomba tamko lako ili tuokoe hii pesa, tupate pesa za TARURA, tutengeneze barabara zetu. Ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika Wizara ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa dada yangu Mheshimiwa Mhagama kupata uteuzi huu katika Ofisi hiyo, lakini pia mdogo wangu Ndejembi kupata nafasi hiyo nina imani wanakuja kufanya kazi kwa weledi kwa ajili ya kuwasaidia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimpe ushauri Mheshimiwa dada yangu Mhagama katika jambo la kwanza; namwomba sana atengeneze clinic za kusikiliza matatizo ya wastaafu katika nchi hii, atengeneze Makamishina Wasaidizi waende katika mikoa, wazee wastaafu wanapata shida sana, wanatembea na mafaili, mtu anakwenda kustaafu ana mwaka mmoja hajalipwa mafao yake. Sasa hili ni tatizo kubwa sana. Serikali inapata dhambi bila kujua tuna shangaa mvua hainyeshi, kwa sababu kuna watu wamedhulumika haki zao, hizo zinaitwa dhambi baridi. Kwa hiyo, wawatendee haki hawa wastaafu, mtu ameajiriwa, amefanya kazi Serikali miaka 40, halafu bado unamwomba akulete salary slip ya kwanza aliyoajiriwa nayo, akuletee barua ya uteuzi, ana miaka 40 ameitunzaje hiyo kitu. Sasa hii ni hatari kubwa sana, hizi dhambi hebu waziache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akiweka makamishna wakasikiliza, wanatoka katika wilaya anakuja, kwa mfano, akitoka Sengerema katika Jimbo langu anakwenda Mwanza nauli Sh.3,000 anapeleka hoja zake pale, anasikilizwa, anarudi na wale makamishna waje pia katika Makao Makuu ya Wilaya wanasikiliza kesi za wastaafu. Kwangu kuna askari mmoja ana miaka 40 amefanya kazi Serikalini halafu amekosa pesa za kumsafirisha kurumrudisha kwao, hazipo. Sasa hii ni tatizo kubwa sana, ametumikia kwa uweledi na kwa uaminifu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, Mheshimiwa Waziri ni suala la hawa watumishi ambao ni Makatibu Tarafa na DAS. Sasa ifikie katika nchi hii tubadilishe huu Muundo wa Utumishi hawa wapo kwa Mheshimiwa Waziri kwenye utumishi lakini asilimia 98 wanafanya kazi TAMISEMI. Hebu waangalie huu muundo haujakaa vizuri, wanaishi kwa shida, wanafanya kazi, ni watumishi wa Wizara ya Utumishi, lakini wakati huo wanafanya kazi za TAMISEMI, wakiamka asubuhi ni kazi za TAMISEMI, lakini mwajiri wao ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais. Sasa hili ni tatizo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bajeti zao, unakuta Katibu Tarafa ana Kata 13, hana pesa za madaraka, lakini waliopo chini yake Mkuu wa Shule, sijui nani, Waratibu, Watendaji wa Kata, wote wana fedha za madaraka, Katibu Tarafa hana, hana Ofisi Katibu Tarafa na hao Makatibu Tarafa wanahitaji wasaidizi, lazima wapate Makatibu Muhtasi wale wa kuwachapia barua zao, lakini wawe na matarishi wa kupeleka zile barua pia, Wahudumu wa Ofisi, sasa hao Makatibu Tarafa wanakaa kule kama nani, lakini wanafanya kazi kubwa sana za kumsaidia Mheshimiwa Rais, wao ndiyo wa kwanza kupata taarifa, wanapeleka kwa Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Wilaya anapeleka kwa Mkuu wa Mkoa, inafika sasa waheshimike hao Makatibu Tarafa. Makatibu hao hawana usafiri na kama wana usafiri hawana mafuta. Kwa hiyo, Mkurugenzi hawajibiki kumpa mafuta yule Katibu Tarafa, sasa hili ni jambo ambalo liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa ma-DAS wetu sisi pia wanaishi kwa hisani ya Mkurugenzi wakati yeye DAS ndiyo anatakiwa akamsimamie Mkurugenzi katika utendaji wake wa kazi. Hili naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie na kwake sina mashaka yoyote, hili atafanikiwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la kupata mafunzo Wakurugenzi wanaitwa sana, wao ndiyo watendaji, kwa miezi mitatu anaweza akaja Dodoma mara sita, lakini DAS ambaye ndiyo msimamizi wa shughuli zote za wilaya kupata mafunzo Mungu nihurumie sijui wanakuja lini kupata mafunzo, sasa hili ni tatizo. Akiitwa Mkurugenzi kupata mafunzo basi na DAS aitwe, kwa sababu ndiyo mtendaji wa shughuli za kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la pili ambalo nataka nizungumze na Mheshimiwa Waziri katika kukushauri, ni suala la TASAF, TASAF imekuwa ni mtihani mkubwa katika nchi hii. Waheshimiwa Wabunge wote anaowaona hapa katika majimbo yao wana malalamiko ya TASAF. Kwa kuwa yeye ni Waziri na ana Naibu Waziri basi mmoja ashughulike na kutembea nchi nzima kuona matatizo ya hawa wazee wetu wanaopata misaada hii ya TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu siyo mzuri unaambiwa kwamba wazee wanalipwa kwa mtandao, mzee hajui kusoma na kuandika, halafu leo alipwe kwa kutumia mtandao, pesa ya swadaka tena inakwenda kudhulumiwa umeshaona wapi. Serikali inatoa msaada na ule msaada unakwenda kuibwa tena. Sasa hili jambo la TASAF liangaliwe, hawa wazee wetu kwa sababu tayari tumeshawaweka katika huo mfumo.

Vilevile wanaokwenda kupewa hizi pesa za TASAF kuna wengine wana nguvu, lakini ni ndugu wa mtu Fulani, hilo ni tatizo na unaambiwa kwamba kwa sababu labda ni balozi wa CCM, hana sifa kwa sababu anafanya kazi kama balozi wa CCM au sijui balozi wa chama gani? Haiwezekani kwa sababu kile ni cheo ambacho anacho hakina mshahara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la watumishi nimesikia humu Wabunge wanalalamika kwamba watumishi wa kike wanakuwa hawakai katika maeneo yao, hapa natoa tu ushauri kwamba, wazungumze na watu wa Ustawi wa Jamii waliopo kule katika wilaya, lakini nataka nimshauri pia Waziri atuambie na sisi Wabunge kule waache malalamiko haya kwa sababu ukisikia mtumishi anahama kwamba eti hakuna huduma muhimu hasa hawa mabinti wa kike wanaokwenda katika maeneo kama Walimu, Manesi na watu wengine kwamba hakuna huduma muhimu, siyo huduma hizo ni huduma za kifamilia, waolewe kule tuwaambie watu wetu waoe.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakwenda kufanya mkutano kwenye kata anayelalamika, Diwani analalamika Mheshimiwa Mbunge wanakuja watumishi wanaondoka, analalamika Mwenyekiti wa Kijiji, sasa unamwambia mbona ninyi mna tatizo…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naheshimu mchango wa kaka yangu Tabasamu, mabinti au wafanyakazi wa kike hawahami kwa hicho anachokisema, wengi wanapata shida mazingira magumu ya kazi ikiwepo nyumba na gharama za usafiri kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine, halipo suala la uchumba au kuolewa hapa. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasamu, unapokea taarifa?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa hii, kwa sababu ninachotaka kukwambia, akisikia kwamba mazingira magumu, ni haya ya kifamilia. Mwanamke akipata hayo, hawezi kukimbia wala kuondoka kwa sababu ya nauli. Kwa hiyo, ushauri wangu, hawa wananchi huko kwenye Majimbo yetu wasichague wakaweka ukabila kwamba amekuja Mzaramo asiolewe na Msukuma, waoeni Wasukuma. Hii massage mimi ndio napeleka. Amekuja Mgogo, eti kwamba kaletwa hapa Nurse Mgogo, muoeni huyo Mgogo. Kwa sababu utafiti uliopo kwanza ni kwamba familia ya Walimu, watoto wa Walimu ndio wanaofanikiwa kuliko Walimu. Sasa leo mnakuja kulalamika kwamba Mheshimiwa Waziri… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kuna Mheshimiwa Mbunge amesimama. Mheshimiwa Esther Matiko, umesimama kwa kanuni gani?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, akija Mnzanzibari aolewe.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam!

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Naam.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa...

MWENYEKITI: Umesimama kwa kanuni gani?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kwa kanuni ya 77 kutoa taarifa.

MWENYEKITI: Endelea.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa Mheshimiwa Tabasam taarifa kwamba wanaoomba kuhama ni both sides, wanaume kwa wanawake, lakini anapojielekeza kwa wanawake, nimpe tu taarifa tu kwamba nature ya wanawake ilivyo anaweza akavumilia muda mrefu hayo anayoyasema bila kuathirika kuliko wanaume walivyo. Kwa hiyo, naomba ajenge hoja yake bila kudhalilisha jinsia nyingine. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wakati Mheshimiwa Mbunge anazungumzia kuhusu kuhamisha watumishi, wengine unakuta tayari wako kwenye ndoa zao, wanataka wahame wawafuate wenzi wao. Kwa hiyo, ajenge hoja bila kuweka udhalilishaji wowote ule. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam, unapokea taarifa hii aliyoisema Mheshimiwa Matiko?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo hoja yake. Siipokei kabisa taarifa yake. Naomba ulinde muda wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wanaume wanaokuja katika maeneo yetu vijijini, nao wanakosa watu wa kuwaoa kwa sababu tu kwamba amekuja Mmasai pale au amekuja Mzaramo kule Usukumani, na huyo Mzaramo aruhusiwe kuoa Msukuma, ndiyo haja yangu mimi. Watumishi watabaki kuwepo.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naona hizi taarifa zinakula muda wangu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam muda wako umekwisha. Nakuongezea dakika moja kwa ajili ya kuhitimisha hoja yako. Kaa chini Mheshimiwa Bulaya.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la watumishi, Serikali itaajiri watumishi 32,000. Ushauri wangu ni kwamba katika hao watumishi 32,000 tunayo Majiji yetu saba, wapewe mia tatu, mia tatu; na Makao Makuu ya Wilaya tupewe mia mbili mia mbili. Huko ndiyo tunafanya upekuzi, tutawajua watu wetu. Huu ndiyo Utaifa. Habari ya kuingia online halafu wanaenda kuajiriwa watu wa mkoa mmoja, hatukubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanteni sana kwa mchango huo. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema, naomba kuchangia hotuba ya Bajeti ya Serikali za Mitaa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza kabisa, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kumteua Mheshimiwa Ummy Mwalimu kuwa Waziri wa Serikali za Mitaa. Ni kwamba mashine iliyotoka ilikuwa ni ya kusaga na kukoboa na mashine iliyoingia sasa hii ni ya kusaga na kupepeta. Kwa hiyo, shukrani sana Mheshimiwa Samia kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najikita katika sehemu ya utawala bora katika Halmashauri zetu na Serikali za Mitaa katika nchi hii. Serikali imekuwa ikitafuta fedha hizi kwa shida; inakusanya kodi kwa wananchi kwa ajili ya kuhudumia miradi ya maendeleo iliyopo katika Halmashauri zetu. Hii miradi inayopewa fedha ni ya maendeleo kwa ajili ya kuwaondolea wananchi kero na adha walizonazo katika miradi ya elimu, afya, barabara, maji na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa na utaratibu wa kufanya kazi zake za miradi ya maendeleo za ujenzi kwa kutumia force account. Utaratibu huu umekuwa na mafanikio kwa ajili ya kupunguza gharama za uendeshaji katika miradi hii katika nchi nzima. Kuna maeneo hatua hii imekuwa ni sehemu ya chaka la kuibia fedha za Serikali kwa kiwango cha kuchota kwa koleo; siyo kiwango cha kuchota kwa kunywa kwa mrija; zinachotwa kwa koleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, katika Jimbo la Sengerema, namshukuru sana aliyekuwa Waziri wa Fedha na sasa hivi ni Makamu wa Rais, kwani nilikwenda kwake katika kumlilia kuhusu fedha za miradi ya maendeleo ambazo zimekwama katika Halmashauri ya Sengerema na bahati nzuri nilipewa fedha karibu shilingi 2,212,000,000/=. Fedha hizi zilikuwa katika mgawanyo ufuatao:-

Mheshimiwa Spika, kuna fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Wilaya shilingi milioni 749 ambazo ni za kuanzia. Wakati huo huo nikapewa fedha nyingine kwa ajili ya ujenzi wa madarasa kumi shilingi milioni 125. Bado nikapewa fedha tena shilingi milioni 188 kwa ajili ya kumalizia maabara zilizojengwa na wananchi kule kwa nguvu zao wenyewe kwa ajili ya kufanyia finishing; nikapewa fedha nyingine kwa ajili ya kumalizia zahanati shilingi milioni 150; na nimepewa fedha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kumalizia Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, kipi kilichotokea katika hali hii? Kule kuna kazi. Kwa mfano, kazi moja tu ya ujenzi wa Halmashauri ya jengo la Halmashauri kwa kutumia nafasi hii ya kuwaachia wazi hawa Wakurugenzi wetu, tayari hao ma-engineer na watu wa manunuzi wanatumia nafasi hii kuchimba msingi na kujenga msingi wa jengo la Halmashauri hiyo na structure za nguzo fundi analipwa shilingi milioni 160. Hii ni hatari kubwa sana. Jengo ni dogo, halina upana wowote. Sasa kama kwangu Tabasam kuna hali hii, je, katika Halmashauri nyingine karibu 200 kukoje?

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Ummy Mwalimu akija kumalizia hotuba yake, atoe na majibu kwa hili, kwa ajili ya ndugu yake mimi Tabasam, vinginevyo nitaing’ang’ania shilingi na kama hali hii kule Sengerema itaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Spika, katika ujenzi huu kuna hii shilingi bilioni moja inajenga majengo matano. Wodi inajengwa kwa shilingi milioni 204; kuna ujenzi wa kujenga incinerator, hii tu ya kuchomea takataka shilingi milioni 30. Kajengo kadogo, yaani kakizimba, sijui tunaitaje kwa Kiswahili, maana yake ni kichomea taka, kwa shilingi milioni 30. Jengo kwa ajili ya kufulia nguo shilingi milioni 115; jengo kwa ajili ya mortuary ambayo haina cold room shilingi milioni 130. Hii ni hatari kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, hili suala la Sengerema Mheshimiwa Ummy, unafahamu kuna Wakurugenzi wengine wanajua tayari wanatakiwa kuondoka, kwa hiyo, wanafanya haraka sasa kunyakua hizi hela. Nakuomba sana uzuie matumizi ya hizi fedha kule Sengerema haraka iwezekanavyo. Peleka timu ikaangalie ile hali iliyoko kule, kuna wizi wa kutisha! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri hizi tunashangaa zinapewa hati safi, lakini Sengerema imepewa hati yenye mashaka. Ni maajabu makubwa! Kuna fedha zinazokusanywa katika hili suala la utawala bora na makusanyo ya Halmashauri ya fedha za masoko na magulio katika own source. Fedha za kwenye kutumia POS hizi mashine za kukusanyia ushuru shilingi milioni 350 zimeibiwa, lakini watumishi bado wapo kazini.

Mheshimiwa Spika, katika hali hiyo, alikuwepo pale DT Sengerema, ameondoka na shilingi milioni 250. Pamoja na Mheshimiwa Jafo kuja Sengerema na kuagiza kwamba wakamatwe mara moja, bado wapo kazini. Mheshimiwa Jafo aliagiza watu wa TAKUKURU Mkoa wafanye kazi hiyo, jamaa anaendelea kupeta na anaendelea kula ulanzi huko kijijini. Hii ni hatari kubwa sana katika nchi hii!

Mheshimiwa Spika, huko kwenye Wizara ya TAMISEMI ndipo ambako ni chaka la kupotezea pesa za Serikali. Ukisikia pesa za Serikali zinakusanywa; na tundu lipo wapi? Tundu lipo kwenye Halmashauri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ummy Mwalimu una kazi kubwa sana dada yangu. Una kazi kubwa sana kwenye kuzuia hilo tundu. Atakuwa anachota Mheshimiwa Mwigulu Nchemba halafu tundu kule linatoboka na wananchi wanaendelea kupata shida.

Mheshimiwa Spika, tunavyozungumza na wewe hapa ni kwamba majengo ambayo yanafanyiwa kazi kule hayalingani na thamani ya fedha. Wanaleta maelekezo kutoka TAMISEMI yanakwenda kule kwamba jengo moja la kumalizia kupiga ripu na kumalizia bati shilingi milioni 12, siyo kweli. Wananchi wanajenga jengo, wanamaliza boma kwa shilingi milioni sita, halafu kulimalizia jengo, kupaka rangi na kuweka madirisha na milango shilingi milioni 12; ni jambo ambalo halikubaliki.

Mheshimiwa Spika, kuna haya maboma ambayo anayataja Mheshimiwa Ummy Mwalimu katika hotuba yake; maboma yaliyopo kwetu kule ni mengi. Halmashauri moja kama Sengerema tu ina maboma karibu 200 na kitu. Sasa maboma haya hatujaambiwa yatatekelezwa namna gani. Haya maboma hayako kwangu tu, yapo karibu kwa Wabunge wote wanaotoka katika Halmashauri za Wilaya. Wanayo maboma ya kutosha; maboma ya zahanati hatujaelezwa kwamba kuna maboma labda 1,000 yatatekelezwa hivi; ya zahanati, kuna maboma ya madarasa, kuna maboma ya nyumba za walimu, kuna maboma ya vituo vya afya yatamalizwa namna gani? Hili hatujaelezwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ummy katika hotuba yake amesema amekarabati shule, mimi nashukuru. Shule ya Sengerema Sekondari imekarabatiwa kwa shilingi bilioni 1.2 lakini shule hii…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. Ahsante Mheshimiwa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Namwomba tu Mheshimiwa Ummy Mwalimu aangalie suala la Sengerema kwa upande wa watumishi wake kuanzia Mkurugenzi, Engineer na DT, ni kwamba tayari sasa hivi wanajua safari yao imeiva, wanataka wanyakue hizi fedha haraka. Nakuomba sana uzizuie hizi fedha kwa haraka sana. Hizi fedha zizuiwe leo dada yangu, la sivyo nitakunyang’anya shilingi.

Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bajeti hii ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niko katika maeneo mahususi kama matano. Eneo la kwanza ambalo naomba kuelekeza mchango wangu ni miradi inayokuja katika maeneo ya majimbo yetu na miradi inayopelekwa katika halmashauri zetu nchini. Wasimamizi wa miradi hiyo ni Waheshimiwa Madiwani tukiwemo sisi kama sehemu ya Madiwani katika maeneo yale. Lakini pia wasimamizi wengine ni wenyeviti wa serikali za vijiji, na tatu, wapo wenyeviti wa Serikali za Mitaa na vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uwiano wa mapato na matumizi; kinachopelekwa kule katika bajeti zetu unakuta halmashauri inapewa bajeti ya bilioni 42, 46. Lakini wanaokwenda kusimamia bajeti ile ni Waheshimiwa Madiwani ambao wanapewa posho ya shilingi 300,000. Wapo watendaji wa kata wana mishahara zaidi ya shilingi 700,000 na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu uwiano kwamba Mwenyekiti na msimamizi wa shughuli za maendeleo za kata ni Mheshimiwa Diwani. Nilikuwa Diwani wa Kata ya Nyampulukano, Sengerema Mjini, najua matatizo wanayopata Waheshimiwa Madiwani katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, suala la Waheshimiwa Madiwani kupewa posho na posho zenyewe zinakuja kwa kuchelewa, jambo ambalo haliwezekani, halikubaliki hata kidogo. Taarifa ya CAG, wizi mkubwa unatokea katika halmashauri zetu, wasimamizi wa miradi ile ni Waheshimiwa Madiwani ambao mishahara yao, posho zao haziko katika sehemu ya ajira; haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mafiga matatu tunaachania wapi? Tukienda kutafuta kura tunatafuta kura za Mheshimiwa Rais, tunasema mafiga matatu; tunatafuta kura za Mheshimiwa Mbunge, tunatafuta kura za Mheshimiwa Diwani. Kwenye maslahi tunaachana; haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuwe wakweli; Chama cha Mapinduzi ni chama kikubwa katika Afrika, kina heshima katika Afrika, lakini kinaendesha Serikali ambayo ina matabaka. Kama Mheshimiwa Diwani hataingizwa katika sehemu ya ajira, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, dada yangu, nakupenda lakini safari hii nakamata shilingi kwa mara ya kwanza. Nimekuwa Mbunge huu mwaka wa pili nakwenda wa tatu, naangalia maslahi ya Madiwani, inashindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napata shida kule kuendesha halmashauri kama Mbunge. Kila tatizo linakuja kwa Mbunge; Diwani kwanza atasafirije, posho ya Diwani ya kikao, vikao vyenyewe vinahesabika. Diwani akiamka asubuhi ana watu kama nane nyumbani kwake; huyu mtoto anaumwa, mwingine anatakiwa kufanyiwa operation, nilikuwa Diwani, nilikuwa nayaona haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu huyohuyo Diwani ndio akasimamie madarasa. Sasa kama kuna mifuko kule kumi inatakiwa ijengee akiambiwa miwili Mheshimiwa Diwani na wewe utapata shilingi 20,000, kwa nini asikubali? Naomba sana jambo hili ulifanyie kazi tuone namna gani maslahi ya Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maslahi ya wenyeviti wa Serikali za vijiji; mapato yanakusanywa katika halmashauri zetu, ni kutoa mwongozo tu kwamba posho za Waheshimiwa wenyeviti wa Serikali za vijiji zitokane na halmashauri. Wapunguze katika mapato yao, tunapata asilimia 40, hii asilimia 40 iliyopatikana sisi inakwenda katika miradi yetu ya maendeleo. Asilimia 60 inakwenda kutumika kwa watendaji ambao wanaletewa OC, wana mishahara, wanaletewa OC, wana semina, wana kila kitu. Wapunguze kule wapelekewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina vijiji 71 katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema. Lakini wenyeviti wangu wa Serikali za vijiji posho watoe kwa Mbunge; hiki kitu hakiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja kwa Waheshimiwa wenyeviti na watendaji wa Serikali za Mitaa. Hawa wenyeviti ni kwamba wanapewa mishahara yao ni mihuri, na nilisikia mkuu wa mkoa mmoja anasema anataka kuwanyang’anya mihuri. Hiyo mihuri inasaidia mtu akienda kuuza mfugo wake katika mnada, Mheshimiwa mwenyekiti wa kitongoji ndiyo anapata 5,000; mtu anakwenda kuweka dhamana anapata shilingi 5,000. Hatuwezi kuwa na tabaka la utawala bora watu wengine wanaishi kwa mhuri halafu wanasimamia mapato ya halmashauri; haiwezekani hata siku moja. Hili ni jambo ambalo siwezi kulikubali mimi kama Mbunge wa Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kwenye uchaguzi mwaka kesho. Hawa wenyeviti wa Serikali za vijiji ndio wanakwenda kutoa sura ya nchi hii. Tunaanza nao wao kwenda kuwatafutia kura, tunawatafutia kura wakachaguliwe tu hatutafuti malshi yao; inakuaje Waheshimiwa Wabunge? Hili tunataka lije katika majumuisho ya Mheshimiwa Waziri, wanawekwa namna gani hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato ya halmashauri; mapato haya yako katika server moja katika nchi hii. Kule sisi tunaona kabisa kwamba kwa mfano nina maeneo ya mashine za mpunga zinapakia malori kumi, mtu akichomoa tu kile ki-server kinachokaa katika mashine anaanza kutoa risiti zinatoka na unaona kabisa lori moja pale lina shilingi 600,000, unaona hapa kuna milioni sita. Kwa nini wale wasipewe na wao password wakurugenzi waone? Sisi Wabunge kuna dhambi gani tukipewa password tukaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu unaona kabisa kwamba leo yamepakia malori kumi ya mbao, lakini unashangaa linalokwenda kulipiwa ni lori moja; haiwezekani. Mapato yaanaza kupigwa kuanzia huko chini. CAG anakuja kukagua kitu ambacho tayari kimeshaibiwa. Kwa nini msitupe password tukaanza kuona sisi hayo mapato? Kuchungulia. Kama tunaweza kuchungulia sisi kwenye statements zetu za benki, unaangalia kwenye mfumo leo tumeuzaje. Leo mtu mmoja tu anaangalia TAMISEMI nchi nzima; upigaji ndio uko kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unamwamini Mkurugenzi kumpa bilioni 42, unashindwa kumuamini mapato ya shilingi bilioni tatu; inawezekana wapi unashindwa kuwapa wao password wakaangalie kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya utawala, ametoka kuzungumza kaka yangu hapo; naangalia tu kama mikoa hii, Mkoa wa Tabora, tunaangalia Mkoa wa Morogoro, tuangalie Mkoa wa Geita ulivyo mkubwa, tunaangalia kuna wilaya ziko kubwa; Wilaya ya Kahama; Kiteto, Sengerema. Mimi Wilaya ya Sengerema kata zangu nne, kata moja tu ya Nyamatongo Katunguru, ukichukua Katunguru ukachukua na Ngoma B ukachukua na Chifunfu ni sawasawa na eneo moja tu la Jimbo la Nyamagana; kata nne. Ukichukua kata zangu tano, Igalula, Kagunga, Buyagu na Kishinda ni Jimbo la Nyamagana. Halafu leo hii tunavyozungumza hapa… (Kicheko)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: …mimi leo Mbunge nina kata 26; haiwezekani maneno kama haya.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge wa Nyamagana, taarifa.

TAARIFA

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa kaka yangu, Mheshimiwa Tabasam, tunapozungumza ukubwa wa Jimbo na bajeti, siyo ukubwa wa eneo ni wingi wa idadi ya watu waliopo kwenye eneo husika. Kwa hiyo, atambue kwamba anapoizungumza Nyamagana, anazungumzia Jiji la pili kwa ukubwa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam, unapokea taarifa hiyo?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa yake kwa sababu kwanza ninachotaka kukwambia, hiki ninachozungumza mimi ni sehemu ya taarifa ya sensa. Sengerema nina wananchi 500,000…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: …Ukichukua wananchi wa Jimbo la Buschosa 450,000, ni wilaya ya tatu katika nchi hii kwa idadi ya watu. Haiwezekani kitu kama hiki. Na watu wanaokwenda Nyamagana wanatoka Sengerema.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mnzava.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Waendelee kunipa hizo taarifa.

TAARIFA

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Tabasam, kwamba naungana na anachokisema kwa sababu hata ukiangalia kwa mfano Halmashauri ya Mji wa Korogwe ni ndogo kijiografia lakini kwa sensa ni watu 58,000, Korogwe DC ni kubwa kijiografia lakini kwa sensa ni watu 200,000 na. Lakini mara nyingi migao inatoka sawasawa.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa Mheshimiwa Tabasam?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, imekaa vizuri. (Makofi/Vicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumwambia Mheshimiwa Waziri wa Serikali za Mitaa kwamba idadi ya wanafunzi wa shule ya msingi kwangu ni 116,000, madarasa niliyonayo ni 950. Upungufu wa madarasa katika Halmshauri ya Wilaya ya Sengerema ni 1,600. Nyumba za walimu ninazo 52 tu, upungufu ni nyumba 600 za walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu nilionao hawatoshi kuwafundisha wale wanafunzi. Shule moja ya Chifufu, Shule ya Msingi Bugumbikisa ina wanafunzi 3,700, watoto wa awali 350, wanafunzi 4,000, walimu 22; hawa walimu kweli wako sawa na walimu wa Nyamagana? Shule moja ya Nyamagana ina wanafunzi 2,000 walimu 110; haiwezekani mgao kama huu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza na wewe tunaomba bajeti ya Serikali za Mitaa igawanywe kwa mujibu wa sensa. Mheshimiwa Rais karuhusu pesa, tumetumia zaidi ya bilioni 400 kwa ajili ya kuhesabu watu na makazi. Tuje kwenye bajeti kwa usawa, hakuna maneno haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatutakubali, safari hii bajeti hii itakuwa ni ngumu. Dada yangu nakupenda sana, umeangushiwa zigo bovu. Amesema Mheshimiwa Shabiby hapa, gari hili ni jipya lakini lina engine ya bajaj. Ninachotaka kukwambia anza kukarabati...

MWENYEKITI: Haya.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunisikiliza, Watanzania msikie haya tuliyoyasema. Safari hii mgao ni kwa bajeti, keki ya nchi hii tuipate wote. Hakuna haya maneno watu wengine wapate keki ya nchi hii, watu wengine tuwe wasindikizaji kwenye nchi hii, hapana. Hapana, hatukubali. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Sengerema, naomba kuchangia katika Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, napenda kuzungumzia kuhusiana na suala la wawekezaji. Tunao wawekezaji wengi ambao wamefanya kazi ya utafiti wa madini katika nchi hii. Wawekezaji hawa mpaka sasa hivi wako ambao wametoa taarifa zao na wako ambao taarifa zao bado hazijaenda katika Wizara kuonyesha kwamba wametafiti kitu gani na wamepata madini ya aina gani. Pamoja na hali hiyo, wako watafiti ambao tayari wameshamaliza utafiti wao na wako katika ngazi ya kupata leseni.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana mdogo wangu Mheshimiwa Doto Biteko, kafanya kazi kubwa sana. Kwa mfano, Sengerema tuna Mgodi mpya wa Nyazaga, ameshakuja Sengerema zaidi ya mara sita, tumefanya vikao pale. Vilevile tumeshakwenda na Waziri wa Uwekezaji wa wakati huo, Mheshimiwa Kitila Mkumbo tumepanda juu ya milima yote kule Nyazanga na wamemlalamikia kuhusiana na suala la kuchelewa kupata leseni. Wakati Waziri anakuja kufanya majumuisho ya bajeti yake, naomba anieleze lini leseni ya Mgodi wa Nyazaga itatoka? Kama hatatueleza leseni hiyo itatoka mwaka huu, leo ni mwaka wa nne, shilingi ya mshahara wake japo ni mdogo wangu nitaing’ang’ania kwa niaba ya wananchi wa Sengerema, haitawezekana, hatutakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hali hiyo naishauri sana Wizara hii wajaribu kutengeneza sera maalum ya wachimbaji wadogo katika nchi hii. Leo hii sheria zilizopo haziendani na sera. Kwa hiyo, lazima tujue nchi hii imeandaa nini kuhusiana na hawa wachimbaji wadogo?

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, leo tunazungumzia wachimbaji wadogo, wanagundua wao, wanafanya uvumbuzi wao wenyewe, wanaangalia eneo hili lina dhahabu, kesho kutwa anakuja mtu anakwenda pale na GPS anawahi kwenda kusajili. Waliogundua ni watu wengine wamekaa kule porini miaka sita au miaka mitatu, anakwenda mtu anapata leseni, anaanza kuwahangaisha hawa wananchi. Naomba sera yetu ya madini kuhusiana na wachimbaji wadogo na uwezeshwaji wao iwe bayana katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, la tatu katika jambo hili la hawa wawekezaji, wakati wanakwenda kupewa leseni lazima wawekewe masharti maalum. Masharti haya ni kwamba watoe eneo la wachimbaji wadogo na lililopimwa. Siyo wanatoa eneo la wachimbaji wadogo hawaelezi kwamba mwamba uko wapi? Wanaendelea kuachwa pale, wanakaa wanahangaika kwa miaka mingi. Wale wanafanya roho mbaya, waeleze kwamba mwamba umeelekea Mashariki, watu wachimbe kuelekea eneo hilo na wapate dhahabu waendeshe maisha yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la vifaa vya uchimbaji, tunaiomba Wizara kupitia STAMICO; kama STAMICO wameanza kutoa mafunzo, hawa STAMICO pia wanunue vifaa ambavyo vitakuja kuwasaidia wachimbaji. Kwa mfano, pump za kutolea maji katika mashimo ya migodi, sasa hivi migodi mingi ina maji.

Mheshimiwa Spika, tunamwomba Waziri, yeye mwenyewe bahati nzuri anatoka katika lile eneo, anajua maji yanavyosumbua wachimbaji wetu. Umeme tunamshukuru Mwenyezi Mungu umeanza kupelekwa katika maeneo ya wachimbaji, lakini pump zilizopo ni za China ambazo zina muda mdogo sana wa kufanya kazi. Watafute pump kutoka Japan, kutoka Uingereza, zije zisaidie uchimbaji wa dhahabu mwone dhahabu itakayozalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la mwisho tunaomba vifaa vya wachimbaji wadogo na vyenyewe vipewe ushuru. Kama mchimbaji mkubwa anapewa nafuu ya kodi, halipi kodi kwa miaka kadhaa, anaingiza vifaa vyake bila kodi, hawa wachimbaji wadogo ambao ndio wenye nchi yao, hawapewi nafuu ya kodi katika vifaa vya kuchimbia. Jambo hili linahatarisha sana amani katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, tunamwomba Waziri, tunamwona anavyofanya kazi, anachakarika na maeneo mengi anakwenda, tafadhali sana wawahurumie wachimbaji wadogo katika nchi hii. Suala la vifaa vya uchimbaji kwa mfano gololi za kuchimba za kwenye makarasha, kuandaa makarasha, hayo ni mambo ambayo mngeyapeleka SIDO, wakatengeneza makarasha ya gharama nafuu mkawapelekea wachimbaji wakakopeshwa haya makarasha, tungekuwa tunazalisha dhahabu nyingi sana ya kutosha. Leo karasha mtu anakwenda kununua kwa shilingi milioni saba, shilingi milioni kumi, ataipata wapi mtu masikini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wasaidieni wananchi katika nchi yao. Naombeni sana katika jambo hili. Nakuomba sana katika jambo hili la hawa wachimbaji wadogo hata wewe Spika unaweza ukafanya ziara; ukipata nafuu ya pumziko, uje uwaangalie wachimbaji wadogo wanavyopata shida. Nawe utaomba kabisa kwamba sasa tutengeneze sera maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika nchi hii.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kupata nafasi ya kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri. Nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa uteuzi wao katika nafasi hiyo nyeti sana katika uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Mawaziri nawaamini na hii nafasi waliyopewa ni nafasi yao kubwa sana katika icon ya nchi hii lakini nawapa pole pia kwa nafasi hii kwa sababu wengi wamepita sana katika Wizara hii baada ya kutokuitendea haki. Naamini safari hii Mheshimiwa Ulega kwa sababu alikuwa ni mchezaji wa akiba yaani Naibu Waziri kwa Mawaziri wawili waliopita sasa leo amepewa zigo hili yeye mwenyewe. Ninaimani atalitendea haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ya wavuvi, matatizo ya wafugaji, Mheshimiwa Ulega anayajua lakini ni watoto wa wavuvi na mmoja yule ni mtoto wa mfugaji; Mheshimiwa Silinde. Kwa hiyo ninaamini watatenda haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nakuja katika suala la hereni, suala la hereni hili limekuwa ni tatizo katika nchi hii. Wajikite sana katika kuleta sera ya namna gani tutaweza kuboresha mifugo yetu wakaacha kupambana na wafugaji kuhusiana na suala la hereni. Huu ni ulaji tu wa watu wametengeneza wajamaa wakaleta hapa wanataka kuja kusumbua nchi na hili litaleta hatari kubwa sana.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jackson Kiswaga taarifa.

TAARIFA

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru mchangiaji anachangia vizuri lakini napenda nimpe taarifa kwamba katika nchi hii inasemekana kwenye mapori yetu kuna mifugo mingi sana ambayo siyo ya kwetu. Hereni ina nia nzuri kabisa ya kutaka kutambua mifugo tuliyonayo nchi hii kwamba ni mingapi na ni ya nani? Hakuna upigaji hapo. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Tabasam taarifa unaipokea?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, haina nafasi ya kukubaliwa. Huyo ni mchana mbao hawezi kujua habari ya ng’ombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unamuona anaondoka na kuondoka kwa sababu ni mchana mbao. Naomba uendelee kunipa nafasi ni kwamba kama ni nchi huru ambayo tayari inalindwa na mipaka yake na Mheshimiwa Rais kishaapa kwamba atalinda wananchi, atalinda nchi na mipaka yake, hao ng’ombe wamepitia wapi? Haya ni maneno ya watu wapigaji baba. Njaa inasumbua sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuja kuharibu heshima ya nchi yetu sisi kama ng’ombe wanajulikana, wananchi wanajulikana wafugaji wa ng’ombe, Tabasam ana ng’ombe kadhaa, kule chini tuna mabalozi, tuna Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, Wajumbe. Hakuna mtu ambaye hajui ng’ombe wa fulani wako kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata buchani ukienda huwezi ukakuta ng’ombe yaani katika label ya ng’ombe pale buchani mguu unawekwa ulionona. Hatujawahi kuona kichwa kimewekwa kina hereni kuonesha kwamba ng’ombe unayenunua nyama hii ina hereni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kuja na mpango wa kuzalisha majani. Huu mpango wa kuzalisha majani Mheshimiwa Waziri usiupeleke tu kwenye mashamba yenu. Huu iwe ni Sera ya Serikali kila mfugaji awe na shamba la ekari moja au mbili na tuleteeni mbegu. Kama Serikali imeweza kwenda kupeleka ruzuku katika mbolea, haiwezi Serikali kushindwa kuleta ruzuku ya majani. Kwa sababu majani yale watu wakishaona faida yake, tayari watu wataendelea kulisha mifugo yao bila hata wasi wasi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili litapunguza habari ya kusafirisha ng’ombe kuwatoa Sengerema kuwapeleka Mtwara, kuwatoa Sengerema kuwapeleka Mbeya. Sisi tutabaki na ng’ombe wetu kwa sababu tayari tumeshafundishwa namna ya kufuga kisasa. Haya masuala mbona yanawezekana? Unao wataalamu, wataalamu tunao mpaka ngazi za wilaya. Tutengenezeeni sera nzuri, wafugaji tuwe huru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari ya kutuletea habari ya muda wote tukifikiria hereni, kesho chanjo, kesho chanjo ya miguu, chanjo ya midomo na bado tena mtatuletea zigo jingine la hereni, hili haliwezi kukubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu nina malambo. Mimi nina malambo ambayo yamepasuka na haya malambo umekuja kuyaona wewe mwenyewe ukiwa Naibu Waziri na leo wewe ni Waziri. Sasa Mheshimiwa hivi tunavyozungumza hili jambo la Mheshimiwa Waziri la malambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina Lambo mimi la Nyanchenche unajua lina kata tatu. Nina Lambo la Bitoto, hili Lambo la Bitoto Mheshimiwa Ngeleja lilimuondoa kwa sababu ndiyo nyumbani kwao. Sasa siwezi kukubali niondolewe na Wananchi wa Bitoto. Malambo yako tisa, haya malambo sisi kwetu ni kitu adimu, kitu cha thamani sana. Nakuomba Lambo la Nyanchenche umekwenda umeona, Lambo la Kishinda, Bitoto, Nyampande, Kasungamile, Buzirasoga, Sima. Haya malambo yote yamepasuka. Lambo liko Nyamizeze, ndugu yangu nisaidie sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ni kwamba miradi yenu yote ya uvuvi na mifugo hebu ileteni wilayani. Ninyi mko watumishi wachache. Nimekuja ofisini kwenu kaofisi kako hapo NBC wamebanana mle wataalamu hata hewa hawana bado mnang’ang’ania miradi ya nchi nzima mkae nayo mtaweza wapi? Tuleteeni hizi fedha wale wataalamu mlionao ninyi muwaweke huku lakini pia zile ofisi zako siyo nzuri sana kwenye suala mtu akija pale ofisini anashangaa kwamba humu ndiyo kuna wataalamu ambao wanasimamia Sekta ya Uvuvi? Sekta ya Mifugo kuna watu wengi sana ambao wameajiriwa katika mifugo na uvuvi. Ndiyo sekta pekee katika nchi hii ambayo ina ajira ya moja kwa moja. Hebu ilindeni hii sekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ng’ombe, hawa ng’ombe mnaowaona ninyi tunawafuga sisi miaka minne ndiyo anakwenda kuuzwa mnadani. Nendeni mkaangalie Argentina. Ng’ombe wa miaka minne ana tani 1.5. Sisi ng’ombe wa miaka minne ana kilo 88, kilo 110, mnafeli wapi? Mbona wataalamu mko wengi, hicho Chuo cha SUA kimekuwa ni chuo cha nini? Maana yake sielewi. Hebu pelekeni hao wataalamu waende field waende na Argentina. Hawezi kusoma SUA akaja field Sengerema kwenye ng’ombe wa kilo 80 wa miaka minne. Mpeleke akaone ng’ombe wa miaka minne Argentina na Brazil kule. Hata wewe angalia uwezekano wa kusafiri sasa kwenda kule, Mama ata toa kibali nchi imefunguka hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uvuvi. Mheshimiwa Ulega suala la uvuvi angalia sana hizi taa za solar. Hizi taa za solar zinapiga mpaka chini. Ziwa letu Victoria halina urefu mkubwa, kuna mita tisa, mita 20, mita 90. Sasa hizi taa zinapiga mpaka chini kwenye mazalia ya samaki. Litabakia ziwa la maji ya kunywa. Sisi tunakula samaki hawa kuanzia furu, nembe, gogogo, ngere yaani hatuna mahali chakula kingine sisi zaidi yetu hapo. Mmeona wenzenu sasa hivi wa Wizara ya Mambo ya Ndani. Anayetaka kuendesha pikipiki anapata leseni. Sasa sisi wavuvi suala la leseni.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Tabasam malizia mchango wako.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie.

MWENYEKITI: Haya malizia.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la hawa wavuvi. Mtu anakuwa ana kambi ya watu 120 hana hata mtaalamu mmoja kwenye kambi yake. Kwa nini msifanye na wenyewe mtu anayepata leseni apeleke siku saba aende Chuo cha Uvuvi Nyegezi pale anakaa siku saba anafundishwa namna ya uvuvi anakwenda kuwafundisha watu kambini. Hakuna mtu anayeendesha chombo halafu akakosa kuwa na taaluma.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba sana naunga mkono hoja lakini nakuomba hawa watu wetu wa Wizara ya Uvuvi waangalie Ziwa Victoria sasa linabakia kuwa la maji ya kunywa, samaki wanaisha kwa ajili ya uvuvi haramu, 75% ni wavuvi haramu.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tabasamu muda wako umeisha.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi katika Ziwa Victoria. Ahsante sana Mheshimiwa Ulega nakutakia kazi njema. Mungu akujalie sana na watu wako wamekuja Sengerema nimeona nategemea Soko, kwenye soko la Samaki Nyapukalo na cold room, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kupata nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyekujalia wewe kuwepo leo hapo na kumjalia Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuiona nafasi ya bajeti hii ya Kilimo kama chachu ya maendeleo na sehemu ambayo tunakuja kukabiliana na suala la njaa, ameongeza asilimia 29 katika bajeti hii, tumpigie sana makofi, Insha Allah! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nataka nishukuru kwanza. Namshukuru sana Waziri wetu Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa. Tumekwenda kwake kwa ajili ya kumwomba mahindi ya njaa kwa ajili ya kupunguza bei. Hali ya chakula Sengerema ilikuwa ni ngumu, gunia moja la mahindi liliuzwa mpaka shilingi 130,000 na baadaye tulikwenda kwa Mheshimiwa Bashe, Waziri wa Kilimo na akakubali kutupatia tani 2,000. Ametuokoa sana, Mungu akujalie sana Mheshimiwa Waziri Bashe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nishukuru kwa suala la ndege waharibifu. Tumekwenda kwake kumwomba ndege kwa ajili ya kunyunyuza dawa ya kuwaua ndege waharibifu wa mazao kule Sengerema, akatutumia ndege. Ila ndege ile ilipokuja kwetu ilitokea Kilosa, na baadaye ndege ile ilikwenda kutua Mwanza halafu ikaja kupuliza dawa. Ikimaliza kupuliza dawa, ndege ile inarudi kwenda kutua Mwanza. Sasa naziangalia zile gharama za ile ndege, kwamba kama wanapulizia dawa, kwa mfano, wanapulizia dawa Bunda, lazima ije Mwanza halafu irudi kule Bunda.

Mheshimiwa Spika, nataka kutoa ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri wetu wa Kilimo. Pamoja na msaada wake, sasa waende mbali Zaidi, wafikirie kupata helicopter ambayo itaweza kutua mahali popote katika suala la umwagiliaji. Kwa sababu kuua ndege waharibifu kwa kutumia gharama kubwa kama hizi, kwamba kama Kahama hakuna uwanja wa ndege, kwa mfano, labda Ngara hakuna uwanja wa ndege, ndege mpaka ikatue Bukoba halafu ijazwe dawa, irudi Ngara, hili ni jambo ambalo tunaona kama Wizara inatumia gharama kubwa sana. Kwa hiyo, watumie helicopter.

Mheshimiwa Spika, vile vile miradi iliyopo, na wao wataweza kusafiri na ile ndege. Siku ikihitaji kumwagilia, itamwagilia; lakini msafiri na helicopter, miradi ni mingi, mtazeeka. Sasa hivi Mheshimiwa Bashe umechoka kweli kweli nakuona, alhamdulillah unafanya kazi, lakini lazima ujionee huruma. Utaacha hii nafasi, unachoka, wanakuja wengine tena. Kama kuna suala la kununua ndege, peleka maombi, leta hapa, bajeti imeongezeka, wakuruhusu ununue helikopta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naanza kuchangia. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, suala la umwagiliaji. Miradi ya umwagiliaji ndiyo pekee inaweza ikalinusuru Taifa hili. Ni kwamba, tumeona kilimo chetu sasa hivi kwa kutumia hali ya hewa ya mvua, mvua zinabadilika. Leo kanda ya ziwa mvua zinanyesha mwezi wa Tatu, wakati mahitaji yetu ya kupata maji, ni mwezi wa Tisa, wa Kumi, na wa Kumi na Moja. Tungekuwa tuna miradi ya umwagiliaji; na ninakushukuru kwenye bajeti hii umeiangalia sana kanda ya ziwa. Ushauri wangu kwa Wizara, Wizara hebu njooni tumwagilie maeneo yetu yanayofanyika katika irrigation kwa kutumia pipeline kutoka ziwani.

Mheshimiwa Spika, wenzetu Misri wanatumia maji haya haya ya Ziwa Victoria, lakini yanapita katika mto. Sisi wenye ziwa hatupati thamani ya maji haya, kwa sababu hii miradi ya irrigation pia ukichimba bwawa tunategemea mvua inyeshe, maji yajae ndiyo ukamwagilie, wakati ziwa tunalo. Kwa nini usipandishe maji katika milima, halafu ukafungulia mabomba watu wakamwagilia?

Mheshimiwa Spika, mfano, kwangu kuna mradi wa Isole, alikuja Mkurugenzi wa Umwagiliaji, Mr. Ray tumezunguka naye Sengerema, ameona ile miradi. Tunayo miradi mitano ya irrigation. Kuna Isole/Kishinda, pia tuna mradi mwingine ambao uko Rwenge, Rwenge - Kagunga - Shimaka; tuna mradi mwingine ambao unaanzia Sima, huo uko katika sehemu inaitwa Ishokeya. Huo ni mradi mkubwa sana wa irrigation, aliuona Mr. Ray kule. Vile vile tuna mradi wa Ibanda - Igaka ambao tunashirikiana na mwenzangu kutoka Geita, Mheshimiwa Kanyasu. Huu mradi umetangazwa, tunashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, pia tuna mradi wa Katunguru ambao na wenyewe ulikuwa umekwama. Tunakushukuru Mheshimiwa Bashe, leo kuna Mchina yuko kule anamalizia kazi. Sasa kuna na mradi ambao ulikuwa unataka design na kujengwa, ni mradi ambao unatoka Kashindaga – Butonga - Nyamizeze – Nyamazugo. Kule sisi tuna mradi wa maji na kuna matenki kule. Ukijenga tenki kubwa mlimani, sisi tutamwagilia kwa maji ya ziwa. Sasa tunakuomba miradi hii kwa sababu Mkurugenzi wako alipita kule, tuone kama safari hii na sisi Sengerema tutabahatika kupata nafasi hiyo.

Mheshimiwa Spika, la pili ni suala la ushirika. Ushirika tumeona kwenye hizi gharama za kupanga bei za pamba. Bei za pamba, Mheshimiwa Bashe unapanga pamoja na watu wako wa Wizara ya kilimo, lakini mnapanga na wanunuzi wa pamba, Wakuu wa Mikoa wanakwenda pale. Kwa nini sisi Wabunge tunaotoka kwenye mikoa inayolima pamba tusiwemo katika upangaji wa bei? Mnaficha nini? Hivi mkitualika sisi tukaja pale hizo siku tatu au nne, tukakaa tukaangalia hicho mnachokifanya, ili tuwe mabalozi, turudi kwa wananchi, lakini mnawachukua watu wanakwenda kuwa mabalozi wa pamba, wameshastaafu, sisi tuko kazini; mnatuachaje sisi kuwa mabalozi wa pamba? Mimi nakushangaa, sijui unafeli wapi mdogo wangu katika jambo hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni sula la ushirika. Ushirika mnawatengea pesa pale, naona shilingi 20kwenye kila kilo. Sijui kuna AMCOS, sijui kuna nani mnawatengea, sasa huu ushirika uliofilisika; ushirika kama Nyanza, wakati unaanzishwa mwaka 1972, wakati huo Mwanza kwa Mkoa mzima wa ilikuwa na wananchi 760,000. Leo wananchi tuko 3,600,000. Ushirika huu umeshindikana, umeshakufa, unaung’ang’ania wa nini Mheshimiwa Bashe? Mwisho tuje tugombane humu ndani, una tu-lock sisi kuendelea. Tuna Ginnery Buyagwi iko pale, inatakiwa ukarabati, wewe mwenyewe ulikuja ukaona.

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

TAARIFA

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Bashiru Ally Kakurwa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa iwe na afya.

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba suala la ushirika ni sera ya CCM na iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Tabasam unaipokea taarifa hiyo?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Namheshimu sana bosi wangu, lakini kama kuna kitu kiko ICU tukiacha kusema kwamba mgonjwa huyu ana hali mbaya, kwa sababu tu kiko ndani ya sera, sasa hii ni hatari. Kwa hali hiyo, tunavyozungumza, sisi ushirika tunautaka, lakini uwe ushirika wenye manufaa. Kwa mfano, kama ushirika wa KACU, walijiondoa SHIRECU, lakini leo KACU ndiyo kanunua mbolea, viuatilifu na kila kitu. Kaenda kukopa, ni ushirika ambao hauna deni.

Mheshimiwa Spika, ushirika wetu wa Nyanza, tuna godown Dar es Salaam, leo zinaweka marumaru badala ya kuweka pamba; zinaweka mabati na nondo; tuna godown ziko Mwanza, Mheshimiwa Bashe alikuja akaona, leo wanaweka cement na magodoro. Pia tuna ofisi zetu za Nyanza, hata mimi nina ofisi kule ndani, zilikuwa ni ofisi za ushirika, lakini leo tunapangishwa sisi kama ofisi. Kuna mabenki na kila kitu. Kwa hiyo, ule ushirika hauwezekani tena.

Mheshimiwa Spika, leo Mwanza hawalimi pamba. Nyamagana sasa hivi ni Jiji, hawana hata nafasi ya kwenda kutengeneza makaburi. Hawa wanatakiwa ushirika wa nini tena? Ilemela hawana hata sehemu ya kulima pamba, ushirika wa nini? Ushirika sasa unatutaka sisi watu wa Sengerema na Buchosa, unamtaka mtu wa Misungwi, Kwimba, Ngudu na Magu. Pia ushirika huu wa Nyanza unavyouona, pesa wanazo kule, tumeomba tuletewe CEO pale, tuweze kuja kugawana sisi. Huyo Mrajisi anachukua pesa karibu Shilingi sita kwa kila kilo ya pamba; ya nini? Huyo Mrajisi anafanya kazi gani, wakati ushirika umekufa? Leo Nyanza hajanunua pamba miaka 23. Sera ya CCM; miaka 23! Pamba inanunuliwa na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, washirika tumekaa sisi wenye ushirika wetu, tuna hali mbaya Mheshimiwa Bashe. Unashindwaje kuvunja hii? Nakamata kule kwenye fungu lako, ukurasa wa 15 kwenye ushirika, nitakukamatia kule mdogo wangu. Sina jinsi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Najua kabisa wewe ni mzalendo, lakini kama hutakuja kusema unakuja kuugawa ushirika wa Nyanza, watu wamebakia kuwa walaji tu pale, wanakula pesa za Nyanza. Wewe mwenyewe njoo uje useme hapa, Nyanza inafanya kazi gani?

SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu, kengele ya pili ilishagonga. Ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba sekunde moja nimalizie mchango huu.

SPIKA: Ahsante sana. Kuna wenzio wameomba kuchangia nao, sasa inabidi uunge mkono hoja.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia eneo hili nyeti sana kwa uchumi wa nchi yetu. Wahengwa wana msemo wao wanasema, kila shida huzaa fursa na kila fursa huzaa shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie, kila shida yoyote inayompata mtu, inayotokea hapa duniani huzaa fursa na kila fursa unayoipata inakuzalia shida. Sasa nchi yetu imepata fursa ya kuwa na binadamu, kuwa na watu wengi, hii ni fursa, kuna nchi hazina watu. Sasa fursa hii hivi tunavyozungumza inakwenda kutuzalia shida, tunaanza kuhangaika sasa tutafanyaje vijana wetu? Watapataje ajira? Watafanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio tunakuja na mtaala mpya. Sasa huu mtaala unaouona huu mtaala ulioanzishwa sasa hivi unaokuja na ndugu yetu Mheshimiwa Profesa Mkenda, namheshimu sana, mtaala huu lazima Serikali ichukue tahadhari kubwa sana. Maneno haya nayasema, mimi ni mdau wa elimu, leo zaidi ya miaka 32. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili nataka niseme maneno mengine makubwa sana ya wanafalsafa wa elimu. Wanasema, kuna watu sita bora sana duniani, watu wote ni bora, lakini kundi la hawa watu sita ni bora sana duniani. Kundi la kwanza la heshima bora duniani ni wazazi wawili; Kundi la pili la heshima duniani ni viongozi wa dini au viongozi wa kimila; Kundi la tatu la muhimu sana ni Walimu. Mtu anayeitwa Mwalimu ni kundi la tatu la watu wenye heshima duniani; Kundi la nne ni la watu wanaotoa haki, yaani Mahakimu na watu wengine wote wanaosimamia haki; Kundi la tano ni la Matabibu, Waganga, Madaktari; na Kundi la sita la watu muhimu ni watawala, kwa upande mwingine tunasema wanasiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya makundi sita wakikosa uadilifu dunia si mahali salama pa kuishi. Wazazi wasiposimamia nafasi yao kuwa wazazi, basi ni hatari kubwa sana, lakini viongozi wa dini wasipochukua nafasi yao ni hatari kubwa sana. Walimu wasipochukua nafasi yao ni hatari kubwa kote mpaka juu. Sasa leo tunakwenda kubadilisha mtaala na huu mtaala ni sehemu kubwa sana, nafikiri katika mitaala iliyobadilishwa huu unaweza ukawa ni mtaala wa saba au sita katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtaala wa kwanza ni wa Mjerumani ambao ulikuja kubadilishwa na Mwingereza mwaka 1914. Baada ya hapo tulikaa na mtaala wa Mwingereza mpaka mwaka 1967, zaidi ya miaka 53 na baada ya hapo mtaala ukabadilishwa na Baba wa Taifa mwaka 1967 mpaka mwaka 1977, huu ni mtaala wa tatu. Mtaala wa nne umebadilishwa mwaka 1977 mpaka mwaka 1984 akiwepo baba wa Taifa. Sasa tunakwenda katika mtaala wa tano ambao aliubadilisha Mzee Mwinyi mwaka 1997, baada ya hapo Rais wetu Benjamin Mkapa, marehemu, alibadilisha mtaala ambao umekuja kubadilishwa mwaka 2008. Sasa tumekuja 2014 ukabadilika mtaala, huu tunakwenda mtaala wa saba, tuwe na tahadhari kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nimeyasema haya? Ni kwamba, wanazuoni waone, wapime, kwamba, tokea mwaka 1905 mpaka 1914, waone Mjerumani alifundishaje, Mwingereza naye hivyohivyo mpaka 67, baada ya hapo sisi ule mtaala tumekuja kuupokea. Tuwaangalie Waingereza ule mtaala ambao walituletea sisi tukaubadilisha mwaka 1967, je, wameshabadilisha mtaala mara ngapi? Hii ndio tahadhari yangu kubwa. Tusije tukawa abunuwasi, tukawa tuko juu ya mti, tunakata chini tuanguke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani nasema hivyo? Haya masomo ambayo ni ya amali yanayokuja kufundishwa sasa hivi ni kwamba, lazima tuwe tuna tahadhari, tusome masomo yetu. Tuangalie mtaala uliopita na mtaala huu, tusome kuanzia saa moja na nusu mpaka saa nane. Baada ya saa nane tuwe na masomo mengine matatu au mawili kwa masaa haya mawili au matatu, elimu yetu sasa hii ya amali ifundishwe. Vinginevyo tutakataa haya masomo mengine tuje tufute haya masomo, tutakuja kuingia kwenye hatari kubwa sana. Sasa lazima tuchukue tahadhari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya nayasema mimi kama Tabasam lakini natoa ushauri kwa wasomi wetu, hii Mheshimiwa Profesa Mkenda, nakuomba tu, pamoja na kwamba nimeuptia mtaala wako vizuri kabisa kwa heshima, kwa sababu ni lazima tuandae vyuo vya elimu, kwamba tutakuwa tuna vyuo vya elimu kumi vitakavyokwenda kuwafundisha walimu elimu ya amali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakuwa na shule ambazo watoto hawa wakitoka wanakwenda kufundishwa walimu kule kwenye zile shule za sekondari wapo pia vyuo vyetu vya ufundi katika kuendelea wapo na utoaji wetu wa certificate, tunakwenda na mitaala hii lakini mtu akimaliza form four basi apewe certificate hata kama hakufaulu lakini ni mjuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi nakupa sasa hivi elimu iliyoko mtaani, kuna mafundi baiskeli, unaileta baiskeli kwenye boksi anakuja anaiunda yule mtu, anaifunga anaiunganisha, hana certificate, na huyu mtu hatambuliki kwa sababu hana cheti. Kuna mafundi pikipiki hivyohivyo, wanakwenda kutengeneza pikipiki, anaiunda inakuwepo lakini hana cheti. Sasa je, Serikali inakwendaje kuwatambua hao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unamwona Profesa kabisa kama Mheshimiwa Prof. Mkenda anapeleka gari lake mtaani na anayekwenda kulifanyia kazi hana cheti, Profesa Mkenda yuko pale anasubiri, anamwona fundi anamwaga oil, anabadilisha tairi, anafanya nini. Je, hawa umewaweka katika upande gani unawapa vyeti lini? Kuna mafundi wanakujengea nyumba wewe mwenyewe, Mheshimiwa Profesa Mkenda na ukenda pale mainjinia wako wanasema hii nyumba iko sawa. Je, huyu naye cheti chake atapata lini? Lazima tuangalie haya makundi yote tumejipangaje kwenda kuwapa vyeti hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wafugaji. Hawa Maprofesa na Madaktari wote mnaowaona wanakwenda kufanya research kwa wafugaji, mtu amefuga ng’ombe ana miaka 30, mtu amelima mtama au mpunga ana miaka 30, anayekuja kufanya research pale anakuja kumuuliza Mzee hii mbegu yako inatoa magunia mangapi, gunia 30, ukifanya hivi inakuaje, ukiacha maji yanakuwa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo mtu akitoka pale anakwenda SUA kupata degree, lakini amekwenda kumuuliza mkulima wa darasa la pili, ndiyo anajua kabisa kwamba ukipanda mbegu ya karanga ambayo inazaa tatu, itatoa watoto watatu, ukipanda karanga inatoa mbegu mbili utatoa karanga mbili. Haya anayajua Bibi yangu hakwenda hata shule, hana degree, sijui unaniulewa vizuri, lakini anayekwenda kufanya research mnakuja kumpa degree. Sasa lazima muangalie hivi vitu. Tunakwenda katika mitaala tusije tukaacha ya kwetu tukaenda kubeba kila kitu kipya. Sisi tuko vizuri unatuona hapa akina Tabasam, tumesoma mtaala huu unaouona, ulibadilishwa mwaka 1967 tukaenda nao mpaka mwaka 1984 ukaja kubadilishwa, siwezi kulinganishwa na mtoto sasa hivi unayempeleka akapata degree SUA. Atanishinda kuongea Kiingereza tu lakini mambo mengine yote tukiyatunga Kiswahili hanipati ng’oo. Haya nakueleza hapa hapa tu, leteni paper tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lugha inayotakiwa kufundishwa ni ile ya kumfanya mtu aelewe, nieleweni vizuri. Kwa sababu utamtoa mtoto huku anasoma Kiswahili halafu ukija ukambadilisha baadae huyu mtoto anakwenda kufeli kwa sababu tu ya kushindwa kujua Lugha ya Kiingereza. Lugha ya Kiingereza itolewe maksi zake na lugha nyingine itolewe maksi zake vilevile kwa sababu yule mtoto ukimfundisha kwa Kiswahili anafaulu ule mtihani, halafu somo la Kiingereza aje alisome ni la muhimu sana kusomeshwa na lenyewe lipate cheti chake, lakini habari ya kutuambia kuitengeneza meza na kupiga msumari mtu aje afanye mtihani wa kiingereza, kutengeneza gari halafu mnasema kwamba amefeli, haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabsam, muda wako umeisha naomba umalizie mchango wako.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongeze kidogo tu nimalizie.

MWENYEKITI: Haya, sekunde 30 malizia.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ni suala la usajili wa shule. Suala hili limekwenda kwa Mheshimiwa Prof. Mkenda anajua, mmekuwa mnazifungia hata sekondari zenu za Serikali. Mara hazina kichomea taka, ulipeleka bajeti hiyo? Unazuia kichomea taka unashindwa kusajili shule, watoto wanakaa 800 darasani. Shule ya Msingi ina watoto mpaka 300. Kuna shule nyingine iko pembeni wamejenga wananchi unaiita shule shikizi unashindwa kuipa usajili. Haya maneno inakuaje upande wa ukaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani ninyi wenyewe shule ni za kwenu bado mnaziwekea masharti makubwa wakati hamjapeleka bajeti? Hii nchi tunakwenda wapi? Tumsaidie Mama Samia Suluhu Hassan, kule mmeweka Polisi kwenye sehemu ya elimu hata kwenye shule zenu, tukabeni kwenye shule binafsi hivyo lakini siyo shule za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi nichangie kwenye bajeti ya nishati. Pamoja na kukushukuru lakini tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu katika safari hiyo uendako Mwenyezi Mungu akujalie upate ushindi na ushindi ulio mnono. Watanzania wote sasa hivi dua zetu zielekee kwa Mheshimiwa Tulia, inshallah na Mwenyezi Mungu atakujalia katika hilo. Wanaokwenda Kanisani, wanaokwenda Msikitini kwa sababu hili jambo litaleta heshima katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naanza kuchangia, na ninaanza na hao wenzetu wa REA. Ni kwamba kazi ya REA ni kubwa sana katika nchi hii. Wamefanya miradi mingi mizuri sana katika hii miradi ambayo imefanyika. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini, tumepita nafasi ya kuangalia miradi, kwa kweli imefanyika kwa ustadi mkubwa, na Wizara tunaishukuru sana, wamekuja na jambo la kupeleka ma-engineer kila Wilaya ambao wanakwenda kusimamia miradi ya REA na kutoa taarifa Serikalini na kwa sisi Waheshimiwa Wabunge. Tunaipongeza Wizara kwa ubunifu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika jambo hili nikwamba mwanzo ni mgumu sana, sasa katika mwanzo huu tunataka Wizara waje watueleze hapa katika majumuisho yao.

Mheshimiwa Waziri ni kwamba hawa mainjinia walioko kule wamejiegesha katika ofisi za TANESCO. Maeneo mengi ofisi za TANESCO ni za kupanga ambavyo wana vyumba vyao na watumishi wao. Sasa hawa Mameneja ambao mliowapeleka wa REA wanakuwa wameelea. Hadhi ya kumuita injinia ambaye ni Meneja wa REA katika eneo hilo inakosekana.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ni kwamba hawana usafiri hata kwa kuanzia pamoja na bajeti zetu ndogo hizi pikipiki boxer ni 2,700,000, na kama zitatolewa ushuru hizi pikipiki zinaweza zikawa msaada mkubwa sana katika kutembelea na kuona miradi ya REA inayoendelea, na ninyi kama Wizara mtapata taarifa mnazozitaka kwa haraka, kwa sababu tayari waratibu mnao katika makao makuu yote ya wilaya nchini. Lakini la pili ni wakandarasi wanaofanya kazi. Ni kwamba mnao wakandarasi wengi, wako wakandarasi wazuri wanaofanya kazi tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, Lakini kuna mkandarasi Mheshimiwa Waziri, ungenisikiliza, kwa sababu huyu mkandarsai anafanya kazi katika Mkoa wa Tanga na Wilaya jirani ya Korogwe na Lushoto. Huyu mkandarasi tumekwenda kule Kwenda kuangalia kazi yake, ni kwamba amepewa fedha kwa ajili ya kufanya kazi Korogwe, Mkinga pamoja na Pangani.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sisi wanasiasa ni kwamba hili tunaloliona, huyu mkandarasi pamoja na kwamba alifanya kazi nzuri huko nyuma za miradi mikubwa na akapata hii kazi na akachukua advance zaidi ya bilioni tatu na kitu, sasa tunaomba aanze kukatwa penati kuanzia muda alioacha kukamilisha mradi ule. Na kwa sababu kesi za kuishitaki nchi zinakuwa nyingi nendeni naye kwa utaratibu mzuri, kaeni vizuri sana kisheria, apigwe penalty yule, na hizo penati ni takriban milioni 33 kwa siku. Tangu sisi tumetoka kule nafikiri sasa hivi huyu anakaribia kufikia asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, m-terminate contract yake, lakini isiwe sababu ya kuilaumu REA kwa sababu REA imesimamia miradi mingi kwenye kandarasi zaidi ya 60, mkandarasi mmoja si sababu hiyo. Kwa hiyo tunaomba watu wa REA wawe makini katika kuangalia wakandarasi tena wa aina hii, na huyu mkandarasi, kwa sababu tayari anapofanya kazi ni kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na huyo Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati, Mheshimiwa Kitandula, anapita kusimamia miradi yetu kila kitu.

Mheshimiwa Spika, leo hata kwa kwenyewe Mwenyekiti nako kumepata mkandarasi wa hovyo, sasa inakuwa ni tatizo kubwa. Tukija humu ndani ya Bunge lazima tuwe wakweli, tuseme, Mwenyekiti hawezi kusema lakini sisi tunaoyasimamia haya mambo tunayaona, sasa lazima tuseme. Kwa hiyo sisi tunawapongeza sana REA kwa kazi nzuri wanayoifanya, wapo wanaoweza kuangalia huyu mkandarasi mmoja kati ya wakandarasi 60, mtu kama huyu anataka kaharibu sifa. Lakini tunaipongeza sana REA kwa kazi na miradi mikubwa.

Mheshimiwa Spika, katika hili tunaomba sasa REA umeme huu unaopelekwa vijijini, kuna watu masikini. Waheshimiwa Wabunge wengine wamezungumza hapa, huu umeme wa jua mnaouona huu shilingi 27,000 shilingi labda 50,000 akifanya na installation ndani takriban inafika shilingi 100,000. Kule mngeenda Guangzhou Mheshimiwa Waziri, maonesho ni tarehe tano mwezi wan ne takriban mpaka mwezi wa sita. Kaangalieni, kule kuna taa za sola nzuri, kuna watu hawahitaji huu umeme wa kuchoma welding wanataka umeme wa taa, friji na Tv. Tumieni umeme wa jua kwenda kuwapelekea hawa watu.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali inatoa ruzuku kwenye kuunganishia mtu umeme, toeni sasa hiyo ruzuku ifanye kazi kwenye taa za sola na wakipelekewa watu masikini huko vijijini watashukuru na kuliombea Taifa hili hakuna mfano wake, na wao waonje ladha ya keki ya nchi hii, kwa sababu huu umeme wa jua hauhitaji gharama kubwa za kiasi hicho. Juzi tumeenda kuweka saini wewe mwenyewe Mheshimiwa ulikuwa shahidi, umeme wa upepo. Umeangalia gharama kuna megawatts 50 gharama zake zile ni tofauti. Japo gharama za kwanza zitakuwa ngumu lakini badaye tunaanza kunufaika.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala ambalo Mheshimiwa Iddi hapa amelizungumza, suala la hawa vijana wetu. Vijana wanamaliza katika vyuo na wamesomea umeme. Sasa hawa vijana wakiwa wanakosa kazi na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwenye Ilani tunataka ajira milioni 10 tutazipata wapi ilhali kuna ajira manzifunga? Hawa vijana tayari wangepata leseni hawa wenzetu wa EWURA usajili CRB. CRB wanasajili wakandarasi wa ujenzi class seven mpaka class one, sasa hawa EWURA wangesajili hawa vijana wangepewa class, kama ni class seven waanzie huko.

Mheshimiwa Spika, hawa vijana wakafanye kazi ya installation, mmewafundisha umeme, watashindwa kutengeneza umeme vijijini wa taa tatu au taa nne? Kwa hiyo kila kazi itafanyika kwa class yake. Hawa vijana mngewapa na gharama zikawa ndogo za kulipa. Kama mnakwenda kujenga vituo vya mafuta vijijini mnashindwaje kuwapa leseni hawa vijana wakaenda wakafanya kazi? Wapo ma-engineers wengine wamemaliza vyuo, hawa ma-engineers waliomaliza vyuo nao wanatakiwa kusaidiwa. Wangefanya kazi hizi ambazo zinakuwa ni nyepesi na mnapunguza gharama za uendeshaji.

Mheshimiwa Spika, muhuri shilingi 50,000, fundi shilingi 100,000 bado installation ya umeme. Mtu akinunua installation ya umeme anunue mita, socket breaker, tayari inafika kama shilingi laki tatu na zaidi, hizi gharama zinakuwa kubwa kwa hiyo ziangalieni hizi gharama. Huyo mtu akimaliza kufanya kazi haitaji muhuri, yeye mwenyewe awe ni muhuri, anagonga muhuri wake. Na kwa sababu ana leseni anapeleka TANESCO wanakwenda kutoa. Mheshimiwa Waziri hili haliwezi kukushinda. Nafikiri hili na tulilishauri mpaka kwenye kamati. Kwenye majumuisho, uje ulisemee kwa sababu litakuwa ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la TBS. Hawa wenzetu wa TBS ni wachanga wamepewa kazi ya kuweka kinasaba katika magari. Ushauri wetu sisi tunachosema ni kwamba waongeze jitihada na juhudi katika kazi; tunajua ni wachanga. Aliyekuwepo pale TFI alifanya kazi kwa miaka 11 ndipo akawa giant, sasa hili ni shirika la Serikali lipunguzieni milolongo. TBS apewe fedha ili anunuee magari, aweke katika kanda, asaidiane na EWURA hii kazi ili tupunguze dumping ya mafuta nchini.

Mheshimiwa Spika, lakini automation machine tulielekeza sisi kwenye tenda zake sasa anazokuja kufanya sasa hivi TBS aje kwa automation machine ili yale magari yaweze kuwekewa kule. Lakini kuna kelele na minung’uniko midogo midogo, TBS amalize, aweke session mbili. Asubuhi wawepo wafanyakazi watakaofanya kazi saa mbili mpaka saa kumi na wawepo watakaofanya saa kumi mpaka saa nne usiku, ili magari yasilale depo yanapakiwa mafuta. Kila gari iliyopakiwa depo iwekewe mafuta, ikishawekewa kinasaba ifungwe seal. Lazima TBS naye afunge seal yake ili kusudi hiyo gari ifungwe seal ya deport na itafungwa seal ya TBS. Tumpe uwezo TBS aweze kufanya kazi. Taifa hili liweze kuokoka na mafuta ya dumping nchini.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; ninaomba dakika moja tu. Ni kwamba katika Jimbo langu umeme unakatika, Mheshimiwa January mwenyewe alikuja ukaona, na akatueleza kabisa kwamba anatengeneza line nyingine kutoka Mpovu Geita kuja Sengerema. Wananchi wa Sengerema wamenituma katika jambo hili na umeme visiwani, niletewe umeme visiwani.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana…

SPIKA: Haya, ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: … hongera sana Mheshimiwa January Makamba baada ya kutoka hapa basi uniambie sasa lini Sengerema tunapata umeme? Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia mchango wangu katika eneo hili la Bajeti Kuu ya nchi na leo kidogo niko kizalendo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu ni majemedari wa kupiga kelele na kuzungumza sana maneno makali katika mitandao na kila maeneo mengi sana. Maneno haya yangekuwa yanatoboa mwili wa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, leo angekuwa amejaa bandage mwili mzima. Kwa hiyo anachotakiwa hapa sasa hivi ni kuwa na ngozi ngumu tu na kujenga imani halafu baadaye anatoboa. Nchi inatukanwa kila kona na sababu ya nchi kutukanwa kila kona ujue watu wamechoka, hawana pesa mifukoni. Kwa hiyo, mtu akikaa akafikiri hana cha kufikiri anaingia kwenye mtandao anaanza kutukana, sasa hili lazima Waziri alijue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uandaaji wa bajeti huu ni kwamba wakati wanaandaa bajeti, hawa watalam wetu wawe wanaita na sisi tuliyochomwa jua sana huku mtaani tuje tuwashauri namna ya kuandaa bajeti. Kuna vitu ambavyo sisi tutawaeleza hiki weka, hiki punguza, hiki toa, lakini wakijifungia ndani wenyewe waliokaa kivulini wanakaa kwenye AC, magari yapo yapo kwenye AC na kila kitu, wakimpelekea Waziri huku, huku Waziri anaendelea kutukanwa sana. Sasa naye ana wataalam wanaomzunguka hali siyo nzuri, huku chini Mheshimiwa Waziri wa Fedha miradi mingi sana inafanyika, tembea nchi nzima mabarabara yanatengenezwa, majengo yanajengwa na kila kitu kinakwenda katika nchi hii, maendeleo yanazunguka kama tairi la gari. Nchi inakuwa kama imepata uhuru sasa hivi, kila kitu kinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote kuna jambo la kujiuliza, kwa nini kelele zinakuwepo? Huku chini kuna watu wakitoka ndani saa kumi na mbili asubuhi kwenda barabarani kutafuta pesa wanachomwa jua mpaka saa kumi na mbili jioni, anarudi na elfu tatu na elfu mbili, anapitia dagaa anakwenda kula nyumbani kwake, hawa watu wapo wengi kwenye nchi hii. Sasa Waziri alete mipango ya kupata pesa, wananchi huko wapate pesa na zenyewe zizunguke sasa kama tairi la gari, kelele zitapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipi kifanyike? Lazima waangalie huku chini wananchi wanatakiwa sasa wapate miradi itakayowaendesha, yatengenezwe masoko ya gharama nafuu. Haya masoko yanayokwenda kujengwa, Mheshimiwa Waziri wa Fedha angekuwa ananisikiliza ananiangalia, unafahamu akianza tena kula story mambo yatakuwa magumu sana huku, kwa sababu kuna mambo makubwa hapa ndani anatakiwa ayasikilize…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam, unaongea na kiti…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti na yeye awe ananiangalia na ananisikiliza…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam naomba ufuate utaratibu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

MWENYEKITI: Ongea na kiti.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Sawa, ananiangalia kwenye TV, haina neno. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza na Waziri wa Fedha ni kwamba iko miradi mingi inayokwenda na pesa nyingi zimekwama. Kuna magari mabovu, kila Halmashauri kwenye yadi zao wana magari mabovu mengi yamekaa. Haya magari yalikwenda pale kupakiwa yamesimama ni mabovu. Haya magari kwa nini yasiuzwe? Msajili wa Hazina amepita kukagua magari nchi nzima, yako kwenye ofisi zote, polisi kila mahali kwa nini hayauzwi haya magari tukapata pesa ili zirudi kwa wananchi huku chini zikafanye kazi? Kwa nini wanakuwa na vitu vibovu wamevishikilia, wanayasubili na yenyewe kwa ajili ya kuja pata urithi, nani aje apate urithi wakati sisi tuna shida leo? Yauzwe haya magari, watu tupate pesa huku za kuendesha ofisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pointi nyingine ninayotaka kuieleza hapa, nataka kumweleza Waziri suala la msingi sana ni suala la kilimo. Huko kwenye kilimo sasa hivi Serikali imeweza kutoa pesa kwa ajili ya ruzuku ya mbolea, ruzuku ya petroli, dizeli na kila kitu, mabilioni ya shilingi. Kama tumeweza kutoa mabilioni ya shilingi kwenye ruzuku kwa nini tusitoe pesa zikanunuliwe trekta za gharama nafuu? Massey Ferguson, zikanunuliwa Swaraj, hizi trekta wakagawiwa wananchi kule, wakakopeshwa, wakapimiwa mashamba, hapa yuko Waziri wa Ardhi, wapime mashamba kwa Hati za Kimila zitumike kama dhamana, watu wapewe matrekta kule kwa ajili ya kuboresha kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mitambo ya kuchimba visima, sasa kwa nini ile mitambo ya kuchimba visima kama wanaweza kutoa ruzuku kwa nini isingie tukaagiza mitambo mingi zaidi, ikapelekwa sasa Wizara ya Kilimo? Wizara ya Maji wanachimba visima vyao na Wizara ya Kilimo wakachimbe visima, tusitegemee kilimo hiki cha mvua, tulime zaidi ya mara tatu kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupa mfano, nina eneo tu Sengerema, Sengerema imezungukwa na Ziwa kwa asilimia 68. Tunao vijana kule sisi Sengerema wamekaa katika makundi, leo mwaka wa tatu wanakaa wanasubiri kupewa mitambo ya irrigation. Waziri Jafo alisema, Waziri nanii, Waziri nani huyu? Waziri Bashe anasema kwamba anakwenda kutengeneza irrigation Kanda ya Ziwa. Wasilete miradi mikubwa ya bilioni nane, bilioni sita wanunue mashine za dizeli, mashine za water pump umeme sasa hivi upo kila kona, tufanye irrigation, sisi tuna uwezo wa kuzalisha na kulipa ile mikopo kwa haraka. Haya ni mambo ambayo wanatakiwa wayafanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la uwekaji wa stempu, uwekaji wa stempu wa ETS ni wa muhimu sana kwa manufaa ya nchi. Sasa bidhaa zinazowekwa sasa hivi yule bwana wakati anapewa kazi alikuwa na viwanda vichache. Leo viwanda vimekuwa vingi zaidi ya mia tatu, lakini kuna bidhaa nyingine bado zinatakiwa wakaweke mpaka kwenye majani ya chai, majani ya chai yanatengenezwa ya paketi wanatengeneza kila kitu, leo Mheshimiwa Waziri ameweka mpaka kwenye maji. Sisi tuna shida na kodi na hawa wanavyokuja kuweka basi kelele zipungue kwa sababu hao wenye viwanda vikubwa wanadai shilingi nane inayowekwa kule ni kubwa. Basi wakae na huyu mtu SICPA apunguze bei angalau shilingi tatu hivi viwanda sasa, hawa wawekezaji wetu wa ndani wakawalinde. Hakuna namna ya kulinda viwanda vya ndani isipokuwa kuvipunguzia mzigo uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekaji wa stempu uende kwenye bidhaa zetu ikiwezekana kwenye cement, sukari kila kinachozalishwa kwenye nchi hii kiwe kina nembo ya kwetu na hawa watu stempu zao, stempu wanaleta kutoka nje, kutoka Uswisi kwa nini wasiweke kiwanda hicho cha kutengeneza stempu hapa hapa? Vitu vyote vikafanyika hapa hapa Dar es Salaam, kama ni Dar es Salaam au kama ni Dodoma tutakuwa tumepunguza mzigo mkubwa kwa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la msingi na ninachotaka kuomba kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, suala hili linalopigiwa kelele, hili la bandari. Suala la bandari, watupe fedha sisi Wabunge, huku tunavyozungumza twende Majimboni tukapige mikutano tuwaambie wananchi. Hakuna namna nyingine ya kwenda kueleza wananchi kutoa huu uongo, hawa watu walikuja na hoja ya kuzuiwa kufanya mikutano. Wakafunguliwa kufanya mikutano, wakaja na hoja ya Katiba mpya, Rais yeye ndiye alikuwa Makamu Mwenyekiti anaendesha hapa kiti cha Katiba mpya wakaikataa Katiba mpya na yeye ndiye alikuwa Makamu Mwenyekiti. Mwenyekiti wake amekufa, Mheshimiwa Sitta yeye akabakia, ndiyo Mwenyekiti sasa hivi wa Katiba, hilo na lenyewe limejifuta, wamehamia kupotosha kwenye bandari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa twende kule sisi tukawashughulikie, tukawaeleze wananchi ukweli kuhusiana na suala la bandari. Bandari ndiyo mlango pekee utakaokuja kututoa sisi kwenye matatizo, bandari ile inaingiza trilioni 1.6. Haiwezekani ikaingiza pesa ndogo kiasi hicho halafu tukaacha ile bandari ikaendelea kukaa pale. Walio wengi wanaopotosha pale ni waliokuwa na maslahi na ile bandari, wanandugu wa ile bandari wanapotosha, wanapewa pesa kwenye mitandao, wapotoshe kwamba bandari inauzwa, bandari inauzwa kwa lipi? Kitu kipo katika mikataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inahitaji tutoe elimu kwa wananchi waeleweshwe zaidi na sasa hivi hawana sehemu nyingine yeyote wanayotegemea kupiga kelele isipokuwa ni hiyo. Mheshimiwa Waziri awe na ngozi ngumu na ninachotaka kumwambia aendelee kusimamia, lakini awakumbuke wachomwa jua, hakuna namna nyingine ya kuweza kuwakumbuka wachomwa jua isipokuwa hilo jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la mwisho ni suala la elimu. Haiwezekani tuna misitu kuanzia kule kwako, iko misitu Mafinga, Sengerema kule sisi Buyingi tuna misitu mingi, kwa nini Serikali isitoe cubic meter elfu kumi ikachana mbao za moja kwa nane au moja kwa kumi, wakanunua square pipe, tukatengeneza madawati nchi nzima? Watoto wanakalia mawe wakati tuna misitu imejaa hapa. Inakuwaje namna hii? Mheshimiwa Waziri wa Fedha angekuwa amekali mawe, angekuja kuwa Waziri Fedha? Khee! Inakuwaje namna hii lakini na Naibu Waziri wa Fedha wangekuwa wamekalia mawe wangekuja kuwa katika hali hiyo? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tusitengeneze madawati nchi nzima? Madarasa yaliyotengenezwa kwenye nchi yote ya Mama Samia yalikuja na madawati yake, haya madawati yaliyokuwa ya Marais wengine waliotangulia, watoto wanakalia mawe kwenye nchi hii. Kwa nini tuna misitu mikubwa namna hiyo? Mafinga iko pale imejaa, Sao Hill imejaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie katika jambo hili, hili jambo ni gumu. Hatuwezi kujenga madarasa mapya, yale madarasa yaliyokuwa zamani yote yana hali mbaya, hayana madawati na hatuwezi kuwa salama sisi Wabunge kama watoto wanakaa chini, tuone huruma katika jambo hilo. Najua nchi ina mambo mengi, lakini kama tumeweza kutoa ruzuku, Wizara ihakikishe watoto wanakalia madawati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo Waheshimiwa Wabunge wanatakiwa waniunge mkono kabisa, hoja ya madawati iwe ni hoja ya nchi, hoja ya madawati ni hoja ya nchi, madarasa ni mengi hatuna jinsi. Walimu namna ya kuwafundisha hawa Watoto, wanapata tabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, namshukuru sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa kunijengea jengo la TRA, Sengerema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Waangalie Sheria za Kodi…

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, Mheshimiwa Mwigulu, ahsante sana, hali siyo nzuri huku hela hakuna. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia katika Bajeti Kuu. Kwanza, naipongeza Wizara kwa kuandaa bajeti ya wananchi na kwa mara ya kwanza katika nchi hii tunapata bajeti ya kijamaa, lakini nasikitika kwamba Waziri wakati anakuja kuiwasilisha ile bajeti hakuja kijamaa lakini nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nataka nianze na Bandari, bandari ni mlango ambao tumepewa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya sisi kutokupata shida, uwekezaji wa bandari kwa mwaka jana tu Mheshimiwa Rais Samia wakati anaingia madarakani kulikuwa kuna mradi pale ulikuwa unahitaji shilingi bilioni 210, baadaye mwezi Desemba ikatolewa shilingi bilioni 290, tukapata shilingi bilioni 500 katika kutengeneza kupanua bandari.

Mheshimiwa Spika, bandari ndio mlango pekee ambao unatakiwa kutusaidia kupata fedha nyingi, kwa mfano kwa mwaka huu tunapata Trilioni Moja na katika hiyo Trilioni Moja ambayo tunakuja kuipata katika bandari kwa magati 12 tu, sasa tukiangalia nchi ambazo zinatuzunguka, tukiwaangalia Kenya, wenzetu Kenya wanajenga bandari ya pili Lamu ambayo itakuwa ina magati karibu 40, wana bandari yao ya Mombasa ina magati 25, leo tuna mtu mwingine ambaye ni mshindani wetu Beira ana magati 17 anapanua magati Sita kupata 23. Pia tunae mshindani wetu mwingine wa nne ambaye sisi tunamuona siyo mdogo ni mkubwa ana magati 52 Durban.

Mheshimiwa Spika, sasa ukichukua wenzetu wanapakua meli za kutosha, kwa mwezi Mombasa anapata meli kama 240 kwa siku anapata meli sita hadi nane. Dar es Salaam tunapata wastani wa meli mbili au tatu kwa siku, sawa na wastani wetu sisi ni meli 60 hadi 70 kwa kipato cha Trilioni Moja. Wenzetu Bandari ya Beira wanapata meli nne hadi tano, wenzetu Bandari ya Durban wanapata meli kuanzia10 hadi 15 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, sasa tunakwama wapi Mheshimiwa Waziri? Ni kwamba tunao uwezekaji wetu Kwala kutoka Dar es Salaam kwenda Kwala ni kilometa 90, lakini Kwala kama tutasafirisha reli yetu hii tuliyonayo ambayo siyo ya mwendo kasi, hii reli yetu tu ya Mjerumani tuliyoirithi, kutokea Dar es Salaam tukaweka vichwa vipya vikachukua yale makontena kutuletea Kwala kwenye eneo ambalo limekwenda kuwekezwa na Bandari ni hekta kama tano ambalo linaweza likakaa na makasha kontena zaidi ya 3,600, bandari inakuwa wazi tunapata nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri hapa leo mimi naomba nikushauri nachukua ndani ya Katiba Ibara ya 72 inasema Kazi ya Mbunge ni kuishauri na kuisimamia Serikali, leo pokea ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeniteua kuwa Balozi wa mafuta nitakuja kwenye mafuta leo nipo kwenye bandari halafu nitakuja kwenye mafuta. Sasa kule Kwala nakushukuru mmetenga eneo la kuwapa wenzetu Warundi mmetenga eneo la kuwapa Wazambia, Wakongo, mmetenga eneo la kuwapa Wanyarwanda na Waganda, sasa…

SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu, hiyo mmetenga unaniunganisha mimi na nani?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nasema Serikali.

SPIKA: Maana wewe unazungumza na mimi na kama unasema Serikali sema Serikali imetenga.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga.

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam kwa sababu ukisema mmetenga na Spika wako unamuweka huko, maana wewe unaongea na mimi hapa.(Kicheko/Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru endelea kunilinda.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga eneo kwa ajili ya kuwapa wenzetu sehemu ya kushushia mizigo na hiyo itakuwa fursa kupakuwa mizigo mingi, sasa kwa hatua hiyo mwendelezo wa lile eneo la Kwala toka mwaka 2017 eneo linatengenezwa haliishi, na kutokea Vigwaza kwenda kule Kwala ni kilometa 15, kutokea Ruvu kuja Kwala pale ni kilometa moja na nusu. Reli tayari imeshatengenezwa pale, kwanini kunakuwa kuna mlundikano wa makontena Dar es Salaam tunashindwa kushusha mizigo kwa wakati? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, meli ukipita nenda kule Sea Cliff, ukiwa eneo la Msasani Dar es Salaam unaona meli zimefunga gati kule, zile ni demurrage charges tunapata hasara Watanzania. Kwa mfano, meli ikisimama kule kwa ajili ya kushusha mafuta demurrage charge peke yake tunapaka kwa mwezi Bilioni Mbili, Bilioni 24 tunapoteza kwa ajili ya demurrage charge. Bilioni 24 ukizipigia hesabu kama Kituo cha Afya kimoja kinajengwa kwa Milioni 500 angalieni Billioni 24 tunapoteza vituo vingapi vya afya. Leo bado Waziri unakwenda kuchukua asilimia tano kwamba uitoe kule wakati kuna fedha tunakaba hapo bandari tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa hatua hiyo ni kwamba tukiimarisha bandari yetu, tukawekeza katika bandari kwenye mifumo na teknolojia pale bandarini, tutashuka hadi reli 300 kama leo meli 70 tunapata Trilioni Moja, kwanini tusishushe meli 300 tukapata Trilioni Nne. Naomba Waziri wa Fedha uzingatie jambo hili tukiwekeza katika bandari tunaweza kufaulu, na hizi kodi ndogo ndogo zinatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa niongelee kuhusu suala la ushindani. Suala la ushindani kama wenzetu wana magati mengi kiasi hiki hatutaweza kuja kupata hizi fedha, tuangalie nafasi yetu ya kusafirisha haya makasha, tufanya haraka kwa ajili ya uwekezaji wa Kwala, tukiifungua Kwala bandari itakuwa wazi, tutaweza kushusha mizigo yetu vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo bandari ina miaka 75 imeanzishwa mwaka 1947 lakini leo bandari zinazoanzishwa mpya zinatuzidi sisi wenye miaka 75. Pale bandarini kuna mifumo 36 yaani uki-log ili utoe kontena mifumo 36 unaingia kwanini usiwe na mifumo mitatu, huko na kwenyewe tunakwenda kuvujisha pesa. Tunakuomba ukija kwenye majumuisho yako utueleze lini Mheshimiwa Waziri utarejekebisha hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mafuta. Kuna bwawa la kushushia mafuta kule Kigamboni - Mji Mwema, wanaita SPM. Bomba lile lipo tunaweza tukashusha mafuta pale metric tani 120,000 lakini tukilisogeza mbali kidogo tu kwa kilometa mbili meli itakayoweza kushusha pale ni meli ambayo inaweza ikabeba metric tani hadi tani laki tano za mafuta. Tunaweza tukachanganya mafuta ya petroli na dizeli tuweke la pili litakalopakia petroli kwa sababu ndani kule Kurasini meli zinazoingia kule ni metric tani 39 zina oda moja ya mafuta inatolewa Tanzania vimeli vidogovidogo vya metric tani 40. tender moja inatoa meli nane, lazima wananchi wanakuja kuumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri uliniteua mimi kuwa Balozi wako wa mafuta, hebu tukae tuongee sasa na mimi nitakuletea na watu wengine tuje tukae tuzungumze tunaumizwa wapi kuhusiana na suala la mafuta, ukiniita tukaja na hao wanaokataa kwamba hatuumii katika mafuta, tuje kwenye mjadala wa Kitaifa kimya kimya tu utaona tunaokoa hizi fedha nyingi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu TPDC ukiona watu wanapinga TPDC isiwezeshwe ujue hao ni maadui wa Taifa hili. Yapo makampuni duniani makubwa ngoja, nivae miwani naona hata macho sioni vizuri sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika kuna makampuni kwa mfano kama Abu Dhabi kuna kampuni inaitwa ENOC - Emirates National Oil Company ni kampuni giant kampuni kubwa kuna ENOC kuna Malaysia wale wanajiita PETRONAS kuna Saud Arabia ARAMCO kuna SONATRACH ya Algeria, kuna kampuni ya Nigeria inaitwa NNPC kuna Oman OTI, kuna Urusi wanajiita Rosneft, lakini wapo wale mpaka Brazil. Brazil wana kampuni kubwa za mafuta ambazo zinafanya kazi zote. Mheshimiwa Waziri, Kampuni hizo zinatafiti mafuta, kampuni hizo zinasafirisha zinauza, sasa sisi tunafeli wapi kuiongezea mtaji?

Mheshimiwa Spika, leo TPDC inaidai TANESCO Bilioni 552 hiyo ilikuwa hadi mwezi wa Machi, hadi leo kama deni lile bado linaendelea kwa Bilioni 50 kila mwezi leo limefika Bilioni 700, hivi tunavyozungumza na wewe kama wataiwezesha TDPC tunatoka,. (Makofi)

SPIKA: Muda umeisha Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja nizungumzie Hazina tu tuwasaidie kuwafungua TPDC naomba.

SPIKA: Sekunde thelathini.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ahsante TPDC Mheshimiwa Waziri ni kwamba…

SPIKA: Ongea na mimi Mheshimiwa unavyomwongelesha Waziri ndiyo maana muda wako unaenda haraka zaidi.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, kuna TIPER, TIPER kule tumewekeza tuna asilimia 51 ya kwetu kwa ORYX lakini kuna hawa watu wa BP ambao wameuza PUMA tuna asilimia 50 ile ni mali ya Serikali, PUMA wale watu wa PUMA tunakuomba tu hawa watu wa Wizara ya Fedha, Msajili wa Hazina achukue zile hisa akamkabidhi TPDC.

SPIKA: Haya ahsante.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa mchango wangu.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango huu wa Serikali.

Kwanza, nataka niwaeleze wananchi kwamba, Chama Cha Mapinduzi katika Ilani yake ya Uchaguzi wa mwaka 2025, Mheshimiwa Rais kama alivyojua yaani nafikiri kwenye maono yake akaona Mheshimiwa Kitila Mkumbo anafaa kuwepo hapo katika sehemu ya Mpango, ndiyo Mwandaaji. Ndiyo aliyeandaa hii Ilani ya Uchaguzi halafu leo ndiyo amewekwa kwenye mpango, baba ukitufelisha tumekwisha na wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, Chama Cha Mapinduzi ni chama cha kijamaa. Vilevile viongozi wake wote ni wajamaa lakini sisi tunafuata Sera za kikomunisti. Kwa hiyo, hauwezi kumtenganisha Mheshimiwa Rais na ukomunisti wa ujamaa. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais ana dini na imani tena kwa mapenzi makubwa kwa wanachi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, sisi ambao tumemtanguliza Mheshimiwa Rais mbele na sisi tuko nyuma yake, sisi pia ni wajamaa lakini pia ni wakomunisti. Sasa, mimi hapa kama Tabasamu hauwezi ukanitenganisha na ukomunisti.

MHE. DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasam kuna taarifa. Mheshimiwa Dkt. Bashiru.

TAARIFA

MHE. DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachangia vizuri sana Mheshimiwa Tabasamu. Namuomba radhi ni mara ya pili nampa Taarifa katika maisha ya Bunge hili. Sisi ni wajamaa siyo wakomunisti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tabasamu, unaipokea hiyo Taarifa?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiunga mkono mimi mjamaa, sasa nikikataa kwamba siyo mjamaa, itakuwa ni hatari sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba sisi wajamaa tunapekea sana miradi na huduma za wananchi kule kwa wananchi. Ndiyo maana ya Sera ya Chama Cha Mapinduzi. Ni kwenda kuwasaidia wananchi wake kule chini. Sasa, Mheshimiwa Profesa Kitila nakuamini kwa kuandika, wewe ni Profesa. Vilevile wewe ni Mwalimu wangu. Kwa hiyo, sina shaka na wewe. Kwa hiyo, siwezi ku-doubt mahali popote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndugu yangu ni kwamba, tuna vijana zaidi ya milioni 20 katika nchi hii, vijana wenye ajira ya kazi, wenye uhakika wa ajira rasmi hawazidi 300000 mpaka 600000. Sasa, huu Mpango wako uje na kuondoa tatizo la hawa vijana kukosa ajira. Lakini vijana wa Kitanzania hawana shida, wakitengenezewa mahala pa kufanya biashara na kufanyia kazi, wako tayari kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Rais mwaka 2022 alielekeza yajengwe masoko ya Machinga kuanzia kule kwenye ngazi za halmashauri mpaka ngazi za kata. Mheshimiwa Waziri, ninaimani wewe ni bingwa kabisa wa kuandika. Hivi ukitengeneza yale magulio yakapata nafasi wale vijana wakaanza kufanya biashara zao kule, mbona tungepunguza sehemu kubwa ya ajira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Chama Cha Mapinduzi tulisema tuna ajira milioni 10. Ninaimani unaweza ukatengeneza ajira milioni 15. Sasa tunachokuomba, kwa mfano Sengerema inazungukwa na ziwa kwa asilimia karibu 72, asilimia kama 30 hivi ndiyo nchi kavu. Sasa, siyo Sengerema peke yake, Buchosa, ukichukua Geita vijijini, ukichukua Ukerewe, ukichukua Magu, Bunda mpaka Musoma moja kwa moja mpaka Tarime huko. Maeneo haya yote ukija ukachukua hiyo Kagera mpaka Chato, maeneo haya yote tunaweza tukafuga Samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wanaofuga Samaki na kuzalisha Tani za Samaki wanategemea maji yanayotiririka kutoka kwenye Ziwa Victoria kupitia Mto Nile. Sasa, tulikuwa tuna uwezo wa kupeleka vijana Misri au tuwachukue Wamisri waje huku tuwape vizimba wawekeze na tuwape kwa gharama nafuu kabisa ili watu wetu waje kujifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wamisri wakija, wafanyakazi wao watakuwa ni watanzania. Sasa, andikeni maandiko muwakaribishe wamisri tuje tufuge Samaki ndani ya Ziwa Victoria. Mheshimiwa Mkumbo, hili kwako siyo tatizo.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Cherehani.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumpa taarifa mzungumzaji kuwa, wenzetu Misri pia walitengeneza ziwa la kutengeneza na wanafuga samaki vizuri, pia linasaidia mambo mengi ikiwepo umeme. Kwa hiyo, sisi sasa hivi kipindi hiki cha masika maji ya mvua yanapotea, kwenye madaraja yetu maji yanapotea. Tunauwezo wa kutengeneza benki ya maji ya mvua katika kipindi hiki cha masika.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeikubali hiyo taarifa.

MWENYEKITI: Haya ahsante. Endelea Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ufugaji na uvuvi. Huko kwenye ufugaji tungeunda Mamlaka ya Uvuvi, Mamlaka ya Mifugo. Nasema kama tutafanya kama walivyofanya TARURA na TANROADS yaani maeneo yote ambayo yameundiwa authority yote yanafanya kazi vizuri sana. Tungekuwa tuna Mamlaka ya Mifugo ingesimamia Minada, ingesimamia zahanati kule za mifugo, ingesimamia mambo mengi, uzalishaji wa nyasi mambo yote mazuri yangefanyika kule, lakini kule kwenye Uvuvi pia tungesimamia mambo mengi makubwa tukazalisha. Tunakwama wapi katika Mpango kuweka suala la Mamlaka katika huu Mpango na Mamlaka ya Mifugo na Mamlaka ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la huduma za afya. Hapa kwenye Mpango mimi nimeona kwamba tumeboresha na tunapanga kuboresha huduma za afya, lakini kama hatutatafuta wawekezaji wakaja kuweka madawa kuweka viwanda vya kuzalisha dawa nchini, ni kwamba tu madawa peke yake, tunanunua dawa nje ya nchi asilimia 85, asilimia 15 ndio inayozalishwa nchini. Jamani hata syringe tu ya kuchoma sindano miaka sitini ya Uhuru hatuwezi kutengeneza Kiwanda cha syringe tu ya kumchoma binadamu, shilingi mia na yenyewe tunaagiza kutoka Korea, tunaagiza kutoka India.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa Wahindi kule kwao wana dawa za gharama nafuu, dawa zao ni za gharama nafuu sana, kwa nini tusiwafuate Wahindi wakaja kuweka viwanda hapa Tanzania, tukakubaliana wasilipe kodi lakini tupunguze nakisi ya kuagiza madawa nje ya nchi. Hili naliomba sana kwenye Mpango Mheshimiwa Profesa Mkumbo aliweke pale ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la mitambo ya maji, mitambo ya maji tumenunua mitambo ya maji mingi sana hii mitambo ya maji kweli kama ilivyokuwa inazungumzwa hapa na Mheshimiwa Monni, Mbunge wa Chemba kule, alizungumza akasema mitambo hii imesimama. Ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Mkumbo hata mimi kwangu Sengerema hii mitambo ipo, nina visima 39 sijui vimechimbwa viwili tu, hii mitambo imesimama, imekosa mafuta. Ukiwauliza wanakuambia hakuna mafuta. Kama tumeweza kununua mitambo ya karibu bilioni 250, Serikali inaweza ikakosa mafuta?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maneno siyo sahihi, tujue tatizo ni nini kwa sababu Serikali haiwezi kukosa Wazabuni wa kufanya kazi hii. Kwa hiyo, tunaomba kwamba aje na majibu mazuri tu. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kutuletea mitambo, Mheshimiwa Rais kununua hii mitambo alikuwa na nia njema sana katika nchi hii. Sasa tunawaomba tu, hii mitambo kwa nini isimame kwa sababu ya kukosa mafuta, ifanye kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la mwisho ni suala la Mkataba wa Bandari, Mkataba wa Bandari huu tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maono yake, lakini tuliomba hawa Dubai World pia wangepewa Gati la Mafuta kwa sababu kule ndio ingerekebisha ile mifumo ya uzalishaji wa mafuta, wakatujengea hub na matenki tumezungungukwa na zaidi ya nchi nane, wanategemea hapa kwetu. Sasa tunaomba sana, kwamba tungerekebisha mifumo ya ushushaji wa mafuta, angalau hata meli zenye metric tons 500,000 zishushe mafuta kwa muda mfupi na tupate storage, matokeo yake gharama za mafuta katika nchi hii zitapungua. Tunaliomba sana hilo Mheshimiwa Mkumbo aliweke katika mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii tunamwombea sana Mheshimiwa Rais apate maisha marefu sana, mpaka kijijini kwangu sasa hivi kuna watoto wanazaliwa wanaitwa Samia, inaonekana wananchi wamemkubali sana Mheshimiwa Rais katika jambo hilo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Segerema naomba kuchangia mchango wangu katika hotuba ya Waziri wa Ulinzi kama ifuatavyo; nimeusikiliza mchango wa Mheshimiwa katika maombi yake ya kupitisha bajeti, lakini kazi nzuri zinazofanywa na wanajeshi wetu katika ulinzi wa mipaka ya nchi hii, lakini kufanya kazi za kijamii katika nchi hii tunaomba tushauri kama ifuatavyo:- (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba Wizara ya Ulinzi lazima iwe na kitengo cha kisayansi, leo tumekutwa na gonjwa kubwa kama hili la Covid, lakini wanajeshi wetu wangefanya kazi hii, na wao ndio wangekuwa wa mwanzo katika mstari wa mbele kwenye tiba na kila kitu. Tunayo Hospitali yetu ya Lugalo kule Mwanza tunayo Hospitali ipo Pasiansi kule. Lakini wanazo hospitali zao nyingine za kijeshi ambazo zingeweza kutumika katika hali hii ya kupambana na hali kama hii kwa sababu kwa mfano mwishoni mwa mwaka jana hospitali zetu zote zilielemewa, lakini hatukuona jeshi kuchukuwa msaada katika jambo hili wanayo mahema, wana kila kitu sasa inamaanisha kwamba jeshi limeandaliwa kwenda kupigana vita tu, sasa ni hatari sana kuwa na jeshi la namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunahitaji jeshi kama nafasi za kuajiri basi waajiri wataalamu, hii ni jambo ambalo kwenye mpango wenu kama jeshi basi mgeweza kuajiri wataalam na wakapelekwa katika nchi ambazo zimeendelea sana kisanyansi, mfano Cuba, labda India wakapelekwa China, Urusi hawa wangekuja kama madaktari wa akiba wakuja kufanya kazi za kuokoa nchi kama hiko katika hali mbaya kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ambalo nataka kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi, ni kwamba wanajeshi sasa hivi tabia zimebadilika, wanajeshi wetu sasa hivi wanaishi na raia sio kwa ugomvi kama ulivyokuwa mwanzo. Mara nyingi sasa kungekuwa na mikutano hata kama kuna hali ya mipaka, wanajeshi sasa hivi wanakaa na wananchi. Kwa mfano kule kwangu katika eneo la Sengerema wana uwanja wao waliacha kambi ya jeshi ilihamiishwa kutoka Sengerema kuhamia Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kambi hii inakuwepo miaka 1980 na 1985 sasa tumesikia tena wanajeshi wanakuja kuchukuwa eneo hilo ambalo lile eneo lilibakia kwa Halmashauri.

Sasa tunamuomba waziri pamoja na kazi nzuri mnayofanya hili eneo letu la Sengerema katika eneo la Nyatukala mnakuwa na eneo lingine katika eneo la Nyamterera eneo lingine mlikuwa kule eneo la Nyamazugo kama sehemu ya mafunzo ya kijeshi na eneo la kambi, kwa sababu maeneo haya mliyakabidhi basi tunakuomba Mheshimiwa Waziri hili lenyewe uliangalie limekuwa ni shida, leo mkitaka kuja kudai maeneo yenu kule, wananchi wameshajenga, Serikali imejenga ofisi ya kata, imejenga ofisi yake ya Idara ya Ujenzi, tunayo shule ya msingi Mweli pale, zote ziko katika eneo ambalo tayari mnadai kwamba mipaka hii ni ya kwenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea jeshi hili sasa ni Jeshi la Wananchi, likisha kuwa Jeshi la Wananchi basi hebu pelekeni mipango mizuri kwa wananchi, maeneo mengine yapo Sengerema tunayo maeneo ambayo mnaweza mkaja mkachukua kule ambayo yako vizuri sana kwa ajili ya ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwamba tuna ujenzi wa daraja kubwa la shilingi bilioni 700 kuna eneo la Kigongo Ferry ambalo kama mlipanga kama jeshi leo na lenyewe lile lina miaka kama 40 halijafanyiwa kazi. Basi ni vizuri Mheshimiwa Waziri katika hotuba yako ukija katika majumuhisho basi uangalie hilo eneo la Kigongo Ferry mwende kiustaarabu na huku Sengerema mje muangalie maeneo mengine Halmashauri inaweza ikawapa, lakini hili eneo la Sengerema Mjini kweli itakuwa ni shida kwa wananchi wa Sengerema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata mimi kama mwakilishi wao nitakuwa niko katika hali mbaya sana kwa sababu kwanza hatuwezi kubishana na jeshi, kwa nafasi yenu na mamlaka ya ulinzi wa nchi, basi maeneo kama haya yapo nchi nzima, basi ni vizuri mkayapitia upya muone kama kuna maeneo ambayo sasa hivi wananchi wameshavamia wako katika maeneo hayo, basi jeshi linaendelea kutafuta eneo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu ndio huo, nakupongeza sana Mheshimiwa kwa usikivu wako na nina imani hili utalisikia kwa ajili ya wananchi wa Sengerema na kwa nchi nzima, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii. Nataka kuwaeleza Watanzania kwamba kazi kubwa aliyoifanya Mheshimiwa Rais Samia anazo sifa zote za kupongezwa kama binadamu. Binadamu katika asili akifanya vizuri akasifiwa basi anamshukuru Mwenyezi Mungu, kwa hiyo kwa hatua hii hatujafanya kosa lolote leo ndani ya Bunge hili kupeleka maono yetu na kuyasema yaliyopo katika vifua vyetu nafsi zetu ziweze kuridhika, kazi alizozifanya Mheshimiwa Rais ni kubwa sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi anazozifanya Mheshimiwa Rais za usiku na mchana kwa ajili ya kuja kuhakikisha ustawi wa Taifa hili, Mheshimiwa Rais anajitahidi kuweka hali ya hewa katika nchi hii iwe salama. Pamoja na kuweka hali ya hewa kuwa salama katika nchi hii, yapo pia matatizo makubwa sana ya utawala bora sehemu kubwa sana ya utawala bora, kutumia hii dhana ya utawala bora watu wanapata nafasi kubwa sana ya kumrudisha Mheshimiwa Rais nyuma, katika jambo hili ni kwamba tunatakiwa kuwa makini sana wasaidizi wake hasa Bunge ni wasaidizi namba moja kwa kazi anazozifanya Mheshimiwa Rais katika kumuunga mkono.

Mheshimiwa Spika, taarifa ya CAG imepokelewa na kikanuni inatakiwa ije hapa ndani baada ya siku Saba, haya yote Mheshimiwa Rais aliyoyasema wakati anapokea taarifa ile alikuwa katika saumu, alichukia akiwa amefunga, sasa nasi tunatakiwa tuchukie huku tumefunga tuko ndani ya saumu. Hii siyo dhambi na wala hatutatengua saumu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti iliyokuwa imepitishwa hapa haikuwa na fungu la wezi, naomba nirudie, tulipitisha bajeti pesa ziende kwenye shughuli za maendeleo hakukuwa na fungu la wezi. Sasa fungu la wezi linatokea kila taarifa ya CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Mama amepokea taarifa ya pili ya CAG na akaonesha ujasiri kusema hadharani amekerwa na akatumia lugha ambayo siyo ya staha ndani ya mwezi wa Ramadhani. Mimi mwenyewe siku hiyo wakati anatumia ile lugha nilichukia zaidi yake sina nafasi tu, ngoma iletwe Bungeni hapa halafu tuoneshe hali ya hewa kwamba tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais kwa dhati, tumechoka na wizi.

Mheshimiwa Spika, tulitegemea kabisa pamoja na mambo mazuri yanayofanyika huko wataalamu wetu wanafanya kazi lakini wako Wataalam ambao siyo wazalendo, wako Viongozi wenzetu ambao siyo wazalendo, taarifa hii kwa sababu haijawa dhahiri lakini tukiipitia ripoti ya CAG safari hii tunaomba dakika 20 kuchangia ili tutoe adabu isije ikajirudia tena. Kanuni ziko kwako leo tunamsifia Mheshimiwa Rais tunataka tukusifie na wewe safari hii utuwekee hii taarifa tuinyambue sawasawa, uingie kwenye historia kuzuia wezi katika nchi hii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema, naomba kushauri kama ifuatavyo katika hii bajeti ya Wizara ya Kilimo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, nashukuru Wizara ya Kilimo kwa kuwa na wataalam wengi sana katika Wizara yao. Katika nchi hii ukiondoa Wizara ya Elimu, Wizara ya Afya, Wizara ambayo ina watu ambao ni maprofesa na madaktari ni Wizara hii ya Kilimo, lakini mpaka sasa hivi, pamoja na kuwa na elimu kubwa kiasi hicho, hawajaweza kutatua kilio cha wananchi katika nchi hii. Nchi hii asilimia 75 wanategemea kilimo; na hiki kilimo kimeshindwa kumsaidia mwananchi toka nchi hii ipate uhuru. Sasa linakuwa ni tatizo kubwa sana. Hatujui tatizo liko wapi?

Mheshimiwa Spika, ili nchi hii iweze kupata maendeleo katika sekta ya kilimo, tunahitaji mjadala wa Kitaifa. Ufanyike mjadala wa Kitaifa tupate solution kwamba tufanyeje? Yaani tuwe tumeondoa matatizo. Bila kwenda na mjadala wa Kitaifa katika Wizara hii, watabadilishwa sana Mawaziri. Kwa sababu katika Wizara ya Kilimo kuna watu wana roho mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kukwambia, sijui tutafanyaje katika hii Wizara. Bahati nzuri wewe ni mtoto wa mkulima, unajua, umekaa huko Ushirombo, umeona ile hali iliyoko kule. Umekuja tena huku kwenu Ugogoni umeona hali iliyopo; lini wakulima wa nchi hii nao watakuwa matajiri? Sasa ujue kuna roho mbaya iko pale.

Mhehimiwa Spika, tunasomesha mtoto, anatoka huko kwetu kijijini na ameona hali ya wazazi wake ilivyo; anakwenda SUA. Akitoka SUA pale anaishi mjini, harudi tena kuja kumsaidia mzazi wake lima hivi, kama alivyosoma, haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa kwanza kabisa, naomba hii Bodi ya Kilimo ivunjwe. Bodi ya Pamba hii kwa sisi wakulima wa Mkoa wa Mwanza ivunjwe. Iundwe Bodi ya Pamba ya watu ambao wanajua kilimo cha pamba ni nini?

Mheshimiwa Spika, mimi nataka kuzungumzia pamba tu. Tuna Chuo chetu pale cha Ukiriguru, kimekuwa hakina tija. Pale Ukiriguru kuna TARI wako pale. Kwa mfano, Mheshimiwa Bashe, hivi ninavyozungumza na wewe, bahati nzuri nawe ni mtoto wa mkulima, lakini utachoka, yaani utazeeka kabla ya muda wako, kwa sababu umezungukwa na watu wenye roho mbaya. Mimi ndicho ninachotaka kukwambia, utatembea sana, lakini mpaka utatoka kwenye hiyo Wizara bila kuwasaidia wakulima wa pamba. Umezaliwa Nzega wewe, unajua kabisa pamba inavyotusaidia sisi. Haya maneno gani haya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tuna tani 350,000, leo tunakuja kurudi kwenye tani 120, haya maneno gani? Tutafikaje kwenye Ilani ya Uchaguzi tunasema tuwe na tani milioni moja? Tunahitaji mjadala wa Kitaifa katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo mchezo, hili ni jambo ambalo ukisimamia nafasi yako hapa vizuri kabisa ndani ya hili Bunge, kutusaidia wakulima wa pamba, tukienda kwenye mjadala wa Kitaifa tutakuletea jibu sahihi tufanyeje ili tuweze kupata mapinduzi makubwa ya kilimo cha pamba? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Waziri, Profesa pale, hebu wakulima wa kilimo cha pamba, wasajiliwe nchi nzima. Wakulima wako katika mikoa 17, wako katika wilaya 54; wapeni vitambulisho tujue kwamba katika kilimo cha pamba tuna ekari ngapi zinalimwa mwaka huu? Hawa wakulima wa pamba wanahitaji kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe mwenyewe umekwenda kuona, bahati nzuri Mheshimiwa Bashe nilikuwa ofisini kwako juzi, nimekwambia kale kadawa kanaitwa heka pack peke yake kanauzwa shilingi 9,000/=, leo umekwenda kusema waagize kwa jumla, kamekuja kuuzwa shilingi 4,500/=. Hiyo shilingi 4,500/= bado ni kubwa. Tunakuomba uendelee kuwa mzalendo hivyo hivyo japo watakuchukia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo wanakuja kuagiza mbolea kwenye high season, kitu ambacho ni cha ovyo kabisa. Sijui nisemeje? Wakati wa low season hamuagizi mbolea, mnakuja kuagiza mbolea mwezi Septemba, mwezi Agosti, kwenye high season wakati kila nchi inataka mbolea. Leo Serikali ya India inaagiza tani 1,100,000, wewe una tani zako 50,000, unasubirije mpaka mwezi Septemba huko? Kwa nini usinunune mwezi Februari?

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge humu ndani, jamani mnielewe. Ni habari gani hii? Ninyi badala ya kuagiza kwenye low season mkatoa tender hiyo mkaagiza kwa bulk mbolea ikaja hapa ya bei rahisi, mnakuja kuagiza mbolea ambayo inafika hapa kwa bei kubwa! Sasa ukiwasajili wakulima, hapo hapo una haki ya kwenda kuzungumza na watu wa Wizara ya Ardhi mwapimie vipande vyao hivyo vya ardhi, tupime mashamba yote tujue tatizo ni nini ili wananchi sasa waweze kuja kupata tija na hiki kilimo chao.

Mheshimiwa Spika, leo Misri ekari moja inatoa tani moja na nusu mpaka tani mbili. Wenzetu wa Chad wanatoa tani mbili na nusu. Leo hapa tuliko pamba inalimwa hapa chini Msumbiji, wanatoa tani moja na nusu. Sisi iweje ekari moja inatoa kilo 150, kilo 300? Nani atapenda kuilima pamba? Ardhi imechoka, inalimwa toka mwaka 1960 mpaka leo bila mbolea, unawezaje ukazalisha hizi tani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa Maafisa Ugani wetu tulionao na wenyewe ni tatizo, wapelekeni pia kwenye semina. Sisi wakulima wa pamba tunaijua pamba. Bila hata kumleta Afisa Kilimo, mimi nailima pamba tu; nimekuta nyumbani inalimwa, mimi mwenyewe nimeilima, tena tunailima kwa jumla. Hili najua ni tatizo.

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine liko kwenye ushirika. Wamekuja kuunda hizi wanaziita AMCOS, majambazi wakubwa kabisa. Yaani hatujawahi kuona ujambazi kama huu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Bashe amepita mwenyewe ameziona hizi AMCOS; mnakuja kuleta matatizo kwa wananchi tu wanakuja kudhulumiwa pesa zao. Badala ya kuimarisha ushirika, mnaleta maneno ya AMCOS, wajanja fulani watatu, wanne wanakaa kwenye kijiji wanajiita AMCOS. Hebu mzipitie hizi AMCOS zote katika nchi hii mje mwone. Hawa watu wanatakiwa kupelekwa Mahakamani. Hata sasa hivi tunashangaa bado wako huru. Hii ni hatari sana katika nchi hii. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ninachotaka kuwaambia ninyi watu wa Wizara,…

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, yaani nina kamchango kadogo, kaendelee…

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam, muda hauko upande wako.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ninachoomba tu ni kwamba…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Ameshamaliza. Malizia Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, lakini muda wangu umekuwa ni mdogo sana. (Kicheko/Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Wizara hii kufanya kazi kwa uzuri sana ya kupongezwa, lakini nina masikitiko makubwa sana kutokana katika Wizara hii. Wizara hii inayo wataalam ambao watalaam hawa ili wawe watalaam waliandika maandiko sasa tunashangaa katika hiki Chuo chao cha Mwika kuna tatizo la wafugaji na hawa wasimamizi wa wanyamapori watu wa TAWA. Hawa ng’ombe kisheria wanaitwa ni wanyama na tembo, simba na wenyewe ni wanyama kwa lugha nzuri ya Kiswahili wanaitwa hayawani. Kwa hiyo ng’ombe anaitwa hayawani pia na ndio maana wanachungwa hawana akili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni kwamba tunasikitika sana, maliasili maana yake katika Kamusi ni kitu ambacho sisi tumekikuta kama urithi, ambacho kinakuwa ni sehemu yetu. Kwa hiyo ng’ombe ni maliasili katika nchi hii. Tunashangaa ng’ombe wakienda kwao, wale wametoka tu porini kuja kukaa na binadamu wakafugwa. Sasa wakirudi kwao wanakuwa ni adui, wanapigwa faini wakati tembo wakija kwa binadamu hatujaona Sheria ya Maliasili inasema, wanapigwa faini kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunawaomba watu wa Wizara ya Sheria na Katiba watutengenezee sheria ya tembo akitoka katika eneo lake akaja kwa binadamu faini yake itakuwa ni bilioni moja, milioni mia tano ili wananchi tujue. Haiwezekani sheria ikawa ya upande mmoja, hakiwezekani kitu kama hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kukwambia ni kwamba, hakuna kitu kibaya zaidi kwa wananchi wanachoona kwamba wanatungiwa sheria wao, wakati wale wanyama wengine hawatungiwi sheria, kwa sababu hawa ng’ombe sisi tuliwakuta, tumewakuta kama maliasili na wakakubali kuishi na binadamu wafugwe, ni kama vile sasa hivi ukija ukaenda Thailand, ukienda India, hawa tembo wanavalishwa mpaka mashada, wanatembea barabarani na ndio maana utalii wao umekuwa kwa sababu ya jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda India, nyani, tembo wanavishwa mashada, sasa sisi inakuwaje ng’ombe wanaenda kwao, linakuwa ni tatizo, kwa sababu hawa ng’ombe walitoka porini wakaja kuishi na binadamu, ni sawasawa na nyumbu akichukuliwa anakuja kuishi na binadamun wakapata mafunzon wanakuwa ni jamii katika sehemu yetu.

Sasa ifikie, sheria wanazozitunga za kuwazuia wananchi kuingia katika maeneo hayo na wao watunge sheria hao wanyama wasije katika maeneo yetu, tuwe balanced, vinginevyo kwamba ng’ombe akipita hata barabarani amekosea mchungaji amesinzia, linakuwa ni tatizo... (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndio.

NAIBU SPIKA: Sheria ni kwa ajili ya binadamu, sio kwa mnyama. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa nini hawa…

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza Mheshimiwa. Kama ulivyosema, vizuri mwenyewe kwamba hana huo uelewa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndio.

NAIBU SPIKA: Hawezi kutungiwa sheria kwa ajili yake yeye mnyama, yaani kwamba mnyama akivuka hapa atafanywa hivi, sheria ni kwa ajili ya binadamu, kwa ajili ya mahusiano ya binadamu. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Sasa hawa ng’ombe wametungiwaje sheria sasa wakivuka mipaka tayari sisi inakuwa ni tatizo kwetu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mimi najaribu kukuweka vizuri kwa sababu ukisema wameenda kwao, basi maliasili wapo sahihi kuwazuia wale ng’ombe wabaki kule. Najaribu kukuweka vizuri ili mchango wako uupeleke kule unakotaka uende. Ukisema ng’ombe wamerudi kwao kwa namna hiyo, maana yake Maliasili wapo sahihi kuwazuia wale ng’ombe kutoka tena, maana si wamerudi kwao, kwa mchango wako yaani, ndio unamaanisha hivyo.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa…

NAIBU SPIKA: Sasa sijui kama ndio lengo lako, maana yake binadamu hawezi kwenda kumchukua tembo akaja naye nyumbani. Kwa hiyo hata hawa ng’ombe wakishaenda kule wabaki huko, si ndio kwao wamesharudi. Ndio mchango wako unachomaanisha ndio maana nakuongoza vizuri uende kule ulikotaka kusema. Ukisema wamerudi kwao maana yake Maliasili wapo sahihi kuwazuia, maana unafuata wa nini wakati wapo nyumbani. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa uelewa huo, lakini ninachotaka kukwambia ni kwamba wale ng’ombe ni hayawani, hii sheria wanatakiwa watungiwe binadamu sio ng’ombe. Kwa hiyo anayetakiwa kukamatwa pale ni binadamu ndio akapigwa faini sio ng’ombe. Sasa hawa watu wa TAWA, watu wa Maliasili ninachotaka kuwaomba sana wakae tuje na mjadala wa kitaifa tukae watu wa Sheria na Katiba, watu wa Wanyamapori, watu wa Wizara ya Ardhi na sisi Wafugaji, kwa sababu hapa Wabunge sisi hapa Wabunge wote hakuna Mbunge anayetoka kwenye jimbo lake hakuna mifugo na hakuna Mbunge anayetoka katika jimbo lake ambapo hakuna eneo la game reserve au forest reserve. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati sheria hizi zinatungwa za kuweka haya maeneo ya forest reserve na game reserve, wakati huo nchi yetu ilikuwa na watu milioni kumi na mbili na hawa watu milioni kumi na mbili mwaka 1960 ni taarifa zilizopikwa, kwa sababu wakati huo kulikuwa hakuna simu, hakuna barabara, hakuna chochote, walipataje orodha ya watu kwamba Tanzania kuna watu milioni kumi na mbili na yalikuwa ni mapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa hatua hiyo, sasa hivi nchi yetu, nchi haikui, ipo palepale ila wananchi wanaongezeka katika nchi yao na wanyama wanaongezeka, tuje na mjadala wa kitaifa kwa ajili ya hili jambo. Leo mifugo yetu, ukiichukua idadi ya mifugo iliyokuwepo mwaka 1960 na mifugo iliyopo leo vitu haviendani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakupa mfano Geita Mjini kuna eneo la game reserve la kilometa mbili, inawezekana wapi na Geita ni Manispaa? Kuna Kwimba mita mia 600 kutoka Ngudu Mjini unaambiwa kwamba ni game reserve, mita 600, haviwezekani vitu kama hivyo na hiyo ukiangalia ramani ni ya mwaka 1953. Sasa leo tunajitawala, hatuwezi hata sisi wenyewe kutengeneza ramani zetu, tunatumia ramani za Mwingereza, ramani za Mjerumani! Waheshimiwa Wabunge hili ni jambo ambalo tuiombe Serikali, tupitie haya maeneo yote ziletwe hizi sheria, afadhali hii Burigi tumeisikia ni ya mwaka jana, sijui hii Selous ilikuwa ni mwaka gani, na hii Serengeti ilikuwa ni mwaka gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa hatua hii, hii mipaka imeingiliana na tunaomba mjadala wa kitaifa twende tukaokoe wafugaji wetu. Hawa ng’ombe wataisha kwa kupigwa risasi huko na hawa ndugu zetu. Bahati mbaya sana wanaowapiga risasi ni watoto wa wafugaji, watoto wa wakulima, tunawashangaa sisi hawa watoto wa maskini wenzetu wanaenda kututia umaskini wazazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwangu lingine nataka kuishauri Wizara ya Maliasili na Utalii, watengeneze Zoo za kila Makao Makuu ya Mikoa, wasitegemee watalii kutoka nje, leo kuna ugonjwa wa Covid, sasa hivi hatupati watalii, tungekuwa tuna watalii wa ndani hapa hapa, Jumapili hii leo mimi nilikuwa naweza kwenda Kongwa na familia yangu tukaangalie wanyama.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kengele imeshagonga Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii lakini nakuomba kidogo Mwenyezi Mungu akikujaalia basi uniongezee muda kidogo kwa sababu nina suala la kuisaidia Serikali yetu katika suala la mapato nakuomba sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naanza kwa kuunga mkono hoja. Nazungumzia suala la uagizaji wa mafuta kwa pamoja. Hili suala la uagizaji wa mafuta kwa pamoja lilianza mwaka 2014 kwa ajili ya kupata zabuni ya kuagiza mafuta, kupata mzabuni atakayetuletea mafuta kwa pamoja. Shughuli hii imekwenda imefanyika kwa vizuri zaidi mpaka leo hii takribani mwaka wa saba, lakini yapo maeneo ambayo katika uagizaji huu wa mafuta tunakosa fursa ya kupata mapato katika eneo hili. Kwa nini nasema hivi, Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni kwamba, katika eneo hili kuna suala la kupata nafuu ya bei katika uagizaji wa mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo nchi marafiki. Tuna nchi kama Saudi Arabia, Iran, Kuwait, Abu Dhabi, Bahrain, Dubai pamoja na Oman. Nchi hizi zote zina Mabalozi katika nchi hii. Kwa nini tusitumie uagizaji sasa wa tender yetu iwe ya nchi kwa nchi badala ya mtu wa kati? Huyu mtu wa kati anaweka faida yake hapa ndani, hili liangaliwe sana katika mfumo huu wa uagizaji. Tunaiomba sana Wizara ya Fedha pamoja na Wizara ya Nishati, wakae Makatibu Wakuu waanze kuangalia upya tathmini ya uagizaji wa pamoja je, nchi inapoteza kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivi ni kwamba, fedha hizi za uagizaji ni kwamba, bei zao za watu wa OPEC wanatoa discount ya asilimia 30 katika uagizaji. Kwa nini tunapoteza kiasi hiki cha asilimia 30 wakati sisi ni maskini lakini wakati huo huo tuna shida na fedha kwa ajili ya kutengeneza barabara zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha katusikia Wabunge na Kamati ya Bajeti wametusikia Wabunge kwa kuweka shilingi mia moja. Hii shilingi mia moja iliyowekwa katika bei za mafuta, bei hizi za mafuta zinapanda na kushuka. Leo hii wananchi wanalalamikia jambo hili kwa sababu bei iko juu, lakini mwaka jana mwezi wa Nane bei ilikuwa chini shilingi 1,500 mpaka shilingi 1,600 kwa lita. Hii gap isingeonekana sasa hivi inaonekana hapa kwa sababu hiyo, lakini fedha hii shilingi 100 ina faida kubwa sana katika nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, haijawahi kutokea nchi hii toka imepata uhuru tumekuja kuweka jambo kubwa sana hili la kutengeneza barabara zetu katika Halmashauri zetu na vijiji. Kwa nini nasema, ni kwamba fedha za toll road ambazo zilikuwa zinakusanywa zinakwenda kwenye Mfuko wa barabara, ilikuwa ni shilingi 263. Katika shilingi 263 TARURA ilikuwa inapewa asilimia 30 na asilimia 30 ilikuwa ni shilingi
78.90. Sasa leo hii shilingi 78.90 ukiongezea shilingi 100 tunapata shilingi 178.90. Ni sawa sawa na makusanyo kwa siku bilioni 2,148,000 pigeni makofi kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa aliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Samia Suluhu kwa jambo hili tunakuambia Mheshimiwa Rais, tunakwenda kutengeneza barabara zetu kwa kiwango kikubwa haijawahi kutokea tokea uhuru. Hongereni sana, hengereni sana kwa bajeti nzuri na wananchi wanakwenda kuiona faida yake. Nini ambacho kinapungua TARURA, kinachokwenda kupungua TARURA ni kwamba tunawapelekea fedha nyingi zaidi ya bilioni 770 tunakuja kupata kwa ajili ya kazi ya barabara za TARURA. Sasa, ninachoomba ni kutengeneza ring fence ya hizi fedha. Mheshimiwa Waziri wa Fedha hizi fedha tunatakiwa tuzitengenezee ring fence zisitoke. Waheshimiwa Wabunge sijui mnanielewa ndani ya hili Bunge! Ni kwamba hizi fedha jamani lazima tutengeneze sheria kabla ya kuondoka hapa kuzi-fence hizi fedha zikawe na manufaa kwetu, zitakwenda kutumika katika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kukuambia hii fedha tunazokwenda kuzitengeneza kule shilingi bilioni 78 ni fedha nyingi sana. Tunakwenda kupata bilioni 770 za TARURA lakini pamoja na hali hii ni kwamba hapa kuna fedha zingine ambazo zinapotea. Hizi fedha za EPS hawa wanaweka stamp katika vinywaji, wanaweka stamp katika sigara, hawa wanachukua shilingi bilioni 94 wakati tunalo Shirika la Posta. Hili Shirika la Posta ndilo kazi hii ikafanye kama walivyoenda kufanya TBS. Posta ndiyo wenye kazi ya stamp katika nchi hii iweje aachiwe mtu binafsi akaweke stamp hizi, wakati Shirika la Posta linakwenda kufilisika na kufa? Tuliokoeni Shirika letu la Posta na hizi fedha bilioni 94 zikienda kule Posta, Posta itatoa gawio kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jamani ninachotaka kuwaambia hapa kuna fedha nyingine zinatumika Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Fedha zinazokwenda MaxMalipo tuna kitengo chetu sisi cha fedha za Serikali GPE. Kama GPE ni watu wa mfumo wa malipo kwa nini tunatumia MaxMalipo wanaondoka na mabilioni ya shilingi kila mwezi? Haiwezekani fedha Mheshimiwa Mwigulu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika moja nimalize jambo la muhimu sana hapa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hapo nilishakupa mbili tayari umeongeza sekunde 30 malizia sentensi yako.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni hawa watu wa mfumo wa malipo ya Serikali. Tunao watoto tumesomesha wamesoma katika hivi vyuo, tunavyo vyuo vyetu sasa hivi tulivyonavyo katika nchi hii, kwa nini tusiwatumie tunakwenda kutumia MaxMalipo anaondoka na fedha nyingi? Haya, kule Posta kuna wafanyakazi ambao hawana kazi sasa hivi na stamp hizo zinatengenezwa na hawa watu wa Posta ndiyo wanatoa kibali kumpa EPS, tunaruhusu jambo hili liende EPS wakati kuna Posta inakwenda kufilisika isifanye kazi hii?

Naiomba sana Serikali, jamani tuweni wazalendo kwenye nchi yetu tumsaidie Mama tuvuke. Ahsanteni sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Tabasamu umeongea jambo la msingi sana hapo, hebu tusaidie hao MaxMalipo ni vijana pia wa Kitanzania au wao siyo Watanzania?

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, hawa MaxMalipo ni kampuni imekuja kutoka nje ikaja hapa, Watanzania wachache sana hapo. Mnabisha nini hayo maneno gani?

NAIBU SPIKA: Aah! ngoja Waheshimiwa Wabunge.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mimi ndiye ninaye muuliza Mheshimiwa Tabasam, vijana tumewasomesha wengi, nauliza hawa wa MaxMalipo ni Watanzania pia au siyo Watanzania?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, hajui.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hata kama watakuwa ni Watanzania ndiyo ninachotaka kuwaambieni.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, basi!

NAIBU SPIKA: Ongea na mimi usiongee na mtu mwingine.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Hata kama watakuwa ni Watanzania lakini si tunalo Shirika la Posta hili Shirika la Posta si liko pale lifanye kazi?

NAIBU SPIKA: Sasa, ngoja nilikuwa nataka kuinyoosha vizuri hoja yako. Kwa sababu, umesema hivi tumesomesha watoto wa Kitanzania, sasa nikafikiri labda MaxMalipo siyo Watanzania. Ahsante sana, Mheshimiwa Tabasamu. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kwamba, naomba nichangie mpango wa bajeti yetu ya 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Kamati ya Bajeti kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuandaa jambo hili, lakini pia namshukuru Mheshimiwa Waziri na timu yake, lakini kuna vitu ambavyo tunaomba sisi kidogo kama Waheshimiwa Wabunge tujaribu kushauri katika jambo hili. Ni kwamba, mpango wowote utakaokuwa umeandaliwa halafu mpango ule ukawa unakinzana na ilani yetu ya uchaguzi, sisi Wabunge tunaanza kupata hofu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba, tulizungumza hapa katika suala la sheria zetu za nishati na madini kule tuliruhusu maduka ya kuuza dhahabu. Leo maduka haya ya kuuza dhahabu yamekwenda kuzingirwa tena kwa ajili ya kuanza kudaiwa kodi kubwa ambazo hazikuweko katika sheria. Sasa leo utoroshaji wa dhahabu umeanza upya mara 20 zaidi ya ulivyokuwa mwanzo hapo. Sasa tunajiuliza nchi gani hii leo inakuwa hivi kesho inageuka hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri na Kamati ya Bajeti hebu nendeni kwenye haya masoko uya dhahabu mkaangalie matatizo waliyonayo. Mambo mengi yamebadilika sasa huku kwenye madini tunataka kuleta tabu nyingine ambayo ilikuwa haipo; hawa wanunuaji wa dhahabu kule kwa wachimbaji hawa wengi ni ma-middle man japo wana leseni wenye pesa zao wako kule ghuba, wako Dubai, wako Madina, wako wapi, wale ndio wenye hizi pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu analetewa bilioni tatu watu wanataka labda kilo 20, kule ndani katika kilo 20 ana faida ya shilingi laki tatu-tatu tu, kilo 20 anapata milioni sita yake na anaweza akakaa miezi mitatu hajapata ile kilo 20 anakuja kudaiwa kodi ambazo haziwezekaniki kulipika. Kwa hiyo, badala ya kupitisha pesa katika mifumo yetu ya kibenki sasa pesa zinaanza kuletwa kwenye magunia kwenye magari. Hii Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana uangalie katika mpango huu namna gani mtakavyoweza kuweka jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala la biashara ya mafuta na gesi. Katika mpango wako hatujaona hiki kitu kwa sababu, lazima tukaziangalie hizi sheria, juzi tumetoa tozo, tumefanyaje, sasa huku tukaangalie. Tuangalie sera zetu za mafuta na sheria ambazo zinaonekana kwamba, kwenye gesi tunachelewa namna gani, kuna mpango wa bomba la gesi kutoka kwa wenzetu kule Mtwara na Lindi, hii biashara sasa hivi inaonekana kama sio biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye suala la mafuta tunashukuru mpaka sasa hivi ni kwamba, Wizara ya nishati imechukua nafasi ya kutafuta mpango mpya kwa ajili ya kushusha hizi bei za mafuta. Lakini biashara ya mafuta ile iweze kuchangia katika uchumi wetu. Hili Mheshimiwa Waziri katika mpango liingizwe tuone namna gani ambavyo tunaweza tukaenda katika mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jingine suala ambalo tunaliona sisi kwamba ni matatizo ni kilimo cha pamba. Kwenye kilimo cha pamba kwenye ilani yetu tumesema tunataka kuzalisha tani milioni 10, leo mwaka unaisha tunakuja katika mpango mwingine tena wa 2022/2023 hatuoni jitihada za pamba tupate tani milioni 10. Tulikuwa tumezungumza kwenye mpango wa 2021/2025 katika ilani na katika mpango huu juzi tumeujadili, huku na kwenyewe Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ni kwamba, tunakuomba uangalie katika pamba. Tulisema mbegu zitazalishwa Igunga, kwenye mpango wako hapa hatujaona kiwanda kinachotengenezwa Igunga kwa ajili ya kuzalisha mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mbegu hakuna kwa wakulima. Mbegu zinauzwa mpaka 1,500; 1,200. Juzi tumemuuliza sisi Waziri, Naibu Waziri wa Kilimo, suala la kuuza mbegu limetoka wapi? Leo mbegu imekwenda kuanza kuuzwa wakati mbegu ilikuwa inagawiwa kwa wakulima halafu badaye wanakuja kukatwa? Hii mnaanza kutengeneza vita kati ya sisi Wabunge tunaotoka kwenye zao la pamba; tutapataje hiyo ajira milioni 10 kwa sababu wakulima wa pamba ni wengi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na huko kwenye pamba tunapata pamba kwa ajili ya nguo, tunapata mbegu kwa ajili ya mafuta, tunapata mashudu kwa ajili ya mifugo yetu, hatukuona kwenye mpango wako. Sasa hili halikubaliki Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine Mheshimiwa Waziri katika hili suala lako la mpango ni suala la, tulikuwa tuna shirika letu sisi hapa la mbolea TFC, leo watu wanaanza kuzungumza tena ruzuku? Nani wa kupewa ruzuku kama sio Shirika la Mbolea? Tunatakiwa TFC tunayo, jambo lolote ambalo lilianzishwa na Mheshimiwa Hayati Baba yetu wa Taifa Mwalimu Nyerere, jamani, leo tunaanza kutoa ruzuku tena kwa mabepari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, aah! Hii inauma sana kwa wastani. TFC, tunaiacha TFC leo tunakuja kununua mbolea, mbolea inaanza kulalamikiwa wakati hii mbolea tumeishauri sisi kwenye mpango kwamba, mbolea inunuliwe wakati ambao sio wa season. Sasa leo mnakuja kuagiza mbolea kwenye high season, inakubalika wapi? Wakati mngeiimarisha TFC mkapeleka kule mtaji mkubwa katika TFC, kwanza mkisema ruzuku kule ndio mahali penyewe sasa; Mheshimiwa Waziri hili suala la mbolea liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho ambalo nataka kuzungumza ni hili suala ambalo limekuja katika nchi yetu. Sijui tumeenda kulipata wapi, suala la ujenzi wa Force Account, nchi inakoelekea Mungu ndiye anayejua. Wenzetu Wakenya miaka 10 walikataa Force Account, leo watumishi wa Serikali badala ya kuja kufanya kazi za Serikali tunawaona kwenye mitandao, unamuona mkuu wa wilaya, mkurugenzi, anachimba misingi, eeh! Hii nchi. Mipango gani hii tunayokwendanayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunakwenda wataalamu wote wanahama ofisi za Serikali wananchi wanaacha kuhudumiwa kwenye ofisi za Serikali unakwenda kuuliza unaambiwa watu wote wako vijijini. Mheshimiwa Dkt. Mwigulu wewe ni mchumi, makandarasi wapo, tunao makandarasi zaidi ya elfu 60, wapeni kazi tutengeneze uchumi katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sasa hivi imekuwa ni wizi, tunakwenda kuziimarisha ofisi zetu kule, watu wanakwenda kuiba hizi pesa zinapelekwa hazina ukaguzi. Kwenye mpango wako hatujaona hapa sisi suala la CAG unakwenda kumuimarishaje CAG? Hatujaona kwenye mpango wako na ndiye anayekwenda kukagua hizi pesa hizi trilioni 1.3 subiri balaa lake utakuja kuliona. Pamoja na vitisho mnavyovitoa sasa hivi ambavyo havina meno wataendelea kuiba hizi pesa kwa sababu, walioiba hawajapelekwa kotini mpaka sasa hivi. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuambie CAG unakwenda kuongeza idadi ya watumishi CAG kwa kiwango gani kwa sababu ofisi hiyo iko kwako? Hawa wakaguzi wetu wa ndani ndio ni sehemu ya wezi wanaoiba kule katika halmashauri, hatujaona kwenye mpango wako unakuja kusemaje kuhusiana na suala la CAG?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili mimi bado napinga huu mpango. Kauandaeni vizuri muulete. Mtuambie namna gani watakavyopelekwa kortini jhawa wat una Mahakama kule za hawa watu mnaenda kuziongezea fedha kiasi gani ili tuwe tuna uhakika na jambo hili. Lakini suala la kuwaondoa makandarasi katika nchi hii tunabakiza wachina, tunabakiza waturuki, habari yake mtakuja kuiona mbele ya safari. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Na mimi naomba nichangie Muswada huu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa niaba ya wananchi wa Sengerema kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza Wabunge wenzangu wakichangia kuhusiana na suala la mafuta na kulalamika bei ambazo zinavyopanda sasa hivi bei zimefikia katika kiwango cha juu ambacho hakijawahi kufikiwa katika historia ya nchi hii. Naomba nirejee kidogo kwa ajili ya kuweka hansard ikae sawa.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1982, 1983 na 1984 Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipata tatizo (crisis) ya mafuta ikabidi kutumia mafuta ya furnace; lakini wakati huo yalikuwa ni masuala ya kiuchumi, ambapo Mheshimiwa Hayati Julius Kambarage Nyerere ilimlazimu sasa kwa kutumia TPDC alikwenda Algeria, Saudi Arabia na kwa wenzetu Kuwait wakakubali kutupa mafuta hali ikaja ikawa nzuri.

Sasa hali inavyokuwa mbaya kama kwa sasa hivi ambako tunakoelekea ni suala sasa la Mheshimiwa Rais tunamuomba, mama yetu Samia Suluhu Hassan sasa ni wakati wa kwenda mwenyewe mahala ambapo kuna hali ngumu kama hii mama asafiri yeye mwenyewe Rais wa nchi akazungumze na hawa wazalishaji wa mafuta ili tuweze kupata mafuta ya gharama nafuu.

Mheshimiwa Spika, huu mfumo wa PPBA mimi nakumbuka ulianzishwa kama si 2012 ni 2014, na leo hii mfumo huu una miaka 10. Si vibaya kama nchi kuangalia, kwamba je, mfumo huu bado uko sahihi tuendelee sisi kama nchi kuutumia? Sisi kama nchi mfumo huu je, una madhara gani na una faida gani kwetu?

Mheshimiwa Spika, faida ya kwanza iliyopo kwenye mfumo wa PPBA ni kwamba tunaweza kutathmini na kutabiri kodi yetu ya mapato kwa miezi miwili, kwa sababu kuna mafuta yatakuwa yameagizwa kwa miezi miwili tunajua kodi yetu tunayokuja kuikusanya hiyo ni faida kubwa ya kwanza. Ya pili ni kupata uhakika wa kuwa na mafuta katika miezi miwili inayokuja

Mheshimiwa Spika, lakini yako madhara sasa ambayo yanaletwa na taasisi hizi mbili, PPBA pamoja na EWURA. Taasisi hizi ni kwamba ziko chini ya Wizara ya Nishati. Hawa wenzetu wa EWURA mguu mmoja wako Wizara ya Maji, mguu mmoja wako Wizara ya Nishati; na hao ndiyo wanaokuja kupanga bei ya mafuta, hao, kwa mamlaka ambayo iliyopitishwa na Bunge, ndio wanaokuja kupanga bei ya umeme. Sasa hii EWURA iangaliwe iwekwe wapi kwa maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na hili suala la PPBA, ni kwamba yeye ndiye anayepokea zabuni za mafuta, zabuni za uagizaji wa mafuta na zabuni za utangazaji wa bei ambazo yeye anajua sasa kwamba fulani ameshinda kutokana na hali hii.

Mheshimiwa Spika, tunalo Shirika letu la Mafuta (TPDC) Shirika hili a mafuta wakati wa marehemu Rais Julius Kambarage Nyerere pale Tipper aliwekeza yeye pamoja na wenzetu wa CALTEX kutoka Italy, Tanzania ikawa na asilimia kama sijasahau 51 au 49; lakini nafikiri ni 51 CALTEX wana asilimia 49. Hata hivyo, Baba wa Taifa hakuishia pale, ni kwamba tukawa na shirika letu la BP. Katika BP Serikali ikawa ina asilimia kule 51 na BP wakawa na 49. Hii inaonesha namna gani Baba wa Taifa alikuwa amejiandaa kukabiliana na hii hali. Sasa kule Caltex wana 49 na huku BP wana 49 hizo ni sehemu ambazo mafuta yetu sisi yangeweza kupitia katika angle hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini huyu TPDC anazalisha gesi pia. Si kwamba hana mtaji lakini pamoja na kuwa anazalisha gesi anaidai TANESCO. Mpaka Januari mwaka huu TPDC peke yake anaidai TANESCO bilioni 502. Ukichukua mwezi huu wa Februari ukachukua na Machi na sasa hivi huu mwezi huu wa Aprili utakapoisha TPDC atakuwa anaidai TANESCO bilioni 652. Huyu TPDC ni kwamba anayo kampuni tanzu inaitwa TANOIL ambayo imetengenezwa kwa ajili ya ku-supply mafuta kwa nchi kama hali ya nchi inakuwa mbaya. Tumekwenda kuanzisha TANOIL wakati tayari sisi kule PUMA tuna asilimia 51. Tumekwenda kuanzisha kule kwenye Tipper kule kuna CALTEX ambako kuna storage kubwa ya kuhifadhi mafuta; zaidi ya lita milioni 300 tunaweza tukahifadhi pale Tipper. Pia, bado tungeweza kujenga uwezo pale Tipper tukaweza kuhifadhi mafuta yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa leo TPDC anadai bilioni 652 na hana mtaji; sasa hili linakuwa ni tatizo kubwa sana. Mimi ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba wamlipe, waje hapa wanatueleza kwamba wanamlipa lini TPDC apate pesa ya kuagiza mafuta. Mashirika kama haya yako nchi zote duniani. Ukienda Algeria, Misri nan chi nyingine zote zinazotuzunguka ina nguvu kubwa, isipokuwa sisi Tanzania hili Shirika limekuja kuonekana mfu kama halina kazi. Lakini kama tungekuwa tumeagiza mafuta yetu ikitokea shida tunafungulia mafuta yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa nakupa mfano, TPDC ameshinda tenda ya Januari kwa premium ya kuagiza mafuta bei ya gharama ya mafuta kuyaleta hapa Tanzania kwa dola 26, amekuja kuomba mwezi wa pili amenyimwa kazi, amekuja kuomba mwezi wa tatu huu amenyimwa kazi. Uzalendo hakuna huko PPBA.

Mheshimiwa Spika, tunamuomba Mheshimiwa Rais tunamuomba aiangalie PPBA kwa haraka mno hawa ni watu ambao watamletea tatizo kubwa kwenye nchi hii. Vilevile Mheshimiwa Rais aiangalie EWURA; hatuwezi kukubali. Tarehe 22 imekuja meli ina mafuta, hii meli ilikuwa inaitwa MTSL Falcon, ilikuwa na tani 39. Watu wa TBS wamekwenda kuipima wakasema kwamba asilimia 90 ya vyumba vingine mafuta yake yako bora asilimia 10 mafuta si mazuri. Hawa Adax ambao ndiyo walikuwa wamepewa tender wakaondoa ile meli wakaipeleka Beira.

Mheshimiwa Spika, kuagiza yale mafuta tayari Serikali imepoteza bilioni sita, sawa na bilioni 14 ilhali yale mafuta asilimia 90 yangeshushwa na asilimia 10 iliyobakia yale ndiyo yakarudishwa; lakini yale mafuta yakaachwa yote yakaondoka yakaletwa mafuta mengine na zile LC zilizokuwa zimefunguliwa zikabadilishwa. Uzalendo! Uzalendo ni bidhaa adimu sana katika nchi hii. Huyu Mheshimiwa Rais tutamsaidiaje kwenye hali kama hii? Hili ni tatizo kubwa sana mfumo wa tender wa PPBA uangaliwe.

Mheshimiwa Spika, na hivi tunavyozungumza na wewe leo kuna kampuni ambazo tayari zimeshinda tender ya kuja kuua wananchi. Leo kuna kampuni iko hapa, naangalia Adax huu mzigo uliokuja alikuwa na dola 28 kwa premium kwa usafiri wake, kuna hawa Vitol Bahrain wakapewa dola 72. Yaani kuna mtu amepewa tender ya dola 28, kuna mtu amepewa tender ya dola 72 kwa tani. sasa dakika hizi na jambo hili ni kubwa sijui nifanyeje nakuomba sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia, unaweza ukachangia kwa maandishi mchango utafika tu, dakika moja malizia.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Amepewa Agusta kwa dola 53, amepewa traffic Gula kwa dola 44,000, akapewa TPDC kwa dola 26 inauma sana. Leo huyu TPDC ana kosa tender yuko PUMA ndiyo mwenye hisa na sisi anakosa tender. Nchi hii naomba mengine yaliyobakia niyaache kwa usalama wa Taifa ahsanteni sana. (Makofi/Kicheko)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Leo naelekeza mchango wangu katika maeneo mawili. Maeneo hayo ni suala la Wizara ya Ujenzi na suala la Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama cha Mapinduzi kilitoa Ilani yake ya Uchaguzi yenye kurasa 303 ambayo mimi ni mwanachama wake na ni Mbunge wa Jimbo la Sengerema kupitia Chama cha Mapinduzi. Ilani hii inanipa nafasi ya kulinda yaliyomo kuhakikisha yanatekelezwa ili Chama changu kiwe salama pamoja na mimi. Ilani hii ya uchaguzi Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni miongoni mwa watu walioiandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa tisa wa Ilani yetu ya Uchaguzi una maneno mazuri sana, unasema katika aya ya 12, “Mapinduzi ya uchumi kwa maendeleo ya watu.” Maneno mengine pale yako hapo. Mheshimiwa Waziri ataenda kuuangalia. Kwa hiyo, mpango wowote atakaokuwa anauandaa lazima basi akaangalie ukurasa huo wa tisa. Tukitoka katika eneo hilo sisi watu aina ya Tabasamu huwa hatukubali, lakini kwa sababu mambo yaliyoelezwa pale yana upana mkubwa katika Taifa hili, Mheshimiwa Waziri atakwenda akaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naanza mchango wangu. Wizara muhimu sana katika nchi hii kwenye ukuaji wa uchumi ni Wizara ya Ujenzi. Kwa ukubwa wa miradi iliyopo katika Wizara ya Ujenzi tunazo kilomita za lami ambazo zinaunganisha barabara zetu kuu za Taifa, barabara zetu za Mkoa. Wakati huo huo tuko na shughuli za kupanua Bandari, kutengeneza Bandari mpya, kutengeneza reli pamoja na viwanja vya ndege. Kazi hii kubwa inafanywa kwa maono ya Mheshimiwa Rais ambaye anachukua katika tafsiri ya mpango wa miaka mitano. Sasa tukija katika mpango wetu huu wa bajeti yetu, ni kwamba lazima tukaangalie mpango huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ina kazi nyingi. Mchango wangu leo nataka kutoa ushauri tu kwa mamlaka kwamba sasa imefika wakati ili tukatekeleze miradi hii, tunatakiwa tuwe na kitu kinachoitwa contract management tukahakikishe kwamba lazima tukazigawe Wizara hizi zipate ufanisi. Tuwe tuna Wizara ya Uchukuzi, wakati huo huo tuwe na Wizara ya Ujenzi kwa sababu miradi hii iliyopo ili twende 2025 imetekelezwa. Kwa kuwatumia Manaibu Waziri halafu Waziri mmoja ambaye yuko safari, hawa wanashindwa kutoa maamuzi, hili jambo linaweza kutuchelewesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti kama Spika wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ushauri wangu ni kwamba hili tuliangalie. Siyo vibaya kuwa na Wizara kwa sababu matirioni ya fedha yanaenda huko Wizara ya Uchukuzi. Sasa hivi tuna reli, tuna bandari, tunataka tukuze bandari. Leo mzigo unaopokelewa bandarini unasafirishwa, na kusafirishwa kwa njia ya reli ni asilimia mbili, kwa njia ya barabara asilimia 98. Hili ni jambo la hatari sana. Sasa hili tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha akaliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Shirika letu la Reli lipewe exemption ya mafuta likajiendeshe lenyewe. Mnakwenda kuwapa exemption wawekezaji wa nje, mnashindwa kulilinda Shirika lenu la Reli mkawapa exemption ya mafuta nao wakaagiza mafuta yakapita hapa zero zero wakapata faida kwa ajili ya kwenda kutanua uchumi unaoelekea huko pembeni kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la nishati kwa miradi iliyopo ya TANESCO na REA. Pamoja na kuwa na miradi mikubwa kama hiyo ya TANESCO, mabwawa ya Mwalimu Nyerere, miradi tuliyonayo zaidi ya ishirini na kitu ambayo inaandaliwa kwa ajili ya kupata umeme wa maji na gesi; lakini ukiangalia usambazaji wa umeme, kuweza kuwafikia wateja, tunaomba Mamlaka kwamba sasa umefikia wakati tuwe na Wizara ya Mafuta na Gesi na tuwe na Wizara ya Nishati ya Umeme (steamer). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndiyo maombi yangu leo kwa Watawala. Ahsante sana, nakushukuru kwa muda huu.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nami nitoe mchango wangu katika sekta hii ya nishati na madini. Ni kwamba, pamoja na kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, na-declare interest kwamba pia mimi ni mfanyabiashara wa mafuta ya reja reja hapa nchini na pia ni mchimbaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru sana Wizara ya Nishati kupitia TANESCO na REA kuwa wasikivu kwa kukubali kupitia upya mpango wa uunganishwaji umeme majumbani kutoka shilingi 360,000 kurudi shilingi 27,000 katika maeneo maalumu ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni kwamba, kuna miji ambayo inaonesha ni Majiji, Manispaa, lakini Halmashauri za Wilaya na Halmashauri za Miji, wana maeneo yao ambayo yako vijijini. Kwa mfano, Dodoma hapa kuna maeneo ambayo yako vijijini kabisa, lakini yanasomeka yako katika Jiji la Dodoma. Kuna maeneo yako Mwanza yanaonekana yako Nyamagana, lakini ukitoka Nyamagana kwenda huko ni kilometa zaidi ya 30. Pia kuna maeneo yako kwa mfano Sengerema Mjini, lakini zinasomeka ni Kata za Sengerema Mjini lakini ni kilometa zaidi ya 30 mpaka 60 ndiyo unafika katika maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa hili ambalo wamelichukua watu wa Wizara kurudi upya kupitia maeneo haya kwa kutushirikisha Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Madiwani na Wakuu wa Wilaya kupita kwenye maeneo hayo kurudia upya na kushusha bei hizo, tunaipongeza sana Wizara kwa jambo hilo. Naomba waharakishe, wananchi wetu wamekaa, wanasubiri kuunganishiwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, ni umeme unaoenda kuunganisha vijiji na vijiji, wilaya na mikoa. Maeneo haya wana ujenzi wa transmission. Haya maeneo miradi iko mingi sana. Kwa mfano, miradi iliyopo tu ni zaidi ya 26, na yote umilikishaji wake hatujui je, ni matatizo ya fedha kutoka Wizara ya Fedha? Hatujui tatizo ni nini? Ni Makandarasi! Sasa tunaomba Wizara ifanye haraka kuharakisha huu ujenzi wa hizi transmission unakamilika, wananchi wanaohitaji umeme waweze kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna maeneo ya migodi. Tunaishukuru sana Wizara kwamba kupitia REA, migodi yote mikubwa na midogo inaanza kupelekewa umeme. Kwa hiyo, hili tunaipongeza sana, lakini bado hawajaharakisha upelekaji wa umeme migodini, bado watu wanatumia diesel.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kama kwangu Sengerema tuna ujenzi mkubwa wa Mgodi wa Sotta Mining, ni zaidi ya kilometa 38 hadi 40 kufika kule kutokea Sengerema Mjini. Ila iliko submission ya TANESCO kule Geita kutoka Mpomvu kuja Sengerema ni zaidi ya kilometa 60. Sasa tunaomba watuharakishie kutujengea line mpya kwa ajili ya mgodi huo. Kwa sababu mgodi ukishaanza kufanya kazi na umeme haupo, na kuna umeme mwingine, waangalie njia rahisi kutokea Kakola - Geita kupitia Msalala - Karumwa au watoe Geita. Kwa hiyo, tunamwomba Waziri katika jambo hili aharakishe kwenye maeneo ya migodi mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vinasaba limekuwa ni tatizo kubwa katika nchi hii. Tulipiga kelele hapa, vinasaba vilikuwa bei kubwa, tulizungumza na baadaye vinasaba vikashushwa bei mpaka Shilingi saba kwa cubic meter za lita za mafuta. Pamoja na hali hiyo, hivi tunavyozungumza uwekaji wa vinasaba unalalamikiwa na wafanyabiashara wa reja reja walioko katika Mikoa. Wao wanatuma madereva wao wanakuja kupakia katika malori, lakini vinasaba vinawekwa kama seal. Ni jambo ambalo katika ma-depot hawajaweka wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawajaweka wazi kuonesha ma-depot yale, lita 7,000 inawekewa miligramu ngapi? Lita 10,000 miligramu ngapi?

Waweke vibao vikubwa. Wakishamaliza kuweka vinasaba, tunaiomba sana Wizara, kwa sababu ni Wizara mbili; Wizara ya Nishati na Wizara ya Biashara na Viwanda ambao wako TBS, na wao wafunge seal. Kwa hiyo wafunge seal watu wa depot na watu wa TBS, Kwa sababu suala la vinasaba linabeba uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa dumping katika nchi hii ni kwamba lazima vinasaba sasa viwekwe kwa seal. Halafu vinasaba kutokea huko vinakotoka visindikizwe ama na Jeshi au na watu wa usalama wa Taifa. Jamani suala la vinasaba kuuzwa mitaani ni suala la hatari katika uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la demurrage charges, Mwenyekiti wa Kamati amelizungumza jambo hili kwa ukubwa kutokana na muda. Hata hivyo, suala la miundombinu toka tunaingia Bungeni hapa tunazungumzia suala la miundombinu. Suala la mafuta limekuwa na changamoto kubwa kwa sababu linachangia Wizara tano. Wizara tano zote hizi zinamulika katika eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Wizara ya Fedha. Kwa mfano, kama sasa hivi uagizaji wa mafuta, meli zinafika hapa zinashindwa kulipiwa kwa sababu ucheleweshaji wa Dola kutoka Benki Kuu unakuwa ni tatizo. Tunaiomba sana Wizara ya Fedha iharakishe mpango wa uagizaji mafuta linalobeba uchumi wa nchi. Tunahitaji katika sekta hiyo zaidi ya Dola milioni 700 kwa miezi mitatu. Sasa hili ni jambo ambalo linachangia waagizaji wa mafuta kupata demurrage charges kule, nao wanaileta huku kwa mlaji. Mtu wa mwisho anayekuja kuumia ni mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, flow meter zinasimamiwa na watu wa Wizara ya Biashara. Flow meter nne ziko kule Kigamboni, ni mbovu leo mwaka wa nne hazitengenezwi. Hata hivyo, suala la ushushaji wa mafuta linasimamiwa na Wizara ya Ujenzi (Bandari). Sasa pale na penyewe ushushaji wa mafuta…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia mchango katika Wizara ya Elimu. Kwanza naipongeze Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri wanayoifanya, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri katika vitu ambavyo wanavifanya vikubwa ni kwenda kuangalia changamoto za elimu kwenye majimbo yetu. Tunawaalika, wanakubali kuja; unapiga simu, wanapokea nawaombeni sana mwendelee na kazi hiyo Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na mchango kuhusiana na mitaala ya elimu. Hii mitaala ya elimu inatakiwa iingie kwanza kwenye kumbukumbu wajue Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwamba leo Tanzania huu ni mtaala wa ngapi unabadilishwa? Mtaala wa kwanza katika nchi hii ulianzwa na Mjerumani mwaka 1905 hadi 1913; miaka minane Mjerumani alikuwa na mtaala wake katika nchi hii ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Mjerumani, mwaka 1913 mpaka 1967, miaka 54 tunatumia mtaala wa Mwingereza. Baada ya mwaka 67, Marehemu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alibadilisha mtaala wa kwanza, huu ukawa ni mtaala wa tatu katika nchi hii. Mtaala huu ulikwenda mpaka mwaka 1977, miaka 10. Ukafuata mtaala mwingine wa nne 1977 mpaka 1984. Baada ya mtaala wa mwaka 1984 ukaja mwingine mwaka 1984 hadi 1997 kwa Marehemu Mheshimiwa Mungai, ndio tukaanzia hapo sasa kuteleza mtelezo wa hatari huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mungai wakati anabadilisha mtaala mwaka 1997 alipiga marufuku michezo, mambo mengi yakafutwa, lakini wakaweka kitengo kinaitwa Book Management Unit. Hapo sasa elimu ya Tanzania ikaanza kuingizwa katika biashara. Kitengo hiki cha Book Management Unit kwenye mtaala huu wa mwaka 1997 yakaruhusiwa makampuni sasa kuanza kuuza vitabu. Yalitengenezwa makampuni mengi, watu wakawa wanachukua vitabu Nigeria na wapi, wanakuja kutafsiri kwa lugha ya Kiswahili, anapata ithibati inakwenda kwenye mashule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya moja kama yangu ya Sengerema, kuna shule zaidi ya 210. Kila shule inasoma kitabu chake, halafu mtihani ni mmoja unatoka katika Wizara. Kichekesho cha ajabu kabisa duniani! Kigoma wanasoma Mtue and company, sijui Ben and company, Tanzania Publishers, sijui wapi, sijui Kigamboni Publishers. Yaani kila mtu mwenye pesa zake alikuwa anakwenda ku-lob katika kitengo hicho cha Book Management Unit, wanapata order kwa Wakuu wa Shule vitabu vinasomwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili jambo, elimu yetu ndiyo ilianza kuharibikia hapo. Mtaala mwingine ukabadilishwa mwaka 2004. Baada ya 2004, mtaala mwingine, wa saba unakuja kubadilishwa. Huu mtaala umekuja mpaka 2014. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Profesa anatakiwa kukaa sasa afikiri, afanye research katika hii mitaala. Hawa waliosoma mtaala wa Mwingereza wana manufaa gani katika nchi hii? Sisi tuliosoma mtaala huu wa mwaka 1967 wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere: Je, tunalinganishwa na hawa waliosoma mtaala wa mwaka 1997?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo unaweza ukaacha chakula ndani; umeacha mahindi, umeacha mpunga, gesi ipo, watoto hawajui hata kusonga ugali? Sasa huyo unategemea aje akusaidiaje? Kwa sababu shuleni hilo jambo halifundishwi. Tulikuwa tuna elimu ya Sayansikimu sisi, tulifundishwa haya. Tulitoka shuleni tunapika keki, tunajua kila kitu, tunajua kuosha vyombo, kupiga pasi, tulifundishwa hizo kazi. Sasa leo inakuja mitaala hii ya kompyuta; haya endeleeni, lakini ninachotaka kukwambia, hiki kizazi chetu kikiisha, tegemeeni bomu linalokuja sasa, litataka ajira kwa sababu hamkuwaandaa katika jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine ambalo tunataka tuwasaidie hawa watu wa Wizara. Kwa kuwa ni wasikivu nina imani watasikia. Kuna suala la vyuo, wenzetu wa Thailand baada ya kumaliza machimbo, nchi hiyo waliichimba sana Thailand, wakabakiza sehemu moja angle ya utalii. Kule kwenye utalii wakaona na kwenyewe sasa kunakuwa na hali mbaya, waliwekeza katika vyuo vya ufundi vya kati. Hivi vyuo vya ufundi vya kati, walipeleka mtaala mmoja tu wakausimamia kwa nguvu kubwa ya ushonaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye kushona walipeleka watu kwenda kuwa ma-designer kule Hongkong, wakapeleka ma-designer kule China, walifundishwa kushona, wakawa wanaagiza vitambaa kutoka Pakistani, kutoka China. Leo Thailand, kila nyumba unayoiona Thailand ni kiwanda ndani. Leo order zote za nguo za watoto duniani, nguo zote nzuri zinatoka Thailand.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna soko hapa, tunazungukwa katika nchi za Afrika Mashariki, tunashindwaje sisi kushona? Tunashindwaje kupeleka kule kwenye vyuo vya ufundi? Ila kule kwenye vyuo vya ufundi, ada ni shilingi 60,000 day; na ukilala boarding ni shilingi 120,000. Hawa mkiwakopesha kama wanaokopeshwa wenye degree, wanaotoka kwenye elimu ya msingi, wanaotoka kwenye elimu ya sekondari wakafeli. Wakopesheni wakasome VETA.

Kwanza mkopo ni mdogo, anasoma miaka miwili shilingi 120,000, huyo analipa tu. Kule anafundishwa welding anafundishwa kutengeneza simu; ni kazi, leteni kozi za watu wanaokwenda kufanya, akitoka pale miezi sita anaweka meza anatengeneza simu. Atashindwaje kulipa deni la shilingi 60,000?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mnakuwa na mitaala ya ajabu kabisa. Yaani watu wanatoka kule hawawezi hata kukata kucha, unakaa unamwona mtu anapakwa na rangi. Yaani hata hawezi hata kupaka rangi kwenye miguu yake, anapakwa na mwanaume, anashikwa namna hii anapakwa rangi, hajui hata kupaka rangi. Mitaala gani katika nchi hii? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri katika jambo lingine kwa ndugu zetu wa Wizara ya Elimu. Elimu ya Sekondari; O’level na Advance pamoja na vyuo lazima mvichukue kutoka TAMISEMI. TAMISEMI ina mizigo mikubwa, mnakimbia jambo lenu. Kwa hiyo, ninyi sasa hivi Wizara ya Elimu mnatusaidia nini sisi watu wenye elimu huku chini?

Mheshimiwa Naibu Spik,a kwa sababu sasa hivi mmebakiza kukaa kwenye mitihani peke yake. Baraza la Mitihani ndiyo lenu. Sasa mtoto anatoka huku TAMISEMI, wana shule 14 za msingi bado mnataka kuwaongezea sekondari, zipo zaidi ya 5,000 halafu ninyi mnafanya kazi gani? Kwa nini mnamkimbia mtoto wenu? Chukueni elimu ya sekondari TAMISEMI, huku chini tuachieni elimu ya msingi na chekea. Sisi tuwaandalie na ninyi mwendelee na kazi, lakini habari ya kukimbia hiyo nafasi, siyo sawa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja nimalizie mchango wangu, nakuomba.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. TABASAM J. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Naomba wachukue shule zao za sekondari; advance na O’level zichukueni Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kunipa nafasi kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Mheshimiwa Aweso kwa kule Mwanza sisi wewe ni bado green guard tu, lakini maskini wa Mungu sasa umezeeka, yani unaota upara kwa ajili ya maji, lakini Mungu atakulipa. Dada yangu, Mheshimiwa Naibu Waziri, Mungu atawalipa; kazi ya maji ni sadaka. Msione Wabunge humu ndani wanalia maji, Mheshimiwa Rais yeye mwenye anajua kabisa kazi anayokuja kufanya ni sadaka kwa wananchi wa Tanzania na Mwenyezi Mungu atamlipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kwetu katika Mkoa wa Mwanza hakuna mahali popote ambapo haufanyiki mradi wa maji. Magu kuna mradi mkubwa wa zaidi ya mabilioni, ambao unakamilika sasa hivi; Misungwi kuna mradi wa bilioni 45; sasa hivi hapa tunapiga hesabu mradi wa Majimbo ya Sumve na Kwimba pekee yake tu wana bilioni 41; Sengerema mimi hapa sasa hivi katika miradi iliopo kuna mradi mkubwa wa bilioni 21 na sasa hivi kuna mradi wa bilioni 17, huyu mama tunataka tumpe nini? Na bado anahikikisha tena tunapata mitambo 25 kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ninachoshauri tu ni kwamba hii mitambo Mheshimiwa Waziri Aweso muhakikishe wataaalam wanaokwenda kuihudumia mitambo hii tusije tukashindwa kufika 2025 hatujamaliza kero ya maji kwa nchi hii; hakuna mtu ambaye atakosa maji. Hawa wanaosema wanakosa maji kutoka Ziwa Victoria kuna mitambo itachimba.

Mheshimiwa Spika, na mimi ninachotaka kukuambia ni kwamba badala ya kuigawa hii mitambo kwa mikoa, iende kwenye kanda ili tufanya kazi kwa pamoja. Wilaya moja inaweza ikashambuliwa na mitambo mitatu au minne ionekane kazi ya Mheshimiwa Rais. Haya ndiyo maono yake, yaonekane kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, hakuna mbadala wa maji kama unavyosema. Na hii Wizara yako mara nyingi nakusikia unasema siyo Wizara ya ukame, na mama ameshatuhakikishia kwamba suala la maji katika nchi hii litakuwa historia. Waheshimiwa Wabunge, kubalini mipango Mheshimiwa Rais anayoifanya sasa hivi kupitia Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso, ushauri wangu ni kwamba kwa kutumia magari haya ambayo uyatumia sasa hivi kuendelea na safari, kutembea nchi nzima unaweza ukachoka kuifikia miradi yote kuikagua. Sasa hivi duniani watu wanakwenda katika mabadiliko. Gharama za kutumia helikopta Watanzania wanatakiwa waambiwe; kutumia helikopta ni gharama ndogo sana, mafuta lita 400 ukitoka na jet kutoka Dar es salaam unaweza ukakagua miradi 10 mpaka kufika Sengerema.

Mheshimiwa Spika, mnashindwaje idara kama hii, Wizara ya Maji mna miradi mikubwa ya mabilioni, kutoa pesa bilioni moja na nusu mkanunue helikopta. Na unakagua miradi yote kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nimekuona juzi unaangalia bwawa unadaganywa bwawa lilikuwa hapa; bwawa linaweza likapotea? Hawa watu wengi wanakuwa sio waadilifu. Sasa unakuja kuambiwa kwamba mara paipu zilipaa. Paipu zinaweza kupaa namna gani zimechimbiwa chini? Sasa hii yote ni kwa sababu unachelewa kufika katika yale maeneo. Jitahidi Mheshimiwa Aweso, wewe ni mdogo wangu, na Mwenyezi Mungu atakulinda na sisi tunakuombea dua.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wenzangu, ninachotaka kuwaambia ni kwamba kazi ya kusimamia miradi hii ya Serikali siyo mchezo. Hii miradi ya maji ni mingi sana katika nchi hii. Tuwe waadilifu, sisi wenyewe Wabunge twende tuka-visit hii miradi, tusisubiri kuja kulaumu ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, tuchukuwe majukumu yetu. Wabunge tuchukukuwe majukumu yetu jamani, tuhakikishe tunamsaidia Waziri kutoa taarifa. Na bahati nzuri ile Wizara yake nimekwenda kule mara nne, unafika unapewa chai unapewa na korosho. Juzi nilipewa korosho nikashangaa mimi, nimekwenda na shida ya maji nikapewa korosho na kukaribishwa chai, nikapewa na maji ya kunywa.

Mheshimiwa Spika, miradi ya ma-tank Sengerema, nakushukuru sana. Umeweka tank Sengerema lita milioni 5; siyo mchezo. Tunaweka kwenye chanzo cha Nyamazugo, Nyamkurukano kuna lita kama milioni mbili; haya maji yaliyoko Sengerema yanaweza yakatosha kuilisha Geita, Boshosa na kila mahali tukamaliza miradi ya maji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso, karibu Sengerema, dada yangu karibu Sengerema, mmekuja mmeona ile hali iliyopo, endeleeni kuwa waadilifu na Mwenyezi Mungu atawalinda.

Mheshimiwa Spika, Katibu Mkuu Sanga, najua unafanya kazi kwa niaba ya nchi. Unatoka hapo DUWASA, mimi nakukuta pale mpaka saa sita za usiku, mimi nipo jirani pale Sanga, Mwenyezi Mungu atakulipa. Hii kazi ni ya sadaka, wananchi wanakuona wala usiwe na wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na wakati mwingine hawa watu wawe wanapewa hata zawadi hapa Bungeni kwa kazi wanayoifanya ya maji. Lakini Mheshimiwa Rais tumuombee kwa Mwenyezi Mungu; Wabunge hapa tumuombee, kazi ya maji siyo mchezo katika nchi hii. Tusiwe tunalaumu tu muda wote.

Mheshimiwa Spika, nchi hii ni kubwa, hii nchi siyo ndogo kama Burundi au Rwanda hapana. Kuna wananchi zaidi ya milioni 60 wote wanataka maji; siyo mchezo. Mheshimiwa Aweso, endelea tu kutusikiliza hivyo hivyo, lakini tunalia kwako na miradi yetu iweze kwenda. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia katika bajeti hii ya Wizara yetu pendwa ya Afya.

Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza sana Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya madaktari wao, madaktari bingwa katika nchi hii, tumeona jitihada zao za dhati kutoka moyoni, kuanzia Jakaya Kikwete Muhimbili hapa Benjamini Mkapa, Bugando Mbeya na KCMC inaonyesha ni namna gani madaktari wetu katika nchi hii sasa wanaanza kwenda mbele zaidi ya uzio.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi ushauri wangu kwa Wizara, ni kwamba lazima ifikie sasa Wizara iunde timu ya madaktari bingwa labda, kwa sababu tunazo wilaya 139 na hao madaktari bingwa wawepo madaktari bingwa ambao ni mobile unit, wanaotembea.

Mheshimiwa Spika, hawa madaktari bingwa katika nchi hii watapunguza mrundikano kule Muhimbili, kwa sababu sisi tunajua kwa kalenda, kama labda Mkoa wa Mwanza kuna madaktari kumi; wanaingia madaktari bingwa wa macho, viungo, figo na moyo. Wakifika pale tunaambiwa kwamba Sengerema watakuwepo kwa wiki mbili au kwa siku mbili; wale madaktari bingwa watasaidia watu wetu ambao ni maskini ambao hawana uwezo wa kusafiri kuja katika hospitali za rufaa.

Mheshimiwa Spika, katika hili tunamshukuru Mheshimiwa Rais sasa vifaa tiba vimeanza kupelekwa nchi nzima. Tuna kila kitu katika hospitali zetu za wilaya. Mnafeli wapi watu wa Wizara ya Afya katika jambo hili?

Mheshimiwa Spika, Tunaona hospitalli zetu za makanisa Wajerumani wale Waholanzi wana ma-flying doctors wale, wanasafiri wanakuja Itigi, Sengerema na kwingine, na wanafanya jambo kubwa sana. Wanakuja na meli, sisi tumewahi kwenda kutibiwa na Wachina kwenye meli bandarini. Hapa tuna madaktari bingwa wamemaliza elimu zao, kwa nini msitengeneze unit hiyo ya madaktari bingwa ambao bado hawajapata ajira lakini wawekwe katika sehemu hiyo? Wale madaktari watasaidia sana kupunguza magonjwa hayo ambayo wananchi wamekaa nayo kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala jingine ambalo nataka niishauri Wizara hii ni kwamba, tunayo magonjwa haya ya mlipuko ambayo yamezunguka katika ukanda huu wa maziwa makuu haya magonjwa hayajaisha naishukuru sana Wizara kwa kuchukua hatua ya haraka katika hili gonjwa lililojitokeza Bukoba watu wengi waliona kwamba wale Watanzania inakwenda kuangamia lakini jambo hili waliweza kulidhibiti ndani ya siku kumi likaisha tunaipongeza sana Wizara katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule Usukumani wamenituma nije nishukuru wanasema yule Mama wa corona mbona hatumuoni, hali sasa siyo nzuri sasa tunataka huyu Mama wa corona sasa leo aje aseme hapa, je, corona imeisha? Kwenye nchi hii? hawa wanaokufa wanakufa kwa mafua tu? Au wanashindwa kupumua?

Mheshimiwa Spika, sasa haya tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri katika majumuisho yako uje utueleze haya magonjwa ya mlipuko ni namna gani mmejipanga nayo; na kama yamekwisha au kama hayajaisha basi tuendelee kuchukua tahadhari. Unayo nafasi kubwa sana kwa mujibu wa sheria kuwaeleza Watanzania nini kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, nakuja kuzungumzia hospitali zetu za wilaya. Hizi hospitali za wilaya sasa hivi zinapelekewa madaktari zimepewa vifaa tiba nchi nzima, lakini tunavyo vituo vya afya na zahanati. Sasa kule kwa sababu kuna madaktari sasa wanahitajika madaktari bingwa. Leo vituo vyetu vya afya vilikuwa havijapata madaktari vinapelekewa madaktari. Sasa, kama mnapeleka madaktari kule kwenye Hospitali zetu na vituo vya afya basi hizi hospitali za wilaya mziweke katika sehemu ya hospitali za rufaa. Kwa sababu, kwa mfano kwenye jimbo langu mimi nina hospitali vituo vya afya ninavyo vinane bado nina zahanati karibu zahanati 30.

Mheshimiwa Spika, sasa unategemea kwamba wagonjwa wale tunawapa rufaa kuwapeleka Bugando au Sekou Toure hospitali inakwenda kuelemewa. Ninachoomba mimi katika sera sasa za Wizara mzitambue kuzichukua hizo hospitali za wilaya ziwe zenu, madaktari bingwa wapelekwe kule ili tupunguze msongamano Muhimbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hili wazo Mheshimiwa Waziri alichukue. Katika majumuisho yake aje atuambie; kama wanaweza kuhudumia, kupeleka vifaa tiba na kila kitu kwa nini wasilete madaktari bingwa kule? Vifaa vya maabara na wataalamu wamepeleka, isipokuwa hatuna madaktari bingwa naomba sana Wizara wachukue jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, jingine ambalo ni la muhimu sana ni suala la huduma bora kwa hawa wagonjwa wetu. Tunakwenda kutoa huduma bora lakini muangalie na madaktari katika nchi hii sasa nao wapewe huduma. Madaktari wanakiumbia katika nchi hii, wanaondoka. Wauguzi nao muwajali sasa ifikie hatua…

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. TABASAM H. MWANGAO: Mheshimiwa Spika, niache basi Mheshimiwa nimalizie.

SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwanaisha Ulenge.

TAARIFA

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nilikuwa naomba kumpa taarifa tu Mheshimiwa tabasamu kwamba, hata vitabu vitakatifu vimeisema vizuri nafasi ya daktari na imeisema; “Innal Muallima Wa Twabiba Kila Humaa, Laa Yanswahan Idhaa Huma Lam Yukramaa Fakna-A Bijahilika In-Jaufata Muallimu, Fasbir Lidaika In Jaufata Twabiba,” kwamba; ridhika na ujinga wako ukimuudhi mwalimu, lakini subiri maradhi yako ukimuudhi daktari. Madaktari ni watu muhimu sana, tusiwaache watoke nje. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu unaipokea taarifa hiyo?

MHE. TABASAM H. MWANGAO: Mheshimiwa Spika, ameanza kwa Aya kwa hiyo amenipiga kwa Aya, na mimi kama muumini naunga mkono taarifa yake.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la utoaji wa huduma zetu za afya. Viongozi wetu wa kitaifa wamekuwa wakipita kule katika wilaya zetu, wanapita katika na mikoa, tarafa na kata, wanatoa ahadi kwamba hapa patajengwa hospitali ya wilaya, patajengwa kituo cha afya, patajengwa zahanati.

Mheshimiwa Spika, sasa tunamuomba sana Waziri wa Afya, hizi ahadi za Marais, ahadi za Waziri Mkuu, ahadi za Mawaziri wao wenyewe mnazozitoa kwa wananchi zinakuja kututesa sisi. Sisi Sengerema tunakushukuru ulitoa ahadi ya kujenga Kituo cha Afya Chifufu, kile kituo cha afya Mheshimiwa Waziri wamenituma nije nikushukuru kimeisha, tunakupongeza sana kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, alipita Hayati John Pombe Magufuli pale Busisi, na pale Busisi ni kwao, akatoa ahadi kwamba kuna kituo cha afya kinajengwa pale akiwa na Naibu Waziri Mollel; hili jambo mpaka sasa hivi mnataka labda mimi nikashindwe uchaguzi, kuna lawama zingine zitakuwa zinanitafuna mimi kwa sababu Mheshimiwa Mollel ulikuwepo. Sasa, naomba leo kwenye majumuisho hapa mkija mseme lini Kituo cha Afya cha Busisi kinakwenda kukamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jamani tuziheshimu hizi ahadi za Marais. Marais wanapopita kule kwetu sisi wanatuacha na hali mbali. Mnakuja kwenye bajeti hivi viyu havimo, inakuwa ni hatari. Sasa naomba kwenye majumuisho ya Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Waziri waje waseme lini jambo hili litakuwepo.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho nina Hospitali ya Wilaya. Wewe mwenyewe Mheshimiwa Ummy ulifika pale na umeiona ile hospitali. Mheshimiwa Jafo alipita pale akaona; na leo wote mmo humu. Mheshimiwa Mollel hii Hospitali ya Wilaya imeshakamilika kila kitu. Ni kwa nini hospitali hii haifunguliwi? Naomba majibu katika hayo.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa nakupongeza leo umekaa kwa utulivu mkubwa na mimi nakuunga mkono dakika zangu kumi hazijatosha nimeacha dakika mbili kwa wengine.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Mungu akubariki sana, amina. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nimesikiliza hotuba ya Waziri Mheshimiwa Bashe. Mheshimiwa Bashe ni ni Waziri wa 27 wa kilimo katika nchi hii toka tumepata Uhuru. Katika hao Mawaziri 27 ni kwamba tulikuwa tuna Mawaziri wanane baada ya kupata Uhuru. Mawaziri hawa wanane walisimama katika uzalishaji wa mazao makuu sita katika tuliyokuwanayo katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hawa Mawaziri wanane tuliokuwanao katika utawala wa Hayati Baba yetu wa Taifa Mheshimiwa Julius Kambarage Nyerere, ni Waziri mmoja tu aliyekaa katika miaka mitano; 1975 mpaka 1980, Mheshimiwa John Malecela ambaye yuko hai, katika miaka yake mitano alisimamia mazao sita ya kimkakati. Zao la kwanza likiwa pamba; zao la pili likiwa kahawa; zao la tatu, mkonge; zao la nne, korosho; zao la tano, chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mazao yalileta pesa nyingi sana za kigeni, lakini mazao haya yalionesha biashara. Mapinduzi ya biashara yalianza kuonekana katika misimu yetu katika nchi hii, ikawa ni misimu yenye kashikashi ya biashara. Unajua kwamba mwezi wa sita bei itatangazwa ya pamba, mwezi fulani itatangazwa bei ya Kahawa na mwezi fulani itatangazwa bei ya kitu fulani, mwezi wa kumi itatangazwa bei ya korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili lilileta mapato makubwa katika nchi hii; na idadi yetu ya wananchi katika nchi hii walikuwa ni wachache, leo nchi inakwenda kuwa na wananchi zaidi ya milioni 60, lakini tumeondoka katika haya mazao yetu ya kimkakati, haya mazao yameachwa. Nawe Mheshimiwa Bashe sasa hivi tunavyozungumza, ni kwamba umekuja kuongeza mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mpo katika Wizara yenu ninyi, hii ya kilimo katika mwaka 2011 mpaka leo, wamekaa Mawaziri zaidi ya wanane na wewe hapa sasa hivi unakuwa ni Waziri wa tisa. Mmeongeza zao la mchikichi, mmeongeza zao la alizeti, mmeongeza zao la mpunga, mmeongeza mahindi na parachichi kama matunda, lakini hayo mazao yote ya kimkakati, ninachoona mimi, ushauri wangu Mheshimiwa Bashe ni kwamba lazima ifikie mahali mkamshauri Mheshimiwa Rais kwamba tunahitaji sasa wawepo Manaibu Wawili katika Wizara yako. La sivyo, utachoka. Huwezi kusimamia mazao ya kimkakati 12, wakati huo huo mwende katika mazao mengine mchanganyiko, na wakati huo huo tunataka mbolea, wakati huo huo tunataka viuatilifu, itakuwa ni ngumu sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba bajeti hii ya kilimo ni ya kwanza toka tumepata Uhuru ya kiwango cha juu kiasi hiki. Inaonesha dhamira ya Mheshimiwa Rais moja kwa moja kwenda kwa wakulima kuwasaidia waweze kutoka. Sasa kama tunataka tutoke kwa kilimo hiki tulichonacho, nimekuona Mheshimiwa Bashe umejitahidi sana. Wewe ni miongoni mwa Manaibu Waziri waliokaa na Mawaziri tofauti karibu miaka sita. Ni Naibu Waziri pekee katika nchi hii aliyekaa kwa miaka mingi, alikuwa ni Sumaye. Sumaye amekaa kwa miaka 10 kama Naibu Waziri, na baadaye akafanya vizuri akaja kuwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na historia ya Wizara Kilimo ilivyo, Manaibu mnaokuja kupata nafasi hii kuwa Mawaziri wa Kilimo mmepita katika changamoto nyingi katika nchi hii. Sasa nafasi yako kama kijana, uende kwa hawa wazee, bado wako hai; nenda kwa Malecela ukamsikilize aliwezaje ku-perform? Nenda kwa Sumaye ukamwulize, aliwezaje ku-perform? Kwa sababu naye alikuwa kijana kama ninyi. Leo mkiacha kuwasikiliza hawa wazee, ni kwamba bado mtapewa fedha nyingi na hamtaweza kuzifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kwamba hizi pesa zilizotajwa kwa wingi wake, ni kwamba kwenye irrigation tayari kuna ongezeko kubwa la pesa tumepewa, kwenye utafiti kuna pesa nyingi tumepewa. Sasa hizi pesa zigawanyike vizuri katika suala la utafiti. Ushauri wangu ni kwamba, hivi vituo vyetu vya utafiti, kuna TARI halafu kuna Mwanza pale Ukiriguru, tunaomba waingie katika utafiti katika mazao haya ya kimkakati. Tuangalie mbegu gani ambazo zitakazoweza kutumika na mbegu ambazo tutaweza kutoa mazao mengi ndiyo zifanyiwe kazi. Pia gharama za utafiti pia mziangalie sana, zinaweza zikawa kubwa na zisije kuwa na tija. Hili uliangalie sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine cha msingi katika jambo hili ni kwamba tunakuja kuzungumzia suala la umwangiliaji. Tumepata skimu nyingi sana za umwangiliaji katika nchi hii, zinakuja kuongezeka na fedha mmepewa nyingi za kutosha. La kwanza ambalo linanitia shaka, kwenye kituo hicho cha umwangiliaji hapo Iringa Road, hao watu wanaokaa pale kwa ajili ya utafiti wa umwangiliaji na kushughulika masuala ya umwangiliaji wanakaa kwenye mabanda ya stoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama hawa watu mnaenda kuwapa zaidi ya Shilingi bilioni 200 na kitu, kama 300, angalia na ofisi zao hao watu wanazokaa. Wanakaa garage. Mimi nimeenda juzi kuangalia, wapo garage Mheshimiwa Waziri. Unayeenda kumpa pesa kiasi hicho, bado hata ofisi hana, itawezekana wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika suala hili ni kwamba usiangalie mabwawa ya irrigation peke yake, lazima mchimbe visima tuingie katika umwangiliaji wa visima. Wenzetu Kenya sasa hivi wanamwagilia mashamba yao kwa kutumia visima. Hapa tumefaulu.

(Hapa kengele ililila kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine, naona kengele imelia…

MWENYEKITI: Ndiyo Mheshimiwa. Muda wetu wa kuchangia asubuhi hii umeisha.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Dah, sasa…

MWENYEKITI: Malizia kuunga mkono hoja.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda ni mdogo, naogopa kuunga mkono hoja.

MWENYEKITI: Muda wetu umeisha kwa sababu time ya asubuhi ndiyo hiyo imeishia hapo.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi kuchangia Muswada wa Sheria ya Mabadiliko katika Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hiki Kifungu cha 16 (47) ambacho kinazungumzia suala la TARURA la hizi fedha shilingi 100 ambazo zinakusanywa. Sasa pesa hizi ni kwamba zilipigiwa kelele na Wabunge na wakaomba mahali gani pa kutoa pesa hizi na tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kukubaliana na Wabunge wenzake na kuona kuna umuhimu wa kutengeneza hizi barabara. Najua na yeye katika Kifungu hiki atatengeneza barabara zake katika maeneo mengi katika Jimbo la Iramba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika jambo hili kuna hii asilimia 30 kama inavyozungumzwa na Wabunge wengine ilikuwa ni shilingi 78.90 kwa hiyo ikichukuliwa hii shilingi 78.90 na ikajumlishwa shilingi 100 ikawekewa ring fence kwa siku kwa uuzaji wa mafuta lita milioni 12 kwa siku tuna uwezo wa kupata bilioni 2 na milioni 148 kwa siku pesa ambazo zitakwenda TARURA na kwa mwezi tunapata zaidi ya milioni kama bilioni 64 hivi. Kwa mwaka inaonesha tuna uwezo wa kupata bilioni 778. Sasa bilioni 778 haziwezi kuachwa hivi hivi, hiki ni kitu kikuba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, ushauri wetu sisi ni kwamba huku kwenye pesa hii ambayo itabakia ya TANROADS wana shilingi 184.10 na TARURA tutakuwa na shilingi 178.90 inamaanisha kwamba Bodi iliyoko pale ya Mfuko wa Barabara bodi hii inaundwa na Waziri wa Ujenzi isipokuwa mtu mmoja tu anayeteuliwa na Mheshimiwa Rais. Sasa wana mfuko wao wao na wana bodi yao, sisi ambao tumepiga kelele kwa sababu ndiyo tunakokaa na wananchi kule vijijini na sisi tunaomba katika sheria hii iundwe Bodi yet una Mfuko wetu ili kumfanya Waziri wa Serikali za Mitaa aweze kuwajibika na hizi pesa kwa sababu wale wajumbe wa Bodi yeye ndiyo mteuzi wake lakini atateua jina ambalo litakwenda kupitishwa na Mheshimiwa Rais ili sisi tuwe na uhuru na hizi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasahivi Serikali za Mitaa ni kwamba hawana Bodi yao hawa watu wa Serikali za Mitaa kwa ajili ya barabara za vijijini na hawana mfuko wao. Itawekwa ringfence tu peke yake lakini Mfuko haupo. Kujua usalama wa hizi pesa bado kutakuwa na mgogoro baadaye. Sasa hii shilingi 30 tuhakikishiwe na Waziri wa Fedha akija hapa kwenye majumuisho tujue sasa kama hii shilingi 30, shilingi 78 na shilingi 100 zote zinakwenda TARURA na ziweko kwenye sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jingine hili suala la sheria hii ambayo inakuja kuingia, hii Sheria ya withholding Tax, sheria hii inaleta kidogo kigugumizi kwamba mwananchi anakwenda kuuza mazao yake iwe samaki au ni embe au chochote kuuza kiwandani akatwe hizi pesa na wakati huo amelipa ushuru kutoka kwenye halmashauri husika.

Kwa hiyo, huyo mwananchi ambaye ni mkulima au mvuvi atalipa kodi mara mbili. Hii asilimia 2 sio ndogo, ni nyingi na kama anauza kila mwezi kwa mwaka anakwenda kufanya jambo hili haya malipo yatakuwa makubwa sana kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfanyabiashara mkubwa, hii withholding tax kwake sio shida kwa sababu atauza na siku akienda kufanya hesabu zake za kulipa kodi yam waka atakata hizi withholding tax atapeleka pale kuonesha katika hesabu. Haya huyu mkulima atapeleka wapi? Kwa hiyo, analipa ushuru katika Halmashauri husika na anakwenda kulipa tena withholding tax huko Serikalini. Tunaomba tu kwamba tusiwakatishe tamaa hawa wakulima wetu. Wanaanza kuona kodi zinakuja hizi inakuwa ni mtihani kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, tusitie mchanga kwenye kitumbua ambacho umekipika vizuri sana. Yaani leo wananchi wanashukuru sana bajeti hii. Wakisikia tena kuna kodi wanawekewa hii italeta shida naomba tu uje uielezee vizuri ili wananchi huko vijijini waone kwamba kazi tunayokwenda kuifanya katika Serikali hii basi na yenyewe kwao inaenda kuwapa manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo nashukuru sana, nakuunga mkono sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa hii bajeti yako na kama huu ushauri wetu utausikia kuunda Bodi yetu ya TARURA kule na Mfuko wake uende kule hongera sana Mungu akujaalie sana katika hii miaka mitano ya utendaji wako kazi. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wa Mwaka 2022
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kuchangia Muswada huu wa Sheria wa Bima ya Afya. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuelekeza jambo hili limalizwe na lipate ufumbuzi. Pamoja na mimi kuunga mkono hoja hii, nina sehemu ambayo napata wasiwasi ambao wasiwasi huu Mheshimiwa Waziri akija katika majumuisho atakuwa kuwaeleza Watanzania wakiwemo wa Jimbo la Sengerema.

Mheshimiwa Spika, hii Bima ya Afya wasiwasi wangu mkubwa upo katika eneo ambalo sijaona mpango wa kina mama Wajawazito watahudumia wa namna gani katika mpango huu, kwa sababu Wajawazito na watoto tumeambiwa wanatibiwa bure. Lazima wawekwe kwenye mapango ili waweze kupata huduma iliyo sahihi, kwa sababu wapo akina mama ambao wanataka wakajifungulie labda katika hospitali kubwa. Hawa wanatakiwa wawekwe katika eneo gani?

Mheshimiwa Spika, la pili, suala la mpango wazee, kwa sababu hakuna yoyote ambaye amekubali yeye kuzeeka, yaani tunajikuta tu tunaenda kuzeeka. Sasa wazee sijaona mpango umekaaje katika Bima ya Afya. Je, wazee watawekwa katika kundi masikini au kundi la watu mafakiri? Ni vizuri Mheshimiwa Waziri akija hapa aje atueleze wazee watawekwa wapi kwa sababu wamelitumikia Taifa hili kwa nguvu kuwa hata ni Mkulima Mfugaji, amefanya kazi katika Taifa hili.
Mheshimiwa Spika, siku moja mimi nilikuwa hotelini nilimuona power mmoja, sikutaka kutoa mfano huu lakini alikuwa ni power maarufu katika Afrika Mashariki na Kati, aliipa heshima sana Tanzania, lakini nikamkuta ni mgonjwa wali maharage sahani ndogo hawezi kuila akamaliza. Nikamuuliza vipi kaka? Akaniambia yeye mgonjwa. Sasa hii hali ya namna hii tayari ameshazeeka lakini kama angekuwa na Bima ya Afya angekuwa yupo vizuri sana katika uzee wake na sisi tunaelekea huko.

Mheshimiwa Spika, jingine ambalo wasiwasi wangu, kuna lugha imetumika watu masikini. Katika Kamusi ya Kiswahili, watu masikini wamekaa katika angle nyingine wapo katika sehemu ya ulemavu na watu wenye mahitaji maalum. Lugha nilikuwa naona ingetumika watu mafakiri. Sasa tungejua, kwamba hawa masikini na mafakiri watakuwa katika eneo lipi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri akija atakuja kutueleza.

Mheshimiwa Spika, jingine wasiwasi wangu upo katika vyanzo vya pesa. Vyanzo vya pesa hivi vilivyotumika nina imani baadaye tutakuja tupate upinzani mkubwa kwa viongozi wa dini, kwa sababu inaoneka pesa tunazitoa kwenye kamari, pesa tunazitoa kwenye vipodozi. Sasa tunataka hawa akinamama waongezewe kodi na wenyewe waache kujipodoa wawe kama wanaume haiwezekani. Lazima akinamama wajipodoe tuwapende. Sasa tukianza kuweka kodi hayo itakuwaje? Hili jambo halijakaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimuelekeze Waziri wa Fedha angalie vyanzo vingine. Jamani ni kwamba kwa mfano, natoa mfano tu ambao kidogo unaweza ukawa siyo mfano mzuri lakini ndivyo ilivyo. Tunakwenda kumaliza Miradi kama ya Bwawa la Mwalimu Nyerere kule kuna pesa tunatenga sisi zaidi ya shilingi 100, katika mafuta. Kwa nini pesa zile zisichukuliwe kwa sababu huu mfuko tunakwenda kuuanza Mwaka 2026.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lazima tuandae vyanzo vilivyo sahihi. Tusilete ugomvi tena tunatoka katika ugomvi tunaleta ugomvi, kwa sababu sisi tunatumia mafuta lita milioni 12 mpaka 13 kwa siku. Kule ikiweka shilingi moja tu, kwenye lita ya mafuta ni shilingi 12, kwa siku na kama tunaweka shilingi tano ni milioni 60 kwa siku. Kwa hiyo, ule mfuko unaweza ukatengeneza fedha zake kwa mifumo hiyo na tukaweka ring fence badala ya kwenda kuchukua pesa kwenye kamari tunamtibu raia, mcha Mungu kama Tabasam nikatibiwe na pesa ya kamari. Sasa hii inakuwa hatari. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine dogo sana, suala la zahanati. Hivi vipimo vyetu vya afya; kule kwenye zahanati kuna vipimo Mheshimiwa Waziri. Mtu anatumia bima ile katika vipimo katika zahanati, akipewa rufaa kwenda kituo cha afya, akifika kituo cha afya vipimo tena. Akitoka kituo cha afya anakwenda hospitali ya Rufaa ya Wilaya. Kule nako tena daktari atakuwa hana Imani, lazima ampime tena. Akitoka tena pale anahamishiwa hospitali ya Mkoa, Sekou Toure tena, vipimo tena. Akitolewa tena Sekou Toure anapelekwa Bungando, kwa sisi watu wa Mwanza, hospitali ya rufaa vipimo tena, daktari ajiridhishe. Akitoka pale tena anahamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, vipimo tena.

Mheshimiwa Spika, sasa hii ni lazima sheria ije; na mimi ninamuunga mkono sana Mheshimiwa Mbunge wa Manyoni aliyesema kwamba hii lazima iundiwe authority, iwe ni mamlaka sasa zitengenezwe sheria.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la bei za matibabu katika hospitali zetu za Serikali zinajulikana, lakini unaweza ukafanyiwa operation hiyo hiyo ya henia kwenye Hospitali ya Wilaya ya Sengerema kwa shilingi laki moja, operation kama hiyo hiyo ya shilingi laki moja na elfu arobaini ukifanyiwa Aghakan ni shilingi milioni tatu na laki sita. Haiwezekani, huu mfuko utakufa hata kama tutapata fedha kutoka mbinguni, haitawezekana.

Mheshimiwa Spika, lazima sasa tutengeneze mfuko wa matajiri na mfuko wetu sisi. Watakaokwenda kutibiwa katika Hospitali za private wawe na mfuko wao na sisi tunaokuja kutibiwa kwenye Hospitali za Serikali tuwe tuna mfuko wetu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine, wasiwasi wangu ambao kidogo Mheshimiwa Waziri aje utusaidie; ni kuhusu haya magonjwa makubwa kama ya moyo, figo na kansa. Haya magonjwa yawekwe pia katika mfuko huu. Mfano, kama hawa wanaotibiwa kwa dialysis. Kila siku ya Mungu mtu anakwenda kutibiwa, sasa kama atakuwa hayupo kwenye mfuko huyu mtu si anakufa?

Mheshimiwa Spika, pia niongelee suala la kulipa bima ya afya. Tunashukuru wameitoa miezi mitatu mpaka mwezi mmoja. Lakini umelipia leo bima yako ya afya una shilingi laki tano au laki tatu, baada ya wiki ukaugua unasubiria unaambiwa bwana bima yako ya afya ku-mature ni mpaka mwezi; na hili pia liangaliwe. Jamani sisi tuna watu masikini, akienda kuitoa fedha yake kama ni shilingi elfu sitini amemaliza ndani. Hili liangaliwe pia.

Mheshimiwa Spika, juzi nilifiwa na Diwani wangu kule Sengerema. Mheshimiwa Diwani yule nilikwenda kumchukua Bugando Hospital na alikuwa na bima ya afya ya halmashauri. Tumefika pale ninaambiwa kwamba mgonjwa wenu anadaiwa fedha za mochwari. Nikauliza vipi? Wakasema bima yake imekufa. Kwamba, alivyokufa tu na bima ikafa. Hii sasa inakuwaje? Mheshimiwa Waziri tuwekee hili jambo tuelewe vizuri, haiwezekani mimi nimekata bima ya shilingi laki tano nimeenda hospitali leo nikafa na bima yangu ife, nilipie tena, ndugu waanze kuchanga fedha badala ya kuchanga fedha ya sanduku wanaanza kuchanga fedha ya kunitoa mochwari ilhali nina bima; haiwezekani. Tukubaliane kwamba mpaka nitakapozikwa ndipo bima yangu ife. Hii tunaomba utusaidie sana Mheshimiwa.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ni kuhusu hivi vitita. Kwenye hivi vitita kuwepo na aina ya vitita vya kutibiwa nje ya nchi kwa sababu kuna wagonjwa wanaopelekwa na Serikali nje ya nchi. Serikali inabeba mzigo mzito sana kutibu wagonjwa nje ya nchi. Mheshimiwa Waziri wa Afya anajua; leo kuna vibali pale vipo vingi na fedha nyingi zinatumika kwa ajili ya kutibu watu nje ya nchi. Sasa raia awe ana haki, kama kutakuwa kuna kitita cha shilingi milioni tano ili akiugua apate nchi mbili duniani. Nchi moja inaweza kuwa Asia, nyingine Afrika na na nyininge Ulaya. Kuwepo na kitita cha namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ninaomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja.