Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Ali Juma Mohamed (3 total)

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri nilikuwa na swali moja tu la nyongeza.

Serikali ina mpango gani wa kutafuta fursa mbalimbali za ajira ambazo ziko katika nchi mbalimbali duniani, kwa ajili ya Watanzania hususan nchi ya Qatar ambayo mwakani ni wenyeji wa Kombe la Dunia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Ali Juma Mohamed, Mbunge wa Shaurimoyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuchangamkia fursa kwa ajili ya Watanzania kwenda kufanya kazi nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kukufahamisha kuwa Serikali imeanza mazungumzo na nchi mbalimbali ambazo zina fursa ya ajira hizo, hasa zikiwemo nchi za Ghuba, ili kuwa na utaratibu maalum wa kutoa quarter maalum kwa ajili ya Tanzania. Ninapenda kutoa taarifa pia kwamba tayari Tanzania imesaini mkataba na nchi ya Qatar kwa ajili ya kuwa na quarter maalum ya watanzania kwenda kufanya kazi huko, hasa katika kipindi hiki ambako tunaelekea kwenye mashindano ya World Cup ambayo yanaanza Novemba mwakani 2022. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nilikuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani kwa kutumia ofisi zetu za kibalozi kuwasaidia wale vijana wetu wa Kitanzania ambao tayari wameshapata fursa ya kufanyakazi nje ya nchi, lakini mara kwa mara wamekuwa wakipata matatizo na shida ambazo wanakosa kusaidiwa?

Lakini la pili Serikali ina takwimu rasmi za vijana wote ambao wanafanyakazi nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mohamed kwa kuangalia sana haya maslahi ya ajira ya Watanzania nimpongeze sana kwa kazi hiyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi yetu, Ofisi ya Waziri Mkuu inashirikiana vizuri na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kwa kuhakikisha kwamba masuala haya yanaratibiwa vizuri na hata hivi sasa tumekwisha kuanza utambuzi huo wa vijana wapo ambao walikuwa wanaenda wenyewe bila kutoa taarifa kwenye ubalozi au kwenye nchi na wamekuwa wakipata matatizo mbalimbali tumewaomba na tumetoa rai kwamba waendelee kujisajili kwenye Balozi zetu.

Lakini zaidi ya hapo pia katika mikataba ambayo tumeingia sasa maalum, kwa mfano Qatar tunakuwa na Kombe la Dunia hivi karibuni wafanyakazi wengi tunatarajia kuwapeleka kule na waweze kupata ajira.

Kwa hiyo, haya tunayaratibu vizuri kupitia Wizara ya Mambo ya Nje kwa kushirikiana na balozi zetu huko nchini na hivi karibuni mmeona Balozi wa Ubelgiji alitoa takwimu za maeneo ambayo Watanzania wangeweza kuchangamkia kuweza kupata ajira. Kwa hiyo uratibu upo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu katika maeneo hayo.
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza hivi sasa shirika letu la Ndege Tanzania limeanza safari zake za kubeba mizigo kwa ajili ya safari Guangzhou China, inaondoka China na kupitia Zanzibar na baadaye inarudi Zanzibar. Shirika hivi sasa wanatumia ndege yake ya Boeing 787 kwa ajili ya kubeba mizigo hiyo. Ndege hii imeundwa kwa ajili ya kubeba abiria na mizigo lakini eneo kubwa ya ndege hii ni kwa ajili ya kubeba abiria. Shirika letu sasa linabeba mizigo bila ya abiria kwa kwenda huko China.

Je, Shirika halioni hivi sasa kuendelea kufanya hivyo ni kuendelea kulitia hasara?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi sasa kumekuwa na ongezeko kubwa la abiria kati ya Zanzibar, Pemba na Dar es Salaam. Je, ni lini Shirika la Ndege la Air Tanzania litaanza safari zake katika Kisiwa cha Pemba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. FREDY A. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ali Juma Mohamed Mbunge wa Shaurimoyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna Ndege aina ya Dreamliner 787-8 ambayo inafanya biashara kati ya Tanzania na China na Ndege hii imekuwa ikibeba abiria lakini kipindi cha Covid 19 China kama tunavyofahamu kuingia abiria yeyote ndani ya nchi ya China. Kwa hiyo tukaona ni heri na bora Ndege hii aina ya 787-8 Dreamliner ambayo ina uwezo wa kubeba tani 40 ifanye biashara ya kubeba mizigo kuliko tungeiacha kuwa grounded na ingekuwa gharama zaidi kuliko hivi sasa ambavyo ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili Mheshimiwa Mbunge anatamani ama anapenda kwamba tuanzishe safari za kwenda Pemba. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote wa Zanzibar kwamba Shirika letu la ATCL litaanza safari zake za Pemba mwaka wa fedha 2023/2024 kwa maana ya kwamba mwaka ujao, ahsante. (Makofi)